Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 31. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 31.

 Jelini alilala mpaka asubuhi anaamka, hajui alipo. Akabaki amejilaza hapo kitandani. Kumbukumbu za jana yake zikamrudia. Akakumbuka shauku aliyokuwa nayo akamfurahishe Zenda na kuishia kushuhudia akipigishwa bao na mwanamke aliyemuapia alimuacha. Machozi yakaanza kumtoka tena taratibu akiwa hapo kitandani asipopajua. Akashitukia mlango unafunguliwa.

“Unajisikiaje Jelini?” Akabaki akimtizama huyo mrembo. Mzuri sana wa sura. Midomo ya rangi kama Colins, akahisi ni dada yake. “Usiogope, hapa ni nyumbani kwa…” Akajaribu kufikiria amueleze vipi. “Si unamfahamu Colins anafanya kazi na shemeji yako?” Jelini akatingisha kichwa kukubali, na kujaribu kufuta yale machozi kwa haraka ili asijue kama alikuwa akilia. “Basi hapa ni kwao na mimi ni mdogo wake, naitwa Connie. Unajisikiaje kichwa?” Hakujibu ila kuendelea kujifuta machozi yaliyokataa kukauka maana kumbukumbu ziliendelea kumletea sauti ya kulalama kwa Koku akishugulikiwa ipasavyo na Zenda, kisha kana kwamba anakomolewa, ikarudia sauti ya Zenda mwenyewe akiwa anapiga bao.

“Tafadhali usilie, unajiumiza.” Akatingisha kichwa kukubali akijitahidi kufuta machozi yaliyokuwa yakiendelea kutoka. Akashangaa huyo Connie anakaa pembeni yake, anamkumbatia huku akimbembeleza kama mtoto, kisha kuanza kumfuta machozi kwa upendo. Akamwangalia. “Nakutolea taulo ili ukaoge halafu ule. Utajisikia vizuri. Sawa?” Akakubali kwa kichwa huku na mshangao wa kukumbatiwa na kubembelezwa kitoto.

Hapohapo chumbani kulikuwa na choo, akaingia kuoga. Haikuwa nyumba ya ajabu ila pasafi halafu patulivu sana. Huyo Connie mwenyewe jinsi anavyoongea ni kama ananong’ona kama mama yake. Mzuri wa kuvutia haswa.

Wakati yupo bafuni, Connie akamtumia ujumbe Colins na kumwambia kama Jelini ameamka ila analia. ‘Nijulishe akitoka kuoga.’ ‘Poa.’ Akamjibu kaka yake na kwenda kwa mama yao pia kama kumpisha avae. Jelini akapata faragha ya kulia kwa uhuru huko bafuni. Kilio kikaanza tena huku akiogaa mpaka akatoka. Akakuta gauni kama tenite hapo kitandani. Connie alikuwa mwembamba haswa, Jelini alikuwa na mwili japo alishaanza kutoa unene wa pombe alizokuwa akinywa na kwenda kulala. Ila alikuwa na mwili mkubwa kuliko Connie halafu mfupi kwake. Ukweli huyo Connie alikuwa mzuri sana. Urefu wakuvutia kama ambaye umshauri agombee taji la warembo wa dunia.

Akamaliza kuvaa akarudi kujiegemeza kitandani akijitahidi kutulia hapo ugenini. Mlango ukafunguliwa, akaingia Connie na mama yake. “Usilie Jelini mwanangu. Unazidi kujiumiza.” Akazungumza huyo mama kwa upendo, akakaa hapo kitandani pembeni yake. “Halafu hujapaka mwili lotion. Nipe lotion.” Akashangaa huyo mama anaanza kumpaka hiyo lotion miguuni. “Makubwa tena haya!” Akajisemea Jelini nafsini mwake ikishangaa hiyo familia inavyopenda kushikashika na kubembeleza, ndipo akamuelewa vizuri Colins.

Mara na Colins naye akagonga na kuingia. “Vipi Jelini?” Walikuwa kama mapacha watatu hapo ndani. Mama huyo ndio karithisha wanae  hiyo midomo. Wamemfanana na wamepoa wote kama maji ya mtungini. Jelini akajiinamia tu. Akamvuta mkono taratibu huyo mama akaendelea kumpaka lotion.

“Mama CJ?” Sauti ya kibaba ikasikika ikiita. “Nipo huku.” Akaitika huyo mama. “Sasa unaniachaje hivihivi bwana? Umeniambia unarudi, hurudi!” “Nipo chumbani kwa Connie, nipo na mgeni. Njoo nikuone kabla hujaondoka.” Jelini akasikia mlango anafunguliwa. Akaingia mtu, ila akashindwa kumuangalia.

“Umependeza dad!” Connie akaenda kumkumbatia, na busu baba yake. “Asante sweetheart. Vipi, si nitakukuta?” “Narudi chuo usiku, kwa hiyo utanikuta.” “Sasa huyo badala ya kuendelea kukaa hapa chumbani, hamieni na mgeni mezani ale.” “Sawa. Ndio unataka kuondoka?” “Njoo uniage bwana! Hata hujaniombea!” “Wewe umeingiwa hofu baba CJ, unataka kila saa nikuombee jambo hilohilo! Utafanikiwa tu, na Mungu yupo na wewe.” Akaonge huyo mama akisimama kutoka hapo kitandani alipokuwa amekaa akimpaka lotion Jelini.

“Mimi nina imani na wewe dad. Utafanikisha tu huo upasuaji na huyo mama atatoka salama.” “Nashukuru Colins.” Akasikia busu jingine. “Asante dad. Uniambie jinsi itakavyokwenda.” Connie akamuachia baba yake maana alikuwa amemkumbatia. “Nitafanya hivyo.” Wakatoka baba na mama yao. Jelini mpaka machozi yakakauka kwa hiyo familia jinsi ilivyo. Ina amani, huwezi leta matatizo yako. Ila akajua huyo baba ni daktari mpasuaji.

Pumu Imepata Mkohozi.

Taratibu Jelini akajilaza na kugeukia ukutani. Colins akamfanyia ishara dada yake, akatoka. Akaenda kuchukua taulo dogo, akaweka maji ya baridi akarudi nalo na kukaa pembeni yake ila upande wa juu. “Lala chali.” Jelini akalia tena kidogo, akasikia akimsaidia kugeuka. Na yeye akaanza kumfuta machozi kisha akamuwekea kile kitaulo kichwani.

“Nisikilize Jelini. Japokuwa sijui nini kimekuumiza, lakini hapo ulipo, mimi nimepita. Unasikia maumivu ya kutoka ndani ya moyo kabisa. Hujui imekuaje! Hujui ni kwa nini! Unatafuta kosa lako, halafu unajihisi umefanya kwa upande wako, hakuna ulichokosea, lakini imetokea kilichotokea. Moyo hauamini kama kweli imetokea, ila kumbukumbu zinakuhakikishia ni kweli imetokea. Uchungu unazidi, unatamani isiwe imekutokea wewe. Si kweli?” Jelini akashangaa sana amejuaje anachopitia ila hakujibu.

“Basi na mimi nilipita hapo. Lakini nataka kukuhakikishia, it gets better. Ruhusu moyo upokee matokeo. Ukifanya hivyo kwa haraka, hutajichelewesha. Utajikuta unavuka hapo kwenye denial/kukataa kilichotokea, kwa haraka. Na utafikia pia kwa haraka swali la ‘nini chakufanya’. Kisha kuishi na maamuzi yako bila kuyumba. Ukichelewa kwenye kukubaliana na kilichotokea, ukabaki hapo kwenye denial kwa muda mrefu, jua niliyokwambia mwanzo yatakutesa sana, tena kwa muda mrefu. Mpaka kuja kukubali, utakuja kujikuta chaguzi ambazo ungefanya au nafasi ambazo ulikuwa nazo mwanzoni kufikiria chakufanya, umezipunguza au zimeisha sababu umechukua muda mrefu sana kwenye denial. Kukataa matokea.” Colins akaendelea kuzungumza naye taratibu akimbembeleza.

“Natamani na mimi ningekuwa si mmoja wa watu waliokwisha kukuumiza, pengine ungeamini hayo. Lakini Jelini, uaminifu wangu kwenye mahusiano ndio umeniponza na kukuumiza wewe usiye na hatia. Na pia sikutaka kukuingiza kwenye matatizo. Yule msichana niliyekuwa naye kwenye mahusiano, alikuwa mkali sana, na hasira zikimpanda, hanaga mipaka na hawezi kujizuia. Ni bora vile nilivyokuita mimi tukazungumza pembeni, yeye asingeweza. Angekuzungumzisha vibaya, tena hadharani, mbele ya watu. Najua ingekuwa vibaya zaidi. Ndio maana niliona nikuwahi mimi kabla hajakuona ukinisogelea. Alikuwa hawezi kuona yeyote karibu yangu. Hata Connie hakuwa akimtaka awasiliane na mimi, nikiwa naye.” Jelini akashangaa sana. Japokuwa alikuwa amefunga macho lakini alikuwa anasikia kila kitu.

“Inamaana yule mchumba naye amemuacha mwanaume aliyekuwa mwaminifu kwake kwa kiasi kile! Kwa nini mapenzi yanakuwa hivi jamani? Hawa binadamu wanataka nini wafanyiwe ili watulie na kuwa waaminifu?” Jelini akawaza, akamuona machozi yanamtoka. Alikumbuka jinsi alivyojitoa kwa Zenda na kuwa mwaminifu kwake akimfanyia kila kitu, leo anamsaliti!

“Mara ngapi amekuwa akifanya hivyo bila mimi kujua?” Akalia sana akijiona mjinga, akidhani amempa penzi lote hawezi kutamani la wengine, kumbe hakuna kitu! Akalia sana kwa kunung’unika akijidharau zaidi kila maneno ya Koku yalivyo endelea na yenyewe kujirudia akilini mwake. Colins akaendelea kumfuta machozi taratibu asijue ni mengi yanaendelea kwenye kichwa cha mwanadada huyo.

“Usilie Jelini. Usizidi kujiadhibu. Hakuna gumu ambalo halina mlango wa kutokea, labda ukatae tu mwenyewe kutoka. Hata kama sasahivi uchungu unakuonyesha umefika mwisho, kataa. Upo mwanga mbeleni. Usiogope ukijiuliza itakuje. Kwa kuwa huna jibu ya itakuaje mpaka uanze kutembea leo. Kila siku itajijibu yenyewe. Umenielewa?” Jelini akatingisha kichwa kukubali. “Basi naomba nyamaza kabisa kulia ili kichwa na chenyewe kitulie. Unaendelea kujiadhibu wewe mwenyewe. Usikubali kujiadhibu. Watu wengine huna uwezo wa kuwafanya wasikuumize, ila wewe unalo jukumu kwako. Usikubali kujitesa.” Akamfuta machozi vizuri.

“Nikuletee kitu kidogo ule?” Akatigisha kichwa kukataa. “Unataka kupumzika?” Akaendelea kumuuliza kwa upendo huku akimpapasa taratibu kwa kutumia vidole vyake akipitisha juu ya mkono wake mpaka chini kama anayemkuna ila kwa vidole. Na hiyo sauti ya Colins, halafu ya kubembeleza, Jelini alijisikia faraja ya kipekee. Halafu ni Colins sasa! Akaanza kusikia kupoa.

“Niambie nini unataka Jelini?” Hapo anamuuliza na kumfuta machozi kwa mkono mwingine na kurekebisha taulo alilomuwekea kichwani. Jelini akafungua macho na kumwangalia maana muda wote hakuwa akimtizama. Macho yakagongana. Colins alikuwa mzuri sana wa sura. Kitu kikatembea moyoni kwa Jelini na kushindwa kuelewa katikati ya uchungu alio nao moyoni, hiyo ni hisia gani!

Akafunga macho. Akahisi anamvuta mkono na kuubusu. Akashangaa nafsini kwake, nakutoelewa. Ila akakumbuka hata dada yake na mama yake wapo hivyohivyo, watu wakushikashika na kubusu. Hakufungua macho tena. Akamsikia akisimama. Akatamani amwambie asiondoke, ila akamuacha tu. Akatoa lile taulo. Akaenda kulisuuza tena, na kurudi. Safari hii alikaa, akamfuta machoni, usoni taratibu kisha akarudi tena kuliosha na kurudi.

“Nikiliweka kichwani lina msaada wowote?” Akamuuliza kwa upendo, Jelini akatingisha kichwa kukubali. “Afadhali.” Akalirudishia kichwani, akarudi kukaa pembeni yake. Akamshika mkono vizuri, kwa upendo. Akaubusu tena, akabaki ameushikilia na mwingine akimpapasa, hapohapo Jelini akapotelea usingizini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alikuja kuamshwa na Jema. “Vipi kichwa?” “Mama yuko wapi?” Ndio likawa swali lake la kwanza bila kumjibu dada yake. “Unakumbuka leo ndio ilikuwa ampeleke bibi KCMC kwa vipimo?” Akaanza kulia tena. “Mama anakuja kesho, Jelini. Ametutuma mimi na James. Ndio maana tumewahi kuja. Usilie. Twende ukapumzike nyumbani.” “Sasa kwa nini nyinyi ndio hamkumpeleka bibi hospitali, yeye akaja?” “Wewe unamjua bibi, Jelini. Hakuna anayemuwezea isipokuwa mama. Swala la hospitali kila mtu ameshindwa isipokuwa mama. Ndio maana kila mtu amemuachia yeye. Mimi na James tusingemuweza bibi, na safari hii pia asingekwenda hospitalini. Mama anakuja kesho, usilie. Twende.”

“Vipi kichwa Jelini?” Akasikia sauti ya James. Ndio akajua hapo chumbani hawapo wao wawili. Akapandisha mabega juu kukataa. “Kinauma?” James akajisogeza, akazidi kulia. “Mimi nashauri umpe simu azungumze na mama kama alivyosema mama mwenyewe.” James akamwambia Jema. Jema akamtumia ujumbe mama yake kwanza, kisha akaona mama yake anapiga hapohapo.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mama anataka kuzungumza na wewe.” Jema akamkabidhi simu. Jelini akazidi kulia. “Kichwa kinauma sana?” Mama yake akamuuliza, akimjua Jelini. “Kila kitu kinauma mama. Mbona huji sasa?” Wakamsikia akimjibu mama yao. “Nakuja kesho Jelini, mama angu. Bila hivyo bibi asingetibiwa. Naomba nenda kwa kina Jema. Mimi nakuja kukuchukua kesho. Kunywa dawa ya maumivu na usingizi, ulale mpaka nitakapokuja mwenyewe. Umesikia?” Akamrudishia simu Jema, akilia. “Ni mimi mama.” Jema akamuwahi maana bado alikuwa akimbembeleza Jelini.

“Naomba mumpe dawa ya maumivu na usingizi. Huyo hawezi kunyamaza mpaka nije mimi mwenyewe na kichwa hicho bado. Kesho mapema sana nitakuwa huko.” “Mimi nashauri utulie mama. Jelini atakuwa sawa. Tukifika nyumbani, atapata utulivu. Atakuwa sawa.” “Sawa. Lakini mwambie kila kitu kikienda sawa, kesho nitakuwa huko.” “Sawa.” Wakakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Mama anakuja kesho Jelini. Naomba utulie. Twende.” Akatoka hapo kitandani akilia. “Acha mimi nimsaidie.” Colins anatoa wazo na kusogea, ikabidi Jema ampishe maana alikuwa amesimama hapo mbele ya kitanda alicholala huyo bidada na tumbo lake. Akaanza kumfuta machozi kama mtoto. Jema akamwangalia mumewe. James akamuona ila akanyamaza tu. “Twende Jelini. Kila kitu kitakuwa sawa. Usilie.” Akaongea naye kwa kumbembeleza. Wakawa bado hawajaelewa.

“Mnisubirie nikachukue kibegi changu.” James akahisi labda mkoba wake anaowekea laptop zake. Maana wao watu wa electronics, basi kuzurula na aina hiyo ya mikoba ni jambo la kawaida sana. Lakini sasa anakwenda nao wapi na inawahusu nini wao wanaotaka kuondoka na mtu wao!

“Sitakawia.” Colins akaweka msisitizo. “Kwamba tunaondoka wote!?” James akamuuliza kwa mshangao kidogo. “Ndiyo.” Colins akajibu na kutaka kutoka. Akawa kama amekumbuka kitu akiwa ameshafungua mlango. “Hivi si una mataulo yakutosha nyumbani kwako? Maana mimi huwa sipendi kurudia taulo.” Hayo anamuuliza Jema. “Subiri kwanza Colins! Kwani unataka kwenda kulala kabisa!?” “Kwani wewe si uliniambia mnavyumba vyakutosha tu pale? Au ulipata wageni!?” Yaani na yeye akawa kama anamshangaa James! Na hayo anaongea mlango upo wazi, nusu ya kiwiliwili kipo nje. Na anaongea kwa sauti tu.

 “Vyumba vipo.” “Basi mnisubiri kwenye gari, sitakawia. Sitaki Jelini aendelee kulia hivi. Daktari amesema kichwa kitazidi kumuua.” “Naomba tuzungumze kwanza Colins.” James akatoka naye nje ya mlango.

“Vipi!?” Colins akamuuliza akimshangaa James kama anayemchelewesha. Jema na Jelini ndani wanasikiliza. “Wewe si uliniambia mzee Kasa alikufuata kukukataza usiwe karibu na Jelini, lasivyo atakupiga risasi?” Jelini akashituka sana kusikia hivyo. “Mimi mwenyewe nina mpango wa kumfuata na risasi. Maana ni kwa nini Jelini alie hivi? Inamaana yeye anahusika na hicho kilio cha Jelini.” James akashituka na kushangaa sana. “Colins!?” “Subiri kwanza James! Mbona kama hutaki kufikiria? Wewe na Jema hamkuwepo hapa mjini. Na mama yao hayupo. Wakumuumiza Jelini kiasi hiki ni nani kama siye yeye aliyebaki hapa mjini?” Colins akauliza kwa ukali kabisa.

“Colins, mimi nashauri utulie, usubiri kwanza.” “Nilifanya hivyo kwa kuwa alinihakikishia atamuenzi Jelini, ndipo na mimi nikamwambia nitakaa naye mbali kama na yeye atasimamia ahadi yake. Sasa siwezi mimi nikawa mwaminifu kwenye makubaliano yetu, wakati yeye ameshindwa! Hata kidogo.” Colins akaendelea akisikika na hasira.

“Kama hawezi kumfanya Jelini kuwa na furaha, akae pembeni. Asitake kunichanganya na kunibabaisha! Na hakuna anayemuogopa ila heshima tu. Akivunja heshima, hataheshimiwa.” Jelini akashangaa mpaka akatoa macho na kumwangalia Jema. “Mimi nakushauri utulie kwanza Colins.” “Hivi wewe James, upo upande gani lakini!?” “Unajua nipo upande wako Colins!” James akamjibu akisikika amechoka kabisa, na mshangao juu,

“Basi nionyeshe kwa vitendo kama kweli upo upande wangu, mimi kama mtu wako. Tena wakaribu SANA.” “Ndio nakushauri Colins! Nashauri usubiri kwanza tujue kwa hakika ni nini kinaendelea, ndipo ujue jinsi ya kuchukua hatua ukiwa umejipanga.” “Kwa hiyo unaona mimi kumtuliza Jelini sasahivi, asiendelee kuumia ninafanya haraka? Kwamba nimuache tu aumizwe huko, halafu mimi eti nisubirie tu! Nasubiria nini na yeye ameumia leo? Halafu kama hatataka kusema kilichotokea huko? Ninyamaze tu, nasubiria?” Colins anaongea na James kana kwamba anahusika na huyo Jelini zaidi yake yeye James. Kwamba jambo limemfika yeye zaidi kuliko mwingine yeyote yule. Kama nani! Hakuna ajuae. Halafu kalivalia njuga na kulibebea bango mpaka James akaishiwa hoja.

“Nisubiri.” “Sasa unahamia kwangu kwa ajili ya nini Colins!?” “Si ndipo atakapokuwepo Jelini!? Au mnampeleka wapi? Maana alikuwa ametulia hapa. Mama na Connie wanampa huduma nzuri za kidaktari, analala vizuri. Wewe umekuja kumchukua!” Ikawa tena lawama. James akachoka kabisa. “Hivi huyu Colins anakumbuka kama mimi ni shemeji yake Jelini, na ndiye niliyempigia simu kumuomba msaada kwa ajili ya huyu Jelini, tena kwa muda tu?” James akawaza akimtizama alivyoshupalia jambo.

“Hapa alikuwa ametulia kabisa! Tena mmemkuta amelala, mmemuamsha!” James akachoka kabisa. “Mama yake ametutuma tuje tumchukue, Colins. Leo atakuwa kwangu mpaka kesho atakapokuja kumchukua yeye mwenyewe.” “Mimi najua jinsi ya kumtuliza. Nataka atulie. Au wewe unaona sawa aendelee kulia huku unajua fika ametoka kushonwa kichwa?” Akauliza kwa ukali. “Hapana Colins! Unajua wote tupo upande mmoja.” “Aisee huonyeshi kabisa kama upo upande wangu James!” Mpaka Jema akashangazwa huko ndani.

“Sawa Colins. Acha mimi nikuache na maamuzi yako. Maana nakujua wewe unapoamua jambo lako.” “Basi nisubiri nakuja. Tuondoke wote.” “Si uje na gari yako Colins?” “Kwamba mimi ndio niondoke hapa na Jelini na gari yangu, tuwafuate hata baadaye?” Na yeye akamfanyia James makusudi. Akijua James hawezi kukubali. “Naona wazo lako la kukusubiria sio baya.” James mwenyewe akasalimu amri. “Basi nitatuma dereva aniletee gari yangu usiku au kesho asubuhi. Sitachelewa.” Colins akaondoka na kumuacha James hoi.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Ukishika, Shikamana.

Itakuaje?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment