Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 34. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 34.

“Unanukia vizuri Colins!” Jelini akamuongelesha akijivuta kama kumpisha. Akajilaza pembeni yake. “Asante. Lakini natamani kuwa msaada kwako Jelini, lakini sijui nini chakufanya! Niambie nifanye nini, mimi nitafanya.” “Nisaidie kufuta nilichosikia. Kinanipigia kelele siwezi kutulia. Natamani nisingesikia.” “Siwezi Jelini. Inawezekana ulitakiwa kusikia ili kujua.” Akaanza kulia taratibu. “Nisikilize Jelini. Sio vyote tunavyotamani vitokee kwenye maisha yetu vinatokea. Mama aliniambia mara nyingi ‘hapana’ ya Mungu huwa inauma kwa sababu hupati sababu hapohapo, tena ukiwa unataka jambo lako kwa nguvu, halafu yeye inakuwa kama anakunyima! Inauma sana. Ila baadaye ndio unaweza kuelewa ni kwa nini Mungu alikunyima, na wakati mwingine unaweza pia kutojua sababu. Tafadhali jipe muda.” Akatingisha kichwa kukubali.

Jema akagonga na kuingia na dawa. “Nimemletea dawa za kichwa.” Colins akapokea na kushukuru. “Nashauri ukapumzike Jema. Akitaka kitu mimi hapa kwako si mgeni.” “Basi ukizidiwa, uje kunigongea chumbani kwangu. Na James naye yupo karibu kuja.” “Wewe nenda kapumzike.” Akamchungulia Jelini pale alipolala. “Jaribu kutulia ili na kichwa kitulie. Usikubali kuendelea kuteswa. Kuna mambo unaweza usiwe na amri nayo kwenye maisha, ila mengine unayo. Usikubali kujiumiza mwenyewe. Tulia kabisa ukijikumbusha unawajibika na maumivu ya kichwa chako. Yakupasa utulie ili kichwa kipoe. Mama anakuja kesho.” “Asante Jema. Nitalala.” “Hayo ndio maneno. Haya usiku mwema.” Akawaaga na kutoka.

Akampa dawa, akarudi kujilaza kwenye mto. Colins akavuta mto mwingine juu yake akawa kama anamchungulia kwa chini alipolala. Akaanza kumchezea masikio taratibu. Huku Jelini akizipata pumzi zake sawia. Akaanza kujisikia raha. Anachezewa na Colins! “Asante kuwa na mimi Colins.” “Karibu. Kuna njia unaweza kutumia kupunguza kelele ya ulichokisikia.” Jelini akanyanyua uso kwa haraka kama aliyeambiwa kuna tiba ya uchungu wake, macho yakagongana. Akahamisha vidole kwenye nyusi. Mwili mzima wa Jelini ukawa kama umepigwa shoti kukutanisha macho yao. Akakwepesha.

“Kila ukisikia hiyo sauti, unaweza kuhamisha mawazo hapo. Au ukaangalia movie mpaka kwa muda fulani, hadi makali yake yapungue. Au nitakufundisha game, uwe unacheza. Itakuondolea mawazo huko.” Jelini akatingisha kichwa kukubali. “Unataka niweke movie? Nitaweka laptop hapo mbele yako, huna haja yakukaa.” Akafikiria kuwekwa hiyo movie inamaana hatashikwa tena. Jelini mpenda mikono. Kubembelezwa. Akilinganisha na kuangalia movie! Akasita. “Ni nzuri. Itakufanya ulale.” Akaweka ushawishi asijue shida ya huyo Jelini ni hiyo mikono yake iendelee kuwepo kwenye mwili wake. Ila mwishoe akakubali. “Sawa.”

Akatoka hapo na kuchukua laptop. Akawasha na kuingia nayo kitandani. Akaiweka mbele yake. “Unaona?” “Unaondoka?” “Unataka niondoke?” Yakawa maswali matatu ambayo hayajajibiwa. “Ni sawa tukibaki wote?” Likaongezeka la nne kutoka kwa Jelini, kwa sauti ya kubembeleza. “Kwamba nilale hapa!” Colins akawaza kwa haraka, akihisi bahati ya mtende inataka kumuangukia, lakini akiogopa asije akawa amejichanganya, Jelini hakumaanisha hivyo. “Kama hutajali lakini.” Akaongeza taratibu. “Basi tutakuwa wote usiku wa leo. Sitakuacha. Ukisikia usingizi, ulale.” Akajisogeza karibu yake, Colins akajua anataka mshike. Akafurahi moyoni.

Alichokifanya Colins ni kurudisha mto juu yake, akalala juu kidogo ya mto alio lalia Jelini, laptop mbele yao. Akajiegemeza kidogo pembeni yake. Uwepo wa Colins ukajaa hapo kwenye hisia za Jelini, akaanza kutulia nafsini. Kwa mbali akaanza kuhisi ndevu zake pembeni ya kichwa karibu na shavu. Jelini akajisogeza karibu zaidi, akaendelea kumpapasa. Hakujua movie ilifikia wapi, ila akalala kama katoto kachanga akipapaswa na Colins.

Uthamani wa Ulicho Nacho.

Huku kwa Jema akabaki amejilaza akiwaza anakopita mdogo wake. Akajifananisha na alikopita. Kwa hakika akamshukuru Mungu kumtumia James. “Inamaana ningekaa na ile fedheha mpaka sasa! Asante Mungu wangu.” Akajisikia kumpenda James sana. Mara mlango ukafunguliwa. “Pole mpenzi wangu.” “Hujalala tu!?” “Nilikuwa nikikuwaza wewe.” “Kwema?” James akamsogelea pale kitandani.

“Niambie kwanza huko jinsi ulivyopakuta.” “Hapana bwana Jema. Wewe ndio muhimu kuliko kila kitu. Niambie.” James akasisitiza. “Mimi nipo sawa, ila namuhurumia Jelini, kwa kuwa hapo alipo, mimi nilikuwepo. Wengine wanaweza wasielewe, lakini mimi nahisi ana roho kama yangu. Alijifunga pasipofungika, ameishia kuumia rohoni, wengine wakimshangaa anacholilia. Mimi nilikuwa hapo, James. Japokuwa yanaweza yasiwe mahusiano mazuri ya kifahari kama Jelini alipokuwa, lakini niliumia sana mpaka ulipokuja wewe, na kunipenda kwa ukweli. Nakushukuru James.” James akainama na kumbusu kidogo tu mdomoni.

“Jema wewe unapendeka bwana! Mtulivu mno. Mimi ndio natakiwa kukushukuru. Huna makuu mpenzi wangu. Unanivumilia na ratiba zangu ngumu, mpaka huwa nakuhurumia.” “Sivyo ninavyojisikia mimi. Mwenzio najiona nipo kivulini. Unanitunza vizuri sana James. Hakuna unachojua nahitaji usinipe! Tena bila hata kuomba! Unanifikiria mpaka huwa naishiwa uhitaji! Najua haya ni maisha tu, tutakuja kutulia. Niambie huko umepakutaje?” “Vizuri aisee. Sikutegemea. Naona sikukuu hizi zimekuja na baraka kwetu. Kila kitu kipo sawa. Acha nikaoge nije tulale.” Jema akaanza kuomba akimshukuru Mungu wakati mumewe akioga.

Alipotoka tu, akamuwahi taulo. James akacheka. “Kweli hizi shukurani nzuri. Leo napata double dozi!” “Utulie sasa ushukuruwe kwa kumpenda Jema.” Jemas akaanza kucheka mara akatulia kadiri utamu ulivyokuwa ukikolea. Tamu yake ilikuwa ikinyonywa vizuri tena ikichuliwa taratibuuu. Jema na tumbo lake akajituma usiku huo mpaka James akafurahi. Wakalala.

Asubuhi.

Jelini akahisi mtu akimpapasa taratibu. Akaendelea kutulia akiwa anatoka usingizini, mwishoe akajua sio ndoto akafungua macho na kukuta Colins akimwangalia. Akacheka kwa aibu na kuficha uso. Ndio akawa amejificha chini ya kifua chake. Akamsikia akicheka. “Ulilala vizuri, nikawa nasikia raha kukuangalia. Jelini wewe ni mzuri hata usingizini!” Jelini akacheka chini ya kifua chake alikojificha. “Sasa mbona wewe hulali?” Jelini akamuuliza akijaribu kujitoa. Ila alitoka usingizini akajikuta wamelala wakiangaliana.

“Acha nikujibu kwa huu wimbo. Nataka uusikilize kwa makini.” Jelini akacheka taratibu. “Nachukua simu nikuwekee.” “Basi na mimi acha nitumie choo ndio nije kusikiliza majibu yangu.” Angalau Jelini aliamka asubuhi hiyo akicheka sio kama jana yake. Akajisahau kuwa amelala na nguo ya kulalia. Akatoka hapo kitandani nguo inaonyesha ndani akili isimkumbushe. Mwili wa ndani unaonekana kwa wazi kabisa. Colins akamuona na kukwepesha macho.

Akaenda kutumia choo na kusafisha kinywa hapohapo bafuni, chumbani. James alijenga hiyo nyumba kila chumba na choo chake. Akajiweka sawa, ndipo akagundua yupo uchi kabisa. Akahamaki alipojitizama kwenye kioo. Akavuta taulo na kujifunga sasa. Kuanzia kwenye matiti mpaka magotini nje ya hilo gauni la kulalia. Ndipo akatoka. Colins alipomuona amejifunga vile na aibu kidogo, akajua amegundua alikuwa uchi. Akatoa chandarua na kukifunga vizuri, akakakaa kitandani na kujifunika tena na shuka.

“Njoo nikwambie kitu Colins.” Colins akarukia kitanda. “Nimepata wimbo wenyewe.” “Asante kuwa na mimi kipindi hiki. Nilikuhitaji. Najua unaweza usinielewe, lakini moyo wangu ulikuwa na maumivu makali sana.” “Nina maswali mawili, lakini nitakuuliza baadaye. Nataka usikilize kwanza wimbo wangu wa kwa nini sikuwa nimelala nakuangalia.” Jelini akacheka akisubiria.

“Unaitwa, ‘I don’t want to miss a thing.’ Mpaka hapo Jelini mpenda Club, akicheza na kuimba usiku kuchwa na pombe, akawa ameshaujua. Alicheka sana na kujificha. “Bwana Colins!” “Mimi sitaki kupitwa Jelini. Hata ukiwa umelala nataka niwepo, nisipitwe na chochote chako.” Akamuwekea nakumfanya Jelini acheke sana huku akisikiliza. Ulikuwa na maneno mazuri sana. Ile tu mwanzo ulisema,

‘Anataka kuwa macho asilale, ili tu kumsikia anavyohema akiwa usingizini. Amuangalie hata vile anavyotabasamu akiwa usingizini, mbali huko ndotoni. Kwamba yeye hana shida maisha yake yote yabakie vilevile akiwa anamtizama yeye tu alivyokuwa amelala. Kwamba huo muda anao tumia hapo na yeye, ni muda anao uthamini sana. Akasema, hataki kufunga macho yake, hataki kulala, kwa sababu atamisi, na yeye hataki kupitwa  na chochote chake.’

 Jelini alicheka sana akisikiliza hayo maneno. “Endelea kusikiliza. Maana kila neno hapo ni jibu lako.” “Mimi nasikiliza Colins.” Yalikuwa maneno mazuri sana. Jelini akajisikia faraja. Akatoa macho kwenye simu na kumtizama, akakuta akimwangalia akitabasamu. Hodi ikawatoa kwenye huo wakati. James na Jema.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Angalau tunafurahi kumsikia Jelini akicheka. Unajisikiaje Shem?” “Vizuri na samahanini kuwaingiza kwenye wasiwasi. Nilikuwa natamani tu ule wakati. Kulia ili nitoe uchungu moyoni.” “Bora kama umepata nafuu. Sasa mpigie simu mama Jema, atulie.” Jema akaingilia. “Acha nimalizie wimbo ameniwekea Colins.” “Mama anawasiwasi Jelini!” “Nataka aje Jema. Namtaka mama.” “Anakuja.” Jema akatafuta mahali akakaa. “Haya weka huo wimbo tuusikilize.” James akamwangalia Colins na kutingisha kichwa. Colins akacheka na kuweka.

Wakasikiliza mpaka mwisho. “Kwa hiyo wewe leo hujalala ulikuwa ukimwangalia tu Jelini?” “Swali lako James, lipo kama husadiki vile!” “Wewe jibu swali.” “Naomba Jelini mwenyewe anijibie.” Kila mtu alikuwa akicheka. “Eti Jelini?” Colins akataka amtetee. “Mimi nimemkuta macho akiniangalia, ndio nikamuuliza, akanimbia majibu yangu yote yapo hapo kwenye huo wimbo.” “Enyi wenye imani haba. Umeamini sasa?” James akatingisha kichwa kwa masikitiko.

“Sasa mjiandae twendeni tukapate kifungua kinywa kizuriiii. Au unasemaje mke ya James?” Colins akaongeza. “Nikipata mtori na sambusa mimi ndio nitafurahi.” “Basi twendeni Break Point. Acha nikaoge chapu, nakuja.” “Hayo ndio maneno.” Colins, James na Jema wakatoka. Jelini akabaki amekaa kitandani akijifikiria.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mara mlango ukagongwa tena, Colins akaingia na kumkuta Jelini amejiinamia magotini kwake. “Naomba twende Jelini. Utajisikia vizuri.” “Sijisikii. Naomba nyinyi muende tu.” “Mimi nafanya hii kwa ajili yako. Nataka uweke mawazo kwengine mbali na kuruhusu hayo mawazo yako kurudi kuchungulia pale pachungu na kuendelea kujiumiza. Ukijiweka kwenye mengi na wengi, itakusaidia. Usikae umejifungia, ukisononeka mwenyewe. Tafadhali twende.” “Nashukuru Colins. Basi acha na mimi nijiandae.”

Baada ya muda wote wakajikuta kwenye gari ya James wakitafuta njia kufikia Break Point kutoka hapo Salasala.

Njiani Jelini akampigia mama yake. “Sijakutupa mama yangu.” “Najua mama. Sema nilikuwa nimekasirika sana. Ndio nikawa nakutaka wewe.” “Pole. Vipi sasa?” “Kichwa kimetulia kabisa. Najisikia vizuri. Usiwe na wasiwasi. Vipi Jeremy?” “Yupo sawa, amelala. Tupo njiani. Tumeondoka usiku usiku ili kukuwahi.” Jelini akanyamaza. “Tutafika mapema tu. Naona Devi amekazana kweli!” “Naomba mwambie awe mwangalifu. Asiendeshe haraka sana. Mimi nataka kukuona nyumbani sio hospitalini.” “Yupo makini. Vipi Jema?” “Njaa inamuuma. Anataka sambusa.” Wakacheka.

“Ungeweza, ungeenda kumtafutia mwenzio.” “Hapa tupo njiani kwenda kuzisaka.” “Sasa mnunue nyingi. Zibakie na za baadaye.” “Ngoja nikupe umsalimie.” Jelini akampa dada yake. “Mjukuu anataka sambusa.” “Wewe sema unataka sambusa bwana! Mjukuu wangu amezijulia wapi sambusa? Acha kumsingizia.” Jema alicheka sana. “Mama wewe! Si yeye ndio amesababisha nipatwe hamu?” Angalau kukawa na kucheka. Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Jelini alikuwa ametulia wakati wapo mezani wakisubira chakula. Kila mtu alimuona alivyokuwa amepotelea mawazoni. Ikawa ni bora vile kuliko kulia. Viliendelea vicheko, lakini yeye alikuwa kimya mpaka chakula kilipokuja. Hakuna aliyemlazimisha, lakini alikula vizuri tu, akatulia mpaka wote wakamaliza kula na kurudi nyumbani kwa Jema kwa makubaliano ya kuangalia movie pamoja. Hao wawili walikuwa na mapumziko mpaka tarehe 5, Jema alikuwa akirudi kazini tarehe 3.

Kulikopewa Nafasi Ya Pili.

Usiku uliopita Vai ni kama alikesha kwa ajili ya kusoma, japo alisoma tena na Bale. Huo mtihani wa Anatomy ulikuwa saa mbili na nusu. Akiwa anajiandaa ujumbe ukaingia. ‘Usiogope.’ Akashangaa furaha imemjaa moyoni. Akaamua kumpigia. “Nashukuru kunikumbuka asubuhi hii. Ila naogopa Bale! Mpaka nahisi sipo tayari.” “Ni kawaida. Lasivyo usingekuwa mtihani. Ila kumbuka jinsi tulivyojiandaa. Wewe ingia ukijiambia wana maswali ambayo wewe unayo majibu yake.” Vai akaanza kucheka taratibu.

“Nakuhakikishia ukiingia na huo mtazamo, utajisikia kutulia kabisa. Utajihisi upo mbele ya mgonjwa, aliyekuja kwako, anahitaji huduma yako na wewe unawajibika kumsaidia. Fanya hivyohivyo kwenye mtihani. Itakufanya utulie na kufikiria jinsi yakujibu maswali yao. Kwa kuwa ulijiandaa, hujazembea, na mimi nimekuombea. Amini utafanya vizuri.” “Nashukuru Bale. Asante. Angalau sasahivi hofu imepungua.” “Nataka iishe Vai. Wewe ni nesi mzuri sana. Watu watanufaika na mtu kama wewe. Usikubali hofu ya mitihani ikafanya ukashindwa kufikia watu wenye uhitaji.” “Basi sasahivi ndio nimetulia zaidi.” Wakazungumza kidogo wakakata.

Kweli ikawa kama amezungumza na nafsi ya Vai. Akaingia kwenye mtihani akiwa ametulia haswa. Kila swali alilolikabili, alitulia, akafikiria na kufanya kwa kadiri ya uwezo wake mpaka akamaliza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati anatoka ili arudi bwenini simu yake ikaanza kuita. Akacheka alipoona ni Bale. “Bale.” Akapokea kwa furaha. “Njoo.” Vai akashangaa na kusimama. “Unataka nije kwako sasahivi!?” “Mimi nipo hapa. Nakuona.” Vai akaanza kumtafuta akicheka. Akamuelekeza mpaka akamfikia. “Mbona kama umejificha hapa nyuma!?” “Niliona unatoka na wenzio kwenye mtihani, sikutaka kukuabisha, kuonekana na mlemavu.” “Bale!” Vai akaumia sana. Akasikia uchungu kutoka moyoni.

 “Vipi mtihanai?” Vai akashindwa kujibu. Akainama kabisa nakushindwa hata kumuangalia. “Vai?” Akabaki kimya ameinama. “Najishuku Vai. Haya ni maisha mapya ambayo sijui jinsi ya kuishi nayo. Ila kama nimekosea, samahani. Nimekuandalia kifungua kinywa. Najua hujalala. Nataka ukila, ulale ndio tuendelee na mipango yetu. Au umegairi?” “Hapana. Ila ungenipigia tu simu, nikaja kuliko kuhangaika na daladala kuja mpaka huku kunifuata! Halafu tena tunahangaika kurudi tena!? Mimi ningekuja tu. Ila asante.” “Karibu.” Wakatulia kidogo.

“Acha nikatoe hizi sare za shule, nakuja tuondoke. Na naomba ukae pale Bale wakati ukinisubiri. Usijifiche. Mimi sikufichi. Kila niliye naye karibu hapa chuoni, anakujua. Na nikiwa kwako huwa namuaga Belinda. Yule msichana tuliyekuwa naye siku ile ulipoanguka. Belinda anajua kama tumekua marafiki. Mimi sikufichi, na sitaki ujifiche ukiwa na mimi. Kwa sababu wewe si mlemavu, ni Bale. Rafiki yangu mimi.” Vai akaondoka kisha akarudi.

“Usirudie tena kujificha ukiwa na mimi.” “Nimeelewa Vai.” “Na usirudie  tena kujitambua kama wewe ni mlemavu. Wewe ni Bale. Ni zaidi ya mguu mmoja au miwili. Hiyo ni kauli ya mtu…” Akasita. Kisha akaendelea tena. “Tafadhali usirudie tena Bale.” “Nimeelewa Vai.” “Hapana. Nahisi hujaelewa.” “Basi niseme samahani. Sitarudia tena. Umeridhika?” Vai akaondoka.

Baada ya muda akarudi Vai ambaye ana nguo za kinyumbani, ila amependeza. Alitoa kofia ya unesi na sare. Akachana nywele zake vizuri, na kujiongezea hereni, mkufu na cheni ya mkononi. Alivaa sendozi tu. Vai ni mzuri. Akapendeza. Bale akamuona anakuja, akasimama pale alipomuelekeza amsubirie.

“Umependeza Vai.” “Umeniumiza Bale.” “Hata nilivyoomba msamaha havijasaidia!?” “Nimeumia kuona hivyo ndivyo unavyojiona Bale.” “Nilikwambia nini wakati nakuomba uwe karibu yangu?” Vai akatulia. “Nilikuomba uwe unanikumbusha Vai. Taratibu na mimi nitajifunza kujipokea. Nivumilie tafadhali.” “Basi yameisha. Ila nimefurahi umenipikia. Nina njaa na usingizi.” “Basi utaenda kula kisha nitakupisha chumbani ulale.” “Mimi hata kwenye makochi nitalala tu.” Vai akashangaa wanaelekea upande yaliopo magari.

“Mbona unataka tuzunguke na huku ndio kwenye njia fupi mpaka kwenye daladala?” “Nimekuja na usafiri.” Vai akawa kama hajaelewa. “Twende.” Vai alikuwa na mikoba miwili, akijua jioni wanatoka kama walivyokuwa wamekubaliana. “Naomba nikupokee. Na ukikataa utanifanya nijisikie vibaya.” Vai akacheka na kumkabidhi mkoba mmoja. Bale akatoa gongo  na kuweka ule mkoba begani, kisha akachukua gongo lake ambalo alikuwa ameegemeza tu pembeni yake Vai akimwangalia.

Belinda akaonekana anakuja kwa haraka. “Utaanguka bure!” Vai akamuwahi shoga yake “Felix amekuja muda, nilikuwa sijui. Simu niliifungia kwenye kabati. Nimekuta jumbe kibao na simu zake.” “Wewe ulikuwa ukipiga mdomo na kina Hawa.” Belinda akacheka kama mazuri. “Kama vile ulivyonikuta. Habari sina. Bwana mwanaume atakuwa kanuna huyo!” “Na hapa napo umeweka kituo, unataka uanze mdomo tena, mwenzio anakusubiri garini.” Belinda akaondoka akicheka, hana mbavu.

Akafika karibu na gari fulani, akageuka. “Nisamehe Bale, sijakusalimia. Maneno mengi.” “Usijali. Wewe wahi tu.” “Mzima lakini?” “Namshukuru Mungu.” “Basi wewe tutaongea vizuri wakati mwingine, kukiwa na amani. Maana leo nishalitibua.” Bale akacheka tu, akaendelea kwenye hiyo gari na kufungua, kisha akageuka tena. “Vai, tuwasogeze?” Belinda akauliza. Vai akamtizama Bale. “Nimekwambia nimekuja na usafiri.” “Sikuwa nimeelewa!” Akamgeukia Belinda. “Asante. Nyinyi endeleeni tu. Wakati mwingine.” “Sasa jua lote hili mtadema mpaka wapi, na mtafika lini?” Bale akaumia sana. Vai akasimama kabisa akimshangaa Belinda.

“Samahani Vai, sikukusudia. Nimeropoka tu shoga yangu. Nisamehe kipenzi. Sikuwa na nia mbaya. Wewe unanijua.” Bale akacheka tu na kuongoza njia, kweli akidema mpaka alipoegesha gari lake. Mpaka Vai mwenyewe akashangaa. “Kwamba huu usafiri ndio amesema amekuja nao!?” Vai akashangaa nafsini mwake. Bale akafungua kwa rimoti, Vai akasogea karibu. “Twende.” “Kwamba huu ndio usafiri ulilokuja nao wewe!” Vai akahamaki haswa. “Ndiyo.” “Nani dereva sasa!?” “Mimi. Twende.” Vai akaanza kucheka, asijue alivyomfariji. Maana alijua angeogopa kuendeshwa na yeye mwenye mguu mmoja.

Akapanda kwa haraka. “Bale naye! Sasa si ungesema tokea mwanzo kama umekuja na gari!” Bale akaanza kucheka. “Nilikwambia Vai.” “Wewe umesema umekuja na usafiri. Sasa na wewe huu ni usafiri au gari?” Bale akazidi kucheka. “Vai!” “Acha utani Bale bwana! Kuna utani mwingine sio mzuri.” Vai akawa amechangamka kweli.

“Mama umefurahia gari! La shemeji yangu ujue?” “Wewe twende tufurahie baraka za leo. Kesho tutapambana nayo.” “Huogopi kuwa sitaweza kuendesha?” “Sasa ungekuwa umefikaje hapa, nikianza kuogopa sasahivi kama si kutaka kujinyima raha tu? Na usianze kuniwekea mashaka. Mimi namuamini dereva wangu.” Bale akapata ujasiri huyo, hofu yote na yeye ikamuisha. Wakaondoka.

“Mbona hukuniambia kama mwenzangu siku hizi wewe sio mpanda daladala mwenzangu?” “Vai, hii gari nimeazimwa mama. Acha kufurahia kupita kiasi.” Vai akazidi kucheka. “Kwamba kuna siku utapokonywa, tunarudia hali yetu?” “Ndiyo.” “Lakini na sisi tutakuwa tumefaidi bwana. Na mwenyewe pia si mchayo. Umekuja kunifuata best yako na gari! Na mimi nioshe mjini.” “Kwani na wewe huna kina Felix?” Bale akamchokoza. “Ungejua stori ya Felix, ungechoka. Bora nijibakie hivihivi tu.”

“Ni nini tena?” “Ni walewale tu. Acha mimi nistaafu. Nishike moja. Labda shule itakubali.” “Kwamba Felix si mchumba mzuri?” “Mume wa mtu na ana watoto wake.” Bale akashangaa sana. “Na Belinda anajua?” “Anajua na anaye mpenzi wake huko kwao, wanampango wa kuja kuona kabisa. Huyu Felix anamtunza hapa mjini. Ninachokwambia ni kwamba, wanachumba kabisa. Ndipo wanapoishi. Felex akiaga kwake anasafiri kikazi, ujue Belinda yupo likizo, ndio wanakwenda huko. Kumuona hapa Felix, ujue mkewe anajua yupo kazini. Mpaka jioni. Anarudi kwake, Belinda chuo au ndio atabaki hukohuko mpaka kesho yake. Ndio siri ya unadhifu wake Belinda. Pesa yote aliyo nayo ni kutoka kwa Felix. Maana Felix anayo pesa haswa.” Bale akapoa kabisa akiendelea kuendesha.

“Nashukuru kunijali Bale.” Vai akavunja ukimya baada ya kuendesha kimya kwa muda. “Hamna kitu nakufanyia Vai! Mimi sina kitu.” “Acha kusema hivyo bwana Bale! Utafananisha wakati tunaokuwa nao na pesa?” Bale akatulia. “Kuwa mkweli Bale. Tumefahamiana siku chache tu, lakini muda tunaokuwa nao tukiwa pamoja, utafananisha na mafanikio ya pesa?” “Mimi mwenyewe sijawahi pata huo wakati kwa muda mrefu sana.” “Sasa kwa nini unataka kufananisha na pesa? Mimi mwenzio sijawahi kupikiwa na mwanaume.” Bale akacheka.

“Kweli Bale. Eti mwanaume anipikie na aje anifuate nikale! Na hangaika yangu yote maishani na wanaume, sijawahi Bale.” “Basi Vai.” “Naomba acha kufikiria tusicho nacho, tufurahie tulivyo navyo.” Bale akajua Mungu amemuamulia kwa aina ya watu anao mkutanisha naye.

Vai alionekena mtoto wa mjini, mpenda kujirusha, lakini akamshangaza sana Bale kwa kadiri alivyoendelea kumfahamu. Bale akatulia kimya. Maana mwanamke wa kwanza kumpenda na kumthamini hapa duniani ambaye ni mama yake, hakuwahi kumsikia ameridhika na kitu ila kulilia maendeleo kila wakati. Alitaka zaidi na zaidi. Hata katikati ya biashara mpya walizokuwa wakijaribisha nyumbani kwao, basi mama yake hakuwahi kuridhika ila kutaka zaidi na zaidi. Ikamuingia Bale. Naye akawa kijana wakutaka zaidi. Akipata, anataka tena. Ikajengeka tabia ya kutoangalia alicho nacho ila ambacho hana. Akatulia kimya hapo garini akiendesha.

Walifika anapoishi Bale, mpaka akamshangaza Vai. “Sasa wewe utakuwa uliamka saa ngapi na kupika vyote hivi?” “Nataka ufurahie Vai.” “Kwa kweli nimefurahi. Na nilivyo na njaa, pamoja na usingizi! Tule nikalale. Ila kesho tunaanza kusoma tena.” “Usijali. Kula huku unaniambia mambo yalivyo kwenda kwenye mtihani.” “Mimi nahisi nilizidisha kujiamini.” Bale akaanza kucheka akimwangalia.

“Usinicheke, ni makosa yako wewe mwenyewe. Yaani nilitulia mpaka mwenyewe nikajishitukia.” “Jinsi ulivyojiamini?” “Usifanye mchezo.” “Sasa katika kujiamini huko, majibu ulikumbuka lakini?” Vai akapoa. “Sasa nesi wangu wewe vipi tena!? Mbona unaniangusha?” “Yale majibu mimi naanza kuyatilia mashaka bwana. Mbona kama nilikuwa nikiandika sana!” Bale akazidi kucheka hana mbavu.

~~~~~~~~~~~~~~~


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment