Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 6. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 6.

 Wakati Jema na James wakijipanga kwa ajili ya mahari siku ya jumamosi, na Kasa naye akaendelea kujipanga kwa ajili ya kumpata Jelini. Lengo ni siku ya harusi aonekane naye kisha kumtenda vibaya akimlipiza kisasi kwa kumuabisha mbele za watu. Ikawa kila mmoja kwake na mchakato wake. Na Jema hakudanganya wala kuyumba. Alijenga mahusiano na ambao hawakuwa wakifikiriwa kwenye jamii kabisa. Viola na Vai! Wasichana wasio na shule wala pesa. Wakasimama na Jema kwa furaha yote, wala Jema hakuwatafuta tena Nanaa na mama G. Ikawa kama Mungu anatumia vinyonge kuwaaibisha wenye hekima. Wakina mama G walijua kuna kulipwa mahari lakini hawakuwa na jukumu lolote wala Jema hakuwatafuta tena, na wenyewe wakatulia.

Akapata uungwaji mkono upande wa mama zake na marafiki zao mpaka akashangazwa. Kazini nako wakatoa michango ya kila sherehe. Wanawake wakachanga kwenye kitchen party na sendoff. Jema alijawa hekaheka za kazi na harusi lakini akiwa na furaha sana. Mama G naye akamwambia Nanaa watulie kabisa ili kumpa nafasi ajiandae kwa siku yake muhimu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kile kitu kikawa kinamla Nanaa ndani kwa ndani hawezi kujisaidia. Majuto yakupitiliza. Akapoa kuliko kawaida ya maneno mengi kama mwanae Magesa. Kuanzia asubuhi mpaka jioni kimya kama hayupo sehemu, kitu kisicho kawaida. Hakuna faraja aliyopokea kwa yeyote hata kutoka kwa mumewe. Ikawa kama amekua mgonjwa tena. Kazi zake ofisini anayefanya ni mumewe. Anadamka asubuhi na mapema kwenda kazini, akimuacha Nanaa akiwa amelala. Geb akabaki na kazi yakumuhimiza kunywa dawa maana bado Nanaa alikuwa ni mgonjwa wa moyo wa kunywa dawa kila siku kusaidia moyo wake kufanya kazi. Hakuna aliyejua jinsi yakusaidia hiyo hali, maana James aliwaambia kabisa, wawe wanamkumbusha asije akasogea alipo yeye wala Jema. Kwamba hata Nanaa akiugua, asiambiwe! Hakuna aliyejua chakufanya.

Ijumaa.

Siku ya ijumaa usiku kuamkia jumamosi siku ya kaka yake kutoa mahari wakiwa sebuleni, Grace akizungumza na mama yake juu ya ujio wao kesho yake kwenye mahari na mapokezi, mama G akamuomba aje na watoto angalau awaone, watabakia nyumbani wakati wao wakienda kwenye shuguli. “Mama bwana! Wewe unataka kunitia shuguli. Nije na wote hawa! Kwanza ni siku moja tu!” “Kwani unawabeba mgongoni au unawapakata huko kwenye ndege? Au kutaka kuninyima tu wajukuu?” “Umeanza mama jamani! Kwanini hukuyasema hayo mapema nikajipanga?” “Ndio nimefikiria nikaona sio sawa mje bila watoto.” Grace akabaki kimya akifikiria.

“Wewe niletee hapa, utaenda kulala na mumeo popote utakako.” Akaanza kucheka. “Ulijuaje?” “Kwani wewe mgeni kwangu?” “Nataka muda na Man bwana, akiwa nyumbani Giana anamganda hataki kushuka mpaka nachoka kusubiri naishia kulala  mimi sijashikwa!” Mama yake alicheka sana. “Basi na wewe ulikuwa hivyohivyo! Ukimuona baba yako, ulikuwa hutaki hata kusogea mpaka upitiwe na usingizi, ndio akuweke yeye mwenyewe kitandani. Hapo muda unakua umeisha, anarudi kwake, mimi na Geb wangu ndio tunaishia patupu. Hatujapata naye muda hata kidogo.” “Bwana Giana kazidi mama! Utafikiri ananifanyia kusudi mimi, Fili na Gian jamani!” Mama G anacheka hana mbavu.

“Na deko lake lile Giana, mama mkwe wako, kama namuona!” “Nakwambia huna utakachomwambia wala kumshawishi, akaelewa! Kwanza inakuwa kama anakua hana masikio tena kwa mwingine, ni baba yake tu! Fili yeye alishajua, basi Man akiingia tu, yeye na Gian wanamuwahi mlangoni na kumvuta pembeni, dada mtu akisikia tu sauti ya baba yao, ni wake. Hapo tena mwanangu yule hataki mtu amuongeleshe baba yake. Yeye tu na vijidonda hata vya miaka iliyopita, anataka baba yake aviangalie, avipulize na kumbembeleza kama ndio akatoka kuumia! Sasa nikafurahia hii safari, nikajiambia nitakuwa na Man peke yangu kuanzia kwenye ndege mpaka hapa na kurudi! Na wewe unataka kunijazia msafara!” Grace akaendelea kulalamika.

“Mimi nitakua nao hapa, wewe utakwenda popote unapotaka na mumeo. Tena mkija asubuhi mnaniletea hapa, nyinyi ondokeni hata mkitaka tukutane huko kwenye mahari, mimi sina neno.” “Kama hivyo sawa.” Nanaa akabaki akisikiliza vile huyo mama anavyojali wanae nakuzidi kuumia yeye kushindwa kumpokea mtu muhimu sana kwenye maisha ya kaka yake! Watu wanamipango ya kwenda kwenye shuguli muhimu ya James aliyekana maisha yake kwa ajili yake, yeye anapitwa! Wakaendelea kuzungumza wakicheka, Nanaa akaona aondoke tu hapo.

Kila Mchuma Janga, Hula na Wakwao.

Akanyuka kochini taratibu, mumewe akamuona. “Unakwenda wapi?” Wanae wote kila kitu kikasimama baada ya mama yao kusimama, macho kwake maana alitoka kitandani ili awe nao hapo sebuleni baada ya kurudi shule na Geb ndiye aliyekwenda kumtoa kitandani ili watoto wake waridhike. Waanze weekend na furaha wakijua mama yao yupo sawa. “Narudi kupumzika ndani. Msiwe na wasiwasi.” Akajibu kinyonge akijaribu kutuliza wanae. “Twende nikusindikize.” Geb akasimama kumfuata maana alijua wazi mazungumzo ya Grace na mama yake yatamuumiza tu. Grace anakuja Dar kwa shuguli ya kaka yake ambayo yeye aliyekuwepo hapo mjini hatahudhuria! Akajua lazima aumie tu.

  Ile anapandisha ngazi ya tatu, akasikia kizunguzungu, giza, Nanaa akaanguka na kupoteza fahamu. Uzuri Geb alikuwa naye karibu akamdaka na kwa haraka sana akampigia baba yake simu. “Mlaze chale na mpe CPR haraka, wakati mimi natuma gari ya hospitali. Mtanikuta hospitalini na madaktari wakimsubiri.” Geb alishafundishwa jinsi ya kufanya CPR na ilikuwa mafunzo mahususi kwa ajili ya huyohuyo mkewe. Watoto wake walikuwa wakilia sana kwa hofu. Walijua mama yao ni mgonjwa, ila kuanguka na kupoteza fahamu na vile baba yao alivyokuwa akimfanyia! Ikawashitua sana. Walikuwa wakilia kwa hofu sana wakimuita mama yao. Ndipo Geb akajua hakuna maisha ya wanae hapo bila huyo Nanaa.

Viliendelea vilio vya watoto, yeye akijaribu kutulia akihesabu kwa makini na kuminya kifua cha mkewe, kisha kumuwekea hewa safi mdomoni akitumia midomo yake ili kumsaidia kusambaza damu mwilini kote mpaka kwenye ubongo. Akafanya kivyo mara kadhaa, mpaka akafungua macho. Baba yake mzazi yupo kwenye simu akimpa maelekezo Geb kitu chakufanya kumpa huduma ya kwanza mpaka gari ya wagonjwa ilipowasili kumchukua ikiwa na maelezo kitu gani cha kumsaidia mpaka kumfikisha hospitalini.

Saa nne usiku Nanaa akawa ameshapewa huduma, yupo kwenye chumba cha hospitalini amepumzishwa. Baba yake na Geb ndio waliokuwepo hapo kwenye hicho chumba. Geb akabaki ameinama tu. “Sijaelewa Geb! Kwani Nanaa aliacha kutumia dawa? Mbona pressure iko mbaya hivi!?” “Anatumia, lakini yupo na msogo wa mawazo ndio maana pressure haitulii.” “Kwa nini hukuniambia mapema?” Ikawa kama analaumu. “Nilijua tumeimudu. Mchana nilirudi nyumbani, nikampa dawa na kumpima, ikaonekana ipo sawa. Niliporudi tena jioni na kumuamsha ili angalau apate muda na watoto, maana walirudishwa nyumbani kutoka shule mpaka mimi narudi jioni walikuwa hawajamuona mama yao, kitu kilichowapa wasiwasi. Ndipo nikamuamsha nakumuomba atoke kidogo tu, wamuone waridhike. Akaniambia anajisikia vizuri akatoka kitandani na kufuata watoto. Alipotaka kurudi chumbani kupumzika ndipo akaanguka, uzuri nilikuwa nyuma yeke, ndipo nikamdaka.” Baba yake akafikiria kisha akawa kama amekumbuka kitu alichosema mwanzo.

“Umesema ana msongo wa mawazo!?” “Hawapo kwenye maelewano mazuri na James. Hiyo ndiyo inamsumbua sana Nanaa.” Ikawa kama amemchanganya kabisa. “Unasema James!? Kwa nini tena!?” “Ni habari yao wenyewe, lakini hicho ndicho kimetibua kila kitu. Na nafikiri ni kama hajui kitu chakufanya kurudisha mahusiano yao.” “Haiwezekani! Kwani James anajua kama anaumwa?” Geb akawa ameshamaliza mazungumzo, na yeye Lubuva alishamjua Geb. Hata hapo alishazungumza sana. Akakumbuka alimwambia hawapo kwenye maelewano, inamaana James hajaambiwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akamuona Lubuva anatoka. Akaenda kumpigia simu James. “Unajua kama Nanaa anaumwa?” “Kwa wewe kunipigia simu, inamaana yupo kwenye mikono salama, na mimi sihitajiki ndio maana mpaka sasa unaona hata sijaambiwa, wewe umeambiwa.” Akajibu James na kumshangaza sana Lubuva. “Yameanza lini hayo!?” Lubuva akashangazwa sana. James aliyemkuta na Nanaa, hawezi kulala kama Nanaa ni mgonjwa! “Upo na watu sahihi sana, wanaoweza kukujibu maswali yako yote.” “James! Hivi umenielewa lakini? Nakwambia Nanaa anaumwa, ni mgonjwa, yupo na hali mbaya sana, anakuhitaji!” “Ndivyo ambavyo ungedhania na mimi ndivyo nilivyokuwa nikidhania hivyo tokea mwanzo. Lakini sivyo ilivyo na yeye Nanaa aliliweka hilo wazi mbele ya familia yake. Hanihitaji mimi. Mliopo hapo ndio watu amewachagua kwenye maisha yake, na ndio amekusudia kuwaweka karibu. Naamini wewe ni mtu sahihi anayekuhitaji hata sasahivi na utamsadia. Usiku mwema.” James akaaga na kumuacha Lubuva haamini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akarudi ndani. “Tafadhali niambie kinachoendelea kati ya James na Nanaa. Hakika sijaelewa!” “Mimi si mtu sahihi wa kukueleza.  Tafadhali naomba rudisha mawazo kwa Nanaa, nimeacha watoto wangu wameingiwa hofu, wanalia, hawajui nini kimempata mama yao. Kumtoa Nanaa kwenye ile hali pale, nafikiri ndilo la msingi.” Ikawa wakati wa Nanaa kula na wakwao, janga alilochuma. Kila mtu na wasiwasi. “Hawezi kutoka kwenye hiyo hali kama hujatibu tatizo Geb! Inamaana hiyo hali itarudia tena, hata kama akitoka hapa kesho.” “Sijui chakufanya Lubuva. Ila najua wewe una jinsi ya kumsaidia Nanaa. Tafadhali msaidie hata kubadili dawa.” “Unakumbuka nilikwambia dawa anazotumia ni za kiwango cha mwisho kwenye tatizo lake?” “Basi nipishe mimi niombe.” Lubuva akatoka, Geb akapiga magoti. Akajaribu kuomba lakini hofu ikawa imemkamata kwelikweli anashindwa hata kuomba.

Akufaaye Wakati Wa Dhiki,…

Akampigia simu Joshua. Joshua akapokea kwa haraka maana ilikuwa usiku, si kawaida yao kupigiana usiku mwingi hivyo. “Kwema kaka!?” Joshua akauliza akisikika kujali, akiwa kitandani na mkewe.  “Nahitaji unibebe mimi na Nanaa kwenye maombi. Nashindwa kabisa kuomba. Nahisi nimeingiwa hofu.” “Upo wapi?” “Hospitalini. Mke wangu amelazwa. Alianguka, pressure ipo juu sana. Mbaya zaidi alianguka mbele ya watoto, alipoteza fahamu kabisa. Kila nikiomba nasikia vilio vya wanangu, nashindwa kutulia mbele za Mungu. Nisaidie.” “Nakuja.” Akamuelekeza walipo. On my way, lakini pia naanza maombi.” “Asante.” Geb akakata simu nakubaki amepiga magoti hapo pembeni ya kitanda cha mke wake, kichwa ameegemeza kitandani. Ametulia tu, picha ya wanae wakilia kwa sauti wakiita ‘mama’ ikaendelea kumtesa. “Mungu nisaidie, nimekwama.” Hilo ndilo aliloweza kuongea mbele ya Mungu wake, akabaki amepiga magoti pale mpaka Joshua alipokuja.

Na yeye akaenda kupiga magoti hapo pembeni yake. Akaanza kuomba bila salamu wala kumuongelesha Geb. “Najua hata sasa unatusikia Mungu wetu na Baba yetu.” Ikawa kama mafuta ya petrol kwenye moto. Geb akapata nguvu ya ajabu. Wanaume hao wawili wakaanza kuomba hapo pembeni ya kitanda alichokuwa amelazwa Nanaa mpaka Lubuva akaingia na kutoka, wao wanaomba tu. Geb ndio alikuwa ameinama kabisa mpaka sakafuni kana kwamba yupo kwenye sakafu ya nyumbani kwake kumbe ni hospitalini. Walinena wakiomba hapo mpaka wakasikia sauti ya Nanaa akimuita Geb.

Geb akainua kichwa kwa haraka na kumsogelea akiwa amepiga magoti. “Nimekosa Geb.” Geb akamshika mkono. “Mimi najua Nanaa. Najua. Tafadhali anza kwa kujisamehe ili utoke hapo.” “Nimekosa Geb. Nimekosa sana.” Joshua akasimama na kwenda kukaa pembeni kabisa akiomba taratibu kama kuwapa nafasi. “Naelewa, ila sasahivi huna utakaloweza kubadili ila kuharibu zaidi. Tafadhali tulia mke wangu ili uje kurekebisha baadaye. Kama nilivyokwambia, sasahivi James amesimama sehemu ambayo hataki chochote kitokee kitakachomfanya Jema akabadili mawazo na kushindwa kumuoa. Mpe muda mpaka wamalize mambo yao yote. Baada ya hapo, Mungu ni mwenye rehema. Atakurehemu tu.” Nanaa akaendelea kulia.

“Watoto wanalia nyumbani, wameona jinsi ulivyoanguka. Hali yako inatuathiri  sisi wote. Naomba tulia, nakuhakikishia unayo nafasi kubwa sana ya kuja kurekebisha baadaye. Hawana dawa nyingine ya kukupa. Ikishindikana hapa ndio basi. Naomba upone Nanaa.” Geb akaanza kulia hapo kama mtoto mdogo hapo, Joshua akaenda kumtoa hapo akaenda kumkalisha kwenye kochi, yeye akavuta kiti na kukaa pembeni ya Nanaa.

“Naomba na mimi unisikilize Nanaa. Sijui kwa undani nini kilitokea, lakini…” “Nimeharibu vibaya sana Joshua. Sijui chakufanya tena. Nimeharibu mno.” Nanaa akaongea akisikika amejawa hofu ya ajabu sana. “Basi hapo akili yako inapogota, ndipo uwezo wa Mungu unapoanzia. Huwa nampenda Mungu, na ndio maana mimi huwa wakati wote namuita Mungu wa impossibilities. Wa magumu, mazito yasiyowezekana kwa akili za kibinadamu. Yeye hajawahi kushindwa. Unakumbuka hata kwenye bibilia Mathayo19:26 Yesu alithibitisha hili?”

“Huyu Mungu ambaye watu wanayemsoma kwenye bibilia akitenda mambo mazito na magumu, Nanaa, mimi nimemthibitisha kwa macho haya ya nyama. Yapo unayoyajua na wewe, ambayo alinitendea na mimi, kama kunirudishia Naya wangu, lakini kwa hakika, nilishafika hapo ulipo. Akili ilishindwa kujua ninatokaje, kama vile Mfalme Daudi, na mimi nikasema, ‘Nitainua macho yangu, niitazame milima. Nikajisalimisha kwa Mungu, nikasema, msaada wangu utatoka kwa Bwana, Muumba wa mbingu na dunia. Hatauacha mguu wako uteleze Nanaa. Yeye akulindaye hatasinzia, kwa hakika, yeye akulindaye hatasinzia wala hatalala usingizi.’ Mstari wa 5 unasema, ‘Bwana anakulinda, Bwana ni uvuli wako Nanaa. Mkono wako wa kuume, jua halitakudhuru mchana, wala mwezi wakati wa usiku.’ Mstari wa 7 unakuhakikishia unasema, ‘Bwana atakukinga na madhara YOTE,’ na ameahidi kwenye mwisho wa huu mstari wa 7, kuwa, ‘Atayalinda maisha yako.’ Mstari wa mwisho wa 8, kwenye hii Zaburi ya 121, unasema hivi, ‘Bwana atakulinda wewe Nanaa, unapoingia na unapotoka.’ Halafu si mara moja. Anamalizia kusema, ‘tangu sasa na hata milele.’ Sijui kama unanisikia?” Joshua mwenyewe akahamasika.

“Nimekosa Joshua. Nimemkosea sana kaka. Hata simstahili huyu Mungu.” “Si kwa Mungu ambaye ni Baba yetu, Nanaa. Yaani huyu Mungu mwenye enzi yooote, anakuahidi wewe Nanaa, kuwa si kwamba ulinzi wake ni pale ukiwa sawa naye! Yaani umepatia sana. Hapana. Yaani jicho lake hata sasa linakutizama hapa ulipo. Anasema, ‘hata milele.’ Huyu Mungu mtakatifu ametoa mwaliko mwingine mzuri sana kwa sisi wakosaji, anasema hivi kwenye ‘Isaya 1:18 Njoo basi tuhojiane’. Mungu anakuita wewe Nanaa sio ukiwa unajiona ni mtakatifu. Hapana. Anakualika kwake vile ulivyo tena akiwa anakutia moyo akijua umekosa haswa. Anakwambia hivi, ‘Ingawa dhambi zako wewe Nanaa ni nyekundu’, mbaya, inatisha kwa namna ya kibinadamu. Anakuita na ahadi ambayo hakuna mwanadamu anaweza kukupa Nanaa ila huyu Mungu wa rehema, anasema hivi, ‘zitakuwa nyeupe kama theluji. Ingawa ni NYEKUNDU SANA kama damu, zitakuwa nyeupe kama SUFU.’ Joshua akacheka.

“Eti naye Yesu, kwenye Mattayo 11:28 Anatualika, anasema, ‘Njooni kwangu, nyinyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha.’ Come on Nanaa! Unataka nini tena? Unataka kipi kingine kutoka kwa huyu Mungu? Anachohitaji ni usemezane naye kama hivi ulivyoniambia mimi na Geb, kuwa umekosa sana. Halafu unamkabidhi yeye ule uzito unaousikia moyoni mwako, that’s it! Halafu anakuhakikishia pumziko! Tena kwa moyo huo wa majuto, hakika jiachie kwa Mungu uone atakavyoligeuza hata hili linalokutisha jinsi litakavyofanyika kuwa jema kwako na kwa James mwenyewe. Ataigeuza hii habari kwa namna ya ajabu sana. Sijui atafanyaje, lakini kwa kuwa YEYE ndiye amesema, hakika ATAFANYA tu. Nakupa muda uitike wito wake. Mwambie Mungu vile ulivyotuambia sisi, kisha mwache akusafishe na dhamira yako pia. Utashangaa sana.” Mpaka hapo neno likafanyika hai ndani ya Nanaa, akaanza kujisikia kuomba.

“Mimi na Geb tutakusindikiza patakatifu pa patakatifu, kuomba rehema mbele za kiti cha rehema. Tutakushika tu mkono tuingie wote, kisha mwachie Mungu uone. You will never go wrong patakatifu kwa Bwana.” Geb akasimama na yeye akaenda kumshika mkono upande mwingine. Wakaanza kuomba naye taratibu. Nanaa akatubu akilia na wenyewe wakiomba vile anavyoomba mpaka akamaliza. Joshua akambusu shavuni. Akacheka. “Vipi?” “Nashukuru Joshua, nasikia kifua chepesi.” “That’s what am talking about.” Akaongea kwa furaha sana Joshua. “Unawajibu mwingine Nanaa, Yesu alimwambia yule kiwete, ‘Inua godoro lako uende.’ Hapo ulipolala si sehemu sahihi ndio maana wanao na mumeo wanalia usiku huu. Kataa hayo maradhi yanayosababisha uwepo hapa. Jiambie na ukatae hiyo hali. Nakutamkia uzima, urudi kulea watoto na mumeo.” “Amina. Na asante Joshua.” Akamwangalia Geb.

“Asante sana.” “Anytime Man. Anytime.” Wakacheka. “Acha mimi niwaache naamini usiku wa leo na nyinyi mtaumalizia nyumbani.” “Naamini hivyo.” “Naomba kukusikia Nanaa.” “Nimepona dhamira. Ile hali ya mzigo ndani yangu imepungua kabisa.” “Naomba iishe tafadhali.” “Basi nasema imeisha.” “That’s what am talking about.” Akarudia Kumu usemi anaoupenda sana akimpongeza. Wakacheka. “Wewe Geb usinisindikize, ili upate muda wa kushukuru na mkeo. Tutazungumza baadaye.” Joshua akatoka.

Kwa Mungu Wa Yasiyowezekana Kwa Wanadamu.

Na kweli Nanaa akaruhusiwa usiku huo wa manane kurudi nyumbani kwa kuwa hakuwa akipewa matibabu ya tofauti na akaonekana anaendelea vizuri. Akashauriwa akapumzike, Geb akaondoka na mkewe. Walirudi nyumbani kila mtu amelala. Nanaa akaenda kumuamsha mama G alikuwa amelala na wajukuu wote kitanda kimoja. “Wote walikuwa wakilia ndio nikalala nao. Vipi?” “Najisikia vizuri mama.” “Utakufa Nanaa uache watoto wewe! Fanya mchezo.” “Basi mama.” “Mimi nakwambia na naomba hiyo ‘basi’ umaanishe. Ushakubali kosa, kama mumeo alivyokwambia, muda utarekebisha. Tulia. Utakufa uache wanao wanaharibikiwa. Ingekuwa wote tunashikilia makosa, unafikiri hao kina Geb ungewakuta hivyo? Unajifunza kutokana na makosa unaendelea na maisha. Jukumu lako la kwanza ni hawa watoto. Leo wanao wamelala wakilia wakiona unatolewa hapa na watu wasiowajua, tena kwenye vitanda vya wagonjwa, hujitambui! Acha Nanaa. Tulia mama. Mimi nakujua huna roho mbaya, ni hasira tu. Hutatumia nguvu nyingi kurekebisha, lakini ukiwa hai sio umekufa.” “Nimeelewa mama. Nimemuachia Mungu, naamini atanisaidia.” “Hayo ndio maneno.” Geb akaanza kubeba watoto wake mmoja baada ya mwingine kupeleka vyumbani mwao kulala mpaka akamaliza.

“Twende tukaoge, ulale.” Geb akarudi kumchukua Nanaa aliyekuwa ameinama pembeni ya kitanda cha mama G. “Mwili umeisha wote! Hapana Nanaa. Badilika bwana.” “Usiku mwema mama. Kesho.” Akatoka na mumewe. Wakaoga na kupanda kitandani mumewe akamvuta karibu na kumkumbatia ili alale. Lakini akamgeukia. “Samahani na pole kukuogopesha Geb.” Kitu kilimpanda Geb, akaanza kulia. Alilia kama huyo Nanaa ndio amekufa. Alilia sana na ndipo udhaifu wake kama mwanadamu ukaonekana wazi. Hakuwa Geb milionea mwenye akili ya ajabu ambayo Mungu alimpendelea. Alilia sana kwa kwikwi mpaka Nanaa akamuhurumia. Ni kama aliona uhai wa mkewe ukitoka mbele ya macho yake na wanae kumlilia, akishindwa chakufanya. Akabaki kuwa Mungu tu.

~~~~~Atafutaye, Hachoki~~~~~~

Huku kwa Jelini Mama Jema akashangaa inakua mchana, inakua usiku, asubuhi Jelini amejaa humo ndani hatoki halafu amepoa si kama kawaida yake ya kelele nyingi. Kukawa kuna kukusanyika hapo kwao kila siku jioni wakija kumuona mama yao, bibi wa wakina Jema. Basi ndugu hao vikao vyao ni vya pombe. Wanakunywa, wanacheka hapo wakiongea hili na lile, usiku mwingi wanatawanyika kwenda kulala makwao lakini si Jelini. Akahisi mwanaume aliyekuwa naye safari hiyo amemtenda. Hakuwa akizungumza mambo yake hapo ndani, kwa hiyo wakati wote walijua anakuwa kwa wanaume.

Siku ya tatu akiwa kazini Doro akapata ujumbe kutoka kwa Kasa wenye alama ya viulizo viwili. ‘??’. Akaelewa anachomaanisha. ‘Leo nimepanga niwahi kutoka kazini nimfuate kwao maana hata baa jana hakuja.’ Akarudisha hayo majibu. Kimya. Asijue swala la kutotokea kwa Jelini baa kwa hizo siku zote Kasa alishalijua ndio maana alikuwa akiulizia mpango wao wa pili.

Doro akawahi mapema sana ili kwenda nyumbani kwa kina Jelini. Akamkuta anajiandaa kutoka yeye na mama yake. “Karibu dada Doro!” Akamkaribisha kwa mshangao, hakutegemea kumuona pale. “Kwanza umepafahamuje nyumbani kwetu!?” “Nimeulizia vijana wa pale kijiweni wa bodaboda ndio wamenielekeza mpaka hapa.” “Kwema!?” Ikabidi Jelini aulize. “Nimekumiss tu.” Jelini akabaki amemtolea macho mama yake akisikiliza akiwa upande mwingine tu hapo ndani.

“Na nimekuja kukuomba msamaha mdogo wangu. Nilikukosea. Nahisi nilikuwa na hasira za kazini nikakumalizia wewe. Naomba usiondoke kwangu. Iwe kama zamani.” Mama Jema akawa hajaelewa. “Nakumbuka jinsi ulivyoniuguza na kunisaidia wakati watu wamenisusa. Ukasimama na mimi kama mtu wako ki ukweli. Nisamehe kwa maneno yote yale.” “Lakini ulichozungumza dada Doro kilikuwa na ukweli. Inawezekana ulizungumza kwa hasira lakini hata mimi nimejifikiria, nimeona upo sahihi. Sijakukasirikia, ila tu nimeona nitulie nyumbani, nijifikirie maisha yangu. Siwezi kubaki nikifurahia mafanikio yako tu wakati mimi sina kitu.” Mama Jema  akakaa kwa mshituko asiamini kama anayezungumza hivyo ni Jelini.

“Kwa hiyo uwe na amani tu. Mimi sijakasirika.” “Kwa hiyo tunaondoka wote?” “Nashukuru dada yangu, lakini hapana. Acha nilale tu hapa kwetu tunakojipepea kwa magazeti. Tutakuwa tukikutana baa, lakini narudi kulala kwetu.” Mama Jema akashangaa sana. “Jelini naye! Ile ilikuwa hasira tu!” “Wala usijali. Mwenzio sijakasirika.” “Twende basi kwa washikaji.” “Hivi hapa umetuwahi kidogo tu. Tulikuwa tunatoka kwenda kwenye kikao cha kitchen party ya Jema. Na huko mama mdogo kaniambia kuna bia za kufa mtu. Acha nikanywe bia za bure.” “Sio za bure. Kuna aliyelipia. Na tuondoke sasahivi maana kikao hakianzi bila mimi.” Mama Jema akadakia na kusimama. “Mama naye! Sasa si bure kwangu!” “Mbona sasa mimi sikaribishwi?” “Wewe wala usilalamike. Kama unataka, twende. Huko ni michango tu.” Ikawa msaada kwao. Wakatumia gari ya Doro kwenda kikaoni.

“Jumamosi kesho naandaa chakula cha jioni kwa marafiki zangu wa karibu. Utakuja nyumbani?” “Hapa tunapeleka mambo mengi kwa wakati mmoja. Leo kikao cha Kitchen Party, kesho siku yake yakulipiwa mahari.” “Jumapili je?” “Tuna kikao kingine tena cha send off. Nitakuwa na mama kwenye kikao na uchovu wa kesho nitataka kurudi nyumbani nipumzike.” “Jumamosi ijayo je?” Doro akaendelea kubembeleza. “Ni kikao cha mwisho cha send off na kitchen party, ndio shuguli zinaanza. Kitchen party jumatano, send off ijumaa, kisha harusi jumamosi.” “Baada ya kikao jumamosi si unaweza kuja?” “Itakuwa usiku na mimi nataka kila usiku niwe kwa mama Jema.” Jelini akaendelea kuweka ngumu. “Sasa hapo Kunduchi na hapa kwenu kuna umbali gani na wewe Jelini? Nitakurudisha.” “Ukiahidi hivyo sawa.” Mama Jema kimya akisikiliza na kujaribu kuelewa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kikao kikawa kimechangamka kwelikweli. Vikajaa vicheko hapo na mipango mizito. Doro na yeye akatoa mchango wake hapohapo na kuchukua mtandio wake ambao ni sare ya kuvaa kwenye kitchen party. Wakiwa wamekubaliana rangi ya kuvaa siku hiyo ni nyeupe na huo mtandio wa gold mzuri sana. Jelini akawa na kazi ya kunywa. Hakuwa amekunywa bia zaidi ya siku tatu ambazo kwake ni nyingi mno. “Nashauri umrudishe nyumbani mama. Inatosha.” “Jema naye! Kwani mimi nimelewa? Nimekunywa kidogo tu!” Jema akamtizama na kurudisha macho kwa mama yake. “Tupe lifti basi.” “Sasa bibi harusi ndio anaondoka tena!? Mama Jema chukua usafiri hapo nje bwana ili tubaki na Jema bibi harusi wetu tupige stori” “Mimi nitawarudisha nyumbani.” Akajitolea Doro. “Si kikao kimeisha?” Jema akauliza. “Ndiyo. Lakini situkae wote ili tupige stori?” “Wewe mamdogo umelewa na kusahau mwenzio mimi bibi harusi. Kesho alfajiri na mapema, natakiwa saluni na mama ananitaka saa sita mchana niwe nimefika kwake. Halafu kuna kitu nataka kuzungumza na mama. Acha mimi mwenyewe niwashushe kwao nikiwa na kwenda kwangu huku tukizungumza.”

Jema akasimama na pochi yake. “Haya, Jelini, inua majeshi.” “Usiku mchanga kabisa huu, lakini naambiwa nikalale kama Jeremy! Jeremy analala saa mbili eti na mimi nalala muda huohuo! Nakuwa kama mtoto mdogo, wakati ningebaki hapa na kina mama mkubwa! Si mamdogo atanirudisha!” “Naomba malalamiko yako ukayamalizie ndani ya gari Jelini. Unanichelewesha.” Jema akamuwekea msisitizo. “Mimi wala sifurahii kuondoka sasahivi.” Wakamsikia akiendelea kulalamika huku anakwenda kwenye gari akawaacha wanacheka.

“Mwenyewe si mbishi kwa..” “Jema tu.” Mama yake akamalizia. “Napo anavitu vyake ambavyo anakubali kushauriwa na vingine hataki.” Jema akaongeza. “Kama kazi?” Mama yao mkubwa akauliza, wakacheka. “Hapendi kazi kama kifo!” “Sasa na wewe Jema ndio tuondoke kabla hajarudi tena.” Wakaaga. “Au abaki mimi nitamrudisha.” Doro akamtibua mama Jema. “Hivi wewe, mbona umemkazania Jelini hivyo!?” “Ni shoga yangu na nikutaka kampani tu!” “Kwa nini hutafuti watu wazima wenzio umemkazania mwanangu na ashakwambia anataka akalale kwao!? Huwa unamuuza?” Mama Jema akawa mkali kwelikweli mpaka akafanya wengine wawageuzie wao macho na masikio.

“Maana umemkazania tokea nyumbani nakusikiliza tu. Na yeye amekuwa muungwana kweli akikwambia kwa yote uliyomtendea amesamehe, ila anataka kuwa kwao. Bado umemkazania mwanangu! Hivi wewe unajua umri wake yule au unadanganywa na lile tako na hips?” Jema kimya maana alimjua mama yake akipandisha hasira, matusi yanatoka kama mvua.

“Umekula pesa ya watu nini ndio unahaha kutaka ukamuuze mwanangu?” “Hapana mama yangu…” “Koma. Mimi sio mama yako. Na koma kumpeleka mwanangu huko unakokazania. Kakunwe wewe, mwache mwanangu. Twende Jema.” Mama zake Jema waliobaki hapo wakinywa wakaanza kucheka maana walimjua mama Jema. “Na bora hukuendelea kumjibu yule. Angekuvua nguo hapa kwa matusi.” Wakazidi kucheka na kubadili stori kama hakuna kilichotokea.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walipoingia tu kwenye gari Jelini akalalamika mpaka akalala. “Kwani ni nini mama?” Akamsimulia Jema kuanzia mwanzo Doro anafika kwao mpaka mwisho. “Inamaana ndiko anakolalaga huko huyu Jelini?” “Sasa sijui kama ni siku zote anakuaga huko au kuna anakokwendaga! Ila leo kwa mara ya kwanza nimeanza kujilaumu kutomfuatilia kwa karibu! Ni kama nilimkatia tamaa mapema!” Jema akanyamaza akitafakari nakushindwa kujua azungumze nini, akihofia kumfikiria tofauti na kuja kujilaumu baadaye. Wakanyamaza mpaka nyumbani.

“Ulitaka kuzungumza nini na mimi?” “Wala sina cha kukwambia mama yangu. Nilitaka tu kutoka pale. Nilishachoka kelele.” Mama Jema akacheka. “Jema na kelele! Sasa utafanyaje ukipata wakwe wenye fujo?” “Nimegundua wanamuogopa sana James. Mno. Na wanasema huwa hawaendi kwake.” “Basi umepona.” “Sana. Tena ndio ushuke nianze kuzungumza na mpenzi wangu.” Mama Jema akacheka.

“Jelini! We Jelini?” Akamuamsha mdogo wake. “Nimechoka!” “Nenda kalale ndani. Mmefika.” Akaangalia nje. “Mama yuko wapi?” “Twende, na mwenzio aende kwake akampumzike.” “Asante Jema. Ila sina hela na ninashida sana.” “Umeanza!” “Sasa mimi nitaishije jamani!?” “Yaani wewe ukiwa hata usingizini unawaza hela tu! Nipigie kesho mapema kabla sijaenda saluni.” “Mimi ndio maana nakupenda Jema.” “Shuka bwana acha kunidanganya.” Mama Jema akacheka na kushuka garini. “Tatizo lake Jema haniamini!” Akafunga mlango na kuingia ndani na mama yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Bado Doro ambaye ameshakula pesa ya Kasa anatakiwa kufanikisha miahadi ya kumfikisha Jelini kwa Kasa huku mama yake akianza kuweka ngumu, na Jelini kuwa na msimamo kwenye maamuzi yake. Ni nini kitaendelea?

 Maandalizi ya siku ya mahari yanaendelea. Bado Nanaa nje ya tukio.

Baada ya yote, je, Geb atafanyaje? Uwenyekiti wa harusi ya James, rafiki wa tokea vijana wadogo kabisa, akaja kuwa shemeji-baba mkwe, bado atataka?

Grace anakuja jijini kukutana na Danny, akiwa mke wa Man.

Nini kitaendelea siku ya mahari?

Kasa atafanikiwa kwa Jelini?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment