Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 1. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 2 - SEHEMU YA 1.

Jema akapatwa na ububu wa gafla. Akashindwa chakujibu. “Taratibu Jema! Maana..” “Jamani, inatosha.” Ikasikika sauti ya James. “Kosa si la Jema, nafikiri mimi ndiye niliyekosea kumueleza vile nilivyopafahamu kwa kina Magesa, vile vya zamani. Sikujua kama taratibu humu zimebadilika.” James akasogea mpaka pale aliposimama Nanaa, Jema na Magesa. “Samahanini sana jamani. Twende mama watoto wangu.” James akamshika mkono Jema pale alipokuwa amesimama.

“Msiondoke bila kula James!” Mama G akamuwahi. “Kama ni chakula tu, tumepita magenge kibao huko barabarani mpaka kufika hapa. Kilichotuleta hapa, ni hiki alichokatazwa Jema. Kufahamiana kwa karibu, kwa kuwa namuoa Jema. Tena namuoa siku za karibuni sana. Sasa kwa kuwa nilijua nyinyi wote mnamfahamu, ilikuwa ni kiasi cha kuendelea tu kujenga ukaribu zaidi, sikuwa na shaka. Sasa kusikia tena mnataka tuanze mwanzo! Tena taratibu! HAPANA kwakweli. Nyinyi anzeni kwa taratibu hizo zenu mpya lakini si kwa Jema huyu, na si kwa kumfoka kama mtoto mdogo.” Hapo James akabadili gia.

“Mnamfoka mpenzi wangu mbele za watoto halafu eti mnatudanganyishia chakula! Kweli jamani au mmemdharau mpenzi wangu?” “Acha hasira James!” “Ingekuwa ni wewe mkeo amefanyiwa hivyo, ungemrudisha sebuleni, asubiri chakula? Eti Geb? Kwa njaa gani jamani ambayo mnatuona nayo?” Kimya. “Acha sisi tukaendelee na ya kwetu.” James akamchukulia pochi yake. “Twende zetu Jema wangu.” Akamshika mkono. Wakatoka.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Samahani James. Nia ilikuwa nikusaidia tu. Nilijiona nimebaki pale sebuleni peke yangu. Sikutaka kutayarishiwa pale kama mgeni rasmi, wakati tulishakutana nao kwa Kumu zaidi ya mara moja. Tena tukafahamiana na kufanya nao kazi pamoja, kwa karibu sana mpaka mwisho wa harusi ya Kumu. Nikajua tumeshafahamiana. Leo nikaona nisaidie nisijifanye mgeni. Sikukusudia kuharibu, tafadhali nisamehe. Sio kiherehere wala ujasiri wa kupitiliza kwenye nyumba za watu.” Akakumbuka hayo maneno yatamuuma zaidi kwa kuwa ndiyo aliyoachwa nayo na Temu.

 “Usingefanya hivyo ndio ningekushangaa.” Wakamsikia James akimjibu. “Mimi ndiye nimekosea kukuelekeza tokea mwanzo. Ila ni kwa vile nilivyomfahamu huyu mama na wanae. Alitupokea tukiwa vijana wadogo hatuna kitu wala yeye hana kitu ila upendo tu kwetu. Akiwa na chumba kimoja alitufungulia milango ya nyumbani kwake, pakawa kwetu bila kujali kabila wala haiba zetu. Nilipokwambia huyu mama ni kama mama yangu wa pili, sikukudanganya Jema.” Wakamsikia akimtuliza kwa Upendo.

“Kuna kipindi niliugua, akaniuguza kama vile mimi ni huyo Geb mwanae. Nikiwa na gumu lakutaka ushauri, ni mtu wangu wa karibu na haachi kuniombea mimi kama mwanae wakumzaa. Nilikwambia nakuamini naye kuliko hata mama yangu mzazi, ni kweli. Kwa sababu ya vile nilivyoishi naye mimi. Kwa hakika kosa ni langu Jema. Mimi ndio unisamehe, nilikosea mpenzi wangu, na naomba usilie.” “Najihisi nimeharibu sana. Hakika sikukusudia.” “Nakuhakikishia hujaharibu, Jema. Ingia kwenye gari, tusisimame juani. Panda twende.” Wakasikia kilio cha Jema kidogo, kisha mlango ukafunguliwa na kufungwa.

Nyongo, Mkalia Ini.

Baada ya muda James akarudi. “Nanaa!” Wakamsikia akimuita bila kuwaongelesha wale waliokuwepo pale sebuleni. Nanaa akatoka, alikuwa jikoni, Geb na mama yake sebuleni, kimya. “Isiwahi kutokea tena katika maisha yako, ukampazia sauti Jema. Iwe mwanzo na mwisho. Huruhusiwi kumfoka Jema. Leo naishia hapa kwakuwa imetokea nyumbani kwenu, ila nitajitahidi kumuweka mbali na nyinyi ili hiki kilichotokea leo, kisiwahi kurudiwa hata kwa kusimuliwa. Iwe mwanzo na mwisho wako.”

“Kwa vyovyote ulivyomuona na kumfikiria, mpe heshima kama unayowapa watu wengine baki. Huko itakapotokea unakutana naye, akatenda jambo ambalo hujapenda, ondoka hiyo sehemu, au zungumza naye kwa heshima. Umenielewa?” “Ndiyo na …” “Na ingetokea kwa mtu mwingine, ningeelewa. Ila WEWE!” James akamkatisha akimshangaa sana. “Hakika SIKUTEGEMEA Nanaa! Watu hubadilika, lakini isingekuwa WEWE!” James akaondoka kwa hasira. Geb na mama yake kimya. Kimeumana ndugu.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Huku kwa Jema akawa kama amepata mshituko. Alichokitarajia kwa hamasa, hakijawa hata nusu yake! Nanaa aliyemuona nyumbani kwa Kumu siye aliyekutana naye kwenye jumba lake. Alimshusha, mpaka Jema akajiona ni mdogo asiyefaa. Akatulia kwenye gari mpaka akahisi baridi, kwa mshituko. James akarudi garini. “Unataka kwenda kula wapi?” “Naomba nirudishe tu kwangu James.” “Hapana. Hatuwezi kufanya hivyo Jema! Leo ni Nanaa. Kesho ukienda kukutana na mama yangu ikawa mbaya zaidi ya hivi ndio tunaahirisha ndoa?!” “Mimi hata sijui tena! Tutakuwa na ndoa ya namna gani ndugu zako hawanipendi?” “Ulitaka tukishaona ukakae pale kwao?” “Hapana James!”

“Niambie tu kama umepalinganisha kule kwangu na kwao, kisha ukapapenda kwao, ukawa umeshapigia mahesabu ya kwenda kuishi pale.” “Hapana James. Mimi sijapadharau kwako. Ila hata tufanyaje, hawa ni ndugu zako.” “Utaolewa na mimi, na nishakupeleka ambako utaishi na mimi. Hakuna wakukubugudhi.” “Wakati yeye ndio anajua kula yako! Anaingia mpaka kwenye mafriji yako na kukupangia ule nini!” James akatulia kidogo. Alishasahau hilo.

“Sitaki kuwa kwenye maisha ya misukosuko James.” “Nilikwambia sasahivi ndio tunajenga msingi wetu. Kila kitu kitakavyokwenda kuanzia sasa ni vile tutakavyokubaliana mimi na wewe.” Hapo Jema akatulia. “Umenielewa? Inamaana kuanzia sasa, hawezi tena kufanya kile alichokuwa akikifanya kabla sijakutambulisha kwao. Mimi nachukulia ndio nimeshakutambulisha, na wenyewe lazima kuelewa kuwa sipo tena peke yangu. Niambie kitu kingine.” Jema akatulia.

“Naomba tukale sehemu kwanza ndipo nikurudishe nyumbani.” “Kama unaweza kusubiri, naweza kupika tukala.” James akacheka. “Umeona mambo hayo! Acha kupaniki bwana! Ujue watoto watakuwa wakikuangalia sana wewe?” “Sikutegemea James! Nanaa niliyekuwa nimekutana naye kwa Kumu hakuwa hivi. Alikuwa mcheshi mno. Imekua ni kama amenipiga kibao cha usoni, tena hadharani!” “Pole. Ila sasahivi tuendelee na yetu. Hakuna tena kuangalia watu. Sisi tu.” Safari ya nyumbani kwa Jema ikaanza. Haikuwa mbali. Alipangisha Sinza, karibu na Makaburini.

Akafungua mlango wakaingia. “Karibu.” “Acha kunyongea bwana Jema!” “Nimeumia James. Nimeumia sana. Ila nashukuru kusimama na mimi pale mbele yao. Ingekuwa mbaya zaidi kama ndio ningetakiwa kurudi kukaa pale na watoto wakiendelea kunihoji!” “Naomba tupange mipango yetu. Njoo ukae hapa.” Jema akaenda kukaa hapo ila mbali kabisa. James akamsogelea. “Utaishi na mimi Jema. Naomba uwe na amani. Hilo limeshatokea, lisituibie muda wetu. Niambie nifanye nini ili utulie na kurudisha mawazo yako kwangu.” Wakabembelezana hapo, akapata mabusu yakutosha, akaanza upishi.

