Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 47. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 47.

Aliporudi ofisini akakuta barua ya James kuanza likizo kwa siku 7. Akampigia. “Nilisahau kukupa hongera James. Am so proud of you, man!” “Nashukuru aisee. Siamini. Mtoto mtamu kuliko pesa, aisee!” Colins akacheka. “Kama wewe unasema hivyo, naamini. Hongera sana. Na mpe Jema pongezi na pole. Pakitulia nitakuja kumuona mjomba.” “Jema atasikia na karibu sana.” “Kabla hujakata simu, utajali nikiwa nikimtumia yule kijana wako aliyekuwa akiwasaidia wewe na Jema hapo nyumbani kwenu? Au sasahivi mtakuwa mkimuhitaji zaidi? Maana ulimsifia ni mwaminifu sana.”

“Bila shaka. Maana kwa sasa hapa ndani kumejaa mno. Tunamsaada kila kona. Na najaribu kumshawishi Jema akubali tuletewe msichana wa kazi kwa ajili ya mtoto. Unajua kwao wamekua bila msichana wa kazi. Sasa namchukulia taratibu sana. Hataki msichana wa kazi kabisa humu ndani. Ila najua tutahitaji atakapokuwa anarudi kazini. Ninachotaka kusema, wewe zungumza na Chaz mwenyewe. Na kwa kuwa alishafika kwako, mpange naye muda na siku. Hapa nyumbani atabakiwa na kazi za nje tu, ambayo najua kwa jinsi alivyo, haitamtosha. Atahitaji pesa zaidi.” James asijue jinsi anavyomsaidia.

“Basi acha nizungumze naye. Tuwekane sawa. Nakushukuru, ila naomba nikuombe msaada James. Najua sasahivi unamtoto, akili zipo kwa mkeo na JJ.” James akacheka. “Au umebadili jina?” “Hilo lilishapitishwa, naona na mwenyewe analijua.” Colins akacheka. “Sawa baba JJ. Lakini naomba niangalizie Jelini wangu.” James akanyamaza.

“Kuhakikisha anapata dawa sahihi kichwa kitulie. Na tafadhali zungumza na mama yake, atulie swala la kazi kwanza mpaka apone kabisa. Kwa jinsi nilivyomsikia yule daktari akizungumza na sisi tulipomrudisha hospitalini na mama, Jelini bado ni mgonjwa, James. Aliona kabisa ndani hajapona. Na yeye alimwambia. Hata mwanga wa nje alimwambia atumie miwani ya jua wakati wote ili kufanya mishipa ya kichwa itulie. Tafadhali naomba ulisisitize hilo. Ni kwa muda tu wakati nikijipanga. Nikiweka mambo sawa, nitakuwepo mwenyewe. Lakini kwa sasa, naona upo sahihi. Nitamuumiza yeye zaidi. Acha nitengeneze mazingira yetu. Ni hilo tu. Nisaidie tafadhali. Na kama kuna uhitaji wa pesa, niambie, utakuwa ukichangia kupitia mfuko wangu.” “Sawa, Colins.” Hakuamini jinsi James alivyokubali. Akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Zilipita siku tatu tu, ramani ya nyumbani kwa Colins ikawa imekamilika. Kazi ikawa inaanza rasmi siku ya jumatatu. Katika siku zote hizo tatu alishatuma ujumbe kwa wazazi kuwa James amepata mtoto, yupo likizo. Kwa hiyo kazi zake zote anafanya yeye. Atakuwa busy, akitoka alfajiri kurudi usiku, hakutani na watu wa nyumbani kwao.

Siku ya jumamosi akiwa saluni akijisafi kichwa, simu ya mama yake ikaingia. Akapokea na kumsalimia. “Mbona huji kula nyumbani.” “Kwa sababu napika kwangu.” Mama yake akatulia. “Kama hakuna jingine, naingia saluni mama, nitawaona kesho asubuhi kabla ya kwenda kanisani.” “Sawa.” Mama yake akakata, akijua wazi hajafurahia ila hakujali tena. Yupo kwenye kutengeneza kwake.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati anatoka saluni, simu ya baba yake ikaingia. Na yeye akamsalimia. “Usiku tumekubaliana kukutana nyumbani kwa mzee Simba.” “Sawa.” Colins akakubali kirahisi mpaka baba yake akashangaa. Ila akaamua kumuaga. Colins akarudisha simu mfukoni, alikuwa na mpango wa kurudi kwake, akaamua kurudi kazini akiwa na mawazo haswa. Akili yote inamuwaza Jelini.

Jumapili Ya Mapinduzi Mazito.

 Asubuhi akasikia mtu akimgongea, akaamka usingizini akaenda kufungua mlango akiwa na usingizi maana alikesha akiwa anacheza game, akishindwa kulala. “Baba anakuita. Amesema sasahivi.” Alikuwa Jose. Colins akatoka baada ya kuvaa suruali.

Akawakuta mezani wakipata kifungua kinywa, na Connie alikuwepo. Akasimama na kumkumbatia kaka yake, Colins akampa busu la kiusingizi, Connie akarudi kukaa mezani na wazazi wake. “Kwa nini jana hukutokea kwa Simba?” Colins akakunja uso kama ambaye hajamuelewa baba yake lakini alijua wazi ni nini anazungumzia. “Colins?” “Sijui unazungumzia nini!” “Usijifanye hujaelewa Colins! Sikukupigia simu kukutaarifu kwamba tumekubaliana usiku ule tunakutana kwenye familia ya Simba? Tena ukasema sawa!” “Kabisa.” Colins akakubali.

“Sasa kwa nini hukutokea?” “Wapi tena baba? Mbona unanichanganya!? Wewe ulinipigia simu na kuniambia mmekubaliana mnakutana kwa Simba. Sasa!?” “Swali ni kwa nini hukuja, na simu ulifunga?” “Labda kama unataka kugomba tu na mimi, baba. Kama mmekubaliana kukutana kwa Simba, hapo mimi nahusikaje!?” Mama yake alitegemea tu. Connie kimya.

“Mimi sikuwa na ratiba ya kwenda huko. Sasa kwa nini nivunje mambo yangu kuungana kwenye makubaliano yenu?” “Kwa…” “Subiri kwanza baba. Nahisi kuna jambo unalipuuza hapa. Simba ni rafiki yako wewe. Au yeye na mkewe ni marafiki zenu nyinyi, mlio wachagua nyinyi tokea zamani. Mkalea familia zenu, mkizijenga kwa makubaliano yenu nyinyi. Ikafaa wakati ule sisi ni wadogo. Lakini si sasahivi. Usitake mimi nijenge familia yangu kwa misingi yenu, wewe na mzee Simba! Hapana baba.” Colins akaongea kwa ujasiri maana alimjua mzee wake.

Nyinyi ndio marafiki. Lakini mimi nafahamiana nao kukupitia nyinyi!” “Na mimi ni mzazi wako.” “Sawasawa. Lakini haimaanishi ulichochagua wewe ndio nitakachochagua mimi! Marafiki zangu, sio marafiki zako. Au marafiki wa mama sio marafiki wa Connie. Tafadhali hilo naomba uzingatie baba. Wakati ule nilikuwa niko na nyinyi kwenye ile familia kila wakati kwa sababu kulikuwa na mahusiano mengine kati yangu na Love. Yale mahusiano yameisha.” “Lakini ameomba msamaha na anakiri ana…” Colins akacheka akitingisha kichwa akikataa.

“Nilisema, simtaki tena Love, na NILIMAANISHA. Sitarudiana tena na Love, baba. Hilo naomba ulipokee.” “Na nisipolipokea?” “Hilo tena litakuwa nje ya uwezo wangu.” Colins akajibu akionyesha hajali tena. “Colins!?” “Nini mama? Nini? Yaani gafla mnataka eti mimi nijenge familia yangu kwa kupitia misingi yenu!? Hapana. Kuna faida gani basi ya kunilea na kunifundisha kufikiria na kufanya maamuzi mimi kama mtoto wa kiume? Si kila wakati mtapenda nilichopenda, na mimi hivyohivyo. Sio wakati wote nimekuwa nikiyafurahia maamuzi yenu!” “Kama yapi?” Baba yake akamuuliza.

“Moja wapo ni hilo na mengine ambayo sitayataja hapa kwa sababu siyo pointi ya sasahivi. Ila ninachotaka kusema, nimeamua kuwa na maisha yangu ya kujitegemea kama vile nilivyokuwa nikiishi nje ya nchi. Nitaishi kwangu nikijitegemea. Nitafanya maamuzi yangu kama mimi Colins. Mimi ni mmoja wa familia hii, si kina Simba na marafiki zenu wengine. Ikitokea mna jambo lenu ambalo linaangukia kwenye ratiba zangu, sitahudhuria. Ila ikitokea kwenye siku ambazo nina nafasi na najisikia kuhudhuria, nitahudhuria. Lakini msiniburuze mimi kama Colins wa miaka 10. Nimekua. Na hilo naomba mkumbuke na kuliheshimu.” Colins akaweka msisitizo.

“Kingine ambacho nilipanga kuwataarifu baadaye mkitoka kanisani, ila kwa kuwa mmeniita sasahivi, acha tu niwaambie.” “Kwamba wewe hutaenda pia kanisani?” “Nitatafuta kanisa ninalopenda mimi. Ambalo ndipo na familia yangu itakapokwenda huko.” “Umechanganyikiwa Colins?” “Labda tumpigie simu babu, tumuulize kama yeye ndiye aliyekuchagulia mke, rafiki na akakupangia sehemu ya kwenda kuabudu.”

“Colins mwanangu wewe!” “Hapana mama. Naona mnataka kuyaendesha maisha yenu na yangu pia! Nimekataa na nashauri hilo mliheshimu. Maana mnanijua. Katika hili sitayumba kama nilivyobaki na msimamo nikiwa na Love, huku akinitesa moyo wangu mchana na usiku bila huruma, lakini nikabaki kuwa mwaminifu kwa ajili mahusiano yenu. Lakini sitafanya hivyo TENA. Sitaendelea kuishi maisha yako baba. Na wewe naomba usiendelee kuishi maisha yako na yangu. Mwishoe utajikuta ukitaka kuendesha familia yako na yangu pia.”

“Toka Colins. Unanivunjia heshima.” “Mimi naondoka, ila mjue kuanzia kesho kampuni ya ujenzi inakuja kuzungushia nyumba yangu uzio. Ujenzi utaendelea, na wameahidi ndani ya majuma matatu watakuwa wamekamilisha. Kwa hiyo mkiona watu pale, msishituke.” Akamgeukia mama yake. “Mama, wamesema upande ule unaopakana na kwangu wanaweza kukuharibia ukoka wako kidogo, ila wamesema watapatengeneza vizuri, kiasi kwamba mpaka panakamilika, na wewe ukoka wako utakuwa sawa. Ni hilo tu.”

“Na mimi pia sitaki tena kwenda nyumbani kwa kina Simba.” Connie naye akadakia kwa haraka kabla kaka yake hajaondoka. “Nyinyi watoto mmepatwa na nini!?” “Mimi nilikuwa sijui jinsi ya kuwaambia mama. Lakini mimi pia nipo kama Colins. Wale watoto wa Simba ni marafiki mnaotuchagulia kwa lazima, lakini mama wewe unajua wazi sio watoto wazuri. Loreta anamsumbua Reji mpaka Reji ameshindwa. Anasema amevumilia na amemuonya Loreta, lakini hakomi. Anamtumia mpenzi wangu mpaka picha za uchi!” Mama yao akashituka sana.

“Haiwezekani Connie!” “Hakika dad. Nimevumilia lakini nimeshindwa. Reji anasema yupo kama amepagawa. Wakati mwingine anampigia simu mpaka usiku kabisa anamwambia halali anamuwaza yeye na kuanza kumtumia picha zake akiwa uchi kabisa.” “Anauthibitisho?” Hilo swali lilimfanya mpaka Colins akacheka kwa masikitiko.

“Yaani wewe baba unafikiri Connie au Reji wanadanganya ili iweje?” “Acha kunihoji mimi kama mtoto mdogo, Colins!” “Maana unachukua upande wa watoto wa Simba bila kutaka kutufikiria sisi! Tangia lini mimi na Connie tumekupa sababu kuwa sisi ni watoto wakaidi kiasi hiki? Ni kwakuwa tumevumilia, tumeshindwa baba. Wale watoto ni shida, na najua mama alishakwambia ila unalifumbia macho ili tu wewe undeleze urafiki na baba yao.”

“Colins unavuka mipaka na sitakuruhusu.” “Unataka kunimalizia mimi hasira bure sababu safari hii ameongea Connie kipenzi cha kila mtu humu ndani na wote tunajua Connie anaishi maneno yake si muongo. Huna jinsi yakutoka ndio..” “Nyamaza Colins.” Mama yake akakaripa. “Sawa.” Akajibu na kunyamaza akicheka kwa masikitiko.

“Ninazo picha alizomtumia Reji. Tena sikutaka anitumie yeye kwenye simu yangu, nimepiga picha kabisa simu ya Reji, sehemu ambayo Loreta anachati naye mpaka muda utaona mama. Sikutaka kumuuliza, lakini kumbe ndio sababu Reji alikataa kuja kabisa siku ya mwaka mpya baada ya kujua Loreta atakuwepo. Anasema ni mbaya mno, tena anasema akijikuta wapo wawili tu sehemu, yupo physical kabisa.” “Haiwezekani Connie!” “Kweli mama. Reji anasema anatakaga kumshika kwa nguvu. Anasema imebidi aniambie isije tokea siku namkuta amemshika sehemu, nikadhani ni tabia yake.” Connie akaendelea taratibu kama mama yake.

“Wote mnamjua Reji ananipenda na ndiye mwanaume pekee aliyekubali kuniunga mkono kwenye ndoto zangu. Ananisubiria bila kuchoka. Halafu Reji ni mwaminifu. Sitaki amjaribu mpaka amshinde nguvu. Hapana dad. Nakwambia ramsi kwa sababu nataka leo jioni mama anisindikize kwa mama yake, tuzungumze na Loreta. Kuanzia hapo mimi wale watoto siwataki tena.” “Sasa hapo Love anahusikaje?” Mzee akaendelea kuhoji na kuendelea kumshangaza Colins.

“Love na Loreta ni wale ndugu wa kufichiana siri za wanaume. Kabla hujauliza nimejuaje, kumbuka nimekua nao. Inamaana kama Loreta amekua akimfuatilia Reji, basi ujue anazo baraka kutoka kwa dada yake. Au dada yake anajua. Wale watoto ni wabaya dad. Ni hivyo Colins hawezi kukwambia kila kitu kwa undani, lakini hata huyo Love unayempenda pia ana mambo ya wanaume. Hatuliagi na mwanaume mmoja. Hatosheki, mkorofi halafu mbabe. Anapenda mambo yaende kama anavyotaka yeye. Anapenda kutupelekesha mimi na Colins tokea tupo wadogo. Yaani eti kwa sababu alizaliwa miezi miwili kabla ya Colins, alikuwa anatuambia yeye ni mkubwa kwetu, anajua mambo mengi kuliko sisi, ndio anatupelekesha! Mimi sitaki tena, dad. Na naomba uelewe.”

“Na kingine kabla sijasahau.” Colins akamuwahi mzee akiwa kwenye utulivi akimsikiliza binti yake, maana kwake huwa ni mtulivu. Wote wakamwangalia. “Nawapa tu taarifa. Maamuzi yangu yote, nimezungumza na babu kwanza.” “Unasemaje Colins!?” “Kwa nini!?” Mama yake akaongeza kwenye swali la mumewe kwa mshangao mkubwa sana.

“Kwa sababu kama hizi. Hakuna mtu ananielewa kwenye hii familia kwa urahisi kama babu. Nimezungumza naye kwa urefu na mapana. Tofauti na nyinyi, babu amenielewa na kunipongeza sana.” “Kwa kuwa hajui kwa undani..” “Baba, wewe unalazimishia mambo na babu nimemwambia. Amesema anakuja uzungumze naye kwa kuwa mimi huwezi kunisikiliza na ameomba rasmi, marekebisho au ujenzi unaoendelea pale kwangu, nimwachie asilimia fulani ya garama, anataka kulipia.” “HAIWEZEKANI.” Mzee akahamaki.

“Wewe mpigie simu mwenyewe, mkatalie kuwekeza urithi kwa vitukuu vyake. Maana yeye mwenyewe amesema nisifanye marekebisho ya kimasikini, yeye anayo pesa. Anamalizia kuuza kahawa yake ya msimu huu, anitumie pesa.” “Sasa mimi sitaki kusaidiwa majukumu yangu. Hiyo ni dharau na baba anafanya makusudi.” “Pengine anaona kwa kuwa uko kinyume na mimi ndio maana.” “Colins!” “Wewe usinikasirikie mimi. Mpigie simu babu wewe mwenyewe uzungumze naye. Au msubiri anakuja yeye mwenyewe, naona yeye akizungumza na wewe ndio utamuelewa zaidi.”

“Kweli Colins unakuwa mkaidi kiasi ya kwamba upo radhi kuona jasho langu na Simba linapotea bure hivihivi!?” “Kwani nilazima mimi nirithi baba jamani!?” “Unafikiria kweli wewe Colins!?” Mama yake pia akazidi kumshangaa.

“Kwa nini mnanilazimishia mim? Mpeni Love na mwanaume atakayemuoa! Sio lazima mimi! Kwani mtoto nimekua mimi tu kwenye hizi familia?” “Mtoto wa kiume kwenye familia zetu hizi mbili ni wewe peke yako! Kweli hilo unashindwa kulithamini Colins, na kuweka tofauti zako na Love pembeni ukafanya maamuzi magumu ya kiume?”

“Nimeyafanya hayo maamuzi magumu na kuweka hizo tofauti zetu pembeni kwa muda mrefu sana, tena kwa machungu makubwa sana baba. Nimeweka kikomo, sitaendelea kujitesa sababu ya ndoto zenu. Kwanza Love ndiye anayejitambua kuwa ni mkubwa kwenye hizi familia zetu. Anasema anahaki ya kutuongoza mimi, Connie na Loreta. Na nyinyi wote mnamsifia ni kiongozi mzuri na anaakili sana. Sasa kwa nini msimpe hizo mali yeye kiongozi mzuri akaongoza mkiwa na uhakika zitakuwa salama!?”

 “Sisi tunachotaka mali zetu zote ziendelee kwa kizazi hadi kizazi chetu. Kwamba wewe na Love ndio mngeendeleza mali zetu na zibaki kwetu tu na vijuu mpaka vitukuu. Ili hangaika yetu isiwe bure! Lakini ikitokea Love anakuja kuolewa na mwanaume mwingine, inamaana mali zote zinakuwa chini ya huyo mwanaume na ukoo wake. Kweli kwa ukaidi wako tu unashindwa kuliona hilo!?”

“Sio ukaidi baba. Siwezi nikawa kwenye ndoa na mwanamke asiyeniheshimu, hakubali mawazo yangu hata kwa mchango mdogo tu, yupo tayari kunibishia hata kwenye mambo ya msingi, ilimradi yeye ndio aonekane ana uwezo mkubwa wa kufikiria kuliko mimi! Love hanipendi, ananidharau. Sasa eti mnataka mimi nibaki kwenye aina hiyo ya mahusiano eti sababu ya mali zenu! HAPANA kwakweli baba.”

“Mimi pamoja na mke wangu tutatafuta zetu na watoto wetu. Na naumia sana kuona mnachotaka nyinyi ni mali tu bila ya kunifikiria mimi! Hakika unaniumiza zaidi. Na kuanzia sasa, mimi binafsi naomba babu ndio azungumze na wewe kwa niaba yangu. Ukiwa na swali lolote juu yangu, wewe muulize babu.” Colins akaondoka kwa hasira. Mzee akanyanyuka ili aondoke kwa hasira.

Connie na sauti yake ya upole akamuwahi. “Ila kanisani nitakuwa nikienda na nyinyi, dad. Mimi bado nitasali na nyinyi ili tuwe tunapata muda mbali na wodini. Ila tafadhali isiwe kwa kina Simba.” Huyo mzee anampenda Connie, roho yake! Akamwangalia tu, na kupotelea chumbani kwake, mkewe akamfuata.

~~~~~~~~~~~~~~~

 Colins aliondoka kwa ujasiri akijua mzee atakuja tu kuwekwa sawa na babu. Hao baba zao, vichwa ngumu na baba yao, yaani babu yao kina Colins ndio anawawezea. Babu yake Colins alikuwa mkoloni haswa, lakini mwenye pesa ambayo akiongea mbele ya hao wanae aliosomesha kwa elimu ya juu mpaka baba yake Colins huyo daktari, wanamsikiliza. Mkali kwa watoto wake kama pilipili kichaa, lakini kwa wajukuu, ni mtu mwingine tofauti. Akisema anakupa pesa, si pesa chache. Hapo Colins alikuwa akifanya ukarabati kwa jeuri, akijua mamilioni ya babu yanakuja, na mzee atawekwa sawa tu.

Kama Penzi Lipo, Lipo tu.

Katikati ya likizo yake ya siku saba ya uzazi, James akapokea ujumbe mwingine tena kutoka kwa Colins. Akafikiria, siku hiyo ya jumamosi akaona amfuate mama Jema aliyekuwa amefika hapo mapema na kuchukua nguo zote za mtoto kwenda kufua nje. “Samahani mama yangu. Naomba tukae hapa kidogo.” “Hata nisisuuze kwanza!?” “Mimi nitasuuza. Naomba nisaidie maana nipo kwenye wakati mgumu kweli.” Mama Jema akaosha mikono na kukausha akiwa na wasiwasi. Wakatafuta sehemu wakaa hapo nje.

“Naomba soma hizi jumbe kuanzia hapa.” James akamfungulia simu yake na kumkabidhi. Mama Jema akaanza kusoma. Akashangaa sana. “Huyu ni nani!?” James akamuonyesha jina kwa juu ya zile jumbe. Akasoma. “Colins!?” James akatingisha kichwa kukubali. “Mbona sasa anachoandika hapa si alivyoniambia Jelini? Jelini aliniambia ni kama amerudi kwa mwanamke wake wa kwanza.” “Ndiyo na hapana. Ndiyo kwa sababu siku miahadi yake na Jelini ilipovunjika, alilazimishwa na familia kwenda kumuona hospitalini. Si peke yake, ila kama familia. Na ukweli baba zao wanatamani sana waoane.”

“Lakini mama Jema, Colins anampenda Jelini, anakaribia kurukwa na akili.” “Nimesoma hapa! Sasa ni nini kinaendelea James!? Maana mimi aliniumiza sana Colins. Sikutegemea jinsi alivyofanya kwa Jelini alipokuwa matatizoni, halafu na kuja kumgeuka!” “Kwa kuwa namfahamu Colins, acha mimi nimsemee na nimuombee msamaha. Si muongo, na wala si muhuni. Ni mtu wa maneno yake. Anajisikia vibaya hata kukuona. Anahisi kukusaliti vibaya sana.” “Mimi?!” James akacheka.

“Unakumbuka juzi usiku kuniona natoka, wewe ukiwa na Jema pale chumbani. Nikamwambia Jema asome ujumbe kisha nikatoka?” “Ukarudi na dawa za Jelini pamoja na juisi sijui na vitu gani?” “Ewaaah! Basi Colins ndiye aliyevileta. Aliishia getini baada ya kujua wewe upo ndani. Akaniomba nikupe umpelekee Jelini, ila niseme vimetoka kwangu. Sasa nimezungumza na Jema, nikamwambia lazima nizungumze tu na wewe. Colins amelelewa…” James akamsimulia historia ya familia ya Colins na kina Love kwa mapana na marefu mpaka mama Jema akapoa.

“Sijui kama umenielewa?” “Lakini tuwe tu wawazi James. Ile familia yao na mimi niliiona. Aina ya watu wao, wote tuliwaona. Mimi sijasoma, sipo kwenye mazingira kama yale yao ya kisomi. Jelini wangu ndiye huyo shule hataki hata kusikia. Kweli unataka mwanangu akajiingize kwenye hiyo familia, wanayotaka mahusiano ya wao kwa wao! Si mnanitafutia matatizo kweli mimi? Maana sitaweza kunyamaza nikiona wanamuonea mwanangu au wanamnyanyasa.”

“Kwa alivyoniambia Colins, anaandaa mazingira ya Jelini kwanza kabla hajarudi kwa Jelini na kumchanganya zaidi. Maana mimi nilimkemea kwanza. Nikimuonya asimchanganye Jelini. Nikimpa wasiwasi wangu kama huo. Baadaye ndio akakiri kuwa, anafanyia kazi udhaifu wote na kuziba mianya yote. Amekiri amekua akiishi kwenye misingi ya baba yake, na amesema ameshazungumza na wazazi kuwa, anaanzisha maisha yake sio yale aliyokuwa akiishi akizungukwa na chaguzi za baba yake.” James alishaaminika kwenye moyo wa huyo mama, hakuchukua muda mrefu sana kumuweka upande wake.

“Kwa hiyo ndio hivyo.” “Mmmh!” “Na kutomuona mpaka sasa ujue ni kwa sababu ya kukuheshimu sana wewe. Colins asingeacha kuingia ndani. Anaishia nje getini akisema hataki kuharibu zaidi. Tafadhali mpe nafasi. Nina uhakika kama Jelini akiishia na mtu kama Colins, hatajuta. Ni miongoni mwa watu waadilifu sana.”

“Sasa mlitaka mimi nifanyaje?” “Cha kwanza nakuomba nisaidie haya mawasiliano kati yake na Jelini unipokee ili nimfurahie mwanangu.” Wakacheka wakimjua Colins. “Sihemi mama yangu! Nakua utafikiri naishi na Jelini humu ndani. Na akianza kuulizia hali yake, inakua ugomvi kabisa. Mwishoe ndio unasikia nina mgeni getini. Na hapo atataka nimpigie simu Jelini, niweke spika, asikie majibu ya anavyoendelea. Mpaka nikamwambia Jema, Jelini atakuwa hanielewi. Maana hata kama ni kujali, vimezidi mama yangu.” “Juzi Jelini aliniambia Chaz ametumwa na shemeji apeleke chakula na kusaidia kazi pale ndani.  Kufua na kupiga pasi nguo zote. Mimi nikamwambia pengine umeona mimi nipo nikisadia sana kazi za hapa kwako, ndio maana ukaamua kutupa Chaz.” James akacheka na kutingisha kichwa kwa masikitiko akimuhurumia Colins.

“Ni yeye Colins, wala si mimi. Tafadhali nisaidie mama yangu. Mwisho nitajivunjia heshima kwa Jelini, bure! Ataona navuka mipaka. Kujali gani huko mpaka usiku mwingi kumpigia simu kumjulia hali! Msamehe tu Colins, na naomba umuelewe.” “Acha nikwambie ukweli James, ni vile umesema wewe. Lakini alishaniumiza sana na nikaona ametudharau akitufananisha sisi na zile familia zinazo wazunguka. Ila nimemuelewa. Na mwambie namshukuru kwa kumjali Jelini. Naona zile dawa alizoleta, zinamsaidia. Jana ameshinda bila kulalamika.”

“Kuna jambo jingine.” “Nini tena!?” James akacheka kama anayesita. “Niambie tu.” “Anavyosema Colins, siku waliyompeleka Jelini hospitalini, daktari alieleza wazi kuwa pale alipoumia Jelini, kwa ndani hapajapona.” “Hata nje hapajakauka kabisa.” “Basi anasema daktari alitoa ushauri mkubwa wa Jelini kutulia ili kutofanya mishipa ya kichwa kuuma. Kwamba Jelini anatakiwa kupumzika. Hata mwanga wa nje anatakiwa kuvaa miwani ya jua.” Mama Jema akabaki kusikiliza akijua silo analotaka kuwakilisha.

James akacheka. “Sasa hili ndilo ombi lake Colins. Kwamba, Jelini asianze kitu kipya sasahivi.” “Kwamba asifanye kazi?” James akacheka na kuendelea. “Amesema yeye anaweza ajiri mtu, afanye kazi za Jelini, atamlipa yeye mwenyewe. Na wewe akupe pesa uwe unampa Jelini kila mwisho wa mwezi ili atulie. Amesema unaweza mwambia Jelini ni pesa yake ya matumizi unampa mpaka apone. Ili kumfanya atulie mpaka apone kabisa.”

“Jelini mwenyewe anataka kufanya kazi, James! Wala si mimi.” “Tukikubaliana, tunaweza kuzungumza naye kwa pamoja na kumsisitiza kwa sasa anatakiwa atulie mpaka apone kabisa. Na kwa sababu anamwangalia sana Jema, tunaweza kumwambia Jema azungumze naye.” “Hapo atakubali. Maana anaona Jema alijikana sana. Yeye kuacha ni kama kukimbia kuwajibika. Ila kwa kuwa kwenye saa nne watakuja hapa yeye na Jeremy, acha tumpange kwanza Jema azungumze naye.” “Nashukuru mama yangu. Nampigia simu Colins, namwambia namuhamishia kwako.” James akalifurahia hilo ila akakumbuka.

“Ila ujiandae. Maana simu zake na jumbe si moja.” “Mbona mimi namjua! Wewe mpe tu.” “Basi acha nimalizie hizi nguo.” “Hapana James. Wewe rudi ndani kwa mkeo na mtoto. Mimi namalizia sasahivi nakuja ndani. Kwanza ni nguo chache tu. Nafua kila siku ili zisilundikane, na sitaki mama James aje akutane na nguo chafu. Iwe chakula tu.” “Nashukuru sana.” James akaondoka na kumuacha huyo mama moyo umetulia kuona kuna mtu anamjali na Jelini kwa kiasi hicho.

Atafutaye Asiyechoka.

Baada ya muda mfupi sana akiwa anasuuza nguo ujumbe ukaingia. Akaangalia simu kwa haraka akidhani ni Jelini, kichwa kimeanza tena. Akakutana na huu ujumbe. ‘Nashukuru sana mama yangu kunielewa. Sikukusudia kumuumiza Jelini.’ Amemaliza tu kusoma, ukaingia mwingine. ‘Nilisahau kukusalimia. Shikamoo.’ Ukawa wa pili. Kabla hajajibu salamu, ukaingia na wa tatu. ‘Sijui hali ya Jelini leo. Ameamkaje?’ Mama Jema akabaki akiitizama simu maana hajui ajibu nini. James akatoka.

“Nimemuhamishia Colins kwako. Nahisi atakutafuta tu.” Mama Jema akaanza kucheka akitingisha kichwa. “Tayari nini!?” “Hapa nina jumbe tatu tayari, sijui nijibu ipi. Na nyingine ya nne hii. Sijui ameandika nini!” James akacheka na yeye kwa masikitiko akimsogelea.

‘Inabidi kuongeza umakini kwa Jelini anayeonekana mzima akitembea, kumbe kichwa kina matatizo. Matukio kama yale ya mahakamani ndio yanayoweza kuonyesha kuwa si mzima.’ “Hakika kazi ipo! Hivi mimi sitaweza James. Sina muda wa kukaa chini na kuandika jumbe, hata wanangu wananijua. Ni bora kupiga tuzungumze, tuyamalize.” “Sasa fikiria ndio mimi. Nimelala na mke wangu, jumbe za kumzungumzia Jelini zinaingia na anataka ajibiwe. Lasivyo ugomvi au unashitukia yupo mlangoni.” “Hivi sitaweza, James. Bora uendelee naye.” James akashituka sana.

“Hapana mama. Tafadhali sana. Mwisho Jema atajikuta alibeba mwenyewe, na kulea mwenyewe, wote tunakwama kwenye jambo moja tu, Jelini. Acha hii likizo ya siku saba isiishie kwangu na Colins ambaye nitarudi ofisini, tuendelee naye. Wewe nipokee tu kwa muda. Tafadhali sana.” “Sasa nafanyaje?” “Wewe usiwe na wasiwasi. Usipomjibu, atakupigia. Na kwa kuwa anajua upo hapa, ndani ya nusu saa atakuwa amefika hapa. Wewe endelea na yako.” Wakacheka. Ila akamjibu.

‘Marahaba Colins. Jelini ameamka vizuri. Na mida ya saa nne atakuja kumuona dada yake na mtoto.’ Hapohapo simu ikaingia. Colins tena. “Usione kama nakusumbua mama yangu.” James akacheka kimyakmya huku akiondoka kwa kunyata. “Bila shida.” “Nilikuwa nikifikiria swala lake yeye Jelini. Kwa mfano wewe upo hapo kwa Jema. Sasa sijui yeye kule inakuaje? Maana bado ni mgonjwa hata kama ataonekana ni mzima, lakini bado Jelini anahitaji msaada.” “Wewe ulikuwa una wazo gani Colins mwanangu?” “Nashukuru mama. Au labda nije kabisa hapo, tuweke mipango vizuri.” “Hilo naona litakuwa la msingi.” “Basi sitakawia.” Simu ikakatwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akaanika nguo na kurudi ndani, Jema akampokea na cheko. “Nasikia umekabidhiwa Colins.” “Mbona ninaye! Hapa yupo njiani anakuja tuweke mipango ya jinsi ya kumjali Jelini.” James akasikia akaingia akicheka. “Acha masihara mama!” “Anakuja. Amesema baada ya muda mfupi sana atakua hapa. Maana anavyoona yeye, inaweza kuwa rahisi sana kumsahau Jelini, tukidhani ni mzima, kumbe ndani ni mgonjwa. Kwa mfano asubuhi hii mimi nipo hapa, kule amebaki peke yake.” Wakaanza kucheka.

 “Jamani Colins! Sasa sijui anataka kuweka mipango gani?” Jema akaongea akifikiria. “Ndio anakuja tumsikie.” “Na ujue yule hana asubuhi wala usiku.” “Mwambie mama. Colins hana asubuhi ya kawaida wala usiku ule wa giza zito. Alfajiri mnaweza kuamshwa na ujumbe wa kujuliwa hali ya Jelini. Saa 11 asubuhi!” “Haiwezekani James!” “Muulize Jema huyu. Mpaka wakati mwingine Jema yeye ndio alikuwa akimjibu  nakumwambia bado nimelala, labda nilikuwa na mtoto usiku ndio mtoto amelala, na mimi nimeweza kulala. Na hatujawapigia nyinyi simu bado, kuulizia hali ya Jelini.” “Na usifikiri hapo ataridhika. Ataniambia nimwambie James ampigie mara atakapoamka.” Jema akaongeza. Wakazidi kucheka. Mara kengele mlangoni.

“Haiwezekani!” Mama Jema hakuamini kama ndio ameshafika. “Wewe usicheze na Colins. Hapo hajalala.” “Bora wapatane, wengine wapumzike.” Kengele tena. “Nenda kamfungulie bwana James, atamuamsha mtoto.” James akatoka akicheka.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment