“Hayo
anakwambia wewe akikiri kosa?” “Anasema kosa ni kuendelea kunivumilia kwa muda
mrefu mpaka kumfanya akamkosea Mungu wake.” “Kwamba wewe ndio kosa?” “Naona
umenielewa.” “Na mlikokuwa mkijenga?” “Stori ilibadilika. Pakageuka kwake.
Yeye ndio aliyenunua kiwanja na kusimamia ujenzi wakati mimi nikihangaika na wanaume
za watu, yeye alikuwa halali. Anasema amejenga kwake na watoto wake, mimi
nilishindwa kusimama naye kujenga nyumba.”
“Pesa
uliyowekeza?” “Ameniuliza bila aibu, ni hela gani nilimpa?” “Jema!”
“Nikimwambia nililia mpaka nikakaukiwa, amini nililia James. Hapa nilipo
nakatwa mshahara kwa asilimia zaidi ya 70. Na yeye ndiye aliyenifundisha kukopa
benki tofauti tofauti. Nimemjengea kwake, mimi naishi kwenye kile kinyumba
chakupanga pale.” “Lakini ni pazuri.” “Ila si kwangu James.” “Ni kweli.”
“Na mbaya
zaidi sina hela zakusema nianze tena ujenzi. Itachukua zaidi ya miaka hata 8 kuja
kumaliza deni na kuanza tena. Halafu Temu ni muongeaji kwelikweli. Huko kote
tunapojulikana mimi na yeye kama tulikuwa wachumba, ametangulia kunichafua hata
kama kungekuwa na mchumba mwingine wa kuoa atagairi tu.” “Kumbe bado nia ya
kuolewa ipo?” “Jana umenijenga James. Umenitoa chini sana, ni hivyo hujui tu.
Leo nimeamka na nguvu mpya.” “Afadhali na pole sana.” Wakatulia kila mmoja
akaendelea kunywa kinywaji chake mpaka chakula kilipoletwa.
“Hujaniambia
juu yako James. Wewe ni kwa nini hujaoa mpaka sasa?” “Wala sina stori ndefu.
Sijawahi kuumizwa na mwanamke kwa kuwa sikufungua huo mlango. Si kwa woga ila
sikuwa tayari sababu ya kwanza Nanaa. Sikutaka kujichanganya. Nikajikuta
nakwama kwenye mambo mengi kwa kuwa kama ungeniambia wakati ule yule Nanaa
niliyekuwa nikimlea, ndiye angekuwa huyu! Pengine nisingeamini, na kama
ningeamini basi pengine ningebweteka kwake. Kwahiyo sikutaka
kujichanganya kabisa. Sikutaka kufikishwa mahali nichague kati yake na mapenzi.”
“Hilo
moja. Pili nilikuwa na malengo yangu kwenye maisha, niliona nisubiri mpaka
nikamilishe. Ila Geb na Joshua wao wananiambia ni sababu tu, sikupata mtu
aliyenivutia.” “Ambayo ni kweli?” “Nahisi pana ukweli. Ila japokuwa
nimezungukwa na wasanii wengi wa mapenzi, lakini pia nina uhakika wa
upendo au mapenzi ya dhati yasiyochanganywa na pesa au usanii. Kwa kuwa
katika hao wengi matapeli, ninao wachache wamelithibitisha hilo na
kunifanya nisiharakishe mpaka na mimi nipate mtu wangu.” Jema akatulia
kabisa na kuendelea kula taratibu.
“Unaonaje
chakula chao?” James akauliza kwa kujali. “Kizuri sana. Na wewe je?” “Na mimi
nimekipenda.” Wakaendelea kula. “Wewe huwa unapika?” James akacheka huku
akijaribu kujifikiria. “Nafikiri naweza kupika mtu akala, japo sina muda na si
kitu nafurahia kufanya. Akinisahau Nanaa, ujue ndio basi tena.” “Kwamba
anakupikia kila siku!?” “Nafikiri anapika kingi. Anajaza kwenye makontena. Anakuja
kuniwekea kwenye friji. Akihisi kimeisha, analeta kingine au sijui mwenyewe huwa
anafanyaje! Sijui huwa anapita kwangu kukagua au la! Ila anajitahidi kwakweli.
Na nisipokuta chakula najiona ni bora kulala tu kuliko kuanza kupika.” Jema akacheka
akifikiria, akaona aulize zaidi.
“Na
unapenda vyakula gani?” “Sijapata muda wa kujichunguza na kujua nini napenda
zaidi. Ila Nanaa anapenda sana nyama choma! Basi amenifanya na mimi niwe mpenzi.
Ukitaka afurahi mpeleke kwenye nyama choma.” Jema akacheka. “Sasa amenilemaza,
najikuta ni kitu nakuwa na hamu nacho. Geb mumewe siwezi kumpeleka huko mara
kwa mara. Ukiwaita yeye na Kumu wanabaki kuwa watizamaji na maswali yanayokera
mpaka hufaidi nyama yenyewe!” “Maswali gani?” Jema akauliza akicheka. “Usafi
wake. Kama imeandaliwa kwa usafi na kama kweli ni fresh sio ngombe au mbuzi
kibudu/mzoga, mpaka nikaona niwe nawaacha tu nakwenda na Nanaa.” “Yeye hana
shida?” “Yule chochote kinachoitwa chakula, hata uweke kwenye jani la mgomba,
atakula bila wazo la pili.” Jema alicheka mpaka machozi.
“Yaani
ungemleta hapa. Angesifia hiki chakula kuanzia kijiko cha kwanza mpaka
anamaliza.” “Nanaa huyo!” “Marafiki wa karibu sana na chakula. Hawajawahi
kugombana.” “Labda akiwa mgonjwa.” “Tena iwe tumbo. Lakini sijui homa tu,
kichwa! Mwenyewe anakwambia haviingiliani.” Jema alicheka sana. “Sasa mbona
hana mwili mkubwa.” “Mama mkwe wake alipata matatizo ya magoti. Kupunguza mwili
kulimsaidia sana. Sasa imebidi wajiandikishe gym na wanamashine za mazoezi pale
kwao. Ndio pona ya dada yangu yule. Ila si kujinyima chakula. Hapo ni
kumnyanyasa.” Jema alicheka sana.
Wakapata
wakati mzuri wakufahamiana taratibu, James akitupia maswali hapa na pale
kujaribu kumfahamu. “Na baba mzazi?” Jema akacheka kwa masikitiko. “Sijui hata
ni nani na mama mwenyewe alituzaa kila mtoto na baba yake. Ukimuuliza anakwambia
ni katika kuchanganyachanganya huko ndio ametupata sisi wawili.” James
akashangaa sana. “Sijaelewa!” “Na mimi ndio hivyohivyo. Ingekuwa maisha
yanakupa nafasi ya kuja kukutana na mama yangu mzazi mimi, ndio ungeelewa
ninachozungumzia. Kile anachokifikiria kichwani huwa hawezi kukiacha moyoni.
Atakisema tu.” “Kama kumwambia Temu ni tapeli?” “Ewaaa! Sasa usimkute
amekasirika au usimuulize swali linalomkumbusha machungu yake. Utajuta kuuliza.
Kwa hiyo kwa kifupi mimi na mdogo wangu hatuna taarifa za baba zetu. Akiwa
ametulia atakwambia alibakwa. Mdogo wangu huwa anamuuliza mara zote
mbili? Anakwambia mimba haiitaji kitanda kutungwa. Ashamaliza. Akiwa
amekasirika atakujibu majibu mabaya, kisha atakwambia nenda kaulize Ustawi wa Jamii.”
James akacheka taratibu.
“Bibi
mwenyewe anasema anahisi alidondoka alipokuwa mdogo akagonga kichwa.” Ilibidi
James acheke. “Huna mfano wa mama yangu.” “Lakini nyinyi aliwalea.” “Kwakweli
siwezi kulalamika. Na ni kwa kadiri ya uwezo wake. Hilo nitamtetea. Sema mimi mwenyewe
nilitamani maisha ya kujitegemea mapema sana. Kwahiyo nilipomaliza tu chuo, mama
mwenyewe ndiye aliyenitafutia kazi pale Coca. Alifanyaga kazi pale zamani,
akawa anafahamiana na watu pale. Kwahiyo baada ya kupata mshahara wangu wa
kwanza, mama mwenyewe akanisaidia kutafuta pakuishi. Akanisaidia kuhama,
nikaanza kujitegemea.” “Kumbe anajali hivyo!” “Sana. Yaani hata sasahivi
nikimpigia simu, nikamuomba aje popote, nikamwambia nina shida naye, hatauliza
mara mbili, ataacha kila kitu na kuja kunisikiliza. Anatujali sana, ila mimi
mwenyewe napenda kujitegemea.” James akarudishwa kwa mama yake yeye mwenyewe. Vituko
vyake na maisha yake mjini kama hana mume! Akapoa kabisa.
“Kwa hiyo
uliajiriwa moja kwa moja kwenye kitengo cha Masoko?” “Ndiyo, lakini nilifanya
pale kwenye ile kampuni wala hakuna aliyekuwa akinijali mpaka alipokuja Kumu.
Na shule yangu ndogo, akataka nifanye naye kazi kwa karibu. Niliogopa James!
Ukumbuke ni Kumu, halafu mimi sijasoma! Nikasahau maombi yote niliyokuwa
nikimsihi Mungu aniinue kwa kidogo nilicho nacho.” “Ulitaka nini?” “Sikuwa
nikijua kwa hakika kwa kuwa sikuwa nimesoma sana. Ila niliona ufanywaji kazi
pale, nikawaona hao walio soma na kazi zao, hakika nilijua na mimi nitaweza tu.
Tena nikawa najiaminisha eti naweza kufanya vizuri zaidi yao.” Wote wakacheka.
“Basi nikawa
sina uwezo wa kurudi shule ila kufunga na kuomba nikimsihi Mungu atumie kidogo nilicho
nacho kuniketisha na wakuu. Sasa eti Kumu kuja kuniambia nifanye naye kazi, nikaingiwa
hofu sana. Kwanza nilishakuwa nimesahau hayo maombi, kwa kuwa ni kama nilikaa
muda mrefu bila kujibiwa. Mpaka akaja Kumu sasa. Alipoona nimeingiwa hofu, ndipo
akaniambia yeye hataki mtu mwenye vyeti vikubwa, ila anataka kufanya
kazi na mtu mwenye tabia kama zangu. Ilichukua muda mfupi sana kumuelewa na
kuanza kufanya naye kazi. Na pesa ninayolipwa pale, kwa mtu mwenye shule yangu,
hakuna sehemu wanaweza kunilipa hivyo.” “Ila imeongezeka ujuzi.” “Kwa sasa ndiyo.
Ila namuombea sana Kumu asije kuondoka pale. Naweza sema ndio kama nguzo yangu
pale. Anatetea sana maslahi yangu.”
“Kwa hiyo
kujibu swali lako, sijui baba yangu ni nani, wala kabila yake. Ila mama yeye ni
mtu wa Kilimanjaro.” James alifurahi sana. Kabila ya mama yake vikaendana.
James mtoto wa kwanza. Alitamani kuoa mwanamke ambaye haitakuwa shida
kumtambulisha hata kwa bibi yake. Akajiambia atasimamia hapohapo, ataachana na
maswala ya baba na hatajali tena ni Kilimanjaro ipi huyo mama yake anatokea. “Ibakie
tu Kilimanjaro.” Akawaza James nafsini mwake.
“Nikwambie
ukweli James?” Akamtoa mawazoni. “Hilo lakutojua baba yangu, lilichangia sana
kutulia kwangu na kutamani sana ndoa. Kuwapa watoto wangu familia na baba
wakueleweka. Najihisi kama kuna kitu au upendo fulani nimenyimwa au kupunjwa hapa
duniani, kupitia baba. Ndio maana najitetea hata kwa Temu, nilibaki kama mjinga
akininyanyasa huku tukiwa na picha ya kuwa ni couple ya wacha Mungu,
nikijua nitabahatika ndoa. Nikajifunga kwake nikimvumilia, na kumuamini Mungu
pengine atakuja kumbadilisha, nikijua nahangaika kwa ajili ya watoto wangu,
lakini imekua tofuati. Aliponitenda nilimlaumu sana Mungu kwa sababu
kuna wakati nilikuwa mpaka nafunga na kuomba kwa jili yake kwamba Mungu abadili
moyo wake. Huku nikijaribu kumpa kila pesa anayotaka! Lakini haikusaidia.
Nilimlaumu sana Mungu na kumwambia kwa hasira kuwa hathamini kujitunza kwangu.”
“Inawezekana
Mungu ndio amekujibu Jema.” Jema akakunja uso. “Kutendwa kikatili kiasi
hicho!?” “Wewe ulikuwa mwaminifu kwa Mungu. Si ndiyo?” “Kabisa James!” “Na
ukamuomba?” “Ndiyo. Tena kwa uwaminifu kabisa, nikijikinga na kila vishawishi, jamani!”
“Ulikuwa na jinsi yako ya Mungu atakavyokujibu. Lakini majibu ya Mungu aisee ni
ya ajabu sana Jema. Mimi si mcha Mungu sana. Lakini kwa kukaa na Geb pamoja na
Kumu, nimekuja kujifunza mambo mengi sana juu ya Mungu. Tunavyofikiri sisi
sivyo anavyofikiri yeye. Njia zake sio zetu kabisa. Wakati wewe
unafikiri hajakujibu, kumbe ndio amejibu kwa kukuonyesha kwa wazi kabisa
yeye ni mtu wa namna gani. Akamshupaza shingo yake kabisa asije hata kukuomba
msamaha ukamsamehe, ili tu kumtoa kwako. Maana kwa jinsi nilivyokusikia
ni kama aliyaendesha mahusiano yenu kibabe.” Jema kimya.
“Nina
uhakika angerudi kukuomba msamaha na kukwambia ilikuwa bahati mbaya, pengine ungemsamehe.
Sasa fikiria ungekuja kuolewa na mwanaume wa namna hiyo. Anayekunyanyasa vibaya
hivyo. Ndio mpaka kifo chake! Inamaana hata hao watoto wenu wangezaliwa
wakawakuta kwenye hiyo hali. Wewe huoni hiyo garama ya deni la pesa
alilokuachia ni dogo sana kulinganisha na mateso ya maisha yako mpaka kufa?”
“Lakini kweli!” “Mshukuru Mungu.” “Ndio maana neno la Mungu linasema tushukuru
kwa kila jambo!” Jema akawa kama amekumbuka mwenyewe.
“Ukute
Mungu alikuwa akiniepusha naye!” Akaendelea kuwaza kwa sauti. “Pengine Mungu
wangu alinihurumia!” “Na ndipo linapokuja swala la kutokata tamaa. Mimi
nilimwambia mama G, kama Kumu na yeye ameoa, basi na mimi nitaoa tu.”
Wakacheka. “Maana mama G alikuwa akitusema sana mimi na Joshua. Anasema
tunazidi kuzeeka. Joshua akanitia moyo akaniambia, upo upendo wa kweli, niwe
mwaminifu kwa Mungu, Mungu si mwanadamu hata aseme uongo, atanipa haja
ya moyo wangu. Ndio na wewe nakwambia hivyohivyo. Endelea kumtumainia Mungu.
Subiri bila kukata tamaa. Atakujibu tu.” “Nakushukuru James.” James akacheka.
“Kweli
umenituliza. Nilikuwa nikijiuliza kweli uaminifu wangu kwa huyu Mungu ni bure
tu!” “Hata kidogo. Inaweza kuchukua muda, na inaweza isiwe kama tulivyotaka
wewe. Kuwa itokee kilaini tu. Ila Mungu anajua walio wake. Jicho lake
lipo kwao, hajawahi kuwaacha.” “Sasa mbona unasema humjui sana Mungu lakini
unahekima ya kimungu hivyo!?” James alicheka sana.
“Kina
Kumu wameniathiri sana. Ndio watu wangu wa karibu. Naweza nikashindwa kwenda
kanisani, lakini huwa jumapili baada ya ibada lazima tukutane kwa kina Magesa.
Hapo tutashinda tukizungumza mpaka usiku. Na mama G ni mcha Mungu sana. Kwa
hiyo wameathiri hata mtizamo wangu mkubwa kwa Mungu.” Wakaendelea kuzungumza
mpaka wakaona watoke hapo.
Kukawa na
kitu kingine kimejengeka kati yao, lakini kama kila mtu akaona achukulie
taratibu au kuwindana. Wakapata utulivu moyoni. James akiwa amemfahamu Jema kwa
asilimia kubwa iliyojibu maswali mengi sana mpaka ambayo hakujua jinsi ya
kumuuliza, Jema akawa ameyajibu.
“Sasa na
kusimama nako ndio inakuaje?” Jema akauliza. “Usubiri Jema! Nakuja kukusaidia
kusimama.” Jema alicheka sana. “Ningeshavuta kiti mimi!” “Acha haraka. Hiyo
kazi yangu.” Wakazidi kucheka. James alishapitishwa shule na Geb, akawa anajua
nini chakufanya. Wapi asimame ili kuvuta kiti wakati akisimama. Akafanya kama
mtaalamu, Jema akicheka sana. “Mwenzio sijazoea.” “Taratibu tu, utazoea. Ukiwa
na mimi uache kukimbilia vitasa vya mlango.” Jema alicheka sana mpaka akainama
James akimwangalia. “James wewe mtundu kuliko unavyoonekana!” “Mimi nakwambia
ukweli.” “Haya, basi.” Wakatoka hapo ndani hotelini.
“James!”
Jema akamuita kabla hajafungua mlango. “Nashukuru kwa usiku mzuri sana.
Nilihitaji kila kitu. Chakula kizuri, mazungumzo yote. Nahisi Mungu amenijibu
kilio changu, maombi yangu mbele zake kwa kupitia wewe usiku wa leo. Asante kwa
muda wako pia. Nashukuru kuwa na mimi usiku wa leo.” “Na mimi nikisema kama
ulivyosema nitakuwa nikiiga?” Jema alicheka sana.
“James!”
“Ni hivyo uliniwahi tu. Na mimi nimekuwa na wakati mzuri Jema. Asante kukubali
kutoka na mimi baada ya kushindikana mara ya kwanza.” “Sema baada ya kunikatalia
mara ya kwanza.” “Hapana Jema. Sikukataa ila nilikuwa na miahadi niliyokuwa
nikikumbushwa na Nanaa karibu siku nzima. Kuna game huwa watoto wake wanapenda
kucheza, zaidi Magesa.” “Yule mwimbaji?” “Ewaa! Huyohuyo. Sasa huwa inachezwa
na watu wawili. Akicheza na baba yao, huwa anawafunga, basi Magesa huwa
anaishia kulia.” “Hataki kufungwa?” Jema akauliza akicheka.
“Kabisa.
Sasa na yeye Geb anamkaba mtoto, hampi mwanya wakufunga hata mara moja. Na Nanaa
hapendi vile mwanae akilia, na Geb hataki kumuachia anasema anamfundisha
kupapanda na changamoto za maisha.” “Ambayo ni kweli.” “Akikusikia Nanaa
mtakosana sana. Mimi napendwa pale kwao kwakuwa huwa namuachia anifunge.”
Wakazidi kucheka.
“Kwahiyo
ile miahadi uliyosema, kumbe ni ya kwenda kufungwa?” “Naona umeelewa. Nilikuwa
nakumbushwa siku nzima, maana asubuhi yake baba yao huwa haendi kazini, ila
mama yao anakwenda. Nasikia wakaamkia game. Geb akamfunga Magesa. Mama yake anasema
akapokea simu kutoka kwa mwanae akilia, anasema yeye anampenda sana. Yeye anaona
amtume dereva ampeleke tu ofisini akafanye naye kazi. Anamtaka yeye. Nanaa
anasema akafikiria kwa haraka, akajua Geb kashamfunga. Ndio nikapigiwa simu
nikiombwa niende, akanifunge, ili alale vizuri.” “Sasa kwa nini Nanaa yeye
hachezi nao?” “Hajui. Na Magesa anaakili sana. Ushindi wake anataka aupate kwa
mjuaji. Yaani akijua unajua halafu akakufunga ndio raha yake. Sasa baba yao
nasikia amepigwa marufu kwa muda. Nanaa hataki acheze naye mpaka mwanae ajue
sana. Ambayo najua haitakaa ikatokea maana na yeye Geb anaongeza ujuzi ili
asije wahi kufungwa na Magesa.” Jema alicheka sana lakini angalau akaridhika
kuwa sio kwamba alikuwa akikataliwa tu. Kweli alikuwa na miahadi.
Safari ya
kurudi kwa Jema ikaanza. Pakazuka ukimya. James akashindwa aendeleze vipi
mazungumzo yanayowahusu wao wawili. Akaona asije akaharibu, akatulia. Jema
akajivuta nyuma vizuri, akajiegemeza kichwa, macho nje ya dirisha, kimya. James
akamrushia macho mara kadhaa akamuona ametulia tu.
“Upo wapi
tena?” Akageuka na kucheka. “Nipo?” “Wapi?” “Nawaza. Ila si kwa vibaya kama
zamani.” “Nini?” “Pakuanzia kwenye maisha.” “Hutakiwi kuanza, ila kuendelea.”
“Unakumbuka nilivyokwambia nimeharibu kwa madeni ambayo ni kama namlipia Temu
na familia yake? Hiyo inaniuma James! Inaniuma sana.” “Mimi naona ni
garama ndogo sana yakulipa kwa uhuru wako. Hebu fikiria Jema, lipi bora? Kulipa
hilo deni huku ukinyanyasika, huna raha au kulilipa ukiwa na akili iliyotulia?”
“Ni bora kulilipa nikiwa nimetulia nipo huru, lakini James, bado ni deni ambalo
natakiwa kulilipa huku maisha yaendelee. Ningekuwa na muda ningesema hata
nitafute kijibiashara nifanye niwe naingiza pesa sehemu mbili. Halafu sitaki
niishi nyumba zakupanga daima na sitaki kurudi kuishi kwa mama kwa
kushindwa kumudu maisha! Kwahiyo nashukuru kwa nafasi ingine ya uhuru, ila
inabidi kujipanga na hili nilikabili.” “Hilo ndilo la muhimu.” James akaongeza
na kuendelea.
“Mimi
nina imani na wewe Jema. Kwa vile nilivyoambiwa na Joshua, naamini hutakwama
hata katika hili. Jipe tu muda utaona mambo yanaanza kukaa sawa. Ile pesa
uliyokuwa ukiigawa kwake, itaanza kutulia mfukoni.” “Ni kweli.” Akaafiki na
kutulia. Mpaka wakafika nyumbani kwake.
“Nikikukaribisha
ndani utakaribia?” “Naomba iwe wakati mwingine Jema.” “Sawa, kama kutakuwa na
wakati mwingine.” “Naamini tutakuwa na wakati mwingine. Au unafikiri leo ndio
iwe mwisho?” Jema akatulia kama anayefikiria. “Vipi? Hutaki tena?” “Sijui James!
Acha wakati uje ujibu hili.” James akabaki amepoa kama aliyemwagiwa maji. “Kwamba
hataki kuja kutoka tena na mimi! Nimekosea wapi!?” James akawaza. “Usiku
mwema James. Na asante kwa kila kitu. Mungu anajua ni kiasi gani nilihitaji
usiku kama huu ulionipa.” “Asante Jema. Usiku mwema.” Akashuka garini baada ya
James kumfungulia mlango. Akamsindikiza mpaka mlangoni. Jema akacheka. “Kwamba
huondoki mpaka niingie ndani?” “Na ufunge mlango kabisa, nijiridhishe upo ndani
salama.” Jema akacheka kujaliwa. “Asante kujali James.” “Karibu.” Akangoja
mpaka alipoingia ndani kabisa na kujifungia mlango ndipo akaondoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jema
alitamani kumtumia ujumbe lakini akaogopa hajui aseme nini. Wazo likamjia.
Akampigia na James naye akapokea kwa haraka sana. “Nakusindikiza.” James
akacheka kwa furaha maana aliondoka pale kwa masikitiko akijua ni kama Jema amehitimisha.
“Nakushukuru.
Nilifikiri ungetaka kulala!” “Nitalala tu. Hata hivyo kesho naenda ibada ya saa
nne, kwa hiyo nitakuwa na muda wa kutosha tu wa kulala. Halafu sitaki ujikute
peke yako huko barabarani ukirudi nyumbani. Au ni usumbufu?” “Hata kidogo japo
sirudi nyumbani kwanza. Kuna mahali napitia.” “Basi nikuache nisiingilie.”
“Hapana. Na mimi nataka unisindikize. Ni mambo yangu ya kibiashara.” James
akaendelea.
“Kuna mzigo
umeingia ndio nakwenda kuangalia. Ni kama biashara mpya nimeanza nafikiri hata
mwaka haujaisha, sitaki kiharibike kitu.” “Hongera japo sijajua ni biashara
gani.” Ikawa kama anayetaka kujua zaidi. “Nilifungua duka la Spare Parts.
Naingiza nchini zaidi vifaa vya Toyota ambavyo ni uhitaji mkubwa hapa nchini na
Nissani ambavyo ni hadimu.” “Unaonaje?” “Aisee siyo mbaya kabisa. Nilianza kama
kujaribu tu. Lakini inalipa aisee, ndio maana sitaki kitu kiharibike. Nipo nayo
makini sana.” “Hongera James.” “Asante.” “Basi ukifika
uniambie ili nikate nikuache ufanye kazi.” “Sitasindikizwa nyumbani?” Jema
alicheka sana.
“Au
usindikizwaji huu ni wa masharti? Mara moja, basi. Nitakapoishia ni hapohapo!”
“Ukinipa ruhusa nitakusindikiza popote uendapo.” “Basi ujiandae kukesha maana
nikitoka hapo, nakwenda na Kariakoo.” “James! Usiku huu?” “Mjini pesa hailali
Jema.” “Lakini kweli! Mpaka umenitamanisha! Kwa kazi nzuri uliyonayo ungeweza
kubweteka!” “Kazi hii ya ofisini ni ya watu. Hii ya pili ni yangu. Hata
nikikosana na Mwajiri, akataka niondoke kazini, siyumbi kiuchumi.” Akazidi
kumvutia Jema.
“Ni kweli
kabisa. Sasa na Kariakoo nako ni nini?” “Ndipo lipo duka kubwa la vifaa vya
magari. Huku nawasogezea huduma matajiri wangu kama mafundi wa wakina Kumu na
Magesa.” Jema akacheka lakini akizidi kushangazwa na James. “Nishasema
hongera nyingi sana, utanichoka.” James akazidi kucheka.
Wakaendelea kuongea.“Acha mimi ndio nikupigie nisikumalizie pesa yako.” “Asante.” James
akampigia yeye. Maongezi yakaendelea. Akamsindikiza mpaka saa sita na nusu
usiku.
“Hujachoka
tu?” “Bado. Nafurahia mwenzio.” “Sasa unafurahia nini? Kukesha na mimi?” “Nafurahia
kampani yako. Mwenzio nilikuwa nakesha kwa mawazo, bora hivi nakesha nikicheka
na kuzungumza vitu vya maana vya maendeleo.” “Basi kama ndio hivyo tuendelee.
Ila baada ya muda mfupi sana nitakuwa nimefika na wewe upumzike ulale. Usikeshe
tena. Au bado unawasiwasi?” James akauliza akisikika kujali.
“Wasiwasi
hapana James. Ila natakiwa kujipanga ili kurudia kwenye mstari na kujijenga kwa
upya.” “Nakuelewa. Na najua utaweza tu. Panga matofali yako taratibu ukiwa na
msingi mzuri, utafanikiwa tu. Na usijali tena maneno ya watu.” “Ila kanisa nitahama.
Pale pameshachafuka, kutanipotezea utulivu.” “Sio kwa kukimbia Jema!” “Hivi
nilikwambia kama Temu ni yule mzungumzaji tena wa jazba?” “Uliniambia.”
“Sasa
ametangulia yeye kujisafisha kwa kunichafua mimi. James, pale sitapata utulivu.
Japokuwa alinikuta pale kanisani, acha tu nimpishe. Makanisa ni mengi sina
sababu ya kujitesa.” “Umeshajua sasa pakwenda kuabudu?” “Naenda kujaribisha
kanisa moja hivi, lipo pale Victoria. Wanapasifia ni pazuri.” “Basi naomba na
kesho tuongozane wote.” Jema alishituka moyoni akabaki kimya kwa muda. James akaangalia
simu yake aliyokuwa ameweka kiti cha pembeni akizungumza kwa kutumia bluetooth.
Akakuta bado yupo hajakata.
“Jema?”
“Kweli James?” “Kama ni sawa kwako. Ila ningekuwa mimi ningekubali tu.” Jema
akaanza kucheka. “Angalau huwi mgeni peke yako.” “Mwenzio
nimefurahi mpaka nahisi machozi kunitoka. Sitaanza kwa uchungu nikiwa mpweke.” “Umeona
mambo hayo. Wewe kila ukitaka kuanza kitu, nipigie nikusindikize huko mwanzo
unakoanzia.” Jema alicheka sana. “Hutachoka?” “Nyumba ni
msingi, mama. Sasa nina shida gani kuwepo kwenye vitu muhimu kama hivyo? Yaani
wewe ukiwa unafanikiwa mbeleni, unakuwa na kazi yakunikumbuka tu mimi
niliyeanza msingi na wewe.” Jema akazidi kucheka kwa furaha.
“Naamisha
Jema.” Hapo Jema akatulia. “Sitaki unisahau Jema. Na
sitaki unisahau kwa ubaya. Ila mema. Siahidi kuwa mkamilifu kama Mungu, lakini
sikusudii kukusababishia maumivu.” Ikamgusa sana Jema. Japo
James hakuongea kwa wazi, lakini ikamfariji. “Kwa umbali gani James?
Nisije weka tumaini nikajiona sipo peke yangu tena kumbe sivyo.” Jema
akauliza kwa sauti ya upole. “Umbali wowote utakao niruhusu wewe.” Jema
akatulia kabisa. “Upo Jema?” “Labda niulize tena. Kwa muda gani? Kwamba hii ofa ipo
mpaka lini? Inaku expire?” “Utakavyoamua wewe.” “James!?” Jema
akashangaa sana.
“Mimi
nakwambia ukweli Jema. Na nilishakwambia sikuwahi kumfungulia mwanamke mlango.
Nilikuwa na sababu zangu. Lakini wewe umekua wakwanza. Na mimi najijua si
muongo. Siwezi na kesho nikamwambia tena mwengine hayahaya niliyokwambia wewe.
Kwanza sijajaliwa huo uwezo. Ndio maana nilipokuwa nikimlea Nanaa, kama
unakumbuka nilikwambia wazi sikutaka kujichanganya.” “Kwahiyo sasahivi unajiona
upo tayari kwa jukumu jingine?” “Kwako, ndiyo. Kwa kuwa nimekusoma na
kusikia sifa zako, naona hutakuwa jukumu ila kampani yakunifikisha mbali zaidi
au mtu wa kuwa naye nisiwe mpweke tena.” Akaongea kama anayejua anachozungumza. Hajakurupuka.
Anamaanisha kwake. Jema akatulia kabisa kusikiliza.
“Mfano hiki
ulichokifanya usiku huu. Kwako kinaweza kisilete maana, lakini ndicho nilichokuwa
nikikitamani. Binafsi sikutegemea kama ungeweza kuwa na mimi usiku wote huu
ukinisubiria kwenye simu. Na usifikiri nategemea ufanye hivi kila siku! Hapana,
kwa kuwa na mimi sitakuruhusu. Nitataka ulale ili uamke na nguvu yakufanya kazi
vizuri. Sikuwa hata na mpango wa kusema haya sasahivi, lakini umenifanya niseme,
Jema. Na sitaki kuchelewa nikaja kujuta. Kama utaona nitaweza kuanza na wewe
huko unakoanza, tafadhali anza na mimi na nakukaribisha pia uendelee na mimi
kama hivi leo kwenye usiku huu.” “Nashukuru James. Asante sana.”
“Kwamba upo
tayari?” Akauliza kutaka na yeye uhakika. “Sina sababu ya
kujichelewesha zaidi, James. Na siwezi kukataa hiyo bahati! Isingekuwa
wewe pengine na leo ningekesha kwa mawazo nikijua Mungu amenisahau. Sina
bahati. Nina mkosi kama wa mama zangu, nakushindwa tena kula. Wewe umekua
msaada Mungu alionitumia. Wala sitafikiria mara mbili. Wewe ukiwa na nafasi nitashukuru
ukinisindikiza popote utakapoweza, na kama unaniruhusu kuomba ushauri, basi
naomba nitumie hekima yako kuanza upya. Ulipomfikisha Nanaa sio pabaya. Na mimi
naomba unishike mkono.”
“Sasa hapo unakaribia
kuharibu tena!” “Kwa nini tena!?” Jema akawa hajaelewa
kabisa. “Nanaa nilimfikisha kwa Geb, unataka na wewe…” Jema
alicheka sana. “Yaani niishie kuitwa shemeji kila siku!?” Jema
alicheka mpaka machozi. “Unataka kuninyima nini tena Jema, mama?” Jema
alicheka, hakutarajia. “Mimi sijakupatia mwenzako.” “Na ibaki hivyohivyo.” “Asipatikane
mwingine?” “Hapana. Sitaki.” “Basi hakuna kupatikana mwingine.” “Hapo sawa.”
“Umefurahi sasa?” “Nani asiyependwa kusindikizwa maishani?” “Hakuna.” Jema
akajibu akicheka.
Hakujua
kama James ni mzungumzaji hivyo. Akawa naye kwenye simu mpaka alipofika na yeye
kwake. “Sasa ulale Jema. Kesho kanisani. Nakushukuru saaaana kuwa na mimi
safarini.” “Karibu na asante kwa wakati mzuri.” “Ni hivyo itakuwa ni kama
nakuigilizia. Basi bwana.” “Lakini kama si kuigilizia?” Jema
akauliza akicheka. “Na mimi ningesema asante kwa wakati mzuri.” “Kweli huko ni
kuigilizia.” “Kama si kuigilizia?” “Ningesema karibu.”
Wakacheka na kuagana wote wakiwa na furaha sana.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
James
akakutana na Jema mbaye hata hakumtegemea! Ile furaha Kumu aliyosema alikuwa
akiipata kuwa na Naya masikioni, usiku wote, wote wawili usiku huo wakaelewa ni
nini Kumu alikuwa akimaanisha. Ile kuwa pamoja ikawatoa upweke na kujengwa
ahadi ambazo kwa mara ya kwanza hisia zilizokuwa zikitembea usiku huo, zikamfanya
James kwa mara ya kwanza kutoa ahadi kwa Jema aliyekuwa akimlilia Mungu na
kusubiri kwa uaminifu. Jema ambaye alishamparamia Joshua akidhani ni wake,
kumbe sio. Alipompiga stop, Jema hakuwa na makuu. Akashukuru Mungu na kujiweka
pembeni akimtumikia huyo Joshua hata alipokuwa akimtuma
kwa Naya. Alifanya bila kinyongo akimwambia Mungu anawekeza
kwake, asiwahi kusahau kuja kumlipa kabla ya kufa kwake. Leo anafurahishwa
na James! Mkaka anayependa maendeleo! Alifurahi Jema, akabaki akimshukuru Mungu
na kufurahia kusubiri kwake.
Kwa Bale.
Wakati
usiku huo ukiendelea kwa furaha pande hii, huku kwa Bale aliyekuwa amefanikiwa
sana kwa mali zake na za Malon, ambazo hazikuwa na maswali na yeyote kwani
hakuna aliyekuwa akijua Malon anamiliki nini na kipo wapi. Akajikusanyia mpaka
akaridhika na nyumba ya Kunduchi akajimilikisha. Akaunti zikawa zinasoma vizuri
sana. Akiwa amelala akasikia kwa wazi kabisa. “Nikiwa nipo hai au
nimekufa, usiwahi kuuza binti yangu!” Bale alishituka sana.
Ilikuwa sauti ya baba yake masikioni kwake ila kwa wazi kabisa mpaka akatoka
usingizini.
Alipofungua
macho, akamuona Malon anatoka hapo chumbani kwake. Bale alishituka zaidi mpaka
akaruka kitandani. Aliyemuongelesha ni baba yake. Aliyemuona akitoka hapo chumbani
ni Malon.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Mziki Ndio Kwanzaaaa Unaanza. Usipitwe.
0 Comments:
Post a Comment