Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 18. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 18.

Joshua na mkewe wakarudi ndani na kukuta ile hali pale. Pako kama msibani. Kumepoa. “Tusamehe Joshua mwanangu. Tumewaharibia siku yenu.” Joshua akacheka na kutingisha kichwa. “Huwezi amini mama. Eti hata siku hii ya leo. Muda huu na uliopita, Mungu alijua kabla yetu. Sisi tunatembea hapa kwa mshangao lakini, nothing takes God into surprise.” Joshua akahamia kwenye kinanda chake. Akakiweka sawa.

“Mimi ninapopita kwenye nyakati ambazo zinanifanya nisijue chakufanya. Nafsi na akili yangu ikiwa imegota. Zaidi nikiwa nimesababisha hilo jambo na sijui jinsi ya kujitoa. Huwa najikumbusha huu wimbo, aliuimba mwimbaji mmoja, mtu mzima sasa. Anaitwa Don Moen. Ameuimba huu wimbo katika mafunuo ya ajabu sana. Anasema, ‘God will make a way’. Sikilizeni tu na mruhusu haya maneno yawaingie, kisha nitawaambia kitu.” Wakatulia.

Joshua alianza kupiga hicho kinanda bila kuimba kwa muda tu, mpaka wakaanza kutulia. Alipoanza kuimba sasa,

‘God will make a way, Where there seems to be no way, He works in ways, we cannot see, He will make a way for me. He will be my guide, Hold me closely to His side, With love and strength for each new day,He will make a way, He will make a way.

Kuwa, ‘Mungu atafanya njia, pasipo onekana na njia. Hufanya njia zisizoonekana au kueleweka kwa uelewa wetu. Atafanya njia kwa ajili yangu. Yeye atakuwa kiongozi wangu akinishika karibu yake, kwa upendo na nguvu kila siku, atatengeneza njia. Naye atakuwa baba yangu, ataniweka upande wake. Kwa upendo na nguvu zake kila siku, atanitengenezea njia.’ Yaani mpaka hapo anamalizia kibwagizo tu, akaona sebule nzima imeanza kujiegemeza kwenye makochi vizuri, ile hali ya hofu ikaanza kupungua kwao. Ukweli Joshua alijua kuimba. Na akichanganya na hisia, lazima utatulia tu. Akaimba na beti zake zote. Taratibu tu akiwaangalia mmoja baada ya mwingine mpaka akamaliza.

“Hapo vipi?” Kidogo wakatabasamu. “Eti Nanaa?” Akainama. “Basi akili ikishaelewa si kwa nguvu zangu ila yupo mwenye nguvu ya kufanya makubwa zaidi ya nifikiriavyo, basi huwa sina jinsi zaidi ya kumpa utukufu na heshima. Namuinulia mikono yangu kulisifu jina lake. Namtambua kama yeye ni mkuu. Nautendaji wake wa ajabu, natambua uwepo wake kwa kumwambia, ‘Wewe ni Mkuu. Unatenda maajabu, hakuna kama weweee. Hakuna kama wewe.’ Joshua akaanzia hapo katikati ya wimbo ndipo akaja mwanzo. Jinsi alivyoimba, wakajikuta wote machozi yakiwatoka, mikono juu wakilisifu jina lake kwa kuabudu wakisema, ‘Twakupa utukufu, na heshima, twainua mikono yetu, kulisifu jina lako!’ Wakarudia hapo. Waliimba hapo mpaka machozi. Joshua alipiga kinanda akiimba huo wimbo bila kuchoka mpaka Geb kuja kumaliza, na yeye yupo magotini. Kila mtu amefunguka. Joshua akamsogelea mkewe, akamshika mikono yote miwili, akaanza kumshukuru Mungu. Wote wakamuombea baraka na afya nje kwenye hiyo safari ya kubeba huyo mtoto.

Joshua akatamka baraka kwa James na Jema pia. Akawaombea vizuri tu na kumaliza. “Mimi nimemkosea anko James, anko. Mimi ni mtoto mbaya?” Magesa akaanza baada ya kusikia akiombewa anko James. “Kitendo chakutambua umekosa tu, tayari wewe ni mtoto mnyenyekevu. Lakini umejua ulipokosea?” “Sijamsalimia anti, nikaanza kumuuliza maswali.” “Hayo ni makosa mawili, lakini jingine ni jinsi ulivyomtambua anti. Ulimtambua isivyo sahihi ndio maana anko alikasirika. Mke wake anaitwa  Jema. Wewe utamuitaje?” “Anti Jema.” Akajibu.

“Ewaah! Yeye ni anti Jema.” “Halafu mimi ndiye nilikosa Magesa. Anti hakuwa na shida yakuingia chumbani kwangu. Mimi niliongea maneno mabaya kwake na kumuumiza.” “Pole mami. Usilie. Mimi nitamuomba msamaha anti. Mimi sipendi kumuudhi anko wangu. Najua ananipenda.” “Hapo utakuwa umefanya jambo zuri sana. Lakini wakuanza kumuomba msamaha ni anti Jema. Na mimi nitakupa simu yangu umpigie. Ila acha nikapige simu moja hapo nje, nikirudi ndipo uzungumze na anti Jema.” “Asante anko.” Joshua akasimama na kumbusu Magesa. “Hakika umenifanya nikupende zaidi Magesa. Sikujua kama ndio unahekima hivyo! Wewe utavuta wengi. Na Mungu hupenda wanyenyekevu. Uendelee hivyohivyo.” “Asante.”

“Jamani, kuna simu lazima niipige sasahivi bila kuzembea. Kisha nitarudi tule, ndipo muondoke, baada ya Magesa kuzungumza na anti wake. Wote wakaitika. “Nisindikize hapo barazani Naya.” Naya akamfuata nyuma. “Wakati tukiimba, nimepata ujumbe wa Bale. Sijui ni kwa nini, lakini hauwezi kusubiri. Lazima nizungumze naye sasahivi. Wewe unaweza kunisubiria ndani tu.” Bila ya kuongeza neno, Naya akaondoka. Joshua akamuacha tu.

Nafasi Ya Pili.

Akampigia simu Bale zaidi ya mara mbili akawa hapokei. Mara ya tatu akapokea. “Kwema?” Joshua akaanza, ila akajua alikuwa akilia. “Mungu hajamalizana na wewe Bale. Na upo na deni kubwa sana ambalo mimi sijui jinsi utakavyofanya kulilipa, lakini nilazima kulilipa kabla hujaondoka hapa duniani.” Joshua akaendelea taratibu tu. “Baba yako alikuwa mtumishi aliyekuwa akitumika kanisani. Kwa jinsi nilivyosikia siku ya mazishi yake, walimtegemea kwenye upande wa maombezi, zaidi kutoa mapepo. Wengi walikuwa wakijilaumu kutotambua uwepo wake wakati wa uhai wake, lakini karibu wote walikuwa wakilia na kuulizana ni nani ataziba pengo lake.” Bale alilia sana.

“Zayoni amekufa na mimba changa. Ndoto nyingi sana ambazo alikuwa akitizamia kuzitimiza hapo baadaye. Ndoto zote  hizo ziliungua moto. Ndio Mungu amenituma kukwambia, HAJAMALIZANA na wewe. Hilo ndilo amenituma kukwambia. Mengine ni mimi tu kwa kufikiria kwangu. Utafanyaje, sijui ila naweza kufikiria kwa makubwa Mungu aliyoniamini nayo, hakuniacha peke yangu. Alinipa Roho Mtakatifu akawa msaidizi, ambaye ukweli ni msaada wangu mkubwa sana. Yeye atakufundisha, kukuongoza katika kweli yote mpaka utashangaa jinsi atakavyotenda na kugeuza hiyo hali unayojisikia sasahivi kuwa baraka kama usipokata tamaa na kurudi nyuma.”

“Unakumbuka Paulo alilitenda vibaya sana kanisa? Akiwaua mchana na usiku mpaka akaja kukutana naye? Leo tunafurahia ukuu wa Mungu kwa aliyoyafanya Paulo. Huna jinsi ya kubadilisha nyuma, lakini Mungu wako amenituma kwako usiku wa leo kuwa, bado anayo nafasi yako kwenye ufalme wake. Na kwa jinsi nilivyomfahamu huyu Mungu, si mwanadamu hata aseme uongo. Kwa hiyo kilichobaki ni wewe kuutafuta ufalme wake, mengine yote atayafanya yeye mwenyewe. Usiku mwema.” “Asante sana Joshua.” Wakakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi ndani kwa Magesa. “Upo tayari kuzungumza na anti?” “Asije akaharibu zaidi, Joshua!” Mama G akaingiwa na wasiwasi. “Hapana. Mimi nimeheshimu wazo lake. Magesa anaakili na anahekima. Mwache Mungu amtumie hata kwenye hili.” Geb kimya akijiangalizia tu. Joshua akapiga, Jema alipoona simu ya bosi wake akapokea kwa haraka. “Samahani Jema. Nina mtu ameomba rasmi. Yeye mwenyewe anataka kuzungumza na wewe. Hajatumwa na mtu. Ni akili zake mwenyewe ila hana simu. Tafadhali naomba msikilize tu.” “Sawa.” Jema akakubali. Joshua akampa Magesa simu.

“Mimi naitwa Magesa. Nimekukosea anti, nisamehe.” Ikamgusa kila mtu. “Nimejua makosa yangu. Kwanza sijakusalimia. Halafu nimekutambua vibaya. Wewe ni anti wangu. Na mimi nakupenda. Ila nimekua mtoto mbaya. Nisamehe anti. Nitakuwa nikikusalimia kabla sijaongea chochote. Halafu mama yangu ameniambia yeye ndio alikosea. Alikwambia maneno mabaya. Hutaki kuingia chumbani kwake. Yeye ndio amekosea. Halafu na mimi sikutakiwa kusema hivyo anti. Nisamehe.” “Kumbe Magesa wewe ndio mtoto mzuri hivyo!?” “Hata anko Joshua amesema hivyohivyo.” Ikabidi wote wacheke.

“Ujue anti mimi sipendi kukuudhi?” “Sikujua Magesa!” “Basi mimi hata bibi anasema nina upendo mwingi. Hata wewe nakupenda. Ujue anko James ni anko wangu, na huwa nacheza naye?” “Ameniambia.” Jema akajibu akicheka. “Basi na wewe ni anti wangu. Na ninakupenda anti Jema.” “Asante kwa upendo Magesa. Kweli wewe mtoto mzuri. Yaani mpaka sasahivi hapa, nasikia kupendwa sanaaa.” Acha Magesa aanze kucheka. Kila mtu akaanza kucheka.

“Umefurahi?”  Jema akamuuliza akicheka. “Sana. Wewe utakuwa rafiki yangu kama anti Naya. Wenzio sisi ni marafiki. Kabla hajanisahau nilikuwa kila mara nampigia simu simu nakumpa stori. Halafu tukawa tunaimba wote. Akanisahau nikawa namuombea kila siku anikumbuke. Ujue nilikuwa nikimwambia nini Mungu?” Mama G akaguna na kutingisha kichwa. Wakacheka.  “Hata bibi alikuwa akisikia nilivyokuwa nikimwambia Mungu. Si ndio bibi?” “Wewe zungumza na simu Magesa bwana!” “Lakini si nilikuwa nikimwambia Mungu asaidie anti Naya anikumbuke, turudi kuwa marafiki, halafu tuimbe wote? Au bibi wewe umesahau? Si kweli dad?” “Hiyo simu kwa Jema ni ya familia nzima!” Akaongeza bibi yake. “Ni kweli Magesa ulikuwa ukimuombea anti Naya.” “Asante dad. Umesikia anti?” “Nimesikia Magesa.” “Basi leo ananikumbuka. Na wewe kwa kuwa utakuwa rafiki yangu, nitakuwa nikikuombea, na usinisahau. Nitakuwa nikikupigia simu na wewe halafu tunaongea. Au wewe hutaki kuongea sana kama Liv, kichwa kitakuuma?” Wakazidi kucheka. Liv na Jimmy wakimwangalia tu Magesa ndugu yao. Wakati wote yeye ndio yupo matatizoni na hakomi.

“Mimi nikiongea sana kichwa hakiumi.” “Basi kumbe ndio maana sisi ni marafiki. Nakupenda anti.” “Na mimi nakupenda Magesa. Nimefurahi umenipigia hii simu. Nahisi nitalala vizuriii.” Akacheka Magesa kwa furaha zote. “Na mimi nimefurahi umenisamehe.” “Haya. Usiku mwema.” “Asante na wewe anti Jema, bibi harusi mzuri.” Wakacheka sana. “We Magesa, harusi iliisha bwana.” Akapokea James. “Sasa hakuna bibi harusi mwingine anko. Mpaka akija bibi harusi mwingine, ndio anti hawi tena.” Walicheka sana. “Wewe hukuona anti alivyopendeza na gauni lake kama malaika?” “Niliona Magesa.” James akajibu akicheka. “Mimi nilipenda mpaka nikawaambia marafiki zangu shule, anti yangu alivaa gauni kama malaika! Kwa hiyo abakie tu bibi harusi.” “Sawa Magesa. Ila ujue umenifurahisha sana kumuomba anti msamaha.” “Asante anko. Usiku mwema.” Akaaga kwa heshima, wakakata kila mtu akahema.

“Joshua, hakika nakushukuru mwanangu.” “Ni Mungu, mama. Mimi huwa namjua anaposhuka mahali. Inaweza kuchukua muda kama hutachukua hatua. Kama hivi kama tungemkataza Magesa asizungumze na Jema, hii amani aliyoweka usiku huu, tusingeipata, kwa kujizuia sisi wenyewe. Ila Mungu anatenda mama. Anatenda kwa ajabu sana. Tuhamieni mezani.” Vikaanza vicheko. Angalau usiku huo ukaisha kwa amani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo ijumaa saa sita mchana, chakushangaza dunia, mzee akawa amemaliza juma. Akamuita Kemi msaidizi wake, ofisini kwake. “Kama kuna jambo lolote tafadhali tuzungumze sasahivi. Natoka, na sitarudi hapa wala sitataka simu za kiofisi mpaka jumatatu.” “Unasafiri!?” Mwanae akamuuliza akishangaa maana kama ingekuwa safari ya kiofisi yeye angejua, na kama ni ya kifamilia au binafsi, yeye kipenzi cha dad angejua. “Umesikia nilichokwambia?” Mzee akauliza kimamlaka kweli, mpaka akamshangaza Kemi. “Sidhani kama kipo. Naona kila kitu kipo sawa.” “Basi ni hilo tu.” Kwamba Kemi aondoke ofisini kwake. “Unasafiri?” Ikabidi Kemi aulize. Jinsi baba yake alivyomtizama, akaona atoke tu, japo hakuzoea.

Penzi kikohozi.

Penzi kikohozi, Zenda akawa hawezi kukaa bila Jelini. Anataka kumuona na kumshika au kushikwa naye kila wakati. Weekend yao walipanga wainze ijumaa mchana. Jelini akafurahi kama amepewa alumasi. “Nilijua utalalamika!” “Kuwa na wewe? Hata kidogo.” Zenda akacheka akiwa amempigia asubuhi hiyo akimuomba weekend hiyo awe naye. Mama Jema alishaanzishiwa mchakato wa biashara ya uhakika, mjukuu anasoma shule ya maana, nyumba inakarabatiwa kuanzia ndani mpaka nje, hakuwa na shida. Akamsubiri mwanae mpaka akatoka shule. Alirudishwa saa nane mchana. Akamuaga. “Nasafiri, lakini nitarudi jumatatu, mapema sana. Si utamsaidia bibi?” Mtoto huyo hakuwa na makuu, akamuaga mama yake, dereva akaja kumfuata, akaondoka kwenda kwa Zenda.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kama kawaida yake akatoka kumpokea. “Nilikuwa nakusubiria kwa hamu!” Jelini akacheka akimsaidia kushuka garini. “Nakuandalia chakula kizuri sana. Utakipenda tu.” Devi ambaye ni dereva akatoa begi la Jelini, mzee akalipokea. “Twende ukanifundishe na mimi siku nyingine nikupikie.” Devi akawa anasikiliza tu kwa kujiiba. Alipofunga tu mlango, akaondoka. Jelini na Zenda ndani. Yakaanza mabusu. “Nitaunguza.” Akamuachia Jelini akiwa na begi lake mkononi. Akapeleka begi chumbani, wakahamia jikoni.

Akaandaa meza very romantic. Mishumaa mizuri akaweka na wine, Jelini akimwangalia tu. “Ujue hii ni kwa ajili yako, wewe tu Jelini. Mimi huwa siachi kazi zangu eti kumpikia mwanamke!” Jelini akacheka sana. “Jelini anapendwa?” “Sana.” Akajibu Zenda kwa uhakika kabisa. Jelini hana mbavu. Basi ijumaa hiyo ikawa nzuri tulivu haswa.

Jumamosi.

Mazoezi ya Zenda asubuhi hiyo ya jumamosi yakaishia kwa Jelini. Basi wakashitua hapo kwa muda wakutosha tu, ndipo kifungua kinywa. Na Jelini hakuwa mvivu kwenye mapenzi, halafu sasa akakutana na Zenda hana papara, mtulivu na hakomeshei. Mapenzi ya ustarabu, si kuumizana mpaka kumchubua, na kushindwa raundi ya pili.

Mida ya saa tano wakatoka kwenda kuogelea. Jelini kwenye nguo ya kuogelea, Zenda alijuta. Yeye mwenyewe yakamshinda. “Bwana Zenda!” “Hakika tuondoke tu. Mimi siwezi hivyo. Mimi mwenyewe mwenye mali tu, nalemewa. Hayo macho ya wanaume wengine je?” “Sasa yanakuhusu nini wewe? Waache tu, sisi tuendelee na yetu.” “Yaani wale vyangu kwa macho! Hapana aisee. Tunaondoka. Usitake kuniua mimi kwa pressure.” Wakaondoka hapo kurudi nyumbani.

Walipofika tu akamdaka. Kweli hali ya Zenda ilikuwa mbaya kwa kumuona Jelini nusu uchi huko walipokwenda kuogelea. Mapenzi yakaanza mpaka hamu zake zikapungua. “Jelini wewe ni mzuri aisee. Mtoto mtamu, huchoshi!” “Upunguze na wivu Zenda jamani! Hutaibiwa.” “Na ibakie hivyohivyo.” Akajibu hivyo na kuendelea kumpapasa matiti taratibu mpaka wakapitiwa usingizi. Usiku wakatoka kwa chakula cha usiku na kwenda kuangalia movie wakiwa na hali ya furaha.

Usiku wa jumamosi wakati wanalala, Zenda akaweka ombi kama la mwanae. “Kesho ni siku ya jumapili. Nilazima niende kanisani. Tutaongozana?” Jelini akaanza kucheka. “Nini?” “Mwenzio huwa siendi kanisani.” “Utakuwa na mimi.” “Na Kasa akiniona nipo na wewe je? Au hamsali kanisa moja?” “Hee! Inamuhusu nini yeye!?” Jelini akashangaa sana.

“Kwamba wewe huna shida kuonekana na wanao ukiwa na mimi!?” “Ndio nauliza, kwani inawahusu nini wao!” “Zenda wewe! Ujue nilimkataa Kasa!” “Ukanikubali mimi. Sasa shida ipo wapi!? Kwani kila wanawake anaotongoza wanamkubali?” Kisha akajirudi. “Labda nirekebishe. Maana najua wanawake wanampendea pesa, lakini kwako imekua tofauti. Japokuwa ulijua anayo pesa, lakini ukamkataa yeye na kunipenda mimi! Sioni tatizo lilipo.” “Hudhani kama watashangaa mimi kutoka na wewe?” “Watakuwa sawa tu. Usijali.” Akajibu kirahisi kabisa. Jelini akacheka na kutulia.

“Labda wewe ndio uniambie hutaki kuonekana na mimi.” “Mimi unanijua Zenda. Sina wakujificha kwake. Halafu mimi nakupenda. Mwenzio nasikia raha kuwa na wewe popote pale. Nilikuwa nikihofia tu wanao.” “Kama ni hivyo, usijali.” Jelini akatulia kutaka kujua hiyo picha Zenda ataichezaje hiyo kesho mbele ya mwanae! Lakini akafurahi sana. Kwamba hamfichi! “Unacheka nini?” Zenda alimuona akitabasamu mawazoni. “Sikujua kama huna shida ya kuonekana na mimi hadharani hata kwa wanaokuhusu kwa karibu! Nimefurahi hunifichi.” “Wewe sitaweza kukuficha. Nakupenda sana Jelini.” “Nimefurahi.” Zenda akacheka akimwangalia pale kitandani. 

Jumapili.

Zenda akamuamsha asubuhi ajiandae. Jelini akajitengeneza mpaka akaridhika amependeza. Lakini kila akifikiria Kasa Kevin, kiroho kikazi kumdunda. Zenda akamwambia watoke. Kwenye gari kimya, kila mtu akiwaza lake. Kwanza ilikuwa asubuhi sana, Jelini hajazoea kuamka mida hiyo. Akajituliza kitini kimya mpaka kanisani.

Kevin alipomuona Jelini pale kanisani akawa hajaelewa. Akajongea karibu yao, akiwa na huyo Kemi kipenzi cha dad na vijana wake wawili. “Huyu anaitwa Jelini. Jelini huyu ni Kemi, dada yake Kevin na hao wawili ni watoto wa Kemi.” “Nimefurahi…” “Wewe si umesema huwa huendi kanisani, wewe!?” Kabla Jelini hajamalizia, Kevin akamuuliza hilo swali kwa mshangao sana. “Mimi hapa nimemfuata Zenda.” “Zenda!?” Kevin akauliza akizidi kushangazwa na Jelini aliyejibu bila woga usoni lakini moyoni mapigo mbio. Zenda alikuwa akisalimiana na wajukuu zake, lugha moja, kingereza. Lakini alisikia swali la kijana wake kwa Jelini. Kemi alibaki akimwangalia tu hakutaka hata kumsalimia.

 “Twende Jelini.” Akamshika mkono wakatangulia ndani, Kemi na Kevin wakabaki wamepigwa na butwaa. Watoto wa Kemi wakamfuata babu yao. Misa kwa lugha ya kingereza ikaendelea mpaka mwisho, Jelini akifuatisha bila kukosea mpaka mwisho na kumshangaza Zenda.

Wakatoka wakasogea pembeni kama kusalimiana zaidi. Wale watoto wakawa wanamuuliza kitu Jelini kwa kingereza. “Mimi nazungumza kiswahili. Kwani nyinyi hamjui kuzungumza kiswali?” Zenda akawa anacheka moyoni. “Kwani wewe hujasoma?” Kemi akamuuliza kwa kumdharau. “Hee! Kwani kusoma ndio kuzungumza kingereza!? Na wewe kwani hujasoma? Maana hapo unazungumza kiswahili!” Jelini akauliza bila wasiwasi wala hofu. Zenda akajua wamepata kiboko yao.

“We Jelini? Kwani umeachana na Colins?” Jelini akashangaa sana, asijue Kasa anamfanyia makusudi mbele za baba yake. “Kwani wewe unamjua huyu?” “Mimi hapa naitwa Jelini sio huyu.” Jelini akamwambia Kemi. “Sana tu. Maana huyu mtoto alikuwa akinitaka sana mimi, lakini nikaja kugundua anatoka na jamaa tunayefanya naye kazi pale ofisini. Nikamkataa, nikaweka ukaribu na rafiki yake. Kila mtu mbona anamjua tu huyu mtoto. Mtoto wa baa tu. Muulize Zilo atakwambia. Kila mwanaume pale mtaani kwao kashampitia huyu. Shida yake pesa.” Jelini alishangaa kitu kimemkaba kooni nakushindwa hata kujibu, akabaki akimtizama Kasa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nini kitaendelea kwa WOTE?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment