Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! – Sehemu ya 63. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! – Sehemu ya 63.

 Baada Ya Fungate, Siku Ya Jumatano.
Nanaa na Geb walitoka pale hotelini tofauti na walivyoingia. Kulikuwa na kitu cha tofauti kati yao. Walionekana wametulia kimawazo. Muonekano wa mume na mke ulikuwa dhahiri. Ni kama kila mtu alipata alichokuwa akisubiria kwa hamu sana. Uhuru kati yao ulitawala. Geb alikuwa huru kumtambulisha kwa kila mtu kama mke wake na Nanaa yeye ndio mama G hakuwa hata akihema. Neno mume wangu lilimjaa mdomoni. “Hatunywi maji! Kwani umesahau jina lake huyo Geb!?” Mama G alimkejeli Nanaa. “Unamaanisha Geb, mume wangu?” Mpaka Grace akacheka. “Kazi nitakuwa nayo!” Mama G akaguna. Walikuwa ndio wanaondoka jijini Arusha baada ya mapumziko ya siku tatu. Ilimbidi hata Grace arudi Dar pamoja nao, kwani alikuwa na jukumu la watoto. 

Walitua jijini Dar siku ya jumatano mchana. Wote wakarudi nyumbani kwa Nanaa na Geb kwanza. Baada ya mazungumzo kidogo Grace yeye akaenda nyumbani kwake. Alipewa ujumbe na msichana wa kazi kuwa watoto wamekwenda shule, jioni watarudishwa. Alipouliza juu ya Danny na Sara, yule dada akaanza kucheka. Alikuwa mzungumzaji sana kwa Grace. “Walihama mara baada yakurudi safari. Waligombana hapa nusu wapigane. Mimi nikachukua watoto, nikaingia nao ndani.” Grace akakaa.

“Wanagombania nini tena?” Grace akauliza. “Eti Sara kachukua pesa bila kumwambia baba Fili, halafu anamjibu mbovu. Anasema alienda kubadili matairi ya gari yake.” “Sara ana gari!?” “Acha dada! Kanunuliwa gari na simu mpya kama hiyo yako mpaka rangi. Basi fujo! Shopping kila siku. Eti anasema ile gari ina matairi asiyoyapenda. Ndio kachukua kadi ya baba Fili, akaenda kutoa pesa bila kumwambia. Bwana nusura wapigane hapa. Baba Fili kakasirika, Sara naye anamjibu mbovu. Lakini wameondoa vitu vyao vyote. Kaka Jeri alituma watu wakusafisha, naona kumesafishwa kila mahali. Sasa hivi ni sisi tu dada.” Grace akapiga magoti akaanza kumshukuru Mungu wake.

  ~~~~~~~~~~~~~~~~~

Walipotulia, mama G akawaita Geb na Nanaa. Wakakaa. “Mimi nataka kuzungumza na nyinyi.” Mama G akaanza baada ya kuwalaza watoto kwa usingizi wa chana. “Kwanza niwashukuru kwa heshima kubwa sana mliyonipa. Nanaa, nakushukuru kwa kurudi na kuamua kunisamehe ili utuweke pamoja. Naomba uniamini tu, kama isingekuwa wewe kukubali yaishe, sisi tusingekuwa hapa, tena tukiwa na hii furaha. Asante mama.” Nanaa akacheka. “Mimi nishakuzoea. Sasa, sasahivi tukigombana, tunanuniana tu, hakuna kutengana.” Wakacheka. 

          “Lakini Nanaa na Geb, kuna kitu amenisimulia James, nimesema niwaambie tu na nyinyi.” “Juu ya nini?” Geb akauliza. “Kumbe yale yote yaliyokuwa yakiendelea usiku ule Nanaa alipotoka hospitalini, ulikuwa ni mpango uliokuwa umepangwa kwa muda mrefu sana. Na Gozi alikuwepo pale, akiwa kama mpeleka habari kwao. Muda wote alipokuwepo pale alikuwa akituma ujumbe.” Mama G akawasimulia kila kitu. “James ameumia sana.” “Hata mimi mama. Imeniumiza sana. Hawa watu mimi nimekuwa nikiwasaidia kupita kiasi. Ni kwa nini wanataka kushindana na mimi!?” “Wivu!” Nanaa akadakia.

“Sawa sawa Nanaa. Ni wivu tu. Wanataka kukuangamiza. Na ninaona kwa upande fulani wanafanikiwa.” Geb na Nanaa wakakunja uso. “Kivipi wakati sisi tunaendelea na maisha yetu?” Geb akauliza. “Maisha haya ya kubanana hapa!? Si wamefanikiwa kuwatoa pale kwenye nyumba yenu nzuri ya thamani wakawaleta hapa, kwa kuwajengea hofu! Sasa hivi mnaishi kama wao.” Geb alijua wazi anachokifanya mama yake. Nanaa akanyamaza kidogo kama anayejifikiria na mama G akanyamaza makusudi.

Akagundua wote wanamwangalia yeye. “Ila niseme ukweli mama, sasahivi hofu imeisha. Muulize Geb. Alinikuta nikiota ndoto mbaya sana za kubakwa. Nilikuwa silali! Usiku kucha naota napambana. Ilibidi Geb aniombee ili kuweza kutoka hapo.” “Nilifunga Nanaaa. Kwa siku tatu mfululizo nikimuomba Mungu akutetee.” Mpaka machozi yalimtoka Nanaa. “Asante Geb. Kweli nilikuwa nikiteseka. Mpaka nilikuwa nauogopa usiku! Ilikuwa giza likiingia nilikuwa najiambia ndio mateso yangu yanaanza.” “Usilie sasa. Utakaribisha tena hofu.” Walikuwa wamekaa kochi moja. Geb akamvuta mkono na kuubusu. “Huko umeshatoka Nanaa. Hutarudi tena.” “Amina. Na mimi naamini hivyo Geb.” Nanaa akajifuta machozi.

Mama G akafyonza kwa hasira kama asiyejua chakufanya. “Lakini ipo siku yao na wao Mungu atawalipa tu.” Mama G akaongeza kwa hasira. “Wamekuachia kovu baya kumbe ni wivu wao kwa Geb! Wajinga kabisa.” “Lakini mama angalau sasa hivi sioti tena. Nimefunguliwa.” “Kwa hiyo tunaweza kurudi pale?” Mama G akauliza. Geb akamwangalia Nanaa. Nanaa akavuta pumzi. “Tutakuwa wote Nanaa. Huna haja yakuogopa.” Nanaa alishaanza kusugua mikono. “Niangalie Nanaa. Upo salama. Hakuna mtu atakayeweza kutuingilia pale tena. Nimebadili mfumo mzima wa ulinzi na wale wote hawawezi kurudi pale tena.” “Sio pale tu, hawatakaa kurudi kwenye maisha yetu.” Mama G akaongeza.

“Tukalalie kitanda kile kile Geb!? Najiona sipo tayari. Nahisi kama sitaweza kulala.” Tayari machozi yalishajaa machoni. “Hujui unyama alionitendea Malii, Geb. Naumia sijui jinsi yakufanya. Naogopa kuingia kwenye kile chumba najiona kama ndio siku ile ananiingiza kwenye kile chumba nakunifunga mikono yangu.” Geb akajisogeza karibu yake zaidi. “Pole mpenzi wangu. Pole sana.” Geb alijaribu kumtuliza. “Naomba unisikilize Nanaa. Naomba utulie kabisa. Kwanza huna haraka yakuhamia pale. Ni mpaka utakapokuwa tayari. Ila pia nataka ujue kile chumba nilikibadilisha kila kitu. Tena kwa kuchoma moto vitu VYOTE vilivyokuwepo pale ndani usiku ule Malii alipoingia ndani ya chumba chetu. Nilitoa kila kitu kikabakia kitupu kabisa ndipo nikaanza kukifanyia marekebisho. Tokea siku nimekufuata au kukupata pale hospitalini ukiwa umelazwa Muhimbili, nilimwambia Jeri aanze kusimamia hiyo kazi. Nilikuwa niko na wewe pale hospitalini, tukahamia kumuuguza wote Magesa, muda wote ule kulikuwa kuna kazi ikiendelea kwenye kile chumba.” Nanaa akashangaa. Hakuwa hata akijua.

“Kimebadilika sana. Twende ukaangalie. Hata rangi ya chumba nilibadilisha. Hakuna kitu hata kimoja unachokifahamu pale ndani. Kila kitu niliweka kingine. Ukiingia pale hutaweza kujua kama ni kile chumba chetu.” Kidogo Nanaa akaanza kutulia. “Twende nikakuonyeshe. Na nilifanya hivyo kwa ajili yetu, zaidi wewe. Ili usipate hizo kumbukumbu tena.” “Asante Geb. Mimi sikujua!” “Basi ujue kipo na kilikuwa kikikusubiri wewe muda wote. Twende ukaangalie. Utakipenda zaidi.” Nanaa akaanza kutabasamu. Akamshika mkono ili kumsaidia kusimama.

“Nakushukuru Geb mume  wangu.”  Mama G akaguna. Nanaa akacheka sana. “Sasa unaguna nini mama?” “Nisikilizeni Geb na Nanaa. Mnaenda kuangalia chumba na kurudi hapa.” Geb na Nanaa wakazidi kucheka. “Unanisikia Nanaa? Nawasubiria hapa tuzungumze. Sio muende huko, safari moja ianzishe nyingine.” “Mama!” “Mama nini? Kwani siwajui nyinyi? Na hivi ni chumba kipya! Ushashikwa mkono hapa na kuambiwa kimetengenezwa kwa ajili yako! Humtakaa mkarudi hapa.” Nanaa na Geb wakacheka mpaka wakarudi kukaa. 

“Kwanza mimi naona nimalize mazungumzo yangu kabisa. Hizi habari zakuwasubiria nyinyi hapa, hapana.” “Kwa nini unakosa imani na sisi, mama G?” Geb aliuliza huku akicheka sana. “Leo yenyewe mlituchelewesha uwanja wa ndege. Ilibaki kidogo tu tuachwe na ndege. Watu wote tumekaa pale chini hotelini tunawasubiria nyinyi! Simu hampokei, na wakati tuliagana vizuri baada ya kifungua kinywa. Mkasema mnaenda chumbani kwenu mara moja mtarudi baada ya muda mfupi. Hatukuwaona tena.” “Ni Geb huyo!” Nanaa akajitetea. “Mmmh!” Mama G akaguna. “Kweli mama. Ni Geb. Na nilimwambia tutakosa ndege, akasema yeye anaenda na muda.” “Lakini kwani nilikosea? Hatukuachwa na ndege.” Geb na yeye akajitetea.

“Mimi ninachoomba tumalize mazungumzo ndio muende mkaangalie chumba mtakavyo!” Wakazidi kucheka. “Sawa mama. Lakini ujue nimefurahi Geb.Asante kwa kubadilisha kile chumba. Nilikuwa nakiogopa sana. Ndoto zangu zote nilikuwa nikiishia kubakwa pale pale kwenye mazingira ya kile chumba. Kwa hiyo nashukuru sana.” Nanaa akampa na busu la mkono. “Karibu.” Geb akajibu, Nanaa akaendelea.

“Halafu nimefikiria, nimeona tukihamia pale itasaidia pia kwa hiyo siku ya jumamosi. Tutakaribisha wakwe wa Grace kwa uhuru.” Mama G akasimama nakuanza kupiga vigelegele huku akizunguka. “Mama mjanja nyie! Yaani kumbe hiyo ndio ilikuwa shida yako? Turudi kwa ajili ya huo ugeni!” “Kumbe! Lakini pia Nanaa, hapa sio kwako mama. Hapa washakaa watu wengi wa kila namna. Pale ndio kwako. Anza ndoa yako nyumbani kwako na wanao. Jenga familia yako sehemu nzuri ambayo Mungu amewajalia. Majaribu yanatakiwa kukukimbia sio uyakimbie.”“Kweli mama.” “Basi naomba leo tukalale kwetu.” Geb akamalizia kwa haraka. Nanaa akacheka. “Sawa.” Mama G akaanza kushangilia tena. 

“Basi nampigia simu Jeri aje sasa hivi na watu wawili watusaidie kuhama.” Geb akambusu Nanaa mdomoni. “Nakushukuru sana.” “Kumbe na wewe ndio ilikuwa shida yako Geb! Kwa nini hukuniambia?” “Nilitaka mapumziko mazuri. Sikutaka uanze kunililia kwenye fungate nililosubiria miaka yote tokea mtoto.” Nanaa alicheka sana. “Nilikuwa nikizisubiria hizo siku tatu kwa hamu sana. Kwanza ni vile tu tulikuwa na watoto na afya yako inasumbua. Nilitaka tupate mapumziko marefu sana. Tunastahili Nanaa.” “Kweli. Lakini ulisema nikijifungua salama, Jimmy akichangamka tu, tunamwachia mama, halafu sisi tunarudi tena fungate? Au umebadili mawazo.” Nanaa aliongea kwa sauti ya chini ili mama G asisikie.

“Siwezi kubadili mawazo. Ujue mwenzio nimeshaanza kusubiria hilo fungate la pili!” “Kweli Geb?” “Kabisa. Maana hapo utakuwa sio mjamzito. Ni mimi na wewe tu.” Nanaa akacheka kwa sauti ya chini.  Wakataka kuanza kupeana mabusu, mama G akawawahi. “Mimi naona umpigie simu kwanza Jeri.” Nanaa akacheka sana. Geb akasimama na kutoka pale. “Yaani mama nyie!” “Mimi nawafahamu nyinyi. Hata hapo kwenye hilo kochi pia msingenyanyuka leo. Mwiteni Jeri aje, tuhame, muendelee na fungate tukiwa kwenye ile nyumba nyingine. Roho yangu ndio itatulia. Hamtanisikia hata nikiwaita. Na hivi mke wa Jeri anaanza kuja kesho kunisaidia kazi, sitakubugudhi kwa lolote.” “Haya mama yangu.” “Lakini Nanaa, umenifurahisha sana mwanangu. Sasa hivi nina amani yakukaribisha wale wamasai. Angalau wakija kwenye ile nyumba nyingine, heshima itaongezeka.” Mama G na Nanaa wakaendelea kuongea.

Nanaa, Na Umama Magesa!

Geb akarudi. “Jeri atakuja na watu wakutusaidia kuhama. Naomba utulie Nanaa. Mimi na mama tutatafanya kila kitu. Nimemwambia pia amtume mkewe aje.” “Leo!?”  Mama yake akauliza. “Ndiyo leo.” “Mimi nilizungumza naye aje kesho.” “Mwache aje kuanzia leo. Tutamuhitaji tu.” “Njoo Geb nikwambie jinsi nilivyofikiria.” Geb akarudi kukaa.

“Mnisahihishe lakini. Binafsi najisikia kumfanyia kitu kizuri Grace. Amekuwa upande wangu tokea ananifahamu. Amenipenda kwa upendo ambao sijui nisemeje. Ananifundisha mambo mengi bila kunikatia tamaa na...” “Sasa hapo utapandisha pressure!” “Bwana mama!” “Kwa nini unalia jambo la kheri?” Nanaa akaanza kucheka huku anafuta machozi. “Usilie bwana. Haya Endelea. Mimi nataka kukusikia.” “Haya mama. Nilikuwa nasema hata katika wanawake wote aliokuwa nao Geb, Grace alisimama na mi.. ” “Nanaaa!” Geb akashituka kidogo. Mama yake akacheka.

“Nilikuwa na Liz tu!” Nanaa akazidi kucheka. “Akaja na Frida?” Mama yake akaongeza kama kumkumbusha. “Mama na wewe! Mambo hayaishi.” “Ndio utulie.” “Kwani nilirudia tena? Mungu mwenyewe alinichukua akaenda kunifundishia jela!” Nanaa na mama G walizidi kucheka. “Na ulikomeshwa!” “Si kidogo mama. Baadaye nikamwambia Mungu, hili somo angenifundisha kwengine mbona ningeelewa tu? Kwani ilikuwa lazima shule ile nikaisomee jela!?” Nanaa alikuwa akicheka mpaka machozi. “Kichwa chako kigumu. Akaona akikufundishia kwenye mazingira mazuri wewe, usingeelewa. Endelea Nanaa.”  Nanaa akafuta machozi. Geb alikuwa akitingisha kichwa.

“Nataka mimi ndio nishugulikie mambo yote  ya Grace kabla ya harusi yake.” Mama G akapiga vigelegele kwa furaha. “Sijamaliza mama.” “Niambie mama Magesa. Naona umepokea jina na majukumu!” “Sitaki utani.” Mama G alizidi kucheka. “Nakusikiliza Nanaa.”  “Kwa sasa, hapa kwenye haya mazungumzo, naomba uniite mama Magesa, Geb. Sio Nanaa.” Yaani mpaka Geb alicheka. “Sawa mama Magesa. Ehe?” Geb akaongeza huku akicheka. “Basi. Nataka kwanza nimwandalie shuguli nzuri sana. Siku ya mahari, sitaki ahangaike kama anavyohangaika kwenye mambo yetu. Mama umsisitizie atulie na sisi tumfanyie. Nitaomba mnipe namba za simu za mpishi. Yule mama anayetufanyia mambo ya ‘catering’. Nitampigia simu na kumpa idadi ya watu tutakao watarajia, na aina gani ya vyakula tutakavyo hitaji.” Mama Magesa alizidi kufurahia.

          “Nitaandaa pale pale nje. Bustanini. Nitaomba Geb aniletee viti na meza za duara. Nitapamba kama alivyonipambia ile siku ya kikao chetu cha kwanza cha harusi nikaishia kupata matatizo ya miguu.” Kidogo wakatulia. Kama waliokumbuka ile siku. “Nitatengeneza vizuri ili afurahie. Nyinyi mnasemaje?” Nanaa akawatoa kwenye mawazo. Kisha akaendelea kabla hawajajibu. “Pia baada ya mahari tu, nitamwambia asirudi tena kwake. Waje wahamie kwetu. Yeye, watoto na msichana wake wa kazi. Atulize mawazo kwenye harusi tu. Sisi tumsaidie swala la watoto. Asijiguse kwa chochote, ni yeye na Mungu wake tu.” “Hakika hapa umepata mke!” Mama G alisikika kufurahishwa sana.

Nanaa akaanza kucheka. “Umepitisha mawazo yangu?” Nanaa alimgeukia mama G. Akionekana kutaka kumsikia yeye zaidi. “Sio katika hili tu. Nilitaka kukuona kwenye umama, na kuanza kufanya mambo mengine mengi. Kwa kasi hiyo! Hakika umenifurahisha. Lazima kuwa na mipango mbali na kujua Geb anakula nini, uwe unasimama na kufanya mambo kama hivyo. Hakika mtafika mbali sana.

Hongera Geb.” “Mimi mwenyewe siamini!” Nanaa akampiga ngumi kidogo. “Kweli Nanaa. Nimefurahi kuona kuwa unamipango. Tena mikubwa na ya kueleweka. Itanisaidia sana, kuliko kuniongezea kazi ya kuanza kukuvuta katika kila jambo. Hicho ndio kitu nilikuwa natamani. Unaona jambo, unatafuta nafasi yako katika hilo, unafanya bila hofu wala kusitasita. Tutajikuta tunafanya mambo mengi kwa wakati mmoja.” Nanaa akajisikia vizuri sana.

“Hata Grace atafurahi sana. Asante Nanaa.” “Na mimi nimefurahi kama mnaona nimefanya jambo zuri. Najifunza. Ukiona kuna kitu nilitakiwa kufanya halafu nikazembea, uwe unaniambia mama.” “Ukitoa ruhusa ya hivyo, mbona itakuwa aghueni kwangu! Tutasaidiana mambo mengi. Na hivi Grace anaondoka, pengo halitakuwa kubwa sana.” Wakaendelea kuzungumza na kuhama.  

Mahari ya Grace.

Siku hiyo ya jumamosi ilijaa heka heka ya namna yake hapo nyumbani kwa kina Magesa.Nanaa na Mama G walikuwa wakihangaika kuandalia wageni wao. Nanaa ndiye aliyekuwa mstari wa mbele. Akipiga simu huku na kule akiagiza vitu gani viletwe na kuelekeza meza zipangwe wapi na kufanywe nini. Asubuhi Geb alikwenda kazini, lakini Jeri alikuwepo hapo na vijana kadhaa ili kusaidia kazi. Geb alisema Nanaa asinyanyue kitu, aagize tu. Mkewe Jeri ndiye aliyekuwa na watoto pamoja na msichana wa Grace.

Huyo mama ambaye huwa anawafanyia shuguli za catering, aliwahi kufika. Nanaa alishamwandalia meza ya kuweka  vyakula vyote. Iliwekwa barazani kwenye sehemu ambayo ilikuwa rahisi kwa yule mama, na wageni pia kupita na kujichukulia chakula. Hapakuwa mbali na sehemu watakayokaa wageni wote. Kulitengenezwa vizuri sana na kukavutia. Na mbali ya kuwa huwa anawapikia chakula kizuri, alijua kupangilia vyakula vyake. Kwa macho tu, utaridhika nakujiona umethaminiwa kuwepo kwenye hizo meza.

Upande wa kukaa wageni, Nanaa alipatengeneza vizuri sana. Ungependa kuwa mualikwa wa sehemu hiyo. Geb alirudi kutoka kazini akabaki ametoa macho. “Naona mama Magesa mambo yako sio mchezo!” Nanaa akacheka sana. “Usinione hivi! Nipo vizuri.” “Nimekukubali.” Geb alikuwa akipita  nakuangalia kile mkewe alikuwa anafanya. “Tulikuwa na mama hapa. Ameingia ndani muda sio mrefu. Amenisaidia kuweka maua yote hayo na kutengeneza hizo napkins.” “Pamependeza sana.” “Asante. Pole na kazi. Naona umechelewa kurudi!” “Nimekuta kuna mambo mengi! Tangia naingia mpaka sasa hivi wala sijatulia. Ule uji wenyewe ulionipigia simu na kunisisitiza niunywe, nilikuwa naunywa huku nafanya kazi. Wala sikujua nimemaliza ile chupa saa ngapi!” Nanaa akacheka. “Bora uliingia tumboni.” Walikuwa ndio wanafikia mwisho. Kila kitu kilishakuwa tayari. Mama G alikuwa ndani akifanya mambo mengine wakati Nanaa akimalizia hapo nje. Vitu vingi vilikuwa ni vyao. Mama G na Grace walipenda kutumia vitu vyao. Kwa hiyo maua mengi yalikuwa yao na vitambaa. Ni meza tu ndio walikuwa wakikodisha. 

          Kwa kuwa zilikuwa familia mbili  tu, na kwa kina Magesa walikuwa wachache, aliongezeka James tu, hawakuweka viti vingi sana na meza pia zilikuwa chache wakijua watakuwa wachache. “Inatosha Nanaa. Twende tukaoge upumzike.” “Na kweli naona nimechoka. Nahitaji kunyoosha hii miguu.” Wakarudi ndani kuoga ili kupumzika, wakisubiria wageni.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Watoto wa Grace walikuwepo hapo. Kila mtu alikiri wale watoto walibadilika. Walikuwa watulivu sana. Wakati wote walitaka wawe karibu na mama yao. Grace aliwatoa shule. Kwa hiyo siku ya alhamisi na ijumaa walikuwepo tu nyumbani na mama yao. Alishinda nao kitandani siku nzima. Kama kuzungumza na Man kwenye simu, walizungumza akiwa hapo hapo kitandani nakuendelea kucheza na watoto wake. Grace alijaribu kuwachangamsha, wakaishia kuangalia tu tv. Walilala hapo hapo kitandani kwa mama yao kwa siku hizo mbili mpaka jumamosi walipohamia nyumbani kwa kina Nanaa.

~~~~~~~~~~~~~~~~

          Tofauti na walivyotarajia, kina Ole walikuwa wamejiandaa kweli kweli. Kwanza walifika wengi zaidi ya hata walivyofikiria. Japokuwa mama G hakutaka mahari, lakini Mzee Ole alisisitiza ni lazima kufika kutoa mkono wa shukurani kwa kumlea Grace na kufahamiana zaidi. Walifika hapo nyumbani mapema tu. Walikuja wengi, Nanaa akabaki akiangaliana na mama G. “Tutawaweka wapi watu wote hawa!?” Kama Malisa alijua mawazo yao. Akawasogelea. “Kwanza naomba msishtushwe na wingi wa watu. Niwatulize kabisa, hawa watu ni wachache sana. Hawa ni ndugu tu. Tena wakaribu.” Nanaa akaanza kucheka. 

“Wote hao!?” Nanaa akauliza. “Unafikiri nakutania Nanaa? Subiri siku ya harusi utaona. Pili, hawana shida. Masai huwa hawajui kukaa.” Wakacheka. “Mimi huwa wananijaliaga kwangu hivyo hivyo. Wala sijigusi. Na nyumbani kwa Mzee Ole ni kama sebuleni kwao. Kuanzia jumatatu mpaka jumatatu wanapishana hapo nyumbani kwake. Watasimama hivyo hivyo wala hawatahisi kuwa kuna upungufu. Wanachotaka nikuwepo tu hapa. Mzee Ole amechinja ng’ombe leo. Nionyesheni sehemu ya kuziweka, watu walioshugulikia kuzitengeneza wapo njiani wanakuja nazo. Wote hao mnao waona hapo, wanasubiria hiyo nyama kwa hamu sana. Msiwe na wasiwasi juu ya chakula.” Kidogo wakatulia maana walishafikiria kitu cha kuwalisha.

Walikuwa wamejaa, ilibidi magari yao wayaache nje. Ni gari la Mzee Ole tu ndilo lililoingia hapo na Malisa. Wengine waliacha nje magari yao. Kulisikika vicheko kwa masai hao wa mjini, na ni kama wengi waliambizana. Ungejua tu ni masai. Kama hawakuvaa hiki, basi kile chakuwakilisha mila zao. Kulikuwa na wazee baadhi ambao walikuwa wakionekana ni Masai wa mjini lakini walitupia shuka za kimasai. Hata Mzee Ole mwenyewe alifunga lubega. Kama alivyosema Malisa, vyakula vilijaa hapo. Walikula na kusaza. Hata wasiwasi wa kuwa walitoshea vipi hapo haukuwepo. Kila aliyesogezewa kiti, alisema yupo sawa tu, watasimama. Vilijaa vicheko na pongezi kwa Man na Grace. 

Mama G alipokea mahari ndogo, kama walivyoita, kutoka kwa Mzee Ole na mkewe.  Hakutaka pesa kabisa. Lakini walimletea zawadi nyingi tu za thamani. Vitenge vya thamani, hereni zilizokuwa na mikufu pamoja na bangili zakuvaa mkononi. Zilikuwa tofauti tofauti na vyote vilionekana vya thamani na vilienda na vile vitenge pamoja na kitambaa kikubwa cha lesi ya hali ya juu. Zile ‘accessories’  zote waliziweka kwenye mikebe mizuri sana na ya thamani pia. Mashuka mazuri meupe ya ‘cotton’ safi, mablangeti ya kisasa. Moja lilikuwa la umeme, jingine la rangi ya dhahabu lenye manyoya mengi, zuri sana kwa kulitizama kwa macho.  Walileta na vyombo mbali mbali vyakupikia. Na vyote vilikuwa vya umeme. Mama G hakuwa akiamini. 

Aliwashukuru kwa zawadi, zaidi heshima waliyompa. Ndipo mipango ya harusi ikaanza. Mzee Ole aliwakaribisha tu. Hakuta wafanye chochote zaidi ya wao kutokea siku hiyo ya jumamosi. “Man anastahili harusi nzuri. Atafunga kanisani. Nimeshazungumza na mchungaji. Amekubali kufunga hiyo ndoa. Baada ya hapo kaka yake amemuandalia tafrija. Kina Ole tupo wengi sana. Hapa hatujafika hata robo.” Wakacheka.

“Siku hiyo mtakutana na Masai wengi sana. Mjiandae.” Wakacheka tena. “Tutakula nyama mpaka mchoke nyinyi. Kwa hiyo mjiandae kwa hilo pia.” Kila mtu alifurahia. “Malisa, nataka kumuona Grace kwenye shela refu sana.”  Wote wakacheka. “Usijali dad.” Walikula, watoto wakacheza, na kuagana kwa ahadi ya kuja kukutana siku ya jumamosi kwenye harusi.

Maandalizi Ya Harusi Ya Grace.

Hiyo week ilikuwa ni ya heka heka kwa Grace na mama yake. Walitakiwa kutafuta nguo na vitu vya harusi ndani ya siku 4. Mama yake alimtaka pia ajitahidi apate siku mbili zakupumzika ndani bila kutoka wala kufanya kazi yeyote kabla ya siku ya harusi. Malisa naye aliungana nao kusaidia kupatikana kwa gauni na shela aliyoitaka Mzee Ole.  Grace ambaye aliolewa kwenye harusi ya pilau na soda. Tena sherehe ilikuwa hapo hapo kanisani, leo anaolewa tena kanisani na shela ndefu, halafu bwana harusi ni Man ambaye anambembeleza kama yai, hakuna jinsi yakueleza furaha ya Grace. Malisa alihangaika nao, mpaka wakakamilisha mambo yote kwa haraka, ndipo akatulia nyumbani kwa Geb. Akijindaa kwa harusi. 

Yeye na wanae na msichana wa kazi walihamia hapo nyumbani kwa Nanaa kwa juma nzima, kama alivyotaka Nanaa. Yeye Nanaa ndiye aliyesimamia swala la watoto na mambo yote ya mle ndani, wakati Grace, Malisa na mama G, wakishugulikia swala la harusi na hata walipomaliza hakutaka Grace ajisumbue na chochote. Alimwambia ajifikirie yeye tu na aagize chochote atakacho, atafanyiwa.

Grace na Danny

Ilipofika siku ya alhamisi akiwa ametulia ndani akisubiria harusi yake, akapokea ujumbe kutoka kwa Danny. ‘Kesho saa 12 jioni nitafika kuchukua watoto. Tunasafiri jumamosi asubuhi sana. Naomba mwambie Tere, watoto wawe tayari kwa wakati.’ Grace akakaa kwa mshituko. Akaamua kumpigia. “Nisikilize Danny. Weekend ile wakati Geb anaoa, hukutaka wanangu wahudhurie harusi yake. Mimi nilichumbiwa siku hiyo, wanangu hawakuwepo. Weekend hii naolewa. Lazima watoto wangu wahudhurie harusi yangu. Washuhudie na wajifunze kuhalalisha mambo na wajue mahusiano yote ni lazima yafikishwe mbele za Mungu, ili wasidhani sisi wote tuna akili zakufanana. Tunaishi tu na watu bila ndoa.” Kimya.

          “Kwa hiyo, hutaweza kuwapata hawa watoto ijumaa mpaka siku ya jumapili. Utaletewa pale nyumbani. Kwa sasa hatupo pale. Kwa hiyo usije nyumbani kuwachukua siku ya ijumaa. Wataletwa pale siku ya jumapili asubuhi ya saa 4. Ukija hutamkuta mtu hapo.” Kimya. Grace akajua ni jeuri ya Danny, asijue mshituko uliompata mwenzie.

Akili zilimchukua Danny mpaka siku alipomuona Man akibusu shingo ya Grace, mbele yao, baada ya kukamilisha talaka. Kitu kilimtembea Danny kutoka utosini mpaka kwenye unyayo. Akahisi kuishiwa nguvu. Uzuri alikuwa amekaa kwenye kiti, ofisini kwake. Akahisi giza machoni lakini akashangaa kuona mikono ya Man, imepita kwenye kiuno chembamba cha Grace huku amemuegemea begani, akiwa amesimama nyuma ya Grace, karibu sana, wakati mama G akizungumza naye. Akashangaa kwani siku ile alikuwa kama hajaona. Lakini leo ile picha ikajirudia sawia. Man alinong’ona kitu sikioni kwa Grace, kisha akambusu kichwani. Akakumbuka kuona tabasamu usoni kwa Grace baada ya kunong’onezwa. Hilo likamjia tena Danny.

Grace akaangalia simu kama imekatwa. Akaona bado. Danny maneno mengi yupo kimya! Grace mwenyewe hakuamini akaona ni wakati mwafaka wakuendelea kumuweka sawa. “Na ninakuonya Danny, acha kupiga wanangu. Kama unamahasira yako, jimalizie wewe mwenyewe. Acha kabisa kutesa watoto na kuwanyima raha. Usifanye wanangu kama watu wazima nakushindwa kucheza! Hapana Danny. Kama wewe umeshindwa kuona wanangu wakizungumza kwa uhuru, na kucheza, basi niachie mimi mwenyewe mpaka watakapokuwa watu wazima ndipo uwatafute. Acha kujifanya kama umechanganyikiwa.” Grace akakata simu.

Danny hakujua ile simu ilikatwa saa ngapi, ila simu ya Sara ndio iliyomtoa mawazoni. Mambo mengi yalikuwa yakipita kwenye akili za Danny baada ya kumsikia Grace akimwambia anaolewa. Alipigwa na butwaa asielewe imekuaje au ni nini kinaendelea kwenye maisha yake. Kwa dakika kadhaa ni kama maisha yalipoteza dira bila yeye kujua. Kama ndio anatoka usingizini, akiwa bado haelewi vizuri. Ndio alikuwa ameingia ofisini asubuhi hiyo ya saa mbili. Alipofika tu ofisini alikusudia kuwa jambo la kwanza nikumtumia ujumbe Grace juu ya watoto kabla kazi kuchanganya hapo ofisini, akasahau. Kwani alikuwa akisafiri jumamosi. Kwa hiyo alitaka kuweka mambo sawa juma hilo ili akirudi kazini asikute viporo vingi, kwa hiyo alikuwa na kazi nyingi. 

Alipoangalia simu wakati anataka kupokea simu ya Sara, akagundua tayari ni saa tatu na nusu. Inamaana alibaki ameduaa pale zaidi ya lisaa! Grace alipiga na kutoa taarifa za kuolewa kwake. Hakujua hata alichoendelea kuzungumza baada ya pale lakini alijua hawezi kupata watoto siku hiyo ya ijumaa kwa kuwa jumamosi wanatakiwa kuhudhuria harusi ya mama yao.

“Grace anaolewa!?” Danny akawaza kwa sauti, asijue ni kwa nini. Lakini hata masikio yake yakasikia.  Hakuwa tayari kuzungumza na Sara kwa wakati ule. Alimuacha amelala. Lakini ni kama  alijua sababu ya kupigiwa simu mida ile. Akajua ndio ametoka usingizini. Kama alikuwa akimuona pale kitandani alivyokuwa amejifunika kama mgonjwa huku ameegesha simu yake sikioni. Akaamua asipokee.

~~~~~~~~~~~~~~~~

Mama G akaingia. “Mbona umeamka na hasira? Kwema?” Mama yake akakaa. “Si Danny anataka kuniletea ujinga mimi! Eti anataka watoto kesho. Kwa maana nyingine wanangu wasihudhurie kwenye harusi yangu, wote tuonekane tunaishi na watu tu bila ndoa! Unafikiri tutakuwa tunakuza watoto wa namna gani?” “Kwa hiyo mmefikia vipi?” “Nimemwambia aende akachukue watoto pale siku ya jumapili saa 4 asubuhi.” “Sasa atawarudisha lini?” Grace akabaki kimya.

“Ukumbuke utakuwa kwenye fungate.” “Nilizungumza na Man, tufanye fupi ili tuje tuwahi watoto. Tutapata mapumziko ya siku chache, halafu tunarudi. Na yeye alisema atarudisha watoto hiyo siku ya ijumaa. Aliwataka kwa siku 7 tu.” “Sasa ijumaa utakuwa umerudi?” Grace akafikiria kidogo. “Itabidi niwepo mama, ili niwe na wanangu na yeye asipate sababu.” “Sawa.” Nanaa akaingia.

“Kwema bibi harusi?” Nanaa akauliza. “Basi mama nipishe hapo mimi ndio nijilaze, wewe kakae pale kwenye kochi.” “Lakini umenikuta Nanaa.” “Mama naye! Mimi mgongo unaniuma.” “Si ukalale chumbani kwako?” “Naona uvivu bwana mama. Sogea.” “Nanaa naye!” Grace akaanza kucheka. “Nataka kulala na Grace.” “Umbea tu! Unataka kujua alikuwa anagomba nini asubuhi hii.” Nanaa akaanza kucheka. “Muone. Wewe kakae pale utasimuliwa.” “Sitasikia raha nikiwa mbali na nyinyi. Havitanoga. Wewe nenda kakae pale kwa kuwa ushasimuliwa, sasa hivi zamu yangu.”

“Nanaa acha umbea wewe mtoto! Ndoa itakushinda.” “Akuu! Nishamuaga mpenzi wangu vizuri tena kwa kituo. Usinione hivi. Shule yako  na ya Grace mbona nimeielewa?” “Sasa yuko wapi?” “Atakuja kukuaga sasa hivi, kabla hajaenda kazini.” Nanaa akajilazimishia hapo kitandani, akamsukuma mama G kidogo mpaka akapata nafasi hapo kitandani. Akalala pembeni ya Grace. Lakini mama G hakuondoka.  “Nanaa yupo huku?” Wakasikia sauti ya Geb. “Wewe si ulisema umeaga wewe!” Nanaa akaanza kucheka. “Njoo mpenzi wangu. Ni mama huyo!” “Nanaa wewe mtoto! Mimi nimefanyaje?” Geb akaingia mpaka pale. “Umesahau kunywa dawa. Umeziacha pale mezani. Naomba kaa unywe sasa hivi kabla sijaondoka.” “Mwenzio kaletwa na umbea ndio maana dawa kasahau!” Nanaa akakaa huku anacheka. “Mama hana dogo!” Nanaa akapokea dawa.

“Vipi G?” “Si Danny anataka kuniletea ukorofi.” Grace akamsimulia kaka yake kila kitu. “Nataka kuwa na wanangu Geb. Wanione ninaolewa.” “Hata kama hatakubali hapa hawezi kuingia kwa kuwa hataruhusiwa. Na siku ya harusi hawatatoka hapa mpaka jioni. Naomba utulie. Pata muda wakupumzika. Acha kuwaza mawazo unayojua yatakunyima raha.” Grace akatulia.

          “Lakini Grace amezungumza jambo kubwa sana. Nyinyi mnaweza msione kwenye ulimwengu wa roho. Lakini kuna roho za kurithi. Lazima kusimama na kumlilia Mungu juu ya hili. Mnaweza msielewe ni kwa nini nilikuwa mkali sana kwa Grace, kujitunza mpaka ndoa. Nilijua yale niliyoyafanya mimi na baba yenu. Sikutaka hiyo roho ihamie kwa Grace. Naona tukajitahidi wee, vikawezekana kwa Danny lakini kwa Man tukarudi kule kule.” Grace akanyamaza.

“Nanaa na Geb, na nyinyi watoto wote mmepata nje ya ndoa. Jamani hiyo ni roho! Lazima tuikatae na iishie kwetu tu. Kwa Grace iwe mwisho. Tumlilie Mungu isiende kwa kizazi cha tatu kina Fili na Oliva! Lazima kufanya juhudi za makusudi kumlilia Mungu. Kwa kutubu haswa, ili Mungu aturehemu. Mnaweza msione sasa hivi, lakini inauma sana ikitokea kwa mtoto uliyemzaa wewe. Ukiwa wewe unafanya hivyo, unajihesabia haki nakuona ni sawa kwa sababu hii na ile. Sasa subiri aje afanyiwe hivyo Oliva au aje aishi hivyo Fili. Inauma sana. Tuombeni rehema.” Kulizuka ukimya wa gafla kila mmoja akiwaza lake.

Geb alibaki amesimama kama sanamu. Mama G aligusa pabaya. Oliva! Liv wake aishi na mwanaume bila ndoa! Akahisi ataua mtu. “Ndio tunafanyaje?” Geb akauliza. “Lazima kukiri kuwa ni kosa. Tutubu kabisa. Ingekuwa tumefikiria hili kabla, Nanaa na wewe, mngetubu kwa pamoja mbele ya mchungaji kabla hajawafungisha ndoa. Lakini hamjachelewa. Mpate muda nyinyi wawili, mtubu. Kwa kumaanisha na kumsihi Mungu arehemu kizazi chenu chote.” Akamgeukia Grace.

“Wewe na Man, mnayo nafasi. Zungumza na Man, kabla mchungaji hajawafungisha ndoa, mtubu. Mungu awasamehe kwa kuwa mlitenda dhambi. Nyinyi mnataka ndoa takatifu, basi muingie mkiwa mmejitakasa.” Grace akavuta pumzi kwa nguvu. “Nitazungumza na Man.” “Sawa na pia itabidi mkishatulia. Tutafute siku moja ambayo wote tutafunga na kuombea kizazi chetu. Katika hilo eneo tu.” “Wazo zuri.” Geb akachukua glasi kutoka kwa Nanaa, na kumbusu mdomoni. “Utanipigia ukifika kazini?” “Nitakupigia.” Geb akamjibu Nanaa. Akambusu mama yake kichwani pale alipokuwa amekaa. “Uwe na siku njema. Ulinzi wa Mungu usiondoke kwako. Uzidi kufanikiwa.” “Amina mama.” Geb akatoka.

“Mimi naomba tuombeni mama. Wala tusisubiri siku nyingine. Leo leo tutubu. Tutubu kwa niaba ya Geb & Man. Grace aliniambia maombi ya mama yana nguvu sana. Mimi naombeni tuombe mama. Tutubu na tuombee watoto wetu. Hiyo roho ikome kabisa.”   Wakaanza kutubu. Waliomba hao wanawake watatu bila kuchoka. Grace na mama yake walipiga magoti, Nanaa alikuwa amesimama akizunguka hapo chumbani. Walimuita Mungu na kumsihi awasamehe.

Sara kwa Danny!

Huwezi kukwepa simu ya Sara, hasa akikusudia kuzungumza na wewe. Labda uzime simu yako. Napo Danny alijua endapo atazima simu, baada ya muda mfupi atakuwa amefika hapo ofisini kwake. Aliendelea kupiga kama nyumba inawaka moto na yeye amefungiwa ndani. Mwishowe Danny akaamua apokee tu japo alijua ni nini anataka. “Ni nini Sara?” “Kwa nini hupokei simu zangu sasa!?” “Wewe si unajua kama nipo kazini?” “Mimi ni mpenzi wako, natakiwa unipe kipaumbele. Kama nina tatizo je?” “Unataka nini?” Danny akaona afupishe maneno. Alikuwa amepoa kama sio yeye Danny. 

“Mbona hujaniachia pesa ya matumizi?” “Matumizi gani?” Danny akauliza. “Uliza wanaume wenzako wote hapo ofisini kama wanaondoka majumbani kwao bila kuacha pesa! Wewe vipi Danny?” “Kwa kuwa wake zao wanamatumizi ya hizo pesa. Kama kununua chakula ili wapike, au sabuni ili wafue nguo na kusafisha. Wewe hayo huyafanyi. Na kama ni pesa za matumizi yako binafsi nimekupa juzi. Ukasema umemaliza pesa yote kwenye nywele, kununua nguo za ndani na kubadili kucha. Nikakuuliza kwa hiyo umekamilisha kila kitu, ukasema ndiyo. Sasa ndio nakuuliza, unataka pesa ya nini tena?” Danny alimuuliza taratibu tu.

“Ikitokea dharula?” Sara akauliza akionyesha kuishiwa nguvu. “Dharula ipi na wewe ndio unaamka? Hata kitandani bado hujatoka! Gari yako nimejaza mafuta. Sasa unazungumzia dharula ipi?” “Huwezi kujua.” “Basi utakapojua, utanipigia tena simu. Naomba kurudi kazini.” Danny akakata simu. Baada ya sekunde kadhaa ikaanza kuita. Sara tena.

Danny akapokea. “Mbona unanikatia simu!?” “Nimekuaga Sara. Labda kama unataka ugomvi tu na mimi?” “Unanidharau Danny. Unaniona mimi sina maana sababu sijapata kazi.” “Sema huna kazi. Ukisema ‘sijapata’, inamaana umetafuta halafu umekosa.” Ukaanza ugomvi asubuhi hiyo hapo kwenye simu. Sara yupo nyumbani kwao, kitandani amelala, anamlalamikia Danny anamdharau. Danny yupo ofisini, kazi haziendi analumbana na Sara.

Man kwa Grace.

Moyo wa Grace ulijawa furaha mara baada ya kuona simu yake ikiita na Man ndio mpigaji. Akapokea kwa haraka. “Mbona unasikika kama huna furaha?” Man akamuuliza Grace asubuhi hiyo alipompigia simu. “Hapana nipo tu sawa. Usiwe na wasiwasi. Vipi umeamka salama?” “Nimeamka salama. Sema nimechelewa kukupigia simu sababu kuna mambo nilikuwa nafanya tokea saa 10 asubuhi. Nilitingwa.” “Pole. Nini tena?” Grace akauliza. “Ni mambo tu ya hapa. Ila nimesharekebisha.” “Utarudi kulala?” Grace akauliza akisikika kujali. “Siwezi. Nataka nikazane kufanya kazi niache mambo sawa. Ili nikija huko akili ziwe kwako tu sio niwe nawaza na huku.” Ilimgusa sana Grace. “Nina hamu na wewe Grace, mpaka nahisi kuchanganyikiwa. Nishazoea kuamka pembeni yako.” “Pole. Tumebakisha siku chache tutakuwa wote. Na mimi nina hamu na wewe Man.” Nanaa na mama G wakatoka kuwapisha.

“Ila sipendi hivyo unavyosikika. Umekasirika kwa kuwa nimechelewa kukupigia simu.” “Hata kidogo Man. Najua upo kazini mpenzi.” “Ni nini sasa?” Man akaendelea kuuliza kwa kubembeleza. “Tutaongea ukija.” “Hapana. Nikija nakuhitaji wewe Grace. Naomba tumalize matatizo yote kabla ya siku yetu.” Grace akatulia. “Niambie tu.” “Labda ukapumzike. Ukiamka ndio tuzungumze.” “Nilikwambia sitarudi kulala Grace. Na siwezi kutuliza mawazo kama nikijua kuna jambo linakunyima raha.” “Sio kuninyima raha. Ni jambo la kuzungumza tu. Ila nahisi Danny naye alinikera asubuhi alivyonipigia.” “Ni nini tena?” “Nafikiri pia nimemchukia tu. Hakuna baya amefanya. Ila alitaka watoto ijumaa wakati harusi yetu ni jumamosi. Nimemkatalia.” “Ikawaje?” Man akaendelea kuhoji taratibu.

“Sidhani kama tatizo ni hayo mazungumzo. Ni kile kitendo tu cha kumfikiria kuwa nitakuwa naye daima na hawa watoto! Hilo linanikera Man, siwezi kujisaidia. Halafu anapiga sana wanangu, hilo ndilo linaniumiza zaidi. Watoto wamebadilika. Fili ananiambia huwa anawachapa sana. Najilaumu naona ni tabia niliyofungia macho tokea kwa Fili, sasa sasahivi ndio mbaya zaidi kwa kuwa sipo nao kipindi hiki. Nawaza akishawachapa hivyo, ni nani anakuwepo kuwatuliza? Fili ndio anawabembeleza wadogo zake! Naumia Man. Na makosa yenyewe wanayochapiwa hawa watoto, ukiwauliza au ukimuuliza dada yao, ni ya kitoto Man. Kuruka au kucheza! Kweli? Sasa sijui wameingiwa na hofu, unajua hawataki hata kucheza? Wamekaa tu hapa kama wajinga! Hawa mapacha mpaka wamejifunza kunyonya vidole. Nahisi ni kama njia yakujiliwaza. Naumia sana Man.”

“Naomba usilie Grace. Umebaki muda mfupi sana tutakuwa nao. Hesabu siku. Halafu hatujachelewa. Tukiwa nao, tunaweza kuwarudisha wakawa watoto wa kawaida. Kuwaambia kwa vitendo kuwa ni sawa kucheza, kuzungumza wanachofikiria na mengineyo. Nakuhakikishia watarudi kwenye hali ya kawaida. Usihofu mpenzi. Nikifika tu jumamosi nitakuja kuwachukua, nikae nao kidogo, kabla ya harusi.” “Sidhani kama watakubali Man. Wameingiwa hofu, wapo kama wanaogopa watu! Wamening’ang’ania hawataki hata niwaache kwa dakika 5! Wananifuata mpaka chooni!” “Basi baada ya harusi, wakirudishwa tutapata muda nao. Kila kitu kitakuwa sawa. Umenisikia?” Grace akatulia.

“Sawa.” “Na nini tena?” Man akaendelea kuuliza. Grace akamueleza kila kitu juu ya yale aliyoambiwa na mama yake. Man alitulia akisikiliza. Hakuwa hata na wazo. Hakujua kama ni dhambi. Kwanza si anamuoa? Tatizo liko wapi akila vyake kabla ya ndoa! Akasikiliza hapo, kimya. “Man!” “Nipo mama. Nasikiliza.” “Sasa upo tayari kutubu?” Man akaanza kucheka. Bwana Man!” “Kwani si nakuoa mwenyewe? Tatizo liko wapi?” “Kwa hiyo unataka tukija kuzaa watoto wetu, labda tuseme ni wakike, aje afanye kama sisi? Aanze maisha ya ndoa kabla ya ndoa, ni sawa?” “Nitamchoma mkuki huyo mwanaume. Na nitahakikisha hatawahi kuja kulala na mwanamke mwingine tena.” Grace akaanza kucheka. Alicheka sana.

“Acha kutoa mifano hatarishi bwana Grace! Ujue mdomo unaumba?” Grace alizidi kucheka. Akili ya Man ilirudi likizo kwa haraka. Gafla maandiko ya bibilia yakaanza kumrudia.  “Ujue imeandikwa kwenye  {mithali 18:21 Mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi; Na wao waupendao watakula matunda yake}.”  Grace alizidi kucheka. “Acha kutamka hivyo kwa binti yangu!” “Ndio uje tukatubu halafu tuanze kutamka uzima.” Hapo Man akapoa na kukubali kwa haraka. “Na ukemee kabisa hiyo roho.” Grace akazidi kucheka. “Umesikia Grace?” “Uje tukemee wote.” “Wewe anza. Nitakuja kuongeza nguvu.” Grace alizidi kucheka.

Siku Ya Harusi Ya Grace & Man

Man alitua jijini siku ya jumamosi asubuhi  tayari kwa harusi. Grace hakutaka kwenda saluni. Aliletewa watu pale pale nyumbani. Walihamia nyumba ndogo ya kina Geb ili kuwa huru kutengenezwa. Walikuwa wakisimamiwa harusi na kaka yake mkubwa Man, na mkewe. Kwa hiyo mke mwenzake Grace na wasimamizi wa kike walikuwepo hapo           kwenye hiyo nyumba tokea asubuhi wakitengenezwa. Ni kama walihamisha saluni ya huyo dada kwenye nyumba hiyo.

Alikuwa na wasaidizi wengi wa kumsaidia mambo ya nywele, kucha na makeup. Alikuwepo hapo na marafiki zake. Malisa naye alifika mapema kidogo kuhakikisha kila kitu kipo sawa. Hakika      alishugulika   mpaka mama G akamshukuru. Alionekana alikuwa na kazi nyingi sana. “Pole mama. Pole sana.” Malisa akacheka. “Asante. Nimeamka saa 11 asubuhi mama yangu, na nililala saa 7. Mzee Ole anapenda vitu vizuri sana. Sitaki afike kanisani au ukumbini aanze kugomba. Maana huwa hanaga aibu yule. Asipopenda kitu, hafichi.” Wakacheka.

Hakika Grace alipendeza. Alikuwa kama binti mdogo. Geb aliwanunulia watoto wake suti nzuri sana. Tena zilifanana na Magesa. Oliva kama kawaida yake alipendeza usingechoka kumtizama. Alifundishwa kumwaga maua. Nanaa ndiye aliyekuwa mwalimu wake wa kwanza. Alikuwa akimfundisha kumwaga hayo maua lakini yeye akashindwa kumfundisha Liv. Ilikuwa ndio kazi yake week nzima hapo nyumbani. Baba yake alinunua mengi. Akawa na kazi yakufanyia mazoezi. Anatembea hatua mbili anamwaga katikati, kulia na kushoto. Hapo atacheka mpaka anakaa chini, kuja kuamka hapo, Nanaa ambaye ni mwalimu anakuwa ameshachoka. Wote wanacheka. Atagaragara kwenye hayo maua na kuyamwaga yote chini kisha anayalalia. Huku akitaka mama yake amwangalie. Nanaa alimwambia Geb hadhani kama Liv ataweza. Heri atafutwe mtoto mwingine. Yeye anafanya mchezo. Geb aliamua kumfundisha yeye mwenyewe. Tena hakuchukua hata muda mrefu, Liv akaweza. Alikuwa akimwaga huku akicheka lakini sio kukaa chini.  

~~~~~~~~~~~~~~~~

Man alishafika kanisani mapema, akabaki akimsubiria Grace wapate muda wakutubu mbele ya mchungaji kabla ya harusi. Ilikuwa wafanye hayo yote siku moja kabla, lakini bado Man alikuwa na majukumu huko Arusha akashindwa kufika siku ya ijumaa. Malisa alimtuliza na kumwambia atamfikishia hapo bibi harusi mapema tu tena akiwa amependeza. Waliingilia mlango wa nyuma ili kufika ofisi ya mchungaji. Man na Grace wakaeleza kuwa wanahitaji kutubu. Wakapiga magoti, wakaombewa ndipo wakahamia kanisani kwa ajili ya kufungishwa ndoa.

Hakika watu walijaa hapo kanisani na kushangaza familia hiyo ya Magesa. Wazee walivaa suti za maana lakini walitupia mashuka ya kimasai begani. Mzee Ole mtu wa watu, kila mtu alitaka kuhudhuria. Liv alifanya kama alivyofundishwa na baba yake, Geb alikuwa akimpiga picha na kumchuku video. “Dad!” Liv alimwita baba yake mara alipomuona. Nanaa akaanza kucheka. “Basi hapo tena kazi ndio imeisha. Geb asingemsogelea au asingeingia huku ndani kumpiga picha. Angebaki huko huko nje alipo Grace! Ataacha kile kikapu pale pale chini ili abebwe.” Mama G akacheka. “Nimemsikia akizungumza naye asubuhi. Akamwambia baba yake ameelewa. Na hivi hasahau, subiri tuone.” Wakabaki wakimwangalia. Wasimamizi walishaingia wote.

Ilikuwa zamu ya Grace kuingia. Liv ndiye aliyekuwa msimamizi wa mwisho kupita hapo akimwaga maua ili apite bibi harusi na baba yake, ambaye atasimama Geb, badala ya Mzee Magesa, kumkabidhisha kwa Man. Sasa Geb aliamua kwenda kumpiga picha na kumchukua video mwanae, wakati akifanya hilo zoezi, ndipo arudi amshike mkono dada yake amwingine ndani, ibada ianze. Liv alikuwa akimwaga maua kila sehemu ambayo anti yake anatakiwa kupita. Alimwaga na kumpungia mkono dad wake, Geb naye anampungia ndipo anamwaga tena. Alifanya hivyo mpaka akafika pale mbele, baba yake akaondoka.

Kama aliyekumbuka kitu. Akarudi nyuma kidogo, akaonekana anahesabu hatua mpaka mbele kabisa madhabahuni, katikati. Akamwaga kulia na kushoto. Akasimama. Hapo baba yake alishaondoka. Kabla ya ibada kuanza, Malisa na Geb waliingia hapo ndani kumfanyia mazoezi. Wakajua amekumbuka. Wakampigia makofi. Akacheka. “Sasa pale ndio mwisho wake mama. Muone.” Liv alimaliza kazi yake kwa wakati ule. Ila pakusimama ndio ukawa mtihani kwake. Aliangalia upande aliotakiwa kusimama na wasimamizi wa kike, hakuona sura anayoifahamu hata moja. Wakamwita. Akacheka tu hata kusogea. Nanaa akajua tarayi. 

          Bado alikuwa amesimama katikati. “Usimwangalie mama. Akituona tu, atakuita palepale mbele ukambembe. Inama.” “Anatafuta sura ya mtu anayemfahamu.” “Nakumpenda yeye. Lasivyo bibi harusi atamkuta palepale.” Nanaa akamaliza kwa kunong’ona. Man aliyekuwa amesimama upande wa wanaume akamwita. “Liv!” Akamgeukia na kucheka. “Njoo!” Akamchekea tena na kumsogelea Man. Fili alikuwa pembeni yake na wadogo zake, wametulia sana kama sio wale watoto wa Danny. Alipowaona na wale watoto, akafurahia. Kakaenda kusimama pembeni ya Man na kina Fili. Ni yeye peke yake msimamizi wa upande wa kike aliyekuwepo upande wa kiume. Matron au msimamizi wa Grace alikwenda kutaka kumchukua. Akamnong’oneza Liv kitu. Liv akamwangalia Man akiwa ameshabadilika rangi. “Akimgusa tu, atalia. Na akilia yule, tutabeba mpaka harusi iishe. Nimfuate?” Nanaa akataka kusimama. “Mwache kwanza.” Wakamuona Man anamnong’oneza kitu yule shemeji yake ambaye ni msimamizi wa Grace. Wakacheka,  na kuondoka pale kurudi alipokuwa amesimama. Akamuacha Liv, uso umeshakuwa mwekundu. Cheko imeisha.

Watu  wakasimama baada yakusikia wimbo ulioashiria bibi harusi anaingia. Geb akiwa amemshika Grace mkono wakaanza kuingia taratibu. Hakika walipendeza. Ile shela ndefu aliyoitaka Mzee Ole, alivaa Grace. Ilikuwa imebebwa na watoto wanne nyuma. Walipofika katikati ya Kanisa, wakaiachia. Ilisambaa vizuri, Grace akawa anaivuta kwa mwendo wa taratibu. Ilikuwa ni shangwe ya namna yake. Mzee Ole alisikika akishangilia pia. “Hapo amependa!” Malisa akanong’ona. 

Liv alifurahi sana kumuona baba yake. Akaweka kikapu cha maua chini. “Dad!” Geb akampungia mkono kwa chini kidogo. Alicheka kwa sauti kisha akaweka vimikono vyake juu akishangilia kama amepata mkombozi. “Pale ujue ndio kamaliza mama. Sidhani kama ataendelea! Hawezi kusimama na wale watu asiowajua ndio maana alikwenda kwa Man.” “We subiri.” Geb akamfikisha Grace mikononi kwa Man, akarudi alipokuwa amekaa  Nanaa na Mama yake.

“Dady!” Hapo Liv alikuwa amenyanyua mikono juu, uso mwekundu tayari. “Pale amemaliza yule. Muone upande aliokaa, na kikapu kaweka chini. Mikono yote juu anakuita. Nenda kamchukue kabla hajaanza kulia pale mbele.” Nanaa akamnong’oneza Geb. Geb akasimama na kumfuata pale mbele. Akainama kumnong’oneza kitu. Wakamuona Liv anambusu baba yake shavuni. Akaokota kikapu na kuhama upande. “Ahaaa!” Nanaa akashangaa sana. “Jamani nyie Liv anakusudi huyu mtoto!” Mama G alizidi kucheka.  Geb akarudi kukaa.

 “Lazima uniambie ulichomwambia Liv akakuelewa kwa haraka kiasi hicho! Hakika kama mimi ningemfuata pale, tungetumia zaidi ya nusu saa kuelekezana na pia asingekubali kubaki pale.” Geb akacheka. “Ila anakusudi Liv nyinyi! Anachagua nani wakumuelewa na nani asimuelewe.” Nanaa akalalamika kidogo. “Liv hana tatizo la kuelewa hata kidogo.” Geb akaongea kwa kusifia, Nanaa akabaki bado haamini. Alikuwa ametulia,  upande wa wasimamizi wa kike na kikapu cha maua kashika mkononi. Hakuweka chini tena. Kila wakati alimpungia baba yake mkono mwanzo wa ibada mpaka mwisho. Wakati wakutoka alimwaga maua baada ya wasimamizi wote kutoka. Yeye akawa wa mwisho kabla Man na Grace hawajatoka. Akamwaga huku akimwangalia baba yake aliyekuwa mbele yake akimpiga picha na kumchukua video.  Alikuwa akicheka sana huku akimwaga maua na kumpungia baba yake mkoni. Na vile alivyopendeza, ungependa kumpiga picha.  Kila mtu alikuwa akicheka na yeye alikuwa akicheka zaidi lakini anamwaga maua.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Kufika saa kumi jioni, Grace akawa mke halali wa Man na si Danny tena. Zilichezwa ngoma za kimasai hapo nje ya Kanisa, kama wapo Masaini. Japo kulikuwa na minong’ono mingi ya kuwa inawezekanaje Grace kuolewa tena kanisani akiwa alikuwa na ndoa ya kwanza ya kanisani? Ndoa za wakristo hazivunjiki! Walilalamika. Wengine walisema ni sababu ya utajiri wa Mzee Ole, amehonga Kanisa. Wengine walisema aliachika kihalali sababu ya kosa la uzinzi. Wengine walisema Kanisa hilo limefanya upendeleo kwa Mzee Ole, sababu ya michango yake hapo kanisani, ingekuwa ni mtu masikini au muumini tu wa kawaida, basi Kanisa lisingekubali kufunga ndoa ya aina hiyo.

Basi ikawa ulalamishi wa hapa na pale wa chini chini. Wengine wakijiuliza inawezekanaje kijana kama Man kwenda kumuoa mama mwenye watoto watatu kama Grace wakati alikuwa na uwezo wakuoa binti mdogo tena mzuri tu zaidi ya Grace!? Wakuendelea kusengenya waliendelea, lakini Man alishapata mke. Waliocheza walicheza mpaka jasho lilikuwa likiwamwagika. Grace ni wa Man! Nyimbo za kimasai ziliimbwa ndipo wakaelekea kwenda kupiga picha. 

Wakiwa kwenye kupiga picha, Man na Grace walibadilisha nguo wakavaa za kimasai. Hakika walipendeza na mavazi hayo ya asili. Walipiga picha nyingi sana. Na watoto wa Grace pia walikuwepo kwenye kuweka kumbukumbu ya siku hiyo. Man alianzisha familia akiwa amempokea Grace na watoto wake wote. Picha nyingi walipiga wakiwa wamebeba wale watoto kama ni wa Man na Grace waliozaa pamoja.

Ukumbini!

Walipotoka hapo ndipo wakaenda ukumbini. Hapo ndipo walikutana na Masai halisi. Wengi walivaa kimasai. Wazee kwa vijana. Wanawake kwa wanaume. Hapakuwa na wavaa suti wengi. Wengi walivaa kimasai. Ilikuwa ni hoteli kubwa kama ile anayosimamia Man kule jijini Arusha. Lakini hiyo alikuwa akisimamia kaka yake. 

Kulijazwa nyama kama alivyosema mzee Ole. Nyama za kila namna zilikuwepo. Vyakula vingine vilikuwa vichache, lakini nyama ndizo zilijaa. Grace alikuwa akitembezwa na Man hapo ukumbini kusalimia watu mbali mbali. “Kweli Grace safari hii amebahatika!” Nanaa alinong’ona. “Na ameingia kwenye ukoo mkubwa! Na wanaonekana wana umoja sana.” Mama G akaongeza. 

Nanaa akaanza kucheka. “Unacheka nini?”  Geb akauliza. “Muone Magesa. Ameshiba mpaka anasinzia na nyama mkononi. Mtoto kwa kula huyo!” “Sijui karithi wapi!?” Geb akauliza. “Mimi hata sijui!” Nanaa akajibu huku aking’ata nyama. Geb na mama G wakacheka. “Utafikiri hujala mwaka!” Mama G akamchokoza Nanaa. Alikuwa anakula kwa juhudi zote. James alikuwa akimwangalia dada yake na yeye anacheka. “Mambo kama haya hayatokea kila mara. Acheni mimi nile jamani. Meza imejaa nyama na wahudumu wanapita kila mara kubadilisha aina ya nyama! Mungu anipe nini mimi Nanaa!?” “Basi mwangalie mwanao. Kashiba, lakini hataki kuweka nyama chini.” Nanaa alikuwa akicheka huku wakimwangalia Magesa. Geb akajaribu kutoa ile nyama mkononi, Magesa akapiga kelele akitaka nyama yake. Wakazidi kucheka. “Mwacheni mwanangu. Kula baba. Kula ni karama ya Mungu. Hata mbinguni tutakuta kuna kula.” Nanaa aliongea huku akiendelea kula zile nyama.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Mzee Ole alipewa nafasi ya kuzungumza. Akamshukuru sana Man kwa heshima aliyompa. “Nilikuwa nikiogopa kufa kabla sijamuona Man akioa. Mama yake alinitia moyo akasema nizidi kumuombea. Lakini siku zilizidi kwenda bila kuona matunda. Niliposikia yupo Grace. Nikasema hiyo ndio Grace yangu mimi. Mungu amenirehemu kabla sijafa. Nikamwambia mama yake, Mungu ametuletea Grace, ndio muujiza wangu. Maana huyu Man, bwana! Hapakuwahi hata kutokea fununu ya mwanamke!” Watu wakaanza kucheka.

“Kila siku nauliza vipi huko Arusha, hujapata mtu? Majibu hayaeleweki! Sasa niliposikia tu yupo Grace, nikasema niletewe haraka sana. Nilipomuona tu, na mama Ole alipokaa na Grace kwa muda mfupi tu, akasema huyu ndio mke wa Man.” Watu walianza kushangilia. Vigelegele huku wakicheka.

“Tukakubaliana siku ya leo. Mvua inyeshe, jua litoke, lazima Grace awe Ole.” Watu wakashangilia sana. “Sikutaka habari ndefu. Nikaita wanangu. Wakagawana majukumu. Na nyinyi mliponiambia mpo tayari kuja kuungana na mama yake Man, kumchukua Grace, nikasema asante Yesu wangu. Nashukuruni sana kwa kuja. Sasa Grace!” Akamgeukia Grace. “Karibu mama. Karibu kwenye ukoo huu mkubwa sana kama unavyotuona. Nawaombea maisha marefu na uongozi wa Roho mtakatifu.” “Asante na amina baba.” Grace aliitika taratibu. Vikainuka tena vigelegele.

“Sasa kwa niaba yangu na mke wangu, zawadi yetu ni kukuongezea share kwenye ile hoteli.” Vigelegele vikaongezeka. Wakashangilia sana.  “Katika hoteli hii hapa, kaka yako yeye ni asilimia 70, mimi 30. Sasa na wewe kwa kuwa unaanza maisha na familia tayari, itakuwa hivyo hivyo na wewe. Yangu ni 30 tu ili tuendelee kunywa maziwa hapa mjini. Na bado niweze kumnunulia mama yako magauni.” Man akasimama, akaenda kupiga magoti mbele ya baba yake. Akamuwekea kichwa pale magotini alipokuwa amekaa kama kushukuru.

Malisa akamsogelea Mzee Ole akiwa na mumewe. “Na sisi. Kina Ole wadogo.” Malisa akimuonyeshea mumewe. Watu wakacheka. “Tutagaramia mapumziko yote ya honeymoon.” Vigelegele tena. Malisa alikuwa msomi sana na kazi yake ilikuwa ikimlipa vizuri. Kwa kumwangalia tu yeye na mumewe ambaye naye alikuwa na kazi ya maana, ungejua ipo neema. Ndipo wakaona uwe ni wakati wa zawadi tu. Kwa kuwa hakuna aliyekuwa amechangishwa, watu walikuja na zawadi nyingi sana. Nyimbo zilipigwa, sherehe ikakolea.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

“Daah! Hakika mimi bado siamini mwenzenu!” “Nini kaka?” Nanaa akauliza. “Namuhurumia sana Danny. Nahisi nipo ndotoni.” “Wala usimuhurumie. Ni vile ulikuwa hujamsikia alivyokuwa akimsema vibaya Grace. Hakujua kama Grace atakuja kuolewa kwa haraka hivi. Alijua vile alivyozaa watoto wa tatu ndio amekwisha. Akawa anajisifia eti yeye anaoa msichana mdogo. Sasa nasikia ameshaanza kusoma namba za kichina. Sara anamuendesha kama gari bovu.” Wote wakamgeukia Nanaa.

Akaanza kucheka. “Haya, wewe umejuaje?” Mama G akamuuliza Nanaa. “Mimi ni rafiki wa Tere.” “Nanaa wewe mtoto acha umbea wewe!” “Yeye mwenyewe ananipenda mama. Akiniona nimejilaza sehemu, ananifuata.” Geb alikuwa akimwangalia na kutingisha kichwa. “Haya kakwambia nini?” “Umeniambia niache umbea mama. Heri tu ninyamaze” “Nanaa usinitanie!” Nanaa akazidi kucheka. Alimjua mama G. “Mimi mwenyewe nataka kusimulia.” “Nanaa!” Geb akashangaa. “Kidogo tu mume wangu.” Geb akatingisha kichwa na kugeukia pembeni.

“Haya anza.” Mama G akamgeukia vizuri. “Basi nasikia kanunuliwa gari jipyaaa! Tere anasema akataka na simu kama ile ya Grace mpaka rangi. Danny akamnunulia. Akaiba kadi ya benki ya Danny akaenda kuchukua pesa kwenye ATM, akaenda kubadilisha matairi.” “Kwenye hilo gari jipya!?” Mama G akashangaa. “Kumbe! Pesa si ipo bwana? Ana shida gani?” “Atamfilisi Danny mpaka amchanganye akili. Sara hatosheki na pesa.” “Subiri sasa mama. Unaambiwa shopping ya nguo na viatu ndio kila siku. Anavaa nywele za milioni. Kucha ndio za malaki. Na akirudi anazungumza na simu zake anajingamba hapo mbele ya Tere kuwa amehamia saluni za watu wazima.” “Anafanya makusudi kwa kuwa anajua Tere anampenda Grace. Kwa hiyo anajua ujumbe utafika tu.” “Sasa huo ugomvi wao!”  Nanaa akaendelea.

“Unaambiwa mpaka watoto wa Grace wanakimbia. Tere anasema wakianza kugombana hapo! Huwezi kukaa. Watoto wanalia wanaenda kujifungia chumbani, wanaogopa.” “Na wamekutana. Danny anahasira, na Sara hawezi kunyamaza. Ndio maana wale watoto wamekuwa kama wanahofu! Hawaongei, wakimyaa!” Mara Grace na Man wakaja kwenye meza yao.

Wote wakasimama kasoro Nanaa. “Niambie bibi harusi wangu.” Grace alimchokoza Nanaa. “Anakazi ya kula tu hapo. Kama huyo mwanae. Hata kusimama hawezi.” Wakacheka. Man akamnyanyua Magesa kutoka pale alipokuwa amekaa kwenye kigari chake, anasinzia.“Naona kaka ananyama mkononi.” “Ukitaka aamke hapo, mpokonye.”  Wakacheka huku wakimwangalia Magesa. Anasinzia na nyama yake mkononi.

“Hongereni sana.” Geb akatoa mkono. James alibaki akimtizama Grace. Grace akacheka. “Nimefurahi umekuja James. Inayofuata ni harusi yako.” “Mniombee. Na mimi nimetamani. Ila sitaki aina ya kina Sara.” Wakacheka. “Nitakutafutia kaka yangu.” “Yamekupata Nanaa! Amesema tuombe.” “Na kumsaidia mama.” Geb alikuwa akimwangalia. “Si eti Geb?” Nanaa akauliza kwa mumewe ili kupata utetezi. “Mimi naona tukazane kuomba.” Wote wakacheka. “Geb naye! Hongereni mwaya. Mmependeza sana. Grace wifi yangu pongezi.” “Asante. Hapa nina raha zote.” “Mmmh!” “Sasa mama wewe unaguna nini?” Man akacheka. “Twende zetu mwaya mume wangu.” Nanaa akafurahi sana. “Graceee! Sema tena umrushe roho mama!”  “Mume wangu Man. Kwa raha zote!” “Hata mimi nakuona.” Mama G akajibu nakurudi kukaa. Kila mtu alikuwa akicheka. Man alimrudisha Magesa kwenye kiti chake. Akambusu, wakaondoka kuelekea meza nyingine kusalimia.

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wakufungua mziki, alikaribishwa Man na mkewe kwanza. Kama kawaida yake Man alitafuta zilipendwa za enzi hizooo. Wimbo wa mwana dada wa kimarekani, Brandy, ‘Have you ever!’  Kama kawaida yake Man alitaka apewe kipaza sauti. Malisa akasikika akitangaza. “Huu ni wimbo aliouchagua Man mwenyewe. Lakini anatuuliza sisi wote hapa. Ni maalumu kwa Grace, tusikilize maneno kwa makini pengine wengine wetu hapa tutapata majibu ya maswali yetu ya ‘kwa nini Grace na si mwingine!?’.  Man alishaniuliza hayo maswali, akiwa ametulia kabisa. Binafsi niliguswa. Naomba msikilize na nyinyi. Ila kwa kifupi Man anauliza, ‘Ulishawahi kumpenda mtu mpaka ukajikuta unalia! Anaendelea kuuliza zaidi, Ulishawahi kumuhitaji mtu maishani mpaka ukashindwa kulala usiku?’ Karibuni mumsikilize Man mwenyewe.” Malisa aliongea na yeye kwa hisia sana na kuvutia watu kusikiliza.

Wimbo ukaanza. Kwa hakika Man alijaliwa sauti. Ungependa Brandy atulie kidogo, Man asikike. Aliimba mpaka akamtoa machozi Grace. Walicheza blues vizuri sana. Ungependa kuwaangalia wanandoa hao. Ukumbi mzima ulikuwa kimya, wakiwatizama wao tu na kumsikiliza Man akiimba kwa hisia mbele ya Grace. Kuna wakati mwingine alimkumbatia kwa mkono mmoja, kwa kuwa mwingine ulishika kipaza sauti, wakati mwingine alimwachia na kumzungusha huku akiuliza, 

Have you ever loved somebody so much It makes you cry,

Have you ever needed something so bad

You can't sleep at night

Have you ever tried to find the words

But they don't come out right

Have you ever, have you ever

Have you ever been in love

Been in love so bad

You'd do anything to make them understand

Have you ever had someone steal your heart away

You'd give anything to make them feel the same

Have you ever searched for words to get you in their heart

But you don't know what to say

And you don't know where to start

Have you ever loved somebody so much It makes you cry

Have you ever needed something so bad

You can't sleep at night

Have you ever tried to find the words

But they don't come out right

Have you ever, have you ever

Have you ever found the one You've…

Have you ever found the one

You've dreamed of all of your life

Just about anything to look into their eyes

Have you finally found the one you've given your heart to

Only to find that one won't give their heart to you

Have you ever closed your eyes and

Dreamed that they were there

And all you can do is wait for the day when they will care

Have you ever loved somebody so much It makes you cry

Have you ever needed something so bad

You can't sleep at night

Have you ever tried to find the words But they don't come out right

Have you ever, have you ever

What do I gotta do to get you in my arms baby

What do I gotta say to get your heart

To make you understand how I need you next to me

Gotta get you in my world

Cause baby I can't sleep

Have you ever loved somebody so much

Man alicheza kwa hisia huku akitengeneza mlio mzuri kwa vidole vyake uliondana na bits za huo mziki. Alicheza Man akiuliza ulishawahi kupenda na kusubiria kitu uje kukimiliki? Alicheza mpaka wimbo ulipoisha. 

Akaomba kuongea kidogo wakati akimfuta Grace machozi huku amemkumbatia. “Watu husema, ‘Love comes once in a life time’ Ndicho kilichonipata kwa Grace. Mungu aliponikutanisha naye kwa mara ya kwanza, nikavutiwa sana mpaka nikajishitukia. Nikajaribu kujisogeza, lakini kitu cha kwanza alichoniambia, ‘mimi sio msichana, ni mama wa watoto watatu’. Wale pale ndio watoto wenyewe. Wana macho mazuri kama ya mke wangu.” Watu wakapiga vigelegele.

“Lengo la Grace lakuniambia hivyo ni kunisukumia mbali. But guess what? Nilishindwa hata kulala. Kwa mara ya kwanza, Man mwenye maneno mengi niliishiwa maneno sahihi yakujieleza kwa Grace ili anielewe. Nilihangaika kutafuta maneno yakuzungumza naye bila mafanikio. Lakini kama mnavyomjua mke wangu, ni mkimya sana. Ukifanikiwa kuwa naye karibu utajua nini naongelea. Upo utulivu ambao sikuwahi kuupata maishani, mpaka nilipofanikiwa kuwa karibu naye. Hapo nikathibitisha kuwa ni wangu. Swali ni jinsi gani nitammiliki moja kwa moja ndio ikawa changamoto. Vikwazo vikawa vigumu. Lakini Mungu akatuvusha. And thanks to my precious sis, Malisa…” Malisa akasimama. “That’s me people. ‘The precious sis’, ndio mimi.” Watu walicheka sana. Maana Malisa alisimama kama mshale nakujitambulisha.

“Yeap, that’s her.” Man akathibitisha kwa kumnyooshea kidole dada yake. “Yeye ndio aliharakisha mambo. Kwa mara ya kwanza anamuona Grace, akampenda sana. Akaanza kufanya juhudi za makusudi awe wangu. Namshukuru Mungu na mama yangu akampenda sana Grace. Nakumbuka siku Mzee Ole alipotaka kumuona Grace, akataka nimpeleke nyumbani, moyoni nilikuwa na wasiwasi na mama. Mzee Ole huwa mnamjua jamani. Kila mwanadamu kwake ni mzuri tu.” Watu wakacheka na kushangilia. Wakaimba wimbo wa “baba, baba, babaaaa…”

“Ila mama mpaka azungumze, ujue hicho kitu kimemgusa sana. Hana neno na mtu. Kimyaa.” Wakaimba tena “Mama mama mamaaa..”  Mpaka Man akaanza kucheka. “Grace alipofika nyumbani, akapata muda na mama. Sikujua hata walizungumza nini! Mimi nilikuwa na Mzee Ole tunazungumzia mambo ya biashara. Tulipoondoka, akanipigia simu siku inayofuata. Akaniambia kama nataka pumziko hapa duniani, basi nihakikishe Grace anakuwa mke wangu.” Vilisikika vigelegele, watu walishangilia sana. 

“Mama yangu ananijua kuliko nitakavyoeleza hapa. Yale mabaya yote ambayo ninaficha kwa watu, yapo moyoni mwa mama yangu. Kwa yeye kusema Grace ndiye, nikajua ni jibu langu kutoka kwa Mungu. Kama kawaida ya Mzee Ole, huwa hajui kusubiri, akasema leo lazima Grace awe wangu kihalali. Nawashukuruni woote kwa kuacha shuguli zenu zooote, kuungana na Mzee Ole, kuhakikisha leo tunamfanya kuwa Ole, kama alivyosema mwenyewe Mzee wa Ukoo.” Watu wakashangilia sana. 

“Sasa naomba msituchoke. Leo ni siku yetu mimi na Grace. Naomba wimbo mwingine wakucheza na mke wangu. Anaupenda sana huo wimbo. Kuna siku aliniomba niusikilize wote vizuri. Anajua huwa napenda zilipendwa. Najua leo ukipigwa atakamilisha siku yake vizuri.” Grace akacheka kama aliyekumbuka.

“Huo kweli ni mzuri Man. Uwe kwa ajili yako.” Grace aliongea kwa upole. Man akambusu. “Najua hamjamsikia Grace wangu. Lakini amesema uwe kwa ajili yangu.” Watu wakacheka. “Si ni siku yetu jamani! Hata tukitaka kucheza nyimbo tatu si ruksa?” “Ruksa kaka.” Malisa akajibu na vigelegele juu. Watu wakampokea vigelegele. Na yeye alivaa kimasai. Alipendeza sana Malisa. 

“Basi naomba mtuwekee ‘Brown eyes wa Destiny’s Child’. Najua Malisa alishaziandaa.” “Zipo kaka yangu. Dj fanya vitu vyako, tumsikie na Grace na yeye anamwambiaje Man!” Wote wakacheka mpaka Grace mwenyewe. Malisa alikuwa mtundu wa bila kujizuia.  Man alikuwa akicheka. “Thanks Mal.” Man akamshukuru, Malisa akamkonyeza kaka yake. Alikuwa amekaa meza ya mbele kabisa na mumewe pamoja na wazazi wao.

Remember the first day when I saw your face

Remember the first day when you smiled at me

You stepped to me and then you said to me

I was the woman you dreamed about

Remember the first day when you called my house

Remember the first day when you took me out

We had butterflies although we tried to hide it

And we both had a beautiful night

 

The way we held each others hand

The way we talked the way we laughed

It felt so good to find true love

I knew right then and there you were the one

 

I know that he loves me 'cause he told me so

I know that he loves me 'cause his feelings show

When he stares at me you see he cares for me

You see how he is so deep in love

I know that he loves me 'cause it's obvious

I know that he loves me 'cause it's me he trusts

And he's missing me if he's not kissing me

And when he looks at me his brown eyes tell his soul

 

Remember the first day, the first day we kissed

Remember the first day we had an argument

We apologized and then we compromised And we haven't argued since

Remember the first day we stopped playing games

Remember the first day you fell in love with me

It felt so good for you to say those words

'Cause I felt the same way too

 

The way we held each others hand

The way we talked the way we laughed

It felt so good to fall in love

And I knew right then and there you were the one

 

I know that he loves me 'cause he told me so

I know that he loves me 'cause his feelings show

When he stares at me you see he cares for me

You see how he is so deep in love

I know that he loves me 'cause it's obvious

I know that he loves me 'cause it's me he trusts

And he's missing me if he's not kissing me

And when he looks at me his brown eyes tell his soul

 

I'm so happy so happy that you're in my life

And baby now that you're a part of me

You showed me

Showed me the true meaning of love

And I know he loves me

 

I know that he loves me 'cause he told me so

I know that he loves me 'cause his feelings show

When he stares at me you see he cares for me

You see how he is so deep in love

I know that he loves me 'cause it's obvious

I know that he loves me 'cause it's me he trusts

And he's missing me if he's not kissing me

And when he looks at me his brown eyes tell his soul  

He looks at me and his brown eyes tell his soul

          Man alikuwa amemkumbatia kwa karibu sana, wanacheza. Mara kadhaa walimuona Man akimnong’oneza kitu masikioni na Grace anacheka sana. Jinsi alivyomshika na kumwangalia, ungejua tu Grace yupo kwenye mikono salama. Alikuwa akicheka wakati wote na Man alionekana kumfurahia mikononi mwake. Alionyesha ni kama aliokota lulu. Walicheza vizuri sana. Zaidi ile furaha kwa Grace, ungejua kuwa wawili hao walikusudiwa tu.

Baada ya hapo ikawa Man na mama yake. Na wenyewe walicheza wimbo wa ‘nani kama mama’. Akaja Grace na mama yake. Wakacheza huo huo, ulipofika nusu, Nanaa na Geb nao wakaunga msafara. Man naye akaenda. Mziki ukaendelea. Wakacheza kama walivyocheza jijini Arusha. Wakimtunza mama G. Wajukuu wote walikuwa wamelala. Wakacheza tena mpaka mwisho. Wakawa hawajaridhika. Malisa akamuomba DJ arudie, na yeye akaunga msafara. Wakacheza hapo mpaka mama Ole naye akasimama. Ukarudiwa tena. Wadogo zake wengine Man wakasimama. Wakacheza mpaka wakaridhika ndipo wakaruhusiwa wengine kuingia kucheza.

Jumapili, Kwa Danny

Siku ya jumapili asubuhi ambayo ilikuwa ni safari ya Danny, Sara pamoja na watoto, ilikuwa ni kama moto unawaka huko kwa Danny na Sara. Danny aliamka akiwa haoni kadi yake ya benki. Sara anaapa hajachukua. Wapo wanaishi kwenye apartment hiyo wao wawili tu. Nani kachukua? Ndio swali lililozua ugomvi. Danny hakuwa amepoteza wallet, na wala hakuwahi kuisahau popote. Inamaana mtu aliyemwibia ni wakaribu naye sana, ambaye anauwezo wakuichomoa alipovua suruali. Ni nani kama sio Sara? Sara naye anasema anatafuta sababu yakummalizia tu hasira zake kwa kuwa amejua Grace ameolewa, anaona wivu.

Angalau hapo Sara akafanikiwa kubadilisha mazungumzo. Kutoka kwenye kadi ya benki, mpaka kwa Grace. Ugomvi ukawa ni Danny anamtumia wakati mapenzi yako kwa Grace. Alimdanganya ili amvue tu nguo. Danny akamuuliza kwa nini atumie uongo kulala naye wakati ni yeye mwenyewe Sara alijileta kwake!? Hapo napo yakatokea matusi ya haja. Kila mmoja anampaka matope mwenzie. Sara akamkumbusha matusi yote aliyomtukana Grace, akimsifia yeye. Mwishoe Danny akajitetea hana hisia zozote kwa Grace, alishamtaliki hana shida naye, Sara anamwambia ni muongo. Kwa nini akose raha gafla baada yakujua Grace anaolewa? 

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Danny mwenyewe ndiye aliyerudi nyumbani siku alipozungumza na Grace akiwa kama mgonjwa. Sara alipomuuliza kulikoni, akajikuta anaropoka, “Grace anaolewa.” Sara akashangaa sana.  “Kwa hiyo ndio unaumia roho!?” “Kwa nini niumie roho? Ninachomaanisha ni kuwa, Grace anaolewa siku ya jumamosi, anataka watoto wahudhurie harusi yake. Inamaana ametuvurugia sisi mipango yetu. Ilitakiwa tuondoke jumamosi, sasa itabidi tusafiri jumapili.” “Kama sio uongo ni nini!? Kuna ubaya gani wakuondoka jumapili na si jumamosi? Kwani tulikuwa tunawahi wapi? Usinifanye mimi mjinga Danny!” “Mimi nakwenda na mipango Sara.” Danny alijitetea.

“Mipango gani ya kipuuzi hiyo!? Kutumia mahela yote hayo eti kwa ajili ya kwenda Tabora kwa wazazi wa Zinda ndio mipango ya maana hiyo kama sio upuuzi mtupu!?” “Unanitukana mimi!?” Danny kahamaki zaidi. Haamini Sara anayemuweka mjini na kumgaramia pesa zote hizo kama anadiriki kumwita yeye mpuuzi!

“Sijakutukana nakwambia ukweli. Kwanza wanakutumia tu. Wale sio ndugu zako na wala hawatakaa wawe ndugu zako. Mtoto wa kiume unajipendekeza kwa mwanaume mwenzio, ili iweje kama sio upuuzi huo?” “Sara angalia maneno yako wewe?” “Utanifanyaje? Unataka kunimalizia hasira za kuolewa kwa Grace? Wewe ulifikiria hataolewa? Ukisema cha nini wenzio wanalia watakipata lini. Hata mimi ukiniacha leo, ujue kesho nipo kanisani na shela nyeupe!” Danny akaamua atoke pale kwa haraka kabla hajamchapa makofi. Hiyo siku ikaisha kwa kuwa Danny aliondoka pale

~~~~~~~~~~~~~~~~~~

Sasa na leo Sara akaona ni wakati mwafaka wakumgeuzia kibao kumchanganya zaidi ili asikumbuke maswala ya kadi aliyokuwa ameificha. Alishakusudia amwibie pesa ya maana. “Najua sana kuwa unanitafutia sababu. Unatafuta kunimalizia mimi mahasira yako  kwa kuwa Grace ameolewa na mwanaume mwingine tena baada ya wewe kumchafua! Umeamka asubuhi hii ukakumbuka mwanaume mwingine anamfaidi sasa hivi Grace huko hotelini. Ndio unajidai mimi mwizi. Sasa ujue Grace kaolewa, na hatakaa arudi. Jamaa kaanza jana usiku kula mzigo kihalali. Pasuka sasa!” Sara akambadilikia kweli kweli.

“Kinachokufanya uhangaike na maswala yangu mimi na Grace ni nini Sara? Yanakuhusu nini?” “Ahaaa! Unaona unavyojifunga mwenyewe? Kwa hiyo ulitaka kumrudia? Inamaana mimi nikipoozea kiu chako, kumbe mawazo yapo kwa Grace?” “Acha kelele Sara. Mambo yangu na Grace hayakuhusu hata kidogo.” “Maadamu nipo hapa na wewe kama mwanamke wako, basi jua yananihusu na sitanyamaza. Usinichezee mimi akili.” Sara alikuwa anawaka kwelikweli.

“Wewe mwenyewe ndio ulimuacha Grace. Sikukushauri wala kukuingilia. Kwa akili zako mwenyewe ulisema umelogwa, unajitoa kwa kina Magesa. Ukasema humtaki Grace kwanza hajui mapenzi, maji matupu! Sasa kinachokutoa povu sasa hivi ni kipi? Mwenzio kaonjeshwa mara moja tu, katangaza ndoa. Wewe unajidai kununa! Kama mambo huyawezi, ungesema tu. Sio kila mwanaume kaumbiwa shuguli nzito.” Nusura Danny asimame ampige lakini na hapo akatoka.

Ndipo akaenda sasa kumpigia simu Tere, kutaka watoto wake haraka sana. Asichelewe. Akamuwashia moto Tere, ikabidi Tere kuanza kuandaa watoto wa Grace kwa haraka. Mama G alihakikisha wameshiba. Geb alitoka akacheza nao kidogo mpaka Jeri alipokuja. Hao watoto hawakuwa wakitaka kuondoka pale. Nyumba zima iliamka kwa kilio chao. Mama yao hakuwepo hapo. Walitokea ukumbini kwenda kwenye fungate. Man aliwaambia ijumaa baada ya kuchukua watoto, watakuwepo hapo kwa chakula cha jioni. Kwa hiyo akabaki Geb, mama G na Nanaa kuwatuliza hao watoto. Geb alizungumza nao akawaambia baba yao anataka kusafiri nao. Wakirudi, mama yao atawachukua na kuwaleta tena hapo.

Walikuwa wakilia mpaka Nanaa naye akaanza kulia. Ilibidi kupandishwa kwenye gari hivyo hivyo ili wasimchelewe baba yao ambaye alishaanza kumpigia tena simu Tere akiwa anafoka sana. Kuwa yupo getini nyumbani kwa Grace, mlinzi amemwambia watoto hawajarudishwa. Hao watoto waliondolewa pale wakiwa wanalia sana. Fili alimng’ang’ania shati Geb, hakutaka kumuachia. Waliacha ile nyumba imepooza kila mtu akiwahurumia.

Msiba Mzito.

Ilikuwa yapata saa kumi jioni wakati James anaingia akionekana amechanganyikiwa. “Kwa nini hampokei simu jamani!” James aliingia akabaki amesimama mlangoni, bila salamu ila lawama. Alikuta wamekaa tu hapo sebuleni. “Tumechoka baba. Tumelala siku nzima sababu ya uchovu wa harusi ya jana. Sijui kata simu yangu yenyewe iko wapi!” Mama G akakaa. “Pole kaka. Mimi simu yangu nimeacha chumbani, nafikiri imezimwa!” “Na mimi yangu nilizima na kuiacha makusudi huko chumbani ili nipumzike leo. Kwema?” Geb akauliza akimtizama. “Sio kwema kabisa.” James akawasogelea mpaka pale walipokuwepo kwenye makochi, akakaa.

“Mbona unatetemeka kaka? Kuna nini?” James alibadilika rangi akawa mwekundu sana. Hata Nanaa aliyekuwa amelala, akakaa.  “James!” Geb akamuita. “Sijui nianzie wapi aisee!? Ndio maana nilitaka Geb aje, asikilize na kujionea mwenyewe. Mungu nipe nguvu.” Geb akasimama. “Ni Grace?” Geb akauliza kwa kwa wasiwasi sana.

~~~~~~~~~~~~~~~~~

Shetani huwa hana usingizi wala hajawahi kuchukua LIKIZO.

Wakati mapacha hao wameshampamba mama yao vilivyo mbele ya umati wa watu, Geb kampata Nanaa wake & Grace kaolewa baada ya talaka ya aibu.

Ni jana yake tu walikuwa ukumbini wote na wajukuu wote,

wakicheza kwa furaha nakumtukuza Mungu, leo James

naye anakuja na taarifa za kustua! Nini kimetokea tena katikati ya Amani hiyo!?

ENDELEA KUFUATILIA.

 

 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment