Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 30. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 30.

Zenda akagundua sauti inatoka hapo nje ya mlango. Aliruka kitandani nusura aanguke, Koku akimtizama. Anatokaje bila nguo! Akaanza kusaka sasa japo pensi tu huku amepaniki kuliko maelezo. Anakimbia humo chumbani mpaka akafanikiwa chakujisitiri chini. Akafungua sasa mlango akitetemeka mpaka Koku akashangaa kumuona KASA anatetemeshwa na mwanadamu! Ikabidi akae vizuri na kuvuta shuka kujisitiri maana alikuwa na yeye kama alivyozaliwa, macho yakimsindikiza Kasa vile anavyo haha.  

Kufungua mlango na kutoka, lahaula, Jelini! Amekaa chini kabisa, uchi zaidi ya mnyama aliyesitirika na manyoya. Amefukia uso katikati ya mapaja. Analia kwa kwikwi akijitahidi sauti isitoke, mikono ameziba masikio kama aliyekuwa hataki kusikia. “Mungu wangu!” Akasikika Zenda. “Mungu wangu Jelini!” Akasikika tena Zenda kwa mshituko wa ajabu. Mikono kichwani Koku akimtizama pale mlangoni akichungulia nje kama anayeogopa kutoka kabisa.

Kile kitu kikamkera Koku na kumpandisha hasira ya ajabu. “Acha utoto Kasa. Unachanganyikiwa nini hapo kama mtoto mdogo!? Nani alimwambia aje kwenye majumba ya watu asubuhi asubuhi bila taarifa? Yeye hajui kama una maisha yako? Au yeye ndio alidhani ni Livingstone kwamba ndio amekugundua hapa duniani!?” “Nyamaza Koku.” “Unapaniki nini wewe?! Ndio madhara yakutembea na vitoto vidogo visivyo na akili. Havina mipaka! Ona sasa unafuatwa mpaka chumbani! Si wazimu huo?” Kasa akatoka, Koku naye akatoka pale kitandani kajifunga shuka tu, ndani mtupu.

Akatoka mlangoni, akamkuta Jelini kwenye ile hali. Kunyanyuka aondoke hawezi, mwili umekufa ganzi kabisa. “Acha ujinga wewe mtoto, hebu nyanyuka hapo nenda kwenu. Wewe ulifikiri Kasa atakuoa?” Koku akamuuliza kwa kumdharau. “Umenikuta na Kasa, tumetulia kimya. Umeingia hapo siku mbili tatu, tayari unajiona mmiliki halali! Si ujinga…” Jelini akasikia kibao cha nguvu. “Unanipiga Kasa wewe sababu ya malaya huyu?” “Ondoka Koku.” Kikasikika kibao kingine cha nguvu, Jelini akazidi kujificha uso asiwatizame.

Kumbe Koku alimrudishia Kasa kibao. Na yeye akampiga Kasa. “Usiwahi kunipiga maishani mwako kote Kasa. Uliniita hapa wewe mwenyewe ukiniomba, tena ukaniambia hujaridhika kwa muda mrefu, unahamu na mimi. Iweje leo uanze kunipiga? Tena usirudie tena.” Koku akamfyoza kabisa.

“Kinakuchanganya kitoto hiki, unakua kama mwehu, kwa kipi mno? Malaya tu huyu wa hapo Tegeta! Analala na kila mwanaume hata Kevi alimkataa!” Hasira na wivu zikamfanya Koku atoe siri ambayo alionywa asije akaropoka kwa baba yao hata neno moja juu ya Jelini. Lakini Koku akaonyesha anataarifa zake zakutosha.

Akaendelea kubwatuka. “Anajiliza nini hapo kama si uongo tu? Ingekua amekufumania hapo sawa. Amekukuta nyumbani kwako, ukiendeleza starehe, kama kawaida yetu! Anachojiliza nini sasa? Acheni kunichanganya.” Koku akarudi chumbani na kuwaacha hapo akiwa ameharibu haswa. Ameridhika kuwakosanisha haswa. Jelini amepata habari yake kamili. Kasa alikuwa ameishiwa nguvu, hajui afanye nini. Akaenda kukaa kwenye kochi la hapohapo, akainama, Jelini akiendelea kulia kwa uchungu kama kafiwa na mama Jema.

Kimya, Zenda hajui aseme nini, Koku yeye akioga ndani bila hata wasiwasi. Kazi aliyopewa kaimaliza, tena kaikamilisha vizuri haswa mpaka mwenyewe akashangaa. Mwishoe Jelini akajikaza, akajikusanya, akanyanyuka pale, uchi vilevile akarudi sebule kubwa alikokuwa ameacha nguo zake. Akaanza kuvaa akilia sana. Kamasi na machozi vikimtoka kama mvua. Zenda akamsogelea ili amshike. Jamani Jelini aliruka, kama anaye epuka moto, au amepigwa na shoti ya umeme, nusura aanguke mpaka akamtisha Zenda. Akachukua pochi yake, sidiria alishindwa kuvaa, akaiweka kwenye pochi, nakutoka. “Nisubiri nikusogeze Jelini. Usi…” Mlango ukafunguliwa, nakufungwa, Jelini akatoka.

Zenda akamkimbilia kwa haraka akiwa na pensi nyepesi sana, kifua wazi, bado analia, anatembea hapo kwenye ua wake mrefu akielekea getini atoke. “Jelini! Jelini! Akakimbia mpaka mbele yake. Naomba usiondoke. Tafadhali mpenzi wangu.” Jelini akamzunguka na kuendelea kutafuta geti. Jumba la Zenda kubwa sana. Zenda akakimbilia ndani kuvaa na kuchukua funguo ili amfuate na gari, akamkuta Koku anavaa taratibu hana haraka. Hakumsemesha.

Akaanza kuokota nguo za jana hapo sakafuni, alizokwenda nazo kanisani nakuanza kuvaa kwa haraka ili kumuwahi Jelini. “Unapaniki nini wewe Zenda?! Mbona hueleweki? Jana unalilia penzi langu, leo unapaniki na katoto hako ambako hakana mbele wala nyuma? Wewe muache, atarudi mwenyewe sababu ya pesa. Maisha magumu hivi, unafikiria kwa mjinga kama yule, atakula nini?” “Katika wote, yeye ni mtu wa kwanza maishani ambaye anajua ninazo pesa, na hajawahi kuniomba hata shilingi, ila upendo wa kweli. Kwa hiyo kujibu swali lako la kwa nini na paniki, basi hicho ndicho kinanipanikisha.”

“Jelini ni watofauti na nyinyi wote. Nyinyi mmesoma na mnalipwa mishahara yenu, ila mpo na mimi sababu ya pesa zangu, lakini Jelini amenifuata leo kwa sababu jana kwa akili zangu nilimlalamikia nipo mpweke, nimemmisi, nina hamu naye.” “Basi ndiyo hayohayo uliyoniambia na mimi.” “Mimi najijua Koku. Na sijui jana nilinyweshwa nini, lakini WEWE, siwezi kukulinganisha na Jelini hata nikiwa usingizini.” Hapo akamuudhi Koku mpaka mwisho.

“Wewe ni mshenzi Kasa.” “Sikutusi, lakini kilichoniamsha asubuhi hii nikiwa kwenye usingizi mzito nikidhani ni Jelini ndiye anayecheza na mwili wangu, lakini haikuchukua hata dakika moja nikashituka nikijua wewe si Jelini. Mwili wangu ukiwa mikononi kwa yule mtoto, ni hisia ambazo nina uhakika kwa asilimia 100 wewe hujawahi kuzisikia. Na kwa jinsi ninavyokujua, nina uhakika utakufa kabla yakupata hizo hisia. Kwa hiyo usiwahi kujifananisha na Jelini, Koku. Haupo hata robo yake. Siku njema.” Kasa akatoka kisha akarudi.

Utatamani lile kofi nililokupiga, usingenirudishia, itoshe vile. Lakini ulinirudishia, tena mbele ya Jelini!” “Utanifanya nini? Nakuuliza Kasa, utanifanya nini?” Koku akauliza kwa hasira kali sana. Kasa akamwangalia kwa sekunde kadhaa, akacheka kwa kumsikitikia, kisha akatoka akiwa amemuumiza sana Koku. Yaani yeye hayupo hata nusu ya Jelini aliyemdharau kwa kiasi kile! Akaumia sana akabaki akimfyonza Kasa na kumtusi kwa sauti. Alimsikia, lakini akatoka kumuwahi Jelini.

Ukweli Mchungu.

Zenda akakumbuka shuka, kweli kumekuchwa. Akatoka kwa kasi kumkimbilia Jelini, hakumkuta kwenye uwa wake. Walinzi wakamwambia alishatoka. Akarudi kuchukua gari ili kumfuata akijua atampata tu kama siku ya kwanza kukutana kwao Jelini alipoamkia asipopajua, baada ya harusi ya Jema. Kasa aliendesha kama mwehu asimpate Jelini. Jelini aliyelelewa jijini bila usafiri wa nyumbani, huna utakapomuacha asifike anakokutaka. Alishapata usafiri na kuomba apelekwe hotelini maana nyumba walifunga, wakiwa wanaenda kwa bibi. Alirudi bila funguo akijua atakuwa kwa Zenda mpaka mama yake na Jeremy warudi jijini. Hakuchukua funguo za nyumba. Uzuri alikuwa na pesa, akachukua chumba kwenye hiyo hoteli, akaingia hapo nakuzidi kulia.

Kila akikumbuka sauti ya mapenzi aliyokuwa akiisikia kati ya Zenda na Koku alizidi kulia akigandamiza mto masikioni kama asisikie tena. Mbaya zaidi dhihaka za Koku ziliingia mpaka moyoni, akili ikawa na kazi ya kujichotea tu huko moyoni nakurudisha kwenye kumbukumbu. Akakumbuka mazungumzo ya jana yake kati yake, mama yake mdogo na mama yake. Akaumia kugundua mama yake alikuwa sahihi, wakati akimtetea Zenda. Jelini akazidi kuumia, akishindwa kunyamaza kabisa.

Kuliko Ungua Mpini.

Huku nyuma baada ya kukata tamaa hampati Jelini, akarudi kwake. Hakumkuta Koku. Akakaa akiwaza. Akili ya mzee ipo kichwani. “Hata kama nilikuwa nimelewa kwa kiasi gani, maneno aliyosema Koku nilimwambia, si kweli.” Akapinga kabisa mawazoni. “Halafu sikuwa nimekunywa kiasi chakunifanya nilewe hivyo!” Zenda akaendelea kuwaza. “Na Koku anaonekana anafahamu habari zangu na Jelini mpaka Kevin!” Taa kichwani zikawaka. Zenda alijaliwa akili ya kufikiria sana, na wanae walimjua ndio maana walimuomba Koku asije ropoka jina la Jelini mbele yake. Hasira na wivu kuona Jelini amethaminiwa kuliko yeye, vikaushinda ubinadamu. Akamwaga mchele kwenye kuku wengi.

Zenda akasimama kama mshale. “Walinilevya!” Akashituka sana baada ya akili kukubaliana na hilo. “Sasa ole wao nikakute madawa mwilini mwangu.” Akatoka kwa haraka kama simba aliyejeruhiwa kwenda hospitalini kupimwa damu. Hakuwa ameoga wala kusafisha uso. Alikuwa amepaniki kama mwehu. Damu kutolewa na kupimwa, wakakuta madawa kwenye damu yake. “Wamemwaga mchele, acha niwamwagie mboga. Wamemtoa Jelini kwangu, nawatoa na wao kwangu.” Akatoka hapo mpaka polisi.

Mzee akatoa mashitaka kuwa jana alikuwa nyumbani kwa familia ya Rweza akiwa amekaribishwa chakula, walimpa madawa. Anahofia maisha yake. Kwamba wanataka kumuua. Hapo mzee anafungua kesi na wakili wake alishafika hapo, ila akashangazwa sana na hao watu anaowashitaki. Wanae wote wawili, mume, na Koku! Akawashitaki wote akisema ndio aliokuwa nao, sasa hajui ni nani alitaka kumdhuru kwa hakika. Kesi ikatengenezwa, ikawa ni shitaka la kukusudia KUUA. Akatoa vipimo vya hospitalini, wakajiridhisha.

Mwisho Wa Ubaya, Ni Ubaya.

Usicheze na aliyekutangulia, halafu mwenye hela aliyetafuta kwa kutumia kichwa chake! Mwisho wake si mzuri. Koku akiwa nyumbani kwake, akagongewa na polisi, akaambiwa yupo chini ya ulinzi kwa kusudio lakutaka kuua. Alishituka Koku, akapigwa pingu akatolewa hapo kwenye jumba lake kama mtuhumiwa kwelikweli na Kasa alitaka washugulikiwe kama majambazi haswa. Pesa anayo, ashatanguliza kwa watakao kwenda kukamata wabaya wake, na kweli msomi na tajiri Koku akiwa na harufu nzuri mwilini, akatupwa nyuma ya gari, akakimbizwa rumande asiamini.

Kemi naye akiwa ameshapongezana na mama yake pamoja na ndugu yake kuwa wamefanikiwa kumrudisha Koku kwenye maisha ya baba yao, wasijue Koku alivunja sharti kubwa walilomsisitizia hata kama awe amelewa vipi, asije onyesha anamfahamu Jelini mbele ya baba yao, maana mzee ataunganisha matukio, wote watakuwa matatizoni. Na kweli alishindwa kirahisi sana. Hasira ikawa hasara yao wote.

Akiwa na wanae wametulia tu nyumbani, mume ametoka kwenda mtaani kwa marafiki zake wa jijini, Kemi naye akaambiwa ana wageni. Akatoka kwenda kuwasikiliza maana hakutaka mtu asiyemfahamu ndani kwake. Hapohapo akasomewa shitaka lake, akaulizwa alipo mumewe, akasema hajui, basi yeye akapigwa pingu, polisi. Hivyohivyo kwa Kevin.

Noah akiwa baa akifurahi na marafiki zake kitajiri, wakinywa mapombe ya garama, akapata simu kutoka kwa vijana wake, wamepaniki kwelikweli. Wakamsimulia. Pombe yote ikamuisha, akakimbilia polisi ndipo na yeye akakamatwa. Wote wakawekwa ndani. Mbaya ni msimu wa sikukuu, shitaka ni la kukusudia kutaka kuua. Hakuna DHAMANA. Hapo ndipo Zenda akaridhika na kurudi nyumbani sasa.

Bahati Ya Mtende.

Takataka Kwako, Hazina Kwa Mwengine.

Inafika jioni Jelini kichwa kinamuuma hawezi hata kusogea. Ikabidi awashe simu ampigie mama yake. “Nakufa mama.” Mama Jema alishituka kumsikia mwanae analia. Mama wa kichaga anapenda hao binti zake, kuliko roho yake. Akaanza kutetemeka. “Upo wapi?” “Kichwa kinauma, nahisi ule mshono unapasuka, mama. Nipo peke yangu hotelini. Nitakufa mama, niache mwanangu.” Hapohapo akampigia simu Jema. Amepaniki kwelikweli. “Naomba tulia mama, ili nielewe.” James akachukua simu. “Kuna nini mama?” “Sijui. Ila Jelini amenipigia simu, ule mshono wa kichwani unataka kupasuka na yupo peke yake. Atakufa mwanangu, mimi ndio nibaki sina kitu. Watoto wenyewe ni wawili tu. Sina..” Mama Jema na yeye kilio, ameshapaniki. Udhaifu wake kila mtu alimjua, ni hao binti zake. Ni jeuri, roho ngumu yule wakuweza banwa kidole na mlango, asishituke ila si kilio cha hao binti zake. “Naomba tulia mama yangu. Acha nimpigie mimi simu.” Akakata kwa mama Jema na kumpigia simu Jelini.

Jelini alipoona simu ya James akapokea. “Pole Jelini. Nini shida shemeji yangu.” Jinsi alivyoanza naye, ikamfanya Jelini atulie. “Nipo peke yangu hotelini. Kichwa kinaniuma sana, kinakaribia kupasuka.” James akafikiria kwa haraka, nani wakumtuma hapo. Maana ndugu zao wote wapo Moshi. “Nampigia simu mtu, aje akufuate na kukupeleka hospitalini. Hakikisha hujaloki mlango ili aweze kuingia. Na kingine, naomba nyamaza kabisa. Usilie hata kidogo ili kichwa kitulie. Sawa?” Akakubali.

James akabaki akifikiria mtu wa kumtuma hapo kwa haraka, siku hizo za sikukuu, mtu ambaye hana mengi yakufanya ni nani? Wazo likamjia ni Colins. Na hivi mama yake ni muuguzi, akampigia na kumueleza. “Nilikuwa nikitaka kutafuta mtu wa kunisaidia, amfuate hotelini na kum….” Colins nusura aruke. “Wewe vipi James!? Nakwenda mwenyewe.” Uzuri alikuwepo tu kwao, wamekaa wote sebuleni kama familia, wakiangalia movie, wakila na kunywa. Siku hiyo walikuwa wanapumzika tu baada ya sherehe za krismasi walizo sherehekea pamoja na familia nyingine nyumbani kwa kina Love ambaye baba yake ni rafiki wa tokea ujanani na baba yake Colins. Walikesha nyumbani kwao, walitawanyika kurudi makwao karibia panapambazuka.

Walikwenda kulala wote ndio wameamka mida hiyo ya jioni, Colins akaenda nyumbani kwa wazazi wake, nyumba ya pili tu, uzio mmoja, ndio wamekaa hapo wamepumzika, ndio na simu ya James kuingia. Colins akamuomba mama yake amsindikize, akatoka na mama yake mbio wakiwahi hotelini. Wakaendesha Colins akiomba Mungu amkute Jelini salama.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walifika na kuelekea chumbani moja kwa moja bila hata kuulizia mapokezi wakamkuta amelala chini ya mto. “Jelini mama!” Jelini akashangaa sauti nzuri sana ya kimama ikimuita. “Pole sana Jelini.” Akatambua sauti ya Colins, akatoka chini ya mto. Akajitahidi kufungua macho, akaona kwa shida kama mapacha wamemsimamia ila akagundua ni mama yake. Akafunga macho nakutamani asingekuwa Colins amemkuta kwenye hali ile. Akajisikia aibu!

“Samahani kwa usumbufu.” Jelini akaongea akijitahidi kugeuka vizuri. “Pole.” Colins akarudia tena akiwa anamwangalia anavyojiweka sawa pale kitandani. Kugeuka na kumwangalia vizuri! Alikuwa amevimba uso, macho mekundu kwa kulia mpaka wakashituka. Colins akakimbilia upande wa bafuni, akachukua taulo na kulilowesha maji ya baridi, akaenda kuanza kumfuta huku mama yake akimpima pressure. “Pressure siyo mbaya. Nashauri twende hospitalini ili wamwangalie zaidi.” Colins akamuweka sawa, Jelini akachukua pochi yake, Colins akaibeba na kumshika mkono kama mtoto mdogo anayemvusha barabara mpaka kwenye gari. Safari ya hospitalini ikaanza. Mama Colins akashauri wampeleke kwenye hospitali anayofanyia kazi, ili wamsaidie kwa haraka.

Ikawa wazo lake lipo sahihi. Walifika tu na walipomuona mama Colins wakamsaidia kwa haraka. Wakaangalia kichwa, kila kitu kipo sawa. Daktari akamuuliza Jelini ni nini kinamfanya alie vile. Akidhani ni kichwa ili akafanyiwe MRI. Jelini akasema hapana, ila kulia ndio kumesababisha kichwa. Ndipo wakaelewa.

“Sasa nisikilize Jelini. Huu mshono unawezekana umepona kabisa kwa nje ila ndani kunaweza kukawa bado. Unapoendelea kulia unafanya mishipa ya kichwa kukakamaa na kusababisha kichwa kuuma zaidi. Nakupa dawa ya maumivu na ya usingizi ili ulale kabisa. Na ukiamka, marufuku kulia.” Akakubali kwa kutingisha kichwa huku amefunga macho. Wakazungumza na mama Colins. Kwa kuwa na yeye ni muuguzi, akaomba aondoke naye, akapumzike.

Colins tena akamshika mkono mpaka kwenye gari, ndipo mama Colins akampigia simu mama Jema kumtuliza. “Tafadhali usiwe na wasiwasi. Huyu ameshafika kwetu, atakuwa sawa tu. Wewe malizia likizo yako, Jelini atakuwa na sisi nyumbani. Wamemchoma sindano, amelala. Usiwe na wasiwasi kabisa.” Mama huyo ongea yake yenyewe itakufanya utulie tu. Mama Jema akauliza maswali yake mengi hapo ya hofu mpaka akaishiwa. Akatulia. “Kesho nampeleka mama KCMC kila kitu kikienda sawa, nitarudi Dar kesho kutwa. Naomba niangalizie mpaka nirudi.” “Mama Jema, nimekwambia usiwe na wasiwasi. Huyu Jelini anakwenda nyumbani. Wewe hata ukikaa huko zaidi ya mwezi, atakuwa sawa tu.” “Nitakufa kwa ungonjwa wa moyo, mama angu. Acha nirudi tu mwenyewe.” Akacheka taratibu huyo mama. “Basi kukutuliza, asubuhi akiamka nitamwambia akupigie ili utulie.” Wakakubaliana na kuagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Bahati Haiji Mara Mbili. Anguko La Zenda, Bila Kutarajia Jelini Mikononi Kwa Colins.

Nini Kitaendelea?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment