Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 35. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 35.

Jioni hiyo ya tarehe 30 mama Jema akaingia mjini, moja kwa moja nyumbani kwa Jema. Akamkuta Jelini ametulia pembeni ya Colins. “Njoo Jeremy.” Akamsogelea mama yake. “Mbona kama unausingizi?” “Alikuwa amelala, ndio nimemuamsha ili ashuke kwenye gari.” Mama Jema akajibu yeye, akiweka pochi yake chini. “Shikamoo anko na anti.” James na Jema wakaitika. Akamgeukia Colins. Akamsalimia kisha akapanda kwenye kochi na kumlalia mama yake. “Bado usingizi haujaisha?” Jelini akamuuliza mtoto wake kwa upendo akimpapasa kama anayembembeleza, akakubali. “Basi twende nyumbani ukalale vizuri. Njiani ulikuwa ukisoma kitabu gani?” “Sijamalizia, nikapitiwa na usingizi.” “Pole. Basi twendeni.” Akakaa.

“Colins huyu ni mtoto wangu. Anaitwa Jeremy.” Jelini akamtambulisha akidhani Colins hamfahamu. “Nimefurahi kukuona tena Jeremy.” “Tena!?” Jelini akauliza kwa mshangao. “Siku ya harusi ulimtangaza kuwa ni mtoto wako.” Jelini akaanza kuingiwa hofu, hakuwa akikumbuka. Ila kwa alivyosimuliwa maajabu aliyofanya, kumbe mpaka kina Colins walisikia! Akamtizama na kukwepesha macho kwa aibu.

“Siku ile ulivyokuwa ukinigawa, ulinitangaza pale mbele za watu wote.” Mwanae ikabidi kumkumbusha. Jelini akaumia sana. “Samahani Jeremy. Nilizidisha pombe, hata sikujua kama nilifanya mambo ya ajabu kiasi hicho! Unajua mimi sitaki kukugawa hata iweje utabaki na mimi pamoja na bibi. Wewe ni mtoto mzuri sana Jeremy, na nakupenda.” Mwanae akamuegemea tu na kunyamaza. Jelini akazidi kuumia. Wengine kimya.

“Jeremy wewe ni mtoto mzuri sana. Na unafanana sana na mama yako.” Colins akamsifia akimchungulia pale alipokuwa amejilaza. “Asante.” Akashukuru na kupoa. “Acha kulia Jelini. Kichwa kilitulia kwa muda mrefu, usifanye kikaanza tena. Una kitu unataka kuchukua chumbani kabla hujaondoka?” Akafikiria akakumbuka ana vitu vyake vichache alivyokuwa akizunguka navyo nyumba hadi nyumba kutokea Moshi, kwa Zenda, hotelini, kwa kina Colins mpaka hapo.

“Kaa vizuri nakuja sasahivi tuondoke ukapumzike.” Akamwambia mwanae ili atoke pale alipomuegemea. Akakaa vizuri. Jelini akanyanyuka kuelekea chumbani. “Nakushukuru Colins kuwa naye tokea sisi tuko Moshi.” “Karibu mama, japo sisi ni familia.” Akajibu Colins kiungwana. “Sasa sijui itakuaje maana pale kwetu sisi tuna vyumba viwili, cha tatu ni ndio kimemaliziwa kujengwa upya kwa ndani. Kitupu kabisa. Jelini alitaka vyumba vyote kujengewe vyoo na kufanyiwa ukarabati. Kwa hiyo hicho kilichobaki cha tatu ndio cha mwisho kutengenezwa ambacho ni cha Jeremy. Tumebakiwa na viwili tu. Changu ambacho natumia na huyu kaka, na hicho cha Jelini.” James akamtizama Colins kama anayemwambia umeshikwa pabaya!

“Hakuna shida kabisa. Naona hata yeye ameanza kutulia. Nitakuja tukae mpaka usiku ndipo nirudi nyumbani. Ila nilitaka kuwakaribisha nyumbani kesho. Tunafunga mwaka kwa tafrija ndogo tu, ila tukiwa na marafiki wa karibu. Zipo familia kadhaa huwa tunakutana. Ni marafiki wa wazazi tangia sisi ni wadogo sana. Tunapeana zamu kila sherehe. Hii ya mwaka mpya itakuwa nyumbani kwetu. Tunapata muda wakumshukuru Mungu pamoja, kisha kula na kunywa tukisubiria mwaka mpya. Inakua nzuri kwakweli. Ningependa na nyinyi muwepo.”

“Mama yako ameniambia. Lakini nikamwambia inategemeana na hali ya Jelini. Kichwa kikiwa sawa, tutakuja.” “James na Jema, je?” “Kama kuna nyama choma mimi na mke wangu hatuna neno. Au unasemaje Jema?” “Na mimi mama Colins amenipigia leo kunikaribisha. Wala nisiwe muongo, nilikubali haraka maana aliniambia kunakuwa na vyakula vingi na sambusa.” Wakaanza kucheka.

“Hivi nilisahau tu kumwambia James. Ila kwa kuwa hatukuwa na ratiba ingine, na alisema kutakuwa na maombi, wala sikuona shida.” “Basi maadamu Jema ameshakubali, sisi tutakuwepo Colins.” “Basi nashukuru.” Jelini akatoka na kimkoba chake. Kilionekana kizuri na cha thamani pamoja na pochi. “Mimi nipo tayari mama. Jema na shem, nawashukuru kunivumilia na kuwa na mimi.” “Wala usijali Jelini shemeji yangu. Naamini kila kitu kitakuwa sawa.” “Na mimi naamini hivyo shem. Muwe na jioni njema.” “Acha mimi niwatoe.” “Wewe tulia hapo. Unatutoa wapi na jua kali hili?” Jema akaanza kucheka. “Mama Jema hutaki kukarimiwa?” “Utaniangukia bure na hilo jua hapo nje. Wewe kaa, nitakupigia baadaye.” Colins alishaingia ndani kukusanya vyake na yeye. Akatoka.

“Naomba niwafuate nyuma nikiwa na Jelini, na Jeremy.” James akatingisha kichwa. “Sasa wewe James unashida gani?” “Sijawahi kukupatia mwenzio Colins! Hivi kwa nini ukipanga jambo lako kichwani, na kulipitisha, nilazima libakie hivyohivyo? Huna aibu wewe hata kwa wageni?” “Mama Jema ni mama yangu. Sasa aibu ya nini? Halafu ujue bado sikuelewi upande ulipo wewe James!” “Basi bwana. Lakini mimi nisingefanya hivyo.” Colins akacheka na kumgeukia mama Jema. “Yaani tunakua tukiendesha nyuma yenu tu.” Akaongeza ushawishi. Mama Jema akacheka akiwa ameshapewa taarifa zake na Jema pamoja na mama yake huyo Colins, jinsi alivyomganda Jelini.

Akamtizama Jelini. Jelini alikuwa ameshika mwanae mkono wanakaribia mlango. “Asante Colins.” Akajibu hivyo wakajua amekubali. Akawahi mlangoni kumfungulia mlango, James na Jema wakicheka. “Tunashukuru kwa kutuhifadhi, jamani. Mama mwenye nyumba wetu?” “Wewe muda na wakati wowote, karibu Colins. Milango ipo wazi.” Jema akajibu. “Nashukuru sana.” Wakatoka hapo na kumuacha James na mkewe. Kikao kikahamia nyumbani kwa mama Jema.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Njiani Jelini alikuwa kimya akiogopa hata kumuongelesha au kumwangalia Colins. Na Colins alijua. Macho chini muda wote akimbembeleza mwanae kiti cha nyuma. “Utakuwa sawa, Jelini. Usiogope.” Akajaribu kumrushia neno la faraja akimwangalia kupitia kioo cha katikati ya gari. Lakini Jelini akashindwa kujibu, akabaki ameinama nakushindwa hata kujibu. Akaona amuache tu. Safari ya kwenda Tegeta nyumbani kwao ikaendelea mpaka wakafika.

Akamsaidia kumbeba Jeremy alikuwa amelala. Akamuingiza ndani, bibi yake akamwambia amlaze kwenye kochi, atamuingiza ndani baada ya kuingiza mizigo. Jelini akaelekea chumbani kwake kubadili nguo. Akakaa huko kwa muda mpaka aliposikia kumetulia, akajua Colins amekaa peke yake sebuleni. Akatoka. Akaenda kukaa kochi la pembeni kabisa.

Ukweli nyumbani kwa kina Jelini kulibadilika. Na anavyopenda vitu vizuri! Palivutia. Aliweka marumaru nzuri sana. Makochi ya hadhi, na meza pia. Hiyo tv, kama ya ukumbi wa sinema. Kubwa. Wakapapangilia vizuri hapo na sehemu ya kulia chakula na meza pamoja na viti vyake vya thamani sana. Pakapoa vizuri. Yote hiyo pesa ya Kasa.

Akachukua rimoti akawasha tv. “Unataka kuangalia nini nikuwekee?” Akamuuliza akionyesha kujali lakini bado akishindwa kumtizama. “Nataka ukae karibu yangu Jelini. Huko mbali!” Jelini akajifikiria akiwa ameinama. “Au unataka nikupe nafasi, niondoke.” Akapandisha mabega kukataa akiwa ameinama. “Basi naomba tukae wote.” Na sauti ya Colins ilivyo nzuri, nzito na yakubembeleza, Jelini akahamia kwenye kochi alipokuwa amekaa, akamsogelea na kumuegemea. Alifurahi Colins! Akapitisha mkono kwa juu. Jelini akajivuta vizuri, akawa kama amemlalia ubavuni. Wakatulia.

Mama Jema kutoka hapo, akachoka kabisa. “Sasa nyinyi wawili, hamli?” “Tumekula mchana kwa kuchelewa. Eti Jelini, unataka kula nini?” “Hivyo ulivyomshika huyo, atalala sasahivi na hatakumbuka kula. Mimi namjua Jelini jinsi anavyopenda mikono. Yupo hivyo tokea mtoto. Ukimuweka chini tu, kilio. Ndio maana nilikuwa nikimfunga mgongoni masaa yote ili nifanye kazi. Basi unadeki humu ndani na yeye umemfunga mgongoni mpaka mwisho. Lasivyo kazi haziendi. Na ndio yupo hivyohivyo.” Colins akacheka na kumwangalia vile alivyotulia. Na alitulia kweli, kama paka.

“Jelini, chakula?” Akakataa. “Mbona mimi sishangai. Sasa sisi tulikula wakati tupo njiani. Kaka ameshiba ndio maana usingizi mwingi. Natoka mara moja kuangalia mambo yangu, nitarudi.” “Basi mimi siondoki mpaka urudi.” Mama Jema akacheka. “Haya Colins.” Wakasikia gari, wakajua ameondoka maana Devi alipoacha tu gari hapo na kuingiza vitu ndani, kazi yake kwa siku hiyo ikawa imeisha. Mama Jema akamlipa kwa kumuendesha. Akaondoka.

Kwa Zenda.

Alipokuwa akitoka hapo, Mzee Kasa akampigia kuwa afike nyumbani. Kwa haraka akatoka hapo Tegeta mpaka Mikochini nyumbani kwa mzee. “Mlisafiri salama?” Hilo ndilo likawa swali la kwanza. “Ndiyo.” Akajibu Devi. “Ulifanikiwa kumuona Jelini?” “Ndiyo. Lakini nafikiri ni mgonjwa. Binafsi hakuniongelesha kabisa. Ila uso na macho vilikuwa vimevimba na vyekundu sana. Na nilimsikia mama yake akipiga simu huku tukiwa njiani akiulizia hali yake kutoka kwa dada yake. Nafikiri ni mgonjwa.” Mzee akatulia kimya kwa muda.

“Ila nimewarudisha wote nyumbani kwao.” “Kemi ulimwambia mngerudi lini?” Likawa swali la mtego, Devi asijue. “Kama tulivyokuwa tumepanga na Jelini. Kuwafuata baada ya mwaka mpya. Tarehe moja. Maana Jelini alisema niwapeleke, kisha niwaache. Wangesherehekea sikukuu ya krismas na mwaka mpya. Akataka niwafuate na kuwarudisha huku tarehe moja ya mwezi wa kwanza.” “Kwa hiyo na Kemi ndivyo ulivyomwambia hivyohivyo?” Mzee akataka uhakika. “Ndiyo.” Devi akajibu asijue ametegwa na kutegeka vibaya sana.

Mzee alikuwa akimsubiri kwa hamu ili kujua wanae na mkewe wamejuaje kwa undani juu ya Jelini? Alipo kwa wakati huo mpaka kuweka mipango ya Koku kuja kulala kwake! Akafikiria kwa muda, akajua lazima tu atakuwa Devi. Ndipo akatumia akili ya haraka jinsi ya kumtoa ukweli.

Sasa hili swali linalofuata ndilo lililomfaya Devi ajue si shari. “Na nini kingine walikuuliza juu ya Jelini?” Devi akatulia. “Nakuuliza, na sitataka kujirudia.” “Hakuna kitu kingine.” Devi akashindwa kuwa muongo mzuri kwani tayari alishakuwa na hofu. “Nilazima nijue ukweli. Na kwa kuwa nilazima, basi ujue utaniambia tu. Aidha itakua hapa au polisi.” Devi akazidi kuingiwa hofu. Akashitukia wanaume wawili wanawasogelea hapo barazani. Kama waliokuwa wamejificha na kusimama nyuma yake kwa karibu sana. Devi akatishika sana.

“Nitarudia kwa manufaa yako. Swali, ni mambo gani uliyokuwa ukiwaambia juu ya Jelini?” Devi akameza mate na kuwatizama hao wanaume nyuma yake. Kwamba hakuna jinsi akakimbia hapo na kubaki salama. “Kiukweli dada Kemi alitaka kujua habari zake, Jelini. Anakaa wapi na anaishije hapa. Aliuliza kwa uzuri tu. Na mimi nikamwambia. Na nilimwambia mambo mazuri tu kuwa, unaonekana umempenda sana Jelini. Kwa jinsi mnavyoishi naye. Hata ile kutoka kuja kumpokea nje nikimleta. Na vile unavyomjali hata kwao.” “Kivipi?” Zenda akataka kujua zaidi.

“Kwanza ni yeye mwenyewe dada Kemi alitaka kujua kama unamjengea nyumba mahali. Ndio nikamwambia sijui. Ila ni kama unajenga kwao upya. Kuanzia nje mpaka ndani, umepabadilisha. Umemwaga mafundi kama mchwa wakishambulia nyumba yao kuijenga kisasa. Kwamba hata paa ya nyumba ulibadilisha na kuweka vigae na madirisha. Kwamba ilibidi wahame pale kwa muda kupisha ujenzi.” “Yoote hayo unayatoa kwangu na kuyahamisha pasipo wahusu!?” Devi kimya.

“Sasa nakupeleka ndani, walipo hao wenzako kwa kuwasaidia kuweka njama za kutaka kunidhuru mimi. Wewe umewasaidia kuwapa habari zangu na kuhatarisha maisha yangu. Kitu kilichosababisha kumuumiza Jelini. Mchukueni.” Mzee akaingia ndani, Devi asiamini. Akaanza kuomba msamaha. Mzee akafunga mlango. Wale askari kanzu wakaondoka na Devi.

Huyo mzee akawa amefunga wanae wote wawili, mume wa Kemi, Koku na huyo Devi. Anawakwa hasira utafikiri alishikiwa bastola kulala na Koku mpaka kufumaniwa. Alijawa chuki akitaka waumie kama anavyoumia yeye. Wamemtenga na Jelini! “Hakika watalipa.” Akaapa kila wakati alipokumbuka makubaliano yake na Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwamba kifo cha mahusiano yao, ni pale mmoja wao atakapolala na mtu mwingine. Hilo walihakikishiana ni kosa ambalo hawataruhusu mjadala. Kwamba siku mmoja wao atakapokuwa kitandani kimapenzi na mtu mwingine, ndio amehitimisha mapenzi yao.

Kingine kinachomliza Jelini, ni maumivu ya kuchaguliwa Koku, na kuachwa yeye. Akakumbuka sarakasi zote alizozifanya kwa huyo mzee, akijua ndio amemfunga, amemdhibiti hawezi kwenda kwa mwingine, amempa kila kitu mwanaume atakacho, halafu kuja kumfumania, sio katikati ya tendo, akiwa mzee anashangilia goli, kwamba yuko aliyefanikiwa na yeye kumfikisha kileleni!

Halafu ni Koku aliyemuapia amemuacha, hana sababu ya kurudi kwake tena! Jelini alijisikia kufedheheka sana. Ujanja wote ukamuisha zaidi kwa Jema na kwa ndugu alioanza kuingiwa hofu wakijua ameachwa sababu ya mwanamke mwingine! Kwamba ni mjuaji asiyejua! Akasikia aibu hata kabla hajachekwa. Akajitengenezea visa vyake vya kudharaulika, vikazidi kumuumiza yeye mwenyewe.

 Na Mzee naye kinachomuumiza alijua kabisa, no point of return. Ndio mwisho wake na Jelini kitu alichokuwa amehakikishiwa na Jelini kuwa naye mpaka kifo. Jelini aliishi hicho kiapo na Zenda kana kwamba ni mke wa ndoa, akifungia macho vishawishi vyote, akimuhakikishia ametulia. Na mzee alimuona jinsi alivyotulia, maana alimchunguza na kumbana atakavyo, Jelini hakuingia mtegoni. Hakujua kama Zenda ndio angekuwa chanzo chakuvunjika mahusiano yao, japo haWAkuwa wamefikiria muendelezo wao. Yaani asubuhi ya fumanizi ndio Koku akawafungua wote akili na kumfanya mzee afikirie zaidi.

Yupo na binti mdogo hata hajafikisha miaka 25. Kwamba angetaka kuwa na watoto. Je, angekuwa tayari hapo alipofika kimaisha nakuanza kubadili diaper kwa kachanga kake na Jelini? Je, angempa ndoa huyo Jelini kwamba waanze kuishi humo ndani asubuhi mpaka asubuhi, akijulikana Jelini ni mkewe? Kwamba maisha yake yabadilike yaongezeke mtu? Sio penzi la kuiba la weekend tu. Ni mpaka kifo! Koku akawapigia kengele asubuhi hiyo ya fumanizi, ndio wakaamka na kukutana na ukweli wa maisha. Jelini akabaki akiwaza kwake. Na mzee kivyake huku akitoa adhabu kali kwa kila aliyemuhisi.  Swala la kuhamisha maneno kutoka nyumba moja kwenda kwingine, likamponza Devi, tayari akabambikiziwa kosa la kusaidia kutaka kuua.

~~~~~~~~~~~~~~~


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment