Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 45. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 45.

 Vai alishushwa na Victor nje ya hosteli yao ikiwa bado mapema tu. Akatembea cheko limemjaa. Victor alimpa pesa ya nguvu, bado vitu alivyonunua walipokuwa hotelini. Akawa amelala masikini ameamka tajiri.

Jini Likujualo Halikuli Likakwisha.

Bado ilikuwa mapema tu, ndio wanafunzi wengine wakijiandaa kwa siku ya shule. Akamkuta Belinda na Fei ni kama wanamsubiria chumbani kwake. Alikuwa ameshika mizigo aliyotoka nayo hotelini. Roho ikazidi kumuuma Belinda akijua hiyo yote ni pesa ya Victor maana ingeingia mfukoni kwake na si kwa Vai. Akawasalimia akiweka mizigo yake kwenye kabati lake huku akiwatizama vile walivyojawa jazba.

“Kwema?” Akawauliza. “Malaya wewe! Umeona mimi nafaidi sana kurudi na vitu hosteli, ukaona umchukue mwanaume wangu. Yule boya wako alikuwa akikurudisha hapa mikono mitupu, ukaona ujitongozeshe kwa Victor, mpaka akulale wewe, aniache mimi!” “Belinda umekasirika, unatukana bila sababu.” “Kwani uongo?” Akadakia Fei. “Tafadhali sana Belinda. Usimuite Bale boya. Hausiki katika hili. Na Victor si mtoto mdogo wa kushawishika na mtu mgeni kama mimi. Nafikiri anajua analolifanya.” Vile Vai alivyomalizia tu kusema hivyo, wakamvamia na kuanza kumpiga.

Matusi huku wakimpiga sana. “Na tutakukomesha na hiyo sura inayokupa wazimu.” Vibao na ngumi za usoni vikaanza, ndipo ikabidi Vai asalimu amri, apige magoti na kuficha sura. Akashindwa kujibu mashambulizi. Aliyekuwa akilala naye aliporudi na kukuta hiyo hali na kushindwa kuamualia, akakimbilia nyumbani kwa matron maana wengine walikuwa wakishangilia nje ya mlango. Mpaka matron anafika pale, Vai alikuwa amepokea kipigo cha paka mwizi.

Alikuwa akilia na kutema damu. Na vile alivyokuwa mweupe, basi uso ulishavilia damu wala si kuwa mwekundu. Alikuwa akilia matron akashindwa kujua damu zinapotokea, ila akaamuru achukuliwe apelekwe hapohapo hospitali ya Muhimbili kwa madaktari wakamuangalie. Vai akatolewa hapo akilia kwa uchungu wa maumivu na kudhalilishwa. Ilibidi wamvalishe nguo maana alizokuwa nazo walimchania kwa makusudi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Hapohapo matron akampigia simu mwalimu wa nidhamu kuripoti tukio zima. Akaambiwa kitaitishwa kikao cha dharula. Belinda machozi. Akajua mpaka hapo hana chuo. Maana katika moja ya sheria za chuo chao ilikuwa kupigana au kumpiga mtu ni kosa la nidhamu. Moja kwa moja akajua hakuna msamaha, ila kuadhibiwa. Zaidi kusimamishwa chuo.

Anarudije kwao, nakusema amefukuzwa chuo sababu ya kupigania mwanaume wakati nyumbani anaye mchumba aliyekwisha toa mpaka mahari inasubiriwa tu ndoa! Fei naye machozi. Ushabiki na kupenda kula vya bure vimemponza. Nia yao ilikuwa kumpiga Vai, kama kumtia adabu, basi. Hawakujua kama atalia vile na mwenzie kwenda kumuita matron. Maji yakawa yameshamwagika.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Huku kwa Vai yeye akasubiria kumuona daktari. Wakamuangalia vizuri tu, hapakuwa na madhara ya ndani isipokuwa hayo ya nje yaliyokuwa yakionekana. Akapewa mapumziko ya siku saba. Akarudi nayo kwa matron ndipo akaambiwa asubiri atatakiwa kwenye kikao cha walimu hapo chuoni.

Baada ya muda wote wakaitwa kikaoni. Vai akiwa na ushahidi wake wakutosha, muonekano wake wa kipigo. Hakuongea sana ila tu kusema walimvamia na kumpiga. Uso ulikuwa umevilia damu. Kina Belinda walikuwa wakilia sana na kuomba msamaha. Wakasimamishwa chuo kwa miezi 6 na kutakiwa wakirudi, warudi na wazazi. Kwa maana nyingine, huo muhula mzima watakosa shule. Ni kama wanarudia mwaka tu. Ukawa uchungu wa kupitiliza. Wakatakiwa kuondoka chuoni.

Usitukane Wakunga, Na uzazi ungalipo.

Vai akaruhusiwa kurudi bwenini, lakini akaogopa hao waliofukuzwa chuo wasije mfanyia kitu kibaya cha kumuaga, na aibu. Akarudi chumbani kwake akachukua vitu vyake muhimu na kutoka hapo na kwenda kutafuta sehemu, akakaa akiwaza. Anakwenda wapi? Kwao asingethubutu kurudi. Maana aliahidi kubadilika ndio akarudishwa chuo. Sasa anarudije na majeraha ya ugomvi wa mwanaume! Hathubutu.

Kwa Bale, aibu. Aliondoka kwa nguvu zote, asijue Belinda alishamwambia yupo na mwanaume hotelini. Akabaki amekaa nje tu hapohapo Muhimbili, hajui pakwenda.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa upande wa Belinda yeye akajifariji, akijua Felix yupo tu. Yeye mtakuja wake. Hata amfanye nini, alishamdhibiti, hana pakwenda. Japokuwa ni kama hawakuwa kwenye maelewano naye tokea walipotoka kwenye chakula cha mwisho cha usiku walichokaribishwa na Victor. Walitoka hapo hotelini na Felix akimfanyia atitude za aina yake. Huwa wakati wote Felix humbembeleza sana. Si ni nyumba ndogo yake! Basi hupewa mapenzi zaidi ya mkewe. Basi humfanyia Felix vitimbwi vya namna yake.

Belinda ni mzuri. Anajiamini. Hata Victor kumkataa alimshangaza kidogo. Ila akajua ni kuongeza tu nguvu. Na akajua tatizo ni Felix. Akiachana naye, Victor anaweza mfikiria. Ndio akawa anamfanyia Felix visa, ilimradi tu amuache lakini naye Felix akawa mtulivu kwake. Hata usiku ule walipotoka hotelini baada ya kushindwa kula na kina Victor na Vai, bado Felix alimtaka arudi naye kwenye chumba walichokuwa wamepangisha, wakazungumze, lakini Belinda akamkatalia, tena kwa kumtusi haswa, akarudi zake hosteli. Hakupokea simu zake wala kujibu jumbe zake tena. Ndio ukawa mpango wa kumuacha moja kwa moja ili Victor asijemkataa kwa sababu ya kusema ni shemeji.

Kwa hiyo hapo wamefukuzwa chuo, akamtuliza Fei. “Usijali. Twende kwangu. Tukajipange vizuri. Tunaweza kuishi wote hapo kwenye hicho kijinyumba. Si pakubwa. Maana ni chumba kimoja na sebule, jiko, choo na bafu vipo humohumo ndani. Tena unaweza hata usirudi kwenu mpaka baada ya hiyo miezi 6, tukaishi wote. Muda ukifika wakurudi chuo tutatafuta wazazi wa bandia, tutawaleta.” Wakaanza kutiana moyo na kupambana. Hofu ikaisha.

 Ukaanza ushabiki na kushangilia. Wenzao wanarudi kwa mapumziko, wakawakuta wamejawa furaha, mabingwa wao. Hawajali tena. Na neno lao ni, “Hatucheki na kima sisi. Ukileta ujinga, tunakuchapa mpaka unakimbia chuo wewe mwenyewe.” Wakazidi kumsema Vai ambaye ndiye aliyetakiwa kuwepo hapo, lakini ameondoka kwa kuwaogopa wao.

Fujo zilipozidi, matron akafika hapo kuwaambia waondoke. Wakakusanya vilivyo vyao. Wakaita taksii, wakapandisha mizigo yao wakishangilia kwelikweli. Wanachuo wengine wakiwaangalia tu na wapambe wengine kuwashabikia.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Safari ya Mkwajuni ikaanza. Mipango mingi. Fei na Belinda wakipokezana maneno kwelikweli humo ndani ya gari. Cheko limewajaa mpaka wakafikishwa. Wakashushiwa mizigo yao, wakamlipa mwenye taksii, akaondoka.

Belinda akatoa funguo zake za nyumba. Kila alipojaribu kufungua, ikawa hapafunguki. Akahangaika wee, mwishoe akaamua sasa kumpigia simu Felix. “Umenikumbuka mrembo?” Felix akaanza kwa kebehi. “Mbona milango haifunguki!?” “Milango gani tena!?” “Acha ufala Victor! Si hapa Mkwajuni?” Akamsikia anaanza kucheka. “Wewe vipi Victor?!” “Fala kaishiwa. Fala mwanaume suruali, kashindwa kumiliki nyumba mbili. Kaachia wenye visu vikali wale nyama. Fala karudi kwa mkewe bwege.” Hayo yote yalikuwa matusi ya Belinda kwa Felix kila wanapokwaruzana. Lakini huwa hujishusha. Anabembeleza nyumba ndogo. Anapewa penzi, anatulia. Lakini safari hii bubu kasema!

“Umeelewa mrembo?” “Sasa kwa nini unaparudisha bila kuniambia? Pengine ningelipia mimi mwenyewe kwa pesa yangu!” “Wala usianze matusi yako ya nguoni. Bado mwenye nyumba hajapata mtu. Hiyo nyumba nimeirudisha juzi tu nilipokuwa nikikupigia simu, hupokei.” “Sasa si nilikuwa naumwa!” “Basi maadamu sasahivi ni mzima, na pesa unayo, nenda kamlipe mwenye nyumba, muandikishane mkataba mpya.” Akaendelea taratibu tu bila jazba.

“Na hapa kwangu usipige tena. Maana sasahivi nitakuwa na yule bwege wangu. Na kama unavyomjua, kanishika masikio, na simu nitampa kabisaa. Sasa sitaki fujo kwa mke wangu. Hana matusi kama wewe, usimvuruge mama watoto wangu. Ukijichanganya tu na kunipigia, ujue na mimi nampigia yule mwanamme wako uliyenidanganya ulimuacha, kumbe maandalizi ya harusi yanaendelea. Nitajitambulisha kwa kina na picha zetu zote namtumia yeye na baba yako mzazi aliyekula mahari yake.” Belinda akashituka sana.

“Wanakudanganya Felix. Mimi yule mwanaume nilisha…” “Hayo hayanihusu tena. Ukimya wako na jeuri yako ndio vilinifanya kukuchunguza kwa kina. Ndio nikajua wewe tapeli tu. Unanibana mimi kwa mke wangu, kumbe wewe unafaidi kotekote! Sasa nakuonya. Ukinianza, ujue nakumaliza Belinda. Habari zako zote ninazo. Na kama ulikuwa ukimpigia mahesabu Victor, andika maumivu. Hutampata Victor. Labda iwe sio mimi niliye kutambulisha kwake. Sasa usinijaribu. Ukimtibua tu mke wangu, au kumtafuta ili kumjaza maneno ya kipuuzi kama kawaida yako, jua mjini na kijijini kwenu, utapaona pachungu. NISIKUSIKIE. Tafuta soko kwengine. Ila si kwa wanaume wa hapa Bandari ninakofanya kazi mimi.” Simu ikakatwa. Huo ukawa mwisho wa Felix. Cha mtu mavi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Vai akabaki akiwaza bila jibu. Joto la nje na maumivu, vikamshinda. Akamtumia ujumbe Bale. ‘Nimekwama. Nina shida. Naomba msaada wako.’ Akatuma huo ujumbe na kusubiria. Ilikuwa tayari mida ya saa saba mchana. Akasubiri bila jibu. Akakata tamaa akijua Bale amemkasirikia. Akabaki akichungulia simu kuona kama hata amesoma!

Ilipofika saa 8 akaona Bale anampigia. “Kwema?” “Uliniruhusu muda na wakati wowote nikiwa na shida nikutafute, Bale. Hiyo ahadi bado ipo?” Bale hakujibu, kukawa na ukimya kidogo. Wasiwasi ukazidi kumuingia. Akajua ameshanyea kambi. Bale hambabaikii tena kama zamani. “Kama upo na mambo mengi basi. Lakini nilikuwa nimekwama. Naomba msaada wako.” “Hamna shida. Kuna ujumbe umeingia sasahivi ndio nilikuwa nikiusoma wakati ukizungumza. Ulitaka nini?” “Unihifadhi kwa muda wakati nikijiuguza. Siwezi kurudi nyumbani.” Bale akashituka kidogo.

“Unaumwa nini?!” “Ni maumivu tu. Nimepewa mapumziko ya siku saba ndipo nirudi chuo. Sina pakwenda Bale. Vinginevyo nisingekusumbua.” “Hunisumbui hata kidogo. Unajua kama ingekuwa amri yangu, au kupenda kwangu, ungekuwepo hapa kila siku Vai.” Vai akatulia. “Upo wapi nikufuate?” “Sitaki kukusumbua. Wewe ukiniruhusu, mimi nitakuja tu mwenyewe.” “Tokea lini imeanza kuwa usumbufu?!” Kimya, lakini hilo swali likamfariji.

“Eti Vai? Kuna ishara yeyote nimeshawahi kukuonyesha kuwa unanisumbua?” “Hapana Bale. Nahisi ni kujishuku tu. Na kuona sistahili tena.” “Si kwangu. Na nilishakwambia, kidogo nilicho nacho, sitakuwa na shida kugawana na wewe. Hiyo ni mpaka muda wangu. Usijali. Niambie ulipo nitakufuata.” “Nipo hosteli. Lakini sio pale. Nimekaa upande wa huku kwenye daladala.” “Basi nakuja. Sitachelewa.” “Nakushukuru Bale. Asante.” “Usijali.” Bale akatoka kwa haraka kumuwahi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Alishituka sana kumuona vile alivyo. Ila akajua ni kipigo, hakutaka kumuuliza sana. Maana ni kweli Vai alijawa fedheha. “Pole sana.” “Asante.” Bale akasubiri alipokaa sawa kitini na kufunga mkanda, akaondoa gari. “Umekunywa dawa ya maumivu?” “Ndiyo.” Bale akabaki akijiuliza huku akiumia moyoni. Moja kwa moja akajua ni Victor ndiye aliyempiga.

Baada ya muda akamwangalia, akagundua ametulia tu, hajalala. “Nimefurahi umenipigia Vai. Nilishakuwa na hamu na wewe!” Akashindwa kujibu hata kumtizama, akanyamaza tu. Bale akaamua kumuacha. Akaendesha mpaka kwake. Akafungua mlango, akamkaribisha.

Akaingia, Bale akafunga mlango. “Sijaweza kula wala kupika tokea uondoke. Niambie unahamu ya kula nini, nipike tule.” Vai alishangaa, akamwangalia na kushindwa kujibu. Alitisha usoni. Akaweka mkoba wake kwenye kochi na kuelekea chooni. Bale akaelekea jikoni na kuanza kutayarisha nyama ya mifupa kwa ajili ya supu.

Vai akamfuata. “Nikusaidie nini?” Bale akamtizama akiendelea kukatia kitunguu kwenye yale mafupa na minofu baadhi. “Natengeneza supu ya harakaharaka. Nachanganya kila kitu humohumo. Hamna chakusaidia.” Bale akamjibu akiendelea kukatia na kitunguu swaumu vipande vidogovidogo bila kutwanga. Kimya kwa muda.

Bale akamtizama pale alipokuwa amesimama kama mgeni na kuendelea na hoho. Kimya. Taratibu kama anayejiiba, akatafuta mahali pakukaa hapo jikoni. Ni jiko la ndani. Pasafi sana. Na wawili hao kukaa jikoni pamoja ni kawaida yao. Na mpishi wakati wote ni Bale. Pakazuka ukimya kwa muda, Bale akifanya yake mpaka akabandika kwenye jiko la gesi la sahani 4.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Zamani jumbe zangu ulikuwa ukinijibu kwa haraka, Bale! Leo mpaka nikaingiwa na wasiwasi! Umenichukia?” Ikawa kama analalamika. “Kwa nini ufikiri hivyo?” “Pengine vile nilivyoondoka!” “Na kwenda kwa Victor?” Vai alishituka, mpaka mate yakapitia njia ya hewa. Akaanza kukohoa mfululizo. Akampa maji. Baada ya muda akatulia. Bale kimya akimtizama.

“Alikuwa na mke na watoto wawili. Ila wametengana na mkewe.” Ikawa kama anayejitetea. “Kwa hiyo ni kama vile ulivyokuwa ukitamani? Kupata mwanaume mwenye watoto tayari?” Bale akamuuliza. Akashindwa kujibu kwa muda kama ambaye anafikiria.

“Ila nafikiri sikufikiria vizuri. Niliharakisha.” Bale akamtizama akiendelea kusafisha pale alipokuwa akitumia. “Sidhani kama nitaendelea naye.” Akaongeza. Bale kimya, hakumjibu.

“Kwa hiyo kumbe ni kweli umenikasirikia Bale!?” “Kukasirika? Hapana. Kuumia? Ndiyo. Najiambia kama na mimi pengine ningekuwa na uwezo kama wake, pengine usingeniacha Vai!” Akaumia sana.

“Mungu wangu ni shahidi sijamfuata Victor kwa sababu ya hela. Nilimfahamu kupitia Belinda. Akaniambia alikuwa akinifuatilia muda mrefu ila Belinda alikuwa akimzungusha akimwambia nipo kwako. Lakini yeye hakukata tamaa maana alijua ni kama Belinda alikuwa akimbania. Belinda alikuwa akimtaka yeye, mimi sijui. Kwa hiyo ndio akanipiga.” “Huko hotelini ulipokuwa naye muda wote?” Vai aliishiwa nguvu, hakutegemea.

“Aliyenipiga sio Victor! Ni Belinda na Fei ndio walinipiga. Belinda akidai nimemchukulia mwanaume wake. Victor hajanipiga.” “Pole.” “Sasa wewe umejuaje!?” “Alinitaarifu Belinda.” Vai hakutegemea. “Kwamba Belinda ndiye aliyekutafuta mwenyewe!?” “Nakuniambia umejifungia hotelini na mume wa mtu.” Vai alitamani kugeuka upepo. “Kwanza sikuamini! Kwa sababu wewe mwenyewe uliniambia maisha anayoishi Belinda huyapendi. Hutaki kuwa na mahusiano na mume wa mtu. Sasa kuja kusikia upo hotelini na mume wa mtu! Nikahisi kuna kudanganywa. Ila sasa ndio nimeamini uliponiambia wewe mwenyewe.” Vai akawa kama hajamuelewa.

“Si umesema ni kweli ni mume wa mtu na ana watoto naye wawili?” “Lakini wametengana!” Bale akamtizama kwa kumsuta. “Mimi ndivyo alivyoniambia.” “Vai! Kwamba wewe unafikiri kuna ndoa isiyo na matatizo?” Kimya. “Kwamba watu wakitengana kwa matatizo yao ya ndoa ndio tuseme wameachana? Ruksa kutembea nje ya ndoa!” Kimya. “Wewe unajua ni kwa muda gani Victor ametengana na mkewe?” “Ameniambia muda mrefu.” “Sasa kama amekusudia kuendelea na maisha yake, ni kwa nini hajamuacha mkewe ramsi kwa talaka?” “Amesema sababu ya watoto.” “Kwa hiyo unakubaliana na mimi kuwa bado ipo ndoa?” Kimya.

Bale akaondoka hapo jikoni kuelekea chumbani kwake. Akiwa chumbani akamsikia Vai nje ya mlango. “Unakumbuka nilisema nahisi niliharakisha?” Bale akafungua mlango kumchungulia akiwa ametoa shati. “Ulikuwa na haraka ya wapi?” “Hata sijui Bale! Sijui nilipatwa na nini!” “Ulitumia kinga?” Kimya. Bale akashangaa sana. “Kwamba wewe ulimuamini tu kwa maneno yake, ukalala naye bila hata kinga!?” “Hapo ndipo nilipokosea Bale. Mimi ni mtu wako, naomba usini…” “Mimi ndivyo nilivyodhani, mpaka ulipoondoka hapa, ukiniacha bila huruma. Ukijua mimi ni mpweke Vai! Nakutegemea wewe kwenye kila kitu! Ukaondoka, na kukimbilia kwa Victor. Inamaana kama isingekuwa kina Belinda kukuumiza inamaana leo nisingekusikia Vai!”

“Ila ujue niliondoka kwa sababu nakufikiria wewe Bale.” “Nilikwambia unizalie mtoto?” Kimya. “Eti Vai?” “Hata nikikwambia hutanielewa Bale. Bora ubakie ukinichukia tu kama itasaidia.” “Mimi sikuchukii hata kidogo.” Bale akarudi ndani na kufunga mlango. “Ila ni nini?” “Nimekwambia nimeumia.” Akajibu akiwa ndani. Kisha akafungua mlango.

“Nimeumia kwa kudhani mimi ni mtu wako, kama ulivyosema. Kumbe sivyo. Unaweza kuondoka hapa muda na wakati wowote na nisiwe na chakufanya. Na kingine, nimeumia nikidhani nakufahamu Vai, kumbe sikufahamu. Unaweza ukafanya kinyume na ulichopinga na ukawa sawa tu. Maana Vai niliyemfahamu mimi, asingeweza kujifungia na mume wa mtu kwa siku zote hizo na akawa sawa, kiasi cha kutetea. Vai niliyemfahamu mimi asingeniacha mpweke, hata iweje.” “Niliondoka kwa ajili yako Bale! Mbona hilo unakataa kuamini?!” “Lipi? Maana mpaka sasa sijui niamini nini Vai! Sijui.” Akaegemea mlango, Bale akarudi ndani kumalizia kubadili nguo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akatoka akiwa amebadili nguo. Akiwa na Vai huwa huru kuvaa pensi, mguu wake nusu akiuacha wazi tu bila shida. Akampita hapo mlangoni na kuelekea jikoni kuongeza sasa maji yakutoshea supu. “Sasa kama ulitaka nibakie mbona hata hukuning’ang’aniza nibaki?” Bale akatulia. “Maana kama kweli unayosema ni kweli, mimi ningekuwa wewe kwanza nisingekuruhusu uondoke, Bale. Lakini wewe mpaka ulinisindikiza! Na wala hata hukunipigia simu au hata ujumbe kama kawaida yako ukitaka nilale salama na kujua niliamkaje! Mimi nikajua hunitaki tena hapa kwako.” “Vai unataka kunitupia lawama mimi bure tu.” Hapo akaanza kulia.

“Ningekua hapa kwako, nikijua wewe upo sasa ningeendaje kwa Victor?” Bale kimya. “Ulinirudisha chuo na kuniacha Bale, mimi nikiwa nimekwambia hofu yangu na sababu ya kuondoka. Ila wewe ukasema huko ninapokwenda mimi ni zaidi ya kumpa mtu watoto na mambo yako mengine uliyoniambia. Ila hukutaka hata kunibembeleza nibaki! Nikaenda nilikojua natakiwa.” Akaendela kulia.

“Victor alinipokea na kuniambia hana neno hata kama sitazaa. Akawa kama amejibu hofu yangu. Ndio ikawa kila analoniambia mimi naamini tu, nikijua pengine Mungu amenijibu. Na yeye nilimwambia nimeondoka kwako nikiumia sana, kwa kuwa sizai!” “Naomba utulie Vai. Utazidi kujiumiza.” Akaondoka hapo kurudi bafuni.

Ikawa zamu ya Bale kumfuata. Vai ndani chooni, Bale nje ya mlango. “Nahisi siku ile nilipaniki Vai. Hata Joshua nilimwambia. Nikajua ni katika muendelezo wa Mungu kuniadhibu ndio maana anakutoa kwangu. Ndio maana nikabakia mnyonge, nisijue chakufanya.” Kimya. “Njoo nikwambie habari njema.” Baada ya muda kidogo Vai akatoka. Akamshika mkono mpaka sebuleni, akamfanya akae pembeni yake.

