“Japokuwa
Naya alitolewa pale kwenda kupata huduma ya kwanza, ikawa ni kama bado
anasubiria mpaka kuna nesi mmoja akasema nilazima kumruhusu ndipo ataondoka.
Nakumbuka Naya mwenyewe alipozinduka aliomba arudishwe kwa baba yake. Sijui ni
nini Naya alikumbuka au alijua, lakini ni kama yule mzee alikuwa akisubiri
ukiri wa kila mmoja wetu pale.” “Kwani hakuwa akizungumza?” Ikabidi
Bale kuuliza.
“Bale, baba
yenu aliungua vibaya sana. Alichoweza kufanya ni kuangalia na kuhema tu. Kama
si kuambiwa kama ni yeye ndio amelala pale, usingeliweza kumtambua. Alibadilika
akawa kiumbe kinachotisha mno. Anyways, Naya akazungumza naye na kumwambia
anakumbuka wosia wote aliokwisha kumuachia, na akamuahidi atafanyia kazi.
Akanitizama na mimi. Nikamwiga Naya. Nikamwambia ya kwangu, alipomalizia mama G
kutokana waliyokuwa wakizungumza naye na kumwambia wote tunakumbuka kila kitu
na tutafanyia kazi, asiwe na wasiwasi juu ya Naya, hatabaki peke yake
akamuahidi atamtunza kama mtoto wake, akamruhusu apumzike ndio baba yenu
akafunga macho na ikawa amemaliza mwendo.”
“Ninachotaka
kukwambia ni hiki, wosia aliomuachia Naya, Mimi, Geb, Nanaa na mama G ni
tofauti kwa vile walivyojisogeza kwake. Yaani sisi baada ya pale ndipo tulikuwa
tukikumbuka moja baada ya jingine, na havikuwa vikifanana. Kwa hiyo hata wewe
tulia, utakumbuka tu alichotaka kukuacha nacho. Mimi si mtu sahihi wakujibu
hilo.” Bale akatulia. Lakini akahisi ana kitu anashindwa kumwambia.
“Pengine
uwe na swali jingine.” “Je, juu ya nyumba?” “Unamanisha kiwanja cha Kiluvya?
Maana nyumba ndio ile mlichoma wewe na Malon.” Hapo Joshua akamuweka
sawa. “Ndio hapohapo. Kwani alisema hata kusijengwe!?” Hapo
akawa amemchanganya Joshua. “Nina mambo mengi sana Bale, na hapa nawahi
kazini. Utarahisisha haya mazungumzo kama utakuwa muwazi zaidi.” “Ni vile
ambavyo nilitaka kupatengeneza pale.” “Unamaanisha kujenga?” “Ndiyo.” Bale
akajibu na kuendelea.
“Maana nilianza
na mafundi tu wakaiwada, wakashindwa. Nikatafuta kampuni kabisa. Huyo mwenye
kampuni anasema wajenzi wake wamemwambia eti ardhi
imekataa kujengwa. Wewe umeshasikia kitu kama hicho?” “Kuwa mkweli tu kwako Bale,
sijawahi kukutana na mazingira kama yako.” “Unamaanisha nini?” Bale
akauliza kwa ukali kidogo.
“Mimi sijui
nafsini kwako unajiambia nini na kujiaminisha nini. Lakini kwa kule
ulikopitisha familia yako, namaanisha mbali na mama yako, unahitajika rehema
Bale. Mungu angilie kati. Unavilio vya watoto wa bibi yako wote.” “Nitakwenda
kuzu…” “Hawawataki Bale. Na walizungumza kwa wazi kabisa kuwa baba yenu
anamkosi ulioambukiza watoto wake. Yaani nyinyi. Wanasema ndio maana kila
anayejaribu kuwa karibu naye yeye au nyinyi, anakufa.”
“Wanasema alianza
dada yao, yaani mama yenu. Wanalalamika wanasema na mama yao alipomsogelea tu,
ili kuishi naye amsaidie baba yenu, akafa kifo kibaya sana ambacho si cha
kawaida. Na pia wanalalamikia kifo cha Luka, mtoto mdogo asiye na hatia. Wanasema
alikuwa mtoto mwenye maisha yake mazuri, lakini kila kitu kiliharibika pale tu
aliposogezwa na kwenu, ambako alikuwepo baba yenu. Wanawaogopa, hawawataki.
Na wamesema upande wa kwao chochote kikitokea, nimkataze hata Naya kwenda.
Hawataki msaada wowote kutoka kwenu.” “Sasa hapo kosa la baba ni lipi!?” Bale
akauliza kwa mshangao. Joshua hata hakumjibu.
“Mimi
nilitaka tu kupaendeleza nyumbani.” “Nashauri utulie ukumbuke chochote
alichozungumza baba yako na wewe Bale. Hata kipindi kile mlichokuwa mkibishana
naye sana kwenye maamuzi yako. Kumbuka tu. Ukiweza hata uandike. Mimi
nimegundua kuwa Naya alikuwa akiandika sana kila anachoambiwa na baba yake.
Hata sasa nafikiri japokuwa hakumbuki kabisa, ila akilini mwake kunarudia
wosia wa baba yake. Nimesoma kitabu chake cha siri, nimegundua huwa wosia wa
baba yenu unamrudia na anaandika. Ni kama mwanzoni hakujua ni nani alizungumza
naye au nini anakumbuka kila siku, lakini anaonekana alirudia diary yake ya
nyuma, akalinganisha matukio ndio amejua ni baba Naya. Nashauri na
wewe utulie, ukumbuke.” “Mimi kila kitu kinachohusu yeye kwangu ni lawama tu.” Akalalamika.
“Basi
katika hizo lawama zake, japokuwa hukuwa ukimsikiliza, jaribu kukumbuka
alichokuwa akisema, utagundua ndio wosia wako. Kama utaniruhusu naweza
kukukumbusha kitu.” “Juu ya nini!?” Bale akauliza kwa mshangao
kidogo. “Unakumbuka siku ambayo ulisema umeamua kuondoka kumfuata Malon?” Kimya. “Uligomba
sana siku ile ukimlaumu sana baba yako, na Naya kuwa alianzisha mapenzi mapema
na bado baba yako alimuunga mkono, nia yako ni maendeleo ila hakuna anayekuunga
mkono na..” “Nakumbu..” Bale akamkatisha kama ambaye asiyetaka kukumbushwa maneno yake
mwenyewe.
“Hapana
Bale, ninachotaka kukwambia wewe HUKIKUMBUKI na ndio maana unakumbana na
ugumu huko kwenye ujenzi unaotaka kuuendeleza pale kwa siri bila ruhusa
ya Naya.” “Pia kuendeleza pia natakiwa kuomba ruhusa!?” “Unapaendeleza kwani ni
kwako?” Joshua na yeye akamuuliza kwa ukali kidogo. Bale akashangaa sana.
“Unashangaa
nini Bale na kila kitu uliambiwa mpaka na yule mwanasheria!? Na mbali ya hapo,
si ulikuwepo siku baba yako akitamka wazi kabisa mbele za watu siku ile pale
nyumbani kwetu, Goba, kuwa Kiluvya ni pa Naya! Na alisema wazi kabisa hata
alimuomba mama yenu ambaye wewe unamuamini sana. Au naye mama yako utasema hana
akili ya kufikiria? Maana alikubali.” Kimya.
“Baba yako
alitamka Bale, na akaacha mpaka kwa mwanasheria! Sasa wewe unatoka vipi kwenda
kuendeleza kwa mtu bila adhini yake?” “Sasa Naya si hakumbuki!” “Haraka hiyo ni
ya nini Bale!?” Joshua akauliza kwa ukali kabisa akisikika kuumia. “Haraka
hizo kwenye mambo yako ni lini utajifunza kusubiri? Unataka nini
kitokee ili uwelewe kuna wakati mwingine japokuwa tunakuwa na tamaa ya mambo
fulanifulani, lakini Mungu anaposema subiri, SU-BI-RI.” Hapo hata Joshua akabadilisha
sauti ikawa ya ukali.
“Wewe
unajua Naya atapona lini?” Bale naye akamuuliza. “Mimi sijui!
Ila wewe uliyemsababishia hivyo mke wangu ulitakiwa uulizie hali yake
sio kwenda kinyumenyume kuanza kujimilikisha mali yake.” Joshua akambadilikia.
“Nia
ilikuwa nzuri Joshua.” Bale akashuka. “Nia yako nzuri ni ipi Bale? Ipi na katika nini?” Kimya.
“Kitu
nilichotaka kukumbusha kabla sijakuaga maana nakaribia kuingia ofisini, n..”
“Si ulishasema..” “Tafadhali sikiliza Bale. Usiwe mwepesi wa kuzungumza na ndio
maana unapishana na jumbe zako, kwakuwa kila mtu anapojaribu kuzungumza
na wewe, tayari wewe umeshakuwa na jibu la kumjibu. Ndio maana umekosa hekima
za baba yako.” “Acha kuniambia hivyo Joshua.” “Bale! Unakataa nini wewe?
Utajichelewesha mpaka lini? Labda nikuulize. Ni kwa nini tunazungumza asubuhi
hii?” Kimya. “Ni kwasababu HUJUI baba yako alichokuwa akikisema japo mimi
nakumbuka!” Kimya. Bale alishakuwa amekasirika anatamani kukata simu na
Joshua alijua akaamua aachane naye.
“Uwe na
siku njema, Bale.” “Sasa mbona hutaki kuniambia!?” “Hujataka kunisikiliza na
mimi sitawahi kubishana na wewe Bale. Mimi ni mkubwa sana kwako. Na nina
majukumu mengi sana yakufanya. Sina muda wa kujibishana na wewe. Uwe na siku
njema.” “Nakusikiliza.” Bale akasikika ametulia.
“Siku uliyoaga
kuwa unaondoka unamfuata Malon. Baba yako alikwambia hivi, ‘utakapofanikiwa
huko, usijekurudi kujenga kwangu’. Unakumbuka jinsi ulivyomjia
juu baba yako mpaka ukaanza kumuanika Naya huku ukimfoka baba yako kuwa mbona pesa
za Naya ambazo hazikuwa hata zikijulikana zinapotoka zilikuwa zikipokelewa pale
nyumbani, kwa nini wewe mtoto wakiume ukataliwe? Unakumbuka baba yako
alikwambia uende ukajenge kwako sio kwake?” Hapo Bale alipoa kabisa.
“Mungu
amekufikisha kwenye amri moja tu yenye ahadi Bale. ‘Waheshimu
baba na mama yako, upate miaka mingi na heri duniani.’ Kwa
vyovyote ulivyokuwa ukimchukulia baba yako, lakini ujue kabisa, Mungu alikuweka
kwa aina ile ya baba si kwingineko. Yeye Mungu alijua aina hiyo ya Bale,
inamuhitaji baba kama baba
Naya wala si mzee mwingine. Ukachezea hiyo nafasi
kwa fujo nyingi mpaka kumuua baba yako mzazi ukiona hana akili ya
kufikiria. Lakini Bale, natamani ungesoma diary ya dada yako pengine
ungemfahamu baba uliyempuuza wewe, lakini akamfaa sana dada yako. Ukimsoma baba
Naya aliyeandikwa na Naya, unaweza ukadhani si baba
aliyekuwa akiishi na wewe ukimfoka hata mbele za wageni kama mimi.” Bale kimya.
“Ninakukumbusha
hili tena, pengine tu utaelewa hilo wanalokwambia hao wajenzi. Adamu alipomkosa
Mungu pale bustanini, unakumbuka laana yake? Tena Mungu mwenyewe alimwambia hivi,
‘Kwa sababu umemsikiliza mke wako na
ukala kutoka kwenye mti niliokuamuru Msile tunda lake’ Yaani Mungu
anamwambia kabisa, kwa sababu alimsikiliza Hawa, akatenda dhambi.
Unakumbuka laana yake?” Kimya. “Acha nikukumbushe maneno ya Mungu wala si yangu. Alimwambia
hivi, ‘Aridhi imelaaniwa
kwa sababu yako,…. Na kuendela, nafikiri
unakumbuka.” Kimya.
“Kukuleta
karibu kabisa na ninachotaka kukwambia ni juu ya Kaini alipomuua
ndugu yake, yale maneno Mungu aliyomwambia. Unakumbuka?” Bale akaanza kulia
kwa uchungu sana. Maana alikumbuka kwa wazi kabisa. Bale mtoto wa kanisani,
amekua kanisani, hata kama hatatendea neno kazi, lakini analijua neno la
Mungu kwa hakika. Naye Joshua akaendelea kumwambia. “Sikwambii
hivi kama kukuhukumu. Nakuelekeza njia pengine itakusaidia kufika unakotaka
kwenda, kama utataka. Kaini aliambiwa hivi na Mungu, ‘Basi
sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi iliyofumbua kinywa chake ipokee damu
ya ndugu yako, kwa mkono wako. Utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake. Utakuwa
mtoro na mtu asiye na kikao duniani.’ Nafikiri
unakumbuka Bale. Na pengine ndicho unachokumbana nacho. Kama upo na swali
jingine karibu. Vinginevyo nikutakie siku njema.” Joshua akasikia simu imekatwa. Ila akaridhika kwamba angalau amefika
kwenye machozi, inamaana moyo uliopondeka bado upo.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ni nini Kitaendelea?
Usikose muendelezo kujua Penzi Jipya la J&J. Joshua&Naya?
Bale!
Nanaa dada mpendwa, wifi
wa Jema!?
Usipitwe.
0 Comments:
Post a Comment