Akajaribu kusogea
mlangoni ili ajaribu kutoka, milingo ilikuwa imefungwa na hapakuwa na funguo
kama alizozoe kwao. Akashangaa sana. Akaenda dirishani ili kuangalia nje
pengine atapatambua. Akaona mtu nje kwa kupitia kioo cha dirisha akiwa anasogea
mlangoni. Akanyanyua pazia vizuri kwa
haraka huku akijitokeza.
Yalikuwa madirisha
mazuri sana. Juu mpaka chini sakafuni. Akampungia mkono kwa nguvu kama
amwangalie. Alikuwa mwanaume msafi sana, aliyevalia ramsi. Mtu mzima si kijana
mdogo. Akamuona Jelini. Akasogelea upande wa dirisha. Jelini hakuwahi kumuona
kabla na akashindwa kumtambua. Wakabaki wakiangaliana.
“Unataka kuingia humu
ndani?” Jelini akamuuliza. Akamuonyeshea ishara yakukubali, ila akamwambia
asifungue. Hapo akamchanganya Jelini. “Kwa nini sasa!?” Jelini akamuuliza
akimshangaa kwamba anataka aingie lakini asimfungulie! “Alam.” Akamwambia
hivyo, Jelini akawa hamuelewi. Kila alivyokuwa akitaka kuondoka akamfungulie,
alimkataza. “Hutaki kuingia!?” Ikabidi amuonyeshee simu yake na kumwambia na
yeye akachukue simu yake. Akaelewa na kukimbilia chumba alichoamkia kujaribu
kuangalia kama alifikishwa hapo na vitu vyake!
Akaangalia pale
kitandani hapakuwa na pochi. Chumba kilikuwa kikubwa na makochi, makabati
yanayofanana na hicho kitanda. Meza nzuri sana za muuondo nadhifu. Jelini akashangaa
sana. Huyo tajiri hivyo alimtoa wapi kwenye harusi ya dada yake! Chumba chenyewe
chaweza kuwa nyumba na thamani ya familia nzima. Akarudisha mawazo kwa
yanayomuhusu. Kwa harakaharaka hakuona chochote kinachomuhusu ila kumepangwa
nadhifu, takataka yake angeona tu. Akataka kukata tamaa, akaamua kuzunguka
kitanda na kutafuta hata chini ya uvungu, ndipo akakutana na viatu vyake
alivyovaa harusini pamoja na pochi yake, akaiokota na kutoka nayo kwa haraka
akimuwahi aliyemuona nje amsaidie kujua hapo ni wapi na kama hayupo salama,
basi amuokoe.
Akamkuta bado
amesimama palepale nje upande wa dirisha. Akachukua simu. Akamwambia aandike
namba yake ya simu kwenye simu yake kisha amuonyeshe. Jelini kwa kusoma midomo
yake akaelewa. Akaandika namba yake upande wa ujumbe kisha akamgeuzia simu.
Akamuona anachukua namba na kumpigia. Akapokea.
“Cha kwanza
kabla ya salamu, hii nyumba inalindwa na mitambo. Ukishika kitasa kabla hujatoa
alam, itapiga kelele sana. Na askari watajaa hapa.” Jelini akashituka
sana na kurudisha kichwa ndani kuingalia tena hiyo nyumba. Akaona kweli inastahili
kulindwa hivyo. “Sasa nenda karibu na mlango wa nyuma
kuna kiboksi chenye namba, bonyeza…” “Subiri
kwanza. Mwenzio mimi hapa mgeni, hata sijui nilipo. Nahisi nililewa sana
nikabebwa na mtu, nimeamka hapa peke yangu hata sijui nilipo. Wewe ni nani?”
“Kasa.” Akajibu na kumfanya Jelini achanganyikiwe. Akamchungulia vizuri
hakuridhika.
“Wewe
muongo. Kasa ni mweusi, wewe mweupe. Au wewe ni jambazi!” Akamuona anacheka. “Usicheke bwana! Sasa wewe ni nani?” “Mimi pia ni Kasa.”
Jelini akamchungulia tena vizuri akajaribu kumfananisha na Kasa anayemjua yeye,
akili yake ikakataa kuwaweka hata kwenye ukoo mmoja. “Mama
yako wewe mzazi huwa anakuita nani?” Hilo swali lilimfanya huyo Kasa
azidi kucheka. “Kwani wewe unaitwa nani?” “Mimi hapa
naitwa Jelini. Haya niambie na wewe jina lako nani? Na usinidanganye. Maana
mimi sijakudanganya.” “Kweli naitwa Kasa.” “Sasa kwa nini na wewe uitwe Kasa!?”
Jelini akauliza, lakini hapohapo akili ikaanza kufanya kazi kidogo na kushituka
sana.
“Kwamba
hapa ni nyumbani kwa Kasa!?” “Ndiyo.” Jelini akashituka sana akamuona ametoa
macho na kufunga mdomo. “Mimi sinywi tena pombe. Sasa
nilifikaje hapa!?” Akamuuliza huyo Kasa wa nje ambaye na yeye ndio
amefika hapo. “Sijui Jelini, kwani Kasa hayupo humo
ndani?” “Hata sijui! Mimi nahisi jana nilizidisha pombe, akanileta hapa kwake.
Sasa wewe kwa nini na wewe uitwe Kasa bwana!?” Ikawa kama tena anamlaumu
huyo Kasa anayemtizama nje ya dirisha. “Katafute sehemu
ya kutoa alam, unifungulie ndio nikujibu maswali yako. Ukifika huko anza kwa
kubonyeza *2345#. Umeelewa?” “Vikipiga kelele?” “Usipokosea, hakutakuwa na
kelele.” “Basi sikosei.” Jelini akaanza kuzunguka nyumba mpaka akapata
kicho kiboksi chenye namba. Akabonyeza, bado akiwa kwenye simu naye. “Ewaaa! Sasa unaweza kufungua mlango wowote ule.”
Akaanza kufungua akimuelekeza
kwani hapakuwa na funguo ila nobs tu. Akamuelekeza mpaka akamaliza wa mwisho.
“Wewe unafanya nini hapa?” Jelini akamuhoji bila hofu kama pale ni kwake.
“Nimetoka kanisani, sijamuona Kevin, ndio nimekuja kumuangalia.”
“Unanichanganya. Kwani Kevin ni nani tena!?” “Anayeishi hapa.” Jelini akatulia
akimwangalia. “Kwani wewe unafanya nini hapa?” Ikabidi na yeye amuulize.
“Nilikwambia hata sijui wenyeji wangu ni kina nani na nilifikaje hapa. Mimi
jana nilikuwa kwenye harusi ya Jema, nimeshangaa nimeamkia hapa.” “Unamfahamu
Kevin Kasa?” “Kasa namfahamu. Sasa na wewe kwa nini uanze kuniambia unaitwa
Kasa!?” “Kasa unayemfahamu wewe, jina lake analoitwa na mama yake mzazi ni
Kevin.” Jelini akaanza kucheka vile alivyojibu kwa kumuigilizia.
Akacheka hapo
akimwangalia kwa tabasamu akikishangaa hicho kiumbe mbele yake. Akavutiwa hata
vile alivyo. Hapo ndio ameamka hata hajaosha uso, hana viatu, lakini alivutia mno.
Akabaki akimwangalia mpaka akamaliza yaliyokuwa yakimchekesha. “Sasa na wewe mama yako mzazi anakuita nani?”
Jelini akaendelea kumuhoji na cheko kubwa, kashasahau yake. “Alexender.” “Jina
lako zuri. Ila ningekuwa mimi ningejiita Zenda.” Akacheka akitingisha kichwa
akimtafakari Jelini kwa kuvutiwa naye.
“Au wewe
hujalipenda?” Akamuuliza kama padre aliyekwisha mbatiza. “Sijawahi kuitwa
hivyo, ni kama unanibatiza upya!” “Usijali. Utazoea tu. Haya, Zenda Kasa, hapa
unafanya nini?” “Dad!?” Akatoka Kasa akiwa ameshituka sana. Jelini akajishika
mdomo kwa mshituko. “Wewe kumbe ndio baba yake Kasa huyu!? Kwamba wewe ndio
mzee Kasa?!” Jelini akashituka sana na kuendelea bila kusubiri jibu. “Sasa
mbona hujaniambia kama wewe ndio mzee Kasa? Samahani sana. Mimi bora tu
niondoke jamani!” Mzee Kasa akabaki akimwangalia Kasa na Jelini.
“I can explain.” Akamsikia Kevin Kasa
akizungumza na baba yake lugha nyingine ila kwa hofu ya ajabu sana akiomba
ajitetee. “Sijaja kanisani kwa kuwa ni kama unavyoona, nilipata wageni,
tuliokuwa nao kwenye harusi mpaka karibu kunakucha. Nilijaribu kuwapa lift ili
kuwarudisha makwao, lakini wakaishia kulala kwenye gari, ikabidi kuwaleta tu hapa
kwenye nafasi kubwa. Mungu nishahidi, sidanganyi. Sipo hapa kufanya umalaya.”
Jelini akashangaa vile jeuri Kasa alivyoingiwa hofu kwa huyo mzee ila akamfanya
afikirie kwa haraka.
“Samahani Kasa. Ukisema
wageni, unamaanisha nipo na nani humu ndani?” Hilo swali la Jelini likazidi kumuogopesha
Kasa akawa kama aliropoka, hakukusudia kusema hivyo kwa huyo baba yake.
Alipoona hajibiwi, Jelini akaingia ndani kumtafuta huyo mwenzie. Akamtafuta
huyo wa pili kwenye chumba alichokuwa amelala yeye mpaka chooni, akamkosa,
akatoka. “Sasa mbona kwenye chumba nilichoamka mimi hamna mtu mwingine?” “Kwa
sababu huyo wa pili atakuwa chumba alicholala yeye huyu.” Mzee Kasa akajibu na
kumfanya Jelini akunje uso. Pakapita ukimya wa muda. Akafikiria, akili zake
asizopenda kuzichosha zikakosa jibu na yeye akaona asijichoshe.
Akaona aage tu. “Mimi
naomba niondoke jamani. Kasa wewe, asante kwa msaada wa kunifishisha hapa.
Nachukua vitu vyangu naondoka.” Jelini akarudi ndani. Wakati anaingia ndani tu,
uso kwa uso na Doro. “Dada Doro! Yaani umelala na Kasa!?” Akashituka kwa sauti
ya juu sana mpaka wa nje wakasikia. “Acha kupayuka wewe.” “Lakini si vizuri
dada! Huyu bado kijana mdogo sana!” “Kwani wengine tukoje!? Wewe Vipi Jelini!?”
“Mimi nimesema tu dada yangu. Kasa ni mtu mzuri sana, usimfanyie hivyo.” “Kwani
mimi nilikuwa mtu mbaya!? Wewe vipi?” “Mimi naondoka, lakini shauri yako.”
Jelini akaingia chumba alichoamkia, akachukua viatu vyake akatoka hajavaa viatu,
pochi na simu mkononi.
“Kwa nini unataka
kujiangamiza kizembe wewe!? Unataka nini kitokee kwako ili utulie?” Jelini
akasikia Mzee Kasa akimgombesha kijana wake kama mtoto mdogo. “Ulikumbuka
kumpima?” Kimya. “Na usinidanganye?” Mzee Kasa akampiga mkwara. “Nilitumia
kinga.” Akamsikia Kasa akijibu kwa hofu ya kujitetea. Jelini akatoka kwa kunyata
kama asionekane, wakati ni mchana kweupe, wote wapo nje mwangani. Wakawa wakimwangalia
vile anavyoondoka bila hata viatu miguuni. Akatembea mpaka kufikia geti dogo
kabisa la pembeni, mlinzi mwenye sare akamfungulia, akatoka akinyata vilevile.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Kwanza hakujua alipo
wala anapokwenda ila akakusudia kutoka hapo. Akiwa anatembea gari ikasimama
pembeni yake. “Ingia nikusogeze.” Jelini akamwangalia, alikuwa mzee Kasa.
“Kwanza samahani. Mimi sikujua kama wewe baba yake Kasa.” “Ndio maana ukaniita jambazi?”
Jelini akakumbuka na kuanza kucheka. “Sasa wewe baba gani mweupe pee, halafu mtoto
wako mweusi kabisaaa!” “Kwa hiyo wewe baba yako ni mweupe?” “Wenzio sisi hatunaga
baba.” Kasa akakunja uso. “Ila umenifanya sasa nichanganyikiwe. Maana mimi
nilikuwa nikidhani pengine nitakuwa nikifanana na baba yangu! Sasa kumbe
unaweza kuwa usifanane na watoto wako!” Mawazo hayo yanaendelea kichwani kwake pembeni
ya gari ya mzee huyo yeye hana habari ya muda wala wazo la pili. “Kevin
amefanana na mama yake.” Ikabidi amjibu, Jelini akamwangalia na kumuuliza.
“Mama yake ambaye yupo ulaya?” Mzee Kasa akacheka akitingisha kichwa akimtizama
Jelini.
“Nijibu sasa!” “Ndiyo.”
“Mmmh!” Akaendelea kuwaza taratibu kama aliyechanganywa zaidi. “Sasa mbona mimi
sifanani na mama yangu? Ila Jema anafanana rangi na mama. Mimi nipo tofauti!” Akawa
anawaza hapo nje ya gari ya mzee Kasa, mzee Kasa akimwangalia. “Lifti.”
Akamkumbusha. “Mimi mwenzio huwa sitaki misaada. Watu wengine wanakusaidia
jambo, halafu wanakuja kukudai kitu kingine kabisa! Sasa unajiuliza, huyu mtu
kakupa bia moja tu anadai, akikupa gari itakuaje!” Ikabidi mzee Kasa acheke.
“Kweli tena! Mimi
bora tu nitembee sitaki msaada wako. Kwanza sikujui, zaidi ya kukusikia tu.”
“Umesikia nini juu yangu?” Ikabidi amuulize akicheka. “Eti wewe una mahela mengiii,
ndio maana mtoto wako anaringa na ana kiburi. Halafu kwenu nyinyi mnadharau.
Hata mtoto wako wa kike naye eti yupo kama Kasa. Uongo?” “Si ni ndugu? Lazima
wafanane.” “Ndio wanafanana mpaka majivuno! Lakini wanasema eti wewe ndio
unawapa wanao mahela mengi. Akuu! Mimi sitaki.” Jelini akakataa akibetua mabega
yake.
“Sasa unaogopa nini
kitatokea kwenye kukupa lifti?” “Ukinitamani je?” Mzee Kasa akacheka, akacheka
sana. “Wewe cheka tu.” “Sasa umeshajiuliza kama ukitokea wewe ndio ukanitamani
mimi, itakuaje?” Jelini alicheka mpaka akakaa chini kabisa. “Unajichafua bwana,
simama.” “Unavyojiamini Zenda! Mimi nikutake wewe!?” “Nakutahadharisha tu.”
Jelini akasimama akicheka. “Mimi wala sitakutaka.” “Unauhakika?” “Kabisa.
Asilimia zote.” “Na ikitokea unanitaka, utafanyaje?” Akamfanya Jelini afikirie,
kisha akamwangalia, akakuta mzee Kasa akimtizama.
Akacheka na
kupandisha mabega akikataa. “Akuuu!” “Sawa Jelini. Ila hii nyumba ipo mbali na
usafiri. Hujavaa viatu, jua limeshakua kali. Utaungua miguu na utachomwa na jua
sana. Mimi nitakusogeza unapotaka, na nakuahidi sitakudai.” “Wanasemaga
hivyohivyo.” Jelini akajilalamisha hapo kwenye dirisha alipokuwa amekaa huyo
dereva akimtizama kiumbe hicho kigeni kwake, ila kweli kinavutia. “Nakuahidi
sitakudai. Twende.” Akakubali na kuzunguka kuingia garini.
“Wewe kweli una mahela.
Humu ndani pananukia vizuri, halafu gari yako safi kama wewe mwenyewe! Unawaka
utafikiri umepaka sijui mafuta ya maji, sijui! Ngozi yako safii. Mimi mpaka
napata shida kukaa humu kwenye gari yako bwana! Bora nishuke tu nijitembelee.”
“Usijali. Upo sawa tu. Unaishi wapi Jelini?” “Naishi na mama yangu, na mtoto
wangu.” “Baba mtoto wako yuko wapi?” Akanyamaza kabisa na maneno yote
yakamuisha. Na yeye akawa muungwana, akanyamaza wakitoka hapo.
Akavunja ukimya kwa
swali. “Ungependa nikusogeze mpaka nyumbani, au nikushushe sehemu na nikutafutie
usafiri wa kukufikisha nyumbani?” Akapandisha mabega kukataa. Akamuacha hajaelewa. Ila akaendesha, akiwa ametulia hapo
kitini, kimya kabisa. Hamuongeleshi tena wala hamwangalii. Kama aliyemnunia.
“Jana ulikuwa kwenye harusi ya nani?” Akamjaribisha. “Jema ameolewa. Amependeza
huyo! Kila saa mume wake anambusu tu! James anampenda sana Jema. Hata mama
amesema.” Akakumbuka kitu. “Halafu akamnunulia gauni zuri hilo! Kwanza sio
kumnunulia. Ilibidi watengeneze. Ungemuona Jema, ungemtamani.” “Mimi sina tamaa
na visivyo vyangu.” Jelini akamwangalia akiwa amekunja uso. “Sasa sio kihivyo
na wewe! Kwamba ungesema amependeza! Zenda naye!” Akacheka kidogo vile
alivyoongea. “Ila hata wewe unaonekana ulipendeza sana.” “Mimi kawaida yangu.”
Mzee Kasa akaanza kucheka. “Sijisifii. Ila mimi mwenzio napenda kupendeza.”
“Sawa Jelini. Nionyeshe basi picha za jana.” Akawaza na kuonekana kukosa jibu.
“Haki naacha pombe!
Sinywi tena.” “Kwa nini?” “Yaani nahisi kitu kibaya sana kilitokea jana na
sikumbuki. Niliishia niki…” Akawa hakumbuki kabisa. “Na sijui niliingiaje
kwenye gari ya Kasa, Kevin! Bwana wewe unataka kunichanganya. Acha yeye abakie
Kasa, wewe Zenda. Sawa?” “Sawa.” Akakubali akicheka. “Kwani wewe hukukubaliana
na Kasa baada ya shuguli muende nyumbani kwake?” Jelini akashituka sana. “Akuuu!
Mimi mwenzio sina mambo hayo. Siku hizi kuna magonjwa. Na watu wanaambukiza wenzao
makusudi tu kulipiza kisasi. Nimekoma. Sitaki kabisaa.” Mzee Kasa akacheka na
kufikiria kwa haraka akawa kama amekumbuka kitu.
“Wewe umemfahamia
wapi Doro?” “Baa! Ila mengine sikwambii, ni siri yetu.” “Wewe na Doro?” “Ndiyo.
Doro rafiki yangu sana japo mkubwa kwangu. Yupo karibu na mimi kuliko hata Jema,
dada yangu kabisa.” Ndipo sasa akajua huyo Jema anayetajwa ni dada mtu. Akauliza
swali jingine. “Kwa hiyo Doro ndiye mpenzi wa Kasa?” “Hapo sasa mimi sijui! Ila
mimi nilidhani Kasa hana mtu maana ni kama alitaka ukaribu na mimi. Mimi
nikamwambia tokea mwanzo, hataniweza. Kasa mstaarabu sana, mimi mwenzio
sio mstaarabu. Halafu kama mkali hivi! Mimi napenda kuongea na tucheke. Kwa
hiyo tokea mwanzo nilimwambia waziwazi mimi sitaki. Ila..” Akawa kama
amekumbuka kitu.
“Ujue kuna siku
nilimkuta nyumbani kwa dada Doro! Ila sikuuliza kwa kuwa hatukuwa kwenye
maelewano mazuri na dada Doro, alikuwa ameniambia ukweli lakini kwa matusi
makali. Ndio nikaondokaga kwake nikiwa nimeumia. Baadaye ndio akanibembeleza
nirudi kwake niwe naenda kulala, mimi nikamwambia sitarudi tena nyumbani kwake.
Nitakuwa nalala kwetu, ila nimemsamehe. Aliniumiza sana, hasa nikikumbuka jinsi
mimi nilivyomsaidia! Ndio nikawa nimerudi kwetu, kwa mama Jema. Akaja kwetu na
kunipigia simu kila saa eti ananikaribisha nyumbani kwake kwa chakula. Nikaona
asije dhani sijamsamehe, ndio nikaenda kwake, na ndipo kwa mara nyingine tena
ndio nikakutana na Kasa nyumbani kwake.” Mzee Kasa akawa akimsikiliza tu na kununa
kukaisha, amechangamka anaongea na kujibu yote ila akamgundua hataki kabisa
kusema maswala ya baba mtoto wake.
“Mara ya kwanza
kukutana na Kasa ilikuwa wapi?” Akaendelea kumuhoji taratibu. “Anafanya kazi na
shem, aliyemuoa Jema. Kwa hiyo nilikutana naye nyumbani kwa shem, siku
aliyomchumbia Jema. Alifanya kama kitafrija. Wafanyakazi wenzie na marafiki
wakahudhuria na mimi nikaenda ndio nikakutana na Kasa.” “Ooooh! Hapo sasa
nimeelewa. Na Doro naye anafanya kazi hukohuko?” “Hapana. Mimi hata sijui
amekutana wapi na mtu kama Kasa, maana dada Doro mtu wa baa kama mimi tu, japo
mwenzangu yeye amesoma na anakazi nzuri sana. Ila mshinda baa kama mimi tu.”
“Nilifikiri umesema
unaacha pombe! Maana ukiendelea kushinda baa lazima utapata vishawishi.”
“Lakini kweli! Ila washikaji zangu je? Stori za baa hazina wasomi wala wasio
soma. Wenye nazo wala wasio nazo!” “Lakini zinakufanya unajisahau Jelini! Leo
umeamkia nyumbani kwa Kasa. Hajakugusa. Iweje siku nyingine uje uamkie kwengine,
kwa mtu mwenye gonjwa baya, akakubaka na kukuachia ugonjwa? Huoni
kama ni hatari kwako?” Hapo akaogopa maana hayo maneno yalimuingia mpaka kwenye
mifupa. Akapoa kabisa. “Mimi naungana na ushauri wako wa kuacha pombe, Jelini.
Sidhani kama ni rafiki kwako.” Akanyamaza.
“Ungependa nikupeleke
mpaka nyumbani?” Akamwangalia. “Umenikasirikia?” “Hapana. Najifikiria tu.”
“Tafadhali ujifikirie zaidi, Jelini. Wewe ni binti mzuri sana. Nitakuja
kusikitika sana nikija kusikia kitu kibaya kimekupata.” “Kweli utasikitika au
umeongea tu?” “Namaanisha! Unajua kwa nini nimekua mkali kwa Kasa kama
unavyomuita wewe?” “Sijui.” “Bado ni mdogo na ahadi nzuri mbeleni kwenye
maisha. Kwa nini anataka kujiua mapema? Hilo namsisitiza bila kuchoka na ndio
maana nilipomkosa tu kanisani, nilijua kuna kitu hakipo sawa. Kevin si mlevi wa
kushindwa kujielewa, kwamba amezidisha pombe akashindwa kuamka kwenda kwenye
ibada! Hapana. Akikosa kanisani najua si pombe hata kidogo. Usicheze na maisha
Jelini, hayana spea!” Hapo akamgusa Jelini. “Basi wewe baba mzuri.
Natamani na mimi ningekuwa na baba yangu pengine..…” Akasita. “Hujachelewa
kubadilika Jelini. Unaweza kubadili kila kitu na ukawa sawa.” “Nashukuru
kunishauri japo hunifahamu. Nitajitahidi.” “Naomba kujua maendeleo ya hizo
jitihada zako, Jelini.” Akamshangaza sana na kumfanya kama asielewe tena.
“Kwamba niwe najua kinachoendelea
kwako.” Akaongea kwa kubembeleza mpaka akamlainisha Jelini cha maneno. “Sasa
utajuaje!?” Akauliza taratibu. Safari hii akaonekana mtulivu kama siye yeye. “Kama
ukiniruhusu, nitakuwa nikikupigia kujua maendeleo yako.” “Kweli Zenda!?”
“Kabisa.” “Mmmh! Unanidanganya bwana! Mimi nimeambiwa wewe ni tajiri sana. Na
mtu tajiri anakuwa na mambo mengi ya kufanya, utakuja kunikumbuka mimi kweli?”
“Najua umezoea kudanganywa. Mimi nikikwambia nitafanya jambo, ujue nitafanya.
Nina watoto wawili tu. Na ndio utaongezeka na wewe. Haitakuwa shida.”
“Mbona sasa hujamtaja mkeo? Mama Kasa.” “Kama
unamaanisha mama yake Kevin, yeye alishaolewa na anayo familia yake huko
alipokwambia Kevin alikwenda.” Jelini akashangaa sana. “Sio mke wako tena?!” “Hapana.
Tulishaachana zamani sana. Nafikiri ni zaidi ya miaka 20 sasa.” “Na hukuoa
tena!?” Akacheka. “Unamaswali wewe?” “Mimi nataka kujua bwana! Niambie.”
“Hapana sikuoa, japo nilishakuwa na mahusiano baada yake.” Jelini akanyamaza
kama anayefikiria kitu.
“Ungependa
nikurudishe nyumbani?” “Sidhani kama itakuwa jambo zuri. Watadhani wewe ndiye
uliyenichukua jana. Halafu mimi mama yangu anaongea kama hivi mimi, ila yeye
mkali sana. Atakwambia maneno mabaya. Nashukuru kwa kunisadia, ila nishushe
popote ambako unajua naweza kupata usafiri wa kunifikisha nyumbani.” “Umewaza
vizuri.” Akaendelea kuendesha.
Akawa kama amekumbuka
tena kitu, akamgeukia. “Sasa kwa nini wewe ni mweupe hivyo!?” Mzee Kasa
alicheka na kucheka sana. “Jelini!” “Umenishangaza na kunifanya nichanganyikiwe!
Sasa unawezaje kuwa na watoto weusi ukiwa na rangi hiyo?” “Mama yao au upande
wa mama yao wana damu kali sana. Hata Kemi amefanana sana na mama yake, kama
alijizaa.” “Na Kasa naye?” “Ukija kumuona mjomba wake, ndio utaelewa ni kwa
nini nakwambia upande wa mama zao wanadamu kali. Yupo kama hivyo Kevin. Na huko
alikoolewa aliolewa na mzungu, hao watoto ukiwaona, utawafananisha na Kemi.
Wote ni wa kike. Wamefanana na Kemi, huwezi kuuliza kama ni ndugu.” Jelini
akatulia kabisa mpaka akamfikisha karibu na taksii.
“Nakushukuru Zenda.
Nitajitahidi kuacha pombe. Hata hivyo huwa nakunywa kama kujificha tu au
kutojifikiria. Wakati mwingine huwa najichukia sana. Pombe inanisaidia
kujisahau.” “Ni nini kinakuudhi kwako?” “Ni siri, siwezi kukwambia.” “Ila nilazima
tuje kukizungumza. Lazima itakuja kukusaidia tu. Ukiendelea kukificha, ujue
ndio kitakuumiza zaidi. Nenda ukapumzike. Lakini naomba nikulipie taksii.”
“Akuuu! Mimi sitaki. Ninazo hela zangu.” Akashuka haraka garini na kumuacha
Kasa akicheka huku akimtafakari.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Akampigia simu hapohapo.
“Unijulishe utakapofika salama.” “Sio itakuwa usumbufu
tena?” “Hata kidogo.” “Wewe usiwe na wasiwasi, nitafika tu salama.” “Nataka
kujua Jelini.” Akacheka. “Asante kujali. Basi
nitakujulisha.” Wakajikuta wakicheka. “Umepata
usafiri sasa?” “Napanda pikipiki.” “Acha Jelini bwana! Tafadhali chukua taksii,
nitalipa.” “Mwenzio ndio usafiri wangu.” “Unafurahia kukumbatia hao wanaume
huko barabarani?” Jelini alicheka mpaka machozi.
“We Zenda!”
“Ndicho unachoking’ang’ania! Sasa kwa nini unakataa usafiri wa heshima?” “Sio
wote tuna pesa kama wewe Zenda!” “Sasa mimi mwenye pesa ndio nakwambia
nikulipie, hutaki. Unataka nini Jelini?” “Basi nachukua taksii, na nitajilipia.”
“Usikate simu.” “Huniamini kama nitachukua taksii?” “Nataka uhakika kuwa
amekufikisha salama.” “Unavyojali!” “Na mimi ni kawaida yangu kama wewe
kupendeza.”
Jelini alicheka sana. “Kumbe ulikuwa ukinisikiliza!”
“Sana tu. Ila sikusikii ndani ya gari.” “Dakika moja.” “Na usikate.”
“Nimeelewa. Hata mimi napenda kujaliwa.” Akamfanya acheke.
Akamsubiria mpaka
akapanda kwenye gari wakawa wanaendelea kuzungumza. “Sasa
leo jumapili, unafanya nini baada ya kutoka kanisani mbali ya kumfuatilia
Kasa?” “Leo napumzika tu nyumbani. Kusoma magazeti na vitabu.” “Hujisikii
mpweke?” “Nafikiri nimeshazoea au nimekubaliana na hiyo hali. Hata hivyo ukweli
nina mambo mengi, hujakosea. Na wewe?” “Naenda kutulia zangu nyumbani, kimya.”
“Humtafuti Doro?” “Zenda wewe kumbe unafutialia mambo hivyo! Mwenzio sikujua
hata kama unanisikiliza!” Jelini akashangazwa maaana alishajijua ni
muongeaji sana, ni ngumu mtu kumtilia maanani. Kwanza hajazoea mtu kumtilia
maanani.
“Mimi
nilijua hunielewi!” “Nilikuwa nikikusikiliza sana na nilikuelewa kuwa ndiye
kampani yako huko baa!” “Sasa hivi ukute yupo na Kasa. Na pia naona nimuache
kwa muda.” “Lakini kama isingekuwa kumuacha kwa muda ungefanyaje?” “Ndio
kampani yangu, mwenzio. Tungeenda zetu baa. Tukakaa mpaka usiku sana.
Akinikaribisha kwake, naenda kulala kwake.” Akamshangaza sana, ila akaona hilo
aliache kwa muda.
“Kama ndio
hivyo, basi karibu kwa chakula cha usiku. Tule wote halafu urudi nyumbani
mapema tu.”
Akanyamaza. “Unaogopa?” “Mmmh!” “Kwamba nitakudai?”
“Mimi sijui bwana! Ila sema wewe haupo kama Kasa. Angalau wewe tunaweza
kucheka. Mwanao yule yupo serious sana bwana mpaka anatisha!” “Kuna
ulichomnyima ndio maana.” Jelini alicheka sana. “Zenda
wewe!” “Kumbe unafikiri angekununia hivihivi!” “Ila mimi sikusema neno baya.”
“Hilo zuri kwako, baya kwake. Sasa tutakula wote?” “Nakuonea aibu.”
Alimfanya akacheka sana.
“Kutoka
kuniita mimi jambazi mpaka kunionea aibu!” Jelini akaanza kucheka na yeye. “Sasa, saa zile si nilikuwa sijui kama wewe ndio Kasa
mwenyewe! Sasahivi nishajua, nakuonea aibu.” “Usijali, nitakuziba macho.”
Akacheka wee. “Kwa hiyo utakuja?” “Mimi sitoki na kila
mtu bwana. Mpaka nikujue vizuri, ndio nitakubali.” “Sasa utanijuaje na hutaki
kuja tule wote!” Akamsikia kimya. “Jelini?”
“Unataka kwenda kula wapi?” “Popote utakapochagua wewe, isiwe tu baa.”
Akaanza kucheka tena. “Au nikusaidie kuchagua mimi?”
“Mimi nasita bwana. Nipe muda Zenda.” “Nitaheshimu hilo japo nimehuzunika!”
“Kweli?” “Sasa kwa nini unahofu na mimi?” “Sikujui Zenda.” “Nakupa ruhusa ya
kuniuliza swali moja litakalokutoa hofu.” “Unaniahidi hutanidanganya?”
“Nitakwambia ukweli hata kama utakuwa mchungu.” Jelini akaridhika.
“Wewe
umesema hujaoa. Sasa unafanya mapenzi na nani na unajikinga vipi?” “Hayo ni
maswali mawili Jelini. Nilikwambia moja. Mengine nitakujibu taratibu. Sasahivi
chagua moja.”
Akatulia akifikiria. “Ukinijibu yote ndio nitafurahi.”
Akacheka akifikiria. “Sawa. Binafsi ni mchaguzi sana
linapofika swala la wanawake, haswa baada ya kuvunjika ndoa yangu. Nipo makini
sana na wanawake. Na kwa kuwa sitafuti kuoa, nahakikisha namvulia nguo mwanamke
atakayekuwa amenivutia haswa.” “Haaa!” Jelini akashituka sana
hakutegemea. “Wewe si umetaka kujua wewe? Tulia sasa
nikujibu.” Akamsikia akicheka.
“Swala la
kinga, ni lazima. Lakini kabla sijaanza kufanya mapenzi na mwanamke ambaye itanilazimu
kutumia kinga, lakini pia lazima kumpima. Ninacho kipimo kinachotoa majibu
hapohapo. Umeridhika?” “Nina swali jingine.” “Hapana Jelini. Kama unanikatalia
niambie tu. Nimekujibu zaidi ya tulivyokubaliana.” “Basi nakukatalia. Sitaki.”
“Sawa. Lakini bado ningependa kujua kama utafika salama.” “Nitakujulisha kwa
ujumbe. Kwaheri.”
Akamkatia na simu. Alishangaa Kasa, hakutegemea! Ameshazoea kutetemekewa. Leo
Jelini aliyemkuta akitembea peku, hana hata usafiri wa baisikeli anamkatia
simu! Kikampata kilichompata mwanae. Akabaki ametoa macho.
Zimwi Likujualo.
Jumapili hiyo ikawa
njema kwa wengi waliotoka harusini kwa James na Jema, lakini ikawa tofauti kwa
Joshua. Alishindwa hata kupata kifungua kinywa. Hajui pakumpata Bale, na yeye
kikampata kilichompata baba Naya. Hajui aeleze vipi hata mkewe akamuelewa. Kwa Naya
yeye Bale ni mtu hatari sana. Hakumbuki hata mahusiano naye zaidi ya kumpiga sana
kikatili akiwa analia ugonjwa. Akatulia kimya anaogopa asije akapatikanika huyo
Bale, akijua ndio mwanzo wa kumrudisha kwa Malon.
“Njoo ukae hapa Naya
mpenzi wangu.” Naya akajisogeza maana alikuwa akimwangalia kwa kijiiba. “Naomba
unisaidie, kukumbuka nyumba ya Malon hapa Dar.” “Sikumbuki.” “Hapana Naya. Umejibu
haraka sana. Tena umejibu kwa woga ukiwa hutaki hao watu maishani.” “Naogopa
sana Joshua.” “Mimi nakuhakikishia, utakuwa sawa. Usiogope. Sawa?” Akatulia. “Kuna
kitu si sawa kwa Bale na sijui jinsi ya kueleza. Siwezi kula wala kulala. Tafadhali
nisaidie.” Akamuhurumia mumewe. “Niahidi tena kuwa utalinda Joshua. Wasije nichukua.”
“Mungu atanisaidia mpenzi wangu. Sitazembea tena. Si umeona nipo makini na
wewe?” Akajirudi maana Joshua alikuwa akimlinda mpaka kwa wengine ikawa kero. Akamuona
ameridhika.
“Kuna mahali nilisoma.
Niliandika zamani wakati nikiuza vitu vya Malon ili kumtoa jela. Niliandika mali
zake zote na mahali zilipo. Ya hapa Dar niliiandika ipo maeneo ya Kunduchi, na
nikaandika kuwa sikuiuza. Pengine inaweza kuwa ndiyo.” “Nakushukuru mke wangu. Umeandika
wapi?” Naya akanyanyuka kwenda kuleta hicho kijitabu chake cha kumbukumbu. Akamkabidhi.
Wakati akisoma, simu
ya Joshua ikaita, alikuwa Geb, akapokea. “Vipi GM?” “Safi.
Nakucheki tu. Kila kitu kipo sawa? Maana jana tuliagana ukiwa sivyo ndivyo.” “Kuna
hali napitia, sina jinsi yakumueleza mtu akanielewa.” “Nijaribishe mimi.”
Akaongea Geb akionyesha kujali. “Kuna kitu hakipo sawa
kwa Bale. Sijui ni nini kwa hakika! Ila nashindwa hata kula aisee.” “Unajua
alipo twende tukamuangalie?” “Wewe si una wageni?” “Man na familia yake wameshaondoka.
Nipo tu hapa peke yangu, mama na Nanaa wametoka na watoto kwenda kwenye
birthday ya mtoto wa binamu yake Nanaa. Mimi nikaona nipumzike tu. Kwa hiyo, am
all yours.” Geb akaonyesha utayari wa kutumiwa na Joshua atakavyo. “Aisee nitashukuru sana. Nilikuwa sijui jinsi ya kumpata,
lakini kuna kijitabu hapa nasoma. Aliandika Naya zamani. Naomba tukaanzie hapo.
Ni Kunduchi.” Akaanza kumsomea vile Naya alivyokuwa ameandika. “Naona kama hayo maelezo yanajitosheleza! Tunaweza kugonga
nyumba mbili tatu, lakini nina uhakika hatuta kwama. Tukutane huko basi.”
Wawili hao wakakubalina.
Hujafa, Hujaumbika.
Baada ya kama lisaa
wakajikuta wapo Kunduchi. Wakakisoma tena kile kijitabu cha Naya cha kumbukumbu,
wakaamua kuanza maeneo ya kuzunguka karibu kabisa na bahari. Walipoenda nyumba
ya pili tu, mlinzi akaonekana alishawahi kulinda hapo kwa Malon kwa kupitia
kampuni yao na anamfahamu Bale vilivyo. “Ila ile nyumba imegeuka gofu aisee. Inavyosemekana
mwenye nyumba alimuacha kijana mmoja pale, yule mtoto bangi halafu alianza kwa
jeuri, dharau kwa sisi wote tuliokuwa tukimlindia pale. Nafikiri alipoanza
kuishiwa pesa, akaanza kuuza vitu vya ndani. Mbaya zaidi akawa analeta wateja
palepale wanaingia ndani anawaonyesha vitu vya kuwauzia. Sisi tukamshitaki kwa
uongozi wetu kwa sababu tulimwambia kwa vizuri tu kuwa, anaita wezi yeye
mwenyewe, akawa jeuri.”
“Ndio akapewa onyo
lakini ujue hapo kila mtu akawa anapajua pale mpaka ndani. Sisi tunavyohisi wenzie
walewale waliokuwa wakimsaidia kutafuta wateja, walimgeuka. Wakamzidi mahesabu.
Wamemuibia kila kitu. Nikisema kila kitu, kwamba walihamisha nyumba mpaka
kitanda. Akawa ameishiwa kabisa, anashindwa kulipa pesa ya ulinzi, ndipo kampuni
ikasitisha mkataba. Na sisi tukaondolewa pale tukapewa malindo sehemu nyingine
wakati kampuni ikimshitaki awalipe pesa yao. Nilikuwa nikimuona anapita na
magongo yake hapa maana magari yaliharibika yote, akaja kuyauza.”
“Bale na magongo!?”
Joshua akawa kama haamini. “Yaani alikuwa akipita hapa unamuona akichechemea, anaongea
peke yake kama kasharukwa na akili vile. Nafikiri bangi imemzidi. Ila sijamuona
siku mbili hizi. Sasa sijui.” “Unasema huyo kijana unayemzungumzia wewe
anachechemea!?” Joshua akaanza kuingiwa na wasiwasi pengine si Bale. Bale
wanaomjua wao ni mzima. Hana ulemavu wowote. “Mimi wakati nikilinda pale, ni
kama alijiumiza huo mguu. Akawa hataki kwenda hospitalini, akisema atapona tu. Ndio
mwenzangu akamuona na kusema ule mguu utakuja kuoza tu, yeye hajui sababu ya
bangi, maana ulivilia ukawa mbaya kweli. Nafikiri alikaa nao ukamzidia. Nafikiri
sijui bangi ilishindikana kutuliza au aliishiwa akawa hana hata pesa ya bangi! Hatujui
ila alishindwa kuvumilia. Anavyosema alikuja kwenda hospitalini wakamwambia
amechelewa. Umeoza mpaka mifupa. Ndio wakamkata katikati. Wala si muda mrefu
maana hata donda lenyewe halijapona. Utamuona tu akipita amelifunga na
linaonekana linamvujia.” Joshua aliumia sana.
“Na nyinyi mnamdai
nini? Kwake sio mbali kabisa. Ukipita nyumba mbili mbele, yake ipo ndani kidogo
maana imekaribia baharini zaidi. Kila anayekwenda kwake ni kumdai ila naona
wanashindwa na hali yake. Sio mbali kabisa.” Akawaonyesha. Joshua na Geb wakashukuru,
na kurudi kwenye magari yao na kuongozana kwenye hiyo nyumba wakiwa na wasiwasi
sana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Nini kitaendelea kwa Jelini. Usipitwe na aliyoyafanya ukumbini akiwa
hajitambui kwa pombe.
v
Zenda kimempata kitu kama mwanae. Jelini!
v
Joshua naye kimempata kitu kama baba Naya.
0 Comments:
Post a Comment