Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 27. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 27.

Akiwa ofisini kwake katikati ya majukumu mazito Joshua akapokea simu kutoka kwa mtu aliyemuomba ahakikishe anapata idadi yote ya mali za Malon huko Mbeya, mpaka na mashamba na aombe kwa maandishi kutoka kwa mwenyekiti wa kijiji uthibitisho wa umiliki wa hizo mali kwa jina la Malon Seduki. “Aisee nakushukuru sana.” “Ila kuna jambo jingine.” “Nini tena!?” “Katika moja ya shamba lake ambako ndiko kulikokuwa na gala lake kubwa, wanavyosema kwenye nyumba ambayo alikuwa akiishi, walifanikiwa kupata fuvu lake na baadhi ya mifupa yake.” Joshua akaingiwa na simanzi kubwa moyoni.

    “Viliwekwa wapi?” Akajikaza na kuuliza. “Inavyosemekana, kwa kuwa hawakujua chakufanya nayo, walizika hapohapo kwenye shamba lake.” Joshua akaumia sana. “Nashukuru kwa tarifa. Basi hiyo tutaongezea tutakapokwenda kuwaona wazazi wake. Tafadhali nitumie hiyo orodha ya mali zake mapema. Na sehemu sahihi walipomzikia, ili ndugu zake wafahamu.” Wakawekana sawa, wakaagana. Joshua akabaki akifikiria.

Akufaae Kwa Dhiki.

Mara simu yake ikiwa bado mkoni ikaanza kuita na kumtoa mawazoni. Akaingalia na kuipokea kwa haraka. “Huwezi amini, nilikuwa nikikufikiria sasahivi! Yaani simu bado ipo mkononi nilitaka kukupigia.” “Kwema?” Geb akamuuliza. “Nimepata taarifa juu ya mali za Malon, na walipozika mifupa yake.” “Daah!” Geb akasikika akisikitika. “Lakini bora tutakapoenda kwao, tukiwa na hizo taarifa. Si faraja, lakini angalau watajua jinsi ya kutunza kumbukumbu yake.” “Sijui kwa nini nimeumia, Geb!” “Hakuna jinsi ya kujifaraji kwenye lililompata hata kama alitukosea sana. Bado alikuwa kijana, na ni roho ambayo sina uhakika kama Mungu alijishindia. Itakuwa imepotea hivihivi!” “Nafikiri hilo ndilo linaloniuma zaidi. Alikuwa akifanikiwa vizuri sana kwenye mambo mengine yote, lakini shetani aliamua kukamata roho yake. Sijui bwana! Mimi naona tulimalize hili, niachane naye kwa amani.” Geb akabaki kimya akifikiria.

“Nafikiria jumamosi nikitoka kazini, ndio twende Moro, nyumbani kwao. Unaonaje?” “Mimi sina neno. Nipo tu. Wasiwasi wangu ni Naya ambaye ni muongoza msafara na hali yake. Unafikiri sasahivi ni wakati muafaka kufanya hivyo?” “Nimeshazungumza naye na nimemuweka sawa. Hana neno. Yeye ndiye aliyekuwa akisimamia hata ukarabati wa ile nyumba ya Malon ya Kunduchi. Amefanya kwa moyo tu ili wazazi wake wanufaike. Anasema japokuwa Malon alikuwa mbaya sana kwa wengine, lakini kwao alikuwa akitegemewa sana. Ni kama yeye ndiye aliyewainua kwao wote.” “Daah!” Geb akabaki kuhuzunika. Wakakubaliana aina ya watu wa kwenda nao huko kwa kina Malon. Mpaka Polisi waliokuwa wakifahamu utekaji nyara wake, wakawaomba kuongozana nao wasije kufika kule, wakageuziwa wao kibao.

Kuliko Mwagika Maji.

Akampigia simu na Bale kumueleza walipofikia. “Nikikwambia najutia kila kitu, unaweza kuniamini Joshua?” “Mimi ni mtu wa mwisho kabisa kuwa na wasiwasi naye, Bale. Nilikwambia tokea mwanzo na sitaacha kukukumbusha. Wamuhimu sana ni Mungu. Kaa sawa na Mungu, utabaki salama.” “Lakini natamani kukusikia unaniamini Joshua!” “Itakusaidia nini Bale? Maana hata nikikuamini au nisipo kuamini, Mungu wako yupo na wewe. Anakutafuta wewe mchana na usiku. Inamaana wewe ukikaa sawa na Mungu, hata mimi nikikupinga, haitasaidia. Tafadhali naomba hilo ukumbuke Bale. Katika kila unachofanya na kuwaza kuanzia sasa, jiulize swali unalohangaika kuniuliza mimi, kama je, Mungu yupo sawa juu ya hilo? Hilo ndilo la msingi. Utashangaa sana jinsi atakavyoweka mambo mengine sawa. Tafuta kwanza ufamle wake na haki yake,” “Mengine yote mtazidishiwa.” Akamalizia Bale mwenyewe.

“Umemaliza.” “Ila nina hofu sana. Sijui ndugu zake watanifanya nini wakijua kama…” Akasita. “Umemuua ndugu waliyekuwa wakimtegemea sana?” Joshua akamalizia, Bale akabaki kimya. Safari hii akashangaa Bale hajajitetea kabisa akitoa sababu ya kumuua Malon kama alivyoua familia yake na kumlinda naye na Naya. Akapoa kabisa bila kujitetea. Joshua akajua ameanza kubadilika.

“Nalo hilo ni moja ya jambo nililotaka kukwambia maana lilitushangaza hata mimi na Geb. Sijamuhonga mtu wala Geb hajapindisha mambo, alichofanya alitumia askari walewale tuliowatuma mwanzo kukutafuta ulipokuwa umejificha kwa Malon, kwenda kuchukua taarifa kamili juu ya Malon huko Mbeya. Maana ilikuwa ngumu mimi na Geb kuamini kama kweli uliua. Ndipo wakarudi na ripoti kutoka kwa polisi wenzao ambao na wao walichukua ushahidi kutoka kwa wanakijiji pale na mmoja wa mfanyakazi wa Malon aliyeenda kuripoti juu ya uharibifu aliokuta kwenye mji wa Malon.” Bale akashituka sana akikumbuka jinsi alivyoweka mipango yake ya mauaji akimtoa Mbaki pale ili amchome moto Malon. Akajua kwa hakika ni Mbaki ndiye aliyezungumza na Polisi. Je, hakumtaja? Akabaki akiwaza kwa hofu kubwa na ndipo akakumbuka Joshua anazungumzia hilo akarudisha akili hapo kwa haraka ili kutaka kujua Mbaki alisema nini!

“Mmoja wa wafanyakazi wake anayesemekana alikuwa akiishi hapo alisema walikuwa na tatizo la shoti ya umeme kwa muda mrefu hata Malon alikuwa akijua na kujipanga kutafuta fundi wazuri kufanya wiring upya kwenye hilo eneo. Kwa hiyo akasema anahisi walipata shoti mbaya na kuunguza eneo zima mpaka kifo cha Malon. Kwa hiyo hiyo ndio taarifa waliyoikuta huko, na ndiyo wanasema watakwenda kuwasomea wazazi wa Malon.”

“Sasa mimi sijui Mungu wako amefanyaje! Maana wale polisi wamesema wataeleza hata sababu ya kujua kifo chake ni juu ya uhalifu alioufanya. Alikuwa akitafutwa na polisi kwa kosa la kuteka nyara mke wa mtu, ndipo wakakutana na taarifa za kifo chake. Kwa hiyo hayo mengine, mimi sijui. Ninachokwenda kufanya ni kuhitimisha maswala ya Malon. Nina uhakika mama yake anayo haki yakujua kilichompata kijana wake. Atakuwa kwenye mateso akitafuta kujua alipo mwanae.” Bale kimya.

“Kilicho kikubwa japo si faraja, ni angala nimepata mpaka ushahidi wa mifupa yake ilipo. Acha nikamalizane nao. Niwakabidhishe mali zake zote, na baadhi ya mifupa yake. Nimtoe kwenye maisha yetu kabisa.” “Nashukuru Joshua. Asante hata kukarabati nyumba ile ya Kunduchi. Nilipita pale, kwakweli umefanya kazi kubwa.” “Ni Naya huyo. Alitaka kuiweka kwenye muonekano ambao hata ndugu zake wataipokea nakuona ni kitu cha thamani si pagala kama ilivyokuwa.” “Basi nifikishie shukurani zangu kwa Naya.” “Hapana Bale. Nilikwambia mimi sitakuwa katikati yako na Naya. Muombe Mungu aingilie kati mahusiano yetu. Ayaponye, siku moja uje umshukuru mwenyewe.” “Nimeelewa Joshua.”

“Vipi mguu lakini?” Joshua akabadili mazungumzo. “Nilianguka vibaya, nikatua kwenye kovu lenyewe, nikajiumiza tena. Hapa nipo kwenye kutibu tena kidonda.” “Aisee pole sana Bale. Pole. Kwa nini hukuniambia!?” “Ahaaa! Naona kama ni adhabu ambayo nastahili kuipata. Acha tu niteseke mpaka Mungu mwenyewe aweke kikomo. Pengine amekusudia nisirudi kuja kutembea tena.” “Huo ni uongo wa shetani na usikubali. Mungu sio kama sisi wanadamu. Hayupo kwenye kukuadhibu. Yeye mwenyewe analipa garama ya kuwa na mahusiano na sisi. Yaani kabla wewe hujataka kuwa na mahusiano naye, yeye anabisha hodi akisubiri ufungue mlango, aingie.” “Unajua ilikuwa ndio nakwenda kujaribisha mguu siku nilipoanguka?” Joshua akamuhurumia sana.

“Aisee pole sana Bale. Usikate tamaa. Uguza kidonda ukijua ni ajali kama ajali nyingine tu. Mungu wako yupo na wewe. Nina uhakika anakuwazia mema zaidi ya akili zetu zinavyoweza kufikiria. Utapata mguu na utarudi kutembea kama zamani. Vuta subira.” “Nakushukuru Joshua. Asante sana.” “Aisee usinyamaze Bale. Ukiwa na shida yeyote ile, usiache kusema.” “Hivi unavyonisaidia inatosha Joshua. Una mambo mengi sana, sitaki na mimi niwe ajenda ingine.”

“Ni kweli, mambo ni mengi. Lakini familia kwanza. Wewe ni familia. Usiugue peke yako.” Ikamfariji sana Bale. “Nashukuru kujali.” “Anytime. Uwe na wakati mzuri. Nitakujulisha kilichoendelea kwa kina Malon, tutakaporudi.” “Sawa.” Wakaagana.

Uchungu Wa Mwana, Aujuae Mzazi.

Siku ya jumamosi Joshua ni kama alichungulia tu kazini na kumuachia maagizo yote Jema. Dhamana aliyokuwa amepewa Jema na Joshua, ikawa ni kama akizungumza Jema, basi ujue ni kama mdomo na sikio la Kumu. Aliheshimika sana Jema.

Mida ya saa tano asubuhi msafara wa Morogoro nyumbani kwa kina Malon ukaanza wakisindikizwa na hao askari waliokuwa wamebeba taarifa za kifo cha Malon. Naya akiongoza njia. Akisindikizwa na familia ya Geb. Nikimaanisha mama G, Nanaa na Joshua. Wote walikuwa kwenye gari moja, kama kawaida, Geb ndiye dereva. Wanawake hao walikaa kiti cha nyuma maongezi yakiendelea mpaka mji kasoro bahari.

Mama yake Malon alipomuona tu Naya na umati wa watu, akaanza kulia. Wakashangaa maana hawakuwa hata wamezungumza kitu. Walikaribishwa tu sebuleni, wakaambiwa anakwenda kuamshwa ndipo akatoka na kuwakuta, akaanza kulia kwa uchungu sana. Akalia kwa muda, kisha akatulia kidogo. “Nilikuwa naumwa Naya mwanangu. Najua unamjua Malon. Kwa vyovyote alivyokuwa, hata akiwa anaishiwa mpaka mwisho, basi hataacha mawasiliano na mimi. Hiki kimya cha muda mrefu, nilijua kabisa hayupo kwenye dunia niliyopo mimi. Nilijua kwa hakika. Ila sikujua watanifikiaje kuniambia.”

“Pole mama. Ningewahi kuja kukwambia lakini na mimi aliniteka nyara, mara tu baada ya kumzika baba. Akanifungia mahali na kunitesa sana. Alikuwa akinipiga kama mnyama mpaka nikapoteza fahamu kabisa. Sikuwa nikijua mimi ni nani na wala nilitokea wapi. Nilipoteza kumbukumbu kabisa. Na hawa ni moja ya polisi waliokuwa wakinitafuta.” “Na kumtafuta na yeye mwenyewe Malon. Tulijua alipo ndipo atakapokuwepo Naya. Maana alishatoa vitisho vya kuja kumdhuru Naya.” Akaongeza mmoja wa wale polisi waliokuwa kwenye msafara. Wakazidi kulia. Zaidi mama yake.

“Hatuna nia ya kuwaumiza zaidi ila ninataka kuwaambia sababu ya kutowafikia kwa haraka. Ni mimi tu ndiye niliyekuwa nikipafahamu hapa na sikuwa nikijitambua kwa muda wote. Nilikuwa kwenye matibabu na yeye akitafutwa mpaka taarifa zake zilipopatikana. Wakawa hawajui jinsi ya kuwafikia kuwapa taarifa za kifo chake. Lakini hawa ni polisi walio na taarifa zake kamili. Naomba uwasikilize.”

“Naya mama, najua mwisho wako na Malon haukuwa mzuri. Lakini naomba umsamehe na ujue katika wote, wewe alikupenda sana. Sema tu alikuwa ameshaharibika. Mtu asiyejua jinsi ya kuishi na watu au hata kutunza upendo wa kweli. Ila Malon alikupenda sana Naya.” “Sana. Hakuna anayemjua Malon asijue wewe ndiye uliyekuwa kipenzi chake. Katika yote, na wote. Naona nyinyi wawili. Wewe na mama yake ndio mlifanikiwa kupendwa na Malon. Ni hivyo tu kama alivyosema mama yake, Malon aliharibika zamani sana. Hakujua jinsi yakuishi katikati..” Mzee Seduki akaongeza na kukwama. Wakamuona ameinama kwa simanzi mkewe akazidi kulia kwa uchungu sana.

“Naya, naomba umsamehe mwanangu.” “Mimi nimesamehe mama. Wala huna haja yakupiga magoti. Na hata nimemsaidia kukarabati ile nyumba yake ya Kunduchi. Kwa sasa ni nzuri kabisa inaweza kukalika.” “Nashukuru kama umemsamehe.” Huyo mama alikaribia kupiga magoti akimuombea msamaha mwanae, Naya akamuwahi.

“Mtakuwa na muda niwaite ndugu zake?” Baba yake Malon akauliza. “Maana wote tulikuwa na msiba usio na uhakika. Hapajawahi tokea ukimya mrefu kati ya Malon na mama yake. Labda awe mgonjwa ndio hatataka kumwambia mama yake. Lakini kama yupo hai, na hana uwezo. Basi ni bora akaibe, apate pesa yakumpigia simu mama yake. Wote tulijua amekufa ila hatukujua jinsi ya kupata uhakika.” Wakaona wasubiri tu.

Wakaitana ndugu, baada ya masaa mawili nyumba ikawa imejaa ndugu. Na wao wakawa waungwana. Hawakusema mengi mabaya ila juu ya kifo chake na kukabidhi waraka wa mali zake zote na sehemu zilipo. Joshua akawapa funguo za nyumba ya Kunduchi. “Tafadhali msidharau ile nyumba na eneo lilipo. Nipazuri sana. Nyumba inaweza kuwa ni ya kawaida, lakini wazazi wangu, Malon amewaachia kitu cha thamani sana. Msiwe na haraka kupauza. Na hakikisheni mnapata pesa nzuri sana endapo mtapauza. Ipo sehemu nzuri sana.” Geb akawatajia kiasi cha pesa baada ya kumsikia Joshua anawaambia hivyo juu ya hiyo nyumba. “Msiuze chini ya hapo.” Geb akaongeza msisitizo na kuwashangaza zaidi.

“Jamani tunashukuru kwa uaminifu wenu. Maana hata msingesema, sisi tusingejua.” Kaka yake mkubwa Malon akashukuru wakati wengine wakiendelea kulia. Wakamshukuru Naya kuleta msiba wa Malon nyumbani, ila wakasema watakwenda kuomba kibali ili wakafukue kule alikozikwa, aje azikiwe nyumbani kwao.

Wakaondoka na kuwaacha wakilia msiba. Ila na wao wakatoa rambirambi yao ya maana tu. Ni Geb na  Joshua. Pesa ipo! Wakapata nguvu ya kuanzisha msiba ramsi. Wao wakaondoka kurudi Dar, wakawaacha na msiba kana kwamba ndio umetokea. Huo ukawa mwisho wa Malon kwenye maisha ya Joshua. Anarudi Dar akijisikia amani kwamba hana mpinzani tena kwenye ndoa yake.

Anahangaikia Maisha Yetu.

Wakiwa wametulia njiani, simu ya Jema ikaingia kwa Joshua. “Kwema?” Akamsikia akishangilia. “Usiniambie imepita?” “Imepita Kumu, bosi wangu. Yaani sasahivi ndio nimekata simu. Walinipigia kunijulisha sisi ndio tumeshinda.” “Yeess!” Joshua akashangilia. “Jiandae Bonus ya mwaka huu. Utafurahi. Asante sana Jema. You are the Best.” Jema akasikika akipiga kelele. Kumu amesema! Akajua pesa haitakuwa ndogo. Kumu akakata simu akicheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Huyu Mungu ni wa ajabu aisee! Yaani amenituma kufanya haya yote tokea mwanzo nikiwa na mambo mengi kweli. Nikakubali tu kutii lakini sikutaka kabisa muingiliano kipindi hiki nilichokuwa na mimba yangu. Akili ilikuwa kwenye mambo mengine kabisa. Nahangaika nisije haribu mimba, huku moyoni nasukumwa lazima kukamilisha hili. Simu za yule jamaa kule Mbeya naye akiuliza vitu hata visivyo maana zikawa hazikomi mpaka vikaoni!” Wakacheka.

“Kweli tena. Unamwambia jambo asubuhi, mchana anapiga simu kuuliza jambo hilohilo mpaka nikaona hatakamilisha! Sasa nikawa namwambia Mungu, kwani lazima iwe sasahivi? Nikawa nampa mipango yangu sasa. Kwamba nikimaliza hili aliloniamini nalo  tokea zamani, yaani kazi ya ajira aliyonipa, basi nitafanya hili. Lakini wapi! Na nilikuwa na sababu zote, tena nzuri tu, za kugairi. Kumbe mimi nahangaika na Yake, yeye anahangaika na yangu!”

“Hongera Joshua mwanangu. Japokuwa haikuwa kwa wakati wako, lakini umemtoa yule mama kwenye kusubiri kwa uchungu. Maana angeendelea kulia msiba bila kikomo na pengine angekufa asijue ukweli juu ya mwanae. Umefanya jambo zuri, kufanya yote haya.” “Mpaka kurudisha na mali zake!” “Kabisa Geb. Si ungeachana naye tu kwa mabaya aliyokufanyia? Ndio maana Mungu amekulipa. “Asante mama.” Wengine nao wakampongeza.

“Kwani ni nini tena Joshua?” Naya akamuuliza. “Mama Kumu!” Naya akaanza kucheka kama wengine jinsi Joshua alivyomuita kwa hisia na kumgeukia kabisa. “Niambie Joshua mume wangu. Ehe?” “Acha mama! Yule simba wa kabila la Yuda, amenguruma tena. Coca watamsimulia Mungu wa Kumu mpaka wachoke.” Akaongea kwa ushindi kisha akageuka na kuanza kuabudu kwa kuimba taratibu. Nanaa akamwangalia Naya, wakacheka. “Hapo kafurahi kupitiliza!” Akamnong’oneza. Wakacheka, Naya akampokea kuimba. Waliimba  hao mpaka wanafika Dar.

Adui Wa Mtu Ni Wa Nyumbani Kwake.

Akiwa ofisini kwake akapokea ujumbe kutoka kwa Kemi akimkaribisha nyumbani kwake. ‘Kwa mara nyingine tena, tutakuwa wote kama familia. Na Kevin pia safari hii amesema hatakwenda kwa mama, atakuwa na sisi kama kuniunga mkono. Tafadhali naomba usikose, dad. Pengine mume wangu akiona tupo pamoja na yeye atarudisha moyo kwenye familia. Sipendi hivi wanangu wanavyokuwa katikati ya ndoa kama yetu. Nimekusudia kurekebisha kwa garama yeyote. Tafadhali na wewe niunge mkono.’ Kemi akatuma huo ujumbe akiweka na uzito wa ulazima wa kukutana, akimtumia mumewe kama chambo akijua lazima mzee ataingia mtegoni tu ili kunusuru ndoa ya mwanae.

‘Bila shaka.’ Mzee akarudisha majibu. Kemi alipopata tu hayo majibu, simu kati ya mama na wana zikaanza kutembea wakipongezana kwamba wamefanikiwa kumtia ndege mjanja tunduni. Maana baba yao akisema jambo si mtu wa kigeugeu. Ikabaki kazi ya kumpanga Koku tu.

Ilikuwa ni kawaida yao kukutana nyumba moja na kubadilishana zawadi za krismas na kula na kunywa pamoja. Huo utaratibu ukafa mara baada ya ndoa ya Kemi ilipoanza matatizo. Ikawa wakikutana basi ni kesi zao wao tu, mpaka Zenda na Kevi wakaanza kutoa udhuru. Kevin akaanza kwenda kusherehekea sikukuu za krisimas kwa mama yake na Zenda kivyake. Sasa baada ya miaka zaidi ya mitatu kupita ndio Kemi akalianzisha tena. Lakini si kwa ajili ya ndoa hata kidogo. Nia ni kumtoa Jelini kwenye maisha yao.

Kila Mtu na Mtuye.

Tarehe 24 ya mwezi wa 12 siku moja kabla ya siku ya krisimasi, wakiwa wamekaa tu ndugu hao wanakunywa na kula wakijiandaa na sikukuu hapo kwa mama yao, James akaingia majira ya saa tano asubuhi. Jema alikuwa amejilaza tu kochini anabembelezwa na kibaridi cha jiji la Kilimanjaro, mama zake wakiongea na kucheka wakati Jelini na Mode wakitoa vitimbwi vya wanaume wa jiji.

Hakuamini kumuona mumewe pale, tena mida ile. Akaanza kulia kwa furaha. “Jema naye!” “Mimi aliniambia hataweza kusafiri, sababu ya majukumu mengi.” Jema akamjibu mdogo wake akifuta machozi ya furaha. “Usilie sasa! Mimi nimekufanyia surprise wewe na mtoto, nataka mfurahi.” “Nimefurahi James! Nimefurahi sana, ila siamini kama umenifuata mpaka huku kijijini! Sikutegemea!” Wakacheka.

“Karibu James mwanangu.” “Asante mama. Nimekaa Dar, akili ikawa hainipi, nyumba haikaliki. Chumba ndio kikawa kikubwa. Kila nikiingia chumbani nakumbuka Jema wangu hayupo! Nikashindwa kulala. Juzi nikalala kwenye makochi.” “James!” “Kweli mama. Nasikia upweke, halafu huruma kwake. Nikajiambia hizi pesa zinatafutwa na hazijawahi kutoshea. Nikamfikiria Jema wangu, nikamuhurumia na huyo mtoto aliyebeba na hawezi kumtua mchana wala usiku, mpaka Mungu aamue kumtoa kwa wakati wake! Nikajaribu kulala havilaliki.”

“Saa sita usiku nikampigia simu mama kumtaarifu nakuja huku kama kuna maagizo ya nyumbani basi anipe. Wakaniambia Vai anamitihani baada ya sikukuu, hataki kuondoka chuoni. Anasoma, anaogopa kufeli. Viola akaomba nije nae na mwanae waje kumsalimia na wao baba. Nikaenda kuwachukua usiku huohuo na kuanza safari kumfuata mke wangu.”

“Shem anampenda Jema!” Jelini akaongea kwa kuwatamania. “Sana. Nampenda Jema wangu. Hana makuu. Huna utakachomwambia akabisha, ndio maana nimemuonea huruma, nikasema acha nije nilee naye kidogo. Angalau kumpokea huyo mtoto kwa kumsaidia hata anitume tu, apumzike.” Jema alifurahi sana.

“Ila sasa hapa sisi tunaondoka. Jema anatakiwa kwenye mji wake. Baba amesema nije nimfuate nimrudishe kwake. Tusikae huku.” “Jamani!” “Kweli. Ndio nimekuja hivyo na hata kina Viola wanamsubiria.” “Mlikula mahari ya watu, muache kigugumizi hapo. Jema anaenda kwao.” Mode akawakazia hukumu. Wakaanza kucheka. Ila Jelini na mama yake wakasikitika sana. Walitaka wabakie pamoja hivyohivyo watatu mpaka wanarudi Dar.

“Kesho basi mkishatosheka hapa, mje na kule mjini tumalizie sikukuu pamoja.” James akawakaribisha. Na kwa kuwa wanagari, wakaona sio wazo baya kujumuika nao. Jema akasaidiwa kufungasha vya kwake, akaondoka na mumewe.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Jema amebahatika sana aisee. Mwanaume mzuri, anapesa halafu anampenda kweli!” “Kabisa dada.” Mode akadakia na kuongeza. “Wanaume wengine huu ndio ungekuwa wakati wao wakufanya umalaya huko mjini kwa kuwa mke hayupo.” Wakamfanya Jelini aanze kujifikiria. Ataishia wapi na yeye kwenye maisha! Akapoa, kimya akitafakari mahusiano yake na Zenda. Anakila kitu, lakini Zenda si mume. Anayofanya James kwa Jema, si garama ya pesa au mali, lakini akajua Zenda hawezi kuyafanya. Kwanza kwa nafasi yake kwenye maisha na umri. Japokuwa ameonyesha kumpenda sana, lakini hajawahi kuzungumzia hata kwa kuropoka swala la kuja kuishi pamoja kama mke na mume au mtoto!

“Kwa hiyo Mode, umeamini sio wanaume wote malaya?” “Nahisi ni huyo James tu. Wengine wote zipu wazi.” Wakaendelea kuzungumza wakisifia ndoa ya Jema, Jelini kimya akijifikiria. Mwishoe akajionya. “Lakini siwezi kupata kila kitu kwenye maisha.” Akajiambia akijitia moyo. “Zenda ananipenda sana. Na kwake nina uhakika wa kuwa peke yangu, sio kama malaya wengine. Acha nijitulize nisianze kuwaza makuu ya kutunyima raha.” Akaendelea kujionya, ila tayari shauku ya kupata alichopewa Jema na James ikawa imeshamuingia. Akapoa. Hilo nalo akakubali kulizika ili atulie kwa Zenda.

Sikukuu!

Ikawa kweli ni siku iliyo Kuu kwa wengi. Wengine kukumbuka ya siku ya kuzaliwa kwake Yesu. Wengine wakisherehekea kuwa pamoja kama familia. Hakuna kazi wala shule. Kila mmoja siku hiyo ikawa na umuhimu wake, kivyake, siku KUU. Ila kwa kina Kasa ikawa ni siku ya mtego wao kufanikiwa. Roho mkononi. Jambo lisiharibike, mzee anaswe.

Hiyo siku ikawa imewadia Kemi akiwa ameandaa tafrija ya kitajiri haswa nyumbani kwake, kutokana na hadhi yao. Baada ya misa wanayohudhuria ya kingereza kuisha, wote wakaelekea nyumbani kwa Kemi wakiwa wanasubiriwa kutumikiwa kitajiri haswa. Kuanzia matayarisho ya hapo kwake, meza ya chakula, wahudumia meza, wagawa vinywaji, walikuwa wachache lakini wataalamu ambao wapo nadhifu mpaka tai kuendana na madhari ya hapo. Ungefika hapo, ungedhani wahudumu na wao ni waalikwa. Safi.

Mume wa Kemi anafanya kazi kwenye ofisi moja wapo ya Kasa kama kiongozi huko Shinyanga kwenye kampuni ya madini. Analipwa mamilioni mengi mno na baba mkwe wake. Kitendo cha Kemi kufukuzwa kazi, wala hakikutingisha uchumi wa familia, bali kiburi kilikuwa kikimsumbua. Iweje yeye mwenye baba asiwe na kazi halafu mumewe ndio abakie kazini akiheshimika na baba yake! Kosa ni Jelini.

Na hata Noah, mumewe Kemi siku hiyo alikuwepo mjini kusherehekea sikukuu hiyo japo hawakuwa kwenye maelewano na mkewe. Ni kama walibakia ndoa jina sababu ya watoto tu. Mzee anafika hapo hana hili wala lile asijue shuguli nzima inamuhusu yeye. Hata Noah mwenyewe hakuwa akijua mipango yao iliyojaa hila. Alikuwa kwake akijua safari hiyo wanakutana tena kama ndugu, na yeye akiwa ameambiwa yake na Kemi akidanganywa ili aje jijini kwa sikukuu, kumbe na yeye ni chambo tu ya kumuingiza baba mkwe nyavuni.

Karibia na muda wa chakula, maharage yakatiwa nazi, tena tui la kwanza. Kiungo kisichoongopa kwenye pishi la maharage. Koku akaingia hapo, akiwa amependeza haswa. Kemi akamchagamkia haswa akijua mambo yamekolea. Lakini chakushangaza hata kumuumiza Koku mwenyewe ni mzee Kasa. Hata hakuonyesha kuna utofauti. Alinyanyua macho baada ya kusikia kelele za Kemi akimchangamkia kisha kurudisha macho yake kwenye simu na kuendelea kuchati na Jelini huko alipo, kana kwamba hamjui kabisa Koku!

Mara kadhaa walimuona akicheka na kutingisha kichwa akisoma jumbe kwenye simu yake, kisha anajibu. Akawa busy na simu yake, kana kwamba hayupo pale kabisa kitu ambacho si cha kawaida kwao. Wakazidi kukereka.

Ila mpania maji, lazima ayanywe. Koku hakutaka kuonekana ameshindwa kirahisi kwa kiasi hicho. Kwanza anajiamini vilivyo. Kwa sifa zote ya mazingira yao, yeye yupo juu sana. Halafu eti leo aonekane amepuuzwa mbele ya macho ya watu wote! Hata kidogo. Akaamua amsogelee. Akamsalimia kwa karibu kabisa ili kumtoa macho kwenye simu, naye Zenda akawa muungwana, akamjibu na kurudisha macho kwenye simu yake.

 “Sikujua kama upo mjini! Umekua kimya kweli!” “Nipo.” Kwa mara nyingine tena, Kasa akawa muungwana, akatoa macho kwenye simu yake aliyokuwa bado ameishikilia mkononi, na kumtizama  akimjibu. “Nani anakuficha?” Koku akaendelea. “Maisha tu.” Akajibu Zenda wazi akiashiria hataki kuendeleza naye yale mazungumzo. Na kuweka msisitizo ili aelewe anamuingilia kwenye anachofanya, akasimama kabisa. “Nitarudi baada ya muda mfupi.” Akaongea hivyo na kutoka nje kabisa na kuwaacha hapo ndani hoi.

Kwa kuwa mume wa Kemi hakuwa akijua kinachoendelea. Ilikuwa siri ya Kemi, Kevi, mama yao na huyo Koku ambaye alisimuliwa yote juu ya Jelini. Akiwa anawajua wote hao watatu, kwanza hawapatani, na yeye siku hiyo hakutaka maneno mengi nao, Noah akawa mtizamaji bila kuchangia chochote, akaendelea kunywa zake pombe pombe kali. Akitaka baada ya hapo awe amelewa vyakutosha, alale bila hata malumbano na Kemi. Akishinda hapo kesho yake na vijana wake, siku inayofuata ananyanyua majeshi, anarudi zake Shinyanga, kimya. Maisha yake yakaendelee huko kwa amani, akifanya yake kwa uhuru wote.

 Aliachwa Koku amesimama hapo kama amevuliwa nguo hadharani. Dharau ya hali ya juu. Wazi alionyesha amemsogelea kumsalimia, eti anamjibu kifupi na kuondoka kabisa! Koku akazidi kuumia na wivu kuzidi kumsumbua maana aliambiwa na Kemi kuwa Jelini ni kama amehamia hapo nyumbani kwa mzee. Mwanzoni Koku mwenyewe hakuamini kabisa. Maana yeye alikuwa akiitwa na mzee anapojisikia hamu, tena mara moja moja. Yeye akiwa na shida naye basi anamwambia, anaandaa mazingira, wanakutana na kufanya yao, kila mtu anaondoka. Sasa kuja kusikia eti kwa Jelini mpaka anauguzwa! Hilo likamsumbua sana ila akajikaza siku hiyo mbele ya Kemi alipomtafuta kumpanga rasmi kwa siku hiyo, mpaka hapo alipohisi kudhalilika sana ndio akawa kama amemtibua na kuamini alichokisema Kemi. Kuwa, LAZIMA waungane kumtoa Jelini. Ameshakuwa tishio kwao. Morari na hasira vikampanda Koku.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Je, Ndio Wasomi Hao Wa Mjini Wamemshindwa Zenda?

Usikose Mikasa Ya Mpania Maji.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment