Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! – Sehemu ya 61. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! – Sehemu ya 61.

Danny akatoka kama mshale. “Grace! Grace!” “Ameshatoka nje.” Wenzake wakamjibu wote wakionekana kuishiwa nguvu sio kama walivyoingia kwa makeke wakisubiri kusulubishwa kwa kina Magesa. Danny akatoka nje akimkimbilia Grace. Yule mama aliendelea kucheka huku anatoka pale ofisini. Akawasogelea rafiki zake Danny. “Naomba kuuliza jamani.” Kimya. “Eti hapo mlipokaa nyinyi, wangapi wenu wameoa na kuacha wake zao wakiwa na watoto wadogo, au mmekuja kumshabikia mwenzenu akiharibu familia yake tu halafu nyinyi jioni mnarudi kwa wake zenu na watoto?” Kimya.   

“Eti jamani?” Yule mama akasisitiza swali lake akiwatizama kwa zamu. “Lakini wale walizidi ushirikina sista.” Gozi akajibu. “Nyinyi wake zenu wamewaambia hawawalogi? Au labda niulize hivi. Bora vipi, vile alivyokuwa amelogwa akatulia na kusaidiwa kufika hapo alipo. Akapewa maisha na watoto. Jioni anarudi nyumbani kwa mwanamke aliyetulia kama Grace, au hivyo mnavyosema hajalogwa, yupo kama kachanganyikiwa? Anajibu watu hovyo, hata mwanasheria aliyemtafuta yeye mwenyewe pia amesahau kama yuko upande wake!”

“Hamumuurumii mwenzenu? Leo akiwa na watoto watatu ndio akumbuke mke aliyemuoa siye!? Kwa kuzungumza na Grace kwa dakika chache tu, utagundua ni mwanamke wakuoa na kuweka ndani. Na ndio maana aliweza kumvumilia rafiki yenu muda wote huo. Kwa shangwe zile mlizokuwa mkishangilia kabla hawajafika kina Grace hapa, nikajua huyo Grace ni kituko. Grace mwenyewe kapoa kama maji ya mtungini! Neno moja kulitoa kinywani mwake ni shida. Roho yake inaonekana safi mpaka usoni! Leo mnamshangilia mwenzenu aache mke kama yule na watoto!? Ili aende wapi?” Yule mama aliwakazia macho wakashindwa hata kujibu.   

“Sasa macho ya Mungu yapo juu yenu nyinyi wavunja amani kwenye majumba ya watu. Kila shida watakayopata hao watoto wao, ni pigo kwa watoto wenu. Sasa endeleeni kushabikia. Umati huo ni wa kwenye harusi tu, wakivunja ndoa, mnawaacha wenyewe wawili. Tena mnakaa mbali kabisa. Nyinyi ndio mnakimbilia kujilaani!” Wakaanza kutoka mmoja baada ya mwingine.    

Akabaki Zinda. Akamgeukia “Wewe ndio msimamizi wao wa harusi?” Kimya. “Umeoa?” Kimya. “Kwa hiyo wewe ndio rafiki wa karibu? Umekuja kumuunga mkono mwenzio akijizika mwenyewe? Umekuja kushabikia au?” Kimya. “Huogopi kushabikia kuvunjika kwa agano la Mungu wewe!? Unajua Mungu alisemaje katika hili?” Kimya. “Alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe. Sasa naona wewe ndio umekuja kusimamia kuvunjika kwa agano la Mungu. Subiri Ole yako inakuja. Utajibu mapigo ya Mungu.” Kimya.

“Sasa jua wazi leo ndio umeshuhudia kifo cha mwenzio. Amejizika hivi hivi ukiwa unamshangilia. Hamuwezi kushindana na mama mwenye watoto wadogo, halafu anayo pesa.” Yule mama akataka kuondoka, kisha akamgeukia Zinda aliyekuwa akitaka kutoka nje. “Au shida yako na wewe ni hawa watu waachane?” Kimya. Yule mama akacheka kwa kusikitika. “Kweli kikulacho ki nguoni mwako. Wewe haupo hapa kumkomoa Grace kama Danny anavyofikiri. Upo hapa kuhakikisha unamtoa rafiki yako kwenye neema! Umesimama naye kwa makini sana mpaka mwisho kuhakikisha habadili mawazo. Umesimama naye bega kwa bega mpaka umehakikisha amemtaliki mkewe, ili abakiwe hana kitu!” Yule mama akawa kama amegundua hila  ya kweli ya Zinda.“Sasa,…” Zinda akatoka kwa haraka asitake kumsikiliza zaidi huyo mama.   

~~~~~~~~~~~~~~~~

Grace alitoka pale na hasira, wote wakimfuata nyuma, hakufika mbali akaangua kilio kama amefiwa. Man akamuwahi. “Ni nini?” Grace aliendelea kulia kwa hasira sana. Mama yake akasogea na Geb naye akaja.  “Huna haja yakulia Grace. Nitaenda kuzungumza na mtu sasa hivi, haya mambo yatakuwa sawa.” “Nataka kuwaona wanangu Geb. Ni haki yangu.” “Naelewa. Rudini na mama nyumbani, ukapumzike. Nitakupigia simu baadaye kidogo.” Grace akaendelea kulia.

“Naomba unyamaze Grace. Unahitaji tu muda. Kila kitu kitakuwa sawa.” “Hapana Man. Sihitaji muda, nahitaji watoto wangu. Sara ni mtoto wa juzi kabisa. Hawezi kunilelea wanangu. Mimi wale watoto nawajua. Niwatundu sana. Na Danny anahasira sana. Watakuja kuwaua bure wanangu.” “Zipo njia nzuri tu na sahihi tunaweza kutumia ili kuwapata watoto. Kama nilivyokwambia ni haki yako. Mimi nafahamiana na watu wengi sana ambao hawawezi hata kumaliza week moja watakuwa wamekamilisha hili. Lakini watakuhitaji wewe Grace. Hivi ulivyo kwa sasa huwezi kutetea watoto wako. Unatakiwa utulivu mkubwa sana. Unakumbuka?” Grace akatingisha kichwa kukubali, nakujiegemeza kifuani kwa Man, akampitishia mikono kwa juu na kubaki akimsugua mgongoni.   

“Atakuwa sawa tu Geb. Naomba tupate muda wakufikiria kwanza kabla ya kuchukua hatua tukiwa hatujatulia.” Akambusu Grace kichwani pale alipokuwa amemuegemea na kumuuliza taratibu. “Vipi lakini hatua ya kwanza, mmefikia wapi?” Grace akanyanyua uso na tabasamu. “Tumeachana rasmi.” Grace akajibu. “Pole na hongera.” Grace akacheka kwa deko. Man akaanza kumbusu pale pale huku amemkumbatia. Mama G alishageuka pembeni. Geb alitoa simu yake nakuanza kuperuzi. 

“Unaweza kumtuma mtu akaja kuchukua watoto.” Wote wakageuka. Man aliacha kumbusu Grace. Alikuwa Danny. “Pale ni kwangu Danny. Sihitaji kutuma mtu kufuata wanangu. Nitakuja kuwachukua mimi mwenyewe. Wewe niambie muda wa kuja kuwachukua.” “Lakini lazima uwarudishe Grace. Nimeshakata tiketi za ndege kuondoka ijumaa jioni kuelekea Mwanza, kisha Tabora.” Grace akanyamaza.    

“Eti babe?” Man akamuuliza kwa upendo na kumbusu kichwani kwani alikuwa amempa mgongo wote wakimtazama Danny. Grace akaanza kulia tena kwa uchungu. “Huwezi jua jinsi nilivyohangaika na huyu mwanaume Man. Ukiniambia malipo yake nikuwafanya wanangu wanatangatanga kama upepo hivi! Hakika Mungu atakulipa Danny. Hatakuacha.” Grace akaendelea kulia. “Naomba unyamaze Grace.” Man akajaribu kumtuliza. “Nilimuuliza kabisa kabla sijabeba mimba ya hawa mapacha. Tena afadhali Fili alikuja bila taarifa. Nikamuuliza kama anauhakika anataka watoto wengine. Akajibu ndiyo. Leo amegeuka na matusi juu wakati yeye ndio aliwataka hao watoto! Leo wamezaliwa, anatesa wanangu! Kila siku watoto wako barabarani wanasafirishwa huku na huko! Kila weekend unasikia wanangu wapo Tabora! Na mazingira ya kule mimi nayajua Man. Ni nini wanachotaka na hao watoto wangu!? Kwa nini usiwe unaenda wewe mwenyewe angalau kuacha watoto wapumzike jamani!? Kimya.

“Mungu atakulipa Danny. Hakika utavuna unachopanda kwangu na wanangu, tena bila hatia!” Danny kimya. “Nitakuja kuchukua wanangu jioni.”  “Sawa.” Wakashangaa Danny ametulia. “Na kesho wakati narudisha watoto, ndio nitakuja kuchukua mizigo yangu yote. Kwa hiyo naomba nisikute kuna chumba hata kimoja kimefungwa.” “Sawa.” Danny akakubali. Grace akakunja uso kama anashangaa kulikoni.    

“Mimi naomba kukuaga rasmi Danny.” Mama G akajisogeza. “Lakini kwa hakika nakuhurumia. Nakuhurumia kwa kuumia sana. Najiuliza, hivi baada ya hii hekaheka yote hii kuisha. Grace akachukua watoto. Na..” “Grace hawezi kunipokonya watoto.” “Usibishe Danny. Usibishe hata kidogo. Kwa kuwa haitakaa ikatokea katika ulimwengu huu ambao MIMI, Oliva Magesa ninaishi, eti nikaruhusu wewe na Sara mkalea watoto wa Grace! Naomba hapo usibishe. Kwa kuwa unajua hutaweza kushindana na sisi ukashinda. Na ninakushauri usithubutu. Wewe mwenyewe umeshindwa kuelewa nguvu inayofanya kazi kwetu. Umekaa na sisi umeona vile tunavyopita kwenye moto, kisha tunatoka tukiwa tunang’aa. Usibishe hata kidogo. Unaweza kuharibu zaidi.” Danny kimya. Mama G aliongea kwa kutulia lakini kwa ukali. Rafiki zake nyuma wakisikiliza kwa kujiiba.   

          “Ila ninachojiuliza, baada ya hii hekaheka yooote hapa. Wapambe wako wote wanakuacha sasa baada ya kuridhika wewe kutengana na familia yako. Utafanyaje Danny!? Usinijibu kwa haraka, kwa kuwa nakufahamu Danny. Nimeishi na wewe kama mtoto wangu. Nalia kwa uchungu nikikuhurumia Danny. Nakuhurumia sijui mwisho wako utakuwa upi! Kweli umeruhusi yaliyowapata wazazi wako yakupate na wewe!?” “Sara ametulia.” “Nilikuomba usinijibu Danny. Ila unisikilize. Naomba kukupa ushauri wa mwisho.” Danny kimya.

          “Wewe ni yatima kama mimi tu. Tena yatima ambaye huna hata ndugu mmoja au ukoo unao ufahamu. Walio upande wako sasa hivi, hawajui umuhimu wa familia. Mimi naelewa ndio maana nilikubeba kwa kukuvumilia sana kwa miaka yote hiyo. Kwa kuwa sasa hivi unataka kuanza upya, tulia, anza vizuri mwanangu. Anza ukitaka historia ya baba yako usikurudie. Namfahamu Sara, kwa kuishi naye nikiwa nimemchagua awe mke wa Geb. Kwa hiyo ujue sikuwa nimemchukia. Nilimpenda sana tu. Namfahamu yeye, nakufahamu na wewe. Sasa ili kilichotokea leo kati yako na Grace kisitokee tena kwako na Sara, tulia. Muombe Mungu akusaidie Danny. Anza upya ukikusudia kujenga vizuri, sio kama ulivyoanza na Grace. Ukiwa umejaa chuki, hasira, jazba, kutokujiamini, hali yakutaka kutawala, kutaka wewe ujulikane na kuheshimiwa hata ambapo hukuwa unastahili tena ukiwa huna chochote ila suruali uliyokuwa umevaa tu.” Hapo Danny pia hakujibu. Geb alikuwa karibu sana na mama yake.

Madume wawili, wanaojielewa kimaisha walikuwa upande  wake.  Wamesimama  kama  wanaume wanaojielewa. Wametulia. Kwa kuwaangalia tu, utajua pesa ipo na wana uelewa wakutosha. Utamwambia nini mama G? Aliongea kwa kujiamini bila hofu. Aibu waliodhani atapata mtoto wake Grace siku hiyo imewarudi  wao  wenyewe!  Wakawa  wamepoa. Walimchambua Grace watakavyo. Walitukana mwili wake, Danny akiwasaidia kumdhalilisha kwa undani sana kana kwamba Grace alikuwa changudoa aliyelala naye siku moja tu na si mke! Sasa ameshasaini talaka, mwanaume Man ameshikilia kiuno na mabusu ya kichwani na shingoni kila wakati. Utamueleza nini mama G?    

Man alionyesha wazi alishaonjeshwa anachokitukana Danny, na amekolezwa na Grace. Wakati mama G anaongea, Man alishamvuta Grace karibu kabisa. Grace akiwa amempa mgongo, Man aliegemeza uso wake pembeni ya shingo ya Grace na yeye akimsikiliza na kumtazama mama G na kina Danny. Mara kwa mara alirudia kubusu shingo ya Grace huku mikono imezunguka kiunoni kwa Grace aliyekuwa ameinama lakini akimsikiliza mama yake. Ni mama G tu ndiye aliyekuwa akiongea. Kwa ukorofi wake wa asili aliweza kuzungumza na Danny bila hofu.

“Nazungumza na wewe leo, kwa kuwa sitarajii kupata muda na wewe tena. Nisingependa kuja kukuona karibu na nyumbani kwetu. Sitaki hata baya litokee kwa wajukuu zangu ili tusije pata sababu ya kuwepo chumba kimoja na kunitukana kama ulivyonitukana leo. Leo ndio mwisho wako wakunitukana Danny. Wewe si mume wa Grace tena, kwa hiyo kwa kuja kuinua kinywa chako na kunitukana tena. Kwa namna yeyote ile, ninakuahidi nitakuadhibu vibaya sana. Hakika hutakaa ukanisahau maishani mwako. Sikutishi, ila ninakuhakikishia nitakuadhibu vibaya sana. Tunakuacha leo ramsi, tena kwa amani kabisa. Kwa hiyo huna sababu yakuendelea kutufuata nyuma wala kututukana.” Danny na marafiki zake kimya.   

“Naomba Mungu, akuweke mbali kabisa na sisi ili uyaishi maisha unayofikiria sisi tulikuzuia kuyaishi. Na ninakushauri pata muda wa kumsihi Mungu akusamehe kwa mabaya yote uliyomtendea Grace. Umemtenda ubaya ambao hakustahili. Umemlipa mwanangu adhabu ambayo hakika hastahili. Umemchafua sana moyo wake. Lakini Danny, Mungu ni mwenye rehema. Naamini atamrejeshea Grace miaka yake yote aliyopoteza kwako. Alikupenda na kukuheshimu hata pale ambako hukustahili. Hakika pata muda umuombe Mungu msamaha. Mimi naelewa ninachozungumza Danny. Patana na Mungu kwa haraka ndipo utakuwa salama. La sivyo, nakuhurumia.” Mama G akaendelea.   

 “Cha mwisho, nasisitiza, kwa kuwa hujatoka kwenye asili ya pesa, na huijui pesa, ndio umekutana nayo sasa hivi, kuwa makini sana.” “Hapo unanitukana mama.” “Nakwambia ukweli. Wote sisi hapa mpaka rafiki zako waliosimama na wewe sasa hivi wakikushangilia hapa, tunafahamiana vizuri sana. Hakuna siri kati yetu. Hakuna hata mmoja wenu hapo ambaye hajafanikisha jambo fulani kama hakupitia kwenye mfuko wa Magesa. Bisheni.” Kimya.

“Kwa hiyo nakusihi uwe makini na pesa ya ukubwani. Pesa inaleta baraka, na pia huleta laana. Haina tabia yakuishi sehemu isiyo na amani. Huwa inakimbia na kabla ya kukimbia huwa inamtindo wakuharibu kwanza. Itakuchafua halafu ndipo ikimbie. Mungu awe nawe katika mwanzo wako.” Mama G akawa amemaliza. “Twendeni wanangu.” Mama G akatangulia. Geb, Man akiwa amemshika mkono Grace wakamfuata nyuma. Walipoondoka Man na Grace, ndipo na Geb akaondoka na mama yake.   

~~~~~~~~~~~~~~~~

 Ilibidi wote warudi nyumbani kwanza kama alivyoshauri Man. Wakaingia sebuleni wakakaa. “Umeridhika?” Geb akamuuliza Grace. Grace akafikiria kidogo na kuanza kulia. Alilia sana. Kila mtu akabaki kimya, Man alibaki akimsugua mgongoni. Mwishowe akamshika mkono na kumtoa nje. Alilia Grace mpaka akakaa chini. Hakuna aliyejua anacholia. Mama yake akabaki kimya. Kila mtu kimya.

“Naomba mnisaidie maji ya kunywa.” Man akarudi ndani. Geb akaenda kuchukua na kurudi nayo kwenye glasi. Baada ya muda wote wawili wakarudi ndani. Grace alikuwa ametulia. “Geb! Naomba nikushukuru kusimama na mimi kuanzia mwanzo wa hii ndoa yangu na Danny mpaka leo. Kunivumilia kwa kila namna. Kazini na kila mahali. Anaweza Danny akashindwa kukushukuru, lakini naomba mimi nikushukuru. Asante kwa kutubeba tokea tunaanza maisha mpaka leo bado nataka mnisaidie.” Grace akaanza kulia tena.

“Naomba  unyamaze Grace.” “Nina hasira sana Geb. Nina hasira siwezi kujizuia. Nina hasira, sijui nifanye nini.” Geb alijaribu kumtuliza dada yake. “Jipe muda.” Geb akaendelea. “Mpaka lini? Niambie Geb. Mimi nakuwa mtu wakuanza kila siku! Hapa nafikiria pakuweka mizigo yangu mara baada ya kuchukua kutoka kule anakoishi Danny na Sara, sina. Nafikiria pakulala na wanangu usiku wa leo. Wawe na furaha, wacheze. Sina! Nimepoteza muda mwingi kujenga kwenye mchanga. Mvua imenyesha kila kitu kimeparanganyika. Utafikiri mtoto niliyemaliza shule jana!” Grace aliendelea kulalamika.   

“Hamjui ni kiasi gani nilivyokuwa nimechoka nikidhani labda siku moja nitapumzika. Pesa yangu yote ya akiba nilitoa nikawekeza kwenye ile nyumba. Imejaa vitu vya mamilioni ya pesa zangu. Nina hasira yakushindwa kujisaidia. Zaidi nikifikiria ni Danny, mtu ambaye hana hata shukurani na heshima ndio anakwenda kuishi pale! Nimenunua kile kiwanja kwa pesa zangu mimi mwenyewe na Geb. Tena Danny akiwa hana kazi, mimi namlisha. Amewekeza pesa kidogo tu, tayari nyumba ndio yake anatangaza anataka kuoa aweke mkewe pale ndani! Naumia sana. Nimepoteza muda na pesa zangu nyingi.” Grace aliendelea kulia akilalamika.   

“Zaidi yeye kuwa ndio mwanaume wangu wa…” Grace akanyamaza na kuendelea kulia. “Nasikia hata kutapika. Nasikia hata kufa sijui!” “Nisikilize Grace. Kwanza tuongelee kitu cha msingi kwanza. Ya Danny yameshaisha. Naomba tuanze taratibu tu.” “Sina muda Geb. Sina huo muda mimi.” “Hapana G. Sasa hivi unaanzia pazuri sio kama zamani tukiwa hatuna pesa.” “Nianze ujenzi upya!? Hapana Geb.” Grace akazidi kulia.   

          “Niangalie G. Naomba tulia. Baada ya harusi tu, tutachukua siku 7. Mimi na wewe, tunatafuta nyumba popote unapotaka wewe.” “Ile nyumba nimeijenga kwa muundo wangu mimi Geb. Wewe unajua jinsi nilivyokuwa nikihangaika kuchora kila chumba na kupangilia kila kitu. Kila kitu pale ndani nilikaa chini na kufikiria ndio nikawapa mafundi. Sitaki majumba ambayo  watu  wanayajenga  tu  hata  hawajui yana ukubwa gani! Sina muda huo Geb.” Grace aliendelea kulalamika.   

“Basi baada ya harusi, tutatafuta kiwanja. Kizuri unachopenda wewe. Halafu mimi mwenyewe nitatafuta kampuni ya ujenzi. Wazuri. Tutawakabidhi ile ramani. Tena kwa kuwa ulishakaa humo labda kuna kitu utataka kirekebishwe. Utarekebisha kwenye michoro yako. Nitawapa. Nakuhakikishia Grace, ndani ya mwaka mmoja unahamia kwako. Kwa sasa hivi kuna nyumba hiyo hapo pembeni ya huo ukuta. Kubwa, tupu. Weka vitu vyako na wanao, muishi kwa kadiri ya unavyotaka wewe kwa muda ambao unasubiri nyumba yako ijengwe.” Geb aliendelea.   

“Siwezi  kuishi  hapo  na   wakati  najua   hapo ulipahangaikia kwa ajili ya Nanaa na wanae!” Grace akaendelea.  “Mimi nakaa hapa na mama. Huko sitaki kurudi.” Nanaa akawahi  kwa  haraka.  Grace kashangaa. “Kwa nini?” Kimya. “Wewe Nanaa!? Kwa nini hutaki kuishi kwenye nyumba yako nzuri unataka kuendelea kuishi hapa kwa kubanana na watoto?” Ikabidi Grace atulie, amuhoji Nanaa vizuri. Hapa hatubanani Grace. Tunatoshea tu.” Grace hakuwa ameelewa.    

          “Mama wewe!” “Mimi nimefanyaje? Ni Nanaa mwenyewe. Ukimwambia arudi kwake, pressure zinapanda, hatakula siku nzima hapa. Atalia tu. Huna utakachomwambia akarudi pale. Wewe muache tu humu humu ndani wabanane na wanae. Wewe nenda kakae pale kama alivyokwambia Geb. Na unyamaze maisha yako yaendelee.” “Danny amenipotezea muda mwingi sana.” Grace akalalamika tena. “Basi ujue anazidi kukupotezea muda.” Mama yake akamkatiza.    

“Sikubali.” Grace akakataa. “Wewe jana tuliongea vizuri hapa. Tumepanga mipango mizuri ya leo na kesho. Na unajua kabisa kwenye swala la mipango wewe ndio tunakutegemea. Sasa badala maisha yaendelee, unakuja hapa, unaanza kumlilia Danny.” “Aku mimi simlilii Danny!” Grace akabisha. “Tokea uje hapa, jina ni hilo moja na nyumba. Kwa nyumba gani bwana wakati sisi tumelala mpaka chini!? Unalilia baraka za jana, unasahau yale Mungu ametutendea na anatutendea mpaka sasa? Angalia mambo mazuri yanayotuzunguka na yanayokusubiri wewe uyafanyie kazi ili yatimie!” Mama G akaendelea.   

          “Wewe ndio umeshika mipango mizuri sana ya harusi ya mwezio. Harusi kesho kutwa, Nanaa hana gauni anakutegemea wewe. Wote hapa sisi tunakutegemea wewe mtu wa mipango. Usikubali Danny aendelee kukukandamiza. Ni juzi tu hapa tulikuwa tunafurahia na Geb, kwamba Grace wa mipango amerudi. Ukawa kama Grace tunayekujua wa miaka ile kabla ya Danny. Hata jambo liwe baya vipi, una uwezo wa kulitengeneza mpaka linakuwa zuri. Mungu kakurudishia akili zako, leo unakubali tena kuchanganywa na Danny!? Huko umeshatoka mama. Shukuru Mungu umetoka salama, tena umezungukwa na watu wanao kupenda na kukutia moyo.” Mama G akaendelea.

Haki haililiwi Grace. Kama ni haki yako ni yako tu. Itakujia. Mungu wako yupo. Tumemwita kwenye magumu mangapi na  akajidhihirisha kwetu? Eti Grace?” “Mengi.” Grace akajibu. “Basi naomba utulie. Mimi najua ulivyohangaika na Danny. Lakini leo ulimuweza vizuri sana pale mbele ya mwanasheria wake, mpaka amejirudi. Sasa simama hivyo hivyo. Asikurudishe tena chini. Panga mipango yako ukiwa umetulia. Ukiwa huna pressure. Geb amekupa mipango mizuri kabisa. Wamekupa nyumba yao. Nenda kaishi hapo na wanao huku ukifikiria chakufanya. Huyu Nanaa hapa ndio kafika. Jioni kachukue wanao. Wakafanye fujo pale usiku kucha, asubuhi warudishe kwa baba yao. Tena kwa amani tu bila ugomvi wala hasira. Shukuru Mungu. Jioni tuondoke zetu twende Arusha.” Mama G akaendelea.   

          “Wewe si ulitaka siku 30 za mapumziko?” Grace akanyamaza huku ametulia. “Basi ujue Mungu ndio amekupa hizo siku 30. Kaanze upya. Ukiwa huru ukijua sasa huna Danny, ila watoto watatu. Kapange mipango yako vizuri. Ukirudi hapa unanguvu na akili safi. Na nina kuhakikishia Grace, anguko lako lipo kwenye kukaa chini na kulia. Aliniambia baba yenu mimi wakati ananiacha. Wewe ukiona unadalili za kukaa chini na kuanza kujuta mambo ya nyuma na kulia, basi ujue ndio unaharibikiwa kabisa. Huna utakachoweza kubadilisha kwenye yaliyopita. Chukua mazuri, mabaya yaache, endelea. Ndio siri iliyonifanya kuwafikisha nyinyi hapa.”  

“Lasivyo mngekuwa kama watoto wa kawaida tu, kama ningeamua kukaa chini nilie na kujilaumu kwa maamuzi mabaya niliyofanya nyuma. Mimi sio mjinga. Najua wapi nilikosa, wapi nirekebishe na garama ipi inabidi kulipa kwa maamuzi mabaya niliyofanya nyuma. Sasa hivi unalipa garama kwa maamuzi mabaya uliyochukua zamani. Danny yupo hivi hivi, hajawahi kubadilika tokea tunamfahamu mpaka leo. Hakuwahi kuficha makucha yake, tuseme kwamba alikubadilikia! Wehu wake upo hivyo hivyo, lakini ukakubali kuolewa naye. Garama ndio hiyo. Jifunze, endelea. Tena endelea kwa makini ukijua una watoto watatu unaotakiwa kuwafikisha si pazuri tu, pazuri sana. Basi.” Kila mtu akaelewa.   

“Unanielewa Grace?” “Nimeelewa mama.” Grace akajibu. “Haya, naomba ukaoge. Badili nguo twende tukazunguke madukani mapema kisha ukachukue wanao. Harusi ya jumamosi lazima ifungwe.” “Nguo zipo hotelini.” “Kwani wewe hutembei na nguo Grace bwana? Utanicheleweshea mambo.” Nanaa akacheka. “Muone naye huyu! Wewe cheka tu wakati huna gauni.” “Naenda kuoga na kubadili. Nakuja sasa hivi.” “Na nakuomba urudi Grace.” “Narudi mama! Mbona huna imani na mimi!?” “Mimi nakujua wewe. Rudi hapa mapema. Sitaki unikwamishe.” “Mama kwa mipango!” “Uliianza mwenyewe. Na ujue mwenzio niliiandika chini yote. Na tutaitimiza tu.” Grace akacheka. “Twende mwaya Man.” Kidogo kukatulia.   

“Labda mimi niwaage kabisa.” Man akasimama. “Ukiondoka ndio hutarudi tena?” Mama G akauliza. “Najua Grace atahitaji muda na nyinyi na baadaye watoto. Nafikiria kurudi Arusha, ili apate nafasi bila mimi kumbugudhi.” Grace akabaki amezubaa. “Man!” Akamuita kwa upole. “Hapana babe. Ni sawa kabisa. Najua unahitaji muda na watoto. Mimi nitakuwa Arusha nikikusubiri.” Grace akapooza sana. Man akamshika mkono.    

“Twende uniambie vile unavyotaka Grace. Mimi nipo hapa kwa ajili yako. Lakini sitaki nikuzuie kufanya mambo ya msingi.” “Unanikimbia?” Grace akaanza kulia. “No no nonononooo! Mungu wangu nishahidi Grace.” Man akastuka sana. “Nafanya hivi kwa ajili yako. Ukitaka nibaki, nitabaki. Hata ukitaka nikusindikize kutafuta gauni la harusi la Nanaa, tutaenda wote. Naomba usilie Grace. Niliacha kila kitu, ili niwe hapa na wewe. Ila nilijua unataka muda na watoto. Kama unaona ni sawa mimi niwepo, basi twende tukaoge, tuje tuwachukue au tukutane kokote kule. Tuzunguke, kisha tukachukue watoto, halafu jioni twende kwa Mzee Ole. Au unasemaje?” Kila mtu alimuona vile Man alivyokuwa amepaniki kwa haraka kama aliyekuwa akiogopa asiharibu.   

“Twende.” Grace akabaki ameinama. “Babe!” Man akaita. “Twende. Twende tukazungumze huku tunaenda.  Najua tutafikia muafaka tu. Twende.” Akamshika mkono na kumvuta. Grace akasimama. Wakatoka. “Siwezi kukukimbia Grace. Wewe unajua.” Wakamsikia Man akiendelea kujitete huko nje, kwa kubembeleza. “Kweli?” Wakamsikia Grace akiuliza. “Naenda wapi?Au nikimbilie wapi? Haya yote mimi niliyategemea. Ndio maana nilitaka kuwa hapa na wewe. Hakuna talaka nzuri. Kila talaka inamadhara mpenzi wangu. Naelewa.” Wakasikia milango ya gari inafunguliwa na kufungwa, gari ikaondoka. “Mmmh!” Mama G akaguna.   

Kwenye Shopping siku hiyo Ya Jumatano Ya Talaka.

Walikutana madukani. Grace alikuja amechangamka kama sio yeye! Man  alikuwa pembeni yake. Geb alisisitiza Nanaa asiwe anazunguka. Kwa hiyo alibaki naye kwenye gari. Ikitokea mama G, Grace na Man wanapata nguo nzuri, wanamwita Nanaa, anaingia ndani kwenda kujaribu, Geb na Man wanabaki kwenye gari. Walifanya hivyo kwa maduka mawili, wakati wanaenda duka la tatu, Nanaa akiwa ameongozana na Grace na mama yao, wakakutana na Gozi.    

          Gozi alibaki ameduwaa. Kwa asili Gozi ni muongeaji na muhamisha maneno sana. Alikuwepo asubuhi akishangilia talaka ya Grace. Ndiye aliyesambaza habari za kubakwa kwa Nanaa. Ndiye aliyemwambia hata Malii kuwa Geb alimuacha Nanaa. Sasa hawakujua anachoshangaa ni nini! Lakini tayari Nanaa alikosa raha. “Twendeni wanangu.” Mama G akatangulia. Hakutaka hata wasalimiane. Wote walimuona jinsi Nanaa alivyopooza. “Gauni hili zuri. Nimelipenda.” “Mbona sasa furaha yote imeisha?” Grace akamuuliza. Nanaa akacheka. “Labda kuchoka.” Akajibu taratibu, lakini wakajua liko jambo tu. Kwenye duka hilo hilo Nanaa alipata kila kitu walichokuwa wamebakiza. Maana vingine Grace na mama yake walikuwa wakinunua wakati Nanaa yupo kwenye gari.

“Basi rudi ukapumzike kwenye gari wakati sisi tunasubiria hapa kwenye foleni ili tulipie.” Grace alimgeukia, maana Nanaa alikuwa amezubaa akiangalia sehemu moja. “Acha tu niwasubiri.” Nanaa alijibu na tabasamu la uongo. Bila kujua, Grace akamtumia ujumbe Geb. Ndani ya dakika mbili Geb akawa amemsimamia nyuma yake.   

“Umepata gauni unalopenda?” Nanaa akamgeukia Geb. “Nimelipenda.” Geb akabaki akimtizama machoni. “Vipi?” Geb akamuuliza. Akamuona anaanza kulia. Akamshika mkono wakatoka pale. “Gozi ameniona.” Geb akawa ameelewa. Akavuta pumzi kwa nguvu. Mama yake akatoka. “Kuna nini?” “Mlikutana na Gozi?” Geb akauliza. “Tulimuacha hapo akishangaa. Kwani vipi?” “Nanaa hakutaka Malii ajue kama ni mjamzito.” Geb akajibu. “Na akijua Gozi, basi ujue ulimwengu mzima utajua.” Wote wakatulia kwa muda.   

“Nisikilize Nanaa. Tusimpe shetani nafasi. Tufanye kama tulivyomwambia James. Kila changamoto tutakabiliana nayo kwa wakati wake. Tusijibu changamoto za baadaye sasa hivi. Kwa sasa hivi Jimmy ni mtoto wetu. Hata Malii akijua hana atakachofanya.” “Sitaki kuiona sura yake sasa hivi Geb. Bado sipo tayari kukutana naye. Na ninamjua akijua hivyo, atapata sababu yakutaka kukutana na mimi.” “Tutashugulika naye siku       atakapokuja. Naomba usipaniki. Tulia kabisa.” “Mimi nakubaliana na Geb. Kwanza Malii anakabiliwa na kosa la ubakaji. Hiyo ni fimbo ya kwanza yakumchapia. Pili, tunaweza kumfanyia kama tulivyowafanyia wenzie mpaka wakanyamaza.” “Mmewafanyiaje?” Nanaa akauliza.   

“Geb aliwafungulia mashitaka wale wote na wameambiwa chochote kitakacho tupata sisi wote, ni jela. Mbona wamepoa! Wewe usipandishe pressure ukashindwa kuolewa. Usikubali na wewe Malii akurudishe nyuma. Niliyomwambia Grace na wewe yazingatie. Kila kosa lina garama zake. Usikubali Malii akupokonye na ndoa. Unanielewa?” “Nimeelewa mama. Nilishaingiwa na hofu.” “Hata kidogo. Sasa hivi tunasonga mbele kama ulivyoniambia wewe.  Tuendelee na mipango yetu mpaka washangae. Kupaniki, kulalamika na hofu, ndiko kuanguka kwetu. Tumesameheana, tuendeleeni kusonga mbele. Tena tunaendelea kwa kushikana mikono. Akianguka mmoja, tunanyanyuana. Haya futa machozi, tujiandae kwa harusi.” “Asante mama.” Nanaa akasikika ametulia. Wakarudi kwenye gari walipowaacha Man na watoto. 

          “Wamekusumbua?” Nanaa akauliza wakati wamefungua mlango wa gari. “Hata kidogo. Wako kama vile mlivyowaacha. Mwanao haongei kama nyinyi hampo.” Nanaa akacheka. “Mama!” “Amemwimbia anko Man wimbo wa Diego?” Liv akamwangalia na kucheka. “Utamwimbia baadaye?” Akakubali kwa kichwa. “Basi nasubiri Liv. Sawa?” Man akamuuliza.  Liv akacheka tu na kidole chake kimoja mdomoni. “Vipi? Mmefanikiwa?” Man akauliza huku akimwangalia Grace. “Naona kila kitu kipo.” “Afadhali. Lakini nina ombi moja.” Man akamgeukia Mama G na Geb.    

“Karibu.” Geb akaitika. “Twendeni niwapeleke sehemu tupate chakula cha mchana. Binafsi nina sababu ya kusherehekea.” Wote wakacheka. “Kweli Man umekusudia.” Nanaa akadakia. “Bahati haziji mara mbili Nanaa.” “Mimi mwenyewe nakuunga mkono. Twende tu tukasherehekee. Kwanza Grace wifi yangu anastahili kupumzika.” “Wewe unakubali kwa haraka sababu ya chakula tu.” Mama G alifanya wacheke.“Asante Man.” Grace alishukuru. Man akamgeukia Geb. “Sawa. Pia itatusaidia kuwa kwenye ukurasa mmoja kwenye upande wa mambo ya harusi.” Wakaondoka.   

Mchana Wa Siku Ya Jumatano Ya Talaka.

Walifika kwenye mgahawa huo ikiwa imetimu saa saba na nusu mchana {7:30}. Kila mmoja wao alikuwa na njaa. Wakaagiza vyakula. Kucheka kukakolea. Walikula na kunywa, Nanaa na Man wakiwachekesha. Nanaa anauliza maswali, Man anajibu na kucheka kwanza yeye mwenyewe huku akisimulia kwa tahadhari mbele za wakweze. Geb kama baba yake Grace na mama G. Lakini wakawa na wakati mzuri sana. Hakutajwa Danny hapo. Vilikuwa vimejaa vicheko tu.   

Grace na yeye alikuwa akicheka mpaka machozi. Kwa muda mfupi waliokuwa pamoja ni kama Man alimjulia Grace vilivyo. Hakuacha kumsifia kwa hili au lile. Alimtizama na kutaka kumsikia akizungumza kitu chochote tena kwa kirefu zaidi.  Alimtaka asimulie labda kituko fulani walichokiona wakiwa pamoja. Grace alipokuwa akifupisha, Man alimtaka arudie kipengele hiki au kile, ilimradi tu kumfanya azungumze. Waliwasikiliza kwa muda huo mfupi, lakini tayari walishakuwa wameandika historia nzito pamoja. Hapakuwa na ubishi kama wawili hawa wanaendana au walikusudiwa.

Mama yake alijiridhisha, hata Geb alikuwa akicheka, ishara kuwa amempokea au ametoa baraka zake kwa Man. Man alikuwa na utundu wa maneno. Akichanganya na kicheko chake chakutoka rohoni, nilazima utacheka tu. Akakutana na Nanaa ambaye kucheka ndio kwao, basi ungependa kuwepo hapo. Na wala usingeamini kama ni hawa kina Magesa waliokuwa kwa mwanasheria asubuhi ya siku hiyo marafiki wakiimba wasulubishwe.   

Saa 10 Jioni Ya Siku Hiyo Ya Jumatano Ya Talaka.

Waliwarudisha nyumbani Nanaa, watoto na mama G. Grace, Man na Geb wakaenda kwenye nyumba ya Geb. Wakazungumza kidogo huku wakizunguka humo ndani. Geb akawaachia funguo kwamba wawe huru. Watakapochukua watoto, warudi hapo. “Nimemwambia Jeri atafute vijana wawili, watakusaidia kuhama. Utawakuta wakikusubiria nyumbani kwako getini na ile gari kubwa. Watakusaidia kubeba mizigo na kukuingizia hapa. Atakuletea msichana wa kazi wa kukusaidia kwa usiku huu mpaka kesho utakapo warudisha watoto. Nimemuomba alale hapa na nyinyi ili usihangaike na watoto.” Grace akaanza kulia.

“Ni kwa muda tu G. I promise. Utapata kwako soon. Na sitakubali uhamie sehemu ambayo hutaipenda. Nakuahidi utapata kitu bora. Usilie.” Man alikuwa akiwasikiliza. “Asante Geb.” “Basi mimi nawaacha. Muwe na wakati mzuri. Msalimie wazazi.” “Nashukuru Geb. Watasikia.” Man akajibu na kumpa mkono. Geb akawaacha hapo   

Mama ni Mama Tu.

Walishahamishia mizigo yao hapo kwa Geb. Waliitoa hotelini, wakahamishia hapo ndipo wakaenda nyumbani kwa Grace kuchukua watoto na mizigo ya Grace. Hapakuwa mbali na pale anapoishi Geb. Hata Man alielewa ni kwa nini Grace alililia ile nyumba. Haikuwa kubwa ya kutisha, ila ilipangiliwa kwa ustadi sana. Kuanzia getini mpaka vyumbani. “Unauhakika hii ramani yote imetoka kichwani kwako!?” Man aliuliza kwa mshangao. “Kila kitu Man. Hakuna hata jani ambalo limeota hapo nje kwa bahati mbaya. Nimefikiria ndipo likapandwa hapo. Nikikwambia nimetumia mamilioni ya pesa hapa, niamini Man. Hamna kitu cha bei nafuu hapa. Hakuna. Nimemwaga pesa kwa ajili ya wanangu. Wala si mimi na Danny. Kwa kuwa mara nyingi sisi wawili tulikuwa kwenye wakati wa hekaheka. Hata kama ni mapenzi, sio kwa kubembelezwa. Ni fujo tu.” Man aliendelea kuangaza macho kila mahali.   

“Itabidi na mimi unichoree. Nilifikiria kununua nyumba, lakini umenitia shauku ya kuwa na kitu kizuri na chatofauti. Na Geb amesema kuna uwezekano ndani ya mwaka mmoja nyumba inaweza kukamilika. Sioni sababu ya kutokujenga. Unafikiri utanisaidia?” Grace aliendelea kukusanya vitu vyake. “Nitafanya Man. Tukiwa mapumzikoni tutaanza taratibu kuhu ukiniambia ni vitu gani unataka.” “Naamini tutakuwa na wakati mzuri Grace. Tulia tu.        Tufanye kwa hatua.” “Nakushukuru Man. Nakushukuru kusimama na mimi.” “Nakupenda Grace. Nakupenda sana.” Grace akamsogelea nakuanza kumbusu mpaka Jeri alipogonga.

“Naona dada ameshaandaa watoto wote wapo tayari. Kama kuna kitu chakusaidia niachie nimalizie.” Grace hakumkuta Danny wala Sara. Alikuta watoto wake wote wamelala. Akawaamsha. Isivyo kawaida au ambavyo hakutegemea akaona watoto wake wamefurahia sana kumuona. Fili alitaka kuondoka na mama yake. “Utanichukua na mimi?” Fili alimuuliza na kumliza mama yake. “Ngoja dada akakuogeshe kwanza ndipo tuondoke.” Grace alizungumza naye kwa upole, akambusu.   

Man alishamsadia kuweka kila kitu kweye maboksi aliyokuwa ameleta Jeri. Wakawaacha Jeri na wale vijana wakichukua mizigo ya Grace,  wao wakaondoka na watoto pamoja na msichana wao wa kazi. Alimwambia Jeri hatahitaji tena msichana mwingine. Yule aliyenaye atamtosha. Kwanza amezoea watoto na anamuheshimu sana Grace. Hakutaka mtu mgeni kwa usiku huo mmoja tu ndio awahudumie. Jeri akaelewa. “Mbona watoto wenyewe wametulia Grace? Sio watundu kama ulivyosema?” Man akauliza. “Mimi mwenyewe nimeshangaa. Labda usingizi.” “Halafu wote wanamacho kama yenu!” Wakacheka.    

Ukweni.

          Grace hakutegemea mapokezi makubwa aliyoyapata nyumbani kwa kina Man.   Alikuta ndugu zake Man wote wakimsubiria mpaka huyo kaka yake mkubwa na familia yake. Walimfurahia na kumuonyesha upendo wa namna yake. Kwa kuwa kulikuwa na watoto wadogo, michezo iliendelea huku wao wakifahamiana. Mama yake Man alikuwa mtulivu, lakini sio Mzee Ole.   

          Vilijaa vicheko na utani. Ndipo alipojua utundu wa Man aliiupata kwa baba yao. Wajukuu walimfuata na kucheza naye kisha kuondoka. Ulikuwa ni usiku ambao Grace aliufurahia sana. Picha nyingi zilipigwa. Watoto wote walionekana kuzoeana, kasoro mke wa kaka yake Man alionekana kuwa mbali kidogo na wao. Grace aliliona hilo lakini akanyamaza. Watoto walipoanza kulia, Malisa akasema ndio ishara kuwa wamechoka. Yeye na mumewe wakaanza kuondoka na watoto wake. Man na Grace nao wakaondoka na watoto wao.    

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wapo njiani Fili akaanza. “Unaturudisha kwa dad?” “Hapana. Kwani unataka kurudi?” “Nataka twende wote mama.” Grace akanyamaza kwa muda. Man akaona anafuta machozi. “Labda kunakuwa na upweke dada. Siku hizi Sara hataki wawe wanakimbizana mle ndani. Anasema hataki kelele.” Dada yao akadakia. “Ndio maana wamepooza! Huwa anawachapa?” Grace akauliza. “Hapana. Ila baba yao ndio huwa anawachapa wote hawa.” Grace akanyanyua simu nakumpigia Geb.   

“G?” Geb akapokea. “Grace?” Geb akaita tena. “Ni nini tena!?” “Nataka nyumba yangu. Sitaki Sara akae pale. Nimebadili mawazo.” “Naomba usilie Grace. Niambie kuna nini?” “Sara anakataza wanangu wasikimbie ndani ya nyumba yangu! Yaani yeye anawapangia wanangu kitu chakufanya nyumbani kwangu? Nataka nyumba yangu. Zungumza na mwanasheria wako, mwambie nipo tayari kupigania haki yangu. Siogopi hata kwenda mahakamani. Lakini Sara hataishi pale.” “Basi usilie. Hilo tutalifanyia kazi. Wanaendeleaje lakini?” “Wamepooza kweli, kama sio wao! Si unajua Danny anavyopenda kuchapa? Sasa nasikia anawachapa mpaka hawa wadogo. Watoto wamepoa Geb, kama wagonjwa!” Geb akatulia kidogo. “Mwambie aniletee niwaone.” Akasikia sauti ya mama yake. “Mama anaomba awasalimie.” “Ngoja nizungumze na Man, nitakupigia.” Kidogo Man akapumua. Alihisi amesahauliwa.

“Mama anataka kuona watoto. Unafikiriaje? Twende leo au kesho?” Grace akauliza. “Unajua Danny alikataa kabisa mama na Geb wasiwe karibu kabisa na wanangu?” “Kwa nini?” Man akauliza. “Anasema tutawaloga kama yeye tulivyomloga.” Man akacheka sana. “Usicheke bwana!” “Duniani kuna mambo! Yaani kuna vitu vingine unasikia unafikiri ni utunzi tu.” “Mmmh!” Grace akafikiria.

“Lakini Man, Danny amenichokoza. Sitakubali. Hakika nimeamua sikubali!”  Man akanyamaza. “Unafikiriaje sasa?” “Juu ya nini?” Man akauliza. “Kuwapeleka kwa bibi yao.” “Ni sawa tu. Twende.” Wakaenda mpaka nyumbani kwa Geb. 

          Liv alifurahi sana kumuona Fili. Mpaka kila mtu akashangaa. Aliruka ruka huku akiimba jina la Fili wakati ndio alikuwa anasinzia wakati Grace anaingia na wanae. “Lakini hawana afya mbaya.” Mama G aliongea huku akiwatizama kwa zamu. “Si kwa kuwa nimemuacha dada yao? Yaani bila yeye naona hawa watoto wasingekuwa hivi.” Geb alikuwa kimya akiangalia. Liv alianza kumbusu Fili. “Naona mama mzazi alikuwa na hamu kweli na Fili.” Nanaa akachokoza. “Mimi nataka kukaa hapa na Liv, anko. Sitampa pipi. Nitacheza naye tu. Simfundishi kuruka. Nitakua siongei sana.” “Njoo kwanza Fili.” Geb akamvuta karibu.   

“Nitatulia anko.” “Nisikilize. Cha kwanza wewe ni mtoto mzuri sana. Hivyo ulivyo ndivyo Mungu anataka uwe. Wewe umeshaona mtoto mdogo anayezungumza kifasaha na vizuri kama wewe?” Fili akanyamaza.   “Huyu Danny sijui kafanyaje wanangu. Wote wamekuwa kama wajinga!” “Baba Fili hataki kelele dada.” Msichana wa kazi akadakia. “Sasa mbona yeye anapiga kelele? Aache kuniharibia watoto.” Grace alishakasirika.    

“Naomba mnisamehe jamani! Nashindwa kujizuia. Sijui ni kupaniki!” “Hakuna mtu anayejiandaa kwenye tukio kama hili Grace. Mimi naomba nitoe hoja yangu.” “Karibu Man.” Geb akamkaribisha, wote wakamgeukia. “Tulikuwa tuna mpango wakusafiri na Grace kwa siku kadhaa. Lakini kwa hali jinsi ilivyo, najua Grace hawezi kutulia. Au niseme hata mimi siwezi kutuliza mawazo wakati tunajua wazi watoto wanamlilia Grace. Itakuwa tunajidanganya tu. Hatuwezi kuwa na mapumziko wakati kuna vilio vya watoto.” Man akaendelea.   

“Kwa kuwa Danny amekusudia kusafiri nao weekend hii. Na Grace alishamkubalia. Basi, baada ya harusi tu, sisi turudi hapa Dar, tushugulikie swala la watoto.”  “Amesema anasafiri nao tena.” Grace akadakia. “Tutampelekea watoto uwanja wa ndege hiyo siku anayotaka kusafiri nao tena, au popote atakapotaka yeye. Sisi tutamwandalia kila kitu atakachohitaji cha hao watoto huko safarini, tutampelekea. Akirudi nao tutakuja kuwachukua tena mpaka mtakapoweka sawa mambo ya watoto. Hawa watoto bado ni wadogo sana na wanamuhitaji Grace.” Kila mtu alishangaa hekima ya Man.     

“Kabla hamjanijibu kuhusu wazo la kwanza, naomba niende kwenye pendekezo la pili.” “Lakini wewe Man kweli unaakili za kiutuuzima. Na ni kweli una upendo wa dhati. Umebeba matatizo ya Grace kama yako! Binafsi nimeshakupenda gafla.” Mpaka Man mwenyewe alicheka. “Nanaa huyu mtoto jamani!” “Kweli mama. Nani anataka kuanza maisha mapya na mtu akiwa na watoto wa mtu!? Mimi naelewa mama. Najua hofu aliyonayo Grace kwa kuwa nilikuwa hapo. Ni Geb tu ndiye ananiwezesha kuwa hapa. Nilikuwa nalia na hili tumbo mchana na usiku. Hofu, na itakuaje ndio vilikuwa vikinisumbua. Wawili ni wawili mama. Tena mmoja akawa na uwezo wa kushika taa na kuongoza njia! Hakika safari inakuwa rahisi. Binafsi nakubaliana na wazo la Man. Jamani Danny ni mkali nyinyi! Wote tulikuwa tukimuona anavyomchapa Fili. Sasa leo awe kwenye hali ile, hawa watoto hawatakuwa salama.”

“Lakini si mnamjua jinsi Danny alivyo mbishi? Itachukua muda mrefu sana kufikia muafaka wakati wanangu wanahangaika.” Grace alilalamika. “Nisikilize Grace. Hawa wanao mpaka sasa hivi hapo walipo hawapo hatarini. Panga karata zako kwa makini sana ili ukiweza kuwa nao, unakuwa nao moja kwa moja. Kama alivyosema Man, tupange haya mambo kwa utulivu na kwa umakinifu. Hakuna jeuri mbele ya sheria. Na pesa inaongea mahali popote. Harusi ikiisha tu, hata kama bado hawajarudi, tuanze kufuatilia swala la watoto. Tutafanikiwa tu. Mungu yupo.” Mama yake akamtuliza Grace, akatulia kidogo.   

“Una wazo gani la pili?” Grace akauliza kwa upole. Liv alishaondoka muda mrefu sana na Fili wakaenda kucheza michezo yote Magesa aliyokuwa akimvurugia. Na nikweli alifurahia. Mara kadhaa walimsikia akicheka huku akimfundisha Fili na Fili naye akimwelekeza Liv. Waliwageukia na kuwatizama. Liv alikuwa anacheka sana. “Leo dada kapata alichokuwa anakitaka. Liv sio wakucheka mida hii. Sasa hivi angekuwa anajizungusha pale kwa mama yake au kifuani kwa baba yake.  Kumuona amechangamka vile, ujue kafurahi sana.” “Alikuwa anamuulizia kila siku.” Nanaa akamjibu mama G.   

“Mungu atasaidia tu.” “Mimi ndio kauli nilitamani kukusikia ukiiongea kwa muda mrefu sana G. wewe mtu wa mipango, kwa nini unakatishwa tamaa bwana?” Geb alimuuliza. “Wewe umeshajua sasa hivi ni nini unataka, ujue hapo umeshatatua matatizo kwa asilimia 85. Kule kujua tu nini unataka, umeshatatua tatizo lako. Basi sasa hivi tuanze kufikiria jinsi yakupata.” “Sawa.” Grace alijibu safari hii akasikika ametulia.   

“Karibu Man kwa wazo la pili.” “Lakini msinielewe vibaya kwenye hili wazo la pili.” Man akajaribu kuwatahadharisha. “Karibu tu.” “Okay. Nina taka kusema hivi, ipo tofauti ya mtu aliyezaliwa kwenye pesa na ambaye amepata pesa ukubwani. Kuna vile viwango vya pesa mtoto kama Liv ameshazoea kuvisikia tokea anazaliwa mpaka anakuwa mkubwa. Akienda dukani anapomuona dad au mama ananunua vitu halafu analipa bila shida. Anapomsikia bibi yake amemnunulia dhahabu. Yaani dhahabu yeye ameivaa tokea ni mtoto. Hatasumbuliwa na viwango vikubwa vya pesa au dhahabu anapokuwa mkubwa. Tofauti na mtoto aliyekuwa katika mazingira ambayo anaona wazazi wanalalamikia mpaka bei ya chumvi.” Wakacheka kidogo. 

          “Zipo pesa ukimtajia mtu, hata kama ni mkorofi kiasi gani, lazima anatulia na kufikiria mara mbili mbili. Ni rahisi kwa mtu ambaye hajazoea kushika pesa nyingi kumpokonya kitu chake cha thamani kwa pesa ndogo sana. Na kuna useme unasema, everybody has price’. Hakuna mtu ambaye hanunuliki. Hata Danny ambaye Grace anamuhofia na kusema ni mkorofi sana, anaweza kununulika tu tena bila ugomvi. Kwa mfano. Grace ameniambia aliwekeza pesa nyingi pale kuliko Danny. Tunaweza kukisia tu kutokana na mshahara wake, tukapata hicho kiwango. Halafu tukakizidisha mara mbili. Unamfuata na pesa taslimu kwenye mkoba.” Wote wakacheka. 

“Mimi sio tapeli jamani! Ni mfanyabiashara tu. Msinielewe vibaya.” Man alijitetea, wakacheka zaidi. “Hakika Danny atakubali. Ninavyomjua yule.” Grace akadakia. “Si umeona sasa?” “Lakini ili kuongeza nguvu, uende akiwa amekaa na Sara. Sara anapenda sana pesa. Mimi nimeishi naye hapa, namfahamu linapokuja swala la pesa, hajiwezi. Akikataa Danny, Sara atamuweka sawa mpaka akubali.” Grace akaanza kucheka.

“Si umeona mambo yanavyokwenda vizuri?” Geb akamuuliza Grace. “Sasa hivi ninafuraha. Asante Man.” “Karibu. Ila mimi sio tapeli.” Wakazidi kucheka. “Hapana. Hatukuelewi vibaya Man. Tunashukuru kwa mawazo. Nafikiria kufanyia kazi kesho asubuhi tu, tukiamka. Nataka Grace aondoke hapa Dar akiwa ametulia. Kwa kuwa ndege yenu yakuwapeleka Arusha ni ya jioni, asubuhi nitazungumza na yule mwanasheria wetu. Amuombe mwanasheria wa Danny, tukutane kwa kikao cha dharula na kifupi. Atamwambia nilazima Sara awepo kwa kuwa anahusika kwenye maisha ya hao watoto. Tutakapokutana ndipo tutatoa mawazo yote mawili ya Man. Tuone watasemaje. Na akikubali, tunasainishana kesho hiyo hiyo na kuacha hati ya nyumba ikibadilishwa. Atoe jina lake kabisa kwenye hati ya nyumba. Ibaki kuwa ya Grace tu. Yeye na Sara wakatafute sehemu nyingine yakuanza maisha. Tutaweka wazi kuwa hatupo tayari Danny na Sara waanzishe familia nyingine pale ndani. Wanawajibika kwa watoto wao, sio sisi.”

“Asante Geb. Nakushukuru. Lakini itakuaje endepo atataka pesa kesho hiyo hiyo?”  “Si ndivyo tulivyokubaliana tuwe na pesa yote taslimu na alipwe papo hapo ili asije badili mawazo baadaye? Tusimpe hata muda mrefu wakufikiria na tumjengee hoja ngumu sana ambazo hataweza kushinda hata akitaka kupeleka kesi mahakamani.” Nanaa alibaki kimya. Ndipo alipoamini kuwa ni kweli Geb anapesa na anampenda dada yake.

          “Kwanza amekiuka masharti mengi sana ya kampuni anayofanya kazi. Nayo hiyo nitazungumza na yule mwanasheria. Nimpe nakala za sheria za kampuni yao ili kumtuliza kesho. Na nitamwambia akicheza, atapoteza vyote. Kazi na familia.” Grace akatulia kabisa. “Leo naweza hata kulala.” Grace akasikika ametulia kabisa. “Asante Man.” “Karibu.” Wakabaki wakiangaliana. Wakacheka.   

“Jamani naomba mimi nikapumzike. Nimefurahi mmeweza kufikia muafaka. Tutaonana kesho.” Nanaa akaaga akionyesha kutulia zaidi ya kawaida yake. “Asante Nanaa. Ulale salama.” Grace akajibu. “Sasa yule dada mimi namuacha. Kumtoa pale ni kumkatili.” “Kwanza hatakubali.” Bibi yake akaongeza. “Liv! Njoo mbusu mama. Naondoka.” Akaja anakimbia. “Twende wote mama.” “Mimi naenda kulala.” Liv alishabadilika.  “Twende mama. Twende.” “Liv! Mimi nakwenda kulala ndani chumbani, mwanangu. Siendi popote.” Nanaa akamuhurumia. “Liv! Unataka kumsindikiza mama kulala?” Geb akaingilia. Alishakuwa mwekundu. Akatingisha kichwa kukubali.

“Haya, mshike mkono umpeleke chumbani.” Liv akafanya kama alivyoambiwa na baba yake. “Usilie sasa. Twende. Fili twende mnisindikize kulala.” Fili aliyekuwa ameduwaa akimtizama Liv, akafurahia mualiko. Wote wakaenda kupanda kitandani. Liv aligoma kutoka pale kitandani. Geb aliingia nakukuta wote wamelala. Akacheka. Akamtoa Liv wa kwanza na kumuweka kitandani kwake, ndipo akamchukua Fili. “Watakuwa wamechoka. Nasisi tunaondoka. Man anatakiwa na yeye kupumzika.” Grace akasimama. Akaenda kumuamsha dada. Alikuwa amelala na mapacha chumba alichokuwa akiishi Grace na Danny. Wakaondoka.   

~~~~~~~~~~~~~~~

“Njoo hapa.” Mama yake alimuita Geb baada ya kufunga milango yote na kujikuta wamebaki wao wawili tu pale sebuleni. “Sasa hivi kuwa sana makini kwenye mipango yako. Haupo tena peke yako upo na Nanaa. Anapokusikia ukitamka mipango mikubwa hivyo na yeye hajashirikishwa, yeye kama binadamu ni lazima ataumia. Halafu unakuwa ni kama unamtuma akafanye hivyo hivyo kwa kaka yake. Nilikwambia Geb. Unaweza usione madhara yake sasa hivi, lakini Nanaa hatakuwa mjamzito milele. Au hatakuwa anaishi humu ndani milele. Wewe mwenyewe uliona jinsi ulivyochanganyikiwa wakati ule alipokuwa na mipango na kaka yake. Kuwa makini sana.” Mama G akasimama na kuondoka.   

~~~~~~~~~~~~~~~

Geb alielewa kila kitu. Ni Grace! Grace pacha mwenzie. Grace aliyehangaika naye kwenye biashara ile mpaka sasa imekua! Grace ni jukumu alilokabidhiwa na baba yake tokea mdogo! Haitaji kuomba ushauri akitaka kumsaidia. Kwa nini? Mbona ni jambo la kueleweka tu! Geb aliwaza. Akili ikamkumbusha vile alivyochanganyikiwa baada ya kujua James anataka kumsaidia Nanaa, kununua gari na kufanya naye biashara. Taratibu akajirudi. Akakumbuka ule wivu aliojisikia na kuona James anamwingilia kwenye mambo yake. Kweli akaona hamtendei haki Nanaa. Akanyanyuka kwenda chumbani.   

~~~~~~~~~~~~~~~

Alimkuta Nanaa ndio anatoka chooni. “Vipi?” “Naona leo nimekuwa na siku ndefu. Sijatuliza mawazo. Nimeshituka sasa hivi na kunywa dawa ya usingizi ili nilale kabisa niweze kutulia. Na pressure nayo nimepima naona imepanda kidogo.” Akapanda kitandani. “Lakini nitalala tu. Nimeshajisaidia kabisa, ili nikilala nilale nisiamke tena.” Geb akakaa pembeni ya kitanda. “Nikuletee kitu chochote cha kula?” “Hapana. Nipo tu sawa. Usiku mwema. Acha nipumzike tu.” Akajilaza. Ni kweli Geb akamuona amekuwa mtulivu zaidi. Akajua aliyozungumza mama yake ni kweli.   

“Basi na mimi ngoja nisafishe meno, nakuja tulale.” Geb akaenda maliwatoni, kurudi Nanaa alishakuwa amelala. Akabaki akiwaza. Afanye nini! Amuombe ruhusa yakumnunulia dada yake nyumba!? Yalikuwa ni maisha mageni ambayo hata hakuwahi kufikiria kuja kuyaishi. Anatafuta pesa yake kwa shida sana. Halafu leo aje aanze kuomba ruhusa jinsi ya kutumia!? Akakumbuka maneno ya Man ya asubuhi hiyo. Juu ya kuhangaika maishani. Unafanikiwa. Unaoa mwanamke, unaishi naye mwaka mmoja tu, anataka muachane halafu mahakama inaamuru mgawane mali! Geb akabaki akifikiria.

Lakini akajua kipimo hicho hicho anachompimia Nanaa, ipo siku na yeye atampimia na hatakuwa na haki yakuuliza. Swali likawa je, yupo tayari kuishi kwenye nyumba moja na famle mbili tofauti!? Nanaa ahangaike kivyake na watu wake, na amgawie amtakae bila kumuuliza? Geb akabaki akijiuliza na kujijibu mpaka akapitiwa na usingizi.   

Alhamisi.

Nanaa aliamka asubuhi na kufuata ratiba yake kama kawaida, akamlisha mtoto na yeye akala. Alipomlaza  Magesa, akarudi chumbani kwao. Alimkuta Geb ameamka, ila yupo tu kitandani. “Vipi?” “Narudi kulala tena. Najisikia kuchoka!” Nanaa akajibu wakati anapanda kitandani. “Kuna maumivu yeyote?” Geb akauliza. “Hata sijui!” Bado Geb aliona hana furaha. Akajilaza.  “Nikuulize  kitu   Nanaa?”   “Mmh!” “Nimekuudhi?” “Kwa nini unafikiria hivyo?” “Hapana. Nilitaka tu kujua. Maana usiku umelala bila kunisubiri.” “Nafikiri nikuchoka tu. Halafu mambo mengi yanaendelea sasa hivi. Hamna utulivu. Nawaza hili na lile. Kwa hiyo nafikiri akili imeanza kuchoka. Nalala kwa haraka.” “Kama ningekuwa nimekuudhi, ungeniambia?” “Kama ni jambo la kuzungumzika, ningekwambia tu ili tuwekane sawa.” Nanaa akajibu kwa jumla.   

“Kwa hiyo kuna mambo naweza kukuudhi na ukashindwa kuniambia kwa sababu hayazungumkiki?” Nanaa akafikiria kidogo. “Sijui. Ila nitajua siku itakapotokea na kushindwa kukwambia. Sasa hivi sijui. Ila mimi najua kuna mambo mengine wakati mwingine hayana majibu ya papo hapo yanahitaji muda. Halafu Geb, mimi na wewe tumetoka katika ulimwengu miwili tofauti. Kuna mambo hata kama utanioa, huwezi kuyaelewa ila kaka James tu. Hivyo hivyo wewe. Kuna mambo utakuwa huru kwa Grace na mama kuliko mimi. Kwa kuwa unajua watakuelewa kwa haraka na kukushauri kwa haraka. Kwa hiyo kujibu swali lako nafikiri mimi na wewe tuna mambo fulani fulani hata kama tunapendana, lakini hatuwezi kukaa chini pamoja tukayazungumza. Na hatuwezi kuepuka hilo.” Kimya. Lakini yale maneno yalimwingia Geb mpaka moyoni. Akapata ujumbe wake.   

“Baadaye nitatoka kwenda kufanya kile kikao kama tulivyozungumza jana.” “Ni vizuri.” Nanaa akajibu kwa kifupi tu. Akajigeuza mara kadhaa. “Vipi?” “Nampanga Jimmy, ili nilale.” Akatulia. “Nilikuwa nikifikiria kumsaidia Grace kununua ile nyumba.” “Nilikusikia jana pale kwenye kikao. Hongereni sana. Naamini Mungu atawasaidia kufanikisha.” Nanaa akajibu. Geb akabaki kimya. “Uji upo tayari kama njaa ikianza. Nimekuwekea kwenye chupa na bakuli kubwa. Nataka nilale tena kidogo.” “Umeangalia pressure?” “Sikutaka kujinyima raha. Ila nimekunywa dawa. Nitakuwa sawa tu.” Nanaa akalala.   

Kikao Cha Pili.

Kikao kilianza ila kama walivyopanga mwanzoni tu, wakafungua mkoba wenye pesa. Sara alikuwa kama amechanganyikiwa baada  ya kuona mamilioni ya pesa, tena tasilimu, yamepangwa kwenye mkoba, halafu eti zikiwasubiria wao! Danny alipotaka kukataa, Sara akamshangaa sana. Geb akatumia akili ya haraka sana. Akawashauri wakapate muda nje ya hapo wakazungumze. Mpaka wanarudi ndani, Danny alitaka alipwe akaanze maisha yake sehemu nyingine. Mwanasheria wa Grace alimwambia ni heri akubali hiyo pesa kuliko wakifikishana mahakamani, atatakiwa kumwachia Grace nyumba na atatakiwa pia kumpa Grace pesa ya matumizi kila mwezi. Alipofikiria, na Sara alipoongeza nguvu na kuthibitishiwa na mwanasheria wake kuwa ni kweli, akaona heri achukue hiyo pesa akaanze kwake. Kwanza itakuwa mbali na kina Geb. Mpaka inafika saa tano asubuhi ya siku hiyo, nyumba ikawa kwa jina la ‘Grace Magesa’.

           “Asante sana Geb. Nakushukuru sana kaka yangu. Sijui niseme nini!” Grace alijikuta machozi yakimtoka mara baada yakutoka kuandikishana na Danny. Alikubaliwa kuchukua watoto wake mara baada ya kurudi safari na baba yao. Na nyumba ilishakuwa yake. Hakuwa na jinsi yakumshukuru Geb kwa pesa yote aliyomlipia na kusimama na yeye mpaka mwisho. “Cha kwanza ujue unastahili. Ile nyumba ni yako. Nilikuona jinsi ulivyokuwa ukihangaika nayo. Cha pili, umesimama na mimi G, tokea naanza ile biashara mpaka sasa. Hayo ndio matunda yake. Hongera.” Grace akabaki kama akifikiria.

“Nini tena?” “Naomba tukae sehemu tuzungumze.” Alikuwa Grace na Geb tu. Wakaenda kukaa kwenye gari. “Nampenda Man.” Geb akacheka. “Nafikiria hata akitaka kuja kunioa, sitafikiria mara mbili. Itakuaje?” “Kuhusu nini?” Geb akamuuliza akiwa anajua kabisa ni nini anafikiria. “Maisha yetu sisi wawili.” Grace akaanza kulia.   

“Hatujawahi kutengana Geb.” “Na wala hatutatengana.” “Man anaishi Arusha. Amejijenga sana kule. Na wewe umejijenga sana huku. Siwezi kuishi mbali na Man wala wewe. Nitafanyaje?” Geb akacheka. “Naomba utulie G. Kuna mambo mengine hayana majibu kwa haraka. Lakini mimi nataka kukuona unafuraha. Nataka kukuona upo kama ulivyokuja na Man. Full of yourself. Na kwa kuwa yeye ameweza kukufanya hivyo, nakushauri usiachie hiyo nafasi endapo atakutaka kwa ndoa.” Grace akamwangalia.   

“Na kazini?” “Kumbuka na mimi naoa Grace. Mungu amenipa Nanaa. Anaakili na anajituma. Akishajifungua, nitampa kazi zako. Atakuwa anazifanya nyumbani. Kwa hiyo usiwe na wasiwasi. Mungu amenipa msaidizi. Na wewe ukawe msaidizi huko.” Grace akacheka. “Hicho ndicho kilikuwa kinaniumiza kichwa.” Grace akafikiria tena kidogo. “Ila umebadilika Geb! Umekuwa na akili za kiutuuzima kwa kweli. Mungu akufanikishe kwenye ndoa yako.” “Amina. Usiache kuniombea.”  “Siwezi Geb.”  Wakarudi nyumbani.

~~~~~~~~~~~~~~~

“Naona unacheka.” “Namshukuru Mungu mama. Amenitetea. Namshukuru na Geb. Amenirudishia nyumba yangu na watoto. Wakirudi tu kutoka safari, wananipa watoto wangu.” Nanaa alikuwa amejilaza kwenye kochi. Geb moyo ukampasuka baada ya dada yake kusema anamshukuru kwa kumrudishia nyumba yake. Nanaa hakuwepo kwenye picha.  “Sara aliposikia mamilioni ya pesa, Danny akataka kukataa. Naona akaenda kumpanga. Akarudi anataka pesa. Halafu hapo wanasheria wote wakamuogopesha kuwa anaweza kukosa vyote. Geb akamkabidhi ule mkoba wote wa zile pesa. Ungemuona Sara alivyofurahi!” “Mimi namuhurumia sana Danny. Anajizika mwenyewe! Hana mshauri. Waliomzunguka wote hawana akili.” “Na alivyomjuaji yule, atawapa wapambe wake zote, aanze upya. Lakini haanihusu tena. Sasa hivi nipo huru mama. Ngoja niende zangu kwa Man, nimemuachia watoto. Tutakuja baadaye tukisharudisha watoto kwa Danny, ndipo tuje kujiandaa kwa safari.” Grace alikuwa amechangamka kweli.   

          “Vipi   bibi   harusi  wangu?”   Nanaa  akacheka. “Hongereni kwa kufanikisha kila kitu.” “Mbona sasa hujachangamka wakati harusi kesho kutwa?” “Nasinzia hapa, kama mlevi!” “Vipi pressure lakini?” Geb akauliza. “Mama amenipima, nashukuru Mungu imeshuka. Tangia ulivyoondoka nilikuwa  nimelala, ndio nimeamka muda sio mrefu.” “Afadhali. Sikutaka usafiri ikiwa ipo juu.” Wakatulia. “Sisi tupo tayari. Kila kitu kipo kwenye gari. Nilikuwa naweka kimoja hadi kingine kuanzia asubuhi ili nisisahau. Sasa wewe usitucheleweshe.” “Siwezi mama. Usiwe na wasiwasi.” Grace akatoka.   

 ~~~~~~~~~~~~~~~

Baada ya yakurudisha watoto na kuweka mambo yake sawa, Grace aliwapigia simu kina Geb kuwataarifu wao wapo tayari, wakutane uwanja wa ndege. Geb aliwasindikiza familia yake mpaka uwanja wa ndege. Nanaa alikuwa akiondoka na watoto wote, pamoja na mama G. Alikaa kiti cha mbele akiwa ametulia kimya. Geb alikuwa akizungumza na mama yake wakati Nanaa amevuta kiti nyuma, amejilaza. Dawa za usingizi alizokunywa mchana wake zakusaidia kutulia ili pressure isipande ilikuwa sababu tosha ya Nanaa muongeaji kuwa kimya. Man aliwaahidi watapata mtu wa kuwasaidia kazi huko waendapo. Kwa hiyo wasihangaike swala la mfanyakazi. Grace na Man walikuwa wakiendeshwa na Jeri ambaye alitakiwa kurudisha gari ya Grace na kesho yake achukue gari hiyo yenye mizigo ya Nanaa na watoto wake, awafuate Arusha.   

~~~~~~~~~~~~~~~

v Ndoa ya Grace na Danny imeisha rasmi. Kwa haraka kila mmoja kati yao amepata alichokuwa akitaka. Penzi na pesa. Danny anaye Sara. Grace anaye mwanaume wa nguvu, Man.  Mwanaume wa ndoto zake. Kama mwanaume aliyekuwa akimtaka tokea utoto. Mungu ampe nini? Kaka yake amemnunulia nyumba na watoto atapewa baada ya kurudi safari.

Furaha ya watoto wao je? Hatima yao?

v Nanaa amekubali kwa hakika wao ni wamapenzi tu. Hawezi kuingilia mahusiano ya Geb na ndugu zake. Hata hivyo alimkuta yeye na dada yake wakihangaika pamoja kuzisaka pesa. Anaanzia wapi? Kinachomchanganya na kumfanya akose raha ni pale Geb anapomzuia na yeye kuwa na mahusiano na kaka yake.

Ni kwa nini? Kukubali kuingia kwenye aina hiyo ya ndoa ni sawa? Itampa uhuru au ndio kifungo? Akakumbuka ugomvi alioanzisha Geb juu yake na kaka yake. ‘Akinioa je?’ Ndio swali alilokuwa akijiuliza Nanaa akiwa njiani kuelekea uwanja wa ndege ili waende Arusha kwenda kufunga pingu za maisha.

v “Kweli hizi zinaweza kuwa pingu za maisha!” Nanaa akaendelea kuwaza. Akajiangalia tumbo la mtoto aliyebeba. “Inamaana mimi na huyu mtoto wa Malii tutaishi kwa kudra za Geb tu!? Hataniruhusu nijishugulishe wala kufanikiwa wakati yeye na ndugu zake wanastawi!”

Nanaa aliendelea kuwaza wakati Geb akiendelea kukanyaga mafuta kuelekea uwanja wa ndege.

               Ni Nini Kitaendelea? Usipitwe.


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment