Mpaka
siku hiyo ya kitchen Party kina Magesa hawakuwa na mualiko wala sare. Kama kawaida Grace akatua jijini asubuhi ya
siku hiyo na familia yake yote, wakakutana na hiyo hali. Man na yeye alikuwa
tayari kwa Bag Party jioni yake iliyokuwa imeandaliwa na kina Joshua na
Geb. Walipanga kwenda kuifanya kisiwani na maboti yao. Ilikuwa ya watu wa
karibu na James. Wakaiandaa kitajiri, wanaume hao na wao wakataka kwenda
kumfunda James.
“Sasa
itakuaje!? Maana kama ningejua tungekuja hata usiku! Nimeacha shuguli nyingi
kweli! Ningepunguza kidogo.” Grace akauliza kwa mshangao na kujuta kuwahi
kufika bila taarifa za kutosha. “Hata sijui! Acha nimpigie James.” Mama G
akampigia James akiwa katikati ya shuguli. “Nakusumbua James mwanangu,
lakini mpaka sasahivi hatuna taarifa za kitchen party.” “Si ni leo?! Au
nimeshachanganya madesa!” James akauliza kama ambaye hana uhakika. “Ndiyo, ni
leo. Lakini sisi hatujasikia chochote.” “Acha nizungumze na Jema.” “Nashukuru
mwanangu. Na Grace ameshafika kwa ajili hiyo.” James akaona kuna uzito,
akampigia Jema.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Najua upo
busy, lakini nina swali la haraka. Mambo ya mualiko wa kitchen Party,
nani anashugulika nayo?” “Ukimaanisha nini?” “Upande wa wanaotaka kuhudhuria.” Jema
akafikiria kwa haraka akawa hajaelewa. “Ukimaanisha upande wako?” Jema
akauliza. “Ndiyo.” “Ni nani aliyetaka kuhudhuria na hajaalikwa mpaka sasa?
Maana nilisema hata ile siku ya kikao cha kwanza nyumbani kwako siku
uliyonichumbia, kuwa kina Viola na mama yako watatupa idadi ya watakao taka
kuhudhuria, niwape kina mamdogo kisha wawafanyie taratibu. Maana mama zangu
ndio wameandaa. Nahisi kila kitu kinakwenda sawa. Na kila kikao kina Viola
wamekuwa wakihudhuria vizuri tu na kuchukua sare pia.” “Kina Magesa hawajapata
mpaka sasahivi.” Jema akashangaa.
“Kwamba
hawana mawasiliano pia na kina Viola na mama James!?” Hapo
ndipo akili ikamrudia James. Ni kambi mbili tofauti. Kimya. “Au wao
kina Magesa walitakiwa kupewa huduma ya tofauti na waalikwa wengine?” Jema
akauliza. Ila ile uliza yake, James akaona itampotezea amani. “Nafikiri
watawasiliana nao tu. Wewe usijali. Vipi lakini?” “Sitaki nionekane kama
nawanyima shuguli, ikazua maneno mengine. Wakanipa sifa nyingine mbaya zaidi.”
“Usijali. Acha mimi nitaliweka sawa hilo. Nataka kujua wewe unaendeleaje. Mbali
na kila kitu, mke wangu mimi anaendeleaje?” Kidogo Jema akatulia maana
kifua kilishaanza kujaa hasira akikumbuka mara ya mwisho alipokuwa nyumbani kwa
Nanaa na jinsi alivyomjia juu.
“Wanakuandaa
lakini kwa fungate! Maana mwenzio nipo tayari, jumamosi usiku ni usiku wetu.” Jema
akaanza kucheka. “Usiniambie hakuna maandalizi yeyote!” “Ujiandae kula kuku kwa
mrija.” James alicheka sana. Hakutegemea kumsikia Jema akiongea hivyo.
Alicheka sana. “Jema huyo!” “Utachoka mwenyewe! Mimi nipo tayari.” James alicheka
sana na kumfanya Jema atulie zaidi. “Sasa ujue na mimi naendelea kujinoa
zadi. Wewe si unapagawishwa na kiss za mdomo tu?” Jema alicheka. Hapo
akashindwa, akakata simu akicheka sana. Na James alimfanyia makusudi akijua
ataona aibu atakata aendelee na mambo yake. ‘Acha matusi James.’
‘Nilishakwambia hayaitwi hivyo.’ James akarudisha majibu
kwa haraka akijua huko atakua akicheka kwa aibu. ‘Mimi naona tuyaite tu
hivyohivyo.’ ‘Unakosea Jema!’ ‘Mimi sina neno. Nayapenda makosa yangu’ James
akacheka sana.
Wifi.
Alipoagana
na mpenzi wake tu, akampigia Viola wakasalimiana vizuri tu, akaamuuliza. “Kwani kina
Magesa wanapelekewa mualiko na nani?” “Na nani wifi yangu? Sisi nyumba za
mamilionea hatukaribishwi.” Akajibu Viola na kuendelea. “Nanaa
amepandishwa juu sana na Mungu, sisi tena hatufai kwenye maisha yake. Hata
hivyo kwake hata sipakumbuki. Tulifika hapo siku moja tu, tena usiku.
Tulikwenda kumuomba msamaha kwa mabaya tuliyomtendea wakati tukiishi naye.
Tulikuwa na kaka pamoja na mama. Nanaa alipotuona tu tumefika sebuleni kwake, akaaga
na kupandisha juu gorofani kwao.” “Haiwezekani Viola!” “Muulize
kaka ambaye anampenda sana Nanaa. Atakwambia kama nimeongeza jambo. Tena
tukamwambia tumekuja kuomba msamaha, tuzungumze. Akasema tuzungumze na mumewe.
Yeye amechoka kutusikiliza sisi. Ashatusikiliza sana tokea anakua. Mungu amempa
masikio mengine, yaani huyo mumewe, milionea. Yeye hachoki kusikiliza.
Sisi tuongee mpaka tuchoke. Nanaa akapandisha juu tukimtizama hivi. Hata maji
ya ukaribisho ya kudanganyishiwa, hatukupewa. Tukaondoka, mimi na Vai
tukajiambia tumuache kabisa.” Viola akaendelea taratibu.
“Sasa kama
hali zetu sisi unavyozijua. Maeneo tunayoenda, si atakayoenda Nanaa wa siku
hizi. Kwa hiyo kwa kifupi, hatujawahi kugongana hata kwa bahati mbaya
barabarani, ila tulimuona siku ile alipokuja pale kwenu siku ya mahari. Na
hatukutaka kumkera. Maana Nanaa ni roho ya kaka James, na sisi tuliambiana
tusimuudhi kaka, atulie aoe kwa amani. Tukajiweka pembeni kabisa. Alikuwa
amekaa pale katikati ya wale matajiri pale, tungemfikiaje?” Jema
akazidi kushangazwa na Nanaa, kwamba alishindwa hata kusalimia ndugu zake!
“Sasa
kujibu swala la mwaliko, sisi hata hatukujua kama wanataka kutusikia au
kualikwa na watu kama sisi. Kwanza nahisi wangekataa kualikwa na sisi, labda
wewe mwenyewe. Kingine, hatuna namba zake za simu. Hatuwasiliani kwa la kheri
wala la shari. Kwa hiyo kwa kifupi, mialiko michache tuliyopewa na mama mdogo wako
Mode, mama kawapa mashoga zake, wakamchangia ndio huyo akawapa mama zako pesa.
Na nafikiri hicho kikundi chake alichowaalika wamejipanga wenyewe mpaka na
zawadi zao. Mengine mimi siyajui wifi yangu. Kaka ndiye yupo karibu na hao
watu. Sio sisi.” Jema akachoka kabisa na kuamini Nanaa anao watu wake.
Akakumbuka
hata kutomuona siku alipochumbiwa nyumbani kwa James, lakini alimuona kwa Kumu
akiwa bega kwa bega na Naya. Akakumbuka siku ya kulipiwa mahari jinsi
walivyokuwa wamekaa kivyao, tena kitajiri! Akaumia sana. Akajua anamdharau.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
James
akampigia Viola. “Nani anamialiko ya kitchen party?” Akauliza baada ya salamu. “Mama yake
mdogo Jema alitupa na vikoi, tukamkabidhi mama. Mama amewapa mashoga zake wanaocheza
nao kikoba huku mtaani, na waliokuwa wakifanya nao kazi Moshi. Naona
wamejiandaa kweli. Watakwenda kama kikundi.” Viola akajibu kwa heshima
tu na kujiweka pembeni maaana alimjua kaka yake na Nanaa. James akakwama, akawa
ameachwa njia panda. Inamaana kina Magesa hawajaalikwa. Akamuaga na kukata.
Kila Mchuma Janga, Hula Na Wakwao.
Akatumia
akili akampigia simu mama G. “Na mimi nilisahau kabisa, ndio Jema ananikumbusha
vile alivyosema siku ile pale nyumbani kuwa kina mama na Viola ndio
wangeshugulikia. Kwa hiyo hao ndio waliokuwa wakisaidia maandalizi ya kitchen
party pamoja na mama zake Jema. Wamepewa mialiko na nafikiri kwa kuwa hamna
mawasiliano nao, hawakujua jinsi ya kuwafikia au hawakujua kama mngetaka
kuhudhuria. Nilivyosikia kutoka kwa Viola, ni kama mama amewapa marafiki zake.”
“Hakuna shida James mwanangu. Bora kufanikisha hili.” “Unisamehe. Mambo yamekua
mengi nikasau kuwa hampo karibu hata na kina mama pia.” Hiyo
kauli ikamuumiza mama G.
“Ningefuatilia
mwenyewe, ili kuwapa.” “Hakuna shida kabisa. Sisi tunawaombea kufanikiwe.” “Amina.” James
akaaga na kukata. Akakumbuka mbali na wadogo zake na mama yake, alimpeleka na Jema
pia hapohapo nyumbani kwao, wakamshindwa wao wenyewe. Akaona asijiingize kwenye
kuvuna kwao. Bila kutarajia Nanaa akawa amechuma janga, anakula na
wakwao. Na James naye hakutaka kurudi kabisa kulizungumzia hilo kwa Jema.
Akajua anaweza kumuudhi bure akaharibu shuguli nzima. Akaachana nalo kabisa.
Kitchen Party
Jema
alikwenda saluni. Akatengenezwa vizuri sana. Kitchen party ikawa ya
kiswahili haswa. Mamdogo akaleta mashangingi ya jiji. Lugha za aibu tupu humo
ndani. Kila kiungo kinatamkwa kile kilivyo. “Mwali hafundwi hadharani, ndio
maana tumejifungia humu ukumbini, tumfunde mwali wetu. Atakayesikia, na
hayamuhusu, ajue kajitafutia.” Basi kazi ikawa ya kukata mauno, Jema anacheka
mbavu hana. Kina mama wa kichaga wakakutana na Wazaramo wenye jiji lao. Hawajasomea
udaktari lakini kila kiungo mwilini wanakijua na kazi yake. Viuno feni. Mabonge
kwa wembamba. Mwanamke nyonga, makalio majaliwa. Ndio ukawa usemi wao usiku
huo wakisema usisingizie huna tako kubwa, kinachokatwa ni nyonga si tako. Hakuna
tafsida, mambo hadharani.
Kukachezwa
taarabu humo na mambo ya chumbani matupu. Ikafika saa ya kusasambua begi.
Muandaaji mamdogo Mode. Halafu akakodi msasambuaji kabisa. Anatoa nguo huku
akimuonyesha jinsi ya kutumia na mwendo wake. Jamani Jema alikuwa akicheka
sana. Na msasambuaji akawa anaonyesha nyingine na staili zake za mapenzi. Jema
alikuwa akicheka mpaka kuficha uso. Aibu! Watu wakawa wanashangilia humo ndani
kupita kiasi.
“Jema
kafurahi!” Jelini akamnong’oneza mama yake. “Namuona anavyocheka mpaka machozi.
Ila umemfaa!” “Sitaki dada yangu akaonekane mjinga huko chumbani.” “Kweli
umeamua. Na pombe hunywi!” “Wote tukilewa hapa, hakuna atakayeendesha mambo.
Naenda kulewa nyumbani baada ya hapa.” Jelini akamsaidia kweli dada yake,
akitaka mambo yaende vizuri na wasipoteze zawadi. Akakusanya zawadi zote na
kuingiza kwenye gari ya Jema. Akapanga mpaka kiti cha mbele. Kisha akaweka na
kwenye gari za mama zake mpaka vikaenea. Akatulia mpaka ikaisha na kumrudisha dada
yake nyumbani.
“Nawashukuruni
mama zangu. Nimekua na wakati mzuri mno.” Wakaanza stori. “Mamdogo nimefurahi
sana. Asante. Na Jelini mdogo wangu, asante sana. Umenijenga mno. Mpaka
najisikia wa tofauti!” “Upunguze aibu Jema. Bado unaaibu sana. Utashindwa kumnyonya
mumeo kwa uhuru.” “Na wale wanawake pale walikuwa wanasema kabisa. Tamka viungo
vya mumeo.” “Mamdogo siwezi. Yale maneno mazito sana kumwambia James eti
niingizie…” Akasita nakufanya wote wazidi kucheka mpaka machozi.
“Ila
bwana vile vimezidi. Haaah!” Mama Jema naye akakubaliana na Jema. “Basi ndio
mjue hao wanaume zenu wa uzunguni ndio wanayafuata kwa malaya wa uswahili. Wewe
unafikiri wakifika huko wanaambiwa kwa kizungu?” Mamdogo akafanya wazidi
kucheka. “Mimi nawaambia kweli. Sasa wewe mfikirie mumeo ndio kachepuka, halafu
kakutana na mwanamke kama yule aliyekuwa akifundisha staili za bafuni, halafu
akulinganishe na wewe kama atarudi leo au kesho.” “Mamdogo usiniogopeshe
bwana!” “Mimi nakwambia kweli. Na ukweli umeletwa mbele ya macho yako. Kwa hiyo
kila unapokua chumbani na mumeo, acha uvivu na kiasi. Jua yapo
magumegume kama sisi tunasubiria pande ya pili. Ukishindwa tu, ukajidai kuleta
ya kizungu, sijui umechoka, unanunia mchezo, sisi huku mtaani tunakurekebishia
mumeo.” Zikaanza stori hapo wakicheka sana.
Bag Party.
Huku kwa
wasomi, mamilionea, wakampa shule ya kutosha James. Kuanzia kumuandaa mwanamke,
jinsi ya kufanya naye mapenzi, na maisha ya unyumba wakimjadili mwanamke. Kila
mmoja akaongea lake kuhusu mwanamke. Mizunguko yao ya hedhi na joto lao. Nini
wanapenda, udhaifu wao. Maisha kabla na baada ya watoto. Yakawa mambo mengi
kila mmoja akapata muda wakueleza juu ya ndoa yake, James akisikiliza kwa
makini. Kukawa na kula na kunywa. Kina Geb, Man, Joshua na Lubuva ambao
hawanywi wao wakakubalina kuondoka mapema na James kwa kutumia boti yao.
Walimshauri James akapumzike sababu ya send off siku inayofuata.
Kila Kazi Na Malipo Yake.
Wakati
wanataka kuondoka, Man akamuita Danny. Nusura Danny akimbilie wito. Akajikwaa
kabisa wakati akiwasogelea. Alikuwa Geb na Man, Joshua pembeni kimya.
“Nimezungumza sana na Grace. Hayupo tayari kumkutanisha Fili na wewe. Bado Fili
anakuogopa sana, na anavyosema haachi kumuuliza kama ipo siku atakuja
kumrudisha kwako. Na wakati wote anamsihi mama yake asije akasahu
akamrudisha tena kwako. Mimi hilo sikuwa nikijua, kumbe ndicho
kinachoendelea kati ya Grace na Fili. Anasema kila akisikia safari ya kuja huku
Dar, anamuita mama yake kwa siri na kumkumbusha ahadi yake kuwa alimuahidi hatamrudisha
tena kwako.” Danny alilia sana.
“Safari
hii nikaamua kumvizia ili kujua kwa hakika anachozungumzia Grace. Juzi usiku
wakati nikiwaambia leo tutakuja huku Dar, nikaona wadogo zake wanafurahia, lakini
Fili akakosa raha kabisa. Ndipo na mimi nikajilaumu kuona sikuwa nikitilia
maanani hiyo hali. Sikuzungumza naye kitu ili kuona atakachofanya. Ila baadaye
nikamsikia akimsihi mama yake yeye abaki tu Arusha, atusubirie mpaka turudi.
Ikabidi kuzungumza naye. Mbaya zaidi Fili anakumbukumbu ya ajabu sana.”
“Alinisimulia
siku aliyomsihi anko wake asiwarudishe kwako, yeye na wadogo zake, anasema tena
aliahidi hataongea tena. Atabadilika, lakini anasema walirudishwa, na
wewe ukaua wadogo zake huku ukimpiga yeye makofi.” Kitu kilimpanda Geb,
maana alikumbuka vile Fili alivyomuomba kwa machozi mpaka akapiga na magoti.
Akalia kwa uchungu, mpaka akaondoka hapo kabisa. Yeye alishasahau hiyo siku
kabisa, yaani siku hiyo ndio anakumbuka kwa wazi kabisa, hakujua kama ni
kumbukumbu aliyotunza Fili.
Walisikia
kilio cha Geb akilia kwa sauti ya wazi kabisa akielekea botini, Joshua
akamfuata. “Ni nini tena?” James na Lubuva ambao walikuwa wakisubiri botini
wakauliza. Geb akaenda kukaa chini kabisa na kuzidi kulia akiwa ameinama.
Joshua akakaa pembeni yake bila yakumsemesha kitu.
“Ilibidi
kuzungumza na Fili upya.” Man akaendelea. “Na kumuhakikishia hakuna atakayemtoa
kwenye maisha yangu isipokuwa kifo. Ilikuwa ngumu kufikia naye muafaka, maana
na Grace naye alikumbuka kama hivi alivyokumbuka Geb. Alilia sana na kushindwa
kujitetea kwa mwanae. Kwa kifupi, huyu mtoto anakuogopa Danny. Anakuogopa
sana. Sasa ni hivi.” Hapo Man akabadilisha na sauti. “Fili atakuwepo kwenye
send-off na harusi. Tafadhali nakusihi, hakikisha hakuna mazingira
unakutana naye na mpo peke yenu hata chooni. Ulichokifanya kwangu siku ile kunivizia,
usikifanye kwa Fili. Sitakuruhusu. Na utanikasirisha sana Danny, kwa
kuwa mimi sitamdanganya wala sikusudii kubadili kauli yangu kwake.”
“Fili
anakumbukumbu kali sana. Anazungumzia mambo kana kwamba yote yalitokea jana!
Nimetumia pesa nyingi sana na muda mwingi sana kumfikisha alipo sasahivi,
amepoa, ila hajasahau kabisa. Sitaki turudi huko tena. Naamini umenielewa.” “Nitaliheshimu
hilo kabisa. Hata mimi sitaki kumuumiza zaidi. Nilitaka mahusiano tu.” “Bado hayupo
tayari na wewe.” Akajibu hivyo Man, nakuondoka.
Send-Off.
Siku ya send-off
Kasa hakuwepo kati ya walio alikwa kwenye kuhudhuria, kwa upande wa bwana
harusi kwa sababu hakuwa karibu sana na James. Ila alijua kama siku hiyo
ingekuwa siku ya send-off. Akamuacha kabisa Jelini, ila akakubaliana na
kuwa tokea mwanzo ni kweli Jelini hakumpenda. Maana tokea waachane siku
walipokwenda kula ice cream hakukosea hata kumtafuta kwa ujumbe kitu ambacho si
kawaida ya wanawake kwa Kasa. Wanampenda sababu yakujua honga yake ya pesa
nyingi, akitaka tu sifa. Hilo halikumsumbua kabisa Jelini japo alimuonyesha kwa
vitendo ni nini atapata akimkubali. Kilimshangaza sana Kasa kwa msichana kama
yeye asiye kitu mbele yake, lakini akabakiwa na ajenda moja tu, kusafisha hadhi
yake kwa wenzake wanaofanya nao kazi.
Shuguli
ilikuwa nzuri sana. Wakahakikisha Jema anapendeza haswa. Wakala na kunywa kwa
furaha. Kama alivyofanya kwenye kitchen party na hapo Jelini alikuwa
msimamizi wa shuguli nzima kuhakikisha mambo yanakwenda sawa akisaidiwa na mama
yake mdogo.
Alimuona
Colins na mchumba wake. Akajua meza aliyokaa. Akahakikisha hakosei kupita hapo
hata mara moja. Wakati wa waalikwa kupata chakula, alipomuona yeye na mpenzi
wake wanasogelea meza ya vyakula, yeye akiwa anasimamia ugwawaji wa vyakula,
alitoka kabisa hapo kama kuwapisha. Colins alimuona akashangaa kinamuuma rohoni
kabisa. Akatamani hata kungekuwa na salamu tu, lakini Jelini alimkwepa kabisa.
Akatulia na huyo mpenzi wake akisumbuka rohoni mpaka akajishangaa wakati ni
yeye mwenyewe alimuomba huyo Jelini akae naye mbali.
Akahisi hukumu ndani yake. Akasikia maumivu ya
ajabu akijutia kuzungumza vile kwake. “Nimemuumiza Jelini.” Akashangaa
gafla anajali hisia za Jelini! Akabaki amekaa pembeni ya mpenzi wake, mawazo
yapo kwa Jelini muda wote akijionya arudishe mawazo pale, nakushindwa. Akatamani
hata achomoke, amfuate nje, arekebishe kwa kusema hili au lile, lakini mpenzi
wake alikaba mpaka mwisho hata chooni hakwenda.
Wakati hiyo
hali ikiendelea kwa Colins, wengine walikuwa wakifurahia shuguli nzima. Walichekeshwa
na maneno mengi ya Msema Chochote, MC kwa utani mwingi akimsifia Jema
kwa mumewe kwa maneno ya heshima, lakini utani wa kuvutia. Kila mtu alikuwa
akicheka lakini wao, Colins na mpenzi wake walikuwa kimya, kama wapo kwenye
vikao vya bunge la Ulaya!
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Natamani
leo ndio ingekuwa kesho.” James akamnong’oneza Jema sikioni, wakati wakila.
Jema akacheka taratibu. Kumbe hajaelewa kwa hakika anachomaanisha mumewe, yeye
akidhani akitamani hizo shuguli ziishe, wapumzike. Maana walifululiza
mpaka wao wenyewe wakachoka, kumbe hamaanishi hivyo kabisa na James akajua. Akaona
asimuache, afikishe ujumbe wake. Akamnong’oneza tena. “Lile swala letu la matusi.”
Jema alishituka mpaka akapaliwa. Akaanza kukohoa, James akampa maji watu
wakiwaangalia. “Bwana James!” Jema akalalamika baada ya kutulia na kumfanya
James aanze kucheka. Alicheka James mpaka machozi.
“Wala
havichekeshi!” “Mimi nilijua nijiandae kula kuku kwa mrija!” “Sasa si kesho!”
James akazidi kucheka akimwangalia. “Acha kuniangalia hivyo bwana!” “Mimi
nakuhisi wewe unataka vitendo tu, sio maneno. Au nimekosea?” “Na ulikumbuke
hilo bwana James! Acha matusi.” “Hayaitwi hivyo Jema mpenzi wangu! Mbona
umekazania?” “Naomba usiniambie vinavyoitwa.” James alikuwa akicheka sana. “Leo
kiss hutaki?” “Vyakuuliza wala havinogi.” “Unataka nikushitukize?” Jema
alicheka sana. “James! Mimi sijakupatia mwenzio.” “Na ibaki hivyohivyo. Sitaki
msaidizi.” Jema na James wakabaki wakizungumza wao wawili bila kujali watu
wengine mpaka shuguli ikaisha. Ungejua tu, Jema amefurahi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Napo
Jelini hakunywa, akamrudisha dada yake nyumbani akiendesha gari yake. “Mwenzenu
nimekuza.” Mama Jema akamtania. “Mimi najielewa ila nyinyi ndio hamnielewi.” Jelini
akajibu akiendelea kuendesha. “Hilo nakubaliana nalo. Hata pombe hujanywa!”
“Hii shuguli ni yetu. Sikutaka kuharibike jambo. Sasa kesho! Nahisi
nitaogelea.” “Kwani kuna shida gani ukinywa kiasi au ukaacha kabisa?” “Starehe
dada yangu. Kwa nini kupunja nafsi? Unakunywa na kusahau matatizo yote.”
Jema akamtizama tu na kumuacha.
Waliofanikiwa, Hawakukata Tamaa.
Wakati
anaingia kulala akaona ujumbe umeingia. Akajiweka sawa hapo kitandani huku
akichukia kutozima simu yake, akapumzika. Kwani ni kweli alikuwa amechoka na
shuguli nzima maana yeye aliianza hiyo shuguli kuanzia asubuhi kwa maandalizi.
Kumbe Kasa aliangalia muda wa nchi ya Tanzania na kujua watakuwa wamemaliza
shuguli nzima. Ndipo akamtumia ujumbe. ‘Nilisubiri ukaribisho wa sendoff,
mpaka nikakata tamaa.’ Jelini akasoma akiwa kitandani akacheka baada ya kuona mtumaji na
kurudisha ujumbe. ‘Nilijua hata ningekukaribisha usingekuja Kasa, nilijua haupo
nchini.’ Kasa akaamua kumpigia.
“Kwa hiyo
kama ningekuwa nchini ningekaribishwa?” “Ningejaribu. Kwema lakini huko?”
“Nilikuja kumuona mama kidogo kwa siku chache tu, ninarudi kesho asubuhi kabla
ya harusi.” “Basi msalimie mama Kasa.” Kasa akacheka. “Nakudanganya
mwaya. Usije ibua maswali bure!” “Hamna shida. Vipi lakini send-off?” “Ilikuwa
nzuri sana. Tulikuwa na dada Doro. Hajakwambia?” “Na picha zenu nimeona.” Jelini
akacheka sana.
“Dada Doro
naye!” “Ulipendeza sana Jelini. Wewe ni mzuri.” Hapo Jelini akacheka sana.
“Sema basi,
asante.” “Asante, lakini ujue mwenzio nilipania kupendeza.” Kasa
akaanza kucheka. “Kweli. Kwa hiyo kuanzia juu mpaka chini nilipania.” “Basi
ulijitendea haki.” “Asante mwaya.” Wakacheka kidogo. “Ungependa
zawadi gani?” “Lete stori za Ulaya, na mimi nifahamu japo kwa stori na upige
picha nyingiiii, nipaone Ulaya bila chenga.” Kasa akacheka. “Kama hilo
tu, usijali.” Hawakuendelea sana, wakakata simu lakini Kasa akishangazwa sana
na Jelini. “Ameshindwa kuomba hata pafyumu kama wenzake au Doro!” Ikamuwia
vigumu pakumuweka kwenye kundi la namna gani! Alifanania kuwa mchunaji, lakini
tena sivyo! Mwenzie Doro ameomba pafyumu mbili! Haya, akaonekana kama mwanamke
wa kukubali kila mwanaume, lakini tena sivyo! Akabaki akimtafakari Jelini na
kuzidi kuvutiwa naye. Akabaki hajui chakufanya.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hatimaye Imebaki Harusi Tu. Usipitwe Na Siku Ya Harusi
Ya James Na Jema, Bikra Hawa Ambao Ni Kama Mambo Yao Yanakwenda Kwa Mteremko Yakiwa
Na Baraka Zote.
Nini Kitatokea Siku Hiyo?
Ø
James Amepania Usiku Wake Wa Kwanza Na Mwanamke Kitandani. Wote wamepewa
mafunzo. Watafanikisha?
Ø
Siku hiyo ya harusi Kasa Anataka Kurudisha Heshima Kwa Rafiki Zake
Na Imeshamgarimu Pesa nyingi sana. Sasahivi Hisia Zinaanza Kumchanganya, Japo Doro Ndiye Anayeonekana Kufanikiwa
kwenye mipango yake. Kuwa Karibu na Kasa. Amefanikiwa Mawasiliano Ya Karibu Sana Na Kasa
Akimtumia Jelini kama chambo huku na yeye akisubiri fainali siku ya harusi.
Yaani, anausubiria usiku Wa Harusi kama yeye
ndio Jema.
Ø
Colins naye hisia kwa Jelini, mchanganyiko. Sitaki ataka. Kimempata
cha rohoni. Atakuwepo harusini na mpenzi wake.
Ø
Danny mwenye hamu na majuto kwa mwanae ataweza kujizuia atakapomuona Fili
siku ya harusi.
Usipitwe na
harusi ya James&Jema.
0 Comments:
Post a Comment