Kwa Magesa.

Huku kwa kina Magesa kukapoa. Nanaa akajua wazi ameharibu kupitiliza. Angalau mama G akajipongeza safari hii yeye hajaharibu. Nanaa alishinda huko jikoni na kushindwa kutoka mpaka akamaliza kila kitu, akaweka mezani akataka kukimbilia chumbani, mama G akamuwahi. “Usiende kujificha, njoo hapa.” “Mimi naenda kuoga.” “Mpaka tuzungumze.” Mumewe akabaki akimwangalia. Akajishauri na kurudi kukaa.

“Wewe umeruhusu hasira ya muda mrefu imekukosanisha na kaka yako. Unakumbuka sababu aliyotupa James ya kusubiri kuoa?” Nanaa kimya, ameinama anasugua mikono. “Kaka yako alisema hakutaka ajichanganye. Hakutaka kufika kwenye mahusiano ambayo yatampasa kuchagua kati yako na huyo mpenzi, endapo mpenzi akatokea kukuchukia wewe. James anakupenda kiasi ya kwamba aliweka maisha yake pembeni, ili akufikishe wewe mbali. Alikosana na wazazi wake, na kupoteza furaha ya mzaliwa wa kwanza, kwa ajili yako Nanaa. James hajui mambo nusunusu.” “Nimekosa mama. Hata sijui ilikuaje nikamlipukia vile! Kaka amenichukia.” Nanaa akaanza kulia.

“Basi na sisi kwetu alikuwa hivyohivyo lilipokuwa likifika swala lako. Ni vile tulikuwa hatukwambii. Siku ile Marangu ilikuwa karibu ampige Liz, ndio akashikwa. Ilikuwa ugomvi, James hashikiki akikutetea wewe. Sasa na wewe ukaenda kuharibu kulekule ulikomuona miaka yote akisimamia. James ni wale watu ambao hawajui kuyumba akiamua kufanya jambo au akiwa na kitu chake mkononi.” “Naenda kumuomba msamaha.” “Sio leo.” Akadakia Geb kwa haraka sana. “Sawasawa Geb. Leo ndio utaharibu zaidi, maana sasahivi yupo kwenye kutengeneza kwa Jema. Kupiga sasahivi ni kumuingilia. Na utamtibua zaidi.” Nanaa kimya.

“Sisi wote tunajua ni hasira tu, maana hata wewe siku ya kwanza umekuja kwetu, ulifikia jikoni, ukiwa umepita sebuleni. Au umesahau?” Mama G akamuuliza kwa kituo. Nanaa asijue ndio anakumbushwa alikotoka au la! Akashindwa kujibu. “Sikumbuki kukaribishwa kwako jikoni ila uliingia na kuanza kusaidia kazi. Na sisi sote tukaona ni jambo Jema tu. Si ni kweli Nanaa mwanangu?” Akamng’ata na kumpuliza. Nanaa akashindwa hata kujibu akabaki akilia. Mama G akaona anyamaze akijua ujumbe wake umefika.

Maji Yameshamwagika, Hayazoleki Tena.

Jumatatu.

Siku ya jumatatu asubuhi, James akaitwa kuwa anawageni. Akahisi ni kina nani ila akaamua tu kwenda. Ni kweli akawa amepatia. Akakutana na Geb, mama G pamoja na Nanaa. “Naomba tuzungumze James mwanangu.” “Nashukuru sana mmekuja ili tuzungumze bila wasiotufahamu sisi. Watoto na Jema. Njooni hapa kwenye chumba cha mkutano. Hakuna mtu.” Wakamfuata. James akawapisha mlangoni ili waingie, Danny naye akawa anapita. Wakatizamana lakini ni kama aliyejionya, Danny hakuwasemesha. Na kweli hali yake ni kama ilianza kurudia kuwa ya kawaida. Ule udhaifu wa maradhi haukuonekana tena.

Wakaingia wote ndipo James akafunga mlango. Akakaa mbele yao kama kuwaambia anawasikiliza. “Nimekuja kuomba msamaha, kaka. Nilikosa.” “Hapana hukukosa Nanaa. Hapo unataka kunifanya mimi mjinga. Labda nianze kukumbusha unazungumza na mimi, nipo kwenye maisha yako tokea unazaliwa, na nipo kwenye maisha ya kina Magesa kabla yako.” James akaanza taratibu bila jazba.

“Ninachotaka kukwambia ni kwamba, SISI tunafahamiana, kwa undani sana. Nimekuona jinsi unavyokarimu wageni uliochagua wewe. Tuanze kwa upande wa Kumu.” Wote kimya. “Nilikuwepo na kukuona jinsi ulivyompokea Naya alipoletwa kwenu na Kumu. Ulimfungulia milango yote bila hata yeye mwenyewe Naya kuomba, tena alikuwa akikukatalia zaidi ya mara moja, na hukuwahi kuchoka kumfungulia milango hata ya nyumbani kwako. Tuje kwa Man, mume wa Grace.” Wote wakashituka kidogo.

“Unamkarimu yule jamaa, kwa kutetemeka. Nilikuwepo nyumbani kwako mara ya kwanza wakati dada yake Man, Malisa, alipokuja na yeye pale kwenu, kukutana nao, kina Man na Grace walipokuwa wamekuja hapa Dar. Bila hodi wala ruhusa, kama wewe umesahau, acha nikukumbushe. Yule dada alienda mpaka jikoni akiwa ametuacha sisi wote sebuleni, akaongea kwa sauti akisema, amekimbilia jikoni kama anayepafahamu vile, akiwa anataka glasi ya pili apunguze juisi ya mtoto wake alipewa nyingi ataishia kuchezea tu. Unakumbuka Nanaa au umesahau?” Kimya.

“Ulikimbilia jikoni kwenda kumsaidia kupata glasi huku ukicheka na kumwambia haina shida, anakaribishwa, ajisikie yupo nyumbani.” Wote kimya. “Nikurudishe kwa ndugu uliowapata juzi upande wa baba yako mzazi. Hao ndio hawana mipaka. Wanaingia pale kokote, na kufanya chochote ukiwa huna neno nao. Siku ya kwanza alipofika mke wa baba yako hapa nchini, ukumbuke na mimi nilikuwepo Nanaa. Yule mama alisimama akiwa anataka kuongeza nafikiri juisi hiyohiyo. Alisimama na kuelekea jikoni, ndipo akakuita. Sikumbuki kukusikia ukimkaripia kuwa anakiherehere. Ujasiri wa kuzunguka kwenye nyumba yako anaupata wapi! Na wala sikumbuki ukiwakaripia hao wote kuwa wamekaribishwa sebuleni, wanataka kufika mpaka chumbani!” Hapo James alishabadilika kuwa mwekundu, kilio cha Nanaa kilisikika. Geb na mama yake kimya.

“Anakuja Jema. Mtu anayenihusu mimi. Nikisema mimi, namaanisha MIMI. Eti leo ndio unamkaripia kwa kutaka kusaidia! Halafu si kwa neno moja useme uliropoka! Unamuhoji mfululizo mkisaidiana na mwanao! Ukionyesha wazi ulikusudia, uliendelea kumfoka mpaka nikashindwa kuvumilia, ikabidi kuja kumuokoa na kinywa chako.” James akaendelea.

“Mbaya zaidi, Jema si mgeni kwako! Anakufahamu kwa kukuona unapokuwa na wengine! Labda mimi nikuulize, ungefanya hivyohivyo kwa mtu aliyeletwa na baba yako mzazi, au Kumu au Man?” “Nimekosa kaka.” “Huo ni unafiki na sitakuruhusu unidanganye ili kujisafisha dhamira yako. Wewe umechagua aina ya watu wa kuwapokea kwenye maisha yako. Watu wenye hadhi fulani ndio unawatetemekea na kuwakubali. Jema amekuwa tatizo kwa kuwa ameletwa na mtu kama mimi na si Kumu, wala Man au baba yako.” James akaendelea.

“Nimejuta kujipa nafasi kwako ambayo nilidhani ninayo kumbe sina! Nikamuaminisha Jema jambo ambalo halipo! Sasa hivi mimi ndiye nalipa garama. Umeyapa mahusiano yangu na Jema picha ambayo sikuitegemea! Msingi niliokuwa nimejenga naye mwanzo, inabidi nianze upya kwa kumjenga yeye kama Jema. Kwa kuwa ameshakuona ukiwa na Naya pamoja na Kumu. Jinsi ulivyo au unavyokuwa ukiwa katikati yao ukiwatetemekea. Inabidi kuanza upya kumueleza mimi si Kumu na yeye hatakaa kuja kuwa Naya. Hilo naweza nikafaulu kulijenga kwa upya, ila kigumu ambacho kinaniuma ni, maneno yakitoka au kutamkwa, huwezi kuyarudisha. Hakuna jinsi nikamjenga sasa hivi nikikanusha maneno yako uliyomtukania ila kumjenga juu matusi yako kwake.”

“Mbaya zaidi, umetonesha donda ambalo nilikuwa nikilitibu kwa muda wote niliowaomba mnipe ili kuweka msingi. Nilikwambia wewe na mumeo. Tena nilikwambia wazi kabisa, nivumilie kwakuwa kujenga msingi ni kazi. Jema ametoka kwa mwanaume aliyekuwa akimpa maneno makali na matusi yanayofanana kabisa na uliyomwambia jana!” “Pole sana James mwanangu.” James akacheka akitingisha kichwa.

“Yaani ni kama shetani alitumia kinywa chako wewe mtoto, kumtesa mpenzi wangu! Maneno yaleyale aliyokuwa akiambiwa na mimi kumjenga, eti na wewe unakuja kuyarudia vilevile! Tena kwa kiumbe kama Jema! Hakika Mungu afanye jambo. Umefuta tumaini zima nililokuwa nimempa Jema, mpaka ananiuliza pengine yule mnyanyasaji wake hakuwa akikosea, kweli yeye ni tatizo kama ulivyomsema jana!” “James mwanangu, naomba usamehe tu.” “Nikishatamka nimesamehe, inamsaidia nini Jema ambaye mmeharibu moyo wake? Au mpo hapa kurudisha amani na furaha ya Nanaa tu kisha muondoke, niwaonyeshe kila kitu ni sawa?” Akawatizama wote kwa zamu.

“Halafu nikishatamka hapa msamaha. Nikawaambia yamekwisha, mnataka iweje kwa Jema?” “Na yeye tutamuomba msamaha.” Akadakia mama G. “Utamwambia nini? Tafadhali naomba kusikia. Maana neno samahani tu, halitoshi kufuta ulichomwambia jana. Huku ukimfoka mbele ya watoto wenu. Na kumwambia eti uliropoka, ulikosea si kweli. Utakuwa ukimdanganya na sitakuruhusu. Maana mtu huwezi kuropoka mazungunzo mazima au kukosea kwa kumsema kwa kumuhoji kwa muda mrefu vile. Utamwambia nini kufuta ubaya wote ule?” James akamuuliza akiwa anamtizama.

“Jamani, kwa vyovyote mtakavyoniona nipo. Au vyovyote vile ulivyonipima wewe Nanaa, ukinilinganisha na kina Man, au Joshua, vyovyote vile, lakini Jema amenipokea kwa upendo mkubwa sana na ananiheshimu. Na kwa vyovyote mlivyomuona Jema. Mkampima kwa vipimo vyenu mkimlinganisha na kina Naya, Malisa, Grace na wengine wote, vyovyote vile mnavyomuona, lakini kwangu Jema amebeba sifa zote za kuwa mke wangu mimi na nimeridhika naye. Na ndio maana wakati wewe ukimfoka, hata mumeo na mama G hapa walinyamaza kimya, lakini mimi nilishindwa. Siwezi nikaona anateseka kwa namna yeyote ile, nikanyamaza. Siwezi na sitaruhusu labda iwe nje ya uwezo wangu.”

“Na ndio maana hata kwako wewe Nanaa, nilikubali kutoa kafara upendo wa wazazi wangu kwangu kama mzaliwa wa kwanza na furaha ambayo mama yangu alikuwa akiitafuta mpaka kunipata ili tu kukulinda wewe. Unajua ni kiasi gani nilijitoa kwako nikihakikisha upo salama, kwa vile nilivyo wezeshwa na Mungu. Sasa kwa kipimo hichohicho nitamlinda Jema.” Nanaa akazidi kulia akishindwa hata kumwangalia mtu.

“Sasa basi. Kwa kuwa sasahivi Mungu amekuweka kwenye daraja jingine ambalo mimi binafsi silijui. Maana lile nililokufahamu nalo, ndilo nililomwambia Jema na kumtambulisha kwako na ndio maana nilimleta kwenu. Huyu Nanaa mpya, mwenye kufanikiwa sana. Ambaye Mungu amekupa na baba yako mzazi na ndugu zako wote. Watoto wazuri na jamii unayojitengenezea wewe kwa kuchagua kwako, umeweka wazi mimi na Jema hatufiti kwenye hiyo jamii yako.”

“Jema hana familia kama yako. Hana baba. Narudia tena, kwa namna yeyote ile unayoniona na kunilinganisha na vipimo vyako, mimi ni majibu ya Jema kutoka kwa Mungu. Nimekusudia kumpa nafasi kama wewe uliyopewa na Geb, kujenga jamii yake itakayomkubali na kutupokea sisi kama tulivyo. TENA, nataka aijenge jamii na familia yangu akiwa ametulia kabisa kama wewe nilivyokutoa kwenye kelele za Moshi, nikakuleta hapa Dar, nikakuwekea mazingira tulivu, nikipambana mchana na usiku mpaka ukafanikiwa, ndivyo nakusudia kufanya na kwa Jema. Ila zaidi kwake kwa sababu atakuwa mama wa watoto wangu.”

“Nataka ajenge akiwa ametulia, bila kujishuku, au mtu wakumshika mikono. Sasa basi. Tafadhali naomba unisikilize Nanaa, maana katika hili ndio sitakusamehe kabisa.” Nanaa akazidi kulia. “Na naomba wote mnisikilize ili atakapotulia na kujaribu kukiuka, mumkumbushe, maana katika hili sitatoa mwanya wa kukosea tena kama jana. Na Nanaa ananijua, ninapolinda, sina undugu. Nakua mwaminifu kwa nguvu zangu zote na akili zangu zote. Ninaposhindwa au kupelea ni ubinadamu tu. Mama yangu atalithibitisha hili kwa vile nilivyokuwa linapofika swala la Nanaa.” “Hata sisi ni mashahidi James mwanangu, ulifanya kwa kadiri ya uwezo wako.”

“Nashukuru kukumbuka mama, tafadhali usisahahu kumkumbusha na Nanaa. Huruhusiwi kufika nyumbani kwangu.” “James, unazidisha!” Geb akashituka sana. “Unaongea nini Geb wewe!?” Akamuuliza kwa hasira kabisa. “Si wewe uliniambia wanawake wanapenda kulindwa na wanataka mwanaume ambaye anamsimamo si myumbaji? Kwamba James aliyekutana naye leo ndiye huyohuyo akutane naye kesho! Au hukuwa ukimaanisha?” Kimya.

“Unataka niwe najenga huku halafu nyinyi mnabomoa!? Mimi namwambia nakukutanisha na familia yangu. Nanaa ni mtu mwema sana, anaupendo na kila mtu, halafu anakuja kwenu inakuwa tofauti. Halafu napata kazi yakuanza kurekebisha kwa shida maana huwezi hata kukanusha aliyokutana nayo kwenu, maana inakuwa kama ulimdanganya. Ulichosema na ulichokutana nacho ni tofauti! Hujui hata ukisema utetee unatetea nini maana hata huyo Nanaa niliyedhani namfahamu siye Nanaa huyu aliyekuwa na baba daktari bingwa ulimwenguni. Mume milionea na mama aina yako wewe mama G! Nanaa huyu mpya ameketisha na wakuu, si ninayemfahamu mimi! Unatetea nini kama si kuanza tena upya!?”

“Umebomoa msingi na picha nzima ya mahusiano yangu na Jema. Ni vile ananipenda, inakua rahisi kupokea picha hii mpya na kuanza kujenga upya na kumbadilishia kibao. Kumwambia Mungu anamtaka yeye ndio aanze kujenga kwake sio kulilia kujiingiza kwenye majumba ya watu yenye misingi yake. Jana umeanzisha jambo jingine jipya kabisa! Lakini nashukuru Mungu naanzisha na Jema mwenye moyo wa utayari. Sasa siwezi kuanza kila siku wewe ukiwa katikati yangu ukibomoa. Sitakuruhusu Nanaa. Sijui kama unanielewa?” Kimya akilia.

“Nitajitahidi sehemu nitakazojua nyinyi mpo, kumuweka mbali kabisa ili asije kuwa kwanzo kwenu nyinyi, na wewe fanya juhudi za makusudi kukaa mbali na Jema. Kama kuna chochote nimeacha kwenu, tupeni. Na chochote ulichoacha kwangu, sitarudisha kwenu. Kwanza nyinyi mnahela nyingi. Wala hamtapata shida kununua vingine. Kwa kusema hivi, tafadhali usilete tena chakula kwangu. Iwe kwa kutuma dereva au wewe mwenyewe kuja. Maana kwangu kutakuwa kwa Jema. Mkifika kwangu mnaweza kukutana naye na kumvuruga akili bure. Haya, naomba funguo zangu za nyumba.” Nanaa akazidi kulia.

“Geb, mkeo anazo funguo zangu za nyumba, tafadhali nisaidie kubania pesa maana nataka kufunga ndoa ya ndoto za Jema. Sitaki kutumia pesa chache nilizo nazo kubadili vitasa vya nyumba. Naomba funguo zangu.” Akawa anamwangalia Geb akimaanisha kama hawatampa funguo zake za nyumba, anakwenda kubadili vitasa. Geb akachukua pochi ya mkewe akatoa funguo za James na kumkabidhi.

“Hili ni kwa wote, kwa mara ya kwanza tokea chuoni, nitabadili namba ya simu ili kuwasaidia nyinyi wote. Msinitafute kwa la kheri wala la shari. Hata mkisikia nipo hospitalini, tafadhalini msije kushawishika mkaja.” “James mwanangu umekasirika na unafika mbali.” “Sasa mkifika nilipo mimi si mtakutana na Jema yuleyule mliyeshindwa kumpokea jana nyumbani kwenu!?” Akamuuliza mama G akimshangaa.

“Si mimi jana nilimleta kwenu na mkashindwa kumpokea? Au wewe hukusikia wakati akifokwa na Nanaa?” Kimya. “Japokuwa jumba lenu ni kubwa, lakini wala Nanaa hakufanya kwa unafiki. Alipaza sauti yake kwa juu kabisa mpaka mwanae akatoka chumba cha michezo na kufuata kujua kulikoni. Akawa akimuhoji Jema na nyinyi wote mkiwa kimya mkimsikiliza anavyomsulubisha Jema kama anayestahili! Sasa mnataka kumfuata tena ili iweje!?” Kimya.

“Msitufanye sisi ni wajinga jamani! Pole ya hospitalini si dawa au uzima. Wewe mama ni muombaji. Ukisikia nipo kwenye shida, tafadhali niombee tu, ila mkae mbali na mimi pamoja na Jema. Na mimi sitawabugudhi, kwanza hakuna mnachohitaji kwangu tena. Mimi sina mamilioni ya pesa wala si daktari bingwa. Sina hadhi ya kina Kumu wala kina Man. Kunifuata popote ni uchokozi na sitaruhusu. Naachana na nyinyi kwa amani kabisa. Hata Ibrahimu na Lutu japokuwa walikuwa ndugu, wakatembea kwa muda mrefu pamoja, lakini ilifika sehemu walishindwa kuendelea kuwa pamoja kwa vile Mungu alivyowajalia kwa vingi. Ilibidi watengane tu. Sisi si wa kwanza. Mungu ametujalia vingi, naona imeshindikana kuwa pamoja. Kwa hiyo mimi kama Ibrahimu, nimempa nafasi Nanaa ya kuchagua kwanza. Amewachagua nyinyi na uzuri wenu wote na watu wenu, acha mimi na Jema wangu tukaanzishe kwetu.”

“Na mtanisamehe, mimi si mnafiki. Sitawadanganya. Na siwezi mambo nusunusu. Nanaa kila la kheri kwenye jamii yako, tafadhali mwache Jema akajijenge kwake. Sikudai kwa chochote na narudia tena, kama unanidai itabidi usamehe tu au utamdai Geb kwa chochote unachonidai. Atakulipa. Yeye sina shaka naye. Najua huwa habadiliki. Geb aliyenisaidia kuniandikia darasani akiwa hana kitu, ili nije kukuona nyumbani, amekua Geb yuleyule hata alipokuwa milionea aliyenisaidia kunilipia mahari yako, mama yangu aliyonidai, na kubaki akinitizama mimi kama James. Haya, kwaherini. Acheni mimi nikawajibike. Mimi sio kama nyinyi. Nalipwa na mwajiri.” James akasimama. 

“Mkimaliza hapa, mnaweza kutoka. Ila nashauri msichukue muda mrefu zaidi, hiki ni chumba cha mkutano, kinatumiwa na watu tofautitofauti.” Akatoka na kuwaacha wamekaa hapo. “Nashauri mama urudi na Nanaa nyumbani akapumzike, mimi niwahi kazini. Nitajitahidi kuwahi kutoka jioni.” “Twende Nanaa, mwanangu.” Mama G akamshika mkono kumsaidia kusimama, wakatoka hapo Nanaa akilia kama amefiwa.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

‘Tafadhali naomba namba ya simu na ruhusa ya kuwasiliana na mama.’ Ujumbe ukaingia kwenye simu ya Jema. Jema akakunja uso na kumpigia. “Upo mzima mpenzi wangu?” “Nipo.” “Mbona sasa umenyongea?” “Hapana. Nipo na mambo mengi kidogo.” James akatulia. “James?” “Mimi nilijua ukinisikia ndio ungefurahi!” “Nimefurahi James. Sema bado nipo kama….” “Unanifanya nikose raha Jema. Kweli Nanaa ndio anatupa hatima ya mahusiano yetu?” “Hata iweje James, Nanaa ni ndugu ambaye ulisema ni kama mtoto wako. Siwezi kukwepa ukweli kuwa yupo kwenye maisha yetu. Imenivuruga James. Nimekaa leo naanza kurudia kote nilikopita na Temu na jinsi nilivyotenda.”

“Sio jana tulikubaliana tuyaache hayo?” “Mimi ni binadamu James. Aliyozungumza jana ni kama malalamishi ya Temu tu. Lazima akili itanirudisha huko.” “Sasa labda iwe unataka kurudiana na Temu. Ila mimi namtaka Jema huyohuyo wanayemsema.” “James!” “Sasa wewe unafikiri ni kwa nini wewe na sio wasichana wengine waliokuwa wakinizunguka miaka yote?” “Mimi sijui James!” “Kwa kuwa hawakuwa na sifa zako Jema. Au wewe unafikiri ni kwa nini nakutaka wewe?” James akamuuliza.

Jema akatulia akijitafakari. Maana kwa ukweli hata yeye alijijua sio kwamba alikuwa na sifa kama za malaika au umbile la kushitua mtu au kumfanya mwanaume kugeuka mara mbilimbili. Hakuwa na vya ajabu mwilini mwake. Akajirudi. “Jema?” “Sijui James!” Hapo akapoa. “Basi ndio ujue. Nilivutiwa na hizo sifa zinazowashinda wengine. Hizo ndizo zilizonivutia na kunifanya sasa kuanza kukuangalia vizuri na kugundua uzuri wako.” Jema akaanza kucheka.

“Acha kunidanganya bwana James!” “Kwamba wewe hujui kuwa una macho ya rangi ya udongo. Ugoro fulani hivi?” Jema akazidi kucheka. “Rangi yako wewe huoni kama nzuri?” “Hapo unanidanganya kabisa James. Mimi mweusi.” “Kwa hiyo? Kwamba ukiwa mweusi ndio nini? Kwanza hiyo rangi yako inafanya mpaka meno yako yanakuwa meupee! Jema wangu laini, nikikushika tu mimi hali mbaya.” Jema alicheka sana mpaka akajisahau.

“Mimi nataka ucheke hivyo sio unalilia sifa za watu ambao sio waume zako. Haya, naomba ruhusa yakuzungumza na mama Jema.” “Sasa unataka nini?” “Nimuulizie maswala yangu yakuoa. Naona wewe utanichelewesha. Nimekupa dhamana yakujenga kwetu, mwenzangu naona upo unalilia waume za watu na…” “Bwana mimi simlilii Temu.” “Unamlilia sana tu ndio maana nimekupigia tu, ukaanza kumtaja. Mimi nisingekuwa nakutajia tajia wapenzi zangu wa zamani.” “Basi James, naomba nisamehe. Natoka huko. Naanza kuwaza yetu.” “Wewe nipe namba ya simu ya mama Jema, bwana. Utanichelewesha.” “Unataka kuoa mwenyewe!” Jema akamtania. “Tena kwa haraka! Unanipasha tu joto, nakunitesa bure. Bora nioe ili ukinipasha joto, namaliza kabisa.” Jema alicheka kwa mshituko na kukata simu. James akacheka akiwa ametegemea.

Mara namba ya simu ikaingia, na jina la mama Jema. Akamrudishia ujumbe wa kushukuru. ‘Asante.’ ‘Uache matusi James.’ Jema akamrudishia huo ujumbe. James akacheka sana. ‘Hayaitwi matusi.’ ‘Wala sikuulizi yanaitwa nini.’ James akacheka sana baada ya kupata huo ujumbe. ‘Kweli hutaki kujua?’ ‘Hakika sitaki.’ Jema akajibu. ‘Ujue ukibadili mawazo baadaye na kutaka kujua, naweza kugairi.’ ‘Sitakulaumu.’ Jema alijibu vile nakumfanya James acheke sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Shilingi imempindukia Nanaa. Ilikuwa kwake, akitetewa, Sasa anaonja upande wa wengine.

James amekusudia kuoa kwelikweli. Nini Kitaendelea?

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment