Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni Wangu! – Sehemu ya 60. - Naomi Simulizi

Ni Wangu! – Sehemu ya 60.

Wakati geti likifunguliwa, tayari ilishakuwa saa mbili kasoro. Kila mtu alijua ni Grace na mgeni wake ndio wanaingia. Jeri alienda kumuachia gari yake uwanja wa ndege. Kwa hiyo Grace alipofika tu, akakuta gari yake kama alivyoelekezwa na Jeri, na sehemu alipoficha funguo. Vilisikika vicheko kuanzia wanashuka kwenye gari mpaka mlango wa kuingia barazani. Wakasikia wakinong’ona kidogo, kisha wakasikia kengele.

Geb alikuwa amemuweka Magesa begani, Liv amemlalia mama yake. Wote wamevaa nguo zao zakulalia tayari kwa kwenda kulala baada ya salamu na anti yao. Geb akasimama kwenda kufungua mlango na kuwakaribisha. Walimsikia Geb akisalimiana nao hapo nje. Grace akatoa utambulisho. “Geb, huyu ni Manase au Man kama wengi walivyozoea kumwita. Na Man, huyu ni Geb. Magesa mkubwa na huyu ndio Magesa Jr.” Wakasikia wakisalimiana. Mwishowe wakaingia ndani.  

Alipomuona tu Man, mama G akainama na kuguna huku anatingisha kichwa. Grace akaanza kucheka. “Sasa mama unaguna nini jamani!?” “Mie huyu? Akuu! Nasafisha koo. Karibuni.” Kila alipokuwa akiwatizama vile walivyosimama pamoja, tabasamu lilimjaa mama G. Man alikuwa na umbile na muonekano kama ndoto za Grace. Aina ya mwanaume aliyekuwa akimwambia mama yake ataolewa naye.  

          “Karibu baba.” Mama G akampa mkono akiwa amekaa. “Asante mama. Shikamoo.” “Marahaba. Poleni na safari.” “Asante. Lakini safari yenyewe ilikuwa fupi. Hatujachoka.” “Afadhali. Karibuni.” Mama G akarudia. “Asante.” Man akajibu kwa heshima zake zote. “Na huyu ndio mama mwenye nyumba wetu. Mke ya Geb! Mama Magesa mwenyewe.” Grace akaendeleza utambulisho. “Nanaa?” Man akauliza. “Haswaa!” Wakacheka. “Karibu Man.” Wakapeana mikono lakini Nanaa alikuwa amejiegemeza kwenye kochi.   “Ningesimama. Lakini unaliona lile jicho la mama pale? Basi kunyanyuka hapa labda kwenda msalani tu, si vinginevyo.” Nanaa aliongeza. Wakacheka kidogo. “Grace aliniambia unatakiwa mapumziko. Usiwe na wasiwasi, hata kule Arusha, tutahakikisha unapata mapumziko yakutosha tu.” Man akaongeza. “Asante. Karibuni sana. Nimefurahi kukuona Grace. Nilikuwa na hamu na wewe?”   “Hata mimi Nanaa. Naamini ulipata salamu zangu zote.” “Geb alizifikisha.” Grace akainama na kumkumbatia.

“Geb ameniambia presha ipo juu kidogo.” “Ndivyo tulivyoambiwa. Lakini wala sijisikii vibaya! Ila tumeona tufuate tu kile wanachotuambia ili tusogeze siku.” “Pole sana.” “Asante. Umependeza sana Grace. Unaonekana unafuraha tofauti na nilivyokuona mara ya mwisho!” “Namshukuru Mungu. Ni neema tu Nanaa. Najua wewe unajua.” Nanaa akacheka, Liv akambusu mama yake pale alipokuwa amemuegemea.  

          “Umemsahau mama mzazi! Ndio anakukumbusha hivyo.” Mama G akaongeza. “Nampenda mama.” “Hata mimi nampenda Liv. Umemuona aunt?” Liv akacheka huku akitingisha kimguu chake. “Anasubiri busu lake hivyo!” Nanaa akaongea naye kwa upendo. Liv akasimama pale kwenye kochi. Grace akamkumbatia na kumbusu. “Ngoja nikubebe kabisa. Nilikuwa na hamu na wewe Liv!” “Nampenda aunt.” Liv akaongea kwa kudeka. “Na mimi nampenda Liv wangu.” Akamkumbatia. “Msalimie anko.” Liv akamchungulia Man, akarudisha kichwa kwa aunt yake kwa haraka. Wakacheka.   

“Kwa maringo huyo! Msalimie anko bwana.” Mama yake akasisitiza, lakini Liv akagoma. “Mpaka amzoee.” Grace akamtetea. “Karibuni jamani. Twendeni moja kwa moja mezani. Wote hatujala tulikuwa tunawasubiri nyinyi.” “Poleni. Nilijua mkila tu mtapata usingizi na mimi nilitaka kuwaona.” “Hamna shida.” Nanaa akaongeza. “Ngoja nikawalaze hawa. Kesho mtapata nao muda vizuri. Sasa hivi watakuwa wamechoka. Wamekuwa na siku ndefu. Tuliwapeleka kwa James pia.” Geb akaaga. “James anaendeleaje?”  Grace akauliza. “Anaendelea vizuri. Amesema atakuwepo kwenye harusi yetu.” “Afadhali.” Grace aliitika.  

“Naomba kumsalimia Magesa. Kama yeye atakubali.” Man alimuwahi Geb. “Man anapenda sana watoto. Yeye ndiye aliyeomba kuona watoto.” Grace akaongeza. Geb akamsogezea Magesa.  Akambeba. Alikuwa ameshasinzia. “Kaka Mkubwa huyo!” Man akasifia. “Mwili ndio mkubwa kuliko umri.” Geb aliongeza. “Halafu wanafanana sana.” Man akaongeza. Liv alikuwa akichungulia tu. “Kesho utacheza na anko?” Grace akamuuliza Liv. Akacheka tu bila kukubali au kukataa. “Eti Liv? Tutacheza wote?” Man akauliza, Liv akajificha kwa aunt yake.   

Walimuona Man akimbusu Magesa kwa upendo mara kadhaa. “Na mimi nina mtoto mmoja wakiume. Nilimlea tokea siku anazaliwa. Mimi mwenyewe. Alikuwa na rangi kama huyu, ila hakuwa mkubwa hivi.” Man aliongea huku akimsugua Magesa mgongoni taratibu na kwa upendo. “Napenda sana watoto.” “Sasa hivi ana umri gani?” Nanaa akauliza. “Atakuwa amekuwa kijana mkubwa sasa. Mama yake alimchukua. Sijamuona zaidi ya miaka 8 sasa.” Man aliongea huku akimtizama kwa upendo na kumpapasa mgongoni Magesa. “Watoto wanasiri kubwa sana. Labda ndio maana Yesu alisema kama tusipokuwa kama watoto, hatuwezi kurithi ufalme wa Mungu.” Man aliongeza taratibu huku akiendelea kumpapasa Magesa na kumtizama.   

“Hongereni kwa watoto wazuri.” Man akaongeza kisha akacheka. “Grace aliponiambia mnawatoto watulivu, nikapata shauku yakuwaona. Nilikuwa na hamu yakubeba mtoto hivi. Yaani nimshike mkononi halafu atulie kama huyu au kama hivyo Liv. Maana ukoo wetu una watoto hao! Huwezi kuwagusa.” Grace akacheka. Akakumbuka watoto wa Malisa. “Yaani kama ungeingia hapa, ndio ikawa ndio kwao, na wao wapo ndani, vile umegonga kengele, unafunguliwa mlango na wao wanakusukuma hapo hapo mlangoni. Wanashindana kutoka hapo mlangoni na wewe mgeni umesimama hapo hapo, ili wawahi nje wakaruke ruke. Kama hujakaa sawa hapo mlangoni, umesimama kihasara halafu hufahamu kama kuna watoto wa namna ile pale, unaweza kuanguka hata ndani hujaingia! Hawana mchana, wala usiku wale watoto!” Wote wakacheka. 

“Huwa tunamuuliza mama yao anachowalisha wale watoto, hamna anayeamini. Watoto wako kama vipepeo!” Wakazidi kucheka. “Ni hali ya utoto tu.” Nanaa akatetea. “Mmh! Muulize Grace kama wale watoto ni wakawaida. Anawajua. Wakiwepo mahali, huitaji kuuliza. Mpaka hamu ya kuwashika inakuja na inaisha, hujawaweka mkononi! Angalau hawa wanashikika. Kesho lazima kulazimishia undugu. Eti Liv?” Man alizunguka akaenda kumchungulia. Liv akacheka.   

“Unaonekana wewe ni mtoto mzuri sana, Liv. Unanywele nzuri kama za aunt. Nani amekusuka?” “Mama.” Liv akajibu huku akijishika kichwani. “Jamani mama anajua kusuka!” Liv akatingisha kichwa. “Nampenda mama.” Liv akaongeza kwa upole. “Hata mimi nampenda Liv.” Man akaigiza. Liv akacheka huku anatingisha kimguu chake, kidole kimoja tayari mdomoni. “Hapo mtapatana. Anavyopenda kupendwa huyo!” Bibi yake akaongeza.   “Umbebe kama hivyo halafu umkumbatie na kumwambia maneno mazuri kwa sauti iliyotulia, hapo mtaelewana.” Bibi yake akaongeza, wakacheka.   

“Basi kesho tutacheza wote. Sawa Liv?” Liv akatingisha kichwa kukubali. Man akafurahia sana.  “Kwani wewe unajua kucheka mpira?” Man akamuuliza. Liv akatingisha kichwa akikubali huku anacheka, kidole chake kimoja bado kilikuwa mdomoni. “Nacheza na dad wangu!” Liv akaongeza kwa sauti ya kitoto na upole. “Basi utanifundisha na mimi.” Liv akatingisha kichwa kukubali. “Asante sana Liv. Basi nitakuja kesho unifundishe.” Liv akakubali huku anacheka. “Umekazana mpaka umekubaliwa!” Grace akamtania. “Si mchezo. Na ameniongelesha bwana!” Man akajibu. Wakacheka kidogo. “Nakushukuru sana Geb. Asante.” Akamrudisha Magesa kwa baba yake, wakaenda kuwekwa kitandani, Grace akisaidiana na kaka yake. Waliongozana Grace akiwa amembeba Liv, Geb amembeba Magesa.  

~~~~~~~~~~~~~~~~

Geb na Grace wakarudi baada ya kulaza watoto, wakahamia mezani. Baada ya kuombea chakula, Nanaa akawakaribisha. “Jamani naomba nishukuru kwa kunikaribisha nyumbani kwenu.” Man akaanza kabla ya kula. “Karibu.” Geb akajibu. Wakajua Geb ataendelea lakini akawa ndio amemaliza. “Anzeni wageni kupakuwa.” Nanaa akasogeza vyakula upande wao. “Nikupakulie nini?” Man akamuuliza  Grace. “Kila kitu. Zaidi ndizi. Napenda ndizi anazopika Nanaa.” Man akacheka kidogo.  

“Haya mama. Nitazila na mimi.” “Ndio utaamini hata  Yusufu haoni ndani.” “Naona hata harufu inavutia.” Man alishachukua sahani akampakulia Grace na kumuwekea mbele yake. Nanaa akamkonyeza mama G. Mama G akatulia tu anajiangalizia. “Kina vutia kwa macho na kinaonekana ni kitamu sana!” Man akaendelea kusifia. Hakuna ugumu kama kufika ukweni. Tena ikawa ni nyumbani kwa kina Geb! Wazito kuongea. Wasikilizaji tu.

“Kwa hiyo Man wewe unaishi Arusha?” Ikabidi Nanaa aulize. “Ndiyo. Nipo hapo Arusha kwa sasa.” “Ooh! Vipi Arusha? Unapaonaje kulinganisha na Dar? Au kwa nini Arusha?” Nanaa akaendelea. Wakacheka. “Nanaa kwa kupenda stori!” Grace akacheka. “Mimi heri niulize tu. Maana namjua mpenzi wangu. Hataongea hata neno moja. Mpaka Man anaondoka humu ndani, tutakuwa hatujamjua.” “Basi hapo mtakutana na Man. Anapenda stori huyo!” Wakacheka. “Hamna shida.” Man akaongeza.

“Nisimulie mwaya Man.” “Basi hapa tutakesha. Hamalizi huyo maswali! Ukimwendekeza huyo, utajuta kuja usiku hapa.” Mama G akaongeza, wakacheka. Nanaa akacheka sana. “Nimeuliza maswali mawili tu jamani!” “Mengine yanakuja. Mimi nakujua wewe. Akijibu hilo, anajingine.” “Hamna shida mama. Ndio mwanzo wakufahamiana.” “Haya baba. Endelea.” Wakacheka. 

“Wazazi ndio walipata ufunuo wakuwekeza Arusha. Walikuwa na hoteli moja ambayo ndiyo hapo mtakapofungia harusi. Baba alipougua ndipo akanikabidhi mimi. Na kwa bahati nzuri na mimi ndio nilikuwa nimerudi nchini kutoka Sweeden ambako nilikuwa nikiishi huko. Na ndiko nilioa na kupata huyo mtoto ambaye nilimwacha kwa mama yake hukohuko Sweeden.” Man akaendelea.  

“Kwa haraka, Arusha haukuwa mji ambao ningefikiria kuishi kwa wakati ule, lakini majukumu yakanifanya niwepo. Nilirudi nikiwa sina chakufanya. Kwa hiyo biashara ya hoteli ndiyo ikawa nafasi pekee yakujishugulisha. Kwanza kusaidia wazazi, pili hata mimi mwenyewe. Lakini kadiri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda ndivyo nilivyoona kuna nafasi ya kuwekeza zaidi hapo jijini. Nahisi nikanogewa. Nimewekeza zaidi kwenye huo mji.” “Hongera. Kwa hiyo biashara kubwa hapo unayofanya ni hoteli?” Nanaa akauliza na kufanya kila mtu acheke. 

          Man akameza huku anacheka. “Chakula nikizuri sana.  Grace umeshinda. Kweli hii ndizi ina shahada zote. Asanteni jamani!” Man alionekana mtu wa shukurani sana. “Karibu.” Nanaa akajibu. “Ni rudi kwenye swali. Biashara hiyo ya baba, iliibua ideas nyingi ambazo nimefanyia kazi baadhi na nyingine bado. Naendelea taratibu. Niliweza kufungua hoteli nyingine mbugani. Ndiko tulikuwa huko na Grace mpaka siku tatu zilizopita.” “Ni pazuri sana. Naamini siku moja na nyinyi mtakwenda kupaona.” Grace akasifia, Man akacheka.  

“Asante Grace.” Man akamtizama kwa upendo kama kitu cha thamani na tabasamu usoni. Nanaa akamkanyaga tena mama G, kama kumkonyeza. “Kwa hiyo Nanaa. Mbali na hizo hoteli, nikafungua kampuni ya utalii hapo hapo Arusha na usafirishaji pia. Ili kuhakikisha wageni wanaofika hapo kwa utalii, wanapata usafiri wa kuwapeleka kwenye hoteli zetu na kuwatembeza hapo mjini.” “Waw! Hongera Man.” Nanaa akasifia. Geb na mama yake kimya.  

“Kwa hiyo huko ndiko mlikokutana na Grace?” Nanaa akaongeza swali lililowafanya wote wacheke mpaka Man. “Si nilikwambia? Hapo ndio ameanza huyo.” Mama G akaongeza. Geb akacheka huku akimwangalia Nanaa. “Eti Geb? Hilo ni swali baya?” “Hapana Nanaa. Unafanya vizuri kuuliza ili ujue.” Geb akaongeza. “Si umeona hata Geb hana wasiwasi. Tuendelee mwaya Man.” “Naomba mimi nimjibie Man ili ale.” Grace akaingilia. “Mimi naomba nimsubirie  tu Man, bwana! Wewe Grace mvivu wa kuongea. Utanijibu kwa kifupi sana.” Walicheka, mpaka Grace akapaliwa. “Nanaa wewe!” “Kweli Grace. Usinielewe vibaya. Wewe upo kama Geb. Mnajibu maswali tu, bila stori ya ziada.” “Sasa wewe ulitaka kujua nini?” “Kila kitu.” Nanaa akajibu. “Nanaa wewe mtoto!” Mama G akaongea huku anacheka.  

“Haya Nanaa. Mimi nilioa mwanamke wa ki Swedish. Huko huko Sweden. Ndoa iliisha miaka 6, kabla sijarudi nchini. Na niliishi kwenye ndoa ambayo nilitamani kuja kuoa nyumbani. Lakini baada ya mikasa mingi sana ya huko ugaibuni, nikakinahiwa hata ndoa. Kwa kujibu swali ambalo najua ungekuja kuuliza, nilioa na nina mtoto mmoja. Kama nilivyokwisha kusema. Na ndoa ilidumu kwa miaka 4, ikaisha kwa talaka.” Wakacheka.  

“Nilirudi nchini nikiwa na maumivu makali mno. Akili na mawazo yangu yote nikawekeza kwenye biashara. Ndio maana umenisikia nina miradi mitatu ambayo ni kama yote inalenga watalii tu. Sasa maisha yangu yalikuwa wazazi na kazi. Nikisema wazazi ni huku Dar. Ilibidi baba kuhamia huku jijini kwa ajili ya kuwa karibu na madaktari wake. Kwa hiyo nikiwa hapa Dar, ujue nipo kwenye kifamilia na nikipanda tu ndege, akili inarudi kikazi.” Man akacheka.  

“Nina mtindo nikiwa kwenye ndege au hapo uwanja wa ndege kabla sijapanda ndege, tukiwa kwenye kusubiria, huwa naangalia abiria kwa makini ili kupata wateja. Endapo nikigugundua wewe ni kuku mgeni, basi nitajitahidi kukushawishi ushukue kwenye hoteli zetu, kuhu nikikuuzia huduma zote nilizonazo.” Man akamwangalia Grace akacheka tena kidogo. “Wewe ni mchokozi Man. Huna lolote.” Grace akalalamika. 

“Hapana bwana.” Man akajitetea. “Haya basi. Nikamuona Grace. Kwanza nikavutiwa na rangi yake. Nikataka kumsemesha, nikaona ukimya kama huu aliosema Nanaa. Nikaona nitulie mpaka kwenye ndege. Wale wahudumu wa ndege nimezoeana nao sana. Tulipangiwa viti mbali mbali, nikaomba nihamishiwe alipo kaa Grace. Nia ya kwanza ilikuwa nimuuzie huduma zetu. Kwa kuwa nilimuona ananukia pesa. Nikajua atamudu huduma zetu. Lakini nilipohamia kukaa naye pale. Nikasahau hata mambo ya biashara. Nikawa kama nishachanganyikiwa. Kwanza alinipuuza. Nikahangaika wee mpaka akanigeukia. Wewe fikiria mtu mmekaa naye kiti kimoja, anakujibu bila kukuangalia! Nikajua nimepuuzwa. Nikahangaika wee, mpaka nikaazima gazeti la jirani ili nimpe yeye ili tu anigeukie anitazame!” Watu wote wakacheka.  

“Sasa kule kuangaliwa ndiko kukanifanya nisahau sasa mambo ya biashara. Nikawa kama nimepigwa na bumbuwazi. Sijui niseme nini! Sasa kabla hata…” Man akainama na kuzidi kucheka. “Uchokozi tu umekujaa! Eti mimi nilimuwahi nikamwambia mimi ni mke wa mtu na nina watoto watatu. Basi ndio mpaka leo hayaishi!” Man aliendelea kucheka mpaka wote wakaanza kucheka. Alikuwa anacheka huku anamwangalia Grace.

“Bwana Grace alinipiga stop! Mpaka nikaishiwa nguvu.” Man alizidi kucheka mpaka machozi. “Ukiangalia kidoleni hana pete! Akajishtukia.” “Waliniibia pete zangu, cheni na hereni zangu zote za dhahabu pale nyumbani. Hata mama nilimwambia.” “Sawa Grace, lakini sasa mimi wakati ule ningejuaje? Ungeniacha hata niongee mpenzi wangu. Sio vile ulivyonishushua.” “Mimi nilikuwa nakutahadharisha bwana.” “Sasa ikawaje?” Nanaa akauliza.

“Basi hapo mmekutana na Man. Anapenda stori huyo! Na hamalizi jambo. Na anachekaga mwenyewe kwenye stori zake, yaani mpaka wewe msikilizaji hata kama hukuwa na mpango wakucheka utacheka tu.” Grace akaongeza. Wote wakacheka, maana kweli Man alipenda kucheka.

“Basi tena. Wewe si unajua vile Grace alivyo mtulivu. Kwanza kashaniwahi yeye mke wa mtu. Nikamwangalia kidoleni makusudi, akajitetea ameacha pete yake nyumbani. Ila ana watoto watatu wa kiume. Anazo picha zao. Haya tuone sasa hizo picha. Akaingi mkobani. Akaanza kutafuta simu, akakumbuka na simu pia hana. Hapo ndio nikamuona ameishiwa nguvu. Nikamuhurumia kweli! Maana alipooza mara mbili yake. Lakini ndipo nikampenda Grace.” Grace akainama.  

“Kwanza nilifurahia kile kiwango cha uaminifu wake kwenye agano alilokuwa nalo na mwenzie. Halafu hakujificha kwangu swala la watoto. Kile kiwango cha ukweli na uwazi kwangu, ni kweli mama yangu, sijawahi kukipata kwa mwanamke yeyote tokea nilipofika hapa Tanzania au hata kule nilipokuwa mpaka nikaoa. Kwanza nilioa kwa kutegwa. Mwanamke niliyekuwa nimemuoa alinitega tena kwa kamera na kuniambia lazima nimuoe ili asinishitaki. Nimekuwa nikikutana na wasichana warembo tu, lakini tokea mwanzo wa hata salamu unahisi uongo mtupu.” Man akaendelea.  

“Sasa kutokea pale, Grace akaamua kunikwepa. Lakini akajikuta amepanda taksi ya kwenye kampuni yangu iliyomleta mpaka pale hotelini kwetu bila yeye mwenyewe kujua. Kwa kuwa nilishaanza kuvutiwa naye, nikataka kuwa naye karibu tu. Ili kufahamu aina hii ya wanawake kama bado wapo hapa duniani. Nakutaka kujua wapo wapi ambako wenzetu wanafanikiwa kuwapata! Wanafanya nini na sisi tunakosea wapi! Maana kwa majukumu niliyonayo ninakuwa nakutana na wanawake wa kila namna. Washindanao urembo, mavazi, sijui nywele. Kila aina ya wanawake huwa nakutana nao kwenye shugli zangu sababu hutumia huduma zetu zaidi kumbi ya pale hotelini. Niliokutana   nao   haikuwa   kwa   uwazi  huo.”  Man akaendelea.  

“Ndipo nikaanza juhudi za kujisogeza sasa. Lakini Grace akawa ananikwepa kitu kilichozidi kunishangaza. Huwa natafutwa kusalimiwa, lakini Grace akawa ananikwepa! Akiniona sehemu hii hapa, anaondoka. Ndio shauku ikaongezeka kutaka kumfahamu Grace. Naamini nimejibu swali lako.” “Haaah! Usinifanyike hivyo Man!” Nanaa alilalamika kwa huzuni sana. Kila mtu alicheka tena. Man alikuwa akicheka huku akimwangalia Nanaa. Alicheka na kucheka mpaka wote wakaanza kucheka tena.  

“Nimalizie tu.” “Acha mwenzio akapumzike Nanaa.” Mama G akaingilia. “Kwani Man umechoka?” “Nilikuwa nakuchokoza tu.” Man akajibu. “Afadhali. Ehe?” Wakacheka tena. “Basi. Baada ya kuhangaika sana nikafanikiwa kukaa naye meza moja akiwa ametoka kukaa nje siku hiyo jioni. Ndio ukawa mwanzo wetu. Lakini nikajikuta mimi ndio nina shida na Grace kuliko hata yeye. Nilikuwa nimebeba mambo machungu moyoni ambayo ni Grace pekee aliyaweza kuyabeba na bado akanitazama kama mwanaume.” Man akainama na kufikiria kidogo.  

“Unajua Grace anautulivu fulani hivi, ambao unaambukiza mtu yeyote anayebahatika kuwa naye karibu, nakukufanya ujisikie umetulia. Ndio kitu nilikuwa nikihitaji. Usiku wa kwanza kuwa naye baada ya kumtoa ili tukaangalie sinema, nikajikuta nimeishia naye kwenye gari, nikitua mizigo yangu moyoni.Unajua kama vile wakatoliki wanavyoungama kwa padre?” “Mimi nilikuwa nasali huko.” “Basi wewe utaelewa zaidi. Basi ndivyo ilivyokuwa kwangu usiku ule kwa Grace. Niliongea machungu ambayo sikuwahi kumwambia mtu yeyote hapa duniani, kwa aibu na kuhofia fedheha. Hata mama yangu kuna mambo sikuwa nimemsimulia, lakini nikajikuta nayaongea kwa Grace mpaka nikapata aghueni moyoni.” Grace alikuwa ameinama huku akimwangalia mara moja moja. 

          Man akamvuta mkono. Akamshika. “Najua watu wanaweza kusema ni mapema sana. Au nimemfahamu Grace kwa muda mfupi sana. Haifai kusema mambo fulani juu yake. Lakini kama nilivyomwambia Mzee Ole, kwa mara ya kwanza maishani ninaujasiri wakusema nimependa. Sijui Mungu atanipeleka wapi mimi na Grace, lakini am in love for sure. Sina shaka juu ya hilo. Na sina hofu kuonekana na Grace popote. Kwanza amebeba sifa za mwanamke wa ndoto zangu. Hata familia yangu walipomuona Grace kwa mara ya kwanza tu, walijua ni kwa nini yeye. Kuanzia rangi yake, utulivu, werevu na ile heshima kwangu. Vyote vimenivutia kwake.” Man aliongea bila hofu.  

“Mama na Geb! Sijawahi kufika nyumbani kwa mtu au kwenye familia ya mtu kukaa kwenye meza hivi kwa ajili ya binti yao. Lakini kwa Grace imenibidi. Nampenda Grace. Tulitumia siku tano mfululizo kufahamiana tu. Najua Grace alipotoka, alipo, ila sijui Mungu atakapompeleka kuanzia sasa. Ila nimemuomba Mungu niwepo kwenye maisha yake. Sio kwa ajili yake Grace tu, ni kwa ajili yangu pia. Najua inaweza kuwa ni kama kwake sio wakati muafaka kufikiria vizuri. Kufanya maamuzi fulani fulani kwa sasa. Lakini nilimuahidi kumpa muda wa kufikiria. Baada ya mambo yake kesho kukamilika, mpaka atakapojiweka sawa. Nimemuahidi kumsubiri mpaka atakapokuwa tayari. Hata kama akitaka nisiwe karibu kabisa ili nisimsumbue kwenye kufikiria. Lakini nilitaka kuwa naye kesho. Angalau niwepo tu kama itatokea atanihitaji mara baada ya kumalizana na mwanasheria au kwenye kipindi hicho.”  

“Pia sitawazonga. Kwa kuwa ameniambia Geb atakuwa naye. Mimi naweza hata kusubiria nje. Akitoka na kuniambia yupo sawa, nitaondoka kabisa kurudi Arusha. Nipo hapa kwa ajili yake tu. Mambo yakiwa sawa, nitaondoka kurudi Arusha kuendelea na mambo ya maandalizi ya harusi yenu. Na baada ya harusi hata kama sitamuona kwa muda ili apate muda wakufikiria zaidi pia nimemwambia nitasubiri. Sitaki mfikirie nitamshawishi vibaya katika kipindi hichi. Nampenda Grace na nimekusudia kuwa naye.”  Man akaendelea.

“Najua na ninaelewa anakopita sasa hivi kwa kuwa na mimi nilipita hapo. Najua maumivu ya kutalikiwa na hofu ya kupoteza watoto. Kwa kuwa na mimi nilishapita hapo. Tena kwa machungu makubwa sana. Hakuna jinsi  yakumuelezea mtu mwingine akaelewa. Ila mimi niliyepita naelewa.” Man akacheka kidogo. “Najua Danny ni mume wa Grace. Na amemuumiza sana. Lakini hata Grace nilimwambia kama ikitokea kesho Danny anamuomba msamaha na kutaka warudiane walee watoto, na yeye akaona ni sawa moyoni mwake, pia asisite kumkubali. Japokuwa nitaumia kumkosa, lakini pia nitamuunga mkono katika hilo ili watoto wao wasiteseke.” “Na kama ataachiwa watoto wote?” Nanaa akauliza.  

“Nitamlea Fili na wadogo zake bila shida. Na hilo nimemwambia hata Grace. Nimemwambia umuhimu wa mama kwa mtoto. Lakini kama ni mama anayetaka watoto wake. Wapo wanawake hawapendi watoto, jamani! Mimi nimeona. Lakini kwa kuwa Grace anapenda wanae, natamani awe karibu na watoto wake na mimi nitakuwepo kumsaidia. Tumezungumza naye. Ataenda kuomba kama Danny anaweza kumkabidhi yeye watoto. Achague siku gani anazotaka kuona watoto. Ataletewa watoto bila shida, ili Grace alee watoto wake.” “Basi wewe una upendo wa kweli.” Grace akacheka nakuinama.  Wengine wakanyamaza. Mama G akabaki anafikiria. Geb ndio na yeye akabaki kimya.

“Geb wewe jamani!” “Nimesikia Nanaa.” “Sema basi hata kitu mpenzi wangu!”  Nanaa akaendelea. Geb akacheka kidogo. Akavuta pumzi. “Labda mama yeye ndio aseme. Mimi nasikiliza tu.” “Mimi nimesikiliza. Labda nianze kwa kukushukuru kwa kumshauri mwenzio vizuri. Ni kweli hatujui kitakachotokea kesho. Kikubwa ni watoto ndio wanao tuweka macho hapa. Lakini mali si tatizo hata kidogo. Hizo zinatafutwa. Ila watoto! Ndio kilio changu. Kwa hiyo nikuwaombea tu.” Mama G akaendelea.  

“Unajua Manase mwanangu, hakuna mama aneyemuozesha binti yake akiwa amejipanga kuja kuona talaka, ila wajukuu. Haya mambo yametokea na kutushtua wote. Yamekuja kukiwa na amani. Hakuna hata aliyejua kutakuwa na machafuko kama haya. Najua Grace atakuwa amekueleza, lakini Danny kwangu hakuwa mkwe tu. Alikuwa mtoto kama Geb. Tena alikuwa karibu na mimi kuliko ambavyo ungeweza kudhani. Tulikuwa marafiki mno. Grace hana tofauti na Geb. Wana ukimya wakuzaliwa na wala sijui wamepata wapi! Lakini Danny ndio alikuwa rafiki yangu. Kinachotokea kesho si kuvunjika tu kwa ndoa ya Grace rasmi, kwangu mimi ni kama msiba. Kuzika mtoto wakumzaa. Ni mtoto yatima ambaye nilimchukua kwangu kama mtoto.” Mama G aliongea kwa huzuni.  

“Pole sana mama. Poleni sana.” Man alitoa pole. “Nashukuru. Kwa hiyo naungana na wewe Man. Najua alikotoka Grace, alipo, lakini sijui kesho yake. Anakopita sasa hivi ni maumivu makubwa sana kwangu. Hasa nikijua vile alivyojitunza na alivyohangaika na Danny huku wanaume wenye uwezo wakimsumbua, najuta sana. Najuta kutoa baraka zangu kwao kwa wakati ule. Najuta, lakini hata sijui ningefanyaje! Nilimpa baraka zangu wakati ule nikijua ndio mwanaume anayeweza kuja kuzikana na  Grace. Sikujali uwezo wa kimali. Lakini ona yanayotokea sasa hivi! Nafikiria wajukuu zangu. Naumia nakujilaumu sana, lakini basi, tumuachie tu Mungu. Najiambia kama mimi yatima, ambaye nilitupwa tu. Sikujua hata wazazi wangu au ndugu zangu walipo, nimeweza kufika hapa, basi, namsihi Mungu aliyetenda kwangu, akatende na kwa wajukuu zangu pia. Awarehemu wajuu zangu. Na kwa kuwa sisi wote tupo hapa, na endapo Mungu atatujalia maisha marefu, naamini tutasaidiana tu ili wakue vizuri.” Mama G akamaliza.  

Wakamgeukia Geb. Japokuwa mama G, hakutoa jibu la moja kwa moja, lakini walitaka kumsikia na Geb pia. “Labda kwa niaba yangu na Nanaa, tukushukuru kwa kumsaidia Grace kutuandalia harusi yetu. Najua una mambo mengi sana muhimu yakufanya, lakini umesimama na Grace kufanikisha hilo. Na asante kukubali kunisimamia kwenye harusi. Najua ni gafla, lakini ilikuwa lazima nimuoe Nanaa jumamosi.” Geb akaongea. Nanaa akamkodolea macho Geb kama anamshangaa. “Naendelea Nanaa. Sijamaliza.” Wakacheka kidogo. 

“Namfahamu Grace mpaka wakati mwingine huwa naogopa. Najua anapokuwa na furaha au huzuni. Hata tukiwa tunaongea kwenye simu, au hata kama akiwa anazungumza na mtu mwingine chumba kingine mimi nikiwa napita nje, nikisikia mazungumzo yao tu, najua Grace yupo kwenye hali gani. Thanks for making her happy.” Geb aliongea taratibu lakini kwa hisia. Grace akafuta machozi.  

“Sijui mtafika wapi, lakini ninaweza kusema, Grace huyu wa sasa au ambaye nilikuwa nikimsikia kwenye simu, sijamsikia kwa muda mrefu sana kitu ambacho kilikuwa kikiniumiza na kushindwa kujua mwisho ni nini. Grace amerudisha furaha na kujiamini ambako alikupoteza muda mrefu tu bila yeye mwenyewe kujua. Niliona mabadiliko hayo muda mrefu sana, na nilikuwa nikisumbuka moyoni bila kujua jinsi ya kumsaidia. Lakini kwa muda mfupi tokea atoke hapa na kuniambia amefika salama, amebadilika sana. Binafsi nimeshukuru. Kwa Grace huyu wa sasa, sina wasiwasi na maamuzi atakayoamua kesho. Kwa kuwa hajajawa hofu wala woga. Ataamua kutokana na anachojisikia yeye. Na Grace ananijua, kwa maamuzi yeyote yale, mimi huwa namwambia ukweli bila kumficha. Na ikifika kwenye kutakiwa nichague, huwa yeye anakuwa wakwanza. Namtanguliza yeye tokea tupo wadogo. ” Geb akaendelea.  

“Kama alivyosema mama. Pesa haijawahi kuwa kipaumbele kwetu. Tokea hatuna kitu mpaka sasa hivi Mungu ametubariki. Pesa haijawahi kuwa kipaumbele, ila utu. Danny tulimfungulia milango yote, lakini akaja kumuumiza sana Grace. Binafsi sijali anachofanya kwangu na mama, lakini kwa Grace na watoto ndicho kinachoniumiza sana. Kwa hiyo naomba usirudie kufanya alichofanya Danny. Kama kuna upungufu wowote kwa Grace, hata ukawa mdogo vipi, lakini ukauona na kufikiri utavumilia tu, tafadhali mwache Grace. Mwache mapema kabisa. Habari zakuja kusema ulivumilia hili au lile hapo baadaye, hapana Man. Nasisitiza, usije kumuumiza Grace. Acha mapema. Usiishi naye kama unamsaidia yaani unamuhurumia kwa hapa alipo sasa au kwa kumvumilia. Nimeishi na binadamu wengi sana, lakini Grace ni mwema. Ni mwema mno. Mwema wakutokujitahidi. Ndivyo Mungu alivyomuumba. Anastahili mema.” “Nampenda Grace, Geb. I handle her with care.” “Ni kweli.” Grace akamtetea Man. Wakacheka. “Basi Mungu awasaidie.” Geb akawa amemaliza.

          Wakaendelea kuzungumza hili na lile. Mpaka Grace na  Man wakaaga. “Grace!” Mama yake akamuita pembeni, wajitenge na Geb na Man pale walipokuwa wamesimama nje wakizungumzia mipango ya harusi. “Tumekuandalia chumba hapa.” Mama yake akamchokoza tu. “Siwezi kumuacha Man peke yake mama. Amekuja hapa kwa ajili yangu. Sioni kama ni sawa kumuacha hotelini peke yake.” 

“Grace wewe mtoto wewe!” Grace akaanza kucheka.  “Kwanza sasa hivi siwezi kulala bila Man. Ananichezea nywele mpaka nalala. Silali huku nalia. Hamna wakunigombesha. Nasikilizwa mawazo yangu. Kwanza naulizwa nitoe mawazo yangu. Hamna mapenzi ya kijeshi. Kuna kuaminiana. Wamenipokea kwao kama nilivyo mimi na watoto wangu. Sijifichi kwa Man. Ananipenda. Akianza kunibusu, hamalizi mama. Uthamani wangu umerudi. Nasifiwa rangi yangu ya mwili! Nina amani. Si ndicho tulikuwa tukiomba hicho?” Mama G akanyamaza.  

 Man akarudi. Alikuwa akizungumza na   Geb mbele kidogo. Walishamuacha Nanaa ndani akiwa ametangulia kulala. Geb alitaka kujua zaidi mipango ya harusi hasa mambo ya garama. Man alimuelezea kwa kifupi garama nzima za harusi na mipango yote. Wakakubaliana jinsi yakulipana pindi Man atakapomtumia garama nzima. Geb hakutaka vya bure. Man akamuheshimu kwa hilo. Wakazungumza wapi pakupata suti zao za harusi ili zifanane na mipango mingine ndipo akarudi kwa Grace.

Hata jinsi alivyomuangalia tu Grace, ungejua anampenda. Alisimama nyuma yake akambusu kichwani, Grace akageuka. “Mmemaliza?” Grace akamuuliza. “Kwa leo naona inatosha. Tuwahi ukapumzike kwa ajili ya kesho ili uamke una akili nzuri na nguvu. Siku ya kesho itakuwa ndefu sana kwako, unahitaji kupumzika.” Man alizungumza naye taratibu kwa sauti ya chini, Grace akiwa amemgeukia. “Okay.” Grace akajibu na tabasamu. Geb na mama yake walibaki kimya wakisubiri.   

Grace akageuka. “Usiku mwema. Ngoja sisi tukapumzike.  Si wote mtakuja kesho?” Grace akauliza. “Lazima mama. Siwezi kukuacha peke yako. Na ujue nakuombea pia.” “Asante mama yangu.” Grace akamshukuru mama yake. Akashangaa machozi yanamtoka. Geb akabaki kimya. “Msiwe na wasiwasi, Grace atakuwa sawa tu. Na kesho Mungu akipenda atakuja akiwa ametulia. Usiku mwema.” Grace na Man wakaondoka.  

Hatima Ya Grace & Danny.

Kikao kilikuwa saa tatu asubuhi. Geb na mama yake walifika pale kwenye ofisi za mwanasheria Upanga, ambako walikuwa na jengo lao la wanasheria wakashangaa marafiki zao karibia wote wapo pale. Geb akacheka na kutingisha kichwa. “Mmmh!  Watoto wamenigeuka vibaya hawa! Siamini kama ni wao.” Mama G akaongea wakati Geb akiegesha gari. “Ila naomba Mungu mtu asikuguse wala asikuongeleshe vibaya.”  “Hapana Geb. Acha tu. Wanatafuta sababu.” Japokuwa walikuwa hawasikii maneno wanayozungumza, lakini Danny muendesha kikao alionekana akikiendesha kwa ushabiki sana. Walikuwa wakicheka na kushangilia.

          “Inamaana wote wale wameacha kwenda kazini leo, asubuhi hii, siku ya kazi, wapo hapa mida hii kushuhudia kuachwa kwa Grace!” Mama G aliongea kwa kuumia sana. “Danny ame..” “Mama! Naomba acha mazungumzo yatakayo kunyima raha. Naomba weka akili zako sehemu unayojua itakufurahisha. Kujiumiza huko ndiko wanakokuta wao. Usiwape nafasi hata kidogo.” Geb alimkatiza mama yake. Mama yake akanyamaza.  

“Hivi unajua yamebaki masaa mangapi nioe?” Geb akamfanya mama yake acheke. “Masaa au siku!?” “Nimekuuliza masaa mama.” “Basi kazi ipo! Unahesabu masaa?” “Sasa je? Namuoa Nanaa, mama. Mwanamke aliyenizalia watoto wazuri. Anajua kasoro zangu zote, na bado amekubali nimuoe.” Mama G akamwangalia huku akicheka. “Hongera.” “Na ninastahili hongera kweli kweli!” Geb akajisifia. Mama G akazidi kucheka. Wakazungumza hili na lile huku wakicheka humo humo ndani ya gari wakisubiria Grace afike.  

Ilipofika saa tatu kasorobo wakaona gari ya Grace inaingia. “Lazima kushuka mama. Sitaki mtu msogelee Grace na kumbugudhi kwa chochote. Sitaki hata wamsalimie. Nataka ile furaha aliyokuwa nayo jana ndio aingie nayo kwa mwanasheria ili awe ametulia. Lasivyo ataishia kulia muda wote nakushindwa kuzungumza chochote.” Wakashuka.  

Man ndiye aliyekuwa akiendesha gari ya Grace. Wakaegesha pembeni ya gari ya Geb wakashuka. Walionekana walikuwa wakicheka. Angalau mama yake akatulia. “Nakuombea Mungu ukue hata kidogo Man!”  Grace alisikika akiongea  wakati  anafunga  mlango. “Umependeza sana Grace.” Grace akacheka na kujizungusha. “Asante mama yangu.” Wote wakawasogelea.  

“Shikamoo mama.” “Marahaba Man, mwanangu. Hata wewe Umependeza.” Wakacheka. “Asante. Sijui mlipata kifungua kinywa? Sisi tulipitia kula kwanza, nahisi ndiko tuliko chelewa.” “Wala hamjachelewa. Sisi ndio tumewahi. Geb alitaka Grace amkute hapa. Lakini tulikula. Nanaa alituandalia kifungua kinywa, tumekula ndio tukaja.” Mama G akajibu.     

“Si mlisema bibi harusi wangu anatakiwa apumzike!?” Grace akauliza huku akishangaa. “Hawezi yule. Kwanza yeye mwenyewe na mwanae Magesa lazima waamke saa 12 asubuhi, wale kwanza ndio warudi kulala.” Wote wakacheka. “Huna utakachomwambia Nanaa akaweza kukaa na njaa. Kama mwanae. Naye yuko hivyo hivyo. Basi akiwa anaamka kula, ndio anapika hapo hapo. Basi na mimi naponea hapo hapo. Lakini tumemuacha amerudi kulala, saa tatu hii mke wa Jeri ataenda kumsaidia mambo yote. Kwa hiyo atapumzika tu.” “Afadhali.” Grace akajibu huku wanacheka.  

“Hongera kwa familia nzuri Geb.” Geb akacheka. “Asante. Namshukuru Mungu kwa kweli.” “Sasa umeshaandika Vows?” Man akamuuliza Geb. Geb akafikiria kidogo. “Natakiwa kuandika eeh!?” Geb akauliza. “Sijui utaonaje. Lakini kwa jinsi nilivyosikia mlikotoka na Nanaa, anastahili kiapo kutoka kwako sio kile cha kila mtu kilichotungwa na watu wengine. Binafsi nimejiapia, kama nitafanikiwa kufikisha mwanamke ninayempenda kanisani, nitatoa vows/kiapo nilichokitengeneza mimi mwenyewe. Kuoa mwanamke unayempenda na anayekupenda hapa duniani ni hadimu Geb. Mimi nimetoka huko. Upo kwenye harusi, badala ya kuona mchungaji mbele yako, unaona ni kama upo mbele ya hakimu anakuhukumu kifungo cha maisha!” Wakacheka.  

“Basi na mimi nitapata muda wakuandaa kiapo changu kwa Nanaa. Nitasubiri mpaka akiondoka kesho ndio nitaanza kuandika ili asije kukiona kabla ya siku.” Wakacheka. “Na mimi nitamwambia Nanaa akundikie.” “Acha kuiba mawazo yangu Grace!” Man alimwambia Grace, wakacheka kidogo. “Sasa unataka sisi upande wa bibi harusi ndio tuonekane duni? Hapana. Na nitahakikisha vow ya Nanaa, inakuliza Geb.” Grace akasifia. “Sasa sio uende ukamwandikie mwenzio!” “Hapana bwana Man! Ila nitahakikisha namvuta hisia zote ndipo nimwambie aandike.” “Mama umekamia! Haaa!” Grace akampiga ngumi. “Maana wazo ni langu, lakini naona mwenzangu umelichukua na kulikuza! Itabidi na mimi nipitie vow ya Geb. Sio asimame pale na mstari mmoja tu. Tukaingia aibu.” “Sasa huko ndio kujazana maneno yasiyo kweli.” Grace akaongeza. Wakazidi kucheka. “Sasa inamaana wewe kumsaidia Nanaa ni sawa, lakini mimi kumsaidia Geb sio sawa?” Man akauliza.  

Upande Wa Pili, Maisha Yanaendelea.

Vikaendelea vicheko na kutaniana kwa muda mrefu mpaka wakajisahau walipo. “Jioni Mzee Ole ameniambia niende nikamsalimie na watoto.” Geb na mama yake wakamgeukia vizuri Grace wakabaki wanamshangaa. “Sasa mbona mnanishangaa!? Anajua kama nimerudi hapa Dar. Man alimwambia tutakuwa na mapumziko ya siku mbili, akaomba nifike kwao nikamsalimie. Kwani mama ni vibaya?” Grace akauliza kwa upole.   “Mmmmh!” Mama G akashindwa chakujibu pale mbele ya Man.

“Ni chakula cha jioni tu mama. Hamna kitu kikubwa sana.” Man akaongeza. “Wamekuwa wakimsikia na kuziona tu picha za Grace. Baba na mama ndio wameomba kumuona. Kama tukiweza kupata watoto, pia ingekuwa vizuri ili na wao wakamuone babu Ole. Anaakili kama wajukuu zake! Kama wakimkuta leo ana hali nzuri, nina uhakika watafurahia sana kuwa nae.” Man akaendelea kusisitiza. Mama G akanyamaza.  

“Sasa mama mbona hujibu jamani!?” “Sijui niseme nini Grace!” Mama G akajibu. “Chochote kile.” Mama G akanyamaza. Wakamuona anafuta machozi nakuondoka pale. Geb akataka kumfuata. “Naomba mimi nikazungumze naye, Geb. Wewe baki hapa na Man.” “Mama ameingiwa na hofu G. Naomba umuelewe.” “Mimi najua Geb. Lakini…” Grace akanyamaza akaanza kulia na yeye.  

“Nisikilize G, mimi nipo hapa tokea saa mbili na nusu, ili kuhakikisha unaingia kwa mwanasheria ukiwa umetulia. Naomba nyamaza kabisa ili uweze kukamilisha jambo lililotuleta hapa. Sitaki uingie kule ukiwa unalia, nakushindwa kuzungumza kabisa. Unanisikia?” Grace akatingisha kichwa. Man akamvuta pembeni kidogo na kumkumbatia. Alizungumza naye maneno machache sikuoni, Grace akafuta machozi na kwenda alikokuwa mama yake nyuma ya gari ya Grace.  

Man Kwa Geb.

Man akanza “Nampenda Grace.”  Kimya. Geb akabaki akimtizama. “Si kwa kutaka kumpotezea muda au kwa kuja kumuumiza tena baadaye. Nampenda dada yako, Geb.” Man akaendelea kujieleza. “Mimi ni mtu mzima kwenu. Japokuwa naweza nikawa sijawapita sana, ila ni mtu mzima ninayejua maisha ni nini na wanawake wakoje. Kwangu Grace sio mtu ninayetaka kupoteza naye muda tu. Sina huo muda wakucheza na wanawake, na sio asili yangu.  Nampenda Grace kwa hakika. Sijawahi kumpeleka mwanamke nyumbani kwetu, Grace ndio mwanamke wangu wa kwanza, na ninaomba Mungu asije kutokea mwingine.” “Na huyo uliyekuwa umemuoa Sweeden?” Geb akauliza.  

“Huyo hata wazazi wangu hawamfahamu. Ni mwanamke ambaye..” Man akamuelezea Geb kwa kifupi sana, lakini Geb akaelewa. “Pole kwa matatizo.” Geb akajikuta akimuhurumia. “Asante. Kwa hiyo nilirudi hapa nyumbani kwanza nikijihami sana na wanawake, pili nilikinahiwa Geb. Sikuwa na hamu na mapenzi kutokana na mahusiano au ndoa niliyokuwa nayo. Ilikuwa ngumu kuliko ambavyo naweza kukusimulia na ukaelewa. Heshima hamna. Alinitumikisha kama mbwa. Vile anavyotaka yeye yule mwanamke, tena mbele ya mtoto wangu.” Man akaendelea.  

“Nikikwambia nipo kwenye hoteli ya baba yangu, ujue niliikuta ikitaka kufa. Nikazama humo ndani kuifufua. Akili na mawazo yangu yote yalikuwa huko mpaka juzi nilipokutana na Grace. Nilikuwa sina muda na kitu kingine ila miradi yangu tu. Na nilipopatwa na hamu ya kuanzisha familia tena, nikajaribu sasa kuangalia wanawake kama wake sio wateja. Napo ndio nikaona ni heri nirudi tu kazini. Utapeli mwingi. Hakuna uhalisia wa chochote. Moyo ukaingiwa na hofu tena. Nikajua historia itajirudia tu. Nitaangukia kule kule. Nikaachana kabisa na wanawake.”  

“Najua wewe ni mfanyabiashara. Unajua jinsi pesa inavyotafutwa kwa shida. Halafu uje ufike mahali, uishie sehemu ambayo aidha huwezi kuitumia kwa raha sababu ya karaha ya mwanamke, au muishie kugawana na mwanamke mliyekutana naye mwaka mmoja, mkafunga ndoa, halafu mahakama inaamuru mgawane sawa sawa! Usinifikiri mimi ni mbinafsi, lakini hilo nalo likanifunga sana. Nikaona ni heri kuacha kwanza.”

“Ninapokwambia nampenda Grace, ni kwa kuwa nimeona uzee wangu na Grace. Simuoni Grace kama mwanamke anayekidhi haja zangu leo, halafu kesho nakimbilia kitandani na mwanamke mwingine. Kwanza mimi ni muoga. Kwangu Grace, ni Grace ya Rehema kutoka kwa Mungu. Nasema Mungu amenirehemu na kunipa Rehema au Grace kama nyinyi mnavyomwita kwa lugha ya kingereza.”   Man akaendelea.

“Si kwamba nampenda Grace kwa uzuri kama wengi wanavyoniambia sasa hivi. Kwamba nimechanganywa na urembo au umbile la Grace. Hapana. Ni zaidi ya muonekanano wake. Dada yako ametulia Geb! Najua hilo unalijua. Lakini sijui niseme nini, ila Grace ananifanya napumzika. Sina hofu. Kuna hali fulani ninaipata ninapokuwa karibu na Grace. Sasa sijui ni ule utulivu wake au am in Love, sijui! Ila ninachojua kwa hakika namuhitaji Grace. Swala la kwamba ninaharakisha kusema hivyo wakati nimemfahamu siku chache hata mwezi haujaisha, hilo sikubaliani nalo. Kwa kuwa mimi ndiye ninayejisikia. Nilikuwa natafuta kitu nilichopata kwa Grace tu.” Geb akavuta pumzi na kuzishusha akimwangalia mwanakaka huyo mtanashati. Mtoto wa mjini akitoa sera zake mbele yake. Ni kweli Man  alionyesha  ipo  Neema  ya  pesa. 

“Ninachoomba Mungu, ni hiki anachokipitia Grace leo, kisije wahi kutokea tena maishani mwake. Ni hilo tu Man. Kwa hiyo naomba kuwa mwangalifu sana. ‘She is very delicate’ kwa kuwa anajua kupenda sana. Naomba usimfikishe mbali ambako unajua huna mpango naye wa muda mrefu. Tafadhali sana Man.” Geb akasisitiza. “Nakuahidi Geb. Leo tumesimama hapa kwa jambo lisilo heri, lakini nakuhakikishia, kama Mungu atatupa miaka mingi zaidi, ujue utaendelea kuniona nimesimama pembeni ya Grace daima. Nakuhakikishia Geb. Mimi sio tapeli. Na sina sababu ya kuwa hapa kama nina nia yakumchezea Grace. Mbona nazungukwa na vitoto vidogo tu! Si ningeishia naye hotelini na ndio ikawa basi? Lakini nipo hapa kwa sababu nimempenda Grace, na ninataka kushuhudia akiwa huru. Wakati Danny anamtaliki leo, ni huzuni kwenu, lakini kwangu ndio nimejibiwa maombi.” Wakacheka kidogo.

“Kweli kabisa. Naogopa hata asibadili mawazo, japo ahadi ya kumuunga mkono endapo atataka kurudiana na muweme ipo pale pale sababu ya watoto, lakini upande mwingine naomba Mungu leo muujiza wangu ukamilike.” Geb na Man wakaendelea kuzungumza taratibu wakisubiria muda.  

Grace kwa mama yake.

Grace akaanza mara alipomsogelea mama yake. “Nampenda Man, mama. Na yeye ananipenda.” Akaendelea.  “Hajanilazimisha kumpenda. Amenipa uhuru wa kumpenda na safari hii nimependa mama. Naomba Mungu asibadilike. Kama yupo hivi alivyo kiukweli na asibadilike, basi ujue kufunga kwangu Mungu amekusikia. Kunikataa Danny, sio fedheha.  Man ndio mlango wangu wakutokea mama yangu. Nimemwambia yote kuanzia mwanzo wangu mimi na Danny mpaka hivi leo niliposimama naye hapa. Bado Man ananipenda na kuniheshimu.” Grace akaendelea.

“Tulikuwa naye huko mbugani. Akaniacha hapo siku moja ili nipate muda wangu peke yangu wakufikiria. Akaniambia niwe huru kumuuliza yeyote na kama nikijisikia moyoni sipotayari kuwa naye, basi niondoke. Alinitafutia hoteli nyingine jijini Mwanza. Kwamba niende nikapumzike na huko. Akaniambia nipo huru kutorudi pale mpaka nitakapokuwa tayari naye. Au hata kama sitakuwa tayari, basi. Yeye anaelewa. Akaondoka na kuniacha pale.” “Nimepata muda wa kumuomba Mungu. Nimetulia mama yangu. Naona Man ni mwanaume atakayenifaa. Ananiheshimu na kuniamini.”

“Hamna tena kutukanwa na kudhalilishwa mbele za watu. Najua hata nikiwa naye nitakuwa na amani. Yale mambo ya ugomvi kila siku kama nimefumaniwa hayatakuwepo. Halafu ananifanyia mambo ambayo hata sikuwahi kufanyiwa kwenye mapenzi. Nilikuwa nasikia tu kama yapo. Danny alikuwa hajui na wala hakutaka kujifunza, alisema ni uchafu.” “Grace wewe mtoto!!” Mama yake akashituka sana.  

Grace akacheka. “Kweli mama.” “Naomba unyamaze.” Grace akazidi kucheka. “Mwenzio siku hizi nafurahia kweli mapenzi. Sichubuki tena. Yale mambo yakupaka mafuta kila nikitaka kufanya mapenzi yameisha. Man anani…” Grace akaangalia kulia na kushoto akamwinamia mama yake sikioni na kumnong’oneza. “Grace wewe mtoto!” “Kweli mama.” “Haya naomba unyamaze. Nyamaza kabisa usiniambie uchafu wako.” Grace akazidi kucheka. “

“He is a love machine’, mama. Ninafuraha.” “Mmmh!” Mama yake akaguna huku akimwangalia kwa pembeni maana aligeuka baada ya Grace kumnong’oneza. “Sasa unaguna nini?” “Nakuona ulivyo furahi!” Grace akazidi kucheka. “Sasa geuka nikwambie kitu kingine.” “Usiniambie mambo yako machafu.” Grace akazidi kucheka. “Sasa nitamwambia nani mama, wakati mwenzio sina rafiki halafu nikiwaambia watu wengine wataniona mshamba.  Watanicheka. Watashangaa na uzee huu sijui mapenzi! Hata yeye mwenyewe Man sijamwambia. Nikajidai najua.” “Wanaume wanajua sana kama mwanamke ni mgeni kwenye jambo au la. Amekustahi tu mwenzio.” “Mama!” “Kumbe. Wewe niambie hicho unachotaka kuniambia.” Grace akacheka.  

“Nimejiambia hivi, hata kama atakuja kubadilika baadaye, ni angalau huyu nitakuwa nimefaidi kidogo mama yangu kuliko Danny.” Grace akatafuta uungwaji mkono. “Nisikilize tu mama na uwe mkweli. Tokea naanzana na Danny imekuwa ni hekaheka mpaka leo. Sisi ni shida tu. Kama sio shida ya kifedha, basi maisha yakijeshi tu. Hakuna kuaminiana. Tulianzia chini mnoo. Mungu akatutokezea kwenye upande wa pesa, ukaona jinsi alivyobadilika. Siwezi hata sema kama nimepumzika na Danny. Acha nipumzike mama yangu. Hata kama ni kwa muda. Acha na mimi nile starehe kidogo. Tafadhali mama yangu naomba niunge mkono.” Grace akambembeleza mama yake.  

“Kwa hiyo unaenda kwa wazazi wake?” Mama yake akamuuliza. “Acha niende mama. Japokuwa naogopa, lakini acha niende kwa ajili ya Man. Anasema hajawahi peleka mwanamke kwao. Kwake yeye hii ni heshima. Halafu wamenikubali japo mimi si msichana. Wamenikubali mimi na makinda yangu yote! Watoto watatu mama! Wala si mmoja. Wanawajua watoto wote na bado wanataka nifike kwao! Nishazungumza nao kwenye simu. Mzee Ole anaonekana nimtundu kama Man au Malisa ambaye ni dada yake Man, lakini mama yake ni mkimya kidogo. Lakini na yeye anaonekana kunikubali. Kwanza hata hawajaonyesha tatizo kwanye swala la kwamba mimi nilisha kwisha kuolewa. Tena Mzee Ole alikuwa akimtania Man kuwa anatakiwa anizalishe harakaharaka ili  Danny akijua azire kabisa. Amwachie.” Mama yake akacheka kidogo.

          “Kwa hiyo utazaa tena?” “Mungu akinijalia mama, nitamzalia Man bila shida. Hata akitaka watoto wawili, nitazaa tu.” “Grace wewe mtoto!?” “Kabisa mama. Nina shida gani?” “Mmmh!” “Lakini nisifie basi mama! Najua unaogopa nisije kuingia tena matatizoni. Lakini tuwe wawazi. Safari hii nimekuletea dume la ukweli. Au unasemaje?” “Hapo sina ubishi. Na hakika mnapendezana. Wote warefu. Na nikijana anayeonekana anabusara.” “Asante mama yangu. Namshukuru Mungu pia amejawa upendo sana. Anajali mno.” “Anaonekana.” Mama G akajibu na kupotelea mawazoni.  

Kwa Danny Na Wapambe Wake.

Danny na marafiki zake bado walisikika wakishangilia. Mara kwa mara vilisikika vicheko vya sauti ya juu huku wakishangilia kishabiki. Geb alijua wazi wanataka kuwakera wao. Walitenganishwa na magari. Kina Geb walisimama nyuma ya sehemu ya kuegeshea magari, japo walionekana wakiingia na wao waliwaona walipokuwa wamesimama kama kundi wakati ndio wanaingia sehemu ya kuegesha magari. Geb na Man wakawasogelea mama G na Grace. 

“Naona muda umefika. Watu wameanza kuingia ndani.”Geb akaongea wakati wameshafika. Grace akavuta pumzi.“Njoo.” Man akamuita. “Mimi nitakuwa hapa nje nakusubiri.” Akaongea kwa sauti ya chini na kumbusu midomoni. “Naomba twende wote.” Wakamsikia Grace akiongea taratibu. “Unauhakika?” Grace akatingisha kichwa kukubali. Man akamgeukia Geb na mama yao. “Eti ni sawa na mimi nikaunga msafara?” “Unamaanisha mpaka ndani kabisa kwenye chumba cha kusainishana!?” Geb akauliza akimwangalia Grace. Grace akatingisha kichwa kwa wasiwasi. Geb akamwangalia mama yake. “Naomba niwe muwazi kwako Man. Danny nikijana asiye na staha ya maneno hasa sasa hivi akiwa na hasira na sisi, na akiwa na lengo la kutukomoa. Ana maneno machafu na ya kukera sana. Sitaki upite huko. Kwa kuwa amekuwa tatizo letu, tumelea huo uozo kwa muda mrefu sana, acha sisi tukamalizane naye, uanze na sisi kukiwa kuna amani.” Kidogo wakaelewa mama yao anachomaanisha.

“Ni kweli Man. Danny anaweza kuchafua hali ya hewa, ukatoka pale hata ukashindwa kumtizama mama usoni. Sikuwa nimefikiria hilo.” Grace akaongeza. “Nimeelewa. Basi ujue mimi nipo na kama utanihitaji jua nakusubiria nje ya chumba cha huo mkutano.” Man akamshika mkono. “Naombeni tuombeni kwanza.” Mama G akatoa wazo kabla hawajaondoka. “Hatuna kimbilio jingine isipokuwa Mungu. 

Naomba tujitakase. Tuombe toba kwa chochote kile au popote pale tulipokosa. Kisha tuombe rehema na hekima za Mungu katika hili.” Wakashikana mikono, mama yao ndio akaanza kuomba. Aliomba huyo mama kwa machozi, akimwita Mungu ajidhihirishe hata katika hilo. Akatubu na kujinyenyekeza huku akiomba rehema. Akamaliza. “Amen.” Kila mmoja akaitikia.  

~~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati wanaingia mlangoni wakasikia minong’ono wakiwasema. “Wamekimbia nini?” Wakawa wakicheka. Walipotokezea tu wote wakanyamaza. Man alikuwa mgeni kwao. Hakuna hata aliyemsalimia mama G. “Habari zenu?” Man akasalimia, wachache wakajibu. Geb akamsogelea secretary, akajitambulisha. “Nafikiri mnasubiriwa nyinyi tu.” Akamjibu Geb. “Ni chumba kipi?” Yule dada akasimama ili kuwaelekeza. “Grace!” Walipofika mbele kidogo Man akamvuta mkono.  

Walikuwa wamepita lile kundi la wale vijana. “Nitakuwa hapa kwenye hivi viti nikikusubiri. Sawa?” Grace akainama, akaona anafuta machozi. Alishamuona amebadilika baada yakuona lile kundi la wale vijana. “Niangalie Grace.” Man akamshika kwenye shingo na mikono yake yote miwili. “Utakuwa sawa, usiwe na wasiwasi. Na ukitoka, utanikuta hapahapa nikikusubiria.” Tayari machozi yalishafika kidevuni. Man akamkumbatia huku akinyonya midomo yake mpaka akatulia. “Utakuwa sawa?” “Nipo sawa.” Grace akajibu na kuanza kuondoka.

Man akamkimbilia na kumvuta tena mkono. “Usisahau nakusubiria.” Grace akatingisha kichwa kukubali. Man akambusu tena. “Nakupenda Grace.” Man akaongea taratibu huku akimtizama. Grace akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha taratibu. “Nisubiri. Usiondoke.” “Siwezi.” Man akajibu. Grace akajisogeza karibu naye, na yeye akambusu kwa muda kidogo. “Nitakuwa sawa. Hata hili nitalimudu!” Grace aliongea kwa ujasiri. Man akacheka. “Nakuaminia.” Wakacheka, Grace akaondoka. Wapambe wa Danny waliona na kusikia kila kitu, wakanyamaza kimya. Grace akaingia ndani.  

~~~~~~~~~~~~~~~~

Grace aliingia akakuta upande wa kulia wa meza amekaa Danny na Zinda. Katikati ya ile meza upande wa juu alikuwa amekaa kijana mtu mzima kidogo, ambaye baadaye kidogo alikuja kujitambulisha ndio mwanasheria na mwanamke mwingine ambaye alijitambulisha kama mtu anayehusika na Ustawi wa Jamii alikaa upande wa chini wakiangaliana na yule mwanasheria. Geb na mama yake walikuwa wamekaa upande wa kushoto, Geb alisimama akamvutia kiti dada yake alipoingia ili akae. Akakaa. “Asante.” Grace akamshukuru. Wazi walionekana walikuwa wakimsubiria yeye.  

           Baada ya salamu, mwanasheria akaeleza kilichowaleta pale. Kwamba Danny anataka Grace asaini hati ya talaka. Grace akaomba zile karatasi, akamkabidhi Geb zile karatasi zote. Geb alianza kusoma moja hadi nyingine huku akimpa kila aliyosoma yeye nakuridhika, asaini. Kulikuwa na ukimya wa namna yake ndani ya kile chumba wakati Grace akisaini talaka yake. Alikuwa ametulia tu, pembeni yake akiwa Geb akipitia zile karatasi kwa makini kabla dada yake hajaweka saini yake. Walipomaliza, wakamkabidhi yule mwanasheria. Akazipitia. Akaona zipo sawa.  

“Limebaki swala la watoto na mali.” Mwanasheria akaanza tena. “Ile nyumba nimewekeza pesa nyingi sana. Siwezi kuhama pale. Uzuri kwamba nimetunza kumbukumbu za garama zote.” Danny akadakia. Geb alishazungumza na Grace wakawa wameelewana. Grace alibaki tu kimya. “Unasemaje Grace?” Mwanasheria akamuuliza. “Mimi nina mapendekezo. Lakini naomba nitoe la kwanza.” Grace akaanza. “Karibu.” “Lengo la kujenga ile nyumba, ilikuwa si kuiuza. Tulitaka watoto wetu wawe na kwao. Akiishi baba yao na mimi, ita..” “Haitakaa ikatokea tena.” Danny akadakia.  

“Naomba tumpe nafasi Grace amalizie. Tafadhali Danny.” “Nataka kumfupishia maneno. Asiwe amekuja akiwa amejiandaa na kilio akifikiri nitamrudia. Huo ni ukurasa ambao nishafunga.” Grace akanyamaza. Geb na mama yake hata hawakuongea neno. “Endelea Grace.” “Okay. Ndio nilikuwa nikisema, yeyote atakayeishi pale, iwe ni baba yao au mimi, lakini tujue ni garama tuliwekeza pale. Iwe ya mali au hali, ni kwaajili ya watoto. Binafsi nisingependa iuzwe.” “Kwa hiyo ulitaka na wewe uje uishi pale? Maana mimi naoa?” Danny akakatisha tena.  

“Hapana.” Grace alijibu akiwa ametulia kabisa. Akili ikafanya kazi kwa haraka. “Kwa kuwa wewe unakaribia kuanzisha familia, nafikiri ni busara ukaishi tu pale. Lakini mimi nitachukua watoto.” “Ati nini!?” Danny akahamaki. “Naomba umuache amalize. Au ndio umeshamaliza Grace?” Mwanasheria akauliza. “Hapana.” Grace akajibu taratibu. “Afanye haraka. Watu tunashuguli zetu. Hata kama wanatuona hatuna pesa, tunashuguli zakufanya hata sisi. Tuache dharau.” Hata yule mwanasheria akapigwa na butwaa. Kimya.  

“Anaweza     kuendelea?” Ikabidi yule           mwanasheria amuulize Danny. “Ndio maana yake!” “Karibu Grace.” “Nisingependa watoto wangu wakue bila baba yao. Lakini wale watoto bado ni wadogo sana. Ningetamani kuwakuza mimi mwenyewe. Ni watoto wadogo, halafu ni wakiume. Najua wanangu niwatundu sana. Hakuna..” “Sio..” Danny akamkata Grace. “Nisikilize Danny. Wote tunashuguli zakufanya. Naomba tuheshimiane. Unapozungumza wewe, watu wote wanakusikiliza. Kwa nini anapozungumza mtu mwingine unashindwa kusikiliza? Anachozungumza Grace ni cha msingi sana. Hapa tunaweka hisia zote pembeni tunataka kujua hatima ya watoto. Na ndio maana kisheria nipo Hapa. Ukishindwa kutulia, utataka ifunguliwe kesi ambayo nakuhakikishia, utakosa watoto na nyumba. Kwa kuwa kisheria watoto chini ya miaka 7, wanatakiwa kuwa chini ya uangalizi wa mama yao, endapo mama yupo hai. Na kwa kuwa wewe ndio humtaki Grace, kisheria unatakiwa utoke na mizigo yako tu, umuachie Grace ile nyumba na bado uwe unampa pesa za matumizi kutokana na mshahara wako. Sasa useme kama unataka tufike huko sasa hivi au tunamsikiliza Grace.” Yule mwanamke wa Ustawi wa jamii, akamjia juu Danny. Alionekana kukereka tayari. Kimya.

“Naomba kukusikiliza Grace.” “Asante.” Grace akaendelea. “Nilitaka kulea watoto wangu mimi mwenyewe kama nilivyotangulia kusema. Hakuna mwanamke ambaye anaweza kulea wale watoto, akaweza kuishi nao kwa amani isipokuwa mimi mwenyewe ambaye nimewazaa. Sidhani kama kuna mwanamke yeyote atakayefurahia kuingia kwenye ndoa yenye watoto wadogo watatu. Tena ambao bado wanavaa diaper! Najua kulea jinsi ilivyo kazi jamani.” Grace akaendelea.  

“Naombeni nilee watoto wangu mimi mwenyewe. Sihitaji hata shilingi ya Danny, na wala sitataka ahame pale. Ila asije akawahi kupauza, au kuja kurithisha watoto wake wengine. Ibakie nyumba ya wanangu tu. Na tukirudi kwenye swala la watoto, nitahakikisha lazima wanamuona baba yao. Kwa kadiri ya nafasi ya Danny. Mimi nitahakikisha wanamuona baba yao na wanamtambua Danny kama baba yao. Ni hilo tu.” Grace akamaliza.  

“Umesikia Danny?” Yule mwanasheria akauliza. “Kwa hiyo sasa hivi naruhusiwa kuongea? Maana nilijaribu kuzungumza, naona nikakatishwa.” Yule mama akaguna na kutingisha kichwa. “Karibu.” Yule mwanasheria akaona aende kwenye pointi. “Mpaka mwisho wa mwezi huu nina ratiba na watoto wangu. Nimeshaomba likizo kazini, nataka kusafiri na wanangu. Kwa hiyo kama ni kwenda kwa mama yao, iwe baada ya safari.” Danny akajibu kibabe.  

“Ambayo itakuwa tarehe ngapi?” Yule mwanasheria akauliza. “Nimesema nitamjulisha.” Danny akajibu. “Hapana. Tumekubaliana leo ndio tuweke hitimisho la kila kitu. Unaishi na watoto wadogo sana ambao kisheria huruhusiwi. Nilazima kuweka mikakati yakueleweka.” Kimya.   

“Naomba niombe kitu kimoja.” Grace akaongea kwa upole. “Karibu Grace.” “Hii ilikuwa nafasi yangu yakuzungumza. Mbona mnampendelea Grace? Au mmeshakula pesa yao?” Danny akalipuka kama moto. “Nimekuuliza, ukakaa kimya

Danny.” “Kwani siruhusiwi kufikiria? Mnataka nijibu kama mashine halafu mje mnigeuke? Nina haki yakufikiria. Acheni dharau.” “Nisikilize Danny. Hii kampuni haiendeshwi kwa rushwa, ila sheria. Ulikuja kwangu wewe mwenyewe. Hata hawa watu mimi sikuwa nikiwafahamu. Grace ndio leo namuona hapa kwa mara ya kwanza. Punguza hasira, tumalize hiki kikao.” Mwansheria akajibu.  

Zinda akamgusa. “Tulia Danny. Tulia tumalize.” “Sitaki kuonewa! Kama watu wanatumia ushirikina hata humu ndani kupumbaza watu, ndio wajue uchawi wao hauwezi kunipata mimi. Waliyonilisha nilishatapishwa. Tena nimewekewa ulinzi ambao hawawezi tena kunigusa.” Danny akaendelea. Kimya. Hakuna aliyejibu.

Palipotulia, Mwanasheria akamuuliza tena. “Umepata tarehe?” Danny akataja tarehe ambayo ni mwezi mmoja kuanzia hapo. “Haiwezekani! Hao watoto ni wadogo sana Danny. Hawawezi kuishi mwezi mmoja bila mama yao!?” “Muulizeni Grace kama mimi sikuwa nikihusika kuwalea hao watoto. Tena ni kama niliwalea mwenyewe. Grace hana uwezo wakulea watoto. Alikuwa akilia mara nyingi tu akitaka nirudi nyumbani kwa kuwa watoto wamemzidia nguvu. Hawawezi wale watoto. Hata ushahidi wa jumbe alizokuwa akinitumia nirudi nyumbani haraka, watoto wanamsumbua ninazo.” Grace akaingiwa hofu.  

 “Kwa hiyo kwa akili zako wewe kama wanaweza kumliza mama yao mzazi, unafikiri mama wa kambo atawaweza!? Nipe mimi huo ushahidi nimpelekee jaji. Na kama unafikiri kwa aina hiyo ya watoto ni sawa kulelewa na mama wa kambo, nitakutafuta baada ya miezi sita kama hujaniambia mlishawazika kwa kufungiwa kwenye friji au oven au hata kupigwa mpaka kifo. Tena kama unaenda kuoa kasichana, ujiandae Danny. Kwa hivyo ulivyo wewe mwenyewe, na aina ya watoto mnaowazungumzia hapa, halafu unaanza ndoa mpya! Utaishia jela wewe. Na utanikumbuka.” Yule mama wa Ustawi wa Jamii, akamuhakikishia akisikika ameshakerwa na Danny.  

“Naomba nisikie ombi la Grace.” Yule mwanasheria akamgeukia Grace. “Sijawaona wanangu kwa majuma zaidi ya matatu sasa. Nafikiri ni zaidi ya hata mwezi. Naomba leo jioni nipewe.” “Hivyo sivyo tulivyokubaliana.” Danny akahamaki tena. “Nitawarudisha jumatatu. Leo ni jumatano. Jumamosi ni harusi ya anko wao. Naomba na wao wahudhurie.” “Hapana.  Haiwezekani. Tayari jumamosi ninasafiri nao.” Grace akaanza kulia.  

“Usifanye hivyo Danny. Na mimi nina haki na hao watoto. Nimekuachia siku zote hizo! Na nimekukubalia ukae nao mpaka huo muda uliosema. Unashindwa kuniruhusu nikae na wanangu kwa siku tano tu!? Tena kwa kitu maalumu kama hicho! Mimi sidhani kama unanitendea haki Danny.” Grace akalalamika.  

“Cha kwanza sio kwamba wewe ndio umeniruhusu kukaa na wanangu. Hata mimi najua sheria. Msinigeuze mjinga. Cha pili mnatabia yakufanya mipango yenu ndio muhimu kuliko wengine sababu ya dharau tu. Sasa kama wewe unaona kuna umuhimu wa harusi, basi ujue na mimi naenda kuwatambulisha wanangu upande wa baba yao. Msifikiri mimi ni yatima nisie na watu. Hata mimi ninao watu. Kama mlikuwa mkinichezea kwa uchawi ili nigombane na ndugu wanaonipenda na kunijali, basi ujue nina safari yakuwapeleka watoto wangu Iringa, kuwaona watu walionilea mimi na baadaye kwa familia yangu uliyonitoa  kwa madawa. Tabora kwa kina Zinda.” Ni Grace tu alisikika akilia.   

Alilia kwa uchungu. Wote walikuwa kimya. “Naomba sisi tuondoke.” Grace akataka kutoka. “Subiri kwanza Grace.”  Yule mama akamzuia. “Hao ni watoto wako. Ni wadogo. Wanahitaji   wewe  uwapiganie.  Hakuna   mwanaume anayejua uchungu wa uzazi ila wewe. Usiondoke bila kujua hatima ya watoto wako. Ikishindikana hapa, tutakwenda mahakamani.  Hata  Ustawi  wa   Jamii  utakutafutia mwanasheria. Usikubali kirahisi.” Yule mama akawa mkakamavu.

“Naomba kujua hao watoto wanaenda lini kwa mama yao, na watakuwa wakimuona baba yao siku gani tena kwa masaa mangapi.” “Masaa!?” Danny akamuuliza yule mama wa Ustawi wa Jamii, kwa ukali huku akishangaa. “Naongea na mwanasheria wako Danny. Mimi siwezi kuzungumza na watu kama…” “Naomba turudi kwenye jambo la msingi.” Mwanasheria akamkata yule mama akataka watulie.  

“Kama nimekuelewa vizuri Danny, safari yako ni ijumaa, sio leo usiku wala kesho. Ni sawa?” “Ndiyo. Lakini leo jioni nina appointment yakuonana na dakatri wao kuhakikisha wanachanjo zote. Ili nikisafiri nao wasiugue. Siku ya kesho nitatumia kufanya nao shopping ndipo nisafiri siku ya ijumaa.” “Mmmh!” Yule mama akaguna na kutingisha kichwa.  

“Hata kama hamniamini, mjue ndio hivyo. Walipokuwa wakiishi na watoto wangu sikwenda mahakamani kuwakataza. Wamezaliwa kwao na kuwafanyia yote waliyoyataka. Sasa safari hii ni zamu yakwenda kwa upande wa baba yao na wao wakawatizame hayo waliyolishwa upande wa mama.” Danny akaongea kibabe.  

“Naomba turudi kwenye pointi jamani.” Yule mwanasheria akaingilia tena.“Kwa hiyo mpaka hiyo tarahe mliyokubaliana, ndiyo Grace ataona watoto?” “Ndio maana yake.” Danny akajibu. “Umesikia Grace?” “Nimesikia.” Grace akajibu huku akifuta machozi. “Unafikiri ni lini utakuwa na uwezo wa kuwarudisha kwa baba yao?” “Inategemea.” Grace akajibu. “Ati nini?” Danny akasimama.  

“Naomba tumsikilize Grace. Kaa chini Danny.” “Asianze kubadilika eti kwa kuwa sasa hivi wote mpo upande wake sababu ya machozi. Hiyo ndio silaha yake. Inategemea na nini?” Danny akapayuka. “Unakaa chini tumalizie kikao, au tuandike kuwa umeshindwa kumaliza kwa amani?” Yule mama akauliza. “Khaa chini Danny. Tumebakisha pafupi sana.” Mwanasheria wake akamsihi, kisha akamgeukia Grace. Geb akampa dada yake maji ya kunywa na tissue yakufutia machozi. Grace akanywa yale maji huku akijifuta machozi mpaka akatulia.   

“Eti Grace, inategemeana na nini?” Grace akasafisha koo kidogo, kisha akaongea. “Hawa watoto sijawaona. Mpaka wanakuja kwangu nitakuwa sijawaona zaidi ya miezi miwili. Sijui watakuwa na hali gani. Sijui watahitaji nini! Nilazima na mimi kuweka mazingira yakuwaweka sawa, ndipo nitakuwa na uwezo wakujua nawakutanisha na baba yao lini. Siwezi kufanya watoto wangu wamange mange barabarani kama adhabu. Jamani hawa watoto hawana kosa. Kama ni kosa ni langu mimi lakuendelea kufuga uozo kwa muda mrefu.” “Uozo!?” Danny akauliza lakini Grace akampuuza na kuendelea.

“Siwezi kuadhibu wanangu kwa kuwazungusha hovyo. Lazima kujua maendeleao yao, ndipo nitakupigia simu wewe, wewe utamjulisha Danny utaratibu kamili. Lakini inategemea kama nilivyosema. Kama nikiwakuta na hali mbaya, hakika itamchukua muda mrefu sana Danny kuja kukutana na hao watoto. Nitafika popote kukushitaki Danny. Sitaogopa.” Grace akabadilika. 

“Kwani nani amesema unaogopa? Si pesa ipo?” Danny akauliza kwa kashfa. “Sasa utaona vile pesa inavyofanya kazi na utajuta kuzaliwa masikini.” Yule mama akaanza kucheka. “Simba kajeruhiwa.” Yule mama akapiga meza huku akicheka.

“Hunitishi Grace.” “Hakika utatishika Danny. Omba Mungu urudishe watoto wangu wakiwa wazima. Wakija hata na michubuko, ujue ndio mwisho wako na wanangu.” “Hapo ndipo utanijua.” “Hapana Danny. Hapo ndipo utanijua mimi ni nani. Nilivumilia umaskini wako, matusi, ukorofi, dharau zako, na kuniendesha vile utakavyo wewe, lakini sio watoto wangu.” Grace aliongea taratibu ila kwa ukali.  

“Hakikisha   unarudisha watoto wangu salama. Nimemaliza kuzungumza na wewe.” “Unani..” “Nimekwambia nimemalizana na wewe Danny. Sina muda wakupoteza kupigishana kelele na wewe. Unalilia nyumba, nimekupa wewe na mwanamke wako. Mkae bure maskini nyinyi wa nafsi na akili. Unachotaka kingine tena ni..”

“Sijalilia nyumba. Nyumba ni…” “Nyumba nini Danny? Nyumba nini? Tafadhali acha kelele, na ukue hata mara moja maishani mwako. Huna adabu kwa yeyote yule wala huna shukurani. Kelele tu na matusi. Unalalamika kulogwa! Unalogwa kwa lipi maksini wewe!?” Grace akapatwa jazba.  

“Akuloge nani Danny wewe hata kuvaa mimi ndio nimekufundisha? Unalogwa ili usaidiwe?” “Ili mnitumie.” “Umetumiwa na nani wakati wewe ndio ulikuwa ukilishwa na kulazwa bure?” “Si huku mnanufaika na mimi?” “Basi tutakuona sasa hivi kama utafanikiwa halafu sisi tutakuwa maskini. Na nyumba nimekuachia ukae wewe na mkeo, bureee. Wewe uliyelogwa. Acha ujinga wakudanganya watoto wangu.” “Kwani ni uongo kama mliniibia nyota yangu? Mliniibia nyota yangu ili muitumie kujipatia mali.”

“Wewe ni mshezi usie na shukurani tu Danny. Kwa nini hujiulizi kwa nini hiyo nyota yako isikusaidie wewe mwenyewe ije isaidie wengine? Nimekuokota ukiwa unanuka mikojo na chupi moja tena imechanika, leo unajidai tumenufaika na wewe!” Danny akasimama kwa hasira na Geb akasimama kama mshale. “Usithubutu hata kumgusa Danny.” “Utanifanya nini Geb? Utanifanya nini?” “Utakapomgusa Grace, ndipo utanijua kwa hakika mimi ni nani. Na sikutanii.” Geb aliongea kijasiri.   

“Mungu akusaidie usimguse Grace. Nakuapia Danny. Utaona maisha yako machungu kuliko sasa.” “Maisha yangu mimi sio machungu. Nyinyi ndio mliyafanya maisha yangu machungu.” “Mnafiki mkubwa wewe. Ulikuwa unapewa mpaka nauli ya kupanda daladala, halafu unasema umelogwa! Ulikuwa ukilishwa na kulazwa bure! Unajitakasa kwa watu kwa kutupaka sisi matope! Wewe ni mshezi tu Danny. Sasa subiri wewe na Sara mrudishe watoto wangu na tatizo, utajua nguvu ya pesa na uchungu wa kusukuma watoto leba. Kuzaa bila ganzi. Hakika hutakaa ukasahau jina la Magesa mpaka kifo chako.” Grace akachukua pochi yake. Wote watatu walikuwa wamesimama.  

“Twende mama.”  Grace akaongea huku anavuta kiti. “Na swala la watoto?” “Nisikilize Danny. Utasikia kutoka kwa lawyer wangu. Sizungumzi na watoto wadogo mimi. Halafu kuna kitu kinaitwa muda, masikini huwa hamkitambui ndio maana mmeacha kazi zenu wote mmejazana hapa kuja kutushangaa kina Magesa. Unanyamazishwa tokea mwanzo wa kikao mpaka mwisho hunyamazi, umejawa jazba kama nini!” “U..” “Shashi Danny. ‘Shashi please!’. Tushakusikiliza vya kutosha. Tangia nakufahamu mpaka muda mfupi uliopita nilikuwa nasikiliza ujinga wako. Mwanaume huna hoja, ni kelele tu. Huchoki!?” Grace akazungumza naye kwa dharau akionyesha amechoka.  

“Jamani asanteni kwa muda wenu. Na samahanini sana. Lawyer wangu atawatafuta.” Akimjulisha yule mwanasheria wa Danny. “Siwezi kuendelea kupoteza muda wangu hapa. Nishapoteza mambo yangu mengi sana kwa ajili yake huyu. Siwezi kuendelea kubishana naye. Inatosha.  Twende mama yangu.” Grace akatangulia kutoka, mama yake akafuata, akaja Geb.   

Wachuma Janga.

Alipofika mlangoni, akahakikisha mama yake na Grace wametoka, Geb akarudi. “Naomba uwaambie wenzako na wake zao, siku nilipowakuta dukani kwa mama yangu wakifanya fujo, iwe mwanzo na mwisho. Isikae ikarudia tena, Danny. Waambie wote nimewaonya.” Geb akajiweka sawa. “Nimewafungulia mashitaka polisi. Masharti yote mliyo andikiwa yapo hapa kwenye hili faili. Waambie ndugu, jamaa na wake zenu wote, chochote kibaya kitakachompata mama yangu, Grace, Nanaa na watoto wangu, wapo matatizoni. Majina ya wote waliomfanyia fujo mama, nimewapa polisi. Wapo kwa kesi ya kumtishia mama yangu kifo.” Geb akaendelea.

“Wewe si mume wa Grace tena, hukaribishwi tena nyumbani kwetu. Vivyo hivyo na marafiki zako na wake zenu pia. Tumeagana hapa kwa amani. Waambie wahakikishe wanakaa mbali na sisi kabisa.” Geb alikuwa amesimama katikati ya mlango. Waliokaa nje wanasikia, na wandani wanasikia. Kimya kikatanda. Geb asiyemzungumzaji akiongea, nilazima usikilize. Utisho wa pesa yake ulimuwakilisha vizuri sana. Kwanza ni kama alikuwa akiwadai wote waliokuwepo pale.  Ilikuwa lazima kumsikiliza.

“Hakuna anayenidai. Na waambie ninaowadai wote ifikapo mwishoni mwa mwezi ujao, pesa yangu yote, bila kukosekana hata shilingi, iwe imefika benki, ukiwepo na wewe pia Danny. Majina yenu na kiwango cha pesa ninachowadai nimeorodhesha kwenye faili nitakalomkabidhi mwanasheria wako. Ipo akaunti ambayo nitataka hiyo pesa iwekwe. Nimewaandikia namba ya hiyo akaunti na jina lake. Ukishalipa, mtafute tena huyu mwanasheria ili kumkabidhi hiyo slip itakayokuwa imegongwa muhuri wa kupokelewa hiyo pesa benki. Huyu mwanasheria atamkabidhi mwanasheria wetu. Mtu asinitafute tena, kwa sababu yeyote ile. Narudia tena, maelekezo yote ya malipo na kiasi ninachowadai kipo humo kwenye faili nitakalomkabidhi mwanasheria wako Danny. Kama umesahau ni kiasi gani ulinikopa, taja jina lako kwa huyu mwanasheria kisha atawatajia kiwango unachodaiwa. Waambieni na wake zenu hivyo hivyo, walipe pesa yote bila kupungua hata shilingi moja.” Geb akaendelea. 

“Yapo madhara yakutokulipa hiyo pesa yote kwa muda niliopanga mimi. Yameorodheshwa hapohapo kwenye hilo faili. Nashauri wote msindoke kabla hamjazungumza na huyu mwanasheria. Ipo tarehe uliyokopa na tarehe utakayotakiwa kulipa, endapo kama yupo hata mmoja wenu atakayekuwa amesahau ni lini alikopa basi jiridhishe kwa huyu Muheshimiwa hapa.” Geb akaendelea.

“Sitataka kupokea simu kutoka kwenu au wake zenu TENA. Nalo hilo lipo kwenye hili faili. Kusogea karibu na familia ya Magesa, kwa nia yeyote ile na kwa njia yeyote ile, nikukiuka masharti haya. Nitamkabidhi mwanasheria wako hili faili zima. Atawaeleza vizuri, nashauri muelewe ili kuepuka madhara yake.” Geb alitulia kidogo akimtizama Danny.  

“Danny! Huruhusiwi hata kuleta watoto nyumbani kwangu. Kama alivyokwambia Grace, utaratibu wa kukabidhiana watoto, utausikia kutoka kwa lawyer wetu. Narudia. Huruhusiwi au hatutaki kuwaona tena kwenye maeneo yetu. Kuna umbali umewekwa hapo, hakikisha unaelewa. Walinzi wangu wanayo picha yako na rafiki zako wote, tena na wake zenu pia. Watakapowaona tu maeneo ya kwetu, ujue watakukamata.” Kimya.   

Geb akamkabidhi yule mwanasheria faili alilokuwa ameshika muda wote. “Tafadhali sana. Baada yakumsomea Danny mambo yaliyoandikwa hapo, na ukaridhika kuwa ameelewa, hakikisha anaweka saini kukubali kuwa amesoma na kuelewa. Nitamtuma mwanasheria wetu aje kutoa copy ili kusiwe na kugeukana baadaye. Na atawasiliana na wewe juu ya slip za malipo yangu utakazokuwa umekabidhiwa. Endapo hutapokea malipo yeyote yale, tafadhali usisite kuwasiliana naye. Yeye atajua jinsi yakuwasiliana na waajiriwa wa wadaiwa wote walioorodheshwa hapo ndani ili kupata hiyo pesa na malipo ya usumbufu. Naomba nikushukuru sana kwa muda wako na niombe radhi kama kuna tulipoupoteza. Asante sana.” Geb akampa mkono. Yule mama akaanza kucheka upyaa huku anagonga meza kishabiki. Geb akatoka. Kila mtu kimya. Aliwapita wale marafiki zake, kama viti tu.   

~~~~~~~~~~~~~~~~

“Bwana pesa inajeuri mbaya! Imenyamazisha wanaume wote. Eti mtasikia kutoka kwa lawyer wetu!” Yule mama akakusanya vitu vyake.  “Sasa subiri kusikia kutoka kwa lawyer wake. Maana ataanzia kutoka kwangu, kujua nilikuonaje hapa kwenye mazungumzo ya awali. Kama unafaa kuwa na watoto au la. Atafuata huyo mwanasheria wako uliyesema amepewa hongo. Hapo ndipo utakapojua miezi tisa ya kubeba mtoto tumboni, na uchungu wa leba ni upi. Heri umkimbilie myamalize humu ndani. Lasivyo anza kutafuta nyumba ya kupanga.” “Haiwezekani!” Danny akabisha.   

“Hakutanii Danny. Nina uhakika hutaki haya mambo yaende mbali. Kwa nilivyokuona leo wewe! Huna stamina yakusimama kwa jaji hata dakika moja. Una jazba. Na kisheria, kwa kuwa wewe ndio umeomba talaka, ndio utatakiwa utoke pale ndani. Halafu pia, wakati wote sheria inamwangalia mama na mtoto. Mna watoto wadogo sana. Hata hiyo kukaa nao kwa mwezi mzima bila uangalizi wa mama yao, tena anayewalilia watoto! Ni kosa jingine. Ndio maana watu huwa wanapenda kumaliza mambo wao wenyewe.” Mwanasheria akagongelea msumari. 

~~~~~~~~~~~~~~~~

Bubu kasema. Grace amemjia juu Danny. Geb amegeuka rafiki zake. Hataki tena urafiki wakushikana miguu. Anadai pesa zake, hataki tena mahusiano na mtu. Madhara yote yapo kisheria na amemkabidhisha mwanasheria wa Danny. Katika mashabiki wale wa Danny waliojaa dharau na nia yakuwakomoa kina Magesa, nani wakufuata nani wa kupuuza. Kitakachowapata??   

v Jazba ya Danny yaanza kumrudi yeye mwenyewe. Yupo hatarini kukosa nyumba na watoto. Je, ataweza kujishusha na kuzungumza na Grace aliyemwambia hataki kumsikia tena? Hatima ya watoto wao itakuaje?

v Marafiki waliokuwa wakimcheka Grace, wamenyamazishwa baada ya dume Man kutoa mabusu ya nguvu mbele zao. Hakuna aliyewahi kumuona Man. Mgeni kwao. Man naye  hana kiasi kwenye kubusu. Kabusu tena na tena bila haraka huku akimsisitiza Grace, yupo nje anasubiri. Kama aliyekuwa akimuomba Grace asije badili mawazo.   

Yapi yatajiri?   

   Usikose Muendelezo.

 


CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment