“Huwezi
kutugawa James. Hiyo tumekataa. Tutabebana hivyohivyo na Jema ajifunze
kutuvumilia.” “Nashukuru Joshua mwanangu.” “Kabisa. Familia nyingi zina
matatizo, sidhani kama yetu yamezidi kipimo. Hapana James. Sisi tumekataa.”
“Basi Joshua. Basi.” Ikabidi James apoe lakini Jema hakujua kinachoendelea.
“Naona mpaka sasa mambo yamekwenda vizuri. Leo najua Jema atakuwa amechoka.
Lakini tungependa kujua mnataka ukumbi gani. Hilo tu. Halafu mambo ya wasimamizi,
mavazi yake bibi harusi na wasimamizi wao, mapambo ni…” “Mimi, Nanaa na Grace.”
Akadakia mama G.
“Labda
mngemuacha kwanza Nanaa.” “Hataachwa mtu James. Nanaa ni mdogo wako, kama
mtoto. Mtoto akinyea mkono haukati. Na Jema ampokee wifi yake
hivyohivyo. Kitakachoongezeka hapa ni mama James. Kwa hakika mama yako
amefurahi James.” “Sana. Nimemuona eti hata bia amekataa ili asiharibu!” “Basi
huyo tutamuingiza kwenye kundi letu. Na mama Jema ili afurahie harusi ya
mwanae, na watu wetu wengine tutakao wachagua. Tutapanga mpaka mambo ya kitchen
Party. Si sawa Jema mwanangu?” James akamwangalia. “Sawa mama. Mimi nashukuru
kwa kutaka kunisaidia. Lakini nilikuwa na ombi.” Akaongea Jema
akimtizama James.
Maneno Yakitamkwa Yametakwa, Harudi.
“Sema tu usiwe na
wasiwasi.” James akamtia moyo. “Nashukuru kwa kusimama na sisi. Ila naomba kwa
upande wangu. Nikimaanisha mambo ya kitchen party, saluni, mavazi na wasimamizi
wetu wote mpaka watoto, nishugulikie mimi nikimaanisha upande wa kina
mama zangu. Kwanza itanirahisishia mimi binafsi kufanya kwa haraka kama James
anavyotaka tufunge ndoa kwa haraka. Na pia nitakuwa huru nao kwa kuwa wananifahamu
na wameshanizoea vile nilivyo. Kingine mama zangu wamekuwa wakitamani kushiriki
kwa karibu sana. Yaani ni kama wameshajipanga kwa hili japo tumewashirikisha
kwa muda mfupi.” Wakajua Jema ameshajenga ukuta kwao. Yaliyotamkwa na Nanaa
nyumbani kwake, yameshamtenga nao. Hawahesabu tena kama wapo pamoja.
“Kwa kufupisha tu, naomba
tugawane. Nyinyi niwaachie mambo yote ya harusi mkisaidiana na James.
Nikimaanisha mbakiwe na shuguli ya siku ile ya harusi tu. Ila kitchen Party,
sendoff na hao wasimamizi wetu wote, mimi nifanye na kina mama zangu. Na
kwakuwa leo nimefanya kazi na hawa mawifi zangu wawili, Vai na Viola,
tukisaidiwa na Naya. Nimeona tumekwenda kwa kasi nzuri tu bila shida. Kila kitu
tumefanya kwa haraka bila kuchelewa. Tena tulikuwa tukicheka hapo jikoni na
Naya, imekua kila ninachokifikiria, na yeye ndio alikuwa akikifikiria
kukifanya, na kina Viola wakatusaidia kwa haraka. Basi naomba Viola na Vai
wasaidie upande wangu. Najua ni ndugu wa James, walitakiwa wawe upande wa
harusi, lakini naona watanisaidia kwenda kwa kasi yangu. Wawe kama ndio watakao
wawakilisha kwenye maandalizi ya upande wetu. Kuwapa taarifa ya kitakachokuwa
kikiendelea.” Kina Viola ndio wamesimama naye! Ikawa ngeni kabisa kwao na
kuwauma kuona wamekosa hiyo nafasi ya kuendesha mambo kama walivyozoea. Jema
amechagua watu duni. Kina Viola wasio na kitu, hawajasoma, wasichana wa
mtaani tu huwezi kuwafananisha na upande wa Nanaa hata kidogo! Ikawa kama
wamefikishiwa ujumbe.
“Kukiwa na kualikwa
kwenye kitchen Party, watawasiliana na nyinyi kupata idadi yenu ambao pengine mngependa
kuhudhuria kwenye hiyo kitchen Party na Sendoff na kuwawakilisha kwenye kamati
za upande wetu. Na mama James amemuomba mama rasmi kusaidia kwa karibu. Kwa
hiyo naamini hakutakuwa na pengo, na mambo yote yatakwenda kwa haraka na
urahisi tukiwa tumegawana. Viola na Vai wakiongozwa na mama James,
watawawakilisha kwetu wakati na nyinyi mkiendelea na James ili kuwa ukurasa
mmoja.” Pakazuka ukimya hapo, maana ni kama wakina Magesa wamepigwa STOP.
Lakini wakakumbuka
pia jeshi la ndugu waliokuwepo usiku huo, wakapoa. Jema si yatima kama Naya au
vile walivyojiwa na Danny kwenye maisha yao. Analo jeshi lake, na wamejipanga.
Mama zake wakubwa na wadogo ni wachaga wa mjini. Wamama wa nguvu na walionekana
wanaelewa mambo, sio wazubaifu. Hawataendesha mambo kama walivyozoea wakigawana
majukumu. Mama G akapoa kabisa. Na kwa aina ya ndugu zake, ndipo wakaamini Jema
alikwenda kwao si kwa shida ila kuomba mahusiano ambayo aliyakosa kwao, sasa
amejitenga na mali zao pia.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakamuona
Naya anamnong’oneza kitu mumewe kisha wakamuona Joshua anakataa. “Ni nini?” James
akauliza. “Anataka kusaidia upande wa bibi harusi. Awe na Jema. Lakini hapana.
Nitashindwa kufanya kazi ya kumsaidia Mwenyekiti, na mimi nitajikuta kwenye
kamati ya Kitchen Party bure.” Wakaanza kucheka. “Kweli! Acheni tu.” Joshua
akaweka msisitizo. “Ila leo nimefanya naye kazi kwa wepesi kweli! Amekua msaada
sana. Naya anaakili ya kufikiria na kutenda kwa haraka. Meza ya chakula
ameandaa yeye mwenyewe akipanga na kuweka napkins kama vile mlivyoona.” “Tatizo
wala si yeye. Ni mimi. Siwezi nikamuacha mahali ambako macho yangu hayamuoni.
Asee nitashindwa kufikiria. Niombe kitu kingine Jema, lakini si huyu.
Tafadhali.”
“Unajua
sijawahi kukuangusha Kumu.” Jema akaendelea kumuombea Naya. “Jema wewe unataka
kuniua kwa pressure.” “Itamsaidia na yeye. Nakuahidi akihitajika popote,
atakuwa na mimi na jicho langu haliondoki kwake mpaka nakukabidhisha mkononi
mwako. Halafu sio kila sehemu atatakiwa kuja. Mambo mengine nitakuwa
nikiwasiliana naye kwa simu tu.” Joshua akafikiria, akakumbuka maneno yanayofanana
na hayo, alipewa na Nanaa, akaishia mikononi kwa Malon. Wakamuona kama
anayefikiria kisha akatingisha kichwa kukataa mawazoni. “Aisee hapana. Labda
siku zenu za vikao vyenu msipange siku moja na vikao vyetu vya harusi. Kama
nyinyi mnafanya jumapili, sisi iwe jumamosi. Ikitokea ni siku moja, iwe mida
tofauti ili niweze kuhudhuria naye. Utanisamehe Jema. Huyu natunza kama mboni
ya jicho langu.” “Sawa. Basi siku zitapishana. Usijali.” Jema akamtuliza.
“Kwa hiyo
mzee utakuwa ukienda kwenye vikao vya Kitchen party pia!?” Swali la James
likafanya waanze kucheka. “Ninapokwambia natunza kama mboni ya jicho, jua sina
mipaka James. Nitahakikisha nakaa sehemu ambayo namuona wakati wote.” “Asante
Joshua. Mimi nitakuwa muangalifu naye. Nakuahidi.” “Nashukuru Jema. Ila
tafadhali tuwasiliane. Kila unapomtaka tu, niambie nijipange.” “Sawa.” Hilo
likakaa sawa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Na mimi
niwe kama Jema. Kuna jambo inabidi kuliweka wazi mapema. Bado nina mahusiano ya
karibu sana na Danny. Na kama mlivyoona hapa, na leo alikuwepo.” Kimya kwa muda,
mama G akamwangalia Geb. Wamebanwa kila kona. Jema ni kama amejitoa kwenye
umoja wao, wa wakina mama Magesa. Na James naye anakuja na Danny ambaye
hawakutaka hata waje wajikute chumba kimoja kama mama G alivyomwambia siku
wakiagana kwenye talaka yake na Grace! Leo James anamrudisha kwao! Pagumu!
“Ulitaka
tufanyaje?” Geb akatumia akili na hekima akauliza. “Na yeye atakuwepo kwenye
kamati.” James akaongea akiwatizama. “Ulitaka afanye nini?” Geb akauliza tena.
“Chochote kile ila nilitaka mjue atashiriki.” “Nafikiri uamuzi ni wako
James. Sisi tupo kukusaidia kwa vyovyote utakavyotaka. Hata kama umeshapanga
timu yako, ukitupa sisi nafasi zingine, haitatusumbua kabisa, ilimradi
kufanikisha tu hilo.” “Sina hata kamati.
Sasa wote hawa waliotoa ahadi, watu wa Danny wakaribu sana. Nashauri tumpe yeye
uweka hazina, kesho pombe zikiwa zimewaisha kichwani, watuambie haya
mamilioni ya pesa waliyokuwa wakitamka hapa ni wao au pombe.” Wakacheka.
“Lakini
kweli. Maana wote waliondoka hapa wamelewa! Tunaweza sema tunapesa nyingi kumbe
pombe ndio ilikuwa ikitoa ahadi.” “Basi acheni Danny awafuatilie. Atawapanga
hata wao ili mpate watu wakuwasaidia kwenye kamati.” Kukawa kama hakuna tena
chakuongeza. Maharusi hao ni kama walikuwa na misimamo yao na watu wao. Wakawa
wastaarabu wakitaka kufuata matakwa yao. Wakaona waagane tu wasubiri siku ya
kikao cha kwanza wakiwepo watu wengine, ambacho James aliwaambia atawajulisha
baada ya kulipa mahari.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati
wanawasindikiza, Jema akamuita Naya kwa kumgusa maana alikuwa akitembea nyuma
ya mumewe kidogo. Akageuka. “Nashukuru kunisaidia.” “Nimefurahia! Wewe ni mtu
mzuri Jema. Nimefurahi umeniamini na wageni.” Jema akacheka. “Sijui kama unajua
hili Naya, wewe unaakili sana ya kubuni vitu. Kuna mfumo ulibuni pale kazini
kiasi ya kwamba umesaidai kuziba pengo la mtu aliyekuwa ameondoka. Anaitwa
Njama. Mumeo alituambia ni wewe ndio ulibuni, akatengeneza vizuri tu akisaidiwa
na watu wa IT. Natumia bila shida. Sipigizani kelele na watu, na kazi siku hizi
zinakwenda zaidi ya zamani.” Naya akacheka. “Aliniambia Joshua. Ila na wewe
umeniamini Jema. Asante. Nimefurahi kufanya kazi. Mwenzio sifanyi kazi yeyote.
Nakaa tu nyumbani. Kwa hiyo leo nimefurahia.” Kumbe Joshua alikuwa
akiwasikiliza. Akageuka. “Asante sana Jema. Ni kweli alihitaji hiki
alichofanya.” Joshua akaongeza.
“Hata
kwenye mambo yako ya maandalizi, ukimuhitaji tuwasiliane tu. Nitakuwa
nikimleta, na mimi pia itanisaidia kuanza kumpa vitu vingine vya kufanya.”
“Basi nitakuwa nikikwambia Kumu. Ili ajikute na vitu vingi vyakufanya.” Mama G
na Geb wao wakawa wakitembea kimya kimya kurudi kwenye gari. Kila mmoja akiwaza
lake. James kimya. Akiwajua hiyo familia na ugumu wanaokutana nao kwa wakati
huo. Danny anarudi kwenye maisha yao bila kupenda na hawawezi kumkwepa tena, na
Jema ameshajitoa kwao! Ikawa ngeni. Walishazoea kuvuta watu karibu na watu
kuwakimbilia, lakini safari hii ikawa tofauti. Akawaacha tu. Wakaaga na
kuondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakajikuta
wamebaki wawili. “Nimefurahi James, nimefurahi sana. Asante kwa heshima uliyonipa
hata mbele ya familia yangu. Mama zangu wote wanakusifia sana. Wanasema umewapokea
na wao vizuri na umewaheshimu.” “Nimeona jinsi mama yako mkubwa alivyokuwa
akizungumza na mimi. Amesema wanaandaa mazingira jumamosi nikalipe mahari,
kunipunguzia mlolongo. Na bibi atakuwepo. Amesema wataandaa tafrija nzuri tu
hapo kwa mama Jema, naweza kualika watu wangu wa karibu, ili tupate muda kama
huu.” “Wamefurahi sana.”
“Nina surprise
nyingine.” Jema akacheka. “Nini tena?” “Unakumbuka gauni ulisema ulikuwa mpaka
ukiliota umevaa kwenye harusi yako?” Jema akabaki ametoa macho. “Tunaweza
kulipata.” “James! Sikujua kama ulikuwa ukinisikiliza na kutilia maanani!” “Nisipokusikiliza
wewe, nimsikilize nani?” Jema alifurahi sana. “Kuna mama anashona, lakini
ameniambia kwake itachukua muda mrefu sababu ya nilivyomuelekeza, ila anayo
sehemu, sio hapa lakini. China. Anasema ukizungumza naye, atawasiliana nao na
kuwatumia vipimo vyako, watatoa gauni kama hilo, hivyohivyo.” Jema akafurahi
sana. Usiku huo kwao ukaisha ukiwa na furaha ya namna yake.
Kisa Kimempata Kasa.
Lakini ikawa
kinyume na Kasa. Wote waliondoka pale wakiwa na furaha lakini si Kasa. Alihisi
kudhalilika vibaya sana. Akaapa ni lazima afanye kitu. Alipoingia tu garini
akampigia simu kijana wanayemtumia sana kwenye familia yao. Hata baba yake, mzee
Kasa mwenyewe alimpenda sababu alikuwa mwepesi na mtekelezaji wa kila jambo
bila vipingamizi. Walimtumia mchana na usiku. “Niambie bosi.” Akaanza
Zilo. “Kuna mtoto anaitwa Jelini. Najua kwa hakika anaishi Tegeta Mwisho.
Sasa nataka unitafutie habari zake kamili.” “Anafanya kazi au biashara wapi?”
“Na usinicheleweshe.” Simu ikakatwa. Zilo akatingisha kichwa.
“Pesa
mwanaharamu! Yaani unaweza kuta mwanaume mwezio anakutumikisha bila heshima
hivihivi!” Akalalamika kwa wenzie kijiweni. “Nani? Kasa nini?” “Kumbe mwingine
nani? Bora baba yake anaadabu na utu, kuliko yeye. Naona kapata demu, anataka
habari zake.” “Tuchangamkie mwana. Si unajua anavyojuaga kulipa?” “Kesho.” “Acha
masihara Zilo! Hela ya leo unataka ilale?” “Sasa usiku huu utapata wapi
habari…” “Twende kwa masela wa Tegeta. Kama mwingi wa habari, usiku huu huu
tutapata habari zake, tulipwe.” Zilo akabaki akijishauri. “Wewe unashida ya
hela, huna?” “Twende.” Zilo akatoka na rafiki yake wa karibu mpaka Tegeta
Mwisho na kuanza kumuulizia Jelini.
Kabla ya
kupambazuka, Kasa akawa na habari kamili za Jelini. Baa anayoweza kupatikanika
bila kukosa, kila siku. Akazitunza hizo habari, ikabaki kazi ya
kujipanga maana baa anayoshinda Jelini haiendani na hadhi ya Kasa kabisa.
Kwanza si mkaa baa. Ila kwa kulipa kisasi, alijiambia lazima ajipange.
Mahari.
Maandalizi
ya kupokelewa mahari yakaanza kwa James, na Jema kutolewa mahari. Nyumbani kwao
pakaanza kuandaliwa, na bibi yake akakusudia kufika mjini kupokea mahari ya Jema.
James alipotumiwa orodha ya vitu vinavyohitajika, akamwambia baba yake, na yeye
akaja mjini kwa ajili ya hilo. Hata James aliona jinsi baba yake alivyofurahi. Alifika
Dar na ndugu zake wengine wawili, na wote wakafikia hapo nyumbani kwa James
wala si kwa mama James. Kwa hiyo James akawa na baba zake watatu hapo nyumbani,
tayari kwa kwenda kulipa mahari. Viola akawa anafika hapo yeye na mdogo wake
kumsaidia kupikia baba zao na usafi. James akashangazwa na hao dada zake waliokuwa
wameshindika, ila akajiambia pengine wamekua, utoto umewaisha. Au wamekutana na
uhalisia wa maisha. Akawa na kazi ya kuwasaidia nauli kila siku akienda kazini
anaacha nyumbani pesa ya matumizi na nauli yao ili wakija waikute.
Mama G
alipotaka kusaidia, James akamwambia mama yake amechangamkia hivyo vitu vya
mahari, amebakiza vichache alivyochukua Danny. Akapoa na kumwambia hata Grace. “Basi mama.
Mimi nashauri tufanye kama alivyosema Geb. Tushiriki vile tutakavyo pewa
nafasi.” “Bado utakuja?” “Lazima mama. James tumetoka naye mbali hata kabla ya
Nanaa. Ila tutakuja siku yenyewe ya shuguli, hiyo jumamosi asubuhi. Nitakuja na
Man tu, tunaacha watoto. Jumapili asubuhi tunageuza.” Grace alishajua
kuwa Danny angekuwepo na anashiriki kwa karibu sana. Man mumewe akamwambia
asiwe na wasiwasi angekuwepo naye wakati wote.
Ndugu wa
mama Jema wakaanza kutayarisha mazingira ya nyumbani kwake kupokea wageni na
sherehe ya siku hiyo. Mama Jema alijenga Tegeta Mwisho miaka mingi sana watu
wakipakwepa. Yeye akanunua eneo kubwa tu. Kwa kuwa hakuwa na pesa akajenga
nyumba ya kawaida sana. Vyumba vitatu tu. Choo kimoja ndani. Hapohapo na bafu. Akatulia
na hao binti zake wawili mpaka Jema alipoondoka. Nje ya nyumba akawa akilima tu
vitu mbalimbali ila migomba ndio ikawa mingi. Mbele ya nyumba akapanda maua
yake ya kawaida tu, nyuma ndio hiyo bustani au shamba. Kukawa shamrashamra kila
ndugu macho na masikio kwa mama Jema wakichangishana kumsaidia kufanikisha
shuguli nzima. Jema akawa ameleta kitu cha tofauti kwao, ndoa!
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakati
James anajipanga kuoa akisaidiwa na marafiki zake wakaribu, Kasa yeye alikuwa
akijipanga jinsi ya kumpata Jelini. Kwanza alijua ni mropokaji, hakutaka amfuate
kwa gafla aingie aibu tena. Hapo akabaki akiwaza. Kasa anapenda kuabudiwa na
kujulikana kuwa yeye ni bora kuliko mtu mwingine. Akampigia tena Zilo. “Huko baa,
anakuwa na wanaume au?” “Tulivyosikia huko baa wanakundi lao wanakunywa pamoja.
Mchanganyiko wa wanaume na wanawake ambao ni wao wawili. Yeye na msichana
mwengine ambaye ni rafiki yake sana wa karibu na ndiye anayeonekana anayo hela
ya kumnunulia pombe kila siku. Kwa hiyo huwa anakuwa naye hapo kila siku jioni
baada ya kazi.” “Kwa hiyo kwenye hilo kundi hana mwanaume?” “Labda niulize
zaidi.” Simu ikakatwa. Zilo akajua ndio ametumwa tena.
Akakimbilia
tena Tegeta, ila safari hii akaamua kuuliza ila pia kujithibitishia. Zilo
akakusanya habari zote. Saa usiku, Kasa akapigiwa. “Sasa
safari hii nimekwenda umbali mrefu zaidi. Nipo hapa baa. Na imebidi mpaka
kuzungumza na muhudumu ambaye anawahudumia wao. Inavyoonekana hili kundi ni la
watu tofautitofauti. Wote, kasoro Jelini wanafanya kazi hizi za maofisini.
Jioni baada ya kazi huwa wanakutana hapo kunywa mpaka usiku mwingi tu. Msichana
niliyekwambia ni rafiki wa Jelini, kwa kumuangalia yeye anaonekana mkubwa kwa
Jelini. Maana nimemsikia akimuita ‘dada Doro’, na ndiye nasikia kampani ya
Jelini. Na hata Jelini ndiko anapokwenda kulala huko kwake.” “Kwa hiyo hapo
hana mwanaume?” “Kwa pale baa nasikia yeye anamfuataga Doro, ili apate bia za
bure na hataki kufanya kazi.” “Nani?” Kasa akauliza. “Huyo
Jelini. Hana kazi wala biashara yakumuingizia kipato.” Akajibu Zilo na kumfanya Kasa afikirie sasa, kwa uzuri na
unadhifu ule, nani anamtunza!
“Ila
nilikwenda umbali mrefu kidogo bosi wangu, japo hujanituma.” “Nini?” “Kutafuta
habari za Doro na kujua pakumpata endapo ungetaka kumfikia yeye kwanza.” Ni hivyo
tu ni Kasa alishindwa kumsifia kwamba amefanya jambo zuri. Lakini hata yeye
alimkubali Zilo. “Kwamba?” Akauliza Kasa kwa jeuri.
“Doro
nasikia yeye ndio anafanya kazi hizi za waliosoma maana nasikia anayopesa haswa.
Hakuna anayejua ni kwanini, lakini ni dada mzuri tu ila kila siku lazima awe
baa ndio maana alipenda kampani ya Jelini ambaye hana kazi na anamsindikiza
popote anapotaka yeye Doro. Nasikia Doro amejijenga vizuri sana, anaishi
Kunduchi. Na hata leo ameondoka na Jelini. Hata usafiri wake wenyewe ni wa
ukweli.” “Anafanya kazi wapi?” Akamtajia. Simu ikakatwa. Ila kwa pesa
aliyotumiwa baada ya kukatiwa simu akajua Kasa amefurahi sana. Asijue jinsi alivyomfanikishia
Kasa. Akawa ameshajua pakuanzia. Kwa Doro.
Atafutaye Hachoki.
Kesho
yake mida ya chakula cha mchana Kasa akawa amewasili ofisini kwa Doro. Baada tu
ya salamu, Kasa akaanza kwa ujasiri kwani alishamuona Doro amechanganywa naye.
“Unakitu ambacho nahitaji msaada wako kukipata.” Doro akafurahi sana akijua ni
mapenzi tu kwani hata yeye alikuwa akilipa. “Hata hunifahamu!” Akaongea kwa pozi
akicheka kike. “Taka cha uvunguni shuruti ainame, si ndivyo?” Doro akacheka.
“Nakufahamu sana Doro. Nafahamu mpaka unapoishi. Ulichonacho ambacho nakihitaji
kwa pesa yeyote ile ni Jelini.” Doro alishangaa sana na kuishiwa nguvu kabisa.
“Jelini!?”
“Ndiyo. Na najua jana aliondoka na wewe pale baa mkielekea nyumbani kwako
Kunduchi.” Ikabidi Doro ajiweke sawa akiwa na mshangao mkubwa sana usoni. Kasa
akacheka. “Si nilikwambia unacho kitu ninachokitaka? Kwa hiyo macho yangu yapo
kwake.” “Na nimemuacha amelala. Mvivu hataki kazi. Yeye kula kulala tu.”
Akaanza Doro kwa jazba. “Basi, nisaidie mazingira ya kumpata.” Wivu ukazidi
kumkaba Doro na kumshangaza asichoelewa nini! Kwamba hajamsikia au!?
“Wewe
humfahamu Jelini. Uzuri ule unawachanganya wengi, lakini wakishamfahamu Jelini
mwenyewe wanakimbia, ndio maana unamuona kakwama kwangu. Wanaume wote
wanajaribu na kujiachia. Sasa wewe unaonekana ni kaka uliyetulia, unajielewa,
ndio nakuokoa. Usijipotezee muda na yule mtoto. Hamuendani kabisa.”
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Huyo ndiye anayesemekana rafiki wa karibu sana wa Jelini. Maneno
yake kwa Kasa aliyeonekana na nia naye ndiyo hayo.
Nini kitaendelea kwa Kasa aliyekusudia kumpata Jelini na Doro ndiye
aliyebakia kama njia ya kumfikia?
Hatimaye Danny na Grace, wanandoa walioanza tokea Chuo, wakiwa wamebeba historia ngumu kwenye mahusiano yao, watakutanishwa na shuguli ya James.
Itakuje?
Usipitwe.
0 Comments:
Post a Comment