Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 1 - Sehemu ya 41 - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 1 - Sehemu ya 41

Jema naye ikawa hivyohivyo. Jema wa viwango jioni hiyo hakuna nguo aliyoipenda.Kwanza hakuwahi kutolewa kwa namna hiyo. Alikuwa na mchumba, lakini hakuwa akiyajui hayo ya kina Geb yakutoka Dinner ya visu na Umma. Hakujua kumtoa sehemu kwa chakula hata cha vibandani. Labda Jema atoe wazo wakiwa wanatoka kanisani, tena atataka kitimoto au nyama choma. Na Jema akawa ndio mlipaji, yeye hakuwa na ajira ya kueleweka alilalamikia kipato wakati wote. Halafu alikuwa mkali sana kwa Jema. Muda wote kumkosoa kwa hili na lile, akimpanga kwa ukali akitumia umungu ndani yake, maana wote walikuwa wameokoka. Jema akaonekana ni dada wa kileo kwa nje, lakini hajui maisha mengine zaidi ya walivyoishi na huyo mwanaume.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

James aliambiwa kuchelewa iwe mwiko. Ilipofika saa 12 kamili jioni hiyo akawa ameshaegesha nje ya nyumba aliyokuwa akiishi Jema. “Sikutegemea kama utafika kwa urahisi hivi!” “Kwako hapapotezi. Rahisi kama ulivyonielekeza kwa ujumbe. Umependeza sana Jema.” “Nilikuwa najishuku! Sijui nitokaje.” “Umependeza sana.” “Wewe umebadilika sana James. Tokea tukutane kwenye harusi ya Joshua na nilipokuona majuzi! Hakika ningekukuta sehemu nyingine nisingekutambua.” “Nimebadika vibaya au vizuri?” “Vizuri sana. Na leo zaidi. Umependeza na unanukia vizuri sana.” Ushauri wa Geb ukaanza kulipa. “Asante. Twende basi. Au bado?” “Nipo tayari.” Wakatoka.

James akawa muungwana kama alivyofundishwa na Geb. Akamfungulia mlango na kumfungia. Jema akawa wakucheka moyoni haamini. Hakutaka hata kuuliza wanapokwenda ila kufurahia tu. “Gari yako safi!” “Siitumii mara kwa mara, natumia ya ofisi ndio maana unaiona hivyo.” “Ila na wewe unaonekana mtunzaji.” James akacheka na kushukuru kwa sifa. Kimya mpaka sehemu aliyochagua James.

“Hukuniambia una hamu ya kula nini. Na mimi nilitaka leo ule maana umeniambia haukuwa ukila vizuri. Kwa hiyo nimepachagua hapa makusudi kwa kuwa wanavyakula vingi, na hata kama hamna, wanatoa nafasi ya kutaja unachotaka, wanakupikia.” Jema akacheka kwa furaha. “Nashukuru kujali James. Asante.” “Basi twende tukapate muda wa chakula.” Wakati James anataka kwenda kumfungulia mlango, Jema akawa ameshashuka.

“Nikusaidie kubeba pochi?” Jema alicheka mpaka akainama. “James!” “Mimi nimeuliza tu.” “Ni ya urembo!” “Kwa hiyo?” “Sasa si ndio viendane na nguo!” “Mimi sina shida hata yakubeba karibu na nguo yako ili bado umachi, upendeze.” “Hii pochi ni ya kike James!” “Na wewe mwenye nayo si utakuwa ukitembea pembeni yake?” Jema akazidi kucheka. “Bwana James acha bwana!” “Ni katika kutaka kusaidia tu. Ila kama unapenda kubeba kipochi chako mwenyewe, basi twende.” Wakaingia wakicheka.

James alikuwa akikumbuka kila kitu. Akamvutia kiti, akakaa. “Asante James. Ndio upo gentleman hivyo!” “Ni vile uliharakisha kushuka garini. Lakini pia ningekufungulia na mlango.” Jema alicheka sana. “Nilikuja kukumbuka wakati nishashuka, nafunga mlango. Nikajiambia ni ushamba tu.” “Basi ukiwa na mimi usijali maswala ya mlango.” “Ndio itakuwa kazi yako?” “Bila shida.” “Inamaana safari kama hizi niendelee kuzitegemea?” “Sana tu.” Jema akamwangalia kama ambaye hana uhakika.

“Ahadi hii ni wewe wa kwanza kukupa, na sina mpango wa kumpa mwingine. Nanaa yeye hajawahi pewa hii ahadi ila kwake nawajibika.” “Kivipi?” “Nanaa ni kama mtoto wangu. Nimemlea tangia anatolewa hospitalini, baada ya mama yake kufariki akiwa anajifungua yeye. Acha tuagize kinywaji kwanza.” Wakaagiza na mpaka vyakula.

“James! Ukisema kumlea unamaanisha nini?” “Kama mama. Yaani mimi ndiye nimemsafisha mpaka kitovu cha uchanga na kikakatika mikononi mwangu. Kumlisha na kumuogesha. Nimemtunza mpaka kumfikisha kwa Geb.” Akamsimulia kwa kifupi na kumfanya Jema avutiwe zaidi. “Ndio maana upo hivyo James!” “Nikoje?” James akamuuliza akicheka. “Una upendo fulani hivi! Ambao na mimi jana nikaona upande wako mwingine. Unajua kumtuliza mtu kwa namna fulani hivi. Unabembeleza.” James alicheka sana.

“Kweli James. Jana nilishindwa kuelewa aina ya ule upendo, lakini sasahivi ndio nimekuelewa kwa nini upo hivyo. Nilikuwa na hali mbaya! Chakula kilikuwa hakipiti kooni na nilikuwa nikilala kwa dawa za usingizi.” “Haiwezekani Jema! Ndio ilikuwa mbaya hivyo!” “Acha James. Nimelizwa mpaka machozi yamekauka. Natamani kulia sina machozi. Halafu sasa sina wa kumlilia. Mama niliye naye alishanionya sana, ila sikumsikiliza. Aibu, sina pakuficha uso, ila kazini. Ndio maana Kumu alipotingwa na majukumu yakifamilia, nilishukuru sana. Nikafanya hata ambayo hajanituma! Ilimradi tu kupoteza mawazo.” “Pole sana. Ilikuaje?”

Historia Ya Jema.

“Sisi tumezaliwa watoto wakike wawili tu. Mama hakuolewa, alituzaa kila mmoja na baba yake. Akatulea yeye mwenyewe. Au tuseme anatulea mpaka sasa, maana mdogo wangu yeye bado yupo kwa mama na bado anamtunza. Mwenzangu alikataa mambo ya shule mapema tu na akazaa. Mtoto wake wa kiume ndio kama mtoto wa mama. Mama anamlea na kumsomesha.” “Kwamba ndio mkubwa kiasi hicho!?” “Mama anasema anahisi alipovunja tu ungo akashika na mimba. Hata yeye mwenyewe ni mdogo tu. Wala si mkubwa. Anyway, mama yangu ni mkristo jina. Hana mambo ya kanisani, anasema ni utapeli.” Jema akaendelea, James akisikiliza kwa makini akijua katika hiyo historia, yatajibiwa mengi. Akaongeza umakini.

“Mimi niliokoka nikiwa sekondari. Kidato cha 3 mwishoni naingia cha nne. Mama akalipinga sana hilo. Akawa ananiambia nakaribisha ujinga kwa wakati ule ninaohitajika sana shuleni, nitaishia kujichanganya na kuharibu maisha yangu. Wakati huo angalau mimi ndiye aliyekuwa akinitegemea kwenye mambo ya shule, tuseme nilikuwa nikijitahidi shuleni kuliko mdogo wangu. Ubaya ulikuja nilipomaliza kidato cha nne, nikafeli. Mama aliumia sana. Akalalamikia wokovu ndio umeniponza. Maana matokeo mengine yote ya nyuma nilikuwa nikifanya vizuri tu mpaka hayo ya mwisho yaliyochanganyikana na wokovu ndipo nikafeli. Mahusiano yetu yakabadilika kabisa. Sio marafiki tena kama zamani. Akawa akichukia nikiwa naenda kanisani. Nilikaa nyumbani zaidi ya mwaka, ananiambia hawezi kunisomesha tena kama bado naendelea na mambo ya wokovu.”

“Lakini sijui ilikuaje James! Nilikutana na Yesu kwa kipekee, nilikuwa siwezi kuacha. Nilikuwa nimefika sehemu ni bora kukosa kila kitu nibakie na Mungu wangu tu. Na ukumbuke injili ya wakati ule tuliyokuwa tukihubiriwa ilikuwa tofauti na hii ya sasahivi.” James akacheka. “Ya sasahivi ikoje?” “Imechanganywa kiasi ya kwamba haimpi mtu pumziko ila inakuwa kama mwanadamu ameongezewa vita na shetani. Anahubiriwa aokoke, akishakubali kumpa Yesu maisha, kisha inakuwa kama yale Yesu aliyokuwa akiwaambia wataalamu wa sheria ambao ni kama hawa wanaojiita watumishi wa Mungu wanao aminiwa sana na kizazi hiki.” James akawa bado anataka ufafanuzi zaidi.

“Kitabu cha bibilia, Luka 11 pale. Kuanzia mstari wa 46, Yesu alikuwa akiwaambia wataalamu wa sheria kuwa, ‘Ole wenu, kwa sababu mnawatwika watu mizigo mizito ambayo hawawezi kubeba, wala ninyi wenyewe hamwinui hata kidole kimoja kuwasaidia.’ Mstari wa 52 anaendelea kusema hivi, ‘Ole wenu ninyi wataalamu wa sheria, kwa sababu mmeuondoa ufunguo wa maarifa. Ninyi wenyewe hamkuingia kwenye ufalume, na wale waliokuwa wanaingia mkawazuia.’ James akaanza kucheka akawa ameelewa.

“Kweli James. Sasahivi kila mtu anatumia vibaya bibilia kujipatia wateja. Wanaona wakisema kazi aliyofanya Yesu pale msalabani tu inatosha, inamaana hawatapata watu wakuwategemea wao. Wanatafuta kufanya watu mateka ili kuwa na wateja wengi watakao jinufaisha nao. Kujipatia wateja wakudumu wakitumia bibilia lakini maneno yao. Sisi tulikuwa tukihubiriwa wakati ule, ukiokoka unawekwa huru kwelikweli. Nikutembea kutokana na kanuni za kibibilia tu, na hapo utakuwa salama. Kama, asiyefanya kazi,” “Asile.” Akamalizia James.

“Ewaaa! Sasa siku hizi hawa wahubiri badala ya kufundisha watu kweli, na kanuni za kibiashara, kuwa kutofanikiwa mara ya kwanza na ya pili ni jambo la kawaida. Angalia makosa, rekebisha. Hawataki kuwaambia hivyo watu, wanawafunga na kuwaambia ni laana. Labda ya ukoo, au mambo waliyofanya nyuma na mambo yanayofanana na hayo. Basi mtu anakazana kwenye kuomba. Kufuta laana za ukoo, kutubu na mengine mengi wakijitakasa mpaka vitomvu! Lakini huyu mtu aliye kwama kwenye biashara, hatafundishwa kanuni za waliofanikiwa kwenye biashara, au kwenye ajira, ufugaji, ndoa na mengine yanayofanana na hayo ila kuongezewa kifungo. Watamwambia afunge na kuomba. Atoe laana za ukoo. Ajitakase. Ajiunganishe na madhabahu fulani na mazinga ombwe mengi tu, wakihangaikia mafanikio haya ya mwilini wanayoita ni BARAKA.”

“Siku hizi mtu akitafuta mafanikio kwenye chochote kile na kukwama kidogo tu, bila kujali ukiukwaji wa kanuni kwenye njia nzima alizotumia mpaka kukwama kufikia yale mafanikio, basi wanapunguza nguvu ya Msalaba kabisa. Wanawatafutia matatizo yanayosikika ni ya kiroho kabisa, kuwafanya wawe nao makanisani au kwenye simu kuwaombea. Huyu mtu anakua na kazi ya kuomba huku akipingana na kanuni alizoweka Mungu mwenyewe na wakihangaika kufanya alichokifanya Yesu msalabani. Uhuru tuliotangaziwa kupewa baada ya kumpokea Yesu, wao wanaweka pembeni na kuanza kupigana na shetani kwa maneno mengi wakiutafuta uhuru huohuo.” James akacheka sana.

“Inauma! Acha tu James. Huyu mtu ambaye ameshaokolewa, amewekwa huru, badala afundishe kuishi maisha ya ushindi ndani ya Yesu, anafundishwa jinsi shetani alivyo na nguvu. Na anaweza kuwashinda wakati wowote kama hawajapigana naye vita yakutosha. Unajiuliza hizi injili wanatoa wapi, mbona hata Yesu mwenyewe hakuhubiri hivyo! Hizo laana, mtu aliyeokolewa, na bibilia inatamka wazi kabisa, unakua kiumbe kipya, hizo laana wanazowaanzishia hawa walioitwa ni warithi pamoja na Kristo wamezitoa wapi? Unajiuliza, hivi kazi nzima ya msalaba, mateso yote aliyopitia Yesu ilikuwa ni nini? Yesu aliposema IMEKWISHA, alimaanisha nini kilikwisha, na nini kilibakia? Bibilia inaposema mtaijua kweli nayo itawaweka huru! Mbona hawa watu hawawekwi huru? Mbona hata hawaitafuti kuijua hiyo kweli yenyewe ila kutafuta kazi za shetani mchana na usiku?”

“Tunarudi kulekule mtume Paulo alipowakemea Wagalati mpaka akawaita wapumbavu. Ilikuwa ni kama hivi injili hii ya sasa. Paulo alipita akawahubiria injili nzuri tu. Wakaamini. Paulo akaondoka, wakaja wahubiri wengine waliowaambia kama hivi watu wanavyoambiwa sasahivi. Kuokoka tu haitoshi. Mnatakiwa kufanya hivi na vile. Washirika walewale walioamini injili ya uhuru, ya mtume Paulo, wakaja tena wakaamini injili hii ya kujishugulisha kama hii ya sasa. Wakafuta yote waliyohubiriwa na Paulo, wakaanza kufanya kama watu wa leo wanavyofanya. Kuombea mambo ya mwilini kabisa. Kujiunganisha na madhabahu. Kupanda mbegu. Kujipaka mafuta na mambo mengiiii kama ushirikina tu ila unafanywa kanisani!” James akacheka sana.

“Hakika siongezi James. Kasome kitabu cha Wagalatia. Alichokikemea Paulo, ndicho kinachoendelea sasahivi kanisani. Badala mshirika awekwe huru, ndio wamejawa na vita na shetani mchana na usiku. Sikiliza maombi yao. Ni vita na shetani, wakijikomboa katika kila eneo la maisha yao ambayo Yesu alishalipia garama, mpaka unawahurumia. Wanaishi kwa hofu kuliko mlevi anayekesha baa. Unaweza kumwambia mlevi atoke baa arudi kwake usiku akitembea, akarudi kwa amani kabisa akipiga miluzi kuliko mshirika aliyeokolewa. Wamejawa na hofu. Shetani yupo midomoni mwao kuliko Mungu. Wanajua nguvu za shetani kuliko uwezo na mamlaka ya Mungu kwao. Roho mtakatifu tuliyeachiwa sisi atusaidie, hawana habari naye, wapo kwenye vita na shetani wakijikomboa mchana na usiku. Hakika inaniuma.” “Mbona na mimi nayaona sana tu. Najua unachozungumzia.” James akaongeza akicheka.

“Anyway. Binafsi nilikutana na wokovu ule wa kina Paulo na Yesu. Hakika nilitulia kabisa nyumbani nikiwa na pumziko nafsini mwangu. Nikijua nimekua kiumbe kipya. Nikaamini andiko linalosema nimehamishwa kutoka kwenye ufalme wa giza, na kuhamishwa katika ufalme wa mwana wa pendo lake. Nimesamehewa dhambi. Sina laana na mikosi yangu yote imabadilishwa kwa kazi ya msalaba. James, nilikuwa na amani na utulivu wa hali ya juu. Sina hofu nikijua uhai wangu umefichwa ndani ya Yesu. Si mimi tena ninayeishi, ila Kristo ndani yangu. Namtegemea Mungu tu. Vita zangu zote nikamuacha Yeye. Namtii mama kwa kila kitu. Nafanya kazi pale ndani bila hata kutumwa, ila kanisani sikuacha kwenda. Naomba hapo ndani, asubuhi na jioni. Nikipata tu kinafasi, napiga kabisa magoti, naomba kuwa na ushirika na Mungu wangu. Basi mama akinikuta hivyo anazidi kukasirika. Tukaendelea hivyo, huku akinihakikishia hatanisomesha. Nikatulia tu. Maisha yakaendelea.”

“Nakumbuka dada yake alikuja kumwambia ni bora vile naenda kanisani kuliko ningekuwa nakimbilia kwa wanaume kama mdogo wangu. Akamsema wee, ndio ikawa kama mama amefunguliwa macho. Akaniambia hana pesa ya kunirudisha shule hizi za sekondari. Ila anaweza kuhangaika anipeleke nikafanye kozi fupi itakayonipatia ajira. Tukaanza kufikiria kitu gani chakufanya. Ndio nikasomea mambo ya Masoko kwa Mwaka mmoja tu.

“Sasa katika huko kutafuta ushirika na Mungu, kumjua zaidi, ndipo nikajiingiza kwenye kanisa nililolipenda kwa sababu ya neno. Kama nilivyokwambia, kwetu tulikuwa wakristo jina.” “Kwamba mama hakuwa akienda kanisani?” “Si krismasi wala pasaka. Labda kwenye harusi alizoalikwa na misiba ya watu.” James akacheka. “Kwenye hilo kanisa ndipo nilipokutana na Temu. Na yeye alihamia kwenye hilo kanisa. Hapo nishamaliza chuo huo mwaka mmoja, mama amenitafutia kazi pale Coca. Akanifuata na kutangaza nia. Kwamba anataka kuja kunioa.”

Anyway, nilisikia watu wakisema upande wa wakina mama wanamkosi huwa hawaolewi. Ndio maana bibi aliachika, mama na dada zake hawajaolewa. Sasa mimi nilimuombaga Mungu nikamwambia anisaidie nije kupata mwanaume mcha Mungu, tuone nije niwe na familia. Isiwe kama kina mama. Maana kwao kuna waliosoma na wenye hali nzuri tu kama kina mama yangu. Nikimaanisha wanaoweza kuyamudu maisha yao, ila wote hawajawahi kuolewa. Alipokuja Temu, nikafurahia sana na kujua Mungu amenipa haja  ya moyo wangu.”

“Nikaingia na moyo wangu wote.  Tukaanzana na Temu. Ila nafikiri niliharibu tokea mwanzo wetu.” “Kwa nini?” “Nilikuwa muwazi sana kwake, na yeye hakuwa mwanaume au niseme mwanadamu mwema. Alitumia niliyomwambia vibaya.” “Ulimwambia nini?” James akaendelea kudodosa akinywa kinywaji chake taratibu. “Nilimwambia, kuna makosa yametendwa kwenye familia yetu, sitaki kurudia kosa. Kwamba namlilia Mungu anipe mwanaume atakayenioa. Na ambaye atanisubiri mpaka ndoa. Kwa kuwa sitaki kuja kuzaa nje ya ndoa. Basi Temu akaanza kama mcha Mungu haswa na yeye akasema anataka kusubiri mpaka ndoa. Nikampeleka mpaka kwa mama. Mama alipomuona tu, akamwambia wewe ni mlokole tapeli.” “Kwamba alimwambia mwenyewe!?” James akahisi hajamuelewa.

“Hivi, usoni kwake. Nikiwa nimempeleka kumtambulisha kwake. Nilichukia James, ikawa chanzo cha ugomvi wangu tena na mama. Nikaacha hata kumtembelea. Ila akawa akinipigia simu kunijulia hali na kunihimiza kazi, ‘si kubweteka hapa mjini. Wanaume hawana pesa, matapeli tu, hawajui kuhonga, maneno mengi tu ya bure. Wanaume suruali,’. Na mambo mengi tu anayosema anayoyajua kwa wanaume wa mjini.” James akacheka.

“Wewe acha aisee. Nina mama na nusu. Lakini ukweli ni muhangaikaji, anayependa kujishugulisha si kukaa tu bure. Na akiamua kufanya jambo, hata kazi ya mtu, hutakuwa na pakumlaumu. Anafanya kwa nguvu zake zote na akili zake zote.” “Ndiko ulikorithi?” Jema akacheka. “Labda, ila naona yeye amezidi. Basi uchumba ukaendelea na Temu kila anayetufahamu anajua tumechumbiana. Akashauri tununue kiwanja. Wazo si baya. Ila sasa yeye hana kazi ya kueleweka. Pesa hana, kiwanja alichoniambia amepata kipo maeneo mazuri kweli, bei kubwa. Nikakopa benki kwa mshahara wangu. Tukanunua. Ikaanza kazi ya ujenzi.” Akamuona anacheka na kutingisha kichwa.

“Nini?” “Hivi unajua nilijimaliza haswa! Isingekuwa safari anazonipa Kumu, ningekuwa mtu wa kuishiwa hata sina mafuta ya gari. Lakini nikajikaza. Bwana Temu ni mkali. Simu zake na jumbe hataki zisubiri.” “Ndio maana ulinishangaa mimi!” “Bwana anaweza akaanza kugomba, na hapo unasubiriwa na Kumu, yeye anagomba hujajibu au kupokea simu kwa wakati.” “Na anakuwa na dharula?” “Dharula yake pesa. Kila ukigeuka pesa ya ujenzi. Nikawa nikiishi kwa wasiwasi, na katumaini kidogo kuwa najenga kwetu. Watoto wetu watapata kwao. Tukaendelea hivyohivyo huku nikimtetea kuwa ukali ule ni kuchoka na ujenzi.” “Kwamba alibadilika?” James akauliza.

“Hapana James. Ni kule kujifariji tu maana nilifika mahali ilibidi kuepukana na uhalisia. Nilijiona nimefika naye mbali, siwezi kurudi nyuma.” “Kifedha?” “Aisee sijui James! Inawezekana, ila pia nafikiri aligundua madhaifu yangu, akajua kunibana kwenye kona nikawa kama siwezi kutoka tena kwa hofu. Nikajikuta sina kimbilio, yeye ndio amebeba majibu ya maombi yangu.” “Baba wa familia?” “Ndio ilikuwa shauku yangu James. Pia nilishajiapa hata kwa mama, mimi nilazima nitaolewa tu. Sasa ile hofu ya kuja kuachika, nafikiri ilinisumbua. Basi na yeye sijui alishaona sina pakwenda!”

“Jamani alikuwa mkali kwangu na mbaya zaidi hapendi ninachokifanya, anasema kazi ya kitumwa nalipwa kidogo hata pesa haionekaniki. Gafla ikawa ni kama mimi sina mchango mkubwa kwenye hiyo nyumba, anahangaika yeye peke yake! Hakuna utulivu, mkali kweli akinisimanga kwa hili na lile hata mambo madogo kama kuchelewa kupokea simu. Kwamba namuabudu sana Kumu, siwezi kumkatalia jambo.” “Jamani! Hajui kwamba unawajibika kwake kama kiongozi wako!?” “Huna utakalomwambia, akaelewa.”

“Haya, tukaja swala alilonimaliza nalo kabisa kuwa mimi siwezi kuwa mwanamke wa kuja kuwekwa ndani!” “Kivipi!?” “Sijui James! Ila anasema haiba yangu ipo kama mama yangu, siwezi nikaweza kuwa mke wa mtu na kumtambua mume kama kichwa cha familia. Mara awe kama ananisifia huku akinisanifu kuwa mimi ni jasiri kama simba. Kwamba tukiwa ndani ya nyumba, tukiingiliwa au kukiwa na matatizo ya kifamilia, eti basi mimi ndio nitakuwa nikikimbilia hilo tatizo, bila kupitia kwa mume wangu!” James akashangaa sana.

“Mara aseme eti mimi nina mtindo wakumfanya mtu ajisikie dhaifu kwa kuwa kila tatizo nalifanya sio tatizo hata kama mwenzangu akisema ni tatizo kubwa, eti mimi napuuza na kufanya aonekane dhaifu!” “Basi acha nikwambie kitu kingine anachokusifia Kumu na kunifanya kunivuta kwako. Ni hicho anacholalamikia huyo mchumba wako.” “Kitu gani!?” “Kumu anasema ni kiasi cha kukupa tu tatizo, wewe unatafuta ufumbuzi na huna tabia ya kutolea sababu jambo wala kulalamika. Utapambana nalo mpaka unafanikisha. Anakusifia kuwa, eti wewe ni wale wanawake unaoweza kuwapa mahindi kwa chakula, lakini ukarudi na kuvuna shamba zima.” Mpaka Jema akajisikia machozi kutoka.

“Kweli!?” “Kabisa. Nisingekudanganya na ndio maana ikabidi kuanza kukuangalia kwa makini. Joshua anajivunia sana wewe. Anasema katika wafanyakazi bora, wewe upo. Na usidharau kazi yako Jema. Unafanikisha mambo makubwa sana, ni hivyo tu Joshua hawezi kukwambia mara kwa mara usije bweteka. Na ndio maana nakwambia usijibadilishe hata kidogo ila kujiongeza. Sasa mchumba anaendeleaje!?” “Acha kunisanifu bwana!” James akacheka sana.

“Tena! Mimi namuulizia mchumba Temu.” “Mchumba amempa mimba msichana mwingine.” James akatoa macho na kicheko kikakoma.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Itaendelea..


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment