Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Mapenzi & Pesa! - PART 1 - SEHEMU YA 46. - Naomi Simulizi

Mapenzi & Pesa! - PART 1 - SEHEMU YA 46.

Maumivu makali ya tumbo yakamtoa usingizini. Akabaki pale kitandani akigugumia maumivu akiogopa hata asigeuke asije kumuamsha Joshua. Kumbukumbu za usiku uliopita alipojiandaa kwa ajili ya penzi kwa mumewe akaishia kwenye maua zikamjia. Kilicho cha ajabu hofu ya usiku wake ikamrudia tena. “Joshua atanichoka kama nakua sikumbuki. Ananitarajia kwenye mambo fulanifulani, lakini napelea. Atanivumilia mpaka lini!” Akawaza Naya nakuzidi kujiogopesha. Sauti ya Joshua akitaka apokelewe maua kwanza ikasikilizishwa sikioni kwa Naya tofauti kabisa. Naya akaipata kama mtu aliyekuwa amejawa jazba kwake. Akazidi kuingiwa hofu.

Taratibu akatoka hapo kitandani kwani tumbo lilizidi kumuuma na hali ya kutapika ikamjia. Akatoka hapo kwa kunyata na kwenda kwenye chumba cha chini chenye vitu vyake. Akakimbilia chooni akakuta ameloa damu, na kuanza kutapika huku akizuia sauti kama mtu asimsikie. Alitapika Naya mpaka panapambazuka asijue afanye nini. Akakaa sakafuni chooni kichwa amening’iniza chooni. Akatapika mpaka akabakiwa kutapika tu mate.

Joshua anaamka asubuhi, mke hayupo kitandani. Akashituka na kwenda choo cha chumbani, hakuwepo. Akashuka sebuleni. Hakuwepo. Akafikiri atakuwa kwenye meza ya kulia ya jikoni akila kwa sababu alilala bila kula chakula cha usiku. Hakuwepo. Akili ikamjia kwenda kwenye chumba alichoanza kukizoea. Chumbani hakuwepo. Pakawa kimya sana. Akabaki hapo chumbani akitafakari alipo. Akarudi chumbani kufuata simu yake kuangalia kama kuna mlango ulifunguliwa huku amejawa hofu yakupita kiasi. Simu ikaonyesha hakuna mlango uliofunguliwa, kidogo akatulia na kujaribu kufikiria anapoweza kuwepo.

Akarudi kwenye chumba ambacho alidhani angekuwepo, lakini safari hii akaamua kwenda kumuangalia na chooni. Akamkuta amepitiwa usingizi ila amening’iniza kichwa chooni. Damu mpaka sakafuni. Akamuhurumia. “Naya!” Akashituka sana. “Samahani kama nimekuamsha.” “Vipi?” “Safi tu, sikutaka kukuamsha.” “Unatapika?” “Nipo sawa. Sikutaka kukuamsha.” Joshua akaumia, akajua amembadilikia, ameanza kumficha.

“Naya, naomba usinifiche. Niambie ukweli tafadhali. Usiogope.” “Naogopa Joshua. Sikumbuki kitu. Na nasema ukweli, sidanganyi. Sikumbuki. Kila nikijitahidi sikumbuki.” Naya akalia akijitetea. “Najua hunidanganyi Naya. Naomba utulie mke wangu. Na samahani kwa kukufanya ujisikie unatakiwa kukumbuka. Haikuwa nia yangu kukuogopesha ila nilitaka kukufurahisha zaidi. Pengine nilitumia sauti ya msisitizo mpenzi wangu, ila sikuwa na nia ya kukushutumu.” Bado akaonekana kama haelewi tena, kichwa kimevurugika tayari.

“Na sikukusudia kukuamsha, ndio maana nilitoka. Sijui nifanye nini! Nakosea kila wakati! Ni kama akili yangu inashindwa kujua nini chakufanya kwa wakati.” “Nisikilize Naya. Tafadhali tulia uniangalie.” Akarudi kuanza kutapika tena. Joshua akamshikilia mbavu, hakuna kitu kikawa kinatoka. “Naomba usimame hapo, utoke ukaoge ili uvae pedi.” “Acha mimi nibaki tu chumba hichi ili ukilala nisikuamshe. Nataka kubaki hapa. Peke yangu ili nitulie. Nahisi sielewi tena. Kichwa kinazunguka.” “Basi tulia, acha nikuletee vitu vya kujisitiri.” Akataka kutoka. “Hapana. Acha tu.” Joshua akarudi.

“Sasa utajisaidiaje, Naya?” “Nataka kutulia, nifikirie mimi mwenyewe nijue nini natakiwa kufanya. Usinisaidie kitu. Niache tu.” Akazidi kulia tena akionekana maumivu yamemzidia. Kisha akainamia tena choo. “Hakuna kitu kinatoka mpenzi wangu. Naomba utulie na ndipo utaweza kufikiria.” Akaendelea kulia, Joshua akatoka kwenda kumletea chupi na pedi nyingi tu. Akarudi akamkuta akioga. Kisha akaanza kutapika tena. Joshua akataka kuingia amsaidie, lakini akaona amuache. Analia huku akitapika halafu akioga. Joshua akabaki akimwangalia mpaka akamaliza. Akamkabidhi taulo. Akajikausha huku upande mwingine akipaka damu hilo taulo. Joshua akajua ni kweli ameshituka, damu zilikuwa zikitoka nyingi sana.

“Naya! Huwa tumbo kama hilo lilipokuwa likiuma na kupatwa hiyo hali, kuna dawa ulikuwa ukinywa inakusaidia sana.” “Sikumbuki.” “Mimi nakumbuka na nafikiri ninazo, nikuletee?” “Nielekeze nikachukue mwenyewe. Sitaki kukusumbua zaidi.” “Hunisumbui hata kidogo. Nisubiri narudi sasahivi.” Joshua akatoka hapo akikimbia mpaka anapoweka dawa kwenye kabati ndogo. Akarudi na soda ya Sprite. Hapo kunywa napo ikawa shuguli. “Nitatapika zaidi. Siwezi kuweka kitu mdomoni.” Baada ya kumbembeleza kwa muda mrefu akakubali kunywa hizo dawa na hiyo soda. Akakataa kurudi chumbani kwao. “Hapana. Kule nitakusumbua.” “Hutanisumbua Naya!” Akazidi kulia, Joshua akaona amuache tu hapo. Alipotulia na kupanda kitandani, ndipo akatoka kwenda kujiandaa kwenda kazini.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Joshua alitoka hapo hajui hatima yake na Naya. Naya huyu amerudia hali kama amechanganyikiwa, mtiririko wa mawazo yake ni vile anavyochagua yeye, halafu akawa na msimamo na anachokitaka sio rahisi kama mwanzo aliporudi na kumuuguza kirahisi. Amesimamia kukumbuka. Hataki kuwa tegemezi. “Amehama na chumba!” Joshua akawaza na kuamua kujisalimisha kwa Mungu wake.

Penzi Kikohozi.

‘Acha kumnyima raha na kumtia wasiwasi mke wangu. Mpigie simu.’ Ujumbe wa Geb ukaingia kwenye simu ya James, ndipo akakumbuka. Hapohapo kabla hajasahu tena akampigia simu. “Kwema kaka!?” Nanaa akauliza kwa kulalamika kidogo. “Kwema, unisamehe nilitingwa.” Nanaa hakuridhika. “Kiasi chakushindwa hata kunijulia hali hata kwa ujumbe tu!? Ni nini kinaendelea kaka? Au nini nimekuudhi!? Kama nimekosa tafadhali uniambie tu nirekebishe. Wewe..” “Nanaa! Ni habari njema tu nitakuja tuzungumze.” “Umepata mchumba?” Nanaa akauliza swali la moja kwa moja.

“Ndiyo.” Nanaa hakutegemea. Akabaki kimya kabisa, James asielewe kama ndio amefurahi au bado anahasira ya kutorudishiwa simu. “Nanaa?” “Hongera kaka. Lakini usingeacha kuwasiliana. Niliingiwa na wasiwasi!” “Unisamehe. Nilikuwa kwenye kuweka sawa mambo, ndio maana niliona nikutafute nikiwa nimetulia.” “Sawa. Uwe na siku njema.” “Usikasirike sasa! Mimi nilijua ungenifurahia!” “Nimeumia kuona unanitenga kaka!” “Pole mdogo wangu. Nisamehe. Ila mwanzo ni mgumu. Nipo kwenye kuweka msingi. Nivumilie tena kidogo tu, mambo yakikaa sawa, nitakutafuta na nikutambulishe. Ni sawa?” “Sawa. Kila la kheri.” James alijua wazi hajaridhika, na yeye hakuwa na muda wa zaidi, alikuwa akichat na Jema. Akamuaga  kwa ahadi ya kuja kumpigia tena baadaye. Akakata.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika mchana Joshua akajaribu kumpigia mkewe bila mafanikio na mpaka anatoka kazini hakuwa amemsikia. Akaona amuache. Ila akawahi kutoka kidogo ili kumuwahi. Akafika nyumbani akamkuta amelala, hajanywa hata chai. Akaenda kukaa pembeni yake. Akashituka. “Joshua!” “Vipi tumbo na hali ya kutapika?” Akatulia kama anayejaribu kufikiria.

“Najisikia vizuri. Lakini nina swali.” “Uliza tu.” “Eti Zayoni ni nani na yuko wapi?” Joshua akashituka sana, hakutegemea. “Alikuwa mdogo wako.” Naya akawa hajaelewa. “Mlizaliwa watatu. Wewe ndio dada mkubwa, halafu Bale na wa mwisho ni Zayoni. Unakumbuka nilikwambia sisi ni yatima?” “Nakumbuka. Kwamba sina ndugu hata mmoja aliyebakia hapa duniani?! Kwamba kama vile wewe ulivyokuwa ukienda kwa kina Magesa, mimi sina mtu hata mmoja kweli!?” Hilo swali likazidi kumtia wasiwasi Joshua.

“Naomba upone kabisa, nitakusimulia juu ya ndugu zako Naya. Nakuomba isiwe sasahivi.” Akamuona machozi yakimtoka ila hakuongea tena. “Ni kwa faida yako. Sitaki kukuchanganya. Ni sawa?” “Nitasubiri japo nilitamani sana kujua. Nimekuwa na maswali yasiyo na majibu, yanaanza kunisumbua.” Akaongea hivyo na kujirudisha kulala vizuri. Joshua hakutaka kuongeza chochote kwenye hilo kwani kwanza ni kama hawapo kwenye maelewano na anaumwa. Msisitizo wake ni hataki amsumbue. Hakujua kama anauliza kwa nia ya kwenda kwa ndugu zake na kurudi, au la! Akasimamia alichosema, atasubiri. Akakaa hapo kimya kwa muda.

“Naya?” Akajigeuza na kumwangalia. “Nikuletee supu? Niliomba upikiwe.” Akakataa kwa kutingisha kichwa. “Umekula kitu chochote?” “Tumbo limejaa mpaka linakuwa kama lina vichomi. Siwezi kunywa hata juisi. Ila nakunywa maji.” “Pole Naya.” “Asante. Naomba kurudi kulala.” Joshua akatulia kidogo akijua ndio anamfukuza.

Akatumia akili kwa haraka kabla hajapotelea usingizini. “Leo tunalala huku?” “Hapana. Ila mimi nataka kulala hapa ili iwe rahisi kutumia choo. Nisikusumbue.” “Unakumbuka nilikwambia hunisumbui!” Akanyamaza akamuona machozi yakimtoka. “Siwezi kulala bila wewe Naya. Usipolala na mimi ndio nitasumbuka. Naomba nije tulale wote.” Akanyamaza hakujibu.

Joshua akaenda kupiga magoti pembeni ya kitanda mbele ya uso wake. “Nakupenda Naya. Na maisha yangu yanakuwa magumu kama sipo na wewe. Kila kitu unachoona nafanya, hata kwa kukosea, ujue nafanya kwa ajili yako mpenzi wangu. Naomba unisamehe na univumilie.” Akamuona anatingisha kichwa kukubali. “Asante. Basi naomba turudi kitandani kwetu. Na uwe huru kutumia choo muda na wakati wowote ule, hutanisumbua.” “Hapa nilipo nimechafuka mpaka nimechafua magodoro. Nataka kujaribu kusafisha tena, ndipo nikimaliza nije.” “Unajua kwa nini mchana nilikuwa nikikupigia sana?” “Sijui simu

ilipo.” “Nilitaka kukumbusha kuwa huwa ulikuwa ukitumia pullups wakati ukiwa kwenye siku zako ndipo unalala vizuri, huchafuki.” Naya akatulia.

“Nenda ukaoge, mimi nitabadilisha hapa, ukimaliza nitakupa pullups ili uvae, ulale vizuri.” “Acha tu nitasafisha mimi mwenyewe. Wewe nenda ukapumzike. Najua umechoka na kazi.” “Sijachoka Naya. Naomba niruhusu niwe na wewe.” Akakaa. “Ni sawa?” “Nikikwambia nimechafua, ujue nimechafua mpaka godoro. Mchana ilibidi nilifute na taulo la maji. Hapa nimelalia taulo. Ndio maana naona nisafishe kila kitu.” Wakavutana hapo, Joshua akibembeleza mpaka akakubaliwa. Naya akatoka hapo kitandani, Joshua akabaki amehamaki. Ni kama kulichinjwa mbuzi. Akajua hilo godoro halitafaa tena na ndio maana alikuwa akikataa kurudi chumbani akihofia kuchafua na huko nako. Lilijaa damu na bichi kuashiria alishaliosha na kubakia bichi. Inamaana siku nzima alikuwa amelalia maji. Akamuhurumia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Alichokifanya nikukusanya yale matandiko yote na kwenda kuyaweka kwenye mashine yakufulia. Akayaona yale maua pale chumbani wakati akifuta damu sakafuni, yakamtia hasira kabisa. Akaanza kuyakatakata kwa hasira na kwenda kuyatupa. “Haya ndiyo yameniponza.” Akalaumu maua. Akafanya kila kitu kwa haraka kisha akamfuata chumbani. Akamkuta akilia peke yake upande wa bafuni, damu zinachuruzika mpaka kwenye nyayo. “Niambie nikusaidie nini.” “Sijui natakiwa kufanya nini!” “Tuanze kwa kuoga kwanza, uvae nguo za kulalia na pullups. Nitakupa tena dawa, utajisikia vizuri.” Akamshika mkono mpaka bafuni. Akaamua kuoga naye kabisa. Wakaoga, Joshua akawahi kutoka yeye. Akamtafutia taulo jeusi kabisa ili asichanganyikiwe tena pindi atakapoona damu. Akahangaika naye mpaka akamuweka kitandani. Na yeye akafanya yake na kupanda kitandani. Akawa amegeukia kwengine amejifunika. “Umeshalala?” Akamjaribisha. Kimya. “Umenichukia?” Kimya.  

Akakumbuka heating pad, akamzungushia chini ya tumbo, akaanza kumsugua kiuno taratibu. “Asante, najisikia vizuri.” Akashukuru akiwa amelala vilevile amempa mgongo wala asigeuke. “Basi jaribu kulala. Ila nataka usisahau kuwa nakuhitaji Naya. Humu ndani maisha si sawa bila wewe mpenzi wangu. Nakupenda, na ujue sitabaki sawa bila wewe. Usinichukie.” Hakumjibu lakini akajua amemsikia. Baada ya muda akamsikia akihema kama aliyelala.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Usiku hakuamka hata mara moja, ila alfajiri na mapema Joshua yeye akaamka na kwenda kuabudu. Akaimba akipiga kinanda kwa sauti ya chini mpaka akamaliza. Alipojisikia anataka kuomba, akapiga magoti sakafuni kabisa, akawa kama amesujudu akaanza kuomba akajisikia kulia mbele za Mungu. Akamimina moyo wake mbele za Mungu, na kupotelea kwenye maombi. Akiwa anakaribia kumalizia akamuhisi Naya pembeni yake, anapenyeza mkono amshike kama alivyozoea kuomba naye akimshika mkono. Alifurahi Joshua, karibu ahitimishe kwa kusema Amen. Lakini akapiga magoti vizuri, akamvuta mikono yote miwili akaanza kuomba kwa sauti akiomba naye. Hakuomba muda mrefu ila alitubu kibinafsi, kisha akamuombea afya nje, amani kutoka ndani ya moyo wake na utulivu wa fikra. Akamuombea kwa upendo mpaka akamaliza. Akatamka baraka, umoja na upendo juu yao. Ndipo akahitimisha. “Amen.” Na yeye akajibu. “Amen.” Akamwangalia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Pole Naya wangu.” “Sasahivi najisikia vizuri. Sina maumivu ila usingizi.” “Nilijua ungelala vizuri. Nilikupa dawa za usingizi pia.” “Ndio maana nilipitiwa, sikukusikia wakati ukiabudu. Ungeniamsha!” “Nimekuombea.” Akatabasamu na kusimama. “Asante, lakini uwe unaniamsha niwe naomba mwenyewe. Baba Naya aliniambia sitakuwa salama mbali na magotini. Mungu peke yake ndiye atanifanya nibaki salama.” Joshua alishituka, ila akaogopa kumuuliza. “Na mimi pia aliniambia. Nakumbuka nilishabahatika kuingia naye kwenye maombi ya kufunga na kuomba kama mara mbili hivi. Baba yako alimpenda sana Mungu, Naya. Na wewe. Alikupenda sana.” Akatulia kama anayejaribu kukumbuka kitu.

“Twende tukaoge.” “Njaa inaniuma Joshua!” “Kwa kuwa jana hukula. Unajisikije sasahivi?” “Kidogo hofu imepungua. Niliingiwa na hofu kubwa, nikapaniki sana. Ila nimemuomba Mungu awe ananiambia kitu natakiwa kufanya ili nisiwe nakuudhi.” Joshua akazidi kuumia. “Akili yangu nahisi haina uwezo wa kufikiria kwa haraka. Kile nafikiria mimi ni kizuri kumbe si..” “Hapana Naya. Mimi ndiye niliyekosea mpenzi wangu. Amini akili yako haina tatizo na wala usijitilie shaka.” “Usiniambie hivyo kunifariji. Acha Mungu anisaidie tu.” “Hakika hapana. Mimi nilikosea. Hapakuwa na ulazima wa yale maua kwa wakati mzuri kama ule. Maua yangesubiri lakini si sisi. Wewe ndio ulikuwa ukifikiria vizuri zaidi yangu. Nilikosa.” Naya akatulia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Njoo ukae hapa kidogo nikwambie kitu.” Wakatoka sakafuni na kuhamia kochini. “Unaakili sana Naya. Sana. Mungu alikujalia kipaji cha ubunifu. Si kwenye mavazi tu. Hata tulipokuwa tukifanya wote kazi. Kwenye idara uliyokuwa ukifanya wewe kazi, ilikuwa ikinisumbua sana. Ulikuja wewe kwa muda mfupi sana, ukabuni kitu ambacho mimi nimeiga kutoka kwako ndio natumia mpaka sasa.” “Kweli Joshua?” “Kabisa. Sasahivi napata matokeo mazuri sana kutoka kwa watu wa chini yangu kutokana na wazo lako ambalo nililichukua, nikawapelekea watu wa IT nikawaambia walitengeze, likawekwa kwenye kompyuta kitaalamu. Imekua msaada sana mpaka kampuni nzima imeiga. Na sikutaka kuwa mwizi, walipokuwa wakinipongeza, niliwaambia wazi nililitoa kwako.”

“Sasa na hicho kipaji naona kipo mpaka nyumbani. Ulibuni usiku mzuri sana kwetu, mimi ndiye niliyeharibu. Nimejuta sana, na nimemsihi mungu anisamehe, akusaidie ujasiri wa kutengeneza kitu kingine kwa ajili yetu, na naahidi kukusikiliza. Sitakukatili kama jana. Naomba usinichukie.” “Nakupenda Joshua. Siwezi kukuchukia.” “Sasa kwa nini ulianza kuulizia pakwenda?” “Si kwa kukuacha, ila angalau kwenda kujiuguza kwa muda. Nilikuwa sijui kitu chakufanya nikaona nakuharibia vitu vyako.” Joshua akashangaa sana.

“Unamaanisha nini kusema unaniharibia vitu?! Si nilikwambia hapa ni kwetu?” “Kwenye ndoa, ndiyo. Lakini sasa hivi najua hapa ni kwako Joshua. Kuna diary yangu niliandika mambo mengi kipindi cha karibu na ndoa. Najua kwetu kulikuwa Kiluvya, hapa na kila kitu nilikukuta navyo. Mara ya kwanza nilipokugundua wewe ni nani na unavyomiliki, nilipaniki. Si ndiyo?” Joshua akatulia. “Niambie ukweli ili nisichanganyikiwe zaidi.” “Ni kweli Naya. Lakini naomba usipaite kwangu! Inaniuma na ninaona juhudi zangu ni bure kabisa. Nataka upaite kwetu na watoto Mungu atakao tujalia.”

“Na pia nimegundua ulisema hutaki tuwe na watoto mpaka baada ya miaka miwili ya ndoa. Si ndivyo?” “Naya!” “Ndivyo nilivyokuwa nimeandika siku na tarehe uliyokuwa umeniambia, sasa labda uniambie vinginevyo.” “Ni kweli.” Ikabidi kujisalimisha. “Kwahiyo sikuwa nikikukimbia, ila nilitaka kwenda kujiuguza mpaka nipone ili kukupumzisha.” “Kwahiyo na mimi nikiugua kwa muda mrefu utaondoka?” “Hapana Joshua! Najua unamajukumu mazito kazini. Sitaki ukwame kwenye kuniuguza kila mara. Halafu sikujua kama kuna dawa huwa natumia na kunifanya nijisikie hivi. Nilikata tamaa.”

“Nakutaka wewe ukiwa mzima, na mgonjwa. Wewe ni mimi. Ukiugua wewe, ujue na mimi naugua sema maumivu unakuwa nayo wewe. Tutakuja kuzungumza zaidi juu ya familia. Ila nenda ukale wakati mimi naoga kwa  haraka. Na naomba leo uwe na simu mpenzi wangu. Itanifanya nitulie kazini. Nipo kwenye kipindi kigumu huko, nahitajika sana.” “Hata sijui simu ipo wapi! Nitaitafuta.” “Niliipata. Na niliiweka kwenye umeme. Ipo chumbani juu ya meza.”

Akamsogelea zaidi. “Na nikirudi naomba unikumbushe ahadi zako zote ulizonipa, Naya.” Naya akaanza kucheka. “Usicheke bwana! Nahisi kuna kubadilikiwa.” “Mimi sikumbuki.” Naya akajibu akicheka. “Basi kazi yako ya leo. Huko ulikokuwa ukisoma mambo yako ya nyuma uliyoandika, basi leo ukasome zile ahadi zako zote ulizonipa. Ili tubakie ukurasa mmoja.” Naya akazidi kucheka. Akambusu juu ya mdomo, na kukimbilia juu chumbani, Naya akaelekea jikoni akilalamika. “Mimi nilidhani ananisogelea anibusu vizuri! Joshua naye!” Akajilalamisha Naya.

Kisicho Riziki, Hakiliki.

Akiwa njiani simu ya Bale ikaingia. Akashangaa sana, ila akapokea. “Ni asubuhi sana Bale! Kwema?” “Kwamba nakusumbua?” Joshua akatulia, hakumjibu maana aliuliza kwa jazba. “Kama unaona huna muda wa kupokea simu zangu, useme, nisikutafute.” Joshua hakujibu. “Maana unakua kama unaona nakubugudhi! Muda gani ulitaka kupigiwa simu?” Kimya. “Niambie sasa?” “Utakaponiona napokea simu yako. Muda na wakati wowote ule ujue nipo tayari kukusikiliza.” Akamjibu Joshua kwa utulivu tu. “Sasa mbona ni kama unalalamikia muda?” “Niliingiwa tu na wasiwasi juu yako Bale! Sikutegemea simu yako alfajiri hii. Nikusaidie nini?” Joshua akaamua kujishusha amtulize kwani kadiri alivyoongea alihisi hasira inampanda. Kimya.

“Bale?” Joshua akamuita taratibu tu. “Kwani wewe baba alikuachia wosia gani?” Hilo swali likawa pana sana, Joshua akawa hajui amjibu nini! Na kwa nini ampigie simu mida hiyo kuuliza swali kama hilo!

~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment