“Nipe simu yako.”
Baba yake akamuamuru Kevin, akabaki akimwangalia. “Sitarudia mara mbili, Kevin.
Na unipe ikiwa haina namba ya siri.” Akatoa na kumkabidhi. “Ipo namba ya Colins
humu?” “Huyo atakua nayo.” Ikimaanisha Jelini. “Usinizungushe Kevin. Nataka
namba ya Colins.” “Yaani wewe unamsikiliza huyu mtoto malaya tu? Atakuwa
anakudanganya.” “Kwanza anaonekana ni msichana wa uswahilini tu. Hamna shule
kichwani.” Kemi akaongeza nguvu, baba yao akawatizama wote wawili na kurudisha
macho kwa Kevin, kisha akaanza kupekua namba mpaka akaipata namba ya Colins.
Mzee akaenda hewani
akiwa kwenye spika wote wanasikia. “Kwema Mkuu?”
Sauti nzito, nzuri na tulivu ya kiume ikasikika. Colins akijua anazungumza na
Kevin. “Mimi naitwa Kasa, baba yake Kevin.”
Colins akashituka akanyamaza. Kimya. “Upo Colins?”
“Nipo mzee wangu, shikamoo.” “Marahaba.” Kemi alivyosikia tu hivyo
akajua mzee amekasirika, akawapa vijana wake funguo, watangulie garini.
Wakabaki wao tu.“Unamfahamu Jelini?” Kidogo
pakazuka ukimya. Ila alishazoea. Wengi hufa ngazi wakijua ni yeye ndiye yupo
upande wa pili wa simu. “Colins!?” “Najaribu kufikiria.
Maana Jelini ninayemfahamu ni mdogo wake Jema, mke wa James ambaye nipo naye
ofisi moja. Wanaishi Tegeta. Kama ni huyo, hata Kevy anamfahamu. Kwa haraka
ndiye huyo Jelini ninayeweza kumkumbuka. Sasa sijui kama ndiye huyo
unayemzungumzia wewe mzee wangu?” “Ndiye huyohuyo.” “Basi James atakuwa na
taarifa zake zaidi. Ni mdogo wake Jema. Mimi naweza nisiwe na taarifa zake
zakutosha, maana kama sijakosea binafsi nilikutana naye kama mara tatu hivi. Na
mara zote ilikuwa ni kwenye shuguli za kufanikisha ndoa yao. Jema na James. Otherwise,
naweza nisiwe msaada zaidi. Samahani.” “Haina shida. Nashukuru sana.”
Mzee akakata simu.
Wakashangaa anamgeukia Jelini. “Umeridhika?” “Haaa!” Kemi
akashindwa kujizuia, akashangaa kwa sauti kabisa. “Mimi
sio malaya.” Jelini akaendelea kulia kwa hasira. “Mimi najua. Nimefanya
hivi kwa ajili yako wewe, wala si yangu au mwingine yeyote yule kwa
sababu wote tunajua, Kevin amedanganya kukuchafua tu, sababu ulimkataa.
Na Kemi hayamuhusu kabisa. Nimefanya hili nikitaka wewe uridhike tutoke hapa.
Si tunaweza kuondoka sasa?” Mzee akauliza akibembeleza haswa mpaka kushangaza
wanae kwa kiasi kikubwa mno. Jelini akatingisha kichwa kukubali. Akamkabidhi
Kevin simu yake. “Muwe na jumapili njema.” Wakaondoka na kuwaacha wakishindwa
chakuongea.
Kisasi.
Wakati Jelini
akibembelezwa na Zenda huko kwake, huku mama Jema anafanya yake. Alishakamilisha
upelelezi wake, akahakikishiwa mwanae hana chake tena. Siku hiyo ya jumapili akaenda
kumuacha Jeremy nyumbani kwa mama yake mkubwa, safari ya Kigamboni ikaanza ili
kwenda kulipiza kisasi. Alitulia njiani akijipanga. “Akatafute mwanamke wa
kumzalia mtoto wa kuonea, si wangu.” Akawaza mama Jema kwa jazba.
Alikuwa akijua sehemu
mwanae alipokuwa akijenga na mchumba wa zamani. Temu. “Anataka akaishi kwa
jasho la mwanangu! Hakika labda niwe nimekufa. Sipo hapa duniani ndipo wawaonee
wanangu. Lakini sio nikiwa hai, na nisijue.” Mama akashuka kwenye pantoni,
akaingia kwenye daladala mpaka Mji Mwema. Akaanza kutembea. Palikuwa mbali
kidogo na makazi ya watu. Kiwanja cha bei nafuu. Jema kwa pesa zake za
kuungaunga, akanunua mwishoni, mbali. Kutoka kwenye daladala mpaka hapo ni
mwendo wakutosha tu. Mama hakujali. Akachapa mwendo mpaka akafika.
Akakuta kweli
imeisha. Lakini ipo kama aliyekuwa akijenga, ameishiwa, kwa hiyo imesimama. “Alifikiri
nirahisi. Mshenzi wa tabia.” Akachunguza vizuri, akagundua hakuna mtu
anayeishi hapo. Kumeachwa tu. Hakuna madirisha wala milango. Nyumba zipo mbali
na hapo kwao. Akaridhika.
Akaenda kutafuta baa,
akakaa mpaka giza lilipoingia. Akatoka hapo baa, akajifunika vizuri akaenda
kununua mtungi wa gesi. Akarudi kwenye ile nyumba. Kwa kujificha, akaenda
kufungulia huo mtungi mpaka akaridhika gesi imesambaa. Akatoa huo mtungi na
kwenda kuuacha mbali kidogo na hapo. Akarudi na kumwagia petroli kuanzia ndani
akitengeneza kijimfereji mpaka nje ya mpaka wao kwa nyuma.
Aliporidhika yupo
peke yake kwenye mji huo ambako hakuna makazi ya watu wengi, nyumba nyingi ndio
zinajengwa, giza, akatupia njiti za kiberiti. Moto ukaanza kuwaka ukifuata njia
ya petrol mpaka ndani ilipokutana na gesi. Mama Jema akaondoka kwa haraka na
kwenda kusimama mbali kabisa akiangalia jinsi ile nyumba inavyoshuka chini.
Alishaweka bia zake kichwani, akacheka sana wakati ikishuhudia ile nyumba
ikiteketea. “Mshenzi wa tabia. Akamwambie mama yake amzalie mwanamke wa
kumuonea. Sio mwanangu.” Aliporidhika hata wakisaidia kuzima moto haitaokoa
chochote, akaondoka. “Yeye si mwanaume? Sasa aanze ujenzi na kumaliza. Mjinga
wa tabia.” Huyo akarudi zake kumchukua mjukuu wake, roho kwatu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Asubuhi na mapema
sana kabla mwanae hajaamka, Jelini akawa amerudi nyumbani. Mpaka mama yake
akashangaa. “Kweli umeamua!” Jelini akacheka. “Ndio umedamka hivi!” “Sitaki
mwanangu anione tapeli. Acha nijitahidi mama yangu. Ninapoweza, nisizembee.”
“Sasa njoo nikupe mchapo wa jana.” Wawili hao ni mashoga wa kuendana. Chanda na
pete. Akili zao sawa, na wanapikika chungu kimoja. Hakuna mwenye raha bila
mwenzie. Huna jinsi ukamtenga Jelini na huyo mama yake.
“Haya, umefanya nini
tena? Maana mama Jema, huishiwi vimbwanga!” “Ile nyumba aliyokuwa akijenga Jema
na yule mshenzi.” Jelini akaanza kucheka asijue mwisho wake. “Yule mchaga
mwenzio, ukamuita tapeli mbele yake?” “Basi nimemtenda, hapa roho kwatu.”
“Mama Jema! Umeua?” “Nimtoe duniani kirahisi hivi, aringe? Tubanane hapahapa
duniani aonje joto la jiwe.” Jelini akajiweka sawa, maana alijua kinachokuja si
kidogo.
“Umemfanyaje mama
wewe!?” “Nilikwenda jana, nikaitia kibiriti nyumba yote.” Jelini alibaki mdomo
wazi, macho kayatoa. “Yeye si mwanaume kweli?” “Mama Jema!” “Basi ndio aanze tena
ujenzi, tumuone sasa. Mjinga wa tabia. Mwanaume mzima anataka ajengewe nyumba?
Tena na mwanangu mimi! Asinitanie kabisa. Akamwambie mama yake amzalie mwanamke
wa kumjengea. Sio mimi. Mimi sijasukuma leba kwa ajili ya kumtumikia yeye.”
Jelini akaanza kucheka kama mazuri.
“Tuanze taratibu mama
yangu! Sasa hukuogopa kuua?” “Hakika nilihakikisha hafi, ili aanze kule alipotolewa
na Jema. Yeye si kidume cha kubadili wanawake? Sasa tumuone.” Jelini hana mbavu
kwa cheko. “Na usimwambie Jema, asije akatuombea laana bure!” Jelini akazidi
kucheka mpaka machozi. “Mwenyewe amesema amemuachia Mungu.” “Subutu.
Anamwachia Mungu ndiye aliyeijenga ile nyumba? Ndiye aliyesukuma leba?
Asinitanie mimi.” Jelini hana mbavu, anafuta machozi kama mazuri.
“Basi siku ile
unaambiwa muachie Mungu, nikaona umenyamaza mwenyewe kimya,
nikajua mpo pamoja. Kumbe!” “Pale nilikuwa nikifuatilia kisheria mwenzio.
Nikatafuta wanao elewa mambo hayo, kisheria. Nikauliza maswali yangu yote mpaka
nikaridhika kuwa, kisheria, nyumba ni ya Temu. Hatuna jinsi kuja kuipata tena.
Kwamba Jema kaula wa chuya. Nikamuhurumia mwanangu jinsi anavyojua
kujinyima. Halafu mwanaume mwenyewe alikuwa mshenzi, alimfuata yeye kwa kuwa
alimuona mnyonge, hana baba wakuja kumtetea! Akanitizama hali yangu, akanidharau.
akijua sina nitakachomfanya, ndio akamchagua mwanangu amuonee! Hakika
nilisema sikubali. Hata kama sina mwanaume wa kusema atatetea wanangu, mimi mwenyewe
nitapambana nao. Washenzi kabisa.” Hapo akazungumza kwa kuumia, Jelini
akamuhurumia. “Pole mama yangu.” “Mbona hapa nishapoa. Na nishamsamehe kabisaa.
Na hivi Jema wangu sasa hivi anakula kivulini. Nimemsamehe buree.” Jelini hana
mbavu.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwenye mida ya saa
nne simu yake ikaita. “Zenda!” “Ulirudi kulala?” “Hapana.
Nimefurahi nimerudi Jeremy akiwa bado amelala. Ameamka amenikuta namsubiria. Amefurahi
huyo! Nimemsaidia kujiandaa na kumsubiri mpaka basi la shule lilipokuja akapanda.
Sasa hivi nipo tu.” “Unafanya vizuri.” “Uliamka salama?” “Niliamka na swala la
yule mwalimu.” Jelini akashituka sana. “Hapa
tunapozungumza, ameshakamatwa, yupo chini ya ulinzi.” “Zenda! Ulimpataje?!”
“Niliweka mtu wa kumtafuta maana kumbe alikwenda kusoma. Sasa aliporudi shule
akapelekwa wilaya ya Mkuranga kama afisa elimu huko. Ndio wamempata na
kumkamata.” “Nilijua umesahau!” “Hata kidogo. Lakini ujue utahitajika polisi.
Kwanza kumtambua, pili ambapo ni pagumu kwa ajili ya ushahidi, kumpima Jeremy
DNA yake ili kumfananisha na yeye.” “Mmmh! Hapo hapana Zenda.” Jelini
akakataa.
“Mwanangu
amekua bila mimi. Ndio kama kwa mara ya kwanza naanza naye mahusiano, anaanza
kunizoea, halafu nimuanzishie habari nzito hivyo, kisha kesi zakumpeleka
mahospitalini na mahakamani! Hapana Zenda. Mimi sitaki kumuingiza Jeremy kwenye
hayo mambo.” “Upo sahihi. Nina wazo. Unaweza kumchukua na kwenda naye hospitali
ambayo atakutana na daktari ambaye anajua nini chakufanya, halafu wewe
unamwambia tu unakwenda kuangalia afya yake.” “Jeremy muoga wa hospitali na
sindano kama mimi.” “Hii kesi itachukua muda mrefu sana bila hivyo Jelini
wangu. Tafadhali pata muda wa kufikiria kabla hujakataa kila kitu.” “Sawa. Na
nitazungumza na mama pia. Ila ujue nimefurahi sana kuweza kunijali kwa kiasi
hiki Zenda.”
Jelini akaanza kulia.
“Hata
mama na Jema hawajui kilichokuwa kikiendelea kwenye maisha yangu. Wanachojua ni
umalaya ndio ulinisababisha kushika mimba. Yaani nashindwa hata pakuanzia na
mama ili ajue kinachoendelea sasahivi. Nimefurahi hujanipuuza Zenda. Nimefurahi
umejali mateso yangu ya nyuma.” “Usilie sasa. Ila ujue na wivu
unanisumbu.” Jelini akaanza kucheka. Alitegemea. “Mimi nilijua mapenzi!” “Sipendi mtu ashike vyangu. Tena alikushika bila
ridhaa yako! Hakika hatakaa akatoka jela.” “Basi acha nizungumze na mama.”
Wakaagana na kukata.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jeline akampigia simu
mama yake. “Upo wapi?” “Mtaani. Na hivi umenipa pesa,
nataka tufungue duka kama la Mode, lakini hukuhuku Tegeta. Hapa nahangaikia
fremu, nishaongea na Mode, amesema kupata vipodozi nisiwe na shida, ilimradi
niwe na pesa. Sasa naona mwenzangu akaunti yako haikauki pesa, nimeona bora
niiwekeze.” Jelini akashangaa sana. Maana alimuonyesha tu mama yake pesa
aliyonayo kwenye akaunti, tayari mama yake amefikiria chakufanya! “Mama wewe unaakili jamani! Mwenzio nilikuwa hata sifikirii!”
“Kuna leo na kesho Jelini. Hiyo mipesa inayoingia sasahivi, hujui baadaye
itakuaje. Si bora kuyawekeza tusirudie shida. Au hutaki?”
“Wewe
ukitaka pesa yeyote ile sema. Utachoka mwenyewe.” “Hapana. Nafanya hii ya
vipodozi ila kwa kuwa pesa ipo, nafanya kwa hali ya juu zaidi. Duka kubwa na
bidhaa nzuri zaidi. Wakati tukisubiria hicho kituo cha mafuta.” “Wewe endelea
mama yangu, lakini kuna jambo ninataka kukwambia. Sikuwahi kukwambia kabla.”
“Basi subiri nirudi. Naingia kuzungumza na mtu sasahivi. Tukishawekana sawa,
nakuja kukupa hesabu.” “Uwe unaniita mama yangu na mimi unichangamshe!” “Kama
unataka hivyo bosi wangu, ndio furaha yangu. Wawili ni wawili tu Jelini
mwanangu. Halafu kuna leo na kesho. Hujui…” “Naomba usiniambie habari za kufa
kwako.”
Akakata simu hapohapo. Hilo Jelini hakutakaga kufikiria kana kwamba walishazungumza
na Mungu kuwa mama yake ataishi milele.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akampigia simu Jema. “Njooni kwetu leo kwa chakula cha usiku. Kuna jambo zito
nataka kuwaambia nyinyi ndugu zangu.” “Unamaana na James?” “Sasa si ndio
mwanaume pekee kwenye familia yetu!” Hilo likamfurahisha sana Jema. “Mimi sina vikwazo. Baada ya kazi nipo huru, James ndio
inabidi kumpanga mapema. Ila kwa kuwa umewahi kuniambia mapema, nitamuomba
asikose.” Jelini akashukuru na kukata, akaamua kumfuata mama yake aone
mwanamke wa kichaga anavyohangaika.
Mama yake akafurahi
sana kumuona Jelini anajichanganya na kutaka kujifunza. “Kuna jambo nataka
kuwaambia. Wewe, Jema na shem. Nitawaandalia na chakula cha usiku, nimewaomba
waje.” “Mbona unanitisha?” Akanyamaza. Wakazunguka na mama yake mpaka
wakafanikiwa. Ndipo wakarudi nyumbani kwa matayarisho ya chakula cha jioni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika mida ya saa
moja Jema na James wakawa wanaingia. “Mama, nyumba imependeza!” “Asante.”
Karibuni ndani. Jema akawa anashangaa kwao. “Hivi tulipanga tuje kuwaona
weekend hii. Tumerudi na mambo mengi!” “Wala usijali.” “Jema umependeza!”
Jelini akamsifia dada yake. “Nashukuru. Mimi njaa inaniuma. Nakula kama mchwa.”
Akasogea mezani. “Njoo James tukae hapahapa tule huku tukizungumza.”
Akajikaribisha. “Husubiri kukaribishwa!?” James akashangaa. “Hapa!? Hata
kidogo. Njoo bwana James.” “Hapa nyumbani James mwanangu. Njoo tu tuzungumzie
hapa. Naona Jema amegoma kusubiri.” Wakahamia mezani.
“Haya Jelini,
yang’aze.” Jema akasema macho kwenye vyakula akitayarisha sahani ya mumewe.
“Kipindi kile nipo shule, mimi nilikuwa na marafiki wa kiume kama washikaji tu
lakini si wapenzi.” Akaanza Jelini nakufanya Jema atulie maana alijua tu
anataka kuja kuombwa hela. “Nilipokuwa nakaribia kumaliza, akahamia mwalimu
mmoja hivi. Kijana tu. Akawa anatufundisha somo la hesabu. Akaanza kunituma
hiki na kile. Wale washikaji zangu wakawa kama wanatania kumwambia yule mwalimu,
Jelini sio monita. Ili asizidi kunituma. Akawa anazidi kunituma kisha ananifuata
kama ni ofisini na yeye anakuja. Alipoonyesha nia ya mapenzi na mimi nikamjua
tokea mwanzo, nikamuonyesha wazi simtaki. Akaanza kuwa mkali na katili kwangu,
ananichapa bila kosa, na kunisingizia mambo kwa walimu wengine, nikaanza
kuchukiwa na walimu wote pale shuleni.” Wote kimya.
“Akanihamisha siti pale
nilipokua nikikaa na wenzangu, akanisingizia nawaigilizia. Akasema kwa walimu
wote eti mimi naigilizia. Ikawa shida kila siku mimi nachapwa msitarini. Siku
moja akaniita akanimbia yeye ana uwezo wakubadili maisha yangu yakawa mabaya
zaidi ya hivyo. Ataua ndugu zangu wote. Hapo ananitisha mimi nishachoka.
Akanituma kwake. Ile nimefika tu kwake na yeye akaja. Akanibaka kisha akasema
nisithubutu kusema, lasivyo atanidhuru mimi na familia yangu na kusambaza picha
ambazo alisema alirikodi kamera inipige wakati nipo kwake.” Mama Jema aliumia
sana.
“Basi nikawa na kazi
ya kwenda kwake, ananifanya atakacho. Akinituma kwake ili na yeye aje
nikikataa, ananionyesha picha zangu za uchi alizonipiga anasema nisipoenda
atazisambaza kwa kila mwanafunzi na atanichinja kisha kuja kuchinja ndugu zangu
wote. Nikawa naogopa, nafanya kila kitu anachotaka mpaka nikashika mimba ya
Jeremy. Nikamwambia. Bwana alinipiga yule kaka, nakumbuka alinigonga,
nikapoteza fahamu, nikaja kuzinduka ananimwagia maji. Nilipozinduka tu akanitoa
hapo na kunirudisha mpaka hapo karibu na nyumbani akanionya na kuniambia nikija
kumtaja, kilichonipata kitawapata familia yangu yote. Yaani mama na Jema. Hapo alishajua
sina baba. Basi mimi ndio nikafukuzwa shule. Nipojifungua Jeremy mama alipotaka
nirudi shule, ndio maana nilikataa. Nilijua yale mambo yatarudia tena.” Jema
alilia sana.
“Nikawa siwezi
kulala kwa hofu na uchungu na siwezi kumwambia mtu, naogopa. Siku moja
mama alinituma pale baa kumnunulia mamkubwa bia. Alikuwa amekuja hapa ndio
nikakutana na dada Doro. Sasa sijui tulizungumza nini, tukaanza kucheka mpaka
tukashangaa. Wakati nimepewa na muhudumi hizo bia, maana mimi nilifika nikaka
kwenye meza yake wakati nikisubiria hizo bia. Dada Doro akaniambia nirudi
tupige stori, amependa kampani yangu. Mimi nikarudisha bia hapa, nikatoka
kwenda kwa dada Doro baa. Akaanza kuninunulia bia. Nikamwambia mimi sinywi, bia
chungu. Ndio akaniambia yeye anazinywa sababu ya matokeo yake baada ya pale,
analala na kusahau matatizo yake yote.”
“Basi nikaanza kunywa
na dada Doro. Ikawa inanisaidia sana kulala. Akaanza kuniomba nikalale kwake
eti yupo mpweke. Nikakubali kwa haraka. Akaniambia sasa nyumbani utaagaje? Mimi
nikamwambia kwetu mimi wananijua malaya, hawana shida na nilipo. Basi
maisha yakaendelea kunywa kwa pesa ya dada Doro au Jema kama ananipa. Uzuri
dada Doro anakazi inayomlipa sana na anapenda sana kuvaa. Mwenyewe anasema
hawezi kurudia nguo zadi ya mara mbili. Basi na mimi ndio mtu wake wa karibu,
akawa ananipa mimi nguo zake za zamani. Maisha yakaendelea ila hapo nina hofu
na chuki sana ya wanaume kwa kile nilichofanyiwa. Kundi letu pale baa likakua.
Wale wanapesa, lakini kila walipokuwa wakinitongoza sitaki kabisa. Sitaki
tena.”
“Sasa siku ya
jumapili ile baada ya harusi yenu si nikaamkia sehemu nisipopajua! Sijui
nilifikaje wala pale ni wapi! Nikaamka chumba kizuri na pasafi. Nikaanza
kuangaza macho ikabidi nitoke kutafuta. Jumba zuri kwelikweli. Kuchungulia nje
nikakutana na mwanaume msafi sana. Akaniambia nichukue simu tuzungumze mimi
nikijua yeye mwizi.” “Kwa nini?” “Nilimkuta na yeye ni kama anachungulia ndani
anashindwa kuingia ndio akaja kuniambia sasa kwa simu kuwa hawezi kufungua
nyumba inalindwa na mitambo, lazima kutoa sasa alam.”
“Akanielekeza mpaka
nikaweza kufungua ndio nikatoka sasa. Ananiuliza mimi ni nani, na mimi
namuuliza pale ni kwa nani. Ikabidi kumuelezea mimi nililewa sana.” “Tena sana
Jelini, mpaka ukagawa mtoto!” “Nisameheni jamani. Nimeacha pombe. Muulizeni
mama. Sijanywa tena na nimemuomba Jeremy msamaha. Sikukusudia.”
“Malizia.” “Basi kufupisha habari akatoka Kasa, kumbe alikuwa humohumo ndani
ila amelala chumba kingine na dada Doro, na ndipo nilipojua yule niliyekuwa
nikizungumza naye muda wote ni baba yake.” “Mzee Kasa!?” James akauliza kwa
kuhamaki sana.
“Mimi nilikuwa sijui!
Kwanza hawafanani kabisa.” “Hata sisi tulikuwa tukimwambia Kasa unaweza sema ni
kaka yake. Yule mzee ni mtu wa Burundi. Anasura kama watu wa huko. Halafu
hajafanana kabisa na wanae. Hata huyo Kemi dada yake Kasa, tena bora Kasa, yeye
ndio anasura kama mwanaume tena mweusi tii. Halafu baba yao yupo kama shombe!”
“Ewaaa! Kumbe shemu wewe unawajua vizuri.” “Malizia Jelini.” Mama yake akataka
amalizie. Hapo uchungu umemkamata, kama azae tena.
“Basi mimi
nilivyogundua kuwa yule ndio mzee Kasa mwenyewe maana habari zake
nilishazisikia kuwa ndio chanzo cha kiburi cha mwanae, kwa kuwa huyo mzee
anapesa sana.” “Unapoishia kusema sana, ongeza sana nyingine. Anamigodi
ya madini huko Mwadui. Anamakampuni yake makubwa sana hapa nchini. Na Kasa
anasema ni kichwa chake mwenyewe. Anaakili sana na nidhamu ya kazi. Hata mwanae
wa kike amemwajiri kwenye makampuni yake. Unaambiwa dada anapesa huyo!” “Basi
shemu ameshamaliza.”
“Sasa mimi nikaondoka pale kwa kujinyata maana mzee alikuwa
anamfoka mwanae, kulala hovyo na wanawake. Basi wakati nipo njiani natoka kwao
kwenda kutafuta usafiri akanikuta akasema anipe lifti. Mimi nikamkatalia
nikamwambia sitaki msaada wake asije akanitaka baadaye.” Wote
wakashangaa. “Kweli tena. Nikamwambia mimi kwangu watu wanaanzaga kutaka kunisaidia
mwishoe wanataka kadhalika. Akacheka sana na kuniambia yeye hatanidai
ila pale ni mbali sana na usafiri, ananisogeza. Ndio nikapanda kwenye gari
yake.”
“Akaanza kushangaa nawezaje kuishi maisha kama yale yakulewa
vile mpaka kutojitambua! Akazungumza sana na mimi. Basi akaniambia anirudishe
nyumbani. Nikamkatalia. Nikamwambia itakuwa picha mbaya kwa mama, atajua
nililala kwake. Akashukuru akaona ni kweli. Ila katika mazungumzo yake akaomba
niwe nampa maendeleo ya kubadilika kwangu maana nilimwambia nabadilika. Ila
kufika hapa nyumbani mwanangu kuniambia na nilimgawa, na wewe utamchukua.
Niliumia sana.”
“Mimi jamani nampenda sana mwanangu. Japokuwa sijui
kumtunza, lakini ndio sababu hata kama napapenda kwa dada Doro, huwa narudi
nyumbani ili tu nimuone. Basi nikakaa nikajifikiria, hivi siku kama ile
kuamkia nisipopajua, imetokea mara ngapi! Halafu wale wanaume wote ambao
nawakatalia, nikilewa sijitambui, watakuwa wakiniacha kweli! Nikaingiwa hofu.
Sasa katika mazungumzo Zenda akasema yeye anacho kipimo.” “Zenda ni nani
tena!?” Akawa kashamchanganya Jema.
“Anaitwa Alexender Kasa, ndio mimi nikambatiza jina la Zenda.”
Mama Jema akatingisha kichwa, Jema akashangaa sana. “We Jelini! Huyo baba
tajiri!?” “Mimi nilimwambia atanichanganya. Nimeshamzoea mwanae kuwa ni Kasa,
nikamwambia yeye nitamuita Zenda. Lakini mwenyewe amependa. Basi kufupisha
habari ndio nikakimbilia hospitalini kupima kwa hofu nikidhani watakuwa
wakinifanyia mambo mabaya nikiwa nimelewa maana kumbe nikilewa nakuwa kweli sikumbuki
si matatizo tu, sikumbuki chochote.” “Na mama alikwambia Jelini.” “Sasa wakati
ule nilikuwa sifikirii, Jema.” “Wewe utampoteza. Mwache amalizie.”
“Siwezi mimi…” “Acha maneno mengiii. Wewe endelea.” Jelini
akacheka nakuendelea. “Nilipokuwa hospitalini nikamtumia ujumbe Zenda maana
nilimgombesha na kumkatia simu.” “Jelini!” “Wee mwache wee.” Jema akawa
haamini. James kimya anataka kujua mwisho wake. “Basi nikamwambia Zenda nipo
hospitalini, napima Ukimwi na anisamehe. Akaja kukaa na mimi. Nilikuwa naogopa
maana mama alinipa mwezi. Niwe nimepata kazi na kumletea ada ya mtoto lasivyo
anakupa wewe mwanangu. Akaniambia na pia kama nimeathirika anakupa wewe
mtoto. Sasa mimi hapo nikawa naogopa, sitaki kumpoteza mwanangu. Ndio Zenda
akawa ananipa moyo mpaka majibu yakatoka. Tukatoka naye pale kwenda kula, maana
mwanzo nilimkatalia. Ila kile kitendo cha kuja kukaa na mimi pale mpaka mwisho,
kikanigusa.”
“Basi katika mazungumzo baadaye ndio nikamuuliza mtu kama
mimi naweza kufanya nini maishani. Akanishauri kurudi shule. Mimi nikakataa
kabisa. Nikamwambia shule sitaki kabisa. Ndio baadaye akaunganisha mazungumzo
yangu akajua naogopa sana shule. Halafu akajua nilizaa nikiwa shuleni. Moja kwa
moja akajua nilibakwa, haikuwa hiari yangu. Akaniambia nimsimulie
ilivyokuwa. Nikamsimulia kila kitu.”
“Mimi nikajua amesahau bwana. Leo asubuhi amenipigia simu
akaniambia ameshamkamata yule mwalimu, yupo jela.” “HAIWEZEKANI!” Mama Jema na
Jema wakahamaki kwa pamoja. “Mimi naamini. Jema, mimi nikikwambia mtu anayo pesa,
niamini. Yule mzee anayo pesa ya
kuamuru mambo yatokee, na yakatokea. Mwanae huyo Kevin, anaishi pale
kazini, utafikiri ametuajiri sisi wote na mabosi wetu. Kwa dharau ya pesa ya
baba yake, sema tu ananidhamu ya kazi.” “Ni baba yake ndio anamlazimisha
kazini. Zenda ameniambia amemwambia akifukuzwa pale, ajue na mshahara anaomlipa
unakoma.” “Subiri kwanza Jelini. Kwamba Kasa analipwa na baba yake kufanya kazi
pale?” “Ndiyo. Mbali na mshahara mnaolipwa nyinyi na mwajiri wenu, kila mwezi
Kasa analipwa na baba yake. Na si pesa ndogo. Nyumba zote anazokaa Kasa ni za
baba yake.” “Wewe umejuaje?” Swali la Jema likamfanya Mama yao aanze kucheka huku
akimwangalia Jelini kama anayemwambia umekamatwa.
“Sasa unacheka nini mama?” “Wewe Jema kakuuliza swali, jibu.
Achana na mimi.” “We Jelini?” “Mimi hapa Zenda mpenzi wangu.” Jema na mumewe
wakabaki wametoa macho. “Sasa mnashangaa nini?” “Huyo baba yake Kasa ndio
mpenzi wako!?” “Ndiyo, na tunapenda sana. Kamlipia mwanangu ada ya mpaka darasa
la saba. Hapo Hopac.” “Haaa! Kwamba Jeremy anasoma hapo!” “Zenda huyo. Anasema
pesa ni nyingi lakini elimu nzuri.” “Si nilikwambia yule mzee anapesa? Sasa uamini
anayo pesa haswa.” “Sasa hujaona kituo cha mafuta anachomjengea huyu!
Hutaamini.” “Acha masihara Jelini!” “Bwana mama unanipoteza nilichowaitia.”
Jelini akalalamika.
“Subiri kwanza Jelini. Kwamba na Kevin anajua?” “Bwana
watoto wameumia hao mimi mpaka nikawashangaa! Maana Zenda mwenyewe alitaka
niende nao kanisani. Mimi nikamwambia namuogopa Kasa kwa sababu yeye nilimkataa,
iweje leo anikute na wewe!” “Kwani mwanae pia alikutaka!?” “Kevin alikutaka?”
Jema na mumewe wakafululiza maswali wakiwa bado na mshangao. “Ndiyo. Ila mimi
nilimkataa mapema sana. Alianza kunihonga, nikamwambia mimi sipendi mambo
yakuhongwa halafu aje anitake baadaye. Mimi sitaki. Bwana aliumia huyo!
Sasa sijui hajazoea kuachwa mimi nikamkataa.” “Kasa kwa kupenda ushindani, hapo
ni kwa sababu ulisema Colins ndio mchumba.” “Heee! Kwani ni madogo Shem? Acha
palepale kanisani anisingizie kwa baba yake na mbele ya huyo Kemi na
wanae, eti mimi mwanamke wa Colins. Mimi malaya. Eti nilimtaka, akanikataa.”
“Jelini!” Mpaka mama yake akashituka.
“Kumbe sikukusimulia mama? Bwana mimi nikaanza kulia,
kuongea siwezi. Na Kemi yupo kama anashabikia. Ila sasa Zenda ananipenda sana.
Akaniambia twende. Mimi nikamwambia siondoki pale mpaka ampigie simu
Colins amuulize mbele za wanae. Bwana watoto wanamuogopa Zenda wale! Kama
mungu!” “Si ndiye anayewapa kiburi mjini? Nasikia hata mume wa Kemi ameajiriwa
na baba yao. Ikawaje?” James akataka aendelee.
“Zenda akachukua simu ya mwanae akampigia simu Colins,
Colins akasema yeye ameniona kama mara tatu tu ila wewe ndio unataafa zangu
kamili. Alipomaliza akaniuliza kama nimeridhika. Bwana wanae walikereka.
Akasema yeye alimpigia simu Colins kwa ajili yangu wala si wanae. Akasema kwa
kuwa Kemi hayamuhusu na Kasa anajua ni muongo, analia wivu sababu nilimkataa.”
“Jelini wewe mtoto!” “Mimi mwenzenu nampenda Zenda, kufa na kupona. Nampenda
haswa.” Wote wakabaki wakimwangalia.
“Huna haya na baba anayeweza kukuzaa!” “Bora lipi mama
yangu. Vijana wenye tamaa na kunibaka, au Zenda anayenipenda mimi na mwanangu?
Ananitunza na kunifikiria haswa. Sasa leo ndio alisema ili mashitaka ya yule
mwalimu yaende haraka, lazima kumpima Jeremy na yeye DNA. Mimi nikakataa kesi
kwa manangu. Sitaki mwanangu asimamishwe mahakamani na yule jambazi.
Sitaki apite hapo. Huyu mtoto amelelewa na mama bila shida. Wakianzisha tu kesi
na yeye, watamchanganya mwanangu.” “Lakini huyo mshenzi lazima anyongwe. Huyo
mzee niwakumshukuru.” Mama Jema akaongea kwa jazba. “Naomba usimuite
mpenzi wangu mzee. Anaitwa Zenda, ukitaka wewe muite Kasa.” Jema akaanza
kucheka.
“Usicheke bwana Jema!” “Kwani Jema huyo baba ukimuona
utafikiri kaka yake Kasa!” “Jamani mwanaume mzuri yule! Acha nikuonyeshe picha
zetu tulikwenda kisiwani na bonge ya boti. Na ni yake. Nzuri ndani ipo kama
nyumba!” Akampa simu na kumfungulia. “Haaa!” “Si nilikwambia! Huyo ndiye baba
yake Kasa.” “Au kabambikiziwa watoto!” Jema alimfanya mumewe acheke sana. “Sasa
hujamuona mwanae wa kike.” “Bora Kevin kuliko dada yake. Halafu maringo sasa!”
“Si wanayo pesa!” Akaongeza James.
“Turudi kwa ya leo. Ndio Zenda akatoa wazo kuwa tumuepushe
Jeremy na mahakamani, ila nimpeleke hospitalini kwa daktari ambaye atakuwa
amemuandaa. Amfanyie vipimo tu, halafu basi. Jeremy asionekanike mahakamani
wala polisi. Mimi nikamwambia mwanangu anaogopa sindano.” “Kwa hiyo huyo Zenda
ndiye anayejenga hii nyumba?” “Mwaya Jema!” “Acha nishangae mdogo wangu! Maana
sasahivi ndio nikiangalia hapa ndio naona haya mabadiliko hata ya humu ndani!”
“Nakwambia ndani ya juma moja, kulichimbwa kisima hapa, maji yanatoka mpaka
ndani.” “Mama!” Jema akashangaa. “Mzee anayo pesa si…” “Msimuite mzee.
Ni Zenda.” “Haya, baba anayopesa. Wanaingia watu na kutoka mchana kwa alfajiri.
Ukiingia hapo jikoni kwetu, hutaamini. Ni kama pametengenezwa upyaa. Kila kitu
kipya, mpaka makabati ya ukutani yamejengwa. Friji na majiko vyote vipyaa. Ndani
ya juma moja nyumba imechukua sura yake. Sakafu nafikiri waliitandua na kuweka hizi
marumaru unazoziona hapa nafikiri ndani ya siku tatu walikuwa wamemaliza. Vyumba
ndio vinakarabatiwa mpaka vyoo vinajengwa kila chumba. Uzio wenyewe umejengwa
kwa kushambuliwa kama mchwa!” “Mama!” Jema hakuwa akiamini.
“Nakwambia kila kitu mpaka kiwanja amenunua kwa jina la
Jelini, ujenzi ni hivyo kaniachia mimi nikisimamia ndio naamini ni vya Jelini,
hamdanganyi. Lakini kila kitu kwa jina lake huyu mtoto.” “Ila huyu Jelini,
naamini.” Wakaanza kucheka wakikumbuka mambo ya Jelini aliyokuwa akimfunda Jema
na kumuacha James haelewi. “Hongera mwaya Jelini. Umeuchinja.” “Sasa swala la
yule mwalimu?” James akataka warudi kwenye lamsingi. “Kwanza nasikia
alijiendeleza. Sasa hivi anafanya kazi wilaya ya Mkuranga kama afisa elimu si
mwalimu tena.” “Mshenzi kabisa. Yeye maisha yake yanaendelea halafu yako
aliyakatiza, mimi nitaenda na Jeremy hospitalini. Mwambie amuandae huyo
daktari.” “Mwanangu anaogopa sindano mama.” “Wewe unajua mpaka sasa hivi ameshachomwa
sindani ngapi huyu mtoto?” Kimya.
“Akiumwa unajua huwa anapewa dawa gani?” “Basi mama, ila
mimi najua huwa anaogopa sindano.” Jelini akajibu kwa upole maana kweli huyo
mtoto amekuzwa na mama yake yeye hana taarifa. “Au nyinyi mnasemaje?” Akataka
ushauri wa Jema na mumewe. “Hakika achukuliwe hatua asije umiza watoto
wengine.” James akaongeza. “Na Zenda naye amesema hivyohivyo.” “Jema mke wangu
mbona unaanza kuninyima raha! Macho hayaondoki kwenye hizo
picha!” Jema akashituka, maana alishapotelea kwenye picha, hamalizi! Jelini
alicheka sana. “Naona mwenzangu hamalizi!” “Hizi picha nzuri James bwana, wala
hakuna kingine.” “Mmmh! Mpaka umenisahahu?” “Siwezi mpenzi wangu.” Akarudisha
simu kwa Jelini wakicheka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ni nini Kitaendelea?
Watoto wa Kasa ndio wamemkubali Jelini?
Ticha aliyebaka Mali ya Zenda?
0 Comments:
Post a Comment