Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 13. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 13.

Faraja aliyokuwa akiipata Jelini, kama aliyetembea kwenye jua muda mrefu, akapewa maji na kuwekwa kivulini mpaka mwenyewe akajishangaa nafsini kwake. Akabaki ametulia hapo mwilini kwa Zenda, kimya kama si yeye. Mwishoe akamchungulia kule alikoweka uso wake. “Unawaza nini?” Ikabidi avunje ukimya maana alitulia sana. “Vitu vingi.” “Kama nini?” “Sitaki wamgawe mwanangu!” “Lakini huna mipango naye Jelini. Kulea ni kazi mno. Ni zaidi ya kumnunulia kitabu na kumuacha nacho. Kuna garama za kulipa, usifikiri hao wanao amka asubuhi na mapema kuwahi maofisini ni kwa sababu wengi wao wanapenda! Hapana. Ila majukumu ya watoto yanabadilisha kabisa maisha ya mzazi. Kwa hiyo na mimi nipo kama mama yako kwako. Toa mipango endelevu itakayoahidi maisha ya baadaye ya mtoto.” “Nitabadilika.” “Hiyo haitoshi, Jelini. Unabadilika katika lipi litakalomnufaisha yeye na wewe pia?” “Ndio nafikiria chakufanya.”

“Naomba niangalie. Kaa vizuri.” Akajishauri kama ambaye alikaa pazuri hataki kutoka. Zenda akatulia tu akimsubiria. Mwishoe akajitoa hapo alipokuwa amemlalia. “Niambie nini unafikiria kufanya.” “Sasa kama ni shule si  nitahitajika kusoma, kulipa na ada! Hapo nitamsaidiaje mtoto tena?” “Una elimu gani?” Akanyamaza. “Lazima unijibu.” “Niliishia kidato cha pili, ndio nikashika mimba, sikurudi tena shule.” “Kwa nini?” Akapandisha mabega juu kukataa. “Lazima unijibu Jelini.” “Ni siri.” “Sasa nitakushaurije?” Akanyamaza. “Niambie.” Akamsihi kwa kumbembeleza, akaanza kulia.

Moyo Wa Mtu, Msitu.

“Ni mwalimu ndiye aliyekuwa akikuchezea mpaka kukupa mimba?” Akatingisha kichwa kukubali. “Ulimwambia mama?” “Aliniambia nikisema atanichinja mimi na familia yangu yote. Mimi nahisi ni mvuta bangi yule.” “Mlikuwa mkikutana wapi?” “Alikuwa akinituma kwake halafu ananifuata baada ya shule. Inaniuma Zenda, halafu eti nilivyoshika mimba akanipiga, akaniambia mimi ni mjinga. Najiachia mpaka nashika mimba hovyo. Akaendelea kunipiga eti ananiambia nimtaje aliyenipa mimba maana si yake na wala nisiwahi kumtaja popote. Nikimtaja atanichinja kama kuku. Hapo alikuwa amenipiga kupita nitakavyokwambia, halafu akanifukuza kwake. Nilikuwa siwezi kulala mpaka nilivyojua kuwa pombe ni dawa. Kuwa ukilewa kabisa unakuwa hukumbuki tena.” Hapo akaelewa kwa nini anashinda baa.

“Pole sana Jelini. Sasa Doro ulijuana naye vipi?” “Baa tu. Na yeye alikuwa na matatizo yake, tukakutana wote pombe zinatusaidia kulala, ndio tukawa tunaongozana. Tukishakunywa, tunaenda kwake kulala.” Jelini akaendelea. “Ila baadaye yeye akasema yeye hatakubali lazima alipe kisasi, ndio akaanza.” “Naomba usinifiche. Niambie.” “Ndio akaanza kulala na watu makusudi ili kuwaambukiza huo ugonjwa. Sijui alikutana na mtu mwenye gonjwa la zinaa kali, akamuambukiza huko kwenye kulipa kwake kisasi, lakini aliumwa. Aliumwa sana. Sasa hapo ukumbuke anavyo hivyo vijidudu, hana kinga ya mwili, halafu akapata huo ugonjwa wa zinaa! Zenda! Yule dada aliumwa. Nilimuuguza mpaka mimi mwenyewe niliingiwa hofu nikadhani atakufa. Anavuja usaha tu, unanuka! Lakini akaja kupona.”

“Sasa eti amepona badala atulie, akaapa hataacha kulipiza kisasi. Ataendelea tu kuusambaza na wengine wapate kama yeye. Ndio mimi nikaingiwa hofu kabisa ya kulala na wanaume.” “Ni kwa nini sasa analipiza kisasi?” “Ila usimwambie mtu. Wewe nimekuamini.” “Sitamwambia mtu.”

“Dada Doro alikuwa mlokole kama Jema. Kwa anavyodai yeye alikuwa mwaminifu sana mpaka akapata huyo mchumba ambaye walikaribia ndoa kabisa. Anasema alikuwa amejitunza. Wakati wanakaribia ndoa anasema siku moja huyo mchumba wake akamwambia yeye amezidiwa, amsaidie. Anasema akamuhurumia maana alimbembeleza sana, halafu hakuona shida kwa kuwa alijua atakuja kuwa mumewe. Wakaanza taratibu mpaka ikafanyika mazoea wakawa kama wana ndoa.”

“Maisha yakaendelea lakini akaanza kuona anambadilikia. Hata swala la ndoa nalo anaendelea kulipiga teke kwa sababu zisizoisha. Ikabidi sasa kuanza kumfanyia uchunguzi,  ndipo akaja kugundua kumbe huyo mwanaume alishakuwa na mke kabisa, alioa. Mkewe akaja kufa na mtoto kwa ugonjwa mbaya.” “UKIMWI.” Akaweka sawa. “Ndiyo. Na mbali ya hilo akaja kugundua kuwa ni tapeli tu na mengi aliyokuwa amemwambia alikuwa akimdanganya. Ndio ikabidi aende akapime kujithibitisha. Bahati yake mbaya, akakutwa ameshaathirika. Ndio hasira hizo kwa wanaume wote na kuwalipiza kisasi. Bila bia kichwani, hawezi lala.”

“Kabla huyo mwalimu hajakuharibu akili, ulitamani kuwa nani maishani?” “Nesi. Nitibu watu wagonjwa. Mtu akija hospitalini anaumwa sana, basi nambembeleza na kumpa dawa.” Zenda akacheka. “Si unajua bado unaweza kuwa nesi?” “Sitaki kusoma tena. Kila mwanaume akiniona ananitaka tu kimapenzi. Halafu wakishajua nipo chini yao, wanatumia nguvu. Sitaki.” “Haitakuwa kama mwanzo Jelini. Naomba fikiria kabla hujakataa.” “Mimi sitaki kusoma. Sitaki kurudi tena shule.” “Unataka nini?” “Kitu kitakachoniingizia pesa ya kumtunza mtoto wangu na mimi.” “Sasa ofisi gani itakuajiri na wewe huna vyeti? Ndio utaishia kupata kazi ya kuwagawia mabosi chai, unarudia mtindo uleule.” Jelini akacheka sana.

“Acha dharau bwana!” “Nakwambia ukweli.” “Basi nifanye biashara.” “Biashara gani?” Akabaki akiwaza, hata hajui watu wanafanyaje biashara wakati amezungukwa na mama zake wote wafanyabiashara. Akakwama kabisa. “Jipe muda wakufikiria halafu utaniambia.” “Nimefurahia kukaa hapa na wewe.” Zenda akacheka. Akavuta mkono wa Zenda kwa upendo, mwenyewe akimwangalia tu, kisha akaushika vizuri. “Asante kuwa na mimi.” “Karibu. Na mimi nimefurahi umeongea na mimi lakini huyo mwalimu lazima akamatwe ili asichezee watoto wengine.” “Mimi sitaki kesi.” “Unafikiri wewe ulipoondoka, aliacha hiyo tabia yake?” “Sidhani. Aisee ni mkatili yule kaka! Anakufanya mchezo mbaya kama vile wewe ni mnyama. Na akimaliza anakufukuza kama mbwa!”  

“Nitumie jina lake, shule uliyokutana naye, nitamfuatilia tu. Ila uwe tayari kujitetea wewe na kwa niaba ya wengine wanaopitishwa hapo.” “Acha kwanza nitulie kwenye maisha Zenda. Kesi zitanichanganya, watanichukulia mtoto wangu.” Hapo anaongea, anachezea vidole vya Zenda. Anavipanga hivi na vile.

“Nakupa kazi.” Jelini akamwangalia kwa mshangao akidhani anataka kumuajiri. “Kesho nenda katafute shule nzuri sana ya mtoto. Usiogope bei. Kisha unijulishe. Mimi nitamlipia mpaka amalize darasa la saba.” Jelini alibaki akimwangalia. “Umenielewa?” Kimya. “Acha kufa ganzi bwana! Niambie kama umeelewa?” Akaanza kulia. Safari hii akajirudisha kifuani kabisa na kumkumbatia akililia kifuani kwake. Usicheze na Jelini.

“Nilijua ungefurahi!” Akajiliza hapo mpaka akatulia akimbembeleza mgongoni. Wakatulia kwa muda, Jelini hata hatikisiki, kamkumbatia, kimya. “Tutachelewa kitabu cha mtoto.” “Asante Zenda. Asante sana.” “Basi kesho ufanyie kazi. Uliza kila kitu, mpaka usafiri, nguo, na michango mingine. Ikiwezekana tukikutana tena, unijie na fomu zote.” “Kesho si siku ya kazi, nina uhakika unakuwa busy.” “Jioni itakuwa muda mzuri.” “Saa ngapi ili nisikusumbue na simu.” “Nitakupigia. Ila kama kuna swali, usisite kunipigia kuniuliza. Ila isiwe pesa ya ada. Hiyo nimekupa ruhusa, ilimradi iwe shule nzuri. Kiasi cha ada kisikuogopeshe.” “Mimi napenda vitu vizuri.” “Najua.” Kisha akamsaidia na kumfuta machozi vizuri.

“Tuondoke hapa.” Zenda akashauri. Akajitoa hapo kifuani, wakahamia viti vya mbele. Akamuona Jelini ametulia. Akamuacha tu mpaka akamfikisha sehemu, akamsaidia kununua vitabu viwili vya mtoto wa miaka 8, akamsogeza mpaka karibu na usafiri. “Si umeshasema unaniamini?” Akamuuliza baada ya kuweka gari pembeni. “Wewe nakuamini.” “Basi naomba safari hii mimi nikulipie usafiri na wa kesho wakati ukitafuta shule.” “Nashukuru sana Zenda. Asante.” “Karibu.”

Hakujua anamuagaje. Anampa mkono au! Akajifikiria Zenda na yeye ametulia tu akimchukulia taratibu. Akamuona anachukua vitu vyake. “Ukalale salama, Zenda.”Akamwambia kwa upendo. “Na wewe.”Akashuka akiwa haamini. “Akija kubadilika kesho!” Akaanza kuingiwa na wasiwasi. “Nisije kumtafutia mwanangu shule halafu apotee!” Akawaza Jelini akielekea kwenye taksii. Akaona hilo asimwambie hata mama yake, asije akaendelea kuonekana muongo.

Moyo Umependa.

Wakati akimsindikiza kwa macho, hapohapo akampigia  simu Zilo. Zilo alipoona tu simu ya Mzee Kasa mwenyewe, akapokea kwa haraka sana. “Unamfahamu Jelini, anaishi Tegeta?” “Yule binti ambaye Kevin alitaka nimfuatilie?” Mzee Kasa akafikiria kwa haraka akajua atakua ni yeye tu. “Uliambiwa nini juu yake?” “Ila mimi nilimwambia ukweli kwa vile nilivyopata taarifa zake. Kama kuna jingine, basi nitakuwa nilidanganywa, au Kevin mwenyewe hakuwa amenielewa.” Ikawa ni kama anajitetea.

“Wewe ulimwambia nini?” “Huyu binti ni wa Tegeta. Ana mtoto alizaa nasikia akiwa shule. Maskani yake ni baa akiwa na msichana mwingine anaitwa Doro yeye ndio kama anayemnywesha.” “Ana mwanaume gani?” Mzee akaendelea kuhoji. “Kwa nilivyopeleleza, anakunywa na huyo Doro na ndiye anayeondoka naye kila siku kama hatarudi kwao. Inavyoonekana japo Jelini mwenyewe hajajua, ni kama huyu Doro anamchukulia wanaume. Yule muhudumu wa pale baa wanayopenda kunywa, nilivyozungumza naye alisema kwa jinsi walivyomchunguza, ni kwamba kila mwanaume anayemsogelea Jelini, Doro anajitahidi kumuwahi yeye na kuishia kuwa naye. Wanavyodhani ni kama Doro anamuweka Jelini karibu ili kujinufaisha naye kwa wanaume watakaokuwa wakimtongoza. Maana mtoto mwenyewe si mchezo! Mimi mwenyewe nilipomuona huyo Jelini, nikasalimu amri na nikamuelewa Kevin kwa nini ahangaike na mwanamke wa aina hii.” Zilo akaendelea, mzee akaweka umakini.

“Kwa hiyo huyo Doro anamuweka karibu na kuwa naye kila siku hapo baa. Japo wanakunywa kama kundi. Wapo wanaume wengine mpaka wazee tu na nyadhifa zile za juu haswa hata ukiona, utawashangaa, ndio wanakuwa nao hapo. Nilipotaka kujua ni yupi kati yao anatoka naye au alishawahi kutoka naye, sijapata uhakika kwa ukweli.” Hapo akamshitua tena. “Unamaanisha zipo fununu yupo na mtu!?” Wivu tayari.

“Hapo ni kama tena pana utata. Ukitaka kujua ni yupi kati yao kwa hakika, inakuwa kama hakuna uhakika tena. Ila ni wale wasichana walioshindikana makwao. Mtoto wa baa asubuhi mpaka usiku. Sio msichana wa maadili wa kama hadhi ya Kevi. Na hilo hata Kevin mwenyewe sikumficha.” Zilo anaongea, asijue mzee anajiulizia mwenyewe sio mkwe tena.

Kukumbatiwa na binti mdogo kama Jelini, kachezewa vidole, na akapewa jina jipya! Hali ikawa imeshatibuka ndani ya mzee. Akili imevurugwa. Akawa anamtaka Jelini haswa. Akaona aachane na Zilo. Anataka kumchanganya tu. Akamshukuru na kukata simu. Kisha akamrushia  pesa kitu anachokipenda sana Zilo. Pesa itoke kwa mzee mwenyewe. Habani.

Penzi Kikohozi.

Akaanzwa na tamaa. Wivu, hataki mtu amsogelee tena Jelini. Akatamani kumpigia, akaona awe mstaarabu, ajikaze kiume asije onekana amepagawa kama wanaume wengine aliozoea kuwaona Jelini jinsi wanavyotapatapa. Akaanza kutuma pesa bila kufikiria asijue anatuma kwa Jelini ambaye hajazoea kuhongwa. Akatuma zaidi ya mara tatu huku akihisi ni chache. Mwishoe akajiambia atulie.

 Jelini kuona pesa zinaingia mfululizo akampigia. “Zenda, nahisi unabonyeza sehemu, pesa zinajituma kwangu!” “Nataka zikusaidie.” “Hii pesa ni nyingi sana Zenda!” “Usijali. Utanipigia kunijulisha kama umefika nyumbani salama?” “Safari hii nitafanya hivyo Zenda. Ila nimeshakuwa na hamu na wewe.” Zenda akacheka taratibu na kutulia akijikaza kiume asije onekana fala kwa Jelini aliyezoea kubabaikiwa.

“Nimefurahia muda na wewe Zenda.” Akaweka msisitizo kwa upendo. “Na mimi pia. Tutatafuta muda mzuri zaidi. Ila naomba ukumbuke ahadi zako Jelini.” “Nitabadilika Zenda.” “Hapana. Niambie umebadilika. Jelini niliyemkuta leo asubuhi, asirudi tena. Ukijihisi upweke, nipigie. Na achana na Doro kabisa. Tutalipa kisasi kihalali, si kwa kuuza miili.” Jelini akajisikia vibaya. “Sitarudia tena Zenda. Nakuahidi.” “Nashukuru.” Hapo akajisikia vizuri haswa. Bila kutarajia Jelini akajikuta anajitia kitanzi yeye mwenyewe kwa mzee.

“Ila sasa hivi napitia hapo baa kuchukua kuku wakupeleka nyumbani.” Hapo akamtibua kabisa. “Jelini! Kwa nini hukusema wakati tunakula ili wafungiwe na wao?” Zenda hapo akalalamika na kujisahau kabisa kana kwamba yeye ameshakuwa mmiliki halali. “Sitakaa Zenda. Nakuahidi sitakaa.” “Hayo mazingira ukirudi haitachukua muda kukuridisha nyuma. Tafadhali usiende Jelini. Utaninyima usingizi na kunifanya nishindwe kufikiria kabisa.” Akajikuta anasalimu amri. Wivu umemlemea. “Basi Zenda.” “Sio kwamba sikuamini! Ila hakuna sababu yakujitia vishawishini. Tafadhali mtume mtu akakununulie.” “Naona nitafanya hivyo.” Wakatulia.

“Sitakwenda Zenda. Acha nirudi tu nyumbani, nitampigia mtu wa pikipiki akafuate chakula.” Yale aliyomwambia mwanae kuwa yeye hayataki, mtu kutawala maisha na ratiba zake. Kumpangia wapi awepo, akajikuta anayakubali kwa baba mtu bila kujijua. Tayari akajihisi anawajibika na furaha ya Zenda. “Hilo ni wazo zuri. Upo kwenye taksii tayari?” “Tayari, hapa napita baa ilikuwa niingia lakini naelekea nyumbani. Sisimami tena. Na wewe umeshafika nyumbani?” “Bado. Nimekutana na foleni kidogo.” “Pole. Basi nitakupigia tena baadaye. Acha nimtume mtu akachukue chakula.” “Usinisahau kama asubuhi.” “Sitakusahau Zenda. Nitakupigia.” Wakaagana. Zenda akitamani ageuke upepo amfuate awe naye. Gafla akawa anajihisi anaibiwa.

Nyumbani.

Akafika kwao akamkuta mama yake na Jeremy wamekaa sebuleni kimya, macho kwenye luninga yao ya kawaida tu. “Nimepima na cheti hiki hapa.” Mama yake akaanza kucheka. “Sasa unacheka nini? Kama nimeathirika je?” “Mbona wewe nakujua! Ungekuwa ukilia, ningekufuata hukohuko hospitalini. Sasa tulia Jelini.” “Nimekoma mama. Ujue kwa nini nilienda kupima?” Mama yake akabaki akimwnagalia. “Mwenzio nilikuwa nikienda kulala kwa dada Doro wala si kwa wanaume. Ana nyumba nzuri yule dada, sasa napenda chumbani kwake usiku anawasha A/C unalala usingizi mzurii.” “Tafuta vyako, acha kutaka vya watu.” “Nimesema nimebadilika.” Akaendelea kusimulia.

“Sasa ile kuamka leo nisipopajua, na mkasema nilimgawa Jeremy, nikasema usijekuta nikiwa nimelewa huko, wananifanyia mambo mabaya. Ndio nikaona nipime.” Mama yake akamwangalia na kunyamaza.

“Nimekuletea zawadi ya vitabu Jeremy.” Akaongea kwa kujikomba kwa mwanae. Akamuona amefurahi sana mpaka akatoka pembeni ya bibi yake na kumsogelea. “Vitabu gani?” Akavitoa kwenye pochi na kumkabidhi. “Au sio aina ya vitabu unavyosoma?” “Sasa hivi nasoma chochote tu nitakachokipata. Asante.” “Unisamehe jana nilikugawa. Wewe ni mtoto mzuri Jeremy. Mimi ndio mama mbaya. Lakini nimebadilika. Na naacha pombe kwa ajili yako. Umesikia?” “Utakuwa ukirudi kulala hapa?” “Sasa hivi sifanyi kama zamani nita…” “Wewe mjibu mtoto, acha maneno mengi.” “Namuelezea!” “Hapana Jelini. Wewe jibu maswali yake aridhike.” “Nataka kusema hata kama nikutoka nitakua naaga na kuwaambia ninapokwenda na kurudi.” “Hapo sawa.” Akatulia.

“Nimeagiza chakula, wanaleta. Nimekuagizia na bia mbili, mama. Na wewe fanta yako, wataleta.” “Na wewe?” Mwanae akamtega. “Mimi sitakunywa.” Jeremy akafurahi, mama yake akacheka. “Makubwa! Lakini nashukuru.” Jelini akacheka na kujituliza. Mama yake akamuona amepoa. Macho kwenye tv tu. Kisha akamuona kama amekumbuka kitu, akatuma ujumbe. ‘Nilifika nyumbani. Nipo nimekaa tu.’ ‘Nataka kukusikia Jelini. Ukipata nafasi unipigie.’ Akacheka akisoma ujumbe wa Zenda. ‘Unalala saa ngapi?’ ‘Huwa nawahi kulala kwa sababu naamka mapema sana.’ ‘Kwa nini?’ ‘Nitakujibu tukizungumza.’ ‘Sawa.’ Akajibu na kutulia. Kimya.

Kweli chakula kikaletwa na bia mbili tu, na fanta moja ya mwanae. “Wewe huli?” “Nilishakula na rafiki yangu tulipotoka kupima.” “Anaitwa nani?” “Mama jamani! Mimi sitaki kusema uongo. Nimebadilika. Acha kunichimba.” “Si umtaje tu jina?” “Anaitwa Zenda.” Mama yake akashangaa hilo jina. “Wa wapi?” “Usiendelee mama bwana! Ila ujue ni mtu mzuri, yeye ananiongoza vizuri.” “Bora.” Akasema tu hivyo na kuendelea kula. Wakamuona anasimama. “Naenda kuzungumza na simu, nitarudi.” “Zenda huyo?” Akamchokaza, Jelini akacheka sana. “Mama Jema!” “Au kuna mwingine tena, Zenda anaibiwa?” “Sijaona wakumuibia Zenda, mimi.” Mama yake alicheka sana, Jelini akakimbilia nje.

Moyo Haujafundishwa Kupenda, Umependa.

“Nakuwahi kabla hujalala.” “Nisingelala mpaka nikusikie.” “Kweli Zenda?” “Kabisa. Hapa nimebakiwa na harufu yako kifuani mwangu.” Jelini akacheka kwa kudeka. “Kujibu swali lako lile uliloniuliza. Nimeshajizoesha kuamka alfajiri na mapema tokea kijana mdogo sana. Kichwa changu kinafanya kazi vizuri mwanzoni mwa siku. Nikishafanya mazoezi asubuhi, naanza kazi. Kwa hiyo na kulala pia huwa najitahidi kulala mapema ili angalau kuupa mwili masaa angalau nane yakupumzika.” “Ndio maana unaonekana kama kaka yake Kevin.” Zenda alicheka sana.

“Kweli! Una mwili mzuri sana.” “Mazoezi na kula sahihi. Na pia namshukuru Mungu, sina magonjwa yanayokuja na uzee. Kwa hiyo mwili haujapatwa shuruba nyingi.” “Hongera. Kwa hiyo unajiandaa kulala?” “Nimeshakusikia hivi, na najua upo sehemu salama, naingia kulala sasa.” “Asante kujali.” “Tutazungumza zaidi kesho.” “Usiku mwema.” “Na wewe Jelini.” Wakakata simu, kwa mara ya kwanza Jelini akasikia upendo wa ajabu sana ndani ya moyo wake. Akasahau hata swala la umri.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi ndani na kutulia. Hata wao hawakuwa wamemzoea Jelini huyu. Akakaa hapo mpaka wakakubaliana kwenda kulala. Alilala akimtafakari Zenda na kutamani kukuche amuone tena. Gafla alichokisema Zenda kikatimia. Yeye ndio akaanza kumpenda. Akakumbuka na kujicheka mwenyewe hapo kitandani, gizani, asijue kwa Zenda ndio zaidi. Alimpenda huyo Jelini kuliko alivyopenda kwa… Akabaki akiwaza mwenyewe kitandani. Akasita kila alipojaribu kuvuta aina hizo za hisia kama alishazipata kabla. “Aisee sidhani!” Akajipinga mwenyewe akiwa hapo kitandani kwake. “Jelini ni wa tofauti aisee!” Akawaza Zenda huko upande wa pili. Yeye anawaza kwake, na Jelini akabaki akiwaza vyake huku akiogopa asije kuwa tofauti kesho yake. Akabaki akiwaza mpaka akapitiwa na usingizi mawazoni. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nini Kitaendelea?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment