“Nisaidie
mama yangu. Huo mlolongo ni mrefu mno. Mimi sitaki makuu. Kuna aina ya harusi
aliyokuwa akiiwaza Jema. Anasema alikuwa akiiwaza tokea mtoto. Hiyo ndiyo naona
ni ya msingi na pengine aina hiyo ya gauni ndio nitaruhusu inicheleweshe, ila
hivyo vitu vingine naomba unisaidie tufupishe mama yangu.” “Kama nini James
mwanangu?” “Nisaidie tuvuke vyote, twende kwenye mahari moja kwa moja. Wakati
tukisubiri gauni la Jema, mnaweza kumfanyia mambo yote. Gauni likiwa tayari tu,
tunafunga ndoa.” Mama Jema akacheka.
“Kwani huyo
Jema anataka gauni gani?” James akacheka. “Naomba umuulize yeye mwenyewe, ila nafikiri
inabidi kutengenezwa. Anasema alikuwa nalo akilini tokea mtoto mdogo, akitamani
siku akiolewa ndio avae hilo. Na mimi nilipata hiyo bahati ya kulijua kutoka
kwenye mazungumzo yake tu. Sijamwambia kwamba nitahangaika mpaka alipate maana
ni kama amekata tamaa ya kulipata, ila hapa kazini kuna mama ameniambia anamfahamu
mtu anayetengeneza magauni mazuri sana ya harusi, anauhakika akikutana na Jema
mwenyewe akamuelekeza, ataweza kumtengenezea japo inaweza kuchukua muda. Kwa
hiyo nataka jumamosi akitoka kazini, nimkutanishe na huyo fundi.” “James
unampenda Jema!” Ikabidi tu mama mtu aseme akisikika kufurahia.
“Sana mama.
Ni msichana aliyetulia, halafu nimejikuta anavigezo vyote vya ninayetaka awe
mke wangu. Si mgomvi kabisa, kitu kinachonifanya niwe na uhakika wa pumziko
hapa duniani.” “Basi kumbe umemjua. Jema hapendi ugomvi na ndicho kilichomtoa
hata hapa nyumbani. Kelele zangu na Jelini zilimshinda kabisa. Hawezi ugomvi
mpaka utamuhurumia.” “Nimemgundua. Nisaidie mimi ndio nimuoe mama yangu. Sitaki kuja
kuzidiwa mahesabu.” Mama Jema alicheka sana.
“Hawakawii!”
“Hapa mjini hakuna waoaji wa hivyo James mwanangu. Wachezeaji watupu. Ndio
maana unamuona mpaka leo huyo Jema yupo. Ila usiwe na wasiwasi. Acha nizungumze
na bibi yake pamoja na mama zake, niwaambie hivyo.” “Asante mama yangu.” Akakata
simu na kubaki akifikiria.
Mama ni Mama.
Akajua
kwa hakika alimpunja mama yake mengi sana tokea anakua. Ndoto za mtoto wa kiume
alizokuwa nazo akiwa anamtafuta James, zilikuja kuisha pale James alipoweka
msimamo kwa Nanaa. Kukaanza kuvutana kati yao. Akajiona anajukumu katika hili,
kumtaarifu kuwa amepata mchumba. Akaamua kumpigia simu mama yake. “Shikamoo
mama.” “Marahaba. Vipi huko?” “Nimepata mchumba naoa.” James
akaongea hivyo moja kwa moja. Akamsikia mama yake akicheka. “Unacheka
nini sasa?” Akamuuliza mama yake na yeye akicheka. “Nimefurahi.
Mlete basi nimsalimie.” “Ili uanze kumkagua?” “Kwani namuoa mimi? Hata akiwa
chongo, ni wako. Tutapapasana hivyohivyo.” James akacheka sana. “Huna
neno?” “Hata nikiwa nalo, ni wako. Unaishi naye wewe. Mimi nataka kumuona tu
mkwe wangu, tufahamiane, basi.” “Kama ndio hivyo basi nitamleta.” “Lini?
Maana si unishitukize, nishindwe hata kumpikia!” James akashangaa sana.
“Sasa mbona
hata huulizi kabila!?” “Litanisaidia nini wewe? Niambe lini unamleta.” Ikawa
tofauti na alivyotarajia. Ikamshusha kabisa James aliyekuwa amejiandaa vita kwa
upande wa mama yake. “Wewe ndio upo busy mama. Niambie wewe.” “Mbele ya mkwe. Hata
ukitaka leo, nitawahi nyumbani nipaweke sawa, nipike, aje ajue nyumbani.” James
alifurahi sana. “Nashukuru mama yangu. Basi naomba iwe kesho ili leo nimuandae.”
“Sasa sio upotee James, bwana! Maana umeshaniamsha morari!” “Kweli mama?” “Sana
James! Dada zako wote hakuna aliyeolewa. Wewe naye muendeleza ukoo ukawa kimya!
Wewe unafikiri najisikiaje? Angalau na mimi nitaonekana nina uzazi jamani! Sio
uzazi wangu unaishia kwenu tu. Kama mwenye laana!” “Basi nitamleta mama yangu.
Hapo umenipa moyo. Kesho.” Mpaka James akamshangaa jinsi mama yake alivyofurahi
na kujutia kumuogopesha Jema juu ya mama yake.
Wema Hauozi.
James
akabaki akiwaza lakini na tumaini jipya. Danny akamfuata. “Kwema kaka?” “Kwema
Danny. Nataka kuoa.” Danny akacheka sana. Alikuja kuulizia aliyoyaona
alipowaona kina Magesa, hakutarajia kusikia maswala ya James kuoa. “Jamesss!”
“Nimepata msicha aisee!” “Hongera sana. Lini?” “Hata pete bado sijamvalisha. Na
sijui namvalishia wapi?” “Pete yenyewe unayo?” “Sina aisee.” “Twende
tukaisake.” “Acha masihara Danny! Kwamba kweli unanisindikiza?!” “Wewe! Huna
utakaloniomba nikasema hapana James.” Danny akacheka na kutingisha
kichwa.
“Labda
iwe roho yangu, napo ni kwakuwa sina jinsi ya kukupa. Ila wewe! Hata ukiomba
mshahara wangu wa mwezi mzima. Wote, nakupa.” James alicheka sana. “Sikutanii
James. Ulinitizama nikiwa sitizamiki kwa dhambi chafu, mbaya ambayo
nilisababisha mwenyewe kwa ujinga wangu. Najua hata malaika mbinguni
walishindwa kuniangalia ila wewe.” “Acha hizo Danny!” “Ooh! Najua nilichokifanya
James. Najua. Niliua watoto wangu vibaya sana. Ni kama niliua wote.
Nasikia Fili hanitaki kabisa. Ni kama siku ile nilipoua wadogo zake, ni
kama nilimuua na yeye. Niliua ndoa yangu mimi mwenyewe. Nikiwa kwenye ile hali,
sijui pakwenda maana hata wauguzi wenyewe walikuwa wakiingia pale si kunisaidia
ila kuniona kiumbe kikatili, kibaya kilichokuwa kikisemwa mitandaoni. Lakini
James, hata mimi ulinishangaza aisee! Mimi mwenyewe sikujua uliwezaje!” Danny
akatingisha kichwa kwa masikitiko.
“Miezi
miwili upo na mimi hospitalini bila kuchoka. Ukiniosha kama mtoto mdogo na
kuhakikisha nakula! Bila kulalamika wala kunisimanga! Umenitunzia kazi yangu
hapa, ukiandika barua kila mahali ukihakikisha sifukuzwi kazi! Nimetoka
hospitalini bado ukahakikisha sikosi mazoezini ili kuweza kurudi kutembea tena!
Haya, nimekuja kugundulika nimeathirika, pia hujawahi hata kuniangalia
tofauti ila kuuliza dawa sahihi kwangu na kuhakikisha nakula vizuri! Upo na
mimi nikiwa nimepoteza kila mtu! Hakika twende tukatafute pete na wewe uoe.”
James akacheka sana. “Unalipa fadhila” “Wala sitaweza.” Wakatoka wakicheka.
Chanda Chema, Huvikwa Pete.
“Nipe
basi wazo jinsi ya kumsuprise. Maana yupo busy mno na kazi.” Wakaendelea
kuongea wakiwa njiani wakienda kutafuta pete. “Cha kwanza jua ni nini anapenda.
Maeneo yepi yanamfurahisha.” James akatulia akifikiria. “Aisee muda mwingi
anakua kazini.” “Kanisani je?” “Ndio tumeanza kwenda naye kanisa jipya. Sina
ninayemfahamu huko.” “Duuuh! Hapo sasa kazi ipo.” “Kwani nikimvalisha kazini
kwao sio sawa?” Danny akatulia akifikiria.
“Wewe
unayafahamu mazingira ya kazini kwao?” James akatulia akitafakari. Hakutaka
kumuhusisha Kumu. Lakini akawa hana namna. “Yupo mtu anayeweza kunisaidia
kuandaa mazingira. Japo ni bosi wake, na yeye anamuogopa sana.” “Mbona humtaji
jina huyo msichana mwenyewe?” James akacheka.
“Ni
nani?” “Nahisi na wewe utakuwa unamfahamu.” Danny akatulia akijaribu kufikiria
katika watu anaowafahamu yeye pamoja na James, halafu aolewe na James! Akafika
mwisho. “Acha kunipa wakati mgumu bwana. Niambie ni nani?” “Unamkumbuka yule
msichana wa Coca, yule aliyekuwa..” “Jema!?” James akadakia kwa mshituko. “Wewe
umemfahamia wapi Jema!?” Danny akacheka sana.
“Kasa
alikuwa akimmezea mate kuliko nitakavyokwambia. Kuna kipindi Jema alikuwa
akishugulikia mambo ya kampuni yao, akitaka aunganishwe na mtu wa Utawala anayekusika
na jengo zima, ili azungumze nao waje wafanye biashara hapa. Akakutana na Lela,
naye Lela akamuelekeza kwako, ndio Kasa akamlalamikia Lela eti kwa nini
hakumuelekeza kwake, yeye anamtaka. Ndio Lela akamwambia hata angemleta kwake,
Jema sio type yake.” “Haiwezekani! Hamjui Kasa nini?” “Alimfanyia kusudi ili
kumkera tu. Anasemaga Kasa anaringa sana. Si unajua ile sema yake. Yupo hapa kazini,
lakini si kwa shida kama sisi wengine. Kwao mamilionea. Sasa hicho kinamkera
sana Lela. Halafu anamsema Kasa anajidai matawi ya juu sana. Kwahiyo alimfanyia
kusudi, kumdharaulisha tu. Sasa bwana Kasa amemmaindi Lela vibaya sana. Hataki
hata kumuongelesha, akipita hamsalimii.”
“Sasa
siku moja mimi nikamuona Kasa anagawa vinywaji pale mbele kwa wale wasichana wa
pale mapokezi wote kasoro kwa Lela. Nikamuuliza kulikoni?” James akacheka
akitingisha kichwa. “Kasa! Sasa akakwambia nini?” “Si ndio akanisimulia kisa
kizima. Mimi nikawa nacheka tu. Ndio na Lela si unajua anavyopenda kunitania
mimi mkwewe? Akaniita na kunisimulia kuwa amemkomoa makusudi. Na ashamwambia
na Jema kuwa Kasa tapeli, asiwahi kumsikiliza.” “Haiwezekani!” “Nakwambia
wanabifu la waziwazi. Na mpaka leo namaanisha leo hii, Kasa amemnunia Lela
sababu ya Jema. Kumbe ndio unataka kumuoa!? Sasa amekubali?” “Acha maswali ya
ajabu. Ningeenda vipi kutafuta pete kama hajakubali?” Danny akacheka sana. “Mpigie
huyo bosi wake basi kuweka mazingira.” Danny akaweka ushawishi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
James
akafikiria na kuamua kumpigia Kumu. Akapokea kwa haraka tu. “Umepotelea
wapi wewe?” “Nipo. Vipi Naya?” “Namshukuru Mungu anaendelea vizuri aisee.
Kwema?” “Leo nataka kumchumbia Jema.” Kumu hakutegemea. “Upo Kumu?” “Subiri
kwanza James, wewe ndiye uliyekuwa ukileta maua na zawadi kwa Jema?” “Sijui
kama kuna mwingine, ila na mimi nimekuwa nikileta.” Joshua
akajikuta akicheka. “Nimekukubali James.” “Kwa nini kaka?” “Aisee mimi mpaka nikawa
najiambia, huyu mtu amekusudia kwelikweli. Ila kwa kuwa ni wewe, furaha yangu
imeongezeka. Jema is like a little sis God gave to me. Anastahili
mwanaume kama wewe. Na hongera sana.” “Nashukuru Joshua. Sasa nataka kumchumbia
leo. Itawezekana au anamajukumu mazito?” Akaomba kiustarabu.
“Kwa Jema!
Aisee kila kitu kitasimama kwa muda ili kufanikisha hili. Wewe niambie tu ni
saa ngapi unataka kuja, ili nikutayarishie mazingira mazuri.” “Aisee
nakushukuru Kumu.” “Lazima aisee. Unakumbuka jinsi alivyojitoa kwangu na Naya?” James
akacheka tu. “Aisee sina jinsi ya kumlipa ila kwa njia hii. Unaye mpiga picha
sasa?” “Sijafikiria umbali huo.” “Basi acha nimpange jamaa aliyenisaidia kwenye
shuguli zangu zote. Amenitengenezea kumbukumbu nzuri sana. Utamkuta
akikusubiria hapa.” Wawili hao wakapanga mipango vizuri, James hakutegemea uungwaji
mkono wa kiasi hicho. Juhudi ya Jema kazini, na kujinyenyekeza kwa bosi wake, siku
hiyo ikamlipa. “Aisee nakushukuru Kumu.” “Kwa Jema, wewe tamka tu kaka, mimi nitakimbia.”
Wakacheka na kuagana Joshua asiamini kama ni James kwa Jema!
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
James
alikwenda kulekule alikonunua Joshua pete ya Naya. “Hapa ni garama kaka!” Danny
akamtahadharisha. “Kwa Jema, acha nitoe tu.” Danny alicheka sana. “James
umependa!” “Aisee nimependa. Nampenda Jema. Sana. Ni watofauti na vile
anavyoonekana. Amebeba unyenyekevu fulani hivi! Aisee namtaka yule mtoto kwa
garama yeyote ile. Halafu hana makuu!” “Mbona lakini anaonekana viwango vizito
sana!?” “Na mimi nilishangaa sana baada ya kumfahamu. Unaweza kumuonea
kirahisi sana. Ule ujasiri wake nimegundua ni kwa vile huyu Kumu, bosi wake, alivyo
muamini sana na kumuonyesha anaweza, ndio ikamfungua na kumpa
ujasiri wa kufanya kama vile anavyoonekana kwetu. Lakini ukiwa mpuuzi
tu, unaweza kumdhulumu kirahisi sana. Ana moyo mnyenyekevu na anaimani kubwa
sana. Nampenda Jema, aisee. Acha nimuoe roho yangu itulie.” Danny akamsikiliza,
wakashuka garini lakini Danny akawa kama amepotelea mawazoni.
James
alimuona ila akamuacha tu. Akajua lazima atakuwa na majuto makubwa sana. Danny
anaishi sasahivi kama mseja tu, tena ameathirika. Wakati alishamiliki mke wa
maana na watoto watatu! Akaweka heshima kwenye jamii kama mwanaume mwenye
familia bora! Amebakiwa na kumbukumbu mbaya za vifo vya wanae. Ila anajua kama
sasahivi Grace ni kama alilipwa na Mungu. Amerudisha idadi ya watoto watatu
vilevile, akaongezewa na wakike. Akatulia kimya.
James
alishawahi kumuuliza Jema anavaa pete kwa saizi gani, Jema akamjibu. Lakini
jinsi alivyomuuliza na kumjibu, hakujua James alikuwa na maana yake, maana
aliichomekea tu katikati ya stori. Basi siku hiyo akakutana na aina za pete
nzuri hata Danny mwenyewe akazikubali. Akalipia ndipo akampigia simu Joshua.
Wakapanga tena vizuri, na Joshua naye akamwambia anajipanga kumfanyia Jema surprise
nzuri.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Wakakata
simu Joshua akatumia watu wote wa kitengo chake kasoro Jema kuwa wanataka
kumfanyia Jema surprise, baada ya dakika 45, kila mtu atoke ofisini
wawepo eneo la nje tu, lakini wajibaraguze, asijue. Akawaambia na watu wengine
wa vitengo vingine ila sababu hakutoa akijua wapo wasio na kifua wanaweza
kuharibu kwa kumwambia Jema mwenyewe. Kwa hiyo akabakiwa na sababu yeye
mwenyewe. Ila wengine wakishangaa na kuulizana Kumu anataka kumfanyia Jema surprise
gani! Ikabakia kila mtu anahamu yakuona hiyo surprise.
Muda
ulipofika, James akawasili na kuandikisha jina getini akisema ni mgeni wa
Joshua Kumu, na Kumu akaruhusu aingie. Akampigia simu Jema na kumwambia wotoke
waende kitengo cha Uzalishaji, kuna mambo anataka kuweka sawa. Haraka sana Jema
akachukua Tablet yake na kutoka kwa kasi kama kawaida yake na kiatu chake cha
juu. Kumu ametangulia mbele yeye
anafuata nyuma kwa haraka asimchelewe. Wakatoka mpaka nje ya jengo la kitengo
cha Masoko sehemu ambayo aliomba James apelekwe. Walipofika, Kumu akajidai amepokea
simu, anazungumza. Ikabidi Jema kumpita ili kumpa faragha kwenye mazungumzo
yake.
Mara akamuona James. Kitu kikaruka moyoni kwa
Jema na kushindwa kujizuia. Akaruka kwa furaha na kumkimbilia akiwa amesahau kuwa,
bosi wake yupo nyuma yake. Kumu! “James!”
Akamkumbatia kwa furaha zote. “Unafanya nini huku!? Au umemfuata Kumu?”
“Nimekufuata wewe.” Jema akakunja uso akicheka. “Mwenzio nina kazi, James. Nipo
katikati ya…” Akashangaa James anapiga goti, akawa hajaelewa kabisa. Maana
mawazo ya Jema hayakuwa kwenye kuchumbiwa kwa kuvishwa pete, ila kulipiwa
mahari. Hicho kipengele cha kuvalishwa pete, akawa kama amekisahau kabisa.
“We James!?” Akatoa pete akiwa amepiga goti kwa
mguu mmoja, mbele yake. “Nimekuja kukuchumbia Jema. Nataka kukuoa, uwe mke
wangu!” Jema alishangaa sana mpaka akajifunika uso na tablet aliyokuwa
ameishika. Kumu akaikimbilia na kuichukua, akicheka. Jema akashangaa sana huku
machozi yakimtoka. “Kubali Jema wangu tuoane.” “Mimi nakupenda James!” James
akamvuta mkono na kumvalisha pete. Jema akashangaa watu wanapiga makofi.
Akamwangalia James na Kumu huku bado machozi yakimtoka, James akamalizia
kumvalisha pete.
“Umeipenda?” “Mimi sikutegemea James!
Asante.” James akamvuta, akamkumbatia na kupata busu palepale juani, watu
wakazidi kupiga makofi na miluzi. Na James hakumuachia akabaki akinyonya midomo
yake watu wakizidi kushangilia. “Naye James hana kiasi bwana! Mpaka tujute!” Danny
akafanya James na Jema kuachiana na kuanza kucheka. “Nimefurahi sana.” Jema
akaongeza asiamini. “Tuone Jema.” Kumu akamsogelea, Jema akampa mkono. Joshua
akacheka na kutingisha kichwa. “Vipi?” “Heshima yako.” Wakazidi kucheka ndipo
watu wengine wakampongeza na kuondoka taratibu maana Kumu alikuwa hapo, na ni
muda wa kazi.
“Mimi nilijua tunakwenda Uzalishaji!” “Hapa ndio
Uzalishaji kwenyewe. Vipi Jema wewe! Au uzalishaji ni lazima uwe wa vinywaji
tu?” Wakazidi kucheka. “Nimefurahi sana. Hata sijui niseme nini! Natamani..”
“Kurukaruka?” Kumu akamuuliza, Jema akajifunika kwa aibu. “Ukimletea zawadi
huyu, mimi na Fina tunakoma. Anajifungia ofisini kwake halafu anaanza
kurukaruka kwa shangwe.” Joshua akaongeza. “Mimi sikujua kama napiga kelele.” Wakazidi kucheka.
“Hongereni sana.” “Tunashukuru aisee.” “Sasa kusherehekea ni wapi?” Hapo James
akakwama.
“Aisee sina mipango endelevu. Yaani nilikuwa
napanga nikienda. Nimekaa ofisini, nikammisi Jema wangu, nikasema bora
nimvalishe pete tu. Danny akanikuta nawaza, nikamwambia wazo langu, na yeye akaniambia
tutoke tukasake pete. Ndipo na wewe ukanifanikishia hapa. Acha mengine niwaze
taratibu.” “Basi acha mimi niwaandalie chakula cha jioni, niwakaribishe
kwangu.” James akaonekana kusita. Joshua asielewe.
“Tunaweza kuzungumza pembeni kidogo?” Joshua
akakubali. Wakajitenga wao wawili tu. “Nashukuru sana Kumu, lakini najua aina
ya watu unaowafikiria kwenye hicho chakula utakachokiandaa, kwa sasa nimeamua
kumuweka Jema mbali nao kidogo.” “Hakika sijaelewa James.” “Kama utaniruhusu
nisiende kwa undani, nitashukuru. Ila kwa sasa sitaki Jema awe karibu na kina
Magesa. Nilimpeleka nyumbani kwao jana, haikuishia vizuri. Sitaki kumchanganya
Jema sasahivi.” “Japokuwa sijaelewa, lakini pia tunaweza kukuandalia chakula
wewe na Jema tu. Mkaja kula pamoja na mke wangu. Tukawa wanne tu. Hatuna sababu
ya kualika watu wengine.” “Ni sawa tukimkaribisha Danny, mama Jema pamoja na
mdogo wake?” “Bila shaka. Nipe idadi tu, kisha niweke mazingira mazuri
nyumbani.”
“Haitakuwa usumbufu kwa Naya?” “Naona kama
itamsaidia kupata kitu chakufanya mbali na kujifikiria yeye mwenyewe.”
“Nashukuru kaka. Basi acha nizungumze na mama Jema nione kama atakubali kuja.
Ila nikuombe jambo gumu kidogo.” “Karibu.” “Naomba na Jema naye apate nafasi
kama uliyompa Naya. Aandae nyumbani kwangu.” Hapo Joshua akasita. “Tafadhali
Kumu.” “Basi nitakuja na Naya mimi mwenyewe. Huyo bado simuamini na mtu aisee.
Nalinda kama mboni ya jicho langu. Mimi na Jema leo tutafunga ofisi
mapema. Nitakwenda kumchukua Naya na kuja naye kwako. Ila mpishi nitamwambia
akimaliza tu kupika, alete chakula nyumbani kwako. Nafikiri tunazo sahani
nyingi tu, tunaweza kumpa azilete pamoja na chakula na kuandaa mazingira mazuri.”
“Hapo utakuwa umenisaidia sana.” Wakazungumza kidogo, Kumu yeye akarudi
ofisini.
“Acha nirudi ndani James. Tuongee kwenye simu.
Mimi ndio nashika ratiba yake yote. Hana anachokifanya bila mimi.” James
akambusu. Jema akacheka. “Sasa leo bosi wako amesema atakuruhusu mapema ili
ukawaandalie wageni wetu chakula. Waje washukuru Mungu pamoja na sisi kwa hatua
yetu ya kwanza kwenye maisha.” Mpaka hapo akawa amemchanganya Jema. “Tunaandaa
tafrija fupi nyumbani kwetu Salasala. Mimi nitaalika watu, nitazungumza na mama
Jema. Nakumuomba yeye na mama James ili waje waungane nasi. Nitawaambia ni
gafla, lakini hatukuwa na jinsi. Itakuwa vizuri pia wapafahamu nyumbani.” Jema
alifurahi sana.
“Uwahi mama, ili kupokea wageni na kuwakarimu.”
Jema akazidi kucheka na machozi. “Acha kulia sasa. Njoo.” Danny akawapisha.
Akamshika mkono na kumsogeza kivulini. “Umeelewa lakini?” “Nahisi.” James
akacheka. “Kumu atakuruhusu mapema. Kimbia nyumbani kwako. Chukua nguo, funguo
hizi hapa za kwetu Salasala.” Jema akawa kama haamini. Akakabidhiwa fungua
aliyokuwa amepewa Nanaa na kupokonywa asubuhi hiyo. Akabaki akiiangalia na
kucheka huku akifuta machozi.
“Mpishi ataleta vyakula na sahani. Msaidiane
jinsi ya kuandaa. Kumu atakuja na Naya kukusaidia baadaye. Na watu wote
nitawaambia wafike nyumbani saa moja usiku. Si umeelewa.” “Nimefurahi
James! Hujui tu.” James akamsogelea zaidi na kupata busu la muda tu kisha
akamuachia. “Wahi kazini tusiharibu na usilie bwana. Mimi nilitaka ufurahi.” “Nimefurahi
James, siamini! Sikutegemea kuvalishwa pete kwa namna hii! Sikutegemea hata
kidogo. Bado siamini!” James akacheka. “Acha nikatulie na kuangalia pete yangu
vizuri. Nzuri sana. Kuliko hata ya Naya!” James akazidi kucheka na
kufurahia furaha aliyoiweka kwa Jema. “Nakupenda Jema.” Jema akambusu kidogo. “Asante
James. Asante kwa kila kitu. Na sitachelewa. Nitajitahidi kuwaandalia wageni
wetu vizuri.” “Hayo ndio maneno. Kuna mtu unataka kumkaribisha kwenye hiyo
tafrija ili tuweke idadi ya kutosha ya chakula?” “Sasahivi akili imevurugika,
sijui tena. Acha nikatulie nitakujulisha. Lakini kwa hapa kazini sina ushoga na
mtu wakusema kumkaribisha nyumbani. Labda ndugu.” “Haya nenda usichelewe. Tuwe
na kiasi.” Jema akarudi ofisini kwa haraka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Zungu la
nguvu!” Fina akamtania mara alipoingia. “Nimefurahi Fina! Sikutegemea! Wewe
ulijuaje?” Fina akamvutia ofisini kwake na kufunga mlango. “Nini?” “Bosi wako
huyo. Kumu ndio kaandaa watu wote waje washuhudie ukivalishwa pete.”
“Haiwezekani Fina!” “Kweli. Nafikiri walipanga na huyo mzungu wako.” “Fina mimi
napendwa!” Fina alicheka mpaka akakaa kwenye kiti. “Unapendwa?” “Sana. Hivi
hapa na funguo za nyumba nimepewa. Nimeambiwa nikaandalie wageni wetu, kwetu.”
“Jema huyo!” “Napendwa mwenzio. Na nina kwangu na mpenzi wangu!” “Hongera.”
“Asante dada. Nimefurahi sana.” Simu ya mezani kwa Fina ikaanza kuita. “Kumu
huyo.” Akatoka mbio.
Kisha
akasikia anaitwa. Akatoka kuelekea ofisini kwa Kumu. “Nashukuru bosi wangu.
Asante Kumu.” “Hongera sana Jema. Sasa kabla hujaanza kunichanganyia ratiba kwa
furaha, naona leo uchukue off. Nenda kajiandae na tafrija jioni.” “Na wewe?!
Bado mapema sana, acha nifanye kazi hata angalau ifike mchana, nisogeze kazi
usilemewe!” Jema hakuamini, akaanza kubabaika yeye mwenyewe. “Nitumie ratiba
yangu yote. Na majukumu yako, mimi nitafanya.” Jema akajishangaa anaanza kulia
mbele ya Kumu.
“Sasa
unalia nini?” “Mimi sikutegemea!” “Wewe ulinibeba sana miezi
michache iliyopita, Jema. Ni hivyo huelewi tu. Nilihitaji mtu kama wewe, na
wewe ukakubali Mungu kukutumia kwenye kipindi nilichohitaji sana msaada. Sina
jinsi ya kukulipa ila kukusaidia katika hili. Nilimwambia hata James, wewe umekuwa
kama mdogo wangu, niliyepewa na Mungu.” Jema hakutegemea kusikia hivyo kutoka
kwa mtu kama Kumu kumwambia hivyo. “Nenda kajiandae na siku yako. Ni muhimu
sana, najua utahitaji.” “Nashukuru. Nimefurahi sana.” Kumu akacheka na kurudisha
macho kwenye kompyuta yake bila ya kujibu. Jema akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hatimaye Jema Naye Amechumbiwa kwa Staili ambayo hakutegemea!
Mambo yanaendelea.
Nini kitaendelea mbeleni?
0 Comments:
Post a Comment