Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 1 - Sehemu ya 40. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 1 - Sehemu ya 40.

Wakapata mlo wa pamoja, akamuona James anatuma ujumbe. ‘Ulifanikiwa kupata chakula?’ Ndio ujumbe aliomtumia Jema. Geb akamuona kila wakati anachungulia simu yake. Akajua hajajibiwa. Akasikia kumcheka sana moyoni, akifurahia shida yake. Wakati anakaribia kutoka Geb akakimbilia juu na kutoka naye nje wakati Nanaa akitangulia kulaza wanae. “Hii pafyumu nilinunua lakini sijaitumia kwa kuwa Nanaa alininunulia ingine inayofanana na hii, nikaona nitumie aliyonipa mke wangu. Katumie na sio siku za sikukuu tu.” James akacheka akitingisha kichwa.

“Sasa sio unipe pafyumu ya kulingana na mshahara wangu halafu ikiisha nabakia..” “Acha kujiliza James! Tumia pafyumu kila siku tena nzuri, sio zile unatumia halafu ukitoka chumbani na yenyewe unaiacha hapohapo! Unatoka hunukii kitu!” “Sawa Geb. Lakini nafanyaje kama hajanijibu?” “James wewe umepaniki na utaharibu.” “Kwa nini tena?”

“Wanawake hawapendi wanaume wasiokuwa na msimamo. Mbambaishaji na asiyejielewa na hili hata Joshua tulikuwa tukizungumza naye na wewe ulikuwepo. Wanawake wanataka uhakika wa usalama wao. James waliyekutana naye leo ofisini, ndiye huyohuyo akutane naye kesho, hutatumia nguvu nyingi kumpata.” “Wewe niambie nifanye nini kuanzia sasa.” “Wewe unataka kwenda umbali gani?” Geb akamuuliza.

“Acha nikwambie ukweli Geb. Kuna vitu vilinivutia kwake tokea mwanzo. Ila nikaambiwa na mtu wake wa karibu kuwa tokea anamfahamu alisikia anamchumba waliyekuwa wakikaribia kufunga ndoa. Ila akashangaa siku zinaenda, kimya. Nikaona nimuache tu. Sasa alipokuja leo na kuniomba nitoke naye kwa chakula, japokuwa mwenyewe alisema ilikuwa ni kutoka yakawaida tu, lakini kuna jinsi alikuwa kabla, nikahisi labda kutomjibu ndiyo au hapana tokea mwanzo nilimuogopesha ndipo akajirudi kwa haraka akajitete ni ukaribisho wa kikazi. Ila ukweli nataka kupata naye muda ili nimfahamu zaidi na kujibu swali kama bado anaye mtu au la.”

“Basi nenda umbali mrefu kidogo ila si kwa haraka usije kumuogopesha.” “Huu ndio ujumbe nimemtumia, hajanijibu.” Akamuonyesha. “Inawezekana ameona au hajaona. Na kama ameona, pengine anajiuliza maana yake. Ni mtoto wa kike, hataki kuharakisha na kuharibu. Lazima kuonyesha unamaanisha huo ujumbe. Usitume wa pili kwa haraka usije ukaonekana huna mipaka na upo desparate. Tulia mpaka kesho uone atakujibu nini.” “Asante kwa pafyumu.” “Na acha kufunga vifungo vya shati mpaka juu kama Jimmy anavyofungwa na mama yake akijitetea anaogopa baridi kwa mwanae kumbe ni wewe ndio umemuharibu mke wangu. Unataka kufunga tai?” “Geb umeniamulia!” “Muonekano una matter James. Mwanamke anapenda mwanaume ambaye hatamuonea aibu mbele za wenzake. Fungua hivyo vifungo viwili vya juu.” “Geb! Kifua kitaonekana!” “Unakificha kwani una matiti? Hata cheni yako haionekaniki!” Geb mwenyewe akamfungua. “Geb!” “Na usifunge James. Tafadhali uwe unajiwakilisha vizuri. Usiku mwema. Naenda kulaza wanangu.” Geb akamuacha. Akaondoka akitamani kutuma ujumbe wa pili akakumbuka ushauri wa Geb. Akatulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kesho yake mida ya saa nne asubuhi akapata majibu. ‘Nashukuru kwa kila kitu.’ James akasoma akajua amejibu kwa jumla sana na ni kweli anamtega. ‘Ulipenda ulichokula?’ James akaongeza hilo swali msisitizo wa kujali. ‘Niliamua kwenda kulala tu. Hata hivyo muda ulikuwa umekwenda.’ ‘Basi wakati mwingine itabidi tuwahi.’ Jema akarudia huo ujumbe mara kadhaa kama ambaye hajaelewa. James akaelewa. Akaamua kuongeza ujumbe mwingine. ‘Huwa unapendelea vyakula vya aina gani?’ ‘Si mchaguzi sana. Ni kama nikipata utulivu naweza kula kitu chochote.’ ‘Utulivu wa ndani!?’ James akaongeza swali kuonyesha anazingatia na kuelewa anachomwambia. ‘Naona umenielewa.’ James akacheka akiendelea kusoma.

‘Basi tuanze kwa kuandaa mazingira matulivu ya nje kwanza ili tukapate chakula pamoja.’ ‘Tafadhali usijisikie deni kwa kukuomba jana. Nakiri nilivuka mipaka, ila sikuwa na nia mbaya.’ ‘Hakuna nia mbaya kwenye chakula. Na kama isingekuwa miahadi ambayo nilishaiweka tokea mwanzo, ningependa kwenda kula na wewe.’ ‘Kweli?!’ ‘Nisingekutafuta tena, Jema.’ Ikamgusa sana moyo wake akatulia.

‘Najua huwa unakuwa na majukumu mengi. Sitaki kukupotezea muda. Lakini jumamosi zako zinakuaje? Tunaweza fanya jioni tu baada ya majukumu yote kuisha. Tukapata sehemu nzuri, tukaenda kula.’ Akafurahi sana kusikia hivyo. ‘Sawa. Na asante.’ James akashindwa kuelewa shukurani hiyo ni ya nini. ‘Japo sijaelewa shukurani ni ya nini, ni sawa nikipiga simu ijumaa jioni.’ ‘Ni sawa kabisa. Na asante.’ James akacheka.

Ujumbe mwingine tena ukaingia kwenye simu ya James. ‘Asante kwa muda wako sasahivi na asante kwa utayari wa kukutana jumamosi kwa chakula.’ Ikawa kama anamjibu shukurani ni ya nini. ‘Karibu na mimi sikushukuru kwa ukaribisho wa jana. Samahani na asante.’ ‘Haina shida na karibu.’ James akawa hajui azungumze nini tena, akaona awe na kiasi. ‘Kazi njema Jema.’ ‘Na wewe. Uwe na siku njema na mkono wa Mungu usiondoke juu yako.’ Hilo likamfanya James atulie atafakari kidogo ila akajibu. ‘Amina na kwako pia.’ ‘Amina.’ Ikawa mwisho wa kuchat japo wakafurahia huo mtiririko wa maongezi yao.

Jema akajifikiria vile atakavyokuwa na James. Mawazo yakamfikisha mpaka aina ya watoto atakao kuwa nao. Akawafananisha na watoto wa Nanaa. Alifika mbali akiwa ameshakuwa mke wa James mpaka akajishitukia. Akaogopa na kusimama kwa haraka. “Nawaza nini hiki! Ndio maana naishia kuumizwa.” Akatoka kabisa hapo ofisini kwake akijionya asije fika mbali ambako atajiumiza yeye mwenyewe endapo James hakuwa na nia ya kwenda umbali huo.

Ijumaa.

Aliisubiria hiyo simu ya James mpaka akahisi amesahau. Mpaka anarudi nyumbani kwake usiku, kimya. James hakuwa hata ametuma ujumbe. Ikamuuma sana. Akashindwa hata kuweka maji mdomoni kwa wasiwasi na maumivu ya moyo. Akiwa anajiandaa kulala, ujumbe ukaingia. ‘Samahani sijui nimechelewa sana? Naweza kupiga au tuzungumze kesho mida mizuri kidogo?’ ‘Haina shida.’ Hilo jibu likamfanya James ashindwe kuelewa. Aliuliza maswali mawili, amejibiwa hivyo! Asijue huo ujumbe wake jinsi ulivyoeleweka kwa maumivu na kuzidi kumnyong’onyesha Jema aliyedhani siku ya jumamosi ndiyo yakutoka, anasikia ndio siku ya kupigiwa simu! Akajihisi ni mkosi. Uchungu ukamzidia moyoni. Akajisikia kuumia sana. “Kweli sisi tuna mkosi wakutokuolewa!” Akasalimu amri kwa machozi hapo kitandani akiwa peke yake.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akapiga picha yale mazungumzo yake na Jema nakumrushia Geb. ‘Nifanye nini?’ Akamtumia na hilo swali. ‘Ni usiku sana James! Nipo na mke wangu.’ Geb akamjibu hivyo akilalamika kusumbuliwa. ‘Unazidi kupoteza muda, Geb. Maneno yote hayo, ungeshanishauri chakufanya.’ ‘Mpigie. Na USIKU MWEMA.’ James akacheka akijua ndio anaambiwa asimtafute tena.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kwa haraka sana akampigia simu Jema. “Pole na majukumu.” Jema alianza mara alipopokea. “Asante. Pole na wewe.” “Asante.” Kimya. “Upo Jema?” “Nipo.” “Bado unadhani kesho tunaweza kutoka?” “Nilijua umeahirisha James!”  James akashangaa kidogo. “Ni nini kimekupelekea kufikiri hivyo!?” “Uliposema unipigie kesho.” “Hapana. Labda nilishindwa kuiweka vizuri. Nilimaanisha kukupigia kesho mapema kabla ya miahadi yetu jioni. Mimi bado naisubiria kwa hamu.” Hapo akamgusa Jema, na kusahau yote. Akacheka. “Na mimi pia.” “Basi tujiandae kwa chakula cha kesho. Vipi lakini siku yako.” “Namshukuru Mungu amenipa uwezo wakukamilisha majukumu yangu yote.” “Unaifurahia kazi yako?” “Sana James, japo inaniponza.” “Tena!?” “Acha tu.” “Itabidi kesho tupate muda tuzungumze vizuri unieleze ni kivipi.”

“Nitakuchosha bure. Niambie na wewe siku yako iliendaje?” “Hutanichosha bwana.” “Utanikimbia James. Tuyaache tu.” “Sio kirahisi hivyo. Siku yangu haikuwa mbaya. Na mimi nashukuru Mungu nimeimaliza vizuri.” “Umekula sasa?” “Nimechoka, hata kula sitaki. Nataka kulala tu mpaka kesho. Sitaki kupika.” “Sasa si unalala na njaa!?” “Mchana Nanaa alimtuma dereva kuniletea chakula kazini. Kilikuwa kingi. Nipo sawa. Na wewe umekula?” “Nilipata kifungua kinywa asubuhi, mchana nikakosa muda, usiku hamu yakula haikuwepo, nikaamua kulala tu.”

“Kwanini hamu ya kula imepotea tena? Au hukupata unachopenda?” “Kuna hali napitia nafikiri hiyo ndiyo inanifanya napoteza hamu ya kula.” “Nilikuona umepungua sana, nikafikiri ni kusudi!” Jema akacheka tu. “Pole sana. Na hilo nitataka kujua.” “Pengine umeshasikia.” “Linalokuhusu wewe, hapana. Ningeshakutafuta kukupa pole.” “Sio kweli James. Tunaongea leo kwa sababu nilikuomba msaada. Bila hivyo usingenitafuta.” “Hapana.” James akakanusha kwa haraka.

 “Kwamba si kweli!?” “Kwamba tunazungumza leo kwa sababu uliongeza kitu kingine mbali na kazi ndipo nikapata ujasiri wa kuzungumza na wewe Jema. Wakati wote unaponijia ofisini kwangu, au hata tunapokutana unakuwa umejibeba kikazi tu, na mazungumzo yako ni ya kikazi tena kuashiria unaratiba ngumu kwa siku hiyo. Huna muda wa jingine.” “James!” Jema akashangaa sana.

“Kabisa Jema. Nakwambia vile ulivyojitambulisha kwangu. Na hata salamu yako inatoa ruhusa ya jibu moja tu. ‘Salama au Nzuri’ basi. Kisha unaendelea na kilichokuleta kwangu na ndio maana uliniona siku ile nilinyamaza kidogo kama kukupa nafasi utafakati ulichozungumza ili upate nafasi yakurekebisha kabla sijakujibu. Na kweli ukakanusha.” “Jinsi ulivyolipokea ndio iliniingizia hofu, nikajua nimevuka mpaka. Lakini nilikuwa na nia ya kukukaribisha chakula.” “Na jinsi ulivyokanusha ndipo nilipojua nia yako ya kweli na kukufahamu Jema wa namna nyingine ambaye sikuwahi kumjua.” “Jema gani huyo?” Ikabidi Jema aulize. “Ambaye ni mkarimu mwenye moyo mnyenyekevu si kama ambaye anaonekana akiwa na majukumu ya Joshua.” Jema akaona hapohapo ajiridhishe kwa maoni ya James pia.

“Eti nikuulize swali?” “Juu ya Jema wa kwanza au wa pili?” “Wa kwanza.” “Karibu?” “Eti huyu Jema wa kwanza anatisha kiasi kwamba hawezi kuwa mke wa mtu?” “Inategemea na muoaji.” “James! Hilo jibu ni la jumla sana, bwana.” “Ni kweli Jema. Inategemea na mtu. Nikwambie ukweli lakini usitishike.” “Niambie tu. Nahisi moyo wangu umekufa ganzi James. Nimeumizwa sana, kiasi ya kwamba maumivu mengine yanakuja juu ya yale makali yaliyotangulia, mpaka sioni kama kuna jipya.” “Pole sana. Na yote haya yanatokana na…” “Huyo Jema unayemzungumzia wewe.” “Huyu wa kwanza?” “Huyohuyo. Ameniponza na sijui chakufanya sasahivi ambapo nahisi Kumu ananihitaji sana. Najihisi nikiyumba tu, nitamwaribia sana na yeye.” Jema akasikika kama amekwama sehemu.

“Cha kwanza labda nitengeneze kauli yangu. Binafsi sioni tatizo la Jema wa kwanza maana ndiye aliyenivutia mpaka nikaweza kumfahamu Jema wa pili.” “Kweli James?!” “Hakikaa. Napenda jinsi unavyojibeba Jema. Unajua ni nini unataka, na kukifanya kwa nguvu zako zote na akili yako yote. Hujui jibu la hapana na hukubali kukatishwa tamaa. Hilo umelithibitisha hapa mpaka ulinishangaza, na Kumu nilimsimulia na akaniambia ndio maana bado hajakupatia mtu mwingine na akasema unaweza wewe usijue, lakini unamrahisishia sana mambo yake. Hiyo ni siri nakupa. Joshua anakuheshimu sana na anakutegemea. Hiyo ni siri ingine nakupa.” “Nashukuru kwa kuniuza kwake.” James akacheka.

“Ila sikudanganya. Nilipenda jinsi ulivyo handle hii ishu ya hapa mpaka ukafanikiwa wakati wengi walikuja kutaka kufanya biasha hapa, walishindwa. Na uadilifu wako kwenye mambo unayoaminiwa nayo. Nasemea kwa upande wangu, binasfi nilivutiwa. Naomba nishauri kama naruhusiwa lakini?” “Nishauri tu. Sasahivi sina chakupoteza.” “Unacho. Tena kikubwa sana. Huyu Jema ninayemzungumzia mimi wapo aina yake wachache sana.” “Sio kwamba nimezidisha ujasiri?” Hapo Jema akauliza kwa kupoa kidogo. “Kuzidisha sijui. Lakini usipoteze ulichonacho kwa kushindwa kwa mtu mmoja au wawili kukuhimidi. Sijui kama unanielewa?” “Nakusikiliza.” Jema alishachoshwa na shutuma, akatamani kusikia na upande wa mtu kama James anayejua shule yakutosha ipo kichwani kwake na amefanikiwa kwenye taaluma yake, kama bosi wake, huyo Kumu.

“Mimi nimeishi na watu wengi, tena kwa karibu sana.” James akaendelea. “Nikafanikiwa kumfahamu mwanadamu kwa kuishi naye. Tena mimi nilibarikiwa kuishi na wenye haiba tofautitofauti. Ninaposema kwa karibu. Ni sana. Nikimaanisha kukua nao pamoja kama watoto wa mama mmoja na kuwa pamoja kila wakati na kila sehemu. Katika mambo mengi niliyojifunza kwa hawa wanadamu wenye haiba tofautitofauti ni, usithubutu kubadilika kwa ajili yao hata siku moja, kwa sababu na wao huwa wanabadilika. Sijui kama unanisikiliza?”

“Nakusikiliza James.” “Huyo Jema mwingine wanayemtaka kutoka kwako sasahivi, utashangaa sana utakapobadilika na kuwa kama watakavyo wao. Watamtaka tena Jema huyu wa kwanza, wanayemsema abadilike. Bakia kama ulivyo. Ili watakapobadilika wao, wakirudi wakutane na Jema huyu ambaye siye kinyonga.” “Naona Mungu alikutuma kwangu James. Nilikuwa nashindwa hata kula, sijui chakufanya. Aibu tupu!” Jema akapata tumaini akaanza kujisikia kufunguka kwa James aliyeonyesha angalau yeye anamkubali jinsi alivyo.

“Japo sijajua ni kwa upande upi ila na mimi marafiki walinipitisha hapo. Nikakonda nikawa kama kijiti kwa msongo wa mawazo. Na mimi Mungu akanitumia Geb. Mpaka leo nina uhakika hajui kama alinisaidia mimi. Ila alinipa somo lililonifunza sana.” “Somo gani?” “Kuwa, wapo watu sahihi. Waaminifu. Wanaoweza kusimama na mtu hata kipindi kibaya kisichoweza kutamkika. Namaanisha cha aibu na fedheha. Na akanipa moyo kuwa, yapo mapenzi ya kweli.” “Kweli James?” Hapo akamleta karibu kabisa Jema aliyekata tamaa haswa kwenye mapenzi. “Ooh kabisa Jema! Mimi nimeshuhudia kwa mifano. Hata nikutane na watu wenye mfano mbaya kwa kiasi gani kwenye mapenzi, NAJUA kwa hakika, mapenzi ya kweli yapo hapahapa duniani. Na unaweza kupendwa wewe kama wewe. Ndio maana katika hilo sina hofu kabisa.”

“Kumbe bora tumezungumza! Hakika nilikata tamaa kabisa.” “Maadamu bado Mungu yupo na ndiye mwenye enzi, marufuku kukata tamaa na kujibadilisha sababu ya mwanadamu. Vile alivyokuumba Mungu ni kwa ajili ya mazingira anayotaka kukuweka hapa duniani. Ukijibadilisha tu, ujue hutaweza kuyamudu mazingira yako. Na utafeli vibaya sana. Acha nikuache ulale, tutazungumza vizuri kesho.” “Nakushukuru sana James. Utanifanya nilale vizuri na niamke na ujasiri wangu. Asante.” “Karibu. Usiku mwema.” Wakakata simu. Hapohapo Jema akalala, wakasahu hata kuweka mipango ya kesho yake.

Jumamosi.

Waliamka wakiwa wamejenga kitu cha tofauti ila kila mtu akaogopa kumtafuta mwenzie wa kwanza. Wakabaki kujiwinda kila wakati macho kwenye simu wakivizia kama kuna jumbe. Kwa kuwa Geb alizima simu ili alale alipowasha mida ya saa 4 akakuta jumbe tatu kutoka kwa James. Mama yake akamuona anacheka. Akampigia. “Nyumba inaungua James?” “Unakumbuka jinsi nilivyokufanikishia mpaka wewe ukaoa huku mimi nikitukanwa?” Geb alicheka sana. “Unarudi kudai kulipwa fadhila?” “Tafadhali usinizimie simu, Geb.” “James, unajua jumamosi huwa sifanyi kazi, nakuwa nyumbani na watoto. Na ninachelewa kuamka.” “Mkeo ameniambia amekuacha ukiwa umeshaamka.” “Kwamba umempigia mpaka Nanaa simu huko kazini!?” Geb akashangaa sana.

“Kumbe! Kwa nini hupatikaniki Geb?” “Mambo yaliendaje jana?” “Acha kunicheka bwana!” Geb akazidi kucheka. “Na kwa taarifa yako tu, yamekwenda vizuri sana. Leo nataka kumtoa kwa chakula cha jioni.” “Wapi?” “Kuna sehemu wanachoma..” “Naomba uishie hapohapo James!” Geb akamkata akiwa ameshituka sana. “Kwani vipi!? Wanachoma mbuzi vizuri!” “Unataka kumpeleka viwanja unavyoendaga na Nanaa?” James akanyamaza.

“Wewe vipi James!?” “Nanaa anapasifia sana. Na anapapenda.” “Kuna sehemu kunakochomwa nyama Nanaa asipapende?” Mpaka mama G akacheka huko jikoni. “Hata stendi ya mabasi ukimpeleka Nanaa ukimwambia kunachomwa nyama vizuri, yeye na mwanae Magesa wataenda kula bila kujali eneo ilimradi wafikie hiyo nyama.” “Lakini kweli asiee! Sijafikiria vizuri. Huyu Nanaa ataniponza bwana!” “Acha kumsingizia mke wangu. Wewe mwenyewe unashindwa kufikiria.” “Basi tuanze taratibu.”

“Nimpeleke wapi? Na usisahau nilikwambia ni mtoto wa mjini na amesoma. Anauwezo halafu..” “Acha kupaniki. Tuanzie kwenye swala la uvaaji wako kwanza wewe halafu utapata picha.” “Usianze Geb.” “Ulitaka uvae nini sasa?”  Akatulia. First impression matters a lot James. Usiende kutuabisha.” “Sasa nivae vipi?” “Casual simple, and smart.” Akatulia. “Umenielewa lakini?” Kimya. “Kwani wewe huwa hutuonagi tunavyotoka na mke wangu?” “Sijawahi kuzingatia! Inakuaje?” “Kwanza jipange kiasi ya kwamba hata kama yeye atapendeza sana, hutamuangusha. Na hata kama atavaa kawaida, bado hakutakuwa na utofauti. Nakutumia picha zangu na Nanaa upate picha ya nini nazungumzia. Na huwa nikitoka na mke wangu simpeleki kwenye nyama choma. Nampeleka kwenye sehemu wanazokula kwa kisu na uma. Kwa hiyo andaa walet.” “Sawa.” Geb alicheka sana. “Hakika James umekamatika! Umekubali kutoa pesa kwa haraka hivyo!?” “Tuma picha Geb.” James akamkatia simu akimuacha Geb akicheka sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akaamua yeye ndio aanze kumtumia ujumbe Jema. ‘Uliamka salama?’ Baada ya kama lisaa ndio Jema akampigia. “Samahani James. Nimebanwa hapa kazini nimeshindwa kushika simu. Niliiacha ofisini.” “Usijali kabisa. Chapa kazi.” “Hujakasirika sasa?” “Nini kiniudhi!?” James akawa hajaelewa. “Kwamba sijajibu ujumbe kwa wakati.” “Hapakuwa na deadline ya majibu Jema! Acha wasiwasi. Umeshamaliza kazi lakini?” “Bado kikao cha mwisho cha Kumu, ndipo nifunge siku.” “Basi usichelewe. Ila ukitulia naomba nijulishe ungependa nije kukuchukua saa ngapi? Na unataka kwenda kula wapi au unahamu yakula nini?” Jema akacheka.

“Kuja mpaka kwangu si usumbufu? Au tukutane?” “Hiyo itakuwa siku nyingine tutakutana huko. Leo nilikuomba mimi ndio nikutoe, kwa hiyo leo mimi ndio dereva wako.” Jema alifurahi sana. “Mbona unacheka?” “Sikutegemea! Nimefurahi sana.” “Basi wahi kazi, tutawasiliana ukipata nafasi.” “Asante James.” Jema alikata simu akiwa haamini. James hana neno kusubirishwa majibu ya simu yake! Anakata simu ili Jema arudi kufanya kazi! Jema akabaki ameshikilia simu haamini. James alifanya kila kitu alichoshauriwa na Geb. Hata kwenda kumchukua nyumbani ni wazo la Geb.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Akafanya shuguli zake ndipo na yeye akaenda saluni kutengenezwa kichwa. James mweupe kama dada yake Nanaa. Damu ya upande wa mama zao. Akachongwa vizuri na kulambishwa dawa kichwani. Nywele zikalala kama zakishombe. Wakamuwekea rangi nyeusi kwenye sehemu ya ndevu/mustachi na kichwani. Alipendeza James, mpaka mwenyewe akajikuta akicheka mbele ya kioo. Akasita kununua nguo mpya asije Jema kumgundua. Akarudi kwake kuanza kutafuta nguo, akiangalia picha za Geb. Akakwama kwenye viatu. Hakuwa na aina hiyo ya viatu.

Akampigia Geb. “Nimekwama viatu.” “Bora umenipigia maana nilikuwa nikiwaza, naomba Mungu usije ukatokea na zile raba zako.” “Zina nini?” “Wote tunajua hazikuwakilishi vizuri ndio maana umenipigia.” James akapoa. “Basi nielekeze huko unakonunua zako.” “Usilie bei.”  Geb akamtahadharisha asijue James alishayavulia maji nguo. “Wewe niambie.” “Kweli umepania mzee!” “Unanichelewesha Geb.” Akamuelekeza wanapouza sneakers anazovaaga yeye na Joshua. James akakata simu akaondoka kwenda kuzisaka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usipitwe na Dinner ya James na Jema. Ipi Historia ya Jema naye. Mara ya mwisho James alisikia anakaribia kuolewa. Kipi Kiliendelea kwake. Na yapi yatajiri kwao?

Je, Hatimae James amepata?

Usikose muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment