Alipokuwa tayari
akamsindikiza. “Unatoka shule saa ngapi?” Mwanae akamwangalia akitembea. “Kwani
utakuwepo?” “Hata kama hutanikuta nyumbani lakini nitawahi kurudi kabla
hujalala. Shuleni wanakuonea?” “Ni Maliki tu ndio anapenda kuchukua vitu vyangu
bila kuomba. Ukimkatalia anakupokonya kwa nguvu.” “Ulimwambia mwalimu?”
“Anasema nikimsemelea atanipiga.” Akamuhurumia mwanae na kumkumbusha jinsi
alivyokuwa akionewa, tena na baba yake huyohuyo Jeremy halafu anamtisha asiseme.
“Ulimwambia bibi?”
“Hajauliza.” Jelini akakwama. “Sasa huwa unakula nini shule?” “Bibi ananipa
hela.” “Kwa hiyo hapo unayo hela?” “Ndiyo.” “Inatosha?” “Tumepanga na bibi,
huwa inatosha mpaka nirudi kula nyumbani.” “Jeremy wewe ni mtoto mzuri sana.”
Akanyamaza tu akitembea. “Umenisamehe nilivyokugawa?” Hakujibu akaendelea
kutembea. “Bado umekasirika?” “Nimesamehe mama.” “Mimi ni mama mbaya?” “Umesema
umebadilika.” “Na naacha pombe kabisa. Halafu ukitaka kitu uwe unaniambia mimi.
Na ukirudi uniambie habari za Maliki. Ila leo akijaribu kukupokonya kitu,
mkatalie na akikichukua kwa nguvu na wewe kichukue.” “Akinipiga je?” “Na wewe
mpige kwa nguvu zaidi yake mpaka kiume, ndipo atakuogopa. Ukimpiga kama yeye,
hatakuogopa. Hakikisha unamkatalia kwa ukali. Akikunyang’anya, chukua kwa nguvu
zako zote. Na mwambie asirudie tena.” “Nikimpiga anaweza kunipeleka kwa
mwalimu.” “Mkifika kwa mwalimu akitaka kukuchapa, kataa mwambie anipigie mimi
simu. Kataa kabisa, mwambie mama ameniambia usinichape, kwa kuwa ni haki yangu.
Lasivyo wanipigie mimi simu.” Jeremy akacheka.
“Wakinilazimisha
kunichapa?” “Ndio kataa kabisa. Halafu lia kwa sauti waambie wampigie mama yako
simu. Nitakuja.” Hakuna siku aliyokuwa na furaha kama hiyo. Hata akabadili
kutembea kwake. Akaanza stori kwa mama yake. Wote wazungumzaji halafu akafanana
na mama yake. Mtoto wa kiume mzuri, ikawa kama Jelini alijizaa. Wakaanza
kuongea wakipokezana maneno, wanacheka
mpaka akamfikisha. “Usije acha kupokea simu!” “Siwezi. Na jioni kabla ya kulala
nitakuwa nimesharudi kama hutanikuta nyumbani ili unipe stori za Maliki.”
Akacheka. Akamsubiria apande kwenye daladala, akarudi nyumbani.
“Sasa hayo yasiwe ya
siku moja Jelini. Sio iwe leo tu, kesho haupo hapa. Utamchanganya mwanao. Ona
alivyofurahi ulivyomwambia unamsindikiza!” “Nimebadilika mama. Na hata nikiaga
natoka, siendi tena baa, kuepuka vishawishi.” “Sawa.” “Mbona itika yako ni kama
hauna imani na mimi!?” “Wewe usiwe na wasiwasi na mimi, ila jiangalie tu
Jelini. Mwenzio Jema kang’ang’ania kwenye aliloamini mpaka amefanikiwa mwanaume
wamaana. Ona thamani aliyowekewa na mumewe. Sasa wewe uzuri wako wote huo unautumia
vibaya, wakati ulitakiwa ukunufaishe zaidi.” Akanyamaza na kuingia ndani kuoga.
Akajitayarisha vizuri kama mdada anayelipwa mamilioni ya mshahara. Akatoka.
“Kuna mambo
nafuatilia. Yakikaa sawa nitakwambia. Ila siende baa na nitawahi kurudi.” “Hayo
unayoniambia mimi, uyakumbuke huko kichwani mwako.” “Hivi mimi katika safari
zangu zote nilishakuwa nikikuaga au nilikuwa nikiondoka tu?” “Wewe
usinikasirikie mimi bure.” Akaondoka bila yakuongeza neno.
Pesa Huongea Popote.
Mtihani ikawa hakuna
uhakika wa kipato kuaminisha Utawala wa kila shule za maana alizotaka mwanae
ajiunge, kuwa anauwezo wa kulipa ada bila kuchelewa au kushindwa
katikati. Kila alipokuwa akienda, akiulizwa elimu yake mwenyewe na kazi
anayofanya, wakaishia kumwambia hakuna nafasi. Akaanza kukosa raha. Akazunguka
mpaka majira ya saa sita hajafanikiwa.
Akaona simu ya Zenda
ikiingia, akapokea. “Uliamka salama?” “Ndiyo. Na wewe?”
“Mimi nipo sawa. Siku imeanza na mambo mengi, lakini nilitaka kukwambia kuna
shule niliifikiria, nikamtuma sekretari awapigie simu na kuwaomba nafasi ya
mtoto mmoja wa miaka 8. Wameomba uende naye ili wakamfanyie usaili wajue
wanamuweka kwenye darasa gani. Sasa nashauri uchangamke. Iwe leo. Maana ni
shule nzuri na nafasi zake wanabania sana, mpaka ufahamike.” Alipomtajia shule yenyewe akaumia sana.
“Mimi
mbona wameniambia hakuna nafasi hapo!? Nimezunguka kila mahali wananiambia
hakuna nafasi!”
“Naomba usilie Jelini. Hao watu mbali ya kutoa elimu
kwa watoto, ukumbuke pia wanafanya biashara. Wanataka uhakika wa pesa yao kila
muda wa kulipwa unapofika. Sasa wakiona huna
kitega uchumi cha kueleweka, lazima watakukataa tu.” Jelini akaumia
sana. “Sasa naomba utulie. Nakutumia gari, ukamchukue
mtoto kwenye hiyo shule aliyopo, umpeleke wakamfanyie usahili. Halafu
utaniambia watakachoamua. Ila wanakutegemea hapo.” “Asante Zenda.” “Karibu.
Tutazungumza baadaye.” Wakakata simu baada ya kuelekezana na kuelewana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jeremy alifurahi sana
mama yake alipompeleka kwenye hiyo shule. “Nitakua nikisoma hapa?” “Ngoja
tuwasikilize kwanza.” Ikawa Jeremy hajawahi kusoma shule za kingereza. Hajui
kuzungumza kingereza ila anajua kusoma na kuandika. Walipotaka arudie darasa,
hapo Jelini akakataa kabisa. Na anavyochukia shule, akakataa mwanae asirudie
darasa. “Mimi mwanangu anaakili. Akisoma hapa kwa muda mfupi tu, ataelewa,
mpeni nafasi muone. Ila kama ni kurudia, mimi sitaki, naondoka na mwanangu.
Mnataka mwanangu azeekee shule!? Hapana kwakweli.” Hapo hakutaka tena
kushauriwa wala kumsikiliza mtu.
Akashangaa
hawambishii, ndipo akahisi pengine wanafahamiana na Zenda. Wakashauri masomo ya
ziada ambayo atapata hapohapo shuleni. Hapo akakubali. Akapewa kila kitu juu ya
mtoto. Akazungushwa na kupewa ratiba ya basi. Muda na sehemu itakayopita
kumchukua. Jelini akafurahi sana. Akapewa na sare za shule, tayari kuanza kesho
yake. Yaani shule ileile aliyoambiwa hakuna nafasi, ikawa kuna nafasi mpaka
yakuanza kesho yake! “Wanaosemaga pesa sio kila kitu, waongo.”
Akajisemea Jelini wakati akimsikiliza mwanae anavyofurahia. Maneno mengi kwa
furaha akimsimulia hata yale waliyokuwa pamoja kama mama yake hakuwepo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akampigia simu Zenda
akilia kwa furaha. Zenda akacheka. “Acha nikupigie baadaye.
Kutakuwa kumetulia kidogo. Nimebanwa. Ila usilie, nataka ufurahi.”
Jelini akakata kwa haraka. Akaenda kutafuta sasa viatu na begi la shule.
Akamnunulia mwanae vitu vizuri sana, tena vya hali ya juu ili tu aendane na hiyo
shule. Kuanzia nguo za ndani mpaka viatu na begi. Aliporidhika hata akifika
huko hataonekana ni wa hali ya chini ndipo akarudi nyumbani.
Mama Jema hakuamini. “Kumbe akili yako
inafanya kazi! Sasa usinywe tena pombe. Ukiendelea hivyo naona hata kujenga
utajenga.” Jelini akacheka sana. Mwanae akaanza kumsimulia bibi yake habari ya
shule ya kizungu. “Nakuja kuchukuliwa na gari, bibi.” Akajisifia Jeremy. Hilo
likamfurahisha mama Jema zaidi.
Kwa Zenda.
Jelini hakutoka.
Akakaa hapo nyumbani mpaka mida ya saa kumi na moja ndipo akaona simu ya Zenda.
Akatoka kuzungumza naye. “Ndio unakuwa busy hivyo!?”
Akacheka taratibu “Siyo mbaya sana. Vipi siku yako?”
“Nilikuwa tu nyumbani, baada ya kuweka sawa mambo ya Jeremy. Amefurahia huyo!
Anaanza kesho. Wanakuja kumchukua na gari ya shule.” “Afadhali. Naona na malipo
yamekamilika. Ahadi yangu nimemakamilisha. Ada imelipwa mpaka amalize darasa la
saba.” “Nashukuru Zenda. Asante sana. Mama amefurahi sana. Na pia nashukuru kwa
kunielekeza vizuri.” “Karibu.” Akataka kusema kitu, akasita. Wakatulia.
“Mbona kama
kuna kitu unataka kusema, unasita?” “Natamani kukuona Zenda, hata kwa muda
mfupi tu! Ila najua upo busy.” “Leo nimeshamaliza siku ya kazi. Natoka ofisini
muda si mrefu. Unataka nikutumie dereva akulete nilipo?” “Ningefurahi, angalau nije
kukukumbatia kidogo tu.”
Zenda akacheka sana. “Sasa kwa nini kidogo?” “Sijui
bwana! Lakini unakumbuka jana nilikwambia nilishakuwa na hamu na wewe?” “Basi
acha nimtume dereva, na mimi nitoke hapa. Tutaonana nafikiri baada ya lisaa.”
“Sawa.” Akarudi ndani kwa furaha.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Nitatoka, kwenda
kukutana na Zenda. Sitachelewa sana kurudi. Jioni ndio anakuwa na muda. Kwa
hiyo lazima kukutana naye jioni. Mle, msinibakishie. Na Jeremy uwahi kulala,
ili kesho uende shule ukiwa hujachoka.” “Lakini huendi baa?” “Hapana Jeremy.
Siendi tena baa. Na nitarudi. Hata kama utalala kabla sijarudi, ujue asubuhi
nitakusaidia kujiandaa na kukupiga picha na nguo zako mpya.” “Na viatu na begi
langu la shule.” Jelini akacheka. “Kabisa. Na ninajua utapendeza sana.” Mwanae
akafurahia, akaingia ndani kuoga tena ajiandae.
Baada ya muda mama
yake akamfuata. “Lile gari lililowaleta, limerudi tena. Naona ndio umekuja kuchukuliwa!” Jelini
akaanza kucheka. “Sasa utulie. Maana huyu anaonekana ni mwanaume anayejielewa.
Mpaka anakusomeshea mtoto!” “Lakini ujue ni mtu mzima.” “Hata kama ni mzee.”
“Kweli mama!?” “Sasa bora lipi? Vile ulivyokuwa ukishinda baa, au huyu
anayekujali na kukuongoza vizuri? Ameoa?” “Mkewe ameolewa tena huko Ulaya, na
mzungu.” “Kwa hiyo hana mwanamke?” “Sijui mama!” “Basi ndio kumbana mpaka ubaki
peke yako. Na kumbana kwa kutulia. Tulia mwanangu, fanya anachokwambia.
Anaonekana ana uwezo. Shule anayokusomeshea mwanao ni ya mamilioni ya pesa!”
“Na anamlipia na masomo ya ziada pia. Nimefurahi mama. Na asante kunihimiza.”
“Basi usichelewe huko.” “Nitajitahidi kuwahi kurudi. Ila kama muda wa Jeremy
akifika wa kulala sijarudi, usikasirike.” “Siwezi. Maadamu nishajua upo na mtu
mwenye akili nzuri, hapo sina ugomvi. Ila mpime kabla ya chochote.” “Sawa. Ila
nampenda. Mzuri huyo! Mweupee. Anangaa kwa usafi kama katoka kikaangoni.” Mama
yake akacheka. “Nenda usichelewe.”
Kivulini!
Jelini akatoka
amependeza haswa. Akamuaga mwanae, akatoka. Gari safi, akaingia na safari
ikaanza akipelekwa asipopajua. Akatulia kimya mpaka Mikocheni karibu na kwa Mwinyi.
Geti likafunguliwa, akaingia ndani, Bonge la jumba! Zenda akatoka amevaa nyeupe
tupu mpaka sendozi. Alipendeza sana na kuvutia. Akamfungulia mlango.
“Uliniambia unaniamini, na huna hofu na mimi, si ndiyo?” Akakubali akitingisha
kichwa akicheka. “Basi twende ndani. Nimekupikia kitu kizuri.” Akashuka garini.
“Umependeza mpaka unavutia, Jelini!” Akazidi kucheka, dereva akaondoka kabisa
hapo. “Hapa ni kwako Zenda!?” “Samahani sijakukaribisha vizuri. Karibu sana
nyumbani.” “Asante. Pazuri sana kama wewe mwenyewe! Msafi.” Akacheka.
“Nashukuru. Twende ndani.” Akaingia amemshika mkono.
“Kaa hapa sebuleni
nilete kinywaji, kisha nitakwambia kitu.” “Natamani hata kukukumbatia kidogo
Zenda. Nimefurahi mno swala la mtoto.” “Utanikumbatia mpaka uchoke wewe na
kuniaga. Muda wote huu mpaka saa mbili, ni wako wewe tu Jelini. Chochote
utakachotaka kufanya na mimi, ruksa.” Jelini akaanza kucheka, Zenda akaenda
kuchukua vinywaji akaja na juisi zilionekana nzuri sana kwenye glasi. “Hii
juisi ni ya nyanya tu, nimetengeneza na kuweka asali kidogo na ndimu kuweka
ladha.” “Inavutia! Asante.” Akamuwekea pembeni.
“Sasa kabla
hatujaendelea, unakumbuka jana ulipima, mimi sikupima. Acha nipime hapa mbele
yako.” “Na kile kipimo chako ulichonikatalia?” Zanda akacheka sana. “Lakini
ilinisaidia kujua kuwa wewe ni mtoto mzuri. Ukikosa unajua kujishusha. Nakuja.”
Akaondoka hapo, baada ya muda akarudi nacho. Akamuelekeza jinsi ya kupima na
matokeo yanakuje ndipo akajipima. Jelini akafurahi alipoona hana maambukizi ya
vijidudu vya Ukwimwi.
“Hongera Zenda.”
“Nipo makini sana, kwa sababu wazazi wangu walifanikiwa sana wakiwa bado
vijana, ila wakafa pia wakiwa bado wanadai kabisa. Ndio nikaishia kumiliki mali
zao zote. Nilijiambia sitaki kurudia kosa. Ndio maana nipo sana makini. Na
nikiwa na mtu kwenye mahusiano, kosa la kunisaliti hata mara moja tu, halina
msamaha.” Jelini akainama na kukalia mikono yake. “Mimi nina wivu mbaya sana
Jelini, na nipo makini mno. Siwezi na sitaki kuchanganywa.” Jelini akaishiwa
nguvu akabaki ametulia kimya. “Umenisikia na kuelewa?” Akatingishwa kichwa
kukubali.
“Nina swali na naomba
uwe mkweli kwangu. Hakuna jibu sahihi wala baya kwenye hili swali. Umenielewa?”
Jelini akakubali kwa kichwa akiwa amenyongea. “Je, unaye mwanaume ambaye upo
naye kwenye mahusiano kwa sasa?” “Hapana, sina.” Zenda akatulia akimwangalia.
“Sidanganyi Zenda. Nimebadilika.” “Naomba kukuamini Jelini. Sitaki uniue.”
“Siwezi. Hata mimi sitaki kufa nikamuacha mtoto wangu. Mimi sio mtu wa kulala
hovyo na wanaume. Kwanza naogopa.” “Na mimi unaniogopa?” “Wewe nakuamini
Zenda.” “Nashukuru.” Akachukua glasi yake ya juisi, na kurudisha vifaa ndani.
Akarudi akiwa ameshamaliza. Akapitiliza jikoni.
“Njaa imeanza kuuma?”
“Bado. Njoo ukae hapa na mimi.” Jelini akamuita kwa upendo, akamsikia anacheka
huko jikoni, baada ya muda akatoka. “Napika.” “Nini?” “Naoka vitu vichache tu.
Nataka ule vizuri, ushibe.” Jelini akacheka akimwangalia, akaenda kukaa pembeni
yake. “Jelini wewe ni mzuri sana. Sana.” Akamvuta vizuri na kujiweka
sawa. “Asante Zenda. Na asante tena na tena. Nimefurahi kuliko
nitakavyokwambia. Umenisaidia kubaki na mwanangu.” “Ulishashukuru bwana Jelini!
Mbona unataka kupoteza muda kwenye jambo moja tu?” “Ile shule ni garama sana.
Mama mwenyewe ameshangaa.” “Sasa umemwambia nini?” “Nimekusudia kubadilika,
sikutaka kumdanganya. Nimemwambia ukweli kuwa Zenda ndiye anayemsomesha.”
Akakunja uso.
“Mama ameelewa na
kuona unaniongoza vizuri kuliko wote. Dada Doro nimekua naye lakini hajawahi
hata kumjali mtoto wangu kwa chochote kile. Na nilikuwa nikishinda naye baa
hanikumbushi hata swala la mtoto. Wewe mama amekufurahia. Anaona utakuwa rafiki
mzuri.” “Kama ndio hivyo afadhali.” Akajivuta. Akaelewa anataka kumlalia kama
jana yake. Akajiegemeza vizuri kwenye kochi, akajivuta mpaka kifuani.
Akapitisha mkono nyuma akaukutanisha na wa mbele, akawa amemkumbatia. Na yeye
akaanza kupitisha vidole vyenye kucha ndogo sehemu ya juu tu alipofikia. Jelini
akazidi kujivuta kwake, kisha akamwangalia kama anayetaka kumuomba kitu,
akasita, na kurudi kuinama. Naye Zenda kimya.
Akaweka mkono mmoja
kifuani kwake akaanza kutembeza vidole taratibu. “Unakua na kazi gani ofisini?”
“Acha kunirudisha kazini bwana Jelini!” Akalalamika nakumfanya Jelini acheke
sana. “Nataka kujua.” “Nafanya mambo mengi sana, nikikwambia utachoka bure,
halafu utanitoa hapa, na kuanza kunifanya nianze kufikiria tena mambo ya kazini
badala ya kuwa na wewe hapa. Mimi nataka muda na wewe. Huoni mpaka
nimekupikia!” “Kwani huwa hupiki?” “Pale tulipokula jana ndio sehemu yangu ya
chakula. Mara chache sana kupika na ni kama sipiki, japo najua sana kupika.”
“Mimi najua kupika, lakini sipendi kushika moto ili nisiungue.” Zenda akacheka
sana. “Wewe mpishi gani unaogopa moto? Twende nikakuonyeshe glovu. Navaa kila
ninaposhika sufuria au sinia zakuweka kwenye oven. Siungui.” Wakaelekea jikoni.
“Mmmh! Jiko lenyewe
zuri, hapa huwezi kuungua.” Zenda alicheka sana. “Moto ni moto.” “Si kwenye
majiko yenu haya! Jiko halina moshi! Hata mimi ningependa kupika. Sasa kule
kwetu mpaka uweke mkaa, upepee mpaka ushike, kabla hata hujabandika sufuria,
umeshaungua!” Zenda akazidi kucheka. Akamuonyesha vitu vingi vya hapo jikoni
Jelini akabaki akishangaa. “Pananukia vizuri! Ndio unapika nini?” “Viazi
nimeponda baada ya kuvichemsha kisha nikaweka cheese na kuweka kwenye oven
kidogo kufanya cheese yangu iyeyuke. Mboga za majani, na nimekuokea nyama nzuri
sana.” “Nikikubusu nitakuwa nimevuka mpaka?” “Mimi nataka uvuke.” Jelini
alicheka sana na kujifunika uso, akahisi mikono yake ikimsogele. Akatulia.
Akapitisha taratibu
mpaka kiunoni. Akamvutia kwake. “Nasubiria busu langu.” Afungua macho akakuta
akimwangalia, akambusu shavuni. “Hapo utavukaje mpaka sasa!?” Zenda akashangaa
akilalamika. “Naogopa.” “Usigope, ilimradi unihakikishie hiyo midomo itabaki kwangu
tu. Isipite kwengine.” “Na wewe hivyohivyo Zenda. Ukijalala na mwanamke
mwingine, ujue umemuua Zenda wangu, na ndio basi tena. Hatutakaa tukarudi kuwa
kama hivi. Tafadhali usinisaliti Zenda.” “Mimi nakuahidi.” Akakubali kwa haraka
mpaka akamshangaza Jelini.
“Kwani huna mwanamke!?”
“Alikuwepo au yupo, lakini!” Akatulia akifikiria. “Sijui nikwambie nini juu
yake. Ni On and Off. Yupo kama hayupo, halafu anakiburi na hasira zisizo na
maana.” Hapo Jelini akamuachia. “Subiri kwanza.” “Hapana Zenda. Mimi hivyo sitaweza.”
“Ni kama tuliachana.” “Zenda!” “Kweli. Sikumbuki hata mara ya mwisho
kuwa naye ni lini!” “Jamani Zenda wewe! Kwa hiyo bado yupo kwenye maisha yako?”
“Ni kama hayupo.” “Ni kama!?” “Labda niseme hivi, hatujaachana ramsi, lakini
hatupo pamoja.” “Basi naomba unitafute utakapokuwa unanafasi yangu.” Jelini
akatoka jikoni kurudi sebuleni alipoacha pochi yake.
“Subiri kwanza Jelini!
Mbona unaondoka hata hatujawekana sawa? Wewe ndio umenifahamu. Unafikiri
nilikuwa nikiishije? Yule alikuwa mtu wangu mfano nikitaka penzi, namtafuta,
basi.” “Jamani nyie Zenda!” Jelini akashangaa sana. Lakini Zenda akaanza
kucheka kama mazuri. “Si bora nimekwambia ukweli? Sio kwamba tuna mahusiano
fulani. Ilikuwa tukisaidiana. Akibanwa, ananitafuta namsaidia na mimi
hivyohivyo. Wanaita booty call.”
“Mimi hivyo sitaviweza.
Hayo maisha nimeyaona, na ningetaka kuyaishi pengine usingenikuta hapa na shida
zangu, Zenda. Nimezungukwa na ahadi nzuri za mali nyingi lakini na wanaume wa
namna hiyo wakulala na wanawake bila shida wala kuwaza mara mbili. Ngono kwao
ni starehe kama starehe yakunywa pombe. Sasa wewe unaweza sema kwako ni
tofauti, unamsaidia yeye tu, kumbe akikukosa wewe kuna mwingine anayemsaidia.
Na huyo anayemsaidia naye anaye mtu wake. Huo mzunguko utakwenda mpaka
unawafikia watu kama kina dada Doro, kisha kuja kunirudia mimi. Mwenzio
mwanangu mdogo. Sitaki kufa nimuache. Hakika hivyo sitaweza Zenda. Samahani
sana.” Hapo Jelini akasalimu amri.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Itakuaje? Maana ni kama Zenda amebeba majibu ya shida zote za Jelini,
lakini Jelini na shida zake zote, anamisimamo yake anayoelewa yeye na kuisimamia
bila kujali jamii inaishije.
Kumbe na uzuri wake wote angeweza kutumia kujinufaisha kimali, ila
hapo, ameweka STOP.
ITAKUAJE NA HARUFU YA MEMA IMESHAMIRI?
Inaendelea?
0 Comments:
Post a Comment