Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 37. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 37.

Jelini alikuwa amejilaza kwenye kochi nyumbani kwako akiwa ndio amefika tu nausafiri wa kuungaunga. Akiwa amepotelea mawazoni hapo kochini, akasikia hodi mlangoni. Akashangaa maana hakutegemea mgeni yeyote usiku huo. Kama ni mama yake, anazo funguo. Akasimama na kwenda kufungua. Macho yakagongana na Colins. Akashituka sana, hakumtegemea kabisa. “Colins!” “Naweza kukaribia ndani?” Jelini akampisha mlangoni. Akapitiliza mpaka kwenye makochi. “Karibu.” Akaongea akifunga mlango na kwenda kukaa kochi la mbele yake.

“Nilifikiri jana tulikubaliana kufunga na kukaribisha mwaka pamoja! Imekuaje tena?!” “Mpenzi wako alikuja Colins. Na wewe uliniambia hutaki nikusogelee ukiwa na mpenzi wako.” Akammaliza nguvu zote Colins. “Ni wakati ule nilipokuwa kwenye mahusiano naye, Jelini!” “Sasa mimi ningejuaje, Colins? Ilinibidi kuwapisha.” Colins akapoa na kubaki ameinama kama anayepiga mahesabu fulani akitaka kuzungumza jambo na kuona si wakati wake.

“Nikuulize kitu Colins?” “Juu ya nini?” “Siku ile ya harusi ya Jema na James. Nililewa sana. Sikujua uchafu niliofanya. Kila mtu ananiambia kwa vile nilivyomuathiri. Natamani kujua picha nzima.” “Itakusaidia nini?” “Nataka kujua, ili hata nikisikia tena, nijue jinsi ya kukabiliana nayo. Au hata kuomba msamaha kwa wale ambao niliwafanyia ubaya. Jeremy nilimuomba msamaha. Sijui wengine.” “Hayo yanatokea wapi tena, leo!?” Akauliza kisha akawa kama amegutushwa na kitu.

“Ni nini Love amekwambia!?” “Hakuna mtu ananiambia kikamilifu. Naambiwa kwa kifupi tu. Na nimesikia wewe ulihusika kwa sehemu.” Colins akafikiria akiwa ameinama kisha akamwangalia. “Unajua ni nani alikuweka kwenye gari ya Kasa?” “Sijui Colins! Nilikuwa sijitambui kabisa.” “Kwa hiyo hata maneno uliyoniambia usiku ule, hukumaanisha Jelini!?” Jelini akashangaa maana Colins aliuliza kwa kuumia haswa.

“Kwani niliongea nini!?” Akanyamaza na kuinama kama aliyevunjika moyo kabisa. “Nisamehe Colins, nilizidisha pombe, sikuwa hata nikijitambua. Nilisema nini?” “Haijalishi tena, Jelini. Basi, tuyaache tu. Lakini mimi ndiye niliyekuingiza kwenye gari ya Kasa na kumuomba asije akakugusa kwa namna yeyote ile. Akusaidie ulale mpaka uamke.” “Nashukuru Colins. Na kama kuna baya nililifanya, naomba unisamehe. Naona pombe hazijawahi kunipenda. Nimeacha kabisa.” Akamwangalia na kurudi kuinama. Jelini akamuona vile alivyobadilika.

“Mbona kama nimekuumiza Colins!? Nilifanya nini?” “Hapana Jelini. Acha muda utajibu kila kitu.” “Nikikuomba msamaha itasaidia? Maana siku ile nilikosea watu wengi sana.” “Mimi hukunikosea. Usijali.” Wakatulia. Jelini hajui aseme nini na nini kimemleta.  Akawa kama aliyepoteza dira tayari. Akabaki ameinamia magoti. “Nikupe kinywaji gani?” Akanyanyua uso na kumwangalia. Macho mekundu.

Jelini akamsogelea pale alipokuwa amekaa. “Colins wewe ni mtu wa mwisho kabisa nataka kukuumiza. Tafadhali niambie ni nini nimekosea.” “Hujakosa Jelini. Hujakosa kabisa.” Akamvuta mkono, akamshika kwa upendo. “Sasa kwa nini umebadilika?” “Kwa sababu kuna maneno uliniambia usiku ule, nikayaweka moyoni nikijua umemaanisha Jelini! Sasa kuja kujua hata hukujua ni nini uliongea, ndio imeniuma.” Jelini akaumia sana.

“Naomba uniambie ni nini nilisema.” “Itasaidia nini Jelini? Acha muda uje ujibu.” Jelini akaanza kulia. “Hujaniudhi, Jelini. Ila nimetamani ingekuwa kweli.” Akanyanyuka kabisa pale na kutaka kuondoka, Colins akamdaka mkono na kumvuta kumrudisha akae. Akakaa na kumvutia kwake, wakakaa wamekumbatiana. Jelini amemlalia. Akamkumbatia kwa mikono yote miwili na Jelini naye akapitisha mkono mmoja nyuma akaukutanisha na wa juu, akawa amemkumbatia na yeye. Akaegemeza kichwa kifuani. Wakakaa hivyo kwa muda, Jelini mpenda mikono, akatulia haswa.

“Nilihitimisha mahusiano na Love, ndio maana nilikwambia uwe na mimi leo, nikijua yeye angekuwepo na wewe ungekuwepo. Sasa hivi hukuna mipaka.” Jelini akatulia. “Umenisikia?” Kimya. “Mimi nafungwa na maneno yangu Jelini. Nathamini ahadi zangu. Ndio maana nipo makini na kila ninachosema maana najua kitanifunga. Nikikwambia wewe ndiyo, ujue nitabaki kwako hata kama utanifanyia vituko, mpaka tubadili makubaliano yetu. Sijui kuahidi hivi na kuishi vingine. Ndio udhaifu wangu huo. Kwa hiyo nilikuwa kwenye mahusiano na Love, na yeye alikuwa na wivu sana, ilibidi kufuata kila sharti lake ili tu tuwe na amani kwenye mahusiano yetu, lakini pia tulishindwa. Haikusaidia mpaka tukahitimisha.”

Jelini kimya kifuani. “Kwa hiyo kuanzia sasa, ukiniona naye ni kwa kuwa ni kama tumekua pamoja na familia zetu ni marafiki wa kama wazazi walinyweshana damu zao au kuwekeana viapo vya mahusiano mpaka kifo. Ila kwa sasa hayupo kama mpenzi wangu. Kwa hiyo uwepo wake pale leo, si kama mpenzi wangu, ila rafiki wa familia. Umeelewa?” Jelini akatingisha kichwa kukubali.

“Naomba tukamalizie na kukaribisha mwaka na familia.” Jelini hakutegemea. “Yaani kwa YOTE hayo niliyokufanyia, bado tu unataka niwepo karibu na wewe!?” “Bado nataka uwe karibu na mimi, Jelini. Kama ulivyoniambia siku ile nilipokwambia nina mpenzi wangu, na asingefurahia kukuona ukinikarimu. Unakumbuka jibu ulilonipa baada ya kubadili ulichotaka kuniambia?” Kimya. “Ulitaka kuniomba msamaha.” Jelini akatulia akijaribu kuvuta kumbukumbu.

“Lakini ukapingana na hilo lakutaka kuomba msamaha. Tena ukasema, ‘Samahani. Sikuwa nimekusudia ku…’ Ukasita. Kisha ukarekebisha. Ukasema, Hapana. Sitaomba msamaha kwa nilichokifanya kwako, kwa kuwa utaniibia furaha yote niliyokuwa nayo Colins. Nilifanya kwako kwa moyo na sijui ni kwa nini! Kwa sababu hakuna mtu nimewahi kumfanyia hivyo! Najihisi sijakosa, ila nimefanya kwa mtu asiye sahihi. Sitarudia tena. Uwe na amani kabisa kufika kwenye hizo tafrija zote ambazo na mimi nitakuwepo, nakuahidi sitakusogelea wewe na mpenzi wako.’ Colins akanukuhu neno kwa neno mpaka akamshangaza Jelini.

“Colins!” “Uliniachia hukumu! Nikabaki nikiyarudia hayo maneno kila wakati na kuzidi kuumia. Halafu ni kama uliniachia mimi ile hali. Sijui kwa nini, lakini na mimi napata faraja kuwa karibu na wewe, Jelini. Labda uniambie kama kuna kizuizi.” Jelini akajivuta na kukaa vizuri. Akajua kuna jambo anataka kumwambia.

“Kwa sasa sina Colins. Nimeamua kuachana na Kasa.” “Una uhakika? Maana yule mzee anayo pesa, Jelini. Hutakuja kubadilika baadaye?” “Mimi sikuwa naye sababu ya pesa. Nilidhani…” Akasita. “Labda nibadilishe. Nilimuumba mtu wangu kichwani, nikidhani yeye anaweza kuwa huyo mtu, kumbe hawezi.” “Ni mtu gani ulimuumba ukitaka awe yeye?” “Natamani kile Jema amempa James, na mimi nikipate.” Colins akakunja uso.

“Najua nataka makubwa. Lakini kama James amempata Jema, naamini na mimi nitampata tu mtu wangu.” “Sijaelewa Jelini. Jema yukoje na kwa nini isiwe Jema ndio amempata James?” “Mimi simjui James kwa undani. Ila nimeishi na Jema, namjua. Ni mwaminifu sana. Ametulia mno. Na yeye yupo kama hivyo ulivyosema wewe upo. Akimkubalia mtu, hata kama huyo mtu ni mbaya, anajua kujifunga kwenye mahusiano. Na mimi nataka mtu wangu Colins. Siamini kama eti wanaume wote ni malaya. Kwamba eti WOTE hawawezi kutulia na mwanamke mmoja! Mimi naamini wapo waaminifu.”

“Basi hata James yupo hivyo. Ila yeye amekwenda umbali mrefu zaidi. Jema ndio mwanamke wake wa kwanza na amemuoa. Hana tamaa za wanawake kabisa. Mimi ni mtu wangu wakaribu sana. Ananijua ndani na nje, hivyohivyo na mimi namfahamu James. Tupo ofisi moja. Mimi na yeye tu.”

“Si umeona sasa? Kama yupo mwanaume kama James, inamaana na mimi naweza kupata wangu. Nasubiri Colins. Mimi sina tamaa na pesa. Hata wanaume niliokuwa nikinywa nao, wanapesa kama hivyo Kasa tu. Lakini kwa tabia zao, sikuwahi kuwakubali. Sitaki kuja kufa na maradhi, na pesa nimeacha benki. Zitamsaidia nini mwanangu au mama yangu?” Colins akacheka akimtizama.

“Usinicheke bwana!” “Mimi nimefurahi kukusikia ukisema hivyo Jelini. Maana nilijua unalilia pesa za Kasa.” Jelini akampiga na mto. Colins akakwepa akicheka. “Kweli tena. Yule mzee anayo pesa haswa. Binafsi nisingekuhukumu.” “Mimi nalia kujidanganya kirahisi Colins. Nilitulia bila mwanaume kwa muda mrefu sana, nikijiambia nasubiria mwanaume wangu. Nilipojaribu kwako ukanifukuza vibaya vile, kisha akaja Kasa akinionyesha ni mtu mtulivu, nikapata faraja, nikamkubali.”

“Nilikuwa kwenye mahusiano Jelini!” “Na mimi nilielewa. Ila niliumia Colins. Sijawahi kukataliwa vibaya vile. Au niseme sijawahi kumkarimu mtu vile. Wewe ukawa wa kwanza na ndio ukani..” Akanyamaza macho chini. “Ila niliomba msamaha, Jelini! Na sikuwa na jinsi nyingine.” “Nilielewa Colins. Hamna shida.” Wakatulia kidogo.

“Utafanyaje?” Akavunja tena ukimya. “Maisha lazima yaendelee Colins. Mimi ni mama. Sina jinsi ya kubweteka tena. Nilimtelekeza mwanangu kwa muda mrefu sana nikijificha kwenye pombe. Na hata jana nashukuru kunitia moyo nisirudie tena pombe. Lakini ukweli mwenzio ilikuwa ikinisaidia sana. Nilikuwa nikijisahau. Nazika maumivu yangu yote, nalala vizuri.” “Lakini ukiamka unakutana na matatizo yako yapo vilevile, hujatatua hata moja! Si ndio?” “Sasa hivi nimebadilika. Mama amenisaidia. Tunajipanga kuendelea sio kurudi nyuma. Nitatulia kabisa.”

“Nikuulize Jelini?” “Juu ya nini?” “Usikasirike lakini.” “Niulize tu, pengine itanisaidia kufikiria zaidi.” “Ulikuwa na malengo gani na yule mzee?” Jelini akatulia kidogo. “Nikimaanisha hivi, ni malengo yapi yamevunjika uliyokuwa nayo na yule mzee?” “Nikwambie ukweli Colins?” “Hilo ndio litanifurahisha.” “Kinachoniliza si kuvunjika kwa malengo fulani. Maana hayakuwepo. Ila ile hali ya utulivu niliyoipata nikijiaminisha nimepata mtu wangu. Ile hisia ya kuwa na mimi napendwa na kuthaminiwa.” Akaendelea.

“Kasa si mnyama au mkorofi sana kama wengi wanavyomuogopa. Tulikuwa kwenye wakati mzuri sana, ndio maana niliweka matamanio yangu yote pembeni, nikakana nafsi ili nitulie naye. Na ilikuwa nikiwa naye, kweli huwa napata wakati mzuri sana. Kucheka kusiko isha na kufanya kutulia mpaka nafsini kwangu. Nilichopambana nacho kwake hapo majuzi, hakikuwahi hata kupita akili, kwa jinsi alivyoniaminisha ametulia na mimi.” “Ulimfumania?” Jelini akainama maana lilikuwa swali la moja kwa moja.

“Umeniambia utaniambia ukweli, Jelini.” Akajicheka taratibu kwa kujidharau. “Nilikuwa nikitamani kukimbia Colins, ili baadaye aje hata anidanganye halafu yaishe. Lakini miguu ilikufa ganzi. Nikashindwa hata kusogea, nikabaki nje ya mlango nikisikiliza wanavyofanya mapenzi ndani.” “Haiwezekani Jelini!” “Kabisa Colins. Sijui nini kilinipata. Kila nilivyokuwa nikitamani kuondoka, nilishindwa. Nilibaki pale nikisikiliza mmoja baada ya mwingine wakipiga bao. Yaani kilio changu ndio kiliwatoa kitandani. Na matusi ya mwanamke wake ndiyo yalinisaidia kupata nguvu na kuondoka pale.”

“Alikutusi mbele yake tena!?” “Hapana. Nirekebishe. Aliniambia ukweli ulionifanya nipate nguvu ya kuondoka pale. Jamani yule mwanamke aliongea Colins, mpaka mimi ndio nikapatwa aibu. Maana ukweli si kwamba niliwafumania. Ni mwanamke wake wa muda mrefu tu, lakini aliniambia alimuacha kwa ajili yangu ili tubaki wawili tu, kwa kuwa mimi mwanzoni kabisa nilimwambia sitaweza mahusiano ya watu wengi. Sitaki kuja kufa na maradhi nikamuacha mwanangu. Heri wao waendelee. Ndipo akanisihi sana nitulie, akiniahidi hatarudi kulala tena na yule mwanamke. Tutabaki wawili tu.”

 “Na wewe uliamini!?” “Ukweli niliamini, Colins. Wala nisikuzungushe kujitetea. Ila kwa nini niliamini, maana wala si kwamba alitumia mbinu nzito sana kuniaminisha, hapana. Maneno yake tu, nikaamini. Ndio ujue sikuwa nikifikiria sawasawa. Na sijui nini kilinipelekea nijione mimi ndio bora zaidi ya mwanamke wake, aliyekuwa naye kwa miaka yote hiyo! Mimi sijui. Lakini kwa jinsi ya ajabu sana, hakika nilimuamini Kasa.” Colins akabaki akimtizama.

“Sasa kujibu swali lako, tulikuwa tukiendelea bila makubaliano yeyote.” “Ungeendelea hivyo mpaka lini?” “Hata sijui Colins! Kuna mambo yanatokea ndio yanafanya mtu afikirie. Kwa mfano yule mwanamke wake alikuwa akinihoji ukweli mtupu, kwamba mimi nilitegemea nini kutoka kwa mwanaume kama Kasa? Kwamba kwa vile alivyo, je nilitegemea aje anioe? Aje aanze kuzaa na mimi tena?” “Ambayo hayo ni maswali ya msingi sana, Jelini!” Colins akaongeza kwa makini ila msisitizo.

“Basi mwenzio sikuwa hata na mawazo hayo, zaidi ya kustarehe tu. Ila nahisi sasa hivi imenifanya nifikirie zaidi. Ila kwa hakika, sikuwa nimempendea pesa. Alinijia kwangu akiwa mshauri mzuri sana. Alinisaidia kufikiria zaidi maishani kuliko kushinda baa na kwenda mziki usiku kuchwa. Akanivutia kwa mengi, akawa rafiki tunayepigiana simu muda na wakati wowote tukiongea na kucheka. Nimepoteza rafiki Colins. Kwa vyovyote alivyo, Kasa alikuwa rafiki ambaye tulikuwa kwenye mahusiano mazuri sana, ndio maana nimeumia.”

“Pole Jelini. Swali jingine. Akikurudia, akaomba msamaha na ahadi ya ndoa na mtoto, au watoto, utafanyaje?” Jelini akainama akifikiria. “Hapo ujue kuna uhakika wa pesa.” Jelini akacheka kwa masikitiko. “Mimi si mlevi wa pesa, Colins. Sina tamaa ya pesa. Kama ningekuwa hivyo, sasahivi ungenikuta silii. Na wala Kasa mwenyewe asingenipata. Nilikuwa na kunywa na wenye pesa zao, Colins! Pesa isiyo na mawazo. Ila tabia ni kama hizi za Kasa, tena wanasema kabisa, si sabuni kwamba itaisha. Kwa maana nyingine Kasa ni walewale tu. Fikiria kama nisingemfumania. Nilikuwa safarini, si ningerudi nisijue kilichoendeleaa huku nyuma?” “Kweli.”

“Sasa kwa nini awe yeye si wanaume wengine? Kasa hana cha ajabu na wanaume niliokuwa nikiwakataa. Ila yeye alifanikiwa kunionyesha ni mwaminifu sana, na mimi nitabaki peke yangu kwake kitu ambacho nafikiri alijua ndio shauku yangu, akatumia huo udhaifu wangu.”

“Hiyo shauku bado haijaisha?” “Maadamu James amefanikiwa kumpata Jema, naamini na mimi nitapata tu, Colins. Sitakata tamaa. Najua nitapata mwanaume wa peke yangu, japo nikisema hivyo watu wanaona kama naomba kitu ambacho hakiwezekani. Lakini najua kinawezekana. Si wanaume wote ni malaya au hawatosheki. Ni bado tu sijakutana na mtu wangu. Na ninajua ni muda tu. Sikati tamaa.” Colins akatulia nakuonekana amepotelea kwenye anachowaza, kisichotoka mdomoni kama mimba ambayo haijatimiza muda wake wakuzaliwa.

“Na mimi nikuulize Colins?” Akaonekana amemtoa mawazoni, akamtizama. “Nipo kwenye kujifunza na kurekebisha makosa. Nataka kujua kwa mtu kama wewe ulivyokuwa kwenye mapenzi na Love. Msichana mzuri tu. Na anaonekana amesoma sio kama kina sie. Na kwa jinsi nilivyomsikia Connie akimtambua, anayo kazi nzuri, nikimaanisha yakueleweka. Halafu ametoka kwenye familia inayofanana na yenu. Nikimaanisha lazima mtakuwa mkiendana kimaadili. Kingine kwa jinsi nilivyokushuhudia wewe, unaonekana ulikuwa ukimpenda SANA, na kulinda chochote kisitokee kati yenu ili usimuudhi mpenzi wako. Sasa ni sababu gani imewafanya  watu kama nyinyi, msitishe mahusiano kama hayo?” Colins akafikiria na kutaka kuzungumza kitu akitaka kurekebisha kauli ya Jelini kwenye uulizaji wake swali, akasita.

Akafikiria tena, akaona endelee tu si kukanusha. “Labda niseme hivi, niliishiwa. Nikimaanisha, sikuwa na kitu kingine tena chakutoa tukaweza kuwa na furaha na amani. Nilifanya kila kitu, na bado haikuwahi kutosha. Ukifanya hiki, atahitaji kingine lakini pia kile ulichomfanyia kinakuwa hakijatosha au hakikukamilika kwa usahihi. Tuliendelea hivyo kwa muda mrefu sana, mwishoe nikaanza kuhisi napotea. Yaani mimi mwenyewe nikaanza kujidharau nikijihisi labda nina matatizo, maana hapakuwahi kuja kutokea ukamilifu kutoka kwangu!” Akaendelea.

“Sikuwahi kumfanya mwenye furaha. Na kila nilipojaribu kufanya kitu, basi ujue kutakuwa kunakukosea tu kiasi ya kwamba hata jambo zuri na la garama, wakati wote linageuka kama si ugomvi, basi kununa. Nikaona si sawa kwake wala kwangu, pengine anaweza pata mwanaume ambaye anaweza kumfurahisha. Nisimzibie. Nikamuomba tuhitimishe tu.” “Alilichukuliaje?” “Alisema sawa tu.” Jelini akabaki akimwangalia kwa mshangao, Colins akacheka na kutulia.

“Mimi hapo ndio huwa nachoka Colins. Hawa wanadamu wanatakaga nini jamani!? Maana unajikuta umetoa mpaka utu wako kumpa ili tu kumridhisha, lakini bado!” “Huwa tunazungumzia sana hili na James. Lakini kila wakati tunaishia kuambiana hivi, kuna kubweteka unapopata kitu kizuri. Na ikitokea unampata mnyenyekevu, ndio kabisaa. Ipo hali hata ya kudharau mbali na kubweteka. Unajua si yupo tu. Kwa hiyo unakua hujali. Ndio maana James ananiambiaga, kwa mkewe, anafanya juhudi za makusudi. Maana kwanza mkewe ni mpole sana.” “Sana. Jema mpole jamani! Na hataki ugomvi. Chochote anachojua kitaleta kutokuwa na amani, bora anyamaze.” Akaongeza Jelini.

“Basi na mumewe anasemaga hivyohivyo. Anasema ni rahisi sana kumsahau Jema. Anasema akikumbuka kitu cha kumfanyia mkewe, hata kama yupo busy, anakiwekea alam ili baadaye akumbuke.” “Ndio maana! Yaani mimi na mama huwa tunawasema, hatuwamalizi! Bwana James anampenda Jema, na kumjali mpaka wivu! Ndio maana na mimi nimepatwa hamu Colins. Mimi nilikuwa sifikirii swala la ndoa. Ila baada ya kuwaona wale, nimetamani.” Simu ya Colins ikaanza kuita mfukoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Akaitoa na kuiangalia. “Mama!” Ndio akili ikamrudia anahitajika kurudi nyumbani. “Naomba turudi wote nyumbani.” “Naomba tu uende Colins. Nimeingiwa aibu pale, sijui hata nikirudi nawatizamaje wale watu, zaidi mama yako na Connie. Maana Love aliongea uchafu niliofanya nilipokuwa nimelewa, siku ya harusi! Na mbaya zaidi kumbe alishampa habari zangu dada yako ila Connie hakujua kama ni mimi. Halafu aibu ingine ni kilio nilichoshindwa kujizuia hata pale kwenu, sababu ya yule mzee. Lazima watakuwa wananiona mimi ni hovyo sana. Na kwa ina ya wageni wenu, na familia yenu, mimi pale hapatanifaa. Ninachotaka kukwambia ni SIWEZI kurudi tena kwenu, Colins. Nikushukuru kwa kila kitu, naomba wewe ukaendelee tu na wageni wenu.”

“Uliposema umebadilika, ulikuwa ukimaanisha pombe tu au tabia kwa ujumla?” Jelini akashituka moyoni. Ila akajikaza. “Najitahidi Colins.” “Kufanya nini?” “Kubadili maisha yangu kwa jumla.” “Basi ujue ni pamoja na kusimamia maneno yako mwenyewe, na kuna usemi unasema, own your own mistakes. Unanielewa Jelini?” Jelini akatulia.

“Mwaka huu umeniahidi kumaliza na mimi na kuanza mwaka mpya pamoja. Gafla unanibadilikia! Halafu unakimbia makosa yako mwenyewe! Ili nani arekebishe?” “Siwezi kubadilisha nyuma Colins!” “Ila unaweza kubadili kuanzia hapa. Au unataka kuanza ‘kesho’ ambayo haijawahigi kufika kwa yeyote?” “Mbona nilishaanza!” “Kwenye nini na nani? Au wengine hatuna maana, ni rahisi kupuunzwa tu?” Jelini akashituka sana.

“Nakuthamini Colins na wewe unajua!” “Najuaje?” “Mbele ya wenzio nilikuweka kipaumbele Colins! Unafikiri huwa najali hivyo kila mtu?” “Kwa hiyo ilikuwa ni kwa mara moja, basi?” Jelini akakwama. “Nilikuomba ramsi tuwe wote leo. Ukakubali. Gafla unanibadilikia!?” Kabla Jelini hajajibu ujumbe kwenye simu ya Colins ukaingia.

‘Pokea simu yangu Colins mwanangu. Unanipa wakati mgumu.’ Aliposoma tu, hapohapo akampigia mama yake kwa haraka. “Samahani mama. Lakini naombeni nyinyi muendelee tu.” “Kweli Colins mwanangu? Tunaalika watu kwenye mji wetu, halafu unakimbia? Sidhani kama ni sawa. Nikatalie kitu kingine lakini si hicho.” “Sio kwamba nakukatalia mama, lakini..” Akasita.

“Ni juu ya Jelini?” Mama yake akamuuliza. “Nataka kuwa naye, mama!” “Kwa nini usirudi naye tu?” Colins akanyamaza kama anayefikiria. “Colins?” “Nakuja mama. Usihuzunike. Nakuja.” “Sawa, lakini ujue sijala nakusubiri.” Pakazidi kuwa pagumu. Ameshindwa kumtoa mama yake barabarani kwa ahadi ambayo hata hakuwa amemaanisha. Hakuwa na mpango wa kuondoka hapo na kumuacha Jelini usiku ule hata kidogo. Akihisi ndio nafasi pekee ya kujisogeza karibu ya mrembo huyo aliyepo majonzini, akitaka yeye ndio aweke historia moyoni kwa Jelini. “Colins?” Mama yake akaita akitaka kujua kama amemsikia na kumuelewa kuwa hatakula mpaka yeye arudi nyumbani. Colins akakumbuka bado mama yake yupo masikioni. Nani zaidi?

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Colins akabaki njia pamba. Mama masikioni, mrembo mbele yake. Anakwenda, au anabaki? Mwaka anamaliza na mama au Jelini? Akabaki hajui chakuzungumza tena.

~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment