Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 32. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 32.

 James akarudi ndani. “We James?!” Jema akampokea kwa mshangao. “Mimi sijui aisee! Na usimuone hivyo Colins. Kila mtu anamjua pale kazini. Ana msimamo usio yumba. Akiamua jambo, ameamua. Na mkikubaliana jambo, ujue yeye atasimamia hata kama mabosi watabadilika, si yeye. Na usimuone vile na sura yake ya upole ukafikiri ni mjinga! Si nilikwambia ndiye supervisor wangu?” “Nakumbuka uliniambia ni kama kiongozi wako.” “Sasa ni wa kitengo chetu tu. Lakini kichwa yake na electonics, pale wamemnyanyulia mikono. Mkimya hivyohivyo na sura yake kama mtoto mpoleee, lakini mpaka kina Kasa wanakuja kuomba msaada kusaidiwa kwenye kitengo chao, kwake yeye huyo. Pale kazini anajulikana kama Electronics Genie. Ukisikia anatafutwa Genie, ujue kuna lililoshindikana mahali, ndio wanamtafuta yeye. Kwamba akitamka jambo, kwa kushika kifaa chochote pale kazini, lazima mtandao wowote ule ujibu na kutii. Kwa hiyo si mjinga. Anajua sana anachokifanya hapa.” Pakazuka ukimya hapo. Anasubiriwa yeye.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda akagonga mama yake. “Jema mama, naomba ukanifungulie mlango wa gari dada amuwekee mataulo. Akioga na kutumia taulo mara moja, hawezi kurudia tena.” “Ila na mimi ninayo mataulo mengi tu yakutosha mama yangu.” “Wewe wala usijali. Acha nikuwekee tu na haya. Akiyatumia, anajua jinsi ya kuyaweka vizuri mpaka yaje kufuliwa hapa na mashine. Nisikupe kazi zaidi. Na jioni dereva akimletea gari yake, nitampa na chakula awaletee wote mle. Ili upumzike na safari, usihangaike kupika.” Jema akacheka.

“Mbona huu ugeni mzuri! Na chakula!” Wakacheka. “Ila usingehangaika mama yangu. Tungekuwa tu sawa.” “Sitaki huu ugeni uwasumbue. Mimi namjua Colins.” Wakacheka tena. “Ila atatusaidia kutupa taarifa kujua Jelini anaendeleaje. Mkitaka ushauri wa kidaktari Connie au mimi nitawashauri.” Mama Colins akaongea akicheka akionekana alisikia mazungumzo yake na James. “Yupo hivyo kama baba yake. Mumvumilie. Najua James ameshamzoea. Ila Jema, itabidi umvumilie tu.” “Wala usijali mama yangu.” Connie naye akaingia.

“Jelini, chukua namba yangu. Ili muda na wakati wowote ukijisikia sivyo, unipigie, nikushauri.” “Kwani wewe Connie ni daktari pia?” Jema akamuuliza. “Ila ndio nipo intern. Namalizia.” “Hongera Connie.” “Asante. Nafuata nyayo za dad.” “Kwamba unataka kuja kuwa surgueny pia!? Sio muda mrefu sana!?” Akacheka vile Jema alivyouliza kwa kushangaa. “Napenda mwenzio, anti. Naona wala sio muda mrefu. Nafurahia kila hatua.” Akamgeukia Jelini. “Utakuwa sawa Jelini. Sisi wote tupo kwa ajili yako. Na ukisikia upweke tu. Muda na wakati wowote, nipigie mimi hata mama. Ila mama ndio zaidi. Mzuri sana kwenye kusikiliza. Usiumie peke yako. Umesikia?” Jelini akajifuta machozi na kutingisha kichwa kukubali. Jema akashangaa anamkumbatia na kumbusu. “Kila kitu kitakua sawa.” Akambembeleza taratibu.

“James.” Wakasikia sauti ya Colins. “Bado gari imefungwa, tunashindwa kuweka mizigo!” James akatingisha kichwa nakutoka. Wakacheka. “Nitampigia simu na mama Jema kumwambia juu ya Colins.” “Wala usiwe na wasiwasi mama. Huyo Colins pale kwetu tumeshamzoea ila kulala tu.” Wakacheka tena. “Acha nimuandae tu. Maana kesho habari inaweza kuja kuwa kama hii hii ya leo huko kwa mama Jema.” Baada ya hapo wakatoka hapo kuelekea nyumbani kwa Jema na James.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Abiria wao, Jelini na Colins wamekaa nyuma. “Niambie nini kinauma sasa hivi.” Wakamsikia Colins akimuuliza kwa sauti yake nzuri, tulivu ila kwa chini. Jelini akajifuta machozi na kujishika moyo, kumuashiria maumivu yanatoka moyoni. Mbele hawakuona. “Pole Jelini. Lakini nakuhakikishia, it gets better. Sasahivi kwa kuwa umeumia, unaweza usiniamini. Lakini it gets better. Promise.” Jelini akatingisha kichwa kukubali kisha akajiegemeza kitini akiangalia nje. James akaendelea kuendesha kurudi kwao. Hapohapo Jema akapitiwa na usingizi. Kimya.

Uzuri kilikuwa kipindi cha sikukuu, hapakuwa na foleni sana, haikuchukua muda mrefu, kutoka nyumbani kwa kina Colins, Mbezi Tangi bovu mpaka kwa James Salasala. “Twende ukalale ndani, Jema. Chakula kikiwa tayari nitakuamsha.” James akamwamsha mkewe kwa upendo. “Twende. Na usibebe kitu. Mimi nitakubebea mpaka pochi.” “Asante. Mgongo unauma! Naona sababu ya safari.” “Pole. Basi nenda kajilaze. Nakuja.” “Nisaidie kubeba nini?” Colins akauliza. “Wewe mwenyewe una mizigo yako humu!” James akamjibu, Colins akaanza kucheka. James akamwangalia na kuanza kuingiza masanduku yao maana na wao ndio walikuwa wametoka safari hata kwao hawakuwa wamefika. “Twende ukapumzike Jelini.” Akatoka garini na kumfuata dada yake nyuma mpaka kwenye chumba ambacho angelala.

Mara Colins akaingia bila hodi. “Wewe nipe mashuka, mimi nitatandika.” “Kumbe bora umekuja maana nina usingizi, nataka nikajilaze. Nakutolea kila kitu na mashuka ya chumbani kwako, kisha naenda kulala.” Jema alichofanya ni kutoa mashuka na mataulo, akaenda kujilaza na kuwaacha hapo. Jelini amekaa kiti cha hapo chumbani amejiinamia.

Colins&Jelini.

Akamtandikia vizuri na kumwangalia. Bado Jelini alikuwa amejiinamia hapo kitini. Akaenda kuchuchumaa mbele yake na kumshika magoti akimchungulia pale alipoinama. “Niambie unataka nini Jelini.” Jelini akamwangalia na kupandisha mabega kukataa. Mawazo yalikuwa mbali. Akitafakari maneno ya Koku, yalimtesa sana Jelini. Akaanza kujidharau na kujiona mjinga. Aibu, akijiuliza alikuwa akifikiria nini kitaendelea kati yake na Zenda! Akashindwa kupata jibu. “Ila sikutegemea mwisho wa namna hii! Zenda!” Akashindwa kukubali, ila sauti ya Zenda akipiga bao chumbani kwake ikamuhakikishia, si mawazo.

“Nakukera, unataka niondoke?” Colins akauliza lakini akiomba Mungu asifukuzwe. Jelini akatingisha kichwa kukataa. Colins akafurahi sana. “Nifanye nini ili utulie?” Akatingisha kichwa kukataa. Kwamba hakuna chakufanya. Vile Colins alivyo mzuri na sauti yake, vilikuwa vikimtuliza Jelini nakushindwa kujielewa. Japokuwa alikuwa na uchungu wakusalitiwa, lakini alishindwa kumfukuza Colins. Kule kumbembeleza, kulimpa hisia ambazo hakuwa akijielewa. Zenda alikuwa mawazoni. Sasa hichi kinachompata kwa Colins ni nini tena! Hakujua kwa wakati huo. Ila hakutaka aondoke.

“Basi njoo nikubembeleze ulale.” Akili zilikuwa zikikataa kabisa, na japokuwa hakuwa akijua anabembelezwaje, lakini moyo ulikubali. Akabaki ameinama vilevile. Akasimama pale alipokuwa amechuchumaa, akamshika mkono, na kumvuta taratibu ishara ya asimame. Akajishauri, lakini akasimama, akamuongoza kitandani. Jelini akapanda na kujilaza ubavu akiangalia ukutani. “Kichwa bado kinauma?” Akamuuliza kwa kumbembeleza. Hiyo sauti ya Colins yenyewe tu, inatuliza.

“Naomba zungumza na mimi Jelini. Tafadhali.” “Sisikii kuzungumza Colins. Nataka kunyamaza tu peke yangu.” “Basi nakubembeleza kimya kimya. Ila naomba usilie, ulale.” Akatingisha kichwa kukubali.

“Nigeukie Jelini. Usinipe mgongo.” Jelini alishangazwa moyoni, nakushindwa kuelewa. “Hivi sijasema kama nataka kulala?!” Akawaza mawazoni. “Nakukera?” Akauliza kwa upendo kama mtoto mkiwa. Jelini akamuhurumia vile anavyojitoa kwake, akajirudi. “Hapana Colins. Ila nimejawa fedheha!” Akamjibu na kumgeukia. Akamfuta machozi. “Kwa nini?” “Sijui Colins! Ila nimejidharau sana, nakujiona mimi mjinga! Nimekua ndege mjanja. Lakini nimebanwa kijinga sana. Ndio maana nina maumivu. Nisamehe kama nakua mbaya kwako. Lakini hunikeri. Nakushukuru kwa ukarimu wako, hata kuwa hapa na mimi.” Akamvuta mkono na kuubusu kwa muda mrefu akiwa amefunga macho kama anayesikilizia hisia fulani, nzuri hivi, asijue na Jelini naye anapata faraja.

Kisha akafungua macho na kumuangalia. Akakuta Jelini akitoa machozi. Akamfuta. “Asante Colins. Ila sitaki ubakie hapa na mimi. Sitaki tukwame wote. Mimi nitakuwa sawa. Nahitaji tu muda kujiweka sawa mawazoni. Wewe rudi nyumbani uendelee na mambo yako.” “Mimi nataka kuwa hapa na wewe Jelini. Tafadhali usinifukuze. Niache tubaki wote. Nakuomba.” “Sitaki tukwame wote.” “Kuna usemi unasema, wawili ni bora kuliko mmoja. Maana mmoja akianguka, mwenzie anamuokota. Naomba nafasi ya kuwepo tu.” Sauti ya kubembelezana hapo, ungejua tu hakuna anayefukuzwa.

“Na nikwambie ukweli Jelini?” Jelini akamwangalia akijitahidi kufuta machozi. “Sijisikii kukwama hapa. Nikijiuliza sehemu sahihi ya mimi kuwepo muda huu, najikuta najiambia ni hapa tu, ulipo wewe. Mimi nataka kukaa hapa ulipo.” Jelini akatingisha kichwa kukubali. Akamlaza mkono juu ya mapaja yake akaanza kumpapasa taratibu huku mkono mwingine ukimpapa kichwa na kuweka nywele sawa. Kisha kuchezea vinyweleo. Jelini alikuwa akisisimkwa mpaka akajishangaa. Faraja aliyokuwa akijisikia! Halafu ni Colins! Hakuna mchana wala usiku ukamwangalia akawa havutii! Roho ya Jelini ikaanza kutulia na kupitiwa usingizi hapohapo.

Kule Kuliko Ungua Mpini.

Mzee akiwa bado anawakwa moyoni akaweka mipango kuhakikisha na Koku anafungiwa alipo Kemi ili ajue ukweli. Hapo pesa yake ilikuwa ikitembea kwa hasira asijue amwadhibu nani na kwa umbali gani. Kila dakika iliyokuwa ikizidi kupotea bila Jelini, ndivyo chuki ilivyozidi kumpanda. Akataka kuwakomoa vilivyo, ili wapate maumivu aliyo nayo moyoni.

Koku anaingia alipokuwa amefungwa Kemi, Kemi akashituka sana. “Kama wewe siye uliyetuchoma kwa baba, yeye amejuaje!?” “Yaani wewe ulifikiri mimi ndiye niliyewageuka!?” Koku naye akauliza kwa kushangazwa sana. “Kabisa. Nilijua ulikolezwa, ukaishia kuropoka kama mjinga.” “Jiangalie Kemi! Baba yako hana uwezo huo.” “Uwezo upi? Wakukulala au kukuhonga mpaka kufikisha hapo ulipo?” Wote wakiwa na hasira wakaanza kutukanana, sasa Koku ikawa zaidi. Anamtukana Kemi na baba yake.

Ugomvi. “Kama kweli hana uwezo huo mbona hatujakuona ukiolewa na kijana akakukaza kweli, umebaki ukimng’ang’ania tu yeye?” “Kama utakumbuka vizuri ni wewe mwenyewe ndiye uliyenitafuta, na kutaka niwasaidie kumtoa Jelini kwenye maisha ya baba yenu. Wala mimi sikuwa na mpango naye tena, mtu mzima hovyo, anaye tetemesha na kijitoto kisichojua chochote! Siwezi kuwa na mwanaume dhaifu, mjinga kiasi hichi. Kasa niliyemjua mimi enzi hizo alikuwa mwanaume kweli, ukiwa naye unajisikia upo na mtu! Sio wa sasahivi, upuuzi mtupu”

“Kama mpuuzi, mbona yamekushinda umeishia hapa?” “Kwanza kwa taarifa yako nipo hapa kwa sababu nimefanya kazi yangu vizuri. Wewe ndiye uliyeshindwa kufanya upande wako mpaka tumekamatwa.” “Sijashindwa chochote. Mambo yalikuwa sawa, ndio maana nashindwa kuelewa baba ameshitushwa na nini mpaka kujua yote haya!? Ni nini kilichomfanya ajue kama na wewe ulifanya kwako kama tulivyokwambia?” “Acha maswali ya kijinga kama vile humfahamu baba yako. Swala la Kasa kufikiria ndio unalijua leo baada ya kuishia lupango? Wewe ndio mjinga kama kale katoto. Na sitakuficha kama nilivyomwambia Kasa na Jelini. Wote nyinyi ni wajinga. Hamuwezi kufikiria. Kale katoto kanajiliza mbele ya Kasa akijidai kamemfumania Kasa, yeye kama nani? Alitegemea ataolewa na Kasa, malaya anayeng’ang’ania wanaume tu! Eti na Kasa naye anatetemeshwa! Kwa lipi mno!? Malaya wa Tegeta yule!” Jazba likampanda zaidi akaanza kuropoka hapo, wasijue wanarikodiwa na askari magereza aliyekuwa zamu.

“Usiniambie na hayo uliropoka pale mbele baba, sababu ya wivu wako!?” “Wivu wa nini mimi? Kama ningekuwa namtaka zee lile si ningekuwa naye? Sina shida na babu. Na yeye analijua hilo ndio maana alivyompata Jelini, ameng’ang’ania akijua ameshaisha soko. Nguvu yenyewe yakumuweka mwanamke kitandani hana. Anahangaika kitandani kama mpumbavu wa mwisho! Yule mtoto anamlia tu pesa yake, anamtapeli. Mzee amechanganyikiwa mpaka amempa sehemu ya kuweka nguo! Yaani Kasa anampa sehemu ya closet yake mtoto mchafu kama yule wakati mimi hataki hata niache mswaki wangu pale!” Hapo akaonyesha chuki yake kwa waziwazi. Akaropokwa zaidi, mtaka hataki. Anajikoroga na kujichanganya.

“Nilikuwa nakusubiri nijue ulipojichanganya ni wapi. Yaani hasira yote hiyo, mpaka kuropoka kwa baba, na kusababisha wote tuingie matatizoni, ni kwa sababu uliona nguo za Jelini kwenye closet ya dad!?” “Sina shida.” “Shida unayo, maana ndicho kilichokufanya uropoke na wote kuishia hapa. Wewe mbinafsi na mjinga wa mwisho. Jumba lote ulilonalo lile bado unalalamikia sehemu ndogo aliyopewa Jelini kuweka nguo zake?!”

“Acha kelele na fikiria Kemi kama mtu mzima. Swala si sehemu ya kuwekea nguo. Kufanya hivyo kwa Kasa, ni zaidi ya hivyo na wewe unajua. Na kwa taarifa yako si sehemu tu. Ni kama nusu ya chumba cha kuwekea nguo za Kasa, amempa Jelini wakati mimi nikiacha tu hata mswaki ananiambia nisipochukua, anatupa! Hataki kitu cha mtu yeyote yule, kibakie kwenye nyumba yake, kichukue sura ya mtu mwingine mle ndani kwake, isipokuwa yake yeye mwenyewe Kasa. Leo, Kasa anayethamini mavazi, na wote tunamjua, anayo mpaka sehemu maalumu yakuwekea saa zake za mkononi, eti ajibane, halafu ampe Jelini sehemu ya kile chumba kinacholindwa na kamera! Kweli Kemi?”

“Halafu badala unishukuru nimemtoa yule mtoto kwenye maisha yake, unanitukana! Unafikiri bila hivyo wote nyinyi na mama yenu mngeishia wapi kama sipakavu? Maana mwisho wa Kasa ungekuwa ni kumpa mali zote yule mtoto na nyinyi kuambulia patupu?”

“Sasa, sasahivi hapa hizo mali zinatusaidia nini, tukiwa wote tumekwama hapa na shutuma za kutaka mumuua? Kwa ujinga wako, bila kutumia akili, kuwazidi mahesabu, kufanya mambo kama tulivyopanga, umeharibu, wote tupo ndani kwa kosa la kukusudia kuua. Tunatoka lini na kunufaika na hizo mali, kama si ujinga huo unaozungumza ukijitetea kama mtoto mdogo? Tukushukuru kutufikisha hapa, wewe kubwa jinga uliyezidiwa wivu kwa mwanaume uliyejua fika hakutaki!”

“Nishakwambia sina shida na baba yenu, acha kuniita mimi mjinga. Nilisha…” “Wewe ni mjinga tu Koku hata ukikataa. Ulijua fika hutakaa ukawa kwenye maisha yake, hakutaki kwa maisha marefu. Ni kukutumia tu, sasa kwa nini kupatwa wivu na jazba kwa Jelini tuliyekwisha kuweka mipango ya kumtoa ili asifike mbali?” “Kwa taarifa yako alishafika mbali. Shukuru mimi niliyefanikiwa kumtoa. Na usifikiri Kasa alikuwa akinitumia peke yake, hata na mimi nilikuwa nikimtumia. Mimi si mjinga.” “Huna lolote mpuuzi tu wewe. Unapoteza malengo katikati mipango mizuri tuliyoweka sababu ya kukutana na mtoto aliyekuzidi mahesabu! Na sisi tulikwambia kabisa na tukakuonya! Kama si ujinga huo ni nini? Hata kukataa hapo ni ujinga zaidi.” Hapo akazidi kumuudhi Koku.

“Wewe ndiye mjinga wa mwisho Kemi, usiyeweza kufikiria na kutafuta mtu wa kumlaumu badala yakujilaumu mwenyewe. Wewe kwa akili zako hukujua madhara ya kumgeuka Kasa?” “Kama sio wivu wako wa kijinga, mipango yetu yenye akili ilikuwa ikienda vizuri tu, mpaka wewe ulipoingiza mapenzi kazini.” “Mimi sitaki ujinga. Kasa hawezi kunichezea.” “Sio hutaki ujinga, ni hutaki kushindwa. Umeona umeshindwa na mtoto mdogo ambaye hana hata shule kichwani, lakini baba amesalimu amri kwake, amempa anachokataa kukupa wewe, ndio wivu huo.”

“Nani amekwambia mimi nina shida na Kasa? Kashanitimizia yangu, nimeridhika, nikatulia kwangu. Nyinyi na mama yenu ndio hamtosheki naona mpaka mpate roho ya Kasa ndio mtatulia. Kutwa mpo mfukoni kwake mkichota pesa yake bila kuchoka, huku mkilinda isije kwenda kwa mwingine isipokuwa nyinyi watatu tu. Tena mpaka na mumeo chupi anategemea kwa Kasa. Ndio maana wote mmeishia hapa, wala sio mimi. Mchawi wako kamtafute kwenye kioo, na mama yenu asiyetosheka na pesa ya mwanaume aliyesema hamtaki, akaolewa uzunguni akidhani ni bora, ila chakushangaza kutwa macho yake yapo kwenye mifuko ya Kasa.” Hapo akakanyaga pabaya zaidi. Kemi akamrukia wakaanza kupigana, wafungwa wengine wakiwaangalia nakushangilia, mwishoe wakaja kuamuliwa na askari magereza, na kutenganishwa wakiwa wameshachukuliwa ukiri wao wote.

Kuliko Baki Shoka.

Yakiwa yanawarudia wenyewe, yeye Jelini alilala akibembelezwa, akalala asijue alipo mpaka jioni kabisa, akashituka na kujikuta peke yake kitandani. Akatulia tu akijitafakari na kurudia maneno ya Koku. Ukweli juu ya utofauti wake na Zenda, ukaanza kuingia akilini. Akavuta pumzi kwa nguvu na kujituliza hapo kitandani. Akatamani kulia, akakumbuka tena Koku akimuuliza anacholilia. Akajisuta ila kuumia rohoni. “Hata kama asingenioa, lakini nilikuwa nikifurahia kampani yake! Tulikuwa tunakuwa na wakati mzuri!” Jelini akazidi kuumia asijue alitegwa na kutegeka vizuri sana. Japokuwa waliishia lupango, lakini lengo lilitimia kwa hakika. Walifanikiwa kuuchafua moyo wa Jelini vilivyo.

Sauti ya Zenda katikati ya penzi akisikika kumfurahia Koku, ikamrudia Jelini akilini na kufanikiwa kumtoa machozi aliyojionya asilie tena. Akijiambia hana sababu ya kulilia kisichowahi kuwa chake. Ni Koku! Alishamsikia alikuwepo kwenye maisha yake, ila  “Amenidanganya kwa kipindi chote hicho! Ameshindwa kabisa kumuacha mpenzi wake!” Alishazoea kutesa wanaume wanao mpapatikia, sio kuteswa. Jelini akazidi kuumia. “Ananidanganya kumbe anamaisha yanayoendelea bila mimi kujua! Nimekua mjinga kiasi gani jamani! Haya yameendelea kwa muda gani?” Jelini akakumbuka siku ambazo hakuwa akilala nyumbani kwa Kasa, bila Kasa kumuita, akajithibitishia ndio muda Kasa alikuwa akiendelea na yake, kwenye kitanda hichohicho alichokuwa akipiga sarakasi zote za mapenzi akidhani anamkoleza. Jelini akazidi kulia kwa fedheha akidhani alikuwa kila kitu kwa Kasa. Sauti ile ile aliyokuwa akihitimisha kwake, ndiyo aliyoisikia akihitimisha kwa Koku. Hapakuwa na mlio wa tofauti kwamba yeye alikuwa akifanya cha ajabu saaaana. Mwisho ni uleule.

Kumbe Kasa alishaacha wote kwa ajili yake, siku hiyo ilikuwa siku ya kufa nyani. Zenda akatelezea pabaya, akaangukia pua. Wenye uchu na pesa zake walimfanyia mipango, na shetani hakuwa na usingizi, hajachoka, na hana kwingine pakwenda, alikuwa upande huohuo, akawafanikishia kiurahisi. Akiwa anaaga zilipendwa wake, na Jelini akatokea bila kutarajia, na kuachwa na kumbukumbu mbaya sana moyoni.

Jelini akazidi kulia kwa uchungu na hofu ya kuambukizwa maradhi. Mzee si mla pipi kwenye ganda. Anapiga kavukavu. Hofu ikazidi. “Ataniua, nimuache mwanangu!” Ukawa ni ukweli wake anaotaka kuupitisha mayoni, lakini mchungu mpaka machozi yakawa yakimmwagika peke yake hapo kitandani. Giza la nje lilishaingia ndani. Akageukia mwanga wa taa iliyokuwa imewashwa nje, mwanga wake umefanikiwa kupenya ndani. Akalia mpaka ikabidi atulie maana maumivu ya kichwa nayo hayakukawia kumkumbusha kilema alichokipata alipokuwa kwenye maisha ya huyo mzee.

Akatulia kabisa mpaka akili zikamkumbusha faraja anayopata kutoka kwa Colins. “Mhh! Hiki ninachojisikia kwa Colins nacho ni nini tena!?” Akawaza na kujishangaa. Anaposhikwa na Colins, anapatwa hisia za ajabu, hajawahi kujisikia hivyo kabla. “Mwili mzima unakuwa kama umepigwa shoti ya umeme!” Akawaza na kusikia mlango ukifunguliwa taratibu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ni nini Kitaendelea? Usipitwe.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment