KISASI KWA MALON.
Bale
alitoka pale, akarudi Kunduchi nyumbani kwa Malon, akaambiwa ameingia hapo muda
si mrefu. Akazidi kuumia kwamba ni kweli ametoka jela. Akaingia ndani bila
kutaka fujo naye. Akamkuta ametoka kuoga. Wakazungumza maswala ya biashara tu.
Wala hakumzungumzia Naya kabisa, ndipo Bale akajua bado anamipango na Naya,
hataki amuingilie tena. Na yeye hakumtaja kabisa dada yake. Akampa majukumu
yakufanya hapo Dar, Bale akatoka hapo, akamuacha akipumzika. Mipango yakumtoa
Dar, na kumfanya Malon arudi Mbeya ikaanza.
Akazungumza
na Mbaki aondoke pale anapoachwa kama mlinzi wa mali yote kwenye mji wa Malon
huko Mbeya kwa kumwambia Malon kuwa amepatwa nadharula, lazima aondoke ili
Malon mwenyewe arudi. Bale akamlipa pesa nzuri sana, akijua Malon hamuamini mtu
yeyote na pale isipokuwa Mbaki tu, kwa hiyo lazima atarudi kwa haraka sana. Na
kweli. Wakati anarudi nyumbani Kunduchi, Malon akawa anamuga kuwa lazima arudi
Mbeya kwa haraka, Mbaki amepatwa dharula. Hilo likamfurahisha Bale.
Malon
anatoka tu Dar, Bale naye akamfuata nyuma baada ya kama masaa mawili tu
akihofia asije akamchelewa, akaweka mambo sawa huko Mbeya kwa haraka, na kurudi
tena Dar kwa Naya. Bale aliendesha mpaka alipofika Mbeya mjini. Akanunua
petroli nyingi, madumu mengi yakutosha, ndipo safari ya kuelekea kwenye mji wa
Malon ikaanza tena akiwa ameshajipanga vizuri tu.
Mida
anafika kwenye mji wa Malon, alijua kwa hakika Malon atakuwa na yeye amefika na
amelala kwa uchovu wa rumande. Hakutaka hata papambazuke. Gari aliyokuja nayo
mida hiyo, ambayo nayo ni ya Malon aliyokuwa akitumia Bale kwa shuguli zake
binafsi na anazotumwa na Malon akaegesha mbali kidogo ili Malon asimsikie akija
hapo na pia kumsaidia kukimbia baada ya kufanya yake.
Akaenda
moja kwa moja mpaka sehemu lilipo ghala lake. Sasa kwa kuwa mbwa walishamjua
Bale, na akawa amewaletea nyama aliyokwisha tia sumu, walipomuona, hawakupiga
kelele kabisa wakati anaingia hapo. Akawapa ile nyama yenye sumu, wakafa wakati
akibebelea madumu ya petrol na kumwaga kuzunguka ghala nzima la Malon. Kisha
kuzunguka kijijumba chote alicholala Malon na mlangoni pia.
Akafunga
komeo taratibu analopenda sana kutumia Malon kila anapotoka hapo na kuweka na
kufuli ili mtu asiingie kwenye hicho chumba chake endapo hayupo. Akiwa ndani
kufuli huwa nalo ndani. Sasa Bale akalirudishia hilo komeo na kufuli ambalo
alishanunua wakati akinunua hiyo petroli. Tena akarudiarudia kumwaga petroli
nyingi kuzunguka hiyo nyumba mpaka akaridhika.
Wakati
Malon yupo kwenye usingizi mzito, uchovu wakulala rumande na kuendesha safari
ndefu, Dar mpaka Mbeya bila kupumzika, akasikia mtu anamgongea dirishani. “Malon!
Malon!” Bale akawa anamuita. “Nini?” Malon akaitika akisikika alikuwa
usingizini. “Usiku huu wa leo, nakulipiza kwa kumuua baba yangu
kikatili. Ulichomfanyia Zayon kiumbe asiye na hatia, bibi na Luka. Usiku wa
leo, utaonja kile walichoonja wao. Nakwambia, ili wakati ukiteketea hapo ndani
kwa moto, jua Bale AMEKULIPIZA.” “Unaongea nini wewe!?” “Na bila wewe kuondoka hapa
duniani, Naya na mimi wote tutakuwa watumwa wako milele.” Bale akaendelea.
“Sasa,
sasahivi nasimama nafasi ya baba, kumtetea Naya. Hii dunia itakuwa
salama sana bila wewe Malon.” “Acha upuuzi wewe.” “Kama
unafikiri ni upuuzi vuta harufu uniambie kama hupati harufu ya petroli! Eneo
lako zima, mpaka ndani ya dirisha hapo ulipo nimemwagia petroli. Nikitupia
njiti moja tu ya kiberiti, wewe na mali zako zote ni jivu. Angalia mafuta hapo
dirishani.” Malon akakurupuka kwa haraka na kusogelea dirishani akagusa kwa
kidole, pamoja na harufu, ndipo akajua Bale hatanii. Akakimbilia mlangoni.
Ukakataa kufunguka. Akajua Bale amemfungia kwa nje.
“Naweza
kukufungulia endapo utaniambia ukweli ni kwa nini Naya amegeuka kuwa tahira.
Asiye na kumbukumbu.” “Nifungulie nikwambie.” “Unanipotezea muda Malon na ujue
unawajibika na kilio cha mama yako. Wewe unafikiri kutokuwepo kwa Mbaki leo ni
bahati mbaya? Nilimtoa hapa kusudi ili nikuweke shule wewe uliyekimbia
shule na kudharau waliosoma.” Malon akarudi tena kusukuma malango kwa nguvu
tena na tena mpaka akachoka.
“Kama
umemaliza naomba tuendelee. Na safari hii nakupa dakika moja tu Malon. Niambie
ukweli lasivyo nawasha moto.” “Sawa. Naya alianguka akagongesha kichwa kwa
nguvu, mpaka anakuja kuamka akawa hajitambui tena.” “Hapo nimeshaelewa kuwa
ulimgongesha dada yangu kichwa kwa nguvu. Haya, dawa gani ulimpa? Na usiniambie
ni za usingizi maana amepimwa, akaonekana ni madawa ya kulevya ila hayajulikani
ni yapi.” “Nilikuwa nikichanganya tatu ili kuingia mwilini mwake na kuzoea damu
yake kwa haraka.” Akamtajia. Bale akaumia sana.
“Aisee
wewe ni mshenzi Malon! Na ni kina nani uliwatumia kuua familia yangu?” Akiwa
amejawa hofu kubwa, akitambua umbali aliopo na walipokuwepo wanakijiji ambao
wanaweza kumuokoa, Malon akawataja mpaka sehemu anayoweza kuwapata. “Nirushie
simu zako zote nje kwa kupitia dirishani ili kuwatafuta. Nikiwapigia kwa simu
yako, watapokea kwa haraka.” Malon akiwa amepaniki akijua na bangi za Bale
zimeshawaka kichwani, hatashindwa kumchoma kweli endapo akikaidi, akatoa simu
zote huku akikwepa yale mafuta pale dirishani.
“Sasa leo
hukumu yako ya hapa duniani imefika. Leo nakuhukumu, sitakusamahe.
Naanza kukuchoma moto wewe ndio ghala na shamba lako. Sitaondoka hapa mpaka
nihakikishe umeteketea Malon. Nitashibisha masikio yangu kwa kilio chako ndipo
niridhike, mshenzi wewe. Teketea ukijua Naya yupo kwa Joshua na
ametulia, na mimi nakwenda kuchukua pesa zako zote.” Akawasha moto dirishani na
mlangoni kwake. Malon akaanza kupiga kelele kwa hofu akimsihi Bale amsaidie na
kumsamehe.
Bale
hakumjibu kitu akawahi kuwasha na kule galani kisha akatupia moto mwingine
shambani kwake kwa haraka ili wanakijiji ambao ni kweli walikuwa wakiishi mbali
sana na eneo alilonunua Malon wasije wakaja kumuokoa. Ila alifarijika kadiri
alipokuwa akimsikia Malon akiteketea kwa uchungu sana. Wakati huo alishakuwa
amerudisha yale madumu ya mafuta yote kwenye gari. Akakumbuka maneno ya Nanaa
kwamba wamejua kwao kumechomwa moto kwa makusudi sababu ya ushahidi wa chupa
iliyookotwa yenye petroli. Bale hakutaka ushahidi. Akamsikia Malon akipiga
kelele kwa maumivu makali sana kama anayeteketea. Akajua hata wanakijiji
wakitokea wakati huo wakazima moto, hatapona. Akaridhika hivyo na kuondoka hapo
kwa haraka sana. Usiku huohuo akaondoka mjini Mbeya kurudi Dar.
Huko Jijini.
Bale
alirudi Dar, palepale nyumbani kwa Malon, Kunduchi, akalala kama hakuna
alilofanya. Alipoamka, akampigia simu Joshua na kumwambia anajua jinsi ya kuwapata
moja kwa moja waliochoma familia yake. Akampa wazo arudi kwa anayehusika na
kesi yao, atafute wale walinzi wa usiku ule, kisha wahojiwe. Akamuahidi
kumfanikishia kukamatwa kwa watuhumiwa wenyewe pindi atakapopata ukiri kutoka
kwa walinzi walio linda nyumbani kwao usiku ule palipoungua moto na kusababisha
kifo cha ndugu zake Kiluvya.
Wakati
Joshua anafufua kesi ya kina baba Naya akiwa na ujasiri wote kwa kuwa safari
hii ana ushahidi wa kutosha, huku Bale akawa anajinufaisha. Kwa kuwa
alimjua Malon ni mtu wa peke yake. Hakuna hata ndugu au
rafiki anayejua mali zake au hakuwahi kumkaribisha yeyote kujua mambo yake
zaidi mali. Hata nyumbani kwao hakuna hata mmoja aliyemjua Malon na
anachomiliki kwa hakika isipokuwa kuwapa tu msaada. Alijua hata wakifanikiwa
kujua Malon amekufa, haitakuwa kwa haraka labda yeye ndio awapelekee taarifa za
kifo chake kwa kuwa alikuwa na simu za Malon, alijua akitaka, anaweza
kupata namba za wazazi wake kupitia simu hizo. Hakufahamiana na wazazi wa Malon
na hakupajua kwao Morogoro. Naya ambaye anamfahamu mpaka kwao, ndiye amemgeuza
tahira. Bale akajiambia hata kama wakijua Malon amekufa, hakuna anayejua mali
zake. Kwahiyo zimeshakuwa zake.
Bale
akaanza kujichotea pesa za Malon akiwa amelala nyumbani kwa Malon. Akajihamishia
pesa yote mpaka akaridhika. Akachukua namba za simu za muhimu alizojua
sitamsaidia kwa kuendeleza baadhi ya biashara za Malon, kisha akazitupa zile
simu chooni kabisa kupoteza ushahidi. Akahamia kuhamisha pesa za Malon benki
kwa haraka kabla benki hawajapata taarifa za kifo chake na kufunga hizo
akaunti. Na kwa kuwa akaunti yake ya biashara na yeye Bale alikuwa akijua ilipo
kwa kuwa alikuwa akienda kumuwekea pesa huko na alikuwa akimtuma hata kuchukua,
Malon alishamtambulisha hata kwa wahudumu wa benki ili awe anahudumiwa kwa
haraka. Bale akaanza yake mapema siku hiyo bila hofu ya kukamatwa.
Kwa Joshua.
Wale
walinzi wakafikishwa kituo cha polisi, mahojiano yakaanza upya. Ikajulikana
kumbe yuleyule aliyepiga simu kwa Magesa kutoa taarifa kuwa Kiluvya kumeteketea
moto ndiye aliyefanya mipango na Malon, hata walipoingia kulala, yeye ndiye
aliyempigia simu Malon kama alivyomuomba. Akawaambia baba Naya alishaingia
ndani, na amefunga mlango. Akakiri hajui ni kwa nini alitaka hiyo taarifa ila kwa
kuambiwa na kuthibitishiwa na Malon mwenyewe, alijua Malon ni kama mtoto wa pale.
Alipoambiwa
ilikuwa ni njama ya kuwachoma moto, yule mlinzi akaonekana kwa hakika hakuwa
akijua hilo. “Hakuniambia ni kwa nini anataka nimwambie pale mzee
atakapoingia na kufunga mlango. Sikujua kama atafanya ukatili kwa mzee mwema
kama yule!” Mlinzi akakiri kwa uchungu akiwa ameshapigwa na kuteswa
sana. Ndipo Joshua akampigia simu Bale kumwambia pale polisi walipofikia, na
yeye akamwambia afike kwenye baa fulani maeneo ya Mbezi ya Kibamba. Akiwa na
askari kanzu.
“Sasa
nyinyi muwahi kabla yangu. Mkae kwenye meza, mimi nikifika tu nitawapigia
wafike pale. Nikiwaona nitajitahidi tukae kwenye meza karibu na nyinyi ili
msikie mazungumzo yetu, na mimi nitawarikodi wakati nikifanya nao mazungumzo.
Nitawadanganya kuwa nimepata kazi ingine kama ile waliyomfanyia Malon, na
nitawadanganya kwamba mimi nitawalipa zaidi. Wakishakiri tu kuhusika, ndipo hao
askari wasogee mezani kwetu wawakamate.” Bale akaongea na
Joshua akisikika amejipanga vizuri.
“Sawa Bale.
Lakini kabla hatujaagana, maana najua tunaweza tusizungumze tena. Naomba
nikwambie kitu na nikushauri. Nisikilize tu, huna haja yakutendea kazi
ninachotaka kukwambia ila naomba unisikilize. Cha kwanza, sina haja ya kuchukua
kiwanja chenu Kiluvya, wala Naya hana shida nacho. Kwa msaada wa GM tunavyo
viwanja vingi sana tu na vyote nimeviendeleza. Lakini sitakupa kiwanja
cha Kiluvya, kwa sababu ni kitu alichotaka baba yenu. Ila GM anaweza kukusaidia
kupata kiwanja kizuri na sehemu nzuri tu.” “Sina shida.” Akajibu
Bale kwa jeuri.
“Sawa. Kingine
na cha mwisho, ulipofika sasa hivi hujachelewa kurudi. Umebaki wewe tu kama
ndugu yake Naya. Na anakuhitaji.” “Ananihitaji vipi na hanijui?” “Naya atakuja
kupona. Na akipona atahitaji kukuona Bale. Viko vituo vingi tu vinaweza
kukusaidia kutoa hiyo sumu ya madawa mwilini mwako na kuacha akili yako ikaweza
kufanya kazi vizuri.” “Kwamba unafikiri mimi sina akili?” Bale
akauliza kwa ukali.
“Unajua
simaanishi hivyo Bale. Lakini kumbuka maisha na maamuzi ya Malon. Kuna umbali
amefika Malon, anafanya mambo si ya kawaida lakini ni kwa sababu ya
kutumia bangi kwa muda mrefu mpaka kumuharibu akili. Tafadhali usiruhusu ufike
huko Bale. Unayo maisha marefu sana mbeleni.” “Cha kwanza Malon si tatizo tena.
Nilikwambia nitamdhibiti, ujue nimemdhibiti milele.” Joshua
akashituka sana.
“Umefanya
nini Bale!?” Joshua akamuuliza kwa tahadhari. “Alicho
mfanya baba yangu, Zayoni, bibi na Luka ndicho na mimi nilichomfanya.” Joshua
akahisi mwili kuishiwa nguvu. “Hakuna wakumsogelea tena
Naya. Lakini nataka kumalizana na watuhumiwa hao wa mwisho ambao wao naacha
vyombo vya sheria viwashugulikie. Nikiona hawawafanyi kitu, nitawahukumu mimi
mwenyewe. Sasa na wewe usichelewe pale baa na hao askari kanzu. Na leo nakwenda
kumalizia deni la Magesa. Nataka na wewe ujue kuwa baba hatakuwa
akidaiwa tena, kachukue hati kwa Magesa, muhifadhie Naya.” Simu
ikakatwa. Joshua akabaki akiangalia simu yake akimtafakari shemeji aliyebakishiwa
naye hapa duniani.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Joshua
akampigia simu Geb. Akamsimulia kila kitu alichozungumza na Bale. “Daah! Hivi
utafanyaje Joshua?” “Aisee sijui! Lakini kwani wewe umesikia taarifa zozote juu
ya moto ulioteketeza huko Mbeya?” “Bado.” Wakatulia kwenye simu
wanaume hao hawajui waseme nini. “Daah!” Akasikika
Joshua. “Lakini kwa upande fulani yupo sahihi.” “Juu ya nini?” “Utapumzika.
Angalau utakuwa na uhakika kuwa Naya yupo salama.” “Japokuwa hatujathibitisha,
ila njia aliyotumia si sahihi! Kuua si kitu kirahisi. Hatabakia salama.
Itamsumbua tu.” “Na kweli. Si unakumbuka hata na kauli ya Mbabe?” “Bora
kufuatwa na pesa kuliko damu ya mtu?” Akauliza Joshua. “Sawasawa.”
“Ndio ninachokwambia GM, hawezi kubakia salama hata iweje. Itamsumbua
tu. Lakini sina chakufanya. Anaonekana amekusudia kabisa kuniweka mbali na
maisha yake. Na mimi nitamuacha kabisa.” Nanaa akaingia ofisini kwa
mume wake akajua anazungumza na Joshua.
“Joshua?”
“Nipo.” “Tafadhali naomba zungumza na mke wangu.” Joshua akawa ameshaelewa,
akasita akiwa ameelewa nia yake. Akabaki kimya. “Msikilize tu tafadhali.
Amekua akitafuta jinsi ya kukufikia, naona inamuathiri na kumnyima raha.
Nakukabidhi.” Nanaa akachukua simu. “Umenichukia sana Joshua?” Nanaa
akauliza kwa upole. “Hapana Nanaa, ila niliingiwa hofu.” “Nikiomba tena msamaha
itasaidia?” “Sisi ni ndugu Nanaa. Hilo haliwezi kubadilika, ila naomba kwa sasa
nimfungie tu Naya. Tafadhali sana. Na mama nitamwambia. Mpaka angalau aweze
kujitambua. Bado hayupo tayari kukabiliana na mambo haya yanayoonekana ni
madogo madogo tu kwa wengine. Kwake bado kabisa. Ukikaa naye na ukawa huna kitu
kingine cha kufanya ukaweka mawazo yake kwake tu, utagundua bado.
Anahitaji muda. Acha nimsaidie kwa namna hiyo.”
“Nimekuelewa
Joshua. Na tunaomba msamaha kwa kuzembea. Ila ujue tunawapenda. Mtakapokuwa
tayari na sisi, mjue milango ipo wazi muda na wakati wowote. Na mtakapo
tuhitaji wakati wowote, tafadhali msisite.” “Hilo najua. Na hata usingesema
sasahivi, bado najua nyinyi ni ndugu zetu wa kwanza na wakaribu. Na nilipanga
kukutafuta kukuomba unisaidie mtu wa kumtengeneza nywele, lakini iwe nyumbani.
Hataki kutoka kabisa.” Hilo kidogo likamfurahisha Nanaa.
“Ninao
wasusi wanaokuja nyumbani kwa ajili ya kumsuka binti Magesa. Anampenda kwa kuwa
anasema hamvuti nywele. Naona huyo atamfaa na yeye Naya. Basi mkiwa tayari
mniambie aletwe.” “Hapo utakuwa umenisaidia sana. Nakushukuru sanaaa.” Kidogo
wakacheka ndipo wakaagana. Na kumrudisha kwa Geb.
“Nashukuru
Joshua. Na kama alivyosema Nanaa. Utusamehe sana. Kilikuwa kitendo cha muda
mfupi!” “Usijali GM. Malon alikuwa hatua moja mbele. Hata walinzi hapa kwangu
nilibadilisha. Tafadhali mwambie na mama asijilaumu.” “Kama utaweza, atajisikia
vizuri kusikia kutoka kwako mwenyewe.” “Basi nitampigia. Acha nikamtendee haki
baba Naya. Sijui kwa nini Geb, moyo wangu hautatulia mpaka nihakikishe haki kwa
yule mzee imetendeka. Walimtenda vibaya pasipo sababu bwana!” “Ni kweli.
Wamemwaga damu za watu wasio na hatia! Mungu aingilie kati.”
Wakazungumza kidogo na kuagana.
Bale.
Kweli
Bale akafanikisha kumalizia deni la kina Magesa lote hata kabla ya kwenda
kukamata hao vijana walioshirikiana na Malon kufanya uhalifu nyumbani kwao.
Akaondoka ofisini kwa kina Magesa bila nyongeza wala kuulizia hati. Na wenyewe
wakamuacha kabisa, wala hawakumuongelesha. Akatoka hapo akielekea kukamata
waliohusika na kifo cha familia yake.
Na Joshua
naye hakuzembea. Alihakikisha anapata hao askari kanzu na kwenda nao
walipokubaliana na Bale na wakafanya kama alivyosema Bale. Walipokiri tu kuwa
walipokea malipo mazuri kutoka kwa Malon na wanaweza kumfanyia kazi nzuri zaidi
endapo atawalipa vizuri, ndipo wakatiwa nguvuni.
Kazini.
Huku
kazini sababu ya mambo ya kifamilia, hata utendaji kazi wake Joshua ulibadilika
sana. Jema ndiye akawa mtu wa kumsaidia Joshua kupita anavyotakiwa, akiendesha
mambo kama Joshua mwenyewe. Kila wakati alikuwa akijiuliza kama Joshua mwenyewe
angekuwepo, angefanya nini au angechukua hatua gani. Akafanyika kama malaika
aliyetumwa na Mungu kwa wakati huo ili kumsaidia, mpaka akamshangaza Joshua
mwenyewe. Bado pengo la Njama halikuwa limezibwa, kwa hiyo alifanya kazi zao
zote bila kuchoka wala kulalamika, hilo nalo likamgusa Joshua zaidi.
Mkataba
wa Coca na kwenye jengo wanalofanyia kazi kina James uliisha, walitakiwa
kusaini tena. Hilo Jema akalikumbuka. Akachapisha mkataba mpya lakini
unaofanana na wa kwanza. Akampa mwanasheria wa kampuni yao. Akaupitia kama
mwanzoni na kuusaini. Jema akampa dereva aupeleke kwenye ofisi husika kwenye hilo
jengo. Sekretari akawa akifahamiana na Jema. Alishampigia simu na kumuomba
apokee. Kwa hiyo alishajua dereva anapeleka hizo nyaraka. Alipofikisha akapokea
na kupeleka kwa muhusika.
Mida ya
saa kumi kama na nusu jioni Jema akiwa busy sana, akapokea ujumbe kuwa ipo
tayari. Akajua kumtuma dereva kwenda kufuata, itakuwa si sawa maana ndio karibu
na mida yake ya kutoka. Akamtumia ujumbe James. ‘Samahani bosi, inawezekana
ni matumizi mabaya ya namba yako binafsi, lakini nimebanwa sana, na mkataba
wetu upo tayari hapo kwenye ofisi za hilo jengo. Niombe kama utakuwa na muda
unichukulie halafu nitakuja kuupitia hapo ofisini kwako.’ Hapohapo
akajibu. ‘Sawa.’ Mpaka akamshangaza Jema. “Kwamba alikuwa na simu mkononi!”
Jema akajiuliza na kushangazwa. Ila akapata aghueni maana alijua angechanganya
ratiba na hilo lisingemfurahisha Kumu.
‘Nashukuru
Bosi. Nitajitahidi kabla ya saa 12 niwe nimefika hapo, ili nisikuweke sana.’
‘Haina shida.’ James akarudisha huo ujumbe kwa haraka. Jema akacheka na
kurudisha simu mezani akimtafakari James na kupotelea mawazoni.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alipomalizana
na shuguli za kiofisi na kumtumia Joshua ripoti ya siku na kupata ujumbe wa ‘You are
the BEST.’ Akajua amemfurahisha. Akatoka kwa haraka kwenda ofisini kwa
James, hakuwa amemuona kwa muda mrefu tokea kwenye harusi ya Naya na Joshua.
James alibadilika haswa. Alifuga ndevu na Geb ndiye aliyemwambia. “Acha kuweka
muonekano kama kina Magesa bwana! Au unataka kuwa na baby face mpaka uzeeni? Nobody
will take you serious.” “Unamaanisha wanawake?” “Namaanisha acha kunyoa
ndefu zote. Weka sura ya kiume.” Geb akamalizia hivyo. James akacheka na
kuondoka. Ila kikamuingia na kuanza kutengeneza ndevu mpaka zikapata muonekano
wakueleweka ndipo akapeleka saluni na kuchongwa vizuri. Kweli akapendeza.
Sasa siku
hiyo Jema kumuona, akababaika mpaka akamshangaza James asielewe anababaishwa na
nini, asikumbuke jinsi alivyojibadilisha. “Haina shida kabisa. Tena ameniletea
hapahapa wala sikuifuata. Kwa hiyo haikuwa usumbufu hata kidogo. Karibu, muda
na wakati wowote.” “Umekula?” Hilo swali likamfanya James atulie na kubaki
akimwangalia. Nakuzidi kumbabaisha Jema. Akaanza kujitetea. “Ni kama malipizi
tu na shukurani kwa ulichonifanyia. Nikutoe kwa chakula cha jioni. Kama
ungependa lakini.” “Nashukuru lakini kuna mahali nakwenda baada ya hapa.” Jema
akajisikia vibaya, ujasiri wote ukamuisha na uchangamfu usoni ukapotea.
Akahisi
amejitongozesha kwa James na amemdharau. “Sikuwa na nia mbaya. Ingekuwa
ni chakula tu. Kwa kuwa na mimi mwenyewe sijala kwa muda mrefu, nikajua
isingekuwa tatizo kwenda kula pamoja. Lakini si kwa nia mbaya. Na unisamehe
kama nimevuka mpaka.” “Haina shida kabisa. Ila ni vile nina miahadi sehemu.”
Jema akaangalia ile bahasha mkononi. Akatoa tabasamu la kunyongonyea.
“Nashukuru James, na jioni njema.” Akatoka bila hata kusubiri nyongeza na wala
hakumwangalia tena. James akatafakari na kuangalia saa, akatoka kuwahi kwa kina
Magesa ndiko alikokuwa na miahadi.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Alipofika
na kukuta gari ya Geb nje akamtumia ujumbe. ‘Toka nje bila ya kumwambia
mtu. Kuna kitu nataka nikuulize.’ Geb akasoma ujumbe.
Akasubiria kidogo na kutoka. “Vipi?” James akasita kidogo. “Nini wewe? Kwanza
shuka kwenye gari watoto wote wanakusubiria wewe ili wakufunge ndipo wakalale.”
“Subiri kwanza Geb.” Geb akatulia akimtizama. Akashuka garini. Na kubaki
amesimama.
“Wewe
vipi!?” “Mbona huna subira Geb bwana?” “Umenitoa katikati ya game, James. Na
nilikuwa nakaribia kumshinda tena Magesa.” “Acha kushindana na mtoto Geb! Wewe
unajisikia raha akilia?” “Wewe cheza nao unavyojisikia, na mimi nacheza nao
ninavyojisikia. Siwezi kumuachia anifunge eti sababu ni mtoto! Sitakuwa nao
huko duniani wakati wakikumbana na changamoto.” “Hata mara moja moja tu bwana?”
“Basi ndio maana wanakusubiria wewe huko ndani. Wewe nenda kawaachie wakufunge.
Mimi nacheza kwa haki. Wajifunze kukabiliana na changamoto.” James akacheka na
kutingisha kichwa kwa masikitiko.
Kila
Magesa akicheza na baba yake, lazima ataishia kulia tu. Maana Geb anahakikisha
anamfunga. Ila walimpenda James alikuwa akiwaachia wamfunge. Basi Nanaa akiona
wanae wanalia na Geb anazidi kuwafunga, anamtoa Geb kwenye mchezo na kumuomba
kaka yake aje acheze nao ilimradi wamfunge, zaidi Magesa afurahie.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Inaweza
kuwa si kitu.” Akaanza James akijihami. “Lakini unachukuliaje mtu akikuambia
mtoke naye kwa chakula cha jioni?” “Inategemea na mazingira.” “Acha bwana
kunijibu kama unaongea na mtu mwenye kichwa kama chako.” Geb akaanza kucheka.
“Labda uongeze maelezo.” “Labda tuache tu.” Geb akatulia akijua yeye mwenyewe
hawezi kuacha. Kuna linalomsumbua. Akaenda hatua chache kama anayeingia ndani,
lakini akarudi palepale akakuta Geb amesimama palepale kama aliyejua atarudi
tu.
“Kwa
mfano ukamkatalia halafu akaonekana ameumia kidogo?” “Nisikilize James. Mimi na
wewe tunajua kabisa huyo sio mwanamke wa kwanza kukukaribisha chakula…” “Ni..”
“Subiri James. Kwa mara ya kwanza unaonekana umepata mtu anayeanza kuleta maana
kwako ndio maana upo kama ulivyo.” “Mimi..” “Subiri kwanza James!” “Sasa
unacheka nini Geb?” “Nimefurahi hatimaye na wewe unapita tulikopita na sisi.
Maana ulikuwa ukiishi kama huna hisia bwana! Halafu wenzako tukaonekana kama
wanaume dhaifu!” “Mimi sijasema nina hisia kwake.” James akabisha.
“Hivyo
ulivyo. Maswali uliyo nayo juu ya mlichozungumza na kutoridhika juu ya hali
uliyomuacha nayo, hizo ndizo hisia zenyewe kwa kuwa hujawahi
kujali unavyojibu wengine ila yeye.” James akarudi na kuegemea kwenye gari
akabaki kama anayefikiria. “Sasa usipoteze muda James. Hicho unachojisikia,
kitafutie majibu ya haraka bila kusuasua.” “Umesikia maelezo yangu lakini?”
“Nayakumbuka na ndio maana nakwambia usipoteze muda.” “Nafanyaje sasa wakati
nishakuwa kama nimeharibu tokea mwanzo? Anahisi nimemkatalia! Halafu yule
ni msomi na anajielewa.” “Nani?” “Nice try. But NOPE.” Geb alicheka sana
kwani alimuuliza kwa haraka ili kumjua huyo msichna aliyemudu kumchanganya
James, Mgumu. James akamshitukia.
“Sawa.
Lakini ndio anza kwa kujirudi.” “Nimwambiaje tena!?” “Unataka nikusaidie
kukutongozea?” “Acha hizo Geb! Wewe unaakili ya kufikiria. Na nishakwambia
tatizo lilipo.” Geb akazidi kucheka akimwangalia James ambaye hakuwahi kuwa
hata na dalili ya mwanamke. “Unanisaidia au?” “Kwa mfano nikikukatalia,
utafanyaje?” James akacheka akitingisha kichwa.
“Ukiwa
unatoka hapa, mtumie ujumbe wa kuonyesha ulijali ila kweli hukuweza
kwenda kula naye.” “Acha kunipa mambo nusunusu Geb!” “Kwahiyo unataka
nikuandikie na ujumbe wenyewe!?” “Kwani utapungua wapi?” “HAPANA James! Mimi
mume wa mtu, siwezi kuweka moyo wangu kwa mwanamke mwingine. Maana hapo
atakuwa akisoma moyo wangu sio wako. Nishakwambia chakufanya, fikiria
mwenyewe na andika maneno yako.” “Lakini kweli.” Akabaki akifikiria.
“And
stop smelling cheap.” “Acha dharau Geb! Hii pafyumu nimenunua agali.” “Gali
kiasi gani James?” “Hela nyingi lakini si kama pafyumu zako na Joshua. Hapo hapana.”
“Sasa umeelewa ninachokwambia? You smell very cheap, na haivutii. Huna
majukumu James, kwa nini usijigaramie? Mbona wakati ulipokuwa ukimlea Nanaa
ulikuwa ukitumia pesa kwake, kwa nini unajionea ubahili wewe mwenyewe mtafutaji? Ni wakati
wakujigaramia na wewe James. Maisha ni hayahaya. Na ipo siri kubwa sana kwenye
harufu. Mimi wakati mwingine mke wangu ananitaka sababu ya kupata tu harufu
yangu. Na wakati mwingine hata katikati ya siku sihitaji kuoga kupata penzi.
Akipata harufu yangu tu, ananing’ang’…” “Acha bwana Geb!” Geb akacheka sana.
“Nilisahau
baba mkwe wangu. Ila..” “Basi bwana. Nitanunua hiyo pafyumu. Acha kunitukana.”
Geb akazidi kucheka kila akimtafakari James na hisia mpya. “Kama nakuhisi
unachocheka sasa hivi ni zaidi ya pafyumu!” Geb akazidi kucheka. “Acha
kunicheka Geb!” “Acha nifurahie kupatwa kwa James.” James akaondoka na
kuingia ndani.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
“Atakufuata
yeye mwenyewe.” “Lakini si umesikia maonyo ya mama yake?” “Ndiye huyohuyo
atarudi kukuomba ukacheze naye.” “Na ajue nitamfunga tu mwanae.
Sitamuachia kama hivyo James.” Geb na mama yake wakazidi kucheka wakiwateta
Nanaa na mwanae.
~~~~~~~~~~~~~~~~~~~
Ø
Kwa Mara ya Kwanza JAMES kujali hisia ngeni. Hatua gani atachukua.
Ø
Bale amelala masikini, ameamka tajiri wa kupindukia.
Ø
Sababu ya USIRI wa Malon kwenye anayomiliki, Bale amejishindia mali zake
kilaini. Hana wakumuuliza. Hata wakijua
kama Malon amefariki, hakuna ajuaye alikuwa na MALI
gani, wapi na kwa kiasi
gani.
Malon
alilala akiwa na mipango mingi, hakujua masaa machache mbeleni, hakuijua
kesho yake, kama wengi wetu tunavyoepuka ukweli wa KIFO.
ILA Mfamle Daudi aliomba hivi Zaburi 90:12
{‘Tufundishe
kuzihesabu siku zetu vizuri, ili tujipatie moyo wa Hekima’}
0 Comments:
Post a Comment