Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 3. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 3.

Akamrushia Kumu kazi zake zote na kutoka bila yakuchelewa. Akampigia simu James. “Nimeruhusiwa kutoka na Kumu. Amesema nikajiandae na jioni, yeye atafanya kazi zangu.” “Acha na mimi nitamshukuru. Nimetoka kuzungumza na mama Jema. Amefurahi huyo! Amesema atakuja ila Jelini aliondoka tokea jana tulivyotoka nyumbani, hajarudi tena. Amesema akirudi mapema atakuja naye. Ila ameomba aje na mama zako wengine.” “Mimi nimefurahi James, nimefurahi sana.” “Umenisikia lakini?” “Wewe uamue tu mwenyewe, ukiona sawa, mimi nitashukuru angalau waje na wao washerehekee. Sio watu wabaya.” “Basi nitamwambia anitumie idadi. Na mama James naye atakuwepo na dada zangu.” “Angalau tukutane. Mama huyo ananipigia. Acha nimpokee, najua atakuwa na furaha.” James akacheka na kumuaga.

Hatimaye Na Kwa James Nako Kunaliwa.

Jema aliwahi nyumbani kwa James akidhani itabidi kusafisha kwanza, akakuta ni kama kuna mtu ametoka kusafisha hapo. Ikawa kupanga tu. Dereva wa Kumu akaleta vyombo. “Naamini sijakosea nyumba. Nimeelekezwa mpaka hapo getini. Nimeleta vyombo na vitambaa vya kujifutia.” “Karibu na asante sana. Wakasaidiana kuingiza ndani, ndipo dereva akaondoka. Jema akaanza kupanga taratibu. James naye akafika. “Naomba kazi.” Jema akacheka. “Njoo kwanza unikiss mpaka nitulie. Bado siamini.” Akasikia sauti ya Jema upande wa jikoni. Akamfuata. Wakaanza kupeana midomo bila kutosheka.

“Umenifuta machozi James. Asante.” James akacheka akiwa bado amemkumbatia. “Pete nzuri, na ya hadhi. Umenifanyia surprise nzuri, mpaka naona raha na fahari pale ofisini. Halafu wewe mzuri.” James alicheka  mpaka akamuachia na kuinama. “Kweli tena. Mwenzio najivunia uzuri wako. Nimefurahi. Halafu napenda unavyoniletea vitu pale kazini, sasahivi na mimi najulikana nina mpenzi anayenijali. Asante James.” “Karibu Jema. Furaha yangu ni kukuona unafuraha. Ila nina zawadi ingine.” “Bwana acha mimi nikupe yangu kwanza. Utanizidi sana.” “Sio mashindano, mama!” “Sawa, lakini acha na mimi nikupe. Nimetoka kukununulia ndio nikaja hapa.” Akaenda kwenye pochi yake akamtolea cheni nzuri sana ya dhahabu ya kiume na kidani kimeandikwa J&J.

“Kabla hujanivalisha acha nione kwanza. Nzuri sana!” “Kweli umeipenda?” “Kwa sababu imetoka kwako na ina jina lako pia. Kithibitisho kuwa ndio umenikabidhi Jema wangu?” “Mpaka kifo changu. Mimi nitakuwa na wewe tu.” Yakaanza mabusu mengine bila papara. Ndipo Jema akamvalisha. “Na hivi wewe mweupe, ndio imekupendeza zaidi.” “Nakwambia ninavyosifiwa! James anapendwa rangi yake!” “Sana! Natakaga unishike tu, nikusikie mwilini mwangu.” James akamshika tena na kumbusu tena na tena. Ndipo akamuachia.

“Naona mama James amekua tofauti na nilivyotegemea!” “Amekuaje tena!?” Kidogo akaingiwa na wasiwasi. “Acha nisiongee sana, tuje tumuone. Nisije nikazungumza kwa haraka, yakawa kama jana.” Jema akapoa. “Hawatakuja hapa.” Jema akawa kama hajaelewa. “Nanaa hatakuwepo hapa. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi.” “Kwa nini sasa?” “Hapa ni kwako Jema. Sitaki mtu akunyime raha.” Jema hakutegemea. Ni Nanaa ambaye sifa zake zilikuwa zikiimbwa na huyo James kila siku! Akatamani aongee kitu, akaona ayaache kama yalivyo.

“Naona nimeletewa vyombo vingi! Kwani tunategemea wageni wangapi? Na watakaa wapi?” “Mama Jema ameniambia yeye watu wake watakaa hata jikoni au hata nje hawana neno. Na watakula hata kwa kuonja, nisiwe na wasiwasi.” Jema akafurahi sana. Japokuwa hapakuwa kama nyumbani kwa Kumu, lakini bado nyumba ilikuwa mpya kabisa na ni ya kisasa. Kutoka kutapeliwa nyumba mpaka kukabidhiwa funguo za nyumba! Huna utakalomwambia Jema akaelewa mbali na anachoambiwa na James.

Kumbuka Shuka, Kumekucha.

Maandalizi yakaendelea, Danny naye akaleta vinywaji vingi sana mpaka pombe, kisha akaondoka na ahadi ya kurudi usiku. Ndio akili ikamrudia Jema kuwa anaolewa na James ambaye hajawahi kumsikia kama ameokoka japo anampeleka kwenye makanisa ya walokole. “Njoo kwanza James. Hivi harusi yetu itakuwa na pombe?” “Wewe kwa nini hujaniuliza kama mimi nakunywa au sinywi?” Hapo Jema akapoa kidogo. Akamtizama kwa wasiwasi ila akaona aulize tu. “Kwani wewe unakunywa?” “Mbona sasa umekosa raha?” “Mimi siwezi kuolewa na mlevi James. Siwezi na nilijiambia sitafanya hivyo.” James akaweka mikono mfukoni. “Mimi huwa nakunywa ila si mlevi.” Akamjibu akimtizama machoni. “Mmmh!” Jema akaishia kuguna.

“Inamaana gani?” “Hapo tena nimekwama James.” “Kwa nini?” “Sasa tutakuwa na maisha gani hayo? Mimi sitaki pombe.” Jema akaongea akilalamika. “Tokea tumeanzana mimi na wewe umeshaniona nikiwa nimelewa?” Jema kimya, macho chini. “Mimi sina tatizo na pombe. Unywaji wa chupa mbili kwangu si tatizo.” Jema akabaki ameinama ametulia kama anayefikiria.

“Unakumbuka maneno uliyotoka kuniambia sasahivi wakati unanipa hii cheni?” “Nakumbuka.” “Kwa hiyo tafrija ya usiku ipo au nianze kupigia watu simu kuwaambia wasije, bibi harusi amegairi kwa sababu amegundua mimi sina tatizo na pombe ndio hanitaki tena?” “Mimi sijasema hivyo. Ila nafikiria tu.” “Unafikiria nini?” “Sasa kwa nini unywe!?” “Mimi sina ugomvi na pombe na wala hazijawahi kunifanya kitu kibaya kilichonifanya nijutie kunywa. Sasa tatizo lipo wapi?” Jema akakwama.

“Kwani wewe unashida gani na pombe?” Jema akaitizama ile pete na kuishika kama aivue. James kimya akimtizama. “Mimi siwezi pombe. Na sitaki pombe.” “Hilo nimelisikia. Kwa hiyo?” “Naomba muda James. Ni uamuzi ambao natakiwa kufikiria na kukubaliana nao kwamba nitaishi nao mpaka kufa.” “Kwa hiyo ukishakubaliana nao. Na mimi nikagundua kuna kitu kwako ambacho sikikutegemea kwa atakaye kuwa mke wangu, naomba muda wa kukufikiria?” Kimya.

“Eti Jema? Pengine hapo tunakuwa tumeshaoana. Tuna mtoto mmoja tayari,  au umjamzito. Halafu nagundua kuna jambo ambalo WEWE unalo, na sikuwahi kutaka kutoka kwa atakayekuwa mke wangu, nakuacha kwa muda ili nifikirie kwanza ndipo nijue kama nakurudia wewe au naoa tena mwanamke mwingine?” Hapo Jema akaanza kupoa. “Sio wewe niliyekuomba unichunguze udhaifu wangu wowote utakao kutana nao, unibebe hivyohivyo ukijua mimi ni wako?” Kimya.

“Ukafanya nikakuamini! Nimekupa moyo wangu, unakuja kuniadhibu leo hadharani!?” “Sijasema nakuacha James! Nikufikiria tu.” “Kwa hiyo hawa wageni leo natakiwa kuwapigia simu na kuwaambia mchumba ameomba muda wakunifikiria, akimaliza tutawajulisha?” “Naomba usiwe unalewa James. Mimi pombe sipendi.” “Sawa.” James akakubali haraka bila shida mpaka akamshangaza Jema. “Sawa nini sasa!?” “Nisilewe. Au?” “Na ujitahidi kuacha. Mimi nakuombea uache.” “Sawa.” James akakubali tena.

“Sasa kwa nini unakubali kila kitu!?” “Ulitaka sasa nifanyaje na mimi leo ndio nimekamatwa na ‘udhaifu’? Si ndio nakubali kila kitu.” “Si kwa vibaya.” James akabaki akimtizama, Jema akaanza kujisikia kusutwa. “Zile sifa zote zimefutwa kabisa?” “Mimi nakupenda James.” “Ila unataka kwenda kunifikiria kwanza?” Kimya. “Ila ujue mimi sitakufanyia hivyo Jema. Nikikutana na kitu ambacho sikukitarajia kwako, sitakukimbia. Nitazungumza na wewe kama ni kitu cha kurekebisha, urekebishe na kama ni cha kukuombea, nitakuombea lakini si kukukimbia. Sitafanya hivyo.” “Nakupenda James. Mimi nisingekukimbia.” Jema akabadili gia. Lakini akawa ameshachelewa. James alimuona vile alivyotaka hata kuvua pete. “Ndicho ulichotaka kufanya Jema! Umenifanya nijisikie sipo salama kwako.” Yale maneno yakamuuma sana Jema akajikuta anaanza kulia.

“Na kwa taarifa yako tu, mimi nilishaacha pombe, ndio maana hujawahi kupata harufu ya pombe mdomoni kwangu hata mara moja. Niliacha nafikiri ni miaka miwili imepita sasa. Ila Danny amekaribisha wafanyakazi wenzetu ambao wao wanakunywa. Aliponiomba kama alete pombe hapa, nikamwambia sioni kama ni tatizo. Kwa hiyo usinikimbie sababu ya hilo.” “Mimi nisingekukimbia James, ila niliona ni tatizo.” James akanyamaza.

“Nisamehe James. Nitajifunza mpenzi wangu. Na kuanzia sasahivi nakuhakikishia nitakuwa na wewe hata iweje.” Kimya. “Usinichukie James.” “Sijakuchukia ila nimeingiwa hofu.” “Tafadhali usiogope tena James. Mimi ni wako. Niambie udhaifu mwingine wowote, uone. Sitakimbia tena.” “Basi Jema. Leo nataka ufurahi. Naomba acha kulia.” Jema akaelekea chooni na kujifungia mlango. James akamsikia akiendelea kulia. James akasogelea mlango akakuta umefungwa kabisa na funguo ndani.

“Mama mwenye nyumba wangu! Wageni watakuja wanakutana na mama mwenye nyumba macho mekundu, hakuna chakula.” Jema akaosha uso na kutoka. “Mimi nimejisikia vibaya.” Akajilalamisha. “Ujisikie vibaya hivyohivyo.” “Sasa mbona hata hayaishi!?” “Ubakiwe nalo rohoni kabisa, ili siku nyingine ukumbuke Jema. Tunasafari ndefu sana mimi na wewe. Hujui ninakuaje ninapokasirika au kuchoka! Hujui nalalaje! Naweza nikawa mbaya kwako kwa namna nyingine na pombe sinywi!” “Nitakuombea mpenzi wangu. Ila mimi nikilala sikoromi. Na si kisirani hata nikichoka.” “Basi mimi nikilala nakoroma sana.” “Basi acha nikakufikirie kwanza.” Jema akamchokoza. “Ujue Jema usianze utani wakati hata hapajapoa! Umetoka sasahivi kuonyesha unanikimbia halafu unanifanyia utani!”

“Mimi naanza kujiona sipo salama na wewe James.” Akarudia maneno ya James mwenyewe na kuendelea. “Jambo haliishi jamani! Sasa najiuliza nikiwa nakosea huko kwenye ndoa, na pengine nimeshakuzalia mtoto mmoja, au ni mjamzito, nani atanisitiri” James akashangaa sana. “Jema! Yaani hapahapa unanigeuzia kibao?” Jema akaanza kucheka. “Mimi na wewe mpaka kifo James bwana! Tutabebana wala usihofu.” “Muone!” Jema akacheka na kukimbilia jikoni.

Tumaini Jipya.

Ilipofika jioni, kwenye saa kumi na mbili, mama James na binti zake wakawa wa kwanza kufika hapo. Mpaka Jema akashangaa James alimaanisha nini juu ya mama yake. Mama James akawa mwema kwa Jema kuliko mama G alivyofanya walipokwenda kwake. Akamfurahia Jema kwelikweli na kuwapongeza sana yeye na James mpaka James mwenyewe akashangaa. Wadogo zake walikuja wasafi na watulivu. Wakaonekana kumpenda Jema na kutaka ukaribu naye. Heshima ya hali ya juu kwake. “Sisi tumewahi ili kukusaidia wifi yetu. Tuelekeze kitu chochote chakufanya, tutafanya tu. Mama hataki uchoke.” Jema akacheka. “Nashukuru mama yangu. Basi wewe kaa hapo uzungumze na James, wakati sisi tukirekebisha mambo. Nakuletea kinywaji sasahivi.” “Iwe maji tu. Tena mpe huyo Vai alete.” “Sawa mama yangu.” Jema na wifi zake wakaongozana jikoni. James akawa anasikia vicheko tu huko kwa Jema na wadogo zake, mpaka akashangazwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Giza lilikuwa limeshaingia nje wakati Joshua na Naya nao walipoingia. Wakamuona Joshua akimnong’oneza kitu. Halafu akatulia. “Hujambo Naya?” Akamwangalia Joshua. Jema naye akatoka kusalimia baada ya kumsikia James akisalimiana na Joshua kisha Naya ambaye akaonekana hajui ajibu nini. “Usimpe shikamoo. Msalimie tu kawaida ila mama yeye msalimie.” Akamuona ameshakosa raha kama aliyekwisha changanyikiwa na mengi wakati ni salamu tu. “Unataka kunisaidia huku jikoni au mezani?” Jema akamuwahi. Akamwangalia Joshua. “Wewe unataka nini? Maana huyu ni Jema.” “Kama kumbukumbu inanijia Joshua! Ila haijakaa vizuri.” “Nisikilize Naya. Hilo ni jambo zuri. Na uache woga. Fanya kile watakachokuelekeza.” “Nikikosea?”  Akawa kama aliyeingiwa na wasiwasi tena.

“Tutakuwa wote. Usihofu. Twende.” Jema alishaambiwa habari zake na Kumu mwenyewe ila akaomba asije akatangaza kazini. Jema naye akawa muaminifu kwenye hilo. Akimsaidia kazi Kumu ili awe na mkewe bila hata kuropoka kwa Fina. Kwa hiyo kazini kwao hakuna aliyejua kinachoendelea kwa mke wa Kumu ila Jema tu. “Utakuwa na mimi Naya. Na nitakuelekeza vizuri tu, wala usitie shaka.” Jema akazungumza naye kwa utulivu, ili atulie. Akamgeukia mumewe. “Usije kuniacha Joshua!” Akamsisitiza mumewe. “Sithubutu. Nitahakikisha jicho na masikio yangu vipo kwako muda wote na nitakuwa nakuja kukuangalia kila wakati. Naomba ukamsaidie Jema.” Akakubali.

“Ila hakuna kitu chakufanya Joshua. Mwache akae na wewe tu hapa. Kina Viola wapo na Jema kumsaidia.” James akamuhurumia vile alivyoondoka akiwa amejawa wasiwasi. “Nataka achangamke kidogo. Si umeona kumtoa leo amesema ameanza kumkumbuka Jema? Acha afanye kitu cha tofauti. Atakuwa sawa.” “Ila amependeza! Amebadilika sana.” “Nashukuru Mungu asiee. Mungu amenirejeshea mke wangu.” Mama James alivyoona Joshua anakaa na James hapo sebuleni, akaona ni bora kuwaacha. Akahamia jikoni walipokuwa wanae na Jema pamoja na Naya.

Baada ya muda Jema akamuachia kazi Naya. Ila akaenda kumwambia Joshua amemuacha peke yake, yeye anakwenda kujitayarisha. “Atakua sawa. Mwache tu. Si mlango wa nyuma umefungwa?” James akasimama kwenda kuhakikisha mlago wa jikoni, wakutoka nje kama kweli umefungwa na funguo kabisa, yeye Jema akaenda kuoga chumbani kwa James.

Wakwe.

Baada ya muda tena  wakaja ndugu wa Jema. Jema aliposkia kelele zao akamuita mama yake akiwa mlangoni chumbani kwa James. Mama yake akamfuata akasimama nje ya mlango. “Mmekuja na Jelini?” “Alivyoniambia yeye, atakuja. Sasa sijui. Maana ilibidi kumtumia ujumbe na kumwambia. Ndio akarudisha majibu hayo.” “Sasa asije akaja hapa usiku mwingi na amelewa.” Mama yake akabaki akimwangalia kama vile anamwambia unauliza makofi polisi! Jema akaona ajiachie tu. Akarudi chumbani, kaka yake akarudi kwa ndugu zake na kina mama James.

Wakashangaa Naya amechangamka ndiye anayekaribisha wageni wakati Jema akijiandaa chumbani. Joshua akafurahi kumuona vile. Akabaki akimsindikiza kwa macho kila anapokwenda na anachofanya. James alimuona vile anavyomtizama mkewe kila wakati. “Kwa nini unawasiwasi naye?” “Aisee sitaki kutendeke kosa tena. Anatakiwa kuchukuliwa taratibu sana na simuamini naye na mtu yeyote yule. Naona watu wakimuona amesimama vile, wanaona yupo sawa. Rahisi kumsahau. Na akiingiwa na hofu tu, ndipo utagundua hayupo sawa. Kwa hiyo sitaki kufanya kosa. Jicho langu lipo kwake masaa 24. Hata wafanyakazi pale nyumbani sitaki wakutane naye ili asiogope.” “Joshua!” “Hakika katika hilo sizembei. Na ukimuona akiwa ameingiwa na hofu, ndipo utaelewa ni nini nazungumzia James. Bado. Yaani leo nimemtoa makusudi nikijua mimi mwenyewe nitakuwepo.” “Na yeye anakuangalia kila wakati kuhakikisha bado upo!” “Nikiondoka tu hapa bila yeye kujua nilipo, utamuhurumia na kujua bado anahitaji msaada.”

“Jana usiku nilitoka kwenda kwenye gari, kuna karatasi niliziacha huko. Nikakutana nazo, nikakaa kwenye gari nikaanza kuzisoma na kujisahau. Na mbaya zaidi nilisahau kumuaga. Nikafunga milango na simu nikaacha ofisini. Nilirudi akiwa na hali mbaya sana mpaka nikamuhurumia. Aliingiwa na hofu ya ajabu sana.”

Kina Magesa.

Wakashangaa Geb na mama G wanaingia. James hakuamini. “Haiwezekani!” “Mimi nihangaike kufunga na kuomba. Upate mke ndio unifukuze! Hakika hii harusi hainipiti. Wewe utajuana na mdogo wako.” Mama G akapiga vigelegele, ndipo wangine wakapokea. Gafla pakachangamka kwelikweli. Mama G akajaa hapo kama hawakufukuzwa asubuhi yake. Geb akakaa kwenye kochi bila ya kukaribishwa. James akamtizama na kutingisha kichwa. “Hongera James.” “Hivi wewe ninapokwambiaga jambo huwa unanisikia lakini?” Geb akabaki akimtizama. “Geb?” “Nakusikia James, ila naamua kutofanya kama unavyotaka.” Mpaka Joshua akacheka.

“Basi bwana.” “Umenyanyua mikono?” Joshua akamuuliza akicheka. “Yaani asubuhi ya leo, nimempiga marufuku kukanyaga hapa, yeye na mkewe. Nikisema asubuhi, namaanisha ya leo. Akaonekana ameelewa! Nashangaa yupo hapa!” “Mambo ya familia ni magumu James. Itabidi Jema ajifunze tu na kutuvumilia. Wewe sitakupoteza.” Geb akajibu na kutulia.

Shuguli Watu.

Mara ikaingia kelele ya Danny na wafanyakazi wengine. “Hawa wamenichelewesha. Wameagiza nyama na vinywaji, mimi ndio nikabaki na kazi ya kuvifuata.” “Leo tunakesha. James anaoa!” “Kesho kazini jamani.” James akawatahadharisha akiwapokea. “Wewe tuwekee sisi viti nje, tuanze kunywa.” Wakasaidiana na Danny na wadogo zake, wakawatolea viti nje. Wakaa wao tu. Ikawa ni kundi la wafanyakazi wenzake James, Wakaanza kunywa na kelele nyingi. Wakibishana mambo hata yasiyo maana. Kukawa na shamrashamra ikasaidia kutokuwa karibu kwa Danny na kina Magesa. Danny akabaki na wafanyakazi wenzao muda wote huko nje, Geb kimya kwenye kochi akiangalia tu. Mama G akawa na wakina mama upande mwingine.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

 Jema akatoka chumbani akiwa amependeza haswa. Zikazidi shangwe. Akamuona mama G na kuingiwa hofu. Wakasalimiana vizuri tu, lakini ukweli Jema alijitahidi kumkwepa hata yeye alijua. Kila alipojaribu kumsogelea akaongeza shuguli akimpa tabasamu huku akimuonyesha ana hili na lile lakufanya akihudumia wageni.

Baada ya kuona kama wote walio waalika wamefika, James akaomba patulie na watu wote wakusanyike sebuleni amtambulishe mchumba wake. Watu wakapiga vigelegele wakisogea. “Nilishamchumbia asubuhi, kazini kwao. Naona baadhi ya picha nimeshatumiwa wakati nikimchumbia asubuhi. Zitaanza kurushwa hapa sebuleni kwenye luninga. Atakayependa kuona, karibu hapa sebuleni. Ila sasahivi nataka tu mumtambue. Na mimi naoa jamani. Aliyekuwa akisubiriwa ni Jema. Ameshakubali, naoa.” Vigelegele vikawa vingi. Mama G amechangamka kwelikweli, mwanae anamtizama tu, kimya. Utambulisho ukaendelea hapo.  

James akamtambulisha mama yake kwa furaha zote na dada zake. Kisha  akamkaribisha Jema atambulishe ndugu zake na yeye akampa nafasi mama yake mkubwa atambulishe wote waliokuja naye. Akafurahia hiyo heshima. “Mama amefurahi sana. Ni hivi imekua gafla tu, ila anasema leo na yeye angekuwepo.” Mama yake mkubwa akaongea hapo, akimuwakilisha bibi yake Jema pia. Ila ni kweli mama James alikuwa amefurahi haswa. Kila mtu alimuona jinsi alivyokuwa mwema. Akamletea Jema vitenge kama zawadi.

Jelini.

Jema akawakaribisha chakula kwa kukiombea. Wakati kila mtu anasahani yake wakila, Jelini akaingia. Jema akamtizama tu. “Sasa unakasirika nini wakati hata sijachelewa!” “Umechelewa sana.” “Usafiri wa shida dada yangu. Nikisema mnichangie na mimi ninunue gari, mnaanza…” “Usianze Jelini. Salimia bwana! Wewe ukoje?” “Mamkubwa naye! Basi shikamoo.” “Wewe kwa nini mambo yako ya usiku usiku?” “Basi ninunulie gari mama yangu mkubwa.” “Haya nenda.” Akaanza kucheka. “Mimi nahama ukoo. Naenda kutafuta koo tajiri. Ukoo mzima mnashindwa kumnunulia mtu mmoja gari!” Jema akabaki akimtizama.

“Nimepita kwa haraka, lakini kule nje nimeona kama kuna bia za kumwaga! Acha nikachukue ndio nije kushushia na chakula.” Mama yake hakumuongelesha kabisa, akabaki akimtizama tu. Akaenda hatua chache mbele kisha akarudi. “Ila bwana Jema umependeza halafu umeuchinja dada yangu. Pazuri hapa! Bonge la jumba! Hongera.” “Asante.” “Na mimi natafuta mwanaume mwenye hela kama shem, anioe.” Ndugu zake wote wakaanza kucheka kwa sauti. “Tatizo lenu nyinyi dharau. Na kwa taarifa yenu naweza sana kuwa mke wa mtu na nikatulia.” James akasikia sauti yake maana alipitia mlango wa jikoni. Akaamua kwenda kumsalimia.

“Hujambo Jelini?” “Sijambo shemeji wangu wa nguvu. Hongera, nyumba yako nzuri kama wewe mwenyewe.” Jema akashituka sana. “Mama!” “Sasa mimi hapa nimefanyaje!? Si nimemsifia tu!” “Wewe nenda kafuate bia nje.” Mama yake mkubwa akamfukuza. “Eti shem naweza kwenda?” “Kuwa tu huru. Ila nilitaka kukutambulisha.” “Umeona mambo hayo? Twende mwaya shemeji yangu. Huwezi jua, harusi ijayo inaweza kuwa yangu!” Ndugu zake wote wakaguna, wengine wasiomjua wakacheka. “Watu hawana imani jamani! Jema dada yangu ataniombea.” “Utapata wa kanisani.” Mama yake mkubwa alimfanya Jelini acheke mpaka akakaa chini sakafuni. Wote wakaanza kucheka.

“Basi Jema dada yangu. Yale maombi sitaki tena. Acha nitatafuta mwenyewe.” Mpaka Jema na James wakacheka. “Jelini!” “Wee mamkubwa, sasa hivi nipate mlokole mimi si msala huo! Nafanyaje naye mimi.” “Wewe si unataka ndoa?” Mama yake akamuuliza. “Siyo kihivyo mama na wewe! Kwamba iwe adhabu! Usiombe mwaya Jema. Tuache nitatafuta wakufanana na mimi.” Wakazidi kucheka.

“Si ndio hivyo ilivyoandikwa kwenye vitabu vya Mungu?” “Ni bibilia Jelini.” “Hukohuko. Nitapata wakufanana na mimi. Twende mwaya shem ukanitambulishe kwa sampuli za wanaume kama wewe.” “Wakoje?” “Shem kasoma na anahela.” “Sasa uwe na kiasi kuanzia maneno na vitendo.” “Basi twende wote Jema. Maana wewe huniamini.” “Tunakujua wewe.” “Utakuwa sawa tu, twende.” “Afadhali wewe una imani na mimi, shem.” Akanyanyuka kutoka hapo sakafuni alipokuwa amekaa.

“Umependeza mwanangu Jelini!” “Lakini kawaida yangu mimi. Ushanikuta nipo hovyo?” “Hata siku moja.” “Biashara matangazo, mamkubwa.” “Sasa na wewe unaendeleao kumuongelesha huyo ujue  unamfanya asimame hapo aendelee kuongea, na kunyamaza huyu hawezi. Mnayemchosha ni James.” “Bora mama.” Jema akadakia. James na Jelini wakaondoka hapo. “Ana moyo wa ajabu huyu!” Mama yake mkubwa akaongeza. “Anaweza kukufanya ukasirike, halafu yeye hasira yake sekunde. Kashamaliza na kashakusamehe na kukutaka ushoga hapohapo.” Jema akaongeza.

Wakamsikia akisalimia huko sebuleni kwa heshima. “Kama mtu vile!” Wote wakacheka wakimsikiliza. “Ndiyo, mimi mdogo wake. Sema mimi sijulikani sana sababu kwetu mimi ndio mpole sana.” Ndugu zake walicheka mpaka James. Ilibidi Jema aende huko sebuleni. Akamkuta ametulia kama siye yeye. “Nashukuru kuwafahamu, ila kuna sehemu shemeji ananipeleka. Acha mimi niwaache.” James akawa hajaelewa wanakwenda wapi.

Akamvuta pembeni. “Twende ukanitambulishe kule nje kwenye bia za bure. Ili niwe huru kuchukua wasije sema mimi mwizi.” James akatoka naye akicheka. Jema akamuita. Akarudi akichungulia mlangoni. “Na urudi hapa Jelini.” “Raha ya pombe ni unywe na wanywaji.” “Usinitanie Jeline! Angalia maneno yako huko na vitendo.” “Jema naye! Mbona hapo sebuleni nimekutana na wasomi sana, na wanaonekana wanamahela lakini nimekua mstaarabu?” “Basi na huko nje ikawe hivyohivyo na urudi hapa.” “Havina hata raha!” Akaondoka akilalamika. “Na Jema angalau anamuwezea. Atarudi tu.” “Akirudi James hapa bila yeye, namfuata.” Wakacheka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

  Walipowakaribia tu, Kasa akaanza. “Mtoto mzuri huyo! James umemtoa wapi?” “Mdogo wake Jema.” “Acha masihara! Kabisa?” “Sasa wewe huamini nini?” Jelini akaanza. “Mimi hapa, mdogo wake Jema. Basi, tushamaliza utambulisho.” “Sasa hutaki kufahamiana?” Kasa akaendelea. “Akuu! Mimi sitaki kufahamiana na wewe. Labda yule pale.” Akamnyooshea kidole, Colins, mmoja wao. Wote wakamgeukia. Colins alikuwa ameinamia simu yake akamtizama Jelini. “Huyo hapo akitaka tufahamiane, ndio nakubali. Ila wewe sitaki.” Mpaka James akapoa. Kasa! Anavyopenda sifa! Leo umkatae mbele za watu!

Ila akajikaza na kuuliza. “Kwani mimi nina nini?” “Yule pale anaonekana akikufahamu anakuwa anakupenda. Halafu anakuheshimu na kukupenda. Anakutunzia heshima halafu mzuri. Wewe msumbufu halafu sikutaki tu kukufahamu.” “Mimi sina kitu. Kasa ndio anaweza kukutunza mtoto mzuri kama wewe.” “Akuu mimi sitaki kutunzwa. Na uache kujiliza shida. Mimi mpaka nitajuta bwana! Utakua sio mchumba wangu tena.” Vikaanza vicheko vile Jelini alivyokuwa akiongea. Lakini kila mtu alijua Kasa amekasirika sana.

“Basi shem nisaidie kubeba tuondoke. Jema atanifuata mwenzio, halafu aanze kunigombesha. Si unamjua mkeo?” James akacheka akitingisha kichwa. “Hawa rafiki zangu wote hawa. Tunafanya nao kazi.” “Sio wewe niliyekwambia nitafutie mchumba ukasema wote wameoa!? Mbona sasa yule pale hajaoa?” “James anatubania!” “James hataki na sisi tuoe!” Kila mtu akamlalamikia kivyake.

“Twende shem. Jema atakuja sasahivi halafu atataka niondoke nikalale nyumbani wakati mimi ndio kumekucha.” “Jelini mtoto mzuri njoo unywe hapa na sisi.” “Akuu! Jema mimi kanikataza. Labda huyu hapa ndio…” “Anaitwa Colins.” Danny akamsaidia kwa haraka. Acha Jelini aanze kucheka. Akacheka mpaka na wao wakaanza kucheka. “Bwana mchumba wangu mimi anajina zuri! Colins! Sasa hilo nitalitengeneza vizuri zaidi.” Wote wakazidi kucheka na Colins naye akawa anacheka tu. “Hutamuita Colins?” Mmoja wao akaendelea kumchokoza. “Akuu! Kwanza hata wewe unalitamka vibaya!” “Wewe ungeitaje?” Acha aanze kucheka tena. Na wenyewe wakawa wanacheka kama yeye.

“Jelini?” Akashituka sana baada ya kusikia sauti ya Jema akimuita. Wakamuona cheko yote imeisha. “Si nilikwambia shem mimi? Ona Jema huyo! Basi zungumza naye asinirudishe nyumbani!” “Basi ndio ukaitike. Mimi nitakujia na vinywaji.” “Moyo wangu ushakosa raha! Nishaanza kuona dalili za kufukuzwa hapa wakati mimi sijafanya kosa! Naonewa tu.” Wakamsikia akilalamika huku akiondoka.

Huku nyuma wanaume wote wanatoa macho. “Acheni bwana! Huyu mtoto mdogo sana jamani.” “James naye! Mgumu hata kwa shemeji yake!” “Kwani si tunaangalia tu!” Wanamjibu hivyo James lakini bado macho kwa Jelini. “Muulize shem kama mimi nimeongea jambo baya pale zaidi ya salamu! Utanionea bure masikini wa Mungu mimi!” Wakamsikia akijitetea hata kabla hajaulizwa. “Haya, nenda kakae pembeni ya mama yako mzazi. Nisikuone ukinyanyuka mpaka mnaondoka.” “Sasa Jema hapo unakasirika nini jamani!? Na ujue nimekuletea zawadi ya hongera.” “Muongo.” “Tatizo lako wewe huniamini. Sasa unafikiri…” Wakapotelea ndani.

“Daah! Pombe yote imeisha!” “Bwana mtoto mtamu huyu! Sema kampenda Colins. Mimi ningempa hata gari!” “Mimi roho yangu kabisa aishike mkononi.” Kila mtu akaanza kutaja lake lakini Jelini kamchagua Colins. Wakaanza kumtania Colins anabahati ya mtende. Kapendwa na Jelini halafu wala hakuwa akiongea. Jelini kafanya kumteua yeye. “Sikuwaambia mimi kama Colins ana kimzizi?” Wakazidi kumtania. Zile sifa zikazidi kumuumiza Kasa. James akachukua chupa baadhi za bia, akaona awaache wenyewe, akijua hawatamudu hiyo hasira ya Kasa hapo baadaye pombe zikiwaisha. Colins alikuwa kama Kasa na baadhi ya wengine. Wao hawakuwa wakinywa pombe, stori tu, ila Kasa akijigamba kwa hili na lile wengine wakinywa na kumsikiliza Kasa mpaka Jelini alipokuja na kumkata kauli.

Alimshushua mbele za wanaume wenzake alipokuwa akijingamba kwao kujionyesha yeye bora! Kasa! Eti hamtaki Kasa ambaye anajiona bora kuliko mwanaume yeyote yule kwenye ile kampuni nzima! Ikamuuma vibaya sana. Jelini akawa ameiba furaha yake yote usiku huo. Ila ukweli Kasa alitokea kwenye familia ya kitajiri sana hapo nchini. Baba yake ni wale walioweza kushika pesa, na pesa ikatulia mfukoni mwao miaka na miaka hata kabla kina Colins hawajaja duniani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Nini Kitaendelea? Usikose muendelezo.

Kikaoni! Kasa! Jelini! Colins! Na maandalizi ya harusi.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment