Lubuva alionekana
anataarifa zote za Nanaa, tena vizuri tu.
“Ndio nakuagiza Geb. Hakikisha Nanaa anakubali matibabu yangu yote na
kufuata masharti yangu yote ili apone. Ukishindwa hapo ujue unaendelea kumuua
Nanaa kwa mikono yako wewe mwenyewe.” “Acha kunitisha na kuniwekea hukumu.”
“Nakwambia ukweli Geb. Na ni kweli wewe na mimi hatufanani. Mimi nilimkimbia
‘girlfriend’ tu. Wini. Tena nilimuacha mikononi kwa mwanaume mwingine
aliyemchagua yeye mwenyewe Wini. Lakini wewe ulifanya unyama
wakupitiliza. Ulimuacha mwanamke ambaye
kisheria tayari alikuwa mkeo.”
“Mbaya zaidi ulimuacha
mgonjwa na kumpokonya watoto aliozaa kwa kuyatoa maisha yake na bado alikuwa
mgonjwa. Angefanyiwa hivyo Oliva ungefurahi au ungeona sawa baada ya kupewa
sababu ya kitoto kabisa kama hii uliyonipa mimi. Eti ‘Nanaa alinidanganya’!
Ndio unafikiri hiyo sababu yako inahalalisha uharibifu uliofanya kwenye maisha
yake? Amefanyiwa upasuaji wa kichwa na moyo wake ni mkubwa kwa sababu yako WEWE
Geb. ‘So, stop whining like a little girl, and grow up already’.” Lubuva
akaongea kwa jeuri ile Geb aliyoisikia kutoka kwa yule nesi, kisha akatoka
akiwa amemwambia aache kujilalamisha kama mtoto mdogo wa kike, akue.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Kama aliyefika nje ya
mlango na kukumbuka kitu akarudi. “Kwanza sikukuona hapa hospitalini juzi
nzima. Unawezaje kulala nyumbani wakati yeye yupo hapa?” “Naomba acha
kunichanganya zaidi ya hivi nilivyo dokta Lubuva. Mimi nilipatwa na matatizo
sababu ya kuamka asubuhi ili kuwahi hapa. Nilichukua taksii ili iniwahishe
hapa. Njiani nikagundua sina pesa yakulipia taksii. Nikamuomba dereva asimame
kwenye ATM. Nimetoa pesa kwenye mashine, wakati nageuka, nikapokea ngumi ya
jichoni. Sijakaa sawa, nikaanza kupigwa. Kuja kuzinduka nipo hospitalini. Sijui
ilikuaje. James ndiye aliyekuja kunihamisha kutoka hospitali ya Mwananyamala,
akanipeleka hospitali ya kulipia ambapo nilipewa matibabu ya haraka na kuweza
kurudi tena hapa. Mimi sio kama wewe. Siwezi kumtelekeza Nanaa.” “Sema ‘siwezi
kumtelekeza TENA’’.” Lubuva akamsahihisha
na yeye kama vile Geb alivyomfanyia hapo awali. Geb kimya akabaki akimtizama
kwa hasira. Kwa mara ya kwanza maishani Geb akawa amepata kiboko yake aliyemudu
kiburi chake.
“Nitarudi tena
baadaye. Na umtoe Jimmy kule ulipomuacha kama mtoto yatima, wakati anapo
nyumbani kwao. Pale watoto ni wengi na ni sehemu ya kupita tu watoto baada ya
kuzaliwa. Sio sehemu au kituo cha kulelea watoto. Mpeleke kwa ndugu zake
nyumbani, awe anakuja hapa kusalimia kama kina Liv. Kama mnalemewa
kuwatunza watoto wote, mseme mtafutiwe msaada.” Lubuva aliongea kwa
jeuri, kisha akatoka na kumuacha Geb haamini kama mambo yamembadilikia. Baba wa
Nanaa amekuja juu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Alikaa pale akiwaza.
Usingizi wote ulipaa. Akavuta kiti karibu na Nanaa, akabaki akimwangalia. Kweli
alifanana na baba yake. Lakini baba yake alionekana na nywele laini. Nanaa
alijaliwa kipilipili, tena kipilipili kikali. Nywele kavu, zilizokuwa
zikijifinyanga. Geb akacheka. “Unacheka nini?” Nanaa alifungua macho na kukuta
akicheka. “Nakucheka wewe.” “Sijui wananipa nini! Nikilala nakuwa kama mfu!
Najikuta napotea kabisa.” “Nina hamu na wewe Nanaa!” “Basi zungumza nao kesho
wanitoe, turudi nyumbani.” Geb akakumbuka maneno hayo hayo alimshawishi nayo
baada ya kujifungua Magesa, na yeye akamshawishi daktari mpaka wakamruhusu
kutoka hospitalini.
“Naomba safari hii
tufuate ushauri wa daktari Nanaa. Tena dokta Lubuva.” Nanaa akakunja uso.
“Anaonekana ni dakatri anayejua anachokifanya. Tuweke pembeni tofauti zetu na
yeye, ili.. ” Geb akatumia muda wakutosha hapo kuhakikisha Nanaa anakubali kama
alivyopewa mkwara na baba yake, dokta Lubuva. “Basi hatutakaa tukatoka hapa.”
“Naomba safari hii uwe mvumilivu. Hata ikichukua muda mrefu, sawa tu, ilimradi
upone. Sitaki kurudia kosa.” Nanaa akakunja uso.
“Kosa gani tena!?”
“Mimi ndiye niliyekusababishia kuwa hapa. Nilikutoa hospitalini ukiwa mgonjwa,
na sikukupa dawa ulizotakiwa kutumia.” Nanaa akavuta pumzi na kunyamaza.
Inamaana na yeye amekubaliana na hilo!? Geb naye akawaza. “Naomba tuvumilie na tupokee matibabu yote.”
“Hata ikichukua mwezi?” “Hata mwaka. Naomba safari hii sisi tuwe wapokea
maagizo tu.” Nanaa akafikiria.
“Na Jimmy?” Nanaa
akauliza baada ya ukimya. “Nafikiria arudi nyumbani.” Nanaa akabaki ameduwaa.
“Ni kwa nia nzuri. Pale sio sehemu sahihi ya yeye kuwepo kwa muda mrefu.
Tunakuwa kama tunamtenga na ndugu zake.” Machozi yakaanza kumtoka Nanaa.
“Hakuna mtu atakayekupokonya tena watoto Nanaa. Ni wako. Na wewe utakuwa na
amri nao. Muda na wakati wowote utakao wahitaji hapa, wataletwa. Sitaki Jimmy
akae pale kama yatima. Anatakiwa kuwa na ndugu zake. Au unafikiriaje?” “Naogopa Geb. Hakika naogopa sana. Sitaki alikopitia
Magesa ndipo apite Jimmy.” “Nakuhakikishia mbele za Mungu wangu, Nanaa,
hakutakuja kutokea mtu yeyote akakupokonya tena watoto. Kwanza wote tumeonywa
na Mungu. Hakuna hata atakayethubutu tena. Nakuahidi. Sawa?” “Sawa.” “Usilie sasa.”
“Nahisi
nimepatwa hofu Geb. Na kwa Magesa ilikuwa hivi hivi. Tulianza vizuri, kwa ahadi
nzuri, nikaishia kuwa na kama majipu ya maziwa!” “Huna haja
yakuogopa. Naomba uniamini kuwa nimebadilika. Nimebadilika Nanaa.” “Na mimi nimekuona umebadilika Geb.” Geb
akasimama, akamfuta machozi na kuanza kumbusu.
Baba yake Nanaa
akarudi tena ndio akawakuta wanapeana mabusu. Geb akamwachia Nanaa, Nanaa
akaanza kucheka. “Unacheka nini?” Dokta Lubuva akamuuliza taratibu. “Nimefurahi
kukuona. Niseme kukuona tena.” “Naweza kukupima?” “Unanipima mara ngapi!? Wewe
sio nesi. Kwa nini unafanya kazi za manesi?” “Nanaa!” Geb akamwita kama
kumkumbusha mazungumzo yao. “Sawa.” Nanaa akakubali bila kubisha tena. Lubuva
akasogea. “Geb ameniambia niwe mvumilivu
hapa, nisikatae matibabu yako wewe. Chochote utakachoniambia nikubali bila
kufanya ubishi. Wewe unaonekana unajua jinsi yakunisaidia.” Lubuva kimya.
Akajua ujumbe wake ulifika na Geb ametekeleza maagizo yake.
“Sasa sijui kama
tutaweza kumudu garama zako!? Eti Geb? Si umesikia kuwa ni daktari bingwa wa
kimataifa!” “Nataka kukupima pressure.” “Kwa hiyo ndio unaniambia ninyamaze?”
“Ndiyo.” Nanaa akacheka taratibu akionekana na usingizi. “Mimi nimefurahi sana.
Nani alijua Nanaa anaweza kuwa na baba ambaye ni daktari bingwa!? Hakika hata
mimi ungeniambia masaa machache yaliyopita, nisingesadiki.” Nanaa akaendelea
huku akimwangalia.
“Natamani
ungenirithisha nywele zako. Muulize Geb, nina kipilipili kikali kweli! Nikianza
kuchana nywele mpaka vyanuo vinavunjika.” Nanaa aliendelea kufanya mzaha.
“Naona wewe nywele zako zipo kama za kiarabu!” Nanaa aliongea huku anamtizama
kichwani. “Sasa hivi nilivyo, nafanana na nani?” “Bibi yako.” Lubuva akajibu
nakumfanya Nanaa acheke tena. “Ila nywele hizo ni za mama yako.” Hapo mpaka
Geb akacheka.
“Naomba uvute kiti
hapa, tuanze kuzungumza.” “Naomba leo upumzike. Baada ya siku mbili, unaweza
kuwa na akili iliyotulia na kuelewa. Bado unahitajika kupumzika. Ona
unavyosinzia!” “Wewe uongee, mimi nitakuwa nakusikiliza tu.” Geb akamsogelea.
“Naomba umpime kwanza pressure ili tujue ikoje. Ni sawa Nanaa?” Nanaa
akanyamaza. Lubuva akampima.
“Siyo mbaya.” “Mbona
sasa uso wako hauendani na unachoongea?” Nanaa akamuuliza. Lubuva akasita. Hata
Geb alijua kuna kitu anaficha. “Wewe tuambie tu ukweli. Sisi tumeshasikia
habari nyingi na mbaya juu ya huu mwili wangu kuliko hiyo ya pressure kuwa juu.
Usiogope.” Nanaa akaweka msisitizo. “Kesho nitakuwa na conference call na
madaktari wote wa mambo ya moyo, tushauriane. Najua watapata tu ufumbuzi. Ila kwa sasa naomba upumzike Nanaa.” “Huyo
bibi yangu ninayefanana naye, yupo hai?” “Yupo hai.” Lubuva akajibu. “Na babu?”
“Wote wapo hai.” Lubuva akajibu.
“Umesikia mambo hayo
Geb? Nimelala yatima, nimeamka na ukoo! Lazima nipone ili nikawaone.”
“Ukiruhusu, wanaweza kuja kukuona.” “Acha mchezo!?” Nanaa akamfanya Lubuva acheke
kidogo na kutingisha kichwa. “Wewe walete woote waje wanione. Nani hataki
ndugu?” “Basi ulale upumzike. Hiyo pressure ikiwa sawa, nitawaleta
wakusalimie.” Nanaa akacheka kama anayefikiria. “Subiri kwanza nizungumze na
mume wangu. Unajua kama nimeolewa?” Nanaa akaanza kusinzia. Aliuliza huku
anafunga macho.
“Nafahamu.” “Basi
subiri nizungumze kwanza na Geb, ndio nitakwambia lini uwalete.” “Sawa, hamna
haraka.” “Ila nataka kumjua mama yangu zaidi. Alikuwa ni mtu wa namna gani!?”
“Kaa ule kwanza kabla hujarudi kulala tena. Kesho nitakueleza vizuri juu ya
mama yako.” Nanaa akabaki amefunga macho. “Naweza kukusaidia kula.” Lubuva
aliongeza. Wakamuona Nanaa anacheka. Akafungua macho.
“Inamaana unilishe!?”
“Kama hutajali.” Akacheka na kufunga macho. “Namtaka Geb ndio anilishe. Nasikia
njaa ila nahisi usingizi unanilemea.” “Basi usirudi kulala ili akulishe.” Nanaa
akafungua macho na kumtizama Dokta Lubuva.
“Unaondoka?”
Nanaa akamuliza. “Ulitaka nibaki au niondoke?” Lubuva naye akarudisha
swali. “Kaa kidogo na Geb. Usimwache peke yake muda mrefu. Anaingiwa hofu na
hivi ninavyoumwa. Mwambie utanisaidia, nitapona na kila kitu kitakuwa sawa.”
Nanaa alimalizia hivyo, nakurudi kulala.
Geb alizidi kuingiwa
hofu. “Ni kweli unafikiri atakuja kupona na kurudia hali yake kama zamani? Ni
kama mikono yake haina nguvu!” Geb akauliza akionyesha hofu yake. “Nikwambie tu
ukweli Geb, hali ya Nanaa sio nzuri. Anatumia dawa za hali ya juu. Nampa dawa
ambazo nimeletewa kutoka Ujerumani. Daktari huyo wa mambo ya moyo aliyenitumia
amesema kama zisipoweza kushusha hiyo pressure kwa masaa 24, anatakiwa
kufanyiwa upasuaji wa moyo.” “Tena!?” “Kumbuka huo moyo ameanza kuutibu kwa muda
mrefu sasa. Amefuata masharti yote aliyotakiwa kufuata, akatumia na dawa pia.
Nimemtumia huyo daktari matokeo yote ya vipimo vyake vya pressure. Tokea ni
mjamzito mpaka sasa. Na ndio maana unaniona kila wakati ninampima mimi
mwenyewe, ni kwa kuwa huyo daktari huko Ujerumani anafuatilia hayo matokeo. Kwa
dawa na mapumziko yote haya kushindwa kushusha hiyo pressure, inamaana
kinachofuata ni upasuji ambao wanaweza kuweka kifaa kitakachokuwa na uwezo wa
kurekebisha mapigo yake ya moyo na usambazwaji wa damu kwenye moyo.” “Mungu wangu nisaidie.” Lubuva alimsikia Geb
akiomba kwa hofu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
“Unajua kuomba?” Geb akamuuliza Lubuva.
“Unamaanisha kumuomba Mungu, yaani kusali!?” Geb akabaki akimtizama. “Mimi ni
mkristo, lakini maswala ya kusali Sali huwa….” Lubuva akakwama. “Labda
tugawane. Wewe Sali, mimi niwe upande wa matibabu.” Geb akabaki akimkodolea
macho. “Wewe huwezi kumtibu kama mimi na mimi siwezi kuwa nasali muda wote kama
wewe! Mbona ni rahisi tu. Tugawane na tusiingiliane.” Wakaanza tena.
“Kwa hiyo wewe huwa
huombi!?” “Kwa nini!?” Lubuva akamuuliza kama anamshangaa. “Huzungumzi na Mungu!?”
“Kwa nini?” Lubuva akaendelea kuhoji. “Kwa hiyo hata kanisani huendi?” “Kufanya
nini na wakati Mungu amenipa kazi ya kutibu watu? Sasa bora lipi, kufanya kazi
aliyonipa au kurudi tena kuanza kumuomba vitu ambavyo tayari ameshanipa au hata
sihitaji!? Sina sababu ya kuomba chochote kwa kuwa kila ninachotaka ananipa!
Sipotezi tena muda.” Geb akamgeukia vizuri.
“Nini!?” Lubuva
akamuuliza. “Wewe omba sasa hivi kwa kuwa hujui chakufanya hapa kwa Nanaa,
unataka Mungu akufanyie kitu. Mimi najua kitu ninachotakiwa kufanya na
ninafanya. Kama wote tukianza kupiga magoti hapa tunaomba muda wote, nani
atamtibu Nanaa!?” Geb akabaki akimshangaa. “Kwa nini unanishangaa kama
hunielewi wakati nakwambia kitu cha kawaida kabisa!?” “Kama unajua kitu
chakufanya kwa nini Nanaa yupo hapo kitandani mpaka leo?” Geb akamuuliza.
“Si ni mgonjwa!” “Sasa
wewe unayejua kitu chakufanya, kwa nini hufanyi ili tutoke hapa?” “Yupo kwenye
matibabu. Ndio maana nakwambia tunafanya kwa hatua. Kama dawa zimeshindikana,
ndio unafuata upasuaji! Mbona wewe unaomba tokea majuzi hajapona na unaendelea
kuomba? Kwa nini na mimi nisiamini kuwa tuendelee na matibabu atakuja tu
kupona?” Geb akatingisha kichwa.
“Nini!?” Lubuva
akamuuliza tena. “Sasa kwa kuwa unanihitaji hapa ili kumfanya Nanaa akubali matibabu
kutoka kwako, na wewe utafanya nitakachokwambia.” Geb naye akambadilikia.
“Nisipokubali?” Lubuva akamuuliza. “Unamaa kama ambavyo hukukubali mimba
ya Wini, ukamkimbia na kumtelekeza bila
hata kujali maendeleo yake?” Geb naye
akamuuliza swali la kumuumiza.
“Sasa ukiendeleza hiyo
tabia yako yakutokukubali mambo ya msingi na muhimu, nakuhakikishia hutamgusa
tena Nanaa. Nitamtoa hapa, na kumpeleka ninapotaka mimi. Nitatafuta daktari
mwingine. Nitampa historia ya Nanaa yote na vipimo vyake vyote. Nitamwambia
kile ulichoniambia wewe juu ya upasuaji na maendeleo yake mpaka sasa.
Nitamwambia aniandikie barua ya kumpeleka Nanaa Ujerumani. Mimi mwenyewe na
huyo daktari ndio tutampeleka huko nchini Ujerumani akafanyiwe huo upasuaji wa
kurekebishwa moyo wake, bila wewe. Tena nakuhakikishia atafanyiwa upasuaji na
huyo daktari wako bingwa unayewasiliana naye.” Geb aliongea kwa jeuri bila
haraka.
“Huwezi kufanya
hivyo!” Lubuva akashangaa. “Try me! I dare you Lubuva, try me!” Geb alijibu kwa
kitisho na jeuri akimwambia amjaribu, aone. Lubuva akabaki akimshangaa. “Kama
huamini, nipe masaa 24, nitakuwa nimeshapata jina kamili la huyo daktari huko
Ujerumani, namba yake ya simu na mazungumzo yenu yote yaliyokuwa yakiendelea
kati yenu. Tokea unaanza kuwasiliana naye juu ya Nanaa mpaka leo.” Geb
aliendelea kwa jeuri.
“Wakati wewe unasomea
kupasua vichwa vya binadamu, mimi nilikuwa nikisomea kupasua kompyuta. Kutafuta
habari zilizozikwa kwa siri na watu, nakuzifanya zisomeke hata na mtu asiyejua
kusoma. So, try me.” Bado Geb alitaka amjaribu. Lubuva alibaki akimtizama Geb
asiamini. “Huwezi kuja leo kwenye maisha
ya Nanaa na kuanza kuweka utaratibu wako wewe. Nanaa ni mke wangu mimi. Na
ananisikiliza mimi kuliko mtu mwingine yeyote. Nikimwambia asubiri mahusiano na
wewe, ujue atasubiri mpaka mimi nitakapomwambia. Kama huniamini, nijaribu
uone.” “Mimi sijui kuomba kwa kuwa huwa sioni sababu ya kuomba.” Lubuva
akakubali yaishe.
Wanaume hao wawili
walikutana wote wajuaji. Wote wamesoma zaidi ya shahada mbili. Wataalamu kwenye
fani zao. Na pesa ipo. Wajeuri wakupitiliza. Wote wanataka kuonyesha umuhimu
wao kwa Nanaa. Sasa nani zaidi? Ndio wanatunishiana vifua.
“Anza kwa kufunga
macho, mimi niombe.” “Huwezi kulazimishia mimi kuomba Geb! Hayo ni maisha yangu
mimi na makubaliano yangu na Mungu wangu.” Geb akaweka mikono kifuani kama
anayemsubiria. “Fine! Ngoja tupoteze muda hapa wote tukiomba, badala yakufanyia
kazi majibu ya maombi yako.” Lubuva akafunga macho. Geb akaanza kwa kutubu kwa
ajili yake yeye Lubuva anayehusika na kutibu mwili wa Nanaa. Akatubu na
kumtakasa. Akamuombea akili tulivu ili aweze kumsikia Roho wa Mungu anapompa
maelezo ya jinsi ya kumtibu mkewe. Akamuombea watu sahihi wakusimama naye
kipindi hicho anachohitaji watu wakumsaidia Nanaa.”
“Akamsihi Mungu akumbuke
rehema juu yake. Watu wote aliowasaidia, akumbuke kujitoa kwake na yeye amjibu
wakati huo anapohitaji msaada kwa binti yake, Nanaa. Akaombea dawa anazotumia
Nanaa, zikakubalike mwilini kwa Nanaa ili apone kwa haraka bila upasuaji
mwingine. Akamalizia kwa kumbariki dokta Lubuva. Kwa muda anaotumia pale na
kupoteza mamilioni ya pesa kwa kumuhudumia Nanaa. Geb akamsihi Mungu asimsahau
Lubuva, aendelee kumbariki mpaka yeye mwenyewe ajue kama ni Mungu ndiye
amembariki. Akamuombea mkewe na watoto wake wote. “Ameen!” Geb akamaliza.
Lubuva akaanza
kucheka. “Nini?” Geb akamuuliza. “Nashukuru kwa maombi mazuri.” Geb akacheka.
“Kweli. Sikejeli. Nimejisikia vizuri.” “Karibu.” Geb akajibu na tabasamu usoni,
akamgeukia Nanaa. “Atapona tu. Amini.” Lubuva akajaribu kumtuliza. “Nashukuru.
Wewe nenda tu kapumzike. Nitakuwa naye. Kukiwa na kitu cha kukutaka ushauri,
nitakupigia.” “Sawa.” “Ila nina wasiwasi sana na kula yake. Hali chakula vizuri
nahisi ndio maana anakuwa dhaifu. Hataweza kunyonyesha akiwa kwenye hali hiyo.”
“Dawa ndizo zinamlevya. Hawezi kuishiwa nguvu kwa sababu ya hizo dripu
alizowekewa. Halafu nashauri kunyonyesha isiwe kipaumbele kwa sasa. Mwache
kabisa atulie. Maadamu mtoto ni mzima na hajakataa maziwa anayopewa, msubiri
kwa sasa.” “Sawa.” Geb akakubali.
“Namaanisha hata na
yeye umwambie hivyo hivyo. Asione amefeli kutimiza jukumu fulani kwa Jimmy.
Mkumbushe ameshamlipia garama kubwa sana. Amemzaa akiwa mzima kabisa. Mwambie
sasa hivi afikirie jinsi ya kutoka hapo ili awe na watoto wake wote.
Atamnyonyesha kwa kadiri ya uwezo wake kama atatulia na kupona.” “Sawa.” Lubuva
akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Lubuva alirudi
alfajiri akamkuta Geb akimnywesha uji. “Vipi?” “Njaa ilikuwa
ikimuuma.Akaniamsha nipe uji.” “Afadhali.” Nanaa akafungua macho. “Vipi?”
Lubuva akamsogelea. “Nahisi kuchoka tu. Lakini nipo sawa.” Nanaa akajibu. “Leo
sitampa hizo dawa, ili tuone leo utashindaje.” “Na hiyo pressure!?” Geb
akauliza kwa mshituko. “Ndio tumeona tuondoe ili tupate uhalisia halisi wa moyo
wake bila dawa. Kama inakuwa juu zaidi ya hivyo, hatua nyingine ifuate kama
tulivyozungumza jana.” “Hatua gani?” Nanaa akamuuliza Geb. “Nitakwambia kama
pressure itaendelea kuwa juu. Kama itarudi kuwa kawaida hakutakuwa na haja
tena.” Geb akajibu. Nanaa akamwangalia na kunyamaza. Akala mpaka akamaliza.
“Kwa nini uliondoka na
kwa nini ulirudi?” Nanaa akauliza taratibu. “Niliondoka nikiwa sina uhakika
kama wewe ni mtoto wangu. Nimerudi kwa kuwa niliambiwa Wini alifariki na
ameacha mtoto wangu.” Lubuva akajibu. Nanaa akamtizama kwa muda kisha akavuta
pumzi. “Kwa hiyo ni kweli kuwa mama yangu alikuwa muhuni sana?” “Hapana Nanaa!
Kwa nini unakubali hivyo?” “Umesema uliondoka kwa kuwa hukuwa na uhakika kama
mimi nilikuwa mtoto wako. Inamaana mlikuwa wanaume wengi kwenye maisha yake!”
“Mimi ndiye nilikuwa mwanaume wake wa kwanza.” “Halafu!?” Nanaa akauliza.
“Alikuja kumpenda
mwanaume mwingine. Nafikiri mimi sikuwa mwanaume wa ndoto zake.” “Sasa ikawaje
aje akutaje kama wewe ndio mwenye mtoto kama alikuwa amepata mwanaume wa ndoto
zake!? Kwa jinsi nilivyosimuliwa, ni wewe tu ndiye aliyekutaja kwa dada yake.
Hakumpeleka kwengine isipokuwa nyumbani kwenu. Inamaana angekuwa amewachanganya
wanaume wengi, angewataja wanaume wote. Lakini wanasema alimleta mama mkubwa,
kwako tu. Na ulivyokataa, hakumtaja mwingine akaishia kulia tu, mpaka kifo
chake.” Nanaa akaweka msisitizo.
“Sasa hivi ndio
nimeelewa kwa nini alinitaja mimi.” “Unamaanisha nini?” Nanaa akaendelea
kuhoji. “Nahisi nilipatwa na wivu. Hapo ndipo nilipokosea na kuharibu kila
kitu. Mama yako hakuwa muhuni, ila mtoto. Mimi ndiye nilianza naye mapenzi.
Nikamtambulisha kwa rafiki yangu..” Geb akageuza kiti kwa nguvu mpaka kikasugua
sakafu, kisha akamgeukia Lubuva. Nanaa na Lubuva wakamtizama. Nanaa hakuelewa,
lakini Lubuva akaelewa. Akapata ujumbe wake vizuri, akabadili alichotaka
kuzungumza.
“Samahani. Endelea
dokta Lubuva.” Nanaa akarudisha macho kwa Lubuva. Na Geb naye akamkazia macho.
“Ndio nilikuwa nasema, nahisi tatizo lilikuwa wivu. Nilipomtambulisha kwa
rafiki yangu, wakaanza kuwa karibu. Ndipo nikaanza kupatwa wivu, nikahisi wana
mahusino ya kimapenzi. Nikazungumza na Wini kumuomba apunguze huo ukaribu. Au
niseme nilimuonya aache kabisa ukaribu na yule jamaa. Siku hiyo ya mazungumzo
tulikuwa na Wini usiku wote. Sasa baada ya siku kadhaa, nikaambiwa Wini
ameonekana tena na yule jamaa!”
“Basi hapo ndio
nikakata mawasiliano nao wote wawili. Tena kwa kumuita yule rafiki yangu na
kumuonya asinitafute tena na amwambie hivyohivyo Wini. Kwa hiyo nikapotezana
nao wote wawili. Baadaye ndio Wini na dada yake wakanijia nyumbani. Wini akiwa
analia anasema mimba ni yangu!” Lubuva akajieleza kwa tahadhari sana.
“Nilikosea Nanaa.
Tokea mwanzo nilikosea. Kumbuka nilisikia tu kuwa Wini alionekanika na jamaa.
Sikumuuliza. Pengine ningemuuliza, ningejua nini kilikuwa kikiendelea. Mimi
nikakasirika tu na kuwapiga marufuku wasinitafute tena. Sijui kama unanielewa?”
Nanaa akavuta pumzi kwa nguvu, hakujibu.
“Wini aliletwa nyumbani na dada yake,
sio kuniambia kuwa ana mimba yangu, hapana. Dada yake alinijia juu akaniambia
anataka kunishitaki kwa kumpa mimba mtoto chini ya miaka 18, maana mimi hapo
tayari nilikuwa nimeshatimiza miaka 18. Alituogopesha. Wakati huo baba
ananiangalia. Ni mkuu wa mkoa, na amehangaika kunitafutia chuo, nina kila kitu
mkononi, natakiwa tu kuondoka. Kwa ujinga na hofu, nikiwa nimemchukia Wini
nikijua amenisaliti, njia pekee iliyokuwa rahisi, nikijua anadanganya mtoto sio
wangu, pengine anataka tu pesa zangu, kwa kuwa mimi nilikuwa mtoto wa mkuu wa
mkoa, na jamaa alikuwa mtu tu wakawada. Nikamkana. Nilitumia kila neno
nililojua nitawaondoa pale na kwenye maisha yangu, ili niwe huru, niondoke
nchini kwa haraka.” Wakamuona machozi yakimtoka Nanaa.
“Nilikosa Nanaa.
Nilikosea tokea mwanzo. Natamani kama Wini angekuwepo nika..” “Ulishawahi hata kumpenda au alijirahisisha tu kwako
ndipo ukawa ukilala naye kila unapohitaji?” Nanaa akauliza huku machozi
yakimtoka. “Kwa sababu namfananisha na mimi. Na
yeye baba yao aliwakimbia sababu walikuwa wakizaliwa watoto wa kike. Pengine
alikuwa akitafuta kimbilio. Kutaka upendo wa mwaume, asijue anajiingiza
matatizoni! Aliangukia kwenye mikono ya rafiki yako, kitu kilichokuudhi wewe na
kumtupilia mbali. Akateseka peke yake mpaka kifo. Na mimi nimepitia hapo.
Kuangukia kwenye mikono ya rafiki yake Geb. Yakanipata kama yaliyompata mama.”
Hapo kidogo Nanaa akaweka usawa kati ya Geb na Lubuva. Lubuva akapata aghueni. Kabla
hajatulia, Nanaa akaendelea.
“Lakini
nikiwa kwenye hali ya kufa. Nimekata tamaa hospitalini, Geb alirudi kuniuguza.
Alisimama na mimi mpaka sasa. Huyo Jimmy, ni juzi nilipojifungua ndipo wote
tumejua ni mtoto wa Geb. Lakini kabla ya hapo, Geb alikubali kumpokea mtoto wa
rafiki aliyemsaliti. Akakubali kunioa akijua au watu wakijua nimebeba mtoto
asiye wake. Sijui kama unanielewa?” “Naelewa Nanaa.”
Lubuva akajibu.
“Ninachojaribu
kusema ni kuwa, hukuwa na mapenzi ya dhati kwa mama. Ulikuwa ukimchezea tu.
Ndio maana alipokosa, au tatizo lilipotokea, uliweza kuondoka kwa urahisi. Wewe
hudhani kama endapo ungekubali pale mbele ya watu, yaani usimkane. Ukazungumza
neno lolote kama vile, labda huna uhakika na mimba aliyobeba, ila unaomba
usubiri mpaka ajifungue ndipo mjue kama mtoto ni wako! Hudhani kuwa pengine
asingekufa? Hata kama ungeondoka kwenda masomoni, pengine ungemuacha akiwa
anaheshimika sio kunyanyaswa kama binti Malaya tu! Hudhani hivyo?”
Nanaa aliuliza kwa uchungu sana, lakini taratibu. Alijaribu kushindana na
machozi yake, lakini yakawa yakimlemea.
“Nilikosa Nanaa.
Nilikosea tokea mwanzo. Nafikiri utoto ulichangia, sijui nilipatwa na nini! Ila
nilimpenda Wini.” “Ulidhani kuwa ulimpenda. Upendo
unajidhihirisha pale mtu anapokosa. Ndipo upendo sasa unapojionyesha. Kusitiri
wingi wa dhambi, huhesabu, huvumilia na kadhalika. Sio wakati kila kitu kipo
shwari. Hukuwahi kumpenda mama yangu.” Lubuva kimya. Nanaa akajifuta
machozi.
“Ulimuacha
akidhalilika na kuteswa. Pengine alikuwa akikulilia wewe. Kuna ahadi zozote
ulizokwisha kumuahidi?” Nanaa akauliza. Lubuva akababaika sana. “Ndiyo au hapana?” “Nilijua angetulia na mimi
mpaka tuje kuoana. Nilimuah…” “Kwa hiyo hakuwa
ametulia!?” Nanaa akauliza kwa kushangaa. Geb akakaza macho. Napo hapo
Lubuva akaanza kurudia hili na lile. “Kumbe ni
alikuwa na mahusiano ya kimapenzi na huyo rafiki yako na sio ukaribu tu!?”
Lubuva akashikwa kwenye kutaka kuficha ukweli. “Alikuwa mtoto mdogo, Nanaa. Ni
mimi ndiye niliyeshindwa kumlinda mpaka akaangukia kwenye mikono ya huyo rafiki
yangu.” Nanaa alilia sana. Alilia kwa uchungu sana. “Naona inatosha kwa leo.
Mtaendelea wakati mwingine. Kama hakuna dawa ya kumpa, naomba umwache
apumzike.” Geb alimwambia Lubuva.
“Naomba nikwambie kitu
nilichofikiria. Pengine kilichokuwa kikimfanya alie sana.” Nanaa akajifuta
machozi akitaka kumsikiliza. “Mara ya mwisho nilipokuwa na mama yako,
nilimbembeleza aniambie ukweli juu yake na yule jamaa. Kwa ahadi ya kuwa
chochote atakachoniambia, mimi nitakipokea, na nitamsamehe hata kama alishalala
naye. Akiwa na hofu, Wini alikiri. Nikamwambia kama ataachana na yule jamaa,
tena kwa kumtamkia wazi, mimi na yeye tutaendelea na tutakuja kuona na kuwa na
maisha ya pamoja. Akakiri na nikamthibitishia kuwa nimemsamehe, ndio tukatumia
usiku huo pamoja.”
“Sasa nafikiri,
pengine alirudi kwa yule jamaa labda kuvunja mahusiano akiwa tayari ameshika
mimba bila yeye mwenyewe kujua. Akaachana na yule jamaa, halafu na mimi
nikamtumia ujumbe kuwa sitaki tena kumuona. Pengine alijiona amekosa kote kote.
Na mimi nilimkataa baada ya kumtumia usiku kucha. Sasa nashuku alipokuja
kujigundua ni mjamzito wa mimba yangu na mimi nilimkana baada ya yote hayo,
halafu alikuwa mtoto, ndio maana alikuwa akilia. Mimi ndiye nilikosea Nanaa.
Nilikosea tokea mwanzo wa mahusiano. Nakiri mimi ndiye niliyesababisha kifo
chake. Na upo sahihi, angalau ningekubali nilishakuwa na mahusiano naye ya
kimapenzi, siku alipoletwa kwetu, na mbele ya kila mtu, pengine ingemsaidia.
Lakini nilikosea Nanaa. Naomba unisamehe. Hakika unisamehe, nilikosa.”
Akamuona Nanaa ametulia, akafunga macho bila kujibu kitu.
“Alikuwa na dimpozi
kubwa kama hizo zako.” Nanaa akafungua macho, akatoa tabasamu. Lubuva
akamsogelea karibu. “Meno yake ya hapa mbele yalikuwa yamepandana kidogo. Ni
kama ncha ya jino moja ilipanda kidogo juu ya jingine. Ungependa kumwangalia
akicheka. Hata kama unahasira, akicheka, lazima moyo wako ufarijike. Na
alipenda kucheka. Hakuna kitu utazungumza, Wini asicheke. Hakuna tatizo kubwa
kwake. Kila kitu ukimwambia kama tatizo, atakipunguza uzito wake, mpaka uone
huna tatizo kabisa.” “Kama Nanaa.” Geb akaongeza, Nanaa akacheka.
“Alikuwa akipenda
kula?” Nanaa akauliza. “Mmmh!” Lubuva akawa kama anavuta kumbukumbu, akacheka.
“Alikuwa mwembamba. Hakuwa na mwili. Ila Wini alipenda kucheka.” Wakamuona
Lubuva ameina kama anakumbuka kitu, akacheka. “Alikuwa na namna yake yakumfanya
mtu ajisikie vizuri. Nafikiri ndio maana nilipenda kuwa naye karibu. Sikumbuki
kucheka hivyo tena. Halafu…” Akataka kuzungumza kitu, akacheka na kunyamaza.
“Kwa hiyo hatujafanana
hata kidogo!?” Nanaa akauliza. Lubuva akacheka. “Nimekwambia hizo nywele ni
zake.” “Mama naye! Ndio nini sasa! Wenzake wanarithisha watoto wao vitu vizuri,
yeye ananipa kipilipili hiki!” Wakacheka. “Na dimpozi hizo ni zake. Kwetu
hakuna mwenye dimpozi.” Lubuva akaongeza, Nanaa akacheka, Geb akaweka kidole
pale shavuni. Wote wakacheka. “Ila yeye kipilipili chake kilikuwa chekundu.”
Lubuva alimfanya Nanaa na Geb wacheke sana. “Alikuwa anakata nywele chini sana.
Hakuwa akithubutu kuacha nywele zake zikue. Alikuwa akisema akichana, nyumba
nzima itajua yupo mahali anachana nywele zake.” Nanaa alizidi kucheka.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Mara akaingia mama G
na Liv. Uso mwekundu na macho kama aliyekuwa akilia. “Mbona mama mzazi analia?”
Nanaa akauliza. “Kwanza mbona hushangai tumekuja mapema? Sasa hivi huu sio muda
wake wakuamka, lakini hakulala vizuri na asubuhi ameamka anakulilia.” Mama G
akajibu. “Pole Liv mwanangu. Njoo.” Nanaa akamwita. Liv alikuwa anavuta pumzi
kama anayetaka kulia. Geb akamvua viatu akampandisha pale kwa mama yake.
“Nampenda Liv.” Nanaa akamkumbatia. Liv kimya.
“Labda aliogopa vile
alivyokuona na hizo mashine, halafu hamkupata muda mrefu wa pamoja.” Mama G,
akaongeza. “Usiwe na wasiwasi Liv. Mimi ni mzima. Jana nilikuwa tu na
usingizi.” Kimya. “Liv!” Nanaa akamwita taratibu akiwa amemlalia. “Mwangalie
mama basi!” Liv akamwangalia na kumbusu pale kifuani.
“Nampenda mama.” “Nampenda sana Liv. Umemuona dad?”
Liv akamwangalia. “Nampenda Liv.” Geb akaongea naye kwa upole. “Nampenda dad.”
“Naomba basi nikusalimie binti Magesa.” Liv akasimama na kwenda kwa baba yake.
Geb akamuweka kifuani.
“Mmmmmmh!” Walimuona Geb akigugumia
huku akifunga macho. Kisha akaanza kumbusu. Liv akaanza kucheka kama aliyekuwa
akisubiria. “Nampenda dad.” “Nampenda sana Liv.” Akacheka na kidole chake
mdomoni. Lubuva akamsogelea. “Liv!” Akamwita taratibu. Liv akamwangalia Lubuva,
akajificha shingoni kwa baba yake. “Kuna kitu nimeficha kwenye moja ya mmkono
wangu. Ni upi?” Akamuuliza Liv.
Liv akajitoa kwenye
shingo ya baba yake. Akaangalia mikono ya Lubuva aliyokuwa amemnyooshea huku
amefunga ngumi. Akaitizama kwa makini, kisha akamtizama na yeye. Akamtizama
kidogo na kurudisha macho kwenye ile mikono. Kila mtu kimya akimtizama.
“Ukipatia, nakupa kazi yakumpima mama yako pressure.” Liv akacheka, na
kunyoosha kidole kwenye mkono wake wa kushoto. Lubuva akafungua. Alipatia. Wote
wakacheka. “Liv wewe ni mtoto mwenye akili sana. Haya njoo tumpime mama
pressure. Subiri kwanza nikuonyeshe.” Geb akamuweka pale kitandani.
“Unapenda kuja kuwa
daktari?” Lubuva akamuuliza. “Kwa akili ulizo nazo wewe, unaweza kuja kuwa mtu
yeyote yule na ukafanya vizuri sana.” Liv akacheka. “Haya, mimi namfunga mama
mkono. Wewe unatakiwa ubonyeze hapa. Namba zikisha andikwa hapa, ndio tutajua
pressure ya mama. Sawa?” Liv akatingisha kichwa kukubali. “Nampenda mama.”
Lubuva akamwangalia. Liv kidole mdomoni, anacheka na dimpozi zake. Lubuva
akacheka nakurudisha macho kwenye mashine. Liv akabonyeza kama alivyofundishwa.
“Safi sana.” Lubuva akamsifia.
Matokeo yalipotoka,
Lubuva akazima bila kusema kitu. Nanaa akajua majibu sio mazuri. “Asante
kunisaidia kumpima mama.” Liv akacheka. “Unataka nikupe kazi nyingine?” Liv
akaitikia kwa kichwa. “Muwekee mama hiyo mashine ndogo ya kidoleni. Mvalishe
kwenye kidole, halafu nakuletea plasta ili uifunge vizuri isitoke anapolala.
Unafikiri utaweza?” Liv akatingisha kichwa kukubali huku anacheka. Kila mtu
alikuwa akiwasikiliza na kuwaangalia.
“Vipi pressure yake huyo?” Mama G akauliza. James naye akaingia. “Shikamoo kaka.” “Marahaba. Angalau leo unaongea. Ulinitia wasiwasi jana!” “Wamenipunguzia dawa. Angalau leo nimeweza hata kula vizuri.” “Vipi pressure?”James akauliza huku akimtizama Lubuva na Nanaa. “Nitatoa majibu kamili kesho. Naona tuendelee kuiangalia tu.” Lubuva akajibu kwa kifupi.
“Si unaona sasa hivi
hizo mashine haziogopeshi tena?” Liv akatingisha kichwa kukubaliana na dokta
Lubuva. “Basi, mimi naomba nikushukuru kwa kunisaidia kumpima mama na kumuwekea
hiyo ya kidoleni. Inaitwaje tena?” “Puz Oximta.” Kila mtu akapiga makofi kwa
jinsi Liv alivyojibu. “Kweli wewe Liv ni mtoto mwenye akili. Sasa unajua kazi
iliyobaki?” Liv akacheka. “Nikuendelea tu kusoma pale, na kumfanya mama
apumzike. Unajua kumbembeleza alale?” Liv akacheka huku anatingisha kichwa
kukubali. “Basi. Hakikisha ukilala, na yeye analala.” Liv akakubali.
Baba.
“Nitawaona baadaye.”
Lubuva akaaga, ili atoke. “Naomba usiondoke, nikutambulishe kwanza.” Nanaa
akamuwahi. Lubuva akabaki akimtizama Nanaa. Wote kimya. Wakamgeukia Nanaa.
Gafla Nanaa akaishiwa maneno. Akawa hajui amtambulishaje. Wakamuona machozi
yanatoka, akanyamaza. Mama G akamgeukia Geb. “Ni nini tena!?” Geb naye kimya.
James akabaki na yeye haelewi. “Huna haraka Nanaa. Chukua muda wowote
unaotaka.” Geb akasimama na kumsogelea. “Ni sawa?” Geb akamuuliza. Nanaa
akatingisha kichwa kukubali. James akabaki kimya akimtizama dokta Lubuva na
Nanaa.
Kisha akamuuliza.
“Wewe ni nani?” James akauliza. Mikono mfukoni, amekunja uso kama aliyeanza
kuhisi kitu. “Wewe ndiye uliyekana mimba ya mama mdogo Wini?” James akauliza
swali la moja kwa moja. Mama G akatafuta sehemu akakaa. “Ndiyo. Mimi ndio baba
yake Nanaa.” James akaanza kubadilika sura. Geb na Nanaa wakajua hasira
zinapanda. Wakamuona anatoka bila kuongeza neno. Ukimya ukazuka. Kimya kikaongezeka.
Hakuna aliyejua aongeze nini. “Nitawaona baadaye. Kwaheri Liv.” Lubuva akatoka
na kuacha kimya. Hata mama G alishindwa chakuongea.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Siku hiyo Nanaa
alishinda hapo hospitalini na Liv. Mama G aliondoka na Jimmy. Nanaa hakuwa na
maziwa yakunyonyesha kwa hiyo mama G aliondoka na kwenda kumpa maziwa huko
nyumbani. Jioni walirudisha watoto wote. Nanaa akaweza hata kuwashika. Magesa
alionekana kufurahi sana kumuona mama yake. Japo fujo zilimzidi. “Jamani
Magesa! Ninahamu na wewe lakini hushikiki mwanangu. Tulia basi!” Cheko
lilimjaa, kuruka ruka ndio kukazidi. Kila mtu alikuwa anacheka. Kila wakati
alitaka amshike Jimmy. Alirudishwa Jimmy akiwa ameshabadilika. Alivalishwa
vizuri, akafanania kweli na kina Magesa. Nanaa akawa ameridhika.
“Hajasumbua?” Nanaa
akauliza huku akimuweka sawa pale alipokuwa amempakata. “Naona huyu atakuwa
kama baba yake. Mkimya kama Liv.” “Mama wewe! Sasa unataka kusema Magesa
amefanana na wewe!?” Wote walizidi kucheka. “Mimi sijui! Ila ninachosema ni
kuwa, Jimmy na Liv, ni wa kimya kama baba yao. Inawezekana wamerithi kwangu.”
Mpaka Grace alicheka. “Mimi naomba tumsubiri kaka aje asema vile nilivyokuwa
mpole kama Liv.” “Ila huwa anasimulia sana stori zako Nanaa.”
“Kuwa nilikuwa mpole
kama Liv?” Nanaa alifanya wazidi kucheka. “Mimi siwaelewi jamani! Mbona sisikii
jibu la ndiyo! Eti Magesa? Wewe umefanana na bibi?” Magesa akazidi kucheka huku
anaruka. “Mwenyewe pia amekataa!” Mama G akajibu, Nanaa akacheka. Siku hiyo
ikaisha vizuri.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Ilipofika saa 10 na nusu jioni, wote wakaondoka. Geb ndiye aliyetaka waondoke na watoto ili Nanaa apumzike. Walipotoka tu, Lubuva naye akaingia. “Kuna kitu nataka kuzungumza na nyinyi.” “Kuna nini?” Geb akauliza. “Leo nilikuwa na mazungumzo ya muda mrefu na hao madaktari juu ya vipimo vya Nanaa, wote wameshauri kuwa Nanaa afanyiwe upasuji kwa haraka. Hawezi kuendelea kuishi hivi akiwa ana pressure ya juu.” Nanaa kimya. “Mungu naomba unisaidie. Please!” Geb alisikika akizungumza na Mungu wake. Mikono akaiweka kichwani, wakamuona anatoka. Nanaa kimya.
Baada ya muda akarudi. “Anafanyiwa wapi na
lini?” “Yule daktari wa Ujerumani, ameniambia siku yeyote nitakayompeleka,
atamuhudumia. Kwa swala la lini, ninataka kukusikia wewe ili nianze kutayarisha
makaratasi yakusafiria.” Geb alionekana wazi zile sio taarifa alizotarajia kwa
aina ya maombi aliyokuwa akimuombea Nanaa. Alijua Nanaa atapokea uponyaji wake.
Kama sio muujiza wa moja kwa moja kutoka kwa Mungu, basi pengine Lubuva
angekuja na dawa au aina nyingine ya matibabu ili kumsaidia Nanaa. Kusikia
Nanaa anatakiwa kufanyiwa upasuaji, tena Ujerumani! Hazikuwa habari njema
kwake. “Usiogope Geb.” Nanaa akamshika mkono. “Nitapona tu.” Geb kimya.
Lubuva akaanza kuwapa
muongozo wa nini chakufanya. Akawaelewesha. Muda Nanaa anaotakiwa kutumia huko
nchini Ujerumani kwa matibabu. Geb alibaki kimya. “Lakini siwezi kuondoka na
wewe bila baraka za kaka. Hajarudi tena hapa. Lazima nizungumze naye kwanza. Na
umueleze kwa kirefu na aelewe kwa nini ulimuacha mama. Mkipatana na kaka, ndio
nitaweza kuwa karibu na wewe. Kaka James ndiye mama, baba na ndugu wa pekee
niliyemfahamu maishani. Sina maisha mengine bila kaka.” “Naelewa. Nilikuwa
nikifikiria nimtafute leo, tuzungumze naye.” “Hapo itakuwa sawa.” Wakakubaliana
hivyo. Wakamuona Geb anatabasamu kama anayefikira kitu.
“Nini?” Lubuva
alimuuliza. Geb akacheka kidogo kama
anayefikiria. “Sijui nikwambie ‘good luck!’ au ‘join the club’?” “Kwa nini?”
Lubuva akauliza. “Nahisi ni kama unahitaji vyote.” Geb akaendelea na tabasamu
usoni. “Kwa nini? Mbona unanitisha!?” “Nashauri ujiandae tu kwenye hicho kikao
chako na James.” “Nitajitahidi kuwa muwazi.” “Na pia uwe na kiasi kwenye uwazi
wako. Maana linapofika swala la Nanaa kwa James, kwanza ujue hana aibu wala
hofu. Hana ndugu wala rafiki. Ni kaka kwa Nanaa kwa utaratibu huu uliowekwa
hapa duniani.”
“Lakini kiukweli, ni
kama mama aliyebeba mimba ya Nanaa. Inakuwa ni kama mama aliyepitia hatua zote
za mimba. Kuanzia siku ya kwanza mpaka mwisho akazaa baada ya kupitia ule
uchungu wa masaa mengi kabla ya kuingizwa kwenye chumba cha kujifungulia. Ndio
James kwa Nanaa. Swala la kutokumuona hapa leo, usifikiri ametingwa na kazi.
Huwa hakuna kitu kinasimama kati yake na Nanaa, wewe ndio utakuwa wa kwanza. Na
hawezi kukubali kwa urahisi. Kwa hiyo nafikiri nikuambie, ‘Good luck as you
join the club’! Maana mimi nilipita hapo ulipo. Tena kwa kuponea ngumi zake
mara kadhaa.” Lubuva akatulia akitafakari huo ukaribisho anapojiunga chamani.
“Hajui maisha mengine bila huyu Nanaa.
Na ni kweli wewe na Wini, mlimpokonya utoto wake, ujana wake na ndoto
zake zote. Mimi nakutana na James tukiwa watoto wadogo au vijana wadogo sana,
kundi letu wote lilikuwa likifikiria kucheza mpira, na stori za starehe za
maisha, lakini yeye James mazungumzo yake yalikuwa ni kama mama aliyetelekeza
mtoto nyumbani. Atakwambia maswala ya poda, nepi, mafuta ya kupaka watoto, uji
na mambo ya kunyonyesha. Nazungumzia James. Mtoto wa kiume wa pekee nyumbani
kwao! Very smart darasani, lakini anashahada moja sababu ya Nanaa.”
“Wengi wetu, tuliokuwa
darasa moja, wameendelea kusoma zaidi ya James, tena wakiwa hawana akili kama
James, sababu ya Nanaa. Kwa hiyo ujiandae vizuri sana. Hata hii safari
unayopanga kwenda na Nanaa, nashauri iwe ya kuomba ruhusa, sio kumtaarifu.”
“Haiwezekanai! Nanaa ni mgonjwa, akikataa!? Hata kama kuna tofauti zetu,
tuzimalize baada ya Nanaa kupona.” Lubuva akabisha. Geb akashangaa sana.
“Unafikiri hapo alipo Nanaa ni mgonjwa wa kushitua mtu! Au unafikiri yupo
kwenye hatari yakumpoteza!? Acha kabisa Lubuva! Tena usirudie kubisa.” Geb akambadilikia kwa hasira.
“Ulikuwa wapi miaka
yote hiyo!? Unajua kitovu cha Nanaa kilisafishwa na nani pale alipotolewa
hospitalini baada ya Wini kufariki? Unajua Nanaa alinyonya wapi baada ya mama
yake kufariki? Wakati mama yako anakuficha kama una mtoto, James aligombana na
wazazi wake sababu ya kumlea Nanaa! Wewe unakiri unampenda sana mama yako,
lakini ujue James amempoteza mama aliyekuwa akimpenda kama mtoto wa kwanza na
wakiume pekee nyumbani kwao, sababu ya mtoto mliyemuacha wewe na Wini, na kwa
sababu ya mtoto aliyekuficha mama yako unayempenda. Umepokonya mapenzi ya James
kwa mama yake! Mmeua mahusiano ya James na mama yake, sababu ya kumtelekeza
Nanaa! Mkamuacha hana wakumtetea ila James!”
“Hivi unanielewa
nikikwambia au baba yake akikwambia umeua malengo na ndoto za James lakini?
Wakati sisi tunasoma, James alikaa chini kama mama akimlea Nanaa. Wakati sisi
tuna wanawake, James alishindwa kuwa hata na wazo la msichana yeyote ili asije
akajisahau kwa Nanaa. James hajui starehe ya mwanamke sababu ya Nanaa! Wakati
mimi na wewe tunazisaka pesa, na kumkimbia Nanaa, James hakuwahi kumtua chini.
Amemtunza Nanaa kwa pesa ya matumizi aliyokuwa akipewa na wazazi wake.
Alipofika chuo kikuu, akawa anamtunza kwa BUMU! Sijui kama unanielewa?” Geb
akambadilikia kwa hasira sana.
“James anakuja shule
hana hata shilingi sababu pesa alizopewa za matumizi, amemnunulia Nanaa vitu
vya shule na vya kujikimu, pamoja na kumlipia ada. Nanaa anavunja ungo, dada au
mama anayemshirikisha na kumuomba pedi ni James! Mimi nilikuwa nikimwandikia
darasani na kuja kumfundisha kama mwalimu wake, kwa kuwa ilikuwa ikimlazimu
James kutoroka au adanganye anaumwa, ili arudi nyumbani akamwangalie Nanaa na
kukaa naye kidogo. Sijui kama unanielewa Lubuva!?” Geb akamuuliza kwa hasira.
“Ukifikiri wewe ndio
una njia moja ya kumtibu Nanaa, wewe mwambie James kuwa umeshindwa kumtibu
Nanaa umsikie. Kama unafikiri mimi ndio nakesha na Nanaa hapa hospitalini, basi
jua James halali huko nyumbani. Anatafuta dawa na hospitali ya kumpeleka Nanaa.
Kama huamini, subiri aje hapa, mwambie matibabu uliyompa Nanaa yameshindwa
kumsaidia, halafu uone. Kila akija hapa, anasoma kile kijalida cha Nanaa.
Anasoma dawa unazompa, na lazima azungumze na nesi. Hutamtisha James kwa
kumwambia eti Nanaa hatapona bila wewe. Mpaka tunazungumza hivi, sitashangaa
kama ameshaweka mpaka appointment ya daktari aliyempata yeye, nchi nyingine,
aliyesikia ni bingwa. Na hatamuomba mtu pesa. Ni kwa pesa zake. Kwa hiyo,
ujipange kweli unapozungumza na James.” Lubuva akabaki hoi.
“Na ujipange sawasawa.
Maana linapofika swala la Nanaa kwa James, hatishwi na pesa wala wadhifa wa
mtu. Na anapoona unasuasua au unashindwa kumsaidia Nanaa kwa haraka, anaweza
kuja na kumbeba kumtoa alipolala Nanaa na kumpeleka anakojia wanaweza kumsaidia
kwa haraka. Mbele yetu, katikati yetu tukimwangalia, anaweza kutoka naye
mlangoni. Hawezi kusubiri linapofika swala la Nanaa. Wewe si unasema unaye
daktari bingwa huko Ujerumani?” Lubuva kimya.
“Sasa ukamuulize yeye
anao wangapi. Atakutajia madaktari bigwa wa dunia nzima, wale wenye uwezo wa
kukabiliana na ugonjwa huo wa Nanaa. Na hakika atamchukua na kumpeleka
akatibiwe. Alimtoa Nanaa kwenye kitanda chetu. Namaanisha changu mimi na Nanaa.
Tukiwa ndio tunaamka, tupo na nguo za kulalia tu, aliingia. Akampita kila mtu
aliyekuwa mlangoni na chumbani na kumbeba Nanaa kumkimbiza hospitalini na
kutuacha tumeduaa.”
“Wakati wewe
unajiuliza ni nini chakufanya na Nanaa, yeye anakuwa ameshajua. Na hata ukiwa
naye huwezi kumdanganya. Muulize Nanaa. Na hajui unafiki, na ni ngumu kunyamaza
akiona humtendei Nanaa anachojua anastahili. Ndio mtu wa kwanza na wa pekee
unayehitaji baraka zake ili uwe karibu na Nanaa. Narudia tena, ni kama mama mzazi,
kwa Nanaa. Nanaa ananyonyesha wanae kwa ziwa, James alimnyonyesha Nanaa kwa
kidole chake hiki kidogo. Tokea siku anatolewa hospitalini mpaka mimi nampokea
Nanaa, James ndiye anahusika na kula, kuvaa pamoja na furaha ya Nanaa. Na wala
sio mama yake uliyemjengea nyumba kwa malipo aliyokutajia. Labda kumpa
hifadhi.” Nanaa aliyekuwa akitokwa na machozi akashituka sana.
Mama
James kwa Lubuva Pia!
Nanaa akajiweka sawa
pale kitandani na kuuliza kwa mshangao. “Umemjengea
mama mkubwa nyumba!?” Geb kimya. “Kwa
nini!?” Nanaa akauliza tena kwa mshangao huku akimuangalia Lubuva. “Kwa
malipo kama vile alivyolipishwa Geb. Lakini mimi ilikuwa zaidi na hakutaka
kunipunguzia kwa kuwa nilimtelekeza Wini, nikamuachia yeye mzigo.” Nanaa alilia
sana.
“Mlikutana
wapi mpaka akulipishe?” “Mimi mwenyewe ndiye ilinibidi kumtafuta ili kujua
ulipo. Ndiye aliyenielekeza kwako na kwa James.” Lubuva akajibu nakumfanya
Nanaa kushindwa kuamini. “Mungu wangu! Kwa nini
ananifanyia hivyo, kuniuza kwa kila anayemuahidi pesa bila kuniuliza mimi
mwenyewe? Nakuwa sina uhuru na maisha yangu! Kwa nini na wewe ulimlipa sasa?”
“Kwa sababu bila hivyo alisema asingeniambia ulipo, na akasema angenishitaki na
kunitangaza katika kila chombo cha habari. Asimulie ubaya niliokuwa nimemfanyia
mdogo wake akiwa mtoto mdogo mpaka kumsababishia kifo. Mara ya kwanza akataka
pesa. Nikampa ile pesa, lakini akanibadilikia. Akaniambia ile ni pesa ya
kunitajia tu jina lako. Akataka nimjengee nyumba hapa Dar ndipo aweze kunitajia
ulipo wewe. Hapo alikuwa amekataa kabisa hata kuniambia ulipo wewe wala James.
Na alinionya kabisa.” Luvuva akafikiria kidogo.
“Yule mama anaakili
sana. Kwa kuwa alishajua najua jina la James na jina lake la ukoo, akajua
sitapata shida kumpata James. Ndipo sasa akaja kwa vitisho vya kunishitaki
endapo nitamtafuta James. Aliniambia mimi na Wini tulimwachia huo mzigo yeye,
na nitachukua huo mzigo kutoka kwake pindi nitakapokamilisha malipo yake yaani
hiyo nyumba. Kinyume na hayo masharti yake, atahakikisha naishia jela.
Akanionya nisiwahi kumtafuta James wala kumshirikisha kwa lolote. Iwe mimi na
yeye tu. Ndipo kazi ya ujenzi ikaanza. Hakuwa na makuu kwenye hiyo nyumba. Ila
tu alitaka nyumba ya vyumba vinne. Nikaanza ujenzi, wakati nakaribia kumaliza,
nikamfuata tena kumuomba anitajie hata ulipo. Nikamuahidi sitakufuata ila tu
kukuona. Akasema nikirudi kwake na hati ya nyumba pamoja na funguo, atanitajia
ulipo. Alikataa katakata.” Lubuva akaendelea.
“Basi, ikabidi
kukazana na ujenzi mpaka nilipokamilisha ndipo nikamtafuta ili kwenda kujaza
fomu za umiliki wa ile nyumba. Alipojaza kila kitu, ndipo nikamwambia kabla ya
kukamilisha hatua ya mwisho, nilazima anipeleke unapoishi wewe.”
“Akanieleza jinsi
ilivyo ngumu kuingia hapo nyumbani kwako. Kuna ulinzi mkali, akalalamika kuwa mlimdhalilisha
sana alipokuja hapo kwenu akiwa na binti zake. Na malalamiko mengi tu ya jinsi
Nanaa ulivyomuacha sebuleni katikati ya watu asio wajua, halafu akaenda kulala,
wakati yeye hakukutelekeza hospitalini baada ya Wini kufariki. Hapo napo
yalikuwa malalamishi ya karibia siku mbili. Kila nikimfuata, analalamikia hili
na lile. Siku ya tatu ndio akakubali kunileta sasa mpaka kwenu lakini
akanionyesha nyumba kwa nje, akasema yeye hataki kuingia tena ndani. Ndio
safari za Tabata zikaanza sasa. Kukusubiria labda utakuja kutoka nikuone.”
Lubuva akanyamaza kama anayefikiria. Akacheka huku akivuta mawazo.
“Siku nakuona pale
dukani umekuja kuulizia dawa ya kukausha maziwa, sikutambulishwa na mtu. Lakini
nilijua wewe ni mtoto wangu au wewe ndiye Nanaa na wala mama hakukosea kuwa
wewe ni damu yetu. Nilimuona mama kuanzia kichwani mpaka miguuni.” Lubuva
akafikiria kidogo.
“Baada ya hapo sasa
ikabidi kuanza kukufuatilia kwa karibu. Nikawa siwezi kusubiri tena sababu
tulikutana ukionekana ni mgonjwa na huna furaha kabisa. Siku nakuona umezidiwa
na pressure upo kituo cha daladala, ukakataa kupanda taksii, nikaamua
kukufuatilia na gari yangu. Sijui yule dereva wa daladala alifanya nini!
Tukapotezana. Nikaja kuiona tena ile daladala tukiwa tumeshafika Ubungo. Nikasimama
kwa haraka, nikatafuta sehemu ya kuegesha gari ili na mimi niingie mle ndani
kama abiria. Nilipopanda ukawa haupo ndani ya ile gari ndio nikawa nimekupoteza
kabisa. Nikawa sijui pakukupata.” “Nilizidiwa ndani
ya daladala kabla hata hatujafika Ubungo. Ndio nikaona ni heri nishuke nichukue
tu taksii inikimbize hospitalini.” Nanaa akajibu.
“Basi ndio sababu. Basi, nikaamua kurudi kukuulizia pale kwa wale walinzi wa nyumbani kwenu kwa kuwa niliingiwa hofu yakutaka kujua kama ulipata matibabu, lakini wale walinzi walinizungusha karibia kukata tamaa. Nikamfuatilia mmoja wao, baada ya kazi. Nikambembeleza sana na kumwambia sitamwambia mtu kama amenisaidia kujua ulipo na unaendeleaje.” Lubuva akanyamaza kidogo. Wakamuona amebadilika mpaka uso.
“Ndipo akanieleza
mkasa mzima. Lakini akaniambia yeye hakuwepo usiku wa tukio hilo la Malii,
lakini anajua kama mumewe na Nanaa alimkimbia na watoto wake. Watoto huwa
wanaletwa hapo, lakini Nanaa haruhusiwi kuwashika. Hapo ndio nikajua chanzo cha
ugonjwa wako. Haya, akasema kuwa uliondoka hapo, hujulikani ulipo, hiyo ni week
ya pili sasa. Hakuna mwenye habari zako. Nikajua utakuwa umelazwa mahali.
Nilichokosea, nilikuwa naulizia madaktari wa mambo ya moyo. Jamani nilihangaika
kukaribia kuchanganyikiwa. Nikahisi labda siku ile ulipopanda daladala,
ulianguka ukafa, ukaenda kutupwa kwenye vyumba vya maiti. Nikaanza kupita sasa
kwenye nyumba za maiti. Sikufanikiwa.” Lubuva akaendelea na kushangaza wote
wawili.
“Ikabidi niulizie
madaktari wote sasa. Sifahamu jina la pili. Najua Nanaa tu. Baadaye ndipo Rweta
akaniambia jina sio geni. Akaanza kunisaidia kutafuta kwenye orodha ya wagonjwa
wake. Ndipo baadaye akaniuliza tena kama nafahamu jina Wini. Hapo ndipo nikajua
amekupata. Ila akasema wewe ni mgonjwa wa Lyamu. Nikitaka habari zako zote,
nimtafute Lyamu maana na yeye alikufahamu au ulipelekwa kwake na Lyamu. Yeye
alikuwa nchini India, msaidizi wake ndio alimtumia jina la Nanaa
Wini.”
“Haya, ndipo ikabidi
sasa kufahamiana na Lyamu ili aweze kunipa habari zako. Lyamu ni mgumu! Hujawahi
ona. Anamlinda Nanaa, kuliko utakavyojua. Ikabidi kumuomba tena Rweta
anitambulishe rasmi kwa Lyamu. Baada ya mahangaiko, Lyamu ndipo akafunguka
sasa. Akanieleza kwa kifupi juu ya afya ya Nanaa. Rweta naye akawa amerudi,
nikamuomba tukutane ofisini kwa Rweta ili tuzungumze tujue chakufanya.”
“Tukafanikiwa kukutana
ofisini kwa Rweta, Lyamu akiwepo na mafaili yako yote kuanzia mimba ya Oliva
ukiwa chuoni mpaka wakati huo.” Nanaa akainama. “Nikaanza kupitia faili moja
hadi jingine na dawa alizokwisha kupewa, na yule daktari wangu wa moyo wa
Ujerumani alikuwa kwenye skype. Swali likawa, je dawa alizopewa mara ya mwisho
na Rweta baada ya kujifungua Magesa, kama alizitumia na kushindwa kumsaidia?
Maana yule daktari wa Ujerumani alisema zile dawa ulizokuwa umepewa na Rweta,
ni nzuri sana. Zilitakiwa zikusaidie.”
“Haya, tukamtuma Lyamu
aje azungumze na wewe, kwa kuwa Rweta alisema nyinyi wawili huwa mnaelewana.
Lyamu kuja kukuuliza ukiwa wodini, ukaonekana hata hujui anazungumzia nini.
Mungu bariki na wewe Geb ukapiga simu kumuulizia Nanaa. Lyamu akakuuliza swala
la dawa, ukaonekana hukumpa. Ndipo sasa tukaelezwa wote kwa pamoja madhara
yake, na yule dada, daktari wa kule Ujerumani, akashauri upewe dawa nyingine.
Zilikuwa za garama kidogo. Tukasema ujaribishiwe ukiwa hospitalini,
zikikukubali, basi ndipo uruhusiwe. Swala la garama Lyamu akasema tusiwe na
wasiwasi. Maadamu Geb mwenyewe amerudi kwenye maisha ya Nanaa, mtamudu tu
garama.” Lubuva akacheka kwa kusikitika.
“Kama kuna kitu kibaya umerithi kutoka kwangu,
ni ubishi na msimamo unapoamua jambo lako. Sijakaa sawa, napokea simu kutoka
kwa Lyamu ananiambia muda ule tunazungumza, ulishajiruhusu pale hospitalini,
upo sehemu ya kuchukulia dawa, unasubiri upewe dawa zako uondoke pale
hospitalini. Umeamua kuondoka. Sikuamini. Nikamwambia akueleze madhara yote ya
kuondoka bila matibabu. Akaniambia umemwambia aache woga.” Wote wakacheka.
“Akaniambia kuja
kukuona wewe tena, ni siku unayorudi mahututi. Ndipo nikamwambia hutakuwa tena
na hiyo nafasi, lazima Rweta akupigie simu, akupe tarehe za kila wiki za
kumuona yeye. Akwambie ni kliniki ya lazima, na iwe na punguzo ili isiwalemee.
Kwa kuwa Rweta ni rafiki, akakubali kuwaona kwenye hospitali ya kulipia, kila
wiki, na mimi nikawa nalipa nusu, nusu nyinyi. Lakini vipimo vikawa vinatumwa
na kwa yule daktari Ujerumani ili washauriane na Rweta. Rweta akafurahia sana
hiyo. Kwanza alijiongezea rafiki na ujuzi pia. Ukaribu kati yetu ukaongezeka.”
Lubuva akaendelea.
“Sasa pressure ikawa
inazidi kuwa juu. Wakaonelea wamtoe mtoto kwa kuwa amekomaa ili wewe utibiwe.
Tulipomwambia hivyo Lyamu, akacheka sana. Akasema haitakaa ikatokea. Nikamuomba
aje akujaribishe. Akasema kwake yeye hutakaa ukakubali, labda sisi wenyewe
tuzungumze na wewe. Alipokuja kukwambia kuwa kuna daktari mwingine bingwa
anataka kukuona au uende ukamuone, ndio ukampa ule ujumbe kuwa dokta Rweta
aende yeye, akafundishwe na huyo mtaalamu ndio aje kukutibu wewe. Wewe hutaki
kubadilisha madaktari.” Wakacheka tena.
“Lyamu akaona
azungumze na wewe na Geb kuwapa madhara yote yakuendelea kubeba ile mimba. Ulichomjibu
Lyamu, akasema umemtuma hata kwa Rweta kuwa, tuache uoga. Kama Mungu
angetaka Jimmy akuzwe kwenye chupa, basi mimba yake ingeanzia kubebwa kwenye
chupa. Lakini alitaka wewe uibebe, kwa hiyo Jimmy atakua hapo tumboni,
hatatolewa, ila sisi ndio tutafute matibabu yakukufanya uishi wewe na mtoto. Mimi
huwa najijua ni mbishi, lakini wewe umezidi, aisee! Tulikaa tunafikiria jinsi
ya kukusaidia mpaka leo.” Mpaka Nanaa mwenyewe akacheka.
“Mimi mimba zangu nazijua. Nikianza kusikiliza
madaktari na sayansi zenu, nisingekuwa na mtoto hata mmoja. Halafu Lyamu ni
muoga sana.” “Kwa kuwa hataki upatwe na madhara.” “Mimi nitakuwa sawa tu.
Kwanza nataka kutoka hapa, nitembee kidogo. Najiona nimelala sana.” “Nanaa!!”
Geb akastuka. “Lakini hilo ni wazo zuri. Anahitaji mazoezi. Nilijua
tukimpunguzia dawa, usingizi utaisha, lakini upunguze shuguli. Kuwa na kiasi
ili usije pandisha hiyo pressure zaidi.” “Sawa.” “Basi hiyo dripu ikiisha,
nitamwambia nesi aje akutoe hapo kitandani. Utoke ukatembee.” Lubuva akatoka.
Nesi alikuja kumtoa kila kitu, akahamia kwenye wheelchair, Geb akawa ndiye
anamsukuma. Wakatoka pale chumbani kwenda nje kutembea kidogo.
Kwa ajili ya kutembea
kwa muda mrefu walipofika nje, huku Geb akimfuata nyuma bila wheelchair na
kushinda siku nzima na wanae hapo hospitalini, Nanaa alipojiweka tu kitandani,
akapotelea usingizini. Geb alikesha usiku huo akiomba. Alimlilia Mungu juu ya
Nanaa, bila kuchoka. Alitubu kwa kumtelekeza Nanaa na kumfikisha hapo alipo.
Geb aliomba usiku kucha.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Usubuhi na mapema
James akawa mtu wa kwanza kufika hapo. “Na mimi ndio nimekutana naye hapa
hospitalini kaka. Sikuwa hata nikimfahamu. Lakini
alikuwa akinifuatilia mimi bila kujua nia yake. Ni juzi ndipo nilikumbuka sura
yake na kumbana mpaka akaniambia. Unajua nisingeweza kukuficha kaka yangu.”
Nanaa alijikuta akiongea mara baada ya kufungua macho na kumkuta kaka yake
amesimama hapo akimtizama. “Sikulaumu. Kwanza anaonekana ni mtu mzuri. Acha kulia
bwana.” “Umezungumza naye!?” Nanaa akauliza
kwa mshangao. “Alinitafuta jana usiku. Tukapata muda wa maongezi. Anaonekana ni
mtu mwenye nia nzuri na wewe. Tumpe nafasi tuone na yeye atafika wapi.” Nanaa
hakuamini. Akajifuta machozi.
“Kwa hiyo mmekubaliana
naye juu ya hayo matibabu ya huko Ujerumani?” Geb akauliza. “Nimemwambia ni
mpaka nikusikie na wewe ndipo tushauriane. Jana siku nzima nilikuwa nina kazi
ya kutafuta daktari atakayeweza kumsaidia Nanaa. Nilipiga simu Afrika ya kusini
na India. Kote wanaonekana wanaweza kumuhudumia kwa haraka endapo nikijiandaa
vizuri kifedha. Napo pia sio garama kubwa sana. Naona tumsikilize yeye, na mimi
niwaambie pale nilipofika, ndipo tufanye maamuzi.” Geb alimjua James. Huwa
hawezi kutulia linapofika swala la Nanaa.
Lubuva naye akaingia.
Baada ya kusalimiana na wote, akamsogelea Nanaa pale kitandani. “Ulilala
salama?” “Nimelala kama kachanga. Nimeamka nikala na kurudi kulala tena. Ndio nimeamka
tena sasa hivi.” “Afadhali. Nataka kukupima pressure.” Nanaa akatoa mkono.
“Lakini nimewakatalia mtindo wakuniogesha hapa kitandani na kunifanya
nijisaidie kitandani kama mtoto mdogo. Sitaki tena catheter.” Lubuva akacheka.
“Waliniambia umekataa
kurudishiwa catheter.” “Ila usifikiri mimi ni mkorofi. Naweza kujisaidia
mwenyewe, sitaki wanifanye kama nipo mahututi au mtoto mchanga!” Lubuva
akacheka tu na kumpima. Habari za ubishi wa Nanaa alishazisikia kabla hata
hajaanza kumuhudumia. Hakuwa akishangaa. Hata hivyo alijua ni ubishi wa
kurithi.
Wakamuona anarudia
tena na tena. Wote wakaingiwa na wasiwasi, wakasogea. “Vipi tena!?” Geb
akauliza. “Naona pressure yake imeshuka!” “Asante
Mungu wangu!” Walimsikia Geb akishukuru huku Lubuva akirudia tena.
“Mkono unauma.” Nanaa akalalamika. “Kwa nini umeamini kwa haraka majibu ya
pressure kuwa juu, sikukuona ukirudia kupima mara mbili mbili, lakini tumepata
majibu ya kuwa pressure ipo chini unashindwa kusadiki!? Acha kumuumiza mkono
kwa kurudia kumpima tena na tena. Kuwa na imani Lubuva.” “Lazima kuhakikisha
Geb. Kwa aina hii ya pressure, inamaana kuna dawa fulani inabidi nisimpe sasa
hivi.” “Basi usimpe. Endapo ikipanda tena, ndipo umpe tena.” “Naona nifanye
hivyo.” Wakamuona anacheka.
“Nini sasa?” Geb
akamuuliza. “Nilikuwa na wasiwasi sana. Sikutaka mwanzo wangu na Nanaa uwe
hospitalini.” “Ulitaka uwe wapi sasa?” Nanaa akauliza. “Kucheza na wajukuu
zangu na mambo mengine. Umenizeesha wakati mimi nilikuwa najiona kijana
kabisa!” Wakacheka. “Ni kweli umebadilisha mtazamo wangu kabisa Nanaa. Sikuwahi
kujiona na kuyatazama maisha kama sasa. Ndoa zangu zote zimekuwa na matatizo
sababu sikuwahi kutoa kipaumbele kwa familia au tuseme kwa mtu wa karibu yangu
kama hivi hapa. Nilikuwa nikijiwekea ratiba zangu, sitaki zivunjwe.
Nitazisimamia na kuhakikisha natimiza bila kukosea. Na mbaya zaidi kazi yangu
inanihitaji sana. Hakuna siku ninakuwa nipo tu, au niseme nakuwa sina kitu
chakufanya kuanzia asubuhi mpaka usiku. Kwa hiyo kama anavyosema Geb, Mungu
asadie utoke hapo. Hata mimi naungana na Geb, Oliva, Magesa na Jimmy
kukusubiria. Maisha yangu yote kwa sasa yamesimama, akili ipo hapa.” Ilimgusa
kila mtu, zaidi Nanaa.
“Mungu
atanisaidia nitapona tu, na tutapata tu huo muda. Naona na kaka amekukubali.”
“Nanaa! Huna siri wewe!?” Wakacheka. “Hapana kaka, nilimwambia siwezi kuwa naye
karibu kama wewe hutamkubali.” Wakacheka. “Ni kweli umejitoa dokta Lubuva.
Binafsi nakushukuru sana. Asante.” Geb akampa mkono. Wakacheka kama
waliokumbuka malumbano yao.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Kufumba na kufungua
kengele masikioni mwa James zinaanza kulia. Nanaa si mzigo wake peke yake tena.
Alishamkabidhi Geb, na sasa baba yake amerudi rasmi, amesimama na mwanae kwa
hali na mali. Mchana na usiku yupo pale. Maisha
yake yanatakiwa yaendelee au yaanze sasa!? Anajiuliza James. Wanaume hao
wawili walioongezeka sio tu kama wanampenda Nanaa, bali pesa ipo na wote
wanatamka kumuhitaji Nanaa. Kipi
kinamzuia James? Lubuva hakuwa amewapita sana. Ni miaka michache tu. Lakini
anao wajukuu kutoka kwa Nanaa, Geb anao watoto kutoka kwa huyo huyo Nanaa
ambaye ni kazi ya mikono yake yeye mwenyewe James. Ni wakati wa James kuanza au
kuendelea? Yapi yalikuwa malengo yake yaliyosimama sababu ya Nanaa? Nanaa ni
jukumu la nani sasa hivi? Ataweza kuwaamini na kuwaachia Nanaa waliyekutana
naye ukubwani? Wakamuona anavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu.
Akaweka tabasamu usoni.
Malii!
“Unacheka nini kaka?” “Nimekuletea
habari njema. Nilikuwa nikisubiri wakati muafaka kukwambia.” “Nini!?” Nanaa
akauliza tena. “Jana jioni, Malii ameingizwa nchini kutokea nchini Uingereza.
Alikimbilia kwa binamu yake huko, akajificha. Wamemsaka mpaka wakamkamata.”
“Kaka!” “Alinipigia simu yule mwanasheria wako, Mazigo, akaniambia kama
nitataka niende nikamuone anavyoingizwa nchini.” “Ulikwenda?” Nanaa akauliza.
“Kwa haraka sana. Yaani wote walinikuta nimeshafika pale uwanja wa ndege, na
nilihakikisha Malii ananiona na ninampa ujumbe wake. Ametolewa uwanja wa ndege
na pingu mkononi. Mazigo hakudanganya.” Nanaa akafurahi sana.
“Hongera kwa
kujipigania Nanaa.” “Asante kaka. Nimefurahi mno. Nikitoka hapa nitamtafuta
dada Mazigo.” “Nilishamwambia bado upo hospitalini, akuache kwanza. Akasema
haina haraka, hata hivyo hukumu yake hawezi kutoka jela.” Hilo nalo likawa
jambo jema zaidi.
~~~~~~~~~~~~~~~
Pressure ya Nanaa
ikaendelea kujitengeneza kitu kilichowashangaza madaktari wote. Geb alimuomba
Mungu akisema afanye kitu si kwa ajili yake tu, bali hata kwa hao madaktari
bingwa, wauone mkono wa Mungu kwa waziwazi ili wajue kuwa yupo Mungu awezaye
kutenda kwa ajabu.
Baada ya siku mbili
mbeleni, wazazi wa baba yake Lubuva na ndugu zake wengine walikuja kumtembelea
Nanaa pale hospitalini. Kweli Nanaa alikuwa akifanana na upande wa baba yake. Nanaa
alifurahi sana. Alishindwa hata kuweka kinyongo kwa kumkataa kwa mara ya pili
tena, alipopelekwa kwao wakati ni mchanga, baada ya kifo cha mama yake.
Walijawa toba na kila
wakati walieleza majuto yao. Babu yake ndio akaongea kama alivyosema Nanaa.
Anatamani asingemkataa Wini moja kwa moja ila kuomba mtoto apimwe baada ya
kuzaliwa. “Ni ubinafsi tu ndio uliniingia kupitia hofu ya vitisho vya dada yake
Wini. Ambapo pia najiambia, ningeweza kuzungumza naye ili kumtuliza tu.
Nilikosa Nanaa mjukuu wangu. Nisamehe mama.” “Hapa
nimefurahi mpaka nimesamehe dhambi zenu wote.” Wakaendelea kucheka na
kuzidi kufahamiana.
~~~~~~~~~~~~~~~
Baada ya siku 3 tena
mbeleni, Nanaa alionyesha kupona kabisa. Yeye mwenyewe ndio alikuwa akihangaika
na Jimmy pale wodini na wanae wengine hasa Magesa, Lubuva akaona amtoe. “Naona
muondoke tu. Mmepageuza hapa kama shule ya chechea!” Nanaa akacheka sana.
Alimkuta Mama G na watoto wote humo ndani mpaka Fili. Alikuta chumba hicho
kimechangamka, Nanaa anakimbizana na Magesa akimzuia asiangushe mashine ambazo
zilishazimwa muda mrefu, kwa kuwa Nanaa hakuwa akizihitaji tena. Amembeba Jimmy
mkononi huku anakimbizana na Magesa mle ndani. Geb alikuwa amekwenda kazini
akamuacha Nanaa wakati mama yake anaingia na watoto.
Alitoka hospitalini na
kurudi nyumbani akiwa na familia ya upande wa baba yake. Walimtafutia wasichana
wa kazi wawili waliokuwa msaada kwa
Nanaa. Upande wa swala la watoto mmoja wao akajitenga akiomba yeye aachiwe
watoto tu, akisema anapenda sana watoto. Hiyo ikawa nafuu kwa wote kwani mama G
na Fili walikuja kuhamia Arusha kuwa na Grace. Bibi yake Nanaa naye akawa bega
kwa bega kwa Nanaa mpaka Nanaa akahisi ni dhamira ilikuwa ikimsumbua kwa
kumkataa na kumficha kwa baba yake. Alikuwa akijitoa kupita kiasi.
Grace
& Man!
Grace na Man walirudi
kwenye fungate kwa muda wa siku 5, ndipo waliporudi kumchukua Fili na mama G,
wakahamia Arusha. Mungu alimbariki Grace, akazaa mapacha wengine. Safari hii
alizaa mtoto wa kike na wa kiume. Wakike ndiye aliyekuwa mdogo, tofauti na yeye
na Geb. Walifanana na Man, kasoro tu macho ndio ungejua ni watoto wa
Grace.
Alifanikiwa
kutengeneza ramani inayofanana kabisa na nyumba aliyojenga na Danny jijini Dar,
lakini hii ilikuwa na mwanaume waliyependana na kuheshimiana, Man, huko jijini
Arusha. Maisha yao yalijawa utulivu, kwani Grace naye aliingia kazini na
kumpokea majukumu mumewe. Na huko nako akawa msaada mkubwa kwa Man kama kwenye
kampuni ya kaka yake. Mama G alikuwa na kazi ya kulea vijukuu.
Hakumtafuta tena Danny. Danny akajua hiyo ndio
adhabu pekee anayopokea kutoka kwa Grace. Kumpokonya mtoto aliyekuwa amebaki,
Fili.
Danny!
Hata hivyo na yeye
Danny alijiona hawezi kuwa karibu tena na Fili. Kumbukumbu ya kumpiga kikatili
wakati akimkumbusha kufunga watoto mkanda ilikuwa ikijirudia akilini na kwenye
mitandao. Danny alichafuliwa na ushuhuda wa mtoto wake mwenyewe, akisimulia
hatua kwa hatua kilichokuwa kikiendelea ndani ya gari mpaka mauti ya wadogo
zake.
James ndiye
aliyemuhudumia kuanzia yupo hospitalini, mpaka akatolewa akiwa anatumia
magongo. Aliishi nyumbani kwa James mpaka alipopona kabisa ndipo akatafuta
kwake. Alianza maisha akiwa hana mke, wala watoto kama kijana mdogo ambaye ndio
amemaliza chuo, wakati umri ulishakuwa umekwenda. Hawakuwa na tofauti na James
tena.
Sara hakumtafuta tena
na yeye hakutaka kumtafuta tena Sara. Sara alimuachia madonda ambayo hayakuwa
yakitibika au kusahaulika kamwe. Alimlaumu kwa mengi, zaidi kusababisha kifo
cha wanae. Na Sara naye aliogopa hata kukutana na rafiki za Danny au Grace,
akijua atakuwa akitafutwa na vyombo vya usalama ili kujibu shutuma zilizokuwa
zimeenea mitandaoni.Kusababisha ajali akiwa anapigana na Danny.
Mwisho Wa Ubaya.
Ni kweli Malii
alikamatwa na kurudishwa nchini akiwa na pingu kama alivyoahidi dada Mazigo,
mwanasheria. Alikaa muda mrefu sana jela kabla ya hukumu yake ya kifungo cha
maisha kutajwa. Kwa ufupi maisha yake ndio yaliishia huko. Gozi naye alipewa
miaka 35, ambayo ukichanganya na umri wake, angetoka akiwa mzee wakutosha tu.
Maisha yasingekuwa na ladha tena. Ni kama naye alipewa kifungo cha maisha.
Safari hii uchawi wa
Zinda haukumsaidia. Mwanasheria wa kina Magesa alisuka kesi yao vizuri sana. Na
kwa kuwa walishasomewa madhara yatokanayo na kuvunja masharti yale, Zinda naye
alipata miaka 6 jela. Hapo ndipo wote wakaelewa ile ‘restraining order’ ya kina Magesa haikuwa ikiongopa na Geb
anamaanisha, hataki undugu tena na wao.
Mama James!
Maisha yake yaliendelea
jijini Dar kama kawaida. Bar yake ilishamiri na kuweza kumuingizia pesa ya kutosha. Alimuhakikishia James na baba
yake anaweza kujitegemea na wala hakukosea kumuacha mumewe. Hakurudi tena kwa
mumewe, akaendelea kuishi na binti zake jijini Dar, huku pesa ikiendelea
kuingia bila shida. Zawadi ya kumpokea Wini akiwa amefukuzwa na kila mtu japo
kwa manyanyaso ilikuwa nyumba ambayo aliendelea kuishi na binti zake. Napo pia
akawekeza hapo. Akatengeneza fremu za maduka mbele ya nyumba hiyo, maisha yake
yakawa yakusaka pesa tu.
Mahusiano yake na
James hayakuwahi kupona. Bado James alimlaumu kumkimbia baba yake, tena
akikumbatia dada zake bila kuwashauri vizuri. James ndiye aliyebaki na
mahusiano na baba yake. Akimtunza na kumtembelea.
Nanaa & Geb
Maisha ya Nanaa na
Geb, yalijawa baraka na amani. Kale kaukoo kadogo kalipanuka kakaongezwa nguvu
na ukoo wa Warangi. Kina Lubuva. Walijaa kwenye maisha yao na wao wakilea
wajukuu kwa bidiii zote. Nanaa alisaidia kurejesha ndoa ya baba yake huku
akisaidiwa na Geb aliyekuwa karibu na ukajengeka urafiki na Lubuva. Wawili hao
walijikuta wana mengi yakufanana na kuzungumza. Vijana waliofanikiwa kwenye
fani zao. Pesa ipo na kiunganishi alikuwa Nanaa anayewahusu wote kwa karibu.
Geb alimuweka sawa
Lubuva na kusisitiza umuhimu wa baada ya mahangaiko yoote ya siku nzima, lazima
kuwe na sehemu anayorudi na kuitambua kama nyumbani na mtu wa
kumkimbilia bila kificho, mke. Lubuva akajirudi kwa mkewe na
kutengeneza.
Nanaa
na Geb walisaidiana kufanya kazi kwa bidii. Ni kweli Nanaa alichukua
nafasi ya Grace kikamilifu na kuwa msaada mkubwa kwa Geb. Baada ya Jimmy
kufikisha miaka 3, Magesa 4 na dada yao Oliva miaka 6, ndipo Nanaa alipoanza
kwenda kazini rasmi. Kabla ya hapo kazi nyingi alifanyia nyumbani akilea watoto
na siku chache ndipo alipokuwa akienda kazini.
Utaratibu
wa kwenda kanisani kwenye familia hiyo ya Magesa, ukamuambukiza Lubuva. Na yeye
akaanza kuongozana nao kwenda kanisani. Kitendo cha Nanaa kupona bila upasuaji,
ukawa muujiza wakumtosha na kumuaminisha Lubuva juu ya uwepo na nguvu za
Mungu. Baadaye Geb aligundua kipo kipawa cha uponyaji ndani yake.
Japokuwa hakuwa akishinda kanisani, au kufungua kanisa, lakini Mungu alimtumia
kwenye mazingira yake. Akabaki akimcha Mungu.
***************MWISHO************
Naomi Simulizi.
(20+) Naomi Simulizi. | Dallas TX | Facebook
Mungu aendelee kukuza kipaji chako dada yangu..
ReplyDelete