Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 68 - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 68

Nanaa alikuwa amelala bila hata taarifa.  Watoto waliletwa mida ya saa 4 asubuhi, hakujigeuza hata mara moja tokea alale pale alipoachwa na dokta Lubuva. “Namtaka mama.” Baada ya muda mrefu Liv akalalamika. Geb akarudi tena kumuamsha taratibu. “Nanaa! Liv huyu hapa.” Nanaa akafungua macho, akamtizama na kurudi kulala bila kumsemesha kitu. Geb akaingiwa wasiwasi. Alirudi kulala tena mpaka mchana, akaamka     mwenyewe.

Liv alikuwa amepooza kwenye kiti, na ndio walikuwa wanakaribia kuondoka. “Liv!” Aliita taratibu. “Mama!” Liv akasimama kwa haraka. “Beba mama!” “Naomba umuweke hapa kifuani.” “Unauhakika Nanaa!? Unaonekana umechoka!” “Muweke tu nijisikie vizuri.” Geb akamnyanyua na kumuweka juu ya mama yake. “Nampenda mama.”Liv akambusu. Wakamuona machozi yanamtoka.

“Nakupenda Liv. Nakupenda sana mwanangu na ninahamu na wewe!” Nanaa alijibu kama anayesinzia. Liv akajilaza kwa mama yake. Hata mama G, Grace na kaka yake hakuwasalimia. Ni kama hakuwaona.

Walishazoea Nanaa akilazwa ndio mtoa stori. Watacheka wakati wote. Lakini Nanaa wa safari hii hakuwa hata akiongea. Kidogo wakaingiwa na wasiwasi. Alikuja kuamka tena usiku. “Vipi?” Geb akasimama na kumbusu kichwani. “Najisikia vizuri.

Ninahamu na wewe Geb!” “Hata mimi. Pona bwana tutoke hapa.” “Endelea kuniombea. Najisikia mwili mzito” “Nakuombea sana.” Nanaa akatulia kama anawaza. “Vipi?” “Liv alikuja leo?” “Tulishinda nao wote hapa.” “Na kaka zake!?” Nanaa akauliza. “Wote walikuwa hapa. Mama, James, Grace, Liv, Magesa na Jimmy. Tulipewa Jimmy karibia siku nzima. Magesa pia amembeba.” Nanaa akacheka. “Atamuangusha!” “Ungemuona usingekubali. Alimbeba kwa nguvu zote. Amembusu weee, mpaka tukamchukua.” “Atakuwa amempaka mwenzie mate!” “Kila mahali.” Nanaa akacheka. 

“Na Liv wangu!” Nanaa akauliza tena. “Si unajua alivyotulia. Nimemchukua video wakati anambembeleza Jimmy. Alikaa pale kwenye kochi. Akataka tumuwekee. Alikuwa anambembeleza bila hata ya Jimmy kulia. Magesa ndio aliwavuruga. Alikuwa anamtaka Jimmy kila wakati.” “Jamani Magesa!” “Halafu sasa yeye hawezi kutulia. Anataka akipewa, ashuke naye chini.” Wakazidi kucheka. “Naamini kesho nitakuwa sawa niwaone. Nimepitwa.” “Nimekuchukulia video, uone fujo za kaka mkubwa.” Wakati wanazungumza, dokta Lubuva akaingia.

Dokta Lubuva.

Lubuva akamsogelea Nanaa pale kitandani. “Unajisikiaje?” “Una duka la madawa karibu na maeneo ya Tabata Barakuda?” Nanaa akamuuliza bila yakujibu swali. Geb akabaki kimya akisikiliza. “Hapana.” Lubuva akajibu kwa kifupi. Lakini Nanaa akabaki akimtizama kama ambaye hajaridhika. “Unaishi maeneo ya huko?” Nanaa akauliza tena. Kimya. Lubuva hakujibu, akabaki akimtizama. “Unajisikiaje?” Lubuva akauliza tena huku akiendelea kumpima. “Kuna siku nilikwenda duka la madawa, kuulizia dawa ya kuzuia maziwa yasitoke. Niliyemkuta akiuza akaniambia hamna dawa. Nakukumbuka kabisa, ulikuwa umesimama pembeni ya lile duka ukiwa kama unatumia simu yako, ukaongeza kuwa naweza kupata homa, ninywe dawa ya kupunguza maumivu na kushusha homa kila baada ya masaa 6. Kisha ukasema kuna dawa ya asili, niweke maganda ya kabichi mabichi, yaliyowekwa kwenye friji. Kisha ukaendelea na kitu ulichokuwa ukifanya kwenye simu yako.” Nanaa akaendelea taratibu.

“Nakumbuka siku nyingine kama baada ya siku tatu tokea unipe ule ushauri, nilikuwa nimezidiwa na pressure. Nakwenda hospitalini. Nilikuwa nimekaa kituo cha daladala. Pale pale Tabata Barakuda. Ukaja ukakaa pembeni yangu. Nakumbuka nilikuwa nimejiinamia tu. Daladala ilipokuja, ukanistua, na kunisaidia kupanda kwenye daladala. Nilikuwa natetemeka sana nusura kuanguka. Tena nakumbuka ulisisitiza nipande taksii, nikakukatalia. Najua unakumbuka. Na haupo hapa kwa bahati mbaya. Wewe ni daktari wa upasuaji. Tena nimesikia wakikusema ni bingwa. Kwa muonekano tu, hufananii kuwa ni mtu unayepanda daladala. Lazima una gari. Hiyo ni moja. Pili, kwa hadhi yako wewe, huwezi kuwa unasimama kwenye maduka ya madawa, tena Tabata, ukiwa unacheza na simu mchana, siku ya kazi au kuwa unalala hapa na mimi na kunitembelea kila wakati. Lazima unanifuatilia mimi.” Hapo Geb akakaa sawa.

“Nimejaribu kukufikiria sana. Na kwa muonekano wako sasa hivi, baada ya kukwambia haya yote, inamaana nimepatia. Sijakosea. Sasa kwa nini unanifuatilia?” Nanaa akamuuliza taratibu huku akimtizama kwa makini. Kimya. “Wewe ni nani na kwa nini unanifuatilia mimi? Unataka nini kwangu au kwa familia yangu?” “Ukipata nafuu kabisa, tutapata muda wakuzungumza.” Lubuva akajibu. “Basi utajulishwa nitakapopona ili uje kuzungumza na mimi. Lakini hapa sitaki kukuona tena na wala usiniguse.” “Sina nia yakukudhuru Nanaa. Mimi ndiye niliyekufanyia upasuaji. Nimekuwa…” “Ukilala na mimi tokea nitolewe chumba cha upasuaji?” Nanaa akamuuliza. Lubuva kimya. “Najua.” Nanaa akaongeza. “Geb, mpigie simu dokta Lyamu mwambie aje au anitafutie daktari mwingine. Naomba wewe uondoke.” “Nanaa!” Lubuva akamwita akiwa ameishiwa nguvu.

“Hakika sikutanii. Hutanigusa tena mpaka nikujue wewe ni nani.” “Huwezi kupata daktari mzuri atakayeweza kukusaidia kama mimi.” “Ndivyo unavyojidanganya!?” Nanaa akamuuliza. “Ungejua nusu tu ya historia yangu ya maisha, ungeelewa wala si kwa nguvu zako ndio maana nipo hapa. Wewe si mungu mtu kama wanavyokuita. Hata usingekuwepo hapa leo, na Mungu angekusudia nipone, angetumia hata nesi kuniponya. Nishapitishwa kwenye maradhi ambayo hayakuwa na matibabu. Madaktari walishindwa jinsi yakunitibu. Hivi unajua Mungu mwenyewe alituma malaika wake kuja kunitibu? Mikono hiyo ya Geb ambayo haijui hata kushika sindano, Mungu aliitumia kuniponya! Toka hapo mlangoni, halafu rudi hapa baada ya kesho kutwa kama utanikuta hapa kitandani. Nenda.” “Nipe siku ya leo, halafu kesho tuzungumze vizuri.” “Kwa nini?” Nanaa akamuuliza. 

“Unahitaji kupumzika.” “Hivi unajua kama nimelala hapa siku nzima? Hata wanangu walipoletwa nilishindwa kukaa nao.” “Nafahamu Nanaa. Hakuna kinachoendelea hapa kwako, mimi nisijue.” Nanaa akakunja uso. “Wewe ni nani!?” Nanaa akazidi kuchanganyikiwa.

“Habari  kamili za Wini nilikuja kuzipata hata miaka minne haijaisha. Sikuw.. .” Nanaa akawa ameelewa kila kitu. Akajiweka sawa. “Subiri kwanza. Naomba kukuuliza swali kabla hujaendelea sana. Samahani lakini, nakukatiza kwenye maelezo yako. Najua unayo stori nzuri sana ambayo umeiandaa, ungependa kuisema au ulitaka niisikie. Lakini kuna kitu kilikuwa kikinisumbua tokea nakuwa, au tokea napata fahamu zangu, vile mama mkubwa alivyokuwa akiniambia kila wakati kuwa mimi ni mzigo ambao hajui atautua lini. Nikawa najiuliza, ilikuwaje mpaka mimba yangu ikashikwa? Nilipata majibu nusu nusu kutoka kwa mama mkubwa lakini hayakuwa yakinitosheleza kwa kuwa alikuwa akiongea kwa jazba akiwa ananitukana au akinilalamikia. Yaliniacha na shauku yakutaka kujua zaidi. Aliniambia ulinikataa mimi na mama. Sasa nikawa najiuliza, ni mazingira gani au ya namna gani mimba yangu ilishikwa?” Nanaa akauliza.

          “Labda nikupe mfano. Na mimi nilifanya kama alivyofanya mama. Nilishika mimba zote nje ya ndoa. Lakini tokea mtoto wa kwanza niliyemzaa, baba yake alipojua tu, alikuwa akimng’ang’ania yule mtoto. Na usifikiri ni kwa huyo mtoto wa kwanza tu, mpaka wa pili. Na usifikiri ni Geb mwenyewe, na mama yake hivyo hivyo. Wanang’ang’ania wanangu kuliko nitakavyokueleza. Watoto wangu ni kama alumasi kwao. Nilipokosana nao au nilipowakosea, walinipokonya watoto wangu. Kwa upande wangu mimi walinitenda ubaya sana, lakini kwa upande wa watoto wangu, ni kwa ile thamani waliyoona kwa wale watoto. Yule mama alikuwa halali mchana wala usiku akilea watoto wangu mimi niliyewaudhi. Peke yake bila msaada wangu wala Geb mwenyewe. Yule mama alikuwa akihangaika na watoto niliowazaa mimi! Tena akiwa mgonjwa. Sijui kama unanielewa? Mimi nilikuwa mbaya sana kwao, lakini sio wale watoto. Yaani mimi hata nikifa leo, sina hofu ya watoto wangu, najua upendo unao wazunguka. Watoto wangu wanavalishwa vitu vya thamani kutoka kwa bibi yao na shangazi yao. Sikumbuki mimi kutoa pesa yangu na kumnunulia Liv hata hereni.”

“Nguo na viatu anavyoleta shangazi yao, huwa natamani angekuwa akinipa mimi hizo pesa. Ni garama, na yule mtoto ni msafi kuanzia kichwa mpaka mguu. Kazi ya bibi yake na shangazi yake. Hata nikiwepo mimi nyumbani, bibi yake huwa anamuhudumia. Na yeye anajua Liv. Kuna vitu anajua hivi ni bibi ndio ananifanyia wala si mtu mwingine. Ule ukaribu na mahusiano aliyonayo bibi yao na wale watoto, au shangazi yao, ni ajabu sana. Na hawana unafiki wala kusema wanajitahidi kumfurahisha hata Geb. Wanafanya kutoka moyoni. Kwamba wale ni watoto wao. Sasa hicho kitu nacho kikazidi kunishangaza na kuzidi kuibua maswali. Nikawa najiuliza, hivi  ilikuwaje mpaka mimba yangu ikashikwa? Au na mimi ni mmoja wa wale watoto wanaoitwa ni wa bahati mbaya!? Yaani mwanamke anashika mimba inakuwa kama amebeba mkosi! Linakuwa kama tatizo la kuhatarisha maisha ya mtu, hasa mwanaume aliyempa mimba! Yaani kuna kuwa na mipango ya muhimu sana mbeleni, halafu katikati ya starehe, mimba inatungwa, na inakuwa ni jambo baya sana la kuharibu maisha au mipango ya watu!” Nanaa alibonyeza kitanda chake ili akae vizuri.

“Naomba utulie Nanaa. Bado hicho kichwa hakijapona vizuri.” Dokta Lubuva alijaribu kumtuliza. “Halafu kweli tumefanana! Yaani sasa hivi nikikuangalia ndio naiona sura yangu hapo kwako.” “Unatakiwa kuchukulia mwili wako taratibu. Upasuaji uliofanyiwa ni mkubwa sana.” “Lakini binafsi nimefurahi kukuona. Muulize Geb. Nilikuwa nataka kukutafuta ili nikuone tu sura yako. Ungeniambia tu mapema, kuliko kunifuatilia nyuma kimya kimya.” Kimya.

          “Halafu wewe ni rafiki na dokta Rweta? Yule daktari wa mambo ya moyo au na pale ulikwenda siku ile kwenye kliniki yake ili unione tena?” Nanaa akamuuliza. “Yaani sasa hivi ndio nakukumbuka vizuri sana. Kuna siku tulikwenda kwake, na wewe ulikuwepo ofisini kwa dokta Rweta. Nilikuwa na mama. Hukuzungumza neno hata moja. Ulikuwa kimya kabisa kama unayesoma kijalida fulani hivi. Ila alikutambulisha kama daktari mwenzake, tusiwe na wasiwasi na uwepo wako pale. Tukazungumza naye, akanipa ushauri baada ya maswali mengiii. Mpaka nikamstukia na yale maswali! Nikamuuliza mbona ananiuliza maswali kana kwamba ndio ananiona kwa mara ya kwanza wakati mimi ni gonjwa wake wa kila siku? Unakumbuka?” Nanaa akamuuliza Lubuva.

          “Sisi tukaondoka na kukuacha pale pale ofisini.” “Rweta ni rafiki yangu. Nilijua kuwa yeye ndiye anayekutibu pia. Nikataka kujua historia yako kutoka kwako wewe mwenyewe. Vile unavyojisikia baada ya kubadilishiwa dawa. Kama zinaendana  na hali uliyokuwa nayo kwa wakati ule au la. Ndio maana nilimpa yale maswali akuulize, ili  nikusikie wewe mwenyewe kwa wakati ule. Ili niweze kutafuta ushauri zaidi kwa marafiki zangu niliokuwa nikifanya nao kazi zamani.” Dokta Lubuva akajibu. 

“Sasa kwa nini hukutaka kuniuliza wewe mwenyewe?” Nanaa akauliza. “Ulikataa Nanaa. Dokta Lyamu alipokwambia kuna daktari mwingine mzuri anaweza kukuona, unakumbuka ulikataa ukasema hutaki kubadilisha madaktari? Tena Lyamu alikuja kunijibu kuwa ulimwambia amwambie Rweta aje ajifunze kwa huyo daktari mwingine mzuri, alafu yeye Rweta ndio akutibu wewe. Wewe hutaki kubadilishiwa madaktari.” Hapo Nanaa akakumbuka na kunyamaza.

“Sasa kwa nini hukujitambulisha muda wote huo? Au ulikuwa ukinichunguza kwanza ili kujua kama nina shida kiasi gani? Kama nastahili kuwekwa karibu kwenye ufalme wako au la! Nisije kukufilisi!?” “Hapana. Hata kidogo. Nili…” Akasita. “Nakusikiliza.” Lubuva kimya. “Kama huna kitu cha kuniambia, mimi naomba niulize swali jingine, japo nimejua unachagua kipi chakujibu na kipi uache. Umeoa?” “Ndiyo. Na nina watoto wawili. Au una wadogo zako wawili wakike na wakiume.” Nanaa akacheka taratibu huku akimtizama kwa makini.

“Sasa mimi leo nimelala siku nzima. Naomba ukae hapo uanze kunisimulia stori zako zoote na mimi nikuulize maswali juu ya mama yangu. Maana sikuwahi kupata mtu anayemfahamu mama yangu vizuri na akawa tayari kunieleza juu yake. Si unajua alikufa wakati anajifungua?” Nanaa akamuuliza.

“Nafahamu.” “Ni kweli unafahamu kwa kuwa nililetwa kwenu mkanikataa.” “Nilikuwa nimeshaondoka.” Nanaa akacheka. “Naomba basi ukae ili unipe stori ya upande wako. Inayohuzunisha na kukuonyesha hukukosa. Wini ndiye aliyekosea. Alishika mimba kizembe. Alikuletea taarifa ukiwa na malengo ambayo hayakuweza kusubiri. Ulishakuwa na VISA tayari ya kwenda kusomea udaktari. Ulishitukizwa! Mlikuwa watoto sana, mimba ikaingia kwa bahati mbaya! Wini alikuwa na wanaume wengi! Au stori yako wewe haiendani na moja ya  hizo hapo?” Geb kimya.

“Basi kama zinaendana na hizo, huna haja yakurudia. Naomba unisaidie kumfahamu mama yangu. Ninakuwa nikimfikiria sana na wakati mwingine nakuwa nikimuhurumia. Angalau wewe uliweza kunikana na kunikimbia, lakini yeye alionekana kushindwa kunikimbia. Si unajua angeweza hata kutoa mimba? Angalau kuficha aibu na yeye akajiweka huru kama wewe. Sasa huwa namfikiria sana. Kwa umri ule, akiwa na shida, hana pakwenda, lakini alihangaika na mimi mpaka mauti. Natamani kusikia upande wake mwingine mbali ya habari nilizozisikia kutoka kwa watu waliokuwa na hasira naye.” Kimya.

“Usiniambie kama hata humkumbuki!!” Nanaa akashituka sana. Akakunja uso. “Nakumbuka.” “Sasa mbona hunijibu, umebaki tu kimya!? Unazo picha zake?” Kimya. “Kwani nyinyi mlikuwa mkikutana wapi huko ambako mlikuwa hampigi hata picha!? Au hapakuwa na mahusiano, ulipita tu ndio akashika mimba?” Kimya. Hasira zikampanda Nanaa, na Geb akajua. Akamsogelea karibu. Maana alimpisha dokta Lubuva azungumze naye, pale alipoingia.

“Labda niulize hivi, wewe ulikuwa ndio mwanaume wake wa kwanza au ni kweli vile ulivyosema wakati unamkataa kuwa alikuwa na wanaume wengine? Namaanisha sio wewe uliyemtoa bikra yake, kwamba ulimkuta..…” “Nanaa! Hapo unavuka mipaka. Naomba upumzike utaendelea wakati mwingine.” “Nataka kujua Geb. Mama alikufa akiwa mtoto mdogo sana. Na yeye alimkataa akisema asipewe mzigo ambao sio wake. Mzigo huo ndio mimi. Akidai  hakuwa peke yake kwa mama. Ndio nataka kujua kama ni kweli au la! Hanijibu kitu, anakuwa kimya. Sasa kwa nini alinikataa na kwa nini amerudi nakunifuatilia kila mahali! Kwa nini yupo hapa?” Geb akamvuta mkono na kuushika.

          “Leo umeletewa watoto wote hapa, umeshindwa hata kuwatizama au hata kujua kama walikuwa hapa. Jimmy ameshinda hapa, umeshindwa kunyonyesha kabisa. Mimi nakufahamu linapofika swala la watoto wako, Nanaa. Kushindwa kuwa na watoto leo siku tuliyoambiwa wanaweza kuletwa, ni kwa kuwa ni kweli hujisikii vizuri. Sasa hivi haupo kwenye nafasi ya kupokea ukweli wowote wa nyuma. Tena uliokuumiza. Nataka turudi nyumbani ukiwa umepona. Kwa kesi hiyo unayotaka kuianzisha hapo, ni njia nzuri sana yakukupandisha pressure, na hapa hatutatoka leo wala kesho. Tutaendelea kutesa watoto. Wote tunakusubiri wewe. Mimi, Liv, Magesa na Jimmy. Wote sisi maisha yetu yamesimama tunakusubiri wewe. Kwa hiyo nakuomba sana Nanaa, kipaumbele iwe ni kupona na kutoka hapo. Mengine yatafuata. Maadamu umeshajua ni wapi pakupata majibu ya maswali yaliyokuwa yakikukera sana, naomba uendelee kusubiri.” Wakamuona anabonyeza kitanda. Kikaanza kushuka upande wa kichwa taratibu. Geb akamfunika, na kumbusu kichwani. “Asante.” Geb akamshukuru.

 “Nasikia usingizi. Nataka kulala.” “Unaweza kujaribu kula tena kidogo?” Nanaa akafikiria kidogo. “Naona nilale kidogo, nimeshajitibua. Nina hasira sana. Nimekasirika Geb. Naona nilale tu, ili pressure isipande zaidi.” “Pole. Ukitoka hapa utapata muda wakutosha wakuuliza maswali yote. Lakini kwa sasa naomba lengo liwe ni kupona na kutoka hapa. Sawa?” Nanaa akanyamaza.  Akamuona anavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu akafunga macho. Geb akaanza kumpangusa machozi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Ni kwa nini analala hivyo!?” Geb akamgeukia Lubuva aliyeshindwa kujibu maswali ya Nanaa. “Madawa anayopewa yanachangia kumfanya alale.” “Madawa ya nini tena!?” “Nanaa ni mgonjwa Geb. Kufanyiwa upasuaji wa kichwa sio kwamba ndio amepona. Kumbuka bado moyo wake ni mkubwa. Hapo bado hajatibiwa hilo. Ametoka kujifungua, amepoteza damu nyingi tu, na bado mwili haujarudia hali yake. Kumbuka pia mimba yenyewe alibeba akiwa mgonjwa. Halafu kufunguliwa pia kichwa kwenyewe anahitajika muda wakutosha kupona kabisa. Lazima awepo kwenye dawa kutuliza maumivu, kufanya pressure iwe sawa na kurudisha huo mwili wake kwenye hali ya kawaida. Anahitaji muda.” Geb akamtizama Nanaa.

“Lakini baada ya hapa, unafikiri atapona kabisa?” “Nimekuona ukiomba sana Geb. Weka imani yako kwa Mungu. Hata hivyo alivyo sasahivi, ujue ni muujiza. Kesi nyingi kama za Nanaa, watu huishia kufa au hata wakiamka wanakuwa wamepoteza kumbukumbu kabisa. Lakini unamuona jinsi anavyopona kwa haraka? Hata jinsi anavyozungumza leo nitofauti na jana. Wengine inawalazimu kufanyiwa speech therapy ili kurudisha uwezo wao wakuzungumza tena. Kwa hiyo anahitaji muda na kuruhusu ahudumiwe na watu wenye uwezo wakutibu tatizo lake.” Geb akawa amemuelewa.

“Lakini sidhani kama wewe ni mtu sahihi kwa sasa wakuendelea kumtibu Nanaa.” “Nafahamu. Lakini nakuhakikishia Geb, utataka mimi ndio niwe karibu na Nanaa. Kila utakayemuuliza, atakwambia hivyo hivyo. Mpigie simu dokta Lyamu na Rweta, watakwambia mimi ni mtu sahihi ambaye unamuhitaji kwa Nanaa.” “Lakini ni kama kazi yako iliisha! Wewe si ni daktari wa upasuaji tu? Naomba nitafutie daktari unayefikiri ana uwezo wa kumtibu Nanaa, ila usiwe wewe. Utamfanya Nanaa achelewe kutoka hapo kitandani. Anazidi kupandisha hasira. Atataka kujua ukweli ambao najua kwa sasa hana uwezo wa kupokea ukweli wowote ule kutoka kwako, atazidi kujiumiza tu. Na mimi najua hataweza kuendelea kunyamaza. Ni mambo yaliyokuwa yakimuumiza sana. Ndio habari za kwanza kuniambia mimi siku ya kwanza kabisa napata nafasi ya kukaa chini na Nanaa na kuzungumza naye.” Geb akaendelea.

          “Nitakulipa pesa yako yote ya matibabu uliomfanyia Nanaa. Hata sasa hivi unaweza kuniletea bili nikulipe ili tu uondoke. Sitaki akiamka akukute wewe. Utazidi kumchanganya. Tafadhali nitafutie dakatri mwingine. Yeyote na kwa bei yeyote ile, ila sio wewe. Unaweza kuja kurudi wakati mwingine wowote, lakini sio sasa hivi akiwa mgonjwa.” “Geb, najua na wewe umesikia upande mmoja wa maisha ya Nanaa, na umenichukia sana na kuniona mimi ni mnyama. Lakini nakuhakikishia mimi ni mtu sahihi kumtibu Nanaa. Nipo hapa kama ‘neurosurgeon’ lakini nina timu ya madaktari bingwa wa Ujerumani, wapo nyuma yangu, wapo na mimi muda wote na wakati wowote nitakao wahitaji kwa ajili yakumtibu Nanaa. Nipo nao kwenye simu mchana na usiku wakinishauri jinsi yakumtibu. Kila tatizo alilonalo hapo Nanaa, nimetafuta daktari bingwa huko Ujerumani, ndio wana mtibu hapa.” Lubuva akajibu na kuendelea.

“Na naomba nikuhakikishie Geb, sina shida na pesa yako hata kidogo. Natengeneza pesa nzuri sana. Kwa kuwepo kwangu mimi hapa hata nusu saa tu, ujue napoteza si chini ya milioni ya kitanzania. Nalipwa kwa kazi ninazofanya kwenye mahospitali. Tokea siku Rweta ananipigia simu na kuniambia Nanaa yupo chumba cha upasuaji, amepoteza fahamu baada ya kujifungua, Lyamu akiwa hajui kama alikuwa na uchungu siku nzima. Maana nilimuomba Lyamu amfuatilie kwa karibu sana ili asishikwe na uchungu, maana aliniambia Nanaa mwenyewe amekataa kabisa kumtoa mtoto ili awekwe kwenye chupa akue. Wakanipigia simu siku ile usiku, nifike hapa kwa haraka, Nanaa ameletwa, amejifungua na kupoteza fahamu. Nilipokuwa nikiwalaumu, waliniambia ni kama Nanaa mwenyewe alificha swala la uchungu. Hata wewe alikuficha ukashitukia chupa imepasuka tu mkiwa nyumbani. Si ndio hivyo?” Geb akakubali.

“Sasa nakuhakikishia Geb, tokea siku ile mpaka leo nimesitisha safari zote za nje ya nchi. Huwa nasafiri nchi mbali mbali hasa hapa barani Africa, kwenda kufanya nilichomfanyia Nanaa, nakurudi hapa. Mimi mwenyewe najijua ni mzuri. Utaalamu ninaotumia mimi, bado haujafika hapa Africa. Nimeufanyia kazi huko nilikokuwa Ujerumani, kwa muda mrefu sana na kupewa awards’ nyingi tu. Kwa mweusi kupata award kwenye nchi kama Ujerumani, utakubaliana na mimi kuwa ninajua ninachokifanya. Na ndio maana wananiita mungu mtu. Sio mimi najiita hivyo. Ni kwa kuwa utaalamu ninaotumia kwenye upasuaji wangu kwa wagonjwa, ilikuwa inawalazimu kusafirisha wagonjwa wao nje ya nchi ili wakafanyiwe kile ninachowafanyia mimi kwa bei nafuu.”

“Nimekuja na vifaa vyangu na bado ninaingiza vifaa hapa nchini. Serikali imeniunga mkono, inakubali na ninachofanya. Hata Afrika ya kusini wananitumia sana. Ninayo kliniki na wagonjwa ninao wahudumia kama hapa. Kwa hiyo Geb, bado nasisitiza, mimi ni daktari sahihi kwa Nanaa na wala pesa sio sababu inayonifanya niwe hapa. Kwa mimi kuwepo hapa kwa Nanaa, ujue ninapoteza pesa nyingi sana zaidi ya utakavyoweza kunilipa wewe.” Lubuva akaweka msisitizo.

“Weka mbali tofauti zetu zote, mfanye Nanaa akubali mimi nimuhudumie. Dokta Lyamu alishanieleza zaidi juu ya Nanaa. Amenihakikishia wewe ukiwepo, Nanaa atakubali matibabu ya aina yeyote ile. Amefika hapo alipo, kwa kutopata matibabu sahihi tokea mwanzo. Nakuhakikishia Geb, hutaki kunikwepa. Kama kweli unamtaka Nanaa kwa kiasi nilichokuwa nikikuona ukipiga magoti pale nje ukiomba mchana na usiku, nakuhakikishia mimi ni majibu yako kutoka kwa Mungu wako. Usinifukuze. Sihitaji hata shilingi yako, ila kuwepo tu hapa.” Geb akavuta pumzi kwa nguvu na kumtizama tena Nanaa.

Lubuva Afunguka Kwa Geb.

Geb akamgeukia tena Lubuva aliyekuwa akiwatizama yeye na Nanaa.  Ulikuwa wapi muda wote huo? Kwa nini unajitokeza sasa hivi?” Geb akauliza kwa hasira na kulalamika kidogo. “Kwa nini hukutokea kabla ya haya yote ili kuwekana sawa na Nanaa?” “Najua unafahamu kwa kiasi watu waliomlea Nanaa.” Geb akanyamaza. “Kitendo tu chakujua mtoto aliyemwacha Wini anaitwa Nanaa, imenigarimu kupita nitakavyokwambia. Haya, kujua napo alipo pia imegarimu muda na pesa yakunifanya nijisikie nimelipa garama. Niliambiwa nilazima kulipia pesa ya matunzo yake, mpaka maziwa aliyomnyonya mama yake mkubwa pia niliambiwa nilipe ndipo niweze kujibiwa swali la kuwa yupo wapi mtoto mwenyewe, aliyeachwa na marehemu Wini.”

“Mbona na mimi nilishalipia hiyo na wakasema hawamdai tena Nanaa!?” Geb akashangaa sana. “Najua. Na waliniambiwa kama na wewe ulilipa, tena mliomba mpunguziwe.  Sasa akasema alikubali kupunguza kwako, kwa kuwa wewe huusiki na Nanaa. Sasa hiyo garama yangu mimi kama baba yake!” Lubuva alicheka kwa kusikitika.

“Nilipewa orodha hiyo. Kuanzia siku namkana Wini mpaka siku Nanaa anahamia nyumbani kwako wewe. Nilitakiwa kulipia kuanzia garama za usafiri aliotumia siku alipomleta Wini akiwa mjamzito nikamkana mbele yake. Alipomleta tena Nanaa akiwa kichanga pale nyumbani na kufukuzwa. Haya, fidia ya kutunzwa Wini mwenyewe akiwa mjamzito wa mtoto wangu, mazishi yake Wini, ndipo ikaja sasa garama za Nanaa mwenyewe. Matatizo aliyopitia huyo mama mwenyewe wakati anamlea Nanaa. Fidia za biashara zake zilizokufa wakati akimlea Nanaa. Pesa aliyopoteza James kwa Nanaa na si kwa mama yake na ndugu zake. Ada za shule, nguo, mpaka pesa ya chupi alizonunuliwa Nanaa, nililipishwa ili tu kujua Nanaa alipo.” Geb hakubisha katika hilo. Alimjua mama yake James.

“Tunapozungumza hivi sasa hapa, ndoa yangu ipo matatizoni sababu ya mama yake mkubwa Nanaa. Jumla ya hiyo pesa yote ilikuwa zaidi ya milioni 250. Akasema nimjengee nyumba hapa Dar.” “Haiwezekani! Kwa nini usimtafute mumewe!?” Geb akauliza. “Nakwambia nilianzia nyumbani kwao. Yule mzee hakuwa mnafiki. Alinieleza ukweli bila kinificha. Akaniambia hakumtaka kabisa Wini. Alimfukuza pale tokea siku ya kwanza amekwenda kuomba hifadhi. Lakini mkewe akamkubalia akae hapo mpaka atakapojifungua, ndipo aondoke. Akaniambi hajawahi kujihusisha naye Wini,  wala mtoto wake ambaye ndio Nanaa. Lakini yule baba aliona shida kutaja jina la Nanaa mdomoni kwake. Akaniambia hajawahi kujihusisha na hao watu wawili, Wini na mwanae, mpaka Mungu alipoamua kuwaondoa hapo nyumbani kwake. Mama mtu kwa kifo, mwanae hajui habari zake. Akasema mkewe alimkimbia yeye na binti zake wawili. Anasikia wapo wanaishi Dar, na wao ndio wanataarifa kamili za mtoto wa Wini.” 

“Hakukwambia kuwa mwanae James ndiye aliyehusika na maisha ya Nanaa?” Geb akauliza. “Aliniambia kwa hasira na kunitukana juu. Huku akinilaumu kuwa mimi nilikana huyo mtoto ili maisha yangu yaendelee vizuri. Matokeo yake nimeharibu maisha ya mtoto wake wa pekee wa wakiume, James. Yeye ndiye aliyebeba mzigo niliokuwa nimekimbia! Maisha yake yameharibika sababu ya mtoto wa Wini. Tena akanionya kwa vitisho vikali sana, nisiwahi kumtafuta tena James na nisithubutu kumwingiza kwenye maisha yangu mimi na mtoto wangu.”

“Akanieleza ugomvi mkubwa kati ya James na mama yake ni sababu ya mtoto tuliyemtelekeza sisi. Akanilalamikia kuwa tokea huyo mtoto ameletwa kwenye hiyo nyumba kutoka huko hospitalini alipokua ameachwa na Wini, imekuwa ni tatizo kubwa sana. Ni kama mkosi uliingia kwenye nyumba yao.” Lubuva akaendelea. “Alilalamika akisema  James alikuwa mtoto mzuri na mwenye malengo makubwa sana maishani. Lakini ni kama yote yalikufa na Wini. Akaishia kuhangaika na mtoto huyo tuliyemtelekeza. Amesahau malengo yake yote.”

“Alisema mbaya zaidi mtoto aliyenaye James sasa hivi, anayemuhesabu ni mtoto wake ni huyo wa Wini pekee. Hafikirii kuoa wala kuwa na watoto wake yeye mwenyewe. Alinifukuza pale nyumbani kwake vibaya sana, na akanionya nisiwahi kurudi tena pale. Nilimsihi angalau anipe namba ya simu ya mkewe. Tena kwa kumpigia magoti, hapo alishanitoa ndani kwake. Ndipo akanitajia namba ya simu ya mkewe, tena akiwa anafoka sana. Niliikariri na kuondoka pale.  Nikarudi hotelini na kuanza kumtafuta mama yake mkubwa.” 

“Kwani nyumbani kwenu nyinyi sio Moshi?” Geb akauliza tena. “Hapana. Kipindi nakutana na Wini tulikuwa tumehamishiwa Moshi. Baba alikuwa amehamishiwa hapo kuwa mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro. Tukakaa hapo kama miaka mitatu na miezi kadhaa, akapata uhamisho tena, tukaondoka hapo. Maisha yetu yalikuwa yakuhama hama. Kwa hiyo Moshi nilikaa kwa muda mfupi tu. Na nilipotoka Moshi, wala sikuhama na familia, niliacha ndio wanataka kuondoka hapo baada ya miezi michache, mimi nikaenda kusomea mambo ya udaktari. Nilijua ningesomea udaktari tu na kurudi, lakini nikapata bahati ya kulipiwa, nikaona niendelee kusoma tu. Nilikuwa mdogo, sina majukumu au kizuizi chakunifanya nisisome.  Nikaendelea na shule tu. Walipoona nina uwezo mkubwa, wakanishauri niingie kwenye mambo ya ubongo. Nikapata hospitali iliyokubali kunilipia ada, kwa masharti yakuwa niwe nafanya kazi chini yao kwa miaka isiyopungua 10.”

“Basi, pesa ikawa inaingia huku nasoma. Hata kuoa kwenyewe nimeoa miaka michache sana iliyopita. Sikuwa na muda wakuanzisha familia. Hivi ninavyokwambia hata hao watoto wawili nilio nao, ni wadogo sana. Nilijaribu kuoa kabla ya mke huyu wa sasa, nikashindwa. Tukaishia kupeana talaka. Sikuwa na muda wa kitu kingine ila kazi tu. Akili zangu zote zilikuwa kazini. Muda wa kufanya kazi kwenye hiyo hospitali ulipoisha na nilipoona uhitaji huku nyumbani unakuwa mkubwa, ndipo nikaamua kurudi nyumbani nikiwa sina hata wazo la Nanaa au tuseme Wini.” “Unamaanisha nini?” Lubuva akafikiria kidogo.

Kilichotokea Kati Ya Lubuva Na Wini!

“Sikutaka kumwambia Nanaa haya mambo kwa undani, ili isimuumize. Lakini acha nikusimulie wewe. Nitatafuta hekima nyingine yakuzungumza naye. Ilikuwa hivi. Nilimpenda Wini akiwa kweli binti mdogo. Hata mimi nilikuwa bado mdogo tu. Tukaanza mahusiano. Ni kweli mimi ndiye nilikuwa mwanaume wake wa kwanza. Tukaendelea na mahusiano kwa miezi kadhaa, nikamtambulisha kwa rafiki yangu. Wini akaonekana kuvutiwa naye kuliko mimi. Nikaona mahusiano na yule jamaa yanazidi kuliko mimi. Na yeye yule jamaa akaanza kama kuchanganywa na Wini.”

“Gafla akasahau kuwa mimi ndiye mpenzi wake Wini, na mimi ndiye niliyemtambulisha kwa Wini. Akaanza yeye kuwa akinipa salamu kutoka kwa Wini! Tena akawa mkali kwangu. Wini akaanza kunikwepa, lakini nikawa nasikia anaonekana mtaani na yule jamaa. Shule zikifungwa, anatoka kwao anakuja mjini kwa yule jamaa bila hata kunitafuta mimi, au alikuwa akiomba ruhusa shuleni akidanganya hiki au kile kuwa anarudi nyumbani kumbe anakuja kumfuata yule jamaa mjini.” Lubuva akaendelea.

          “Ile kitu ikaniuma sana. Nikajiambia lazima nimtafute Wini, nizungumze naye. Kama nikuachana, basi anitamkie yeye mwenyewe kama hanitaki tena, anamtaka yule jamaa, Mchanga mwenzake.” “Kwani wewe ni kabila gani?” Geb akamuuliza. “Mrangi.” Lubuva akajibu. “Oooh! Watu wa Kondoa?” Geb akauliza. “Hivyo unavyomuona Nanaa, ndivyo alivyo mama yangu mzazi, ndio maana…” Lubuva akasita kidogo. “Au subiri nimalizie kwanza. Twende kwa utaratibu.” Lubuva akaendelea.

“Shule zilipofunga, nikajua yupo likizo, nikamtafuta Wini. Tukazungumza kwa muda mrefu. Akakiri kuwa alikuwa na mahusiano na yule jamaa. Nikambembeleza sana turudiane. Wini alikuwa ni msichana wa kawaida tu. Lakini…” Lubuva akasita tena kidogo, akaona asimalizie alichotaka kukiongea. “Anyway, siku hiyo tukapatana. Akaniahidi ataachana na yule jamaa, sisi tuendelee. Aliaga kwao anakuja mjini kwa dada yake. Kwa hiyo tulikuwa na muda mrefu tu. Mambo mengine yakaendelea kama unavyojua. Ni kweli tulipata wakati mzuri na ahadi ya kuanza upya ikawekwa hapo. Sasa kilichoniumiza ni kuja kusikia kutoka kwa mdogo wangu, siku  chache baadaye kuwa amemuona tena Wini na yule jamaa, hapo hapo mjini! Hakika nilikasirika Geb. Sikutaka kumtafuta tena Wini na sikutaka mawasiliano naye kabisa. Hata aliponitafuta, sikutaka kuzungumza naye tena.” “Ulizungumza naye baada ya kuambiwa alikutwa na huyo rafiki yako?” Geb akahoji. Lubuva akababaika sana akijitetea. Mwishoe akajikuta anatulia mbele ya Geb aliyekuwa akimtazama na kumsikiliza kwa makini sana bila kumwingilia.

“Labda hapo ndipo nilipokosea. Sikumtafuta na hata aliponitafuta sikutaka kuzungumza naye tena. Niliona amenidhalilisha. Kuniacha mimi na kutembea na rafiki yangu! Wini alikuwa akifahamika mpaka na baba yangu mimi. Alijua nilikuwa nikimpenda sana, lakini akanisaliti. Basi, nikamtumia ujumbe yule rafiki yangu aliyekuwa amenipokonya Wini, nikamwambia nimemuachia kabisa Wini, ila sitataka kumuona tena yeye wala Wini mwenyewe. Nikamuonya asije kurudi nyumbani kwetu na amfikishie huo ujumbe Wini. Wale watu wote wawili wakapotea kwenye maisha yangu. Ndipo baadaye sasa, miezi kadhaa ilishapita ndipo akaja Wini akiwa mjamzito na dada yake, wanadai mimba ni yangu!”

“Naomba tuwe wawazi Geb. Mimi nilikuwa nikijana tu. Ndio mambo yangu ya chuo yamenikalia vizuri. Mpaka chuo ninachoenda kilikuwa kipo tayari. Visa na tiketi ipo mkononi, halafu ni nje ya nchi! Ujerumani! Ada ipo inanisubiria mimi kwenda tu kusoma ili ilipwe! Msichana mwenyewe alikuwa ni kama amemchagua jamaa! Alishakiri kwangu walifanya mapenzi mara kadhaa, au walikuwa na mahusiano ya kimapenzi. Nikamsamehe, tukalala siku hiyo moja, nikaambiwa ameonekana tena na yule jamaa. Mbaya zaidi aliletwa Wini na dada yake, mama James! Kama unavyomjua yule mama, halafu mbele ya Mzee Lubuva aliyekuwa amehangaika kweli kunipatia hiyo nafasi ya kwenda nje kusoma! Alikuwa ameshatoa pesa zake nyingi tu ili mimi niende chuo. Kweli Geb! Hata ingekuwa wewe umesimama kwenye nafasi yangu, ungefanya kama mimi tu!” “Hapana Lubuva. Kama ingekuwa ni Nanaa huyu, mimi nisingefanya kama wewe.” Geb alimkatalia bila kupepesa macho.

“Mimi nina hasira sana, lakini huwa najirudi. Ni heri nife au nikose kila kitu kuliko kumuachia mwanaume mwingine, Nanaa wangu. Mimi si mkamilifu zaidi yako, lakini huwa najua ninachotaka maishani. Na nikikijua, huwa nahakikisha nakimiliki kwa garama zozote zile.” Lubuva kimya. “Ikawaje?” Geb akataka aendelee. Lubuva akavuta pumzi.

“Niliondoka nchini. Na nilipofika Ujerumani, nilifanikiwa sana. Nikikwambia nilifanikiwa, nilifanikiwa haswa mpaka mimi mwenyewe nilikuwa nashangaa. Nilikuwa ‘among of the best Neurosurgeons in Germany’. Nilisoma kwa kuteleza bila kusimama. Tena nilikuwa nafaulu kwa nafasi za juu sana. Ndani ya miaka 15, nilikuwa nimeshakuwa ‘Neurosurgeon’. Tena mzuri. Sikuwa hata na wazo la mapenzi au Wini tena. Ila kazi tu. Nilikuwa busy mnoo. Wazazi ndio walikuwa wakija kunitembelea, lakini sikuwa nikirudi mara kwa mara.” Lubuva akaendelea.

“Mzee alipostaafu, walikuja kuishi na mimi kule kwa muda fulani. Wakati huo nilikuwa nimeoa mwanamke wa kule. Wakayaona yale maisha yangu. Kazi tu, sina muda na familia. Wakaniambia lazima kubadilika. Nikajitahidi kupunguza kazi, ndipo tukapata mtoto mmoja wa kiume, na yeye huyo aliyekuwa mke wangu, alikuwa daktari. Nikajaribisha maisha ya familia, lakini baadaye tukaishia kuachana tu na yule mwanamke. Nikarudi tena kazini kwa juhudi zote. Maana huyo mwanamke aliondoka na mtoto. Lakini kwa makubaliano yakumuona kila ninapotaka. Hapo hapakusumbua.”

“Nilikaa muda mrefu kidogo bila kuoa tena. Kelele za mama zilipozidi, nikaamua kurudi huku nyumbani na kuoa mtu wa hapa. Lakini napo ndoa yenyewe inasuasua. Ni kama tumetengana. Nafikiri akili yangu ipo kwenye kazi zaidi sina muda na...”  Akasita tena. “Turudi kwenye swala la Nanaa.” Lubuva akabadili tena mazungumzo alionekana kutotaka kuzungumzia na Geb juu ya maisha yake binafsi ila yanayomuhusu Nanaa na mama yake.

“Hakika sikuwa na wazo la Wini tena. Nilijua maisha yake yanaendelea. Kwanza niliondoka nikiwa nimeumia nakumuona ni mshenzi ambaye hakuwa hata akitumia kinga! Amekuwa na mahusiano na jamaa mpaka kumpa mimba! Nilimsusa na kuendelea na maisha yangu. Miaka michache iliyopita, mama aliugua sana.Wote tulijua atakufa. Mimi nikarudi nchini kumuuguza. Na tangia natua uwanja wa ndege, mimi ndiye niliyekuwa nikilala naye hospitalini.”

“Siku moja usiku sana, nikiwa naye hapo hospitalini. Tulikuwa wawili tu, usiku wakati anapewa dawa na muuguzi aliyekuwepo zamu, usingizi ulikuwa umemuishia, mimi nasinzia kwenye kiti. Kwanza ukumbuke tulikuwa tunatofautiana masaa. Kule tulikuwa masaa 7 mbele. Muda wakulala kule, huku mnaamka. Nikawa nimechoka sababu ya mvurugiko wa masaa na mawazo. Kichwa nacho kikawa kinaniuma sababu ya usingizi wa mang’amu ng’amu. Mawazo na hofu ya kumpoteza mama yangu ndio ilikuwa inanichanganya zaidi. Nampenda sana mama yangu. Hofu yakufikiri kuwa atakufa na mimi ni daktari nashindwa kumsaidia nayo ilinizidia, haya, huku nako nikawa natakiwa kazini, vyote vilikuwa vikininyima utulivu.”

“Anyway, nikiwa nimelala hapo kwenye kiti akasema, ‘Wini alijifungua. Mtoto anafanana sana na mimi’. Sasa mimi nikahisi ni kama sikuwa nimemsikia vizuri. Nikahisi amemtaja ndugu yetu mwingine. Nikaogopa kumuuliza vizuri, asije akafikiri bado nina mawazo na Wini, kwa kuwa mama alijua vile alivyokuwa ameniumiza Wini, tena baada ya kujua mimi ndiye nilikuwa mwanaume wake wa kwanza na nilikuwa nikimpenda sana.” Lubuva akaendelea.

“Tuwe wa kweli Geb, inauma kuachwa na mwanamke sababu ya mwanaume mwingine. Unahisi watu wanakuona hufai au unakasoro. Pengine unatatizo kubwa. Halafu nikawa nimeshaachana na mwanamke wa kwanza pia. Sikutaka kuendeleza yale mazungumzo. Hasa na mama. Nikanyamaza tu. Lakini kile kitu kikaanza kunisumbua sana. Nikawa sijui mtu wa kumuuliza.” “Yule rafiki yako uliyemwachia Wini?” “Sikuwa nimemuachia. Nili..” Geb akamtizama kwa macho yakumsuta. Lubuva akajirudi.

“Alifariki miaka mingi ilishapita.” Akajibu kwa utulivu kidogo. “Mama alipona. Akaruhusiwa hospitalini, lakini hakurudia tena yale mazungumzo tukiwa pale hospitalini. Tulitoka pale yeye akijua bado nimemkasirikia Wini ndio maana sikumfuatiliza alichoniambia, kumbe mimi sikuwa nimemsikia vizuri na nilisita kumuuliza.” “Nafikiri neno sahihi ni ‘hukutaka’ kumuuliza zaidi sio ‘kusita’.” Geb akamsahihisha. “Sawa.” Lubuva akakubali kinyonge bila kubisha. “Ulirudia kosa kama lile la kwanza.” Geb akaweka msisitizo. “Ha…” Lubuva akataka kubisha, lakini akaona ajishushe tu.

“Nakubali nilikosea tokea mwanzo, lakini na mimi ni binadamu Geb.” Geb akabaki akimtizama kwa muda. “Lakini hata yeye Wini alikosea pia.” “Labda kama una mpango wakuua uhusiano wako kabisa na Nanaa. Nafikiri unakumbuka maneno yake hapa kabla hajalala. Kama unataka mahusiano naye, nashauri uubadilishe kabisa huo utetezi wako.” “Wini mwenyewe…” Akanyamaza. “Sawa.” “Sawa!?” Geb akamuuliza akimshangaa kidogo. “Nakubali kosa kuwa nilitanguliza hasira.” “Nakushindwa kujirudi.” Geb akaweka msisitizo.

“Si hivi nimejirudi!?” “Kwa Nanaa!?” Geb akamuuliza kwa kumshangaa zaidi. “Yaani unajitetea kujirudi kwa Nanaa ambaye hata hukuwa ukimjua kama yupo!? Hapa hujirudi Lubuva. Unachofanya hapa nikuomba, narudia tena na uelewe, WEWE NDIYE UNAYEMUOMBA, Nanaa undugu. Alipofikia Nanaa sasa hivi, anaweza kuishi vizuri tu bila wewe. Muda na wakati aliokuhitaji hukuwepo. Aliniambia tukutafute ili akuone tu sura yako ajue unafananaje. Hakutaka hata umjue kama yupo. Kwa hiyo put your facts together’ na uelewe kabisa. Upo hapa kwa hiari yako mwenyewe. Kujisafisha kwa kile ulichomtendea Wini sio Nanaa.” Geb akambadilikia.

“Sitakuruhusu uzidi kumtesa Nanaa. Kama hutaweza kujirudi kwa Nanaa, bila kumchafua mama yeke, ondoka. Tena uondoke mapema sana. Na ninakuhakikishia Nanaa atapona tu. Ondoka hata sasa hivi, uone kama Mungu hatamtoa Nanaa hapo kitandani.” Geb akambadilikia Lubuva vibaya sana. Alimpa maneno kama ya Nanaa.

“Ulilala na mtoto ambaye hata miaka 18 hakuwa amefikisha! Umeshindwa kumlinda na ulaghai wa rafiki yako. Akamlaghai, akalala naye. Na wewe ukarudi tena kulala naye! Anarudi akiwa ni mjamzito, ukamkana! Leo unasema Wini alikuwa na kosa!? Are you serious!?” Geb akamuuliza kwa hasira kabisa. Kimya. “Ni vile hapakuwa na mtu wa kumtetea Wini kwa wakati ule. Wewe na rafiki yako wote mlitakiwa mshitakiwe. Ungekuwa umemfanyia hivyo binti yangu mimi, hakika ningekufunga.” Tayari Geb alishabadilika. 

“Na ninakuonya kabisa. Usiharibu sifa ya Wini kwa Nanaa. Ni jina analolithamini sana. Vyeti vyake vyote vya shule na kuzaliwa, vimebeba hilo jina la Wini. Mimi mwenyewe nimefanya kuongeza jina langu mbele ya jina la Wini. Anamuenzi huyo mwanamke kuliko utavyofikiria. Hivi unajua kama tokea siku unamkataa Wini mpaka kifo chake alikuwa akilia tu?” Geb akamuuliza. Kimya.

“Sasa ujue ndio sura pekee na sifa alizoambiwa Nanaa juu ya mama yake kutoka kwa mtu anayemuamini sana na kumuona kama baba yake, ambaye ni James. Alichomwambia juu ya mama yake ni kuwa alikuwa akimuona mama yake akilia kwa uchungu sana, muda wote mpaka anapelekwa hospitalini kujifungua, alikuwa akilia. Na hakutoka chumba cha kujifungulia. Hizo ni hisia ambazo kwanza zinamtesa James mwenyewe  mpaka leo na Nanaa pia. James akiota Wini analia, anasema ndio ujumbe anatumiwa kuwa Nanaa yupo matatizoni. Hata kama ni usiku, James akimuota Wini analia, atamtafuta Nanaa alipo ili ajue anaendeleaje. Na ukifikiria kwa makini, utagundua kuwa ni kweli Wini alipokelewa na dada yake baada ya kufukuzwa nyumbani kwao, lakini utagundua ni kama alitelekezwa na kila mtu kwenye maisha yake. Hakuna aliyemjali yeye kama mtoto aliyekuwa mjamzito!”

“Alikufa sababu ya kutotunzwa vizuri. Hakuna aliyejua kama anakwenda kliniki. Hakuna aliyejua kama ana damu ya kutosha akiwa vile mjamzito. Hakuna anayejua kama alipatwa na pressure kama hivi Nanaa au la! Watu wote walimtelekeza mtoto wa chini ya miaka 18, aliyekuwa mjamzito. Mama yake Wini alishindwa kabisa kumsamehe Wini, na wala hamtambui kabisa Nanaa. Mpaka leo amemkataa kabisa Nanaa, kitu kinachomuuma sana Nanaa. Walimnyima hata kutumia jina la ukoo wao! Ndio maana Nanaa aliishia kuitwa Nanaa Wini.” Geb akaendelea kwa jazba.

 “Nanaa alikwambia jana kuwa alikataliwa na baba yake. Tena mara mbili. Mama yake akiwa mjamzito, na aliporudishwa kwenu mara baada ya mama yake kufariki. Alikwambia ulimkimbia yeye kama mzigo ili maisha yako yaendelee. Huna jinsi yakujiweka wewe upande mzuri, halafu kumuweka mama yake upande mbaya, ukawa na mahusiano mazuri na Nanaa. Hata siku moja.” “Nimeelewa.” Lubuva akajibu kwa upole.

Geb akamgusa Nanaa kichwani kama anayempima joto kwa kiganja chake. Akambusu na kukumbatia mkono wake. Akainama na kuubusu mkono wa Nanaa. Lubuva akaona anafunga macho. Hakujua kama anasali au la. Akaamua atulie kidogo. Alipoona kimya kinazidi akaamua kuvunja ukimya.

“Nataka kuwa na mahusiano na binti yangu.” Geb akamgeukia na kumtizama Lubuva. “Nilifanya kosa mara ya kwanza, nikaondoka. Sasa hivi nataka kuwepo kwenye maisha yake.” Lubuva akaweka msisitizo.

“Ni nani sasa aliyekwambia tena kama yupo?” Geb akauliza. “Baada ya mama kupona, nikatakiwa kurudi kazini. Tukiwa uwanja wa ndege, kabla sijapanda ndege, mama akaniita pembeni. Akasema hata kama nilimkasirikia Wini, lakini siwezi kutupa mtoto daima. Nikamwambia mtoto aliyekuwa amembeba Wini hakuwa wangu. Ndipo akasema Wini alifariki wakati akijifungua. Nanaa akaletwa pale nyumbani mimi nikiwa nimeshaondoka. Mama akasema japokuwa walimkataa Nanaa, lakini yeye alijua ni damu yake kwa kuwa alifanana sana na yeye hapakuwa na jinsi akawa mtoto wa yule jamaa. Kwanza jamaa mwenyewe alikuwa mweusi sana. Na tulikuwa tukifahamu wazazi wake. Japokuwa Wini alikuwa mweupe, lakini anasema Nanaa alibeba rangi ya weupe ya kwetu. Yeye mama anajua. Akasema hata sura tulikuwa tukifanana. Sasa hapo ananiambia, ndio nilikuwa natakiwa niondoke. Yaani ndio nipande ndege. Natakiwa kazini. Nikaondoka niki…” “Kosa la tatu hilo!” Lubuva akanyamaza.

Geb akasimama vizuri pale alipokuwa amemuinamia Nanaa. “Kwa nini upo hapa dokta Lubuva!? Kwa nini sasa hivi!? Unaweza kuwa umekuja kummaliza mke wangu bila hata wewe mwenyewe kujua.” “Geb! Sina nia..” “Subiri kwanza. Swala lakujulishwa kuwa yupo Nanaa, ulilijua lini kwa hakika?” “Miaka kama 3 na miezi kadhaa iliyopita.” Lubuva akajibu. “Ambapo Nanaa ndio alikuwa akitafuta pakwenda! Anahitaji msaada. Ndicho kipindi alifukuzwa kwa James, akahamia nyumbani kwangu.” “Najua. Ndio na wewe ukampa mimba!” “Acha kunibadilishia maneno. Mimi nilimpenda Nanaa.”

“Kilichokushinda kumuoa kwanza ndipo umzalishe ni nini kama sio kuona ni binti wa kuchezea tu, asiye na mtetezi? Ulimpa pakuishi, ukamshikisha mimba na kumtelekeza. Wangemfanyia hivyo Oliva, binti yako ingekuwa sawa?” Lubuva naye akambadilikia.

“Usijifananishe na mimi, kwa Nanaa. Mimi nilijirudi.” “Mara ngapi umekuwa ukijirudi kwa Nanaa? Hivi unajua leo yupo hapa kwa sababu yako wewe Geb?” Lubuva akamjia juu. “Siku nampa ushauri wakunywa dawa za kupunguza maumivu ya matiti kuuma, wewe ulikuwa umemkimbia na kumpokonya watoto wake. Nilimkuta tena kituo cha mabasi anatetemeka kwa pressure kuwa juu, kwa sababu ulikimbia na dawa zake alizokuwa amepewa hospitalini. Unafikiri na mimi sijui uliyomtendea Nanaa?” “Nanaa alinidanganya ndio maana nilikasirika.” Lubuva na yeye akakunja mikono na kuiweka kifuani, akamwangalia na jicho kama kumsuta Geb. Yapi na yepi! Alimsuta Lubuva kwa Wini, na yeye kwa Nanaa!!! Lubuva akabaki akimtizama.

“Lakini mimi nilijirudi mapema sana sio kama wewe.” “Ulijirudi ukiwa umeshamsababishia madhara yakudumu! Akiwa ameshaharibika moyo! Yaani ameugua peke yake, ndio unajirudi! Na wewe ulitumia ukiwa wake vizuri sana kumnyanyasa. Ulishindwa kumlinda na rafiki yako mlaghai mpaka akamjeruhi!” Lubuva akambana Geb kwa maneno yake yeye mwenyewe.

“Umemsababishia maradhi ya kudumu. Na sasa ni lazima umfanye atulie hapo, mimi ndiye nimuhudumie. Unanielewa Geb? Tafuta lugha yeyote yakuzungumza naye atakapoamka hapo, mpaka akubali mimi ndio niwe daktari wake.” “Nikikataa wewe kuwa daktari wake?” Geb akauliza kwa  jeuri kama akitaka kujua atamfanya nini sasa! Tayari alishakasirika.

“Unamaanisha kama ulivyokataa kuweka hasira zako pembeni, na kumtelekeza baada yakumuombea aruhusiwe hospitalini akiwa mgonjwa, ukamuahidi dokta Lyamu na Rweta kuwa utakuwa ukimrudisha hospitalini kwa vipimo na kumpa dawa, halafu kesho yake ukamkimbia na watoto wake pamoja na dawa ulizosisitizwa azitumie?” Na yeye Lubuva akamuuliza akimtizama machoni.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wamekutana mafahari wawili. Lubuva&Magesa. Wote wajuaji. Itakuaje?

Nanaa aliyekuwa akitafuta Ukweli, ameupata, anashindwa kuumudu. Itakuaje kwa baba yake?

Usikose muendelezo.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment