Akaendesha ametulia
mpaka kwa Jema. Wakakuta rafiki baadhi wa James walishafika na vinywaji vyao na
nyama zao. Wameshaanza kula vitu vyao wakati Jema akiwaandalia cha hapo kwake.
Wakaanza kumchokoza Jelini. Colins hakuwepo. “Mimi mwenzenu siku hizi nishakuwa
mtu mzima, sitaki uchokozi na mtu.” “Jelini mtoto mzuri, njoo tutete yetu huku
tunakata kinywaji taratibu.” “Akuu! Mimi sitaki. Nataka kutulia zangu na pombe nishaacha
zamani sana. Mimi nikilewa, naanza kugawa mwanangu wakati mimi nampenda
mwanangu.” Wakazidi kucheka wakimzuia asimfuate mama yake huko alipopotelea
jikoni kwa Jema, ili abaki pale sebuleni alipowakuta wazidi kumchokoza.
“Ila ujue Jelini mimi
nitakua baba mzuri sana wa mwanao?” “Akuu! Sitaki.” “Mwacheni Jelini.” Akaingia
Colins na huo mkwara, wote wakageukia mlangoni. “Mzee upo?” “Nipo.”
Wakasalimiana kwa kupeana mikono wakigonga.
“Wewe ndio umemtoa
Kevin, nini?” Wakamuuliza Colins. “Kumtoa wapi tena!?” “Kwamba wewe hujui kuwa
Kasa mwaka mpya alikuwa rumande?” “Kwa kosa gani!?” “Nasikia mzee wao ndiye
aliyewaweka jela wote, mpaka dada yake na mumewe.” Kila mtu akawa anataka
kusikia, Jelini mapigo ya moyo yakaanza kwenda kasi. “Na ndio maana akampigia
Mdosi akamuwekee dhamana kwa kuwa hakuwa na mtu wa kumtoa.” Mwingine akadakia.
“Basi Mdosi atakuwa
ndiye aliyemtoa ila si mimi.” Colins akajibu akiwa anakaa. “Mdosi kamchinjia
baharini! Unafikiri sisi tulijuaje?” “Mdosi kamtema. Alikuwa anasema yeye si
ananyodo kama mtoto wa kike, basi akatafute matajiri wenzie wamtoe. Akamwambia
hana hiyo pesa yakumuwekea dhamana atoke.” “Acha masihara!” Danny akadakia.
“Kumbe? Yeye si
anasemaga sisi wote tunashida, yeye yupo pale ili kutoka kitandani tu? Ndio
Mdosi akamwambia, hali yake kama anavyoijua. Pesa hana.” “Na kamfanyia
kusudi tu.” “Kwani siri? Amesema ingekuwa mtu mwingine, hata benki angekopa ili
amuwekee dhamana. Amesema amemfanyia hivyo ili atie akili ajue pesa si kila
kitu, ila utu.” Wakaanza kumsema Kevin na familia yake, wakawa
wameshampoteza Jelini.
“Matajiri wana mambo!
Sasa mzee aliwafunga kwa sababu gani?” “Itakuwa walitaka kumzidi tu mzee
mahesabu, akawakamata ndio akaamua kuwatia akili kuwaonyesha yeye ndiye
anayewaweka mjini. Wasijisahau.” “Nasikia mzee wao mkorofi!” “Unaambiwa
ni kama Hitler. Katili hacheki na kima.” Mazungumzo juu ya hiyo familia
yakaendelea, Jelini kimya.
Jema na mama yake
walikuwa jikoni. Mama Jema alishamchukulia Jeremy hizo nyama walizoleta rafiki
wa James, na sahani yake akapitiliza naye jikoni na kumuwekea ili ale. Jelini
akanyanyuka taratibu na kutaka kuondoka, Colins akamuwahi. “Nisubiri.”
~~~~~~~~~~~~~~~
Akamshika mkono na
kumtoa nje baraza la pembeni kabisa wala si mbele wala nyuma. Hapo James
aliweka kwa kujenga bustani ndogo tu. Muundo mzuri ndipo kunapoangaliana na
hilo baraza. Unaweza kujificha hapo na kufanya yako mtu asikusumbue. Akafunga
tv kubwa tu, nzuri. Ndipo marafiki zake huwenda kuangalia mpira kwenye hilo
baraza bila kumkera Jema hata akiwa na wageni wake. Watapiga kelele huko na
kubishana mpaka wachoke. Napo James alipafunika uzio wa wavu pia. Na makochi ya
kukaa hapo mazuri tu na meza zake, kama kwa kina Magesa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wawili hao wakakaa
hapo. “Nisikilize Jelini. Hii familia na mambo yao, hayakuhusu hata kidogo,
wasikuumize kichwa. Unanielewa?” Jelini akabaki ametulia. “Umepita kwenye
maisha yao, umetoka, mengine waachie wenyewe. Usijiumize kichwa kabisa. Huusiki
tena.” Jelini akavuta pumzi kwa nguvu na kuanza kuzishusha taratibu kama
kusafisha kifua. “Wasikuharibie usiku wa leo, wala usiwape mwanya wa kukutesa
zaidi.” “Umependeza Colins! Na unanukia vizuri kama kawaida yako.” Colins
akaanza kucheka.
“Kweli tena. Umeacha
harufu pale kwenye mto wangu. Wakati natandika nikapata hiyo harufu yako.” “Na
wewe umependeza Jelini. Nataka ufurahi usiwe na huzuni.” “Sasahivi inapungua.
Nilitaka kujipanikisha bila sababu!” “Hawakuhusu tena. Hata ukiwasikia, wasikuumize
kichwa. Sawa?” Jelini akakubali kwa kichwa.
“Basi turudi ndani.”
“Mimi naenda kuwasaidia kina Jema, wewe nenda kwa wenzio.” “Sasa tutapata muda
wetu saa ngapi!?” Colins akawa kama analalamika. “Wakati wakula.” Colins
akafikiria, akawa kama hajaridhika. “Usikae sana jikoni. Ukichelewa nakufuata.”
Jelini akacheka. “Au hutaki nikufuate.” “Mimi nataka wewe unifuate kila
mahali.” Colins alicheka sana. “Sikukeri?” “Hata kidogo. Ndio nafurahi. Napata
faraja. Nikiwa na wewe na ukiniongelesha, natulia.” Hawakufanikiwa
kutoka hapo.
Wakabaki hapohapo barazani wanaongeleshana
hawamalizi. Colins amekaa nyuma yake, anaongelea shingoni kwake, akimchungulia
kwa mbele, amemuegemea bega. Mara waangalie simu ya Colins wakipekua hiki na
kile na Jelini ndiye aliyekuwa ameishika.
Hawakukumbuka kula
wala kinywaji. Wakawa kama wamepotea kwenye kusanyiko. Wamebaki wao wawili tu,
upande wa barazani. Wakati wenzao wanakula na kunywa ndani. Danny akawakumbuka,
akaanza kuwasaka bila kumwambia mtu. James akamuona na yeye akamfuata, wakawakuta
wamekaa vile. Danny akakunja uso. Colins hata hakushituka ila kumuuliza. “Vipi,
umeniita sana nini?” “Hata ningekuita, ungeitika kweli?” Danny akamuuliza,
James na Colins hawana mbavu.
Jelini akataka
kusogea ili wasikae vile mbele yao, akashindwa maana hivyo Colins alivyokuwa
amemuegemea! Wengine wote wakawafuata maana hilo baraza si geni kwao.
Wakawakuta vile. Zikaanza fujo. “Colins hatimaye kachukua jimbo.” “Alibana
weee, yamemshinda.” “Jelini namba tasa. Inagawanyika kwa moja tu, na
yenyewe.” Akaongeza mwingine wao, wote vicheko. “Kwa hiyo Jelini hagawanyiki
kwa mbili?” “Ushaona mwingine kama Jelini?” Akajibu na kuongeza fujo wakicheka
kishabiki. “Hata wachoraji hawajaweza kumchora mtu kama Jelini. Yupo peke yake
dunia nzima.” “Basi kweli Jelini namba tasa.” “Nilisema mimi.” “Sasa, sasahivi
Jelini umefurahi?” “Mimi nishasema sitaki uchokozi, nishakuwa mtu mzima.”
Wakazidi kucheka.
“Jelini mtoto mzuri
mimi nina swali.” “Sitaki.” “Sasa mbona hata swali langu hujalisikia!?”
“Kashasema hataki. Muache. Nyinyi kaeni hapa, acheni majungu.” Colins
akaingilia. Kikao kikahamia hapo kula na kunywa hapohapo. Stori zikaendelea,
Jelini katulia kimya hapo kwa Colins mpaka wazazi wa Colins walipofika.
~~~~~~~~~~~~~~~
Colins akasikia sauti
zao akamwambia Jelini amsindikize. James akafuata nyuma. “Tumeleta sambuza za
wajukuu, wala hatukai. Baba CJ kesho kazini, alfajiri. Hata huko tulipokuwa
tuliomba udhuru.” “Nashukuru sanaaa.” James akashukuru yeye. Wakazungumza
kidogo, wao wakaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Na mimi kesho naanza
kazi, Jema.” “Mama ameniambia. Naona umekazana!” “Nataka hela. Na sasahivi
nimejiambia sitaki tena kukuomba. Mchana mama alivyonikatalia hela, nusu
nikutumie ujumbe nikuombe wewe, lakini nikajisuta. Acha na mimi nifanye kama
wewe Jema. Naamini nitafanikiwa.” “Halafu ni kwa muda tu, Jelini. Mwanzo mgumu.
Mambo yakikaa sawa mbona utapumzika?” “Mmmh! Nimeona matajiri jinsi
wanavyofanya kazi mama yangu. Hawana kupumzika kama mimi. Acha tu nibadilike.”
Wakazungumza kidogo, Colins akasema atamsindikiza kurudi nyumbani, awahi
kulala. Gari walishakubaliana kuliacha hapo. Jema alisema yeye atamrudisha mama
yake na Jeremy. Hao wawili wakaondoka na kufurahia kuwa peke yao.
~~~~~~~~~~~~~~~
Wakahamisha kikao
nyumbani kwa mama Jema. Wawili tu, hamna gasia ya watu. Wakajizungusha kwa hili
na lile wakitafuta sababu ya Jelini kuwa mikononi kwa Colins, wakakosa. Jelini
anahangaika ili tu ajikute amekumbatiwa tena, akashindwa kujirudisha, akaenda
kukaa kochi la pembeni mbali na alipokuwa amekaa Colins.
“Njoo nikuonyeshe
kitu.” Akahamia kwenye kochi alilokuwa amekaa ila pembeni. Wote hawakuridhika.
Colins uzalendo ukamshinda. “Mimi hivi najihisi mpweke! Nataka uwe hapa na
mimi.” Jelini akacheka na kujisogeza karibu kabisa. Akarudi kukumbatiwa, ndio
wote roho kwatu. Jelini anasikia raha uso wa Colins kwenye shingo yake huku
akizungumza naye. Colins anasikia raha kumkumbatia vile kwa karibu. Ukabaki
ulimwengu mzima peke yao wakibembelezana kwa hili na lile. Wakati mwingine
wanatulia tu wakisikiliza mziki kwenye simu ya Colins.
Walikaa hapo mpaka
James akawarudisha Jeremy na mama Jema. Hakuingia ndani ila alijua bado Colins
yupo. Walipolikuta gari lake pale nje wakaangaliana na mama Jema na kucheka.
Mama Jema akaishia kutingisha kichwa na kushuka garini. “Usiku mwema Jeremy.” Akawaaga
na kurudi kwa mkewe. Ilashakuwa saa saba usiku. Naye mama Jema hakutaka kukaa
hapo. Akawasalimia na kupitiliza kulala na mjukuu wake. Alishaambiwa Colins
kituo cha polisi, aachwe kabisa, asifukuzwe hapo ndani. Na yeye hakutaka mengi,
akamuacha.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Bosi wangu amerudi,
acha na mimi nikalale. Maana mama anapenda mambo ya kudamka. Sitaki kesho
aniache.” “Kwa hiyo utakuwa ukifanya kuanzia muda gani.” “Mama ameniambia
nikifungua kuanzia saa mbili kamili, na nikaweza kukaa mpaka saa mbili usiku
sio mbaya. Ili na wale wanaotoka makazini, kama wanataka kununua vipodozi baada
ya kazi wanikute. Ila amesema usiku atakuwa anakuja kunipokea ili na mimi
nipate muda na mtoto.” Colins akasikiliza, na kubaki akifikiria.
“Mbona kama kuna kitu
unataka kusema?” “Sitaki kukukatisha tamaa, ila ujue ni ngumu. Si rahisi kama
inavyosikika. Najua nia ipo, ila tafadhali Jelini, unapokumbana na uhalisia,
ukachoka, nakuomba, usije tafuta mbadala. Niambie.” “Kama wasiwasi wako ni kwamba
naweza kurudi kutafuta msaada kwa mwanaume mwingine…” “Kasa.” Ikabidi Colins
awe muwazi kabisa.
“Mimi sirudi tena kwa Kasa, Colins. Bora
nimuombe Jema hela kuliko kuuza utu wangu. Hapana Colins. Mimi sipo hivyo.”
“Niahidi mimi nitakuwa wa kwanza kuniambia kama mambo yamekuwa magumu sana na
unahitaji msaada.” “Na wewe usikimbilie kunihurumia. Fanya kama mama. Nataka
nijenge tabia ingine zaidi ya hii ya uvivu. Mwenzio sijasoma na wala sina
mpango wa kurudi shule. Sasa na biashara pia nishindwe! Sitaki kuwa tegemezi
daima. Kama hivi vitu vya chumbani kwa mwanangu vinaninyima raha! Sasa nataka
kupambana mimi mwenyewe mpaka nimnunulie, au nikomboe vile nilivyoanza mchakato
kwa fundi. Kwa hiyo nitie moyo. Kama hivyo wewe unavyoamka kila siku asubuhi na
kwenda kazini mpaka jioni, na mimi nataka huo uwezo. Nishalala sana.” “Sawa.
Mimi nitakuwepo kukutia moyo.” Ahadi hiyo akatoa na busu la shingoni upande wa
masikio.
Jelini alisisimkwa
nusura amgeuzie mdomo, lakini hakutaka kufanya chochote na Colins. Hata busu la
mdomo, mpaka akapime kwanza. Akajishika pale alipombusu. “Asante
Colins.” Akashukuru akiwa ameinama bila kumuangalia maana alijua akimwangalia
tu, uzalendo utawashinda. Na Colins alijua. Akasimama hapo nyuma alipokuwa
amekaa. Jelini akabaki amekaa na kuinama. “Nitakuona kesho.” “Si unakwenda
kazini?” “Hapana. Tunarudi tarehe 5. Nitakuona kesho.” Colins akatoka kurudi
kwao.
Siku Inayofuata.
Alfajiri mida ya saa 12:30
Colins akarudi hapo na kumshangaza sana mama Jema wakati akimfungulia mlango.
“Sasa wewe utakuwa umelala kweli!?” Mama Jema akamuuliza. “Nimekuja kukumbuka
sijamuuliza Jelini hilo duka analokwenda kufanya kazi litakuwa wapi. Nataka
kuwa naye siku ya kwanza.” Mama Jema akabaki akimtizama. “Kama hutajali
lakini.” Akajirudi. “Kwamba na wewe ukauze duka la vipodozi!?” “Si ndiko
atakapokuwa Jelini? Au sikuwa nimemuelewa?” Mama Jema akaona amuache tu. Jelini
akatoka akionekana bado alikuwa amelala.
“Karibu Colins.”
“Nimewahi sana. Samahani kwa kuwasumbua mkiwa mmelala.” “Usijali. Njoo
unisubiri wakati najitayarisha. Tutatoka kwenye saa mbili na nusu. Nilisahau
kukwambia muda.” Akaenda kumshika mkono kabisa. Mama Jema akajirudia chumbani
kwake. “Nimejisikia vibaya nimewaamsha!” “Basi mimi nimefurahi kukuona.” Colins
akaanza kucheka, mama Jema akiwasikiliza.
“Njoo usinzie
kitandani kwangu wakati mimi najitayarisha.” Ikawa kama amepewa ulimwengu wote.
Akavua viatu haraka na kwenda kujitupa kitandani kwa Jelini wakicheka.
“Leo mimi ndio
nakubembeleza ulale.” “Wewe hurudi kulala?” “Nataka kujiandaa. Ikiwepo
kutengeneza kifungua kinywa. Lala hapa.” Akamuonyeshea kwenye mto. “Bila hata
kukugusa!?” Jelini akaanza kuona aibu.
“Bila kukugusa
sitalala bwana!” “Nitakubembeleza utalala tu.” Colins akabaki kama
anayejishauri, kwamba hajaridhika. “Njoo, utalala. Huwa namfanyia hivyo Jeremy
analala haraka.” “Mimi sitaki unibembeleze kama Jeremy.” Jelini akacheka na
kujifunika uso. Akamuhisi anamlalia mapajani. “Hivi ndio najisikia vizuri,
angalau nimekulalia.” Jelini akaanza kumpapasa taratibu.
“Sasa ukilala
nikikuweka kwenye mto si utaamka?” Akajigeuza chali na kumwangalia. “Lakini
nitakuwa nimekuwa karibu na wewe.” Jelini akacheka na kuanza kumuweka sawa
nyusi kama ambusu, ila ikawa kama aliyekumbuka kitu akarudi haraka pembezoni
mwa nywele na masikio. Akamchezea, akamuona anajigeuza kurudi kulala ubavu.
Wakatulia kwa muda.
“Njoo ujilaze pembeni
yangu.” Jelini bila ya kufikiria, akajilaza akimpa mgongo. Akamuwekea mkono,
Jelini akaukumbatia vizuri kwa mbele akimchezea vinyweleo vya mkono taratibu
huku akipata sawia pumzi za Colins kitu alichopenda maana na hapo alijiiegemeza
uso karibu sana na yeye. Ile harufu na uwepo wa Colins, hapohapo wote wakalala.
~~~~~~~~~~~~~~~
Walikuja kuamka saa tano
asubuhi, wasiamini. “Nimekuponza.” Colins akamwambia. “Hata hivyo tulilala muda
mbaya. Usijali. Acha nioge, nimtafute mama. Maana najua mida hii atakuwa
ashafanya mengi sana.” Jelini akaoga, akagundua mwanae yupo chumbani kwake.
Akamfuata. “Bibi amesema vyakula vipo kwenye friji. Alipika kingi jana kwa
anti, amebeba.” “Wewe umeshakula?” “Nakaribia cha mchana. Bibi ameniwekea
kwenye sahani kabisa, amesema nikisikia njaa, nipashe tu.” Jelini akatoka na
kumuacha huyo Jeremy maana alionekana
ametingwa na hataki kuingiliwa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Akaonelea kumpigia
simu mama yake “Nilipitiwa na usingizi.” “Na mimi
nilijua tu. Nikaona nikuache.” “Nikufuate wapi?” “Sio sasahivi. Mimi nishahama
upande wa pili. Huko tena nishatoka. Kwani Colins anaanza kazi lini?”
Jelini akaanza kucheka. “Mama naye?” “Wewe niambie tu.”
“Tarehe 5.” “Basi naona na wewe ajira yako ianze siku hiyohiyo, usinidanganye
na kunipotezea muda wangu. Kwaheri.” Jelini akabaki akicheka asiamini.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Akarudi chumbani
alikomuacha Colins. “Umefukuzwa kazi?” Akamdaka mlangoni na swali. “Mama
ameniambia nianze kazi, wewe ukianza kazi.” Colins akacheka sana. “Sio jambo
zuri bwana!” “Tunahitaji muda Jelini. Mwenzio sipati likizo kila mara. Acha
tutumie hizi siku zilizobaki vizuri. Unataka tufanye nini? Twende wapi?
Chochote unachotaka.” “Siwezi kutoka, Jeremy yupo busy na ujenzi wake.” Colins
akazidi kucheka. “Basi usiku mama akirudi, sisi tutoke twende dinner
halafu movie, au unasemaje?” Jelini akatulia.
“Mbona unasita tena?
Itakusaidia kuchangamka na kupata muda pamoja.” Jelini akafikiria jinsi ya
kumueleza, akasita. “Pengine niwe nilikuelewa vibaya. Ni kama nilielewa
unafurahia muda na mimi!” “Ni kweli Colins. Natamani hata usiondoke.” “Sasa
shida ni nini!?” “Nimekumbuka vitu vyangu nilivyoacha kule.” Akamuelewa kuwa
alivyoacha kwa mzee. “Kwa hiyo unataka kwenda kuvifuata kwanza ndio tutoke!?”
Wivu tayari. “Hapana. Kwanza nahisi hapa ninavyo vitu vyangu vingine. Nitakuwa
sawa.” Colins akaonekana bado analo jambo.
“Unataka tutoke saa
ngapi?” Akawa kama anamtoa huko alipokwama. “Inamaana unampango wa kuja kurudi
kwake, kufuata tena vitu vyako?” “Si lazima.” “Jelini?” “Yaani ndio nimekumbuka
sasahivi baada ya kusema tutoke. Lakini sio hata kitu nakipigia mahesabu.” “Kwani
ni kama ulihamia huko?” “Kwa sehemu. Zaidi siku za weekend. Ila naomba usirudi
huko. Turudi kwenye mipango yetu.” “Itasaidia nini kama mimi sirudi huko
kimawazo lakini kumbe mwenzangu una safari itakayokulazimu kurudi kwake? Tena
chumbani!” “Colins wewe unafika mbali sana ambako mimi huko wala sipo!”
“Tafadhali kabla ya kurudi kwa yule mzee unishirikishe Jelini.” “Sawa.” Hapo
tena akaharibu maana aliitika bila ya kufikiria, ilimradi yaishe.
“Kwamba tayari kuna
mpango wa kurudi!?” “Colins wewe unawasiwasi wa bure tu! Kwanza hata sikuwa na
mawazo ya huko. Tafadhali tutumie hizi siku mbili vizuri, sio tena kumuwaza na
yeye. Utaninyima raha. Nataka tubaki mimi na wewe tu.” Hapo akatulia.
“Naomba uniamini,
Colins. Mimi si kigeugeu.” “Lakini mlikuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi,
Jelini! Haitachukua nguvu nyingi kukurudisha mlipokuwa. Ndio maana napatwa
wasiwasi.” “Niambie unataka nifanye nini ili uamini ninachokwambia?” “Sijui
Jelini. Hata sielewi tena.” Jelini akaenda kukaa kabisa pale pembeni yake.
“Sina mpango wa
kwenda kwake. Na ikitokea nakwenda, nitakujulisha. Tena tunaweza hata kwenda
wote.” “Sitaki kwenda kwake.” Hapo na ubishi akauweka. “Mimi naona nimwambie
amtume dereva aniletee ili yaishe.” “Jelini! Kwamba mrudishe tena mawasiliano
mpaka kupanga tena mipango!?” Hapo Jelini tena akakwama.
“Basi nishauri wewe
kitu chakufanya.” “Kwani ni vitu vya thamani sana?” “Sana Colins.” “Kwamba
kupita hivi vyote hapa!?” “Sitakudanganya. Nimeacha kule vitu vya thamani sana.
Mpaka dhahabu zangu zipo kule. Tena dhahabu nyingi tu. Nguo za jioni ndio nyingi,
tena za thamani na viatu. Mimi napenda sana kupendeza Colins. Kwa hiyo nikiwa
napesa kwenye kuvaa, sijipunji.” Colins akachoka kabisa, akasimama pale.
“Sasa unaenda wapi!?”
“Nahisi kuchanganyikiwa tu. Bora nitoke kwanza.” “Njoo Colins.
Usichanganyikiwe. Sitakuumiza. Hiyo ndio ahadi yangu ya kwanza, japo
sijui tutaishia wapi. Na nina ujasiri wa kusema hivyo. Ipo siku nitakupa
sababu. Kabla wewe hujaumia, ujue mimi nitakuwa nimeumia zaidi. Hakuna
mali, itanifanya nikukosee. Ni bora nipoteze kila kitu, mimi na wewe tubaki
salama.” Hapo akaupata moyo wa Colins. Akatulia kabisa na kurudi kukaa.
“Mimi sina pesa kama
za yule mzee, Jelini. Sina uwezo wakusema eti nitakununulia mavitu ya thamani.
Sina huo uwezo mkubwa kiasi kama chake.” “Kama ningekuwa na shida na pesa,
ningeanza kulala na mwanae ndio nikaja yeye. Sikutegemei uwe yeye, na najua wewe
si yeye. Na ujue kabisa, haupo kwenye mashindano naye.” “Una uhakika?”
“Asilimia 100.” Akatulia.
Jelini akajipenyeza
mwilini mwake mpaka akafanikiwa kuingia katikati ya mikono yake akajilaza
kifuani kabisa. Na yeye akamkumbatia. “Umeniamini?” Jelini akamuuliza kwa
kumbembeleza. “Sitaki kukupoteza Jelini.” Jelini alishituka, akamwangalia.
“Unamaanisha Colins!?” “Sina sababu ya kukudanganya. Najua umetoka kuumizwa.
Ndio maana naona nikupe muda utulie, ili angalau akili yako hata ije
kunifikiria na mimi, kwamba nikikwambia kitu, uweze kunielewa na kuniamini.
Sasa tena kusikia bado kuna mambo yakuwahusu nyinyi wawili tena! Nafasi yangu
itakuja kufika lini?”
Ikamgusa kweli
Jelini. “Nikikwambia nafasi yako haijawahi kupotea, utaamini?” Colins akakunja
uso wa wasiwasi. “Sijaelewa Jelini!” “Nitakuja kukueleza vizuri nikiwa
nimetulia, Colins. Lakini amini sitarajii kukuumiza na wala usiwe na wasiwasi
naye. Mimi nakupa uhakika.” Colins akatulia. “Twende ukale kwanza.” Kazi ya
kufuatana hapo ndani ikaanza. Kila mahali wapo pamoja. Wakikaa, ni kukumbatiana
kwa huba haswa mpaka ilipofika jioni Colins akatoka kujiandaa
kutoka na Jelini kwa chakula cha usiku wakiwa wamehamasika haswa kuja kupata
tena muda wa pamoja na mipango ya kutumia hizo siku mbili ipasavyo, kabla
yakurudi kazini.
Mtoto wa Jelini
hanaga shida. Yeye bora ale. Muda wote alikuwa chumbani kwake akifanya yake.
Jelini akaoga na kuanza kazi ya kujiandaa.
Machozi Ya Samaki.
Colins anafika kwao,
mlinzi akamuwahi getini. “Mama anakuita ndani.” Colins akakunja uso. “Amesema
ukija tu, nikwambie uende moja kwa moja.” Mlinzi akaongeza msisitizo. Colins
ikabidi atoe simu yake. Haikuwa hata hewani na hakujua ni wakati gani
ilijizima. Akasogeza gari mpaka nyumba ya wazazi. Akashuka kwa haraka kama
akimbie ili asipoteze muda hapo, arudi kwa Jelini kwa wakati.
Akawakuta baba yake
na mama yake hapo sebuleni. Akasalimia amesimama. “Kwa nini unamtia mama yako
wasiwasi!?” “Simu ilikuwa imezima baba. Sijajua. Kwema?” Akauliza akimwangalia
mama yake. “Mbona wimawima hata hukai?” “Nina haraka mama!” “Kwamba huna hata
dakika 10?” “Zote hizo!?” Colins akahamaki kama ameambiwa mwaka mzima.
“Kaa chini Colins.” Mzee
akaweka msisitizo wa amri. Akakaa akilalamika. “Mimi nina haraka.” “Unakwenda
wapi?” “Kwani kuna nini?!” “Love anaumwa. Amelazwa.” Colins akatulia
akimsikiliza mama yake kwa macho ya ‘kwa hiyo?’. “Umesikia Colins?”
“Nakusikiliza.” “Kwamba hutaki kujua anachoumwa?!” “Sasa hata nikijua
itanisaidia nini mama jamani? Mimi nina haraka.” “Colins! Nakwambia mwenzio
amelazwa, hata kutaka kujua kulikoni!?” “Love sio mwenzangu mama. Naomba
rekebisha huo usemi.” “Ujue yupo serious sisi tulikuwa huko karibu siku nzima,
hata wazazi wake wanawasiwasi!” “Basi labda niseme hivi. Mniambie alipolazwa,
nitakwenda kumuona.” “Afadhali hivyo.” Colins akasimama.
“Sasa mbona hata
hujajua alipolazwa halafu unaondoka?” “Amelazwa wapi?” Colins akauliza na
kushangaza wazazi wake, wakabaki wakimwangalia. “Au nitawapigia simu wakati
nikienda. Sasahivi nina haraka.” “Colins, hebu subiri kwanza.” Baba yake
akamuwahi kabla hajaondoka.
“Yule binti anakupenda
sana. Leo alikuwa akiugulia maumivu huku akikutaja! Kwa kukiri kwake kwa baba
yake, mimi nikisikia amemwambia baba yake anajuta na kama angepata
nafasi ingine na wewe, atafanya tofauti. Sasa si bora umfikirie?” “Mimi simtaki
tena.” Colins akajibu bila hata kufikiria mara mbili.
“Si wewe ulisema Love
ndiye mke wako?” “Dad!” “Wewe mwenyewe uliniambia. Na ukasema utafanya kila
uwezalo, kumfanya awe na furaha.” “Basi kama mama hakukwambia, nilishindwa.
Na sitaki tena.” Hapo anajibu akionekana wazi anataka kuondoka.
“Coli..” “Mbona kama
unanilazimisha?! Nimesema SIMTAKI. Simtaki tena. Wewe hujui nilikopita
na Love.” “Najua na usisahau wakati wote kwenye safari yenu na mimi nilihusika.
Niambie ni jipya lipi ambalo limetokea upya.” “Nilikwambia nimechoka.” “Kwa
sababu ulikuwa ukijitahidi peke yako. Sasahivi yupo tayari kubadilika. Na
sasahivi ni mgonjwa. Anatuhitaji sisi kama familia. Jioni hii tunakwenda
wote kama familia. Haijawahi kutokea tukatengana. Sasa sitaki wewe ndio
uanze kuvunja umoja wetu. Tunakwenda wote hospitalini. Na Connie pia
nimemwambia aache kila kitu. Tunakwenda kuungana na familia ya Simba kwenye
kipindi hichi kigumu.” Mzee akaweka amri, akasimama na kuondoka.
“Lakini hivyo sio
sawa mama. Mimi ni mtu mzima, nina uhuru wangu wa kujiamulia mambo yangu. Kwa
nini hunitetei, umenyamaza tu kimya!?” “Kwa sababu katika hili yupo sahihi
Colins. Hatujawahi kuishi hivyo maisha yetu yote. Familia zetu zimekua zikilia
pamoja na kufurahi pamoja. Leo Love ilikuwa ni kama tumpoteze! Halafu
wewe huonekani kujali ndio maana baba yako amekasirika.” “Kwani anaumwa na
nini?” “Hilo swali lilitakiwa liwe la kwanza, Colins! Lakini wewe ulionekana
kupuuza.” Colins akarudi kukaa.
“Nisikilize mama.
Nampenda Jelini, sijawahi penda kwa namna hii.” “Mimi sijakukataza lakini…”
“Subiri mama. Nipo kwenye kipindi cha kuupata moyo wake, kipindi hiki.
Nikizembea tu, nitampoteza. Nilishampoteza mara ya kwanza, sitaki
kumpoteza tena. Na kingine, sasahivi ananihitaji sana. Nimemuahidi
kumtoa kwa chakula cha usiku. Namwambia nini? Eti nimeshindwa kutoka naye
sababu Love ni mgonjwa? Na ukumbuke Jelini anayajua mahusiano yangu na Love!”
“Leo unakwenda kumuona Love kama mmoja wa familia, si kama mpenzi! Ndio maana
hata yeye alipokuwa mgonjwa, kila kitu kilisimama, tukamkimbilia hotelini
alipokuwa na kumpeleka hospitali.” “Mama!” Colins akalalamika kwa kushangaa
yanavyomrudi.
“Ni kipimo hichohicho
tunampimia na Love. Familia yetu hatubagui. Labda wewe leo ndio uniambie,
unaweza vipi kwenda kupumzika nje, halafu familia ya Simba inalia ugonjwa wa
binti yao.” “Kwani anaumwa nini?” “Apendex ilipasuka akiwa kazini.” Colins akachoka
kabisa.
“Sio jambo dogo
Colins! Halafu katikati ya hiyo hali, analia akisema anakufa akiwa amepoteza
mtu muhimu sana kwake, ambaye ni wewe. Watu wote wamesikia. Halafu usitokee!
Kweli Colins mwanangu!?” “Basi mama.” “Huko kutoka na Jelini unaweza kutoka
siku nyingine yeyote, lakini leo umepatwa na tatizo la kifamilia! Kweli Jelini
atashindwa kuelewa hilo?” “Basi acha nikazungumze naye.” Akasimama.
“Lakini mimi simtaki tena Love, mama.
Na nilishakwambia. Huo ukurasa nimeshafunga. Tafadhali jaribu kuzungumza na
baba. Mahusiano yabaki kuwa ni ya kifamilia tu.” “Baba yako hajalazimisha
umuoe.” “Lakini ndivyo anavyotaka. Na wote tunajua. Mimi simtaki Love kama mke
wangu. Mimi nimeishi naye, najua ninachozungumzia.”
“Kwa hiyo
umeshamwambia Jelini kama unampenda?” “Siwezi mama yangu. Jelini yupo kipindi
kigumu. Nataka kwanza angalau nimuonyeshe mimi nipo, na nimwaminifu ndipo
nianzishe jingine. Kumbuka jinsi nilivyomuumiza mwanzo. Nahitaji muda zaidi.
Sasa mambo kama haya yakitokea ndio atazidi kuniona mimi ni mbambaishaji.” “Huu
si ubabaishaji. Ndio ukubwa na unaonekana ni mtu wa familia.”
“Au niende
nikazungumze naye ana kwa ana.” “Hapana Colins. Najua hutarudi.” “Nitarudi
mama.” “Ukiondoka hapa, iwe safari ya hospitalini Colins, na si
vinginevyo. Umenisikia?” Wakasikia sauti ya mzee kutoka ndani.
Colins akanyanyuka
kwa hasira na kutoka hapo. “COLINS?” Mzee akafoka kwa sauti. “SIONDOKI.
Nakwenda kupiga simu.” Na yeye akajibu kwa hasira. “Taratibu ml..” Kabla mama
yake hajamaliza, wakasikia mlango umebamizwa kwa nguvu kwa hasira. Mama yake
alitegemea ndio maana alikuwa akimuwahi lakini akawa amechelewa.
Kisicho Riziki.
Colins akampigia simu
Jelini. “Ukiniona jinsi nilivyopendeza hutaamini kama
ni mimi! Mama mwenyewe amenikubali.” Colins akafunga macho kwa kuumia.
Kimya. Jelini akadhani aliwahi kuongea kabla hajapokea. “Colins?” Akaita huku akiangalia simu yake. “Nipo Jelini.” “Nilifikiri naongea peke yangu!” “Nimekusikia. Ila nina
habari si nzuri.” “Ni nini tena!?” Jelini akapatwa na wasiwasi. “Tumepatwa na mgonjwa. Inabidi twende hospitalini kama
familia.” Jelini akashituka sana.
“Poleni
sana! Nani mgonjwa na ni nini tatizo?” “Apendex ya Love ilipasuka alipokuwa
kazini. Ndio amefanyiwa upasuaji.”
~~~~~~~~~~~~~~~~
Katikati ya mipango yao, nalo hilo limejitokeza. Ilikuwa Kasa,
sasahivi ni Love anayeonekana ni kama hakwepeki, tena amebeba baraka za wazazi!
Nini kitaendelea?
Usikose muendelezo…
0 Comments:
Post a Comment