Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 23. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 23.

Inafika mida ya saa tano chumba cha Jelini kilijaa maua kila kona. Akamletea na mashuka mazuri ya chuichui, mito minne iliyovalishwa silk safi, pamoja na mablangeti mazuri sana ya sufu, kutoka kwake. Vyote ni vizuri na vilionekana vya thamani sana. Na chokleti nyingii lakini Jelini alifungua macho tu akaangalia na kurudi kulala. Jioni Jema anaingia hapo anakutana na chokleti, akatafuta mahali akakaa na kuanza kula.

“Sasa usimalize Jema bwana! Huyu baba atakuja hapa, akute Jelini hajala hata moja wewe umemaliza.” “Wala sio mimi, mjukuu wako huyo!” Jema akaendelea kula. “Mbona jasho litanitoka! Mpaka huyo mtoto azaliwe!” Jema akazidi kucheka. “Kwanza Jelini mwenyewe anashindwa hata kufungua macho. Sijui wamempa nini! Maneno yote kwisha.” Wakaanza kumcheka vile alivyokuwa amelala.

    “Kungwi wako yule.” “Mbona nilimshukuru! Haki ningetia aibu mama. Nilikuwa sina moja! Kwanza hata sikuwa nikiwaza.” “Sasa ulitegemea nini?” “Nilijiambia nitajua mbele ya safiri huko kwenye ndoa.” Wakaanza kucheka. “Jema!” “Nilivyokuwa busy vile! Ningeanza kuwaza saa ngapi kukata kiuno, mama yangu? Kwanza sikuwa hata na wakumkatikia.” Wakazidi kucheka, Jelini kalala hana habari.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Mara mlango ukagongwa na kuingia, alikuwa Zenda. “Sijui nimechelewa?” “Hata kidogo. Hapa tulikuwa tukizungumza tu. Jema alikuja kunipokea mpaka usiku ukija.” “Sasa na Jeremy?” “Nimemwambia bibi yake mwingine akae naye mpaka nifike mwenyewe.” Akaonekana kama hajaridhika. “Jelini hatakuwa na wasiwasi na hilo kweli? Ni kama hamuamini mtu mwingine na Jeremy isipokuwa wewe!” “Wala hujakosea. Ila nakwenda.” Hapo akaonekana kuridhika.

    “Nina zawadi zake hizi, unaweza kumwambia zinatoka kwa mama yake. Aliniambia Jeremy anapenda vitabu.” “Sana. Na asante.” “Karibu. Wameniambia Jelini amekuwa akilala siku nzima, ameweza kuzungumza naye kweli?” “Hapana. Hata Jema naye ametoka kuwauliza sasahivi juu ya kulala kwake. Lakini wanasema kwa siku tatu za mwanzo, ni bora hivyo kuliko maumivu.”

    “Mimi na mjukuu wa mama Jema tunashukuru kwa chokleti.” “Jema wewe mtoto! Ni za mgonjwa bwana!” “Sasa Jelini mwenyewe hazili mama, na mjukuu wako anataka! Tufanyaje?” “Umenyimwa aibu wewe! Si ulisema hutaki kunenepa wewe, utakuwa ukila matunda tu?” “Mama naye! Unamuhesabia chakula mpaka mjukuu!” “Mbona mpaka azaliwe huyo mimi nitakoma! Nitaleta kesho hizo chokoleti.” “Wewe mama unazijua!?” Wakaanza kuchekana wenyewe, Zenda akiwasikiliza.

    “Nitaziulizia pale dukani.” “Kwamba Mangi auze chokleti kama hizi?” “Lazima atakua nazo bwana!” “Mmmh!” Jema akaguna akiendelea kula. “Sasa kama huna uhakika na upatikanaji wake, mbona unaendelea kula bwana Jema? Ridhika bwana!” “Wewe si umesema utaenda kuzinunua kwa Mangi kesho uje nazo?” “Kwa ule ugunaji wako, nahisi kama sitazipata!” “Wala hujakosea. Hizi zakizungu mama yangu, ndio maana mjukuu wako hataki kuacha kula.” Mpaka Zenda akacheka.

    “Wewe na mwanao muwe na kiasi bwana! Halafu acha nimbebee na Jeremy.” Mpaka Jema akacheka. “Hapo sasa ndio tunatia aibu mama Jema bwana! Unataka wajukuu wote wale!?” “Kidogo tu.” “Msiwe na wasiwasi. Nitaagiza nyingine.” Zenda akaingilia. “Basi agiza nyingi ili na sisi pia tupate.” “Jema wewe mtoto umenyimwa aibu, wewe!” “Ni mjukuu wako huyo wala si mimi. Mimi na chokleti wapi na wapi mama yangu?”

    “Usihangaike mwaya. Hawa nitawanunulia za kwa Mangi.” “Sasa mama wewe unataka kuharibu. Nishakwambia Mangi hana chokleti. Wewe acha sisi tuletewe chokleti za kizungu. Achana na chokleti zile za mtaani, zinaganda kwenye meno kama uchafu!” “Haya, simama hapo twende Jema. Unakazi ya kula tu. Twende unisogeze.” “Twende mama Jema. Nikamsalimie na kaka.” “Wewe kwako hupiki?” “James harudi sasahivi nyumbani. Leo mpaka saa tano usiku. Kashanipitia mchana, tukaenda kula, ujue kuja kumuona ni usiku mwingi.” “James muhangaikaji!” “Sana. Mpaka namuhurumia. Ana mambo mengi na yote yanamtaka yeye!”

    “Sasa unafanyaje?” “Tangu namfahamu ndio yupo hivyohivyo. Akitoka kazini anahamia kwenye biashara. Yupo barabarani mpaka saa sita usiku. Nilijua naolewa na nani mama yangu. Namsindikiza kwa simu, nikichoka nalala.” “Bora.” “Basi twende ukale kwangu.” “Wewe mama Jema unataka kuniharibia ndoa wewe! Nikila kwako, kwangu sitapika, James atarudi nyumbani asikute chakula, akutane na mke aliyeshiba, amelala hana habari. Wewe acha nikasalimie, niwahi kwangu nikapike. Au unataka ukapikie kwangu halafu wewe na kaka mkishashiba ndio muende kwenu?” “Wewe unataka kunivurugia ratiba yake yule. Nataka awahi kulala, asubuhi shule. Kapike kwako acha uvivu.” Jema akaanza kucheka. “Ulijuaje? Nilitaka ukifika unipikie na cha kesho.” Wakaanza kucheka wakikusanya vitu vyao ili watoke, Zenda akiwasikiliza.

    Alikuwa amesimama kwenye kitanda anamwangalia Jelini. “Jelini! Jelini!” Wakamsikia akimuita kwa sauti ya chini taratibu. “Fungua basi macho hata unione!” Jema na mama yake wakakonyezana. “Jelini!” Akamuita tena. “Zenda!” Akaitika taratibu. “Umeona maua niliyokuletea?” “Nilikuwa nimelala. Kichwa kizito!” “Pole. Jaribu kufungua macho kidogo. Niangalie.” Akajitahidi. “Unaumia?” “Upande huu. Ndio maana nafunga macho.” “Pole sana. Unataka kumsalimia Jeremy kidogo ili umtoe wasiwasi?” Akafikiria. “Nataka uamke nijaribishe kukulisha kidogo. Wamenipigia simu na kuniambia hauli.” “Nasikia usingizi.” “Jitahidi. Simu hii nimeweka chaji, mpigie mtoto. Pengine ukimsikia utachangamka.” Akakubali. “Basi nanyanyua kitanda kidogo.” Akabonyeza kitanda kikaanza kunyanyuka, akawa kama anakaa.

    “Pole Jelini.” “Jema! Nilikusikia nikahisi naota. Mama Jema yuko wapi?” “Nipo hapa. Vipi?” “Sasa Jeremy!?” Akawa kama amekumbuka. “Hivi ndio nilikuwa naondoka. Nilimwambia mama yako mkubwa amsubirie pale nyumbani, aende naye kwake, nitamfuata. Nimezungumza kama lisaa limepita, yupo sawa tu.” “Mamkubwa anamjulia.” Akaonekana kuridhika. “Nimechoka, natamani kulala tu.” “Jikaze ule, Jelini. Utadhoofu!” Jema akasisitiza, Zenda akadakia. “Nakulisha kidogo tu, halafu nakuacha ulale. Au hupendi chakula chao?” Akamuuliza kwa kumbembeleza, akajaribu kufikiria. “Hata sijui ladha yake!” “Hajala huyo. Alikula kidogo sana, akapotelea usingizini.” “Niambie unahamu ya kula nini?” Zenda akamuuliza, wakamuona anaanza kulia. “Nataka tu kulala, Zenda. Nimechoka!” “Basi usilie, utajitonesha. Nifungulie tu mdomo, mimi nitakuwekea chakula mdomoni. Na sitakuongelesha. Sawa?” Akanyamaza.

    “Nyinyi nendeni tu. Atakuwa sawa. Na kama atashindwa kula, nitawaomba waongeze dripu ya glucose ili asidhoofu, mpaka tena kesho pengine tumjaribishe tena chakula.” Wakazungumza tena wakaweka mipango ya mama Jema kuleta uji asubuhi wakataka kuondoka lakini Zenda akawawahi. “Gari ya Jelini ipo tu ofisini haina kazi. Kwa nini usiitumie ikusaidie wewe na Jeremy?” “Mimi sijui kuendesha magari.” Akajibu mama Jema bila shida. “Nayaonaga tu humo barabarani na kupewa lifti, sijui hata wanawekaga wapi funguo. Nisije kufa nikaacha wanangu bure!” “Basi nitatuma dereva asubuhi aje akuchukue.” “Hapo utanisaidia. Nashukuru.” “Bila shaka.” Wakaondoka.

Upendo, Husitiri Wingi Wa Dhambi.

Wakati yupo njiani na mama yake wakiongea yao, simu yake ikaanza kuita, akapokea alikuwa Magesa. Jema akaanza kucheka. “Mimi Magesa.” “Hujambo Magesa?” “Sijambo. Na mdogo wangu hajambo? Mimi kaka mzuri. Nataka kujua hali ya mdogo wangu. Halafu jumamosi nimuombe bibi anilete, nimletee zawadi zake, halafu nimsalimie. Sitaki akija kuzaliwa awe hanijui kama mimi ndio kaka mkubwa.” Jema alicheka sana.

“Mimi nimekupenda kaka mkubwa. Kumbe na wajibu wako unaujua?” “Ila sasa sijui mtoto anapenda nini! Nimekwambia bibi ndio dereva wangu siku ya jumamosi?” “Uliniambia. Sasa ameshakubali?” “Mimi hawezi kunikatalia.” “Ujue Magesa mimi nina mipango yangu lazima uniombe?” Akamsikia Mama G akiongea pembeni. “Tunaanza mipango yako kwanza. Nakusindikiza. Ikikamilika, na mimi unanisindikiza kwa mtoto. Mama angekua haendi kazini, ningemuomba yeye. Lakini wewe unakua hauna kazi nyingi siku za jumamosi, kwa hiyo tunaweza kwenda.” “Unapenda kunipanga wewe!” Jema anacheka hana mbavu.

“Ujue mimi nikiwa mkubwa na gari yangu, nitakuwa nikikusindikiza bibi?” “Na ulikumbuke hilo. Sio uje uniruke, ujidai umesahau jinsi nilivyokuwa nikikusindikiza kwenye yako.” “Mimi siwezi kusahau bibi.” “Sasa uulize muda mzuri wa kwenda na wapi. Sio ifike siku yenyewe, hatujui sehemu ya kupeleka vitu vya mtoto.” “Anti Jema upo?” Akarudi kwenye simu.

“Nipo Magesa, nilikuwa nakusubiri uweke sawa mipango ya usafiri.” “Bibi atanileta. Ila anataka kujua muda gani mzuri na wapi. Halafu mimi nataka kujua mdogo wangu anataka nini?” “Anapenda kula huyo!” Magesa akaanza kucheka. “Hata mimi napenda sana kula. Kila saa nasikia njaa.” Jema akaanza kucheka na kusikia upande wa pili wakicheka. Akajua na wazazi wake wanasikiliza.

“Basi si bora nikupikie kabisa, ili ukija unakula chakula kingi?” “Kama ni kingi nakuja na mami wangu pamoja na Jimmy.” “Umeanza kualika watu nyumbani kwa watu Magesa bwana!” “Ni kwa anti Jema bibi. Usiwe na wasiwasi.” Hilo likawafurahisha. “Ningekuja na dad wangu na Liv, lakini  wao hawapendi kula.” Mpaka Geb akacheka. “Jimmy yeye anasumbua kidogo, lakini mami akimlisha, anaweza kula kidogo halafu basi kingine namalizia mimi.” Wakazidi kucheka.

“Kama ndio hivyo basi itabidi nipike kingi zaidi ili mkiondoka wote muwe mmeshiba. Lakini sio jumamosi hii. Sasahivi nina mgonjwa hospitalini, sipo nyumbani mpaka kama mida hii.” “Pole anti. Nani anaumwa?” “Mdogo wangu. Na asante.” “Mimi ningekuwa siogopi sindano, ningekuja anti. Lakini sipendi hospitalini, halafu naogopa sana mada..” Akasikia kimya kama kuna mtu anamuongelesha.

“Sijajua bado mtoto anataka nini bibi!” “Nakurudishia Magesa, bwana!” “Ila mwambie anti mimi sijamaliza, usikate.” “Sawa.” “Anti Jema bibi anataka kuzungumza na wewe. Nimpe simu?” Akajua wameshasikia swala la ugonjwa. “Sawa. Halafu tutazungumzia maswala ya anachopenda mdogo wako. Maana na yeye nahisi anapenda kula kama wewe.” Magesa akacheka wee kama mazuri. Akampa simu bibi yake.

“Poleni Jema.” “Asante. Shikamoo.” “Marahaba. Ni nani mgonjwa?” “Ni mdogo wangu, anaitwa Jelini.” “Yule alisema yeye kwenu ndio mpole sana ndio maana watu hawajui kama ni mdogo wako?” Mpaka mama Jema akacheka. “Yaani Jelini!” Mama yake akatingisha kichwa akicheka maana na yeye Jema aliweka kwenye spika akiongea huku akiendesha.

“Huyohuyo kiziwanda wa mama Jema, cha maneno. Alianguka vibaya! Amepasuka lakini mbaya zaidi, pamechimbika. Juu ya nyusi. Ameshonwa lakini pia amepoteza damu nyingi. Ila anaendelea vizuri wala msiwe nawasiwasi.” “Ni sawa kuja kumuona?” “Analala tu. Wanampa madawa ya usingizi, analala tu. Wala msihangaike.” Mama G hakuridhika. “Mbona unataka kuninyima shuguli bwana Jema?” Jema alicheka sana.

“Nakuhurumia usumbufu usio na sababu!” “Hayo ndio mambo ya familia yalivyo. Mmoja akiumia ni wote tunaumia. Si usumbufu. Msiuguze peke yenu.” Hilo likawa faraja. “Haya, tunashukuru. Mida gani nyinyi mnakuwa na nafasi? Maana mama ndiye anayeshinda naye mpaka jioni nikitoka kazini ndio nakwenda kumpokea.” “Basi tutapita kama kwenye saa nne ili kumpitishia mama na mgonjwa kitu cha kula, kisha tutarudi tena jioni.” “Ila Jelini hali. Labda mama.” Wakazungumza wakijipanga.

“Sasa Magesa nimwambie aniletee nini? Sitaki kumsumbua.” “Anapenda shuguli kuliko bibi yake. Hivyo ukimsumbua ndio atafurahi apate chakusimulia. Wewe mtajie kitu unachopenda kula, tutakuletea tu. Na usijisikie ni lazima kukaribisha wageni wake wote.” Wakaanza kucheka. “Hamna neno.” “Wewe ukimuendekeza huyo, utajikuta unakazi ya kukaribisha ukoo wake mzima.” “Msijali. Nyinyi mjiandae mje kula kwangu. Ni kweli Geb na Liv wao hawatakula? Naweza kuwapikia kitu watakachopenda.” “Jiachie tu. Wewe tupikie sisi tunaokula kila kitu. Hawa hutaweza.” Wakazungumza na kucheka.

“Basi muwe na usiku mwema.” “Na wewe Jema mwanangu.” “Asante. Msalimie Nanaa na wengineo” “Tena Nanaa huyu hapa. Bora tu umsalimie mwenyewe.” Nanaa alishituka nusura akimbie. Pakazuka ukimya hapo, Geb kimya akijiangalizia. “Nampa simu Nanaa.” “Naogopa mama.” Akamsikia Nanaa akinong’ona. “Msalimie tu. Hana neno.” “Sitaki kumuudhi tena. Naogopa mama. Naogopa kuharibu zaidi.” “Alikwambia nini Joshua?” Nanaa akapokea simu.

“Halo.” Akaanza Nanaa kwa sauti ya kutetemeka mpaka mikono ilikuwa ikimtetemeka mpaka mumewe akaumia. “Upo mzima mama ya rafiki yangu kipenzi, kaka mkubwa wa ukoo?” Angalau wakacheka. “Mwanangu anapenda ukubwa huyo!” “Lakini bora yake anayependa ukubwa na majukumu yake. Kwa hilo, nimemuheshimu.” “Basi huyu utamchoka.” “Si rahisi. Huyo anayependa na majukumu! Nishindwe mimi tu. Hapa naandaa orodha ya vitu anavyotaka mdogo wake.” “Hapo utakuwa umemfurahisha mwanangu. Na nashukuru mwaya Jema. Asante kwa kila kitu.” “Hata kunifukuza kwako?” “Jema naye? Jambo haliishi!” Angalau wakacheka.

“Mimi bado nimenuna bwana!” “Nisamehe Jema. Sina hata jinsi ya kujitetea.” “Ila mimi nitakwambia kitu Nanaa. Na ninakwambia kwa sababu najua James anakupenda. Hili jambo linamtesa yeye zaidi maana mimi ukweli hatuna mazoea. Hata tusipokuwa kwenye mahusiano, hapatakuwa na shida.” “Shida ipo Jema.” “Hapana. Tumefahamiana ukubwani. Hunijui, sikujui Nanaa. Namaanisha kama isingekuwa James, ungeweza kuishi bila mimi na ukawa sawa tu, lakini si wewe na James. Sijui kama unanielewa?” Nanaa akaanza kulia.

“Maana kama isingekuwa mimi Jema, basi angekuwa mtu mwingine anaolewa na James. Usingekuwa na umuhimu wa kunifahamu. Ila nafikiria mahusiano yako na James. Mimi sitaki nyinyi mkosane kwa sababu yangu. Ila nimekwambia kuna kitu nitakwambia Nanaa, nitakwambia tu. Hivi nilitaka nikinyamazie, lakini mimi nimekataa kuwa wifi wa hivyo. Nakataa mahusiano ya kumnyima raha James.” “Ni nini?” Nanaa akauliza kwa wasiwasi.

“Sasa, sasahivi nina mama Jema kwenye gari. Acha nimalizane naye kwenye mizunguko yake, mimi nitakupigia. Au unawahi kulala?” “Na hivi umenisamehe, nitakusubiri tu.” “Na wewe si kirahisi hivyo! Mbona unashindwa hata kumuiga Magesa rafiki yangu?” “Basi na mimi nitaleta zawadi si kwa mtoto, kwako.” “Niandae orodha?” “Jema naye! Wewe orodha hiyo mpe Magesa. Yangu iwe surprise.” “Basi kwenye surprise ongeza na matenite.” “Jema wewe mtoto huna aibu?” Mama yake akashangaa sana, wakaanza kucheka. “Nina shida sana na matenite ya kimtindo, sio tena magauni makubwa! Hapana. Tulipanga na Naya twende kuyanunua mazuri yakisasa, yatakayofaa na kazini, ndio Jelini akaugua. Najiona sina muda tena.” “Basi mimi nitakutafutia.” “Nitashukuru. Nitakupigia mwaya baadaye.” Wakaagana. Nanaa hakuamini. Alifurahi mpaka mumewe akafurahi.

“Sasa sijui anataka kusema nini!?” “Usianze tena kujinyima raha. Naomba tulia na habari njema za kwanza.” Mumewe akamuwahi. “Ila nimefurahi sana jinsi ulivyozungumza naye. Kumbe mambo unayajua!” “Sijaamini mama! Nilikuwa naogopa mpaka nikakulaumu kuniunganisha naye kwa haraka!” Wakaanza kucheka. “Na mimi nilikufanyia makusudi, maana nilijua hutakaa ukawa tayari kwa hofu.” Angalau kwa mara nyingine tena wakaanza kucheka Nanaa akisikika amefunguka.

Hospitalini.

Huku hospitalini ilipofika mida ya saa tatu na nusu akaingia James na Colins wakamkuta baba ya mfanyakazi mwenzao amekaa hapo na kitabu chake akisoma. Colins alishituka sana. Ni mzee Kasa! Anamuuguza Jelini!? Hilo likamsumbua kidogo asielewe ndio inakuaje! “Naona tumekuja muda mbaya!” “Hata yeye amelala siku nzima. Imekua ngumu hata kuzungumza naye kwa dakika 5.” “Jema ameniambia. Poleni sana aisee.” James akazidi kumchanganya Colins. “Inakuwa vipi apewe na yeye pole!?” Colins akajiuliza.

Akamsogelea Jelini. Akamtizama vile alivyolala na mabandeji kuzunguka kichwa. “Daah!” Akasikika Colins, Zenda akamtizama. Akamuona anamfunika shuka vizuri, na kubaki akimwangalia, Zenda naye akabaki akimwangalia Colins. Colins akapotelea mawazoni akimtizama Jelini asijue Zenda anamtizama kwa makini. Akaingia muuguzi hapo. “Sasa Colins?” James akamshitua kama waondoke. “Vipi maumivu yake lakini?” Akauliza Colins akimtizama yule muuguzi. “Yupo kwenye dawa kali za kuzuia maumivu ndio maana unaona analala sana. Si rahisi kuhisi maumivu.” “Kumbe afadhali. Daah!” Colins akaongea macho kwa Jelini, ikabidi James amsogelee. “Mimi naona twende tu.” “Daaah! Anaonekana ameumia sana.” Akaendelea kulalamika Colins macho kwa mgonjwa. James akaamua kuaga.

Wakawa wanatoka. “Ningejua mapema, ningekuja!” Ikawa kama anajilaumu, Zenda anamsikiliza tu wakiwa wanatoka. “Hata ungekuja isingesadia. Jema mwenyewe hajapata naye muda. Alikuwa amelala siku nzima.” Wakapotelea, lakini kikamsumbua Zenda. Wivu. Akakumbuka hayo madhara amesababisha mwanae.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakawa kama wote, mama G, Geb na Nanaa wakisubiria hiyo simu ya Jema. Simu ya Nanaa ikawa ikiangaliwa kila wakati. Ilipofika mida ya saa nne usiku ujumbe ukaingia. ‘Bado upo macho na unaweza kunisikiliza?’ Hapohapo Nanaa akaruka hewani. “Nilijua utakuwa umeshalala. Umenisahau.” “Hapana. Mambo yamekuwa mengi tu. Ningekujulisha.” “Niambie.” Jema akajiweka sawa.

“Naweza nisiwe mtu sahihi kukwambia hivi, au ukaona hayanihusu. Lakini nilijiambia nitakwambia halafu wewe mwenyewe uamue chakufanya. Na naweza nisiwe na jinsi sahihi ya kukueleza, ila bora usikie tu. Maana naona hakuna jinsi nyingine. Na utanisamehe kama navuka mipaka.” “Wewe niambie tu.”

“Mimi sikufahamu Nanaa, ila mwanzo wangu mimi na wewe umekua mbaya sana. Mbaya zaidi nikazidi kupata habari zako zilizonifanya nithibitishe ulichonifanyia nilipokuja kwako. Lakini mimi mwenyewe nikajiambia lazima kusamehe kwa ajili yangu, James na mtoto niliyebeba. Siwezi kuzungumza na Mungu kama wewe ukiwa katikati yangu na Mungu. Nikaona nikutoe njiani, ili maombi yangu yasizuiliwe. Hilo nikafaulu. Nikapuuza yote, nikajisikia mwepesi nafsini mwangu, maisha yakaendelea, lakini nikajisikia jukumu la kuzungumza na wewe.”

“Narudia tena, mimi sikujui, ila nakufahamu kwa upande ulionifungulia mimi na vile nilivyokusikia. Sikuhukumu, kwa sababu niliona upande wako mwingine ukiwa na mtu kama Naya. Nikajiambia si kwamba wewe ni mbaya, ila upo kama mwanadamu mwingine yeyote yule. Hata mimi si rafiki wa kila mtu, kuna watu nimeamua kuwa nao karibu, wengine ni salamu tu. Si dhambi maana si lazima kufuatana nyuma na watu wote, lakini sitaki kuwa na neno na mtu. Hata kama nikiamua kukuweka pembeni, usiwe mtu wangu wa karibu, basi nahakikisha tunapokutana mahali, hata kama tupo wawili tu, basi tunaweza kukaa, tukachagua chakuzungumza, tukacheka na kuachana bila kufuatana nyuma kwa simu wala ujumbe. Sijui kama unanielewa?” “Nakusikiliza Jema.” Nanaa akataka kusikia zaidi.

“Nimezungumza hivi kwa ajili ya mahusiano uliyokuwa nayo na mliyo nayo sasahivi wewe na kina Viola.” Nanaa alishituka sana. Hakutegemea kabisa kusikia hao watu. “Sikuhukumu kwa kuwa wamenipa historia yenu. Ukweli ni mbaya. Hata mimi nilishangaa na kuumia kwa niaba yako na wao niliwaambia. Mimi binafsi sijui kwa nini Mungu aliruhusu upite uliko pita Nanaa. Lakini Mungu alikupa daraja, ukapita mpaka kufika hapo ulipo. Hukuchagua daraja, aliyekuchagulia daraja ni Mungu. Sijui kwa undani uliishije, ulikuzwaje mpaka kufika hapo, lakini kwa walivyoniambia kina Viola, naweza kuhisi ni pachungu. Narudia tena, sikujui kwa undani lakini acha mimi nikwambie ukweli Nanaa.”

“Wale watu kukulalamikia, wakisema walikuja mpaka kwako kukuomba msamaha, ukawaacha chini, ukaenda juu ukiwaambia unawaachia mumeo awasikilize, wewe umechoka kuwasikiliza. Umewasikiliza sana tokea mtoto. Ukawaacha hata hukuwapa maji ya kunywa. Hukuja kuwatafuta tena. Na mkikutana hata sehemu mnashindwa kusalimiana! Hata mlipokuja kwenye shuguli zangu, hamkusalimiana kabisa. Nina uhakika mlionana. Sijui unasikia jinsi mimi tu ninavyosikika? Ni kama tayari nakuhumu! Kwa nini? Ni kwa sababu unasikika upande wao, wao wakisema walikufuata mpaka kwako, lakini ukashindwa kuwapokea, ukiwa wewe ulipokelewa kwao. Sijui kama unanielewa Nanaa?” “Nakusikiliza.”

“Watu uliokuwa nao pamoja wanaposema siku hizi Nanaa ameinuliwa sana na Mungu, hawezi hata kusalimia watu kama sisi. Hawezi kusamehe. Hawezi kuwa karibu na watu kama sisi ambao tulishindwa shule na maisha. Anakuwa na matajiri wenzake. Anakaa katikati ya matajiri tu. Hataki hata kutambua kama tunafahamiana na tulishaishi pamoja! Halafu mbaya, watangulie kusema walikukosea sana na umeshindwa kusamehe! Sasa hivi ndivyo inavyosikika kwa watu tusiojua ukweli wa mambo. Kwamba wewe huna shukurani. Na umebadilika. Kwa mtu kama mimi niliyekuja kwako kwa mara ya kwanza kabisa, ukanikarimu kwa staili ile. Tena nikiwa nimekuja kuomba mahusiano! Unafikiri inachukua muda gani kuamini wanachokisema?”

“Haya. Inawezekana wanadamu tusiwe na maana, usijali. Lakini Nanaa, watu wakikunung’unikia. Wakilalamika hivyo, je, kwa Mungu aliyeamuru samehe saba mara sabini akisikia manung’uniko hayo, unafikiri anasikiaje?” Jema akaendelea bila kusubiri majibu.

“Kwa hakika mimi nilitaka kuangukia hapo, lakini nikasema hapana. Si lazima mimi nikawa mtu wako wa karibu, lakini si Ukristo kusikia hili na kulinyamazia. Na wenyewe wanakuogopa kukusogela sababu wanajua wewe ni kipenzi cha James. Wanamuogopa James, na wanasema wamekubaliana mpaka na mama yao wakuache kabisa, ufaidi mafanikio yako kwa uhuru bila kukusonga. Sasa anayeachwa katikati ni James. Na hili sijazungumza kabisa na James. Hata malalamishi ya dada zake sijamwambia kabisa kwa kuwa sikutaka kumchanganya James.”

“Naomba nimalizie kwa kusisitiza Nanaa. Mimi sikufahamu. Sihitaji chochote kutoka kwako nikimaanisha mahusiano fulani. Ila sitaki tuwe maadui kiasi ya kwamba eti tukikutana mahali, tushindwe hata kusalimiana! Au tushindwe hata kunywa chai pamoja! Hapana Nanaa. Mimi nampenda Mungu. Nataka kuishi ukristo. Na kwa hakika nimeachilia chochote kilichotokea katikati yetu. Nimekuelewa kwa upande huo. Si kwamba wewe ni mbaya. Hapana. Ila mimi si mtu uliyetaka kuniweka karibu kama Naya, ndio maana uliweza kunipa maneno makali sana ukiwa hata hunifahamu na kukataa ukaribu wangu japo nilikuona mkiwa na Naya, mnaitana mpaka vyumbani! Nilikuona Nanaa na mlikuwa kwenye wakati mzuri tu.”

“Narudia tena Nanaa. Kwa moyo mweupe kabisa, sina neno na wewe. Sitaki tuwe maadui. Nataka mahusiano yako na James yaendelee. Ila nimekufikishia yale niliyoyasikia juu yako. Angalau mimi nimepata neema ya kukufahamu kwa upande mwingine ndio maana nimepata hata ujasiri wa kukupigia na kukwambia hili. Sio nafasi yangu, lakini mimi ningekuwa wewe, hivi ndivyo ningefanya.” Jema akaendelea.

“Kwa ubaya wote uliotendwa ukiwa unakua, jifanye mjinga. Samehe. Watangazie msamaha. Kisha waache. Hutapungukiwa Nanaa ila itapunguza manung’uniko masikioni kwa Mungu. Na sio lazima ukawaweka karibu. Fanya kama ulivyofanya kwangu tu. Hata hivyo wakina Viola wenyewe wapo busy. Mimi mwenyewe hatuna matatizo nao, lakini hata hatutafutani mara kwa mara. Niliwashawishi mpaka wakakubali kurudi shule. Wote wawili sasahivi wamejiingiza shuleni, naona wamekazana kweli. Hawana muda na mtu. Vai analalamika shule yake ya unesi ni ngumu na Viola naye hivyohivyo. Ni mpaka mimi mwenyewe niwapigie kuwajulia hali au watatuma ujumbe wa salamu tu. Nakuhakikishia sio watu wa kufuatana nyuma. Hawana muda.”

“Wewe jishushe tu, na hata kama ulishasamehe, basi watangazie msamaha wajue umewasamehe. Na kingine, itawarahishia hata mkiwa mnakutana mahali, mnasalimiana na kupita kwa amani. Wanakiri walikuwa na utoto mwingi na ujinga. Viola ameniambia hata mtoto aliyezaa alimpata kutoka kwa mwanaume aliyekuwa wako. Lakini ona Mungu alichokupa Nanaa. Familia nzuri sana. Yeye amebaki na hukumu ya kukupokonya mwanaume mpaka leo, wakati pengine wewe hata hukumbuki! Sasa hudhani ukimtangazia msamaha utamuweka huru? Halafu James alinipa siri ya mama yake kuwa anapenda sana pesa. Na ukorofi wake wote, pesa huwa inamtuliza.” Nanaa akacheka taratibu akimjua mama yake mkubwa. Kwamba James hajakosea.

“Sasa niambie mtu kama wewe ukamfuata kwa salamu tu na kumshika mkono, itachukua muda gani kusamehe na kuachana naye kwa amani?” Kimya. “Ni hayo tu, usiku mwema. Acha nimpigie simu na James nilale, kesho kazini.”

“Kabla hujakata Jema naomba kukuuliza kitu.” “Uliza tu.” “Kwa mwanzo tulioanza mimi na wewe, unafikiri kweli hatuwezi kujenga mahusiano mengine ya ukaribu kama hivyo wewe na Naya?” “Mahusiano yanajengwa Nanaa, si kupangwa. Nilichokifanya kwa Naya ndicho nilikifanya kwako. Nikitambua wewe ni mdogo wa James, na Naya ni mke wa Joshua ambaye ni zaidi ya bosi wangu. Kwako likatokea lakutokea, kwa Naya nikashangaa vimenoga zaidi ya nilivyotarajia! Haitaji kunipigia simu akiwa na ajenda. Kwangu si kama kwake, lakini anaweza kuja kulala kwenye kochi mpaka mumewe aje amfuate. Amehamia kwenye saluni yangu ya uswahili na ameipenda. Daktari anayemuona yeye kwa kliniki, nikajikuta nimependa sifa zake, na mimi nimejindikisha hapohapo anapofanya kliniki yake. Tunakwenda siku moja kliniki. Haya, akipikiwa nyumbani kwake kitu anachokipenda, anakibeba, unashitukia amenitokezea ofisini kwangu na chakula. Tunakula, atakaa hapo mimi nikifanya yangu mpaka atoke na mumewe jioni. Hatukupanga au hatupangi, lakini tunajikuta mambo mengi yanaendana sana, bila shida au mipango mizito. Sijui kama unanielewa?”

“Na Naya anakupenda Nanaa.” Hapo akamtuliza. “Anakupenda sana. Anakuzungumza vizuri sana baada ya kurudiwa na kumbukumbu zake. Na nafikiri hata yeye amechangia kunipa ujasiri wa kuzungumza haya na wewe baada ya kutambua kutoka kwake wewe sio mbaya kama inavyosikika. Kwa hiyo kujibu swali lako, sijui. Ila najua mahusiano huwa hayapangwi kwa simu.” “Nimeelewa na nashukuru kwa kuzungumza na mimi. Acha nikuache upumzike.” Wakaagana.

Asubuhi, Hospitalini.

Jelini alilala usiku kuchwa ilibidi kuongezewa tu maji ya glucose ili kumsaidia kumtia nguvu maana alishindwa kabisa kuamka. Asubuhi alipokuja mama Jema, Zenda akijiandaa kutoka akaingia Colins. Akawasalimia na kuulizia hali ya mgonjwa. “Ndio nilikuwa nikiambiwa hapa, alilala usiku, hata hakuamka.” Akajibu mama Jema. “Lakini hivyo ni afadhali, hatakaa akiugulia maumivu.” “Kwani wewe ni nani?” Ikabidi mama Jema kuuliza, Zenda akasubiria kusikia huo utambulisho wake, ila kwa kuwa alishaaga, akajidai anaingia bafuni kuosha mikono ili kuendelea kuwepo hapo na kusikiliza.

Colins akajibu. “Samahani nilisahau kujitambulisha. Na pengine umenisahau tu. Mimi naitwa Colins, nafanya kazi na James.” “Ndio maana sura si ngeni! Nilikuona kwenye shuguli zake na Jema! Asante kwa kuja kumuona huyu. Alianguka vibaya kweli!” “Aliniambia James. Tulikuja jana usiku lakini alikuwa amelala.” Colins akasogelea pale kitandani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati anamfunika, Jelini akafungua macho. Akamtizama kama ambaye haamini. Akashangaa jinsi moyo wake ulivyosisimkwa kumuona Colins pembeni yake. “Pole Jelini.” Jelini akabaki akimtizama haamini kama ni yeye! Hisia za ajabu zilizoamka ndani yake zikazidi kumshangaza Jelini mwenywe! Hakutegemea wala kupanga kujisikia hivyo. Colins amekwenda kumuona yeye! Akabaki kimya anastaajabu nafsini mwake. “Unajisikiaje?” Akamuuliza kwa upendo! “Uliniambia nisikusogelee Colins!” Jelini akasikika kwa sauti ya chini, na Zenda huko bafuni akasikia. Mama Jema akajiweka sawa.

“Nakumbuka, lakini nimekuja kukuona.” “Ili iweje? Huna haja ya kuwa hapa.” “Sikukusudia kukuumiza Jelini! Nilitaka kukuepushia shari.” Colins akamjibu kwa upendo na sauti yake nzito iliyotulia, na kuzidi kuukoga moyo wa Jelini. “Nilikwambia hamna shida. Nikaheshimu hilo, ndio maana nilikuacha kabisa. Tafadhali simamia maamuzi yako, usiwe mtu wa kuyumba.” Jelini akaongea na machozi yakimtoka. Bila kutarajia, Colins akamfuta kwa upendo, tena taratibu mtoto wa kiume bila haraka! “Pole Jelini.” Akaongeza Colins kwa sauti iliyojaa upendo na kutawala chumba kizima, tena huku akiendelea kumfuta machozi taratibu kana kwamba hasikii alichoambiwa na Jelini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Aluta kontinua…


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment