Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 44. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 44.

Wakati akifurahia penzi hotelini, kwa Bale kulikuwa kunawaka moto tokea jana yake Belinda alipomtumia ujumbe kuwa Vai amejifungia hotelini na mwanaume. Tena akaongezea kuwa ni mume wa mtu, ametelekeza familia kwa ajili yake Vai. Kwamba Vai anatesa familia ya Victor kwa makusudi. Zilikuwa taarifa nzito kuliko kipindi anaambiwa kifo cha baba. Zikakaribia taarifa za kifo cha mama yake.

Kwamba Vai yupo na mwanaume mwingine! Ikamtesa sana Bale. Tarehe 3 kuamkia 4 ukawa ni usiku wa mkesha akijishangaa anavyoumia kana kwamba Vai ni mkewe, kumbe walishaagana na akamrudisha chuoni kabisa. Ikamuua. Siku ya tarehe nne ilimkuta kitandani amekosa hata sababu ya kutoka hapo. Akabaki ametulia tu hapo kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Kilichomkera Belinda zaidi ni majibu ya Bale pale aliposoma ujumbe wake. ‘Vai ni mtu mzima, mwenye akili timamu. Yupo huru kuchagua kama mimi na wewe. Nakushauri usiwe na wasiwasi naye, anajua anachokifanya.’ Hayo ndio yakawa majibu ya Bale kwa Belinda, baada ya kusoma ujumbe wake mrefu sana wakumchafua Vai.

Akabaki sasa kumchafua Vai hapo hostelini kwao akilia kuibiwa mwanaume na Vai aliyekaribishwa chakula cha usiku na kina Victor, tena kiungwana tu. Kwamba hawakuwa hata na nia ya kutoka naye. Ila walifanya uungwana kama kumshukuru kwa kumsaidia kubeba mizigo yake, yeye akakubali na kujitengeneza kwa kujipania kama aliyetaka kumtaga mwanaume wake!

 “Bwana Vai ni mshenzi yule mwanamke! Msiwahi kumsogeza karibu ya mwanaume wako! Mambo aliyoyafanya huko baaada ya kulewa, hamuwezi amini kama ni yeye! Alimng’ang’ania  Victor mpaka akaenda kulala naye!” Akaendelea kumchafua.

“Sasa si na Felix alikuwepo!?” Mmoja ya anayeyafahamu mahusiano yao akauliza. “Kwani nimeanza kuwapanga leo, na wewe? Tokea mwezi wa 11, wote nilikuwa nao. Niliwapanga bila shida mpaka Vai alipomchukua mwanaume wangu.” Akaendelea kulalamika mengi mpaka akapata watu upande wake. Akaonyesha uthibitisho wa pesa alizokuwa akirushiwa na Victor pamoja na Felix kwa muda mrefu tu. Mpaka wote wakaamini ni kweli Vai ameingilia mipango yake. Alikuwa akivuna kotekote na yote kumuendea sawa.

Wakamuhurumia sana Belinda. “Na tutamkomesha. Aache ushenzi wa kuibia watu mabwana zao.” Likawa azimio la Belinda na shoga yake Fei, wanalala chumba kimoja. Hawa mshabiki akichochea maana Belinda alikuwa akileta chakula, anakula naye. Maana wakati Belinda akiwa kwa Felix, Hawa anashinda na Fei chumbani kwao kwenye vitu vizuri. Shoga.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Alibaki amejilaza hapo mpaka majira ya saa nne asubuhi alipoona simu ya Joshua. Akaipokea kwa swali, bila salamu. “Hivi wewe ulijuaje kama Naya ni mkeo?” Joshua akatulia kidogo. “Joshua?” Akaita na kuitizama simu kuhakikisha alipokea kabla hajazungumza. “Mzima lakini?” “Nataka kujua.” “Niliwasimulia ilivyokuwa Bale. Na kwangu ilikuwa rahisi kupokea hisia kwake kwa sababu sikuwa nimejizoeza au nisema sikuwa nafungua mlango wa mapenzi hovyo. Haikuwahi au sikuwahi kuruhusu mambo ya wanawake kuwa udhaifu wangu na nahisi ndio maana kwangu ilikuwa rahisi nilipoletewa Naya. Niliomba Mungu anipe mke. Aliponionyesha ni yeye. Nikampokea kama zawadi iliyofungwa, na sikujua kilichokuwa kimefungwa ndani.”

“Nikaanza kufungua nikiwa nimeshapokea na kushukuru. Nikiamini kilichowekwa ndani, Mungu wangu amepima uwezo wangu, ameniamini na Naya. Na kwa kuwa najua Mungu anajua madhaifu yangu, nilijua hataniacha nikashindwa. Nina uongozi wa Roho mtakatifu. Kwa hiyo kuanzia nimempokea, najua na wewe unakumbuka mwanzo wetu. Haikuwa rahisi na nilimkuta yupo Malon, lakini kwa kuwa nilijua ni WANGU. Mungu amenipa, nilijua hatakamilika bila mimi na mimi hivyohivyo. Ndio maana sikutulia mpaka nilipohakikisha amekuwa wangu, na yupo nyumbani kwetu.”

“Na ni kwambie kabisa Bale, hangaika yangu yote, pesa yote na muda niliotumia, nikimtafuta Naya awe wangu kama Mungu alivyonipa kwa imani tu, garama yake nzima, hafikii hata chembe ya aina ya ndoa tuliyo nayo na Naya. Imekua yote yale tuliyopitia ni kwa ajili ya kututengenezea maisha mazuri tuliyo nayo sasa. Kila nikijifikiria na kujiuliza kama ningekata tu tamaa wakati ule, nikamuachia Malon. Pengine kwa akili zangu ningeoa mwanamke mwingine. Lakini nisingekuwa na aina hii ya ndoa au niseme maisha tuliyo nayo na Naya.” Wakatulia kidogo.

“Sijui kama umenielewa?” “Nafikiri, japo nina maswali, sijui niulizaje?” Joshua akatulia akimpa nafasi. “Unanafasi?” “Kidogo. Unaweza kuzungumza tu.” “Na mimi katika mabaya yangu yote kwenye maisha. Mpaka najishangaa, maswala ya wanawake shetani hakuwahi kabisa kupata nafasi kwangu. Linapofika swala la mwanamke, hata kipindi navuta bangi, halijawahi kuwa tatizo nashindwa kulishinda. Tamaa hovyo za wanawake sina. Na pia sijawahi kujiruhusu kuwa mtumwa wa mapenzi. Nafikiri pia ilichangiwa na ndoa ya wazazi wangu. Ni kama niliingiwa na hali ya kutotaka kurudia kosa. Sikutaka kuharakisha kwenye mahusiano ya kimapenzi.”

“Lakini nilipata msichana. Hatukuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi. Urafiki tu. Lakini Joshua, yule msichana ni kinyume na mimi kabisa! Nikimaanisha, kila upungufu unaouona kwangu, yeye ni kinyume. Anaridhika na SASAHIVI, wala si leo tu. Anafurahia ule wakati mlio nao wakati ule bila kuruhusu hofu ya baadaye iibe ile furaha ya wakati ule. Halafu mzuri sana.” Joshua akacheka.

“Yaani ukimpa maji ya kunywa, inakuwa kama sijui umempa kinywaji cha namna gani vile! Halafu mzuri haswa.” Joshua akatulia akimsikiliza. “Wakati tunao kuwa nao mimi na Vai, popote tunapokuwepo, hata kama ni pa hadhi ya chini sana, utafikiri ni watu ambao mambo yetu yote yapo safi sana. Kumbe yeye ni mwanafunzi tu, mimi natunzwa na wewe! Kwamba si kwamba hata tunajua kesho yetu itakuaje! Lakini hatakagi tukose raha wakati huo kwa ajili ya kesho. Analeta hali ya amani na utulivu mkubwa sana, kinyume hata na mazingira ya nilipokulia kwetu! Kile kidogo kilichokuwa kikilalamikiwa nyumbani kwetu, yeye Vai atakipa thamani mpaka unapatwa na hali ya kukitazama kitu kilekile kwa jicho la tofauti! Halafu sasa Mungu akampa uzuri wa aina yake.” Joshua akagundua swala la uzuri wake linarudiwa sana.

“Huwezi kujificha kwake, kwa kuwa hana kuhukumu. Unajisikia upo salama hata kutubu mambo mabaya unayoogopa hata mtu asifikiri nina uwezo wa kuyafanya! Na bado atakusikiliza, halafu anabaki kukutizama kama mtu wa kawaida akikukumbusha jinsi Mungu anavyosamehe. Anautulivu wa aina yake, uzuri uliochanganyika na ucheshi. Mweupe mnoo. Mweupe haswa. Ule weupe wa uzuri. Ni mzuri.” Joshua akacheka na kubaki kusikiliza kujua tatizo.

“Na mimi nikamfahamu kwa undani, nikagundua hana uwezo wa kuzaa. Aliharibu mimba nyingi sana akiwa anakua. Tukaendelea na mahusiano ya kawaida ila nafikiri kuna tulipopitiliza, hisia zikawa tofauti lakini kwa sababu nilijua yupo tu, sikutaka kuharakisha kumwambia ninachojisikia. Tukaendelea tu.”

“Sasa juzi hapa aliniuliza swali lililonifanya kujibu bila kufikiria, akaondoka. Aisee hapa panatisha bila Vai!” “Kwani mlikuwa mkiishi wote!?” Joshua akauliza. “Aisee ni kama nilikuwa nikiishi naye, ila si kimapenzi. Aliondoa upweke wote. Kuna wakati mpaka nikajua Mungu amemleta kunifariji na kuniambia amenisamehe! Maana jinsi nilivyokutana naye pia ingekuwa mtu mwingine asingekuwa na mimi. Nilimfanyia ujeuri, nikiwa nimeanguka pale hospitali ya MOI. Akaniokota na kunisaidia.” Akamsimulia mwanzo wake na Vai kwa ufupu mpaka mazungumzo yao ya mwisho, kisha Vai kuondoka hapo na ujumbe aliopata kutoka kwa Belinda shoga yake kipenzi Vai.

“Nashindwa kulala, Joshua. Chakula ndio kimenishinda kabisa tokea aondoke hapa na rafiki yake ndio amenichanganya zaidi. Vai amepata mwanaume ambaye amemwambia kile nilichoshindwa kumwambia mimi, nikijua ninao muda zaidi au simstahili. Nipo kama mgonjwa! Mpaka mazoezi naogopa kufanya nisije nikajiumiza, kwa njaa na msongo wa mawazo! Nifanyaje?” Bale akauliza akisikika kukata tamaa kabisa.

“Wewe unataka nini? Maana hilo ndilo la msingi.” “Bila kukupotezea muda zaidi, NAMTAKA Vai. Sijawahi kujisikia hivi nilivyo kwa mwanamke yeyote yule hapa duniani, Vai ndio wa kwanza. Sijali hata kama hatutapata watoto, ninachojua namtaka yeye. Maana hata wazazi wangu walikuwa na watoto wajinsia zote, lakini sijawahi hata kuwaona wakiwa na wakati mzuri kama niliokwisha kuwa nao mimi na Vai. Hakuna kilicholeta maana kwao, kama Vai alivyoleta maana kwenye maisha yangu yaliyokwisha kuwa makiwa. Namtaka Vai. Ila najihisi nimechelewa.”

 “Hilo la watoto ndio lilikuwa swali langu la pili. Maana ni bora wewe umejua mapema kuwa hazai. Mimi nilimuoa Naya, nikampokea kama alivyo, nikajua mengine Mungu atayafanya kwa wakati wake. Nilijiambia maadamu ni wangu, na kujithibitishia kuwa Mungu amenipa mimi, hakuna kitu kitasimama katikati yetu. Nitapambana kwa nguvu zangu zote bila kukata tamaa, na msaada wa Mungu, mpaka awe wangu. Mengine sikutaka kabisa kujisumbua nayo. Maana huwa namjua Mungu wangu. Ana jinsi yake yakunipa vitu. Si rahisi aisee, lakini hajawahi kunipa vitu vinyonge.” “Unamaanisha nini?”

“Wewe si unajua kuna watu wanaomba tu, Mungu anawapa vitu vikamilifu? Kama ni mwanamke, basi anakuwa binti mzuri, aliyetulia. Hata safari yao yakufunga ndoa ni kawaida kabisa. Hamna shida. Wanafunga ndoa na maisha yanaendelea bila shida mpaka watoto?” “Ndio!” Bale akaitika na kutaka aendelee.

“Au wengine wanaomba kazi. Unakuta anapewa kirahisi tu. Tena anapewa sehemu nzuri, ofisi kabisa, kazi zinaanza bila shida na mshahara unaingia bila tatizo. Si ndivyo?” “Ndio!” “Basi kwangu si wakati wote huwa inakuwa kama hivyo. Mungu huwa ananipa vitu nakunijaribu haswa. Kama ambaye anayetaka kujua kama anaweza kuniamini na hicho kitu! Ikishakuwa hivyo, najua anataka kunipa kitu kikubwa, uwezo sina, ndio ananitengeneza. Aisee hapo hutanitoa Bale. Hata kwa risasi hutanitisha. Ilimradi nijue ni changu na Mungu anataka kunipa mimi! Aisee nitapambana mpaka Mungu wangu aridhike, anikabidhi sasa kama wengine, ndio natulia, ila si kuzembea.”

“Nilikuona kwa Naya! Kumbe ndio maana umefanikiwa sana Joshua!” “Hutaniyumbisha kwenye ninalojua Mungu amekusudia kunipa mimi, Bale. Hutanitisha, hutaniogopesha. Maana hapo najua Mungu, ambaye ni Baba yangu, yupo kazini. Kila silaha itakayoinuka kinyume yangu najua kwa hakika haitafanikiwa, ni mimi tu kusimama imara, anichonge mpaka nifae kuweza kuishi na hiyo baraka anayotala kunipa. Najua natengenezwa tabia ambayo haipo ndani yangu. Nakwambia, hakuna mwanadamu atasimama katikati yangu na kusudi la Mungu kwangu, endapo Mungu mwenyewe akiamua kufanya kazi kupitia mimi. Kwa sababu wakati mwingine anapigana huko kimyakimya, ananiletea tu ushindi mikononi. Hapo najua anachonipa, anajua naweza kuishi nacho bila shida. Nipo tayari nacho.”

“Na kingine Bale. Kama nikajua kwa hakika ni Mungu ndiye anayenipa hicho kitu. Hiyo zawadi. Hata kama imefungwa vibaya, au imefungwa kwa ustadi wa hali ya juu na zile karatasi za zawadi na riboni kabisa, maadamu inatoka kwa Mungu wangu, na ananipa mimi, sinaga maswali na kuchunguzachunguza ndani nikitafuta kasoro. Huwa napokea, na kujiambia mengine yoooote, nitajua mbele ya safari. Napokea, na kutunza kwa uaminifu sana, kumuhakikishia Mungu, nimepokea kwa shukurani na nitatunza. Basi. Mengine napambana nayo mbele ya safari.”

“Aisee kumbe afadhali tumezungumza! Maana nilikuwa na hali mbaya!” “Usiache kunipigia kila unaponihitaji. Nisipopokea, ujue nitarudisha nikipata nafasi. Na usiache kumshirikisha Mungu.” “Nahisi bado ninahofu na Mungu. Nahisi bado sistahili mambo fulanifulani ndio maana nilijiambia hata kuondoka kwa Vai hapa, ni yeye Mungu alimtoa kwangu. Nikakubali aondoke nikijua ni adhabu yangu bado inaendelea.”

“Hapo ni wewe mwenyewe, ulishindwa kusimama na kutetea kile unachojua unastahili. Na pengine hukujua thamani ya ulicho nacho mpaka alipoondoka kwako na mwingine kuona thamani yake.” “Nahisi nilibweteka nikijua yupo tu.
 “Hiyo pia inawezekana. Lakini Mungu wetu hanyang’anyi kitu alichompa mtoto wake kwa upendo. Ila ujue jukumu la utunzaji ni juu yetu sisi. Anakupa baraka unayostahili, inayobaki ni juu yako wewe jinsi utakavyoitunza. Na si mara zote ni rahisi. Wewe ni shahidi wa historia yangu. Alinipa Naya, mengine akaniachia mimi mwenyewe kupambana. Hana tabia ya kumsimanga mtoto wake. Ukikosa, anakurudi, ukitubu mnaendelea kwa upendo. Ameahidi kutokukumbuka kamwe dhambi zetu. Na alinituma kukwambia bado hajamalizana na wewe. Unakumbuka?”

 “Sasa hapo sikuwa nikijua kama ni kwa wema au ubaya!” “Mungu si wa visasi Bale. Kwanza hawezi. Akikutizama wewe, anakumbuka kazi ya msalaba. Umesamehewa na kununuliwa kwa damu ya thamani sana. Kuna garama utalipa, kwa uliyokosea nyuma, kama ulivyoharibu mahusiano yako na Naya, pamoja na ndugu zenu. Ukiwa unao jisikia ni kwa sababu ya makosa ya nyuma. Lakini haitokani na adhabu ya Mungu. Mungu hakuadhibu. Lakini hata kama amekusamehe, hawezi kurudisha familia yako kama ilivyokuwa zamani. Inamaana utabaki na madhara uliyosababisha nyuma, lakini haimaanishi kila unapojisikia ukiwa ni kwa sababu Mungu anakuadhibu! Hapana. Ni kwasababu familia yako haipo tena. Ni hilo tu. Usikubali huo uongo. Na katika hiyo hali, lazima ujifunze kuishi kama uliye samehewa, ila unayewajibika na kosa lako.”

“Sijui jinsi ya kuishi hivyo Joshua! Ndio namuomba Mungu anisaidie kila siku. Naamini siku moja Naya atakuja kunisamehe. Angalau niwe nimempata yeye.” “Hilo ndilo la msingi. Hutapoteza kwenye maombi. Na hata yale unayoyaona sasahivi hayawezekaniki, muombe Mungu. Omba hekima ya jinsi ya kuenenda. Maana hutaomba tu na kusubiri. Kwenye kuwajibika, omba uongozi wa Mungu, kisha chukua hatua.” Akamuombea Bale na Vai. Akaomba kusudi la Mungu litimie kwao. Wakaagana.

Tarehe 5.

Asubuhi hiyo Colins akaamka mapema kuwahi kazini ila akapitia hospitalini kwanza kitu kilichomfurahisha hata baba yake. Alimkuta mama yale akimsaidia kumsafisha. Kwa hiyo hakukaa hata dakika 10, akaondoka. Akaingia kazini hata saa mbili haikuwa imefika. James hakuwa ameingia. Akaanza kucheza game, James anaingia, akamtizama tu na kurudisha macho kwenye kompyuta yake akiendelea kucheza.

James akamuwekea kimfuko mezani. “Mzigo wako huu kutoka kwa Jelini, nimepewa na Jema. Sina habari zake zaidi.” Colins akapokea, kufungua ndani, akakutana na simu yake aliyokuwa amempa Jelini. Akabaki akiitizama. Chini kulikuwa na bahasha ndago, imefungwa kabisa. Akaifungua.

Colins, nashukuru sana kwa msaada wa simu. Ila nimeamua nisiuze tena ile simu yangu nyingine. Kwa hiyo kwa sasa sina uhitaji tena wa simu. Naona ubakie nayo tu, kunaweza tokea uhitaji kwengine, tena muhimu, ikapata matumizi kuliko kuweka tu kitu cha thamani kama hicho. Pia nakushukuru sana kwa kuwa na mimi kipindi nilichohitaji faraja. Mungu akulipe Colins. Umenisaidia kunijenga. Isingekuwa wewe ningepoteza dira kabisa. Lakini umenikumbusha mimi ninaweza kuamua kitu na nikafanya. Nisiyumbishwe na matukio. Nashukuru. Nitasimamia hapo, na kupambana kwenda mbele, sio kurudi nyuma.

Asante.

Jelini.

Colins akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha. Akajua hiyo barua aliandika kabla hawajakutana. Akabaki ametulia tu. “Kwema?” James akamjaribu. Akamuona ameumia haswa. “Nisikilize Colins, mimi ni mtu wako, unaweza kuniambia chochote kile. Naweza nikakushauri au angalau ukapata mtu wa kuzungumza naye, ukatoa uzito kifuani, ukaweza kufikiria.”

“Nina wakati mgumu James, sikuwahi kufikiria maishani kama naweza kupita hapa.” Colins akaanza. “Tangia nazaliwa, sijawahi sikia kitu ninachojisikia kwa Jelini, na siwezi kueleza, mtu akanielewa.” “Mimi nakuelewa. Kilinipata kwa mara ya kwanza maishani, kwa Jema. Nilishindwa kuelewa mpaka ikabidi nizungumze na Geb.” “Alikusaidiaje?” “Acha kudandia gari kwa mbele, Colins! Mambo hayafanani. Sasa imekuaje?” “Love.” “Mbona kama uliniambia mlishamalizana?” “Aisee amerudi kwa kasi akitumia wazee, wala si kina mama. Wazee kabisa akijua kabisa anachokifanya, tena kwa makusudi! Mpaka ameniharibia kwa Jelini.”

“Hapo sasa si sawa Colins!” James akambadilikia. “Jelini ametoka kuumizwa na yule mzee, na wewe unaanza tena!?” “Si kuanza. Nahisi kwa mara nyingine tena, nimemuumiza Jelini. Na sidhani kama nitampata tena. Imekua mbaya kweli.” Akamsimulia kila kitu. Aina ya mahusiano ya familia walizo nazo. Jinsi walivyoishi wakikua pamoja, wazee wao wakiwa wameapishana katika shida na raha.

“Aisee nasikia kuumwa kabisa. Sikujua kama watu huwa wanaposema wanapenda, ndio hivi! Ni hisia za tofauti!” “Kwani ilikuaje na Love!?” “Love ni kama tulijikuta, tukaona inabidi. Lakini si kwamba kulianza mapenzi. Nimekua naye karibu mpaka tukajikuta tunaanza mahusiano ya kimapenzi wakati tukikua. Lakini si kwa sababu ya tulianza hisia. Na nafikiri ndio maana alikuwa akinidharau na kunitusi sana. Kwa kuwa alijikuta ni kama inambidi kuwa na mimi sababu ya mahusiano ya wazazi.”

“Subiri kwanza Colins. Matusi tena?!” “Acha James. Mpaka aibu kusema. Nina uhakika kwa asilimia 100, matusi aliyokwisha nitukana yule msichana, sitakuja kutukanwa na mwanadamu mwingine yeyote yule hapa duniani.” “Ndiyo mbaya hivyo!” “Nakwambia, nilifika mahali mpaka mimi mwenyewe nikaanza kuamini maneno yake, nikaanza kuishi kile anachonitukana. Nikaanza kuona ni kweli, ndio kama vile nilivyokwambia, nikajua napotea, si sawa. Tukahitimisha vizuri sana, na yeye akakubali vizuri, bila shida, nashangaa ananigeuka kwa kujirudi kupitia wazazi tena kina baba!”

“Mimi sijui bwana Colins! Lakini mimi namfahamu mwanadamu kwa kuishi naye. Ni kiumbe chenye nguvu mno. Akiamua kufanya jambo lake!” James akacheka kwa masikitiko kama aliyekumbuka mbali. “Aisee mimi ndio maana nilijitenga kabisa mpaka nilipompata Jema wangu. Na ndio maana namng’ang’ania kwa moyo wangu wote bila kuzembea. Siruhusu kitu wala mwanadamu mwingine katikati yetu, kwa sababu mimi najua kwa kuona madhara ya kuzembea kwenye ndoa. Nimeshika haswa.”

Akakumbuka historia ya Danny na Grace. Walivyokuwa na ndoa yenye heshima kwenye jamii. Bila ya kutarajia Danny ni muathirika wa UKIMWI. Hana ndoa, kaua watoto wawili kwa hasira. Amebaki peke yake! Mwanamke aliyemkimbilia, akimfananisha na aliyekuwa mkewe, anaishi na wanaume wengine. Hana hata habari naye! Danny amekua darasa lake James. Anaishi kwa kuona, anajifunza bila kupenda. Kila akijisahau kidogo, anajirudi kwa haraka sana kwa mkewe.

“Daah!” Colins akasikitika. “Ila kwa heshima kabisa Colins, tafadhali kaa mbali na Jelini mpaka ujue ni nini unataka.” “Unafikiri mimi sijui nini ninataka!? Ni…” “Hapana Colins. Tafadhali nisikilize. Wale binti wamelelewa na mama tu. Na cha kwanza, nakwambia ukweli, chochote kibaya unachomfanyia Jelini, mama yake huwa anaumia sana kuliko wale watoto wenyewe. Na Jema anasema huwa anasema watu wanadharau binti zake wakijua hakuna mwanaume wa kuwatetea. Wanachagua kuonea watoto wake, ili kukinga binti wenye baba zao.” “James!” Colins akashangaa, asitarajie hilo.

“Hakika hujawahi kuona yule mama akitetea wanae. Hutampenda. Mkali kuliko simba. Muulize Love atakwambia jinsi alivyompandishia mbele ya mama zenu na Connie, pale alipoanza kumsema Jelini akikumbushia siku aliyolewa kwenye harusi yetu. Ilikaribia kuwa mbaya usiku ule, na mama Jema hanaga aibu na katika hilo hana utu wala staha. Akifika kutetea wanae, Jema anasema anapandwa na hasira ya ajabu sana. Wanao mjua, huwa wananyamaza ndipo na yeye anatulia. Sasa pona ya Love usiku ule, ilikuwa kutulia, na kukubali kuondoka pale. Sasa nakutahadharisha. Hutaki kuona upande mwingine wa mama Jema.”

“Hilo moja. Ila la msingi ni muhurumie Jelini. Usimuweke katikati ya haiba ya mahusiano ya aina hiyo ambayo nyinyi mnayo. Unamuumiza bila sababu.” “Nampenda Jelini, James.” “Lakini wewe si mwanaume kama wanaume wengine Colins! Hilo likubali.” “Unanitusi James!?” “Mimi nakwambia ukweli si kukutusi. Wewe unajenga familia yako na ya baba yako. Mimi nimemuoa Jema, tujenge kwetu. Sijui kama unanielewa?” Colins kimya.

“Mimi kwa sababu ni mtu wako nakufahamu, nakuelewa. Lakini mtu mwingine anaweza kukushangaa kabisa. Unasimamiaje mahusiano ya wazazi wako, kama yako!? Utajenga lini kwako!? Lakini kumbe ni mfumo mliokubaliana, na unaupenda. Ndio maana hata kujenga, umejenga pembeni ya wazazi na likawa sawa hata kwa Love. Kwamba mngeoana nyinyi, mnakaa ndani ya mji wa baba yako, maisha yanaendelea kama kawaida, tofauti na sisi wengine.”

“Japokuwa mimi ni mtoto wa kwanza kwetu. Na mzee anamali nyingi huko kwake, mimi sijajenga kwenye mali zake. Nimekuja kuanza huku Dar. Mke nimempelekea mimi. Hata mama yangu mzazi hana mamlaka juu ya Jema, ila mimi. Na kwetu ndivyo tulivyo, haina shida, na tunaishi hivyo kama nyinyi mlivyokubaliana kwenu kuishi hivyo. Sijui kama unanielewa?” Kimya.

“Na aina ya familia zilizobarikiwa kama hizo zenu, ni chache sana Colins. Wewe ni shahidi. Wengi hawajabahatisha mlicho nacho nyinyi. Ukaribu wa familia kwa kiasi hicho! Binafsi sijawahi ona. Sasa kumsogeza mtu kama Jelini ambaye hajakulia kwenye hayo mazingira ni kumuumiza bila sababu. Na mimi kama mtu wako wa karibu, kwa heshima kabisa, nakusihi usimfanyie hivyo. Si sawa. Ishi maisha uliyochagua. Ukipokea faida zake na hasara zake, lakini usimtake Jelini aingie katikati hapo, halafu yeye akaishia kuwa muhanga. Hapana Colins. Ni hilo tu.” Colins akapokea hiyo dozi kama ilivyo, akaimeza na kutulia kimya, siku ya kazi ikaanza.

 

~~~~~~~~~~~~~~~~

Kila Pande Penzi Limechanganyikana Na Pesa.

~ Love Anajirudi Kwa Colins Kwa Kisingizio Cha Kuokoa Mali Za Wazazi.

~ Belinda Anamgeuka Shoga Yake Wa Muda Mrefu, Akitaka Penzi La Victor Sababu Ya Pesa. Na Anadai Yalishakuwepo Mahusiano Kati Yao Kabla Ya Vai. Haki Zote Ni Zake, Maana Vai Amemfahamu Victor Kupitia Yeye. Wameapa Kumkomesha Vai Aliyepo Hotelini Akikoleza Mahusiano Yaliyokwisha Mnogea Victor.

~ Bale Anamtaka Vai Aliyekwisha Toa Ahadi Ya Muendelezo Wa Penzi Kwa Victor.

~ Colins King’ang’anizi Akiwa Anajenga Kwa Baba Yake, Kwake Kunavunjika. Mshika Mawili, Moja Limemponyoka. Katikati Ya Mahusiano Hayo Ya Kifamilia, Na Penzi, Anacheza Vipi Karata Zake Apate ROHO INAPENDA? Jelini.

Nani Kakumbuka Shuka Kumekuchwa?

Usikose Muendelezo.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment