Kwa Jema.
Siku ya Jumapili.
Aliamka
amejawa furaha huyo, kama aliyetunikiwa ulimwengu. Maandalizi ya kwenda
kanisani na kukutana na James yakaanza. Nguo zikawa si nzuri tena. Jema mjua
mavazi asubuhi hiyo akawa hana nguo. Ikawa hivyohivyo kwa James. Alibadilisha
mashati na suruali karibu kugairi kwenda kanisani. Kila nguo ikaonekana haitamuakilisha
vizuri. Gafla viatu vyake vyote vikawa navyo ni kama Geb amevitia sumu. “Hata
hivi havitaniwakilisha vizuri.” Alijisemea James akiwa amevaa shati jingine
na viatu. Swala la suruali ndilo aliamua kuachana nalo kabisa, aliona
vinamchanganya zaidi. Akabaki amevaa shati na viatu akihangaika, na kuchelewa
miahadi na mwanamke aliambiwa ni mwiko.
Saa tatu
na dakika 45 alikuwa ameshafika sehemu ya kuegesha magari akimsubiria Jema
waingie wote kanisani. Nne kamili Jema akawa anavuta gari yake na yeye sehemu
ya kuegesha. Akampigia simu James. “Nipo tu ndani ya gari
nakusubiri wewe.” “Si ulisema nisiwe nakimbilia vitasa?” Wakaanza
kucheka. “Nakuja mama.” James akatoka garini akafuata maelekezo mpaka akamfikia.
Akamfungulia
mlango. “Yaani kwa kukuangalia tu hapo ulipokaa, umependeza sana.” “Na wewe
umependeza sanaaaa. Halafu unanukia vizuri!” “Huko kupendeza sanaaaa! Kunaanza
kunitia wasiwasi. Watafikiri nimevunja kabati.” “Kumbe hujavunja?” “Msema
ukweli mpenzi wa Mungu. Nimevunja.” Jema alicheka sana.
“Ila
umependeza sana James. Umebadilika sana usoni, ukavutia.” James akacheka. “Hizi
sifa zinavyorudiwa! Basi Jema. Sitoi tena ndevu. Zitabaki hivihivi.” Jema
akazidi kucheka na kushuka garini. “Nimeshajua kama ni zawadi ya viatu, viwe
vya juu. Au nimekosea? Maana sijawahi kukuona na viati vya chini hata mara
moja!” “Hapo umepatia. Na ninapenda viatu kuliko chochote. Ni kama ndio udhaifu
wangu. Huwa naanza kununua viatu kwanza, ndipo linakuja swala la nguo.”
“Pochi?” “Nakuwa nimeshaishiwa pesa, nabaki kurudia rudia pochi.” James
alicheka sana. “Nguvu yangu ndogo.” “Itabidi tuongeze. Twende kanisani kisha
uniambie ni nini kingine unapenda mbali na viatu.” “Kuwa na wewe hapa.” “Hicho
umeshapata. Nataka kujua ambacho huna au unacho lakini ungetamani kuwa nacho
zaidi.” “Wewe.” Jema akajibu kwa haraka, James akamwangalia na kucheka
taratibu. “Mbona sasa hujibu!?” “Tukitoka kanisani. Twende kwanza tukamuabudu
Mungu.” Wakaingia ibadani.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ibada ikaisha
muda mzuri tu na ilikuwa nzuri sana. Wote wakapapenda hapo. “Sasa sisi huwa
kila jumapili, tunakutana kwa kina Magesa kwa chakula cha mchana. Imekua kama
desturi yetu kwa familia, kuwa angalau kwa juma tunakutana mara moja.” “Hiyo ni
nzuri sana. Basi acha mimi nikuage, nisikucheleweshe.” “Sikuwa nimemaliza Jema!”
Jema akacheka lakini alishakuwa amenyongea baada ya kusikia hivyo. Akajua James
ndio anamuaga.
“Samahani
sikusikiliza mpaka mwisho.” Akaongea akishindwa hata kumwangalia, na cheko lote
likamuisha. “Hamna neno. Lakini nimewaambia mimi nitakwenda jioni, ili kama
unanafasi twende sehemu tukae wote. Utakapokuwa tayari kwenda nyumbani, ndio na
mimi niwapitie kuwasalimia.” “Mimi nipo tu James. Usiharibu ratiba zako kwa
sababu yangu. Nenda tu. Sisi tunaweza kupanga kukutana hata wakati mwingine.
Familia kwanza.” Akamalizia Jema akiweka msisitizo ambao wazi alionekana
hakuwa tayari kuachana naye kwa wakati huo.
“Wewe
unaratiba gani baada ya hapa?” “Naona nitarudi tu nyumbani kupumzika.” “Ni sawa
tukienda sehemu tukakaa kidogo?” “Mimi ningependa James, lakini sikutaka
kukufunga.” “Hamna neno. Basi twende sehemu tule, halafu tutafute sehemu ya
kukaa kidogo. Unahamu ya kula nini?” “Kuku wa Makange. Nafahamu wanapotengeneza
ila sio kwenye hoteli kubwa kama ile uliyonipeleka jana. Si pahadhi.” “Twende
hukohuko kwenye nyama vumbi. Mimi sina shida.” Hilo nalo likamfurahisha James,
kwamba Jema si wa mahoteli makubwa kila wakati kama Geb alivyomwambia. Kwamba
hata kwenye nyama choma za mtaani anaweza kumpeleka! Pengo la Nanaa likaanza
kuzibwa taratibu.
Wakatoka
hapo mpaka Brekipointi kila mtu na gari yake. Jema akashuka garini na
kumsubiria James mpaka akafika hapo, hapakuwa mbali na kanisani. James akaegesha
na kuteremka garini, Jema akamsogelea. Ila akamuona kama amepoa zaidi, asielewe
ni nini. Furaha aliyokuwa nayo ikawa imebadilika kabisa. Akaona ampe muda,
asimkere kwa maswali. Wakaongozana mpaka sehemu ya kula.
Wakatafuta
meza yao sehemu nzuri, wakakaa. Muhudumu akafika kwa haraka tu. Wakashangazwa
maana watu walikuwa wengi kuashiria walishatoka ibadani wapo hapo kwa mlo.
James akabaki akimwangalia Jema, alionekana yupo pale lakini hayupo. Akaweka
mkono mezani akiwa ameufungua huku akimwangalia Jema aliyekuwa amepotelea
mawazoni akiangalia sehemu ya barabarani kwani ilikuwa nje tu, hata hakuona
mkono wa James.
Muhudumu
alipoleta vinywaji na kuwakaribisha ndipo akaona mkono wa James pale mezani
akiashiria aweke na wake pale. Jema akajishauri, James akijua amemuelewa.
Akaweka kiganja chake taratibu juu ya kiganja chake akabaki akiangalia ile
mikono yao, James akafunga vizuri na kuuminya taratibu, Jema akacheka taratibu
na kumwangalia. “Mbona upo mbali, unaniacha hapa mwenyewe?” “Nipo.” “Mwili
ndio, ila mawazo hayapo na mimi. Unawaza nini?” Akacheka kama anayesita.
“Si
unajua unaweza kuzungumza na mimi chochote kama vile ulivyozungumza na mimi
jana au kabla?” “Sipendi kuonekana kama wale wanawake needy.” James
akatulia tu akimsikiliza akiwa amemuelewa. “Yaani over attach kwako
ukaniona mzigo. Nakuganda na kukufanya ushindwe kufanya mambo yako au
ukashindwa kuwa na watu wako wa muhimu. Sitaki kukuingilia na ratiba zako za
kifamilia. Tafadhali usijisikie nilazima kuwa hapa. Mimi naweza kuagiza chakula
nikala hapa au nikakibeba nikaenda kula nyumbani. Wewe ukaendelea na ratiba za
familia.” Jema akahitimisha James akimsikiliza tu.
Kwanza
James alikuwa amependeza na kujipangilia. Hapo alipokuwa amekaa amekaa vizuri
kama mwanaume anayejitambua. Msafi anavutia. Jema akajiona kama kipanzi kwake.
Kama asiyemstahili huyo James. Uzuri wa James ni kama ulipitiliza sana kwa
viwango vya Jema ambaye kwanza hawakuendana rangi na James. James alikuwa
mweupe wa kupitiliza kama mdogo wake Nanaa na watoto anao zaa Nanaa. Na hivyo
alivyotengeneza nywele na kulambishwa, akawa kama chotara. Akaongeza utulivu wa
pesa aliyo nayo, na elimu ya wanaume wote wawili mfano wake wa mapenzi. Geb na
Joshua. Jinsi wanavyofanyia wanawake zao, James alikuwa ameiva ila tu hakuwa
tayari kwa mwanamke. Jinsi alivyojibeba hapo kwa Jema, akabaki akimbambaisha
Jema. Kwanza ile hali yakumshika mkono kwa namna ile, ilishamsisimua vilivyo.
“Unakumbuka
mimi ndiye niliyekuomba tuje wote hapa?” Kidogo Jema akapoa, na kuinama James
akiwa bado amemshika mkono. Akamvuta kidogo kama akimuita. “Jema! Mimi
nataka kuwa hapa na wewe na wala si kwingineko. Najiona nipo sehemu sahihi na
mtu sahihi, labda uniambie vinginevyo.” “Mimi nipo, ila sitaki kukuvurugia
mipango yako.” “Ushajiuliza pengine ndio unaitengeneza?” “Sijui Jamesi!” “Basi
naomba uwe na amani. Huniharibii chochote. Sawa?” “Sawa.” “Basi karibu
kinywaji.” Akamuachia mkono wakanza kunywa, walishaagiza na chakula. Wakaletewa.
Pakawa na utulivu fulani hivi wakila.
“Umependa
nyama yao?” Jema akauliza kwa kujali. “Hapa pia ni viwanja vyetu na Nanaa.
Tukimuongeza Geb, anabakia mtizamaji akiwa ameonywa na mkewe asiongee
chochote, atulie akinywa maji mpaka tumalize. Kwa hiyo huwa napenda nyama yao
sana tu.” Jema akacheka. “Sikujua.” “Sasa kuna sehemu nyingine hiyo, chini ya
hapa kidogo. Kimara huko. Wanachoma nyama, hatari. Huko ndiko
tunapapenda zaidi.” Jema akaendelea kula na tabasamu usoni kama anayejaribu
kufikiria.
“Uliniambia
ukitoka hapa unarudi nyumbani. Tunaweza kwenda mahali?” “Wapi?” “Nanaa
anavyosema eti ni sehemu yake alipagundua yeye. Anaita ni Pa-siri. Lakini
nikagundua na Geb naye aliambiwa hivyohivyo na Joshua naye alishaelekezwa.”
“Kwa hiyo si siri tena?” Jema akauliza akicheka. “Sidhani. Ila kweli ni
patulivu. Twende tukakae hapo kidogo ndipo nikuache ukapumzike. Au tena mimi
ndio nageuka kuwa Needy?” “Hapana bwana James! Mimi nisiye na mipango
ndio sitaki kuwa Needy.” “Huwa unakwenda kumtembelea mama?”
“Inategemea nipo kwenye hali gani. Kama kipindi hiki nilikuwa nikimkwepa.”
“Sababu ya Temu?” “Aisee nimekukubali James! Unaakili ya kufikiria na
kuunganisha matukio.” Wakacheka.
“Namuogopa.
Namkwepa. Sitaki arudie kuniambia, aliniambia, sikumsikiliza. Yeye anawajua
watoto wa mjini kwa kuwaangalia. Wanaume hawana maana. Wana mwanzo mwisho
hawana. Hakuna waoaji. Wachezeaji watupu. Walioko kwenye ndoa, wanataka wasio
kwenye ndoa. Najitafutia matatizo na lazima nije kumkumbuka. Na mengine mengi.”
“Daah! Mpaka hapo tu yameshakuwa mengi sana.” “Basi ndio ujue ndio maana
namkimbia. Ila pia na yeye nilimkopa pesa nyingi sana sababu ya huo
ujenzi.” “Jema!” “Ilikuwa shuguli James! Siwezi kuhema Temu akitaka pesa.
Nilikopa kila mahali. Sasa najua mama atataka kujua hiyo nyumba ilipofikia.”
“Na huna pakuonyesha!” “Ewaa! Ndio maana najificha kwake. Ila anatujali sana.
Hilo si tatizo kwake. Anaweza hata akanisamehe hiyo pesa. Anatupenda sana.
Asiponisikia hata siku tatu atapiga au kutuma ujumbe kujua kama nipo salama.”
James akanyamaza mpaka wakamaliza kula. Akamwambia amfuate kwa nyuma mpaka hiyo
sehemu waliyotambulishwa na Nanaa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ilikuwa
upande wa baharini. Jema akacheka maana walikuta watu wengine. “Usiwe na haraka
sasa. Sehemu yenyewe bado.” Akamuona James anavua viatu na soksi. “Haiwezekani!”
Jema akashangaa. “Nakuahidi utafurahia hii baridi yake. Vua tu, utajisikia
kupumzika. Kwa huko tuendako kuna kukanyaga na maji kidogo, utaharibu viatu
vyako.” Aliposikia hivyo, Jema mpenda viatu, akavua kwa haraka sana na kushika mkononi.
Wakaanza kutembea upande wa bahari wakiifuata hiyo sehemu. Kweli wakakuta kama
kijipango kwa ndani.
“James!”
“Si nilikwambia! Sasa tukae hapo ndani kidogo.” Wakaingia hapo, Jema akatafuta
sehemu akakaa wakiangalia maji kwa mbele kidogo tu maana ni kama maji
yalizunguka hapo, mtu anaweza asitake kukanyaga maji kuingia huko ndani. Kwa nje
hakuonekana kama kuna kapango kwa ndani. Kwa haraka usingependa kufika huko.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
{Nanaa alipagundua
kwenye Simulizi ya Ni Wangu! Akiwa rafiki na kina Zena. Akataka kumpelekea
Geb kwa mara ya kwanza, lakini Liz aliyekuwa mpenzi wa Geb kwa wakati ule, naye
akafika nyumbani kwa Geb na kumchukua Geb wakiwa wanajiandaa kutoka na Nanaa. Nanaa
akaachwa, Liz mwenye kisu kikali akaondoka na Geb. Akabaki ameumia sana.}
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
James
akaenda kukaa pembeni yake. Wakatulia. Kimya, bado Jema yule wa asubuhi kabla
ya kupewa taarifa za James kuwepo nyumbani kwa kina Magesa kila jumapili, hakuwa
amerudi. Alipoa. James akamuona ni kama anasubiria muda, akijua baada ya muda
mfupi sana, James ataondoka tu. Akamsukuma kidogo kwa bega. Jema akacheka na
kumwangalia, macho yakagongana. “Mimi nataka uwe needy kwangu.” Jema akacheka
taratibu na kuinama. “Umenisikia?” Jema akamwangalia. “Sitaki unichoke.” “Kwako
sitachoka. Nigande utakavyo, na ukiona kitu hujakipenda, au unataka
kifanyike tofauti na ninavyokwambia, nakupa ruksa yakutoa mapendekezo.
Tutajadiliana. Na mimi naomba ruhusa ya kuwa huru kutoa mapendekezo kwako.
Halafu tufikie maamuzi pamoja. Usikae ukinyongea kwa maamuzi ya upande mmoja,
yaani yangu tu. Ukafikiri ndio nakuwa nimechora mstari. Mimi si mbishi sana
japo ninakuwa na msimamo kwenye mambo fulani fulani. Hayo huwa
najitahidi kusimamia bila kukubali kubadilika.” “Mambo gani?” Jema akauliza
akitamani kujua.
“Nitakwambia
wakati mwingine. Ila nataka kujua kama umeelewa hili.” “Nimeelewa. Na samahani
James. Nilikuwa nimejiandaa kuwa na wewe leo siku nzima ndio maana niliishiwa
nguvu uliponiambia huwa unaratiba ya jumapili. Nafikiri nilipanga nikidhania
upo kama mimi tu. Huna mambo yakufanya siku za jumapili.” “Usijali. Kuanzia leo
tuwe tunazungumza.” “Hapana. Usibadili ratiba zako kwa sababu yangu.
Nitaliheshimu hilo. Na nitaacha kupanga mambo ya mbele kichwani mwangu
nikikujumuisha na wewe.” “Hapo tena umeshaharibu.” Jema akaanza kucheka.
“Mimi
nakusaidia James!” “Kwamba hujaelewa swala la kutaka WEWE uwe needy kwangu?” Jema
alicheka sana. “Basi nitakuwa nikikushirikisha.” “Na niwepo kwenye hiyo
mipango.” “Sasa huoni kama nitakuvurugia ratiba zako?” “Ndio alamu yakunitaka nianze
kujipanga upya. Itabidi tutengeneze ratiba mpya.” “Nanaa na wengine waliopo
kwenye maisha yako hawatanichukia?” “Itabidi waelewe tu. Ilimradi kusiwe na
kubadilikana Jema. Sipendi drama za kijinga za mapenzi, kwa kuwa
nishaona watu waliotilia umaanani kwenye mahusiano, na wakafanikiwa,
naomba na kwetu iwe hivyo.” Ikamgusa sana Jema mpaka akatulia kwa muda.
Ilikuwa
sentensi iliyojaa maana kubwa, na James akaiongea kama Jema alishafahamu
wapo kwenye mahusiano. “Umenielewa Jema?” “Hapana. Kwamba unaanzisha mahusiano
ya kimapenzi na mimi?” Hapo James akagundua ameongea lililokuwa
likiendelea moyoni mwake. Akalitamka bila kufikiria. Akajilaumu amefanya haraka
sana. Akatulia kabisa. Akahisi ameropoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Hakuwa
hata amemtongoza! Akapoa kabisa na kukumbuka ushauri wa Geb. Asiropoke na awe
makini na maneno yake. Jema akamuona amepoa haswa. Moyoni kwa James
alishampitisha Jema. Jema kumganda kuanzia usiku uliopita. Wakati mzuri
waliokuwa nao mpaka kulala usiku mwingi, kukamfanya James ajisikie wameshakuwa
kwenye hiyo hali kwa muda mrefu na wameshakuwa kitu kimoja kwani kwa muda mfupi
sana walishaendana kwenye mengi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Jema
akatulia kabisa kumpa nafasi atafakari. Hata yeye hakutaka kucheza tena. Na
hakutaka kupoteza muda akijipa tumaini ambalo halipo. Akatulia na
kupotelea mawazoni. Wote kimya. Baada ya muda James akamsukuma tena taratibu
kama kumtingisha. “Upo?” “Nipo.” James akabaki akimwangalia. Akacheka na
kujiinamia. Akaokota jiwe dogo pembeni akaanza kuchora mchangani.
“Unakumbuka
siku ya harusi ya Kumu?” Jema akamwangalia na kukunja uso kama ambaye anataka
kujua anatakiwa akumbuke nini. “Nilikukuta sehemu peke yako kama uliyekuwa
umejificha, umeshika simu ikawa kama umetoka kulia.” Jema akakumbuka.
Akacheka taratibu na kuinama tena. “Nikakuuliza upo sawa! Ukafikiria kwa haraka
na kunipa jibu la haraka kuwa katika vitoweo vya pale, ulipenda sana Crub. Ukaniambia
hujawahi kula Crub waliotengenezwa vizuri kama wale. Ukaniambia unanishauri na
mimi nikale, nisipitwe. Ukaondoka na kuniacha palepale nimesimama.” Jema
akabaki kimya.
“Najua
umekumbuka. Kwanza nataka kujua ulikuwa ukilia nini ndipo niendelee na
ninachotaka kukwambia.” Akamuona
anajifuta machozi. “Ilikuwa ni nini Jema? Niambie tu.” “Nilikuwa
nimetoka kuzungumza na Temu. Akanitukana sana. Ikaniuma sana, na ni kama
sikujua chakufanya tena James. Kama na mimi kuomba, niliomba sana. Kama ni
uaminifu kwa Mungu niliweka kwa asilimia zote. Nikabaki nikimsikiliza Temu jinsi
anavyoweza kunitukana kirahisi tu bila hata huruma, nikiwa sijakosa! Sikuweza hata
kumjibu, mpaka akamaliza na kunikatia simu. Nikabaki kumuuliza Mungu ni kipi
cha tofauti mtu kama Naya amefanya mbele zake yeye Mungu, tofauti na mimi?” “Pole sana
Jema. Kwa nini!?” Jema akajifuta machozi.
“Swali
langu lipo na sehemu mbili. Japo moja ni kama nimeshapata jibu. Juu ya Naya. Ila
ya pili ni kwa nini Temu akutukane siku kama ile!?” “Kwa upande wa Naya, ni vile
Joshua alivyoweka uthamani kwake. James, Joshua anajua kumuenzi yule msichana! Sijawahi
ona mimi hapa duniani. Na si kwa kujitahidi. Mimi nimefanya kazi na Joshua kwa
karibu sana, nimemuona jinsi anavyokuwa linapofika swala la Naya. Anampenda
kuliko nafsi yake. Na japokuwa Joshua Kumu yupo busy. Nikisema busy, amini yule
mtu yupo busy. Lakini James, wakati wote anafikiria jinsi gani ya kumfurahisha
Naya, lakini mimi natukanwa kama mpuuzi tu! Niliumia sana.”
“Naomba
usilie Jema. Na Temu?” “Temu ni mengi, lakini pia alikuwa akinitukana na kuniambia siku
ile ndio siku nzuri kwangu, nipo huru. Najiuza mbele ya wasomi na wenye pesa
nikijionyesha kama mwanamke,…” Jema akajaribu kufikiria neno sahihi. “Sijui
niwekeje hili neno aliloniambia! Mpaka naona aibu.” James akamuona
anatingisha kichwa kwa masikitiko. “Acha tu.” “Tafadhali
niambie. Usinifiche tena. Maana nilikaa nikijiuliza na kuumia sana. Maana ulikuwa
umependeza. Halafu ulijitoa Jema! Mpaka ukatushangaza.” Jema akacheka tu na
kujifuta machozi.
“Kweli! Ulikuwa
busy sana siku ile ukashindwa hata kukaa!” “Wewe ulijuaje?” “Kwa sababu
nilikuwa nikikufuatilia!” Jema akamwangalia na kuinama kuendelea kuchora.
“Baada ya harusi tulibaki mimi, Kumu, familia ya Geb. Mama yake na Nana. Pamoja
na baba yake Nanaa, tukiweka tathimini ya mwisho na kutaka majina ya
waliohusika kufanikisha shuguli nzima siku ile tutume kadi za shukurani na
zawadi kidogo. Geb akauliza wewe ulikuwa kamati gani? Ndipo Kumu akasema
hakutaka kukupa kazi maalumu akitaka macho yako yawe kila mahali ndipo akasema
ile sifa yako na nyingine. Kuwa, ‘Jema hawezi kukubali jambo limuharibikie
mbele ya macho yake’. Na ndipo aliposema, ‘ni wale wanawake ambao
ukiwapa mahindi kwa ajili ya chakula, ujue utakuja kukutana na shamba la kuvuna’.
Ndio maana alikutaka wewe uwepo pale uangalie kila kitu akiwa na uhakika hapata
haribika jambo hata moja. Na wote pale tukaafikiana ni kweli ulifanya zaidi ya
kawaida. Kumu akasema yeye hashangai, ndio maana yeye asipokuwepo sehemu
anayotakiwa kuwepo, hana wasiwasi kama wewe upo.” Jema akacheka taratibu.
“Lakini
ukumbuke hapo sisi tulishafahamiana ila kikazi. Na wakati wote ulijibeba kwangu
kikazi tu. Kama nilivyokwambia, hata salamu yako kwangu ilikuwa ikionyesha ni
kiungo cha mazungumzo ya muhimu. Unakuwa ukija ofisini kwangu upo na muda mfupi
na agenda nzito uliyoambiwa na yule sekretari mimi naweza kukusaidia kwa
kuwa nafahamiana na wale wahusika wa pale kwa karibu.” Jema akacheka.
“Yeye
ndiye aliyeniibia siri kuwa nikitaka chochote kwa wale watu wa Utawala,
nikwambie wewe. Nikamuuliza mbona wewe upo kwenye mambo ya simu huusiki na
maswala ya Utawala? Akasema anauhakika na anachoniambia, nije kwako,
utanisaidia. Ndipo nikaja kujitambulisha kwako. Nikashangaa mmeishia kuwa
karibu na Kumu, mimi nikawekwa pembeni!” James akacheka sana.
“Halafu
bwana sijui ilikuaje na Kumu! Na yeye tukajishangaa kama tumeshakuwa ndugu!
Kuja kukutana na Geb na Nanaa, akataka nimtambulishe kwao, ndipo undugu
ukanoga. Akafanyika mmoja wa familia. Tukajikuta ni ndugu tunaoendana kwenye
mengi. Ila ni nini nataka kukwambia?” Jema akatulia kumsikiliza.
“Sijakurupuka
kwako, ila sikujua ni jinsi gani ya kukufikia. Nilishavutiwa na wewe mwenyewe.
Nikaja kuzisikia sifa zako. Nikajiambia mbona huyu ni kama ananihusu!
Ila nikaja kusikia tena upo kwenye mahusiano yanayotarajiwa kuwa ndoa. Basi
nikapoa. Ndio maana uliponikaribisha chakula, nikawa kama nimekwama tena. Nikijiuliza
huyu mchumba wa mtu tena vipi! Halafu Jema ninayemfahamu mimi si nje ya
kazi! Halafu tena ikawa natakiwa nikacheze game kwa kina Magesa, ndipo ikabidi
nitulie nikusome vizuri kujua ukaribisho ule ulikuwa upi. Ulipokataa kwa maneno
lakini moyo wako ukazungumza kingine kama leo pale kanisani.” Jema alicheka
mpaka akainama kujificha.
“Mimi
nilikuwa namaanisha James.” “Ila moyo wako ulizungumza vingine nikazidi
kuvutiwa na kukupenda zaidi.” Hapo Jema akaacha kucheka kabisa. Akabaki
kimya ameinama kisha akamwangalia. “Sijakurupuka Jema. Pata muda na wewe
unichunguze ujue kama na mimi ni mtu unaweza kuja kuishi naye. Ukipata jibu,
basi tuendelee kuanzia hapo. Ila kwa sasa naomba tuwe wote kwenye mahusiano. Na
kujibu swali la kwanza ambalo uliliuliza, naomba yawe ya kimapenzi.
Kwamba kusiwe na mchumba Temu tena.” Jema akacheka.
“Yaani
huyo samehe. Na pesa ulizompa iwe ndio sahau ili tuweze kuendelea mimi na wewe
tu. Au sina vigezo vya kuwa mume? Maana mimi nilikuwa nikikufuatilia kwa sababu
niliona unavyo vigezo vya mke wangu.” Jema kimya. “Eti Jema?” “Nikwambie ukweli
James?” “Hilo nitalifurahia sana. Kusiwe na usiri, vificho na kudanganyana kati
yetu.” “Sawa. Ila nataka ujue huwa napata amani na utulivu sana nikiwa
na wewe ndio maana natamani kuwa karibu yako tu. Natulia mpaka nafsini mwangu. Nakuona
una hekima yakunifaa mimi.” James akacheka taratibu.
“Kweli.”
“Basi tujipe muda tuone hizi hisia zitatupeleka kwenye hatua ipi ya maisha. Ni
sawa?” “Sawa. Mimi nitatulia James. Nishang’atwa na nyoka! Sitaki tena.” “Kumbe
bora alipita Temu hapo ili kukushikisha adabu!” Jema alicheka sana. Angalau
wakafunguka na kufurahia mwanzo wao mpya. Walishitukia giza linawafuata hapo.
Ikabidi kuondoka baada ya kupiga picha nyingi sana siku hiyo.
Kwa Bale.
Usiku
wakati amerudi nyumbani anaingia ndani, akamuona tena Malon ni kama anatoka
chumba anacholala yeye, akielekea kilichokuwa chumba chake. Bale alishituka
sana ila akajikaza na kukimbilia kwenye hicho chumba alichomuona akiingia.
Akakuta hata mlango umefungwa, tena alifunga yeye mwenyewe Bale. Akaanza
kusukumana na mlango akisema Malon amemfungia kwa ndani. Hata akili yakusema
atumie funguo afungue hakuipata. Akasukumana na mlango akipiga mateke mpaka
mlinzi akaingia akidhani kuna tatizo. “Kuna nini bosi?” “Hataki kufungua
mlango.” Mlinzi akasogea. “Nani?” “Wewe saidia, acha kuuliza ujinga.” Basi
mlinzi naye akaongeza nguvu mpaka wakafanikiwa kuvunja mlango. Akakimbilia
mpaka humo ndani chooni na bafuni, hapakuwa na mtu. Mlinzi akashangaa sana.
Akahisi amezidisha bangi maana alivuta sana siku hiyo.
“Hakika
nimemuona ameingia humu ndani.” “Nashauri upate muda wa usingizi bosi. Kukiwa
na tatizo nitarudi.” Akatoka na kumuacha Bale na sintofahamu kubwa sana.
“Huwezi kunivizia na kuniua mimi.” Akaongea kibabe akimwambia Malon endapo
amejificha mahali. Alipojaribu kusogea, kumbe ameumiza mguu. Akajikaza na kujivuta mpaka sebuleni. Bangi ikamsaidia
kulala vizuri.
“Usijekuwa unatoka
kutafuta ulichokiacha ndani ambacho wenzako wanakililia na kukihangaikia
huko nje unakokimbilia.” Bale alishituka sana kwani kwa hakika alimsikia
baba yake akiongea masikioni kwake tena kwa sauti iliyoweza kusikika kwa wazi
kabisa. Akakaa akihema kwani ndio alikuwa amepitiwa na usingizi mzito, kwa
kutolala usiku uliopita. Akakumbuka kuambiwa maneno kama yale. Kumbukumbu
ikakataa kumkumbusha msemaji kwa hakika. “Haya maneneno aliniambia Naya, au
baba!?” Akabaki akijiuliza kwa sauti, akihema kwa nguvu.
Akataka
atoke hapo aende kunywa maji. Akagundua mguu unamaumivu makali sana, na ni kama
umejaa. Akajishika akajisikia maumivu. Akachechemea mpaka alipoweza kupata
ganja, akapuliza hapo usiku kuchwa akishindwa kulala kwa hofu. Akamkumbuka mama
yake. Bale akaanza kulia peke yake. Akatamani kama mama yake angekua hai.
Akakaa hapo kochini akishindwa hata kusogea. Alipotaka kwenda chooni ikabidi
kutambaa kwa magoti kwani mguu ulikataa kabisa.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Malon mtoto wa Mjini. Kweli alikufa au yu hai anacheza na akili za
Bale tu.
Au
Bangi inasaidia dhamira kutengeneza uhalisia kwa Bale?
Inaendelea….
0 Comments:
Post a Comment