“Unakumbuka ulinisaidia kumuomba Mungu nipate kazi na kunihimiza kuchukua hatua ya kutafuta?” Akatingisha kukubali. “Joshua amenitafutia kazi benki. Nilipomuamba awaambie wasubiri mpaka nipate mguu, akaniambia huo mguu utakutana na baraka zangu mbele ya safari. Natakiwa nijiandae kwa usahili, sio kusubiria mguu. Akaniandaa kiakili. Sasa jana nilikwenda kwa hatua ya kwanza ya mtihani wa kuandika. Ila kwenye kompyuta. Haikuwa mbaya sana. Jioni wakanipigia kunipa majibu, na kuniambia natakiwa kwa hatua ya pili. Usahili wa mahojiano.”

“Ndio leo asubuhi nikaenda. Aisee wale watu wanauliza maswali! Uzuri Joshua aliniambia nisiogope kutumia biashara zangu za nyuma kama kigezo. Akaniambia na Naya alitumia biashara alizofanya nyuma mpaka alipokuwa kazini, ikamuongezea sana sifa. Nisiache kuwaambia changamato na jinsi nilivyoweza kupambana nazo nakubakia kwenye soko kwa muda mrefu. Aisee ilinisaidia sana. Kila swali walilokuwa wakiniuliza, ilinisaidia kujibu kwa ufasaha. Mwishoe wakaniambia wanamtu mwingine wanamfanyia usahili, wakimaliza, watanijulisha kujua kama nimepata nafasi au nijaribu wakati mwingine.”

“Sasa uliponitumia ujumbe, sikuona. Nilikuwa katikati ya mawasiliano, nikisoma email au barua pepe zao za ukaribisho na hatua zinayofuata.” “Hongera Bale. Subira imevuta heri.” “Mambo mawili nataka kukwambia. Moja, sikukujibu kwa haraka kwa sababu nilikuwa nikisoma jumbe zao na pia nilikuwa katikati ya mawasiliano na Joshua. Kumjulisha kupata hiyo nafasi ya kazi. Kumbe Joshua alishataarifiwa kabla yangu kuwa ningepewa ile nafasi. Walivutiwa na mimi tokea kwenye usahili. Lakini kisheria au kwa kanuni za kampuni ilikuwa lazima na yule mwingine apewe nafasi ya usahili. Ndio maana sikufikia ujumbe wako kwa wakati. Umeridhika?” Vai akatabasamu na kunyamaza. Akamuona, akajua ameridhika.

Chapili. Hiki alichonifanyia Joshua, angenifanyia muda mrefu sana, lakini nilikosa subira. Kama wakati ule ningesubiri kama nilivyofanya safari hii, nakwambia ukweli Vai, si Malon, baba, mdogo wangu wala wale wengineo niliosababisha vifo vyao wangekuwa wamekufa. Haraka zangu zimenifikisha hapa nilipo nikiwa mpweke na mlemavu.” Vai akaumia sana.

“Na Naya aliniambia na kunisihi sana niwe mvumilivu. Nimpe nafasi Joshua. Huwa hafanyi mambo yake kwa pupa. Lakini sikutaka kumsubiri Joshua. Nilikuwa na haraka. Nafikiri pia kutaka kushindana na baba, kulishanipa laana tokea yupo hai. Nikakimbilia kwa Malon, mengine yote ni historia.”

“Ndio maana wakati ule uliponishauri nijaribu kutafuta kazi, nilikuwa nikisita sana.” “Nilikuona. Na ni kama uliingiwa hofu sana, mimi nikashangaa, ndio maana ukaona niliacha kukuhimiza kutafuta kazi. Ulikuwa ukibadilika mpaka sura!” “Joshua ni mtu mkubwa sana. Anafahamiana au kuzungukwa na watu waliofanikiwa sana hapa nchini. Ni kiasi cha kunyanyua simu tu kama hivi, nikapewa nafasi. Sasa ule ukimya wote huku akinilisha kama mtoto mdogo, nikajua Naya yupo sahihi. Anataka kunichunguza, ili akiniweka mahali, nisiharibu, akalaumiwa yeye. Na nakwambia ukweli Vai, angemtafutia kazi Bale wa wakati ule, ningeharibu vibaya sana.”

“Nilijawa kiburi mno. Lakini sasahivi maisha yamenifundisha, hata yeye leo ameniambia nipo tayari kwa ofisi yeyote. Ameniambia anashuhudiwa moyoni, hakuna ofisi nitapewa, nitashindwa kuitumia ipasavyo.” “Kweli Bale!?” “Hakika Vai. Mpaka machozi yalinitoka kumsikia Joshua akisema hivyo. Na usifikiri amenitafutia nafasi ndogo au hizi benki za kawaida! Kubwa na pesa yao ni kubwa mno. Marupurupu kibao. Ukipona macho nitakupa usome uone Mungu alivyotujibu.” “Hongera Bale.” “Asante. Acha nikaangalie supu.” Akasimama, na yeye akamfuata.

Akamuona anaongeza maji na kuchukua simu yake. “Unaanza lini kazi?” Akamuangalia na kumuona anaandika. Akatulia akimsubiria. Akamaliza na kuweka simu pembeni. “Nilikuwa nikimtaarifu Joshua kuwa umerudi.” Vai alishituka. “Bale!” “Sina mtu mwingine mbali na wewe na yeye, Vai. Uliniacha. Ukaondoka. Nilikuwa siwezi hata kutoka kitandani.” “Bale!” “Sikudanganyi Vai. Hii nyama kama ningekuonyesha kabla sijaiweka jikoni, ungekumbuka tulinunua wote. Sijapika wala kula tokea uondoke. Yaani jana na leo imenibidi ninywe chai ya rangi ili niweze kufikiria.”

“Uliondoka gafla tukiwa na wakati mzuri mno Vai. Amani na utulivu wa namna yake. Hatukuwahi kugombana hata mara moja! Halafu ukaondoka gafla tu!Nilikuwa sijui chakufanya! Kutoka kwenye kuniokota, ukawa mtu wangu. Mchana hadi mchana tupo wote. Gafla unaondoka, halafu naambiwa yupo Victor amefanikiwa kukufungia hotelini. Na wewe umetulia naye! Kweli wewe unafikiri ningejisikiaje?” Vai akatulia.

Ukweli Mchungu.

“Nenda akajipumzishe kwenye kochi. Supu ikiwa tayari nitakuletea.” “Nataka tukae wote.” Bale akacheka akimtizama. “Na mimi nilikumisi Bale. Usifikiri ndio nilikuwa nafurahia kuwa mbali na wewe. Mpaka  nilikuwa nikitamani Victor ndio angekuwa wewe!” Bale akanyamaza.

“Mimi sio muongo Bale. Ila ni binadamu. Nimekosea. Sijakudanganya. Ila nimekosa. Nikiomba tuanze tena urafiki wetu utakubali?” “Kwa makubaliano yepi?” “Yeyote yale. Ila safari hii sitakimbilia tena mume wa mtu. Nitatulia kabisa.” “Na ukajiangalie afya yako.” Hapo Vai akapoa.

“Mwenzio haraka zimenipa kilema cha maisha. Ila wewe nakuombea usipate gonjwa la kudumu.” “Nimeingiwa hofu Bale!” “Lazima. Huyu Victor humfahamu. Umesikia na kuelewa kile ulichotaka kukisikia wewe. Ukapime. Na kama hujaathirika, iwe fundisho Vai. Tafadhali jifunze. Na hapa nitakwambia ukweli.” “Sio usubiri nipone kwanza!” “Ukiondoka kabla hujapona! Maana wewe hutabiriki.” “Bale! Si nimesema siondoki tena?”

“Hapana Vai. Tafadhali nisikilize. Unaonekana wewe swala la kinga unapuuzia sana Vai. Kwa hapo ulipo, ningetegemea ungekuwa makini sana na kinga. Umekuwa ukishika mimba hovyo tokea mdogo.” Vai hakutegemea! Akamtizama kwa kumshangaa kwa uchungu, na kunyamaza akiangalia chini. “Mimi nakwambia ukweli Vai, na usichukie. Madhara ya kutokutumia kinga, ukapata mimba ambazo hukuwa ukipanga, kasoro moja nafikiri! Ambayo kama nitakumbuka sawasawa ilikuwa ya yule aliyekuwa mume wa mtu.” “Sikuwa nimejua! Yeye alinidanganya.” Akajitetea.

“Sawasawa. Lakini ukiwa hata humfahamu vizuri! Si mchumba wala mume! Kama tu huyu Victor uliyekuwa ukimtetea hapa. Ukajiachia mpaka kushika mimba iliyokuachia majuto mpaka leo. Hofu na huzuni inayokutesa mpaka sasa. Sikutarajia kama na kwa Victor naye ungekimbilia kitandani bila KINGA!” Vai akamwangalia kwa kuumia sana.

“Acha mimi niwe Joshua wako. Usipokubali makosa. Ukajifunza kwayo. Hakika hutatoka hapo Vai, na madhara yatakayozidi kukupata mbeleni ni makubwa zaidi ya unavyofikiria hata sasa nikizungumza hapa na wewe. Mwenzio Joshua alikuwa akinipa ukweli uliokuwa msaada kwangu japo ulikuwa ukiniuma sana. Nilikubali makosa, nikatubia mbele ya Mungu na kwa niliyeweza kumfikia. Joshua. Ndipo nikaanza kujifunza jinsi yakusubiri. Wewe ni shahidi. Sijakimbia japo kwangu ilikuwa ngumu mno mwanzoni. Mpaka baadaye na wewe ukaja. Ukaongeza tabia nyingene ambazo hata sikuwa nazo! Ikafanyika rahisi KUSUBIRI. Nimesimama hapahapa mpaka majibu yangu yamenikuta. Barua yangu aliyotumwa malaika na Mungu aniletee, imenikuta pale nilipokuwa nikimsubiria Mungu wangu. Leo Mungu amenipa kazi nzuri sana. Na amenirudishia WEWE. Na yote hayo ni Joshua.”

“Alinipigia simu nikiwa siwezi hata kutoka kitandani, kwa uchungu wa kuniacha. Akazungumza sana na mimi na kuniambia sina chakupoteza kwenye maombi. Nikiwa nina hofu. Maana ni kama Belinda aliniambia Victor anayo pesa. Aina ya hoteli mliyokuwepo, hata mimi na wewe hatujawahi kufika huko! Nikajihisi kipanzi mbele yake. Lakini nikawa kama alichonifundisha Joshua. Nikamwambia Mungu mpaka hofu yangu. Na nikamwambia sijui chakufanya. Naogopa. Nimebaki peke yangu. Nahisi akanihurumia. Ndio amenipa kazi na kukurudisha na wewe.” “Sasa unajuaje kama Mungu ndiye amenirudisha na si shetani?”

“Kwenye bibilia kitabu cha Yakobo 1:17 inasema hivi, ‘Kila kitolewacho kilicho chema na kilicho kamili, hutoka juu, na hushuka kutoka kwa Baba wa mianga, ambaye kwake hakuna kubadilika, wala kivuli cha kugeukageuka.’ Shetani hawezi kutoa kitu kizuri kama wewe Vai. Akipate wapi!?” Vai akaumia sana. Akaondoka hapo kurudi sebuleni, akilia. Bale akabaki jikoni akimalizia kupika. Vai akalia mpaka akapitiwa na usingizi kwenye kochi.

 

Atafutaye Hachoki.

Ilikuwa mida ya jioni, Jelini akiwa dukani, simu ikaingia. Akaitizama, alikuwa mwanasheria wa Kasa, akajua tu ametumwa na mzee. Akapokea. “Halo.” Akaitika Jelini. “Mbona umepotea Jelini bwana! Nakusaka kama shilingi ya mkoloni!” “Nipo. Kichwa kilikuwa kikiniuma sana, nikaamua kupumzika kwanza. Kwema?” “Pole sana. Unaendeleaje lakini?” “Sio mbaya sana. Nashukuru.” “Nimekwama mambo kama mawili matatu, nahitaji kukuona ili tuweke muongozo.” “Hatuwezi kuzungumza tu kwenye simu? Mimi siku hizi nina kazi. Ndio nimeanza tu, sitaki kuanza kumangamanga mida ya kazi.” Akasikia kimya.

“Ndosi?” “Nipo Jelini. Unanafasi muda gani naweza kutuma dereva akaja kukuchukua, na kukurudisha.” Akajua wazi anayezungumza hapo ni Kasa, ila hakujua kama yupo kwenye simu au yupo naye hapo. “Shida si usafiri, ila muda. Niambie ni nini unanitafutia kwanza ili nipime kama ni jambo naweza kuahirisha mambo mengine ili nije.” “Muda wa ile kesi ya yule mwalimu umefika. Ndio maana nilikuwa nikikutafuta sana.” Moyo wa Jelini ukashituka kama kumeanguka chuma sakafuni.

“Jelini?” “Nipo. Natakiwa kufanya nini?” “Ni maandalizi tu ya jinsi ya kujieleza mahakamani.” “Lini?” “Ijumaa hii, ndio maana nilikuwa nikikutafuta sana. Lasivyo kesi itaahirishwa tena au kufutwa kabisa endapo hutatokea siku ya mahakamani.” “Kesho ni siku nzuri kwako?” Jelini akauliza. “Ulitaka uje saa ngapi? Asubuhi nina kesi mahakamani mpaka mchana ndio nitakuwa nimerudi ofisini.” “Basi nitakuwepo hapo mida ya saa nane mchana.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usiku alipotoka na kurudi nyumbani akamfuata mama yake na kumueleza. “Nenda, mshenzi yule akahukumiwe kihalali.” Mama yake akamtia moyo. Jelini akarudi chumbani kwake kujiandaa na kesho yake akijua anakwenda ofisi za maana. Akatafuta nguo za kujiwakilisha ipasavyo, ndipo akalala.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wapi Mizani Italemea?

Jelini na yeye mlango mwingine umefunguka kama Vai. Wakati Colins analemewa na familia, Kasa anarudi kwa mlango wa nyuma.

Huku kwa Vai naye, ni Victor au Bale ambaye hajasema chochote juu ya mapenzi, wakati Victor yeye hana shida ya familia. Tayari yupo na familia yake anachohitaji starehe tu. 

Nini kitaendelea? 

Usipitwe.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment