Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 12. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 12.

Pombe si chai. Jelini alifika kwao akakuta bado mama yake amelala, mwanae amekaa anasoma. “Unasoma nini?” “Kitabu tu. Mbona hujavaa viatu?” “Habari yake ni ndefu. Jianchie tu, wewe soma unachosoma.” “Anti Jema ametuma ujumbe amesema anko amekubali baada ya mwezi nihamie kwao.” Jelini akashangaa sana. “Uhamie kwao! Sijaelewa.” “Wewe jana si ulisema unanigawa bure?” Jelini akatoa macho. “Na ulimtangazia kila mtu. Wala usimbishie mtoto.” “Mama wewe! Jana!?” “Jana pale harusini. Ukasema unamgawa bureee!” Jelini akaumia sana. Mama yake akatoka maana alikuwa chumbani.

“Mimi nilikuwa nimelewa!” “Sikukwambia wewe uache pombe hazijawahi kukupenda ukanibishia na kusema mbona mimi nakunywa! Sasa ndio ujue kichwa chako kilivyo kibovu, ukaongea mengi wee, mpaka mtoto akaanza kulia, ndio Jema akamwambia yeye atamchukua, ila wakiwa safarini atazungumza vizuri na mumewe wapange. Ndio kamjibu leo asubuhi. Ujue jinsi mwenzio alivyoumia.” “Mimi nilikuwa nimelewa mama! Sijamaanisha.” “Basi ushamwaga mchele kwenye kuku wengi. Na unamjua Jema hapendi mambo ya vigeugeu. Ushamgawa mtoto hadharani, yeye na mumewe wamesema watamchukua na kumsomesha. Ndio uwe huru sasa, endelea na kuzurura kama kuku wa kienyeji. Halafu sasa nikusikie unabadili mawazo, wakati mimi nataka huyu asomeshwe shule za maana, na wewe hali yako kama hivyo. Kazi huna, una kazi ya kulewa tu na kumangamanga.”

“Ila mimi sijasema simtaki mtoto wangu.” “Jana ulisema.” Mwanae akaweka msisitizo. “Si nilikuwa nimelewa! Sasa mtachukuliaje kama simtaki?” “Ulisema mwenyewe. Sasa nikuone unamgeuka Jema.” “Mimi nataka niishi na mwanangu.” “Unaishi naye wapi na wewe kwanza huwa hulali hapa. Pili kazi huna, kazi yako pombe na kuvaa vizuri? Utaweza kumsomesha shule za maana huyu?” Hapo akapoa. “Nakuuliza wewe.” “Nitatafuta kazi.” “Basi ukipata hiyo kazi. Ukaniletea huo mkataba wa hiyo kazi, na ukalipwa, ukaniletea ada yake huyu, ndio nikusikie unaongea unachokiongea sasahivi. Lasivyo usitake kunifanya mimi mjinga. Wewe ukatae shule. Mtoto atake shule, eti umkwamishe hapa kwa starehe zako zisizoisha!” Mama yake akamjia juu.

“Lakini mimi namtaka mtoto wangu. Sitaki mtu amchukue.” “Wewe mwenyewe hushindi hapa. Kutwa upo baa.” “Mbona nimebadilika siku hizi siendi tena, hata nikitoka narudi kwa wakati.” “Wewe unajua mwanao alilala wapi jana mpaka kumkuta hapa hivi leo?” “Si ulikuwa naye wewe!” “Ujue wewe mtoto unawazimu Jelini wewe! Unashindana na mimi wakati wewe akili huna! Mwenzio nilizaa na nikalea. Nilikuwa nakunywa, na wanangu wanapo pakulala na wanakula. Hamjawahi kushinda njaa. Tena kwa jasho langu. Niliwasomesha mpaka wenyewe mmekataa shule. Wewe unaniiga, huna hata kibanda! Mwanao hujui hata anachosoma hapo ni nini!” “Nimebadilika.” “Jana ulilala wapi?” Kimya.

“Jelini?” “Jana nililewa sana, lakini kuanzia leo naacha pombe. Naanza kumfuatilia mwanangu. Sitaki mtu amchukue mtoto wangu. Mimi ndio maana hata nikiondoka hapa, narudi kwakuwa najua yeye mwanangu yupo. Mkimchukua nitakuwa sina sababu yakurudi hapa. Hata kama mimi ni mama mbaya, lakini nampenda mwanangu na nimesema nitabadilika.” Hapo hata mama  yake akanyamaza.

“Nilikosea jana kukugawa, Jeremy. Nimekosa. Na nishajua pombe inanifanya sifikiriii, sinywi tena. Na nishaachana na Doro, nitakuwa nalala nyumbani. Hata kama nikiwa natoka, nitakuwa nikiwaambia. Lakini msimgawe mwanangu.” “Na shule? Maana sitaki apate elimu ya kuunganisha. Maadamu nimempata mwenye hela na yupo tayari kumsomesha, nataka asome. Sasa labda unipe mpango mwingine.” “Ndani ya huo mwezi nitakuwa nishapata jibu. Lakini usimgawe mwanangu. Hata kama ni Kayumba, atasoma tu.” “Hapo hapana Jelini. Hatasoma Kayumba, kama kuna uwezo.” “Basi nipe huo mwezi.” “Na nikiona tabia zako za ulevi bado zipo halafu hubadiliki, Jema akija kumchukua, ujue nampa.” “Sawa. Na samahani Jeremy. Jana nililewa. Lakini mimi sikugawi.” Mwanae akanyamaza tu. “Hata mtoto mwenyewe hakuamini.” Akamwangalia mwanae na kuingia ndani akilalamika.

“Msimgawe mwanangu kama mzigo. Mimi bado namtaka mwanangu. Pombe ndio zinanifanya vibaya.” “Kwani unanyweshwa?” “Si ndio nimesema naacha sasa! Mbona hamniungi mkono?” “Labda kwa sababu kila siku unasema jambo halafu unageuka.” “Haya, mwanao huyo, umemsikia. Hata yeye amechoka.” “Mimi nataka kusoma. Nataka kusoma sana ili nije kukusaidia na wewe baadaye.” Wakamsikia akilia ndani. “Soma mwaya Jeremy labda kweli utamsaidia huyo.” Akalia wee, mwishowe kimya.

“Kashalala hivyo. Akiamka hapo safari ya baa.” “Sijalala, nawaza. Na wala baa mimi siendi tena. Labda..” Mama yake akaanza kucheka nje baada ya kusikia, ‘labda’. Jelini akaona anyamaze tu maana alishaahidi sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akabaki akijitafakari hapo kitandani mpaka akaanza kuingiwa hofu. Mara ngapi amekuwa akilewa na kuamkia asipopajua! Nini anafanya akiwa amelewa bila kichwa chake kutunza kumbukumbu! Akaogopa sana kila alipokuwa akikumbuka na maneno ya Zenda. Akaamua kujiangalia afya yake. “Wasijekuwa wanakuwa wakinifanyia mambo mabaya wakinipa pombe zao za bure.” Akafikiria bia za bure anazopewagwa baa, lakini akiwa na akili zake anawakataa. “Je nikiwa sijitambui!” Hofu ikamuingia zaidi. Akakumbuka Zenda alimwambia huwa anakuaga na kipimo cha UKIMWI.

Usitukane Mamba, Bado Hujavuka Mto.

Akaoga haraka na kubadili nguo. Akampigia Zenda. Ikaita sana, wakati inakaribia kukatika akapokea. “Uliniambia una kipimo cha kupima UKIMWI. Naomba nije nipime.” “Wewe ni mtu wa ajabu sana Jelini! Umenikatia simu kitu ambacho hakuna mwanadamu anaweza kunifanyia hivyo na kunikatalia kwa jeuri kwa kiasi hicho. Wewe kwa nini unakuwa mtu wa kupenda kutumia watu tu?” Jelini hakutegemea! Kutoka kwenye kubembelezwa mpaka kukaripiwa! “Sasa kwa kuwa umeshindwa kuniamini na unanidharau, na mimi SITAKI. Nenda kaangalie afya yako hospitalini ambako utakuwa salama nao, sio mimi.” Simu ikakatwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Hilo wazo ulilokuwa nalo naunga mkono, na usibadili mawazo. Nenda hospitalini ukapimwe ujijue. Unanisikia Jelini?” “Naenda mama.” “Usikatishwe tamaa. Na achana na huyo Doro. Ndiye anayekurudisha nyuma kila siku. Siku mbili tatu ulizomkatalia kwenda kwake, ukatulia hapa nyumbani, ukawa mtu. Jana umekutana naye tu, akili zikawapaa, mmelewa na kuondoka na mwanaume hata msiyemjua. Hujui anagonjwa gani! Hujui kama alitumia kinga au la. Kama kweli unataka kuanza upya, nakuunga mkono, nenda kapime ujijue.” “Sasa kwa nini unasikiliza nikizungumza na simu zangu?” “Uliyeongea naye huko sijamsikia. Ila wewe tuliyekuwepo wote hapa, hukufanya siri. Wote tumesikia. Na nakupongeza Jelini mwanangu.” Akamtia moyo ili asije gairi.

 “Sasa kama nimeathirika?” Jelini akauliza kwa wasiwasi. “Ndio utaanza kuishi kama muathirika, na kutumia madawa. Ila ujue ndio Jema kajipatia mtoto. Sitakubali umkwamishe Jeremy kwa shida wala raha zako. Ukienda kukutwa na gonjwa huko, jua na mtoto huna.” “Sasa mbona naogopa?” “Mwana kulitafuta.” Mama yake akamjibu yeye akiwa chumbani, mama yake sebuleni na Jeremy anasoma mezani.

“Kwa nini sasa unaniambia hivyo?” Akaanza kulalamika. “Wewe ni mara ngapi umeniona mimi silali humu ndani?” Kimya. “Hata siku moja. Kama sipo hapa mjini nipo kwa mama yangu kijijini nakwenda na Jeremy kwa kuwa sikuamini naye, unaweza ukaondoka na kumuacha hapa. Lakini je, bia sinywi?” Kimya. “Nakunywa na kurudi nyumbani na akili zangu timamu, au nakuja kunywa hapa nikimuona Jeremy, au hata nikitoka naenda kumuacha kwa bibi zake, nawahi kumchukua, na kurudi naye nyumbani. Lakini wewe kichwa chako hakifikirii. Kinakwenda kutafuta pombe, basi.” “Nabadilika. Na…” “Wewe usiongee sana. Anza hatua ya kwanza uliyoamua, na ili pia tukuamini, urudi hapa na majibu. Sio ukutane na bia za bure huko, unywe na kwenda kulipa fadhila huko usiku kuchwa.” Jelini akazidi kuogopa akishindwa kujibu kama kweli analalaga kwa wanaume au la. Akatoka.

Mbio Za Sakafuni, Sasa Ukingoni.

Huku kwa Joshua na Geb wakaegesha magari yao nje ya hiyo nyumba waliyoelekezwa na kuingia ndani. “Kwamba ndio hakuna hata milango na madirisha!” Akashangaa Joshua kwa kuumia. “Nafikiri ndivyo alivyomaanisha yule mlinzi akipaita gofu.” Geb akajibu wakiingia ndani. Harufu mbaya sana ikawafanya wasimame hapo mlangoni wakaangaliana. Kulikuwa kunanuka kama kulioza kundi la panya.

“Bale?” Akaita Joshua. Akaita tena na tena, kimya. Wakaona waingie tu. Ndani kulikuwa kuchafu mno. Wakaanza kuingia kila chumba wakimuita. Wakasikia mtu akikohoa chumba kingine. Wakaingia na kumkuta mtu amelala juu ya maboksi tu na mengine amefunika miguu. Joshua akahisi atakuwa yeye tu. “Bale?” Akamuita tena kwa kumuhurumia sana, hakujibu. “Acha nipigie simu gari ya hospitali, waje wamchukue. Wao wataweza kujua jinsi ya kumtoa hapo nakumuweka ndani ya gari kwa usalama huku wakimpa huduma ya kwanza bila kumdhuru zaidi.” Geb akatoka baada ya kutoa hilo wazo. Joshua akaenda kumshika. Alikuwa anachemka joto, anagugumia kwa sauti ya mbali, kama mwenye maumivu makali sana. Akamtizama mguu kuhakikisha aliyoambiwa. Akawa ameufunika na boksi, unatisha hata hautizamiki.

Joshua akajikuta akilia sana. Alilia, mpaka Geb akarudi ndani. “Tafadhali jikaze Joshua. Gari ya hospitali inakuja.” Geb akajaribu kumtuliza lakini hata yeye alijua hali ni mbaya. Bale aliotwa nywele kama msitu kichwani na mandevu. Chafu. Amekonda kupita kiasi. Ananuka, kuwepo karibu yake ni mpaka uwe ulimfahamu baba yake, na unaishi na dada yake kama mke, na ni rafiki wa Joshua ambaye anakubeba kipindi cha shida yako. Geb akatulia.

Ndani ya nusu saa, gari ya wagonjwa ikawasili wakamtoa Bale pale sakafuni, lakini hata wenyewe walikuwa wakilalamika hali mbaya. Alikuwa akitoa harufu mbaya sana kama aliyeoza. Wakachana maguo aliyokuwa amevaa, wakamfunika shuka la hospitali wakati mmoja akimtafuta mishika ya kumuwekea maji. Wakahangaika naye, baada ya dakika 15 nyingine ndipo wakamtoa hapo akiwa na maji kwenye mishipa, safari ya hospitalini ikaanza. Joshua na Geb wakifuata gari ya wagonjwa nyuma wakikimbilia hospitalini. “Wewe ni Mungu, na badala yako hakuna mwingine.” Hilo akalirudia Joshua bila kuchoka mpaka wanafika hospitalini.

Kulikosifiwa Mgema!

Jelini anafika hospitalini, na Bale naye anafikishwa hospitalini ila kila mmoja kwa shida yake. Hofu iliyokuwa imemkamata Jelini, ilizidishwa na vile alivyokumbuka hali ya Doro, alipogundulika anagonjwa la zinaa kali, huku ana vijidudu vya UKIMWI. Kilio chake na maneno yake akihuzunika kuwa maisha yake ndio yamefika mwisho, vyote vikawa vikijirudia kichwani kwa Jelini anatetemeka kama ameshikwa baridi. Hapo amekaa akisubiria zamu yake, maneno yote ya hofu ya Doro yakawa yakijirudia kichwani mwake, ndipo akaelewa hofu ya  Doro. Hofu ikamzidia, akashindwa kujituliza kabisa.

Akatamani kama angekuwa na yeye na mtu kama vile yeye alivyofanyika faraja kwa Doro. Angalau awe naye hapo, aongee chochote, lakini akajikuta hana mtu. Jema yupo fungate. Mama yake anasubiria majibu nyumbani. Gafla akakumbuka ahadi ya Zenda. Utayari wa kuwa naye karibu kwenye mabadiliko yake. Akaumia jinsi alivyomuudhi. Akaongezeka mwingine tena aliyemuumiza, mbali na Jeremy, akawa na huyo Zenda. Akaamua kumtumia ujumbe. ‘Mwenzako mimi ni mtu mbaya, Zenda. Ninamkosea kila mtu. Ila naomba msamaha. Nilikosa adabu.’ Akatuma huo ujumbe. Baada ya dakika 5 akaona simu ya Zenda inaingia. “Nimekuudhi sana?” “Ndiyo.” Zenda akamjibu. “Nisamehe. Nilikukosea sana. Ila mwenzio nimechukua ushauri wako. Nipo hospitalini.” Zenda akacheka maana alimwambia tu kwa hasira. “Wapi?” Akamuelekeza. “Nakuja tuwe wote.” Jelini akajishangaa anaanza kulia. Wema aliomtendea Doro, ukawa haujaoza. Na yeye akapata mtu. Akajisikia kulia kwani alikuwa ameingiwa hofu na mpweke. “Usilie nakuja.” “Asante.” Safari hii akamuacha yeye ndio akakata simu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hata haikuchukua muda mrefu sana, Zenda akawasili hapo hospitalini. Alipomuona akimsogelea akasimama. “Nimefurahi umekuja Zenda. Mwenzio naogopa sana.” “Njoo tukae hapa na uniambie nini kinakuogopesha.” Wakaenda kukaa sehemu wakijitenga na watu. “Nini kinakuogopesha?” “Mimi najua watu wanao ambukiza watu kwa makusudi kama kulipiza kisasi.” “Kama Doro?” Jelini akashituka sana. “Mimi sijamtaja mtu jina!” “Niliunganisha mazungumzo yetu na vile nilivyokusikia ukimwambia asubuhi ulipogundua amelala na Kevin.” “Kumbe kule nje mlikuwa mkisikia!?” “Sikuwa nimeelewa mpaka tulipokuwa wote garini. Nitataka kujua ni kwa nini anafanya hivyo. Ila nataka kujua ni kwa nini wewe una hofu.”

“Nimejifikiria na kujiuliza, usiku kama ule wa jana kuamkia leo, kwenye maisha yangu imetokea mara ngapi maana huwa sikumbuki! Na je, huwa nikiwa nimelewa, nani ananichukua na nini kinatokea nikiwa sijitambui! Maana inaonekana nafanya mambo ya ajabu sana. Kwa mfano jana nasikia nilimgawa mtoto wangu hadharani. Nimefika leo ananiaga, hata sijui kilichoendelea!” “Usilie.” “Mimi niache nilie tu. Nasikia uchungu. Nilimgawa mwanangu eti na kusema simtaki! Yaani Jema akiwa katikati ya fungate ndio anamfikiria mwanangu na kumtumia ujumbe kuwa wamekubaliana na mumewe watamchukua wamtunze wao, halafu mimi sina habari! Namwambia mama ni pombe tu, sijamaanisha, ameniambia nikirudi na vipimo sijaathirika, ada yake, na mabadiliko ndio hatamgawa mwanangu. Kwa kuwa yeye anataka Jeremy asome sana.” “Sasa nisikilize Jelini. Hiki unachokifanya nakiunga mkono sana.” Akamfuta na machozi kama katoto kadogo.

“Kujua afya yako ni jambo la msingi. Na kingine ambacho lazima kujua, unaweza kurekebisha kuanzia hapa tulipokaa, kwenda mbele. Nyuma huwezi tena. Kama ulishaharibu, umeharibu. Lakini kuanzia sasa, unaweza kubadili. Kujutia, na kujilaumu, nikupoteza muda na haitakusaidia wewe wala Jeremy. Tukitoka hapa tutazungumza zaidi maana na mimi nina maswali mengi. Tulia, pima, kisha tukitoka hapa, tutapata muda.” “Asante Zenda.” Akaendelea kumfuta machozi kwa upendo, Jelini akafurahia kupendwa vile.

 “Kumbe kweli kupendeza ni kawaida yako!” Akamfanya Jelini acheke sana. “Kwa hiyo hata hapa nimependeza?” “Sana tu.” Wakacheka na kutulia. Akajisogeza vizuri kwa Zenda, akapitisha mkono kwapani kwake, akamvuta kwake karibu na kumuegemea. Zenda akacheka akili ya Jelini. Hapo anafanya hana hata wazo la pili kufikiria macho ya watu au hata kama huyo Zenda amemruhusu! Yeye amejisikia kumsogeza kwake akafanya na kujituliza vizuri utafikiri anamfahamu huyo Zenda kwa miaka mingi. “Ukitulia hivi unakua mtoto mzuri!” Jelini akacheka taratibu akifikiria huku amekumbatia mkono wa Zenda kuanzia chini ya bega.

“Nitabadilika. Ila nina hofu sana.” “Kwani wakati mwingine huwa unaamkia wapi?” “Kwa dada Doro. Ila najiuliza kabla ya hapo nakua wapi na huwa nafanya nini! Maana tunakua katikati ya kundi la watu wengi. Mimi na dada Doro tu ndio wanawake, wengine wote wanaume.” “Kati ya hao kuna ambao ulishakuwa nao kwenye mahusiano?” “Kwa akili zangu hizi, hapana Zenda. Ni wale wanaume malaya wakulala na yeyote, tena wala si kwenye nyumba za kulala wageni kitu ambacho ndio kinanitia hofu. Wanamalizanaga nao hapohapo baa! Sasa mimi nilishawakatalia tokea mwanzo, tena niliwaambia wao ni wachafu hata kwa kuvaa kondomu mimi siwataki. Na usifikiri ni wanaume wa hovyo! Watu na hadhi zao kabisa. Wana mahela, kwa hiyo tupo kama washikaji tu kupeana kampani. Ila sasa ndio nimeingiwa hofu.”

Zenda akamshika mkono vizuri akipishanisha vidole kama kumtuliza. “Aisee naogopa Zenda, naogopa sana. Maana ni wale wanaosema sio sabuni kwamba itaishia baa, nakushindwa kufikisha nyumbani kwa wake zao. Wachafu wakulipia hata kunyonywa tu, halafu wanarudi kwa wake zao. Malaya wanawajua kama wanazo pesa na wanataka huduma. Sasa sijui aisee!” Zenda akabaki kimya akiwaza binti kama huyo anaishi vipi maisha kama hayo! Akaminya mkono taratibu kama kumtaka atulie. Wakatulia mpaka ilipofika zamu yake, akatolewa damu na kusubiria majibu.

“Utafanyaje juu ya Kevin?” Akacheka na kumgeukia. “Kwa hiyo sio Kasa tena narudishiwa jina langu?” “Hapana bwana! Wewe utabaki kuwa Zenda. Mbona zuri tu! Au hujalipenda?” “Jinsi unavyolitamka linavutia. Sijawahi kupewa nickname.” Wakacheka. “Kevin ameshapima. Na nimemwambia nitamtaka na vipimo vya hospitalini mpaka magonjwa ya zinaa.” Jelini akashangaa sana. “Kwa nini?! Si anasema alitumia kinga?” “Kumdhalilisha zaidi. Nakumfanya azidi kuongeza umakini.” Jelini akifikiria akimtafakari Kasa, Kevin vile alivyo jeuri. “Asipokubali kupima?” “Hathubutu kwa kuwa hataki kukabiliana na madhara ya kutotii.” Jelini akawa hajaelewa.

“Kevin ni jeuri wa kurithi kwa mama yake, lakini anapenda starehe ambazo pesa yangu ndio inamsaidia kuishi anavyoishi kwenye jamii. Kama isingekuwa ni pesa yangu, nina uhakika asingekuwa akinitafuta kabisa hata kwa salamu, sababu ya upendo kwa mama yake. Sasa kwa kuwa anaishi kwenye nyumba zangu na kutumia pesa zangu atakavyo akijiaminisha yeye ndio mrithi, nikifa kila kitu kitabaki kuwa chake, inabidi aendelee kujinyenyekeza tu kwangu. Lakini si kwa mapenzi kwangu au kupenda kwake. Yeye ni miongoni mwa wengi wanaonifuata sababu ya nilicho nacho ili kujinufaisha. Kwa hiyo hana jinsi. Lazima atafanya kila ninachomuagiza.” Kidogo Jelini akamuhurumia, akamvuta mkono zaidi na kujiegemeza, akabaki kimya akitafakari.

Akaitwa kuchukua majibu yake, ikawa hajaathirika. Alifurahi Jelini, nakujikuta akilia tu. Akatoka hapo hajui aendapo ila machozi tu akiendelea kuongoza njia. “Sasa unaenda wapi?” Ikabidi Zenda asimame na kumuuliza. “Nimefurahi sana Zenda, siamini! Acha tu niende.” “Wapi?” Ndipo akasimama na kujikuta yupo nje sehemu yakuegeshea magari. Akaangalia kulia na kushoto, akaanza kucheka. “Muone!” “Nimefurahi! Nimefurahi sana. Nilikuwa nimeingiwa hofu. Nikajua nitakufa nimuache mwanangu.” “Hilo ni onyo, Mungu amekupa, kisha na nafasi ya pili Jelini. Usibwete, tumia vizuri.” “Nabadilika. Na sasahivi nitaongeza umakini zaidi.” “Twende basi tukale chakula kizuri, kusherehekea.” “Sasahivi nakubali. Tutakwenda wapi?” “Wewe unataka nini?” Akamwangalia na kucheka.

“Umewaza nini huko kichwani kwako kilichokufurahisha?” “Natamani tukae kama tulivyokaa pale hospitalini. Ilinituliza.” Zenda akacheka taratibu akimwangalia, Jelini akaona aibu. Zenda alibeba uzuri wa Kirwanda. Mrefu amenyooka kama raisi wao Kagame. Halafu akapewa rangi nyeupe pee iliyomvutia Jelini mpenda wanaume weupe. Bila kutongozwa akajikuta anaanza kuvutiwa naye. Halafu akajaliwa unadhifu wa pesa. Akajua kuuvalisha mwili wake vizuri. Alivutia, jinsi alivyokuwa akimwangalia hapo Jelini, mwenyewe akalainika. “Nilikuona vile ulivyokuwa ukitetemeka.” “Lakini si uliona nilitulia?” Akamuuliza kwa upendo kama si yeye aliyemkatia simu. “Nilikuona.” “Kuna hali fulani hivi, mwenzio nilijisikia. Nataka nijaribu tena, nione kama nitatulia ili nifikirie na kuweza kujua chakufanya.” “Na chakula?” Jelini akabaki akifikiria. “Twende tukale kwanza halafu tutapata muda wa kutulia.” Akakubali.

Akatafuta sehemu nzuri, ya hadhi yake yeye, tulivu, wakaingia humo. “Nataka kukaa pembeni yako.” “Nataka ukae mbele yangu, nile nikiwa nakuangalia.” Jelini akacheka na kukaa mbele yake. Zenda akaagiza juisi ya embe akiomba iwekwe ndimu ila akaomba starter kwanza. Supu ya mbogamboga. Jelini na yeye akasema aletewe kama Zenda. “Wewe huwa unaongea ukila?” Akacheka na kumuuliza. “Ulitaka kuongea nini?” “Kwa mtu ambaye hajasoma kabisa, anaweza kufanya kitu gani cha kumuingizia pesa?” Zenda akakunja uso akifikiria.

Kisha akamuuliza. “Ukisema hajasoma, unamaanisha hajui hata kusoma na kuandika?” “Anajua hivyo bwana! Sasa wewe unafikiri kuna mtu wa namna hiyo?” Akacheka akiendelea kufikiria. “Kwanza nitataka kujua ni kwa nini hajasoma. Uwezo au mazingira ya shule hayakuwa rafiki au hapendi tu shule! Ikiwa ni moja wapo ya sababu hizo mbili za mwanzo, huyu mtu ni rahisi kumshauri. Lakini kama ni mvivu tu wa shule, hataki ile shida ya shule, kuamka asubuhi na ile kuweka jitihada, inamaana huyu mtu hata akipewa kazi au biashara ataharibu tu kwa kuwa hana ile inayohitajika kufanikisha jambo gumu. Sasa sijui kama unanielewa?” Jelini akanyamaza kabisa.

“Mbona tena kimya?” “Wewe unaongea kisomi sana bwana.” Akalalamika. “Nakwambia ukweli wa maisha Jelini na wala hapo hakuna usomi. Labda uniulize swali katika nilichozungumza ambacho hujaelewa.” Kimya. “Hicho unachokificha ndilo jibu lako lilipo.” “Sasa si ujibu tu! Kwamba kwa mtu ambaye hajasoma sana, ila anajua kusoma na kuandika, anaweza kufanya nini kuingiza pesa?” “Japokuwa unakwepa ukweli wa kwanza, labda niulize huyo mtu anapenda nini?” “Labda hajui.” Akabaki akimwangalia kwa mshangao.

“Basi labda niseme hajafikiria.” “Kwa sababu si wote waliofanikiwa kwenye biashara, wamesoma sana. Na pia hakuna uzee kwenye elimu. Hata mtu kama mimi nikiamua naweza kurudi shule na nikasomea kitu fulani na nikafanikiwa kabisa.” Hapo Jelini akakwama. Arudi shule! Hakutaka kabisa. Akapoa, na yeye akamuacha. Kwa chakula Zenda akataka kiazi ulaya kilichookwa na Crub. Jelini akatoa macho. “Nzuri sana. Ila wewe unaweza kuagiza na samaki au kuku wa kuchoma. Nitakuonjesha crub. Ukipenda siku nyingine ndio uagize.” Akaona wazo zuri, akaagiza hicho kiazi ila na samaki wakuchoma. Wakatulia mpaka chakula kikaletwa.

“Mbona vyako vinaonekana vizuri?” “Acha nikuonjeshe uone ladha. Unaweza kupenda.” Akamuona anatumia kisu na uma kutoa nyama ndani ya huyo crub kisha akamlisha. “Nzuri!” Akapenda. Akamuona anamuita muhudumu. Akamuagiza crub kama wake. “Usiingie garama Zenda! Acha mimi nile tu samaki, siku nyingine ndio nitaagiza.” “Usijali.” Wakaendelea kula. “Nipe uma wako nikuonjeshe samaki. Ana ladha nzuri sana.” “Kwani uma wako una nini?” “Nimetia mdomoni tayari, Zenda!” “Hamna neno.” Jelini akasita. “Sitaki kukulisha uchafu wangu.” “Wewe si mchafu. Nipe tu.” Ikamgusa sana Jelini. Kwamba hamuonei kinyaa! Akamkatia. “Hiyo ni kubwa sana.” “Utafurahia. Fungua mdomo.” Akamuwekea na kubaki akimwangalia ili asikie anasema nini juu ya huyo samaki aliyemuwekea mdomoni.

“Umependa?” “Ulivyonilisha, ndiyo. Ila hawa samaki wa hapa nawafahamu.” Jelini alicheka sana. “Zenda!” “Nisingekuleta sehemu ambayo wanavyakula vya kubabaisha. Huwa nakula hapa karibu kila siku. Napenda vyakula vyao.” Jelini akatulia akimtafakari huyo Zenda. Na Zenda naye kimya akimtafakari mtoto mzuri Jelini. Wakala mpaka wakamaliza.

“Bado unataka kuwa karibu na mimi au umeshatosheka?” “Tena kidogo tu halafu ndio niwahi madukani nikaangalie vitabu vya watoto. Jeremy anapenda kusoma vitabu.” “Vya aina gani?” Hapo akatulia. “Jelini!?” “Sijui.” “Kwamba hujui mtoto anapenda kusoma vitabu vya namna gani?!” “Naomba usinishangae Zenda.” “Labda niulize sasa wewe ungeenda kumnunulia vitabu gani?” “Nilikuwa sijalifikiria hilo. Ila naweza kumpigia simu nikamuuliza.” Zenda akabaki kimya akifikiria.

“Cha kwanza mnunulie tu kama surprise. Hata ukikosea, lakini atajua unamfikiria. Halafu kuanzia hapo tafadhali onyesha unajali Jelini.” “Nitabadilika.” Wakatoka hapo. “Kama una mambo mengi yakufanya nisikucheleweshe Zenda. Mungu atatujalia tutapata muda wakati mwingine.” “Usijali. Twende tukakae sehemu ndipo tuagane.” “Wapi?” “Hofu na mimi imeisha?” Jelini akacheka akimwangalia kwa aibu kidogo, maana Zenda alimtizama kiume. “Eti Jelini?” “Wewe nimeanza kukuamini.” “Kwa hiyo hutaogopa ukijikuta sehemu tuko peke yetu?” “Hapana Zenda. Sitaogopa. Nakuamini.” “Kama ndio hivyo twende.” Akampeleke mpaka ufukweni. Hapakuwa mbali sana na walipopata chakula. Ila hawakuingia kwenye hoteli.  Pembeni tu ya barabara ila upande wa baharini. Akatafuta sehemu nzuri, akaegesha gari.

“Si unataka kukaa karibu yangu?” Akatingisha kichwa kukubali akitabasamu. “Basi tukae hapo nyuma kwa muda mfupi, ukiridhika na kuniruhusu, tutaondoka.” “Sawa.” Wakahamia kiti cha nyuma. Jelini akajisogeza karibu kabisa, akamnyanyua mkono akajiingiza chini ya kwapa kabisa, Zenda ametulia tu akimwacha ajiweke sawa ila akimsaidia kufanya anachomulekeza kwa vitendo. Akajipanga hapo pembeni ya kifua chake, akapandisha miguu juu, akatulia. Akajua ameridhika na alivyokaa. Akamuwekea mkono juu, akambusu kichwani pale alipojiegemeza kwake. Wakatulia kabisa lakini akamfanya Jelini ajisikie kitu cha tofauti.

Akili Za Mungu Zisizochunguzika.

Huku kwa Bale, hospitalini alifikishwa mapokezi, hata daktari akawaambia anahitajika chumba cha upasuaji akatwe sehemu ya chini ya mguu ambako kulishaoza. “Atahimili upasuaji kweli! Yupo dhaifu mno.” Joshua akauliza kwa wasiwasi asijefia chumba cha upasuaji. “Hatapewa dawa ya usingizi kabisa. Itabidi apate ganzi tu ya mguu ili kuweza kukisafisha hicho kidonda na kutoa nyama zilizooza. Ila kwa jinsi ninavyokiangalia, itabidi akatwe tena kidogo.” Joshua akaumia sana.

“Joshua, nadhani kwa sasa huna chaguzi ila kukubali ahudumiwe kwa haraka. Bale anahitaji msaada wa haraka.” Ikabidi Geb amuongeleshe maana ni kama alipoa hivi, akikumbuka maisha ya hao watu jinsi alivyowakuta kwao Kiluvya. Familia ya maana tu, yeye akiona imebarikiwa hata nakutamani na yeye angekuwa ametokea hapo. Bale akiwa na nguvu zake. Amemaliza shahada yake ya kwanza, akiwa na kiu ya maendeleo! Akajikuta akimalizia mawazoni, “Malon!” Akaumia sana.

“Ila mjue kwa hapa na hizo huduma zote kama mtaridhia, itawagarimu sana. Labda mumpeleke kwenye hospitali za serikali.” Daktari akawatahadharisha. “Hapana. Pesa isiwe tatizo. Maadamu yupo hapa, tafadhali msaidie tu.” Joshua akaridhia. Bale akaingizwa chumba cha upasuaji akabaki Joshua na Geb.

“Nashukuru Geb, lakini nashauri wewe rudi nyumbani angalau ukapumzike. Itoshe kwa leo. Kukitokea chochote nitakujulisha.” “Unauhakika Joshua?” “Huna unachokifanya hapa, na kama ulivyosikia, inaweza kuchukua muda mrefu. Wewe nenda tu kwa familia yako. Wasirudi na wewe haupo. Acha madogo wamalizie weekend na wewe. Sisi tutawasiliana tu.” Geb akaondoka, akamuacha hapo Joshua.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamkumbuka mkewe, akampigia. “Ulifanikiwa?” “Nilimpata. Lakini hali yake si nzuri. Ni mgonjwa sana. Sasa hivi yupo chumba cha upasuaji, ndio namsubiria atoke.” “Pole Joshua. Bado upo na Geb?” “Nimemruhusu akapumzike. Maana inaweza chukua muda mrefu.” “Basi mtume dereva aje anichukue nije tukae wote.” “Una uhakika?” “Kabisa Joshua. Ulivyojitoa hivyo! Acha na mimi nitembee kwenye imani yako. Nitajificha mpaka lini?” “Na utakuwa na mimi. Huna haja yakuogopa.” Naya akacheka akianza kujiandaa.

Baada ya muda akawa ameshafika kwa mumewe wakimsubiria Bale nje ya chumba cha upasuji. Naya akaona aulize. “Joshua? Ni kwa nini unafanya yote haya, tena kwenye hospitali kama hii ya garama!?” “Sijui ni kwa nini mimi, Naya! Maana Mungu angeweza kumtumia yeyote kufanya hili, ila naona amenituma mimi nifanye. Ameweka mzigo moyoni mwangu, siwezi kukwepa. Halafu ni vile humkumbuki baba yako Naya. Yule mzee aliwapenda kupita nafsi yake. Angefanya chochote kwa ajili yenu. Sisahau jinsi alivyojitoa mpaka nafsi yake kwa kumtafuta huyuhuyu Bale. Alikubali hata kuuwawa ilimradi tu, ampate huyu Bale. Sasa wewe jiulize, huyu Mungu aweke huo mzigo kwa mtu kama baba yako na kwangu pia, kwa mtu mmoja tu!” Tayari akaanza kuhamasika mwenyewe.

“Yaani huyu Mungu mwenye enzi yote, anasimamisha ratiba zangu mimi! Mpaka kula siwezi kwa ajili ya Bale tu ambaye kwa kibinadamu ni mkosaji sana. Hastahili. Lakini nashangazwa na huyu Mungu Naya! Amekubali yangu yasimame kabisa, ili kufanya alichokifanya kwa Bale! Mimi sijui anakusudi gani naye, ndio maana nimekubali kutii, ili na mimi nishuhudie kwa macho. Maana Mungu anapoamua kufanya jambo lake! Hajui kupunja na hanaga mipaka. Anaweza kuinua hata mawe, ila akatuchagua sisi. Naomba sisi tutii tu Naya.” Akaendelea.

“Sauli alilitesa sana kanisa la Mungu. Akiwaua wana wa Mungu waliompokea Yesu kama Kristo. Akafanya hivyo kwa muda mpaka Yesu mwenyewe alipoingilia kati akiwa tena njiani kwenda Dameski kungamiza zaidi wana wa Mungu. Hakustahili, lakini ona aliyoyafanya baada ya kukubali na kutubu. Leo tunasoma bibilia na inatusaidia wengi wetu kwa sababu asilimia kubwa aliyeandika ni huyu muuaji Sauli aliyebadilika akawa chombo na msaada wa kanisa.”

“Mungu ana mambo yake, Naya! Mimi mpaka huwa naogopaga kumuuliza kwa nini, nabaki kusubiria mwisho wa kazi zake. Kwa hiyo na wewe nakushauri fungua tu moyo, utaona tu mkono wa Mungu. Kibinadamu ni ngumu sana, lakini mwache Mungu afanye yake. Atasawazisha kwa namna yake mwenyewe.” “Nimeelewa Joshua.” Naya akatulia kabisa akiwa amefunguliwa moyo, na yeye akitaka kumsaidia Bale.

Alichukua muda mrefu tu chumba cha upasuaji, lakini akatoka. Angalau harufu mbaya iliisha kabisa. Ila akaambiwa ilibidi kukatwa mpaka karibu kabisa na goti. “Mpaka mfupa mkubwa ulikuwa umeoza. Lakini kwa alivyosafishwa. Na akiendelea na matibabu kitakauka haraka.” “Aliweza hata kufungua macho?” “Yupo macho, ila nafikiri ni mdhaifu tu.” “Nashukuru sana kwa huduma yako. Na wauguzi waliomsaidia pia.” “Karibu.” Akapelekwa wodini ambako kwenye hospitali hiyo hulazwa watu wawili. First class ya garama zaidi ndio mtu mmoja.

Bale akawekwa sehemu yake, akaunganishiwa kila kitu akabakishwa na mirija ya mkojo, akabaki amejilaza. “Pole Bale.” Naya akamsogelea karibu akijaribu kumuongelesha. “Asante. Akajibu akiwa amefunga macho.” “Unasikia njaa?” Naya akaendelea kumuuliza, Joshua akimsikiliza tu. Bale akakubali. “Ataletewa chakula muda si mrefu, na baada ya muda ataongezewa sindani ya maumivu. Atakuwa tu sawa.” Muuguzi aliyekuwa akimalizia kumuweka sawa akawaambia.

Wakakaa hapo wametulia mpaka chakula kikaletwa. Joshua akaanza kumlisha taratibu, akala chote, akamaliza. “Vipi, umetosheka?” Akaomba maji. Akamnywesha na kumfuta, akamrudishia alale vizuri. Kwa mara ya kwanza roho ya huruma ikamuingia Naya. Damu nzito kuliko maji. Japokuwa hakuwa akimkumbuka tokea maisha ya nyumbani kwao ila ukatili kwake, bado akamuhurumia sana. “Tumuombee kabla hatujaondoka.” Naya akatoa wazo.

“Bale!” Joshua akamgusa. Akafungua macho. “Ni sawa tukiomba hapa kwa ajili yako?” Akakubali na kurudi kufunga macho. Joshua akamvuta mkewe pale karibu maana alikuwa akichungulia kwa mbali kidogo. Bale aliyemfanyia ukati alipomteka na huyu ni watu wawili tofauti. Huyu alitisha kwa manywele na ndevu. Amekonda kabaki mifupa. Geb akaanza kuomba rehema kwa ajili yake. Akatubu mbele za Mungu na akikumbusha kazi ya msalaba ni kwa wakosaji, akamuombea rehema Bale. Joshua aliomba kwa uchungu sana akiugua, akimsihi Mungu amguse tena Bale.

Wakati wakiomba, akafungua macho akamuona Naya, akaanza kulia akiita mama. Alilia sana Bale. “Naumwa mama! Nimechoka, nimekosa, sijui nifanye nini!” Akalia kwa uchungu akizungumza na Naya kama mama yake. Joshua akakumbuka kusikia Naya anafanana sana na mama yao. Akajua madawa yamemzidi Bale, anahisi Naya ni mama yake. Aliongea mengi akimwambia Naya kama mama yake mpaka muuguzi akaingia nakumkuta anaongea mambo mengi mpaka mtiririko wa maneno ukapotea akawa kama mwehu. Anaongea kila kitu mvurugiko mpaka mengine wakawa hawaelewi. Naya akawa akilia kwa hofu. Akaitwa daktari kwa haraka maana alikuwa akihangaika, Joshua amemshika ili asije kujitonesha. Akamuongezea sindano, ndipo akapotelea usingizini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Hujafa, Hujaumbika! Hakuna Umbali mwanadamu anaweza kumkimbia Mungu.

Na,

Pombe si Chai. 

Ipi Historia ya Doro Naye?

Itakuaje Kwa Bale?


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment