Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 33. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 33.

Wasiwasi ukamwingia akihofia asije kuwa mzee amemfuata. Na hivi amehusika na kukarabati nyumba! Akajigeuza vizuri ili kujua anayeingia. Akakumbuka wivu wa mzee, akajua anaweza kumbana kwa makusudi ili asije hamia kwa mwingine. Wasiwasi ukamuingia lakini roho ikatulia alipomuona Colins kwa kupitia mwanga wa mlango alio ingilia. Akajiweka sawa, ndipo akajua alishaamka. “Nimekuamsha?” “Hapana.” “Niwashe taa au unataka kuwe giza?” Akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu, hakujua anataka nini.

Akamsogelea. “Ulilala vizuri?” Akakubali kwa kutingisha kichwa. “Vipi kichwa?” “Kinauma, Colins.” Akajibu taratibu. Akamshika kichwani akimpapasa. “Pole sana.” “Nikuulize kitu?” “Niwashe taa ili tuzungumze vizuri?” Akakubali. Akawasha taa na kwenda kukaa pembeni ya kitanda.

“Unataka kuniuliza nini?” “Kwa nini upo hapa na mimi?” “Kwa sababu nataka kuwa hapa na wewe.” Jelini akamwangalia, akiwa amekunja uso kama ambaye hajaelewa, na kutulia na yeye Colins akabaki akimwangalia, Jelini akakwepesha macho.

“Uliniambia sikukeri, Jelini. Au imebadilika, nimekuwa kero?” “Hapana. Wewe sio kero kwangu. Nilitaka tu kujua.” “Kwa hiyo sasahivi umeshajua?” Colins akamuuliza kwa kumbembeleza. “Nafikiri. Labda! Hata sijui! Nipo kwenye wakati mgumu Colins! Sijui chakufikiria. Natamani nitumie njia yangu ya zamani kujituliza, ila naona nitapotea tena.” “Pombe haitakusaidia Jelini.” Akaongea moja kwa moja kama mtu anayemfahamu vizuri sana mpaka Jelini mwenyewe akashituka na kuishiwa nguvu. Hakutegemea, akamwangalia.

“Mabadiliko uliyoyafanya kwenye maisha yako, kwanza nakupongeza. Pili, usirudi tena nyuma. Ukiwa na akili hiyohiyo, sasahivi, na changamoto unayopitia, anza kujifikiria na kuendelea kuanzia hapa. Ukianza na changamoto hii kwa tabia ile ya nyuma, utaharibu msingi mzima ulioanza kujenga na kuaharibikiwa zaidi kabisa.” “Itakuaje kama msingi wenyewe nilianza na mtu? Nakuwa kama nakosa dira Colins. Inakuwa kama mtu amekutoa sehemu moja, anakufikisha sehemu nyingine, halafu anakuacha! Naogopa, nahisi kama kuporomoka.” “Hizo ni hisia zilizoumizwa ndio zinakuogopesha. Umeshawahi kusikia usemi kuwa unaweza kumpeleka punda kisimani na asinywe maji?” Anamuuliza huku akimfuta machozi. Jelini akakubali.

“Basi jua unaweza kupelekwa hiyo ‘sehemu moja’, na kama hujaamua kukaa hapo, hata kama ni Mungu mwenyewe ndiye aliyekupeleka, utaondoka tu. Kwa sababu hujaamua. Wewe umeshafikishwa sehemu, lakini ni wewe Jelini ndio ulikubali kufika, na sasahivi unalo jukumu la kubaki hapo ulipo na kwenda mbele zaidi. Au ukarudia maisha yale ya kushinda baa, na kulala klabu.  Au kushinda baa ukinywa, na kulewa masaa yote. Wewe Jelini ndio unao huo uwamuzi na si mtu mwingine yeyote.” Jelini akamshangaa Colins anavyozungumza habari zake kama anayemfahamu sana! Akajisikia aibu, na kunyamaza.

“Umenielewa?” “Lakini nilibadilika Colins. Niliacha hayo maisha ya kushinda baa, na ulevi.” Jelini akajitetea. “Naomba ujisikilize mwenyewe. Umesema uliacha, na umebadilika. Wewe kama wewe, wala si mtu mwingine. Sasa usirudi nyuma. Usikubali mwanadamu uliyekutana naye kwa muda mfupi, akakuchanganya kiasi cha kuharibu maisha yako. Sikatai yapo maumivu. Lakini ukiwa na akili  safi, itakusaidia kufikiria jinsi ya kuendelea kuanzia hapo. Pole. Lakini hayo maumivu yabebe ukiwa na akili zako timamu. Na usiyazike kwa kulewa, maana hayatakaa yakaisha. Kila pombe itakapokuwa ikiisha, akili itakutuma kwenda kuchungulia kule ulikoficha, kisha kuendelea kunywa zaidi na zaidi. Na ndio maana wanaolewa kwenye matatizo huwa hawaachi pombe mpaka watatue hilo tatizo. Na nikujichelewesha. Usikubali kuchelewa hapo. Jambo limeshatokea, kubali matokeo na jua jinsi yakuendelea kuanzia hapo.” Jelini alishindwa hata kumtizama, akabaki kimya.

“Nikuletee chakula ule?” Jelini akakataa. “Kula kidogo.” “Nimejawa hofu, majuto, uchungu kiasi ya kwamba yote hayo yamejaza tumbo langu. Sina nafasi ya chakula. Acha tu nilale tu.” “Basi acha nilete movie tuangalie wote ili upumzishe mawazo. Ni sawa?” Akakubali. Alipotoka tu Jema akaingia.

Jema Kwa Mdogo Wake.

“Vipi mtoto wa mama Jema?” “Njoo ukae hapa.” Jema akaenda kukaa na tumbo lake. “Hapa nimeshiba chakula cha mama Colins, nahemea juujuu.” Jelini akamwangalia na kunyamaza.

“Pole Jelini mdogo wangu. Japokuwa sijui ni nini kimekuumiza, lakini naomba fikiria afya yako. Kichwa hicho, bado. Utajiumiza bure.” “Nimeanza kukuonea wivu, Jema! Nakutamania! Maisha yako yana uhakika sasahivi.” Jema akamwangalia na kucheka kama anayetafakari hilo. “Tutakuja kuzungumza zaidi. Lakini si unajua chochote nilichonacho na wewe Mungu anaweza kukupa? Ni kutaka kwako tu na kuwa tayari.” Jelini akaanza kulia.

“Mungu hana upendeleo mdogo wangu. Ni wewe tu kuwa tayari kulipa garama kwa unachokitaka. Huwezi kutaka mtoto wa kumzaa, halafu eti hutaki kubeba mimba! Sijui kama unanielewa? Kila baraka inakuwa na wajibu wake. Ndio maana wengine wanaona shida kuwajibika, wanatafuta njia fupi. Sasa labda wewe uniambie unataka upande gani?”

“Una mwanaume anayekupenda Jema! Anakutetemekea, utafikiri nini sijui! Mimi na mama tunakusema hatumalizi. Mumeo anakuthamini kupita kiasi! Japokuwa mimi nimefanya mengi mpaka yale niliyokufundisha na wewe, lakini sijabahatika kupata mwanaume hata nusu yako Jema!” “Sema hujabahatika bado. Wewe bado mdogo sana, halafu sasahivi ndio kama unakua Jelini. Ulicheza sana hapo katikati. Kwa hivi ulivyo sasahivi, halafu ukajua unachokitaka, na kujipa muda, utapata sana tu. Jipe muda na jiwekee malengo bila kukata tamaa na kuyumbishwa. Utafika tu.”

“Unakumbuka mimi nilivyotendwa na Temu?” Jelini akatingisha kichwa kukubali. “Niliingia aibu ya mwaka, maana mwanaume alijua kunichafua yule! Ni vile nilishindwa kumwambia mama, nilijua nitamuumiza tu. Nilishindwa hata kwenda kanisani. Nilikuwa siwezi kula wala kulala. Aibu na fedhea.” “Ulitokaje hapo?” Jelini akauliza.

“Mungu alinisaidia Jelini. Japokuwa nilikuwa nimeumia, lakini sikuacha kuomba. Na sikukata tamaa ya kuja kupata mtu wangu. Mwenzio nilikuwa nikijitunza nikijua kabisa, nitakuwa mke wa mtu fulani. Niliishi kama namtunzia mtu kitu chake. Sikutaka kujiachia kwa yeyote, wala kwa sababu yeyote ile. Hata walipokuwa wakinitongoza, wenye pesa na wazuri, kama hapakuwa na ndoa, nilijitenga bila yakufikiria mara mbili.” Jelini akaumia sana.

“Mimi nitakwambia ukweli Jelini. Haya maisha ya mama zetu, mimi mwenzio siyapendi. Niliionya nafsi yangu, ndio maana nilijikana kabisa. Nilimwambia Mungu anisaidie, nivunje hii tabia za mama zetu, hata watoto na watoto wetu waje wajue zipo ndoa. Sikutaka watoto wasio julikana baba zao kama sisi. Binafsi sikutaka kabisa. Na ndio maana sikujichanganya hata katikati ya majaribu, nilijikumbusha nini nataka. Nikamlilia Mungu mpaka akanipa James wangu. Mume wangu hana makuu, au mamilioni ya pesa, ila ana upendo wa kweli, ndicho nilichokuwa nikikitaka. Basi. Kwa hiyo hata wewe hujachelewa. Jiwekee malengo. Omba Mungu, atakusaidia tu.” Jelini akabaki akilia kwa uchungu.

“Pole sana Jelini, mdogo wangu. Kama anavyosema Colins, ‘it gets better’. Hapo ulipo, mwenzio nilipita. Ila sikuwa na mtu, ila peke yangu. Aibu, kusema huwezi, maana mama alishanionya juu ya Temu, nikashupaza shingo! Halafu kama unavyonijua mimi, sina msiri wa kumwambia mambo yangu ila Mungu. Hakika niliteseka. Ila wewe upo na sisi. Tutumie sisi tuliokuwepo karibu yako kujipatia faraja. Halafu uzuri ni kuwa, na mimi nimepita hapo. Mama Jema yupo na wewe. Usiumie peke yako. Umesikia?” Akatingisha kichwa kukubali.

“Unataka kula kidogo?” “Siwezi. Tumbo limejaa gesi. Nahisi na mshituko pia.” “Nikutengenezee chai hata ya rangi?” Akatingisha kichwa kukataa. “Toka basi hapo kitandani angalau uangalie tv upoteze mawazo.” “Colins amesema analeta movie tuangalie.” Jelini akajibu akijaribu kutulia akifuta machozi. “Hiki chumba hakina tv. Labda akalete ya kule chumbani kwake. Colins?” Akaanza kumuita.

Akafika hapo na kibegi chake kama aliyekuwa akisubiria aitwe. “Labda uhamishe ile tv ya chumbani kwako huku.” “Tutatumia laptop yangu. Asante.” “Basi mimi naenda kuoga nijilaze kitandani wakati nikimsubiria James. Mkitaka kitu, mje kunigongea.” Jema akawaacha hapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ikawa kama kijihofu na aibu kimemuingia Jelini! Colins anamfahamu kuliko anavyodhania. Akakumbuka na maneno ya dada yake juu ya wanaume. Akajihisi vibaya na kujiona mjinga kama alivyosema Koku. Kwamba anajiliza kwa mwanaume asiye mume wake. “Lakini nilimzoea Zenda!” Jelini akajisemea nafsini kwake na kuona machozi yakimtoka. Akakumbuka nyakati nzuri alizokuwa nazo akiwa naye. Vicheko na utulivu. Halafu Zenda alijua kutumia mwili wa Jelini vilivyo!

“Ndivyo anavyofanyia wanawake zake wote!” Akaumia sana kuona amepitisha midomo yake kwenye mashine inayoingia kwa wanawake wengine na yeye akipitiwa! Akajichukia na kuona kinyaa cha hali ya juu.

Akakumbuka vile alivyomsikia Zenda akipiga bao akiwa na Koku, hasira na wivu vikamzidia. Akainamia mto nakuanza kulia akishindwa kujizuia. Akalia akiwa amefunga mdomo na sauti isisikike, akisikia maumivu makali moyoni. Hakuwa na wakumlaumu hata Zenda mwenyewe. Koku ni mwanamke wake. “Lakini aliniambia atamuacha kwa ajili yangu!” Akazidi kunung’unika rohoni.

Akakumbuka alivyokuwa akikataa watu, akijiambia anasubiri wake wa peke yake, kisha kuangukia kwa mwanaume aliyemuaminisha hatamsaliti, na kuja kumfumania akipiga bao kabisa! Jelini alilia sana. Colins akaweka vitu pembeni na kumsogelea pale alipokita uso wake kwenye mto. Akaanza kupitisha mkono mgongoni taratibu akitumia kucha. Akamfanyia hivyo kwa muda mpaka akamsikia ametulia. Akatoka kitandani.

“Unakwenda wapi?” “Nataka kuoga, ndipo nilale.” “Basi acha nikupishe, nitarudi baadaye.” Colins akatoka. Jelini akapiga magoti pembeni ya kitanda na kuanza kulia tena kwa uchungu, sauti ya chini, tena kwa uhuru. Alilia bila ya kunyamaza mpaka kichwa kikaanza kugonga kama kinapasuka. Hapo akakaa kitandani na kuanza kujituliza na kushindwa.

Ikawa kama bahati, Jema naye akawa amepigiwa simu na mama yake, anataka kuzungumza naye. Anaingia na kukutana na Jelini anayelia sana. “Sidhani kama ataweza kuzungumza mama. Acha atulie tu.” “Nilikwambia mpe dawa ya usingizi Jema! Atajiumiza huyo, mimi ndio nipate hasara.” “Acha kulalamika mama, bwana! Alikuwa amelala. Nampa dawa sasahivi atalala tu.” “Najua umechoka Jema mwanangu, lakini usimsahau huyo. Tafadhali mama yangu. Nakuja mwenyewe kesho.”

“Mama, unanilaumu bure! Lakini sijamsahau. Naomba utulie, Jelini atakuwa sawa. Anahitaji tu muda. Hata kama wewe mwenyewe ungekuwepo hapa sasahivi, ingekuwa hivihivi. Mimi nazungumzia uzoefu. Nimekua hapo alipo Jelini. Anahitaji huu muda kupokea ukweli. Akisha kubaliana na ukweli, ndipo atatulia. Hakuna utakachofanya sasahivi akawa sawa, isipokuwa muda ndio utasaidia. Tulia ili na yeye ataulie.” Kimya. “Nampa dawa, atalala tu.” “Nashukuru.” Mama Jema akakata simu akisikika kutoridhika kabisa.

“Nataka nikaoge Jema, ndipo ninywe dawa, nilale.” “Basi vua nguo twende bafuni.” Akamsaidia mdogo wake mpaka akaoga, na kurudi naye kitandani. Alimpa nguo yake ya kulalia. Akamfunika shuka vizuri ndipo akamruhusu Colins kuingia. Jema akatoka, Colins akaingia mpaka ndani ya chandarua na yeye akionekana alishaoga vizuri tu maana alivaa pajama nzuri za kiume.

~~~~~~~~~~~~~~~

Kitakachoendelea Katikati Ya Kilio Cha Jelini Usiku Huo Mikononi Kwa Colins!?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment