Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! - Sehemu ya 64. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! - Sehemu ya 64.

 Msiba Mzito.

Geb aliendelea kumuhoji James akionekana na wasiwasi sana. “Umesema ni Grace?” “Hapana. Nisingeweza kumtafuta Grace mwenyewe mpaka nizungumze na wewe!” “Ni Danny?” Geb aliendelea kuhoji. “Danny alinipigia simu kama kwenye saa nane hivi, akaniambia nimfuate maeneo karibia na Picha ya Ndege, Kibaha. Alikuwa akilia sana. Nikamuuliza ni nini? Akasema wamepata ajali mbaya sana.” “Mungu wangu!” Mama G, akasikika. “Mtu niliyemfikiria kwa haraka ni wewe. Nikakupigia simu wakati natoka nyumbani, hapakuwa na jibu. Simu imefungwa.” James akasimama.

“Naomba niambie kama wajukuu zangu hawajambo James!” Mama G alishapaniki. “Aiseee! Ni mbaya Geb. Mbaya sana. Mtoto mmoja amekanyagwa na gari yao, amekuwa kama chapati. Mwingine kioo kimeingia jicho la mbele imetokea kisogoni. Uwii Mungu wangu nirehemu.” James akaanza kulia mwenyewe. Mama G alianza kupiga kelele kwa sauti mpaka walinzi wawili wakaja wakikimbia. Geb akasimama. “Mungu turehemu!” “Mtoto wa tatu ndiye aliyekuwa amefunga mkanda, yeye amevunjika mkono tu. Danny amevunjika miguu, Eeeh Mungu wangu!” James alifikicha macho.

“Ni mbaya Mungu. Mungu ni mbaya sanaa! Uwiiii! Mleta habari ndiye aliyekuwa akilia hivyo. “Wako wapi?” Geb akauliza. “Tokea mchana, nilikuwa nikihangaika kukusanya mwili wa yule aliyekuwa amepondwa. Wamechukuliwa, mili yao ipo hospitali ya Kibaha. Danny na Fili nimewakimbiza Kibaha hospitali. Sara hakuumia. Lakini tulipofika Muhimbili, amenitoroka. Sijamuona tena. Lakini Danny nimemuacha chumba cha upasuaji. Fili …..” James akashindwa kuendelea. Mikono kichwani, machozi na kamasi vikimtoka kama mvua.

“Binadamu sisi si kitu mama!” James alizidi kulia kwa sauti kama mama G. “Yule mtoto anamwita mama yake kama aliyechanganyikiwa. Alikuwa anaongea kuanzia sehemu ya kwenye tukio mpaka  hospitalini. Anaongea kwa kueleza kila kitu. Daktari anasema yupo kwenye mshituko. Aliwaona wadogo zake wakiwa hawajafunga mkanda. Anasema baba yake na Sara walikuwa wakigombana. Yeye akamwita baba yake kumwambia watoto hawajafungwa mkanda. Anasema baba yake hakumsikia. Akasema kwa kuwa mama yake alimwambia lazima afunge mkanda, akatoka ili kuwafunga wadogo zake. Sara alipomuona ameshuka kwenye kiti, akamsemea kwa baba yake. Danny akamgeukia na kumpiga makofi huku akiendesha na kumlazimisha kurudi kukaa kwenye kiti chake. Fili anasema aliporudi kukaa, akaendelea kumpiga lakini yeye akamsisitizia mama yake alimwambia lazima ahakikishe wadogo zake wamefungwa mkanda ndio alikuwa anawafunga. Anasema baba yake akageuka nyuma na kumpiga kofi jingine la miguu, akamwambia alimuonya asiwe anamjibu. Anasema akarudi kuendelea kugombana na Sara. Akampiga Sara kibao cha uso, anasema yeye Sara hakukubali. Akamrudishia cha usoni tena kwenye macho. Ndipo ajali ikatokea. Mtoto wa kwanza akarushwa kutoka kwenye kiti mpaka kioo cha mbele kabisa. Akanasa pale sababu kilishapasuka. Akaninginia kwenye kioo. Ndiye huyo kiliingia jichoni mpaka utosini. Huyo mwingine yeye ndio alirushwa nje. Inaonekana ile gari ilipinduka mara kadhaa. Maana nilikuta mwili wa yule mtoto umesambaa mbali kidogo ya lile gari. Fili, Danny na Sara kwa kuwa wao walikuwa wamefunga mikanda walinasa ndani ya gari.” Wakashangaa kimya.

Geb kugeuka, mama yake alishazimia. Juhudi za huduma ya kwanza zikaanza. Akafungua macho. Lakini hakuwa akiweza hata kujigusa. Wakahisi amepata stroke. Geb akambeba mama yake kumwingiza kwenye gari ili kumpeleka hospitalini. James akamgeukia Nanaa. “Nilazima, uende kwa yule mtoto. Anahali mbaya sana.” Nanaa akakimbilia chumbani akachukua pochi na simu, akatoka mpaka alipokuwa amelala Tere. Akamwachia maagizo kuwa abaki na watoto, yeye anakimbilia hospitalini Kibaha. Bila maswali mengi akiwa usingizini, Tere akakubali. Geb alishaondoka na mama yake akiendesha kwa kasi kuwahi hospitalini. Ikabidi James ndio ampeleke Nanaa alipo Fili.

Fili Aeleza Yote .

Kufika saa mbili usiku vyombo vya habari vilishaanza kutangaza ajali mbaya ya Danny na familia yake. Alipofika pale akaona hali ya yule mtoto, Nanaa akajua anahitaji ungalizi wakaribu zaidi na afungiwe mahali. Watu walikuwa wamemjalia na yeye anazungumza bila hata kuulizwa. Alikuwa kama anaweweseka. Alikuwa peke yake bila ndugu, wauguzi wakihudumia watu wengine walionekana na hali mbaya kuliko Fili aliyeweza kutoa habari ya kilichokuwa kikiendelea kwenye gari mpaka kupata ajali.

Watu wengine walimuhoji maswali mengine hata yasiyohusu ile ajali. Walioweza kumpiga picha, walimpiga na kumrikodi. Mpaka James na Nanaa wanawasili pale, familia hiyo ya Danny ilikuwa ikijulikana ndani na nje. Walimjua Grace, Sara, Danny na mume mpya wa Grace. Nanaa aliumia sana. Akajua mpaka hapo Fili atakuwa kwenye mitandao yote ya kijamii. Alikuwa amewekwa kati, anahojiwa tu bila hata kupewa huduma yeyote. Aliambiwa anasubiriwa zamu yake.

Nanaa akaamua kumpigia simu Jeri, ili afike hapo awasaidie usafiri wa kumtoa Fili pale kwa haraka na kumuwahisha kwenye hospitali ya binafsi. Kama kawaida ya Jeri, hakuchelewa. Alitokea nyumbani kwake na gari yake. Akamchukua Nanaa na Fili kutoka hapo hospitalini Kibaha akawakimbiza kwenye hospitali ya binafsi jijini walipozoea kutibiwa. Vipimo vingine kwa haraka vikaanza chini ya uangalizi wa Nanaa. Fili alivunjika bega na karibu na kiungio cha kiganja, mkono wa kushoto. Alianza kusimulia tena kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Bila kuulizwa. Alipomaliza akaanza tena. Alisimulia tena na tena.

Nanaa akabaki amemkumbatia. Hakujua ule ujasiri alipata wapi. Hakutoa chozi hata moja. Alibaki akimbembeleza tu Fili. Ikabidi amuombe daktari hata achomwe sindano ya usingizi ili alale. Maana alikua akiongea sana. Na mbaya zaidi muda wote James alipokuwa akisaidia kumtoa Danny, baba yake kwenye gari, Fili alikuwa akiwaona wadogo zake vile walivyoharibika. James hakuwa na kitu cha kuwafunika. Kwa hiyo miili yao ilikuwa wazi tu. Fili akiingalia.

Baada ya Fili kulala, akampigia simu Geb, hakuwa hewani. Akakumbuka alikuwa akichaji simu chumbani, na aliondoka kwa haraka kumuwahisha mama yake hospitalini. Hakuna aliyejua alipo. Alimuacha kaka yake James hospitalini Kibaha na yeye akishugulikia kuhamishwa kwa Danny katika hospitali ya Muhimbili.

~~~~~~~~~~~~~~

Danny alipotolewa chumba cha upasuaji, akapata kitanda, James alipohakikisha yupo sawa, ndipo akaondoka kumfuata Nanaa kwenye hiyo hospitali aliyomuhamishia Fili. Ilishakuwa saa sita usiku. “Nenda kapumzike kaka.” “Siwezi Nanaa. Nimeona na kufanya vitu vya kutisha sana leo. Wanadamu sisi si kitu Nanaa, mdogo wangu! Hii mili huwa inatudanganya sana. Nipo kama nimepigwa na butwaa!” “Pole. Kwa jinsi anavyosimulia Fili! Kweli inatisha.”

“Huyu mtoto sijui maisha yake yatakuja kuwaje! Ameona mambo ya ajabu na yakutisha sana leo.” “Mungu atamsaidia tu. Nimemuomba dokta amchome sindano ya usingizi. Nimemtoa pale bado aliendelea kusimulia. Amefika hapa, akaendelea kusimulia tena. Hapa napo wauguzi wote na wagonjwa tuliowakuta pale mapokezi wameshajua kila kitu. Ila nimewaonya wasimpige picha wala kumuhoji chochote zaidi ya kumpa pole. Hata hiki chumba huku mwisho nimekiomba maalumu. Nimekataa watu wengi wasije humu ndani. Na nikaomba tupewe nesi mmoja tu. Na yeye asiwe anaingia mara kwa mara ili asimtibue. Nataka akili zake zitulie kidogo. Nafikiri akiona watu ndio anakuwa kama anaweweseka zaidi. Yupo kwenye mshituko mkali sana.” “Daah! Sijui itakuaje!” James akabaki bado na mshituko mkali.

~~~~~~~~~~~~~~

Walikesha hapo na Nanaa mpaka asubuhi. Hakuna aliyelala. Ilipofika saa 11 asubuhi Nanaa akaona tumbo la Fili linajaa. Akamwita nesi. “Tumbo la huyu mtoto linajaa. Naomba niitie daktari.” Akaitwa. Daktari alipombonyeza, akaagiza apelekwe kwenye Ultrasound kwa haraka, wakagundua anavuja damu kwa ndani. Ikabidi akimbizwe chumba cha upasuji kwa haraka.

Ilipofika saa moja asubuhi Geb akampigia simu Nanaa. Nanaa akamuelezea kila kitu. Akamwambia na wao ndio wanarudi nyumbani. Mama yake alitaka kupata stroke, lakini amepewa dawa na kuamriwa apumzike. “Nakuja sasa hivi.” Geb akakata. Alimtegemea amkute Nanaa yupo hoi kwa kulia, lakini akamkuta nje ya chumba cha upasuji wakisubiria yeye na James. “Vipi?” “Ndio tunasubiri. Vipi mama?” “Nimemuacha amelala.” Wakabaki kimya kwa muda.

“Geb! Lazima umtafute Grace. Wale watoto wameharibika sana. Kule hospitalini wameniambia lazima nikawachukue leo. Wameharibika kiasi ya kwamba hawana jinsi yakuwatunza pale kwenye ile hospitali. Lasivyo watawatupa kama takataka wakati wanatakiwa mazishi mazuri. Yule mmoja imebidi kumkusanya na kumuweka kwenye mfuko wa plastiki. Na wewe unaijua plastiki. Ikishika joto inazidi kuharibu.” Geb akafunika uso. Nanaa akamuona analia. Nanaa akamuwekea mkono mgongoni. Alilia Geb, mpaka akasimama na kuondoka pale.

~~~~~~~~~~~~~~

Yeye na Grace ndio walikuwa wakijenga familia au ukoo wao. Mtoto wa Grace ni kama wa Geb. Na wa Geb ni wa Grace. Hawakuwa na bibi wala babu. Kila mtoto aliyekuwa akiongezeka kwao, ilikuwa ni zawadi ya thamani sana kwao. Ndugu wa upande wa baba walishawakana tokea uhai wa baba yao. Hawakutaka hata kuwaona wao na mama yao. Mama yao alikuwa adui wakupitiliza kwa upande wao. Kwanza upande wa baba yake hawakuwa na ukoo mkubwa pia. Lakini wale wachache waliposikia kilichotokea kwa Magesa na mkewe wa kwanza, walimlaumu sana Oliva. Walisema yeye ndiye aliyeharibu maisha ya Magesa na kumsababishia maisha mabaya mpaka kifo chake.

Kina Geb waliitwa watoto haramu na wana mkosi. Hakuna aliyetaka hata kuwaona. Matatizo ya Magesa yalianza pale mama G alipokuja kwenye maisha yake. Yule Mzee alikuwa na ndoa ambayo haikuwahi hata kusikika kama inamatatizo ila neema ya utajiri. Alijulikana kama Mzee aliyebarikiwa binti wazuri na mke mchapakazi. Walisaidiana bega kwa bega kutafuta mali. Kwa kifupi hapakuwahi kusikika tatizo kwa Magesa mpaka alipokuja Oliva, mama G. Walimtambua kama mvurugaji.

Watoto wa Magesa waliwakimbia wazazi wao, na hawakuwahi kurudi tena nchini. Mama yao ndio alikuwa yatima aliyeokotwa nje ya kanisa. Hapakuwa na jinsi hata yakujua alitokea wapi au ndugu zake ni kina nani.  Padre aliyewaokota yeye na pacha mwenzie,  na yeye akaona amejishindia mapacha hao ambaye mmoja alikufa. Akamtunza mama G, mpaka kifo chake. Oliva au mama G, alitoroka huko kwa masista alipokuwa ameachwa na yule padre. Hakuwahi kurudi tena.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda Geb akarudi. “Nimewasiliana na hospitali ya Kibaha, nimewaambia nitakwenda kuwachukua baadaye. Nataka kumsubiria Fili atoke chumba cha upasuaji kwanza, angalau nimsalimie.” “Pole mume wangu. Pole sana.” Geb akamshika mkono nakunyamaza. Walikaa pale zaidi ya masaa mawili tena. Ndipo daktari akatoka. Aliwaambia walifanikiwa kusimamisha ile damu. Upasuaji ulienda vizuri, ila ilikuwa ni operation kubwa kwa Fili. Atahitajika uangalizi wa karibu wa madaktari ili kuhakikisha amepona kabisa. Bega lile liliumia sana. Nalo litahitajika mazoezi yakutosha ili kuhakikisha mkono unarudia matumizi yake kama zamani. Akawaambia baada ya muda atatolewa hapo.

Fili akatolewa chumba cha upasuji, Geb akasimama yeye wa kwanza akamsogelea. “Pole Fili.” “Asante.” Wakamsindikiza mpaka chumbani kwake. “Unajisikiaje? Unamaumivu?” Geb akamuuliza tena. “Sio kama kina Fillius. Unajua Fillius yeye amepondeka kabisa anko! Anko James amemuona. Amemuweka kwenye mfuko. Halafu Fillan yeye amekatika shingo. Lakini sio yote. Kioo kimoja kiliingia kwenye jicho kikatoka nje huku kwenye kisogo, na kingine ndio hicho kilimkata shingo. Nilimwambia dad tuwafunge mkanda. Akaniambia niache kelele, yeye akaendelea kugombana na Sara huku anaendesha.”

“Baadaye nikakumbuka mama alisema nisikae kama watoto hawajafunga mkanda, lazima nihakikishe wamefunga mkanda. Nikatoka kwenye kiti changu ili niwafunge. Sara akaniona kabla sijawafunga. Akanisemea kwa dad, dad akageuka nakuanza kunipiga nakuniambia nirudi kukaa, mimi sio mtoto msikivu. Situlii. Nikawaambia watoto hawajafunga mkanda. Dad akanipiga tena hapa.” Akataka kuonyeshea kwenye mguu akashindwa.

“Aaaaa!” Fili akalia maumivu. “Usihangaike Fili, umeumia mkono. Pumzika tu. Tutaongea baadaye.” Geb alijaribu kumtuliza. “Lakini anko, dad angenisikiliza watoto wasingeumia vile. Hakutaka kunisikiliza wakaendelea kupigana na Sara mpaka watoto wakaumia. Unafikiri mama Fili atanilaumi mimi sijawafunga watoto mkanda?” Kila mtu alimuhurumia Fili. “Nisikilize Fili. Wewe ni mtoto mzuri sana. Ndio maana ulimkumbusha dad. Ni dad ndio alisahau kufunga watoto mkanda.” “Kwa hiyo sio kosa langu?” Fili akamuuliza Geb, anko wake. “Hata kidogo. Kwanza atakupongeza. Hata mimi nakupongeza kwa kufunga mkanda. Wewe ni mtoto msikivu sana.” Fili akatulia kidogo.

“Sara amesema mama yetu hatutaki tena.” Fili akaanza upya. “Hapana. Wewe si unakumbuka juzi ulikuwa na mama Fili?” Fili akafikiria. “Atakuja kuniona?” Fili akamuliza tena. “Amesafiri. Lakini akirudi atakuja hapa ili awe na wewe.”  Akatulia kidogo kisha akaendelea. “Fillius yeye amepondeka sana. Muulize anko James. Alimuweka kwenye mfuko. Nilimwambia dad tuwafunge mkanda lakini akanipiga…” Nanaa akaona atoke akamwite daktari ili wamchome tena sindano ya usingizi apumzike. Ndio alitoka chumba cha upasuaji lakini alishindwa kutulia. Bado mawazo yalikuwa yakimjia nakumsumbua sana. Alipolala, Geb na James wakaondoka kushugulikia miili ya hao watoto wawili.

Huko Kwa Grace & Man.

Grace na Man walitoka ukumbini mara baada ya harusi yao. Lakini kabla hawajaondoka Grace alipata muda wakutosha na watoto wake nje ya ukumbi huo. Walimlilia sana mama yao. Nusura Grace aahirishe fungate. Akaingia nao wote kwenye gari ili kuzungumza nao. Man naye akaingia ndani ya gari. Aliwaaga kwa kuwaambia baba yao atasafiri nao kesho yake. Lakini hiyo itakuwa safari ya mwisho. Aliwaambia siku watakayorudishwa na baba yao, watamkuta yeye na Man wakiwasubiria nyumbani. Aliwaahidi wakirudi safari hiyo atakuwa nao, hawatatengana tena.

Dada aliyekuwa akiwatunza wale watoto, Mama G na Geb ndio waliokuwa hapo nje wakimuaga Grace wakiwa na hao watoto. Nanaa na James walibaki ndani na Liv na Magesa waliokuwa wamelala. Man alimsaidia kuzungumza nao mpaka watoto wote wakatulia. Aliwakumbatia na kuwabusu wanae ndipo akaondoka wakiwa wote wametulia.

Grace na Man wakaelekea kwenye hoteli hiyo ambayo wangepumzika kwa usiku huo, halafu wasafiri kwenda mapumzikoni mpaka siku ya alhamisi. Ijumaa wawepo hapo jijini kuchukua watoto wa Grace, maisha yaendelee. Ulikuwa usiku wa namna yake kwa Man na Grace. Zilijaa shukurani na mahaba ya namna yake. Wote walikuwa wanaingia kwenye ndoa kwa mara ya pili. Lakini safari hii waliingia kwenye ndoa wakiwa wamejawa furaha sana. Yalifanywa mapenzi ya jinsia yake. Man alikuwa amejiandaa usiku huo maalumu kwa ajili ya Grace. Kiukweli alimtendea haki Grace. Kwanza alikuwa na hamu naye. Walitengana kwa muda. Man alikuwa jijini Arusha akiweka sawa mambo ya kazini, Grace alikuwa Dar akijiandaa kwa harusi.

“Nakupenda Man.” “Nahisi mimi zaidi.” Grace akacheka. “Uzuri ni kwamba, hakuna kutengana tena.” “Ukinichoka?” “Unakumbuka kiapo changu nilichokuapia kanisani?” Grace akacheka huku akifurahia. “Uliniahidi kunipenda daima. Hata nikikuudhi, umeniahidi utanipenda zaidi. Uliniahidi kunipenda hata katika siku ambazo hutajisikia kunipenda. Umeniahidi utanifikiria mimi zaidi kwa kile ninachotaka sio kile unachotaka wewe kwa kuwa unaniamini. Umenihidi utaniheshimu na kuniunga mkono kwenye maamuzi yangu.” “Bado hujamaliza.” “Naendelea Man.” “Mmh!” Grace akacheka kidogo, kisha akaendelea.

Umeniahidi kusimama na mimi katika kila hali, hata iweje. Umeniahidi utakuwa na mimi mpaka uzee wetu.” “Kweli ulikuwa ukisikiliza. Na ujue nimemaanisha kila neno. Usifikiri ni maneno niliyotamka ili kukufurahisha tu au kuwavutia watu!” “Najua Man. Namuomba Mungu atusaidie.” “Ameshatusaidia Grace. Naamini tutakuwa na ndoa nzuri sana.” Grace akafikiria.

Unapenda nikuzalie watoto wa ngapi?” Man alicheka sana. “Unacheka nini sasa?” “Nilikuwa najibaraguza kwa muda mrefu kweli!  Nikashindwa hata kugusia.” “Kwa nini?” “Niliona bado hujatulia na hao watatu. Nikaona sitakuwa muungwana nikianzisha swala la watoto tena.” Grace akacheka na kumbusu Man kifuani. Man alikuwa akichezea nywele zake huku wakizungumza. Walipofika tu hapo hotelini, Man alianza kumfungua nywele wakati wanapeana mabusu. Alizipenda nywele za Crace, hakutaka hata awe anazibana, zaidi wanapokuwa wakifanya mapenzi au wawapo kitandani. Alipofanikiwa kutoa kila kibanioa hapo kichwani kwake ndipo akaridhika na kumtoa nguo zote sasa.

Grace alikuwa amelala kifuani kwake wakizungumza taratibu wakati wanapumzika ili waendelee na mapenzi. Man alikuwa akipitisha vidole huko kwenye kichwa cha Grace. Mara awe kama anamchana nywele na vidole au kuziviringisha hizo nywele kwa kidole kimoja na kuzivuta taratibu. Alijua Grace alikuwa akifurahia sana.  “Nikiwa na wewe, najua kila kitu kitawezekana Man. Tunasikilizana na kuaminiana. Watoto wangu umewachukulia kama wako. Sidhani kama tutapata shida tukiongeza wengine. Au unaona tutakuwa na watoto wengi?” “Ninavyopenda watoto mimi! Hata unizalie mapacha mara sita. Mbona itakuwa halleluya tu.” Grace akacheka sana.

“Lakini usiku wa leo ni wetu Grace. Acha tuendelee kufurahia. Bado tuna muda mrefu sana wakupanga mambo yetu. Mwenzio bado nakutamani.” Grace alifurahia sana. Ndio walikuwa wamemaliza penzi la muda mrefu ambalo Man alifanya madoido mengi, ilimradi tu kumfurahisha mkewe ambaye hata hakuwa akiyajua au hata kudhani kama anastahili kufanyiwa yote hayo.

Alimpaka ice cream hapa na pale akawa anaila kutoka mwilini kwa Grace kitu kilichokuwa kikimsisimua sana Grace. Alimbusu kana kwamba ndio mwisho wao. Kila alipompaka hiyo ice cream, alimlamba taratibu na kwa kutulia kisha anaendelea. Kwa raundi hiyo tu, yakufanya romance huku akifanya naye mapenzi, wote walijikuta wakifurahia na kufikishana kileleni huku wakiendelea bila kuchoka. Ndio walikuwa mapumzikoni hapo.

Man alisogeza matunda mchanganyiko hapo kitandani wakawa wanakula na kunywa huku wakizungumza taratibu. Kulikuwa na vinywaji vingi na vyote vinawasubiria wao. Juisi nyingine zilikuwa za kuwapa nguvu. Wakajikuta wakiendelea kuwepo hapo kitandani bila uchovu. Uchovu wote wa siku nzima uliisha. “Unaninywesha nini wewe Man? Mbona kama nazidi kuchangamka?” Man alizidi kucheka. “Usiku wetu huu Grace. Acha maswali mengi wewe furahia tu.” “Usiniambie unataka tukeshe!” “Hutaki?” “Nilivyonogewa! Sitaki hata kusinzia.” Man alizidi kucheka. Grace alimuona Man watofauti. Alijawa na furaha kama aliyetimiza kitu kikubwa maishani. Ilimpa ujasiri Grace kuona amefanikiwa kutimiza ndoto za Man. Alijitoa hapo kitandani bila kuchoka.

Jumapili.

Grace alimshwa na ndoto mbaya pamoja na maumivu makali sana. Akaelekea bafuni. Alikaa huko kwa muda mrefu akilia taratibu. Hawakuwa wamelala muda mrefu. Ni kama Man alihisi Grace akitoka hapo kitandani. Kwa uchovu usingizi ukamchukua nakurudi kulala tena. Baada ya muda akapapasa kulia na kushoto, Grace aliyekuwa amelala kifuani kwake hakuwepo hapo kitandani. Ndipo akafungua macho na kugundua hayupo pale kitandani. Chumba kilikuwa kimya sana. Akaanza kufikiria atakapokuwa mkewe.

Akaamua kumwangalia bafuni. Akamkuta akilia taratibu. Kumuuliza kulikoni, Grace hakusimulia ndoto mbaya aliyoota, ila akaeleza maumivu makali yanayomsumbua. Kiuno kilikuwa kikiwaka moto, kitovu chake ni kama kulikuwa kuna mtu anaking’oa. Wakati Man anamshika mkono ili amtoe hapo bafuni, damu zikaanza kumwagika hapo hapo bafuni. Grace alizidi kulia asijue ni nini kinampata wakati hakuwa hata karibu ya siku zake na aliacha kutumia kinga zote za kuzuia kushika mimba ili pengine ashike mimba kwenye fungate.

Walihangaika pale hotelini, wakashindwa hata kusafiri siku hiyo ya jumapili. Wakaamua watulie pale pale hotelini mpaka Grace atakapopata nafuu kwani hakuweza hata kutoka kitandani kwa maumivu. Man alimpigia simu daktari mmoja, ambaye alikuwa rafiki wa familia, akafika pale hotelini, akamchoma sindano Grace, angalau akaweza kulala siku hiyo nzima ya jumapili na usiku wote.

Jumatatu

Alipoamka siku hiyo ya jumatatu akaanza kulalamikia maumivu makali ya tumbo, kama anayetaka kuzaa. Ndipo akamuomba Man ampigie simu mama yake, afike hapo hotelini ili amuulize kulikoni. Grace mtoto wa mama. Akiumwa tu, lazima mama yake awepo na ajue aina ya huo ugonjwa anaoumwa yeye na tiba yake.

Man akapiga simu ya mama G, akapokea Geb. “Nani mwenzangu?” Geb akauliza. “Ni mimi Man. Mumewe Grace.” Geb alihisi yupo ndotoni. “Mko wapi?” Geb akauliza. “Bado tupo hotelini. Tulishindwa kusafiri, Grace alianza kuumwa sana tumbo. Alitaka kumwita mama.” “Asante Yesu wangu!” Man akashangaa akahisi Geb hajaelewa. Asijue Geb anafurahia kumpata Grace. Hofu yakuzika watoto wake bila mama mtu kuwepo ilikuwa ikimsumbua Geb kadiri James alivyokuwa akisistiza hao watoto wameharibika sana. Anamwambia nini Grace akirudi? Kuwa watoto alioagana nao ukumbini wamekufa na wameshazikwa!? Yaani amuonyeshe makaburi tu! Kumpata Grace pekee ikawa habari njema sana kwa Geb. Hata kama hataona maiti ya wanae, basi angalau ahudhurie mazishi na aamue mwenyewe wazikiwe wapi.

 “Upo naye hapo?” “Ndiyo.” Man akajibu. “Naomba utoke nje tuzungumze vizuri, hapo sikusikii vizuri.” Man akaelewa tu. “Unaenda wapi?” Grace akauliza huku akilia. “Nahisi hii simu ya mezani ya hapa chumbani ina matatizo. Hanisikii vizuri, ngoja nikampigie tena mapokezi. Nakuja sasa hivi.” “Sawa. Mwambie mama asichelewe.” “Nitafanya hivyo. Naomba utulie Grace. Kila kitu kitakuwa sawa.” Man akainama pale kwenye ile simu. Akachomoa waya mmoja ili kuhakikisha Grace hawezi kugundua, na awe ameiharibu zaidi, ndipo akatoka.

Alikwenda mapokezi akampigia Geb simu. Geb akamuelezea kila kitu. Kuwa hapo walipo ndio wametoka kununua majeneza mawili, wanaelekea hospitali ya Kibaha kuchukua hiyo miili iliyoharibika sana, waone kama wanaweza kuihamishia hospitali ya taifa ya Muhimbili mpaka kesho ndipo wazike. Kama ikishindikana, basi izikwe siku ileile. Akamtaka amtoe Grace hapo hotelini na kumwambia ampeleke hospitalini kwa ajili ya matibabu, lakini ampeleke alipolazwa Fili. Man alibaki kimya kwa muda kama amechomwa sindano ya ganzi.

“Unanisikia?” “Utahitaji msaada gani mwingine?” “Sijui Man. Nahisi nimechanganyikiwa sielewi tena. Nafanya kile kinachowezekana kwa sasa hivi.” “Sasa kwa kuwa mimi nitakuwa na Grace na Fili, naomba upokee simu ya Ole, mume wake Malisa, na Malisa. Msaidiane.” Geb akavuta pumzi kwa nguvu. “Nitashukuru sana.” Man akakata simu.

Alikata tu simu ya Geb, akawapigia simu hao watu wawili akawapata. Aliwaweka kwenye conference call. Akawaelezea kwa kifupi tu, wote wakasema watamtafuta Geb muda mfupi sana baada ya hapo. Man akakata simu na kurudi chumbani. Akajua habari zitasambazwa kwa kina Ole wote, na Geb atapata msaada.

~~~~~~~~~~~~~~

“Mama amesemaje? Anakuja?” Grace akauliza mara baada ya Man kuingia. “Anataka nikupeleke hospitalini. Tutakutana naye huko.” Grace akakubali bila shida.  Man akamsaidia kumvalisha, wakatoka. Tayari Man akajua asili ya maumivu ya Grace si ugonjwa uliompata. Nafsi yake imeonja uchungu wa watoto wake. Walipofika kwenye hospitali aliyolazwa Fili, akamwambia waende wodi ya watoto kwanza. “Fili naye ni mgonjwa. Aliletwa tokea jana. Hali yake haikuwa nzuri, hivi leo amefanyiwa upasuaji.” Grace akakunja uso akamwangalia vizuri Man.

“Unamaanisha Fili, Fili mwanangu?” Grace akauliza akionekana na wasiwasi sana. “Ndiyo. Lakini kabla hujaingiwa hofu, nataka nikuombe kitu. Fili anakutaka wewe. Lazima uingie pale wewe ukiwa kimbilio lake, sio vinginevyo. Alikuwa na Nanaa muda wote.” Grace hakuwa anaelewa. “Umesema kwa nini alifanyiwa upasuaji!?” Grace akauliza. “Kwanza nani amekwambia kama ni mgonjwa? Kwa nini awe na Nanaa ambaye ni mgonjwa, na sio mama? Geb yuko wapi? Kwa nini Danny hayupo nao?” Grace akauliza maswali mfululizo mwisho akaona atulie. “Samahani. Nahisi napaniki. Ujue hawa watoto walikuwa wasafiri na baba yao jana. Hivi kuwaona kwenye harusi ilikuwa ni kwakuwa nilimkatalia baba yao asiwachukue ile siku ya ijumaa kama nilivyokuwa nimekwambia siku ile kwenye simu. Nikataka wawepo kwenye harusi yetu.” “Twende tukakae pale.” Man akamshika mkono akamsogeza sehemu iliyokuwa na makochi.

“Mbona nimeanza kutetemeka!? Naogopa Man.” “Danny alipata ajali mbaya sana jana.” Grace akafunga mdomo kwa mikono yote miwili. Akasimama. “Njoo kwanza Grace.” “Fillus na Fillan wamefariki?” Grace akauliza swali la moja kwa moja. Man akasimama. “Niambie Man. Niliona kwenye ndoto. Niambie ukweli. Niliota naletewa  vitu viwili vikiwa vimefunikwa mashuka meupe. Nikataka kuwafungua ili kuona ninachopewa, huyo aliyenikabidhi akaniambia siwezi kuangalia. Nikauliza ni nini hiki unachonipa kikiwa kimefunikwa. Akaniambia ni Fillius na Fillan. Nikashituka sana. Nikataka kujifariji kama ni ndoto tu labda niliwaota kwa kuwa niliagana nao wakiwa wote wananililia, lakini hisia zikazidi kuwa kali na yale maumivu kama nataka kuzaa yakawa yanazidi. Nikaogopa kukwambia ile ndoto ili nisikutie wasiwasi. Sasa naomba uniambie ukweli. Ni kweli?” “Ndiyo. Lakini Fili anaendelea vizuri. Anakuulizia. Twende.” Grace akapiga magoti nakuanza kulia pale pale.

Man akaenda kumnyanyua. “Geb ameniambia Fili anakuulizia sana Grace. Naomba tujikaze twende kwa mtoto. Mbaya zaidi, Fili ameshuhudia ile ajali kuanzia mwanzo mpaka mwisho. Yupo kama anaweweseka. Amechanganyikiwa, anahisi wewe utamkasirikia kwa kuwa watoto walipata ajali wakiwa hawajafungwa mkanda. Anasimulia anasema wewe utakasirika kwa kuwa ulimfundisha yeye kuwa, asikae bila kuwafunga mkanda wadogo zake. Geb anasema labda akikuona ukamtuliza, itamsaidia. Kwahiyo Grace, najua unamamivu makali sana mke wangu, lakini sasa hivi Fili yupo kwenye wakati mgumu sana. Halali mpaka achomwe sindano ya usingizi.” Grace akalia tena kidogo, akanyamaza.

Wakaelekea alipokuwa amelazwa Fili. Alimkuta Nanaa amemkumbatia Fili amelala. Grace akaingia chooni. Alilia huko zaidi ya nusu saa. Man alikuwa naye. Akatoka. Nanaa akampisha pale. “Anastuka sana. Inabidi kuwa naye hapa ili asichomoe hizo waya na dripu. Akiamka anataka kukimbia mpaka umtulize ndipo anatulia.” Grace akapanda pale kitandani akajiegemeza nakumuweka kifuani kwake.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya kama lisaa Fili akaruka, Man akamdaka. “Fili!” Grace akamwita kwa upole. Fili akagutuka kutoka usingizini. Akamuona mama yake. “Pole! Unasikia maumivu?” “Nilimwambia dad kabla hatujaanza safari kuwa watoto hawajafunga mikanda. Akanipiga hapa. Akasema ninyamaze. Tulipoanza kuondoka, wao walikuwa wanagombana na Sara. Ndio nikakumbuka ulisema lazima nihakikishe watoto wanafunga mkanda. Sasa kwa kuwa wao walikuwa wakigombana sana, nikasema nishuke taratibu, ninyate ili niwafunge watoto. Nikafungua mkanda, nikashuka taratibu. Sara akaniona, akanisemelea kwa dad. Wote wawili wakanigeukia. Sara akawa ananigombesha, dad akaanza kunipiga makofi. Dad akasema mimi mtoto mbaya nirudi kukaa. Nikakaa lakini nikamwambia mama aliniambia lazima kufunga watoto mkanda. Akageuka na kunipiga tena hapa, na kofi la mdomo, akasema nisiwe namjibisha. Mimi nikafunga mkanda nikabaki kimya. Alisema hataki kusikia sauti yangu tena.” Fili akaendelea huku mama yake akimsikiliza.

“Wao wakaendelea kugombana, ndio dad akampiga Sara kofi la uso. Yeye Sara hakukubali. Akamrudishia na yeye dad la usoni. Gari likaanza kuzunguka kama mpira. Mara ya kwanza likavunja kioo cha mbele nusu. Mara ya pili gari lilipozunguka Fillan akatoka kwenye kiti chake yeye akanasa pale kwenye kioo. Kioo kilingia hapa kwenye jicho kikatoa huku kichogoni. Kingine kilimkata shingo lakini sio yote. Akabaki amening’inia mpaka anko James alipokuja kumtoa.” Grace akafunga macho.

“Ila Fillius yeye alitupwa nje porini kidogo. Halafu gari ikamfuata kule kule ikamponda ponda sana. Tulikuwa peke yetu porini ndani ya gari tumenaswa. Tulikuwa hatuwezi kutoka kwenye gari. Mpaka anko James alipokuja kutusaidia. Akanitoa mimi wa kwanza. Ndio akamtoa dad na Sara. Ndio akaanza kumkusanya Fillius. Alikuwa amepondeka sana. Akawa anamzoa na kumuweka kwenye mfuko. Unajua anko alikuwa analia sana? Muulize mwenyewe. Alikuwa anamwita Mungu aje asaidie wakati anawakusanya Fillius na Fillan. Ila zaidi Fillius aliyekuwa amekuwa kama uji uji.” Fili akaendelea.

“Lakini mama. Usinikasirikie mimi. Mimi nilimwambia dad, ndio dad akanichapa. Nilitaka..” Man alipoona anataka kuanza tena, akamsogelea. “Ujue Fili wewe umenishangaza sana! Kumbe wewe ni kaka mzuri hivyo!” “Hata anko Geb ameniambia. Lakini mimi nilifanya kama mama alivyoniambia. Nilimsikiliza mama. Mimi nasema ukweli mama. Sio kosa langu. Nilikumbuka.” Grace ikabidi atulie. Akamwita. “Fili! Kwanza mimi nimefurahi kuwa wewe ni mtoto mzuri ambaye unanisikiliza.” “Kweli mama? Hujanikasirikia?” “Hata kidogo. Wewe unajua ninavyokupenda na kukuamini.” “Nilimwambia hata Sara kuwa mimi mama yangu ananiamini sana. Akasema mimi muongo eti sisi ni watoto wabaya, hatutulii, tunakelele ndio maana wewe umetukimbia.” “Hapana Fili. Sikuwakimbia. Unakumbuka niliwaaga. Niliwaambia dad anataka kusafiri na nyinyi, ila mkirudi mtatukuta mimi na anko Man tunawasubiri ili tuwe wote?” Fili akabaki kimya kama aliyepotea pale kwa muda.

“Nilimwambia dad tuwafunge watoto mkanda. Dad akanipiga makofi. Dad akasema nirudi kukaa haraka. Nikamwambia mama amesema nilazima tuwafunge watoto mkanda, akanipiga tena hapa. Akasema nisimjibishe. Mimi ni mtoto mbaya. Sisikii. Wakaanza kupigana. Dad ndiye aliyeanza kumpiga Sara….” “Fili! Fili!” Grace akamwita. “Naam!” “Niangalie mimi mwanangu.” Fili akamgeukia. “Nakupenda sana Fili mwanangu. Sana.” “Na mimi nakupenda mama. Lakini Fillius na Fillan wao walikufa. Fillius alipondeka. Anko James alimuweka kwenye mfuko. Halafu Fillan yeye alikatika shingo. Ila sio yote. Halafu kioo kingine kikaingia kwenye jicho kikatokea hapa.” Grace akavuta pumzi.

“Unakumbuka ulimfundisha Liv kuwa watu wakifa huwa wanaenda wapi?” Mama yake akamuuliza. “Wanaenda kwa Mungu. Lakini hawawezi kunyonya tena wala hatuwezi kuwaona. Wataenda kuwafukia kwenye udongo!” Fili alielezea. “Kwanza kumbuka walishaacha kunyonya. Halafu wakifika kule kwa Mungu, Mungu atawatunza vizuri sana. Hata kile kidonda cha Fillan cha jichoni na shingoni vyote havitauma tena. Mungu atamponya kabisa.” “Ila Fillius hawezi mama. Amepondeka kabisaaa.” “Mungu atampa mwili mwingine mzuri.” “Kweli!?” “Kweli. Ukifika kwa Mungu anakupa kila kitu kipya. Ni kweli kwa sasa hatutawaona tena, lakini na sisi tukija kwenda huko kwa Mungu, tutawaona jinsi walivyopendeza.” Fili akatulia kabisa.

Akarudi kukaa kwa mama yake. “Lakini nitawamiss. Unajua walikuwa ni rafiki zangu? Nilikuwa nacheza nao. Dad akiwachapa walikuwa wananikimbilia mimi. Wananitaka tu mimi. Mimi ndio nilikuwa nawabembeleza. Nawaambia nawependa. Kama vile ulivyokuwa ukinifanyia mimi wakati dad akinichapa. Unajua na wao walikuwa wananyamaza?” Grace alizidi kuumia.  Akajikuta akianza kulia. “Usilie mama. Tutaenda kuwaona tena. Mungu atawapa mwili mpya. Hata Fillan hatakuwa na jicho bovu. Mungu atampa mwili mpya na jicho jipya. Ataniona halafu tutacheza nao.” Fili akarudia alichoambiwa na mama yake.

“Naomba kukushika Fili.” Man akaongea kwa upole.  “Nataka kukaa na mama yangu. Mama huwa hanichapi. Huwa anazungumza na mimi. Huwa anasema mimi ninauelewa mkubwa sana. Anaamini akizungumza na mimi huwa namwelewa bila hata kunichapa.” “Hata mimi sitakuchapa.” Fili akanyamaza. “Unapenda kucheza mchezo gani?” Man akamuuliza. “Nilikuwa nachezea timu ya anko Geb. Mpira wa kikapu. Mimi ndio nilikuwa kiongozi wao. Lakini dad alinikataza kwenda. Halafu nilikuwa nacheza na kina Fillius magari. Dad alitununulia magari ya umeme. Halafu video games, na Kompyuta. Tulikuwa tunacheza na dad pia. Najua kuogelea.” “Na mimi utanifundisha kuchezea?” Fili akacheka.

“Unataka nikufundishe nini?” Fili akauliza. “Labda tuanzie magari halafu tuje video game.” Man akatoa wazo. “Sasa hivi sina video game. Sara alichukua ya kwetu. Akasema atarudisha. Lakini nyumbani nina magari ya umeme.” “Basi tufanye hivi, ukilala, ukiamka, nitaleta video game nyingine. Tutaunganisha pale kwenye ile tv, halafu unifundishe.” Fili akacheka tena. “Sawa.” “Basi lala hapo kwa mama, mimi nikatafute video game. Ukiamka, tunaanza kucheza.” Fili akajisogeza kwa mama yake. “Nakupenda Fili.” “Na mimi nakupenda mama.” Akaanza kusinzia. “Nikilala, utasafiri tena?” “Hapana. Sasa hivi sitasafiri tena. Nabaki na wewe.”  Akalala. Kila mtu akahema kwa nguvu.

“Asante Man.” “Pole sana Grace.” Man akamsogelea akambusu palepale alipokuwa amekaa na Fili. “Nanaa! Nakushukuru sana.” “Wala usijali. Lakini naomba nikuache hapa na Man, nikamwangalie mama. Tokea nimeondoka jana, sijui anaendeleaje?” “Anaumwa?” “Geb amemrudisha leo asubuhi nyumbani anasema anaendelea vizuri. Alipata partial au minor stoke. Sababu ya mshituko.” Grace akanyamaza. “Man, nitawaona baadaye.” Wakati Nanaa anataka kutoka, Malisa, mama yake, wadogo zao, mke wa kaka yake wakaingia.

“Poleni sana Grace. Poleni sana.” “Asante.” Grace akaitika kinyonge. “Kaka na Ole, wapo wanasaidiana na Geb. Usiwe na wasiwasi.” Malisa akimaanisha kaka yao mkubwa, na mumewe. “Nashukuru.”  Grace akaitika. “Vipi mtoto?” Mama yake Man akauliza. “Naona Man ameweza kumtuliza. Bado yupo kwenye mshituko. Anavyosimulia, inaonekana aliona kila kitu kilivyokuwa kikitokea. Imemuharibu sana akili.” Grace aliongeza. Akambusu. “Huyo ni wifi yangu. Ndiye aliyekuwa naye muda wote.” Grace alimtambulisha Nanaa. Nanaa akawasalimia. “Naomba mimi niwaachie Grace na Fili, nikamtizame mama. Alianguka kwa pressure baada ya kupata taarifa. Na yeye alilala hospitalini, ndio wamemtoa asubuhi hii. Sasa najua atakuwa peke yake na watoto.” “Hamna neno. Sisi tutakuwa hapa na Grace.” Malisa akajibu, Nanaa akaenda kumkumbatia Grace, akambusu. Grace akafuta machozi. Akatoka.

Safari Ya Mwisho Ya Fillan & Fillius.

Ole na kaka yake mkubwa Man, walihangaikia nafasi pale hospitali ya Muhimbili. Lakini mpaka Geb anawafikisha pale, tayari walishaanza kutoa harufu mbaya sana. Hawakuweza kuhifadhika tena. Ikabidi Geb azungumze na Grace kuwa wale watoto ni lazima wazikwe siku ileile. Grace akamwambia wao waamue chochote kile. Ndipo taratibu za mazishi zikaanza sasa. Grace alitaka watoto wake wazikiwe nyumbani kwao. Wakaanza kushugulikia kibali cha kuzikwa wale watoto pale nyumbani huku akitafutwa mchungaji na watu wakuchimba kaburi.

Kufika jioni, watu wote walikuwa wamekusanyika hapo tayari kwa mazishi. Mzee Ole pia alihudhuria. Mama G alienda kuchukuliwa na Geb nakuletwa msibani. Ilibidi Nanaa ndio abaki na Fili hospitalini ili mama yake akazike wadogo zake. Ni Grace ndiye aliyekuwa akisubiriwa ili ibada ya mazishi ianze. Kulikuwa na familia hiyo kubwa ya Ole, na kina Magesa. Hawakutaka rafiki hata mmoja wa Danny awepo pale.

Grace aliletwa na Malisa, mama mkwe wake, mke mwenzake ambaye ndiye aliyemsimamia harusi na ndiye aliyekuwa mke wa kaka mkubwa na wadogo zake wakike Man. Man naye alibaki hospitalini ili endapo Fili ataamka basi wacheze hiyo game ili kumtoa kwenye yale mawazo. Grace alikuwa akilia kwa uchungu sana. Hakuamini kama siku ile ya jumamosi pale ukumbini akiagana na wanae ndio ilikuwa kwa heri ya mwisho kabisa. Kila alipoangalia vile vijeneza viwili vya mapacha wake, Grace alizidi kulia. Alibaki amejifunika uso akiendelea kulia mpaka mwisho wa ibada. Walizika hapo nyuma ya hiyo nyumba, wakakaa hapo kidogo. Grace akataka arudishwe hospitalini kwa mwanae. Akaoga, na kurudi hospitalini.

~~~~~~~~~~~~~~

Alikuta Fili akicheza na Man. Alikuwa akicheka tu. “Nimemfunga anko. Japokuwa mimi natumia sana mkono mmoja, lakini nimemshinda.” Grace akatoa cheko lililojaa majonzi nyuma yake, Fili asijue. Geb ndiye aliyemrudisha Grace hapo hospitalini. Na yeye akacheza na Man hiyo video game, Fili akishangilia. Mara bibi yake akaingia. Fili akamwita. “Bibi Fili!” Mama G akasogea. Akaanza kumsimulia tena kuanzia mwanzo wa ajali mpaka mwisho.

“Lakini mama Fili amesema wanakwenda kwa Mungu. Mungu atawapa mwili mpya kabisa. Watakuwa wazuri.” Kila mtu akahema. Angalau mwisho wa safari hii ulikuwa mzuri. “Tutawaona tena bibi, usilie.” “Ni kweli tutawaona tena Fili. Lakini ujue ukiwaona watakuwa wajuzi wa mpira kuliko wewe.” “Hapana anko. Mimi narudi kwenye timu yetu. Dad alikuwa akinikataza nisije. Lakini mama amesema nitaendelea. Kwani mlipata kiongozi mwingine?” Akamuuliza Geb. “Aaaah! Kila mtu anakukumbuka wewe. Jamaa hajui kabisa kuongoza. Si unakumbuka wewe ulivyokuwa ukitupanga vizuri?” Geb akamuuliza. Fili akacheka. “Nakumbuka anko. Basi kawaambie wote wasiwe na wasiwasi. Kiongozi wao narudi.” “Hayo ndio maneno.” Akili ikarudi kwenye michezo.

~~~~~~~~~~~~~~

“Sasa wewe endelea kumfunga tena anko, mimi natoka na mama yako mara moja.” Geb alimuona vile Grace alivyojiinamia pale. Wao walikuwa wakicheza, Fili hakuwa na habari tena. Ni kweli walijitahidi akili za Fili zikatulia. Fili mpenda sifa, akacheka. Walimlevya sifa jioni hiyo mpaka akatulia. Geb akaenda kumshika mkono Grace wakatoka nje. Man alitulia kidogo. Akajua mkewe anaenda kuliwazwa na kaka yake.

“Vipi tumbo?” Geb alimuuliza mara baada yakutoka nje na kutafuta sehemu yakukaa. Grace akaanza kulia. Alilia sana. Na hilo ndilo lilikuwa lengo la Geb. Alitaka amtoe pale, apate muda wakuomboleza. Alijiinamia na kuendelea kulia. Geb akamtoa magotini kwake, akamuhamishia kwenye miguu yake. Grace akawa amemuegemea Geb. Alilia kwa uchungu sana huku akimsugua mgongoni taratibu. Mama yao akatoka. Alimuacha Man na Nanaa pale ndani na Fili. Akawakuta watoto wake wamekaa hapo nje. Na yeye akakaa pembeni ya Grace. Akaanza kulia  na yeye huku amejifunika.

~~~~~~~~~~~~~~

Walilia wawili hao bila kutulia. Mama G alishindwa kumnyamazisha Grace. Alijilaumu kwa mengi. Alijutia hili na lile. Majuto yalimpeleka mpaka siku anatoa baraka zake kwa Grace kuolewa na Danny. Wale wajukuu ndio ndugu Mungu anaokuwa anamuongezea huyo mama. Kuondokewa na wawili kwa mpigo, kwake ni uchungu mkubwa sana. Na yeye alilea kuanzia mimba yao mpaka hivyo walivyokuwa. Alikuwepo siku wakizaliwa. Alimpokea mmoja baada ya mwingine. Leo wamezikwa kabla yake! Alilia sana.

Grace alijuta na kujichukia sana. Aliona alikuwa mpumbavu na kushindwa kutetea wanae mpaka kufa kifo cha kikatili kiasi kile! Alichukia uvumilivu wake kwa Danny. Mara nyingi alishawishika kuachana na Danny, lakini wakaishia kusameheana. Lakini alikuja kuishia pabaya sana. Uvumilivu wake ulimpelekea talaka ya aibu. Alitukanwa na kuanikwa mbele za watu. Hata alipokuwa akitembea mbele za marafiki zao, alijiona ni kama hakuwa na nguo. Yale aliyokuwa akiyasitiri, Danny aliyaanika vibaya sana.

Alipuuza tabia ya Danny kuchapa watoto hovyo. Danny alikuwa mkali si kwake tu, hata kwa watoto. Hilo hakuwahi kuliwekea mkazo na kumkataza. Akabaki akimkasirikia tu. Leo Fili anaimba kipigo kisicho nahatia kutoka kwa baba yake na kumsababishia vifo vya wanae. Alilia Grace, asijue kama atakuja kuweza kunyamaza.

~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya muda Man naye akatoka. “Nimemuacha nesi anamuandaa Fili ili alale.” Man aliongea wakati anawasogelea. “Unafikiri watahitaji msaada?” Geb akauliza huku akimsugua dada yake mgongoni. “Yupo na Nanaa. Ameniambia naweza kuja tu hapa.” Akaenda pale alipokuwa ameinama Grace akilia. Akachuchumaa karibu na uso wake. “Grace!” Man alimuita taratibu. “Pole sana mpenzi wangu. Pole sana.” Grace aliendelea kulia. “Naweza kumshika?” Man akamuuliza Geb. “Bila shaka. Lakini nilitaka apate muda kidogo. Akiwa mbele ya Fili inamlazimu kushika uchungu ndani. Itamuumiza sana. Unaweza kukaa naye hapa, mimi nikarudi ndani kuhakikisha Fili analala vizuri.” “Sawa.” Man akampokea Grace, Geb akamchukua mama yake aliyekuwa amekaa peke yake pembeni akilia. Akaanza kumbembeleza.

“Unataka twende tukaombe na Fili?” Geb akamuuliza mama yake. “Sitaweza Geb.” Mama G alijibu huku akilia sana. “Basi nisubiri hapa, nitakuja sasa hivi. Lakini mama, naomba jitahidi kutulia tafadhali. Sitaki hiyo pressure ipande zaidi. Grace anakuhitaji sana wewe. Naomba utulie ili uweze kuwa naye.” “Si-wezi Geb.” “Unaweza mama. Mimi nakufahamu wewe. Tafadhali jaribu kutulia. Nitarudi sasa hivi.” Mama G aliyekuwa amekumbatiwa na mwanae akatingisha kichwa. Geb akarudi kwenye chumba alichokuwa amelazwa Fili.

“Lini utamleta Liv aje anisalimie?” Fili alirusha swali mara baada ya Geb kuingia. “Unajua Liv ni rafiki yangu wa kwanza?” “Sikujua.” Geb akajibu huku akimsogelea pale kitandani. “Tunapenda naye sana. Kwa hiyo sasa hivi atakuwa amebakia yeye na Magesa ndio wadogo zangu. Akijua ninaumwa, najua atataka kuja kuniona.” “Basi nitamwambia halafu nitamleta kesho.” Geb akajibu. “Sasa kwa kuwa umepewa dawa ya usingizi, unatakiwa upumzike kabisa. Ulale.” “Mama Fili ameondoka tena?” Fili akauliza kwa upole. “Hapana. Sema anaumwa na yeye. Akishamuona daktari na kupewa dawa, atakuja mlale wote.” Fili alicheka akionyesha anasinzia. “Nampenda sana mama yangu.” “Hata yeye anakupenda.” Geb akambusu kwenye kipanda uso. Nanaa alikuwa pembeni yake akimpapasa taratibu. Wakamuona amefunga macho.  Wote wakahema kama waliopata aghueni.

Hakuwa amefanyiwa upasuaji wa kuchanwa sehemu kubwa sana. Ni kama alitobolewa tu. Wakarekebisha sehemu iliyokuwa ikivuja damu, na kusafishwa vizuri, kufyonzwa damu iliyokuwepo ndani. Waliwaambia baada ya siku tatu kuisha, kama hali yake haitabadilika, ataruhusiwa. Grace na Man ilibidi walale hapo usiku huo. Grace naye alichomwa sindano ya usingizi, akalala kwenye kochi wakati Man alikuwa amekaa tu kwenye kochi la pembeni. Ndoa hiyo ilianza kwa misiba ya watoto wa Grace. Fungate ndio walikuwa hapo. Grace akiwa hoi, hajiwezi na mwanae ndiye amezungukwa na mashine. Man alibaki akiwaza.

Huko kwa Danny!

Asubuhi ya siku ya jumanne, James alianzia hospitalini alikokuwa amelazwa Danny. Alikuwa ameshahamishiwa hapo hospitali ya Muhimbili katika kitengo cha mifupa, MOI. James aliingia akamkuta ameninginizwa na vyuma vingi vimechomoza kwenye miguu. Akamgusa. “Vipi?” James akamsalimia baada ya kufungua macho. “Vipi Fili?” Danny akauliza swali. James akanyamaza kwa muda. “Nini kimetokea tena?” Danny akauliza kwa wasiwasi. “Hakuna kingine kilichotokea. Lakini yule mtoto! Sijui Danny. Acha tu ninyamaze. Mimi nimekuja kukuangalia wewe. Unaendeleaje?” “Nisikilize James. Mimi sina dalili yakutoka hapa leo wala kesho. Na unajua kabisa nimeharibu. Sitakaa kumuona yule mtoto tena. Heri uniambie tu nijue.” James alimtizama Danny, asijue kama amuhurumie au vipi.

“Hakika umeharibu Danny. Nini kilikupata aisee!? Kwa nini umeharibu familia nzuri vile!? Wakati wote mimi nilikuwa nikikwambia nilikuwa nakutamania jinsi ulivyo na familia nzuri! Ni nini umefanya Danny!? Au ni kwa ajili ya Sara, mtoto wa juzi, asiyejua hata maisha ni nini!? Hivi unajua kuwa amekukimbia?” James akaendelea.

“Fili anakuongelea vibaya sana Danny. Mabaya yote uliyomtendea kwenye gari, tena akiwa anakwambia watoto hawajafungwa mkanda! Anasimulia bila kuchoka vile ulivyompiga. Tena zaidi ya mara moja ulimpiga yule mtoto akiwa anawaambia watoto hawajafungwa mkanda! Amekuwa kama amechanganyikiwa! Anaweweseka tukio zima analirudia kulisimulia kila wakati na kwa kila mtu. Vyombo vya habari vyote vinatangaza unyama uliowafanyia watoto wako, Danny! Nipo njiani nasikia sauti ya Fili redioni, ikisimulia vile wadogo zake walivyokufa kifo kibaya! Anaelezea vile alivyowaona wakiwa wameharibika vibaya sana. Sijui ni wapi na nani alimrikodi yule mtoto! Lakini wamempata vizuri sana. Ameeleza mwanzo mpaka mwisho bila kuficha. Mpo katika kila mtandao hapa nchini. Nini kilikupata Danny!?” James hakuwa akielewa.

“Ulikuwa ukitafuta nini hapa duniani!? Hivi unajua watoto wako wale wawili wamezikwa jana wakiwa wameoza hata mama yao hakuwaaga?” James akauliza tena. “Sijui kama nakulaumu, ila ninachojua ni kuwa nakusikitikia sana Danny. Hakika nakuhurumia. Nilikuwa kwenye harusi ya Grace juzi, nilishindwa kuelewa Danny! Umemuacha yule mwanamke, ukakimbilia kwa Sara! Hakika wamekuwahi vibaya sana. Ulipomuacha tu Grace, mwanaume aliyempata ni kama ameokota lulu. Heshima waliyompa Grace, thamani waliyoiweka kwake, hakika umepiga teke bahati! Shilingi yako imetumbukia kwenye choo cha shimo Danny.”

“Baba mkwe wake anatangaza hadharani kuwa baada tu yakumuona Grace, wakakaa naye na kuzungumza naye, akasema lazima wammiliki Grace bila kuchelewa. Hayo ni maneno ya mkwewe. Sio mumewe mpya Grace. Najiuliza, ulifungia vipi macho, hata kwa sekunde moja, ukasahau thamani ya wazi ya Grace, Danny ndugu yangu!? Grace Magesa!? Hakika sielewi Danny! Umewezaje au umethubutu vipi kumpa talaka Grace!? Umekubali kina Zinda waliokuwa wakikuonea wivu, tena kwa kukutamkia waziwazi, wakupotoshe hivi hivi!? Unasindikizwa na wenzako wanakushangilia kwenda kumtaliki Grace!!? Na wewe unakubali! Ni nini Danny?”

“Ulikuwa salama kwenye ile familia. Ulijipatia heshima kwenye jamii sababu ya yule mama Magesa. Umekubali kutoka kule, ukahamia kwa wahuni wale! Zinda aliyekuwa akikutukana hadharani ndio ukamgeuza rafiki? Mama yake aliyekutamkia laana wewe. Akisema huna uwezo wa kutunza familia, unamkosi na laana. Leo ukamgeukia yeye na kumsahau mama G, aliyesimama na wewe kwenye shida zako! Hakika nakuhurumia Danny. Mungu akusaidie hao uliowakimbilia, waifunike aibu yako. Wakutetee leo, siku ya msiba wako. Na muombe Mungu Grace asikushitaki. Hakika mtoto wako atakufunga Danny. Yule mtoto analiza kila mtu mpaka manesi wa pale hospitalini wanao muhudumia.”

“Na wanamwamini kwa kuwa wote tunajua Fili huwa hadanganyi na hasau. Anasimulia bila kuchoka. Anarudia bila kukosea neno kwa neno. Imebidi kuwa anapewa dawa za usingizi ili angalau apumzike kusimulia aliyoyaona kwenye ajali. Nakuhurumia Danny. Hakika nakusikitikia.” Danny alibaki kimya.

“Kuna kitu chochote unahitaji?” James akauliza. “Nahitaji simu au msaada wa kuwasiliana na watu wa benki ili kuweza kuwataarifu wafunge akaunti zangu zote. Najua Sara atachukua pesa yangu yote benki.” “Kama utakuwa hujachelewa.” Danny akanyamaza kimya. James alitoa simu akamkabidhi Danny. Danny akapiga simu benki. Akajaribu kumtafuta mtu ambaye anafahamiana naye. Kwanza akaomba salio kwenye akaunti zake zote mbili. Ya mshahara na ya kawaida. Akagundua Sara alikuwa na kazi ya kuzunguka kwenye ATM’s hapo jijini akitoa pesa kwenye akaunti zote mbili. Akaambiwa matawi yote aliyokuwa akienda. Hata siku moja kabla ya safari yao, alikwenda usiku akachukua pesa. Ndipo asubuhi yake Danny akagundua kadi yake moja haipo kwenye wallet. Wakaishia kugombana. Sara akamgeuzia maneno. Wakatukanana na kusahau maswala ya kadi. Wakaanza safari hiyo wakiwa wanatukanana mpaka kupigana na kupata ajali.

Sara alimtoroka hapo hospitalini Kibaha lakini alihakikisha anaondoka na wallet nzima ya Danny. Ilikuwa na pesa taslimu na kadi hizo mbili. Hakuchelewa. Siku hiyo hiyo ya ajali alipotoka pale, akakimbilia kwenye ATM. Napo akajichukulia pesa kwa kiwango cha mwisho kutoka kwenye ATM. Jumatatu akafanya hivyohivyo. Asubuhi hiyo aliambiwa bado pesa haijatolewa. Danny akajua ni kwa kuwa bado hajaamka. Inamaana akiamka, safari yake ya kwanza itakuwa kwenye ATM kuchukua pesa nyingine. Danny akaomba wa freez kabisa akaunti zake zote mpaka atakapo pona. Sara alikuwa akitoa pesa kwenye akaunti zote kwa wakati mmoja. Hiyo inayoingia mshahara. Tena kwa Dolla na akaunti yake ya akiba, ambayo pia iliingia ile pesa aliyolipwa na Grace kwa kuuza nyumba.

Zinda na Gozi kwa best yao Danny!

Wakati James anataka kutoka Zinda na Gozi wakaingia. Wamejawa vicheko kama hakuna baya lililompata mwenzao. “Mambo vipi mkuu!” Wakataka kumpa mkono James, James hakutaka unafiki. Akajirudisha nyuma, akaegemea ukuta. Wakaangaliana na kucheka. “Upo baba? Naona wamekutoboa kweli!” Alianza Gozi kwa Danny. “Na kweli wamekutoboa! Vipi maumivu lakini? Nilitingwa nikashindwa kuja kukuona bwana. Mara niambiwe upo Kibaha, mara Muhimbili, nikaona nikuache utulie kwanza ndio nije.” Kabla Danny hajajibu, wakaanza kuambiana wapi walikuwepo jana na juzi nakushindwa kufika hapo hospitalini. Walisimuliana habari za huko walipokuwa huku wakicheka kana kwamba mwenzao hayupo matatizoni au kama vile James hakuwaeleza ukubwa wa tatizo alilopata Danny. Wakati James aliwatumia ujumbe wote. Tena unaofanana. Akiwaeleza  juu ya habari za Danny na wanae. Kuanzia siku ya kwanza ya ajali yenyewe mpaka usiku uliopita. Aliona wakisoma jumbe zake, lakini hakuna aliyemjibu.

“Umemwambia mama kuwa nilipata ajali nikashindwa kufika nyumbani?” Danny akauliza. Wote wakajua anamuuliza Zinda. “Kama unamaanisha mama yangu mie, nilimwambia.” Zinda akatoa jibu hilo na kuendelea na mambo yake. “Anajua kama watoto wawili walifariki?” “Kwanza hivi ilikuaje Danny? Wewe ulikuwa unaendeshaje bwana? Au ndio ulikuwa ukiendesha kwa mkono mmoja, mkono mwingine unachezea paja la Sara?” Gozi akadakia. “Bwana kweli! Maana jamaa alikuwa anamsifia Sara kama ameokota alumasi! Anasema mtoto unabeba popote, unageuza vyovyote. Huna haja yakuwasha taa usiku. Mtoto anawaka!” Wakacheka wao wawili. James kimya.

“Au mzee utamu kwenye gari ulipitiliza ukaamua kutoa madogo kafara!” Gozi akauliza. Wakacheka wote wawili. Ukaanza utani pale. Sifa za Sara ndizo zikaanza. Yale aliyokuwa akimsifia nayo Sara, ndio wakaanza kuyarudia. “Mtoto mwepesiii!!” “Mtoto anawaka kama jua!” “Zinda! Zinda!” Gozi akamwita Zinda ili amsikilize na yeye akirudia maneno ya Danny juu ya Sara. “Usisahau ulaini wa Sara.” “Laini tu, laini kama sufu! Si ndio Danny eeh!? Au tumekosea Mzee wa Dola!?” Zinda akauliza kwa kejeli huku wakicheka sana. “Mtoto anatoa penzi kokote, kiuno feni sio kama Grace!” Gozi akaongeza. Wakacheka sana mpaka wakagonga.

“Kwanza Sara mwenyewe yuko wapi?” Gozi akauliza. “Utamuweza Sara wa Danny kwa usingizi? Anapenda kitanda kuliko nafsi yake. Sasa hivi mapema sana kwa Sara.” Zinda akajibu. “Mtoto wa Danny shida haziwezi. Na hivi dola inaendelea kuingia kwa Mzee, lazima ayafurahie maisha.” Gozi akapokea.

“Naomba simu nimpigie mama.” Danny aliwakatisha. “Mama yupi Danny? Maana wewe hutabiriki bwana. Mara leo mama G, awe mama yako. Wakikutibua huko ukweni, unarudi Tabora! Sasa wapi ni wapi baba? Hata mama yangu naona amechoshwa na hiyo tabia.” “Mimi nimepata ajali na familia yangu nikiwa nakwenda kuwaona wao Tabora! Leo unaniambia sitabiriki vipi!?” Zinda akacheka. “Zinda!?” “Usitoe povu Mzee, mimi nataka uhakika tu.” “Kivipi na wakati ni nyinyi wenyewe mlinipeleka kwa mganga kunitapisha na mkasema natakiwa mpaka kutakaswa kwa niliyolishwa na kina Magesa?” Danny akauliza kwa mshangao. “Kwa hiyo sasa hivi unasema na mama yangu pia mchawi? Maana mara ya kwanza walikuwa kina Magesa, leo mama yangu!?” Zinda akambadilikia.

“Sio nyinyi ndio mlio niambia nimelogwa na kina Magesa!? Tena Zinda ukanisisitizia kuwa hata mama yako ameambiwa na mganga wake, kwa hiyo anataka akaniague mimi na wanangu? Nimekwenda kwenu mara tatu! Na wewe ukinisindikiza! Mkatufanyia dawa mimi na wanangu! Unakumbuka ni wewe ulionisaidia kupata kondoo, mbuzi na jogoo mwekundu wakumpelekea mganga wenu kwa ajili yakunitakasa mimi na wanangu!? Tena safari hii ndio ilikuwa safari mliyoniambia niende mimi na watoto wangu tu, wewe hutaongozana na sisi ili mimi na wanangu tukapatanishwe na ukoo wenu! Mkaniambia kuna tambiko la mwisho natakiwa kufanyiwa mimi na wanangu kwa mizimu ya kwenu! Leo..” Zinda akatoa simu na kumpigia simu mama yake.

Ikaita mara moja ikapokelewa. “Umemsikia Danny? Eti sasa hivi anakutangazia kuwa wewe mchawi, umeua watoto wake wakati yupo njiani akija kukuangalia. Anatangaza kuwa tulimpeleka kwa mganga…” Zinda akaanza kujishitaki pale kwa maneno tofauti ambayo yalimshangaza kila mtu. Danny hakuwa ametamka kuwa wao wameua watoto wake njiani! Zinda ameanzisha jambo lililoanza kumugopesha kila mtu pale. Yeye asijue. Ni kama na yeye alipaniki gafla baada ya Danny kutoa siri ya kile walichokuwa wakimfanyia yeye na watoto wake kila alipokuwa akienda huko kwao, Tabora.

“Mwambie Danny…” “Ngoja kwanza mama, nikuweke kwenye spika.” Zinda akabonyeza kwenye spika. “Anakusikiliza mama.” “Wakati ule nilikwambia kuwa unalaana Danny. Ukanikatalia. Nilikwambia huna uwezo wa kutunza familia kwa kuwa umelaaniwa. Umeamini sasa? Umeua familia yako wewe mwenyewe, leo unataka kushika watu uchawi! Ulimkandamiza mwanangu, ukaiba bahati zake zote ikiwepo hata kazi unayofanya. Vyote vilitakiwa viwe vyake ukatumia ujanja ujanja wako ukamzidi mwanangu mahesabu. Ukachukua wewe. Mwanamke aliyetakiwa amuoe yeye, ukamdhulumu kwa kumlaghai huyo msichana na kaka yake mpaka ameolewa na Geb. Leo yamekugeuka, unahangaika! Nilikwambia mabaya yote uliyomtenda Zinda ipo siku yatakurudi tu. Umeamini sasa? Umerudi kule ulikotakiwa uwe kwa kuwa mwanangu amerudishiwa mambo yake yote. Nyota uliyoichukua ya Zinda sasa hivi imerudi kwake ndio umebakia mtupu. Na ndio maana hata Sara amekukimbia anamtaka Zinda.” Wote walikuwa wakimsikiliza mama Zinda akiongea kupitia kwenye simu ya mwanae. Hilo nalo likawashangaza zaidi, wakashangaa anachoongea huyo mama.

“Mama yake Zinda amejuaje kama Sara amemtoroka Danny? Nani amemwambia? Inamaana Sara yupo kwa Zinda!? Kazi ya Danny ni ya Zinda! Kivipi tena?” James na Danny wakajiuliza kwa pamoja. Danny akaumia sana. “Sara yuko kwako?” Danny akauliza kwa kuumia sana. “Wewe unawazimu Danny! Mama kwaheri.” Zinda akataka kukata simu. “Nakuonya kaa mbali na Zinda, wewe Danny. Umeshaharibu maisha yake vyakutosha. Litakalokupata tena, usilaumu. Unamkosi mkali sana na laana. Hata mizimu imekukataa! Imezuia usifike tena huku kwetu. Na umebakishwa kulipa ubaya wote uliomtend....” Zinda akakata simu kwa haraka. Kila mtu akabaki akimtizama Zinda. Mpaka Gozi alionekana ameingiwa hofu.

“Kabla hujaondoka Zinda. Naomba nikuulize swali moja na la mwisho. Maana najua ulikuja kunisanifu tu. Ni wewe na mama yako ndio mliosababisha ile ajali?” “Danny angalia sana mdomo wako wewe! Umeharibu mambo yako mwenyewe, sasa hivi ndio unatafuta watu wakuwalaumu! Sasa hivi pia utasema sisi ndio tumehusika na kuvunjika kwa ndoa yako, wakati ni wewe mwenyewe ulikuwa ukiyatukana matako ya mkeo!” “Aliyekuwa mke wake. Sasa hivi Grace ni mke wa mtu kaka.” Gozi akamkubusha. “Vyovyote vile. Maana sasa hivi ndio anataka mtu wakumlaumu wakati sisi hatukuwahi kulala na huyo Grace. Hakuna aliyekuwa anajua Grace anakuaje ukilala naye! Yukoje huko chini! Hata hayo matako aliyokuwa akiyatukana pia sisi tulikuwa tukiyaona kwa nje tu! Wewe mwenyewe Danny ndiye uliyekuwa ukimponda kwetu. Hapo tena utasema tumekuloga? Raha uliyokuwa ukitangaza unapewa na Sara, nayo pia tulikuloga?” Zinda alimuhoji kama akimsuta. Alimbadilikia na kubadili maneno kwa ukali sana asimpe hata nafasi yakujibu.

“Sasa kwa taarifa yako tu, yule mwanamke wako wala simtaki. Na yeye amejileta kwangu mwenyewe bila kumuita kama wewe. Kwanza nimeonja ni wa kawaida sana. Sitaki kufuatwa nyuma. Jana usiku nimemwambia leo aondoke nyumbani kwangu. Sitaki mikosi kwenye maisha yangu. Na wewe usinitafute tena Danny. Umedhalilisha familia yangu vyakutosha. Leo unamwita mama yangu mchawi! Wakati ni wewe mwenyewe ulinitafuta! Nilikuomba msamaha wakati ule. Tena nyumbani kwa Geb. Na huyo James alikuwepo siku nilipokwenda na mama yake na wadogo zake. Nikakuomba msamaha, ukasema hutaki na wala kwako nisifike mpaka utakaponitafuta. Kwani ulinisikia tena?”

“Sikukutafuta mimi. Ni wewe mwenyewe ulinitafuta. Nikasimama na wewe wakati ule umechanganyikiwa na familia ya kina Magesa. Nikawa upande wako ili kukusitiri. Kila mtu alikuwa akikushangaa jinsi ulivyokuwa ukimtukana Grace, kasoro mimi na Gozi, ndio tulikuwa upande wako kama kufunika aibu yako! Hivi ndivyo unavyotulipa fadhila! Kweli wewe hubebeki. Huwezi kuishi popote na yeyote hapa duniani. Kina Magesa walikupokea ukiwa huna kitu, ukapata pesa ukawageuka na matusi ya nguoni. Mimi na mama yangu tukakupokea, sasa hivi unasema sisi ni wachawi! Nakushukuru na kwaheri.” Akamgeukia Gozi. “Twende zetu Gozi.” Wakatoka nakumuacha Danny haamini. James alicheka kwa kusikitika sana. “Nitakuona baadaye Danny.” James na yeye akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

“Nimechukua kazi ya Zinda? Ipi tena!?” Danny akawaza akiwa ameachwa peke yake hapo hospitalini. “Inamaana bado Zinda anamlalamikia Nanaa mpaka leo!?” Danny aliendelea kuwaza asiamini kama ule upendo aliokuwa ameonyeshwa na kina Zinda huko nyumbani kwao na ndugu zake, ulibeba hila kubwa ndani yake. “Inawezekana kule kwa mganga nilikuwa nalogwa mimi na wanangu sio kuagaliwa kama walivyokuwa wakiniambia!” Machozi ya uchungu yalianza kumtoka Danny wakati akiendelea kuwaza. Akakumbuka kondoo na mbuzi aliosaidiwa kununua akiwa na Zinda, huko huko Tabora alipofika mara ya tatu kwa mganga na kuambiwa na mganga wanahitajika kwa ajili ya damu yakuwatakasa yeye na watoto wake. Hakupata shida kupata jogoo mwekundu. Aliuziwa hapo hapo karibu na nyumbani kwa kina Zinda. Danny aliendelea kukumbuka.

Akakumbuka pesa yake. Akamshukuru Mungu kuwa angalau alimuwahi Sara kabla hajamaliza yote na kumtoa kwenye maisha yake kabla hajamfilisi. Angalau bado salio lilikuwa likisoma vizuri huko benki. Akitoka hapo, anapakuanzia pazuri. Lakini amebaki peke yake. “Grace atanishitaki! Nitafungwa. Sitakaa nikatoka jela. Lakini nastahili.” Danny aliendelea kuwaza akiwa ameachwa pale hospitalini.

~~~~~~~~~~~~~~

v Yamewapata ya kuwapata.

-       Kosa la nani?

-       Nani wakulaumiwa?

v James anauliza imekuaje?! Hata yeye hakupata jibu. Danny yupo hospitalini. Amepoteza watoto na mke. Mpenzi pia hana. Amelala nyumbani kwa Zinda! Anakazi yakuzungukia akaunti za Danny kwenye ATM.

v Baada yakukamilisha kusudi lake kwenye maisha ya Danny, ndio Zinda amejitoa sasa ramsi. Amemuonya asije kumtafuta tena. Litakalompata tena asilaumu mtu.

-       Je, nani wakulaumiwa?

-       Hasira za kupitiliza za Danny?

-        Au Sara?

-       Au Je, ni mizimu kama alivyosema mama Zinda, kuwa imekataa Danny mwenye laana kali, asifike tena kwao ndipo wakaamua kufutilia mbali kizazi chake?

v Lakini na Fili naye alikuwepo kwa Mganga. Walichofanyiwa kina Fillius na Fillan ndicho alichofanyiwa Fili. Wote walitakaswa kwa damu ya kafara huko kwa mganga. Mama Zinda amesema Danny amebakizwa kulipa ubaya wote aliomtendea mwanae Zinda.

-        Fili je? Amepona mauti?

v Pengine ni kosa la Danny zaidi ambaye alijirudisha mwenyewe kwa kina Zinda akijua wamesameheana na kuapiana wanaanza upya wao kama ndugu!?

v Au Kosa ni la Zinda na Mama yake waliokuwa wamebeba visasi moyoni na kumsubiria kumlipa Danny? Wivu wa muda mrefu kuona Danny anamzidi mtoto wake. Walisoma pamoja. Danny yatima. Lakini alioa, akarudi chuo, akapata shahada ya pili na kazi nzuri. Akajaliwa watoto na kuhamia kwenye jumba la maana. Lakini Zinda hakuwa hana hata mchumba wakumtambulisha kwao. Bado anamlalamikia Nanaa.  Bado anapenda pombe na wanawake, hayupo hata nusu ya Danny. Ametaja swala la kazi ya Danny ni yake, hata Danny mwenyewe hakuelewa. Mama yake ameropoka kuwa Zinda amerudishiwa nyota aliyoiba Danny. Sasa hivi anarejeshewa vitu vyake vyote. Hata Sara anamtaka yeye. Zinda atapata nini tena? Umbali gani wamefika kuchukua haki wanayolilia Danny alimpora Zinda?

v Danny amepokea hukumu yake kutoka kwa mama yake Zinda akiwa hospitalini hajiwezi. Amesomewa mashitaka yake ambayo hata hakuwa na habari kuwa wenzake walikuwa waking’ata meno wakisubiria hiyo siku kwa hamu sana. Anasubiri hukumu ya Grace.

-       Ni ipi? Hatima ya Danny ni ipi ana mamilioni ya pesa aliyoifungia benki?

v Grace analia hospitalini. Watoto wamezikwa nyuma ya nyumba. Maisha ya ndoa yalikuwa yakaanze.

-       Wapi tena!? Dar alipozika wanae au Arusha kwa Man?

USIKOSE MUENDELEZO..

 

 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment