Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 5. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 5.

Doro akasikika kishawishi akitaka kumvuta Kasa kwake asijue ilivyomgarimu muda na pesa mpaka kumfikia. “Mbali na ile baa  mnayopenda kwenda kunywa, sehemu gani nyingine ya hadhi unaweza kwenda naye ili na mimi nije? Mimi nitalipia huko. Usiogope garama, ila naomba isiwe pale tafadhali. Sehemu kama zile mimi siwezi kufika.” Kama kawaida ya Kasa, linapofka swala la hadhi yake haumi maneno mpaka akamfanya Doro abakie bubu.

“Basi niombe namba yako, nikuandalie mazingira mazuri, umfikishe hapo. Nyinyi mkifika muagize chochote mnachotaka, nitalipia. Mengine niachie mimi.” “Kwanini unajihangaisha na Jelini kaka yangu!? Yule mtoto pasua kichwa.” “Samahani Doro. Mimi ni mkweli na muwazi. Na pia si mkurupukaji. Huwa napanga mambo yangu. Tafadhali liheshimu hilo.” Hapo Doro akatishika na kunyamaza.

“Namba?” Kasa akauliza kwa amri kidogo. Akamtajia. Akamuona anafanya kitu kwenye simu yake. Baada ya muda mfupi sana ikathibitishwa. Kuangalia ni pesa ndefu mpaka Doro akamtizama usoni. “Naomba umtumie pesa sasahivi ikiwa bado mapema kwa ajili ya kununua nguo yake yakuvaa jioni na kama angependa kwenda saluni, ili asijisikie yupo out of place akifika hapo hotelini.” Hicho nacho kikamuuma Doro. Yaani ampe na Jelini ile pesa! Alishafurahia kuwa pesa yote ni yake. “Mchana mwema.” Kasa akatoka kwa kiburi. Kwanza alinukia mafanikio. Msafi wa kung’aza weusi wake. Juu mpaka chini kiatu safi. Doro akashangaa sana mtu kama huyo amekutana wapi na mtu kama Jelini! Kikabaki kikimuuma na kumshangaza akitamani ingekua yeye.

Jelini hakusoma. Si mstaarabu, mtoto wa mtaani kabisa. Na ni kama yeye ndiye anayemtunza. Akichoka nguo au akitaka kubadili kabati, basi Jelini alijipatia nguo za maana tu kutoka kwake maana ni kweli Doro alikuwa akijua kujipangilia, na hakupenda kurudia nguo mara kwa mara. Leo Kasa anaonyesha msimamo kwake na kuomba heshima kwenye maamuzi yake. Akapoa.

Tamaa Ikichukua Mimba, Huzaa Dhambi, Na Dhambi Ikisha Kukomaa, Huzaa Mauti.

Akampigia akiwa na jazba, wivu unamfanya anashindwa kuhema kwa rafiki yake kipenzi waliyekuwa wameshibana na kubebana kwenye mengi. Jelini alikuwa amelala kitandani kwa Doro, hana habari. Akaamka na kupokea simu. “Yaani wewe unalala mpaka sasa hivi!? Wewe utakuwa mtu wa namna gani?” Kidogo Jelini akashangaa. “Kwema dada? Mbona kama unawaka asubuhi na mapema?” “Kwanza si asubuhi na mapema. Watu na akili zao sasa hivi wapo kutafuta maisha. Wewe unalala hapo ukipulizwa na baridi safi kwa sababu mimi naamka asubuhi na mapema kuhangaika kutafuta pesa. Ingekuwa watu wote tunalala hivyo si wote tungegeuka mafala kama wewe.” “Hee! Yamekua hayo?”  Jelini akashangaa sana. Kwanza hakutegemea!

“Mimi nakwambia ukweli.” “Yameanza lini yakuambiana ukweli kwa namna hiyo!?” “Tazizo lako wewe ni mbishi, na huambiliki. Nakutunza kwangu na kukulisha. Hata pombe pia ukiishiwa mimi ndio nakunywesha lakini unakuwa na kiburi kwangu?” Jelini akanyamaza kimya akimsikiliza asimuelewe na kuamini kama yote hayo anayaongea yeye tena kwake! Hakutaka kumjibu kabisa. Akanyamaza akimsikiliza anavyomtapikia.

Doro mtu wake sana na hata akiwa na matatizo Jelini ndio faraja na msaada wake. Leo anamuwakia wakiwa wametoka kunywa naye, na anamjua Jelini vizuri tu. Mvivu na kazi yake kula, kunywa na kulala. Urembo ndio fani yake. Avae apendeze, basi. Akaongea mengi akimkumbusha hili na lile, Jelini akimsikiliza mpaka akamkatia simu. Usingizi wote ukamuisha. “Akufukuzae hakwambii toka. Naona hapa tushafika mwisho, nihamishe kikao kwa mama Jema.” Akatoka kitandani na kwenda kuoga. Akajiandaa na kuchukua vitu vyake vyote ambavyo alikuwa akiacha hapo. Hakuacha hata mswaki. Akatoka kurudi kwao.

Nyumbani ni Nyumbani.

Hakumkuta mama yake wala mwanae Jeremy. Akajua mama yake yupo kwenye shuguli zake, mwanae shule. Akashukuru hatapata maswali mengi na mizigo aliyorudi nayo. Akapanga vitu kwa haraka, wakati anamalizi mama yake akawa anaingia. “Bibi yako anaingia leo.” “Best yangu yule, hana neno. Nalala naye.” “Hapana Jelini. Analala na Jema. Jema amesema anakwenda kumpokea na kumleta hapa. Atalala naye. Labda kesho.” “Na mimi nalala naye leo.” “Unataka fujo zisizo na sababu. Na unamjua bibi yako.” Akaanza kucheka. Ila akashangaa ni kama hana hata mpango wa kutoka siku hiyo.

Akamuacha tu mpaka jioni Jema na bibi yake wanaingia hapo na mama zake wadogo na wakubwa nao wakafika hapo kumsalimia mama yao, Jelini hakutoka. Stori zikaanza wakicheka kwa hiki na kile, Jelini yupo hata pombe alizoagiza mama yake mkubwa hakunywa, mama yake akawa akinywa akimwangalia tu bila kumsemesha. Maneno mengi hayamuishi. Mida ya saa moja James naye akawa amewasili nje. Wakamuona Jema anakimbilia nje. “Bwana mwanaume anampenda Jema huyo!” Akaongea Jelini. “Hasikii raha bila kuwa naye. Kamfuata mpaka huku, ilimradi tu awe naye! Na mimi natafuta wangu.” Mpaka bibi yake akaguna. “Ujue bibi mimi sikuelewi!” Vikaanza vicheko kila mtu akiongea lake juu ya Jelini.

 James akaingia na kumsalimia bibi kichaga. Bibi alifurahi sana. “Sasa huyu ndiye mwanaume. Hata katikati ya watu tunaongea yetu.” Akafurahi bibi kila mtu akamuona na lugha akabadili. Uzuri James anaongea lugha ya kwao vizuri tu. Kikaendelezwa kilugha hapo wakicheka sana. Wakala pamoja, wakimuangalia jinsi Jema anavyomuhudumia James hapo mpaka akaaga, wakahamia nje kwenye gari ya James. Walikaa hapo mpaka Jeremy akatoka kumwambia bibi anakwenda kulala, ndipo James akaondoka, Jema akarudi kwa bibi yake baada ya kupata busu la usiku mwema.

Kulikoungua Mpini.

Huku kwa Doro hana habari, alishajiaminisha kwake ni mtakuja kwa Jelini. Jioni baada ya kazi akiwa anaegesha gari nje ya nyumbani kwake, ujumbe ukaingia. ‘Tafadhali iwe mapema kidogo kwa kuwa kesho ni siku ya kazi.’ Akamtajia hotel ambayo anataka ampeleke Jelini na kuongeza ujumbe mwingine. ‘Unaweza kumwambia leo unamtoa kwa chakula kizuri cha usiku ili asishituke mazingira.’ Doro akasoma na kucheka kwa kushangaa. “Yaani huyu ametuona sisi maeneo kama haya hatufiki au?” Na yeye akamjibu akiwa ameshamuelewa amewadharau. ‘Na hivi ni viwanja vyetu sana tu.’ Akamrudishia ujumbe Kasa, lakini hakumjibu tena ila pesa ingine ikaingia. Asijue mpaka hapo Kasa anamfahamu ndani na nje.

Akashuka garini na kuingia ndani kwa kiburi akijua Jelini mwenye shida yupo ndani akimsubiria watoke. Alishamzoea Jelini si muweka kinyongo, kwa hiyo akajua hata kama asubuhi alikasirika, basi atakua alishapoa, asijue Jelini yupo kwao na mama zake akimchokoza bibi yao. Hakumkuta sebuleni akiangalia movie kama kawaida yake. Akajua cha uvivu huyo bado yupo ndani ya mashuka, rimoti mkononi. Lakini hakuwepo hata chumbani kwake kwani Doro asipoleta mwanaume hapo ndani basi analala na Jelini. Akiwa na mwanaume, Jelini anarudi kwao.

Kidogo akashangaa. Akampigia simu akakuta simu haipo hewani. Kuangalia vizuri, alichukua vitu vyake vyote, hana alichobakiza kwake. Akaingiwa hofu kwa kuwa pesa ya Kasa amepokea, na anawasubiri hotelini. Akafikiria kwa haraka. Na kwa kuwa na yeye ni mzuri, tena mzuri haswa, akaanza kujitayarisha yeye mwenyewe kwa haraka ili asimchelewe Kasa.

Kwa hakika Doro alipendeza na akajipangilia haswa kwa kiwango cha aina ya hoteli wanayoenda kukutana na Kasa. Doro mrembo, amesoma na ana exposure. Anayajua ya uswahilini kula nyama choma baa kwa mkono, na ya uzunguni ya kula kwa kisu na uma pia anayajulia. Safari za nje ya nchi kikazi zilimfundisha mengi na kumsafisha fikra zaidi. Kwa hiyo hana shida akikaa katikati ya wenye nazo na wasio navyo pia.

Kisicho Riziki, Hakiliki.

Akatoka mapema tu mpaka kwenye hiyo hoteli. Akaingia na kuangaza macho akijua lazima Kasa angekuwepo huko. Na kweli akamuona kirahisi japo ni kama alijificha ili kama wanaingi Jelini na Doro, basi Jelini asimuone kwa haraka mpaka baadaye. Kasa alikuwa akisoma gazeti wakati Doro akimsogelea, akalikunja na kuliweka pembeni. “Jelini yupo wapi?” Ndio likawa swali la kwanza hata kabla ya salamu.” Doro akacheka kwa pozi akijua na yeye amependeza, maana ukweli Kasa alijua kujipangilia. Hapo alipokaa tu, alionekana yupo vizuri.

Doro akavuta kiti na kukaa mbele yake. “Hamna salamu wala karibu?” “Wewe tulishaonana mchana. Tupo hapa kwa ajili ya Jelini.” “Jelini ni tapeli. Nimempa ile hela akaniambia anakwenda kununulia nguo, amepotea na simu amenizimia. Ila nimeshamzoea. Ni kawaida yake. Akiona pesa anakua kama mwehu! Anatabia ya udokozi pia.” Kasa akabaki akimsikiliza. “Sasa ujue hivyo alivyoipata hiyo pesa ya pombe, hutampata tena. Atainywea pombe yote mpaka aishiwe kabisa ndipo atarudi.” Kasa akatoa simu bila ya kumjibu. Akamuona anaandika ujumbe. Zilo akapokea ujumbe kutoka kwa Kasa. ‘Nataka kujua kama Jelini yupo kwenye ile baa uliyoniambia anapenda kuwa hapo akinywa.’ ‘Sekunde Mkuu.’ Kisha akamuona anairudisha simu mfukoni na kurudisha macho kwake.

“Na wewe sio mwanaume wa kwanza kutapeliwa na Jelini. Yule mtoto anaishi mjini kwa utapeli.” Akaongea mengi akimchafua Jelini mpaka akajisahau yupo mazingira ya uzunguni, analeta uswahili. Kasa kimya akimsikiliza. “Analiza wanaume mjini.” Akasikia ujumbe umeingia kwenye simu ya Kasa. “Samahani.” Akajua ndio anaambiwa anyamaze asome ujumbe. ‘Inavyoonekana leo hajafika hapa kabisa hata kwa supu ya asubuhi ambayo anapata kwenye mida ya saa tano. Nimeulizia mida yake ya jioni, inavyosemekanika mara nyingi huwa anawahi kidogo jioni kama hatakaa kuanzia hiyo asubuhi akija kunywa supu. Au kama nikuchelewa, basi ujue atafika na Doro. Sasa na Doro naye leo hajaonekanika. Haijulikani tena watakuwa wamehamishia wapi kijiwe kwa leo, maana kila siku lazima wawepo hapa.’ Kasa akasoma na kuhisi kuna kitu hakipo sawa.

“Mbali na hapa, maeneo gani mengine huwa unapenda kuwepo?” Kasa akamuuliza kwa haraka akijua maeneo yake ni ya Jelini. Akajikanya akiwa amefurahi akijua anajaliwa. Akataja kwingi lakini akagundua alichoongea Zilo ni sahihi. Wanaipenda hiyo baa na ndiko wanapokuwa muda wote. “Kwa sasa Jelini yupo kwenye mahusiano yeyote?” Swali jingine ambalo kidogo lilimuuma Doro kwani ni kama walitoka kwa Jelini, anamrudisha vipi tena kwake!

“Kwani ni mmoja! Jelini haridhishwi na mwanaume mmoja mpaka utashangaa anataka nini kwenye maisha. Malaya yule asiyetosheka na moja wala mmoja.” “Kwa hiyo kama nimekusikiliza sawasawa na kukuelewa ni kama kwa sasa hana mtu.” Kasa akataka kufupisha. “Hana mtu mmoja.” Doro akamuweka sawa Kasa. “Wapo wengi ndio maana na wewe nakuokoa.” Akaongea mengi akimsikiliza huku akiokota anayotaka juu ya Jelini. Akamuona Kasa anaangalia saa yake ya mkononi. Akapoa kidogo. “Nikikaa kama hivi na Jelini, na yeye unahisi atazungumza nini juu yako?” Hilo swali likamfanya Doro kupoa kabisa. Kasa akasimama. “Uwe na jioni njema.” Akaondoka na kumuacha Doro na mshangao kama aliyempiga kibao cha uso.

Doro akatumia akili ya haraka na yeye akatoka na kumkimbilia Kasa. “Nisikilize tafadhali usiondoke.” Kasa akasimama, mikono mfukoni. “Jelini si mtu wa kuweka kisasi. Mimi naweza kukusaidia kumpata.” “Nakusikiliza.” “Pafahamu kwangu. Mimi nitamuita kwangu. Nitamuomba msamaha. Nitamwambia naalika wageni kwa chakula cha jioni anisaidie kuandaa na kuwakaribisha. Na wewe utakuwa mmoja ya hao wageni. Ukija utakutana naye.”  Akawa amejichanganya, hata Kasa hakuwa akijua kama wamegombana, ila akaona aangalie yake. “Lini?” “Acha niweke mazingira mazuri. Tutawasiliana. Lakini kwanza twende ukapaone kwangu ili siku nikikukaribisha iwe rahisi.” Kasa akakubalina na hilo wazo. Wakaongozana mpaka kwake.

Doro alimkaribisha ndani kwa upendo ili angalau amtege wakiwa ndani, lakini Kasa akaingia bila kukaa. Katikati ya sebule, amesimama, mikono mfukoni. “Ni kama kwa maelezo yako, kwa sasa Jelini hana mtu. Nipe jibu la ndiyo au hapana bila maelezo mengi.” “Hapana. Lakini..” “Tafadhali usichukue muda mrefu kutekeleza ahadi yako. Ningependa iwe ndani ya hili juma.” Alimkatiza, akaongea hivyo na kuondoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kazi ikawa jinsi ya kumpata Jelini. Mpaka anaingia kitandani akawa hajampaka kwa simu na kesho yake ilikuwa siku ya kazi. Alilala akiwa ameumia. Kasa alimuumiza, akaona ni kama amemdharau yeye. Ameweka uthamani kwa mtu kama Jelini na si yeye! Lakini akakusudia kuwazidi wote mahesabu. Kasa na Jelini. Na yeye akaanza kujipanga kivyake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Itaendelea.

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment