Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 20. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 20.

Ilikuwa mida ya saa tatu asubuhi wakati simu ya Zenda ilipoingia kwa Jelini. “Upo wapi! Mbona mapigo ya moyo yameanza kwenda visivyo?” “Huibiwi. Usiwe na wasiwasi. Tena weka video uone jinsi nilivyopendeza mwenzio.” “Jelini wewe unataka kunichanganya bwana! Unapendeza asubuhi hii unakwenda wapi?” Jelini hana mbavu. “Nilitumwa na mama kufuatilia mambo ya biashara mpya tunayotaka kuanzisha. Kuna dada anasaluni anapamba sana maharusi, sasa alitaka nimdodose anapata wapi vipodozi vyake vya maharusi ili sisi tuanze kuingiza mjini. Tumepata sehemu kubwa.” “Hapo mnafanya jambo zuri.” “Hamisha sasa video unione.” Mzee akachangamkia.

“Jelini umependeza! Ukiambiwa nakula tu kwa macho!” “Tena chupi niliyovaa hapa, ni kuitoa tu kwa kidole, kila kitu chako.” Hali ikawa ishakuwa mbaya. “Kwamba hata sasahivi naweza kupata?” “Wewe tu na muda wako.” “Acha masihara Jelini!” “Nihivyo upo ofisini na sipafahamu na wewe ni bosi. Ingekuwa vinginevyo ningekuja kukuinamia mezani. Ukitosheka mimi nakuacha ufanye kazi.” “Kwamba unaweza kuja hapahapa ofisini!?” “Ila uache mabao yako ya kelele.” Zenda alicheka sana. “Wewe mtoto mtamu sana bwana!” “Nakuja kukurekebishia chapuchapu.” “Nakushukuru. Njoo.” Jelini akashangaa ule utayari.

“Sasa huofii macho ya wafanyakazi wako na Kemi?” “Wapo mjini kwa jasho langu. Waache upuuzi na kuninyima starehe. Njoo Jelini wangu. Tena naweka mazingira ya lisaa zima nisisumbuliwe.” Akamuelekeza Jelini akicheka hana mbavu. Ila akampigia simu mama yake, akampa majibu mazuri, mama yake akaridhika. Akamwambia anakwenda kumuona Zenda, atamtafuta baadaye. Mama Jema hakuwa na shida. Bora sio kumsaliti Zenda maana huo ndio ulikuwa wasiwasi wake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ukweli Jelini alipendeza haswa, mwili wake mzima ulitangaza utajiri wa Zenda, ungependa kumuangalia. Aliacha harufu nzuri kila alipopita mpaka akafika kwenye jengo zilipo ofisi za Zenda. Askari aliyemkuta chini akamuandikisha jina lake, na muda alioingia kwenye hicho kitabu cha wageni alichokikuta hapo mapokezi na kumuelekeza zilipo lifti, akapanda. Yeye mwenyewe akaanza kujiona kipanzi jinsi madhari ilivyokuwa. Ofisi ilikuwa safi, kila mtu anayo suti na tai, wanawake ndio utafikiri ni watangaza bidhaa za urembo. Safi kiofisi. Na hakuwepo mshangaaji hapo anayezagaa hovyo. Akaanza kubabaika. “Inamaana wote hawa wamesoma!” Akaanza kujishuku na kujihisi hayupo sehemu sahihi. Hayo mazingira yalimkalia tofauti haswa. Jelini mtoto wa mtaani, hakuwahi kuingia maofisini! Anatafuta nini?

    Akamsogelea sekretari, akajitambulisha kwa jina la Jelini tu. Akawa na taarifa zake tayari kama aliyekuwa akisubiriwa. Akamwambia asubiri kidogo tu, mzee anamalizia kikao na viongozi wa hapo. Akakaa na kutulia. Akaona mlango wenye warembo wawili nje, kama na wao ni masekretari wa hiyo ofisi hapo ndani, unafunguliwa. Akaanza kutoka mwanaume mtanashati haswa. Alionekana amejaa mamlaka. Akatoka na Kemi na sura yake ambayo haijuilikani kama amefurahi, au amekasirika.

Shari Imfuatayo Mtu, Bila kujua.

    Alipomuona Jelini akapandwa na kitu rohoni. “Wewe mtoto unafanya nini hapa?” “Mimi nimemfuata Zenda.” Akajibu Jelini bila hofu. “Hizi ofisi wanakuja watu wenye elimu zao.” “Mimi sijajakuomba kazi. Nimemfuata Zenda.” Akarudia Jelini. “Sasa kama unafikiri utamdanganya ili akupe kazi hapa, ujue utakumbana na mimi na nitakutaka vyeti na ufanye kazi kama kawaida. Usilete uswahili.” Akamsogelea karibu kabisa akimtisha. “Mbona wewe una mambo ya ajabu hivyo! Ukoje wewe? Yaani unanikuta tu hapa na kuanza kuniparamia, wewe vipi!?” “Acha uswahili kwenye maofisi ya watu.” “Mimi sipendi ugomvi na mtu. Na kwa sababu nimekukuta, acha mimi ndio niondoke.” Jelini akasimama, ile anampita tu, akamtega na mguu makusudi.

    Jelini alinguka vibaya sana, akagonga uso kwenye kona ya meza ya kioo nzuri sana iliyokuwa mahususi kwa magazeti kwa wageni wao wakiwa wanasubiria kuingia maofisini.

Kilichoonekana hapo ni damu kuruka kama bomba, akapiga kelele kidogo, akazima. Sekretari akawa anapiga kelele akiomba msaada, Kemi akakimbilia ofisini kwake. Kila mtu ndani ya hiyo ofisi mpaka Zenda wakatoka maofisini kwao kufuata kelele ya sekretari wa mapokezi.

    Wakakuta mrembo amelala fudifudi uso kwenye dimbwi la damu kila mtu akashituka sana. Kwa haraka sana Zenda akakimbilia pale na suti yake nyeusi na shati jeupee, akamnyanyua huku akiamuru gari ya hospitalini iitwe.

    Kumgeuza hivi, uso mzima wa Zenda ukarushiwa damu kutoka kwenye kipanda uso cha Jelini aliyekuwa amezimia, hajitambui. Shati lake jeupe ndani likawa damu tupu. Akamfunika pale panapotoa damu kama bomba, kwa kuminya na mikono yake miwili. “Nataka taulo safi kutoka chooni kwangu.” Akaamuru. Sekretari akakimbia na kwenda kumletea. Akatoa mkono mmoja na kuweka taulo kwa zamu. Akafunga kwa nguvu kuzunguka kichwa, damu ikakata, akakaa kabisa pale chini kwenye damu, na kumuegemeza kichwa chake kifuani kama kufanya kichwa kusimama kidogo. Kila mtu akabaki akimwangalia jinsi anavyomfanyia huyo binti tena kwa makini, wasielewe.

    Askari walishafika. “Kuna nini?” Askari mmoja wao kama kiongozi wa ulinzi akahoji. “Nafikiri hajazoea kuvaa viatu virefu, amejikwaa wakati anatembea, akaanguka na kujigonga kwenye meza. Ameumia usoni.” Akadakia Kemi kwa haraka akiwa mlangoni mwa ofisi yake. Wote wakamgeukia yeye. Zenda kimya akijaribu kumshika Jelini vizuri. “Hata Selina alimuona.” Akaongeza msisitizo kama anayetaka atetewe na huyo Selina ambaye ni sekretari aliyempokea Jelini na kumwambia asubiri mpaka alipotokea Kemi na kuanza kumbwatukia, ndipo akaamua kuondoka na kumsababishia yote hayo.

    “Gari ya wagonjwa imefikia wapi?” Akauliza Zenda kwa ukali. “Nahitaji gari ya wagonjwa sasahivi.” Zikaanza simu kila mtu akitafuta msaada, mzee amelowa damu chapachapa. Baada ya muda lifti ikafunguka na kitanda cha wagonjwa kikaingia hapo. Wakawapisha mpaka wakafika pale alipokaa Zenda akiwa amemshikilia Jelini. “Anavuja sana damu. Nikitoa hili taulo nililomfunga kichwani, damu zitaruka kila mahali. Na amepoteza fahamu.” Wakaweka umakini kumtoa mikononi kwa Zenda bila kusababisha kupoteza damu zaidi. Wakajaribu kumuamsha huku wakimuweka sawa. “Anaonekana amepoteza damu nyingi sana kwa wakati mmoja.” Wakatoka kwa haraka Zenda akifuata nyuma kwa haraka akiwa  na mkoba waJelini.

 

Hakuna Ajuaye Kesho wala baadaye yake.

    Jelini alifikishwa hospitalini na kuingizwa chumba cha upasuaji kwani taarifa zake zilishafika kabla yao kufika kuwa amepasuka sana kwenye paji la uso. Wakati yupo ndani  chumba cha upasuaji Zenda amekaa akisubiri ndio akili ikamjia, Jelini ni binti wa mtu na alimwambia alitumwa na mama yake. Akatoa simu ya Jelini ili ampigie simu mama yake amtaarifu habari za Jelini. Lakini simu yake ikawa imefungwa. Inafunguliwa kwa macho ya Jelini au namba ya siri. Akakwama maana hakuwahi hata kumuona mama yake Jelini na hakuwa na namba zake. Ila wazo likamjia ajaribu namba ya siri. Akazungusha ‘Jeremy’ kwa kuunganisha herufi, ikakataa. Akashangaa sana. “Sasa kama sio mtoto wake, itakuwa nini?” Akawaza.

    Ndipo wazo likamjia ajaribu ‘Zenda’ huku akijicheka kwa kujidharau. “Aniweke mimi kama namba yake ya siri!” Akajikebehi huku akiweka ‘Zenda’. Akashangaa imefunguka. Alishituka mpaka akasimama. “Yaani mimi ndio namba yake ya siri!?” Alijiuliza kwa mshangao akijisikia kumpenda zaidi Jelini. Akafungua na kutafuta namba. Alipoona tu mama Jema, akajua ndio mama yake. Akampigia.

    “We Jelini?” “Mimi ni Kasa, lakini Jelini ananiita Zenda.” Pakazuka ukimya. Alitegemea na kuzoea. Watu wanaomjua yeye, wakimsikia kwenye simu hupatwa na mshituko. “Nimepiga na taarifa zisizo nzuri lakini tafadhali usiogope. Jelini ameanguka vibaya sana na amepasuka akiwa anasubiria kuniona. Sasahivi tupo hapa hospitalini yupo chumba cha upasuaji, anashonywa. Naweza kukutumia dereva aje kukuchukua kukuleta.” “Yesu!” Alisikika mama Jema. “Pole sana.” “Ni wapi?” Akamtajia hospitali waliyokuwepo. “Siwezi kusubiria huo usafiri. Nakuja.” Simu ikakatwa.

Kwa mara ya kwanza mama Jema akalia kwa hofu kubwa na ya ajabu ambayo haijawahi kumpata kabla. Watoto wenyewe wawili tu! Akampigia simu Jema akilia sana. Jema akashituka na kumwambia walikuwa hospitalini na James, wanakwenda hapo. Baada ya muda mfupi Zenda akashitukia anasimamiwa na hao watu watatu aliowatisha sana. “Yaani hiyo yote ni damu ya Jelini jamani!?” Ndipo akajitazama. Ameloa chapachapa. “Sasa yeye atakuwa amebakiwa na damu kweli?” Mama yake akauliza kwa wasiwasi akiendelea kulia. “Kwani ilikuaje?!” Jema akamuuliza kwa wasiwasi zaidi.

    “Mimi nilikuwa nikimalizia kikao cha mwisho, ndipo niliposikia kelele sekretari akiomba msaada. Nilitoka kwa kukimbia nikihofia asijekuwa Jelini maana nilikuwa nikimtegemea. Ndipo nikamkuta ameanguka. Inavyoonekana aliangukia meza ya kioo iliyompasua sehemu ya kipanda uso. Ila nataka kuwahakikishia, yupo na wataalamu wazuri sana, kuhakikisha anatoka salama. Naomba tutulie.” Kimya. Lakini swali la Jema likamfanya Zenda afikirie zaidi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Alimpigia sekretari wake na kumuagiza amwambie Sesi msichana wa mapokezi kuwa anatarajia mgeni. Akifika Jelini, akaribishwe na ataarifiwe yeye moja kwa moja, wakati akimalizia kikao. Zenda akakumbuka kupokea simu kutoka kwa Sesi kuwa Jelini amefika. Kidogo akapatwa wasiwasi alipokumbuka maelezo ya Kemi. Wasiwasi ukamzidia moyoni. Zenda anaakili ya kufikiria sana na ndio chanzo cha utajiri wake. Maana Kemi alikuwa kama akijitetea japo hakumkuta eneo la tukio. “Kama hakuwa pale, alijuaje kama Jelini alivaa viatu virefu vilivyomsababisha kuanguka!” Akawaza Zenda.

    “Kwa nini alizungumza vile akitaka na ushahidi na wa Sesi?” Akazidi kuwaza kadiri sauti ya Kemi ilivyokuwa ikijirudia kichwani mwake. Hofu ya isijekuwa binti yake ndiye amesababisha hiyo ajali ikaanza kumnyemelea! Kwanza tayari amehatarisha maisha ya Jelini. Pili ameshaingiza doa ofisi yake na kampuni kwa jumla. Mambo yanasambaa. Itajulikana ajali mbaya iliyompata Jelini ndani ya ofisi yake! Akabaki ameinama kimya lakini mengi yakiendelea kichwani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    “Pengine ungeenda kutoa hizo nguo na kujisafisha.” Zenda akamtizama James kama ambaye hajamuelewa. Maana alimtoa katikati ya dimbwi la mawazo. “Umejaa damu mpaka usoni, mikononi kila mahali. Pengine ungeenda kujisafisha na kubadili nguo.” Akajiangalia vizuri mpaka mikono ilikuwa imejaa damu. “Siwezi kuondoka hapa kabla sijamuona Jelini. Hawezi akatoka asinikute mimi hapa.” Wote wakabaki wakimwangalia. “Basi nashauri angalau ukaoshe uso na mikono. Inatisha na kuogopesha.” Zenda akasimama kwenda kutafuta choo cha kiume.

    Baada ya muda wakamuona anatoka akiwa kweli ameosha uso na mikono, ila hakurudi pale akawa kama anaelekea nje ya hilo jengo la upasuaji. Alikwenda kwenye gari kutoa nguo za juu. Koti la suti na shati la ndani lililokuwa limejaa damu. Huwa nyuma ya gari yake hutembea na nguo za akiba. Akavaa tu shati jeupe bila tai, akafungua vifungo viwili vya juu, akakunja mikono. Mzee akabadilika akawa vizuri.

Ujanja Kuwahi!

    Akiwa kwenye gari yake akampigia simu kiongozi wa kitengo cha IT kwenye kampuni yake. “Henry, sitaki uzue wasiwasi hapo. Lakini nataka uvute kamera zote. Kila kona, unitunzie video kuanzia Jelini anaingia mlangoni kule chini, anapokelewa na askari pale chini mapokezi, kuletwa na lifti mpaka juu, na mpaka kufikia vile wote tulivyomkuta sakafuni. Isikosekane hata sekunde ya yeye alipokuwepo kwenye jengo langu. Na nataka ufunge chumba kinachohifadhi hizo kumbukumbu.” “Nina habari mbaya kidogo mzee wangu. Askari walirudi hapa na kutaka kitu kama hicho ulichoniagiza wewe sasahivi hapa. Wakitaka kuweka kwenye ripoti yao kujua kwa hakika kilichoendelea wakiwa wameshachukua mazungumzo ya Sesilia. Walipowaleta kwangu niliwakatalia, kwa kuwa kisheria nilijua nipo sahihi lakini pia nilitaka tuzungumze na wewe kwanza. Kwa hiyo niliwajibu tu kwa haraka kuwa wewe haupo na hatuwezi kufanya chochote mpaka utoe idhini.” Zenda kimya akitaka kujua hiyo habari mbaya, maana mpaka hapo hiyo ni habari njema.

    “Walipotoka mimi mwenyewe nikaenda kuangalia kama ulichosema, nilishangazwa kukuta kamera zote zinafanya kazi, lakini hakuna rikodi ya huyo msichana kuwepo kwenye hili jengo kabisa.” “Sijaelewa!” Zenda akahamaki kidogo. “Hakuna kumbukumbu zake kwenye kamera. Yaani muda yeye anaingia kwenye hili jengo haonekaniki kabisa. Hamna.” “Kwamba imefutwa!?” “Kwa uzoefu wangu, kuna mtu anayejua nini anafanya, amefuta kabisa. Ila alichofanya, amerekebisha muda kiasi ya kwamba kama huna uelewa na una haraka ukiangalia kwa haraka huwezi kujua kama hicho kipengele kimekatwa.” Zenda akashituka sana.

    “Haiwezekani! Nani mjinga wa kiasi hicho anayeshindwa kufikiria kwamba huyu binti ameonekanika kuanzia kamera za nje ya jengo, za kampuni ya ulinzi na..” “Si hivyo tu Kiongozi. Hata hili nimemwambia Gelement, ajiandae kisheria. Nikidhani kama anahusika akitaka kuwahi kufunika jambo kuokoa kampuni, maana huyu binti ametolewa hapa na watu wa hospitali, tena na gari la hospitali akionekana wazi amedhurika.” “Kwamba taarifa ya kilichotokea kwake hazipo tu kwetu zipo mpaka hapa hospitalini!” Akaongeza Zenda kwa hasira.

    “Lakini nimekuja kugundua si Gele. Kumbe yeye ni muoga sana wa damu. Ile kumuona vile yule binti, alishituka sana. Anasema alikuwa akitapika muda wote. Hata kufikiria hilo ilikuwa bado. Kwa kifupi si yeye kwamba amefanya kwa ajili ya kutunza sifa ya kampuni. Na aliyefanya anaonekana alifanya haraka, kitaalamu sana, lakini hakufikiria mbali sababu ya haraka.” Simu ikakatwa. Lakini kwa akili yake Zenda ilivyo, akawa ameshajua hiyo ni kazi ya nani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

    Akaamua kurudi ndani maana yote hayo aliyafanya sehemu ya kuegeshea magari. Anarudi ndani akaona Jelini ametolewa ila mama yake analia sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nani Amefuta Kumbukumbu Za Jelini Akiwa Mjengoni?

Je, Ni Kazi Ya Nani Akisaidiwa Na Nani?

Je, Zenda Atafanikiwa Kupata Uthibitisho Wa Kilichotokea? Maana Kwa Sasa Ni Maneno Ya Jelini Against Kemi.

Je, Ukweli Na Uthibitisho Vitaendana Kuhakiki Alichosema Jelini Kupingana Na Alichosema Kemi Tayari Akiweka Ushahidi Wa Sesi?

Zenda Atafanyaje Kabla Na Baada Yakujua Ukweli Juu Ya Binti Yake Kipenzi?

Jelini Amepatwa Na Nini Akiwa Chumba Cha Upasuaji?

Usikose Muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment