Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 21. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 21.

Akakimbilia kwenye kitanda akiwa amejawa hofu. Akamkuta Jelini amelazwa hapo ila amefunga macho. Amefungwa bandeji kuzunguka kipanda uso  mpaka nyuma. Kama kichwa chote kwa juu kimefungwa. Aliogopesha. Akajipenyeza mpaka akamfikia. Wakamuona anamshika mkono. “Jelini, Jelini!” Akamuita taratibu akitaka angalau afungue macho ajiridhishe mwenyewe hata kabla hajauliza kulikoni mbona kilio kwa mama yake! Mapigo ya moyo yakazidi kwenda mbio lakini akajifariji si kifo, maana kama ni kifo asingekuwa na sindano yakupitishia maji au damu mkononi. “Jelini?” Akaita tena ila safari hii akimtingisha mkono ambao ulikuwa na joto kuashiria yu hai. Akafungua macho.” “Pole.” “Asante.” Akajibu kwa sauti ya chini, akarudi kufunga macho.

    Wakamuona anahema kwa nguvu na kumgeukia dakatri. “Vipi hali yake?” Akamuuliza. “Alipasuka sehemu kubwa ya juu ya jicho. Juu ya nyusi.” Akawaonyesha. “Imebidi awekewe damu kwa haraka, amepoteza damu nyingi sana. Na pia atahitaji damu zaidi.” “Mmepima vizuri hiyo damu mliyomuwekea lakini? Msije kuwa mmemtibu mwanangu kwa kumpa maradhi mengine.” Mama wa Kichaga akaja juu. “Damu zote wanazowawekea wagonjwa hapa…” “Acha kunijibu kuhusu watu wengine. Namzungumzia mtoto wangu mimi na kile mlichompa. Usinipotezee muda na majibu ya kiustaarabu. Maana baada ya hapa nitakuja kumpima tena. Sasa ole wako uwe umempa magonjwa kwa damu uliyomuwekea. Hapo utanijua mimi ni nani. Maana nitarudi hapa na vipimo.” Zenda akamtizama mama Jema. Akakumbuka Jelini alishamsimulia habari zake. Akanyamaza kimya, maana aliambiwa mdomo wake huwa hauna kumsitiri mtu tena anapokuwa amekasirika.

    "Umenielewa?” Mama akamuhoji daktari bila kupepesa macho ila kufuta machozi. “Maana huyu amepima na uthibitisho wake kuwa hana magonjwa hatarishi ninao, nimetunza. Sasa ole wako.” “Damu aliyopewa ni salama kabisa. Tafadhali usiwe na wasiwasi.” Akajibu kwa utulivu tu akitaka na yeye huyo mama atulie. “Kichwa kinauma sana, mama.” Jelini akalalamika akitokwa na machozi. “Pole Jelini. Pole sana.” Zenda akamgeukia daktari. “Tutamuongezea tukifika wodini. Naomba akapate sehemu ya kutulia. Kwa sasa hata mwanga unaweza kumuumiza kichwa.” Wakatoka hapo wakimfuata nyuma, Zenda pembeni amemshika tu mkono.

    Jelini akapewa huduma zote na kuachwa apumzike. “Nashauri aachwe kabisa, apumzike. Huyu binti ameumia kwa hakika maana mbali na kupasuka, pia amechimbika. Ameshonwa pakubwa na amepoteza damu nyingi. Anahitaji ukimya kabisa, apumzike. Ataletewa chakula, msihangaike na swala la chakula. Wanavyakula vizuri sana hapa.” Kimya, daktari na manesi wote wakatoka akiwa amechomwa dawa ya usingizi. “Mama, usimsahau Jeremy. Ataogopa akirudi asikukute.” Jelini akaongea amefunga macho. “Sasa na wewe hapa?” “Mimi nalala. Naomba usimuache. Nenda tu ili asianze kulia peke yake.” “Halafu na mimi nitakuwepo hapa. Na kama mlivyosikia wanatoa vyakula. Kama asipopenda, nitaagiza kiletwe chakula kingine.” Zenda akawatuliza.

    Jema akamsogelea Jelini. “Pole Jelini wa mama Jema.” Wakamuona anacheka. “Usianze kunichokoza Jema bwana, mwenzio naumwa.” “Na unavyoogopa hospitali!” Wakaanza kucheka. “Nilitaka kukimbia nilipozinduka eti wananiambia wananipeleka hospitali! Wakanishika kwa nguvu, wakaniambia nikitoka tu pale, damu ndogo iliyobaki itaisha yote mwili. Nikalala mpaka hapa. Eti nafika kule kwenye chumba walikonishona, yule daktari anaanza kuniambia watakachonifanyia, nikawaambia wamuite mama Jema, na asiniambie kitu kingine, mimi naogopa sana. Wasiniguse tena mpaka mama Jema mwenyewe atakapofika pale. Nikashangaa nimepotelea usingizini.” Wakacheka.

    “Watakuwa walikupa dawa ya usingizi. Pole Jelini mtoto mzuri.” Akacheka taratibu na kufunga macho. Jema akamfunika vizuri.” “Nini kilitokea Jelini?” Mama yake akauliza. Kidogo Zenda akaingiwa na wasiwasi. Maana alishajua haikuwa ajali ya kawaida. Akabaki ameshikilia moyo. “Eti mama yangu?” “Nilijikwaa nikaanguka mama. Halafu nasinzia.” Zenda akahema kwa nguvu. “Tukiwa hapa huyu hatalala, mama. Tumuache apumzike. Mimi nitarudi kulala naye jioni.” “Naona mimi ndio nirudi, akili ndio itatulia.” “Bwana mama! Usimuache Jeremy. Atalala na nani?” “Kweli.” Mama Jema akajirudi. “Au nimpeleke kwa Mode?” “Sitaki mamdogo akae na mwanangu. Atamsahau tena, amfungie mwanangu wakati akienda kwenye starehe zake. Nataka wewe ndio ubaki naye. Kwanza kesho shule na ameshaanza kuzoea. Sitaki akose shule.” “Ni kweli. Basi unipigie usiku ili nitulie. Umesikia Jema?” “Usiwe na wasiwasi mama. Mimi nitakuwa naye. Ila acha nikurudishe nyumbani usihangaike na usafiri sasahivi.” Zenda akaona kujaliwa kwa huyo mama.

    Kwanza alionekana ni mama wa kawaida sana. Lakini alizunguka wanae vizuri kweli. Na jinsi Jelini alivyokuwa akimzungumzia mama yake kwake, Zenda mwenyewe alitegemea aje akutane na mama kama Senetor wa Marekani. Lakini! Hapo hakuwa na kipodozi hata kimoja. Nguo alizovaa za kawaida tu kama aliyekuwa kwenye shuguli zake za kuhaso tu. Hana cha manukato wala urembo wowote wa hereni wala pete. Hafanani na mwanae hata mmoja. Ila kwa jinsi alivyosikia sifa zake, na muda mfupi alivyojaa hapo, akiweka ulinzi kwa wanae, Zenda mpenda vizuri, akapita muonekano wa nje mwenyewe akaongeza heshima kwake.

    “Wewe nenda kazini, mimi nitapata usafiri hapo nje nitafika tu nyumbani, usiwe na wasiwasi. Usiharibu kazi.” Kisha akawa kama amekumbuka kitu. “Wewe Jema! Nilipokupigia uliniambia upo hospitali, kwema?” Jema akaanza kucheka. “Bwana mama ulikuwa unalia mpaka nikaingiwa hofu! Nikamwambia James, mama Jema analia, leo maji yamemfika shingoni. Si kawaida yake.” “Niliogopa sana. Maana huyu nilitoka kuzungumza naye muda si mrefu. Tukaweka mipango mizuri tu. Tena nikamsifia maana nilimtuma usiku, nikashangaa alfajiri anaamka na kujiandaa kabla ya mwanae, kisha akamuamsha Jeremy na kumtaarisha akaniambia anampeleka mwenyewe shule, ili waongee njiani. Kisha anakwenda nilikomtuma usiku. Kuja kupata simu eti yupo chumba cha upasuaji, nikajua mwanangu amekufa. Ndio alikuwa kama anamuaga Jeremy. Mengi yakapita kichwani vile alivyokuwa asubuhi, basi mimi moja kwa moja nikajua atakuwa alikuwa akituaga.” Wakacheka.

    “Kwema lakini?” Akashangaa wanaangaliana na James. “Jema ni mjamzito.” Akajibu James na kumfanya mpaka Jelini afungue macho. “Hongera Jema.” Jelini akafungua macho. “Asante. Nimefurahi mama!” “Hongera sana. Basi sisi tukawa tunakusema na Jelini. Mbona Jema asiyependa unene, haishi kutafuna!” Wakacheka sana. “Nakula mama, halafu sishibi mpaka tumekubaliana  na James niongeze matunda zaidi maana nitapasuka.” “Hongera sana. Ila usiwe na wasiwasi na mwili sasahivi.” “Jema na unene huyo, huna utakalomwambia.” Jelini akaongeza. Wakacheka.

     “Sasa kwa nini hospitalini?” “Tulikwenda kwa kliniki tu. Safari hii na mimi nilitaka kuwepo maana mara ya kwanza nilishindwa kwenda. Akaenda peke yake. Lakini nimefurahi kila kitu kipo sawa. Nimemuona na mtoto wangu. Mapigo ya moyo ya nguvu.” James akaongea kwa furaha. “Hongereni sana James.” Jelini akasikia sauti ya Zenda. “Zenda! Kumbe bado upo?!” “Nipo, siwezi kuondoka na kukuacha hapa.” “Mbona sasa upo kimya? Njoo.” Jelini akamuita kwa upendo. “Pole sana.” Akajisogeza mpaka pale kitandani. “Acha kuongea kwa huruma bwana! Mimi nitapona tu. Njoo na unishike mkono.” Akajisogeza karibu maana alikuwa akihofia ndugu wa Jelini.

    “Basi sisi tuende, tutarudi baadaye.” “Tafadhalini msiwe na wasiwasi. Nitakuwa naye hapa.” Pakazuka ukimya kidogo. “Kukiwa na chochote nitawajulisha kwa haraka kama nilivyofanya leo. Vinginevyo msiwe na wasiwasi kabisa. Jelini atakuwa sawa. Na nitahakikisha wanamuangalia kwa karibu.” “Sawa. Ila usijisikie ni lazima. Mimi naweza kuja wakati wowote endapo itakulazimu kuondoka.” “Hata kama nikutoka itakuwa kwa muda mfupi, kisha nitarudi. Asubuhi mama akirudi, mimi nitatoka kidogo na kurudi wakati mama anatoka, ili tusimuache Jelini peke yake.” Wakakubalina. Wakatoka wakimuacha Jelini alale.

Uongo Hujitenga Na Ukweli, Ni Muda Tu.

    “Pole Jelini wangu.” Jelini akafungua macho akamuona anaanza kulia. “Naomba usilie mpenzi wangu, utapona.” “Lakini mtoto wako angeniua, tena bila kosa, Zenda!” Akashituka sana, hakujua kama anajua kilichotokea. “Kemi? Alifanyaje?” Akauliza kwa shauku akijua ukweli utagundulika sasa. “Alinitega makusudi kwa mguu. Ndio nikajikwaa. Tena baada ya kuniparamia kwa maneno mabaya. Nilipoona hanyamazi na pale ni kwao..” “Pale si kwao. Ile ni kampuni yangu mimi, aliyoikuta hapa duniani. Ehe?” Akaongea kwa jazba.

    “Mimi sikutaka ugomvi maana niliona ananidhalilisha bila sababu. Nikasema niondoke tu. Ndio wakati nampita maana alinisimamia mbele ya kiti nilichokuwa nimekaribishwa, ndio akanitega kwa mguu nikaanguka. Ila usimwambie mama. Mama yangu atamfunga au kumlipiza kisasi kibaya sana kama alichomlipiza aliyekuwa mchumba wa Jema, akamdhulumu Jema nyumba. Ila Jema hajui kama mama amemlipiza kisasi. Mama hapendi mtu atuonee. Ndio maana mimi nimemwambia nilijikwaa na kuanguka tu.” Mwili mzima wa Zenda ukajawa hofu na hasira. Jambo hilo likija kugundulika, mwanae yupo matatizoni hata kisheria. Na nishitaka baya sana hata kwa kampuni.

    “Samahani sana Jelini.” “Wewe hujakosea Zenda. Usijisikie vibaya.” Akamfuta machozi kwa tahadhari asimtoneshe. “Hapana. Mimi ndiye niliyekuita bila kuandaa mazingira mazuri kwako. Najihisi nimehusika. Nisamehe mpenzi wangu.” “Basi ni busu ndio nitakusamehe. Umeingiwa hofu mpaka nimekuona!” Japokuwa alishahisi Kemi anahusika, lakini hakujua kama amefanya kwa ukatili wa hali ya juu kwa kiasi hicho! Akaumia sana. Akainama na kuanza kupata denda taratibu. “Unanuka damu Zenda!” “Ni zako hizi. Nilishituka Jeilini. Sijawahi ogopa hivi maishani.” Machozi yakaanza kumtoka.

    “Nilitoka ofisini nikihofia isije kuwa ile kelele ni ya Sesi kuomba msaada kuhusu wewe! Mbaya nimetoka, nimekukuta umelalia dimbwi la damu! Kukunyanyua, damu zinatoka kama mvua! Niliogopa sana.” “Pole mpenzi wangu. Itakuwa nilijigonga vibaya. Lakini usijejisahau ukaropoka hili kwa mama Jema. Hutampenda.” “Nashukuru kujali.” Jelini akafunga macho, hapohapo akapotelea usingizini.

Ubaya Hauna Kwao.

    Alipojiridhisha amelala akatoka barazani upande wa bahari kwenye hicho chumba alicholazwa Jelini. Moja kwa moja akajua ni kazi ya Kevin mtu anayejua kucheza na mitandao. Mwanae alisomea kilekile alichosomea James, lakini yeye alijiongeza zaidi. Kwahiyo Kevina akishika kompyuta, anaweza kufanya chochote kitokee. Akaanza kwake.

Alimpigia simu ikaita mara moja tu. “Kwa kumsaidia Kemi kufuta ile video, unajua kama umeshiriki kwenye kusudio la kutaka kuua?” Mzee akatumia akili na kuruka moja kwa moja kwenye tuhuma. “Kemi hakuniambia ni video ya nini baba. Ila alitaka nimuelekeze jinsi ya kuitoa kwenye system, na isionekane kama hata ilishawahi kutokea.” Akawa amethibitisha maneno ya Jelini. Kevin ameshatoa ukiri. “Nilikwambia nini juu ya kufanya jambo bila kuuliza au kufikiria? Ni mara ngapi unataka nikwambie ili ujifunze?” Mzee akawaka. “Baba unanionea bure. Kemi alinipigia simu akisema ni msaada anaoomba wa kiofisi kwa kuwa timu yenu ya IT imekwama na si mara moja kupata simu za aina hiyo baba yangu. Huwa nawasaidia tu.” “Ulishawahi kupigiwa simu kuomba alichokuomba leo Kemi?” Kimya.

    “Kevin?” Aliita kwa ukali sana. “Nakusikiliza baba.” “Kwa akili yako ilivyo, hapo ulipokaa, wewe unafikiri kukata video ya matukio yaliyokuwa yakiendelea ofisini, hazikuwa sababu za kiusalama kweli, na Kemi asingejihusisha kwa sababu hausiki, pengine Gele ndio angekupigia?” “Alisikika na haraka baba, nikakosa muda wa kufikiria.” Simu ikakatwa. Kwa hakika Kevin alijua yupo matatizoni.

Taka Cha Mvunguni.

Pesa Ya Bure Tamu.

    Akajua kwa hakika matokea ya alichokifanya, hatayapenda kabisa. Mbali ya kuwa ni baba yao, lakini pia ni kama kitega uchumi chao. Lazima kujirudi kwa haraka. Tena kujirudi kwa uhakika. Akafikiria chakufanya kisha akampigia simu baba yake kwa haraka sana. Haikupokelewa. Akamtumia ujumbe. ‘Kama ukiidhinisha kuruhusiwa nikaingia kwenye chumba kinachotunzwa rikodi zote, nina uwezo wakurudisha ile video.’ Zenda akasoma huo ujumbe na kujibu. ‘Kemi asijue kabisa. Na ninataka iwe kwenye simu yangu pia.’ ‘Sawa baba. Ila mimi sijashiriki chochote na ninaweza kwenda baada ya kazi, wafanyakazi wote wakiwa wameshaondoka.’ Hakujibiwa, kwa hiyo akajua ndio ameambiwa aende.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Akampigia simu kiongozi wa kitengo cha IT. Akapokea kwa haraka. “Kevin atakuja baada ya kazi, kujaribu kupata hiyo video iliyofutwa. Tafadhali mtu yeyote asijue kinachoendelea. Ibaki kwako tu.” “Sawa. Nitamsubiri mimi mwenyewe.” Akakata simu na kurudi ndani. Jelini alikuwa amelala, hana habari. Zenda akakaa hapo akiwaza.

    Madaktari walikuwa wakiingia na kutoka wakipokezana hapo alipolazwa Jelini ilimradi tu, huduma kwa daraja la kwanza chochote kisiharibike. Akaongezewa tena damu, Jelini akawa amelala tu. Akiwa amepotelea mawazoni, peke yake ndani ya chumba hicho mwanga hafifu mida ya saa moja na nusu usiku ujumbe ukaingia. Akachukua simu. Akakuta video.

    Wakati anataka kufungua hiyo video aangalie, Jema akaingia. “Nimekuja kukaa naye kwa muda, ili na wewe ukaoge na kubadili nguo.” “Nashukuru Jema. Sitakawia kurudi.” “Mimi naweza kukaa hapa mpaka kwenye saa nne. Kwa hiyo fanya mambo yako taratibu.” “Sawa. Ila anaendelea vizuri. Wamemuongezea damu ndio inakwenda taratibu.” “Maumivu ya kichwa?” “Hajalalamika tena. Wanajitahidi yasirudi na nafikiri wanampa dawa kali kidogo ndio maana analala sana. Usiwe na wasiwasi.” “Nashukuru.” Jema akatafuta sehemu akakaa, macho kwa mdogo wake, Zenda akatoka kama akimbie.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment