Jumamosi Ya Mahari Ya Jema.
Alfajiri
sana wakasikia kengele ya mlangoni. Geb akashituka na kutoka kwa haraka kwenda
kufungua akidhania labda ni Grace ameleta watoto na pia kuwahi asije amsha
wanae waliokuwa wamelala kwa kuchelewa kwa kumlilia mama yao. “Lakini mbona
mapema sana!” Akaingiwa na wasiwasi akiwa anakimbilia chini kwenda
kufungua. Akashangazwa kumuona James pale. “Nimekuja kumuona Nanaa.” “Wewe jana
ulipopigiwa simu na baba yake ulimjibu nini?” “Acha kunihoji Geb.” “Huo ni
usumbufu na kuchanganya watu. Unakua na..” “Haya pisha hapo mlangoni Geb.”
“Huyu anasumbua watu mama na kumchanganya mke wangu. Hajulikani kama anamtaka
au hamtaki! Anataka kumuua mke wangu halafu mimi na wanangu ndio tupate shida!”
“Ndio amekuja kutengeneza na wewe unamzuia! Pisha hapo.”
“Nashukuru,
maana nimeshindwa…” “Hapana James. Anachozungumza Geb ni sahihi. Jana Nanaa
ametolewa hapa hajitambui, wanae wanalia kwa adhabu ulizompa.” “Naona nimejiadhibu
mwenyewe wala si yeye.” “Ungemuua mke wangu James.” “Sasa mbona wewe umekazania
lawama bila kushangaa kwa nini mida hii nipo hapa? Kama ningekuwa nimefurahia
nilichofanya sasahivi si ningekuwa bado nimelala? Sijalala mimi tokea nakata
simu ya baba yake. Sasa nakuja kumuona na wewe unaanza habari zako!?” Wakaanza
kubishana wawili hao.
“Wakati
nyinyi mkibishana, acha mimi nipigie simu gari ya wagonjwa kabisa ije iwe
inasubiri hapo nje ili kuondoka na Nanaa baada ya kumtibua.” “James anataka
kuniulia mke wangu mama.” “Sasa akikosa asikemewe? Aliniudhi je?” “Si kwa…”
“Acha nikachukue simu.” Mama G akawa anarudi ndani. “Basi mama, mimi nanyamaza.
Ila naomba zungumza na James maana…” “Si ndio nimekuja sasa! Wewe Geb vipi!?” “Mbona..” Mama G akaanza
kuondoka tena. “Mimi nanyamaza mama.” “Naona hammalizi!” Wakasikia mlango wa
juu unafunguliwa. “Mmemuamsha sasa huyo mgonjwa, mmefurahi?” “Ni James.” Geb
akajibu na kukimbilia juu akipanda ngazi, James naye akamfuata kwa nyuma.
“Unaenda
wapi sasa!?” “Kumuangalia Nanaa.” “Hapa si hospitali.” Wakaanza tena, mama G akakaa
mbele ya kochi linalotizama ngazi akiwaangalia wakianza kulumbana tena. “Nani
amekwambia nimesema hapa ni hospitali? Wewe vipi leo?!” “Ondoka James acha
kumchanganya mke wangu. Sio unakuja nusunusu, na habari za kumuumiza zaidi.
Unataka wanangu wabaki yatima?” “Kwamba na wewe unakufa?” “Acha ujinga.” Nanaa
akawachungulia hapo kwenye ngazi, James
akampita Geb na kupandisha ngazi mpaka alipo Nanaa.
“Nilikosa
kaka. Ilikuwa ni hasira ya kutokukuona muda mrefu na ukawa hupokei simu zangu.
Hasira nikammalizia Jema. Lakini mimi simdharau.” “Yeye hilo hatajua Nanaa
kwa kuwa alishakuona na watu wengine. Lakini tuyaache hayo. Unaendeleaje?” “Vizuri.
Geb alikuwa akinipima sasahivi ili anipe dawa. Ameniambia sio mbaya. Lakini
naomba unisamehe. Sikukusudia kukuvunjia heshima.” “Mimi
nataka upone. Hayo mengine tuyaache, yatajijibu kwa wakati. Mahusiano
yanajengwa kwa vitendo vya muda mrefu, ila ubaya wake huvunjwa kwa haraka sana
kwa neno hata moja tu. Naomba huko tusipazungumzie tena. Tuache tu kama
palivyo.” Nanaa akazidi kuumia.
James
mwenyewe alionekana anausingizi, hajalala. “Maadamu nimekuona upo salama, acha
niende nikapate usingizi hata wa masaa machache ndipo nianze siku.” “Unaonekana
umechoka James mwanangu. Ingia chumba cha mwisho kabisa, ulale, huko hutamsikia
mtu. Siku ya leo kwako itakua ndefu sana.” “Aisee sitafikiria mara mbili maana
nilikuwa nikiendasha huku nasinzia. Acha nilale kidogo.” Akaanza kushuka.
“Pisha
Geb, wewe vipi bwana!?” “Sijaridhika James.” “Sasa wewe ulitaka kunisikia
nimesema nini wakati aliyeumizwa ni Jema na hayupo hapa?” “Na wewe?” “Mimi
nimesema yaishe.” “Kuisha sio kusamehe, acha kutufanya sisi watoto wadogo.”
“Haya, Nanaa nimekusamehe kama kweli ulikosa.” “Si alishasema amekosa!
Sasa ulitaka kumsi…” “Watoto wote wataamka wawakute mnalumbana hapo.” Mama G
akaingilia.
“Anachoshindwa
kumsamehe mke wangu ni nini? Kwani Nanaa amemuua Jema?” “Sasa kwa nini
unalazimishia mambo yaende unavyotaka wewe?” “Wewe mwenyewe unatesema James
mwanangu ndio maana hujalala, na asubuhi hii upo hapa. Adhabu uliyompa Nanaa
inakutesa wewe mwenyewe na Nanaa pia. Wewe ulidhani ingekuwa rahisi. Nanaa huyo
ni mtoto kwako kama mama uliyemzaa kwa uchungu. Huna jinsi ukamuadhibu roho
yako ikatulia. Samehe ili na wewe leo siku yako iishe kwa amani na furaha.”
“Aisee ni kweli. Mimi mwenyewe nataseka. Ila sina jinsi yakurudisha mambo kama
zamani. Ameongezeka Jema, na sitaki kumchanganya.” “Kwani nani amekwambia Nanaa
anataka kuwaingilia? Wewe umsamehe, nyinyi endeleeni. Hatawaingilia.” “Basi
yaishe Nanaa. Acha undugu ubakie kwetu tu. Huko kwa Jema, muda utajibu.” Geb
akampisha.
James
akacheka na kutingisha kichwa. “Wewe ni mkorofi Geb.” “Huwezi kuua mke wangu
aisee.” “Sasa kwa nini unalazimishia mambo?” “Wewe nenda kalale.” Geb akampisha
na kupandisha ngazi kurudi juu, James akimwangalia. “Umenielewa Nanaa?” “Nimeelewa
kaka, na nashukuru. Ila natamani kama ningepewa nafasi ingine nirekebishe hata
kwa Jema.” “Wewe achana kabisa na Jema. Mwache tu. Nenda kapumzike acha na
mimi nikalale kidogo, nisije nikashindwa kwenda ukweni leo.” “Chumba kisafi na
mashuka tumebadili hata siku tatu hazijaisha” “Hamna neno. Nashukuru mama G.”
James akapitiliza mpaka chumbani, akajitupa kitandani na suruali yake ila
alitoa viatu na shati. Nyumba ikapoa.
“Haya, na
wewe nenda kalale. Wanao wakiamka tu, watakuja hapohapo kitandani kwako.” “Nashukuru
mama.” “Mungu anajibu Nanaa. Ungekufa bure kumbe Mungu wako bado
anakutengenezea njia. Na hata na la Jema, najua linakuuma, lakini jipe muda.
Kila kitu kitakuwa sawa tu.” “Amina mama. Hata sasa angalau nina tumaini.” “Acha
kulia sasa Nanaa! Utaanza kuumwa tena. Tulia mpenzi wangu.” Mama G akaanza
kucheka akisimama. “Sasa na wewe unapigania msamaha kwa nguvu?” Akamuuliza Geb
akienda chumbani kwake. “Vyakubembeleza vimeshindikana. Anataka kuniulia mke,
mimi?” Mama G akazidi kucheka. “Naona leo na maneno yamekutoka!” “Asinitanie
kabisa James.” Wakarudi kulala.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika
saa sita James haamki akaenda kumgongea. “Wewe vipi? Hulipi tena mahari?” James
akashituka kutoka usingizini. “Nilikuwa nimechoka! Kwani sasahivi ni saa
ngapi?” “Saa sita. Toka uende saluni, usitucheleweshe.” James akatoka hapo kwa
haraka. “Vipi Nanaa?” “Naona yupo vizuri. Magesa anamuongelesha huko juu.”
“Utaniagia basi. Acha niwahi. Tutawasiliana kabla ya muda wa kwenda Tegeta.”
“Nije na Nanaa?” “Acha kunichanganya sasahivi Geb. Kwani wewe nilikukaribisha?
Mbona ulikuja kwa nguvu?” “Sasa msianze tena huko koridoni. James nenda wahi
saluni.” “Anataka kunichanganya mimi!” “Nakuchanganya kivipi wakati wewe mwenyewe
ndio misamaha yako haieleweki? Unasamehe nusunu…” “Geb Magesa nakuonya wewe
mtoto!” Kimya.
“Haya,
James pita hapo kimyakimya. Kula au ondoka nenda saluni.” “Mimi njaa inaniuma
mama G. Labda nibebe kitu.” “Geb usiongee neno. James pitiliza jikoni, chukua
unachoweza, uondoke, usitucheleweshe kwenye shuguli ya jioni.” Akacheka wakati
akimpita Geb kwa kumsukuma kidogo kwani bado alikuwa amesimama katikati ya
mlango.
“Grace
ameshafika?” “Jeshi lake liko huko juu na Nanaa. Fujo yote ipo huko juu.” “Na
yeye mwenyewe?” “Wapo hotelini na mumewe, tutakutana nao jioni.” “Na mimi
uniombee ndoa yangu isichuje mama.” “Wewe pia unalo jukumu James mwanangu.
Usibadilike na kumzoea mwenzio. Hao wawili wanakua kama wameoana jana.
Kila wakipata mwanya, wanautumia kwa ajili yao. Watoto hawajawahi kuwatenga.”
“Sema kuwatenga sana. Maana haiwi kama zamani kabla watoto hawajaja. Ila sema
na wenyewe wanafanya juhudi za makusudi kutoua mahusiano yao. Kama wewe
mwenyewe ulivyosema asubuhi, mahusiano hujengwa. Ukizembea tu, rahisi
kuparanganya matofali yote uliyoyajenga.” Akaongeza Geb.
“Halafu
uache mazoea kwa mtoto wa watu. Hata baada ya ndoa, ishi naye kama unatongoza.
Hili hata Joshua atakwambia ndicho kinachofanya ndoa zetu kubaki changa japo
zina muda mrefu.” “Sasa usikae bwana James!” Mama G akamkatisha. “Geb anaongea!”
James akaongea kwa mshangao. Wakacheka. “Acha nisikilize mama.” “Hapana.
Tutakuandalia bag party, hao wote watakuja kuzungumza na wewe. Hata Man
atakuja. Chukua chakula uondoke, leo tusije haribu ukweni.” James akaingia
jikoni akicheka. Akatoka na vyakula wima wima.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
James
alipotoka tu, Geb akamgeukia mama yake. “Naomba nenda na Nanaa saluni.
Akatengenezwe kwa shuguli jioni. Itamsaidia kuchangamka. Mimi nitabaki na
watoto.” “Geb umekazania!” “Niliingiwa na hofu ambayo sijui niisimuliaje!
Unajua ni kama niliona uhai wa Nanaa ukitoka mbele ya macho yangu hivihivi!
Halafu wanangu wanalia, siwezi kuwasaidia kwa lolote! Hakika niliogopa mama! Nikashindwa
hata kuomba, ikabidi kumpigia simu Joshua, akaja kunisaidai.” “Haiwezekani Geb!
Usiku ule!?” “Acha mama yangu. Sijawahi kuogopa maishani kama jana. Nilikuwa nikitetemeka
kama nimeingiwa baridi. Nikawa najiuliza nitafanya nini na watoto wote hawa
bila Nanaa!”
“Lakini
mbona hukuonyesha! Japokuwa wanao walikuwa wakipiga mayoe, lakini nilishangaa
vile ulivyokuwa umetulia na kuendelea kufanya CPR bila kukosea mpaka akaamka!”
“Pale sijui Mungu aliniwezesha vipi kuhesabu na kumpa hewa safi bila kukosea!
Sijui aisee!” Wakaendelea kuzungumza yeye na mama yake huku wakisikiliza kelele
za watoto juu. “Hiyo fujo huko juu huyo Nanaa atapumzika kweli?” “Mwenyewe
anataka hiyo kelele, ndio anasema anajisikia vizuri.”
Mahari Ya Jema.
Iliposika
saa 10 jioni upande wa James wote walikuwa wamekusanyika sehemu waliyokubaliana
wakutane kabla ya kufika kwa kina Jema. Hapakuwa mbali sana na nyumbani kwa
kina Jema. “James ulivyopendeza! Kama siku ya harusi!” “Nimepania Grace.”
Wakacheka. “Asanteni sana kwa kuja.” “Hongera sana aisee!” Wakapeana mkono. Geb
akasogea karibuya Grace na James, na Danny naye alikuwa awasogelee pale, alipomuona
tu Geb amefika hapo, akabadili njia,
akarudi kwenye gari. Geb alimuona akanyamaza tu. Grace hakuwa amemuona, Man
alikuwa akizungumza na simu, alipomaliza naye akaungana nao, stori zikaanza
hapo wakimpongeza James.
Wakajipanga
hapo ndipo msafara wa kwa kina Jema ukaanza. Walipokelewa vizuri sana walikuwa
wakisubiriwa wao tu kwani ndugu wa Jema wote walikuwepo hapo tokea asubuhi.
Jelini akafurahi sana kumuona Colins. “Mchumba umekuja?” “Na mimi nipo Jelini.
Mzima?” “Mimi mzima, eti nimefurahi kukuona!” Akili za Jelini akazungumza mbele
za watu wote huku akicheka. “Na mimi nipo Jelini.” Wakaanza kumchokoza. “Akuu!
Mimi nimemuona mchumba Colins tu. Wengine wala sijawaona.” “Bwana Jelini ni
umependeza!” “Basi mwenzio ni kawaida yangu. Huwa sijui kutisha.” Kila mtu
akacheka, James akamgeukia. “Mimi sijasema neno baya Shem.” “Basi kamsaidie
Jema.” “Jema mwenzio kasema nisinywe bia hata moja. Niangalie jambo
lisiharibike huku. Wote mle na kunywa. Ila nisiongee.” Kila mtu akacheka.
“Ila
unaongea.” Danny akamchokoza. “Nimemsalimia Colins tu mimi. Sijaongea jambo
baya. Eti shem?” “Basi hakikisha kweli watu wana vinywaji.” “Jema
ameshamuambukiza! Mimi nakua mtu wa kufukuzwa tu. Sijaongea jambo baya hata
moja!” “Jelini!” James akawa kama anamsisitiza. “Basi mimi naenda ila
namuhudumia Colins mchumba wangu. Sitaki ahangaike. Akitaka chochote, namletea.
Sitaki apate shida.” “Sasa na sisi Jelini?” “Akuu! Mimi nyie sio jukumu langu.
Kuna watu watawahudumia, ila mimi nimeambiwa niwasimamie kuhakikisha kuna
vinywaji tu.” “Kwa hiyo watamuhudumia na Colins?” “Yeye mchumba namuhudumia
mimi.” Wakataka kuendelea kumuongelesha, James akamuita. “Naenda kuleta
vinywaji.” Akaondoka hapo. “Mahari inayofuata ni mimi kwa Jelini.” Wakaanza
kubishana hapo kama watoto. “Jelini anamtaka Colins tu. Haya nyamazeni.” Danny
akawanyamazisha watu wazima hao na pesa zao, wengine wanacheka.
Nanaa
alikuwa amekaa katikati ya mumewe na mama G. Halafu Grace katikati ya Geb na
mumewe. Kimya kama kawaida yao. Joshua alikuwepo ila Naya alikuwa ndani na
Jema. Alimleta hapo mapema kidogo akawa chumbani na Jema. Joshua akasimama.
“Unaenda kumuangalia nini?” James akamchokoza. “Wasije mtoa mlango wa nyuma.”
“Jema amesema jicho lake haliondoki kwake mzee! Huamini?” “Acha na mimi
nikaridhishe macho yangu.” Joshua akaondoka na kufanya wacheke. Geb akamuona
mkewe ametulia kwa kupoa, akamtingisha kwa kumsukuma kidogo na kumvuta mkono
akaushika. Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu, nakutulia.
Wakaanza
kugawiwa vinywaji kwa vile walivyotaka huku meza ya chakula ikiendelea
kuandaliwa. James mwenyewe alichangia pesa ya kutosha tu kwenye hiyo shuguli
kumsaidia Jema kujiandaa. Kwa hiyo kukawa na vinywaji vyakutosha kwa vile James
na Danny walivyojua marafiki zao. Ilikuwa ni kata mti, panda mti.
Baada ya
shuguli kuanza, James akalipa mahari akiwa na baba zake, mama yake pia.
Wakapeleka mambo kimila. Na hivi bibi alikuwepo, ikawa nzuri na heshima ya
kipekee. Walipokabidhiana mahari, na James kupewa Jema ndipo akatoka naye.
Ukweli walipendeza sana. James alivaa shati rangi sawa na gauni alilovaa Jema. Akatengenezwa
saluni vizuri haswa. Kwa hakika Jema alipendeza. Ungemuona jinsi alivyokaa na
James, ungejua wanapendana na wamekusudia kukamilisha swala la kuishi pamoja.
Majuto, Mjukuu.
Shuguli
ikaendelea watu wakila na kunywa kwa furaha. Lakini akili na mawazo ya Danny ni
jinsi ya kumfikia Man. Macho yake na akili zake vilikuwa kwake wakati wote
akimuwinda angalau ajitenge na kina Magesa azungumze naye. Akashindwa
kufuatilia tukio zima wala hakula kwa uhuru, macho kwa Man wakati wote.
Karibu na
mwisho kabisa, akamuona Man ametoa simu mfukoni. Akaiangalia, akamuona
anamuonyesha Grace, akamuona Grace ameingalia simu ya mumewe, akambusu
midomoni, akasimama na kuondoka pale. Moja kwa moja akajua anakwenda kuzungumza
na huyo aliyempigia simu. Akampa kama nusu dakika, na yeye akasimama kumfuata.
Akamuona amezunguka mbali kidogo na pale kama anayekwepa kelele za kwenye
sherehe, akafuata kwa tahadhari, akajibanza kwenye kona akimsubiria amalize
mazungumzo yake asiingilie.
Alipomaliza
wakati anarudi kundini, Danny akajitokeza kwa haraka mbele yake mpaka
akamshitua. “Kwema kaka!?” “Samahani nimekushitua. Lakini mimi naitwa Danny.”
Man akasimama vizuri akimtizama. “Sitaki kukuudhi mkuu. Nilikuwa nataka tu ujue
nakuheshimu na nakushukuru sana kwa kile unachokifanya kwa Grace na Fili.” “Ukweli
haijalishi kile unachojisikia juu yangu, mke wangu na watoto wetu. Kwa kuwa
Grace ni mke wangu na Fili ni mtoto wangu. Sidhani kama huwa unavizia watu na
familia zao kuwaambia haya unayoniambia sasahivi!” Man akajibu akiwa ametulia
tu.
“Sifanyi
hivyo kwa wengine kwa sababu sijawahi kuwasababishia wengine madhara kama
niliyomsababishia Grace na Fili.” “Sema kwa wengine hujasababisha madhara ya
moja kwa moja. Ila madhara uliyosababisha kwa watu ni makubwa sana,
Danny. Ukisema ni kwa Grace na Fili tu, unakosea.” “Najua nimekosa sana.
Inawezekana nimeshindwa kuliweka hili sawa kwako, tena sasahivi, lakini upo
sahihi. Najua kwa hakika nimekosa.” Man akashangaa anapiga magoti.
“Vipi
wewe!?” “Tafadhali naomba kujua hali ya Fili. Tafadhali sana Man. Hata uniambie
tu kwa mdomo na kama Mungu atakupa rehema kwangu, basi ningeshukuru kama ungenionyesha
picha yak…” Geb akafika hapo wasijue alitokea wapi. Akasimama na mikono mfukoni
akimtizama Danny. Man alimuona jinsi Danny alivyoingiwa hofu na kupaniki. “Nazungumza
naye kwa uzuri tu, Geb.” Danny akaanza kutetemeka mpaka midomo, akisikika
kujitetea kwa hofu ya ajabu. Ukweli iliumiza kuangalia.
Lakini
akajikaza na kuendelea. Akamgeukia tena Man. “Na wewe una watoto Man. Tafadhali
naomba tu kujua hali ya Fili ni hilo tu.” Akawa anaongea huku anafikicha mikono
mbele akitetemeka, na bado alikuwa magotini. “Mimi ni yatima Man. Ndugu wa damu
niliyebaki naye hapa duniani ni Fili tu. Nilikosa sana. Ninachotaka kujua ni
hali yake tu. Na ndio maana nakuuliza wewe kwa heshima, wala si Grace.” Danny
alikuwa mnyenyekevu, usingeweza dhani ni yule Danny aliyekuwa amejawa kiburi.
Man
akamtizama Geb. Geb kimya, macho kwa Danny. Man na yeye akarudisha macho kwa
Danny, akakumbuka na yeye alishapitishwa hapo anakopita Danny sasahivi ila yeye
alikuwa jela, hana wakumlilia wala kumpigia magoti. Kipindi alipofungwa na mke
wake wa kwanza na kumtenga na mtoto aliyemlea kwa mikono yake mwenyewe kama yaya.
Liam. Uchungu ukamuingia.
“Fili ni
mzima. Juu ya kukuonyesha picha yake ni mpaka nizungumze na mke wangu. Grace
akikubali, ndipo nitakuonyesha. Na haitakuwa leo kwa sababu wewe ni mtu wa
mwisho ninayetaka kukutaja kwake leo, haswa akiwa mapumzikoni. Nitazungumza
naye wakati mwingine, akiridhia, utapata picha ya Fili.” “Nashukuru sana Man.
Asante sana. Na naomba uniombee msamaha kwa Grace na Fili.” “Kwa hakika sitafanya
hivyo.” Man akageuka na kuondoka, Geb naye akamfuata nyuma wakiwa wamemuacha
Danny amepiga magoti.
“Nitaipataje
hiyo picha yake, endapo mama yake atakubali?” Akapaza sauti kwa nguvu ikisikika
yakutetemeka. “Utaipata.” Man akajibu akiwa anaondoka wala hakugeuka ndipo
Danny akajikung’uta na kusimama. Akajihisi uchungu wa ajabu, mwanaume akalia.
Akazunguka nyuma kabisa ya nyumba, akaridhika yupo peke yake, akalia sana.
Akakumbuka jinsi alivyokuwa na amri kwenye familia yake. Kwa Grace na wanae!
Heshima aliyoipata kwa ajili tu ya kummiliki Grace! Danny akalia sana
akiombolezea tena wanae. Na kila alipokuwa akifiria Man ndiye anayemmiliki
Grace, mwanamke ambaye hakuwa akitaka hata kuhisi mwanaume mwingine yupo karibu
yake, alilia sana. Tena kwa kwikwi, asijue chakufanya.
Kumbe Geb
alishamfikiria muda mrefu sana. Kabla hajafika hapo, alishajiweka kwenye nafasi
ya Danny kwa kutumia aina ya akili yake. Akajiuliza mengi jinsi ya kumfanya
Grace atoke hapo kwenye hiyo shuguli akiwa hajasababishiwa maumivu mengine na
Danny. Akaweka kila njia akizijadili kichwani mwake. Akajua kwa hakika hata
kama Danny ni mwehu kiasi gani, asingethubutu kumsogelea Grace kwa kuwa itakuwa
ni kama anaweka kidole jichoni kwake yeye Geb. “Hathubutu!”
Akajiridhisha Geb. Akajua atakaye mfuata ni Man tu. Hakumwambia mtu, ila
akabaki akimfuatilia na yeye huyo Man zaidi kama vile alivyokuwa akifanya
Danny. Sasa alipoona Man ametoka tu, akampa muda kidogo na kuangalia alipokaa
Danny. Alipomkosa tu ndipo akawafuata. Danny alilia sana kukumbuka shuka
kumekuchwa.
Kisicho Ridhiki, Hakiliki.
Ukweli
Jelini alimuhudumia vizuri sana Colins tena bila maneno mengi akiwa hajalewa
kabisa. Mpaka chakula alimletea alipokuwa amekaa. Akamkarimu kwa heshima kitu
ambacho si kawaida ya Jelini. Na tena alifanya kwa moyo wa furaha mpaka yeye
mwenyewe akajishangaa. Kwa mara ya kwanza maishani akajisikia kitu cha tofauti
kwa huyo Colins.
Wakati
wanaondoka Colins akamuomba wazungumze. Jelini akacheka akijua anataka
kumshukuru, ila ikawa tofauti. “Nashukuru kwa huduma nzuri sana.” Jelini
akacheka kwa furaha akijua hata yeye ameona jinsi alivyomuenzi. “Lakini naomba
kukwambia jambo na niombe usinichukulie vibaya kama mwanaume asiye na shukurani
au sijielewi.” Jelini akaanza kupoa.
“Nina
mchumba wangu. Na siku ya send off pamoja na harusi, Mungu akipenda na
yeye atakuwepo. Hiki ulichokifanya hapa ni kitu kizuri sana na ninashukuru.
Lakini yeye hatakifurahia akiona unanitamka mbele ya watu, na kunihudumia hivi.
Italeta matatizo.” Jelini alijisikia vibaya, akashindwa kabisa kumuangalia.
Ikawa kama amempiga kibao cha uso mbele ya umati. “Ndio maana nilitangulia
kuomba msamaha, Jelini.” Akamuona vile alivyomuumiza. “Samahani. Sikuwa
nimekusudia ku…” Akasita. Kisha akarekebisha. “Hapana. Sitaomba msamaha
kwa nilichokifanya kwako, kwa kuwa utaniibia furaha yote niliyokuwa nayo
Colins. Nilifanya kwako kwa moyo na sijui ni kwa nini! Kwa sababu hakuna mtu
nimewahi kumfanyia hivyo! Najihisi sijakosa, ila nimefanya kwa mtu asiye
sahihi. Sitarudia tena. Uwe na amani kabisa kufika kwenye hizo tafrija zote
ambazo na mimi nitakuwepo, nakuahidi sitakusogelea wewe na mpenzi wako.” Jelini
alizungumza kama mtu anayejielewa, kisha akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alimuacha
Colins amezubaa hapo. Akataka kuumia pengine hakutakiwa kusema hivyo kwake,
lakini alishazoea kutongozwa na wanawake, kitu kinachowakosesha amani kati yake
na mwanamke wake na kuzua ugomvi kwa wivu wa kupitiliza. Colins alijaliwa sura
ya kike. Alikuwa na uzuri wa namna yake wakuvutia wanawake. Rangi yake nyeupe
hata gizani ungejua ni mweupe. Halafu akapewa umbile la kiume, na urefu wa
kumtoshea kupendeza kwa kila aina ya vazi la kiume analoweka mwilini.
Alichokifanya Jelini kwake si kigeni hata kidogo. Anafanyiwa na mabinti chungumzima
na wamama watu wazima pia huwa wanamtongoza. “Ni wale wale tu, hamna jipaya.”
Akajitia moyo na kuondoka kabisa hapo kwenye tafrija.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jelini akaenda
kutafuta sehemu zilipokuwepo bia, akaanza kunywa. Jema akamfuata baada ya
kuagana na James. “Asante kunisadia
Jelini mdogo wangu. Wageni wameridhika na kila kitu. “Bora yako wewe hata
umeona nimefanya jambo zuri.” “Sasa sio kwa sababu umeona bia, ndio unywe mpaka
ujisahau Jelini. Kuwa na kiasi.” “Sitoki hapa wala siendi popote. Sasa nikilewa
nyumbani pia ni vibaya jamani!?” “Basi. Mimi nakwambia kwa faida yako. Weka
nyingine unywe kesho.” “Mimi nataka kulewa leo. Na sitoki. Nikilewa mama
ataniweka kitandani.” “Wewe unywe kwa starehe zako, halafu shida nipate mimi!”
“Basi niacheni hapahapa labda mwanangu atanisitiri.” Akajibu kwa hasira wasijue
ameumizwa haswa. Wao wakamchukulia ni tabia yake.
“Sasa
wewe Jema unaenda wapi tena?” “Nimeshakubaliana na mama baada ya kitchen party
ndio nihamie hapa. Kwa sasa kakubali nirudi kwangu. Haya sema jingine mama
mdogo.” “Eti dada! Huyu si ashakua mwali?” “Kazi zake huko ofisini utamfanyia
wewe?” Kama kawaida yake akajibu mbovu. “Sasa mwali si anawekwa ndani?” “Umesikia
huyu mmakonde?” Wakaanza kucheka. “Mwenzenu muajiriwa. Likizo naanza jumatano
ijayo. Mama wa kichaga, kaniambia nitulie kazini. Huyo hapo ndugu yenu,
hangaikeni naye.” “Wewe nenda zako. Kilichobaki hapa ni sisi kunywa na kelele,
na wewe huyawezi. Nenda.” “Mimi ndio maana nampenda mama Jema. Ananijua
mwanae.” Jema akaondoka haraka sana kabla hawajaanza kulewa.
Raha ya Penzi, Kupendwa.
Akaingia
tu kwenye gari simu kwa James. “Mwenzio naolewa.” James alicheka sana. “Unampenda
mchumba wako?” “Hilo swali la pili na wewe! La kwanza ulitakiwa kusema unaolewa
na nani?” James akazidi kucheka. “Samahani Jema. Unaolewa na
nani?” “Bwana mpenzi wangu ni mzuri, hujawahi ona maisha! Bwana kaka ananipenda
huyo! Na leo kanilipia mahari. Sema sijafurahi sana.” “Kwa nini tena?” “Anajua
kukiss huyo, ila leo hata haja nikiss.” Jema akawa analalamika kwa
deko. “Labda mazingira hayakuwa rafiki. Si wazazi walikuwepo?” James
akamuuliza. “Kwa hiyo anawaogopa wazazi!?” “Mimi nafikiri ni kuwaheshima tu.
Asifikishe wazazi mbali kihisia.” Jema akacheka na kuongeza.
“Mmh! Basi
nimetoka patupuuu! Nilikuwa nammezea mate! Nikatamani hata anikisi kidogo tu,
lakini wapi! Na alivyokuwa amependeza!” “Kwa hiyo siku haijakamilika?” “Labda
kwa mama mkwe wake maana amekua tajiri gafla. Amelipwa mahari na kupewa zawadi
juu! Huna utakalomwambia mama Jema, asimsifie mkwewe.” James
alicheka sana.
“Lakini si
bibi harusi?” Akauliza akicheka. “Bibi harusi katoka kinyonge.
Na anakwenda kulala kwake kinyongeee.” Akajilalamisha. “Pole sana.
Pengine na yeye alikuwa akikutamani, ila anajikaza tu. Anajiambia huyu,
atanikoma kwenye fungate.” Jema alicheka mpaka akakata simu.
Alipofika
kwake, akakuta James anamsubiria nje ya mlango. Jema alifurahi na kushindwa
kusubiria waingie ndani. Akaacha kila kitu kwenye gari akamkimbilia James.
“Nimekuja kukamilisha siku yako.” Jema akakimbilia midomoni. Alimbusu James
kama aliyekuwa na kiu ya miaka. “Nakujibu swali lako la kwanza, mimi nampenda
mchumba wangu. Sana.” Jema akajibu akiwa amekumbatiwa vilivyo. James
akarudi midomoni, kiss zikaendelea.
Taka Cha Mvunguni.
Ikaendelea
kazi ya kumbembeleza Jelini kwa jumbe ili kumfanya awe upande wake lakini ni
kama akashindwa. Jelini alipigiwa kengele ambayo alijua anatakiwa kuamka lakini
ikawa akibishana nayo maaana hakuwa tayari kuamka upande anaotakiwa, ili
kubadili maisha yake. Colins alimfanya ajidharau sana, maana kwa ukweli Jelini
alikuwa na umbile la mtoto wa kike la kiafrika. Anavutia kwa kumtizama, na yeye
alijua. Kuanzia kichwa mpaka unyayo hata akitembea bila viatu utamuangalia tu.
Kuja kuambiwa vile na Colins, ikamshusha sana. Alishazoea kutetemekewa na
wanaume kama tu Colins alivyozoea kutetemekewa na wanawake. Wote hawajui
kukataliwa. Ile ikamuuma sana mpaka akajishanga inakuje mtu kama Colins
amsumbue kichwa wakati anahangaisha wanaume wa maana zaidi yake!
Doro akazidi
kutapatapa. Anamtaka Jelini kumridhisha Kasa na kumvuta Kasa karibu yake,
lakini Jelini naye ameamua kutulia kwao tu. “Mbona hata
baa huji sasa?” “Mwezio baa nafuata bia za bure. Sasa kama mama Jema ananipa bia
za bure bila masimango si bora nitulie kwetu!”
Jelini akamjibu na cheko. “Kwa hiyo bado
hujanisamehe?” “Kwani ulikosea? Ni kweli japo unauma.” “Kwa hiyo?” “Kwahiyo
nini na mimi ndio nakupunguzia shuguli! Acha nikae kwetu. Ila jumamosi nitakuja
kwako kama nilivyokuahidi. Wala usiwe na shuguli yakunipigia simu kila wakati.
Matusi yako yamesamehewa.” Alimjua Jelini
hawezi hasira za muda mrefu, wakacheka na kuagana asijue jinsi Doro
anavyomchafua kwa kila mwanaume anayemtaka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
v
Safari ya kuoa kwa James inakwenda vizuri si kwa vipingamizi kama
kwa Joshua na Geb watu wake wakaribu. Amefanikiwa kupendwa ukweni. Kitajiri kipi
kwa maharusi hawa wote bikra, na James anatizamia sana fungate?
v
Bado Doro hajafanikisha yake. Lengo lake ni nini? Maana si
kumuunganisha Jelini na Kasa.
v
Kwa mara ya kwanza, Colins amekuwa umiza kichwa kwa Jelini. Kulikoni
hapo?
v
Bale?
0 Comments:
Post a Comment