Ndipo akamnunulia hiyo
sehemu sio mbali na Tegeta, tena barabarani akiwa amehamisha watu kwa kuwalipa
pesa nyingi tu wampishe Jelini hapo. Mama Jema alishangaa kupita kiasi. Hakuwa
akiamini. Na hakusubiri, akaanza kumjengea hicho kituo cha mafuta. “Jelini!
Huyu baba wewe unamfanyaje!?” “Nampenda mama. Nampenda sana Zenda. Na usifikiri
namuomba, ni yeye mwenyewe na huyo mshauri wake. Sasa sijui huyo mshauri anajua
ni vyake au la! Maana naona mawazo mapya kila siku tena makubwa ya pesa nyingi
sana. Hapa amesema anataka kuweka kama mgahawa, kwamba watu wakija kuweka
mafuta kwenye magari, wakutane na huduma ya chakula.” “MmmH! Na vyote vipo kwa
jina lako!?” “Nilikuonyesha karatasi zote mama yangu. Kila kitu ameweka kwa
jina langu. Na anasema hataki ijulikane kama yeye anahusika. Nikahisi labda
anakwepa wanae.” “Pengine hataki waje kukupokonya.” “Labda.” Mama Jema gafla
akawa tajiri, yeye ndio muongoza mambo nyuma ya pazia, Jelini busy na Zenda
kitu kilichomfurahisha zaidi Zenda kuona japokuwa anamsaidia, lakini mapenzi bado
yapo vilevile.
Kila Kosa, Lina Garama Ya Kulipia.
Kwa Umbali Gani! Muda Gani! Ni Rehema Za Mungu.
Bale alikaa
hospitalini kwa majuma manne akipatiwa matibabu ya hali ya juu. Dada yake
huyohuyo ndiye aliyekuwa na kazi ya kumuuguza maana Joshua alikuwa akienda
kazini. Basi alikuwa akimtuma dereva awe naye mpaka wodini alipolazwa Bale na
shariti kuwa jicho lake limuone Naya mpaka anapomrudisha nyumbani. Basi Naya
akawa akienda na vyakula anavyopika mpishi wao, anakaa naye, kisha anaondoka
mpaka Bale akapona kabisa na kurudisha akili zake timamu na kuweza kumtambua
Naya, japo Naya hakuwa akimkumbuka bado ila mtu aliyekuwa katili sana kwake.
Siku ya mwisho
anaruhusiwa, ilibidi Joshua mwenyewe atoke kazini, kuwepo ili kulipa hayo
mamilioni ya pesa anayodaiwa mgonjwa wake. Akaomba kuzungumza na hao ndugu
wawili. “Haijalishi alichokifanya Malon kwenye maisha yake na yenu, lakini mali
zake zote, kama yeye hayupo basi ni haki ya wazazi wake.” Akaanza
Joshua. “Bale, chochote ulichonacho cha Malon, nitakitaka kwa maandishi,
ili wakabidhiwe wazazi wake kihalali.” “Nimeishiwa kila kitu ilibaki ile nyumba
tu ambayo ni kama pagala.” “Ile nyumba inathamani sana kwa pale tu ilipo. Bado
ndugu wana haki nayo. Je, hayo mashamba yake huko?” “Tokea nilipomchoma moto,
sijarudi tena kule.” Naya akashituka sana. Akamwangalia Joshua.
“Naomba usiogope
Naya. Tutazungumza.” “Huyu Bale amemchoma moto Malon?!” “Najuta Naya.” “Bale
wewe ni mkatili sana! Unaweza kuua mtu?!” Bale akaanza kulia sana. “Ni bangi.” “Hapana. Mimi nahisi ni zaidi
ya bangi Bale. Bangi haimpelekei mtu kuua moja kwa moja. Ila labda kumsaidia
mtu kutekeleza azma yake. Inamaana ulikusudia kumuua tokea mwanzo!” Naya akawa
akizungumza naye, asijue si Malon tu alimchoma moto, hata ndugu zake. Bale
alilia sana kwa hofu, maana Naya alimbadilikia kabisa akisikika si Naya asiye
na akili iliyochanganyikana. Anajua anachozungumzia.
“Bado nitataka kujua
huko mlipokuwa na Malon, alimiliki nini ili kuwafikishia wazazi wake taarifa
kamili. Kifo chake na mali zake.” “Kwamba utaenda
kunishitaki Joshua!” “Hapo nitakuachia wewe na Mungu wako Bale. Ila sisi
tunawajibika kujulisha ndugu zake juu ya kifo chake. Hawawezi kuendelea
kuishi hivi bila kujua kijana wao alipo. Halafu mali zake zote, ni HAKI yao.
Kwa hiyo, bado nitataka kujua mashamba yake yalipo na mali zake zote.” Naya
akatoka nje kabisa hakutaka hata kuendelea kukaa pale.
Joshua akamfuata.
“Bale ameokoka.” Joshua akaongea naye taratibu. “Kwani hakuwa amekoka kabla?” Hapo
kidogo akakwama. “Unajua japokuwa sikumbuki sana, lakini nakumbuka kusoma kuwa
tulikuwa tukiimba naye kwaya kanisani. Inamaana huyu mtu akikasirika anakuwa
mbaya Joshua! Mimi alinifanyia vile. Na rafiki ambaye aliniteka kunipeleka
kwake, kumbe alimchoma moto! Wewe huogopi ni nini atakufanya siku
utakapomuudhi?” “Ninachotaka kufanya akitoka hapa akaishi sehemu niliyokwisha
mwandalia ya kuishi. Akiendelea na mazoezi hapa, akarudi kutembea baada ya
kupata mguu wa bandia, nimtafutie kazi itakayoweza kumuingizia kipato, na
kuachia hapo. Tuone Mungu anatupa naye mahusiano ya nana gani.” Naya akawa kama
amekumbuka kitu. Akarudi ndani na kumuacha Joshua amesimama palepale.
“Naomba uniambie
ukweli na usinidanganye.” Bale akamwangalia. “Wewe umesema ndiye uliyemchoma
moto Malon. Je, baba?” Joshua alishituka sana aliposikia hivyo. Hakujua kama akili
ya Naya kwa wakati huo, kama ingeweza kuunganisha matukio kwa namna hiyo. “We
Bale? Na usidanganye.” Naya akawa mkali kabisa mpaka kumshangaza Joshua.
“Malon
alinishauri vibaya.”
Naya akawa hajaelewa. “Usiniambie maneno mengi. Baba na ndugu zetu wengine
nilisikia waliungua na moto vibaya sana mpaka kifo. Nani anahusika?” Ikabidi
Joshua arudi ndani. “Malon aliniambia tuwashe
moto kuunguza tu gala kama kuwakumbusha walipotoka, kumbe yeye alikusudia kuua
kabisa. Ndio moto ukaenda mpaka kwenye nyumba na kuwaua baba, Zayoni, bi…”
Naya akasikia kizunguzungu cha gafla, akaanguka na kupoteza fahamu. Aligonga
kichwa vibaya sana.
Hapana Marefu Yasiyokuwa Na Ncha.
Joshua alishituka,
akapiga kelele maana damu zilianza kutoka kichwani alipojigonga. Manesi wakajaa
hapo ndani, Naya akatolewa hapo hajitambui na kupelekwa sehemu kupewa huduma ya
kwanza. Akazinduka akajikuta amelazwa akashituka sana. “Joshua?”
Hilo ndilo la kwanza alilosema. Akaanza kulia sana kama anayejiokoa. “Mimi ni mke wa Joshua, si mke wa Malon. Ameniteka nyara.
Naombeni mumpigie simu mume wangu atawahakikishia.” Akili ya Naya
ikarudi akiwa mafichoni kabisa. Joshua alikuwa nje ya hicho chumba alichoombwa
asubiri wamsadie mkewe, akafurahi maana alishaambiwa hilo na daktari kwamba
akili inaweza kurudia ilipopotelea.
“Amenipiga
ndio nimezimia. Ananificha kwake, hataki nitoke. Lazima mume wangu atakuwa
akinitafuta sana. Naombeni msiruhusu anisogelee.” Yeye akadhania kile
kipigo cha mara ya mwisho, alizidiwa na Malon akamkimbiza hospitalini asijue
hata Malon hakujali. Aliendelea kumfungia, na ni muda mrefu sana ulishapita.
Joshua akaingia kwa haraka.
“Naombeni mnipishe
mimi nitamtuliza. Na msimshike kwa nguvu, mtamuumiza.” “Anaruka!” Wauguzi wote
wakaongea kwa pamoja wakiwa bado wamemshikilia. “Akiniona mimi, atatulia.
Mwachieni.” Mmoja akampisha, Naya alikuwa akilia sana. “Naya, fungua macho
niangalie. Mimi ni Joshua. Nipo hapa.” “Malon
amenifungia kwake Joshua.” “Najua. Na sasahivi upo salama na mimi.
Sitakuacha tena. Sawa?” “Nishike wewe Joshua.
Naogopa sana. Alikuwa akinipiga sana. Halafu ananibaka kwa nguvu, kikatili kama
mnyama kwa sababu nilikubali kuolewa na wewe.” Joshua akaumia sana.
Naya alikuwa akilia kwa sauti ya hofu, anatetemeka mpaka jasho linamtoka. “Nisaidie Joshua.” “Naombeni mnipishe
nimtulize. Akili yake ndio inarudi leo. Lasivyo anaweza akajidhuru vibaya akidhani
anajiokoa.” Wakampisha.
Joshua akamnyanyua pale alipokuwa amelala, na
kumkumbatia vizuri. “Upo nyumbani Naya. Na upo na mimi salama. Usiogope.” Naya
akaendelea kulia, Joshua akimuhakikishia yupo salama na alisharudi nyumbani
muda mrefu. Akatulia na kumwangalia Joshua kama asiyeelewa. “Ulisharudi
nyumbani mpenzi wangu, ila ulipoteza kumbukumbu. Ulikuwa na uvimbe kwenye
ubongo, ukawa ukitumia dawa. Lakini uvimbe ndio ulisababisha kupoteza fahamu.
Ila sikujua uliipataje?” “Malon alinipiga teke
nikajigonga na kupoteza fahamu. Alikuwa akinipiga sana kila nilipokuwa
nikikutaja. Na Bale hakujali kabisa. Aliniacha naye.” “Basi naomba
utulie Naya. Upo salama. Na upo na mimi. Sawa?”
“Alikuwa akinibaka kikatili sana. Nilikuwa nikilia nikikuita kila wakati
nikimsihi Mungu uisikie sauti yangu. Lakini hukuja Joshua. Niliendelea kuteseka
peke yangu.” Naya akaendelea kulia, akilalamika na kumuumiza sana
Joshua. “Pole Naya wangu. Pole sana.” “Nipime
UKIMWI na mimba, Joshua. Malon alikuwa malaya sana.” “Ulishapimwa
kila kitu.” “Hapana Joshua. Nataka unipime tena,
nione. Mimi naogopa.” Ikabidi Joshua aombe vipimo vyote kwa Naya,
ili kumridhisha tu. Akambembeleza akimfariji. Na vile alivyokuwa ameshituka,
kuumia vibaya kichwani na dawa alizopewa, akapitiwa na usingizi na kulala.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alipohakikisha
amelala kabisa ndipo Joshua akatoka kwenda kumalizia malipo ya Bale na kuomba
dereva amchukue na kumpeleka kwenye kinyumba alichokuwa amemkodia. Na mpishi
wake ndiye aliyemsaidia kumnunulia kila kitu alichomwambia Joshua kingehitajika
kwa mtu kuanza maisha. Na Joshua hakumpunja. Akamnunulia vitu vya thamani tupu.
Kuanzia chumbani, sebuleni mpaka jikoni.
Bale anashushwa
kwenye hiyo nyumba na magongo yake, akaingia na kukutana na sehemu nzuri ya
hadhi ya aina yake. Kama hoteli mpaka kitanda kimetandikwa. Patulivu, kajumba
kadogo tu, ambacho kinajitegemea. Aliona jumba kubwa pembeni yake, akajua
mwenye nyumba anaishi hapo. Akakaa. “Mlo wa kwanza upo tayari mezani, vitu
vingine vipo kwenye friji na makabatini. Namba zangu zipo kwenye hii simu,
pamoja na za Joshua.” Akamkabidhi simu mpya. “Ukiwa na tatizo lolote usisite
kunipigia mimi au Joshua. Ratiba zako za mazoezi mkuu amesema atampa Pelo ili
msikose. Kuna swali?” “Nashukuru sana. Asante.” “Swali?” Akasisitiza. “Kwa sasa
sina. Nashukuru. Akamfundisha jinsi ya kufunga na kufungua milango yote, akaondoka
na kumuacha hapo.
Bale alipobaki peke
yake ndipo akaweza kufikiria. Akaanza
kulia kwa uchungu sana, hajui chakufanya. Picha aliyoondoka nayo hospitalini ni
ya lawama kutoka kwa dada yake, na kuanguka kwake vibaya sana. Akapiga magoti
hapohapo sebuleni, na kuanza kulia. “Nitaua wangapi
hapa duniani Mungu wangu! Tafadhali nirehemu.” Bale akalia mbele za
Mungu na kushindwa kusimama. Alilia akitubu tena na tena kana kwamba Mungu
anatatizo la kusikia.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Huku kwa Naya majibu
yakatoka na kuogopesha hata daktari aliyehusika naye maana walisikia Naya
alikuwa akibakwa huko alipotekwa. Akarudi kwenye sehemu aliyokuwa amepumzishwa.
Joshua akanyanyua uso kumtizama, akamuona na uso uliojawa wasiwasi. Akasimama.
“Ni nini!?” “Nina majibu ya mkeo.” “Kuna nini?” “Kila kitu kipo salama, ila
amekutwa ni mjamzito.” “What?!” Joshua akamuuliza kwa kuhamaki mpaka akamtia
wasiwasi zaidi yule daktari. “Kitanda hakizai haramu ndugu yangu.” “Hapana!”
“Halafu si kwamba alijitakia ni jambo ambalo….” Daktari akataka kuendeleza
ushawishi akimuhurumia Naya.
“Hapana, wewe
huelewi. Huyo mtoto mimi nilikuwa nikimsubiria lakini sikujua ni kwa namna gani
au nianze kuomba vipi maana ni kama nilijifunga mimi mwenyewe kwa maneno
ya kinywa changu mbele za Mungu, nikitaka kuzaa baada ya miaka miwili
baada ya ndoa. Mke wangu alivyorudi nikatamani sana ashike mimba ila nikajiona
nitakuwa mbinafsi kwa kuwa bado hakuwa na kumbukumbu. Hatukuwahi kutumia kinga
ila akawa hashiki mimba, nikajua mimba haishiki kwa ukiri wangu. Na
sikuwahi kumwambia mke wangu wala Mungu. Nikawa najua nimejifunga kwa maneno ya
kinywa changu mwenyewe, nikaamua kusubiri tu mpaka muda niliosema mwenyewe
ufike, ndipo nizungumze na Mungu wangu tena. Maana aliporudi huyu alipimwa kila
kitu hakukutwa na lolote, na hakuwa na kinga na hashiki mimba. Kwa hiyo huu ni wakati
wa Mungu. Nimefurahi sana.”
Daktari akashangaa
Joshua anapiga magoti palepale pembeni ya mkewe, akasema. “Wewe ni Mungu. Na badala yako, hakuna mwingine.”
Acha aanze kububujika mpaka daktari akaondoka! Kwa muonekano wa Joshua,
usingedhani hata anahabari na Mungu. Lakini ni mwanaume anayejua kuomba, na si
kuomba yale maombi ya kiustarabu! Ni yale maombi ya kupiga magoti popote
linapofika swala la Mungu wake. Alilia mbele za Mungu kwa shukurani.
Akashukuru hata katika lililompata mkewe, shetani alitaka kuligeuza kuwa baya,
lakini akamshukuru Mungu kuwa, ameligeuza kuwa jema. Japokuwa alianguka
vibaya na kujiumiza, lakini amerudisha akili ya mkewe, tena akiwa anaiihitaji
kwa ajili yake na mtoto wao. Akambariki mkewe na mtoto aliyembeba. Akabariki
siku atakayozaliwa. Joshua aliomba mpaka akatosheka. Akakaa akifuta machozi na
furaha tele.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hapohapo akampigia
simu Geb, mtu wake wa karibu. “Niambie kaka.”
Geb akapokea kwa haraka akiwa ofisini mida hiyo ya mchana. “Yule Mungu asiyekawia wala kuwahi, ametutokelezea na sisi LEO.”
Geb akacheka. “Ameleta nini?” “Kumbukumbu za Naya.”
“Waw!” Geb akahamasika. “Hapana Geb. Hajaishia
hapo.” Geb akacheka na kuuliza. “Na nini tena?”
“Ametubarikia mtoto. Naya ni mjamzito.” Geb alifurahi sana. “Yupo wapi nimpe hongera?” Ikabidi amsimulie
kilichompata mkewe. “Lile baya shetani alitaka limpate
mke wangu, Mungu wangu ameliwahi na kuligeuza kufanyika kuwa jema. Wamempa
dawa, amepumzika.” “Aisee poleni sana. Tunakuja na Naya.” “Hapana Geb. Msiache kazi kwa ajili ya hili. Naya atakuwa sawa tu, na
ninajua watamruhusu leo. Labda mje nyumbani jioni mkiwa na nafasi” “Kama ni
hivyo basi tutakuja nyumbani jioni.” “Hapo sawa.” Wakaagana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jioni alipoamka, Naya
akawa anajisikia vizuri hata akaamka akiwa na nguvu. “Njoo unishike Joshua.”
Joshua akasimama. “Usiogope Naya.” “Nasikia kuumia
Joshua! Naumia sana. Bale amenitenda ubaya wa kupita kiasi. Na si mimi tu,
ameua familia yetu! Kwa ajili ya nini!?” Naya ndio kumbukumbu ikawa
imemjia vizuri. “Yaani sasahivi nakumbuka kila kitu
jinsi ilivyokuwa. Unajua nilikuwa nimekwenda saluni. Tena nilikuwa narudi
nyumbani. Wakati nikifungua mlango, nikashitukia Bale tuliyekuwa tukimtafuta
kwa udi na uvumba, eti amenisimamia nyuma yangu! Nikashangaa sana. Maana Bale
aliyekuwa akitafutwa tukidhani yupo matatizoni, hakuwa yule niliyemuona pale!
Alikuwa na hali nzuri tu!” Akamsimulia Joshua akilia kwa uchungu sana.
“Naomba utulie Naya.”
“Hapana Joshua. Bale alinitendea vibaya tena akiwa
anajua fika, simtaki Malon! Kweli ananitoa kwenye ndoa na kunipeleka kwa
mwendawazimu yule na kunitelekeza! Hakika Mungu aingilie kati, Joshua. Hujui ni
kiasi gani niliteseka kule.” “Naweza kuhisi, maana ulirudi ukiwa umevilia
damu, mwili mzima Naya. Ulikuwa ukitisha sana. Pole mpenzi wangu.” Akaendelea
kumbembeleza.
“Nina habari ingine.”
Akamfuta na machozi. “Mungu ametubarikia mtoto.” Naya akashituka moyoni ila
akajaribu kutulia. “Umenielewa?” “Kwani miaka miwili tayari tokea tuoane?” Naya
akauliza kwa wasiwasi. Akajua ni kweli anakumbuka kila kitu. “Bado kidogo, ila naona
ni wakati wa Bwana.” Akamuona ametulia akijifikiria. “Nimefurahi Naya.” “Sio unaniona mzembe?” “Hata kidogo. Uliporudi tu
nilikuwa nikitamani ushike mimba, lakini nikaona si sawa kwako na hali
uliyokuwa nayo. Naona Mungu amenihurumia japo nilikuwa nimejifunga kwa maneno
ya kinywa changu mwenyewe. Nimefurahi sana Naya. Naomba ufurahie na mimi.” “Mimi napenda sana watoto Joshua, ila wewe ndio ulisema
tusubiri. Isingekuwa hivyo, binafsi ningetaka kuzaa mara tu baaada ya ndoa.”
“Nilikuja kujutia sana
baadaye, nikajihisi nimekuwa mbinafsi. Halafu nikawa kama nimejipunja
mimi mwenyewe kufurahia baraka za Mungu mapema. Kwa sababu tungeweza kuwa na
ndoa nzuri tu, na bado tukawa na nafasi ya mtoto. Lakini nikashindwa jinsi ya
kujirudi. Nisamehe mpenzi wangu. Hata hili tulitakiwa kuweka mwanya wa
majadiliano, kuamua kwa pamoja si kama mimi nilivyofanya, kama kupitisha
sheria tu!” Yakaanza mabusu hapo wakimfurahia huyo mtoto. Jioni wakaruhusiwa
kurudi nyumbani.
Tamu & Chungu.
Ikawa ni mchanganyiko
wa hisia jioni hiyo. Habari njema za mtoto aliyekuwa akitamani hata kabla
hajaanzana na Malon, halafu akawa amemkumbuka baba
Naya. Kwamba huyo mtoto hatakuja kukutana na baba Naya! Akasikia
kuumia sana. “Kwamba hata nikiamua kwenda Kiluvya sasahivi, si kwamba
sitamkuta tu baba Naya na Zayon, lakini pia hatuna tena kwetu!” Akabaki
amejituliza pale kitini mumewe akiendesha lakini alimuona yupo mbali. Akamuona
anajishika tumbo kama anayetafuta kitu humo tumboni. Akavuta pumzi kwa nguvu na
kuzishusha taratibu, akatulia. “Utakuwa mama mzuri sana Naya.” Akajaribu
kumrudisha kwenye wakati huo. Naya akamwangalia na kuvuta tena pumzi kwa nguvu
na kuzishusha taratibu akijaribu kutulia.
Akagundua msiba
ulishaisha muda mrefu tu, na kila mtu alishaendelea na maisha yake. Yeye
anarudi na kumbukumbu ambazo watu walishazisahau! Inamaana hawezi kulia tena
msiba. Na nani? Akazidi kuumia kimyakimya na kushindwa kujieleza kwa Joshua
mumewe ambaye alishaonekana kuridhika na uyatima wao. Hakuwahi kumuonyesha kama
wanapungukiwa na kitu, wao wapo yatima na Mungu ni baba yao. Basi. Akaona na
yeye asije anzisha jambo jingine tena. Akatulia kimya mpaka wakafika.
“Acha nikukaribishe
tena nyumbani.” Ndipo akaangalia vizuri na kugundua mpaka walifika ndani kwamba
hata geti lilipokuwa likifunguliwa, hakuwa akijua. Naya akamtizama akijitahidi
kutoa tabasamu. “Maana vile ulivyorudi ukiwa huna kumbukumbu. Sihesabu.
Sasahivi umerudi nakukaribisha wewe na mtoto.” Naya akacheka taratibu na Joshua
alilitambua hilo akakusudia kumchukulia taratibu.
Akashuka na kuzunguka
upande wake, Naya akisubiri kwani alishazoea mumewe kumfungulia mlango. Ila
safari hii alimfungulia mlango na kumbeba. Naya akacheka, akamdaka midomo
hapohapo nje. Akaanza kupata kisi ndipo wakaingia ndani akiwa amembeba mpaka ndani.
“Acha nipandishe ngani mwenyewe nisikuchoshe Joshua.” Naya akaongea akiwa bado
mikononi kwa mumewe. Joshua akang’ang’ana mpaka juu kabisa chumbani. Akamuweka
kitandani. “Unakumbuka ahadi uliyoniahidi siku walipokuja kukuteka?” Hapo ndipo
akili ya Naya ikakumbusha deni alilomwambia Joshua.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwamba angemlipa siku
ile akitoka kazini kabla hajatekwa. Alikuwa akiomboleza msiba wa baba yake, kwa
hiyo Joshua hakuwa akipata kitu, ndipo akatoa ahadi kwamba, akirudi usiku huo
atampa penzi lakukata na shoka, hakuna kulala. Joshua akiwa anatizamia usiku
huo kwa hamu, akijitahidi kumaliza kazi kwa haraka, ndipo akapata ujumbe kutoka
kwenye simu ya Naya, eti ameamua kumuacha! Haikuwa imeingia akilini.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Ahadi ni deni,
mama.” Naya akacheka. “Na mimi nimekusudia kulipa deni langu.” Basi penzi
likaanza taratibu na kunogeshwa na furaha ya mtoto. Kukawa na utulivu wa namna
yake. Hisia mchanganyiko. Wakafanya yao na kubaki wamejilaza hapo kitandani
wakipanga yao taratibu. Mtoto huyo apewe chumba kipi ndani ya hilo jumba. Kama atakuwa
ni wa kike au wa kiume. Angalau Naya akapata kitu cha kufikiria na kucheka
wakijaribu kumfikiria huyo mtoto atafanana na nani.
Walishakaribisha watu
wao wa karibu wafike jioni hiyo kwa chakula, kumshukuru Mungu wa Joshua ambaye
huwa hatakagi kumkawiza sifa zake. Siku hiyo akawaomba hao watu wao,
watenge muda, wale na kufanya ibada fupi kumshukuru Mungu. Mpishi akawa
anaandaa chakula cha familia tatu.
Maji Yalishamwagika.
Ilipofika majira ya
12:30 hivi, James na Jema wakawa wameshafika na sheko, wanandoa hao wapya,
furaha. Ndoa si ndoano. Bado wapo fungate. Wametoka kupeana kisi la haja ndipo
wakashuka garini, wenyeji wao wakisubiria mlangoni. “Kwahiyo Naya sasahivi
unakumbuka kila kitu?” “Kila kitu, Jema. Na nakumbuka nikiwa na Joshua,
kukuandikia kadi ya shukurani kwa kujitoa kwa kiasi kikubwa kwenye shuguli yetu
nzima.” “Niliipata. Hongera na karibu tena duniani. Mungu ameona utoke
mafichoni.” “Joshua naye ameniambia hivyohivyo.” Wakakaribishwa ndani.
Hata hawajakaa sana,
jeshi la Magesa wakaingia wakiongozwa na Magesa mwenyewe. Joshua na mkewe
wakasimama kwenda kuwafungulia mlango, Jema na mume wake wakabaki kimya
sebuleni. Wakasikia sauti ya Magesa. “Kwa hiyo sasahivi anti umekumbuka kama
mimi nilikuwa rafiki yako?” “Wewe salimia kwanza Magesa, bwana! Wewe vipi baba
mzazi?” “Samahani bibi. Nilikuwa nimefurahi mpaka nikasahau kuwasalimia.
Shikamoo anko na anti.” Wakaitika. “Kwahiyo unanikumbuka sasahivi?” “Akikazana
jambo huyo!” “Nimekumbuka Magesa. Tena tulikuwa tukiimba wote.” Akafurahi sana.
Wakati wazazi wake na
ndugu zake wanaingia hapo, yeye akapitiliza sebuleni ndipo akawakuta Jema na
James. “Wewe ni anti bibi harusi unayetaka kuingia mpaka chumbani kwa mami
wangu?” Magesa akauliza swali lililozua ukimya mpaka kwa waliokuwa wakiingia
hapo. Jema alishituka, moyo ukawa kama kumeanguka chuma sakafuni, akabaki
kimya. “Mami wako ndiye atakuwa na majibu mazuri. Nenda kamuulize yeye.”
Wakasikia James akijibu, ila si Jema. “Kwahiyo..” “Hata hilo swali unalotaka
kumuuliza sasahivi, na jingine litakalokujia baada ya hilo. Iwe leo au kesho,
juu ya anti na kule nyumbani kwenu, mami wako anayo majibu yake mazuri sana.
Muulize yeye.” James akaendelea.
“Na usijewahi
kumuuliza tena anti. Yaani siku ile nyumbani kwenu, na leo, iwe mwanzo
na mwisho, kumvamia anti kwa maswali juu ya nyumbani kwenu. Usiwahi
kurudia tena kumuhoji juu ya maswali ya nyumbani kwenu, au chumbani kwa
mami wako, kwa kuwa anti hana uhitaji wowote huko nyumbani kwenu wala
chumbani kwa mami wako. Kwa hiyo acha kumvamia kwa maswali juu ya kwenu.
Umenielewa Magesa?” Hapo wakasikia sauti ya amri na ukali kutoka kwa James. “Ndiyo
anko.” Magesa akasikika akijibu kwa utulivu kama ambaye ametishika.
“Na siku nyingine.
Hata kama unafuraha au haraka ya kiasi gani, unapokuta watu wazima sehemu, unasalimia
kwanza kama alivyokwambia bibi. Huanzi kwa kuparamia watu wazima kwa
maswali, bila salamu. Umeelewa?” “Ndiyo anko.” “Haya, nenda kakae pale,
umsubirie mami wako, uje umuulize maswali ya ‘anti bibi harusi aliyetaka
kuingia mpaka chumbani kwake’.” Wakajua disco ishaingia mmasai wa uchi.
“Twende mke wangu.”
Akamshika mkono Jema, akasimama. Wakawa wanatoka na wale waliokuwa wakiingia
hapo wamesimama wameduaa. “Mama G, shikamoo.” “Shikamoo.” Jema naye akapenyeza
salamu yake. “Marahaba. Mnaendeleaje?” “Sisi ni wazima kabisaa. Tunamshukuru
Mungu.” Akajibu James na kuunganisha. “Jamani sisi tuliwatangulia, acha
tuwapishe na nyinyi.” Akaongea James, Nanaa ameinama pembeni ya mumewe. “Lakini
tuliandaa chakula cha pamoja kisha ibada ya shukurani James! Mngesubiri kidogo
tu, hatutachukua muda mrefu nikijua kesho ni siku ya kazi na shule.” “Basi wenzetu
watatuwakilisha kwenye fellowship na swallowship. Acha sisi tuwapishe. Twende
Jema.” Akamvuta mkono mkewe na kutoka.
Joshua na Naya
wakawafuata. “Tungekaa kidogo Jema!” Naya akaongea kwa kubembeleza akisikika
kunyongea tayari. Maana wawili hao walishageuka mashoga tokea harusi ya Jema.
Kupigiana simu na kuchati kwa hili na lile likawa jambo la kawaida. Wakajenga
ukaribu kuliko Naya na Nanaa, ambaye bado hakuwa akimkumbuka kama walikuwa
marafiki. Na kwao hakuwahi kurudi tena tokea siku Malon alipokwenda kwao na
kumchukua wao wakiwa ndani, na mumewe kumuokoa mikononi kwa Malon siku ya
birthday ya Magesa na Liv.
“Acha tu tukapumzike
Naya. Tutakuja wakati mwingine tena. Ilimradi sisi tumeshakuona, na tumepata
habari njema tupu, acha itoshe kwa leo.” Naya akanyongea. “Usiku mwema.” James
akamalizia na kuondoka na mkewe bila nyongeza. Joshua akawawahi. “Nashukuru kwa
kuja jamani.” “Asante sana.” Wakajibu na kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kibao kimegeuka
kwelikweli. Wakati akitetewa na kulindwa yeye, hakujua madhara yake kwa wengine.
Leo anashuhudia ulinzi uleule aliokuwa akipewa yeye, ndio anaupata Jema. Jema
aliondoka pale, nusu aombe kuolewa tena na James. Maana kwanza moyo wake
haukuwa tayari kuwepo pale chumba kimoja na kina Magesa. Na hata hawakuwa
wameyamaliza, ndipo Magesa naye akauliza akiwa hana hila ya kumuumiza mtu, ila
kutumia kumbukumbu zake vizuri, kwa haiba yake ya uchangamfu, akili ya kitoto,
akaweka petrol kwenye makaa ya moto, yaliyokuwa yamefunikwa na majivu tu. Hata
lile jema alilokuwa amekusudia Joshua usiku huo, likaingia doa. Wakabaki yeye
na mkewe wakisindikiza gari kwa macho. Kimya wakila janga alilochuma Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
- Nini
kitaendelea?
- Jelini na
Falia ya Kasa na Zenda mwenyewe?
- Mahusiano ya James na undugu wa muda mrefu aliotengeneza na Joshua pamoja na Geb? Baraka za wanawake walioongezeka kwenye maisha yao zimeshaanza kuwatenga. Wanaponyaje mahusiano yao au ndio mnara wa Babeli Umevunjwa?
0 Comments:
Post a Comment