Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 38. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 38.

Colins nyongo mkalia ini. Jelini hajiwezi, hajitambui kwake. Ni Colins aliyekwisha teka moyo wake, hajui anaishije na hilo. Alipomuona amekwama, akajirudi mwenyewe moyoni. “Twende Colins.” Colins akamwangalia kama ambaye hajasikia au kuelewa sawasawa. “Turudi wote tu nyumbani kwenu. Tutakuwa wote.” “Nashukuru. Na naomba usiwe nawasiwasi na watu wengine, ila mimi. Usikimbie makosa yako wala usizike mawazo yako au changamoto zako kwa pombe. Jifunze kupambana Jelini. Na mimi nitakuwa na wewe. Muda na wakati wowote unapotaka kuzungumza na mtu. Au ukiwa na kitu moyoni, nipigie, mimi nitapokea simu yako.” Kwa haraka sana akawahi kuziba nafasi ya Zenda aliyesimuliwa alikuwa akipigiwa muda na wakati wowote na kucheka sana. Jelini akacheka taratibu kama anayefikiria. “Nakuahidi kusimama na wewe Jelini.” Akaweka msisitizo akibembeleza. “Nashukuru. Basi twende tusiendelee kumuweka mama.” Wakaondoka hapo, safari ya kurudi Mbezi, Tangi bovu ikaanza tena. Wote kimya kwenye gari mpaka kwao.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakawaona wanaingia. “Kazi ipo!” Akaongea mama Jema, na kumfanya Jema acheke akiwaangalia. Wakawasogelea. “Hizo nguvu unazozitumia ungeziweka kule kwenye kupambania maslahi yetu, sasahivi tungekuwa tukilipwa mishahara ya kutisha sana hapa mjini.” Colins akacheka akikaa. Hapohapo akaitwa na mama yake. Akasogelea sikio la Jelini aliyekuwa amekaa pembeni yake. “Hapa nilipokuacha, usiondoke mpaka mimi mwenyewe nikurudishe nilikokutoa. Sawa?” Hayo maelezo anayotoa kwa kunong’ona sikioni kwa Jelini, mwili mzima unamsisimka. “Asiwepo wa kukutoa hapo kwenye hicho kiti, ila mimi mwenyewe. Na nitakuwa nikikuangalia popote nilipo.” Akacheka taratibu na kutingisha kichwa akikubali.

Ndipo akasimama alipopata tabasamu kutoka kwa Jelini. “Hicho kiti pembeni ya Jelini kisikaliwe na yeyote, James.” James akatingisha kichwa kwa masikitiko, yeye akaondoka kwa haraka kuelekea alipokuwepo mama yake. Wakamuona amepewa kazi anaingia na kutoka akimnong’oneza mama yake hili na lile kisha kutumwa tena.  Jelini kimya ametulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Ukawa usiku mtulivu, watu walijua kusherehekea hapo kwa vile wanavyojuana. Ukweli ilipendeza sana na kuvutia. Shuguli zilipomuishia Colins baada ya watu kula na kubaki wakinywa tu huku wakiongeza nyama kwa nafasi, Colins akarudi kukaa pembeni ya Jelini aliyekuwa amempakata mwanae. “Acha nikamlaze.” Akampokea, akaenda kumlaza yeye, na kurudi kukaa pembeni yake. Akamuwekea mkono juu, akamvutia kwake. Jelini akajisogeza mpaka ubavuni, wakatulia.

“Umeshiba?” Akamnong’oneza sikioni. Jelini akatingisha kichwa akimtizama, macho yakagongana. Na vile walivyokuwa wamekaa karibu, moyo wake ukajawa furaha ya ajabu, akarudi kujiegemeza ubavuni. Mambo yakaendelea wao wakiwa watizamaji wakicheka tu.

Baba yake alipochukua kipaza sauti watu wakaanza kushangilia sana. Kina Jema wakawa hawajaelewa. “Kwa nini wanashangilia.” James akauliza. “Pombe ishaingia kichwani, basi anataka kumuimbia mkewe. Ndio kazi yake, wote wanamjua. Huwa wanasubiri akifurahi, aanze kuimba. Baba ana sauti nzuri sana. Tulieni msikilize.” Miluzi ikaendelea kwa wasomi hao kama vijana. Wanaume wote waliokuwa hapo, marafiki wa baba yao ni madaktari wanaojuana miaka mingi.

“Huu ni maalumu kwa mke wangu. Muache kelele asikilize.” Wakazidi kushangilia wakitaka zilipendwa, mama CJ cheko limemjaa. “Nothing’s Gonna Change my love for you.” Wote wakaongea kwa pamoja, wakishabikia kwamba ndio wimbo wanataka aimbe. Wakashabikia mpaka akakubali kuimba huo. Wakamuwekea mlio tu bila maneno. Akaanza huyo mzee kwa sauti yake nzito kama Colins, mpaka vinyweleo vikasimama, maana alianza vizuri sana na hisia zote. Jelini mwenyewe akajitoa ubavuni na kukakaa wima akabaki akisikiliza.

Aliimba huyo baba CJ mpaka akamaliza, watu wote wakasimama. “Kumbe ndio maana!” James mwenyewe akaafiki na kuanza kupiga makofi. Akainama kama anayepokea shukurani za watu akarudi kumbusu mkewe, mziki ukawekwa, wakaingia hapo na wazee wengine ikachezwa twist ya nguvu wakicheka sana mpaka wakamaliza mwaka. Ila mama CJ akataka wote watulie, waombe kwa muda wakiwa wanapokea mwaka mpya. Pakatulia haswa. Wakaomba kwa kumshukuru Mungu wakiukaribisha mwaka mpya na baraka zake zote, ndipo wakaagana.

Mwaka Mpya.

James akaondoka na mkewe. Mama Jema na mtoto wakatangulia na gari ya Jelini aliyokuwa amepewa na aliyekuwa Zenda, akabaki Jelini na Colins. Jelini akasaidia kazi kidogo hapo, vingine wakakubaliana watamalizia kesho yake. Wakatoka Jelini na Colins mpaka nyumbani kwao. Wakaishia ndani ya ua, maana Colins alienda kumfungulia mlango, aliposhuka, akamvutia tena pembeni. Wakabaki wamesimama nje ya gari, Jelini amekumbatiwa vizuri, amejilaza kifuani wanazungumza yao taratibu.

“Kesho tunakwenda wapi?” Akauliza Colins akimchungulia pale alipojilaza. “Mwenzio nabadili maisha. Naanza kufanya kazi. Sijui mama atakua ameamua nifanye nini! Amesema kesho ataniambia na kunipangia majukumu. Na nimemuahidi nitafanya. Nataka na yeye aone mabadiliko. Nimecheza sana.” “Kwani ulikuwa ukifanya nini kabla?” “Kulala.” Colins akacheka na kutulia.

“Mimi mwenzio sijasoma Colins, na sipendi shule wala kufanya kazi. Kuwajibika, au kujishugulisha nimekubali kubadilika. Ila kusoma, sitaki kabisa.” “Si lazima kusoma.” Jelini alishangaa, hakutegemea akamwangalia. “Nakwambia ukweli. Kama kunaunachotaka kufanya kinahitaji kuongeza ujuzi, hapo huna jinsi. Lakini si usome tu kwa sababu kila mtu amesoma! Hapana. Ila lazima kujishugulisha. Na nini, ndio swali la kujiuliza. Je, hicho kitu kinahitaji elimu? Ndipo itakulazimu urudi shule. Ila kama hakihitaji elimu, sasa kwa nini ukasome?” Hapo Jelini akatulia.

“Naomba unipigie mimi simu, mara tu utakapoamka nakujua siku yako itakwendaje.” “Sina simu Colins.” “Simu yako imekwenda wapi?” “Nimeifunga kabisa na sitaki kuiwasha.” “Sababu ya mzee Kasa?” Jelini akatulia. “Naomba tafuta namba ingine ili tuwe tukiwasiliana.” “Naona nitafanya hivyo kesho, kisha nitakupigia.” “Ni sawa nikiweka mpango wa kwenda kuogelea na Jeremy?” Jelini akaanza kucheka akifikiria.

“Wenzio sisi hatujui kuogelea. Kwanza hata hatuendagi bichi. Nilikwenda na Kasa nafikiri mara mbili au tatu tu, napo hiyo siku tuliyopanga kuogelea hata hatukukaa sana, tukaondoka.” “Kwa nini?” “Wivu. Anawivu sana ndio maana sikutegemea kwa msimamo ule, eti mimi ndio nije kumfumania! Ila kujibu swali lako alisema yale mavazi ya kuogelea siwezi kuvaa mbele za watu na kuwaacha waendelee kunitamani. Tukaondoka.” Colins akacheka akimfikiria vile Jelini alivyo, halafu awe na vazi la ufukweni, yaani kinguo tu chakuogelea! Hapo hata yeye akamuelewa Kasa.

“Unafikiri Jeremy atapenda?” “Mwanangu hanaga neno. Bora ashibe.” “Basi nitaenda kumnunulia vifaa vya kuogelea. Ukiniambia muda ambao mpo free, nitakuja kuwachukua.” “Nashukuru kwa kujitoa muda wako na kuwa radhi kuonekana na mimi pamoja na Jeremy. Imenifariji kuona humtengi.” “Alivyo mtoto mzuri vile! Hafichiki wala kutengeka.” Jelini akacheka na kuinama akifikiria.

“Nimefurahi tumemaliza wote mwaka na kuuanza mwaka mwingine pamoja.” “Kwanini sasa unafurahia kuwa na mtu kama mimi, Colins!?” “Sijui unamaanisha nini ukisema ‘kuwa na mtu kama mimi’! Lakini nahisi na mimi nimepatwa na ile hali kama uliyosema wewe uliipata kwangu. Hujui ni kwa nini lakini unafurahia kutoka moyoni ile kunihudumia mimi. Basi na mimi nafurahia kuwa na wewe.” Jelini akamwangalia na kutulia.

“Naomba tujiwekee malengo Jelini?” “Malengo gani!?” Jelini akauliza taratibu akimwangalia ila kwa mshangao kidogo. “Tujipe muda tujue ni nini kinaendelea ndani yetu. Ila.” Hapo akatulia. “Ila nini?” “Ikitokea unaanza mahusiano na mwanaume mwingine au ukiwa unataka kurudiana na mzee Kasa, niombe mimi niwe mtu wa kwanza kujua.” “Sawa.” Akakubali kwa haraka bila shida. “Na mimi itakuwa hivyohivyo. Ikitokea naanzana na mwanamke mwingine, nitakwambia.” Hapo pakawa pagumu kidogo. Akamwangalia na kunyamaza bila yakujibu.

“Kapumzike, tutaongea kesho.” “Asante, usiku mwema.” Wakaangaliana na kucheka kama hawajui waaganaje. Jelini akaondoka. Akamsubiria mpaka akafungua mlango akaingia ndio na yeye akaondoka.

Mambo Mapya.

Jelini akiwa amelala mama yake akamgongea na kuingia. Akatoa chandarua na kukaa kitandani kabisa. “Shikamoo mama.” “Marahaba. Sasa unakumbuka nilikwambia tunabadili gia angani?” Jelini akakaa sawa. “Nipange mama yangu.” “Kwa utayari huo, tunaanza na pesa tuliyo nayo. Ni nyingi tu. Tunaendeleza duka letu vilevile na vitu vya kisasa, na kule ni kama kumekamilika kabisa ila walitaka makubwa tu, ila sisi kwasasa tunafanya tunachoweza ili tusije tumia pesa yote ikaisha.” “Kwa hiyo mimi ulitaka nifanye kazi gani?” “Dukani tumepata watu wazuri na wanapawezea. Ni kuwafuatilia, zaidi pesa ili wasiingiwe tamaa wakaanza wizi au kubweteka. Halafu tuhamishe nguvu pia kwenye kuuza mitungi ya gesi, majiko, Luku na..” “Mama wewe una mambo mengi! Pesa itatosha kweli? Si tuanze na vichache kwanza!” “Pesa tulionayo si chache!” “Hata sijui ni kiasi gani.” “Ni..” Akamtajia na kumshangaza sana Jelini.

“Mama wewe! Kwani yule mzee alikuwa akiweka pesa kila siku!? Mbona nyingi hivyo!” “Si Zenda tena!?” “Akuu! Hana uwezo wa kuwa Zenda hata kidogo. Achana naye.” “Hutajuta?” “Mwenzio nimekuwa na tamaa ya alichopata Jema, mama. Kwake kumetulia! Mwanaume anampenda! Na mimi nataka mama. Hizi pesa na mabwana wasio wako havina raha. Starehe tu, ambazo si za kudumu! Mmmh! Sitaki tena. Vinaishia kukuumizwa tu. Mimi sitaki tena.”

“Kwa hivi nilivyokuona, sasahivi najua unaweza Jelini. Eti mimi nilikuwa na wasiwasi na wewe kuliko hata huyo Kasa. Lakini ikawa tofauti!” “Ujue mama mimi sio malaya kabisa. Kwamba nataka kuvulia kila mwanaume nguo! Kwanza nina kinyaa mama. Na yeye ndicho alichoniumiza nacho. Nafikiria jinsi alivyonichanganya na malaya zake! Hapa nasubiri miezi mitatu ipite nikapime tena Ukimwi, nitulie kabisa.” “Bora.” Mara simu ya mama Jema ikaanza kuita.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Nani mbona umekunja uso?” “Hata sijui.” Akapokea. “Mimi ni Colins, nipo hapa getini. Naomba uwaambie wanifungulie. Si naweza kuingia?” “Karibu Colins, nakuja.” Jelini akaruka kitandani kukimbilia bafuni baada ya kusikia ni Colins, tena yupo getini! “Kazi ipo.” Mama Jema akaonge akitoka. Wakati akivaa akamsikia akizungumza na Jeremy. Akimuuliza maswala ya shule na kutaka kujua kama anapenda kuogelea. “Mimi sijui kuogelea.” Akamsikia Jeremy akimjibu. “Ungependa kujifunza?” Hakusikia mwanae akijibu. “Unaogopa?” “Sijui!” Akajibu kama ambaye hana uhakika.

“Mimi najua sana kuogelea, na ninapenda. Tunaweza kuingia wote kwenye maji. Nitahakikisha hauzami.” Kimya. “Na tutakuwa na mama.” “Na yeye atakuwepo kwenye maji?” “Sijui kama atapenda. Lakini pia sio lazima ikawa leo Jeremy. Kama leo hujisikii kuogelea, tunaweza kufanya wakati mwingine.” “Basi tufanye wakati mwingine.” Jelini akashangaa sana huko alipokuwa chumbani. Hakutegemea kama mwanae angekataa. Bibi yake huko jikoni kimya akisikiliza.

“Unataka nikuitie mama au bibi?” Akamsikia Jeremy akimuuliza kama yeye anataka kuondoka. “Wewe unaondoka?” “Nataka kurudi chumbani. Kuna kitu changu nafanya.” “Ni nini unafanya?” Jelini akamsikia mwanae akianza kucheka kama anayesita kusema.

“Ni nini?” Akamsikia Colins akimuuliza. “Nataka nisimwambie mtu mpaka nifanikiwe kwanza.” Colins akacheka. “Unatengeneza?” “Ndiyo. Lakini…” Halafu akasita. “Pengine naweza kukusaidia.” “Kwanza sina uhakika. Nilipewa zawadi na mama. Bibi aliniletea kwenye mfuko. Nilipofungua, nikakutana na vitu pamoja na kijitabu kidogo chenye picha mbalimbali. Kwa jinsi nilivyosoma, ni kama ni maelekezo ya kuweza kujenga zile picha kwa vile vitu vidogovidogo vilivyopo hapo. Ndio nasoma na kujenga.” “Jeremy wewe unaakili sana. Sasa umefikia wapi?” Akacheka kama anayesita.

“Sina uhakika sana.” “Usisite. Wewe niambie tu.” “Kwa jinsi nilivyoona, na kuanza kujenga ni kama treni na reli. Nimefanikiwa kutengeneza reli. Nahisi nimefanya ndefu sana. Sitaki kubomoa, nahisi labda nikijenga na treni, pengine itakua kubwa itahitaji hiyo reli ndefu. Sasa kwa kuwa sijawahi kuona hata mara moja, ndio najaribisha. Nifanye mpaka nione mwisho bila kubomoa reli kwanza.” Jelini mwenyewe akashangaa ni nani amempa hiyo zawadi maana na yeye mwenyewe ndio anasikia.

“Mimi mwenyewe nimeshaanza kuvutiwa. Naomba nikaangalie. Sitakuingilia.” “Najengea chumbani kwangu, bado bibi hajanirudishia kitanda, kulikuwa kunajengwa. Hamna hata sehemu ya kukaa. Mimi najengea chini tu sakafuni, halafu usiku nalala na bibi.” “Na mimi nitakaa sakafuni.” “Kweli!?” Akauliza akicheka na mshangao juu. “Kabisa.” Colins akajibu. “Ila usiwe na wasiwasi. Nipasafi, bibi alisafisha vizuri tu, ila bado hakujarudishiwa vitu vyangu. Twende nikakuonyeshe.” Jelini akatamani kutoka kwa haraka, ila akaona awape muda kidogo.

“Natengeneza kwa kuangalia picha.” “Na hivyo ndivyo anavyotakiwa.” Wakawasikia wakizungumza wakielekea kwenye chumba ambacho ni cha Jeremy. Na hicho mama yake alikibadilisha vizuri sana. Sakafu ilibadilishwa ikawekwa ya marumaru inayofanana na chumbani kwake na bibi yake. Akamvutia choo ili apate cha kwake peke yake. Madirisha yalishajengwa na kuwekwa vioo vizuri na makabati ya ukutani akawa ameshajengea. Akafunga feni na A/c ndogo tu. Akawa anataka kumnunulia kitanda kipya, meza na kiti chake cha kusomea, na meza yenye kioo kwa ajili ya kuweka vitu vyake vakutumia baada ya kuoga.

Wakaingia huko, mlango ukafungwa, kimya. Jelini akatoka kwenda kwa mama yake. “Ni zawaidi gani hiyo!?” “Alinipa Zenda ulipokuwa umelazwa, akaniambia nimpe, nimwambie inatoka kwako. Nilikuwa na mambo mengi wala sikutilia maanani. Nikamkabidhi mfuko mzima bila hata kuangalia, nikaendelea na yangu. Kumbe mwenzangu ukimya wote huo anakua ndani anajenga treni!” Jelini akutulia akifikiria.

“Ila Jeremy nimemsifu! Akifanya jambo lake hataki kuyumbishwa! Kakataa kuogelea ili amalizie mambo yake!” “Mimi mwenyewe kanishangaza! Sikutegemea kama angekataa kwenda kuogelea! Nilijua angefurahi kweli!” “Lakini mwache. Usimuingilie. Mwache mpaka awe tayari.” Jelini akatoka kwenda na yeye kuangalia.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akawakuta wamekaa chini kabisa sakafuni, wakamwangalia alipoingia, akaenda na yeye kukaa hapo akiangalia. “Umejenga vizuri Jeremy!” “Najaribu mama. Nataka itokee kama kwenye hii picha. Nina uhakika picha zote hizi unazoziona hapa, zinatokana na hivi vipande hapa. Nikifanikiwa kuviunganisha kwa usahihi, vitatokea kama kwenye hii picha.” “Unafanya vizuri. Mimi sitakusumbua.” Akarudisha akili kwenye hivyo vijipande vingi vimekusanywa kwenye boksi kubwa tu vya kutoshea. Jelini mwenyewe akachoka. Kwamba akusanye pale mpaka vitokee treni! Akapotelea mawazoni.

Colins akamgusa. “Ulilala salama?” Akamuuliza Colins, lakini Colins akamfanyia ishara aache kuongea. Jelini akacheka na kumtizama Jeremy. “Tutafukuzwa hapa.” “Nikusaidie Jeremy?” “Muache mtoto bwana!” Jelini akaanza kucheka. “Nilikuwa namchokoza aniangalie.” Jeremy akamwangalia. “Umekula?” “Nishakula.” “Haya Jelini toka huko. Mimi nakujua wewe kunyamaza hutaweza.” Mama yake akaingilia. Wote mpaka Jeremy wakacheka.

“Wala hujakosea. Maana nilitaka kumuuliza tena, atamaliza saa ngapi ili…” “Haya toka.” Mama yake akamfukuza tena. Jelini akacheka akisimama. “Ukimaliza njoo mwaya tupige stori.” “Muache bwana, Jelini.” Colins naye akaingilia. “Hata hivyo sitamaliza sasa hivi. Ni vingi.” “Jeremy naye!” “Haya toka huko.” Mama yake akamsisitiza. Jelini akawa anatoka.

“Basi Colins wewe njoo hata tusalimiane, ndio uje uombe kusaidia.” “Ulijuaje?” “Nimeona jinsi ulivyokaa hapo kama upewe na wewe ujenge!” “Inanikumbusha utoto wangu sana. Nilikuwa nikijenga LEGO kama hivi, mpaka za roboti. Nilikuwa na meza chumbani kwangu, najaza. Na ndio ilikuwa zawadi ukinipa, tunapatana. Ikajenga ufahamu mkubwa sana kwangu mpaka nikaingia kwenye darasa la Engineering la watoto shuleni.” “Kumbe ndio maana James anakusifia unajua sana kompyuta?” Akacheka na kurudisha macho kwa Jeremy.

“Komputa nimeanza kuchezea tokea mtoto sana. Kwa hiyo hichi anachokifanya Jeremy ni kitu kizuri sana. Baadaye atajua ni vitu gani anapenda, basi ndio kumnunulia aina hiyo ya LEGO.” “Basi wenzio na mama hata hatujui jina lake.” Wakacheka. Jelini akatoka na kumuacha Colins bado akiangalia kama aliyekumbuka mbali.

“Kama unataka  kujenga, njoo tujenge wote.” “Nitakupunja. Mimi napenda sana LEGO. Itanichukua muda mfupi sana kujenga hiyo reli nzima na kumaliza.” “Kweli!?” “Kabisa. Nilikuwa nikijifungia kama wewe hivi. Sitaki kutoka mpaka mama alikuwa akinilazimisha kula. Ndio ilikuwa furaha yangu. Nikazoea mpaka nikawa nafanya za watu wakubwa nikiwa bado mdogo sana.” Jeremy akavutiwa na Colins.

“Kwa hiyo na mimi nifanyaje ili niweze?” “Hivyo unavyofanya ndio sahihi kabisa. Lazima kujua ni nini unajenga, ndio uanze. Tena naona wewe utajua mapema na kuwa mfanisi sana. Umeanza vizuri. Endelea hivyohivyo. Na huwa haiitaji haraka.” “Sasa mbona wewe umesema unaweza kujenga haraka?” “Kwa sababu nimefanya hicho unachokifanya sasahivi kwa zaidi ya miaka yako wewe.” Jeremy akacheka.

“Kwamba nina uzoefu na akili imeshaozea kujenga. Sasahivi najenga vitu vya kweli. Hata ukinipa tatizo kubwa kiasi gani juu ya mitandao, kompyuta, macho yakishaona tu, akili inajua kwa haraka sana kitu gani chakufanya. Nimefurahi kuona na wewe unapenda.”

“Kwa hiyo nikiwa mkubwa nitakuwa nikifanya kazi kama yako?” “Si lazima. Ila ujue unafanya akili yako iwe na uwezo mkubwa wa kufikiria chochote kile. Kwa juhudi uliyo nayo na ukiendelea hivyo, ukija kujua unachopenda kufanya ukiwa mkubwa, basi ujue utakifanya kwa urahisi sana, kwa kuwa akili yako ina uwezo mkubwa wa kufikiria nakufanya.”

Zipo Tabia Za Waliofanikiwa Sana,

Na Tabia Za Walioshindwa.

Jelini akamfuata mama yake chumbani kwake. “Nataka nikamilishe chumba cha Jeremy kiwe cha hadhi nzuri. Mwanangu anajitahidi mama.” Mama Jema akamtizama. “Nataka nikamnunuli seti nzuri ya kitanda, meza zake, vikabati vizuri vinavyoendana ili aweke vitabu vyake na vitu vyake, viti vizuri vyakusomea vitakavyoendana na…” “Kwa pesa ipi?” Mama yake akamkatisha kwa swali, Jelini akapoa. “Wewe unataka kidogo tulicho nacho tena tuanze kutapanya?” “Ni hivyo tu mama!” “Hapana Jelini. Tukianza maisha tu yasiyo yetu, ujue hivi karibuni tunarudi kule tulikokuwa. Sijui kama unanielewa?” Kimya.

Uhalisia wangu mimi na wewe nilazima tuukubali na ukumbuke sisi ni kina nani. Nilikuwa nikitamani pesa ikosee njia, ije nifanye mambo ya maana ili tutoke pale tulipokuwa. Sasa pesa tuliyonayo unaweza ona nyingi, lakini isipozalishwa tu, ujue ndani ya muda mfupi sana, tunarudi chini kabisa tukianza kumuomba Jema pesa na kukopa kila mahali. Au wewe unataka kurudia yale maisha ya kuomba omba pesa kama zamani?” Akapandisha mabega kukataa.

“Basi naomba akili ihamie kwenye kuzalisha kuliko matumizi. Ukifanya kazi, ukalipwa, tumia pesa yako utakavyo, ila si mtaji.” “Basi naomba unikope, nitakulipa.” “Mimi mwenyewe bado sijaanza kulipwa, kwa kuwa sijaanza kazi.” “Mama!” “Sasa wewe umeniona nikifanya kazi hapa?” “Si unalile duka pale?” “Lile duka nimeajiri watu. Pesa yote niliwekeza, na itachukua muda kuja kujiendesha lenyewe ndipo nipate faida.” “Basi nipe na mimi kazi nianze kuingiza pesa nimnunulie mwanangu vitu.” “Sasa hiyo ndio akili. Na ujue hapa napo mambo yatabadilika.” “Kama nini tena!?” Jelini akauliza kwa mshangao.

“Hiki anachokifanya Jeremy, kuamka asubuhi kwenda shule na kurudi mchana, ndio itabidi kuwa maisha yako na wewe.” “Mimi nimekubali mama. Nitafanya.” “Sawa. Na huku kulindwa hapa kama sisi ni maraisi, hiyo garama hatutaweza.” “Na hili gari sasa!?” “Yaani hili gari ndio tulilipie pesa yakulindwa? Kwanza hatuna uwezo wa kuendesha hili gari sasahivi. Kiuhalisia, hatuna huo uwezo wa kuendesha Renji. Lasivyo pesa yote itaishia kwenye mafuta. Nilipanga kumuomba Jema na mumewe watusaidie kulitunza kwao, sisi turudie maisha yetu ya zamani. Bajaji na pikipiki. Au hutaweza? Maana hilo gari linakunywa mafuta haswa.” “Mimi nitaweza mama.” Mpaka mama Jema akashangaa.

“Kweli!?” “Nitaweza mama.” “Basi hapo utanirahisishia maana nilijua utaanza kulalamika. Lazima tubadili gia angani. Maisha yamebadilika, tunapinduka nayo. Lasivyo tutakwama muda si mrefu. Na utajikuta inabidi kufanya mambo usiyoyataka ili kujiingizia pesa, na huo ndio umalaya ulionithibitishia huna. Sasa usianze kwa ajili ya maisha ya starehe.” Jelini akapoa.

“Au unataka kurudiana na Zenda?” Jelini akashituka sana. “Maana yeye ndiye mwenye uwezo wa kukupa maisha hayo ya anasa.” “Hapana mama! Yeye na wanae watakuja kuniua bure! Sina sababu ya kurudia maisha ya hatari.”  Akawa kama amemchanganya mama yake. “Kivipi wanae wakuue?” Jelini aliropoka tu akiwa amekumbuka alilofanyiwa na Kemi na kumdhuru vibaya sana. Kwa ajili ya kuwa na baba yao ambaye alishaona hastahili madhara makubwa hivyo. Kwa penzi lipi? Akajiuliza Jelini. Akaona hana sababu ya kuyatupilia mbali maisha yake kwa kujiweka hatarini kwa mwanaume kama mzee Kasa asiye muaminifu. Kwanza alishajua hakuna mwisho mwema wowote kati yake na baba yao.

Akafikiria kwa haraka jinsi ya kumjibu mama yake mlipiza visasi kwa kila anayemuonea mwanae. “Baba yao asije niua kwa maradhi. Na watoto wake bado hawamuamini yeyote na baba yao. Nafikiri sababu ya mali. Hawataki mtu awe karibu na baba yao wakihofia mali zao. Kwa hiyo huko sitarudi mama. Na ninashukuru kunilinda nisirudi. Wewe nipe kazi nitafanya.” “Umenifurahisha Jelini, ni hivyo hujui. Nilijua utasumbua kweli.” Jelini akaanza kulia.

 “Mimi mwenyewe sijategemea kama utakubali kubadilika kwa haraka mama. Nilijua utamtaka mzee Kasa ili azidi…” Jelini akashindwa kuendelea akizidi kulia. “Wewe si kitega uchumi changu. Nilikuacha naye kwakuwa ulisema unampenda. Kama mapenzi yameisha, basi! Huna haja yakujitesa. Hee! Kwa kipi mno? Kama yeye amefanikiwa na sisi tutafanikiwa tu. Tuweke juhudi. Na wala usiogope. Hii ni shida ya muda tu. Kwanza tusiite shida. Ni mabadiliko ya muda tu. Tukiweka juhudi na sisi tutarudia maisha ya gari.”

“Eti ninazidi kumuonea wivu Jema, mama?” “Kwa nini?” “Aliweka juhudi kwenye mambo yake mpaka akafanikiwa kujinunulia mpaka gari na kuwa na maisha mazuri tu. Akatulia mpaka akampata mwanaume anayempenda! Ila nasemea ile juhudi yake tena bila hata wanaume! Ujue mwenzio nilijua Jema alikuwa akihongwa! Sasa kuja kuolewa bikra! Hakika imenigusa mama.” “Ni juhudi na kujikana Jelini. Na wala hujachelewa.” Hilo likamtuliza Jelini, akajifuta na machozi akifikiria.

“Sasa mimi nianze wapi kazi?” Mama yake akacheka. “Usinicheke bwana!” “Unanifurahisha sana Jelini wangu. Kwa moyo huo, tutafanikiwa. Sasa kwa kuwa mimi nataka kuanza ile biashara ingine, nafikiri tugawane. Mimi na wewe tusikae upande mmoja. Wewe mzuri kwa kuzungumza na watu, nataka tufungue upande wa pili wa lile duka, na wewe uwepo na wale mabinti pale. Wajue wewe upo pale ili kwanza wasiibe na wajali wateja. Nitakufundisha mahesabu yake ya biashara nzima. Ili ujue kwa siku umeuza kiasi gani, faida na matumizi yote ya pale. Sio ngumu. Siku tano tu utakuwa sawa. Nakuachia pale, mimi nahamisha akili kwingine na yule kijana. Nakuachia wale mabinti pale dukani muwe wote. Fiona mwepesi halafu hana kiburi kabisa. Mtafanya mambo kwa urahisi.” “Sawa.” Jelini akakubali bila shida. “Sasa kanywe dawa kabla kichwa hakijaanza.”

Kwa Colins.

Akatoka na kukuta Colins ametulia kimya kwenye kochi macho kwenye simu. “Sijui alikuwa akitusikiliza?” Jelini akawaza akimsogelea. “Vipi kichwa?” “Sio mbaya. Ila acha nimeze dawa kabla hakijaanza, halafu tupate kifungua kinywa.” “Sasahivi ni chakula cha mchana Jelini!” “Samahani mipango tuliyoweka jana haijafanikiwa.” “Usijali. Anachokifanya Jeremy ni kitu kizuri sana.” “Sasa unaondoka?” “Wewe unataka kufanya nini? Kama unakazi itakayokufanya usiwe huru mimi nikiwepo, nitaondoka.” “Bosi wangu, mama, amenipa mapumziko ya leo. Kesho kazini.” Colins akacheka.

“Kwa hiyo nipo tu. Tukae wote. Au ulitaka kufanya nini?” “Kanywe dawa kwanza halafu ndio tujue chakufanya. Nikusindikize?” Jelini akawa hajaelwa. “Dawa zipo chumbani!” Colins akasimama na kumfuata, Jelini akacheka. “Sasa maji yakumezea dawa?” “Acha nichukue kwenye friji.” Akashangaa anamfuata. Akachukua maji na kurudi naye chumbani, akajitupa kitandani, Jelini akacheka.

Akashangaa vile Colins anavyoshangaa kile chumba. Akapoa. Maana ni kweli pesa ya Zenda ilitumika hapo ndani. Colins akasimama na kwenda mpaka chooni. “Waw!” Akamsikia akihamaki kwa sauti. “Sijawahi ona sinki la kuogea kama hili! Umelipata wapi?” “Hata sijui Colins. Tulihama kabisa hapa, tuliporudi ndio nikakuta kila kitu unachoona.” Colins akabaki amesimama huko bafuni. Akatoka na kubaki kama ameduaa anayefikiria. Jelini akamuacha tu akijua kinachoendelea huko kichwani. Anapigia mahesabu pesa ya Kasa iliyomwagwa humo ndani.  Akawa anatafuta dawa zake.

Colins akarudi kujirusha kitandani. “Na mimi James amenialika kwao usiku. Naona na kina mama pia walialikwa lakini wanamiahadi kwengine. Ila wamesema watapitia tu kuchungulia kidogo.” “Na sisi tutakwenda kwenye saa 12 jioni.” Akanywa dawa na kwenda kukaa. Akamuona kama kuna kitu anafikiria. Colins akajivuta na mto mpaka pale alipokuwa amekaa. Jelini akamshika. Colins alifurahi huyo. “Sasa unacheka nini?” “Umenishika.” Jelini akacheka sana.

“Colins wewe!” “Napenda tukiwa wote, Jelini.” “Ila nahisi umekuja muda mbaya kwenye maisha yangu Colins. Nina mambo mengi, akili haijatulia. Nipo kwenye majuto! Hata sijui.” “Unajutia nini?” “Naona nimejichelewesha! Jema amezaliwa na mama huyu huyu. Amekuzwa kama mimi tu. Ila mwenzangu alifanikiwa kumsikiliza mama mapema, amefanikiwa. Jema anakazi nzuri, sababu ya juhudi niliyokuwa nikimsikia mama akimkazania. Nakumfundisha jinsi ya kupambana mpaka akafanikiwa.”

“Halafu Jema ametulia Colins! Mimi sikujua kama ni kwa kiasi kile! Na mpaka Mungu amempa mwanaume mzuri, anampenda Jema!” “Nisikilize Jelini. Hujachelewa. Hujachelewa hata kidogo. Hapo ulipo, na kwa akili hiyo, unaweza kufanya makubwa sana. Uzuri unaye mama wa kukuongoza vizuri, hujachelewa. Ila ujue si rahisi. Kuna garama ya kulipa na vishawishi vya kushinda. Popote kwenye malengo kunakua na vishawishi. Unaweza ukachoka katikati ya safari, ukashawishika.” “Unamaanisha kutafuta mwanaume wa kunisaidia?” Jelini akauliza.

“Hata hilo.” Colins akaongeza na kumfuta machozi. “Ni vile hunifahamu mimi Colins. Na umenikituta nikiwa na mzee Kasa. Sina tamaa na pesa na wala shida haijawahi kunishawishi kutafuta mwanaume ili anihonge. Sipo hivyo. Kama ningekuwa hivyo, ningeshakuwa na wanaume zaidi ya mzee Kasa. Kwa kuwa wanaume kama yeye wala si wageni kwangu. Ninao wengi tu, na nilikuwa nikinywa nao baa kila siku.” “Uliniambia Jelini.” Jelini mwenyewe akatulia akijifuta machozi.

“Ninachotaka kukwambia, nimekua na mzee Kasa nikidhani yupo tofauti. Na kwangu kwakweli tulikuwa na wakati mzuri wala nisikudanganye. Watu husema ni mkali sana, lakini mimi alijifunua kwa upande ambao ndio maana nahisi nitammisi sana.” Hapo Colins akaumia. “Alikuwa akinipigia simu, tunazungumza na kucheka kwa muda mrefu sana na hatukosi chakuongea. Tukienda mfano sehemu kutembea, yaani ile sehemu utafikiri tupo peke yetu! Tutacheka mpaka giza linaingia ndipo tunaondoka. Tulikuwa na wakati mzuri na kwangu hakuishi na mimi kama mwanaume tajiri au msomi. Alikuwa wakawaida sana. Ikawa rahisi kuwa naye. Lakini si pesa. Na ninakwambia ukweli, ambao unaweza usiamini, nilikuwa naye yeye kama Alexender wala si kama milionea Kasa. Sikuwahi kumuomba pesa hata mara moja ila uaminifu nikihofia asije akawa na mambo ya kando akaja kuniua, nikamuacha mwanangu. Ni hilo tu, lakini si pesa.”

“Na si kwake tu. Kwa wanaume wote wanaonifahamu mimi kwa karibu, wananijua mimi huwa sihadaiki na pesa.” “Basi mabadiliko yako yatakuwa marahisi Jelini. Usiogope. Hiki anachokifanya Jeremy, ndio na wewe fanya. Soma ramani na kuanza kujenga tofali moja hadi jingine. Taratibu, na kwa makini. Usiogope, utafanikiwa tu. Na MIMI nipo na wewe. Nilikwambia ukitaka ushauri, muda na wakati wowote ule, nipigie.” “Mwenzio nimefikiria, ila sijamwambia mama.” Akanong’ona.

“Nini?” “Nina simu ya mahela mengi, sioni sababu. Kuna mtu najua huwa anapenda sana simu na pesa si tatizo kwake. Nataka nimuuzie, niweke vitu chumbani kwa Jeremy. Halafu mimi nitanunua simu ya kawaida tu.” “Twende.” “Wapi?” “Nifuate kwenye gari.” Wakatoka hapo chumbani.

~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment