Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 26. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 26.

Kesho yake Zenda aliamka asubuhi na mapema kama kawaida, akawahi kazini akimuacha Jelini amelala. Mida ya saa 6 akawa amesharudi nyumbani alipomuacha Jelini. Akaanza kazi ya kumuuguza Jelini yeye mwenyewe. Anamdekeza kupita kiasi. Kukawa na amani ya ajabu kati yao. Jumapili ilipofika,  Jelini akarudi kwao, Zenda kanisani maana alimwambia bado hayupo tayari kuonana na wanae. Zenda akaelewa. Kufika saa moja na nusu usiku, simu ya Zenda ikaingia kwa Jelini. “Mimi siwezi kulala bila wewe.” Jelini akafikiria, akaamua kwenda tu. Wakabembelezana, akalala.

Maisha yakaendelea Jelini akawa akiishi hapo huku akirudi nyumbani kwao kumtembelea mama yake na mtoto. Zenda akienda kazini alfajiri, anaamka naye. Jelini anarudi nyumbani, yeye kazini. Anapata muda na mwanae. Saa nane mtoto akirudi. Anakuwepo naye. Zenda akitoka kazini, anakwenda kwa Zenda ndio mpaka kesho yake.

Taratibu maisha hayo yakaendelea. Mapenzi mazito kati ya Zenda na Jelini, amani kati yao. Jelini akamjulia Zenda, hampi sababu. Akajitenga na wanaume, akawa akichunga sana nafsi yake hataki vishawishi na mwanaume yeyote yule kwani alijiambia Zenda anampa kila anachokitaka. Na kweli, ungefika nyumbani kwa mama Jema, ungejua wamefanikiwa. Mama wa kichaga alikuwa akimiliki kadi ya benki ya Jelini ambayo Zenda anamwaga mihela humo, kama hana akili nzuri. Na yeye akajiweka akijua kuna leo na kesho. Akaanza kujijenga kibiashara kwa kutumia pesa hiyohiyo ya Jelini.

Jelini aligoma kabisa kujenga awe na kwake. Alisema Jeremy amemzoea sana mama yake, hawezi kuwatenga. Huna utakalomwambia Jelini akakubali kuhusu kuhama kwao japo uwezo amekua nao. Basi huyo mama akaona isiwe shida. Akili kwenye biashara na kuimarisha nyumba yake. Zenda alishawachimbia kisima cha maji, nyumba ikabadilishwa ikawekwa madirisha ya vioo na vyuma vizuri sana. Vyumba vitatu vikafungwa AC, kiyoyozi cha haja, starehe ya Jelini. Kupenda kulala patam. Chumba chake ndio ni kama alikijenga upya. Pakawa pa hali ya juu kuliko hata chumbani kwa mama yake asiyetaka makuu.

Marumaru za hali ya juu mpaka nje kwenye ngazi. Kwa mara ya kwanza kukajengwa vitofali mpaka kwenye geti ambalo na lenyewe lilibadilishwa sababu ya uzio wa aina yake uliojengwa hapo. Usingekutana na vumbi kwenye huo uwanja, maana palipokuwa pameachwa bila ujenzi, basi maua ya haja.  Hapo mama Jema akamuongezea kazi kijana wake wa bustanini. Kukawa safi. Nyumba ikawa ya tofauti kabisa. Kufumba na kufumbua mama Jema maisha yakambadilikia.

Maombi yake ya pesa ipotee njia yakatimia. Pesa ya Zenda ikakutana na ndoto za mama Jema alizokuwa akiwaza kwa muda mrefu sana, lakini pesa ikawa tatizo. Kulea kuanzia Jema mpaka Jeremy! Kidogo anachopata ni kwa wanae na mjukuu. Mtaji mkubwa, ikawa ni shida kupatikana. Anadunduliza mchana na usiku, kibubu hakijai. Ndio sasa Jelini akamfuta machozi kwa aina yake. Kadi akamkabidhi. Haulizi matumizi wala salio. Shoping anakwenda na Zenda. Anafanya kukusanya anachotaka huko madukani. Mama yake akapelekwa shule kabisa ya kujifunza udereva. Alivyo mpambanaji, haikuchukua muda, mama Jema akaingia mtaani bila shida.

Yule mama Jema ambaye Jelini alikuwa akimtania wakati mwingine amegombana na sidiria, sababu anaweza akachomoka kwake na haraka, asivae sidiria. Basi Jelini akimuona hana mbavu. Utamsikia, “Leo mama Jema mgomvi wako sidiria. Mshagombana!” Atacheka na kuondoka hivyohivyo, hajali. Hapo kurudi ni baadaye na chakula. Sasa shilingi imepinduka. Anaendesha Range. Mafuta yanawekwa bila kufikiria, Jema ndiye aliyekuwa na kazi ya kuzunguka naye kumnunulia mavazi na vitu vya kumfaa maana Jelini hana muda, analea penzi.

Mama Jema mchaga wa mjini. Akili ya maendeleo alikuja nayo mjini,  shida hazikuwahi kumfanya akasahau ndoto zake. Alizitunza tu akisubiria pesa ipotee njia, iende kwake. Sasa ikapotea njia. Bila kuchelewa, akajaa vizuri sana kwenye ulimwengu wake. Ungemuona, ungekubali uzazi mzuri. Mambo hayakukawia maana ndoto zilishakuwepo, ila uwezo ndio ilikuwa shida. Sasa ndio uwezo ukatoa zile ndoto kwenye uhalisia, mimba haikuchukua muda kuzaliwa, watu wakashuhudia kwa macho.

Alipoona mambo ya biashara ya mama yake yanachanganya, Jelini akajiunga naye kumsaidia. Mtoto akienda shule, anatoka na mama yake kuwahi kwenye biashara. Mama ndiye akawa muendesha mambo, akapata mtu wa uhakika wa kumtuma. Ikawa rahisi kwao kwa sababu Jelini si mbishi hata. Kila akitumwa na mama yake anafanya japo pesa ni zake kitu kilichomshangaza hata Jema na kushangaa huo moyo wake kila akisimuliwa na mama yao juu ya Jelini.

Yaani yeye akawa kama haadahiki na pesa kabisa wala hazimpeleki mbio. Hilo hata Zenda aliliona. Huna mali utakayomtisha nayo na kumzuzua. Yeye neno lake ni sitaki kukosa raha. Anataka kupendwa na kubembelezwa. Mwenyewe anasemaga mama Jema hajawahi kumchoka yeye wala mwanae. Aliwatunza wote tokea wanatua hapa duniani bila kulalamika wala kunung’unika.

Na Zenda hapo akaona apoe. Akiwa na Jelini hawana mazungumzo mazito. Yeye Jelini anataka stori na akae mikononi. Wacheke mpaka machozi. Hana habari na nyumba za Zenda wala mali zake. Wakitoka kwenda mahali, utasikia vicheko vyao wakati wote. Jelini akizungumza ujinga wake, Zenda akimsikiliza na kucheka mpaka akamfanya Zenda mfikiria mazito wakati wote, wakati mwingine kuchukua likizo ya kufikiria magumu na kuanza kufikiria kama Jelini. Machache yakuwafurahisha. Upendo ukatawala kati yao, mimba ya Jema na Naya ikiendelea kukua.

Mtu Heteleza Asipotarajia.

Ilikuwa siku ya jumatano, siku yake Bale ya mazoezi kama kawaida lakini safari hii akiwa na tumaini jipya. Alihamishiwa kitengo cha MOI mahususi Joshua akitaka apate mguu wa bandia, arudi kutembea kama zamani. Kwa hiyo mazoezi yakahamishiwa hapo, ili kuhakikisha anapata mazoezi ya kutosha, kidonda kikauke kabisa, ajaribishwe mguu. Siku hiyo Bale akashushwa na dereva, akashukuru na kuanza kutembea na magongo yake ili kuingia ndani.

Bahati yake mbaya, akajikwaa vibaya sana, alianguka na kutonesha mguu uleule ambao alikuwa akifanyiwa mazoezi. Pakaanza kutoa damu. Aliumia roho! Akapandwa na hasira nakushindwa kusimama akabaki amekaa hapo chini akiangalia ule mguu. Nesi mmoja mwanafunzi akamkimbilia ili kutaka kumsaidia. Bale alikataa kwa hasira sana mpaka akamsukuma, watu wachache wa pembeni walioona akianguka wakiwatizama. Yule nesi akamtizama pale chini, akaona ajishushe. Akamsaidia kuokota magongo yake, akamkabidhi. Bale akayapokea na kuyatupa mbali zaidi kwa hasira na kuzidi kushangaza watu.

“Achana naye, Vai. Twende zetu. Yeye si anajidai jeuri. Mwache.” Mwenzie yule nesi mwanafunzi akamwambia kwa kukereka. Huyo Vai akabaki akimwangalia Bale pale chini alipokaa. Hapakuwa kwenye udongo. Ni sementi ya barabarani, nje ya jengo la MOI. Kwamba ni kavu ndio maana ikamkwangua mguu pale ulipotua tu aridhini.

Bale akajifuta machozi na kuanza kusota yeye mwenyewe kufuata magongo. Kutambaa anashindwa, kwasababu mguu ulikuwa ukitoa damu na hakutaka kuutonesha zaidi. Akawa anasota na matako, mguu ule uliokatika, na kutoa damu amening’iniza juu. Kila alipokuwa akisogea, machozi yalizidi kumtoka. Akasota mpaka akafikia gongo moja, jingine ikawa ngumu. “Si wewe unajidai mjuaji? Sasa utakaa hapo juani mpaka ukome. Twende zetu Vai.” Vai akabaki akimtizama. “Acha ujinga Vai na huruma zako za ajabu ajabu. Twende zetu. Unamuhurumia nini? Yeye si hataki msaada? Mwache.” Vai akabaki akimtizama Bale na gongo moja akijaribu kusimama, nakushindwa.

Jua la saa sita mchana kali. Yupo chini, matako pia yakaanza kuungua. “Unahangaika naye wanini huyo!? Mimi nakuacha.” Mwenzie akaondoka. Vai akaenda kumuokotea gongo la pili akamuwekea pembeni yake bila kumkabidhi. Akalivuta. Ikaanza kazi ya kusimama kutoka chini alipokuwa amekaa. Vai akamuona anaungua.

“Ninajua jinsi ya kukusaidia mpaka ukaweza kusimama bila kujitonesha huo mguu zaidi. Nitasimama upande ambao umeumia mguu.” “Sema ambao sina mguu.” Bale akaongea kwa hasira. “Halafu wewe utatumia nguvu zako zote kwa mguu huo mwingine. Ni sawa?” Kimya.

Vai akaenda kuinama pale, akampa mabega. “Pitisha mkono unishike kwa nguvu zote, ukitumia mguu huo mwingine kusimama, ili usiendelee kujiumiza.” Vai akainama akijua amemuelewa. “Nipe hilo gongo moja nikushikie upande huu, ukiwa wima nitakukabidhi. Akamuelekeza kitaalamu mpaka Bale akaweza kusimama. Akamkabidhi gongo lake.

“Asante.” “Karibu. Unaelekea wapi?” Akajifuta machozi na kujaribu kufikiria na kuangalia alipo. “Nina mazoezi. Kwanza naona haina maana tena. Bora nijiachie tu. Maana hata kama nikupewa mguu, inamaana siwezi tena mpaka kidonda kipone tena.” “Mimi ni mwanafunzi tu. Leo nimepangiwa na mwenzangu hapo kliniki. Nashauri twende wakakuangalie, bila ya kuishia njiani. Wao ndio wataalamu wanajua zaidi.” “Unafikiri huu mguu nilizaliwa hivi ndio nikaumia jana kwamba sijui ninachozungumzia? Najua maana wanashindwa kunipa mguu wa bandia mpaka nipone. Najua kwamba siwezi kuvalishwa mguu wa bandia mpaka nipone kabisa.” Bale akajieleza kwa jazba. “Na unategemea kupona vipi endapo ukiondoka sasahivi na jeraha hilo jipya?” Vai akamuuliza taratibu tu.

“Unajua unaweza kusababisha madhara makubwa zaidi endapo hapo ulipoumia sasahivi hapata tibiwa? Na kabla hujasema unazo dawa za kwenda kutumia nyumbani, nashauri usirudie njiani sababu ya hasira. Wapo wataalamu wanaweza kukushauri vizuri. Ingia ndani, ukawaonyeshe ulipojitonesha, wao ndio wakuruhusu. Usiishie hapa.” Bale akakubali. Akaanza kuchechemea akiingia ndani. Kisha akageuka na kumtizama Vai. “Nilishakushukuru.” Vai akacheka na kuondoka kwa haraka kama anayewahi sehemu.

Bale akaingia ndani, akaenda kujiandikisha, akapewa namba. Ni hospitali ya taifa. Watu ni wengi, yeye akapewa namba 67. Akatafuta mahali, akakaa akisubiria zamu yake. Alikaa hapo mpaka kidonda kikakata damu. Ilipofika saa saba na nusu akamuona Vai anamsogelea. “Vipi?” “Nimepata namba 67.” “Lakini wanaona wagonjwa kwa haraka na wahudumu wapo wengi.” “Nimeona foleni inasogea. Namba 43 ameshaitwa.” Vai akaangalia kulia na kushoto, kisha akapata kama wazo.

“Naweza kukusafisha kidonda wakati ukisubiri. Kitakupunguzia nzi.” Bale alikuwa akishindana na nzi hapo kwenye mguu wake. “Na hata ukimuona mtu mwingine, ni sisi pia ndio itabidi kukusafisha. Kwa hiyo nikupunguza muda wa baadaye. Nikisafishe tu. Sitakifunga mpaka daktari akione.” Bale alishakuwa amechoka kukaa hapo. Akashukuru. Akamuongoza njia bila yakumsaidia wakafika kwenye hicho chumba. Hapakuwa na mtu. Akamuonyesha sehemu ya kukaa. Bale akajitahidi mpaka akakaa.

Vai akachukua vivaa na kukaa mbele yake, akaanza kumsafisha Bale akimuangalia. “Hujaumia vibaya sana. Hapatakawia kupona. Upo kwenye antibotic zozote?” “Nilishamaliza ndio maana nilichukia. Nilikuwa nimebakisha kidogo tu, nipewe mguu.  Tena hapo ni kwa kuwalazimisha sana nikiwaambia mbona kama mguu wenyewe umepona ila wananikawiza tu! Ndio hatimae kwenye kliniki yangu iliyopita wakaniambia leo nikirudi naweza kuanza kujaribu mguu ili nione utakao nifaa. Sasa hii anguka ya leo, ndio inamaana inabidi tena kusubiri! Mpaka najiona nina mkosi unaokataa kuisha!” “Eti mimi nimekuja kugundua, wakati mwingine kusubiri sio jambo baya.” Vai aliongea kawaida tu akiendelea kumsafisha, lakini ujumbe aliopata Bale moyoni ukawa mzito sana. Ukamkumbusha makosa yake yote aliyofanya mpaka kumfikisha kwenye ulemavu huo. Akapoa kabisa.

“Usinielewe vibaya, ukasema naongea hivi kwa sababu nina miguu yote! Naongea hivi kwa sababu maisha yamenifundisha kwa vitendo juu ya haraka nilizofanya nikiwa mdogo….” “Wewe bado ni mdogo Vai.” “Muonekano usikudanganye. Ndani ya huu muonekano, nimeishi maisha ya kama mwanamke aliyemaliza miaka hata 60 hapa duniani. Na sikuachwa salama kwenye haraka zangu. Najuta na kutamani kama ningesubiri mambo mengi, pengine leo nisingekuwa hapa, wala nisingekuwa hivi.” “Ulitaka kuwa nani?” Bale akamuuliza, akajicheka.

“Nilitaka kuwa daktari.” “Lakini upo upande huohuo. Haupo mbali sana.” “Nesi si daktari. Na kwa akili nilizokuwa nazo, na uwezo wa baba yangu aliokuwa nao wakati ule, kama si haraka, nina uhakika ningekuwa daktari. Lakini nipo hapa, kwa haraka zangu.” “Ulisema usingekuwa hivi. Ungekuwa vipi?” Bale akachomekea swali la pili kwa haraka.

Vai akafikiria jinsi ya kumueleza bila ya kutoa undani wake kwa mtu asiyemfahamu, akashindwa. Akamwangalia Bale, akamuona ametulia akisubiria jibu. “Pengine niseme hivi, katika hii miili Mungu aliyotupa dhamana nayo hapa duniani, kuna viungo amewapa wanadamu uwezo wa kuvitafutia mbadala, kama huu mguu wako. Ni kiasi cha muda tu. Kidonda kikipona, unauhakika wa kurudi kutembea kama mwanadamu mwingine yeyote yule na watu wasijue endapo utavaa suruali na usiamue kumwambia mtu kama una kiungo cha bandia mwilini mwako. Ukaishi kawaida, nikimaanisha uwezo wa kutenda kama mtu mwingine yeyote yule.” Bale akabaki akimsikiliza kwa makini.

“Lakini katika hii miili, kuna viungo Mungu aliviumba, bado hajampa akili mwanadamu ya kuvitafutia mbadala. Ukikiharibu alichokupa yeye, ujue ndio basi tena. Unacho mara moja tu. Kikiondoka ndio ujue ni kilema chako cha maisha mpaka unarudi kwa muumba wako.” Hapo akamchanganya Bale, nakumfanya atulie afikirie ni kiungo gani hicho kisicho na tiba mbadala!

“Jicho?” Akajiuliza na kumtizama Vai. Alikuwa na macho mazuri yanawaka kama mwili wake. Vai akacheka kidogo akijua amemuacha akifikiria. Ila akaendelea. “Kwa hiyo Bale, ukiambiwa subiri, nakushauri subiri. Waliotangulia, wametangulia tu. Aliyesomea mambo ya mifupa, anajua ni kwa nini anakushauri alichokushauri. Inamaana aliweka nidhamu darasani. Akasomea hilo jambo ndipo akaaminiwa na kupewa dhamana na bodi ya watu wenye uzoefu wa hicho kitu, kukutana na mtu kama wewe mwenye shida kama hiyo. Chochote watakacho kushauri, fuata ukijua aliweka nidhamu chuoni, tena kwa miaka mingi tu, akijifunza mchana na usiku jinsi ya kusaidia watu wenye hiyo shida. Kazi yako wewe ni kuongeza tu umakini ili hivi ulivyoanguka leo, usianguke tena. Halafu jua unalo tumaini, Bale. Mungu wako amekupendelea. Analo suluhisho la tatizo lako, hapahapa duniani, tena hapahapa MOI. Ni muda tu. SUBIRI.” Bale alipoa sana. Huo ujumbe ukabeba maana nyingine kabisa kwake, Vai asijue. Akatulia.

Vai akamsafisha mpaka akamaliza, Bale yupo mbali wala hajui anachofanyiwa tena. Vai akasafisha pale mpaka akamaliza bado Bale amepotelea mawazoni. Akamsogelea. “Nashauri urudi pale ukasubirie namba yako ili usije ukaitwa, wakakuruka.” Bale akamtizama vizuri akiwa ametuliza mawazo ndipo akaweza kumuona vizuri zaidi. Vai alikuwa mweupe haswa, tena wakung’aa. Hana kipele wala kovu aliloweza kuliona. Hiyo rangi yake ikamkaa yeye vizuri na kumfanya avutie machoni. Hata hapo amevaa sare ya unesi alivutia. Bale akabaki kama ameduaa kana kwamba ndio anamuona kwa mara ya kwanza. “Huyu kiumbe atakuwa amekosa nini hicho kisicho na tiba wala mbadala!” Bale akajiuliza akimtizama nakushindwa kuelewa kabisa.

Vai akacheka na kumuuliza. “Vipi?” “Nashukuru sana Vai. Asante kwa kila kitu na samahani nilikuwa mkali kwako bila sababu.” “Usijali.” Bale akasimama akijishuku. Maana Vai aliyemsaidia si msichana hovyo. Mrembo haswa lakini akajishusha kwake yeye mlemavu! Akatamani kama angekuwa amekutana naye wakati mwingine, tena akiwa si mlemavu na iwe ni zile enzi zake akiwa na pesa alizokuwa akizikusanya kipindi cha Maloni. Angalau angepata ujasiri wa kuzungumza chochote mbele yake. Lakini ujasiri ukamuishia kabisa.

Akachechemea mpaka mlangoni kisha akageuka. Akataka kama kumuuliza kitu, akakumbuka ni mlemavu, hana mguu na hapo alipo anatunzwa na Joshua. Na vile alivyomuona Vai alivyo! Akasita, Vai akimtizama tu. Akagairi na kutoka bila ya kuongeza neno.

Pesa Imepotea Njia.

Ungemuona mama Jema, ungejua amefanikiwa. Halii shida akikopa hata kwa ndugu zake. Anazungumzia mamilioni ya pesa na biashara zakueleweka. Mpaka wanakaribia kufunga mwaka mambo yao yanazidi kuwaendea sawa tu, ikawa kama Mungu amewaamulia wao. Kituo cha mafuta kikawa kipo sehemu nzuri, kinakaribia kukamilika kianze kazi yakuingiza pesa. Mama Jema akiwa anakisubiri, akaendelea kuwekeza nguvu kwenye duka lake hilo kubwa alilokuwa akiuza vipodozi, vitu vya harusi ambavyo alikuwa akinunua nakujua watu wangehitaji. Upande mwingine vitu vya wanawake. Pochi na viatu. Kukubwa na kukawekwa kwa hali ya juu. Ungefurahia kuwepo hapo.

Maisha yakawa yakiendelea, pesa ya biashara inaingia na Zenda naye bado anamwaga pesa kama anayemlipa Jelini mshahara kila wakati wala si mwezi. Jelini akatulia haswa, yeye ni Zenda tu, hataki shida na mtu. Kila anachojua kitamuudhi Zenda, anakwepa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wachaga hawa wanawake na wao kila krismasi lazima waende migombani kwa mama yao. Lazima. Basi kama kawaida yake mama Jema akaanza kujiandaa kwa safari. Jeremy akafunga shule akijua anaenda kwa bibi. Na yeye anamuita bibi kama mama yake. Safari hii wanakwenda na gari ya Jelini. Renji. Wakafungasha vitu vyakutosha. Jelini akaenda kuagana na Zenda, wakapeana penzi kwa muda, wakiagana kuwa krismasi na mwaka mpya Jelini atakuwa migombani na yeye Zenda atakuwa na familia yake mpaka mwaka uanze. Yalikuwa mapumziko ya siku chache tu, lakini ikawa huzuni kana kwamba ni mwaka! Walikuwa wakiondoka tarehe 23 na kurudi tarehe moja. Mama Jema akaacha biashara zao vizuri, safari ya Moshi ikaanza wakiwa na Jema na tumbo lake.

Mchaga James alisema kwake yeye huo muda ambao hayupo kazini ndio wakati wa kuwekeza kwenye biashara, Jema akaona aongozane na mama yao. Gari ya Jelini kubwa haswa, Jema akakaa kiti cha mbele ajinyooshe mgongo, Jelini mwenye gari nyuma na mwanae kama gari si yake. Mama yao pia alikaa kiti cha nyuma na kina Jelini, Zenda alimwambia Devi yeye ndiye awaendeshe kwa sababu ni safari ndefu, kisha kurudi kuwachukua huo mwezi wa kwanza tarehe 2. Safari ikaendelea stori njia nzima wakicheka tu, Jelini asijue mipango mibaya anayopangiwa.

Usiombe Vita Na Akufahamuye.

Halafu yeye ajipange kimashambulizi dhidi yako, huku akikuchekea huna habari. Sasa Zenda yeye mwenyewe ndiye aliyejiweka busy na Jelini, wala si kwamba Jelini alimbana. Lakini wanae wakaona ni kama Jelini ndio sababu. Na Kemi bado hakuwa amerudishwa kazini, hicho kikawa kinamuuma hata mama yao huko alipokuwa. Alikuwa akiumia haswa. Swala la kuumizwa kwake Jelini halikuwa likizungumziwa ila kufukuzwa kwake Kemi kikatili ndio ukawa msiba kati yao na mama yao.

Zenda huwa na wanawake, lakini bado wakawa wakinufaika na pesa yake. Sasa kuona safari hii eti amekuja mtoto mdogo anayesababisha wasitafune pesa ya Zenda watakavyo! Eti ndiye ameshika masikio ya dad! Hasira yote ikawa kwa Jelini. Yeye ndio akawa sababu.

Hapatikaniki kwa simu wala jumbe. Hana muda na familia wala wajukuu ambao huwapenda sana. Hapakaliki kazini wala kwa wanae. Mbaya zaidi Kemi! Kipenzi cha dad, kila mtu analijua hilo! Ukitaka kitu kwa haraka kutoka kwa Zenda, basi mtume Kemi, utakipata kwa haraka tu. Lakini eti Kemi amepokonywa mpaka hati ya kusafiria na haruhusiwi kufika karibu ya mali za dad! Hilo likawa chumvi kwenye chai. Huna kiungo ukatia ikafaa kunyweka tena.

Watoto hao na mama yao wakaona ni wakati muafaka wa kutoa mwiba kidoleni kabla hakijazidi kutunga usaha na kuozesha kidole zaidi. Wafute kabisa kumbukumbu za Jelini kwenye familia ya Kasa wala asiwahi kurudi tena. Wakafikiria kumtafutia Zenda mwanamke mwingine watakayeendana na wao. Na safari hii walazimishie ndoa kabisa ili mzee abaki kuwa upande wao, kosa jelini lisiwahi kujirudia tena.

Sasa nani wakumuweka kwa baba yao na wao wabakie ndio wanufaikaji!  Yaani asiwe mwanamke mwenye shida au uchu wa pesa! Atakayeingia na matatizo yake halafu pesa ya baba yao ndio ianze kumkarabati mpaka afae! Huyo hawakumtaka. Wakabaki wakikuna vichwa na huo ndio ukawa mtihani. Maana walishapita wengi tu hapo kwa baba yao, ila hawakudumu. Nani!?

Simu kati ya mama na wanae, watatu hao zikaendelea wakipanga mipango mizito ya kimapinduzi. Kila wanayemtaja kumuweka kwenye maisha ya baba yao wakawa wakimtoa kasoro, ila mwishoe kura ikamuangukia Koku. Koku ndiye msichana wake huyo wa booty call. Wamekuwa kwenye hayo mahusiano ya kupeana penzi tu, bila kujifunga kwenye mkataba wowote ule, kwa muda mrefu tu, wote wanamjua.

Koku mtumzima, amefanikiwa kiuchumi haswa. Kwa kumwangalia tu utajua hataki ujinga kwenye maisha, na hakuwahi kuolewa wala hakuwahi kutaka swala la kuwa na watoto.  Ila juhudi kwenye kutimiza ndoto zake nzito. Darasani alikaa mpaka vitabu vikaitika, ‘abee’! Kazi nzuri aliyounganishiwa na huyohuyo Zenda ikawa ikimuingizia mamilioni ya pesa ambayo yanafanya wanaume wamkimbie. Kiburi kipo kwa kumwangalia tu. Mwanamke wa mipango, hana shida ndogondogo kama kina Jelini mpaka kukarabatiwa nyumba! Anaishi kwenye hekalu la kujenga yeye mwenyewe na juhudi zake alizoweka kwenye maisha.

Wote walimfahamu na hakuwahi  kuwa tishio kwenye mali za baba yao kwani kwa hakika Koku alikuwa tajiri, hali zikiendana nao. Ila yupo busy sana. “Huyohuyo atatufaa. Kwanza Koku ni mtumzima sana. Umri umekwenda, hana hata uwezo wa kushika mimba tena. Kwa hiyo hawezi kuzaa na Kasa.” Mama yao akaongeza kwa kuridhia kwa Koku na wote wakaafiki kuwa watabaki wao tu wawili ndio watoto wa Kasa na warithi pekee maana hicho hata mama yao alikilinda.

“Sasa jinsi ya kuwaunganisha tena Koku na dad ndio shuguli.” Kevin akawaza kwa sauti wakiwa bado kwenye simu. “Na hapo ndipo pakuwa makini sana. Maana mnamjua Kasa. Anawaza kwa kunusa mbali sana. Kosa dogo tu. Kujichanganya kwa aina yeyote ile, hata kuropoka neno moja tu, mjue tayari amewakamata. Na akihisi tu, mjue ndio tumepoteza nafasi nzima, na hatakaa akatusamehe daima. Sisi tutabakia kwenye upande wa watizamaji timu iliyofungwa uwanja wa nyumbani.” Mama akaweka msisitizo na kufanya wanae wazidi kufikiria wakijua wanacheza na baba yao, kichwa yake inafanya kazi kwa haraka sana tena vizuri mno.

“Hakika tufikirieni kwa makini. Hata mimi sitaki kosa jingine litokee tena. Tulikaachia haka katoto, kakaingia kwenye maisha ya dad kama utani tu, ona kalichonitenda! Amenisingizia mimi nataka kumuua na kunifukuzisha kazi! Hakika lazima atoke na yeye kwenye maisha ya dad.” Kemi akaongea kwa kuumia sana. “Kwanza atafilisi mali zote. Hakajasoma, ni wale wanawake malaya wanao danga tu. Anachohitaji ni kujinufaisha yeye tu.” Akaongeza Kevin kwa jazba.  

“Kama bado hatujachelewa!” Akaongeza mama yao kwa wasiwasi kuwa pengine Jelini alishaanza kuhamisha mali za Kasa. “Nimechunguza kwa makini sana mpaka kwa kumuuliza kijanja yule wakili wake, bado. Dad hajamfanyia chochote kikubwa. Devi anasema ni marekebisho tu ya hapo nyumbani kwao. Lakini sasa mjue muda unavyozidi kwenda, atazidi kumuingia dad akilini, ndipo ataanza kuchota mali. Before we know, yeye ndio atakuwa mama Kasa, wote tunaishi kwa rehema za Jelini.” “Hakika tusiruhusu.” Mama akaongeza kwa jazba wasijue mzee anawajua vizuri sana na anaakili, ndio maana kila alichompa Jelini, alimtumia Godwin, ambaye ni mwanasheria wasiyemjua kabisa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kila alichompa Jelini, alihakikisha kipo kwa jina lake Jelini Kundi. ‘Kundi’ ukoo wa mama Jema. Wanae wote walichukua huo ubini wake. Watoto wasiojulikana baba zao. Siri ya mama Jema peke yake. Mali zote za Jelini zikawa hazina hata dalili kwamba zimetoka kwa Kasa na akamuapisha Godwin. Tena kwa maandishi kuwa siku atakayotoa hiyo siri, atamshitaki kisheria. Kwamba asijewahi kuzungumzia chochote, na yeyote, kile kinachoendelea kati yake na Jelini isipokuwa na Jelini mwenyewe na yeye mwenyewe mzee Kasa. Godwin akakubali ikawa yeye ndiye anayeweka kila kitu kwa maandishi na kufuatilia mambo kisheria kuhakikisha hakuna wakuja kumpokonya chochote Jelini hata kama itatokea mzee mwenyewe hayupo duniani. Na akatunza hayo mambo ikawa ni kati yao tu, wao watatu. Hakuna mawasiliano hata ya barua pepe, akijua wanae wanaakili, wanaweza kufuatilia email yake wakajua mazungumzo kati yake na Godwin juu ya Jelini. Kikubwa wakawa wakizungumza kwa kuonana sehemu mbali na kazini na nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wao wakiendelea kuweka mipango yao wakiwa wamejawa jazba, mzee Kasa alishakuwa amejipanga kivyake kumlinda Jelini, asijue anajilinda upande ambao watu wa nyumbani kwake wanajipanga upande mwingine wakilinda huo upande anao udhibiti yeye, kwa wakati huo. Mali.

Wakaendelea kujipanga kwa makini, ila kwa haraka wakijua huo ndio wakati muafaka wa kufanya yao maana anayembana baba yao, hayupo mjini. Walishampigia simu Devi na Devi kuwahakikishia mzee yupo peke yake, kwani yeye ndiye aliyetumwa kupeleka familia ya Jelini na Jelini mwenyewe Moshi. Hasira zikazidi zaidi. Na Devi ndiye aliyekuwa akiwapa kinachoendelea kwenye maisha ya baba yao.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usiwahi Kuwa Adui Na Anayekufahamu Kwa Undani. Wanapiga Wanapojua Patauma.

Nini Kitaendelea? Watafanikiwa Kwenye Penzi Zito La Zenda Na Jelini?

Usikose Muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment