Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 65. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 65.

 Huko Kwa Fili Hospitalini.

Grace alifungua macho pale kwenye kochi. Ilikuwa asubuhi. Alilala baada ya kuchomwa sindano iliyomsaidia kupata usingizi mzito. Chumba kilikuwa kimya. Ni mashine za Fili tu ndizo zilizokuwa zikisikika akiwa usingizini. Akamwangalia Man. Alikuwa amelala kwenye kiti. Akaumia sana moyoni. “Man hastahili haya yote. Alitakiwa kuwa sehemu nzuri amepumzika sasa hivi na mkewe, kama sio kunioa mimi, mama mwenye watoto na historia mbaya ya ndoa.” Grace akawaza. “Wanangu!” Machozi ya uchungu yakaanza kumtoka kila alipokumbuka wanae. Kumbukumbu ya mwisho ya wale watoto wake, ni vile walivyokuwa wakimlilia aende nao. Yalipita mawazo kadhaa kichwani mwake. Akijilaumu kwa kila hatua aliyowahi kuchukua kwenye maisha yake.

Akatoka pale kwenye kochi alipokuwa amelala, akaelekea bafuni kuoga. Man alipomsikia bafuni akamfuata. “Vipi? Unajisikiaje?” Grace akafunga maji kwenye sinki la kupigia mswaki. “Najisikia vizuri, lakini nahisi nahitaji muda Man.” “Unamaanisha nini?” Man akauliza. Grace akajifuta machozi. “Kwa sasa siwezi kuwa mke mzuri kwako. Nimechanganyikiwa. Nina maumivu na majuto ambayo sijui nitafanya nini na sijui nitapona lini. Naomba unipe muda.” “Unamaanisha nini?” Bado Man alirudia swali lake.

“Nashauri wewe uondoke Man. Rudi kwenye biashara zako. Au niseme rudi kwenye maisha yako kama kawaida. Nitakapokuwa sawa, nitakutafuta.” Man alijirudisha nyuma akaegemea kwenye ukuta akabaki akimtizama Grace. “Sio kwa nia mbaya Man. Ni kwa ajili yako. Hii ndoa inakuwa kama inamkosi! Tumeoana tu nimeingia na misiba! Ndio maana nilikuwa nikisita tokea mwanzoni nikikwambia mimi sio msichana Man. Ona nilipokufikisha!” “Naomba usiongeze neno jingine Grace. Najua umeumia. Lakini naomba usiongeze neno jingine. Tafadhali sana.” Grace akakaa chini kabisa sakafuni nakuzidi kulia.

Man alimchukua kutoka pale sakafuni, akamtoa nguo na kumwingiza bafuni. Grace akaoga akiwa analia kwa uchungu sana, mpaka akamaliza. Alitoka na kukuta taulo likimsubiri mkononi kwa Man. Akajikausha na kuvaa, akabaki kama ameduaa. “Twende ukapumzike.” Wakatoka pale bafuni, wakarudi chumbani alipokuwa amelazwa Fili. Grace akarudi kujilaza kwenye kochi, lakini akageukia ukutani akawa amempa mgongo Man. Akamfunika, nakubaki akimsugua mgongoni mpaka Grace akalala tena. 

Baada ya muda nesi akaingia kusamfisha Fili na kumpa dawa. Grace akaamka. Akauliza kama angetaka msaada, lakini yule nesi alimwambia anamfanyia kitu kidogo tu. Man alivuta kiti pembeni ya Fili, kama aliyelevya na madawa, Fili akarudi kulala. Man akabaki akiwaza.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika kwenye saa 3 asubuhi mama G akaingia akiwa na Liv. Man akasalimia. Grace alibaki amelala vile vile amegeukia ukutani. “Pole baba na matatizo.” “Asante mama. Vipi na wewe umeamkaje?” Man akamuuliza. “Naona nimeamka vizuri.” “Namuomba Liv nimsalimie.” Liv aliposikia jina lake likitajwa akajificha nyuma ya bibi yake. “Nenda bwana kasalimie. Ni nini Liv?” Bibi yake alimchungulia pale alipojificha. “Nenda kamsalimie anko.” Liv akacheka na kidole chake mdomoni. Bibi yake akajua ndio amekataa.

“Umependeza Liv!” Man akamsifia. Liv akamchungulia. “Nywele za Liv nzuri! Sijui nani amemtengeneza?” “Bibi.” Liv akajibu huku anachungulia. “Jamani bibi ni mjuzi! Umemuona Fili?” Man akamuuliza. “Nampenda Fili.” Liv akaongeza. “Njoo basi umsalimie.”  Akaingia Nanaa na Geb akiwa amembeba Magesa. Wakasalimiana. Geb akaenda kukaa kwenye kochi alilokuwa amejilaza Grace. Akamuweka Magesa juu yake. Magesa akaanza kuruka ruka pale alipokaa juu ya anti yake. Grace akamgeukia. Alijawa cheko, Grace akatabasamu.

“Kila wakati wewe ni kucheka tu!” Grace akamshika vizuri. “Muone!” Magesa alikuwa anaruka ruka pale mwilini kwa shangazi yake alipokuwa amekaa, huku akiongea anayoelewa yeye na cheko juu. Grace akabaki akimwangalia huku akicheka. Huwezi kumshika huyo mtoto usiburudike  moyoni. “Wewe amani yako huwa inakutoshea mwenyewe! Muone!” Grace alimwambia Magesa nakumfanya azidi kucheka.

Oliva yeye akajivuta taratibu mpaka kwa mama yake. “Namtaka Fili.” Akaongea kwa upole. Lakini kama Fili alisikia kutoka usingizini akafungua macho. “Liv!” Alifurahi sana. “Njoo uone. Naumwa mwenzio.” Geb akaenda kumnyanyua Liv mpaka pale karibu ya Fili. “Nimeumia mkono. Halafu wamenitoboa hapa.” Liv akainama. Baba yake akajua anataka kumbusu Fili. Akamsogeza akambusu kichwani. “Na hapa mkononi Liv.” Liv akajisogeza kwa nguvu kama kufikia ule mkono alioonyeshwa na Fili. Geb akamsogeza. Liv akabusu mkono. “Pole Fili.” Liv aliongea kwa upendo. Wote wakabaki kimya wakiwasikiliza.

“Nampenda Fili.” “Na mimi nakupenda Liv. Lakini unajua dad wangu alinipiga tena?” Fili akamuuliza Liv. Kila mtu kimya. “Nampenda Fili.” Liv aliongea tena kwa upole. Akainama tena akambusu. “Mbusu dad.” Akamgeukia baba yake, akitaka na yeye ambusu Fili. Geb akambusu na yeye Fili. “Aahahaa!” Liv akamkatalia baba yake, kama aliyekosea alichotaka afanye kwa Fili. Geb akawa hajaelewa kitu Liv anataka tena. “Hapa dad.” Liv akamuonyeshea baba yake kifuani. “Mwenzio anataka umuweke Fili kifuani kama unavyomfanyia yeye.” Nanaa akaingilia. “Aaaahaa!” Geb akaelewa. “Sasa kwa nini wewe usimfanyie? Fili atafurahi sana kama wewe ukimfanyia.” Geb alimwambia Liv. Liv akacheka na kidole chake kimoja akakiingiza mdomoni. Akambusu dad wake. Akataka amshushe, amuweke hapo kitandani.

“Sasa hapo taratibu we Geb na mwanao. Msimtoneshe Fili.” “Liv ni mstaarabu bwana! Eti mama? Utamuumiza Fili?” Geb akamuuliza. Liv akatingisha kichwa kukataa. “Haya. Taratibu usichomoe waya hata mmoja.” Geb akaendelea kumtahadharisha Liv. Kweli Liv alikuwa mstaarabu. Walimtoa viatu. Wakamuweka pale kitandani. Akatembea taratibu huku baba yake amemshika mkono asianguke pale kitandani. Alitembea kwa tahadhari mpaka pale alipokuwa amekaa Fili. Baba yake akamwachia huku akimwangalia. Akamkumbatia Fili, zaidi kichwa chake sio kifua ambako alitobolewa.

Wakamsikia Liv akifanya kama baba yake. “Mmmmmmh!” Kisha akaanza kumbusu kila mahali usoni. Kila mtu alicheka. Alifanya kama anavyofanyiwa yeye na baba yeke. Geb alimtizama mwanae asiamini. Alifanya bila kukosea. Kisha akakaa pembeni ya Fili. “Nampenda Fili.” Akamshika mkono. “Na mimi nakupenda Liv.” Walimsikia Grace akilia.

Tayari akili ya Magesa ikaruka. Akaanza kuruka ruka macho yapo kitandani alipokuwa amekaa Fili na Liv. Mikono hewani ili atolewe pale kwa shangazi yake, apelekwe na yeye pale kitandani. “Huyo ataharibu bwana! Una nini Magesa wewe? Wewe mbusu tu anti hapo.” Magesa alizidi kurukaruka akiashiria achukuliwe na baba yake. Mikono yote juu anaita kwa vidole. Geb akacheka na kwenda kumchukua. “Naomba usije kumuweka pale kitandani Geb. Tafadhali sana. Huyo atang’oa kila kitu pale. Mashine zote zitatupwa na atawavuruga wenzake.” “Nitamshika.” “Na umshike kweli. Unamjua alivyo na manguvu. Akimshika tu Fili, atamvuta mpaka amtoe waya zote mwilini. Naomba yeye ambusu ukiwa umembeba. Hakuna kukumbatia.” Nanaa alizidi kutoa maelekezo juu ya mwanae Mgesa. Kidogo watu wakacheka.

“Umemsikia mama yako? Wewe huruhusiwi kukaa kitandani. Unabusu tu na kuondoka. Sawa?” Magesa akaanza kucheka huku akimwangalia Fili. Geb akamwinamisha, akambusu. Kisha akafungua mikono ili amkumbatie na yeye kama Liv. “Hapana Geb. Huyo mpeleke akamkumbatie anko Man.” Mpaka Grace akacheka. “Njoo Magesa.” Hakuwa na makuu. Akakubali kwa haraka. Akanyoosha mikono kule kwa Man. Man akampokea. Cheko na mate juu. “Uzuri mwenyewe hana shida.” Mama G akamsifia. Kweli akamkumbatia Man, na kumbusu. Akamuachia mate shavuni. “Pole mwaya Man. Chukua kitambaa hiki ujifute. Yuko kwenye kuota meno. Basi kila mtu anamlowesha mate yake.” Man akacheka. “Hamna shida. Mwache tu tupakane hayo mate. Ndio nafurahi.” Man alijibu huku akimwangalia Magesa akimchekea.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mara James akaingia. Nanaa akasimama. “Shikamoo kaka!” “Marahaba. Vipi wewe?” “Hatujambo. Mbona huna raha?” Nanaa akamuuliza kaka yake. James akafikiria kidogo. Akanyamaza kisha akauliza. “Vipi Fili?” Akasogelea kitandani. “Naona Liv anauguza.” Liv akacheka, kidole mdomoni. “Shikamoo anko.” Fili akasalimia. “Unajisikiaje?” James akamuuliza. “Nimefurahi Liv amekuja kunisalimia.” “Nakwambia aliyeingia hapa ni Liv peke yake!” Bibi yake akanong’ona. “Wewe umemkumbatia na kumbusu?” Nanaa akamuuliza mama G. Akaguna. “Maana mwenzio tangia ameingia hapa anaimba ‘nampenda Fili’. Mabusu mpaka ya kichwani! Huwezi kujilinganisha naye.” Wote wakacheka.

“Vipi Grace?” “Nipo James.” “Pole mama. Pole sana.” “Asante.” Grace akajibu kwa upole. Geb akaenda kukaa pembeni yake, akabaki akimtizama. “Umekula?” “Sisikii njaa.” Grace akamjibu kaka yake na machozi. “Lazima ule G. Kula kama dawa.” Wakamuona anamtengeneza nywele. Anazitoa usoni na kuziweka nyuma ya masikio na nyingine anazirudisha nyuma taratibu. Akamfuta dada yake machozi. Man alirushia macho, akamwinamia Magesa akaendelea kucheza naye. Nanaa na mama G, wakaangaliana, wakanyamaza. “Nikumiminie uji kidogo?” “Uji kama mzazi!? Au uji wa Nanaa?” “Ukikataa kuunywa mimi nitaunywa.” Nanaa alijibu wote wakacheka. “Kwanza nashauri nyinyi wawili mkapate kifungua kinywa, mlale kidogo, ndio mrudi. Mimi na mama ndio tumefika hapa.” Nanaa akaongeza.

“Kweli mtabaki?” Grace akauliza. “Tumekuja tukiwa tumejiandaa na chakula mpaka cha mchana. Nyinyi nendeni mkapumzike. Mrudi hata jioni. Mlezi yule pale kitandani. Huyo baba mzazi tumekuja na walker yake. Atatembea hapa mpaka achoke. Nyinyi nendeni tu.” Mama G akaweka msisitizo. “Kapumzikeni Man. Mtarudi baadaye. Mama na Nanaa watakuwepo hapa, na mimi nitarudi baadaye. Naenda kuchungulia tu hapo kazini, nitarudi. Nashauri mkapumzike.” Geb akaweka msisitizo. Man akamtizama Grace. “Twende.” Grace akaongea kwa upole.

Akasimama na kwenda kumbusu Fili. “Unataka nikuletee nini?” Fili akafikiria, akamwambia mama yake hataki kitu. “Basi nitakuona baadaye. Nakupenda sana Fili.” “Mimi najua mama. Nilimwambia hata Sara. Ila yeye ndio alikuwa akibisha.” “Nimefurahi kama unajua hilo Fili. Nimefurahi sana.” Fili akacheka. Grace akambusu tena mwanae na kumuaga kwa ahadi ya kurudi baadaye ili awe naye usiku huo pia. Fili akaridhika. Ndio Grace akapata Amani ya kuondoka.

Wakati wanataka kutoka ndio wapo mlangoni, akaingia mama Ole, Malisa, wadogo zake wawili Man na mke wa kaka yao. Ikabidi Grace arudi ndani. Man akawaambia Grace anatakiwa kwenda kupumzika. Wakasalimiana na kumpa pole Fili, wakaelewa hawatakiwi kukaa hapo muda mrefu. Wakatoka na Grace na Man huku wakizungumza.   

James Na Yaliyojiri!

James alikuwa ameinama. “Umetokea kazini?” Nanaa akamstua kaka yake. “Daah! Sijakwenda. Yaani hapa umenikumbusha. Ngoja niende. Nahisi nimekuwa kama nimepatwa na mshituko fulani hivi. Nashindwa kufikiria. Sijui chakufanya! Akili inazidi kuchanganyikiwa.” Geb akamuweka Magesa kwenye walker yake tayari kwa kuondoka. “Mama!” James akaita akiwa kama anawaza. “Vipi James mwanangu?” Walijua lazima James awepo kwenye mshituko. Ndiye aliyewazoa watoto wa Danny na Grace na kuwaweka kwenye mfuko. 

Akarudi kukaa. “Namfikiria Danny, bila kupata majibu. Nimemuuliza maswali ambayo hata sikumpa muda wa kuyajibu, lakini ni kama nimepata majibu kwa sehemu.” “Kwani umeonana naye!?” Nanaa akauliza swali la kwanza. “Ndio nimetokea huko.” “Unaposema ulimuuliza maswali na umepata majibu, unamaanisha nini?” Mama G akauliza taratibu. “Upo mchezo mchafu sana umechezwa mama. Najua Danny amewaudhi sana. Lakini kuna jambo kubwa sana linaendelea. Na tusipokuwa makini, hakuna kati yetu atakaye simama au kusalia.” James akaanza kusimulia kuanzia alivyoingia yeye, na mazungumzo yake na Danny. “Amebaki kama amepigwa ganzi.” James akamalizia kipengele cha kwanza na kwenda cha pili.

“Hivi tunavyozungumza, Sara amelala kitandani kwa Zinda.” James akaendelea “Sikuamini aliposema amelala na Sara. Tena kwa kumwambia mwenzie hajaona chochote kwa huyo Sara!” “Kaka wewe!” “Mbele yetu. Tena akamwambia amemfukuza kwake, hataki mikosi. Tena wanasaidiana na Gozi kumcheka mwenzao. Sijui mwisho wa Danny utakuaje. Hakika namfikiria simpatii jibu. Alichoweza kufanya asubuhi hii niku freez akaunti zake zote, kwa kuwa siku ya ajali, Sara alitoroka na wallet yake. Tokea siku ya ajali mpaka jana usiku, Danny ameambiwa na watu wa benki, Sara alikuwa na kazi ya kuzunguka kwenye ATMs kutoa pesa.” “Sasa ataamini niliyomwambia juu ya Sara. Nilimwambia mimi Danny kuwa Sara sio muhuni, ni Malaya asiyeona shida kuvulia wanaume hata watatu nguo kwa siku moja. Akabisha. Atamfilisi.” Nanaa akaongeza.

“Ila naona amemuwahi. Bado salio lake ni zuri tu. Na mshahara bado utaendelea kuingia. Hayupo pabaya kifedha.” James akaongeza. Mama G alikuwa amenyamaza kimya. Geb hakuweka hata neno.

“Ameulizia hali ya Fili, nikamwambia ukweli wote. Jinsi mwanae anavyosimulia kisa chote. Na nikamwambia aombe Mungu Grace asimshitaki. Hatakaa akamuona tena huyu mtoto.” “Akasemaje?” “Sio alichosema yeye, ni alichosema Zinda na mama yake ndio kinachonichanganya mimi hata Danny mwenyewe.” Geb na mama yake wakakaa sawa. James akajua wanataka kusikia.

“Niliposema mchezo mchafu msifikiri nazungumzia mambo ya Sara! Hata kidogo. Mchezo mchafu waliocheza Zinda na mama yake.” James akasimulia tena mazungumzo ya mama Zinda, Zinda na Danny. Kila mtu akaingiwa hofu. “Yule mama bado anamlalamikia Nanaa!” “Kaka wewe!? Mimi!?” “Unajulikana huko Tabora. Na kosa ni la Danny. Kuwa alimpokonya Zinda mchumba kwa kutulaghai mimi na wewe kisha akakuozesha kwa Geb. Yule mama bado ana kinyongo.” “Kwa hiyo walimpokea Danny ili kumuangamiza!!” “Sawa sawa Nanaa. Wewe umewaza sawa.” “Shetani ametumia vizuri sana hasira za Danny.” Mama G akawaza kwa sauti.

“Hivi unajua mama yake Zinda alirudia kumwambia Danny yale maneno ya kuwa alilaaniwa!” “Haiwezekani James!” “Kweli mama. Na amemwambia mizimu ya kwao imemkataa. Hawamtaki arudi tena kwao. Amebakizwa ili kulipa ubaya aliomfanyia Zinda. Bahati zake zote alizozichukua kwa Zinda ndio zinarudi sasa kwa Zinda na kumuacha yeye mtupu kama alivyotakiwa awe. Lakini mama na Geb, naombeni mnisikilize kwa makini sana, tusaidiane hili jambo. Maana sisi wote hapa majina yetu na maisha yetu yapo huko Tabora. Tunajulikana.” Kila mtu akatulia.

“Kuna jambo yule mama alitaka kumalizia, Zinda akamkata kwa haraka kama kuficha asiendelee kuzungumza. Lakini kwa mazungumzo yao ya awali, imenifanya nifikirie sana. Binafsi nimeingiwa hofu. Hawa kina Zinda walipompokea Danny. Au tuseme Danny aliporudi kwao akiwa na hasira juu yenu, cha kwanza walichohakikisha ni kumfanya kuwa mateka wao. Mimi nilivyofikiria. Wakamuaminisha kuwa mmemloga. Danny alisimulia mbele ya Zinda kuwa hata mama yake Zinda alimwambia kuwa mganga wao amemthibitishia nyinyi mmemloga. Sasa sikiliza walichoanza kumfanyia Danny.” James akaendelea.

“Wakamwambia inabidi kutakaswa na kukombolewa na nyinyi. Ndio safari za Tabora zikaanza. Kumbe anaenda kuaguliwa kwa mganga wao. Danny anasema alikwenda mara tatu yeye na watoto wakisindikizwa na Zinda. Mara ya tatu ndipo akaambiwa akatafute kondoo, mbuzi na jogoo mwekundu. Vyote hivyo vilikuwa vyakutakaswa yeye na watoto. Zinda ndiye aliyemsaidia kuvipata kivyo vitu. Yeye na watoto wakaenda kufanyiwa walichofanyiwa. Sasa safari hii ya nne, ndio walikuwa waende wakapatanishwe na ukoo wa kina Zinda. Si ndio Danny amepata ajali. Kilichomshangaza Danny ni kuwa, safari zote alikuwa akienda na Zinda. Ila safari hii walimwambia Zinda hatakwenda ni yeye na familia yake tu. Ndio mama Zinda akataka kuropoka kitu, Zinda akamkata. Ila kabla ya kumkata ndio akasema yale maneno kuwa mizimu imemkataa Danny kwa kuwa anamkosi mkali. Imemzuia hata asifike kwao.” Wasikilizaji wote walikuwa wameduaa. James akawaangalia mmoja baada ya mwingine. 

“Danny akamuuliza Zinda kama ni wao wamehusika na ajali yake. Zinda akambadilikia vibaya sana. Amemgeuzia maneno yote. Yaani Zinda amemgeuka mwenzie, hutakaa ukaamini kama ni wao.” James akatulia kidogo. “Sasa nisikilizeni. Hawa watu niwashirikina sana. Kumbukeni mambo ya Mira. Na Mira naye ametoka sehemu moja na Zinda. Kwa kusikiliza tu, bila hata kutaka ufunuo, hawa watu walimtega Danny. Waliwapeleka watoto wote na Danny kwa mganga wao, Danny akijua anatakaswa, kumbe wanamuangamiza. Yule mama anaonekana anahasira sana na Danny.”

“Hakika anasikika anahasira ambazo hawezi kuzificha. Ametaja mambo ambayo yametushangaza mimi na Danny. Anasema mpaka kazi ya Danny ilitakiwa iwe ya Zinda! Sasa kivipi, hakuna anayejua.” Kumbukumbu zikamjia Geb kwa haraka. “James wewe umesahau. Unakumbuka siku moja tulikuwa wote tumekaa, ukaja ukasema kuna nafasi ya kazi ofisini kwenu. Ukasema wanatafuta mtu. Ulipotaja sifa zake, Zinda akasema yeye anaweza kuomba hiyo nafasi. Akakuomba umuunganishie. Ukakubali. Lakini Danny akasema kwa kuwa yeye hana kazi, na Zinda anayo kazi tayari, kwa nini usimuunganishie yeye. Jamaa wote wakakubaliana na wazo la Danny. Tena nakumbuka bila hata kuwekana sawa na Zinda, wewe ukahamisha mazungumzo yote ya ile kazi kwa Danny. Pale pale mkapanga mambo yenu juu ya ile kazi. Ukampa njia ya kuipata ile kazi. Yaani sasa hivi ndio nakumbuka vizuri zaidi. Zinda aliondoka pale wakati wewe na Danny mkiendelea kuzungumza.” Geb alimfanya James akumbuke kila kitu. “Mungu wangu!” James akahamaki.

“Inamaana Zinda amekiweka hicho kitu moyoni mpaka leo!!?” James akauliza akiwa kwenye mshangao mkubwa sana. “Si ndio maana mama yake amekisema tena leo? Inamaana wanayo orodha ya makosa yetu wote sisi.  Sasa hutuwezi kujua waliwafanyia nini! Umbali gani walikwenda au watakwenda kulipiza kisasi! Na kwa nani! Na kama bado wataendelea kufanya! Fili yupo hapa hospitalini, lakini tukumbuke na yeye alifanyiwa kile walichofanyiwa wadogo zake. Sisi tuanze kumwita Mungu wetu sasa hivi. Geb, tuombe kabla hujaondoka.” Mama G akachangamkia eneo lake la kujidai.

“Tuweke kikomo kwenye ajali zote na tumkomboe Fili na mama yake. Tokea jana Grace ameanza kutokwa damu isiyo yakawaida! Tuvunje madhabahu zote zilizoshikilia majina yetu sisi wote hapa na kizazi chetu. Hata wewe James. Lazima kutubu na ujiweke kwa Bwana. Hakuna aliye salama kati yetu. Hawa watu wanaonekana wamebeba visasi na wamekusudia kutuangamiza. Lakini kama Mungu wetu aishivyo, watapigana na Mungu. Tumwiteni Mungu wetu, akaingilie kati. Hata wakituita tena huko kwenye madhabahu zao, wakakutane na simba wa kabila la Yuda. Yesu mwana wa Mungu. Hatutamlipa mtu kisasi. Acha Bwana ashugulike nao.” Hapo wakawa wamemchokoza mama G.

Akasimama akiwa amejawa nguvu ya ajabu. Maombi yakaanza pale ndani. Waliomba kwa nguvu ya ajabu huku watoto wao wakiwatizama. Magesa alitulia kimya akiangalia bila hata kuongea. Chumba kilijaa utisho wa ajabu. Walivunja na kung’oa bila kuchoka. Mara Fili akaanza kutapika, mpaka nesi ikabidi aingie.

Alitapika vitu vyeusi vitupu huku amejinyoosha kitandani kama nyoka. Alipoanza kutambaa kama nyoka, wakajua ni pepo. Mama G akamsogelea maana nesi alikimbia kwa hofu. Fili ni kama alikuwa akijitonesha kile kidonda. Akageuza jicho kama anayetaka kukata roho. James alimtoa kwa haraka Liv pale kitandani. Mama G na Geb wakakemea bila yakuogopa. 

Nanaa akashangaa Geb ameweka mkono juu ya Fili, akaamuru kwa kifupi tu, “Nyamaza na mumtoke Fili kwa haraka.” Hapo hapo Fili akajinyonga na kutulia. Wote wakaduaa na kumshangaa Geb. Geb alikuwa amejawa nguvu za Mungu. Tokea wanaanza maombi alikuwa akiomba kwa roho.  Pakatulia kidogo. Geb akamnyanyua Fili akaenda naye bafuni. Alikuwa amejawa matapishi kila mahali. Na alikuwa amejitoa kila kitu mwilini mwake. Mashine zote zilikuwa zimetolewa. “Unajisikiaje?” Walimsikia Geb akimuuliza huko bafuni.  Nanaa aliita manesi kwa kubonyeza kengele. Wakaja kusafisha na kuleta nguo safi za Fili. Wakamrudisha Fili kitandani.

Ndipo maombi ya shukurani na kuomba ulinzi juu yao yakaanza. Mama G alimuomba Geb ahitimishe kwa maombi. Geb alitaka washikane wote mikono. Walitengeneza duara. Wakashikana mpaka na watoto na Fili pale kitandani. Geb akaanza kuomba na kumwambia Mungu anamshika Grace na Man mikono katika ulimwengu wa roho. Akakemea kutokwa kwa damu kwa Grace na kuruhusu mzunguko sahihi ulioamriwa na Mungu. Wakafunga roho za mauti. Ndipo wakamaliza hayo maombi. Kila mtu alisema amepata amani. Geb na James walitoka kwenda kazini na kuwaacha hapo mama G na Nanaa, wakiwa na watoto.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Umeona jinsi Geb alivyoamuru yale mapepo!?” Nanaa akamuuliza mama G. “Mimi mwenyewe nilishangaa.” “Ujue nilikuwa nataka kukimbia kama yule nesi!” Wakaanza kucheka. “Ni vile kaka James alisema na Fili alifanyiwa kama wadogo zake, nikajua na yeye anakufa. Sasa hofu ikaniingia, nikasema mimi sitaki kushuhudia.” “Mimi nilijua ni mapepo tu, ndio maana nikamsogelea.” “Nilikuona mwenyewe mama. Kama sio wewe!” Mama G akaanza kucheka. “Kumbe mwenyewe una maeneo yako yakujidai?” “Huwa shetani ananikera sana, Nanaa. Mpuuzi wa mwisho. Siwezagi kumvumilia mimi.” “Mama huyo! Kwengine huwa unaganda.” Mama G alicheka sana.

“Acha uchokozi Nanaa.” “Lakini umenitia ujasiri. Nifundishe mama. Mimi sijui hata kukemea pepo.” Wakaendelea kuzungumza. Wakakumbushana Vile Geb alivyotumika kwenye uponyaji wa Nanaa alipoharibiwa miguu. “Lada Mungu ndio amempa huduma ya uponyaji.” “Labda. Lakini ujue Geb anaomba mama, mpaka mimi nashangaa. Kila siku saa 11, utamkuta amepiga magoti kule kwenye ile sebule ya pale chumbani kwetu, anaomba. Halafu taratibu. Na anaomba muda mrefu mpaka nashangaa. Namuuliza unaomba nini? Anacheka, anasema mara nyingi anakuwa anaomba kwa roho.” Nanaa na mama G walishinda hapo hospitalini wakiongea hili na lile. 

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika jioni Man na Grace waliingia hapo chumbani. Grace alionekana akiwa ametulia. Alimwambia mama yake alilala vizuri. Na damu ilikata. Wakaangaliana na Nanaa. “Mbona mnaangaliana?” Grace akauliza. “Naomba tukazungumze kidogo hapo nje.” Grace na Man  wakamfuata mama G. Wakatafuta mahali wakakaa. “Kuna nini?” Grace akauliza. “Unakumbuka siku ya kwanza Zinda kujirudi kwa Danny akitaka Danny amsamehe?” Grace akatulia.

“Tulikuwa nyumbani kwa Geb na Nanaa.” “Siku ile James alipowaleta ndugu zake?” “Ewaaa! Sasa si unakumbuka yale majibu ya Danny kuwa yeye mwenyewe ndio atamtafuta Zinda. Zinda asiende kwake.” “Nakumbuka.” Grace akaitikia. “Sasa inavyoonekana, shetani ametumia hasira ya Danny vizuri sana. Kwanza walianza kwa kumwaminisha tunamloga. Akaingiwa hofu na sisi. Najua kusudi zima, ni kumtenga na sisi ambako alikuwa akifunikwa kwa maombi.” “Mama, mimi sitaki kumsikia kabisa huyo mtu.” Grace akataka kuondoka.

“Nisikilize Grace. Tena nataka unisikilize vizuri sana. Kwa kuwa hasira na ukorofi wa Danny ndizo zimetufikisha hapa tulipo. Wametumia udhaifu wake vizuri sana, sasa hivi wamemuacha anateseka peke yake hospitalini wakimcheka waziwazi. Kama wanaofurahia yaliyompata. Na ninakuhakikishia Grace, ukiruhusu hasira zikuweke mbali na Mungu, hata Fili utampoteza.” Grace akarudi kukaa. 

Mama G, alipomuona Grace ametulia akaendelea. “James alikuja na taarifa zilizotupelekea kuingia kwenye maombi. Alikwenda kumuona Danny, huko ndiko alikokutana na kina Zinda. Akayasikia mazungumzo yote kati ya Zinda, mama yake na Danny.” Mama G akamtizama Grace, alikuwa ameinama tu. Mama yake akaendelea. “Kwa mazungumzo yote yalivyokuwa yakiendelea, hakika wale watu wamebeba mambo mengi sana mioyoni mwao na wamekusudia kulipa kisasi vibaya sana. Wameanza kwa Danny.” Grace akanyanyua macho kumtizama mama yake. 

“Sasa turudi tokea mwanzo. Kipindi kile cha machafuko ya kuingiliwa na Malii, Danny akakasirika, nasikia alimtafuta Zinda akitaka au akimtambua kama ndio ndugu wa kweli. Nasikia kitu cha kwanza Zinda alichokifanya nikumrudisha Danny kwao. Lakini mama yake Zinda akamwakikishia kuwa ni kweli tumemloga, na kumchukulia bahati zake. Lazima yeye na watoto wake wapelekwe kwa mganga ili wamzindike au wamwague, vitu kama hivyo ili sisi tusimguse tena.” Man alikuwa kimya akisikiliza.

“Ndipo safari za Tabora zikaanza sasa. Danny, Sara na watoto, wakisindikizwa na Zinda, ili kwenda kuaguliwa na kuingizwa kwenye ukoo wa kina Zinda. Walipelekwa huko mara tatu. Wakafanyiwa dawa za kienyeji kwa huyo mganga. Sasa safari ya mwisho ambayo Danny alipelekwa na watoto, wanasema walifanyiwa utakaso, sijui! Lakini alipeleka kondoo, mbuzi na jogoo mwekundu kwa huyo mganga. Sasa unajua hayo ya kumwaga damu ni kama unaingizwa kwenye maagano fulani. Danny ameingizwa kwenye maagano ambayo yeye mwenyewe hayajui!” “Mara zote hizo inamaana alikuwa akienda na wanangu!?” Grace aliuliza huku akilia.

“Sio kwenda tu, kwenda kuaguliwa nao huko kwa mganga. Sasa safari hii  walimwambia aende yeye na watoto tu, bila Zinda ili akaunganishwe na ukoo wao. Nasikia ndio ilikuwa yakafanyike mambo ya matambiko. Kufanya kafara na mengineyo. Sasa bila kujijua, Danny ametoa watoto kafara. Hawa watu walikuwa wakimchezea tu Danny na kumloga yeye mwenyewe bila kujua.” Grace akazidi kulia kwa uchungu sana.

“James anasema wamezungumza mambo mengi sana. Wakimlaumu Danny kuwa alikuwa akimfanyia Zinda kama kumdhulumu haki yake. Kuwa amempokonya hata mchumba wake. Ambaye ni Nanaa, akampa Geb.” “Mpaka leo wanamlilia Nanaa!?” Grace akauliza. “Bado wana uchungu naye. Wakajidai wamesamehe, yameisha, kumbe bado. Kuna maswala ya kazi. Si unakumbuka ile kazi aliyonayo Danny ni James alimuunganisha?” “Nakumbuka. Tena tukamshukuru sana Mungu. Ulikuwa ukifunga na kuomba kwa ajili ya Danny apate kazi baada ya kumaliza chuo.” Grace akajibu huku akifuta machozi yaliyokuwa yakitoka kama mvua. “Ewaaa! Kumbe unakumbuka Grace?”

“Siwezi kusahau mama. Niliteseka na yule mtu, hakika sikujua kama mwisho wetu utakuwa mbaya hivi! Nakumbuka kila kitu mama yangu. Siwezi kusahau yale maisha ya wasiwasi niliyopita na Danny. Wewe na Geb mkitulisha kama watoto wa ndege! Hatukuwahi kupumzika na Danny. Mwanzo wetu mpaka leo hii bado ananiliza Danny! Amekuwa ni mwiba ambao sijui utanitoka lini! Unaniuma vibaya sana.” Grace aliendelea kulia. Man akamsogeza karibu. “Pole Grace. Pole sana.” Man alijaribu kumtuliza.

“Ehe mama!” Man akataka mama G aendelee. “Basi, nasikia baada ya James kuwatangazia marafiki kuwa kuna kazi, Zinda yeye ndio aliomba wakwanza. Lakini Geb alivyotusimulia ni kama wakashauriana aunganishwe Danny kwa kuwa wakati ule Danny hakuwa na kazi, na Zinda alikuwa nayo.” Grace akatulia kama anayevuta kumbukumbu. “Ni mambo mengi sana. Lakini kwa kifupi, wamebeba mambo mengi sana ambayo wamekusudia kulipa kisasi. Na wamemwambia mizimu ndio imemzuia kufika nyumbani kwao, kwa kuwa anamkosi mkali sana. Hawamtaki tena, na wamembakisha Danny ili kulipa ubaya wote waliomtendea Zinda. Sasa swali likawa kwa…” “Mwanangu Fili? Mungu wangu mama! Watammaliza mwanangu.” Grace akahamaki. Alimkata mama yake kwa haraka sana akiwa amepaniki.

“Subiri sasa. Tunaye simba wa kabila la Yuda, Grace. Usije sahau hata siku moja. Kumepigwa maombi ya nguvu hapa, hujawahi kuona Grace. Hatujawahi kuomba kama leo. Tulitubu kwa kumlilia Mungu akumbuke rehema kwenye maagano aliyoingia Danny. Tulivunja kila madhabahu iliyoshikilia majina yetu wote. Geb alijawa nguvu za Mungu mpaka mapepo lakamlipuka Fili.” “Mama!” “Alianza kutambaa kama nyoka. Ametapika vitu vyeusi sana. Akajichomoa kila kitu. Nesi mwenyewe alikimbia. Alikuwa amegeuza jicho kama anakata roho. Unamjua Geb hapendi kesi wala maneno mengi. Akaliamuru hilo pepo sijui mapepo, linyamaze na kumtoka Fili kwa haraka. Hapo hapo Fili akawekwa huru. Walikusudia kummaliza yule mtoto pia. Lini, hatujui. Lakini tumeomba Grace. Tumemlilia Mungu akukomboe wewe na uzao wako. Geb akaamuru hiyo hedhi iliyokuwa imeanza gafla, ikome na urejeshewe mzunguko wako kama kawaida.” “Basi ndio maana nikashangaa nimeamka mchana, hamna kitu. Damu imekauka na wakati ilikuwa ikimwagika isivyo kawaida ya siku zangu!” “Basi mshukuru Mungu. Amekukomboa.” Mama G akamgeukia Man.

“Man mwanangu. Najua umeingia kwenye ndoa ukakutana na misiba. Mimi sijui kiwango chako cha imani, na wala sijui ni umbali gani upo tayari kwenda na Grace. Lakini sisi wakati wote imani yetu ipo kwa Yesu. Hatujawahi kutishwa na shetani. Ameshatupitisha kwenye magumu mengi sana. Lakini hatuna nia wala hatuna mpango wakumuacha huyu Yesu. Ndio kimbilio letu pekee. Sina baba wala mama. Sisi na watoto wetu ndio ukoo umekamilika. Wakati wote Mungu amekuwa kimbilio letu. Nilimwambia Geb, na wewe nakushauri. Kama umekusudia kuwa na familia. Iwe Grace au mwanamke mwingine yeyote yule, magoti ndio itakuwa silaha pekee itakayokusaidia kushinda na kuweka ulinzi  kwa familia yako. Nikisema magoti, namaanisha piga goti haswa mbele za Mungu, mwambie unamwitaji akupe uongozi kwenye familia yako.”

“Awe mlinzi wako, ndipo utaishi kwa uhuru. Kwa kuwa shetani yupo na amepewa mamlaka yake na anatawala kwenye hii dunia. Nguvu zake sisi tumeziona sio kusimuliwa. Tumemuona akifanya kazi. Lakini Mungu ametutetea. Sisi wenyewe kwa maombi yetu. Hatujui kukimbilia kwa mchungaji wala kwa jirani, maana mambo mengine ni magumu hata kusikika kwa watu. Tunaishia kung’ang’ana na Mungu mpaka anatujibu.” Mama G akaendelea.

“Sina mpango wakumpokea tena Danny kwenye maisha yetu. Na nitahakikisha hatakuwa karibu na Fili. Sio leo wala kesho, hatarudi kwenye maisha yetu. Atabakia kuwa baba yake Fili kwa kuwa alitoka kwetu akiwa na akili zake timamu. Na alikataa kabisa kubadilika. Swala la hasira na kiburi nilishazungumza naye zaidi ya Grace ambavyo anaweza kujua. Nilishamshawishi tuombe maalumu kwa ajili ya hilo ili kama ni roho chafu zimtoke, lakini alisuasua. Hakuonyesha kutaka kubadilika. Nilikwambia kuwa Danny hakuwa mkwe tu, nilimuhesabu kama mtoto wangu. Kwa hiyo wakati mwingine nilimchukulia kama Geb na kumvumilia hata pale nilipomuona anamuonea na kumdhalilisha Grace. Ukimya huo na uvumilivu kwa Danny, ndio umeniletea makaburi mawili ya wajukuu ambao hata sijafaidi nao! Hakika hatarudi tena kwetu. Namuombea bila unafiki kuwa yaliyompata, yamsogeze karibu na Mungu, lakini si sisi.”

“Alimruhusu shetani amchezee yeye mwenyewe akiwa ameonja vipawa na karama za Mungu. Alituona kule tulikopitishwa na shetani na Mungu akitupigania, lakini akaamua kutoka kwa Mungu. Sasa sijui amefika umbali gani na shetani! Sijui amemkubalia kumtumikia kwa umbali gani! Siwezi kumruhusu tena Danny kuwa na familia yangu. Ila nawashauri wewe na Grace, mumpokee Yesu kwa upya. Shetani hachoki kujaribu. Fili tumemuombea na amewekwa huru. Yale aliyopanga shetani juu yake, wala hayatatimia. Pateni muda, mfikirie juu ya maisha yenu, lakini Yesu awe ndio msingi wenu.” Wakati wanamalizia, Geb naye akawa ndio anaingia hapo hospitalini.

Aliwaona wamekaa hapo, akasogea. Akamkuta dada yake ameinama pembeni ya mumewe analia. Akamsogelea. “Njoo G.” Akamshika mkono akasimama. Geb akamkumbatia. “Jipe muda. Nakuamini. Naamini ile nguvu ndani yako. Naamini ule uwezo Mungu alio kujalia. Kila kitu kitakuwa sawa. Nakuombea sana. Namuomba Roho mtakatifu awe msaada wako sasa hivi. Jaribu kutulia ili uweze kumsikia. Sisi wote tupo kwa ajili yako.” “Sijui hata kama naweza kuomba Geb. Mungu amenichukulia watoto wawili kwa pamoja! Tena kwa kifo kibaya cha maumivu makali sana. Hakika nimeumia. Najiuliza ni kipi kibaya hicho, nilichomtendea Mungu, mpaka kuniadhibu mimi kwa kiasi hicho!? Hakika Mungu amenitenda Geb. Nimeumia vibaya sana. Nafsi yangu imejeruhiwa vibaya sana. Sijui hata namsikiaje tena huyo Roho mtakatifu.”

“Mbaya zaidi nimechanganyikiwa Geb. Sijui chakufanya tena. Nilikuwa ni kama nimeshapa dira. Najua kila kitu. Kipi kinaanza, kipi kinafuata, lakini sasa hivi, sijui tena. Nimekosa hamu ya kila kitu. Ni kama gafla nimehamishwa kutoka sayari hii, nikapelekwa sayari nyingine. Nikiwa peke yangu na natakiwa niishi. Sijui chakufanya Geb. Nina majuto ambayo sijui kama yatakuja kuisha maishani.” Grace aliongea kwa uchungu sana, akilia. “Nashauri pata muda wakutosha na Man. Na naomba pia umsikilize. Sasa hivi wewe upo kwenye maumivu. Ni ngumu kutuliza mawazo. Huwezi kuwaza vizuri.” Hapo kidogo Man akafarijika.

“Niangalie G.” Grace akamtizama kaka yake. “Ujue siku nzima ya leo nilikuwa nikimuuliza Mungu, kwa nini uolewe tu na matatizo yaanze! Yaani hata fungate hujafurahia! Kwa nini anakuwa anamwingiza mtu kama Man kwenye matatizo ambayo hakustahili! Tuwe tu wawazi mama na Grace, hakuna mtu, au hata mimi nisingependa kuinginia kwenye ndoa ya namna hii. Nikasimama upande wa Man, nikamuuliza Mungu. Nikamlilia Mungu kwa ajili ya Grace. Ni kweli G, hastahili kupita hapa anapopita. Wote tunajua jinsi Grace alivyomwema. Amebeba wale watoto kwa shida sana. Maumivu na mateso. Hata kuzaa, amezaa kwa shida sana. Leo wameondoka wakiwa hata hajafaidi au hajawafurahia watoto wake! Nilifika ofisini nikajikuta nikipiga magoti pembeni ya meza yangu na kumlilia Mungu.” Geb akaendelea.

“Mimi sijui ni kwa nini iwe ni Man. Sijui kwa kuwa Mungu hakunijibu hilo. Lakini labda Mungu ameona kuwa ipo nguvu ndani ya Man, ya kukubeba sasa hivi katika hili. Inawezekana pengine ni kule alikopitishwa Man, kwenye maisha yake, ndio Mungu ameona yeye pekee ndiye anayeweza kukubeba kipindi hichi kigumu. Sijui Grace! Maana hawa watoto Mungu angeweza kuwachukua siku nyingine yeyote, lakini akaamua kuwachukua siku Man ameapa atasimama na wewe!” Geb akamtizama Man.

“Naomba unielewe vizuri Man. Tunampenda sana Grace.” “Hilo najua.” Man akajibu. “Hapana Man, hufahamu. Huyu Grace kwangu ni mkubwa, lakini kwangu na mama, ni kama unavyomuona Liv, yule binti yangu. Ndivyo alivyo Grace kwetu. Ndivyo tunavyomtizama. Hajawahi kukua kwetu na hatujawahi kumuona yupo tayari kuondoka kwenye maisha yetu. Hata leo ukiona kina hichi cha maji kwako ni kirefu sana, tutafurahi sana ukituachia Grace. Tutakupa baraka zote na tutakuaga kwa amani kabisa. Hata ukisema unaondoka kwa muda, ili ukapate muda wakufikiria ndipo urudi, basi pia tutaagana kwa amani tu, na bado tukabakia ndugu.” “Grace ni mke wangu, Geb.” Man aliongea bila paniki.

“Unaweza usielewe, au ukadhani nimechanganyikiwa. Lakini namuhitaji Grace sasa hivi, kuliko pengine wewe na yeye mwenyewe Grace angeweza kufikiria. Ukiniuliza kwa nini, mimi sijui! Lakini namuhitaji Grace. Mungu amenipa mimi. Kama ilivyo kwako, hata mimi sijui ni kwa nini Mungu amenipa Grace, na amenipa sasa hivi. Msinielewe vibaya jamani. Ila naomba niwe muwazi tu. Muda mfupi uliopita mama alisema Danny hatakuwepo kwenye maisha yenu, wala hataruhusu awe karibu na nyinyi au Fili, kwangu ni habari njema.” Kidogo wakacheka.

“Kweli. Binafsi nitapata muda wa kujenga familia yangu mimi na Grace tukiwa tumetulia kabisa. Hapatakuwa na vurugu. Tukitulia, tutakuwa tumetulia. Nimetoka kuzungumza na Grace leo, juu ya Fili. Ni kama Mungu ametupa sasa jukumu kamili na kutufungua macho kwenye maisha. Ana uwezo wa kutupa na kutupokonya wakati wowote. Fili amerudishwa kwetu kwa upendo tu. Hatuwezi kupuuza hilo. Nimepewa Grace kwa sababu maalumu. Hata mimi sijui iwe kwa nini Grace. Mungu amenifungamanisha na Grace, siwezi hata kuhema. Sijui kwa nini iwe yeye, tena kwa miaka yote hiyo! Sijui. Ila nampenda sana Grace. Sijuti kumuoa. Nipo hapa leo sio kwa sababu najitahidi au najificha kwa jamii kuwa itanionaje, ni kwa kuwa nataka kuwa karibu naye. Mimi namtaka Grace na kila kitu chake cha nyuma, nimempokea, ni wangu. Nashukuru Geb kwa kumwambia anisikilize. Maana ameshaanza kunifukuza.” Geb akamwangalia Grace.

“G!” “Naona namwingiza matatizoni Geb. Nimemkuta na maisha yake mazuri. Anaendelea na biashara zake. Ona sasa hivi. Ameingia tu kwenye ndoa, tayari mikosi.” “Nisikilize G, Mungu alijua kama unamuhitaji Man, ndio maana akamleta kwako. Mimi nimeishi maisha ya Man, naelewa anachojisikia. Na wewe ni shahidi. Maisha ya kutafuta pesa peke yake, na kuzungukwa na watu wanaokutazama wewe kama ATM, yanachosha Grace. Yupo hapa na wewe kwa kuwa anakuhitaji. Mpe nafasi ya kuwa mume muone mtafika wapi.” “Maisha ya Man hayapo hapa Dar, Geb. Sasa hivi nawahitaji wewe na mama. Unajua kipindi hichi ni lazima niwe na mama. Nitakufa bila wewe wala mama. Na ninajua mama hawezi kukuacha wewe. Naondokaje au naishije mbali na nyinyi?” Grace aliongea yaliyopo moyoni, hata Man akashangaa.

“Umemwambia hayo Man?” Geb akamuuliza. Grae akatingisha kichwa kukataa. “Inamaana hilo jambo la wapi mtaishi, bado hamjazungumzia!?” “Ndio ilikuwa nikamuulize kwenye fungate, maana mimi nilimuona ni kama ameshajua tutahamia Arusha. Na ilikuwa rahisi wakati ule kabla sijapoteza watoto. Hata mimi nikajiambia akinitaka nihamie Arusha, nitahama tu. Lakini naona ugumu kuacha makaburi ya wanangu. Naona ni kama nazidi kuwatelekeza.” Geb akavuta pumzi na kuzishusha taratibu. Akamvuta karibu Grace na kumkumbatia tena. Man alibaki kama amepigwa shoti ya umeme, mama G alijua wazi hilo ni tatizo. Ila alipoona Grace anakubali kufunga ndoa, akajua amekuza binti, amekubali kufunga ndoa na Man ili ahamie Arusha.

“Nikuulize swali G?” Grace akakubali kwa kutingisha kichwa. “Kuwa tu muwazi. Wewe utakuwa na amani kuishi na mimi na mama hapa Dar, halafu umuache mumeo Arusha peke yake?” Grace akanyamaza. “Eti G?” “Nitafanyaje Geb?” Grace akauliza. “Sijui. Lakini mimi nisingekubali kuishi mbali na Nanaa. Kwanza sivyo ndoa inavyotakiwa kuwa G. Utafungua milango mingi sana kwa shetani, tena bila sababu. Arusha ni karibu sana na Dar. Hata masaa mawili hayaishi kufika Arusha. Mimi na mama tupo na wewe hasa kipindi hiki kigumu. Na hata mama unajua hawezi kukuacha katika kipindi hiki kigumu. Kwa nini usisubiri Fili akaruhusiwa hapa hospitalini. Apone kabisa, ndipo mjipange na Man? Popote utakapokwenda, mama atakuwa na wewe. Safari hii nakuachia mama.” Grace akacheka.

“Kweli?” Grace akauliza huku akikausha machozi. “Kama Man atakukubalia lakini. Mimi nitakuachia mama, mpaka aone upo sawa, ndipo atarudi nyumbani. Ila bado nafikiri mnahitaji mapumziko yenu nyinyi wawili.” “Na Fili?” Grace akauliza. “Naona Liv anamuuguza vizuri.” Geb alijibu nakufanya wacheke. “Na alivyokazana. Kila mtu akiingia mpaka manesi anawaambia, ‘nampenda Fili’. Na kidole chake kile mdomoni, na tabasamu usoni.” Mama G akafanya wacheke tena. “Na mabusu ya kila saa.” Grace akaongeza. “Fili halalamiki tena. Akilalamika tu, busu.” Geb akaongeza nakufanya wacheke zaidi. 

“Sasa ndio nilikuwa natoa wazo, kama mtakubali lakini. Sasa hivi mtuachie Fili kwa muda. Mpaka atakaporudia hali yake ya kawaida. Mnaweza kurudi mapumzikoni kama mlivyopanga. Najua mkitulia, mtapata muda wakupanga mambo yenu vizuri. Mkirudi mtatuambia vile mlivyokubaliana. Sisi tuko na wewe G. Chochote utakachotaka, tutakusaidia. Usiogope. Muda na wakati wowote utakao nihitaji mimi nipo, na wewe unajua. Sawa?” Hapo kidogo Grace akapata nafuu.

“Na ninaomba niongezee kwenye swala la makaburi Grace. Naomba yale makaburi ya watoto yasikufunge. Sisi tunajua Fillius na Fillan walipo.” Grace akaanza kulia. “Tutayatunza kama kumbukumbu yetu sisi. Lakini sio kwa sababu eti kwa kuwa wapo pale. Mimi naishi na nyinyi, lakini kaburi la baba yenu lipo Kinondoni. Tumejengea vizuri. Na tukienda, tunaenda kuangalia na kusafisha, sio kwa kuwa yupo pale. Ni kumbukumbu yetu tu. Sijui kama unanielewa?” Grace akatingisha kichwa.

“Muda ukifika, tutajengea yale makaburi vizuri, na tutayatunza daima. Ila usifungwe na yale makaburi. Huko nako utafungua milango mingi sana. Hutakaa utoke hapo. Utachukua muda mrefu sana hapo, ukilinda yale makaburi. Lazima maisha yaendelee.” Mama G, huwa ni muwazi sana kwa wanae. “Umemuelewa mama?” Grace akatingisha kichwa huku akilia. “Pole sana G. Pole sana. Mungu atakuvusha hapo.” “Hakika nimeumia Geb. Nimeumia sana. Ila nashukuru kwa kuwa na mimi sasa hivi. Angalau mmenisaidia kimawazo. Wasiwasi umepungua. Ni kweli nilishaanza kuona uzito wakuondoka na kuacha yale makaburi.”

“Nataka wasiwasi uishe G. Nataka utulie kabisa. Najua sasa hivi unauchungu wa watoto, lakini usisahau faraja Mungu aliyokutumia. Usisahau pole ya Mungu kwako, ukazidi kuteseka ukifikiri Mungu amekuacha. Man, ndio pole yako kutoka kwa Mungu kwa sasa. Ndio faraja pekee Mungu aliyokutumia, kukufariji katika kipindi hiki. Usije ukasahau hilo na kuendelea kuumia. Huwezi kubadilisha ya nyuma, lakini unao uwezo wa kutengeneza mbele. Pokea baraka za sasa, omboleza ukipokea upendo wa watu unao kuzunguka. Hata katika hili, Mungu atakupitisha tu.” Geb akaendelea taratibu.

“Yale aliyokusudia kukuangamiza nayo shetani, Mungu atakutumia kicheko siku moja. Sijui ni kwa nini imetokea, lakini mimi na wewe tumepita kugumu sana. Na bado Mungu akatuonyesha yupo na sisi.” Geb aliongea na dada yake kwa upole.

“Si kwambii kuwa pengo la Fillius na Fillan kama litakuja kuzibika, lakini kwani hivi leo mimi na wewe tulijua tutafika hapa siku ile tunamzika baba?”  Grace akaanza kulia tena na kutingisha kichwa. “Tuliumia sana. Nakumbuka uliumia sana G. Ukawa unasema unahisi na wewe utakufa. Lakini leo tumesimama hapa. Pengo la baba halikuwahi kuzibwa, lakini Mungu hakuwahi kutuacha. Hata sasa Mungu atakusaidia tu. Na hapa pia atakutumia faraja, na utavuka tu.” Grace akatingisha kichwa kukubali. Geb akambusu kichwani.

“Asante Geb.” Grace akashukuru. “Asante hii ni ya kukupa mama?” Grace akacheka huku anafuta machozi. “Ulijuaje?”  Grace akauliza. “Man mwanangu, pole.” “Pole na wewe mama.” “Naona pole yangu iwe kubwa. Maana umesikia hapa wanavyonigawa bila hata kuulizwa!” Wote wakacheka.

“Yaani wanafanya maisha yangu kama yao vile! Vile wanavyotaka wao wawili ndivyo hivyo hivyo mimi natakiwa nikubali tu.” “Hata kwetu utakuwa na wakati mzuri mama.” Man akaongeza. “Nashukuru mwanangu. Akitulia tu huyo. Akili zake zikiwa sawa, tutakuachia moja kwa moja.” Man akacheka. “Wala hamna shida. Muda na wakati wowote, sisi pia tunakuhitaji. Tena ndio vizuri na mimi nitapata nafasi yakumjua Mungu kwa karibu na…” Wakamuona Nanaa anatoka na Magesa. Magesa alikuwa kwenye walker yake anatembea kama anakimbia. Wakacheka.

          “Vipi?” Geb akamuuliza. “Nimemletea bibi yake. Wala sikujua kama na wewe upo!” “Amefanyaje tena?” Geb akamkimbilia na kukanyaga ile walker ya Magesa ili asimame. Akaanza kucheka. “Fujo! Fundi wa zile mashine za mle ndani, ni yeye. Daktari, ni yeye. Nesi ni yeye. Kila kitu! Anataka kuchomoa zile nyaya pale na kumvuta Fili pale kitandani. Sasa sijui anataka akakae pale kitandani kama Liv? Mate tu!” Wote walikuwa wakicheka. “Eti Magesa?” Geb akamtoa pale kwenye Walker ili ambusu. “Hashikiki mkononi, anataka kufanya kila kitu!” Nanaa akaongeza. “Mimi naona mbaki naye tu hapa hapa nje, mimi nirudi ndani kwa Fili na Liv. Nimemuachia nesi mara moja.” “Na mimi nakuja sasa hivi.” “Sawa.” Nanaa alimjibu Geb nakurudi ndani.

Grace akaguna. “Hivi Nanaa ataweza kukaa mbali na mama kweli?”  “Jasho litamtoka.” Mama G akajibu nakucheka huku akimfikiria Nanaa. “Lakini hana shida. Nanaa ni muelewa sana. Ilimradi ajue ni kwa faida yako, hatakuwa na shida.” Wakazungumza kidogo, Geb akaingia ndani.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya siku tatu Fili akaruhusiwa akiwa ananafuu kubwa sana. Geb akaenda kulipia kila kitu, wakakusanya vitu. Wakatoka. Walikuwa Geb, Nanaa, Grace, na Man. Mama G alibaki nyumbani akiandaa chakula, kwa kuwa alijua wataruhusiwa siku hiyo.

Hasidi Haachi Asili.

Wakati wanatoka kwenye hilo jengo, wakamkuta Gozi na Zinda wamesimama kama wanawasubiria. “Habari zenu?” Wakasalimia, lakini wote walinyamaza. Geb alikuwa amembeba Fili. “Nina shida ya kuongea na Nanaa.” Gozi akaanza. “Nakusikiliza.” “Tunaweza kuzungumza pembeni?” “Unamaana mbali na mume wangu?” Nanaa akauliza. “Nimetumwa kwako. Ni ujumbe wako wewe peke yako. Nafikiri ingekuwa vizuri tuzungumze pembeni.” “Huyo aliyekutuma           hajui   kama nimeolewa?” Nanaa akauliza. Gozi akamwangalia Zinda.

“Msitupotezee muda. Huyu ni Geb, mume wangu. Huyu ni Grace na mume wake. Grace wifi yangu lakini pia ndio waliotusimamia harusi. Hakuna utakachoongea hapa kikawa cha hatari wao kusikia. Ukitaka kuongea, ongea. Kama huwezi, utupishe sisi tuendelee na mambo mengine.” “Ni Malii!” Gozi akaongeza. “Subiri kwanza. Kabla hujaanza kuongea.” Nanaa akachukua simu yake kwenye pochi. Akabonyeza vitu kadhaa. 

Kisha akamgeukia Gozi. “Ehe! Nakusikiliza.” Nanaa akamtizama. “Nimetumwa kwako na Malii, ndio nilikuwa nataka tuzungumze pembeni.” “Wewe unawasiliana na Malii?” Nanaa akamuuliza, Geb asielewe ni nini anafanya. “Ndiyo. Na ndio amenituma kwako tuzungumze. Njoo basi pembeni.” “Nisikilize Gozi. Wakati Malii ananibaka, wewe ulikuwepo na wote hawa walikuwepo, kasoro huyu mume wa Grace na huyo Zinda hapo. Lakini wote uliwafikishia ujumbe wa kubakwa kwangu. Hakuna asiyejua kama nilibakwa na Malii. Si ni kweli?” “Ndiyo, lakini..” “Lakini nini cha ajabu? Kilichobadilika ni kwamba sasa hivi nimeolewa. Kwani hujamwambia hilo Malii? Maana kazi yako kubwa hapa mjini ni kuhamisha maneno kutoka nyumba moja hadi nyingine. Kutoka kwenye uhusiano huu kwenda kwenye uhusiano ule. Kutoka kwa huyu kwenda kwa huyu. Kwa hiyo kwa uhakika hata hili la kuolewa na Geb, ninajua umemwambia.” “Lakini yeye anataka mtoto wake.” Kila mtu akashituka, lakini si Nanaa. 

“Kwa hiyo pia ulimwambia kuwa umenipima na umekuta nina mimba yake?” “Sikiliza Nanaa. Kila mtu anajua baada tu ya kubwakwa, wakina Magesa walikufukuza. Kwa hiyo sio siri kuwa huyo mtoto sio wa Geb. Acha kumnyima Malii haki yake ya kuwa baba.” “Kwa hiyo wewe sasa hivi ndio unayegombania haki za Malii?” Nanaa akahoji.

“Hata kama jamaa amekosea, lakini anahaki ya mtoto wake.” “Hayo unaongea wewe au Malii mwenyewe?” “Anasema ameona umesoma jumbe zake. Alikuomba msamaha, lakini hujibu. Anachoshangaaa umeamua kwenda kumuuza mtoto wake kwa Geb.” “Kwa nini asinifuate yeye mwenyewe tuzungumze?” Kimya. “Wewe si umemuhakikishia mtoto ni wake? Sasa kwa nini asije mwenyewe kumdai mtoto wake kutoka kwangu na Geb?” “Yeye anakutambua wewe, hamtambui Geb.” “Basi. Kwa kuwa  sasa hivi tumetoka hapa hospitalini. Kila mtu amechoka, naomba jioni uje nyumbani tuzungumze vizuri.” Geb alishituka sana. Akamtizama Nanaa.

“Jamaa ametuwekea ‘restraining order’. Hataki tufike karibu na kwake. Si umeona hata jinsi alivyokuangalia?” “Si umesema unataarifa kuwa nimeolewa na Geb?” Nanaa akamuuliza. Kimya. “Unajua kama na mimi sasa hivi ninaitwa Nanaa Magesa?” Kimya. “Kwa kifupi tu, pale kwa Geb pia ni kwangu. Yaani nina amri yakualika mtu yeyote ninayemtaka mimi. Kama umetumwa habari za mtoto wa Malii, njoo nyumbani kwangu. Nitakujibu maswali yote uliyotumwa.” “Unauhakika sitaingia matatizoni?” Gozi akauliza. “Mjumbe anauwawa?” Nanaa akamuuliza.

“Nataka tu uhakika wa usalama wangu.”“Basi kwa usalama wako, kamuombe kaka James, uje naye. Utapita pale getini bila shida.” “Sidhani kama James atakubali.” Gozi akajibu. “Mimi nitazungumza naye hawezi kukukatalia. Wewe niambie muda utakao taka kuja jioni ili tuwekane sawa tukiwa tumetulia, tuache kuviziana barabarani.” “Kama kwenye saa moja hivi.” “Sawa.” Nanaa akajibu. “Twendeni.” Nanaa akarudisha simu yake kwenye pochi.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Geb alikuwa ameumia sana. Alinyamaza kimya, mpaka Grace alijua kama kaka yake aliumia. Hakuna aliyekuwa amemuongelesha mwenzake. Wote waliingia kwenye gari. Nanaa akatoa simu akampigia simu James. Akamuelezea kila kitu. “Naomba atakapokuomba uwalete nyumbani, usikatae kaka yangu. Tafadhali sana.” “Umezungumza na Geb? Sitaki matatizo Nanaa. Hawa watu ni washirikina na waharibifu sana. Hakuna sehemu wanayoingia wakaacha salama.” “Ndio nataka kuweka kikomo kaka. Hata mimi nimechoka.” “Kikomo na kina Gozi?” James akauliza. “Wewe walete au mlete hiyo jioni. Utaelewa tu.” James akanyamaza. “Kaka!” “Sawa Nanaa. Lakini nasita sana.” “Usiwe na wasiwasi kaka yangu. Naomba uwalete tu.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

v  Grace bado yupo kwenye maombolezo. Ndio wameruhusiwa na mtoto akiwa salama kiroho na kimwili. Ushauri ni warudi kwenye fungate, ili kupumzika. Ni kama ameshapata suluhu kubwa sana juu ya hatima yake na Man. Kazi kwake yeye.

-      Ni ipi Hukumu ya Danny kutoka kwa Grace?

v  Malii anataka mtoto wake!

Isivyo kawaida, Nanaa anaalika adui wakubwa sana wa Magesa nyumbani kwao! Zinda ndiye anayesadikika kuua watoto wa Grace na Danny. Leo Nanaa anawakaribisha bila hata kuuliza! Kumsogeza tena karibu na Fili waliyemtoa mapepo si jambo hata mmoja wao analotamani! Imemuuma sana Geb na kushangaza kila aliyesikia. James, Grace na Man. 

-      Je, yale aliyosema Man yanatimia kwa Geb? Kuchuma mali kwa miaka yooote hiyo, leo Nanaa ameolewa hata mwezi haujaisha, anatangazia adui wa Magesa na yeye ni mmiliki mwenza wa Geb!

-      Nini nia ya Nanaa? Amesema ndio anataka kuweka kikomo.

-      Kwa nani?

-      Je, ndio Nanaa naye anafungua makucha yake?Jino kwa Jino!’  Kwa nani?

Endelea kusoma…..

 

 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment