“Sawa sawa. Basi ujue bibi ndiye alimfundisha. Bibi
akimpenda mtu, anamfundisha huyo mtu mpaka awe mzuri. Si unamuona aunt Grace
alivyo aunt mzuri?” Liv akacheka. “Kwa kuwa bibi alimchapa mpaka akawa aunt
mzuri. Bibi alikuchapa kwa sababu anakupenda. Anataka kukufundisha uwe mtoto
mzuri kama aunt Grace. Si unapenda kuwa kama aunt?” “Nampenda aunt.” “Basi
ukiwa karibu na bibi, atakufundisha uwe kama aunt. Lakini uwe unafanya kila
anachokwambia ili asikuchape. Kwa kuwa ukiwa humsikilizi, bibi lazima
atakuchapa tu. Na atamchapa na dad na mimi, kwa kuwa hatukufundishi vizuri.
Wewe unataka bibi amchape dad wako na mama yako?” Liv akatingisha kichwa
kukataa.
“Basi.
Akikwambia kitu tena, uwe unamsikiliza na kufanya kwa haraka ili aendelee
kukufundisha bila kukuchapa kwa kuwa hatakubali uwe mtoto mbaya. Usipofanya kwa
haraka anachokuwa akikwambia ujue unakuwa mtoto mbaya na atakuchapa tu. Tena
huwa wakati mwingine anatumia fimbo kabisa kukuchapia ili uwe mtoto mzuri
anayekupenda sana. Si unajua bibi anakupenda sana?” Liv akakubali. “Alikuwa
anakuogesha. Anakununulia nguo nzuri. Unaona hereni nilizokuvalisha leo?” Liv
akakubali. “Bibi alikununulia sababu anakupenda sanaaa.” Liv akakubali.
“Kwa
hiyo ukimuona unamkumbatia na kumbusu.” Liv akakubali. “Utamwambia nini?”
“Nakupenda bibi.” “Eheee! Atafurahi sana, halafu atakuwa anaendelea kukupenda
na wewe.” Geb akavuta pumzi kwa nguvu. Liv akaonekana kuelewa akaongoza njia
kuingia ndani, mama yake akamfuata nyuma.
“Bonyeza
kengele mlangoni, sisi tunakuja, Liv.” Geb akamvuta Nanaa nje. “Nakushukuru
Nanaa. Lakini nilishazungumza na mama juu ya hilo, akaomba msamaha.” “We Geb!
Mama anaomba msamaha wakumchapa Liv!?” Nanaa akashituka sana. “Mimi namfahamu
mama yako. Anawapenda sana hawa watoto. Hakuna jinsi eti kuwa alimchapa kwa
kuwa anamchukia. Ni vile mwanao anatabia na kichwa kama chako.” Geb akacheka.
“Nanaa umenitukana.” “Kweli tena. KaLiv kanachapika. Kana msimamo kweli. Mtu
mwenye mambo yake mengi ni ngumu kukavumilia. Na wakati mwingine inabidi
kukasaidia.” “Anaakili sana.” Baba yake akasifia. “Ni kweli anaakili. Lakini
bila kujenga tabia njema, hatakuwa dada mzuri.” Geb akamtizama. “Kweli
mwenzangu umekua! Naona umekuwa na akili za kimama kweli!” Nanaa akacheka.
“Twende
ndani basi. Au wewe utangulie kwanza halafu uje uniite.” “Acha hizo Nanaa.
Twende.” Wakaingia. Liv alishakuwa amepakatwa na bibi yake. “Na mimi nakupenda
bibi.” Walimsikia Liv akimwambia bibi yake kwa upendo wakati wanaingi. Mama G
alikuwa akilia. Nanaa akamuhurumia sana. Alikuwa amenyongea. Wazi alionekana
mpweke. Akashindwa hata chakuongea naye. “Mwenzenu njaa inauma, naomba
nijikaribishe jikoni.” Nanaa akapitiliza jikoni bila hata salamu kwa mama G,
aliyekuwa akilia.
“Usilie
mama bwana! Kila kitu kitakuwa sawa. Watoto wamekuja kukuona. Pata muda nao.
Sio na wewe unalia tena.” Mama G akafuta machozi nakubaki kimya. Akamweka
Magesa chini. “Vipi, umekula?” Nanaa
akamsikia Geb akizungumza na mama yake. “Midomo imekukauka! Nikuletee maji?”
Kimya. “Juisi?” Geb aliendelea kumuuliza mama yake. “Acha kulia mama bwana!
Njoo hapa.” Nanaa hakujua kinachoendelea hapo sebuleni. Lakini alijikuta
machozi na yeye yakimtoka huko jikoni.
~~~~~~~~~~~~~~~
Ni
nyumba ile ile iliyokuwa imejaa furaha, amani na vicheko vya kila wakati.
Walikuwa wamejaa humo ndani, mpaka wengine walikuwa hawajui wanaishije mle
ndani. Mpaka Liz naye alikuwa akija kulala pale, lakini gafla mama G akabakia
peke yake. Bila hata mtoto, wote wakimkimbia kama mchawi. Alilia huyo mama kama
aliyefiwa. Mwili ule aliokuwa amejipunguza kwa ajili ya ugonjwa wa magoti,
uliisha wote. Na kwa kuwa alikuwa sio mrefu sana, alibaki kama kitoto.
~~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa
alibandika chai huku anapika kile alichokikuta kwenye friji. Chai ilipoiva,
akaenda kuvuta stuli pale pembeni ya mama G, akamuwekea ile chai ya rangi yenye
sukari nyingi kidogo. Ni kweli alionekana hakuwa akila. “Liv, mchukue Magesa
mkacheze mbali na hapa. Nimemuwekea bibi chai ya moto sana, sitaki mtoto
aungue.” “Twende.” Liv akaanza kumuita kaka yake. “Kunywa hiyo chai mama.
Itakusaidia. Unaonekana umekaukiwa.” Geb akamsogezea karibu. Nanaa akarudi
kupika jikoni.
Baada
ya muda Geb akaingia na kile kikombe.
“Nakushukuru Nanaa. Naona ameinywa yote.” “Chakula kitakuwa tayari muda
si mrefu.” Geb akabaki amesimama pale. “Vipi?” Nanaa akamuuliza. “Hamna kitu.
Nimesimama tu ili tuwe wote hapa.” “Nenda kakae na mama. Mimi nitakuja muda sio
mrefu.” “Una uhakika?” “Nipo sawa Geb. Nenda tu. Nitakuja sasa hivi.” Geb
akatoka.
Nanaa
akaendelea kupika kama kawaida yake. Haraka haraka huku akimsikia Geb ambaye si
mzungumzaji akijaribu kuongea na mama yake. Mwishowe wakanyamaza kimya. Akajua
Geb ameshaishiwa maneno. Ni tv pekee ndiyo iliyokuwa ikizungumza. Akaona Magesa
anaingia huku anatambaa. Akacheka. “Liv amekufukuza?” Magesa akacheka. “Wewe
unashuguli nyingi kwa wakati mmoja. Mwenzio hawezi mambo mengi kwa wakati
mmoja, anaona unamchanganya. Muone. Njaa inauma?” Nanaa akaendelea kuzungumza
na mwanae. Akamkatia kipande cha nyanya. “Usijichafue sasa. Kaa hapo ule,
halafu nikimaliza kupanga chakula mezani nitakulisha. Sawa baba yangu?” Magesa
alishakipokea kile kipande cha nyanya nakuanza kukishambulia.
“Mbona
anashambulia kwa nguvu hivyo wakati ametoka kula, au hakumaliza?” Geb akaingia
nakumkuta mwanae amekaa chini kabisa amejaa nyanya kila mahali. “Alimaliza
bakuli lote lile. Nikamuongezea na chupa nzima yamaziwa.” Wakacheka. “Ngoja
niandae meza. Mwangalie hapo chini.” “Nikusaidie nini?” Geb akauliza. “Labda
kumlisha huyo. Kwa kula hivyo, ujue njaa tayari.” Geb akambeba na kumtoa pale
chini sakafuni. “Twende ukale.” Geb alikuwa
akizungumza na Magesa.
“Muulize
mama kama umpelekee chakula pale pale alipokaa au atakuja kula mezani.” Nanaa
akamwambia Geb. “Lakini ngoja. Namuona amechoka sana. Mpelekee pale pale.” Geb
akanyamaza. “Basi nitampelekea mwenyewe.” “Afadhali. Maana hapo
nishachanganyikiwa, sijui nipakue nini niache nini na kwa kaisi gani.” Nanaa
akacheka. “Wewe na mwanao Liv, mpo sawa sawa! Mkisikia chakula
mnachanganyikiwa.” Nanaa akatoka.
Alimpakulia
mama G chakula, akaenda kumuwekea. “Liv! Njoo uombee chakula cha bibi ale.”
Tayari ilishakuwa saa 11 jioni wakati Nanaa ameweka chakula mezani. Liv akaanza
kucheka. “Utakula na bibi?” Liv akakataa. “Lazima ule Liv.” “Mwache nitamlisha
baadaye. Huyo hawezi kula sasa hivi. Na hivi alikula mchana na asubuhi, hapo
mpaka saa mbili.” Baba yake akamtetea. “Ngoja mimi na mwanangu Magesa tuendelee
kula. Eti baba?” Magesa akacheka. Liv akaombea chakula cha bibi yake, Nanaa
akarudi mezani walipokuwa Geb na Magesa.
“Njoo
ule mwanangu hata kidogo.” Nanaa akazidi kumbembeleza Liv. Liv akawa anakuja
kula kijiko kimoja, anakwenda kucheza. Alikula mpaka Nanaa akaridhika ameshiba.
“Ana maringo huyo! Mpaka umbembeleze ndio ale!” Liv alishaondoka baada ya mama
yake kumuosha mdomo. Nanaa akaanza kula sasa. Alikula kama mwanae Magesa. “Hapa
nataka nitafute mahali, nilale. Nimeshiba siwezi kuhema.” Geb alimwangalia huku
akicheka. “Si ungekula kidogo, halafu na baadaye ule tena kidogo?” “Na baadaye
pia nitakula.” Geb akatingisha kichwa.
“Ngoja
nikajilaze kidogo.” Nanaa akasimama akataka kutoa vyombo. “Acha tu, mimi
nitatoa. Nenda kapumzike.” “Mungu akubariki. Acha nikajilaze, maana hapa
nimelevya na shibe.” Geb alikuwa anacheka. “Wewe nicheke kadiri ya uwezo wako.
Lakini mwenzio nimeshiba.” “Umenisahau Nanaa.” “Sithubutu na siwezi mpenzi
wangu. Cha kwako kipo kwenye poti ile ya chuma, uji nimekuwekea kwenye chupa.
Lakini najua sasa hivi huwezi kula. Kwenye saa kumi na mbili na nusu, ukisikia
njaa, ujue uji wako upo kwenye chupa. Cha usiku pia kipo.” Nanaa akamalizia
huku akiingia chumba alichokuwa akilala hapo zamani kabla hawajahamia nyumba
mpya kuishi kama mume na mke. “Asante.” Geb akamalizia kwa kushukuru wakati
mlango unafungwa.
~~~~~~~~~~~~~~~
Hakuwa
amezungumza chochote na mama G, akaelekea moja kwa moja jikoni. Akahakikisha
kila mtu amekula, ndipo akaenda kulala. Nyumba hiyo hakuwa amelala tokea Liv ni
mchanga. Usiku mmoja kabla haijamlazimu kulala hotelini baada ya muda
aliopangiwa kurudi nyumbani na Geb, kumkuta barabarani, ndio siku hiyo anarudi.
Tena alirudi chumbani kwake, kule alikokaribishwa tokea anaingia nyumba hiyo.
Akalala kama aliyekufa kwa kushiba.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Nanaa!
Nanaa!” Geb akamwamsha. “Bwana umenitoa kwenye ndoto ya chakula.” Geb alicheka
mpaka machozi. “Umeniharibia mtoto wewe! Umeacha chakula mezani, unakuja
kukiota na hapa chumbani!” Nanaa akacheka. “Vipi?” “Watoto wanasinzia. Twende
wakalale?” “Wapi tena?” “Si kule kwenye apartment?” Geb akauliza.
Nanaa
akafikiria kidogo. Akaangalia kulia na kushoto. “Nilishajisahau. Nimelala hata
sijui nilipo. Lakini Geb, hatuwezi kumuacha mama hivi. Siwezi. Naona sitaweza
hata kupata usingizi.” Geb hakuamini. “Ndiye mama tunayemtegemea mimi na wewe.
Wote hatuna baba. Kajifamilia kenyewe kadogo sana! Hatuwezi kutengana tena.
Kama hatajali kuishi na mimi na hii hali yangu, nashauri tubaki naye tu.” Geb
akakaa nakujiegemeza.
Mpaka
akasikia machozi yanamtoka. Nanaa akakaa. “Silazimishii Geb. Kama unaona
nitamkera hapa, basi tuondoke tu. Mimi wala sitajali.” “Hapana Nanaa. Unajua
vile Mungu anavyojibu zaidi ya tuombavyo!?” Nanaa akambusu begani, akawa
ameshamuelewa Geb. “Naona Mungu ananijibu zaidi ya nilivyoomba. Siamini!
Nakushukuru sana Mungu wangu. Na asante mpenzi wangu. Asante sana.
Naamini mama atapata nafasi ya
kukuomba msamaha. Mpe muda. Sasa hivi amechoka sana. Nahisi alikuwa kwenye
mfungo.” “Tafadhali Geb! Sipo hapa kwa kuombwa msamaha na mama. Hata mimi nina
sehemu ya kumuomba msamaha. Naomba
tumuache kabisa atulie.” “Nashukuru Nanaa. Basi ngoja nikalaze watoto,
niende nikafuate mizigo.” “Nishapunguza usingizi, ngoja nikusaidie swala la
watoto.” “Wote wanarembua.” Nanaa akacheka, nakutoka pale. “Wote watalala na
bibi yao au tuwahamishie chumba kingine?” Nanaa akauliza, wakiwa wanasogelea
alipokuwa amekaa mama G na wajukuu zake.
“Eti
mama?” Nanaa akamuuliza mama G. Bibi yao alikuwa amejiinamia tu. Magesa alikuwa
amejilaza kwenye kochi. “Hamuondoki?” Mama G, akauliza kwa upole. “Naona ndio
tumefika. Simuoni muondokaji hapa. Eti Liv?” Liv akamwangalia mama yake
nakurudisha macho kwenye tv. Geb alishawaogesha wote na kuwabadili nguo. Kwa
hiyo wote walikuwa kwenye nguo zakulalia. “Njoo baba yangu. Dad
amekupa maziwa?” “Amekunywa huyo.
Usimpe tena.” Geb akamuwahi. “Na ningempa tena, angekunywa.” Wakacheka.
Nanaa
akakaa, Magesa akatambaa mpaka kwa mama yake, akambusu na kumkumbatia. “Una
usingizi?” Magesa akamwangalia mama yake kwa macho yaliyojaa usingizi. Nanaa
akaendelea kumkuna taratibu mgongoni. Magesa akatulia kabisa akiashiria
kufurahia anachofanyiwa na mama yake. Nanaa alimbusu mara kadhaa huku
akiendelea kumpapasa. “Nakupenda Magesa mwanangu.” Nanaa alisikika kwa sauti ya
chini kama akimbembeleza mwanae. Magesa akajiweka sawa, akapotelea usingizini.
“Mchukue huyu, naona alikuwa anasubiri
nimshike tu alale.” “Anashuguli nyingi huyo! Lazima achoke. Ameshazunguka
nyumba nzima. Kila mahali yeye yupo!” Nanaa akacheka huku anamwangalia.
“Mchukue huyu, nipe Liv wangu. Naona ametulia kama hayupo!” “Usingizi tu. Hapo
anategea kama na yeye utamshika.” Bado mama G, hakuwa ametoa jibu. Walikuwa
wakisubiria jibu ili wajue inakuaje. Kama wanaondoka, au wanakaribishwa
hapo.
“Njoo
mama. Njoo kipenzi changu.” Liv akajivuta. “Mlishaomba na dad?” Liv akatingisha
kichwa kukubali. “Ulimuombea mama?” Nanaa akaendelea kumuhoji taratibu.
“Nimemuombea mama na Magesa.” “Asante mwanangu.” Akambusu na kuendelea
kumpapasa. “Nampenda mama.” Liv akasikika akiongea na yeye kwa sauti iliyojaa
usingizi. “Hata mimi nampenda Liv.” Liv akajisogeza zaidi karibu na mama yake.
Akambusu na kufunga macho hapo hapo.
“Naona
wote walikuwa wamechoka.” Nanaa alinong’ona. Geb akabakia amembeba Magesa,
Nanaa amempakata Liv. Hawajui
chakufanya. Nanaa akamwangalia Geb. Geb akajua ni nini anaulizwa na Nanaa. Lakini
na yeye hakuwa na jibu. Mama G, alikuwa ameinama tu, huku ameshika shavu.
“Mimi
naona tumuache mama akapumzike Geb. Tutarudi wakati mwingine.” Nanaa akavunja
ukimya. “Mimi nipo sawa tu. Nimekuwa nikilala humu ndani peke yangu! Naona hata
usingizi umeniisha.” Mama G akamuwahi Nanaa.
“Nitashukuru kama mtaniachia nilale nao kidogo. Hamu iniishe. Nilikuwa
na hamu nao sana.” Mama G aliongea kinyonge.
“Basi
ngoja tukawalaze. Kesho Geb atawatayarishia chumba chao ili kiwe tayari kwa
wakati wowote watakapotaka kukitumia.” Geb akashukuru Mungu tena moyoni.
“Usisimame naye huyo. Subiri nakuja kumchukua.” Geb akaenda kumlaza Magesa,
kisha akaja kumchukua Liv. “Basi mimi ngoja nikaoge. Kwani utachelewa kurudi?”
Nanaa naye akasimama na kumfuata nyuma. “Nimeshamtuma Jeri aende kuanza
kukusanya vitu kule. Aviweke pamoja. Nikifika kule nikulipia tu, na kurudi.
Sitakawia.” “Basi nakusubiria. Sina nguo za kulalia. Nataka kitenge na..
na..” Nanaa akabaki akifikiria. “Nataka
kila kitu. Itabidi nikusubiri tu au twende wote ili nikakusaidie?” “Hamna
sababu. Nitakuwa na Jeri. Nitarudi baada ya muda mfupi sana.” Walikuwa
wakizungumza kwenye korido. Mama G
akiwasikiliza.
“Asante.”
Geb akanong’ona. Nanaa akatoa tabasamu. “Naenda kujilaza wakati nasubiri taulo
nikaoge.” “Nisubiri ili upate mtu wakuongea naye wakati ukioga.” “Basi
nakusubiri.” Geb akaondoka pale. Nanaa akarudi chumbani.
~~~~~~~~~~~~~~~
Geb akatoka
pale akapita sebuleni ili atoke nje kabisa akafuate mizigo kwenye apartment.
Akamkuta mama yake bado amekaa pale ameinama.“Nenda kalale mama. Usikae tena
hapo. Umeshakula, umeshiba, sasa kajipumzishe.” Nanaa alimsikia Geb akizungumza
na mama yake. “Unataka kitu chochote?” “Hapana.” “Basi nenda kajilaze kidogo.
Nikirudi nitakuja kukuangalia.” “Sawa. Grace amekutafuta?” Nanaa akajiweka
sawa.
“Ilibidi kumtafuta.” “Ulimpata? Yupo salama?” Mama G alisikika ana wasiwasi kidogo. “Kuna kitu kinaendelea kwa Grace.” “Nini tena!?” Geb akafikiria. “Unamkumbuka Grace yule wa zamani? Grace ambaye..” Geb akasita. “Sijui nikwambie nini? Lakini kuna linalo endelea. Sio bure.” “Acha kunitisha bwana!” “Hapana. Sio kwa ubaya. Amechangamka. Anasikika anafuraha. Amenipa ushauri zaidi ya dakika kumi tena akiwa amejawa na tumaini. Grace aliyeondoka hapa siku nane au 9 zilizopita, sie huyu niliyezungumza naye jana.” “Afadhali. Maana yule akiwa kwenye shida au raha utajua tu hata kwenye simu.” “Mmmh! Grace yupo kwenye raha ile anayopenda yeye. Subiri, tutajua tu muda si mrefu. Si unajua hajiwezi akipata jambo lake?” Mama G akacheka kidogo.
“Tutamsikia
hivi karibuni. Amechangamka! ‘She is full of herself’. Kule kukatishwa tamaa,
kutukanwa, kukandamizwa, huwezi kupasikia kwenye sauti yake. Anasikika mwenye
amani. Namwambia rudi tu, mbona kama umeshapumzika? Anacheka, huku anakataa
kurudi. Ila ameniahidi kama Nanaa akikubali nimuoe, atarudi kipindi tupo
honeymoon, ili anisaidie mambo ya ofisini mpaka nitakaporudi, ndipo na yeye
atarudi tena mapumzikoni.” Nanaa akakaa kwa mshituko.
“Afadhali.
Sasa na wewe umefikia wapi?” Geb akanyamaza kwa muda. “Sijui mama. Nikuendelea
kumuomba Mungu.” “Mungu atakusaidia mwanangu.” “Sijui mama. Nahisi kama Danny
ameharibu zaidi. Amemjaza maneno machafu sana Nanaa. Hata kama alitaka
kukubali, kuna kusita kutakapojitokeza tena. Amemtisha na mambo ya ushirikina
na maneno mengi.” “Basi asingekuwa hapa.” Geb akamtizama mama yake. Walikuwa
wakizungumza kwa sauti ya chini, lakini Nanaa akajisogeza mlangoni kusikiliza.
“Namfahamu
Nanaa. Kama maneno ya Danny yangemwingia kwa ubaya, asingekuwepo hapa.” “Eti
mama!?” “Mwenzio ni mwepesi sana wakuingiwa na huruma yule. Namfahamu Nanaa.
Lakini Geb, hakika Mungu amenilipa. Amenilipa bila kunibakiza. Alihakikisha
nalipa ubaya niliomtendea huyu mtoto. Mpaka naogopa! Ni rahisi sana kumtendea
ubaya mtu aliyekutenda mabaya, lakini si kwa mtu mwema. Mungu hakuachi.
Anakupatiliza. Nimegeuka kicheko na dharau mbele za watu wote! Kama vile
nilivyomfukuza huyu mtoto, Mungu naye amehakikisha, amemruhusu shetani
anifukuzishe mbele za macho ya watu wote! Nilimtenga huyu mtoto na wanae, nami
Mungu alihakikisha ananitenga na kila mwanadamu aliyekwisha wahi kuniita mama.”
Geb akanyamaza.
“Wote
walinirudi vibaya sana. Mpaka vijana wangu wa dukani wamenikimbia! Nimeletewa
funguo na mlinzi wa pale dukani. Wote wamemuaga kuwa hawatarudi tena pale. Wote!
Hata Side yule kijana niliyeanza naye ile biashara amenikimbia. Tokea juzi,
hapokei simu zangu kabisa. Ikabidi kumuuliza yule mlinzi tena kujua upande wa
Side ambaye tumekuwa naye karibu. Nimeishia kuumia zaidi. Maneno machafu yote
niliyomtamkia huyu mtoto, Mungu alihakikisha anayarudisha kwangu yakiwa
machungu mno.” Geb alibaki kimya.
“Kama
Nanaa akikataa kuolewa na wewe, ni kwa sababu yangu Geb. Nahisi hajui hata
ataishije tena na mimi. Lakini huyu mtoto anaupendo sana. Hakustahili
tuliyomfanyia. Hasa mimi. Tena kipindi cha shida yake mbaya! Aibu!
Kudhalilishwa! Akilia usiku kucha bila msaada, na bado tuliweza kumuacha
sakafuni! Hakika Mungu amenilipa. Amehakikisha nimepita kule alikopitishwa huyu
mtoto. Mungu amenionyesha kwa vitendo mkono wake juu ya huyu mtoto. Mpaka
nimemuogopa!” Mama G aliongea taratibu.
“Wote
tumepitishwa hapo mama. Wote tuliokuwepo siku ile, nakushindwa kumsaidia Nanaa,
Mungu ametuonjesha alichokipata Nanaa. Hakuna kati yetu aliyebaki kama alivyo.
Nikiangalia ni kama usiku ule, ilimwagwa roho mbaya sana ya uharibifu. Hakuna kati yetu aliyeweza
kusimama katika lile jaribu. Hakuna. Na madhara yake yametoka nje. Ulimwengu
unayaona kwa macho.” Geb akaguna.
“Badala
yakumchukia Danny, gafla nimeingiwa na huruma juu yake. Maneno anayozungumza! Yanafanana
na ukweli kabisa. Ni kama amevalishwa roho ya ajabu. Tofauti na yeye. Au tuseme
imeendana na yeye. Shetani ametumia ukorofi wake, kumuangamiza yeye mwenyewe.
Ameweka uongo kidogo tu. Sasa kwa kuwa amejawa na hasira na kiburi, anateseka
sana. Ni kama anayetafuta wafuasi kwa anachokiamini. Nilienda siku chache
zilizopita kwenda kutizama watoto na kuzungumza naye juu ya hatima yake na
Grace!” “Haiwezekanai Geb!” Mama G akashangaa.
“Grace
ni jukumu langu mama. Watoto wao ndio wataishia kuteseka baadaye. Hata kama
sasa hivi Danny anawafurahisha, wote tunajua ni kwa muda tu ili kuthibitishia
ulimwengu yupo sawa. Lakini mama, Danny anahali mbaya. Nilikuwa nikimtizama
vile anavyotukana, ni kama amechanganyikiwa. Anapigana vita kubwa, kwa watu
watatu tu! Mimi, wewe na Grace. Anahaha kukusanya jeshi kubwa liwe upande
wake.” “Na amefanikiwa.” Mama G akaongeza.
“Halafu
ili iweje? Tuseme amefanikiwa kugeuza watu wote. Halafu itakuaje mama? Hakuna
hata kimoja tulichokipata hapa kutoka kwa mganga. Ni mkono wa Mungu juu yetu.
Atashindana na mkono wa Mungu mpaka lini? Hujamsikia vile alivyokuwa
akimwaminisha Nanaa. Yaani hata mimi kama ningekuwa upande wa pili, ningeamini
tu. Halafu jiulize mwisho wake nini?” Geb alikuwa akizungumza kwa taratibu.
“Nilimkumbusha
Danny kuwa asisahau amezaa na Grace watoto watatu. Hakuna faida yeyote watoto
wake watapata katika huu ugomvi. Na hakuna mwanamke yeyote atapenda wale watoto
kama Grace mwenyewe.” “Akasemaje?” Mama G akauliza. “Wewe unamjua Danny, mama. Alijitahidi
kuwa mtulivu ili ahakikishe ananifikishia ujumbe, lakini pia nilimtisha.
Nilimwambia ni lazima atulie anisikilize, lasivyo zile pesa anazotangaza kuwa
nimepata kwa uchawi, ataona zitakavyoweza kumuingiza matatizoni.” Mama G akacheka. “Geb!” “Hakika niliamua
kumtenda ukorofi sana ili anisikilize.”
“Ungefanyaje?” “Kwanza unajua nina hisa kwenye
kampuni anayofanyia kazi?” “Sijui!” “Basi yeye na James wanajua kama nilinunua
hisa pale. Nyingi tu.” “Hongera.” Geb akacheka. “Najua moja ya masharti wanayotakiwa
kuwa nayo pale kama wafanyakazi, hasa wa ngazi ya juu, ni kuwa waadilifu.
Nikamwambia last
time I checked, yeye sio mwadilifu kwa kuwa
ametenganisha watoto wadogo na mama yao, tena anaishi na mwanamke wake humo
humo ndani ya nyumba wanayoishi familia yake. Akataka kujidai kuwa mkorofi.
Nikamkumbusha kuwa nilimlisha na kumlaza nyumbani kwangu wakati yeye anasoma.
Wakati yeye anapata elimu shuleni, mimi nilikuwa nikitengeneza mtandao hapa
mjini. Tena kwa maombi yakufunga. Nikamwambia kitendo cha kuthubutu kunyanyuka
pale tulipokuwa tumekaa kabla yangu, atakijutia daima. Nikamwambia akae chini
anisikilize, anijibu, ndipo nitakapomruhusu aondoke. La sivyo hatakaa akasahau
jina la Magesa hapa duniani. Nilimwakikishia kutumia kila shilingi niliyonayo kumuweka
magotini.” “Geb!” Mama yake alishangaa.
“Ilikuwa
lazima kumfanyia hivyo ili anisikilize.”
“Namjua Danny. Huwa hawezi kusikiliza mtu.” “Basi siku ile alikaa chini.
Japo alijibu kwa kiburi, lakini nilipata majibu yangu yote.” “Nini?” “Mama!
Ujue Nanaa ananisubiri nirudi?” “Jeri ataleta bwana. Hebu nisimulie kidogo ili
nijue naombea nini.” “Kwa kifupi ile ndoa imeshaisha. Danny ameshaandika
makaratasi ya talaka, anataka Grace aweke saini yake, wajue mwafaka wa ile
nyumba tu. Ila hamtaki tena Grace. Ameapa kwa mbingu na nchi kuwa hamtaki tena
Grace.” “Na watoto?” Mama yake akauliza.
“Amesema watapanga na Grace. Hawezi kuzungumzia hilo na mimi. Tena hapo
ni baada yakumtisha na kumwambia akileta mchezo, nitahakikisha Grace anabaki na
watoto kwa kuwa sheria inamruhusu mtoto kukaa na mama yake mpaka atakapofikisha
miaka 7. Labda kama mama huyo hana uwezo wa kiafya au kiakili. Akasema uchawi
je?” “Danny!” Mama G akasikitika sana.
“Nikamwambia namkaribisha
mahakamani. Tukashindanie hiyo kesi ya uchawi, ndipo atakapojua kama
nina uchawi wa namna gani. Atajua nani atakuwa wa mwisho kusimama pale
mahakamani. Na nikamwambia mpaka mahakama inamalizana na yeye pale mahakamani,
atahamishiwa hospitali ya vichaa. Na nikamwakikishia, nitahakikisha mpaka
daktari anakuja kumruhusu atoke hospitali ya vichaa Mirembe, ni pale Fili
anaoa. Nikamwambia kama haamini, anijaribu aone.” Mama G akasikika
akicheka.
“Kweli
ulimuamulia.” “Ameniudhi sana Danny. Kwanza ukumbuke alivyomsumbua Grace kwenye
maisha yake yote. Kila siku fujo zisizokuwa na maana. Tena akisimama kwa jina
la wivu. Muongo mkubwa. Wala hakuwahi kumpenda Grace. Danny ni mtu anayependa
kutawala mama. Atawale kila kitu. Watu wajue anamiliki kitu cha thamani, ili
kujionyesha yeye ni mkuu. Alipoona tunazidi kufanikiwa zaidi yake na Grace
anaonyesha kumpita kwa kipato japo yeye analipwa kwa dola, ndipo akaanza fujo.
Ubaya ni vile Grace alivyoweza kuwa mvumilivu kwake na bado kumnyenyekea.
Ametafuta sababu ndio amepata. Anajidai Grace hafai. Nilimuuliza kwa hasira wakati
namnyamazisha. Nilimuuliza kama Grace hakuwa akifaa na anakasoro anazozitangaza
leo kwa watu, angekuwa akimfungia chumbani masaa kwa masaa?” “Geb wewe!?”
“Kweli mama. Huko ni kunidhalilisha mimi. Hata Nanaa naye alimwambia hivyo
hivyo. Alimwambia ni kama kumtukana na yeye.” “Kweli kabisa.” Mama G
akaongeza.
“Sasa
nikamwambia nikimsikia anatamka tena mbele yangu kasoro za Grace, ajue
atajuta.” “Sasa umemwambia Grace kama talaka inamsubiri?” “Hapana mama.
Nimemkuta na furaha sana. Sikutaka kumtibua. Nimemuacha apumzike kidogo. Danny
amemtesa tokea hajamuoa. Siwezi kuendelea kuruhusu amtese mpaka sasa.” “Sasa
umemwambiaje Danny?” Mama yake akaendelea kudodosa.
“Tumekubaliana
amwachie zile karatasi mwanasheria. Halafu mwanasheria ndio atawasiliana nao wote
wawili. Nimemwambia asimtafute Grace. Yupo mapumzikoni. Akirudi, atasaini hizo
karatasi.” “Ulimwambia hata Grace naye hamtaki?” “Mjinga sana Danny. Sikutaka
kupoteza naye muda zaidi. Nikaondoka. Ujue hapo nilimkuta yupo na wapambe wake
wananisubiri!” “Nani?” “Gozi na Zinda. Nikawaomba watupishe. Na wamefurahia
sana kuwa eti Nanaa ameniacha. Niliwasikia wakizungumza wakati mimi nazungumza
na Danny kwenye sebule ile yao kubwa, wao wamehamia kwenye ile sebule nyingine
ndogo iliyojaa vitu vya watoto. Najua walikuwa wakitaka nisikie kwa kuwa
hawakutaka kwenda nje, wakahamia pale na kuzungumza kwa sauti tu huku
wanacheka.” “Walikuwa wakisemaje?” Mama G akauliza.
“Eti
walikuwa wanacheka huku wakimsifia Danny kuwa yeye ni mwanaume. Haogopeshwi wala
hafungwi na pesa. Zinda akawa anacheka anasema kuwa pesa yangu yenyewe haina
nguvu kwa kuwa nimeshindwa kummiliki Nanaa. Akasema eti Malii ambaye hana kitu,
amefanikiwa kunishinda kilaini, bila jasho. Gozi akadakia akisisitiza jinsi
pesa ya uchawi isivyo na nguvu. Zinda akasema ndio maana hata shujaa Danny,
mtoto wa kanisani anatutoa jasho!” “Lakini Geb, namlilia Mungu rehema.
Hata wao nawaombea rehema. Namwambia Mungu asiwahesabie hatia. Ni uongo tu wa
ibilisi.” Nanaa aliendelea kusikiliza.
“Hakuna
sehemu ambayo shetani anafurahia kama kukiwa na machafuko kama haya. Ndipo
kwenye kiti chake cha enzi. Lazima sisi tunaojua huu ukweli tusimame.” “Sasa
mbona kama unajua hilo mbona unazidi kunyong’onyea?” “Geb! Hao watu wa nje mimi
hawaniumizi kama nyinyi wanangu. Wewe unanijua mimi. Siogopi mtu hata kidogo.
Nilishapambana kipindi cha Magesa, siogopeshwi na maneno ya hao vijana wenzako
waliokubali kutumiwa na ibilisi sababu ya wivu! Shetani anaangalia nani amtumie
vipi kutokana na kile kilichojaza moyo. Ametumia udhaifu wao wa wivu kwenu,
kuwatesa wenyewe wakidhani wananitesa mimi. Danny mwenyewe najua pia alijawa
wivu juu yenu. Si rahisi Geb. Si rahisi hata kidogo, kuwaona hivyo mlivyo sasahivi
wakati mlikuwa wote pamoja! Mmefanya kila kitu pamoja! Leo wanakuja kukukopa
wewe! Umewazidi sana wenzio. Hata jina walilokupa la Milionea, mimi
nilijua limejawa wivu tu.”
“Hata
mimi nilijua ni kejeli tu.” “Basi. Sasa wakakutafuta kila mahali. Danny naye
akahangaika humu ndani, akakuta tumetulia tuli. Amefanya fujo zake zote, tokea
anatufahamu mpaka anazaa na Grace watoto hao watatu. Ametutafuta sababu,
ameshindwa kutupata. Yeye mwenyewe haelewi tuliwezaje kuishi naye!” “Si
ulimsikia alivyokuwa akisema tena kwa kurudia rudia akikushukuru kwa kumpenda
na kumvumilia, kwa vile alivyo mkorofi kuliko sisi watoto uliotuzaa?” “Eheee!
Sasa ameshindwa kujua ni upendo mkubwa wa namna gani huo. Imebidi afikiri
tunampendea uchawi tu. Hamna jinsi nyingine yakueleza jinsi tulivyo mvumilia.”
“Na aibu huko mbele ya watu. Anajua wazi hata rafiki zake wanajua jinsi
tulivyombeba kabla na baada ya kumuoa Grace. Sasa atajisafisha vipi kuwa yeye
hana fadhila, nikusema sio kwamba tulimsaidia kwa upendo, ni kwakuwa tulikuwa
tukinufaika naye.” Geb akaongeza.
“Umeona
sasa? Kumbe umelifikiria hilo? Ni kujisafisha tu kwa kutupaka sisi matope. Hilo
mimi wala halinisumbui. Huwa ukweli wakati wote utakuja kujitenga na uongo. Iwe
leo au kesho, sijali. Wao watakuja kupata majibu yao. Ndio maana huko mimi
sihangaiki nako. Ila kipigo ambacho sitaweza kusimama, na shetani anajua ni
kuwapoteza wanangu. Grace ambaye ndio rafiki yangu wakaribu sana, mimi ndiye
msiri wake, hazungumzi na mimi tena! Japokuwa najua wewe unashindwa kuniacha,
lakini sio kama zamani Geb. Nilikupokonya mwanamke aliyekupenda kwa dhati. Tena
mlikuwa mmebakisha siku chache sana mfunge ndoa. Katikati ya amani na furaha.
Akiwa ndio ametuongezea Magesa kwa mateso makali. Nikamkatili vibaya sana. Kwa
kosa gani?” Mama G akauliza.
“Ni ubinafsi tu. Ni vile
Mungu alikujalia hekima, umeweza kumrudisha Nanaa. Lakini niangalie uharibifu
wote niliofanya.” “Sasa si tumerudi?” Geb akauliza. “Lakini haitakuwa kama
zamani Geb. Watu wanasamehe, lakini kunauharibifu unafanyika, huwezi
kurekebisha.” “Acha kukata tamaa bwana. Nakuaminia. Ukiamua kujenga wewe,
hushindwi.” “Mmmh! Hata hivyo nimeshukuru kwa kuamua kurudi kuishi na mimi
tena. Siamini Geb. Nasema ni Mungu. Kwa mabaya niliyomtendea huyu mtoto, ni
Mungu tu.”
“Basi
kapumzike. Nishakupa habari njema za Grace. Mpe muda tu, atajirudi. Unamjua
Grace. Haya, Nanaa amekurudishia wajukuu zako wote. Tena amezungumza vizuri
sana na Liv.” “Nilimsikia. Si unajua nilisikia geti likifunguliwa, nikasimama
kuja kukupokea. Nilikuwa pale barazani nikikuangalia ukishuka na familia yako
mnakuja. Sikuamini Geb. Haya, gafla namsikia na Liv naye ananisemea kwa mama
yake! Mimi nilijua Nanaa angekasirika kama wewe na kuamua kuondoka. Lakini
nikashangaa jinsi alivyomuweka sawa. Amekuja hapa kweli akanipa busu na
kuniambia ananipenda sana.” Wote wakacheka. “Na chakula ameniombea!” “Sasa?
Huna haja yakusononeka tena. Mungu anaturudisha kwako. Mimi na Nanaa tupo hapa
na wewe. Nanaa naona hataki tena kuondoka hapa. Sasa unachotaka tena nini?” “Ni kweli Geb.
Natakiwa kushukuru.” Geb akatoka.
Nanaa Na Mama G.
Nanaa
akajirudisha kitandani baada yakusikiliza kila kitu. Baada ya muda akasikia
hodi mlangoni. Akajua ni mama G. Akakaa. “Karibu mama.” Akaingia. “Naomba nikae
hapo kwenye kochi.” “Nilikuwa
nimekukasirikia.” Nanaa akaanza. “Uliniumiza mama. Ukaniadhibu kuliko kosa langu!” Nanaa akaanza kulia. “Geb ameniambia sababu ya kunitenga na watoto wangu. Lakini ungeniambia
mimi mwenyewe kuliko ulivyonifanyia.” Nanaa
hakujua hasira ilipomtoka.
“Ulinitukana na kusema nampendea Geb pesa zake. Lakini sio kweli mama.
Nilimpenda Geb kabla hata sikujua kama anapesa. Hata wewe mwenyewe kuna kipindi
ulikiri simpendei Geb pesa. Lakini ukaja kunigeuka. Halafu ukamtafutia msichana
mwingine! Umeniumiza sana mama. Sana. Lakini nimesamehe. Yote nimesamehe.” Nanaa akaendelea kulia. Ni kama alijawa na jazba
iliyomfanya aongee bila kufikiria.
Mama
G alikuwa kimya akisikiliza shutuma zake pale kwenye kochi. “Nanaa mwanangu,
wala sio wewe peke yako uliyenikasirikia. Hata Mungu wako alinikasirikia na
kuniacha yanipate yale yote niliyotaka yakupate wewe.” Mama G akaongea kwa
upole. “Grace alinipigia simu. Akaniambia neno gumu kweli. Akasema hivi, ‘kaburi ulilomchimbia Nanaa, nimetumbukia mimi’. Wala hakukosea. Nimevunja ndoa ya
mwanangu mimi mwenyewe kwa mikono yangu.” “Hapana mama. Danny ni muongo. Wala
asidanganye. Alitafuta tu sababu. Yaani msiba wangu mimi aufanyie matanga yeye!
Muongo kabisa.” Nanaa akaingilia.
“Lakini
Nanaa, hata nikikataa, Danny anaoa mwanamke niliyemleta mimi! Nimehusika
kumletea mke Danny. Niambie wale watoto watatu watakuja kukua wajue hilo!
Wanakuwa mbali na mama yao au baba yao, kisa bibi alileta mwanamke mwingine!”
“Hiyo watakulaumu mama. Wala si uongo. Kama ambavyo Magesa na Liv ambavyo
wangekulaumu.” Nanaa akazidi kumuumiza.
Mama
G akanyamaza. Nanaa akazidi kumuhurumia. Akajua anazidi kumuumiza. “Ila mimi
nimekusamehe. Kwanza nilikuwa na hamu na wewe!” Mama G akacheka kinyonge.
“Hujabadilika Nanaa!” “Nimekata nywele mwenzio.” Wakacheka tena kidogo.
“Nashukuru umerudi Nanaa. Niliipata habari yangu hapa! Sina hamu.” Nanaa
akacheka sana. “Nani alikukomesha zaidi? Danny?” “Umbea hujaacha wewe
mtoto!” Nanaa akacheka sana.
“Bwana
nisimulie mama. Atakuwa ni Danny tu. Maana amejawa jazba!” “Sara pia
alinikomesha.” Nanaa alicheka sana. “Nanaa kwa kupenda stori! Sasa hapo
unacheka nini?” “Niambie stori za Sara. Maana nimezipata nusu nusu kutoka kwa
Jeri. Maana Jeri alikuwa akiniambia kuwa yeye ndio amegeuka kuwa dereva wake.
Anampeleka kwa mashoga zake na sehemu zote anazozitaka Sara. Sasa akawa ananipa
stori zote. Mazungumzo yake na mashoga zake. Mambo anayozungumza kwenye simu na
wakikutana na hao mashoga zake. Jeri anasema akaujua mji na mitaa yake. Mpaka
maduka ya kienyeji alikuwa akimpeleka kwenda kununua Shabuu!” Wawili hao
wakaanza kusimuliana stori tokea walipoachana. Nanaa alikuwa anacheka
sana.
“Na alikukomesha.”
“Sio kidogo! Alikuwa akinitoa pesa kama ATM! Hana analofanya.” “Sasa subiri
akale dola za Danny.” “Hawana muda mrefu. Mimi namfahamu Sara na Danny. Ni kama
ukutanishe moto na petrol. Vitakuja kulipuka muda si mrefu.” Stori
zikanoga.
Vicheko
vikaendelea humo chumbani. Geb akaingia akashangaa. Nanaa alikuwa akicheka
mpaka machozi. Yeye kajilaza kwenye kitanda, mama yake kwenye kochi. Wanacheka.
Wanabadilishana maneno huku wakicheka sana. Geb akabaki amesimama mlango. Nanaa
akakaa. “Pole.” “Nimekuta Jeri ameshakusanya kila kitu. Kwanza hapakuwa na vitu
vingi. Vipi nyinyi?” “Mimi naenda kulala.” Mama G akasimama. “Usiku mwema.” “Na
wewe mama.” Nanaa akajibu, akatoka.
~~~~~~~~~~~~~~~
“Sasa
unashangaa nini?” Nanaa akauliza huku anacheka. “Kweli umeamua kujenga mama.”
“Nilikuwa na hamu na mama bwana. Ujue mama ndio alikuwa rafiki yangu wakaribu
sana?” “Alikuwa au ni rafiki yako?” “Vyote bwana. Sitaki kuendelea kumpa
shetani nafasi. Ashaharibu vyakutosha. Atoke na atuache kwa amani.” “Now you are talking!” Geb akasifia.
“Sasa mbona uko huku tena sio kile chumba kingine kikubwa?” “Kile ulichokuwa ukilala na Liz? Akuu!” Nanaa akakataa. “Nilibadili kila kitu.” Geb akatetea. “Kumbuka Nanaa. Nilibadili kitanda, mashuka, kila kitu.” “Lakini ndio chumba ulichokuwa ukilala na Liz. Mimi sikitaki. Nitalala hapahapa. Najihisi kama mimi nakula makombo yake! Akuuu! Wewe nenda kalale huko.” “Usinifukuze bwana Nanaa! Nionyeshe hata kama unanihitaji basi!” “Samahani mpenzi wangu. Haya njoo tulale hapa.” “Hayo ndio maneno. Ngoja niingize vitu vyako. Jeri ameacha kila kitu barazani. Sikutaka aingize, aamshe watoto.” Geb akatoka.
Nanaa
akajitahidi kumsaidia kupanga vitu vyao pale ndani. “Ona vilivyotoshea.
Tunatosha kabisa hapa. Halafu kile chumba chako ukapange vitanda vya watoto.”
“Naona tukifanye cha wageni tu. Lakini Liv anahitaji chumba chake. Hawezi
kuendelea kulala na Magesa anayeamka usiku kula. Anamsumbua mwenzie.” Nanaa
akanyamaza. Akajua wazi ile nyumba haina vyumba vyakutosha kuwa wao wapate
chumba chao, Liv chake, Magesa chake, Mama yao na pia wapate cha wageni! Ni
nyumba iliyokuwa na vyumba vinne tu. Kwa maana nyingine warudi kwenye nyumba
kubwa. Nanaa hakuwa tayari.
“Nitaanza
kumlisha chakula kizito usiku, ili alale mpaka asubuhi.” “Atazidi kuwa mzito
Nanaa. Kumbuka tulivyoambiwa tulipompeleka kliniki. Ameshazidi uzito. Ni heri
tuendelee kumlisha vyakula vyepesi usiku, tusimwaribu mwili.” “Mimi sipo tayari
kurudi kwenye ile nyumba nyingine Geb.” “Hamna haraka. Nitamtayarishia Liv kile
chumba walichokuwa wakilala kina Grace. Atakuwa sawa tu. Na Magesa anaweza
kulala na mama au tukamuweka hicho chumba cha wageni.” Nanaa akanyamaza.
Ukweli Wa Yote.
Maisha
ya amani na utulivu yakaanza hapo ndani. Kama kawaida ya Nanaa na mama G,
kuamka asubuhi na kukutana jikoni kucheka. “Sasa hapa ni kupendeza na kwenda
mbele!” Mama G akacheka. “Kweli mama. Yale aliyokusudia shetani kutuangamiza,
yageuke kuwa baraka.” “Sasa mbona humtaki mwanangu?” Nanaa akanyamaza.
“Eti Nanaa? Au ni kwa vile nilivyokwambia
unampendea pesa?” “Ndiyo.” Mama G akaanza kucheka. “Usicheke bwana mama! Mwenzio nalia.” “Sasa na wewe Nanaa, jambo haliishi? Kwa hiyo
unataka kunithibitishia kuwa humpendei pesa kwa kumkataa mziwanda wangu?” “Sasa je? Kila mtu anasema nampendea pesa
wakati mimi wala sijui Geb anakiasi gani cha pesa huko benki. Sijui chochote
juu yake, zaidi ya kumjua Geb mwanaume
niliyempenda basi! Hata mkiniambia leo Geb amefilisika, mimi sitajua na wala
haitanithiri kwa kuwa mimi sijui anamiliki nini. Watu wananionea tu.” Mama G akazidi kucheka.
“Heri nimuache na pesa zake.”
Nanaa akafuta machozi. “Ngoja Sara arudi.” “Bwana mama!” “Si umesema humtaki
wewe? Sasa ngoja Sara akusikie.” “Namtaka bwana.” “Kwa hiyo?” “Mimi nasita
mama. Watu wengi wanamwangalia sana Geb. Kila mtu anataka kujua huyo
atakayeolewa na Geb ni nani. Kuna siku tulienda naye kwenye kikao cha harusi
cha Zena. Yaani mama, mpaka ikabidi tuondoke. Kumbe Yasini ambaye ni mume wa
Zena sasa hivi, anafahamiana na Geb. Ndiye anaye hizinisha malipo ya Geb huko
Geb anapopeleka mazao yake, halafu yule Jeff, kumbe anafanya kazi benki. Sasa
sijui anajua Geb anakiasi gani cha pesa huko benki! Yaani mama, mpaka ikakera.
Wamechanganyikiwa, hamna hata anayeweza kuzungumza tena. Kila mtu
amechanganyikiwa kisa Geb Magesa yupo hapo! Hata marafiki zangu walishindwa
kuniongelesha. Tukaona tuondoke tu.” Nanaa akaendelea.
“Haya
juzi napo nilikuwa na Jeri sehemu, akanitambulisha kwa mtu kuwa mimi ni mama
watoto wake Magesa, nikaona vile yule baba alivyobadilika gafla baada ya ule
utambulisho, nakuanza kunitetemekea. Nitapoteza marafiki halafu watu wanaanza
kunitizama mimi kama doli la Geb! Akuu!” “Wewe olewa mtulie na mwenzio. Umri
unazidi kwenda. Halafu unazidi kumtesa mwanangu. Mnalala naye halafu hapati
kitu!” “Mama wewe! Umejuaje?” Nanaa akashituka sana mpaka akamgeukia mama
G.
“Mimi
mtu mzima Nanaa. Na hiyo kitu ni muhimu si kwako tu, hata kwake. Mnatesana bure
wakati wote mnahitajiana. Olewa mfunge hilo swala.” Nanaa akanyamaza.
“Unanielewa Nanaa?” Kimya. “Kwanza hizo sababu zote ulizonipa hazina hata
uzito. Wewe niambie ukweli kinachokufanya usite tena kuolewa na mwenzio ni nini.
Wakati mmehangaika miaka na miaka!” Kimya. Akamuona Nanaa anaanza kufuta
machozi.
“Ni
nini?” “Naogopa mama.
Naogopa sana. Ujue tangia wakati ule naogopa hata kujishika huko? Sijui hata
kunafananaje tena. Ni aibu hata kwenda kwa daktari. Najua natisha sana huko
chini. Nimeshindwa hata kujisafisha! Lakini siwezi kujisaidia.” Nanaa akaendelea kulia.
“Mimi
naelewa Nanaa. Najua kabisa. Lakini lazima ukubali kupona katika hilo eneo. La
sivyo utafungua milango mingi sana. Mshinde shetani. Shinda hofu. Jua unaolewa
na mwanaume unayempenda na aliyekukubali hivyo ulivyo. Huna chakuficha. Na ujue
kukubali kwako kutulia kwenye ndoa kutawanufaisha sana wanao. Unawapa wanao
maisha ambayo hata pesa haiwezi kuwapa. Umeona jinsi wanao walivyo changamka?
Unataka kufungua mlango wa kuwatesa bure wanao. Funga huo mlango, ijulikane Geb
ni mumeo na baba wa watoto wako. Basi. Hakuna atakayeweza tena kukugusa. Kwa
kuwa utakuwa na mamlaka kama Geb. Sio hivyo upo nusu nusu.” Nanaa akavuta pumzi
kwa nguvu na kuzishusha. Akanyamaza huku akifuta machozi.
~~~~~~~~~~~~~~~
Usiku
wakati anajiandaa kwenda kuoga wakati watoto wake wamelala, Geb akamuita. “Njoo
kwanza kabla hujaenda kuoga.” Nanaa akakunja uso. “Usiogope. Siwezi kufanya
kitu ambacho hutataka Nanaa. Naomba niamini.” Nanaa akasogea pale kitandani.
“Lini unaenda tena kumuona daktari?” “Kesho kutwa.” Nanaa akajibu akiwa na
wasiwasi. “Basi naomba leo nikusafishe.” Nanaa akaanza kulia. Ni kweli hakuwa
amejisafisha zaidi ya miezi sita. Akajua Geb alisikia mazungumzo yake na mama
yake.
“Hapana Geb. Nitamuomba dada Fifi anisafishe. Najua nitakuwa natisha.” “Uliniahidi nini?” Kimya. “Eti Nanaa? Sio wewe
ulisema tunarudi kuaminiana tena? Mbona tunaenda mbele na kurudi nyuma?” “Basi labda nikaoge kwanza, nitakuwa nanuka
san..” “Nanaa! Ni mimi Geb. Njoo hapa.”
Geb alipiga kitanda, akatengeneza mto vizuri. “Njoo ulale hapa.” Nanaa alikuwa
na taulo tu, alikuwa tayari kwenda kuoga. Akajilaza taratibu.
Geb
akaanza kumsafisha kwa kuanza kulainisha msitu aliokutana nao huko chini na
shaving cream. Ni kweli alionekana hakuwa amejisafisha muda mrefu. Geb
aliendelea taratibu bila haraka wala kinyaa. Nanaa alijua hadha anayokutana
nayo huko chini. Lakini akaamua ananyamaze na kutulia tu. “Nakuumiza? Naweza
kuongeza shaving cream.” Geb akauliza. “Hapana. Nipo tu sawa.” Geb akaendelea kumsafisha.
Alipomaliza kutoa nywele zote, akaenda kuchukua kitaulo kidogo na maji ya
vuguvugu bafuni. Akaendelea kumsafisha kila mahali taratibu mpaka
akamaliza.
“Naona
sasa hivi hata tukienda kliniki daktari hatanishangaa.” Geb aliongea huku
akimfuta vizuri. Nanaa akacheka kidogo huku akijifuta machozi. “Sasa hivi,
ruksa kuoga.” “Asante. Nakushukuru.” “Karibu.” Akaelekea bafuni kuoga na
kumuacha Geb akisafisha pale.
Alibadili
mashuka wakati Nanaa akioga, alipomaliza kuoga na yeye Geb akaingia kuoga.
Alitoka na kumkuta Nanaa amejilaza kitandani na yeye akaenda kujilaza karibu
ili abembelezwe kama wanae. “Nilimsikia
mama akisema usuke? Unataka kusuka lini?” “Unapenda nisuke?” Nanaa akauliza.
“Unapendeza zaidi ukisuka.” Nanaa akacheka kidogo. “Kwani ile ofa ya
kunioa bado ipo?” “Ukikubali hata kesho, tunabariki ndoa yetu.” “Kweli?” Nanaa akamchungulia
vizuri usoni kama anayetaka kupata uhakika.
“Sasa tunasubiri nini Nanaa? Mpaka Liv anaongea, Magesa anakaribia kutembea, na mdogo wao anakuja, sisi bado hatujakamilisha hilo jambo! Mwenzio sina kipingamizi.” Nanaa akafikiria kidogo. “Lakini bado mwenzio natamani kuvaa shela.” “Hilo halina tatizo. Unataka nini tena?” “Wewe uwepo.” Geb akacheka. “Hayo umepata. Tena Grace ameniambia ukikubali tu nimwambie arudi kukusaidia kuandaa hiyo harusi.” Nanaa akafurahi sana. “Basi mwambie Grace bibi harusi yupo tayari kwa ndoa. Kesho nampigia msusi wangu simu aje anisuke vidogo vidogo. Nikichoka, atakuja kunimalizia kesho kutwa baada ya kliniki.” Nanaa akakaa.
“Nataka
gauni refuuuuuu!” Gafla Nanaa akaanza kuchangamka. Geb akawa anacheka.
“Nataka..” Akamuona amekwama. “Nini tena?” “Sijawasiliana na kaka James tokea
siku ile!” “Tutamfuata kwake na watoto.” “Kweli!?” “Naona hiyo ndio itakua
heshima. Ngoja kwanza twende kliniki hiyo siku ya jumanne. Tuzungumze na
daktari tujue afya yako. Akisema wewe na mtoto mpo sawa, nafikiria jumamosi
ijayo tufunge ndoa.” Nanaa akaanza kucheka. “Siamini Geb!” “Kwa hiyo
umekubaliana na siku ya jumamosi?” “Ni sawa. Wapi sasa?” Nanaa akauliza. Geb
akafikiria kidogo.
“Nafikiria
harusi ndogo tu. Sitaki watu wengi kwa sababu za kiusalama. Ni familia yetu tu,
James na mchungaji basi.” “Sawa. Lakini nani atatusimamia? Au nimuombe Zena?” “HAPANA!” Geb alikataa kwa nguvu mpaka
Nanaa akashituka.
“Geb!”
“Simtaki Zena. Sitaki aje awe kwenye maisha yetu tena. Sio rafiki mzuri kwako.
Yupo kushindana na wewe tu. Naomba unielewe Nanaa. Simtaki Zena awe kwenye
maisha yako.” “Basi Geb. Naona safari hii badala ya kumblock tu, nitamtumia
ujumbe wa kumwambia rasmi nasitisha mawasiliano naye. Asinitafute tena.
Nitakuwa muwazi kwake. Hata hivyo wote tumeona madhara ya marafiki waliojaa
hila mioyoni mwao huku wakituchekea. Inatosha.” “Kabisa. Na kama utafanya hivyo
itakuwa vizuri. Umemvumilia vyakutosha. Nataka tuanze upya na watu
watakao tupenda na kutukubali kwa vile Mungu alivyotubariki. Sio kuonea aibu
baraka zetu! Hapana Nanaa. Hata mimi nimevumilia vyakutosha. Mtu hawezi
kuniona ninapesa na kunifurahia, inamaana huyo sio mtu wa hatima yangu.
Akae pembeni. Sitajifanya mjinga tena. Sina sababu. Utajiri sio adhabu hata
kidogo! Lazima wajue na wakae pembeni. Zena ni mmoja wa marafiki tutakao watoa
kwenye maisha yetu.” “Nimeelewa Geb. Nitazungumza naye. Nakuahidi hutamsikia
tena.” “Asante.” Nanaa akamuona ameridhika.
“Nitamuomba
Grace anisimamie.” Geb akamgeukia vizuri kama haamini. “Wewe hujui jinsi Grace
anavyonifaa. Huwa anazungumza na mimi vizuri sana tena bila kunificha. Akiwa
msimamizi wangu ndio itakuwa vizuri zaidi.” “Na kashfa zote hizo ulizopewa,
bado unamtaka Grace!?” “Danny mwendawazimu yule. Achana naye.” Nanaa akapuuza.
“Samahani kusema hivi Geb. Lakini nahisi Danny alikuwa ni kama akitafuta tu
sababu. Ameishi na sisi wote muda wote, hapajawahi
hata kuonekana dawa ya kienyeji, ya miti shamba humu ndani. Kwanza hata shetani
mwenyewe huwa hatajwi sana hapa kwenu.” Geb akacheka.
“Kweli
Geb. Wewe msikilize mama yako kwa makini. Utagundua jina la shetani kulitaja ni
mara chache sana. Ungekaa na mama yake James ndio ungeelewa ninachozungumzia.
Shetani amepewa nafasi kuliko Yesu. Kila neno ni shetani. Hana jambo
linalotokea kwake ikawa si shetani. Sasa eti leo uishi na wachawi, usijue!
Hakuna mtu aliyelogwa akasema nimelogwa. Muongo tu. Na anatumia ukorofi wake
vizuri tu. Ni kama alimpendea Grace pesa. Sasa amefanikiwa ndio anatoa makucha
yake.” Geb akanyamaza kidogo.
“Yeye
si anasema alilogwa ndio maana akawa kama mjinga kumng’ang’ania Grace? Tumeishi
nao wote hapa. Alivyokuwa akimfungia mkewe ndani huko siku nzima, tena kwa kumg’ang’ania
yeye mwenyewe, kama angekuwa na kasoro anazozisambasa sasa hivi, si tungezijua
tokea zamani! Kwanza tendo la ndoa kwao ingekuwa shida. Yaani ingekuwa mara
moja moja kwa sababu kuacha kabisa angesema alishindwa kwa kuwa amelogwa. Au
angesema Grace alikuwa akimlazimishia. Lakini kutwa alikuwa anamfungia Grace
humo ndani. Grace alikuwa hawezi hata kuzungumza na mama humu ndani, sababu ya
kumng’ang’ania kama hatosheki na huyo Grace! Mnafiki tu na muongo. Acha na
Danny.”
“Kazua
uongo na bahati nzuri kakutana na marafiki zenu wanaokuonea wivu au wanaowaonea
wivu. Wanaona mlikuwa wote kwenye shida, sasa hivi mmewapita. Ndio wanatafuta
sababu. Kwanza mimi sijaona hata wakulogwa pale kwenye kundi lenu.” Geb
akacheka. “Kweli tena Geb. Nani alogwe pale. Zinda?” Nanaa akauliza. “Ili mtu
achukue nyota ya ulevi na umalaya kama Malii? Haya, Danny?” Nanaa akauliza
tena.
“Tena
yeye ndio anyamaze kabisa. Wanaume waliologwa na wake zao wanakuwa kama
Danny!?” Nanaa akaendelea. “Mwanaume aliyelogwa wewe ukimuona utamjua tu. Hawi
mkorofi. Mpole na anakubali kila kitu. Danny alikuwa amejaa humu ndani
utafikiri yeye ndio mwenye nyumba! Akianza kukoroma humu ndani mpaka wale
waliokuwa wakija kusafisha nyumba walikuwa wakimuogopa, wakawa wakijua Danny
ndio Magesa! Amejaa kuanzia getini mpaka ndani! Anasema amelogwa! Muongo tu.”
Nanaa akakasirika kabisa.
Kisha
akamgeukia Geb. “Kwanza naomba uniambie ukweli Geb. Maana nasikia tu kwa watu.”
“Unasikia nini?” Geb akauliza. “Kuwa wewe ni milionea.” “Wewe utawaweza watu
Nanaa? Uzushi tu.” “Hapana Geb. Watu wanakuogopa. Namaanisha wanao kufahamu
wewe. Wanaofahamu mali zako, wanakutetemekea. Unakumbuka jinsi Yasini na Jeff
walivyo changanyikiwa baada ya kukuona siku ile tulipoenda kwenye kikao cha
harusi? Kila mtu alikuwa akinong’ona kwamba wewe ndio Magesa! Haya, juzi
nilipokwambia namtaka Jeri aje anipeleke sehemu. Ili nimwendeshe huku
ananiangalia. Kuna sehemu tulienda, akanitambulisha kama mama watoto wako, na
tulikuwa na kina Liv na Magesa. Yule baba akachanganyikiwa mpaka akawa mjinga
na kunikera zaidi. Nikamwambia Jeri tuondoke tu pale.” Geb akawa kama anayefikiria.
“Labda
uniulize swali jingine. Lakini mimi sidhani kama ni milionea. Bado nina ndoto
kubwa sana ambazo bado sijatimiza. Natamani kipindi mimi na wewe tunafikia
uzeeni, pesa itutumikie sisi. Tuwe tumewekeza kiasi kwamba Magesa na ndugu zake
wakikua, wanachagua kitu chakufanya kwenye miradi yetu. Wao na familia zao wawe
na urithi wakutosha. Sasa ukiniita mimi ni milionea wakati tuna miradi tu hapa
Dar. Tena sio Dar yote, sijioni kama mimi ni milionea, Nanaa.” Geb akafikiria
kidogo.
“Bado
naona nina kazi kubwa yakufanya kuliko nilipo. Kuna kipindi, tena sio mbali, nilitaka
kufikiria kuwa nimeshafanya kazi kubwa yakutosha, lakini nikakaa ofisini kwangu
nikajiuliza maswali magumu. Tena niliyaandika chini. Nilijiuliza kutokana na
nchi yetu ilipo, inapokwenda na tulipotoka.” “Ulijiuliza maswali gani?” Nanaa
akataka kujua.
Geb akacheka. “Usicheke bwana!” “Hapana. Nimefurahi umeniuliza. Ila
moja ya swali nililojiuliza ni hili, kwa teknolojia inavyokwenda kwa haraka.
Uchumi unavyobadilika mchana na usiku. Je kwa jinsi nilivyowekeza mimi,
nitakuwa na uwezo wakusimama kwenye soko kwa muda gani? Unakumbuka stori ya
baba yangu na ufugaji aliokuwa anafanya?” “Nakumbuka.” Nanaa akajibu.
“Lakini
aliniambia anguko lake lilifika pale walipokuja kuanzisha kiwanda cha kisasa,
lakini walifanya biashara kama yake. Kwa hiyo wakachukua masoko yake yote,
biashara yake ikaporomoka. Sasa mimi sitaki nifike huko. Pesa yote niliyonayo benki
au popote kule, nimejiambia sio yangu. Lazima kuzidi kuwekeza zaidi na zaidi.
Kujipanua. Kutafuta kitu cha kudumu ambacho hakitaondoka sokoni. Kuwe kuna
ukame au kuna neema.” “Kama chakula?” Nanaa akauliza. “Ewaaa! Sawa sawa. Ndio
maana sitakaa kuacha biashara ya chakula. Tajiri na masikini, mgonjwa na mzima
wote watataka kula. Ndio maana nimewekeza sana kwenye hiyo biashara. Na
ninajitahidi kufikia watu wote. Tukitoka kwenye honeymoon kabla hujajifungua,
nitakutembeza uone nilichofanya, ninachofikiria kufanya ili na wewe unishauri.”
“Sasa mimi nitakushauri nini Geb!” Nanaa akajidharau.
“Usijidharau
hata kidogo. Na usinione hivi mimi. Hata Jeri huwa nakaa chini na kumsikiliza.
Wakati mwingine huwa namchukua kwenye gari yangu tunakwenda naye safari ya mbali
kidogo, ili kujua kinachoendelea mtaani kwa watu wa kiwango cha chini, kawaida
na vijana. Uhitaji wao ni nini. Na mimi naingia wapi hapo? Kwa hiyo akiwa
haendeshi, mimi namwendesha, huwa anakuwa na wasiwasi sana. Na hapo anaongea
sana.” Nanaa akacheka.
“Na
Jeri alivyo mpole!” “Na ananiogopa sana. Kwa hiyo huwa anaongea kupita kiasi
ili tu kujituliza.” “Geb wewe!” “Mjini hapa Nanaa. Lazima kuishi na watu kwa
akili. Kwa hiyo anapata muda wakupanda gari yangu na kuendeshwa na mimi. Wakati
mwingine huwa nampeleka kupata chakula. Huku na mimi napata yanayoendelea kila
mahali mpaka kwa wafanyakazi wengine. Kila mtu anajua nampenda sana Jeri.
Lakini hawajui vile ninavyonufaika naye.” “Na yeye ananufaika.” “Sio kama mimi.
Yeye analisha familia yake tu. Lakini mimi ananisaidia katika maeneo mengi
sana. Si kwenye biashara zangu tu, mpaka nyumbani. Ni mtu ambaye sina wasiwasi
akiwa na pesa yangu au kitu changu cha thamani. Naweza kumtuma anipelekee Liv
wangu popote, na nikawa na uhakika Liv atafikishwa salama. Lakini sithubu
kufanya hivyo kwa mtu yeyote yule. Hata Zinda siwezi kumuachia Liv.” Nanaa
akashangaa sana.
“Kwa
hiyo, fikiria maswali yote unayotaka kuniuliza, tukiwa honeymoon utapata muda
wakunifahamu zaidi.” “Honeymoon itakuwa wapi?” “Hatuwezi kwenda mbali sababu ya
afya yako na watoto. Ukijifungua ndipo tutaweza kusafiri, lakini sasa hivi
naona tutulie tu.” Nanaa alijawa na furaha sana.
“Safari
hii lazima tuoane Geb.” “Nimemuomba sana Mungu hiko kipengele tukikamilishe.
Unajua nilijua ni rahisi sana! Nikajua ni mipango tu. Na nikajua kama mipango
yangu mingine inavyofanikiwa, ndivyo na hilo litakavyofanikiwa kwa haraka.
Lakini daah! Kila tukipanga hiki, kinatokea kitu. Safari hii nimemuomba Mungu
aingilie kati. Naamini atatusaidia.” Nanaa akambusu shavuni. Geb akacheka.
“Eti
umezidiwa sana?” Nanaa akauliza kwa aibu huku akicheka. Geb akaelewa. “Naweza
kusubiri mpaka jumamosi tukifunga ndoa. Usijali.” Nanaa akamwangalia kwa
kumuhurumia. “Pole.” Geb akacheka. “Naomba kesho upokee simu ya Grace.
Nitamwambia akupigie ili mpange zaidi.” “Sawa.” Akambusu.
~~~~~~~~~~~~~~~~
Simu
ya Nanaa ikaingia ujumbe. “Nani tena?” Geb akauliza kama wamesumbuliwa. Nanaa
akasoma. “Msusi. Nilimuomba aje na watu wanne ili nisikae chini muda mrefu,
halafu nikamuuliza kama anaweza kupata aina za nywele ninazotaka. Ndio
amenijibu.” “Anasemaje?” “Amepata watu na nywele atazifuata asubuhi kabla ya
kuja hapa. Ila anasema itanigarimu sana.” “Naomba usuke Nanaa. Tena wakiwa wengi ndio vizuri ili usikae sana
na waondoke kabla sijarudi kutoka kazini. Nisingependa niwakute hapa.” Nanaa
akacheka. “Basi ngoja nimwambie sawa.” Nanaa akajibu.
“Nimemsisitiza
wawahi asubuhi sana. Nimemwambia akiona wamechelewa kuja, basi. Tutapanga
wakati mwingine.” “Lakini Nanaa, nataka kukushukuru?” “Nini tena?” Nanaa
akaweka simu chini na kumgeukia. “Kuweza kuweka pembeni yale yote
tuliyokutendea na kuirudisha hii nyumba kwenye hali hii!” Geb akajiweka sawa.
“Sio jengo.” Nanaa akacheka.
“Namaanisha hivi ilivyojaa amani na utulivu!
Hata mama ameanza kutulia sasa hivi. Nimerudisha mapenzi na Liv wangu. Nakwenda
kazini, najua narudi nyumbani kwa Nanaa na wanangu. Naamshwa na vicheko. Sina
hofu yakutoka chumbani labda nitakutana na sura za matatizo. Kila mtu anacheka!
Nakushukuru sana mpenzi wangu. Najua sio rahisi, lakini umeweza kunipa ‘home’. Sehemu ninayokimbilia kupumzika baada ya
mihangaika na kelele za hili jiji.” “Asante kushukuru Geb.” Nanaa akajisikia
vizuri kutambuliwa juhudi zake. Ni kweli alisamehe kwa ajili ya Geb.
“Na mimi nakushukuru kunirudia Geb. Asante. Umesimama na mimi kipindi
ambacho hakika nilikuwa nakuhitaji. Unakumbuka siku umekuja kuniona pale
hospitalini?” Nanaa akaanza kulia. “Najiona
nilichelewa.” “Hata kidogo Geb. Ulikuja kwa wakati sahihi. Nilikuwa nimekata
tamaa. Kifo pekee ndio nilikuwa natamani. Nilijawa aibu ya mtoto ambaye sio
wako. Nilijichukia na kujionea kinyaa mimi mwenyewe. Kitendo cha kushika huko
chini kwangu, nilikuwa nakichukia nilikuwa najiambia ni kama nashika mauchafu
gani sijui! Nilijichukia mimi mwenyewe hata mtoto mwenyewe. Nikajiambia labda
nimpe jina la Jimmy, pengine nitampenda kama kaka, lakini wapi. Mandoto mabaya
yakutaka kubakwa kila siku usiku ndiyo yalikuwa yakinipandisha presha.”
“Lakini sasa hivi mpaka presha
imerudi kuwa yakawaida. Mzima, mpaka yule daktari wa moyo alikuwa akinishangaa
juzi ijumaa, nilipoenda na mama. Napata muda na Jimmy wangu. Naona hata
nikimwambia kitu ananisikiliza. Akikaa upande nikiumia, namuomba ahame,
anahama. Naomba naye. Tunazungumza wote wanne. Liv pia anambusu. Kaka mkubwa
naye anambusu. Japo kwa kupaka mate.” Wakacheka.
“Nakushukuru
kwa kuja kutuokoa mimi na Jimmy. Asante.” Geb akambusu tumboni. “Na furaha
itaongezeka jumamosi zaidi kwenye fungate yetu. Nina hamu na wewe Nanaa! Mpaka
huwa nikikungalia naumia.” “Pole Geb.” “Tena safari hii hakuna mtoto
anayenyonya! Nitafaidi peke yangu kwa kipindi cha kama mwezi na siku kadhaa.”
Nanaa akacheka sana. “Ninavyokupigia mahesabu! Naona hii week itaenda taratibu
sana.” “Mungu atatusaidia Geb.” Wakalala.
Grace Kwa Nanaa Tena.
Wakati wanamsuka, simu ya Nanaa ikaanza kuita.
“Naomba hiyo simu Liv mwanangu. Atakuwa dad huyo!” “Na mimi mama.” Liv akataka
na yeye aongee na baba yake. “Haya. Ongea wewe kwanza na dad, halafu ukimaliza
ndio unipe na mimi.” Liv alipoangalia simu ya mama yake, akampa mama yake bila
kupokea. “Sio dad!” Picha ya Geb huwa inaonekana wakati akipigiwa na Geb. Hata
Liv alikuwa akijua hilo. Nanaa akaangalia, akaona namba ngeni.
Akapokea.
“Niambie bibi harusi wangu.” “Grace!!”
Nanaa akashituka na kuanza kushangilia. Grace akawa anacheka. “Naolewa mwenzio!” “Nimesikia. Geb amefurahi huyo. Anacheka muda wote.”
“Mbona hapa kaondoka kimya kimya.” “Alikuwa ana play cool tu kwako. Hana lolote! Nimeongea naye zaidi ya lisaa. Mipango mingiii.
Mwishowe nimemwambia aniachie mimi kila kitu.” “Kweli!?” Nanaa alikuwa haamini.
“Hapa nishawapatia sehemu ya
kufunga ndoa yenu, sehemu ya honeymoon
kwa kuwa amekataa msisafiri mbali. Na hataki muwe mbali na watoto. Msimamizi
wake yeye wa harusi, maana amesema wewe umenichagua mimi.” Nanaa
akacheka.
“Asante kama umekubali.” Nanaa akajua
Grace amekubali. “Karibu. Mimi mwenyewe nimefurahi
kuona bado unaniamini. Kwa hiyo kila kitu kipo tayari. Mtakuwa na harusi nzuri
sana. Nikikata tu simu naanza mipango. Jumanne ameniambia mnaenda kumuona
dokta. Akinipigia simu kuniambia kila kitu kipo sawa, nitakuja jumanne hiyo
hiyo na ndege ya usiku. Ili jumatano tukatafute gauni. Alhamisi tunaondoka wote
kasoro Geb.” “Tunaenda wapi tena!?” Nanaa akauliza na wasiwasi.
“Kwa sasa nipo
Arusha. Nipo kwenye hoteli nzuri sana. Naona hapa patawafaa. Nimeshauliza
nafasi. Kama tunaweza kupata sehemu ya kufanyia hiyo ibada fupi na sehemu ya
chakula, wameniambia ipo sehemu. Wanampishi mzuri sana. Kilichobaki ni
wapambaji tu. Nitaenda kuonana nao leoleo. Ili tuzungumze nao. Kwani una aina
fulani ya mapambo unataka?” “Sina hata ninachojua. Wewe nichagulie tu?” Grace akacheka.
“Sawa. Je
rangi? Kuna rangi unataka kwa ajili ya harusi yako?” “Napenda nyekundu. Ila
kama itasumbua basi.” “Wewe! Hiyo ni siku yako. Chochote unachotaka, lazima
tutatafuta mpaka tupate.” Nanaa akacheka kwa furaha. “Keki je? Unapenda keki gani?” Nanaa akaanza kufikiria. “Labda nikuulize hivi, huwa unapenda kula keki ya namna gani?” Grace akaendelea kuhoji taratibu.
“Take your time. Fikiria tu. Mimi naandika kila kitu. Geb ameniambia niweke kila kitu
unachotaka wewe. Hapa nimeandika kila kitu. Nakuuliza moja baada ya kingine.
Ukiona ni swali unalotaka kufikiria, niambie niruke, nikuulize kitu kingine.” Tayari machozi
yalishaanza kumtoka.
“Nilijua
tu. Kwanza naona umechelewa sana kuanza kulia. Basi tena hapo maandalizi hayo
yatamshinda mwenzio.” Kumbe mama G, alikuwa amekaa nyuma ya Nanaa muda wote akisikiliza.
“Bwana mama!” Nanaa
akafuta machozi. “Sasa hapo badala yakuongea haraka, useme unachotaka,
mwenzio akaanze kuwaandalia, unalia tena!” “Nafikiria.” Nanaa akajibu. “Mmmh!” Mama G
akaguna. Wote wakacheka mpaka wasusi.
“Kafurahi
mama. Ndoa ngumu mama yangu!” Mmoja wa wasusi aliongeza. Kwani ilimlazimu Nanaa
kuweka sauti ya juu, speaker, ili aweze kusikia. Alishindwa kuweka masikioni
sababu ya kusukwa. “Basi mwenzio anakusubiri.” Nanaa akacheka. “Napenda keki ya Vanilla. Wanaweza kuchanganya na chocolate kidogo.
Muundo wowote ule.” “Sawa. Nitawaambia watengeneze mchanganyiko. Vanilla na
chocolate.” Grace akajibu wazi akisikika
anaandika.
“Unapenda kuwe
na maua gani mbali na roses?” “Hayo hayo.”
Nanaa akajibu. Grace akacheka. “Unataka yachanganywe
na rangi gani?” “Sijui ila mekundu ndio yawe mengi.” Grace akaandika. “Nimekupata. Kwa hiyo nimwambie achanganye na yeyote, ila mekundu yawe
mengi?” “Ila zisiwe rangi nyingi. Nyekundu labda na pinki au nyingine. Mbili
tu.” Nanaa akaongeza. “Hayo ndio
maneno. Sio kusema yeyote.”“Mama!” “Ndiyo. Maana unaolewa mara moja tu.” Nanaa
akacheka.
“Eti Grace?” Nanaa akaita. “Nipo. Naandika tu hapa. Niambie?” “Nilionaga kwenye movie, watu
wanafungia harusi nje. Nikapenda. Kwani itakuwa gali?” Kila mtu alicheka. Mpaka Grace. “Nanaaaa!” Mama G
alizidi kucheka. “Bwana usinicheke mama!” “Mwanangu unataka harusi ya kizungu?” Bado mama G alikuwa
akicheka sana. “Kwani ni garama? Kama garama
basi.” “Wewe unaolewa na Geb Magesa. Usiogope garama. Amenituma niandike kila
kitu unachotaka bila kujali garama.” “Basi hapo tena ataanza kulia.”
Mama G akapokea. “Bwana mama!” Nanaa akalalamika na kweli alishaanza kulia. Tayari
machozi yalishafika mashavuni.
“Niambie bibi harusi wangu?
Kwahiyo Unataka harusi hiyo ifungwe nje, bustanini au pembeni ya pool?” Grace akauliza. “Pembeni ya pool si wanangu watatumbukia kwenye maji!” Wakacheka sana.
“Kama hapo
ndio unapataka, watatafutwa watu wa kuwaangalia.” “Roho yangu haitatulia bwana.
Magesa wangu anazunguka kila mahali siku hizi. Nitakuwa roho juu juu wala sitaweza
kumsikia mtu.” Nanaa akasisitiza. “Wala usijali. Wana bustani pia nzuri. Wanaweza kuitengeneza na
kupapamba, pakapendeza tu. Naamini utafurahia.” “Asante Grace.” “Karibu. Nini
tena unataka?” Nanaa akabaki kama anayefikiria.
“Naona ni hivyo hivyo. Sina kingine. Ila nakushukuru sana, tena sana.
Asante kwa kutoa muda wako na kutusaidia. Nakushukuru.” “Karibu. Na mimi
nimefurahi kuniamini na kupata kitu chakunifanya niwekeze mawazo yangu yote
huko.” Grace akajibu.
“Nina ombi la
mwisho Nanaa.” Grace akaongeza. “Karibu.” “Jumanne usiku nitakuja hapo na mgeni wangu. Lakini sitalala
hapo nyumbani.” “Mmmh!” Mama G kaguna. “Huyo ni mama ameguna?” Nanaa akacheka.
“Sasa mama unaguna nini? Kwani wewe umeshajua mgeni wa namna gani?”
“Nakujua sana wewe Grace. Ukiongea tu bila hata kuiona hiyo sura yako, nakuwa
najua kila kitu.” “Mwaya Nanaa, naomba ututayarishie chakula. Hasa ndizi.
Nimemsifia kuwa unajua kupika ndizi kuliko Yusuf mpishi wao, hajaamini. Sasa
nataka aje kula ndizi uliyopika wewe.” Nanaa
akacheka.
“Hilo tu,
usijali. Kingine nini unataka?” Nanaa
akauliza. “Huyo haambiwi hivyo. Shauri yako! Utajuta kuuliza.” Mama G
akaingilia. Nanaa akacheka. “Usimsikilize mama. Wala sina mahitaji makubwa. Ila tu naomba tuwakute
watoto. Maana nilimringishia kuwa tuna watoto wazuri sana na watulivu. Sasa
nataka awakute.” “Wewe usichelewe kufika hapa. Watoto wakiwa na usingizi, mimi
nawalaza.” “Mama naye!” “Kinachokushinda kuja mchana ni nini mpaka uje usiku!?”
“Watu wana kazi mama!” “Basi mtaona watoto kesho yake.” “Mama!” “Mama nini?
Wewe shika yako. Achana na wajukuu zangu.” “Sasa chakula?” “Hayo zungumza na
Nanaa. Hapo siingilii.” Mama G alirudi kushika usukani kwa wajukuu zake.
Majukumu ya watoto alisaidia kwa asilimia kubwa sana. Hapo ndipo Nanaa alipoona
upendo wa huyo mama kwa wajukuu zake. Alifanya bila unafiki.
“Nanaa mwaya
tutaongea ukiwa peke yako. Ila nikikumbuka kitu chochote nitakupigia ili
nikuulize. Nataka upate harusi nzuri utakayokumbuka milele.” “Asante Grace.
Kuhusu chakula usiwe na wasiwasi utakuta vitu vizuri vitupu.” “Nakushukuru
mwaya wifi yangu.” Nanaa alizidi kufurahi kutambuliwa.
“Gauni na viatu ni mpaka nije huko kesho. Jumatano tutakwenda wote kutafuta.” “Hamna shida. Uwe na siku njema.” Wakakata simu. Nanaa akaanza kushangilia. “Si ulikuwa unajidai hutaki kuolewa wewe?” Mama G akamuuliza. “Acha kukumbuka mambo ya kale bwana!” Nanaa akaendelea kushangilia. “Gafla!” Mama G akashangaa, kwa kumchokoza Nanaa. “Mama naye! Mambo hayaishi moyoni!?” Nanaa aliendelea kufurahia. “Kwanza humu ndani fujo zitaanza.” Mama G alikuwa akicheka sana. “Fujo gani tena?” “Nawaza vile kina mama Magesa tutakavyokuwa wengi humu ndani!” Mama G alicheka mpaka machozi. “Ila itabidi uniachie kwa muda mpaka nizoee bwana!” Mama G alizidi kucheka.
“Nanaa
unaakili za kitoto wewe!” “Nakaribia kuwa mke wa mtu mama. Naomba uongeze
heshima bwana!” Wale wasusi walikuwa wanacheka huku wakimsubiria Nanaa akae
waendelee kumsuka. “Liv!” Nanaa akamwita mwanae aliyekuwa akicheka vile mama
yake anavyocheka na kufurahia. “Nampenda mama.” Liv aliongea huku akicheka.
“Hata dad anampenda mama.” Nanaa akajibu na kufanya wazidi kucheka.
“Yaani
Geb angekuona leo hapa, asingeamini.” “Wewe acha kabisa mama. Kuzalishwa watoto
wawili na bado niolewe! Si mchezo.” “Ndio ukae, umalizwe kusukwa kabla hajarudi
humu ndani.” Nanaa akakumbuka akarudi kukaa.
Jumanne.
Siku
ya jumanne ambayo Nanaa alitakiwa kwenda kumuona daktari wa watoto, Geb
hakwenda kazini. Kulikuwa na umuhimu wa yeye kuwepo ili aulize maswali yote
kujiridhisha. Ndiye mtu ambaye angeweza kuidhinisha kama Nanaa anaweza kusafiri
au la. Kutoa tathimini kamili ya afya ya mtoto na Nanaa. Mama G alibaki na
watoto nyumbani, Geb akatoka na Nanaa.
Walikaa
kwenye foleni wakisubiria zamu yao ifike wamuone daktari wa wanawake. Nanaa
alikuwa ameshafanyiwa vipimo vya awali. Uzito ulikuwa mzuri, mkojo msafi.
Wakampongeza kwa kunywa maji mengi. Pressure ndiyo ilikuwa juu kidogo. “Sidhani
kama atasema ni sawa kusafiri. Mimi namjua huyu dokta. Muoga kuliko mimi
mwenyewe.” Nanaa alianza kutoa tahadhari. “Huwa anakwambia ukweli, Nanaa. Kwa
faida yako na mtoto.” “Basi tujiandae kuambiwa tusubiri mpaka nijifungue. Mimi
namfahamu dokta Lyamu. Nimeanza nae tokea Liv mpaka leo kwa Jimmy. Kila kitu
yeye ni tahadhari! Ukimsikiliza yeye hatutakaa kufunga ndoa.” Geb
akanyamaza.
Akamuona
amekosa raha. Akamvuta mkono. “Jumamosi ni lazima
tutabariki ndoa yetu. Usiwe na wasiwasi. Iwe hapa au Arusha, lakini lazima
tutakamilisha. Usiogope.” Nanaa akavuta pumzi na kujiegemeza pembeni. “Unawaza
nini sasa?” “Hii Presha! Kwa nini ipo juu wakati nimekuwa na wakati mzuri?
Hamna hata jambo baya nililowaza!” “Kumbuka sasa hivi kuna tatizo la moyo pia,
Nanaa. Daktari ametuambia hiyo yenyewe inaleta pressure. Bado mtoto mwenyewe
anazidi kukua. Yote hayo yanaongeza pressure.” Nanaa akafikiria.
“Nimechoka
Geb. Nafikiri huyu mtoto awe wa mwisho. Nifunge kabisa kizazi. Wanatosha. Au
wewe unataka zaidi?” “Hata kama ningekuwa nataka zaidi isingekuwa kwa mateso
kayo unayopitia. Nashukuru kwa kuwa wewe mwenyewe umeona hivyo. Watoto watatu
wanatutosha kabisa.” Nanaa akalifurahia hilo.
“Nakushukuru
Geb. Asante kwa kuwa na mimi kila ninapokuwa mgonjwa.” Geb akacheka kidogo.
“Karibu.” Geb akajibu huku akionekana amekumbuka kitu. “Unacheka nini?” “Grace
huwa ananiambia kuwa kwa sababu siwezi kulala bila wewe pale kitandani, ndio
maana huwa inanilazimu kuja kulala na wewe hospitalini. Kwa maana nyingine
ananisema kuwa nakuwa hospitalini na wewe kwa sababu yangu sio yako.” Nanaa
akacheka.
“Anakuchokoza
tu. Tena leo usiku anakuja na mgeni wake. Unajua?” “Ameniambia kuwa umemkubalia
kuwatayarishia chakula cha usiku.” “Atakuwa amepata mchumba?” “Sijui Nanaa.
Tumsubiri tuone. Ila kwa furaha aliyonayo Grace, lazima awe amepata faraja. Aliondoka
akiwa ameumizwa sana.” “Utafanyaje?” Nanaa akazidi kumuuliza.
“Nimezungumza
naye swala la talaka. Ameomba kesho nimsindikize kwa mwanasheria. Ameomba
niwepo wakati wanakamilisha mambo yao.” “Kwani Danny atakuwepo?” “Lazima awepo.
Wana watoto na ile nyumba yao. Grace inamuuma sana ile nyumba. Anasema
amewekeza pesa nyingi sana na muda wake mwenyewe. Hawezi kumuachia Sara aishi
pale bure. Anataka kumlipa Danny pesa aliyowekeza pale. Amwachie nyumba.”
“Danny akikataa?” Nanaa akauliza.
“Basi
waandikishane kwamba ni nyumba yao wote wawili. Ikitokea wanakufa, wapewe
watoto wao.” Nanaa akafikiria. “Sasa kwa sasa hivi wataifanyaje?” Nanaa
akaendelea kuhoji. “Grace amesema inategemea watakavyoamua kwenye swala la
watoto. Atakayekuwa na watoto kwa muda mrefu, ndiye atakayeishi pale. Lakini
anahisi hata iweje, Danny hawezi kuishi bila wale watoto. Ndio ndugu zake wa
pekee.” “Kwa hiyo Danny ndiye ataishi pale?” “Itabidi.” Geb akajibu.“Na Grace?”
Nanaa akahoji. “Grace hawezi kukosa pakuishi. Hilo haliwezi kuwa tatizo hata
kidogo. Ninachomfikiria ni watoto wake tu.” Nanaa akanyamaza akiwaza.
“Wakati
wote kwenye kutengana, ni rahisi sana kwa wazazi. Kama sasa hivi Danny anaye
Sara, ambaye anamfariji kwa namna yake. Grace naye hivyo hivyo. Watoto je? Wao
ndio wanabakishwa bila faraja ila mateso na kumbukumbu mbaya. Maneno
mabaya wanayojazwa na upande wa mama au baba. Ugomvi ulikuwa ukitokea
mbele yao wakiona. Baba na mama wanapata faraja, lakini sio wao. Mara nyingi
huwa tunasahau sana upande wao. Hatukumbuki madhara tunayokuwa tunayasababisha
kwao. Tunaendelea na maisha yetu, kana kwamba hakuna kitu kimetokea kwao.” Geb
aliongea kwa kina huku akifikiria.
“Nawafikiria
wale watoto, nakuwahurumia sana. Niliona vile watoto wangu walivyoteseka. Najua
kwa namna moja au nyingine, hata wa Danny wanapitia au watapitia hapo. Hakuna
mtu anayeweza kulea watoto vizuri kama mama yao mzazi.” Nanaa akabaki kama anayewaza.
Zamu yao yakuingia kumuona dokta ikafika.
~~~~~~~~~~~~~~
Daktari
akajaribu kuzungumza nao kwa mapana na umuhimu wa kuwa makini kipindi hicho
mtoto anapoendelea kukua, kama wanamuhitaji huyo mtoto. Geb akapata nafasi
yakuuliza maswali mengi ili kujua waamue nini. “Kama mtatumia usafiri wa ndege,
haitakuwa na shida sana. Lakini sishauri safari ndefu. Inaweza kusababisha
kutoka kwa mtoto, au kuanza kutokwa na maji ya uchungu kama ilivyokuwa kwa
Magesa.” Daktari aliendelea.
“Najua
mambo ya harusi Geb na Nanaa. Yana mambo mengi sana hasa kwa hii mnayotaka
kuifanya ndani ya juma hili. Shuguli nyingi kwa wakati mmoja, pia hazitafaa kwa
hali ya Nanaa.” “Nitahakikisha maandalizi yote hayatamuhusu yeye. Yeye atakuwa
na kazi ya kuwepo tu siku ile ya sherehe. Muda wote atakuwa kwenye mapumziko.
Vitu vyote visivyo vya muhimu havitakuwepo, na nitahakikisha huduma zote muhimu
atakazohitaji siku ile ya harusi zinamfuata chumbani. Hapatakuwa na shuguli
zozote na baada ya harusi tutakuwa hapo hapo hotelini.” Kidogo daktari
akaridhika.
“Naomba
na wewe uhudhurie. Sio kama daktari lakini mtu ambaye umehusika sana kwenye
maisha yangu. Tokea mimba ya Liv, mpaka sasa umekuwa na mimi bila kuchoka.
Umekuwa zaidi ya daktari kwetu. Naomba usiache kufika. Hata ukitaka tiketi ya
kwenda na kurudi siku hiyo hiyo, Geb amesema atahakikisha unapata. Ataandaa
utaratibu wakupokelewa uwanja wa ndege na kurudishwa. Huna haja yakulala.”
Nanaa akaongeza. Yule daktari akacheka. “Nitazungumza na mke wangu, halafu
nitawajulisha kabla ya alhamisi. Inaweza kuwa sehemu ya mapumziko yetu pia na
angalau nitajiridhisha kuwa upo salama.” Wakazungumza kidogo, wakatoka.
~~~~~~~~~~~~~~
Walitoka
hapo wakiwa wameridhika. Geb akampigia simu Grace nakumwambia aendelee na
maandalizi kwani harusi ipo. Wakapita sokoni kununua vitu baadhi kwa maandalizi
ya ujio wa Grace na mgeni usiku huo. Wakarudi nyumbani. Walimuelezea kila kitu
mama yao. “Hilo halina shida. Hata kesho huna haja yakuzunguka madukani.
Unaweza kuwepo kwenye gari au ukabaki hapa. Mimi na Grace tukakuletea aina ya
magauni utakayokuwa umetuelekeza unayataka.” “Hiyo iyakuwa rahisi mama. Ili asizunguke
sana.” Geb akaongeza.
“Na
pia humu ndani itabidi aache kabisa kujishugulisha na shuguli za watoto. Atulie
kabisa. Kutaliwa kitakachowezekana. Kitafanywa kitakachowezekana. Ilimradi
watoto wawe sawa, mengine tutavumiliana.” “Nashukuru mama. Angalau nisogeze
siku. Sitaki kuja kuhamishiwa tena hospitalini.” Nanaa akaongeza. “Ila utulie
Nanaa. Jitahidi kutulia. Acha kuhangaika na shuguli za humu ndani. Hata kama
ukiona kitu hakijafanywa, vumilia mwanangu.” “Nitafungia macho kila kitu,
ilimradi Geb wangu apate tu chakula.” “Ndio hayo ninayosema.” Mama G
akaanza.
“Nikumpikia tu Geb, mama.” “Wewe
nimekwambia niachie mwenyewe. Hata kama chakula kitachelewa, atakunywa maziwa.
Mwishowe mtahamia tena hospitalini. Maana nyinyi mmoja akilazwa hospitalini,
wote mnahamia huko huko. Mnaacha watoto wanahangaika hapa au wanazungushwa
kwenye gari kama makodakta.” Nanaa na Geb wakacheka.
“Msicheke.
Naomba tulia Nanaa. Mtapoteza huyo mtoto.” “Nitapumzika mama.” “Hata hivyo
nitazungumza na Jeri kama anaweza kutupa mkewe atusaidie kwa kipindi hiki.” “Na
kweli Geb. Mke wa Jeri alikuwa akinisaidia sana pale kwenye apartment siku
alizokuwa akija. Halafu msafi na anaupendo na watoto.” Nanaa akaongeza. “Basi
nitazungumza na Jeri.” Nanaa akatulia kidogo.
“Nini
tena?” Geb akauliza baada yakumuona anafikiria. “Nilazima niende kwa kaka leo.
Siwezi kufunga ndoa bila yeye kuwepo.” Nanaa akaongeza. “Tutakwenda jioni kabla
ya kina Grace kufika. Nilishamtumia ujumbe kumwambia ninashida yakumuona.
Amesema jioni atakuwepo nyumbani.” “Nashukuru Geb. Nilijua umesahau.” “Siwezi.”
Mipango ikaendelea hapo. Wakajikuta wageni walio nao wakuhudhuria harusi ni
wachache sana. Daktari anayemtibu Nanaa na mkewe. James na dada Fifi. Hao ndio
watu wa Nanaa. Kwa Geb ilikuwa ni mama yake na Grace. Mbali na watoto wao na
mgeni wa Grace ambaye ndio atakuwa msimamizi wa Geb. Lakini wakakubaliana ibaki
hivyo hivyo. Wasikaribishe mtu mwingine.
Nanaa kwa Kaka
Ilipofika
saa kumi na 11 jioni Geb, Nanaa na watoto wao walitoka kwenda kwa James. Nanaa
hakuamini baada ya kumuona kaka yake. Alikuwa amebadilika sana. Na James naye
alishituka sana alipomuona Nanaa kwenye hali ile. Mjamzito! Nanaa akajua. Bado
walikuwa wamesimama mlangoni wakishangaana baada ya James kuwafungulia mlango.
Geb alifika pale, akiwa amembeba Magesa. Nanaa amemshika Liv mkono. “Karibuni
ndani.” Wakaingia.
“Unaumwa?”
Nanaa akauliza. “Hapana. Mambo mengi tu. Karibuni.” James akajibu na kukaa.
“Hamna kitu chochote chakuwakaribisha humu ndani. Mimi mwenyewe ndio nimeingia
muda si mrefu.” Nanaa akamuhurumia sana kaka yake. “Pole kaka. Unaonekana
umechoka!” James akacheka kidogo.
“Vipi
na nyinyi? Naona watoto wanazidi kukua!” “Tunamshukuru Mungu wanaendelea
vizuri.” Nanaa akajibu. “Ila huyu kaka anaonekana atampita sasa hivi dada
yake.” James akaongeza. “Mwenzie anapenda kula. Liv mvivu sana wakula. Halafu
nahisi Magesa amechukua urefu wa baba yake. Nguo akivaa week hii, hawezi
kurudia tena week ijayo. Zinambana. Muone na kitambi chake. Njoo.” Magesa
akacheka akatoka kwa baba yake akamwendea mama yake. Wakiwa wamekaa pale pale
kwenye kochi.
“Mpenda
kucheka kama wewe.” James akaongeza. Wote wakacheka. “Eti Magesa. Dimpozi kama
za mama? Muone.” Nanaa akambusu. Muda wote Geb alikuwa kimya tu msikilizaji.
“Mnaendeleaje lakini?” James akauliza. “Tunataka kubariki ndoa siku ya
jumamosi. Itakuwa Arusha.” Hapo Geb akaongea. “Jumamosi hii!?” James akastuka
kidogo. “Ndiyo kaka.” Nanaa akajibu.
“Mbona
tukiza?” James akauliza. “Mimi ndiye nilikuwa sipo tayari. Nilipokuwa tayari
ndio Geb akaona hamna kusubiri tena. Tufunge tu kabla mtoto hajazaliwa.” James
akanyamaza kidogo kama mwenye swali lakini anashindwa aulize nini. Alianza
swali mara kadhaa, akasita.
“Mtoto..
Hiyo mimba..” Akanyamaza. Nanaa akainama akimchezea mtoto wake. Alijua swali
alilotaka kuuliza lakini alijua hajui aulizaje. James akavuta pumzi kwa nguvu,
akanyamaza. Geb aliyeweza kumwangalia alimuona amebadilika rangi akawa mwekundu
mpaka macho. “Yale matatizo
yalinisababishia ujauzito. Nilipata mimba. Ni mtoto wa kiume. Anaitwa Jimmy
James au JJ kwa ufupi.” Nanaa akaongeza huku machozi
yakimtoka. James akasimama, na kuondoka pale. Baada ya kama dakika 18 hivi,
akarudi akiwa amebadilisha mpaka nguo. Wazi alionekana ameoga kabisa.
“Mngependa
nikawaletee kinywaji chochote dukani?” James akauliza. “Hapana kaka. Nataka
tuwahi kurudi nyumbani mapema. Saa mbili usiku natarajia wageni.” “Unaishi wapi?” James akauliza. “Naishi na
Geb, nyumbani kwake na mama yake.” Lile jibu halikumfurahisha Geb. Lakini
akanyamaza. “Mbona Danny aliniambia hauishi pale?” “Baada ya yale matatizo
niliondoka kaka. Lakini Geb akanitafuta. Alinipata nikiwa na mimba ya miezi 5
tayari, ndio akanirudisha nyumbani.” James akanyamaza kidogo kama anayefikiria.
“Kwa
hiyo sasa hivi una miezi 7 na siku kadhaa?”
Nanaa akajua kaka yake amepiga mahesabu. “Ndiyo. Leo tulikuwa kliniki.”
“Mtoto anaendeleaje?” James aliendelea kuuliza. “Anaendelea vizuri.” Nanaa
akajibu. “Na wewe mwenyewe unaendeleaje?” “Naendelea vizuri.” Nanaa akajibu kwa
kifupi tu. James akamwangalia. “Naendelea vizuri kabisa. Sasa hivi nipo sawa.”
Nanaa akasisitiza. Hakuna aliyejua kama Nanaa ni mjamzito. Hakuwa ameonana si
rafiki wa kaka zake tu, hata kaka yake mwenyewe hakuwa ameonana naye tokea siku
ya tukio.
“Umemwambia?”
Lilikuwa swali fupi ambalo James aliuliza, lakini Nanaa na Geb walielewa.
“Hapana kaka. Nimekusudia nisimwambie kama nimebeba mtoto wake. Nitamlea tu
mwenyewe labda mpaka baadaye sana mtoto mwenyewe akitaka kujua. Ila tumekusudia
kuwalea pamoja.” “Watoto wa Geb wanajulikana Nanana. Waangalie hivyo walivyo
hapo. Wapo kama mapacha! Utaficha hiyo siri mpaka lini?” James akauliza. Nanaa
akanyamaza na kuinama.
“Kila
kitu kitajijibu kadiri tunavyokwenda James. Sasa hivi tunaweza tukawa hatuna
majibu yote. Lakini namwamini Mungu kutupa majibu kadiri siku zinavyokwenda.”
Geb akaingilia kati. “Hata hivyo Nanaa alishaandika kila kitu anachojua kitafaa
kujibu maswali yote ya Jimmy pindi atakapokuwa na maswali. Kwa hiyo naamini kwa
sasa tupo sawa.” Geb akasisitiza. James akavuta pumzi kwa nguvu na kuzishusha
taratibu.
“Nakushukuru
Geb. Asante. Nilitaka kusikia kutoka kwako mwenyewe ndio maana ilinibidi
kuendelea kudadisi zaidi. Nitajitahidi kuwepo Arusha siku hiyo ya jumamosi.”
“Kutakuwa na sehemu ya kulala, kama ungependa kulala na tunaandaa usafiri wa
ndege wakuwaleta huko. Hatutakuwa wengi.” Geb akamuelezea idadi ya watu na
jinsi harusi itakavyokuwa.
“Nafikiri
mimi nitaendesha ili nipate usafiri wa kunipeleka Moshi, nikamuone Mzee. Na kama
harusi haitachelewa kuisha, nafikiria kwenda kulala nyumbani kwa Mzee pia. Kwa
hiyo sitahitaji usafiri wa ndege wala sehemu ya kulala. Nitaua ndege wawili kwa
jiwe moja. Ili Jumatatu niwepo kazini.” James akajibu. “Unaweza kuwa na nafasi
ya mtu mmoja kwenye gari?” Nanaa akamuuliza kaka yake. “Nani? Maana siku hizi
sipendi mazoea na watu.” “Kuna huyu dada
anaitwa Fifi, alinisaidia sana kipindi nilipotoka kwa Geb. Mpaka sasa amekuwa
kama dada yangu. Ningetamani na yeye awepo kwenye harusi. Sasa kwa kuwa mimi
naondoka alhamisi, na yeye anashuguli zake, nafikiri kwa kuwa wewe unaenda na
kugeuza, ungemfaa.” “Hamna shida Nanaa. Tutaweka utaratibu mzuri tu ili na yeye
ahudhurie. Mwache James aendelee na ratiba zake. Lakini tunakushukuru sana
James. Asante. Tunategemea kukuona siku ya harusi.” Geb akaongeza. “Siwezi
kukosa. Tuombe uzima.” Wakaaga na kutoka.
~~~~~~~~~~~~~~
Nanaa
amekubali yaishe. Amerudi kujenga ‘home’ kama alivyoombwa na Geb. Amejenga kwa garama kubwa sana, KUSAMEHE. Amefanikiwa kurudisha Amani, urafiki ambao hata mama G
hakutegemea kama ungerudi, Nanaa amerudisha bila kinyongo. Geb amempokea kama
alivyo yeye na mtoto wake. Tena bado akimtamkia anautamani mwili ule ule
ulioubaka Malii.
Michakato ya
harusi imeanza upyaaa. Tena wakiwa wamekusudia kuwepo na watu wanaoweza
kuwapokea na baraka zao.
v Je, safari hii watafanikiwa?
Grace anarudi jijini na mwanaume
wa ndoto zake ili kukamilisha talaka anayotaka kupewa kwa aibu. Amechafuliwa
vilivyo.
v Nini kitatokea kati yao? Grace & Man, Danny & Sara. Watoto nao?
v Je, kuonana ana kwa ana kwa Grace na Danny kutawakumbusha jukumu la
uzazi, nakuamua kuacha penzi jipya ili warudi kulea watoto wao? Au Danny amelevya zaidi na penzi la Sara
kama Grace kwa Man!
J.5 ndio hatima ya misukosuko ya
ndoa hiyo waliyoombea kwa kufunga.
Usipitwe Yatakayojiri Kwa Mwanasheria.
0 Comments:
Post a Comment