Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 46. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 46.

 Kuliko Ungua Mpini. Asubuhi akawahi kazini kama kawaida. Kwenye mida ya saa nne akaenda saluni, kujisafi kama kawaida yake, ndipo akaenda ofisini kwa Ndosi. Sekretari wake akamtania kidogo, akijua bado ni toto ya mzee, anayeingizia kampuni pesa. Akamwambia Ndosi anamsubiria. Jelini akaingia. “Mbona umepotea hivyo kisha ukakata mawasiliano katikati ya mchakato mzito vile! Mtoto wewe hutaki pesa?” “Hapana Ndosi. Nilibadili mawazo. Sitaki tena. Ila samahani sikuwa nimekwambia nilipitia kipindi kigumu kidogo, akili haikuwa imetulia. Lakini sitaendelea na ile biashara tena.” Ndosi akatoa macho nusura yamwagike.

Jelini akacheka tu. “Au labda hujaelewa! Nazungumzia ile biashara ya mafuta!” “Nakuelewa Ndosi. Kama na hilo ni moja ya mambo uliyoniitia, tumalize, twende kwenye jingine.” “Sijaelewa Jelini! Kwamba unakataa ule mchakato wa kituo cha mafuta!?” “Ndiyo.” Ndosi akabaki akimtizama. “Kwa kuwa tunaheshimiana na najua ulihangaika sana na mimi kuanzia gari, labda niseme hivi. Wakati nikipokea pesa kutoka kwa mzee Kasa, nilikuwa kwenye mahusiano naye. Sasa hivi hatuko kwenye mahusiano, sitataka kupokea tena chochote kutoka kwake.”

“Jelini!” “Kabisa Ndosi. Wala sijakurupuka. Mimi ndivyo nilivyo. Sipokeagi vitu kutoka kwa kila mtu. Hata Kasa mwenyewe ananijua. Na kama ungezungumza naye hili, angekwambia usinitafute.” “Yeye ndiye amesisitiza nikutafute.” “Basi mwambie Jelini hataki tena. Tafadhali naomba twende kwenye ajenda nyingine, niwahi daladala kabla foleni hazijaanza.”

“Kampuni ya mzee inataka kukulipa kwa ajili ya madhara aliyokusababishia mtoto wake. Inakulipa fidia na mnasainishana kabisa kisheria kwamba mliyamaliza hayo mambo.” Jelini akashangaa sana. “Wewe unazungumzia nini?!” “Wanakulipa pesa ndefu Jelini! Ndefu mno. Ilimradi tu mmalizane kwa amani. Na anayekulipa si mzee, ni Kemi mwenyewe aliyekusababishia ajali.” “Hakika mimi sielewi wewe unazungumzia nini!” “Wewe hukuanguka kwenye ofisi za Kasa na kupasuka?” “Sasa kila aliyeanguka analipwa na Kemi!?” Jelini naye akamuuliza na kumuacha Ndosi kwenye mshangao zaidi.

“Tafadhali twende kwenye ajenda ingine usianze mambo ambayo mimi siyajui Ndosi. Unataka kuanzisha kitu ambacho mimi sikijui!” “Kwa hiyo utakua tayari kusaini ili kukiri kama haya mambo yameisha?” “Yalianza lini!? Mbona mnataka kunichanganya tu. Tafadhali niache Ndosi. Lasivyo nitaondoka na hutakaa ukanipata tena kwa simu. Usinianzishie mambo ya ajabu. Sina shida ya pesa za Kasa mimi. Na wala sijawahi kuwa na shida ya pesa yake. Tafadhali nenda kwenye jambo jingine.” Jelini akawa amekasirika kabisa mpaka akamshangaza Ndosi.

“Pesa yeyote iliyokuwa ikiingia kwangu kutoka kwa Kasa ni kwa sababu tulikuwa kwenye mahusiano naye. Sasahivi sipo kwenye mahusiano na Kasa, napokea pesa zake mimi kama nani!? Malaya wake?” “Hapana Jelini. Tafadhali usiende mbali. Mimi ni mjumbe.” “Hapana Ndosi. Inawezekana uliniona na yule mzee ukadhani mimi nilimpendea pesa. Mimi nilimpenda yeye kama yeye. Sio pesa zake. Hilo naomba uelewe na UAMINI. Maana baada ya leo, nakuonya uwe mwisho wa kutaka kunihonga pesa mimi kama malaya. Mimi si malaya.”

“Niliishi naye nikijua yeye ni mtu mwingine kabisa. Kumbe mzee Kasa hawezi kuwa mtu niliyedhani ndiye, na ndiye niliyekuwa nikiishi naye, nikimpenda kwa dhati na ndiye aliyenitambulisha kwako. Nilipomgundua huyo mtu sio yeye na hawezi kuwa yeye, nikajiweka pembeni. Kwa hiyo kama unazo pesa za Kasa unatafuta mtu wa kumpa, sio mimi. Mimi sio malaya. Sichuni watu. Sijui kama umenielewa?” “Basi Jelini. Basi mama.” Jelini akaanza kutulia maana alishapandisha hasira.

“Basi naomba twende kwenye swala la mahakamani.” Wakajipanga vizuri, hapo Jelini alikuwa ametulia. Akajaribu kuuliza maswali yote mpaka akaridhika. Wakakubaliana muda, Jelini akasimama. “Naomba nikuombe kitu cha mwisho, Jelini.” Akageuka akinyanyua mkoba wake. “Naomba nikusogeze.” “SITAKI.” “Kwa nini unakataa msaada wa kawaida kabisa, na jua ni kali sana nje? Hukusema kichwa kinakuuma wewe?” “Ndosi, mimi sikufahamu kabisa. Siwezi kupokea chochote kutoka kwako. Ila nashukuru kujali. Asante. Tutakutana hiyo siku ya ijumaa.” “Kwa ajili ya kichwa, unatumia dawa gani?” Akamuwahi kabla hajatoka.

“Kuna dawa walinipa tena niliporudi hospitali. Kichwa kilikuwa kikiniuma sana. Zinakaribia kuisha, ila zikiisha, sitatafuta tena kama hizo walizonipa. Zinanipa usingizi na mimi nafanya kazi, nakua nachoka. Nafikiria kununua tu dawa za kawaida za maumivu. Asante kujali Ndosi.” “Unauhakika hutaki kabisa nikusogeze?” “Kabisa. Uwe na amani kabisa. Jioni njema, acha mimi niwahi.” Jelini akatoka na kurudi kwa haraka.

“Samahani Ndosi. Najua hii kesi inamgarimu mzee Kasa. Utakapo zungumza naye, tafadhali mwambie namshukuru sana. Asante kwa huu msaada.” “Nitamwambia Jelini. Pole kwa matatizo.” “Nashukuru.” Ndipo akatoka sasa, Ndosi akavuta pumzi kwa nguvu zote.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Nafikiri umesikia kila kitu mzee wangu. Sina sababu ya kujirudia na kukupotezea muda.” “Daah!” Mzee Kasa upande wa pili kwenye simu akasikika kusikitika. Jelini alikuwa akizungumza na Kasa kupitia Ndosi. Alikuwa kwenye simu muda wote kupitia bluetooth ndogo alizokuwa amevaa Ndosi masikioni, Jelini asijue.

“Ila kwa jinsi nilivyomsikiliza, sidhani kama atakuja tena kurudi kuwashitaki kwa ajali iliyompata, maana amekataa kukiri kabisa kama imesababishwa na binti yako.” “Lakini natamani hata angepokea hiyo pesa! Daktari aliyemtibu hilo jeraha, aliniambia wazi kupona kwake haitachukua muda mfupi.” Akaongea Kasa kwa kusikitika. “Tafadhali utakapomuona hiyo siku ya ijumaa jaribu kumdodosa kujua ni wapi anafanya kazi.” “Nitajitahidi.” Mzee akakata simu kwa masikitiko.

Ijumaa Siku Ya Mahakamani.

Japokuwa Naya alikuwa amejifungua, hata mwezi haujaisha, ilibidi Joshua aliyekua yupo likizo ya majuma matatu akisaidia mkewe na mama Magesa kulea mapacha ambao hata Naya mwenyewe hakuwa amejua kama amebeba mapacha. Mmoja hakuonekana kabisa kwenye ultrasound japo Joshua yeye alijua mkewe atazaa mapacha. Alimwambia mara moja tu, alipombishia kwa hofu, akamuacha. Na ikawa kila sehemu anaonekana mtoto mmoja tu, tena wakiume.

Siku Naya na Joshua wapo chumba cha kujifungua, Naya akidhani amemaliza, anamfurahia mtoto wake wa kwanza wa kiume, baadaya kama dakika 10 uchungu ukaanza upyaa. Ndipo akapata kidume cha pili. Alimtizama Joshua kwa hofu, asiamini. “Nilikwambia umebeba mapacha Naya.” “Mbona sasa hukusisitiza?” Joshua akacheka tu akifurahia double blessing. Akachukua likizo yake ya mwaka kabisa, ili kulea.

Ila siku hiyo ikabidi aende kazini mwenyewe ili Jema aende mahakamani kama kumsindikiza mdogo wake na mama yao. James naye akasema lazima awepo kwa ajili ya hali ya mkewe, ila pia kama mwanaume wa hiyo familia. Wakampitia Jelini na mama yake, safari ya Kisutu, mahakamani ikaanza. Kwenye gari kimya, James ndiye dereva.

~~~~~~~~~~~~~~~

Walifika wakakuta Ndosi akiwasubiria. Akamsogeza Jelini pembeni. “Mbona unawasiwasi hivyo?” “Sijui Ndosi! Na sikulala vizuri.” “Kwa nini?” Jelini akaanza kulia taratibu. “Niambie Jelini.” “Nahisi ni hofu tu ya kukutana na huyu mwalimu tena. Alikuwa akinifanyia ukatili sana. Sikuwahi kufikiria kama naweza kuja kumuona tena.” “Sasa nisikilize. Kama tulivyozungumza wakati ule, leo ndio siku ya kuhakikisha unasaidia kuhakikisha hatakaa akatoka tena uraiani na kumdhuru mtu mwingine kwa kueleza mahakama yote bila kificho. Na usiogope ukijua sasahivi hana mamlaka tena juu yako. Yupo kuhitaji rehema zako.”

Wakati wakizungumza, akawasogelea msichana mdogo tu, na ujauzito. Akamsalimia Ndosi na Jelini. Wakamuona anapiga magoti na tumbo lake mbele ya Jelini. Jelini akarudi nyuma akimshangaa. “Nihurumie mwanamke mwenzio dada. Msamehe mume wangu.  Shedy amebadilika jamani. Siye yule wa zamani. Sasa hivi ni baba, na tunatarajia mtoto wa pili. Tafadhali usimuhukumu kwa tabia zake chafu za zamani. Anajuta, na anaomba msamaha.” Jelini alipigwa na butwaa ni kama alishindwa kupumua kwa muda.

Mama Jema akasogea kama tembo aliyejeruhiwa. “Kama ulidhani hichi unachokifanya hapa ndio kitamsaidia, sasa kamwambie Jelini yupo na mama yake. Lazima ataadhibiwa. Kama si na mahakama, basi mimi mwenyewe, mama yake Jelini. Nitamuadhibu mpaka paume ndipo nitamsamehe. Lazima aadhibiwe.” “Nihurumie mama, nina watoto wawili. Nitaishije bila mume?” “Mimi mwenyewe nilikuwa na watoto wawili na nikalea mwenyewe. Mmoja ndiye huyo mumeo alikuwa akimbaka, na wapili huyu hapa. Nililea mwenyewe bila mume mpaka wakakua. Kwa hiyo badala ya kupiga hapa magoti, nenda kaanze kufikiria na kujipanga jinsi ya kulea wanao. Maana mshenzi, mumeo, hatakaa akatoka jela. Kama anataka msamaha wangu, ni pale atakapohukumiwa kifungo cha maisha, tena sio kunyongwa, akae ndani kila siku aamke jela, akumbuke mama Jema hakumzalia yeye mtoto wa kumbaka. Hapo mwambie ndio nitamsamehe na si vinginevyo. Haya peleka ujumbe.” Akamshika mkono Jelini na kuondoka naye wakiwa wamejaza watu hapo wakiwasikiliza. Wakamuacha bado amepiga magoti.

Kila Kazi Na Malipo Yake.

 Muda ukafika, wakaingia mahakamani. Shedy akaletwa na pingu. Jelini alishindwa hata kumuangalia. Akajikuta akilia, Jema naye akaanza kulia kwa uchungu sana. “Umeharibu maisha ya mwanangu. Na utalipa.” Mama Jema akaongea kwa jazba. Kilio cha mkewe nacho kikasikika. Ikaanza fujo, ndipo wakaamuriwa wasimame kwa sababu hakimu anaingia. Wakasimama wakati akiingia. Kesi ikaanza. Shitaka likasomwa, Jelini akaitwa kizimbani, akaapishwa na Ndosi akasimama kuanza kumuuliza taratibu.

Jelini akaeleza mwanzo mpaka mwisho. Ukatili wote aliokuwa akimfanyia. Vile alivyokuwa akimbaka kama mnyama, kisha kumfukuza kama paka mwizi. Jelini alikuwa akisimulia huku akilia sana. Mama Jema naye akaanza kulia. Japo ndugu zake walikuja kwa kuchelewa, wakaongeza nguvu. Wakili wa Jelini alivyomaliza, hakimu akampa nafasi wakili wa Shedy.

Hakuonekana na maswali magumu, ila kutaka kujua, kama anachosema ni kweli, ni kwanini hakuwahi kumwambia mtu yeyote au hata rafiki? “Alisema atanichinja mimi na mama yangu, pamoja na Jema. Alikuwa akinionea akijua hakuna wakunitetea. Wakati mwingine alikuwa akinibaka kisha ananipiga hapohapo chumbani kwake, tena bila kosa huku akinitisha nikitoka pale nikimwambia mtu, atanipiga zaidi ya vile.”

Huyu alikuwa akiishi nyumba ya kupanga, kweli unataka kusema hakuna mpangaji hata mmoja aliyeshuhudia hayo?” Akauliza wakili wa mshitakiwa Shedy. “Mimi sijui alikuwa akiwaambia nini wapangaji wenzie. Kwanza alikuwa haniruhusu hata kusimama nje ya mlango wake au hata kusalimia mtu wa pale ndani. Alikuwa akiniambia nikifika pale nipitilize ndani kwake moja kwa moja. Nikifika nikikaa kidogo, na yeye anakuja. Akishamaliza kunibaka, ndio ananifukuza, naondoka.” Vikasikika vilio hapo, kama msibani.

Akaletwa ushahidi wa vipimo vya hospitalini alivyopimwa Jeremy, na yeye Shedy, vikasomwa na daktari ambaye naye alilipwa na Kasa na kuomba atokee siku hiyo mahakamani. Akasema kwa asilimia 100 Jeremy ni mtoto wa Shedy.

Hakuna Msiba Usiokuwa Na Mwenzie.

Lililokusudiwa Kuwa Baya, Mungu Akageuza Kuwa Jema.

Katikati ya kesi Jelini akaanza kumlilia mama yake kichwa kinamuuma sana kinakaribia kupasuka. Hapo mama Jema akapaniki hakimu bado akiwa anaendesha kesi. Jema anasimama kwenda kumsaidia mdogo wake na yeye chupa ya uchungu ikapasuka. Ndio ukawa mchanganyiko mara mbili. Mama Jema anataka yeye mwenyewe ndiye asaidie wanae, mtu asiwaguse. Halafu sasa hawezi kujigawa.

James akamtuliza na kumwambia wote waingie garini waelekee hospitalini. Akakubali kuwa na wanae wote garini. Msafara wa mama zao nao nyuma Ikabidi Ndosi yeye abakie mahakamani. Wote wawili wakapokelewa. James, mkewe na mama mkubwa wao upande wa kujifungulia. Mama Jema na Mode wao wakawa wanasubiria daktari kumsaidia Jelini.

Jelini alipopewa sehemu ya kujipumzisha, sehemu ya mapokezi, akiwa amepewa huduma ya kwanza anasinzia, akabakia na shoga yake, mama yake mdogo Mode. Mama Jema akakimbilia kwa Jema.

Baada ya masaa matatu mbele, Jema na James na wao wakapata mtoto wao wakiume wa kwanza. “Mtoto amefanana na baba yake huyu! James una damu kali sana.” James alikuwa na furaha huyo. Wakwanza kumpigia simu ikawa mama yake kisha baba yake. Ndani ya muda mfupi sana mama James akawa amefika hapo, hata biashara zake akaweka pembeni. Furaha ya mjukuu. Ndipo baadaye akili ikamjia James kumwambia Joshua aliyekuwa amemshikia kazi mkewe kwa siku hiyo.

Maji Yaliyomwagika Mchangani.

Akiwa amepumzika hapo kitandani sehemu aliyopewa ya kupumzika kwa muda, ila amefunga macho akisinzia akaanza kupata harufu nzuri sana manukato ya kitajiri. Akagundua ni manukato ya Kasa. Jelini alishituka mpaka akafungua macho. Akamkuta amesimama pembeni ya kitanda chake. Alikuwa amependeza. Msafi kama kawaida yake. Kiofisi.

“Pole sana.” Jelini akabaki akimtizama. Mama yake mdogo alimuaga anakwenda kuangalia mtoto, angerudi. Maana na yeye alipigiwa simu na dada yake kumtaarifu kuwa Jema amejifungua na amesharudishwa wodini ambapo ni chumba cha mtu mmoja kama James alivyolipia. Ndipo akamuacha Jelini apumzike, yeye akaondoka.

“Unajisikiaje?” Akamuuliza tena kwa kumbembeleza lakini Jelini akafunga macho bila ya kumjibu. Pakatulia kwa muda.

“Jelini?” Akamsikia akimuita taratibu. “Nilikosa mpenzi wangu. Nilikosa vibaya sana. Naomba tafuta jinsi ya kunisamehe. Nimebadili njia zangu zote. Nimebaki na wewe tu.” Jelini akajisikia uchungu wa ajabu, akaanza kulia. “Tafadhali nipokee tena. Najuta. Sina jinsi nikakueleza ninavyojuta ukaelewa. Na sikuwa nimepanga kabisa kulala naye siku ile. Walinilevya, nikaamka pembeni yake, wote tukiwa uchi. Nakiri baada ya kujikuta nimeamka pembeni yake, baada ya hapo nilifanya mengi kwa kupaniki tu nikitaka kumridhisha aondoke asirudi tena. Ila sitetei nilichofanya. Nilikosea. Nimekosa Jelini wangu. Tafadhali nisamehe.” Akaendelea taratibu.

“Nataka nibakie na wewe tu. Na nakuahidi, ukinipokea tena, sitarudia tena kulala na mwanamke mwingine yeyote mpaka kifo changu, ila WEWE tu. Na wewe ndio utanizika.” Jelini hakujibu wala kufungua macho kumtizama tena.

“Na naomba uniamini. Vile ulivyonikuta sio kwamba ndio maisha yangu. Sio kwamba ni kitu nilikuwa nikifanya kwa siri au usifikiri ndio maisha niliyokuwa nikiishi nilipokuwa na wewe. Hapana. Pale nilikosa. Na nasema ukweli, na Mungu ni shahidi. Tokea tuanzane na wewe sikuwa nimelala na mwanamke mwingine ila wewe tu, mpaka siku ile.” Akasikia simu yake imeingia, baada ya kuita tena na tena akamsikia akitoka. Alipojiridhisha ametoka kabisa hapo alipopumzishwa, Jelini akatoka kitandani kama akimbie. Akachukua vitu vyake vyote, akatoka mbio kwa mama yake.

~~~~~~~~~~~~~~~

Wote wakashangaa anaingia hapo, ila mama Jema akaanza. “Si ulisema alikuwa amelala?” “Dada, nilizungumza na Jelini, yeye mwenyewe akaniambia nije kuona mtoto, yeye anapumzika.” “Sasa wewe unamuona amepumzika hapa? Kilichokushinda kutulia kule mpaka mwenyewe nije ni nini?” “Hivi wewe Jelini mbona hunitetei shoga yangu, unakuwa kama hatukukubaliana ulale mimi ndio nije kuona mtoto?” Jelini akaanza kucheka.

“Mimi hajaniaga, mwaya mama. Nimejikuta nipo peke yangu, nikasema bora niende kwa mama yangu mzazi!” “Unapatwa dhambi Jelini wewe!” “Nakutania bwana mamdogo. Kichwa kimepoa nataka niondoke. Jeremy atarudi shule asikute mtu pale nyumbani.” “Sasa umeruhusiwa?” Mama yake mdogo akamuuliza. “Kwani walinileta wao?! Hee!  Nimekuja kwa ridhaa yangu, naondoka kwa ridhaa yangu. Mwishoe wataanza kuniongezea madawa yale ya usingizi.” “Haya ongoza njia tunarudi. Usinitanie mimi.” “Mama jamani!” “Hakika twende. Nikazungumze na huyo daktari ndio akili itatulia. Jema mama, nitarudi nikishazungumza na huyo daktari aliyekuwa akimtibu huyu.”

Mama Jema akatoka naye kurudi alipokuwa amelazwa huku Jelini akiogopa asije kumkuta mzee Kasa. Uzuri hawakumkuta. Ila akaruhusiwa baada ya kusema anajisikia vizuri na anazo dawa, hataki madawa mengine. Akasisitizwa mapumziko. Akakumbushwa tena, nje kunaweza onekana kumepona, lakini ndani ikawa bado.

Ndipo wakarudi kwa Jema na mtoto. Wakakaa hapo kwa muda, Jelini akarudishwa nyumbani na mama yake mdogo. Jema akabakishwa hapo kwa ahadi ya pengine kesho yake ataruhusiwa kwa kuwa yeye na mtoto walikuwa salama.

~~~~~~~~~~~~~~~

Jelini alirudi kwake, na kulala moja kwa moja. Mama yake mdogo akamsubiria mwanae anaposhushwa na gari ya shule. Akafanya yote aliyosisitizwa na dada yake juu ya huyo mjukuu. Ndipo akampa simu apate maagizo kutoka kwa bibi yake. Jeremy aliyelelewa na bibi, akapata maagizo yake. Simu alipochukua Mode, akaambiwa ruksa kuondoka, kazi yake imeisha, huyo mtoto anajua chakufanya. Mode akaondoka akimuacha Jelini amelala, Jeremy mezani akifanya homework zake. Kimya mtoto huyo asiye na makuu.

~~~~~~~~~~~~~~~

 Kesho yake alipomfikisha tu mkewe na mtoto nyumbani akiwa na mama James, mama Jema na Viola, James akarudi ofisini kuandika ruhusa ya uzazi. Alipofika ofisini akakutana na Colins alishafika anafanya kazi. “Mbona ulipotea gafla na simu hupokei wewe!?” “Jana ilikuwa siku ndefu hata sikukumbuka simu. Kuanzia mahakamani…” “Wooo, wooo! Mahakamani tena!” “Jelini alikuwa na kesi ndio….” Mpaka James anamaliza kusimulia, Colins macho mekundu kama nyanya.

“Kwamba yule mtoto alimpata kwa kubakwa!?” Colins akamuuliza kwa kuumia sana. “Na ndio siri ya unywaji ule wa pombe. Alikuja kusimulia, iliumiza sana. Maana kila mtu alijua ni mtoto aliyeshindikana, kazi yake ulevi tu, hataki shule. Kumbe kumbukumbu ya yale aliyokuwa akifanyiwa huku akiteswa, ilikuwa ikimsumbua. Inabidi alewe ndipo alale. Na shuleni akawa hataki kurudi tena, anaogopa asije pitia alipopitishwa na huyo mwalimu.” James akamueleza mengi, Colins akazidi kuumia.

“Ninapokwambia Jelini anahitaji mwanaume aliyekusudia kuwa naye yeye kama yeye Jelini, basi uelewe ni kwa sababu hiyo. Ni mdogo, lakini amebeba historia ngumu sana.” “Nilielewa James. Na nashukuru kwa kuwa naye hata huko mahakamani ambako ulishindwa kuniambia na mimi.” “Unataka kunilaumu bila sababu. Si mimi niliyekuunganisha naye tena safari hii ya mwisho lakini ukashindwa wewe mwenyewe?” Colins akasimama na kuondoka kabisa hapo ofisini kwao.

Maamuzi Magumu.

Akijua wazazi wake hawapo nyumbani, Colins alitoka hapo na kwenda kutafuta kampuni ya fundi kabisa. Akarudi na kiongozi wake hapo kwake. Akamzungusha nje ya nyumba yake na kuyatizama hayo mazingira. “Nataka ujenge ukuta kutenga hii nyumba yangu. Iwe ndani ya ukuta wake kiasi ya kwamba, nipate geti lake, yenyewe. Isiingiliane na nyumba nyingine. Utoe sehemu ya kuegesha magari na ijitegemee bustani yake.” Akawa ameelewa. Akamwambia ampe muda.

“Hicho ndicho kitu pekee ambacho sina. Ila pesa ipo. Sasa uniambie unaweza au huwezi.” Colins akauliza kwa ukali. “Ulitaka ikamilike lini?” “Leo.” Akamjibu akimtizama machoni kumuonyesha uzito wa kazi yake. “Nimeelewa. Ifikapo jioni nitakuwa na taarifa kamili. Lazima nikamchukue muhandisi wetu, aje apaangalie na yeye, atengeneze ramani yake. Ndipo nitawasiliana na wewe.” Akaondoka Colins akiwa ameridhika hilo limekaa sawa.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi nyumbani kwa wazazi. Akamwambia msichana anayesaidia kazi hapo. “Nikusanyie nguo zangu zote. Safi na chafu, ulete nyumbani, sasahivi.” “Sawa.” Akakubali akiwa na mshangao. “Na huruhusiwi tena, kufika pale kufanya jambo lolote. Nashukuru kwa kila msaada uliokuwa ukinipa wewe na Jose, lakini kuanzia sasa, nyinyi mtabaki mkisaidia wazazi tu. Pale kwangu hamruhusiwi tena kufika. Mwenye shida na mimi atanipata kwa simu. Na hata chakula ukiwa unapika, usinihesabie tena.” Fau akabaki na mshangao ila akaondoka. Wakati msichana wa kazi akifanya hivyo na yeye akaanza kukusanya vitu vyake vyote kama anayehama mji. Akahamishia kila kitu nyumbani kwake, ndipo akarudi kazini.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ni nini anapanga kufanya? 

Je, Jelini ameweza kumtoroka Kasa? 

Je, Kasa ndio amemalizana na Jelini?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment