Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 40. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 40.

Wakati mwaka ukiisha na kuanza, hisia zikaanza kujichanganya kati yao kwani muda mwingi walitumia pamoja. Wakifanya kila kitu pamoja. Kama hakuwepo kwake, basi alitaka kumsikia Vai kwa simu. Hapakuhitajika sababu ya kupigiana simu wala mazungumzo maalumu wawapo mbalimbali. Ilimradi tu wawepo pamoja. Na Bale alimjali kwa kiwango kilichomshangaza na kumtuliza Vai. Kila mtu aliyekuwa karibu naye chuoni, alimjua Bale. Kama wasipomuona chuoni, walijua yupo kwa Bale. Yao yakawa yakienda kwa furaha na utulivu wa namna yake.

Wakiwa nyumbani kwa Bale, mwaka ukiwa ndio mpya kabisa. Tarehe moja. Kwani Vai alilala hapo, akamuuliza swali Bale asijue hakuwa tayari na jibu lake. “Najua mwaka huwa ukianza, watu wanakuwa wakijiwekea malengo tofauti tofauti. Wewe mwaka huu una malengo gani?” Bale akafikiria kidogo. Akamuona kama amesita. Vai akacheka. “Unataka ndege nini?” Bale akacheka akaona aseme tu.

“Ahadi ya mguu mpya ni jumatano ijayo. Natamani nimalize hilo. Nijaribu tena kuzungumza na Joshua, nione kama atanisaidia kutafuta kazi. Maisha yaendelee kama si kuanza.” “Unamaanisha nini?” Akafikiria tena. “Maana mimi nilidhani ni kama unaishi maisha tayari!” “Ndiyo. Lakini bado ninashauku ya kuanzisha familia. Mke na watoto angalau wasiopungua watatu kurudisha jina la mzee wangu. Najihisi ninawajibika. Kuacha hivihivi nitakuwa nimemuua yeye mwenyewe na kumbukumbu yake yote.” Ikawa kama kengele masikioni kwa Vai.

Akapoa kabisa. Akakumbuka alivyotolewa kwa Zinda sababu ya kutoshika mimba. Akaanza kuwaza. Bale akamuona vile alivyopotelea mbali mawazoni hata asijue kama alikuwa akimsikiliza. Vai akajua historia inajirudia. Ila Bale hajawahi kumtaka kimapenzi! “Pengine ndio maana hajajisogeza kimapenzi kwangu, akijua siwezi kuja kumzalia mtoto!” Vai akawaza, nakuanza kuumia.

“Mbona kama nimekupoteza hapo katikati!?” Kimya. “Vai!?” “Nipo nilikuwa nikikusikiliza.” “Unanidanganya bwana! Ni nini?” “Hamna kitu. Ila wakati ukizungumza, na mimi nikawa nikijifikiria. Kwa muda fulani, nilijisahau.” “Juu ya nini tena!?” Akatulia, ila akamuona jinsi alivyobadilika.

“Tafadhali niambie Vai.” “Sio kitu cha kigeni. Nilishakwambia. Sema hayo malengo yako yamenikumbusha uwezo wangu wakutozaa.” Bale akashituka moyoni, alishasahau. “Inamaana kwangu mimi, kama ni kuja kuolewa, ni kuja kutafuta mwanaume aliyefiwa na mkewe, tena aliyekwisha kuwa na watoto wakumtoshea, hataki tena mtoto hata wakuunganisha udugu. Malengo kama hayo yako, hayawezekaniki tena kwangu.” “Kwa nini unakata tamaa!?”

“Sikukata tamaa, ila kukubali matokeo. Si kwa bahati mbaya. Ni chaguzi mbovu nilizofanya zamani.” “Namaanisha ni kwa nini unajikatia tamaa yakutopata watoto tena?” “Kwa sababu mimi si kama wewe Bale. Mwenzio niliishi na mwanaume unyumba kabisa, na sikuwahi kushika mimba. Na si kwa mwanaume mmoja tu. Ni kote nilikopita baada ya kutoa mtoto wa mwisho, ilishindikana. Kwa hiyo si kukata tamaa, ni kukubali matokeo.” Bale akapoa kama aliyemwagiwa maji.

Tayari hiyo siku ikabadilika. Kwa mara ya kwanza tokea wafahamiane wakicheka na kuwa pamoja kwenye kila ghali, utofauti ukatokea katikati yao. Vai akajiona hastahili hata kuwepo hapo. Baada ya muda akaona aage tu. “Tafadhali usiondoke Vai! Ni nini?” “Sijisikii vizuri.” “Tokea lini ukijisikia vibaya hapa pamekuwa sehemu ya kukimbia na si kukimbilia?” “Mpaka lini Bale?” “Sijui! Lakini kumbuka sisi ni mrafiki wa nyakati zote. Tunazungumza na kubebana katika kila khali. Kweli unataka kuondoka na mipango yote tuliyokuwa nayo ya jioni!?” “Acha nikatulie chuoni. Mwaka mpya mwema. Tutawasiliana wakati mwingine.” Ikawa kama utani vile. Vai akaanza kukusanya vitu vyake, Bale akimtizama. Mwishoe akakumbuka anakopitishwa. Akajirudi.

Akaanza kumfungashia vyakula wakati akifungasha vitu vyake. Akakusanya mpaka akamaliza. Akamuaga akiwa tayari na mizigo yake yote mlangoni. “Basi acha nikurudishe chuo. Usiondoke kama umefukuzwa!” “Nakushukuru.” Akaingiza vitu vyake vyote kwenye gari, na kuhakikisha haachi kitu hata kimoja. Ndipo akaingia garini na kutulia, akagundua gari inanukia vyakula. Akajua inamaana amemfungashia chakula. Ikamgusa Vai, akajikuta roho ikimuuma, asijue chakufanya. Alishapitishwa kwenye hali yakukataliwa sababu yakutozaa, hakutaka kupita tena hapo. Lakini Bale hajamfukuza, wala kumtaka mtoto. Hisia zilishajichanganya. Akawa haelewi tena nafasi yake. Na upendo ukishazidi mahali, ni rahisi kujisahau.

Bale akaondoa gari. Kimya kikazuka garini. Wakati wanakaribia chuoni, Bale akamtizama. “Najua umekusudia kutorudi tena kwangu. Naelewa kabisa na nipo kwenye kukubali kila adhabu Mungu anayonipa.” Vai akamtizama kwa mshangao. “Na mimi hii hali ya upweke na kukataliwa, nilijitakia. Nilichagua kwa maamuzi yangu mabaya. Sina wakumlaumu. Ila nataka ujue, nakushukuru kutoka ndani ya moyo wangu. Umeyabadili maisha yangu kwa kiwango chake. Najua nisingekuwa hivi nilivyo bila wewe. Ulikubali kupitishwa kwenye maisha yangu ukaweka mabadiliko.” Vai akatulia.

“Kuna mtu alinisaidia kwa kuniambia hivi, mimi ni zaidi ya huu mguu uliopotea. Na wewe upokee hiyo. Wewe ni zaidi ya hicho unachojisikia moyoni mwako na kufikiri huna uwezo wa kukipata. Na hata kama ukishindwa kupata mtoto, usipotelee kwenye hilo. Una uwezo wa kuzaa vitu vikubwa zaidi ya mtoto peke yake. Wewe ni mtu mzuri sana Vai. Umenitoa sehemu mbaya, ukanipa faraja. Unajua kuridhika hata na vitu vidogo. Umejawa na furaha na utulivu wa aina yake. Unazalisha amani na utulivu sehemu isiyo na tumaini kabisa.”

 “Kwa hiyo kabla hujafikiria kumpa mwanaume mtoto, jua unauwezo  mkuwa sana wa kufanya jengo likawa nyumba, sehemu ya mtu kukimbilia na akawa salama. Kitu ambacho nimekua, sijakiona hata kwetu. Wewe unao uwezo huo Vai. Nilikuwa nikizitizamia siku au muda wa wewe kuwepo pale kwangu kwa shauku sana. Maana ulijua kuweka hali ya utulivu, furaha wakati wote, na amani. Huna hasira, hujui kunung’unika hata kwenye ugumu. Kwa hakika naumia unaniacha. Lakini sina jinsi.” Vai akatulia kimya. Bale akamfikisha chuoni kwao. Akaanza kushusha vitu vyake vyote akirudisha chumbani kwake mpaka akamaliza, kisha akarudi kumuaga. Akamuhisi alikuwa akilia peke yake garini japo hakumkuta na machozi.

“Mungu hana hasira na wewe Bale. Alishakusamehe. Na naamini atakupa mwanamke mzuri tu maana hata wewe unalipa.” Bale akacheka akimtizama. “Umeanza Vai.” “Kweli. Kwani uongo? Unalipa Bale. Na unajua kujali sana. Binafsi sijawahi pata mtu anayenijali kama wewe, mpaka najuta uchafu wangu wa zamani. Natamani kama na mimi ningekuwa…” Akasita.

“Acha nikupishe tu, ili uweze kufikia ndoto zako. Tusipotelee kwenye njia itakayotufanya tushindwe au iwe ngumu zaidi kutoka huko pindi muda wakutakiwa kutoka ukifika. Mimi nimeshapitishwa hapo zaidi ya mara moja. Ni chungu mno. Na najua umuhimu wa familia. Ikishafikia muda wa watoto wanahitajika kwenye familia, kunakosekana amani kabisa. Hata upendo mdogo unakuwa unapotea. Nitapita hapo na yeyote, ila si wewe. Kwanza sipangi kuendelea kufanya huo mchezo. Nishajua nilicho nacho na ambacho sina. Sitarudia kujiumiza tena.”

“Jipe tu muda. Mungu atakupa haja ya moyo wako. Mke mzuri na watoto wazuri. Usirudi kwenye swala la kama Mungu amekusamehe au la. Anaendelea kukuadhibu au la! Umesamehewa. Na najua ipo siku utarudi kuiangalia hii siku, utajua nilikuwa nikikutakia mema. Nataka upate unachotamani. Sitaki kuwa mbinafsi. Na kwa kuwa mimi naelewa unachokitaka kwa kukiishi, acha tusipoteze muda.” Bale hakujibu kabisa. Akabaki kimya, mpaka mishipa ya kichwa ikawa imemsimama. “Kwa kheri, Bale.” Vai akaondoka, Bale akimtizama.  

Kwa Colins&Jelini.

Wakatafuta namba mpya ya Jelini, Colins akawa wa kwanza kuipata. Akajipigia na kuitunza kwenye simu yake. Wakamtafuta fundi mbao ambaye wanafahamiana kwa muda mrefu tu na ndiye aliyejengea makabati mapya ya kisasa hapo kwao. Akamuelekeza, wakakubaliana mpaka rangi, na bei ikawa nzuri tu. Jelini akaridhika.

“Naomba na mimi unisindikize.” Jelini akakubali bila ya kufikiria. Wakaongozana mpaka sehemu wanayouza fast food na ice cream. “Mimi huwa nilazima nile kila mlo. Lasivyo akili huwa haifanyi kazi, hata James anajua. Sipitishi mlo hata mmoja.” “Pole nilikusahau. Akili haijatulia.” “Bado tu?!” Jelini akanyamaza, wakashuka garini, wakatafuta sehemu ya kukaa.

“Utakula nini? Na ‘sijisikii’ naomba isiwe jibu, Jelini. Ili kuanza upya unahitaji akili na nguvu. Usijitese na njaa wakati wenzio maisha yao yanaendelea kama kawaida. Na si kwamba napuuza kuumizwa kwako, lakini nataka uvuke hapo. Wewe sio wakwanza kuweka tumaini sehemu isiyo sahihi. Utakuwa sawa tu. Ila unatakiwa kujipanga.” Jelini akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu, akajisikia vizuri. Akatulia. 

          “Nikuagizie nini?” “Kwa sasa sijis..” Akabadilisha maana alimwambia hilo si jibu. “Naona nitakula jioni nyumbani kwa Jema. Sasahivi tumbo lipo kama limejaa gesi hivi! Acha litulie. Nahisi nikiweka kitu humo ndio nitajiumiza zaidi.”  Colins akamtizama na kuondoka pale kwenda kuagiza chakula. Baada ya muda akamuona anarudi na ice cream. Akakaa pembeni yake wala si mbele. Akabaki akimwangali tu.

          Akaifungua na kuchota na kijiko, akamnyooshea kama amlishe. “Hiyo ni ice cream yangu au yako?” Akauliza kabla hajafungua mdomo. “Naomba kula, Jelini!” “Siwezi kushiriki kijiko na wewe Colins. Nina wasiwasi wakupita kiasi. Mpaka nikajipime tena.” Colins akabaki akimwangalia. “Kumbuka maisha niliyokuwa nikiishi Colins. Watu kama mzee Kasa na tabia zao, ndio walikuwa washikaji zangu baa. Nayajua maisha wanayoishi kwa kuyashuhudia. Ni machafu kuliko nitakavyo kuambia. Ngono au kitu alichokifanya Kasa, hata nikitokea kwao sasahivi nikawaambia kuwa ndicho kinacho niliza, watanishangaa sana. Kwakuwa wao ni maisha yao ya kawaida sana.”

    Wake kwa waume hilo si kosa lakusema wanaachana au kugombana. Ni maisha ya kawaida sana, na jamii wameyakubali. Ndio maana mimi nilikuwa nikinywa nao, nakuogopa sana kulala nao. Sikuwahi kukubali kushawishika kwenye hilo. Ni malaya, na ngono ni starehe ya kawaida kama kunywa soda na kusahau hata aina ya chupa waliyotumia kunywea. Ni kama kunywa hapohapo na kuagiza ingine. Niliishi nao nikishuhudia wakifanya ngono kama wanyama.”

    “Vyooni huko baa na kwenye magari yao huku wakijisifu sio sabuni kwamba imeisha, nakushindwa kupeleka nyumbani. Ikanitia kinyaa cha mapenzi, nikabaki kula na kunywa nao tu, huku nikishuhudia miongoni mwao wakisambaza vijidudu vya UKIMWI kwa makusudi.”

    “Kwamba kuna waliokuwa wameathirika miongoni mwao tayari!?” “Kabisa Colins. Na kusambaza kwa makusudi. Ndio maana japokuwa mimi ni hovyo sana,..” “Wewe si hovyo.” Colins akamkatiza kwa haraka. “Ninachotaka kusema, kwa udhaifu wowote nilio nao, linapofika swala la kufanya mapenzi, hapo nimechora mstari. Sina kuzembea. Maana nimeshuhudia kwa macho madhara yake. Starehe ya dakika 5 inaweza kubadili maisha yako yote hata mafanikio uliyonayo yakageuka kuwa machungu.”

    “Nilijipima siku nilipoamka kwa Kevin nikiwa sijitambui. Nikiogopa sana inaweza kuwa nakuwa hivyo halafu japo nawakataa nikiwa sijalewa, nikilewa nikiwa sijitambui pengine wananifanyia mambo mabaya, sijijui.” “Na nilimsisitiza Kevin asije akakosea akakugusa kwa namna yeyote ile kimapenzi.” “Nashukuru Colins. Maana angeweza nifanya chochote na nisijue. Na nilijichunguza nilipoamka, ukweli hakunifanya kitu. Ila nilikwenda kupima. Sasa safari hii najipa miezi mitatu, nikapime tena kujihakikisha Kasa ameniacha bila maambukizi yeyote yale. Tafadhali tusitumie kijiko kimoja. Roho yangu itaniuma sana na sitajisamehe endapo nitakuja kukuambukiza.” Colins akapooza haswa akabaki ameduaa.

    “Kula hiyo ice cream isiyeyuke.” “Ndio maana huna raha?” “Kabisa Colins. Naogopa mno. Na najilaumu kukimbilia kwenye mahusiano na Kasa bila kumchunguza. Nimejawa hofu, yakujitakia mimi mwenyewe.” “Pole. Ila nadhani yupo makini kwenye mambo yake. Hawezi akawa anajiachia tu.” Jelini akakumbuka jinsi Kasa asivyopenda kondumu ndio maana anapima na kila mtu anayefanya naye mapenzi! Akakumbuka yeye alimpima mara moja tu, hakurudia kumpima tena. “Sasa na huyo Koku anamaisha yake. Akirudi wanaendelea walipoachia. Nimejiua kwa ujinga wangu mimi mwenyewe!” Akazidi kuingiwa hofu kila akikumbuka jinsi alivyojiachia kwa Kasa. Akajua inamaana na kwa Koku ni hivyo hivyo, penzi bila kikomo, wala kinga. Akazidi kunyongea.

    “Niangalie Jelini.” Ndipo akarudisha akili pale. “Usiogope.” “Siwezi kujisaidia Colins. Wewe Ukimwi unausikia kwa watu, mimi nimeishi na mtu mwenye vijidudu vya UKIMWI. Nikaona jinsi anavyoteseka kihisia akiwa wala si mgonjwa. Ana kila kitu. Nikisema kila kitu, kwake na alivyo peke yake, naweza kusema amefanikiwa haswa. Lakini amejawa hofu. Hawezi kulala bila pombe kichwani. Na amejawa uchungu moyoni, ndiye huyo anayesambaza kwa kila anayemsogelea. Ukimwangalia hivi, huwezi sema anavyo hivyo vijidudu. Mzuri na afya nzuri tu. Ndio maana nilikuwa nikijihami.

    “Wale watu walikuwa wakisema kuonja sio mbaya. Sasa hebu fikiria, ni wangapi wameonja kwake, na kupeleka huko wanakokula? Na huko wanakokula kwa wenza wao nao wanaenda kuonjwa na wengine, na hao wengine wanapeleka kwengine. Havijamfikia mtu kama Kasa kweli, tena mwenye pesa na kujua kuhonga vile? Mimi je?” “Acha kujitia hofu zaidi Jelini bwana!” Jelini akajifuta machozi.

    “Sio kujiogopesha. Nakumbuka dereva wake siku moja aliropoka nakusema huwa analeta wasichana wengine pale kwake, lakini huwa hatoki kuwapokea kama mimi.” “Jelini!!” “Kweli Colins. Sasa sasahivi ndio najiuliza nilijiachia vipi! Na kujiaminisha vipi? Maana nilimuuliza, akasema atabadilika, tubaki peke yetu.” Colins akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu.”

    “Sasa nisikilize Jelini. Huna njia yakubadilisha nyuma ila kuanzia sasa. Tulia mpaka muda uliojiwekea ufike, nitakusindikiza kupima.” “Na kama nimeathirika?” “Hiyo ni kesho. Naomba tuishi leo. Na najua ukiwahi, unaweza kuanza kutumia dawa na ukaishi vizuri tu. Namfahamu mtu anayeishi na hivyo vijidudu. Ila yeye nimesikia akisema, ameacha kabisa kujamiiana. Anazingatia mlo na dawa. Ukimuona hivi, huwezi kujua aisee. Yupo safi, ila mwenyewe ameamua kujitangaza. Hafichi. Na ana maisha mazuri tu. Naomba utulie. Sawa?” Jelini akavuta tena pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu Colins akimsaidia kufuta machozi.

    “Naomba ule hii ice cream. Fungua mdomo mimi nitakuwekea.” Jelini akacheka. “Sio kwamba ndio nina hali mbaya kiasi hicho bwana! Naweza kula mwenyewe, ila sijisikii.” Akasimama na kwenda kuchukua chakula. Akarudi na chakula alichoagiza ila mara mbili yake, na ice cream nyingine mbili na vijiko viwili. Ile ya mwanzoni akaitupa na kurudi tena pale. “Unataka tukae hapa tule au tukale kwenye gari?” “Ningependa kwenye gari zaidi.” “Basi twende wakati ukila hiyo ice cream isiyeyuke tena. Haitakuwa nzuri.” Wakatoka akiwa amebeba vyakula, Jelini anakula ice cream.

    “Kuna sehemu sio mbali sana na hapa. Patulivu, tunaweza kwenda egesha gari tukala kwa utulivu.” Colins akakubali, wakatoa gari mpaka hiyo sehemu. Akamkabidhi maji na chakula. “Sikujua ungependa kinywaji gani, nimekuchukulia maji tu.” “Nashukuru.” Akapokea, wakaanza kula huku wakisikiliza mziki. “Una nyimbo nzuri Colins! Zinakufanya unatulia.” “Nimefurahi kama na wewe umependa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    “Nikuulize kitu Colins?” Colins akamwangalia. “Juu yako na Love.” “Unataka kujua nini?” “Ni katika kujifunza tu. Mmekuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi kwa muda gani? Na mlikuwa na malengo gani?” “Baba yangu na baba yake walikuwa shule pamoja pale Muhimbili. Kwahiyo na sisi tukakulia pale kwenye magorofa ya Muhimbili. Tulikuwa pamoja  tokea shule ya msingi. Wazazi wakaamua kujiendeleza shule. Ni marafiki tokea vijana. Tukajikuta tuko pamoja tena huko ugaibuni. Tukaanza tena shule huko nje ya nchi. Pamoja tena, wote tukiwa watoto wa kwanza kwenye familia zetu, na kina mama marafiki. Kina baba walipomaliza, kina mama walipoona elimu ya huko ni nzuri, wao wakabaki na sisi ili kumaliza shule. Kwa hiyo tukaishi tena nje ya nchi pamoja na kina mama nao wakaanza masomo ya unesi.”

    “Sisi tulipoanza chuo kwa shahada ya kwanza ndipo tukaamua kujaribisha mahusiano ya kimapenzi. Wakati tunakaribia kumaliza, kina mama, Connie pamoja na mdogo wake Love, wakarudi nchini. Nikabaki naye huko. Ilikuwa mbaya sana. Hatujawahi kupitia wakati mgumu kama huo. Tukajua kabisa, hatutaweza kuja kuona.” “Kwani mliishi pamoja?” Colins akawa kama anayefikiria jinsi ya kujibu hilo swali.

    “Tulipoachwa sisi wenyewe tukiwa chuoni, tukajiamulia tuchukue apartment moja yakututosha sisi. Yalikuwa maisha mabaya sana, lakini ilitusaidia kujua hatima yetu. Ikawa tena tunabaki kwenye mahusiano sababu ya wazazi. Anyways. Akataka kufanya kazi kule baada ya kumaliza chuo, mimi nikawa nimeshachoka maisha ya kule, ndio nikaja kuanza kufanya kazi huku. Ikawa anakuja likizo na kurudi. Akapata kazi anayofanya sasahivi kwa ahadi ya mshahara mkubwa sana. Na kwa kuwa alishafanya kazi kule, ilikuwa rahisi kuzungumzia mshahara mkubwa. Ndio akarudi nchini sasa.”

    “Tukajaribu tena, lakini binafsi nikaona nitapoteza muda wake zaidi. Siwezi kuwa kile anachotarajia. Hakuna kitu ninamfanyia kikawa sahihi, na nafikiri nilikueleza. Mapungufu mengi akawa anayalalamikia, na mimi nikachoka. Nikiwa katika hiyo hali ya kuchoka, nikagundua kumbe na mimi naweza kupendwa zaidi ya muonekano wangu ambao na mimi nadanganywa na wengi tu, wakivutiwa na muonekano wangu.” Jelini akainama kwa aibu. Maana kweli Colins alivutia machoni.

    “Nilipoona nashikilia sehemu ninayoumia, wakati naweza kupendwa na nikatulia, ndipo nikaona nisiendelee kujipunja. Nikahitimisha. Ila malengo ilikuwa kuwa na familia kama wazazi wetu. Inamaana kuja kuoana na kuanzisha familia pamoja.” “Alichukuliaje ulipomwambia unahitimisha?” Jelini akarudia swali akitaka uhakika. “Alisema sawa, Jelini. Unakumbuka nilishakwambia?” Jelini akatulia akiwa kama hajaridhika maana amemuona nyumbani kwao.

    Akaamua kuuliza tena. “Kwahiyo sasahivi yupo kama nani?” “Kama mtoto wa nyumbani. Love ni kama mimi pale kwetu, na mimi ni kama kijana wa nyumbani kwao tu. Tumekua pamoja  na wazazi wetu ni marafi mno. Jinsi baba zetu walivyosoma pamoja, ndivyo mama zetu wakaja kusoma tena pamoja, elimu ya utuuzimani. Ila mama yake Love alikuja kujiendeleza zaidi. Mama akashindwa akitaka kumlea Connie. Hawafanyi kitu bila kuambizana na kila kitu wanafanya pamoja japo baba sasahivi amehamia kwenye mambo ya moyo. Ila wenyewe wanasema ni faida yao wote. Wanaongeza utaalamu kwenye kliniki yao.” “Kwamba wana hospitali yao pamoja!?” “Sio hospitali ni kliniki. Hawalazi. Ni kuona tu wagonjwa.” “Mmmh! Nyinyi mngeoana tu ndio ingependeza.”

    “Kila mtu alifikiria hivyo. Lakini mwishoe kila mtu akatuchoka. Yaani kutengana kwetu ikawa tena pumziko kwa kila mtu kwenye familia. Walishatuchoka kwa mashitaka ya Love. Na mimi nilikuwa sina raha! Nahangaika kama anayekimbiza upepo! Ikatosha.”

    “Swali la mwisho.” Colins akacheka. “Naona umeniamulia! Haya uliza.” “Kwa maisha uliyoishi na watu wanaokuzunguka. Hivi kweli wewe utakuja kuoa au kuwa na mwanamke ambaye sio msomi kweli?” “Kwa haraka, sijui. Maana nilijaribu na msomi, ikashindikana. Ikaniashiria mapenzi si shule. Si kile mlichobeba kichwani ila moyoni.” Hapo Jelini akatulia. “Umeridhika?” Jelini akatingisha kichwa kukubali na tabasamu.

    “Ukitoka hapa unampango wa kwenda wapi?” “Maisha ya kazi yanaanza rasmi kesho, Colins. Nataka kujiandaa. Kufua na kuweka kila kitu sawa kabla ya jioni sijaenda kwa Jema. Si na wewe utakuwepo?” “Wewe ulitaka niwepo?” “Mimi nafurahia kampani yako Colins. Ningependa uwepo. Ila kama una..” “Nitakuwepo. Nishamwambia James nitakwenda na si nilikwambia hata kina mama waliahidi watapitia?” “Nakumbuka.” “Basi tutakuwepo wote. Kuna kitu unataka kabla sijakurudisha nyumbani?” “Hapana. Ila nashukuru kwa chakula. Najisikia vizuri.” “Usiache kula bwana! Utanyongea. Na punguza hofu. Naamini kila kitu kitakuwa sawa.”

    “Najihisi nimejipokonya tonge mdomoni, Colins.” “Kwa nini?” “Mwenzio zamani nilikuwa hata siwazi mambo ya kesho. Mambo ya mipango mizito! Hapana. Nifurahi leo, kesho itajijua yenyewe. Lakini kadiri nilivyokuwa nikimwangalia Jema na James, tamaa ya kuwa na walichonacho ikanipata. Eti na mimi nikatamani niwe kama Jema na mtu wangu na familia yangu. Lakini najifikiria kama nimeathirika, hayo yote ndio basi tena!” “Naomba usifikirie huko. Bakia kwenye hii shauku yako.” “Siwezi kuepuka Colins. Sitaki nijipandishe mukari halafu nije nijikute siwezi kuvipata vyote hivyo! Acha nitulie mpaka nijue hatima yangu. Na asante kunisikiliza. Naona upo sahihi. Nikizungumza hivi na wewe, angalau napunguza hofu.”

    “Basi muda na wakati wowote unapojisikia kuzungumza na mtu, nipigie. Hata kama ni usiku, mimi nitakuwa na wewe. Na naomba tena, Jelini. Najua ni ngumu. Lakini naomba upunguze hofu. Ukianza kujisikia hofu, tafadhali vuta kumbukumbu kwenye unaloweza kufanya. Au furaha fulani ili kutoa mawazo kwenye hofu. Usikae kwenye hofu kwa muda mrefu.” “Nitajitahidi. Twende na wewe ukapumzike.” “Mwenzio hata ukiniambia nikae na wewe mpaka usiku, sitachoka.” “Kweli Colins?!” “Si nimekwambia nataka kuwepo ulipo?” “Hujachoka kusikiliza matatizo?” “Nataka matatizo yako nikusaidie kuyabeba. Usiwe peke yako.” Jelini akamwangalia na kutulia.

~~~~~~~~~~~~~~~

    Akaondoa gari na kutoka hapo kurudi nyumbani kwa kina Jelini. Akadhani anamshusha aondoke, akashangaa anaingia naye ndani. “Ndio unajiandaaje kwa kazi?” “Nafua. Tokea nitoke safari sijafua.” “Unafulia wapi?” “Nje. Ingekua mama hajaninyima hela, ningeshamuita mtu ninayemlipa anifulie.” Jelini akanong’ona, mama yake asisikie. “Kwani huwa hufui?” “Sipendi. Ila acha tu nifue.” “Kwetu kuna mashine ya kufulia. Chukua nguo chafu zote tukafulie kwetu.” “Mwache afue huyo. Hivyo humsaidii.” Wakamsikia mama Jema akizungumza kutokea chumbani kwake. Wakanyamaza gafla wakiangaliana.

    “Umesikia we Jelini?” “Kama una nguo chafu nitolee nifue na za Jeremy mara moja.” “Uje uchukue huku chumbani.” Akaenda akicheka. “Kwani kusaidiwa ni vibaya mama jamani!?” “Utasaidiwa mpaka lini Jelini, mama yangu? Si umesema unataka kuwa kama Jema? Ndio anza kwa kuanza kujitegemea. Acha misaada ikukute upo njiani na umesimama. Unataka kuanza tena maisha mengine, halafu vikiishia katikati uanze tena kulia?” “Basi mama. Naenda kufua mwenyewe. Nipe hizo nguo zako na za Jeremy.” Akamtolea nguo, kweli Jelini akatoka nje na nguo zote. Akatafuta kivuli, akakaa kabisa.

    Colins akamfuata. “Pole.” Akaanza kucheka. “Mwenzio huwa sifuagi. Na sipendi. Nilikuwa nikiwa na kijihela changu, namuita mtu ananifulia na kunipigia pasi kabisa. Acha tu nifue. Kwanza hizi sio nyingi. Nitamaliza sasahivi. Wewe nenda kapumzike.” “Acha nikae hapa. Nikuwekee mziki wakati unafua.” Ikaanza kazi ya kufua na mziki. Colins anaenda ndani kumuangalia Jeremy, anarudi nje kwa mama yake mpaka akamaliza.

    Baada ya kuanika, wakahamia chumbani kupanga. Jua kali na uchovu, Colins akajilaza kitandani na simu yake akibadili nyimbo, Jelini anapanga chumba mpaka akamaliza. Akaenda kuoga chumbani kwa mama yake, akarudi ameshavaa, Colins bado yupo amejilaza kitandani kwake, haondoki.

    Akajipandisha na yeye kitandani. Colins akajisogeza. “Pole, najua umechoka.” “Nasikia na usingizi.” “Njoo nikubembeleze ulale.” Jelini akaanza kucheka. “Nakuahidi utalala vizuri.” Jelini akageuka kumpa mgongo. Akavuta mto juu ya kichwa chake, akawa kama anamchungulia kwa chini, ila karibu kabisa, Jelini akizipata pumzi zake sawia. Akaanza kumpapasa mkono kwa juu mpaka karibu ya bega. Ile kuguswa tu na Colins, kuwa karibu yake vile, roho ya Jelini ikatulia kabisa. Hapo hapo wote wakapitiwa na usingizi mpaka hodi ya mama Jema ikawatoa usingizini.

    Saa moja usiku, nje kumeshakua giza! Kuangalia, wamelala hapo kitandani kwa Jelini wamekumbatiana ila Jelini amempa mgongo vilevile. Colins akambusu karibu na sikio na kumsisimua vilivyo, akatoka akiaga anakwenda nyumbani kwake kuoga, watakutana nyumbani kwa Jema. Jelini naye akawahi kujitayarisha.

~~~~~~~~~~~~~~~

    “Mimi sielewi Jelini! Sasa huyu kijana amehamia hapa au?” “Mimi sijui ila namfurahia.” “Jelini wewe mtoto?!” “Mimi hata sijielewi. Lakini nilikuwa nampenda hata kabla ya Zenda.” “Jelini! Imekua kumpenda tena?” “Si kihivyo mama jamani! Ila napenda kuwa naye. Ndio wakati ule akasema ana mtu wake na wewe nilikwambia kabisa.” “Mimi ningeshauri utulie kwanza ujue hitimisho la Zenda.” “Hitimisho gani tena?! Kwanza si Zenda, ni mzee Kasa.” “Angalau pata muda wa kujifikiria kabla hujaanzisha kingine.” “Mimi sianzi jambo lolote na Colins.” “Sasa usikasirike.” “Naona na wewe unataka kumfukuza kama mzee Kasa alivyomfukuza! Mimi sipendi mtu amfukuze Colins.”

    “Kwa hiyo ulikuwa na Zenda huku mawazo yapo kwa Colins?” “Mimi sijui. Ila naombeni mumuache Colins. Ananipa moyo na…” “Kukuweka mkononi?” Mama yake akamkatiza kwa kumalizia kwa swali akimkejeli, akimjua jinsi anavyopenda mikono. “Mimi nataka kusema yupo na mimi wakati ninaomuhitaji bila kuchoka. Mtu asimfukuze. Nitafanya kila kitu utakachoniambia ila si Colins.” Jelini akaondoka na kumuacha mama yake akimtizama.

~~~~~~~~~~~~~~~


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment