Naomi Simulizi |+1 205 767 8163 |naomisimulizi@gmail.com Ni wangu! – Sehemu ya 56. - Naomi Simulizi

Ni wangu! – Sehemu ya 56.

Fifi alifika hapo asubuhi na mapema. Akamuamsha Nanaa. Akamuomba wajitahidi wasizungumze kwa sauti ili wasiamshe walio lala. Akaingia kuoga wakati Fifi akianza kutayarisha vitu, kisha akaingia chumbani kwa Geb kwa kunyata. Akamkuta amepiga magoti. “Nimekuamsha?” Nanaa akauliza kwa sauti ya chini. “Hapana. Nilishaamka muda mrefu tu. Nimesoma neno, nikaomba. Hapa nataka kurudi kulala. Vipi?” Nanaa akaingia na kufunga mlango.

“Umeniombea?” Geb akacheka. “Sana tu.” “Asante.” Nanaa akajiweka kitandani. “Kwanza nakushukuru kwa kuturuhusu tupikie hapa.” “Karibu. Ila hukuwa na sababu ya kushukuru. Wote tunaishi hapa. Kuwa huru kufanya chochote unachotaka.” “Lakini siwezi kuepuka ukweli kwamba wewe ndio unapamiliki Geb. Ni kwako.” “Kwetu.” Geb akarekebisha, Nanaa akacheka. Geb akaweka kidole kwenye dimpozi zake. 

Kweli alimkumbusha Nanaa mbali sana. Tokea enzi wanaanza mapenzi, Geb alipenda kufanya hivyo. Nanaa akainama kama anayefikiria. Geb akamvuta mkono. Nanaa akatoa kicheko cha kinyonge. “Dada Fifi amekuja. Tunaanza kupika. Ila tutajitahidi tusiwasumbue.” “Usiwe na wasiwasi. Unataka msaada wowote?” “Hapana. Tutakuwa sawa tu. Japo nafikiria vitu tulivyonavyo na gari ya dada Fifi! Nahisi itakuwa ndogo. Itabidi tufanye safari mbili au tatu. Nitaangalia. Ila itabidi kuwahi kuondoka ili nihakikishe vitu vyote vinafika ukumbini kwa wakati.” Nanaa akawa kama anayeweka mipango akifikiria kidogo.

          “Ngoja nikaanze kazi. Wewe pumzika tu. Najua mida ya kaka ndio hii. Akiamka nitampa tu uji wake.” “Wewe hiyo kazi ya watoto niachie mimi leo. Nataka na Liv akimka, niende nao ofisini kidogo. Lakini tutarudi mapema tu kabla hujaondoka. Au niseme nikuombe usiondoke kabla sijarudi.” “Sawa. Nitakusubiri. Nikuletee kitu chakula?” “Nitakula jioni. Asante.” Nanaa akajua na hiyo siku pia amefunga. Akamuhurumia.  Akambusu shavuni, akasimama. “Asante Nanaa.” Geb akashukuru. “Kwa nini!?” Nanaa akauliza. “Kunibusu. Nimefurahi sana.” Nanaa akacheka kama asiyesadiki.

“Kweli. Nimefurahi.” “Karibu. Basi ngoja nikaanze kazi. Wewe pumzika.” Akatoka asiamini kama bado Geb anafurahia busu lake. Hasa baada ya kubakwa na isitoshe amebeba mtoto wa Malii! Hapo napo akawa amemtumia ujumbe mwingine uliomfanya Nanaa aanze kufikiria tofauti.

~~~~~~~~~~~~~~~

Liv alivyoamka tu, Geb akamtayarisha na yeye baada ya kula, wakatoka nakumuacha Nanaa akiendelea na mapishi. Akaanza kuchukia kujaza nyumba yote na harufu ya maandazi, vitumbua, chapati, bajia na sambusa. “Inabidi siku nyingine tusipikie hapa dada.” “Ila Nanaa, mimi naomba utafute watu watakao kusaidia. Hii biashara mwenzio siiwezi. Nimeshaichukia.” “Dada Fifi!” “Kweli tena. Wewe uliniambia nitafute pesa. Nitatafuta kwa njia nyingine sio kwa kupika vitumbua bwana! Wale wapangaji nimewaambia wanipe kodi ya hata miezi sita. Wamekubali. Wameniambia week ijayo watanipa. Mimi naanza kufuga kuku. Mtindo wa kuamka asubuhi na kusambaza maandazi, huo sio wito wangu.” Nanaa akanyamaza akaendelea kupika.

Mwishowe akaona ampigie simu Geb. “Vipi?” “Naomba unishauri. Nataka kumuomba Jeri anitafutie mabinti wawili. Wazuri, wepesi kufundishika na waaminifu. Dada Fifi kasema leo ndio mwisho. Anaanza kujiandaa na biashara yake nyingine. Ni kama alikuwa akinisaidia tu. Halafu ngoja kwanza Geb.” Nanaa akamgeukia Fifi akiwa amekumbuka kitu.

“Wewe dada Fifi, hao kuku unaanza kufuga wapi?” Nanaa akauliza. “Wakati najipanga, naanza na vifaranga pale ulipopakimbia wewe.” “Dada Fifi wewe jamani!! Sasa mizigo yangu utaweka wapi? Halafu nikirudi mimi nitalala wapi?” “Acha kunidanganya Nanaa. Pale hutarudi tena. Labda huyo mwanangu. Naye nitaishi naye pale kwangu. Mimi na yeye tutatoshea tu. Kwanza pale nilipo mimi sasa hivi ni pakubwa tu. Chumba kizima na sebule! Kweli mimi na Jimmy wangu hapatatutosha?” “Kweli dada Fifi unakichukua chumba changu!? Usifanye hivyo bwana!” Geb alikuwa akiwasikiliza.

“Nakwambia najua wewe sio mtu wakurudi. Wamekuganda hawa kina Magesa, huwezi kurudi pale. Mimi nayajua mapenzi kwa…” “Kwa kupendwa.” Nanaa akarudia usemi anaoupenda Fifi. Wote wakacheka. “Sasa je! Nayajua mapenzi kwa kupendwa Nanaa. Si kusimuliwa wala kuyasoma mahali. Na pia nayajua sehemu mapenzi yalipo. Hata kama mtu akijidai kushupaza shingo vipi! Penzi kama lipo lipo tu. Wewe hutarudi pale. Labda mwanao, tena ukifa.” “Kwanza nimegairi kufa.” Fifi akacheka sana. Mpaka akakaa.

“Umeona dunia ilivyo tamu mdogo wangu? Sasa wewe jitangulize kaburini.” Nanaa na Fifi wakawa wamejisahau. Wanaongea nakucheka huku Geb akiwasikiliza. “Lakini wewe sio mtu mzuri dada Fifi bwana! Hutabiriki.” “Acha nitengeneze pesa mdogo wangu. Tena niitengeneze kwa raha. Mimi nilishakwambia kupika sipendi. Halafu leo uniamshe asubuhi kwa ajili ya kupika! Unanitesa bure! Wewe kusanya huku, mimi kule. Tukizichanganya tutakuwa mbali. Au unasemaje?” “Ngoja niongee na Geb wangu nione atanishauri nini.” Fifi akacheka sana.

“Yamekua hayo!” “Kumbe. Wewe upo kama kinyonga bwana. Ngoja nimpigie Geb.” Nanaa akachukua tena simu, akataka kupiga lakini akagundua bado Geb yupo hewani. “Geb!!” Akaita kwa kushituka.  “Nipo.” “Nilijua umekata!” “Uliniambia nisubiri mara moja, Nanaa.” Nanaa akaacheka. “Samahani.” “Hamna shida. Niko na Jeri hapa. Nitazungumza naye kama anaweza kukutafutia watu wa kukusaidia kazi.” “Nitashukuru.” Wakaagana.

~~~~~~~~~~~~~~~

Ilipofika saa 9 na nusu jioni, Nanaa na Fifi wakawa wamemaliza kupika kila kitu. Wakaamua waoge ndipo waanze safari. Alipomaliza kuoga akiwa chumbani kwa watoto, akampigia simu Geb. “Mmepotelea wapi wewe na wanao?” “Njoo hapa sehemu tunayoegeshea magari.” “Nimemaliza kupika Geb. Nataka kuanza kujaribu kupanga vitu kwenye gari ya dada Fifi nione kama tutahitaji kurudi au inatosha ili nisicheleweshe chakula cha kwenye sherehe.” Nanaa alionyesha hataki kwenda.

“Sitakuchelewesha mpenzi wangu. Njoo.” Kwa kuitwa mpenzi na Geb, akaona ni heri aende tu. Akacheka. “Nakuja basi.” Akatoka. “Geb ananiita hapo nje. Twende tutoke na baadhi ya vitu.” Wakatoka. Tumbo la Nanaa lilikuwa kubwa. Na maradhi aliyokuwa nayo, nikweli alikuwa amechoka. Alijikaza kufanya hiyo kazi lakini wazi alionekana amelemewa. Zaidi siku hiyo ambayo alisimama siku nzima akipika. 

Walitoka kuelekea sehemu ya kuegesha magari. Geb alipomuona tu amebeba vitu akamkimbilia. “Nimekwambia usibebe vitu vizito Nanaa!” “Ningefanyaje?

Nitajipanga taratibu.” Geb akampokea. “Nimerudi na Jeri na mabinti wawili ili wakusaidie. Nimeleta na hii gari. Liangalie na wewe kama itakufaa utumie kubebea vitu vyako.” Nanaa alibaki kama ameduaa. “Hivi umesikia chochote ulichoambiwa?” Fifi akamsukuma kidogo.

“Nahisi nimeshituka. Sikutegemea kupata msaada wa namna hiyo. Nashukuru Geb.” “Angalia kwanza kama itakufaa.” “Hata kama gari haitafaa, lakini kile kitendo cha kunifikiria tu, ndio nakushukuru.” Jeri na wale wasichana wawili walikuwa wamesimama upande wa pili, waliposikia Geb na Nanaa wakizungumza wakazunguka.

“Hee! Wana mpaka eproni na kofia kama wapishi!” Fifi akafurahi sana. “Mbona tutaenda kuweka heshima huko! Hata mimi nimefurahi.” Wakasogelea lile gari. Ubavuni ilikuwa imeandikwa Magesa Co. Anuani chini yake. Akajua ni gari yake Geb. “Naona hili kubwa. Halafu safi!” Nanaa akasifia. “Ndio kazi niliyokuwa nayo leo, mama. Nimeisafisha vizuri sana. Hata mkuu ameikubali.” Jeri akajisifia. Kabla hajamjibu Jeri wale mabinti wakamsogelea Nanaa. “Shikamoo.” Nanaa akacheka nafsi mwake. Wale wasichana walionekana wakubwa kuliko yeye. “Wewe dada Fifi, unasalimiwa!” Akamrushia mpira Fifi huku akijua wazi ni yeye. “Wala hawanisalimii mimi.” “Ni wewe.” “Umejuaje? Mbona walikutizama wewe wakati wakisalimia na si mimi?” “Wewe ungeitika tu dada! Wewe ndio mkubwa.” “Ukubwa wa umri na pesa ni tofauti. Si uliniambia heshima haiombwi?” “Basi dada yangu. Tuyafanye mafupi.” Wale wasichana walicheka tu. Kwa kuwa Geb alikuwepo, Jeri akajibaraguza, akaondoka pale. Geb alitulia kimya.

Akamsogelea Geb. “Nakushukuru mpenzi wangu. Asante.” Akajikuta ameongea neno ambalo hata yeye hakutarajia. Akamshika mkono. “Mungu akubariki katika hili.” Geb alitabasamu huku akimtizama. Alijua anatamani amkumbatie, lakini akamuona anasita, akaona amuache tu. “Asante.” Akarudia tena. “Karibu. Nimefurahi kama litawafaa. Sasa uwaelekeza hao wawili kitu chakufanya. Na Jeri naye atakuwepo. Ataendesha hili gari, mpaka huko.” “Asante. Nakushukuru.” Bado alibaki akishukuru kama anayetaka kutimiza kitu baada ya ile shukurani lakini anasita. Akamsikia Fifi anazungumza kwa sauti ya chini. “Umeniita dada?” “Nilikuwa najiambia tu mwenyewe.” Nanaa akacheka. Alimjua Fifi ni mtundu.

“Unajiambia nini?” “Nilikuwa najiambia mpaka tuje tuondoke hapa, tufike huko, sherehe itakuwa imeisha.” Nanaa akacheka. “Yaani wewe! Si nilikuwa nashukuru?” “Sawa!”  Itika ile, ikabidi tu Nanaa acheke zaidi. Akamuachia Geb mkono, akashukuru tena. “Asante.” Fifi akaanza kucheka.

“Naombeni na mimi nipokelewe hii mizigo, jamani!” Fifi aliongea huku anamcheka Nanaa. Jeri akarudi kwa haraka. Maana alisogea zaidi kama kumpa nafasi Geb na Nanaa. Nanaa akaondoka na wale wasichana kurudi ndani. Akawaonyesha vitu vyote alivyotayarisha. Nguvu ilimjaa kwa upya. Akawa amechangamka kama sio mjamzito mwenye tatizo la moyo. Wakamsaidia kupanga vitu vyake ndani ya hiyo gari. Jeri na wale wasichana wakaondoka kutangulia ukumbini. Fifi na Nanaa wakafuata nyuma. Walimuacha Geb na watoto walio lala. Njia nzima Nanaa na Fifi walikuwa wakiongea na kucheka. 

~~~~~~~~~~~~~~~

Walifika ukumbini, Jeri akiwa na maagizo ya kunyanyua vitu vyote vizito. Kabla ya muda wakula haujafika, Nanaa na timu yake wakawa wameshamaliza kupanga kila kitu, na panavutia. Watu walipenda upangwaji wa chakula. Usafi ulioonyeshwa kwenye vile vyakula, na mwisho ladha. Akajitengenezea baadhi ya marafiki/wateja, siku hiyo ikaisha ikiwa imejaa matumaini. 

~~~~~~~~~~~~~~~

Wakati Jeri anapandisha vyombo kwenye gari, huku wale wasichana wakimalizia kusafisha pale, Fifi ndiye aliyekuwa akisubiria amaliziwe kulipwa pesa yake iliyokuwa imebaki kwa ajili ya shuguli nzima,  Nanaa akaanza kusikia vichomi. Akajiweka kwenye kiti wakati anasubiria wote wamalize. Fifi alimuahidi angemrudisha. Alikaa mwisho kabisa wakati sherehe ikiendelea. ‘Vipi?’ Ujumbe ukaingia kutoka kwa Geb. ‘Nimechoka. Nipo hoi!’ ‘Pole. Unafanya nini sasa hivi?’ ‘Nimekaa tu. Jeri na wale wasichana wamenisaidia sana, nakushukuru. Sasa hivi Jeri ananisaidia kupandisha vitu kwenye gari na wale wasichana wanasafisha. Ni kama tumeshamaliza. Tukilipwa tu, tunaondoka. Dada Fifi amekubali kunirudisha.’ Nanaa akajibu. ‘Nipo hapa nje, nakusubiri.’ Nanaa hakuamini. Akasimama kwa haraka na kutoka hapo ukumbini.

Alimkuta Geb na watoto wake kwenye gari wanamsubiri. Watoto wapo kiti cha nyuma wakiangalia cartoons kwa kupitia screen ndogo zilizoning’inia nyuma ya viti vya mbele vya hiyo gari. Wametulia kimya. Nanaa akasogea mpaka kwenye dirisha la Geb. “Mama!” Liv akamuwahi. “Hey baby!” Nanaa akawa hajui asimame pale mbele hapo kwa Geb au arudi kwa Liv aliyekuwa akimchangamkia.

“Usinge hangaika Geb! Dada Fifi angenirudisha tu.” “Tulipitiwa na usingizi. Tumeamka muda sio mrefu. Nikawalisha hawa, ndio nikaona nikufuate. Pole na uchovu.” “Asante. Naona sababu ya kusimama sana, kiuno kinauma, vichomi ndio vimeanza kuwa vikali. Nimekataa oda zote za kusambaza ofisini week nzima.” Nanaa akafikiria.

“Eti nilikuwa nikifikiria. Sijui ni sawa?” “Nini?” Geb akauliza. Nanaa akafikiria tena kidogo. “Kwa sasa hivi na hii hali yangu jinsi nilivyo na watoto, labda niwe nafanya kwenye masherehe tu. Nisisambaze maofisini kila siku asubuhi. Nitashindwa kufanya vyote na afya yangu bado haijakaa sawa. Nisije nikapoteza mtoto au kujidhuru mimi mwenyewe zaidi. Sijisikii vizuri. Au unanishaurije?” “Kwangu ingekuwa furaha Nanaa. Kazi yakupika kila siku na kusambaza sio kitu kidogo, halafu bado na watoto wanakutegemea wewe! Ikiwa mara moja moja, ni afadhali. Lakini sio kila siku.” Akatulia kidogo.

 “Nimegawa namba yangu kwa watu baadhi. Wameniahidi tenda. Nitasubiri nione.” “Panda kwenye gari basi upumzike. Nitamwambia Jeri kuwa upo hapa.” “Afadhali.” Nanaa akapanda. Geb akamuona anatetemeka mikono. “Umekumbuka kunywa dawa leo?” Nanaa akabaki akifikiria. “Hujanywa. Na nafikiri presha imepanda Nanaa. Turudi nyumbani. Fifi atakuchukulia pesa. Nitamwambia Jeri kuwa tumeondoka.” “Na wale wasichana wanalipwa kiasi gani?” “Jeri ameshamalizana nao. Mwambie Fifi asiwalipe tena.”  Akajua yeye ndiye aliyempa Jeri pesa zakuwalipa wale wasichana waliomsaidia kazi. “Asante Geb.” “Karibu.” Wakaondoka. Ikabidi njiani ampigie simu Fifi kumtaarifu kila kitu.

~~~~~~~~~~~~~~~

Akashusha watoto, na kuwaweka chini pale sebuleni. Akaenda bafuni alipokuwa Nanaa. “Nikusaidie nini?” Bafu lilikuwa dogo si kubwa kama la chumbani kwa Geb, kwa hiyo alikuwa akimuona pale bafuni akioga. “Nipo tu sawa. Nataka nimalize hapa, nijilaze kabisa.” “Utataka nikupishe pale kitandani?” Nanaa akanyamaza kidogo. “Nakushukuru kwa kunifuata Geb. Kweli nilikuwa nimechoka.” “Nilihisi tu utakuwa umechoka. Ulisimama siku nzima ukipika!” Nanaa akacheka kidogo. “Nimefurahi kuweza kunifikiria.” Geb akatoa tabasamu tu.

Akamsaidia kukausha miguu wakatoka. “Najisikia vizuri. Natamani kutokee godoro kubwa hapa sebuleni, nijilaze hapo wakati wanangu wanacheza hapa hapa nikiwaangalia.” Geb akaenda kufuata godoro la kitandani kwake. Akalitoa. Nanaa akaanza kucheka. “Litakuangusha hilo godoro!” “Si unataka kulala hapa sebuleni na wanao? Basi acha mimi nitimize shauku yako.” Geb akaliweka chini lile godoro na kulitandika. Nanaa na wanae wakapanda. Magesa alikuwa amemshika mama yake huku akiruka ruka. “Anamwaga ute huyo! Muone. Anakazi yakucheka tu.” Nanaa akamfuta mwanae na kumtekenya zaidi. Magesa akawa anacheka sana. Wakajilaza pale wote mpaka Geb. Nanaa akapitiwa na usingizi muda uleule.

Kinachoendelea Ndani Ya Nanaa.

Mtoto akawa anacheza tumboni huku akiota ndoto mbaya. Geb akamuona anahangaika. “Nanaa, vipi?” Nanaa akashituka, akafungua macho na kugeuka. “Geb!” Aliita kwa mshangao. Alikuwa amelala nyuma yake. Karibu sana. Watoto wamezagaa kila mahali. “Mbona machozi tena?” Geb akamfuta. Nanaa akavuta pumzi huku amejishika tumbo.

“Nilikuwa usingizini naota ndoto mbaya. Lakini Jimmy naye huwa anacheza sana asubuhi. Wakati mwingine anakuwa upande mmoja. Naumia.” “Sasa hivi una maumivu?” “Upande huu.” Nanaa akaendelea kusugua taratibu. “Sijui huyu mtoto nimuite wa bahati mbaya! Wakati mwingine huwa hata sielewi Geb! Nilikuwa nikiweza kuzungumza na watoto wangu wote wakati wapo tumboni. Lakini nashindwa kitu cha kumwambia Jimmy.Nakuwa..” Nanaa akashindwa kuendelea kuzungumza, akaendelea kulia.

“Naweza kumshika?” Geb akauliza kwa upole. Nanaa akatingisha kichwa kukubali. Geb akaweka mkono. Akampapasa kwa muda kama kumtuliza yule mtoto, kisha akabusu tumbo la Nanaa. Akateremka mpaka chini alipokuwa ametuna yule mtoto, akaanza kuzungumza naye. “Umebarikiwa Jimmy. Mungu alikuweka hapa kwa wakati na muda alioona unafaa. Upo sehemu sahihi na kwa mama sahihi anayekupenda kuliko nafsi yake. Mungu amekuweka hapo na baraka zote anazojua utahitaji hapa duniani. Wote tunakusubiri kwa hamu.” Machozi yalikuwa yakiendelea kumtoka Nanaa wakati Geb akizungumza na Jimmy.

“Yupo dada mkubwa Liv na Magesa. Wote watakupa wakati mzuri. Tutakupenda na ninakuombea. Unisikilize Jimmy, huu ni muda wa mke wangu kulala. Sio wa wewe kucheza.” Nanaa akacheka. “Sasa hivi kila mtu amelala, na wewe unatakiwa ulale. Ndugu zako wakiamka na wewe tutakuamsha ucheze. Mwache mama alale. Umesikia?” Geb akambusu. Kweli Jimmy alikuwa anacheza. Geb akaendelea kumsugua huku akizungumza naye mpaka akatulia. “Amekusikia!” Wakacheka. Geb akambusu, na kurudi kulala pembeni yake.

“Tumekupokonya godoro, ikakulazimu ulale chini na sisi?” “Nimependa kulala hapa. Ona wanao.” Wakacheka. “Magesa anakaribia kuanguka.” “Mwache tu. Hata hivyo muda wake wakula umefika.” “Mbona na wewe ulikuwa hujalala?” “Niliamka kuomba. Nimemaliza nikakuona unahangaika. Ulikuwa ukiota nini?” Nanaa akanyamaza. “Niambie tu.” Akamuona anaanza kulia. “Ni ndoto mbaya?” Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Nakuwa napata ndoto mbaya ya kile alichokuwa akinifanyia Malii. Sasa wakati mwingine nakuwa naota sura za wanaume tofauti tofauti. Nakuwa napambana sana kujiokoa.” Geb akamuhurumia. “Pole sana Nanaa. Pole mpenzi wangu na samahani nilishindwa kukusaidia.” Nanaa alilia na kulia. Alilia kwa uchungu sana, Geb akamkumbatia akawa anaendelea kumbembeleza. Alilia kwa kwikwi, mpaka akajihisi uchungu umeisha, ndipo akatulia.

“Nilijua ungekuja hata kunisaidia kuoga!” Nanaa akalalamika. “Lakini ulinikimbia wakati nakuhitaji sana Geb. Uliniacha usiku kucha peke yangu, nikilia kwa uchungu na maumivu.” Nanaa aliendelea kulalamika. “Nilikosa Nanaa. Naomba nisamehe. Hakuna muda unapita, sijajutia. Ni kweli nilishindwa kusimama upande wako. Lakini sasa hivi nipo na wewe. Natubu nimekosa, Nanaa. Nisamehe.” Akaendelea kumbembeleza mpaka akatulia.

“Umenisamehe?” Geb akamuuliza huku akimbusu kichwani. Nanaa akatingisha kichwa kukubali. “Na mimi naomba unisamehe Geb. Sikukwambia kila kitu kilichotokea siku ile tulipokuwa na Malii, kwa kuwa niliogopa. Sikujua ungefanyaje kama ungejua Malii alishaniona nikiwa uchi. Maana ulipiga teke kiti ulichokalia mara nilipokwambia tulikiss. Hofu ya kuniacha iliniingia. Lakini najua nilikosa. Ni heri ningekwambia tu ukweli. Naomba unisamehe.” “Nimekusamehe Nanaa. Naomba Mungu atusaidie yaishe kabisa. Uwe ukurasa tutakaoweza kuufunga kabisa. Unafikiri utaweza?” “Sijui Geb. Kama ulivyosema ni kwa rehema za Mungu. Niliumizwa sana. Nahitaji muda.” “Naelewa. Na mimi nitaendelea kukuombea.” Wakatulia.

Geb akambusu tena na tena pale kichwani alipokuwa amemuegemea, wakiwa bado wamelala pale pale chini kwenye godoro. Wakati Nanaa anataka kurudisha busu, Magesa akaamka na kukaa kwa haraka. Alipowaona tu akaanza kucheka. “Yaani huyu! Amani yake huwa inamtosha yeye mwenyewe. Njoo.” Geb akamuita. Akaanza kutambaa kuwafuata huku akivuta mashuka.

“Taratibu usimwamshe Liv.” Magesa akamwangalia Liv kwa muda, akaendelea na safari ya kwenda kwa wazazi wake. “Kumbe anaelewa!?” Nanaa akashangaa. “Sana tu. Na Liv anampenda kweli. Si unamuona vile alivyolala pale kama amekufa? Hata ukimumsha hataki kuamka, basi ngoja Magesa alie. Hata dakika haiishi, na yeye ataamka. Hata kama ni usiku, akimsikia tu mdogo wake analia hata chumbani kwangu, atanifuata. Hatakuongelesha, lakini atakuja kumwangalia mdogo wake. Huwa pia anamuongelesha.” “Jamani Liv wangu! Kumbe ninaye wakunilelea watoto!” Geb akacheka.

“Muone. Umenikatili busu langu ambalo nilikuwa nalisubiria kwa hamu kweli! Usinichekee.” Magesa alimshika mama yake akasimama huku akimchungulia baba yake na cheko juu. Nanaa alicheka sana. “Geb wewe! Haya hilo.” Nanaa akambusu shavuni. “Wala halikuwa la shavuni. Mimi nililiona sana wakati linakuja.”   Geb alilalamika na kumfanya Nanaa na mwanae wazidi kucheka. 

~~~~~~~~~~~~

Amani na utulivu kati yao vikarejeshwa. Japo haikuwa kama zamani, lakini kulikuwa na utulivu wa aina yake. Nanaa alitaka kukaa karibu na Geb wakati wote. Japo amuegemee tu. Kama si wakiwa wamekaa, ampandishie miguu, basi walale kwenye godoro, awe nyuma yake amsikie akihema mgongoni kwake. Na Geb alijua kama anaanza kufunguka kwa kujisogeza karibu. Akaamua kumchukulia taratibu sana si kwa pupa huku akikazana na maombi.

~~~~~~~~~~~~

Siku hiyo ya jumapili hawakwenda kanisani, walibaki tu nyumbani. Ila Geb akataka kuzungumza naye juu ya ndoto anazoota. “Zinaweza kuwa zipo sababu nyingi zinazokufanya uendelee kuota ndoto mbaya, lakini moja wapo kubwa ni kwa kuwa bado hujasamehe Nanaa.” Walianza kuzungumza mara baada ya chakula cha mchana wakati watoto wanapata usingizi wa mchana. “Nina maumivu ambayo sijui nifanyaje Geb. Nimemuachia Mungu.” Nanaa alianza kwa upole.

“Sijihesabii haki, lakini nahisi niliadhibiwa na kila mtu zaidi ya kosa langu. Niliadhibiwa kikatili, kama niliyekuwa nikitafutiwa sababu ya kukomolewa! Ni kama niliyekuwa nikitafutiwa sababu ya wapi nikosee, nitendwe mabaya. Nashindwa kuamini kwamba kwa kusema uongo tu, au kutokuwa muwazi, ndio watu waliosema wananipenda, gafla kugeuka kuwa kama wanyama wakatili kwangu! Hapana Geb. Sidhani hata kama kulishawahi kuwa na upendo kwangu. Nashindwa kuamini.” Nanaa akaendelea.

“Hujui ni kwa kiasi gani hata huyo Malii alivyokuwa akinisumbua kunibembeleza na kunishawishi kuwa ananipenda kwa dhati. Alikuwa akinisumbua mchana na usiku mpaka nikamtishia kuwa nitakwambia kama asipoacha kunisumbua. Kidogo akatulia. Ili kuepusha ushahidi, akawa anatafuta jinsi ya kuonana hata na wewe ukiwepo ili azungumze na mimi. Safari za nyumbani pia akaongeza ili tu anione. Akawa kama amepagawa! Vyote hivyo alikuwa akiniambia ni kwa vile ananipenda sana. Na hapo nikamuonya.”

“Siku moja wakati akiongea maneno yake bila yeye mwenyewe kujua, nikamrikodi. Alipomaliza kuongea, nikamwambia nimemrikodi. Tena alikuwa kama anakuvizia. Nafikiri alikuwa akikupigia kwanza simu. Akijua hampo nyumbani, au siku za kazi ambazo anajua hata mama hayupo nyumbani, alikuwa akija. Siku hiyo nilipomrikodi ilikuwa siku ya kazi, mchana. Nyinyi wote hamkuwepo. Nilikuwa na Liv tu. Nilipomaliza kumrikodi, nikamsikilizisha mazungumzo yake yote. Nikamwambia akiendelea kuja pale nyumbani na kutafuta kuzungumza na mimi, nikamwambia nitakwambia wewe au mama na nitawasikilizisha hayo mazungumzo yake yote. Malii alisikitika sana. Nakwambia kweli Geb, Malii alilia. Tena hapo nilikuwa tayari ni mjamzito wa Magesa. Analia anasema ananipenda kwa dhati. Nikimkubali tunaweza kukimbia naye hata nje ya nchi, tukaanze naye maisha mapya. Mimi nikamwambia Malii, ile hali aliyonayo wakati ule sio kawaida. Amepagawa mapepo. Akasema si mapepo ni penzi la dhati kwangu. Nikamwambia haiwezekani aendelee kunifikiria mimi wakati mimi nilikuwa na mtoto wako na tayari nina mimba nyingine. Yeye anaye mkewe nyumbani. Dada mzuri tu aliyetulia. Kwa nini asitulie na mkewe? Nikamshauri akaombewe na asirudi tena pale, lasivyo nitakwambia.”

“Hapo tena akatulia kwa muda. Akaacha kuja nyumbani muda ambao anaojua nyinyi hampo nyumbani. Sasa niambie ukweli Geb, hata kama kweli Malii anasema nilikosea kumvulia nguo na kuacha kulala naye, kama kweli ananipenda kama alivyokuwa akiniambia, ndio angeniadhibu mbele za watu!? Mtu unayempenda huwezi kumfanyia vile.” “Alikuwa akinikomoa mimi zaidi.” Geb akaongea kwa upole.

“Na yeye ameniambia hivyo hivyo.” “Kwani mliendelea kuwasiliana!?” Geb akashituka sana. “Alikuwa akinitumia jumbe za kuomba msamaha mchana na usiku kwa kutumia Whatsapp kwa namba yake au tuseme kwa account yake ya zamani. Anasema angetafuta njia nyingine ya kukuadhibu lakini sio kunitendea mimi alichonitendea. Anaomba msamaha, na kuniambia anajutia. Alidhani ingemsaidia kupata furaha, lakini eti baada ya bangi kumuisha, ndipo akili zikamrudia, akajutia. Nimsamehe.” “Kwa hiyo ulikuwa ukisoma jumbe zake?” Geb akauliza kwa kuumia.

“Mwanzoni sikuwa nikisoma kabisa. Nilipogundua kama nina mimba yake, na nimepatwa matatizo ya moyo. Pengine naweza nisiishi baada ya kujifungua, ndipo ikabidi nirudi kusoma zile jumbe. Zilikuwa zaidi ya jumbe 1000. Ikabidi nizipitie tu. Nikajiambia hata nifanye nini, sitaweza kumkwepa tena.” “Kwa hiyo anajua kama na yeye ana mtoto wake kwake?” Geb akauliza akisikika kuumia zaidi. 

“Hapana Geb! Hatakaa akajua leo wala kesho. Labda hapo baadaye, mtoto wake aje amtafute yeye mwenyewe. Lakini sitamwambia kwa haraka. Nimemwambia na kumwandikia hata dada Fifi. Ikitokea ninakufa na sitakuwepo, Jimmy aje aambiwe baba yake alipo. Kama akizidiwa na ulezi kabla Jimmy hajaweza kujitegemea mwenyewe, basi amtafute Malii huko alipokimbilia mpaka ampate. Nikamwandikia mawasiliano yake yeye na  ya wazazi wake Malii. Ili awatafute kama Malii hatamjibu kwa haraka au kama hatakuwa akipatikanika tena.”

 “Maana aliniambia yupo kwenye hiyo nchi akinisubiri kwa muda. Kama sitamjibu kwa miezi sita, atajua nimekataa, yeye atahama tena na kwenda kuanza maisha nchi nyingine ambayo anajua, maisha sio magumu kama hapo alipo sasa lakini anasema hapo alipo au alipokuwepo sasa hivi, panafaa kwa kuanzisha familia. Au kwa maisha ya familia.” “Subiri kwanza Nanaa.” Geb akataka atulie. “Malii hayupo hapa nchini?” “Aliniambia alitoroka siku ileile usiku. Kumbe alikuwa ameuza vitu vyake vyote baada ya kumtaliki mkewe, akawalipa wale vijana na kukata tiketi ya kumtoa hapa nchini usiku ule. Ndio maana alikuwa akirudiarudia kuwa atachelewa. Kumbe alikuwa anawahi ndege.” Nanaa akaendelea kufunguka.

“Sasa sijui alikuja kuambiwa na nani kuwa uliniacha kesho yake baada ya kunibaka, napo hapo akapata chakuzungumza. Akaniambia anajuta hata kwa nini aliniacha. Angejua angebaki ili pengine ningepata mtu wakuwa naye kipindi hicho kigumu. Akazidi kusisitiza kuwa ni kweli hunipendi. Ni heri tu niamini kuwa ulikuwa ukinitumia tu. Na kwa kuwa wakati huo ulishapata jinsia ya mtoto wote uliokuwa ukiwataka hapa duniani, ndio maana umeniacha. Umeona nitakuwa tu mzigo, sina matumizi mengine tena kwako. Ndio maana uliwachukua watoto na kuniacha peke yangu. Akaniambia anitumie nauli nimfuate tukaanze naye maisha. Na ahadi nyingi tu. Lakini sikuwahi kumjibu. Na hayo yote nilikuja kuyasoma nilipojua nina mimba yake.”

“Nili m’block’ kwa muda ili niweze kutulia. Kwa hiyo kwa sasa sipati jumbe zake tena. Lakini nafikiria nitakuja kumfungulia siku za kujifungua zitakapofika ili nimkabidhi dada Fifi simu yangu awe na uwezo wa kuwasiliana naye, kama ikitokea sitatoka chumba cha kujifungulia. Na nilishamwambia dada Fifi kila kitu. Ikitokea hata naanguka leo na kufa halafu Jimmy akapona, basi afungue hiyo akaunti na kuwasiliana naye Malii kama atataka. Asipotaka basi Jimmy atakuwa ndio zawadi yake.” Nanaa akafikiria.

“Najua Jimmy atakuja kujua jinsi mimba yake ilivyoshikwa. Hata akimkasirikia baba yake, ni baba yake tu. Kwa hiyo sikufuta jumbe hata moja katika zile jumbe alizonitumia Malii, ili Jimmy aje aweze kusoma upande wa pili wa baba yake. Labda yeye ataweza kumsamehe, maisha yake yakaendelea. Ninachotaka ni mwanangu aje kuwa na maisha mazuri sio kama mimi.” Nanaa akatulia kidogo kama anayefikiria.

“Lakini hebu niambie Geb. Katika yote hayo, sawa nimekosa. Nimetamkiwa upendo wa kila namna. Kweli ndio nitendwe nilivyotendwa!? Mpaka neno upendo limepoteza maana kwangu. Sielewi tena mtu anaposema anakupenda ndio nini! Ni neno la wakati tu ili kufurahishana au labda hata mimi mwenyewe sijalielewa lina maana gani!” Tayari Geb alijua maneno yalizagaa. Kila mtu anajua kilichoendelea na kinachoendelea kwenye maisha yake.

“Malii alijua udhaifu wangu na ratiba zangu, ndio akaamua kutumia vizuri. Tamaa yake juu yako iliongezwa kwa kuwa mimi nilikuwa na wewe. Malii hajawahi kukupenda. Lakini wakati wote alipenda kile ninachokipenda mimi. Nilikwambia vile anavyohangaika kushindana na mimi tokea tupo sekondari. Tena sio kwamba atataka anifikie, atataka kunishusha ili achukue vyangu. Nakumbuka kumsikia hata James akimuonya wakati tupo sekondari. Alikuwa akiumia vile nilivyokuwa nikipata alama za 100 hata kama anayenifuata amepata 20. Malii akadhani huwa naangalizia. Naiba mitihani halafu nawaficha. Siwapi na wao. Akaanza kusambaza huo uongo. James akamwambia siibii, ila huwa sisahu. Malii hakuamini. Akaenda mpaka kunisemea kwa walimu. Nikawa nawekwa kiti cha mbele kabisa kila siku za mitihani. Na bado nikawa napata 100 wala sio 99. Hapakuwa na jinsi walimu wangeweza kunifelisha.” Geb akaendelea.

“Akaendelea hivyo hivyo mpaka chuoni. Akiona wasichana wanakuja kuomba msaada niwafundishe, basi atajitahidi kulala nao. Na atahakikisha kundi letu lote wanajua. Mimi nilijua kama anashindana na mimi. Ni Frida tu ambaye alimshindwa wakati tupo naye chuoni. Kwa kuwa Frida alikuwa mweusi au maji ya kunde sijui, lakini alimshindwa akasema sio type yake. Ikaendelea mpaka kwenye uchumi na kila mahali.” Geb akaendelea.

“Malii hakuwa hata na mpango na wewe. Kuja tu kukuona na kujua naweza kukupata, ndipo akaanza fujo. Siwezi kumsema vibaya kwa kuwa na yeye utazaa naye kama mimi, ni baba yake Jimmy ambaye nipo naye sasa hivi. Na ninajua atafurahia sana akijua kama na yeye anazaa na wewe kama mimi.” Nanaa akaanza kulia.

“Kwa nini Mungu ameruhusu haya yote kwenye maisha yangu? Kwa nini huyu mtoto asizaliwe na mke wa Malii iwe mimi? Kwa nini mimi!?” Nanaa akaendelea kulalamika na kulia sana. “Sijui nafanya nini! Sijui kwa nini mimi! Lakini sio kitu nataka kinitokee kwenye maisha yangu. Na ninasikitika pengine Jimmy anajua. Lakini sio kitu nilikuwa nataka. Mungu anisamehe kwa kweli. Lakini sio na Malii. Sikutaka huyu mtoto. Na sijui naishije naye huyu mtoto! Sitaweza ni heri kufa tu.” Akasimama na kuondoka pale huku analia. 

          Aliingia chumbani kwa wanae, akaenda kupiga magoti kitandani na kuendelea kulia sana huku ameinamisha uso kwenye godoro. Geb akamfuata. Akaenda kupiga magoti pembeni yake akamuwekea mkono akaanza kumsugua mgongoni.  “Naomba niangalie Nanaa.” Nanaa akamgeukia. “Naomba turudi sebuleni tukamalizie mazungumzo yetu.” Nanaa akakubali. Wakatoka tena.

Bado alikuwa akilia. “Najua ni ngumu sana kuniamini tena. Kwa kuwa si Malii tu aliyekuumiza, mimi nimekuumiza zaidi ya Malii. Ila nipo hapa na wewe. Naahidi kusimama na wewe wakati wote. Sasa hivi ukiwa mjamzito, siku unayojifungua, na wakati unamlea Jimmy. Malii anajua na najua amekwambia kuwa huwa sipiti kule alikopita yeye.” Nanaa akatingisha kichwa kukubali kuwa alishamwambia. “Lakini safari hii amekosea. Ni wewe Nanaa. Wewe ni mke wangu mimi. Hata kama nimeshindwa kuishi chochote nilichowahi kukuahidi tokea nakufahamu, basi safari hii niamini. Nipo hapa, sina ninapokwenda. Nitakuwa na wewe.” Machozi na kamasi vilikuwa vikimtoka. Geb akamfuta.

“Jimmy hajaletwa kwenye maisha yetu ili akutese. Yeye sio adhabu. Hiyo ni baraka. Kwa sasa utashindwa kujua lakini jipe muda. Naomba kwanza tumpokee na kumkaribisha kwenye maisha yetu. Itakuaje baadaye, hata mimi sijui. Lakini ninachojua ni kuwa hata katika hili, Mungu atatupitisha tu.” “Sidhani Geb. Haitakuwa kama zamani.” “Niangalie Nanaa. Niangalie tu.” Nanaa akanyanyua uso na kumtizama huku akilia.

“Niambie ni mangapi magumu tumepitia mimi na wewe na bado tupo pamoja mpaka sasa na Mungu akatubariki watoto!?” Nanaa akaendelea kulia. “Naomba kwa mara ya kwanza nikwambie ukweli Geb. Ila usinishangae.” “Niambie tu.” “Lakini usinielewe vibaya. Ni kitu nimekibeba sina pakusemea.” “Mimi nitakusikiliza.” “Mimi simtaki kabisa huyu mtoto, Geb. Simtaki Jimmy. Wakati mwingine akicheza huwa nalia si kwa maumivu, ila hasira niliyobeba kwa baba yake. Namchukia sana. Na ninajua hata yeye pengine anajua huyu mtoto. Lakini mimi simtaki. Naona ni kama kitu kilichokuja kunitenga na wanangu. Ataniua nisindwe kuwa na Liv na Magesa. Hakika mimi huyu mtoto simtaki Geb.” Geb akamuhurumia sana. “Najua ni vibaya. Lakini angalau umejua kilichopo moyoni mwangu.” “Pole Nanaa. Pole sana. Naomba utulie tuzungumze.” Geb alijaribu kutulia sana usoni ili Nanaa apate faraja.

“Unakumbuka ule ugonjwa wa miguu?” Nanaa akatingisha kichwa. “Unaweza kulinganisha na Jimmy?” “Hapana!” “Unakumbuka Mungu alivyotutembelea kwa namna ya ajabu pale hospitalini?” “Nakumbuka.” “Basi naomba ukumbuke kuwa, Mungu tunayemuamini huwa hashindwi na kitu. Jimmy si tatizo, na wala hatakuwa tatizo. Tutakuwa naye kama mtoto ambaye Mungu ametupa dhamana naye. Kwamba ameangalia hapa duniani ni nani mwenye uwezo wa kumlea Jimmy, akatuchagua sisi. Yaani naomba uone hivi, kuwa Mungu ametuamini, ndio maana akatukabidhi Jimmy. Hatakuwa jaribu kwetu. Na utaona yale shetani aliyokusudia kuwa mabaya kwetu, vile Mungu atakavyoyageuza kuwa mema.” Geb akaendelea.

“Cha msingi naomba unipe nafasi na mimi. Nipe nafasi tafadhali. Tutembee pamoja. Tuzungumze kama tulivyo zungumza leo. Ukawa huru kuzungumza kila kitu bila kificho. Ndio napenda iwe hivyo. Tuzungumze kila kitu. Narudia tena. Hata kama kitakuwa kibaya, unajua kitaniumiza, tafadhali nishirikishe tu. Nakuahidi hakutakuwa na siri kati yetu. Niulize chochote unachotaka kujua, nitakujibu. Ila yale ambayo najua yatakuumiza kwa sasa, naweza nisikwambie mpaka utakapopona kabisa na daktari akanihakikishia utaweza kubeba mambo mazito. Ila sitakudanganya.” “Kwa hiyo bado unanichukulia kama mpenzi wako?” Geb akacheka.

“Nakupenda Nanaa. Nakupenda sana. Wewe ni wangu. Na ukitulia tu, nataka tukapeleke ndoa yetu kanisani.” “Kabla sijajifungua!?” “Ukiwa tu tayari, wewe niambie.” Geb akamsogelea. Akashika mkono wake na kuubusu. Akabaki akimwangalia kama anayesubiria jibu. “Naomba nipe muda tena kidogo Geb. Angalau akili itulie. Sitaki tubariki ndoa yetu nikiwa na hii hali moyoni.” “Bado unapata muda wa peke yako nakuomba?” “Najitahidi.” Nanaa akaongea kama hana uhakika.

“Maombi pekee ndiyo yatakutoa hapo.” Akabusu tena mkono wa Nanaa, aliokuwa bado ameushikilia. “Asante Geb. Nakushukuru.” Geb akatabasamu huku akimwangalia kwa uchu kama anayetamani jambo litokee pale. Nanaa alijua, akainama. “Unakumbuka nilizungumza na wewe juu ya kusamehe?” Nanaa akakubali. “Basi muombe Mungu akupe hiyo rehema. Wakati mwingine usisikilize sana hisia. Huwa zinachelewa kuendana na jambo jema. Fanya tu. Chukua hatua ya kwanza ya kusamehe, utashangaa hisia nazo zinakufuata nyuma.” “Basi niombee.” Geb akacheka.

“Kabla ya kukuombea, nataka kwa mara ya kwanza, mshike Jimmy.” Nanaa akaanza kulia tena. “Mshike tu. Mtamkie jambo jema. Zungumza naye. Jitambulishe wewe ni nani kwake. Ukiweza, muombe msamaha kwa chochote kibaya ulichowahi kumtamkia. Mwambie vile inavyokugarimu yeye kuwepo humo ndani, ili ajue unalipa garama kubwa kwa upendo ulio nao kwake. Mtambulishe kwa Liv na Magesa. Hakikisha wanapata muda naye kama ulivyokuwa ukimfanyia Liv kwa Magesa. Ruhusu watu wengine wawe na ushirika naye. Usimuone kama ni jukumu lako peke yako. Acha na sisi tuwe karibu naye. Halafu mkiwa peke yenu, pata muda naye. Utashangaa kitu kipya kitajengeka kati yenu.”

“Sasa wewe nitakutambulishaje kwake?” Nanaa akauliza. “Vyovyote vile utakavyotaka wewe.” “Wewe hutakuwa na tatizo?” “Hata kidogo. Magesa na Liv hawakuchagua mimi niwe baba yao. Wamejikuta tu. Ndivyo ilivyokuwa kwa Jimmy.

Hakuchagua.” “Ni kweli Geb. Namwadhibu mwanangu bure. Asije kuwa kama mimi akajihisi ni mtu wa kukataliwa. Maana na mimi sikuchagua kuzaliwa na wazazi wangu.” “Basi unao muda wakutengeneza.” “Nashukuru Geb.” “Basi naomba uzungumza na Jimmy ndipo nikuombee.” Nanaa akafanya kama alivyoelekezwa na Geb, huku akilia kwa uchungu sana. Alitubu hata mbele za Mungu. Alipomaliza, Geb akamshika mikono yake yote miwili, akamuombea. Akashangaa mpaka wanamaliza, kuna kitu kipya kimejengeka. Si kwa Jimmy tu, hata vile alivyojisikia kwa Geb. Akawa kama ametua mzigo.

Kwa Grace!

Wakati mambo ya Nanaa na Geb yanaendelea vizuri, kwa Grace bado kulikuwa kunawaka moto. Alishafunga na kuomba lakini mambo yalikuwa vile vile. Danny akawa kama amepagawa. Hasikii wala haoni. Grace alishatumia maandiko yote aliyoyajua kuyakiri ili kunusuru ndoa yake, lakini wapi. Akabaki kuwa mke mwema wa kupika na kupakua. Kusubiria Danny arudi usiku. Akaishia kuumia kila mara alipokuwa akimuona anarudi nyumbani usiku akiwa na Sara. Akaamua kuacha kumsubiri. Akajitahidi kuwepo nyumbani muda watoto wanaporudishwa. Anawahudumia, akishawaweka kitandani anarudi chumbani kuomba. 

Danny alishahama hata chumba. Akamuachia Grace chumba. Hakutaka kujua yanayoendelea usiku lakini Sara aliyasimulia yote kwa msichana wa kazi wa Grace. Danny anapokuwa akiondoka na watoto, Grace naye kwenda kazini, basi Sara hubaki hapo ndani akitawala kwa uhuru wote yeye kama mama mwenye nyumba. Majigambo na kujisifia mbele ya huyo msichana wa kazi, tena kwa kusudi tu ili kumfikishia Grace ujumbe. Kwani Grace alikuwa akishaingia ndani kwake usiku, hatatoka mpaka asubuhi anaposaidiana na msichana wa kazi kutayarisha watoto wake ili waondoke na baba yao kupelekwa shule. Sara akaona Grace anapitwa na starehe anazopewa na Danny. Akahakikisha ujumbe unamfikia hata kama hataki kushuhudia.

          Kwa asili Grace alikuwa mkimya sana. Mpaka afungue mdomo wake, ujue ni muhimu. Sasa hicho kilizidi kumkera Sara aliyekuwa akipenda kuongea. Danny akiwepo, Sara alijitahidi asizungumze ya ndani. Lakini akijua Grace yupo hapo ndani hata kwa dakika kumi kabla muda wake wakutoka kwenda kazini haujafika, Danny akiondoka na wanae, basi Sara alitumia huo muda vizuri sana kumkera Grace. Kama hatajiongelesha koridoni akiwa anapita, au sebuleni akiwa ndio amehamia hapo kujilaza. Akisema anapumzisha kiuno sababu ya shuguli ya usiku, basi atahakikisha kokote alipokuwa Grace, anapata ujumbe wa kile anachotendewa na Danny usiku huko chumbani. Starehe zote za kitandani, ndio zitasemwa hapo. Pesa anazopewa, aina ya nywele zilizopo kichwani mwake na zitakazowekwa tena, na kutoa ratiba yake ya siku nzima. Labda atakwenda huku au kule, ilimradi tu ni kero. Grace alikuwa kimya. Hakuwahi kumjibu wala kumsemesha.

~~~~~~~~~~~~

Ilikuwa siku ya ijumaa, Grace akampigia simu Geb. “Naomba tukutane kwa chakula cha usiku. Tutakuwa na mama. Nataka kuzungumza na nyinyi.” Geb akatulia kidogo. Alikuwa ndio amefika tu nyumbani anataka kupata muda na Nanaa, na watoto wake. “Geb!” “Wapi na saa ngapi?” “Kama unaona ni usumbufu, basi.” Akamsikia ni kama amekasirika. “Nitakuja G. Samahani. Ndio nimeingia tu nyumbani sasa hivi. Hata sija…” Geb akaona abadilishe. “Niambie nije wapi na saa ngapi.” “Kama unataka muda na familia yako, basi Geb. Sitaki kuendelea kuharib..” “Grace! Mimi nimekwambia nitakuja. Niambie unataka kuniona hapo saa ngapi na wapi.” Grace akamuelekeza. Wakakata simu.

Geb akamwangalia Nanaa na wanae. Wote walikuwa wapo tayari wakimsubiria arudi nyumbani watoke. Geb aliwapigia simu akiwa njiani, akamwambia Nanaa awaandae watoto anakuja kuwachukua awapeleke kula na kucheza. Lilikuwa juma zito kidogo kwa Geb. Alikuwa akitoka asubuhi na kurudi jioni giza likiwa limeshaingia. Ilipofika ijumaa, ndipo akaona akatumie jioni hiyo na familia yake. “Samahani Nanaa.” “Wala usijali. Sisi tupo tu sawa. Tulikuwa tukicheza hapa karibia siku nzima. Tutatoka wakati mwingine.” Geb akajiweka kwenye kochi.  “Lakini kula kwanza kabla hujaondoka. Maana hujui ni saa ngapi utarudi na kama utapenda chakula cha huko au la.” “Nashukuru.” Nanaa akamuwekea chakula akala. Akacheza kidogo na watoto wake, akaingia kuoga na kutoka.

 Mchuma Janga!

Alifika pale walipokubaliana kukutana na Grace pamoja na mama yao, akawakuta wameshaagiza vinywaji wanakunywa. Akaangalia saa. “Hujachelewa. Sisi ndio tuliwahi.” Grace akamuwahi kaka yake. “Kwema?” Geb alikuwa na haki yakuuliza kwa kuwa Grace alikuwa naye kazini. Hapakuwa na mazungumzo yeyote yale ya haraka. “Sijui Geb! Ila nilitaka niwashirikishe jambo. Utakula kitu chochote?” “Hapana. Nimeshakula nyumbani. Nipo sawa tu. Labda maji.” Geb akajibu.

“Nanaa na watoto hawajambo?” Mama yake akauliza. “Namshukuru Mungu wanaendelea vizuri.” Geb akamjibu mama yake. Muhudumu akaja, wakaagiza. Geb akabaki akimtizama Grace. “Mbona unaniangalia hivyo!?” Grace akamuuliza kaka yake. “Umebadilika sana, lakini ukapendeza.” Grace akacheka. “Hata mimi nimemwambia amerudi kuwa msichana mdogooo.” Mama yake akaongeza. “Nimepitia magumu mengi. Mwili wote wa umama umeisha. Mpaka tumbo!” “Umesema umepita?” Geb akauliza.

“Ndio maana nimewaita hapa.” Grace akajiweka sawa. “Kwa ufupi tu, naona ndoa yangu imeisha kabisa. Nafikiri nyinyi mmekuwa mashahidi vile nilivyomlilia Mungu kwa ajili ya Danny. Lakini naona amekusudia kuachana na mimi. Mbaya zaidi, naona yeye na Sara, wamekusudia kuniumiza kwa kuwa Danny anajua udhaifu wangu. Hakika anautumia vizuri sana.” Grace akaendelea kuongea, Geb akimsikiliza kwa makini.

“Nipo kwenye wakati ambao, nikiendelea kuwepo pale ndani nikiwa kwenye hali hii, kama sitachanganyikiwa, basi naweza mimi mwenyewe kumuandikia Danny talaka. Kwa kuwa hisia zangu zimekinahiwa kabisa. Kila sehemu ya mwili wangu imemchukia Danny kitu ambacho sikutegemea kama kinaweza kunipata. Nimeanza hata kujuta ni kipi nilichokiona kwake mpaka akanioa. Nimefika mahali hata sitamani tena kumuona. Yaani najiuliza hata akirudi kuniomba msamaha na kutaka turudiane kama nilivyokuwa nikimuomba Mungu, najiona sitakubali kabisa. Kwa ufupi, na mimi nimefika sehemu ambayo naogopa hata kukiri, lakini ukweli simtaki tena Danny.” Grace akaendelea.

          “Nikikaa mimi mwenyewe, najikuta namkosoa kila kitu chake.” “Hudhani nikuchoka?” Geb akauliza taratibu. “Nahisi hivyo. Nahisi nafsi yangu imechoka kiasi kwamba sasa hivi naongozwa vibaya sana nahisia kitu ambacho nakumbuka hata wewe Geb nilishakwambia kuwa mahusiano hayaongozwi na hisia. Kwa kuwa inaweza kufika siku unaamka, hutaki hata kumuona mwenzio. Lakini inabidi tu. Sasa sijui kama hivyo ndivyo nilivyokuwa nikiishi na Danny nikawa najibidisha tu! Sijui! Lakini sasa haya mambo anayonifanyia ndiyo yametibua, sijui Geb. Ila nakwambia ukweli, simtaki tena.” Grace akasisitza.

“Hii yakunikuta siku hizi nimeshafika kazini, sio kwamba nimeongeza juhudi kazini! Ni kwa kuwa nawakwepa. Sitaki hata kumuona sura yake. Najitahidi kutoka asubuhi na mapema kabla hawajaamka, na nikirudi, nahakikisha wamelala, au hata nikikuta gari yake nje, basi nipite mlango wa jikoni, niingie chumbani kwangu nilale?” “Na watoto!?” Geb akauliza kwa mshangao.

“Ndio kinachoniogopesha Geb. Sijali tena.” “Hapana Grace. Lazima kuna tatizo.” “Si ndio maana nimewaita! Hakika kuna tatizo. Mwenyewe anajitahidi sana kutoka nao na kuwapa vitu vizuri ili wasiwe na muda na mimi. Ukiwakuta wakicheza video game na wanae, hata ukiingia, watoto hawataki hata kugeuza shingo kukusalimia. Nyumba imegeuka kama sehemu yakucheza watoto. Kuna michezo ambayo hata mimi mwenyewe sijawahi kuiona. Basi utasikia wakishangilia yeye na wanae, usiku kucha. Vimejaa vicheko. Kwa kifupi, amefanikiwa kutengeneza kambi yake kwenye ile nyumba. Hawajui naingia saa ngapi wala natoka saa ngapi. Hakuna hata mtoto anayeniulizia. Hata kutaka kuja chumbani kwangu kunisalimia, hawataki. Watacheza na baba yao hapo sebuleni na Sara akiwepo hapo na vinguo vyake vya nusu uchi. Basi hata umtume msichana wa kazi akuitie watoto waje wakusalimie chumbani, hawataki. Michezo imekolea. Danny anazungumza na msichana wa kazi tu. Na ndiye anayempa maelekezo yote juu ya watoto.” Grace akacheka kwa kuguna.

“Siku 10 zilizopita, nafikiri Danny alichukua likizo. Nimerudi kutoka kazini, sijawakuta hapo nyumbani. Nimekaa mpaka kesho yake, hawajarudi. Nikamuuliza msichana wa kazi, akaniambia Danny alimwambia aandae vitu vya watoto wote, anasafari ya siku 7. Kwa hiyo amesafiri. Mimi nikacheka tu. Ndio wamerudi juzi. Wapo tu hapo ndani. Mama!” Grace akamgeukia mama yake.

“Natamani wasafiri tena. Ilikuwa bado kidogo nimwambie Danny kama hana pesa naweza kumuongezea ili waondoke tu hapo ndani kuwe na amani. Lakini maneno yakakwama. Nikimuona, hasira inapanda! Sitamani hata kuhisi kama yupo chumba cha pili.” Kimya. Mama G akavuta pumzi kwa nguvu.

Geb alitamani kumwambia waombe, lakini akajua Grace ameshaomba na walishaomba pamoja mara nyingi tu. “Sasa unataka kufanya nini?” Geb akarusha swali. “Nashukuru umeniuliza. Naomba nipe siku 30 za likizo. Nitoke kabisa hapa mjini, nisafiri nikasafishe akili zangu. Mbali na maneno ya kashfa ya Sara anayejisifia kuwa Danny anamtendea haki huko kitandani. Mbali na Danny anayenitukana kwa wazi tena wakati mwingine hata mbele ya yule msichana wangu wa kazi. Na mbali ya wale watoto, pengine itawasaidia kupatwa na hamu na mimi. Wakanikumbuka mama yao, wakataka hata kuiona sura yangu tena. Humuwezi amini hata Fili hataki kukaa na mimi hata kwa dakika moja! Fili aliyekuwa anapenda nimkumbatie, siye huyu. Watoto wote wananifanya kama mimi ndiye mgeni pale, halafu Danny na Sara ndio wazazi wao. Naumia kuliko nitakavyosema hapa.” Kila mtu kimya.

Grace akaendelea. “Kwa aliponifikisha Danny nakujisikia hivi ninavyojisikia sasa hivi, ipo sehemu ndani yangu inaniambia niliharakisha sana kuolewa na Danny. Nimepita naye kwenye magumu mengi sana. Yeye ndio amekuwa mwanaume wangu wa kwanza. Na tukahangaika sana. Kuanzia tunampata Fili mpaka wadogo zake, akili na mawazo yangu yote vilikuwa kwao tu. Ni kama sehemu ya maisha yangu imekuwa wao tu. Danny na watoto wake. Ni kama nimefika mahali ‘I CAN NOT TAKE IT ANYMORE’. Kutoka kwake na wanae. Naona wananilipa visivyo na mbaya zaidi, nafsi imechoka. Halafu sioni sababu tena. Kwa hakika nahitaji mapumziko. Mbali kabisa na yeye Danny. Labda nikirudi, nitajisikia tofauti.” Grace akawa amemaliza.

“Likizo haina shida. Lakini naomba ujue nitakuhitaji kipindi Nanaa anajifungua. Nitataka kuwa naye karibu.” “Amebakisha muda gani kujifungua?” Mama yake akauliza. “Itakuwa miezi miwili kasoro au niseme mwezi mmoja na siku chache.” “Mbona huko nitakuwa nimesharudi! Sitakawia kurudi. Ni likizo yangu ya mwaka.” “Hauna siku zilizobaki za likizo Grace. Ulimaliza siku zako zote.” Geb akamgeuka dada yake.

“Basi nakopa za mwakani.” Geb akamtizama. Alimjua Grace kwa kukopa likizo. “Mambo yalikizo yaache tu Grace. Umeshachukua siku zaidi ya unazotakiwa kuchukua za mapumziko kwa mwaka. Wewe kama unataka mapumziko, mimi naelewa. Lakini naomba nikutahadharishe Grace. Na nakuomba usinichukie. Nisikilize tu kama mimi ninavyokuwa nikikusikiliza ukinishauri.” “Niambie tu. Nakusikiliza.” Geb akamtizama kama kutaka uhakika.

“Wewe niambie chochote.” “Mimi nitakwambia Grace, kwa kuwa umekuwa msaada wangu mkubwa. Nipo hapa nilipo sababu yako. Wewe hujui tu. Lakini umehusika sana kwenye maendeleo yangu ya uchumi, mahusiano na kila mahali. Unajua udhaifu wangu, na kila ninapokosea, japokuwa unadhani huwa sikusikilizi, lakini huwa nakusikiliza sana. Na wakati mwingine huwa nachukia naona unakuwa umechelewa kuzungumza na mimi, mpaka naingia kwenye matatizo.” Grace akacheka.

“Sasa leo naomba na mimi unisikilize tu. Na usiniingilie. Niache nimalize na usianze kulia.” “Bwana wewe ongea.” “Tokea wewe unakua, ndoto zako na usemi wako ulikuwa ukitaka kuolewa na mwanaume kama baba. Wakati wote ulisema utaolewa na mwanaume mwenye umbile kama baba. Kuanzia urefu na haiba yake, vile vile kama baba. Ukasema awe kama vile baba alivyokuwa akikubembeleza kila wakati. Anakuweka mikononi kila unapokuwa naye. Awe muhangaikaji. Yaani mfanyabiashara. Mwenye pesa nyingi na akupende wewe tu. Mama unakumbuka?” Mama yake akaguna tu bila ya kujibu kitu kama anayejua anapoelekea Geb.

“Mliponiambia umeamua kuolewa na Danny. Mwanaume ambaye hana sifa hata moja ya mwanaume ambaye ulikuwa ukiimba unamtaka, nilishangaa sana. Muulize mama kama sikumuuliza kama kweli unauhakika na unachotaka kufanya. Nilimwambia mama nataka kuzungumza na wewe, mama akanikataza. Akasema nikuache tu kwa kuwa wewe mwenyewe ndio umeamua na ulimfuata Danny mpaka Tabora.” Geb akaendelea.

“Nikamwambia mama, upo confused. Ulikuwa umechanganyikiwa kwa wakati ule. Sio akili zako. Sio kweli kama unampenda Danny kwa dhati ni kwa kuwa alikuganda sana, na maisha yenu yote wewe na Danny amekuwa kama amekufunika shuka. Hujui mapenzi yakoje. Danny alikukaba kila kona. Nikamwambia mama, sijui kama anakumbuka. Nikamwambia kabisa mama, siku Danny atakapompa mwanya Grace. Akamuacha apumue hata dakika moja, Grace atajua kama aina ya wanaume kama Danny sio chaguo lake. Na hapo atakuwa amechelewa. Nilimwambia mama maneno kama hayo hayo uliyotuambia hapa sasa hivi, vile unavyojisikia sasa hivi kila ukimuona Danny. Mama unakumbuka?” Mama G akanyamaza.

Nilikutahadharisha mama. Na nikakwambia haya yanayotokea sasa, ni lazima yatakuja kutokea tu. Uliolewa na Danny kwa kuwa aliacha kukufanyia aliyokuwa akikufanyia kwa wakati ule, na akaondoka. Alikubali kuolewa na Danny huku akifungia macho mapungufu mengi sana ya Danny, kwa kuwa tu, alikuwa akikusindikiza bafuni. Sasa, sasahivi hayafanyi hayo yote tena, huoni umuhimu wa Danny tena.” “Lakini…” “Subiri kwanza Grace. Nimekuomba usiniingilie.” Geb akataka kumaliza.

“Unakumbuka mazungumzo yetu ya mwisho niliporudi nchini, kabla hujaolewa na Danny, juu ya Danny mwenyewe?” Grace akanyamaza huku akilia. “Ulimsema vibaya sana Danny. Ukaniapia humpendi kabisa. Hutaki hata kumuona. Kama hivi unavyosema sasa hivi, ndivyo ulivyokuwa ukimsema Danny. Tena ukaniambia huwezi hata kumfikiria eti anaamka pembeni yako. Hana sifa hata moja yakuwa mumeo. Tukazungumza siku ile mpaka usiku. Nimeondoka, hata miezi miwili haijaisha, mama ananiambia unaolewa na Danny! Hakika nilishituka sana. Sikuamini. Kwa kifupi tu Grace, hukuwahi kumpenda Danny.” Mama yake akamwangalia Geb.

“Utanisamehe mama. Lakini lazima niseme ukweli. Hizi zote sasa hivi ni sababu zilizochipua ukweli uliopo ndani yako Grace.” “Danny ndio amechangia.” “Nisikilize Grace. Nyinyi mlijua kilichotokea kati yangu na Nanaa. Alibakwa wote tukimsikiliza. Ana mimba ya Malii. Yaani amebeba mtoto wa Malii. Lakini mama na Grace, garama ya kuishi bila Nanaa, ni kubwa kuliko kusamehe na kumpokea vile alivyo. Maisha yalinipa nafasi yakuchagua mwanamke mwingine. Na nilikuwa naweza kufanya hivyo. Nyinyi ni mashahidi, lakini sijaona mwanamke ambaye anaweza kuchukua nafasi ya Nanaa kwenye maisha yangu. Ndio maana nilikuwa nakonda. Ni kwa kuwa nilikuwa na hasira, lakini bado namtaka Nanaa.” Geb akaendelea. 

“Nimekuja kugundua nampenda yule binti, kwa kila namna. Hakuna kosa au kitu atanifanyia nisitake kuwa naye. Nalala usingizi, nikijua yupo na mimi na mimi ndiye nammiliki. Kwamba ni wangu. Malii alimwambia kwa jinsi anavyonijua, sitamkubali tena baada ya yeye kumbaka. Hakukosea. Kama angekuwa amembaka mwanamke mwingine, hakika hiyo ndio ingekuwa sababu. Lakini ni Nanaa wangu. Ni wangu mimi. Wala sitakaa nimwachie mtu mwingine. Hapo shetani ajue ameshindwa. Akikubali tu, nitamkimbiza kanisani, nifunge mbingu na nchi, ili Nanaa awe wangu wa maisha.” Geb aliongea kwa uhakika.

“Hapo ndipo nilipoelewa mapenzi ni nini. Kabla ya Nanaa, sikuwa najua. Unaweza ukawa umekasirika. Au umemkasirikia mtu, lakini bado ukamuhitaji.” “Hunitendei haki Geb. Wewe hujaona vile nilivyohangaika na Danny? Yeye ndio amenikataa.” “Naomba usilie Grace. Nitashindwa kuzungumza.” “Kwa nini unashindwa kunielewa?” “Nakuelewa. Na ndio maana nataka kukusaidia. Naomba unyamaze G.” Mama yao alikuwa kimya ameinama chini, kashika shavu kama linataka kumwagika.

“Chukua likizo ya hizo siku 30. Nenda kapumzike. Safisha mawazo, lakini ujue wazi huo ndio ukweli utakao kutana nao hata baada ya hizo siku 30.” “Sasa nifanyaje?” Grace akauliza. “Hilo ndio swali la msingi namuhimu. Sasa hivi umerudisha umbile na sura ya kisichana. Haitakuchukua hata siku hizo 30, kupata mwaume wa ndoto zako. Shetani hasinzii wala halali kwa kuwa anajua haja zako, atakutega tu. 1koritho 10: 13 inaeleza juu ya majaribu tunayoyapata kuwa yapo ndani ya uwezo wetu. Kuwa tunaweza kuyashinda. Na Mungu atakupa mlango wakutokea.” Grace akanyamaza.

“Kuachana na Danny isiwe  ni suluhisho lako la kwanza. Ila kupumzika na kurudi ukiwa na nguvu mpya iwe ndio nia ya sasa. Mungu anaweza kukurejeshea yale yote shetani aliyokupokonya. Kama ulivyonituma nikamwambie Nanaa, na wewe pia pokea hayo maneno yakinabii. Omba rehema kwa Mungu. Msihi aumbe moyo safi ndani yako. Moyo uliojaa upendo. Akujalie kumtizama Danny kwa namna ya tofauti. Inawezekana Grace. Utaweza na utafanikiwa kwa kuwa sasa hivi unaanzisha mahusiano yako kwenye madhabahu ya bwana. Ukifanikiwa hapo. Haitakuwa kama zamani. Upendo Mungu atupao, sio ulimwengu unaweza kutupa. Utakuwa mkubwa na wa ajabu. Utarudishiwa ndoa yako ukiwa na upendo wa tofauti.” Grace akanyamaza.

“Wewe Grace!?” Mama yake akashangaa Grace hajibu ameinama kama anayefikiria. “Nimeshaomba sana mama. Nimechoka.” “Grace wewe! Kwa hiyo unataka kumuacha kabisa Danny?” Kimya. “Lakini hivyo sivyo tulivyozungumza Grace. Ulisema unasafiri kidogo, utarudi kwa wanao na mumeo.” “Bibilia yenyewe imeruhusu kuachana kwa kosa la uzinzi!” Grace alimjibu mama yake.  “Grace wewe umeingiwa na roho nyingine.” Mama yake akasisitiza. Geb alikuwa kimya kabisa akiwasikiliza.

Mimi sijaingiliwa na roho yeyote kwa kuwa nilikuwa kwenye maombi. Ukute Mungu ndio amenifungua macho. Simtaki Danny, mama. Simtaki tena. Nimevumilia nimechoka. Analala na Sara humo humo ndani! Sara ananiringishia mambo yao wanayofanya usiku kwenye mapenzi! Siwezi kumruhusu anishike tena. Nimeingiwa kinyaa mimi. Wewe unafikiri hata tukirudiana ndio nitasahau kama alilala na mwanamke mwingine humo humo ndani ya nyumba ambayo anajua na mimi nilijenga kwa jasho langu? Nawezaje kurudiana naye nikijua anafanya kwa makusudi, tena wala sio  mara moja! Au sio kwamba ni bahati mbaya! Anaishi na Sara huku akinitukana mbele ya Sara na mfanyakazi wangu! Kwamba alikuwa anakula makapi usiku kucha, sasa hivi Sara anamlisha penzi kwa mrija. Anakula vitu laini kwa mtoto laini!” “Haiwezekani Grace!” Mama G alianza kutokwa na machozi. Grace hakukusudia kuyasema yote, lakini akajikuta anayaongea tu mbele ya kaka yake.

“Kweli mama. Unafikiri ni kwa nini nakwambia nitachanganyikiwa? Ninatukanwa matusi ya nguoni tena waziwazi. Nenda kazungumze na msichana wangu wa kazi. Ni vile yule dada alitokea kunipenda tu. Lakini mama, mimi nimeshindwa. Sijawahi kudhalilika maishani kama hivi. Najiuliza ni mpaka lini? Na kwa nini!? Au kwa Lipi jamani!?” Grace aliendelea kuongea kwa uchungu sana huku akilia. 

“Mwili huu nimejisitiri hapa kwenu tu. Lakini nikiingia tu pale ndani ya ile nyumba, ni kama nipo uchi kwa vile ninavyochambuliwa huu mwili kwa matusi. Sina thamani.” “Na watoto?” “Ndio hicho kinachoniogopesha mama. Sasa hivi wanatukana kwa lugha ya mafumbo. Ila mnajua vile Fili alivyo na akili. Nahofia ataanza kuelewa, na yeye ashindwe kuniheshimu. Naumia sana. Hakika ningevumilia, na wewe Geb unakumbuka nilikwambia namuombea Danny. Lakini sina hata pakuombea tena. Unafuatwa na matusi kuanzia asubuhi mnaamka, Sara akimsifia hapo koridoni mapenzi waliyofanya asubuhi hiyo, au anatoka huku akitangaza dada akae na watoto kwa muda, wao wanaingia kuoga. Usiku napo mtaagwa kwa sauti. Kuwa wanaenda kuanzisha safari ya mapenzi. Kweli jamani! Mlitaka nifanye nini zaidi?” Kimya. Kila mtu kikawa kimemuingia moyoni. Hasira wote zikawapanda.

          “Unataka kuondoka lini?” Geb akamuuliza. “Kesho.” “Unataka nikutafutie tiketi ya wapi?” Geb akamuuliza. “Nataka kwenda kwanza Arusha. Halafu baada ya hapo nitajua. Lakini nitaacha simu.” “Una watoto wadogo wewe. Wakipatwa na tatizo?” “Naona mama wewe hujanielewa. Nakwambia Danny amefanikiwa kutoa nafasi yangu pale ndani, hata wanae wamejua kama sina matumizi kwao. Sina chakufanya kwa wale watoto na wale watoto hawana habari na mimi. Sijui uzima wao wala ugonjwa. Danny anazungumza kila kitu cha wale watoto na yule msichana wa kazi. Yaani mimi najua maendelea ya wanangu kwa kupitia yule msichana wa kazi.”

“Na ili kujua maendeleo ya huko wanakoshinda shuleni, ilinibidi mimi mwenyewe kwenda kuonana na walimu wao. Nako huko Danny amemwaga sumu kali, ni vile mwenye ile shule naye ni mama na tulifahamiana tokea Fili anaanza kusoma pale. Tunaheshimiana sana. Walimu waliponizuilia, ndipo ikabidi kumtafuta sasa yeye mwenyewe yule mama mwenye shule. Nikamueleza kwa ufupi pale tulipo na Danny, ndipo akazungumza na wale walimu wa wakina Fillius. Hapo ndio nikaweza kupewa maendeleo yao. Hasa Fillius na Fillan. Ndio hao nilikuwa na wasiwasi nao kwa kuwa bado ni wadogo. Kwenda asubuhi na kurudi jioni! Nikaona wanateswa tu. Ndio nikaambiwa wanapata muda wa kulala mchana. Nikazunguka kwenye hiyo shule, na sehemu wanazokuwa wao kwa siku nzima. Nipazuri kwa kweli. Nikaridhika, lakini sio wale watoto wenyewe. Hawanitaki mama. Huna utakalowauliza wakakujibu kwa muda mrefu. Wanakujibu kama wanaharaka na Danny naye akijua umewaita tu, na yeye atawaita hapo hapo. Sina raha mama. Acha niondoke. Labda hata wanangu wanaweza kunikumbuka tena. Sasa hivi hata wao wamechanganyikiwa.” “Naomba unyamaze Grace. Usilie. Pole.” Geb alimtuliza dada yake. “Kunywa maji kidogo.” Geb alitaka Grace atulie kabisa. Alishaumia na kumuhurumia sana. “Pole.” Akarudia. Grace akanywa maji, akatuliwa. Mama yao akabaki kimya. 

Grace ni mkimya. Hawakujua hayo yote yaliyokuwa yakiendelea kwenye maisha yake. “Kuna kitu kingine unataka?” Geb akauliza. “Hapana. Pesa ninazo.” “Safari njema. Ila nitataka kujua kama ulifika salama. Na kila baada ya siku tatu unijulishe kama upo salama. Sawa?” “Sawa. Kwa hiyo natakiwa kukupigia simu mara 7 katika hiyo likizo?” “Naona tumeelewana. Nisipokusikia baada ya siku 3, ujue nitaanza kukutafuta. Kwa hiyo nilazima unitafute, Grace.” “Sawa.” Geb akasimama. 

“Utatumiwa tiketi yako muda si mrefu.” Akamgeukia mama yake. “Usiku mwema mama.” Mama G akabaki kimya akifuta machozi. Alilizwa na mengi. Sara alikwenda kumtafuta yeye mwenyewe. Hakutumwa na mtu. Alitaka awe mke wa Geb, leo amekuwa mke wa mkwewe! Yule mama alijawa na majuto, asijue safari hii anamwita Mungu au Baba wa Yatima yupi wakati alimtenda yatima mwenzake ubaya wa namna ile. Hata Nanaa naye anatetewa na huyohuyo Baba wa yatima, Mungu anayemwitaga mama G. Halafu mchafuaji ni Danny, na yeye ni Yatima. Mtoto aliyempokea kama mwanae! Akabaki kulia, hata kuomba anashindwa. Geb akaenda alipokuwa amekaa, akambusu kichwani. “Uwe na usiku mwema mama.” “Na wewe. Nisalimie Nanaa na watoto.” “Asante.” Geb akaondoka na kumuacha mama yake akiendelea kufuta machozi, akijua anachojisikia huko moyoni. Hata hilo la Grace kuolewa na Danny pia alimuonya mama yake. Geb alimjua Danny kwa kuishi naye miaka 7, tena chumba kimoja, darasa moja.

Kwa Nanaa.

Geb alirudi nyumbani akamkuta Nanaa amejilaza kwenye kochi peke yake, godoro lipo chumbani. “Vipi? Mbona godoro umetoa tena? Hatulali hapa?” “Nimeona kama watoto wanaanza kuzoea kulala hapa na mimi, Geb. Hata mchana wanataka nilale nao. Naona ni kitu ambacho kitaanza kuwasumbua kipindi nitakachokuwa hospitalini na mdogo wao. Ule utaratibu uliokuwa umewazoeza ni mzuri. Kila mtoto alale kitandani kwake. Au nimekosea?” Geb akatulia. “Lakini wapo tu sawa. Niliwatoa kwenda kucheza hapo kwenye mabembea. Wamecheza mpaka wamechoka. Nimerudi nikawaogesha, wamekula ndio wamelala. Tena umewachelewa kidogo tu.” Nanaa akaendelea kujieleza bila kujua kinachomfanya Geb anyong’onyee vile.

“Lakini kama unaona ni sawa tuendelee kulala nao, basi. Tukatoe tena godoro, tuwalete tulale tu hapa. Lakini nilikuwa nakuhurumia wewe kipindi ambacho mimi nitakuwa hospitalini. Wakati umebaki nao hapa peke yako, utateseka.” “Kama hiyo ndio itanisaidia kulala karibu na wewe, sitajali kunyanyua godoro na kulirudisha hapa.” Nanaa akashangaa. Akakaa. Geb aliongea kwa kunyong’onyea.

“Naona tunarudi tena nyuma Nanaa! Mimi na wewe nilifikiri tunasogea mbele, lakini naona tunarudi mwanzo kabisa! Unarudi kulala kwenye kochi, mimi narudi kulala chumbani peke yangu!” “Sikujua kama, kama…” Nanaa akasita asijue amalizie vipi sentensi yake. “Kama nataka kulala na wewe au kama nafurahia kulala pembeni yako? Unataka nifanye nini Nanaa? Niambie.” Nanaa akanyanyuka, “Mimi natangulia chumbani.” Geb akabaki hana chakusema tena. Nanaa akaenda chumbani kwa Geb, akapanda kitandani. 

          Geb akamfuata. “Sasa unalala hapa kwa kuwa unapenda au unaona nimekulazimisha?” “Naomba uje tuzungumze ukiwa umelala hapa, Geb. Najua umechoka. Week hii nzima umekuwa busy. Njoo hapa ulale. Nitakubembeleza utalala kama Magesa.” Geb akacheka, akavua nguo haraka akapanda kitandani.

“Habari za huko ulikotoka?” Nanaa akaanza kumuhoji taratibu wakati akimchezea nywele. “Sijui Nanaa. Ila ujue nimefurahi umelala hapa na mimi.” “Nakusikia unavyoongea kwa kugugumia raha.” Geb akacheka. “Na ushikwaji huo sijaupata tokea nakutoa hospitalini baada ya kujifungua Magesa. Nishaanza kusinzia.” “Wewe lala tu.” Nanaa akajua hataki kuzungumzia habari za huko alikotoka, akaona amuache tu. Alimchezea nywele huku akimpapasa taratibu mpaka akalala. Akamcheka na kumfunika vizuri, ndipo na yeye akalala.

Grace safarini

Grace aliondoka na ndege ya asubuhi ya saa 4, kuelekea jijini Arusha. Alipendeza, ungependa kumwangalia dada huyo. Kama angekwambia ana watoto watatu usingesadiki. Alikuwa akivutia. Alikumbushia enzi za usichana wake. Akajitengeneza na kuvaa nguo aliyopenda yeye. Hapakuwa na Danny wakumrudisha wala mtu wakumuuliza. Kwa hiyo alivaa alichopenda, na akapendeza. Geb alimtuma Jeri akamchukue kumpeleka uwanja wa ndege.

Aliingia kwenye ndege, akakaa kiti cha dirishani. Geb alimpatia kiti kule First class, kwa matajiri. Grace akajiweka sawa. Hakuwa na simu wala kitu chakufikiria ila kule aendako tu. Akaja mtu kukaa pembeni yake akiwa anazungumza na simu. Grace hata hakujisumbua kumtizama. Akageukia vizuri dirishani, akaendelea kuwaza maisha yake. Matangazo yakaendelea, akajua wanakaribia kuondoka. Akahakikisha amefunga mkanda vizuri. Akatulia.

Wakati ndege ipo angani akahisi mtu anamgusa. Akageuka. “Karibu usome gazeti.” Grace akatizama lile gazeti, akapokea bila hata kumwangalia usoni. “Asante.” “Huwa pia wananiita Man.” Ikabidi Grace amwangalie na tabasamu. “Nimejitahidi kukohoa, kuhangaika hapa kwenye kiti, lakini wapi! Imebidi nimuombe jirani gazeti nikupe ili uniangalie. Pia naona umepokea bila kuniangalia!” Grace akacheka. “Naitwa Grace.” “Daah! Afadhali. Mpende jirani yako kama nafsi yako. Huwezi jua litakalo tupata huko angani. Ni bora kufahamiana mapema.” “Kwa hiyo kila unayesafiri naye huwa unajitahidi kumpenda?” “Kwa kweli najitahidi. Katika hilo huwa najisifu.” Grace akacheka na kugeukia gazeti.

Pakatulia kidogo. “Mimi naenda Arusha.” Grace akamgeukia akiwa ametulia. “Nimesema mimi naenda Arusha.” Man akarudia, Grace akacheka. “Sawa.” Grace akajibu na kugeukia gazeti. “Eti mimi nilijua na wewe utaniambia wapi unakoelekea.” “Mimi nilijua umenipa gazeti nisome.” Grace akajibu. “Hapana. Nilitaka tu uniangalie.” Grace akacheka. “Na mimi naelekea Arusha kwa mapumziko.” “Daah! Heri yako wewe.” “Kwa nini unasema hivyo?” Ikabidi Grace amuulize tu. “Mimi natafuta hayo mapumziko, huu ni mwaka wa pili, sijayapata.” “Wakati mwingine unalazimishia.” “Eti eeh!” Man akawa kama anafikiria.

Grace alishamuona ni mtundu. Akacheka. “Hapa nafikiria jinsi yakulazimishia. Lakini najua nitaweza tu. Unajua nilikuona ukiingia humu ndani ya ndege. Kiti changu kilikuwa kile pale. Nikamlazimishia yule jamaa, tubadilishane viti. Alitaka kukataa, nikamlazimishia mpaka amekubali. Sasa nimekuja tena hapa, nikaona huniangalii! Nikajiambia juhudi zote zile, halafu hata nisiione sura kwa karibu, heri nimuombe jirani gazeti.” Grace alizidi kucheka.

“Naitwa Grace. Nimeolewa na nina watoto watatu.” “Woooh! Wooh! Taratibu Grace. Acha kunifukuza kwa nguvu hivyo! Mbona mimi nimesema ni salamu tu! Naona umeamua kunifukuza kabisa!” “Hapana. Huo ndio ukweli.” “Lakini sijaona pete hapo kidoleni!” “Si hii..” Grace akaangalia kidoleni akagundua hana pete. Man akamtizama kama kumsuta. “Kweli tena. Sio kwamba nakufukuza. Nina watoto watatu. Ngoja nikuonyeshe picha zao kwenye simu yangu.” Akafungua pochi, akakumbuka hata simu aliacha. Man akapandisha nyusi juu.

“Naona nimesahau na simu.” Man akajidai anacheka kwa kukohoa. “Bwana wewe ni mtundu Man. Ila ujue sijakudanganya.” “Labda niulize Grace. Kusudi la ule utambulisho mzito vile ni nini?” Grace akaingiwa na aibu mpaka akajikuta anavua miwani aliyokuwa amevaa kwa ajili ya jua na mwanga. Amekuwa mama kwa muda mrefu sana. Hajui kujitenga na wanae.  Akainama kama anayefikiria huku akichezea ile miwani. “Niliona nikwambie tu usije kufikiria umekaa hapa na msichana, kumbe ni mama.” Grace aliongea kwa upole huku akimtizama Man. Na sauti yake na macho, ungependa tu kumsikiliza. “Ila sikuwa na nia mbaya.” Aliongeza kwa upole baada ya kumuona Man amebaki ameduaa akimwangalia. “Nimefurahi kukufahamu, Grace.” Man akapunguza uchokozi, akaongea na yeye kiustarabu. Grace akatoa tabasamu na kugeukia dirishani. Kimya. 

Wakatulia kabisa kwa muda mpaka wakawa wamekaribia kufika. Man akamgusa tena. “Nafikiri hiki kikaratasi ni chako.” Man akamkabidhi, Grace akakipokea na kukifungua. ‘Samahani. Sikukusudia kukuudhi.’ Grace alikutana na huo ujumbe kwenye hicho kikaratasi. Akajua kinatoka kwa Man. Akamwangalia akakuta na yeye anamwangalia. “It’s okay.” Grace alijibu kwa sauti ya chini. “Thanks.” Man naye akajibu taratibu huku akimwangalia. Grace akarudisha macho dirishani mpaka wanafika hakumwangalia tena.

“Ningekuwa sijaharibu, ningekukaribisha jijini. Lakini najua hutakubali tena. Basi naomba nikutakie mapumziko mema.” Man aliongea kabla hajashuka. Grace alitabasamu tu, akarudisha macho kwenye pochi yake. Akaingiza baadhi ya vitu vyake kwenye pochi huku Man akimwangalia. Alipoona Grace hata hamgeukii tena, akasimama na kutoka. Baadaye Grace na yeye akashuka taratibu bila haraka huku akifikiria chakufanya jijini hapo. 

Akachukua sanduku lake kubwa na dogo, pamoja na begi jingine alilokuwa ameweka kwenye ndege. Yote yalikuwa yakifanana. Akayaweka pamoja ili kupata urahisi wakuyasukuma.  Akayaburuza mpaka nje. Akaangalia kulia na kushota akitaka taksii, imsogelee. Lakini ikamsogelea kwa haraka gari ambayo wazi haikuonekana kama ni taksii.

Alikuwa tena Man. Akashusha kioo. “Naweza kukusogeza.” “Hapana. Asante. Nitachukua tu taksii.” Grace alikataa bila hata kufikiria. Man akafikiria kidogo, akaondoa gari. Alipoondoka tu Man, taksii ikamsogelea. Grace akapanda. “Mimi ni mgeni hapa Arusha. Unafahamu hoteli yeyote nzuri.” “Usiwe na wasiwasi dada. Hapa umefika. Nitakupeleka kwenye hoteli ambayo huwa pia wanatoa huduma za utalii. Ni pazuri sana.” Grace akashukuru. Akatulia ndani ya hiyo taksii akimsikiliza huyo dereva taksii akisifia hiyo hoteli na huduma zake. Kadiri yule dereva alivyokuwa akiongea akisifia huduma ya hiyo hoteli, Grace alikuwa akijiambia kama ni kweli, basi ataua ndege wengi kwa jiwe moja. Akajua mapumziko yake yatafanikiwa.  

~~~~~~~~~~~~~~

Dereva alimpeleka mpaka kwenye hiyo hoteli. Akamshusha. Kwa nje tu, Grace akakubali kuwa ameletwa sehemu ya hadhi yake. Alipokelewa mizigo yake na mtu aliyekuwa hapo mlangoni na sare nzuri sana. Akashukuru, akakaribishwa ndani mpaka mapokezi. Kitu alichotaka ni chumba ambacho kitakuwa gorofa ya mwisho kabisa. Ambako hatamsikia mtu ila yeye mwenyewe. Muhudumu akacheka, na kurudisha macho kwenye kompyuta iliyokuwepo mbele yake.

Kwa ukarimu ule aliokuwa akifanyiwa na kutetemekewa kama mfalme, Grace alijua wazi pesa ya kutosha itamtoka. Lakini alikusudia kwa mara ya kwanza maishani, afaidi jasho lake yeye mwenyewe. Akabebewa tena mizogo yake mpaka chumbani. Chumba kilikuwa full suit. Madhari ya pale ndani tu, yakafanya moyo wa Grace usuuzike. 

Muhudumu yule yule aliyekuwa amevaa sare za hapo hotelini, ambaye alimbebea mizigo yake tokea anafika hotelini hapo, aliingiza ile mizigo mpaka ndani na kuuliza kama angetaka kitu chochote. Lakini Grace akakataa. Alimpa pesa kidogo. Kama tip, akafunga mlango. Hakuwa na simu ya mkononi. Ikabidi atumie simu ya mezani kumtaarifu Geb kuwa amefika salama kama alivyomuahidi. “Nimefika salama.” Grace akaongea tu mara baada ya Geb kupokea simu yake. “Mapumziko mema.” Geb akakata simu. 

~~~~~~~~~~~~~~

Akaanza kuwaza sasa. Likizo ile ya siku 30, ataifanyia nini? Tokea yupo chuo mwaka wa pili, maisha yake yote yalijawa Danny tu. Ni kweli alimganda kila mahali. Na baada tu yakufunga ndoa, Grace akashika mimba. Akamzaa Fili. Maisha yake yakawa Danny na Fili. Baadaye wakaja mapacha. Grace hakuwa akijua maisha yake binafsi bila watoto au Danny. Hajui anatakiwa kufanya nini juu yake binafsi akiwa hana mtu mwingine wakumfikiria. Swali la nini afanye, likawa mtihani. Afanye starehe gani ambayo itatunza hadhi yake? Kukaa tu pale chumbani, akajua ndio maisha aliyokuwa akiishi muda wote huo kabla hajapanda ndege yakumtoa jijini Dar. 

“Lazima kufanya kitu cha tofauti.” Grace akaazimia moyoni. “Lakini nini?” Huo ukazidi kuwa mtihani. “Nioge na kubadili nguo, nikakae sehemu wanayouza vinywaji.” Hakuwahi kunywa pombe, wala hajui ladha yake. Akajua soda tu itamchosha kukaa. “Sasa kwani mimi huwa napenda nini?” Grace akajiuliza kwa sauti. Tayari alishasahau hobies zake. Akaoga na kubadilisha nguo, akatoka kwenda mapokezi.

“Samahani!” Alimkuta mrembo yuleyule aliyempa chumba, pale mapokezi. “Umebadili na kuzidi kupendeza!” Grace akacheka. “Asante. Lakini naomba msaada wako.” “Karibu!” Yule mrembo akamtolea tabasamu. Grace akajisikia huru kuuliza. “Kwanza asante kwa kunichagulia chumba kizuri. Nimekipenda.” Yule mrembo akacheka. “Nilijua tu utaridhika. Nikusaidie nini tena?” Akamuuliza Grace.

          “Hivi hapa mjini Arusha kuna vivutio gani? Kitu gani kizuri kinaweza kunifaa?” Yule dada akacheka. “Kwani wewe unapenda nini?” Grace akafikiria kidogo. “Nataka kufanya kitu cha tofauti. Wewe nitajie tu vitu vyote, nitachagua.” “Okay. Kama unapenda kutoka usiku, kuna kumbi nyingi tu za starehe. Hata hapa huwa wanakuwa na ‘Live band’. Kila jumamosi usiku huwa wanapiga mziki. Na leo kuna fashion show hapa. Japokuwa nimesikia kuwa tiketi zimeuzwa zote, lakini naweza kukutafutia ticket, uingie tu uone kinachoendelea. Huwa inakua nzuri sana. Kunakuwa na mambo mengi, huwezi kuchoka.” Grace akaona hamna chakupoteza. Kwanza itakuwa ni hapo hapo hotelini.

“Lakini pia huwa tunakuwa na magari ya Safari. Yanapeleka watalii mbuga za wanyama. Unaweza ukapenda kwenda na huko.” “Kumbe afadhali nimekuuliza. Nilisahau tu, lakini hata yule dereva taksii aliniambia. Afadhali umenikumbusha.” Wakacheka. “Naona vitu vyote nitafurahia sana tu. Huwa nasikia Tanzania kuna simba, tembo na wanyama wengine. Lakini sijawahi kuwaona kwa macho. Ni heri na mimi niende nikashuhudie kwa macho.” “Sawa. Ungependa kwenda lini?” “Kwa kuwa leo nitakuwa huko kwenye fashion show, najua naweza nikachoka. Kesho nitataka kupumzika. Jumatatu naona itakuwa siku nzuri.” “Ungependa nikutafutie hoteli kabisa?” “Mbona hiyo ingenisaidia zaidi! Kama sio usumbufu, nitafutie kila kitu, ili nisisumbuke.” “Hii hoteli ina tawi huko huko mbugani. Kwa hiyo itakupa huduma ya gari na hoteli pia.” “Usisahau chumba kizuri.” Wakacheka.

“Basi wewe jiandae, saa 12 jioni kuwa tayari. Tiketi yako itakufuata huko huko chumbani.” “Asante. Swali la mwisho. Lakini usinichoke.” “Wala usijali. Nipo kukusaidia dada yangu.” “Haya. Vipi chakula? Mnakuwa na vyakula vizuri?” “Kwa swala la chakula, hapa umefika. Tunaye mpishi mzuri sana. Utapenda vyakula vyake. Nenda kajaribu tu.” “Sawa. Tutaonana baadaye. Unaitwa nani tena?” “Beka. Wengi wananijua kwa jina la Beka, lakini ni Rebeka.” “Nashukuru Beka. Baadaye basi. Natumaini nitakuona tena.” “Jumatatu nitakuwa hapa. Kesho napumzika.” Wakazungumza kidogo, akamuelekeza ilipo sehemu ya kulia chakula. Grace akaelekea kule.

~~~~~~~~~~~~~~

Grace aliingia pale mgahawani, akakuta wamekaa watu wengine. Akatafuta meza ya peke yake, akakaa. Muhudumu akamfuata kwa haraka. Mpaka Grace akashangaa. Wala hakusubiri sana na wakati walikuwepo wateja wengine. Akavutiwa na huduma za pale. Akaagiza juisi ya maembe. Wakati anasubiria juisi iletwe, akavutiwa na ule mgahawa, akaamua kuangaza macho.

Alipogeuka ili kuangalia kona ya upande wa kulia kwake, macho yake yakagongana na Man. Grace akashituka sana. Akarudisha macho mezani kwake. Man alikuwa amekaa kwenye meza moja na mwanamke aliyeonekana nadhifu sana. Jinsi alivyovaa, alionekana mdogo kwa umri wake. Hakuwa na mwili mkubwa. Na vijana wengine wawili. Wazi walionekana wapo kwenye mazungumzo ya kikazi.

Grace akafikiria kwa haraka, akaona aondoke pale. Akasimama. “Grace!” Man akasimama na yeye kwa haraka akamfuata. “Huna sababu yakuondoka hapa kwa ajili yangu. Nakuahidi sitakusumbua. Kaa tu ule.” “Hapana. Mimi nilikuja tu kupaangalia. Napita.” Grace akajitetea kwa sauti ya chini. “Wewe sio muongo Grace. Tafadhali usianze kwangu. Nakuahidi wala hutahisi uwepo wangu. Wewe kaa tu. Furahia chakula na kinywaji ulichoagiza. Sitakughasi.” Grace akawa amekamatwa. “Please.” Man akamsihi. Bila kujibu, Grace akageuka na kurudi kukaa. Man akaondoka.

Hakujua kikao cha Man na wenzake kiliisha saa ngapi! Au kama walihamisha kikao au la. Lakini alipomaliza kinywaji chake, akitaka kuondoka, akagundua hawapo. Ndipo alipopata nguvu yakuagiza chakula. Alipenda kila kitu. Akakubaliana na Beka kuwa wanampishi mzuri. Akaamua kurudi chumbani kwake.

“Man anafanya nini hapa? Kwa nini tuna..” Grace akanyamaza. Akaamua kujipumzisha mpaka jioni ili aende kwenye fashion show. Akapitiwa na usingizi. Akalala kama mfu. Uchovu wa miaka yote, mbali na kero za Danny na Sara. Kuwaza wanachofanya chumba cha pili, kelele za watoto, hata hakugeuka, akalala mpaka saa 11 jioni.

Alipoamka tu, akakuta tiketi yake chini ya mlango. Akajua muhudumu ndio ameweka pale. “Mbona hawajanidai pesa?” Grace akajiuliza. “Labda wataniwekea kwenye bili yangu yote!” Grace akaendelea kujiandaa. Akatoa viatu virefu. Akajicheka kwanza. Hakuwa amevaa viatu virefu kwa muda mrefu sana. Kwanza alikuja kunenepa sana. Mwili ukawa unamlemea. Akaanza kuumia kila akivaa viatu virefu. Akaamua kuacha kuvaa viatu virefu. Akaja kuzaa watoto. Unaenda wapi ukiwa umevaa viatu virefu na watoto watundu kama wa Danny? Grace akahamia kwenye viatu vya chini kwa miaka mingi tu.

Akajaribu kutembea navyo pale chumbani. Akaona bado anakumbuka kutembelea viatu virefu. Akavaa gauni ambalo ni refu lakini halina mikono wala mikanda. Linaishia kifuani. Na umbile la Grace, hutakaa ukaacha kumwangalia. Lilikuwa jeupe lenye pindo nyeusi zilizopita kifuani na kwenye V iliyoanguka chini ya kiuno nyuma. Akavaa na viatu vyenye nyeupe na nyeusi, tena mchongoko mbele. Akavaa na hereni ndeni kama cheni. Zilishuka mpaka mabegani. Hata Danny angemuona asingeamini kama ni Grace, mkewe. Rangi yake nyeusi, ikapendeza kwenye lile gauni jeupe. Akajipulizia pafyum. 

“Sijui nimezidisha?” Grace akajiuliza wakati anageuka kwenye kioo. “Wasije wakasema nimepania bure!” Grace akacheka. “Lakini si wamesema ni Fashion show? Nipo sawa bwana!” Grace akatoka.

~~~~~~~~~~~~~~

Akatembea kwa kunyata mpaka kwenye lifti iliyomshusha mpaka chini. Akatoka kwenye lifti. Akatembea kwa mwendo wa taratibu ili asianguke. Aliona vile watu walivyokuwa wakimwangalia. Akacheka moyoni. Akajua hakika amependeza. Akaendelea kusogelea sehemu ya mapokezi ili kumtafuta Beka amshukuru. Alimuona kwa mbali kijana ambaye kwa mgongoni tu, alionekana mrefu vyakutosha. Alivaa nadhifu. Suti nyeusi iliyokuwa imemkaa vizuri sana. Alikuwa amesimama pale mapokezi, na kuegemea pale akionekana amezama kwenye kitu alichokuwa akifanya. Moja kwa moja Grace akajua atakuwa na yeye anaelekea kwenye hiyo tamasha. 

Bado Grace alikuwa akitembea taratibu kusogelea mapokezi, na yule kijana alionekana amezama kufanya hicho alichokiinamia, hakugeuka. Grace alikuwa akimuona kwa nyuma tu. Alifika mpaka pale mapokezi, akagundua mrembo aliyekuwepo pale si Beka japo sare zao za kazi zilifanana. “Samahani. Namuulizia Beka.” Grace akaongea na huyo mrembo aliyemkuta pale mapokezi na yeye alimpokea kwa tabasamu zuri. “Beka ametoka saa 10. Hatakuwepo hapa mpaka siku ya jumatatu. Ataingia tena asubuhi. Lakini hata mimi naweza kukusaidia. Karibu.” Grace ni kama akaishiwa nguvu.

“Asante. Lakini nilitaka kumshukuru na kumpa zawadi kidogo. Amenisaidia sana tokea nafika hapa. Ila kwa kuwa nitakuwepo mimi mwenyewe mpaka hiyo jumatatu, nitamkabidhi tu yeye mwenyewe. Asante.” “Karibu. Ila Umependeza sana. Utafikiri na wewe upo kwenye fashion show!” Grace akacheka. “Asante. Ni Beka huyo ndio amenishauri niende.” Akagundua yule kijana aliyekuwa ameinama pale kaunta, pembeni yake, anamwangalia muda wote na kumsikiliza. Akaona na yeye amgeukie.

“Man!” Grace akashituka sana. Akajikuta anaita jina lake taratibu kwa mshangao. Man akamgeukia vizuri kama na yeye ameduaa akimshangaa yeye. Wakaangaliana kidogo wote wasijue waseme nini, Grace akaamua kuondoka. Kabla hajapiga hatua nyingi akasikia “Waw!” Man ameshangaa kwa sauti. Hakugeuka. Grace akaendelea kutembea kuelekea ulipo ukumbi. Moyoni akacheka. Akajua hata Man amevutiwa. “Kumbe bado sijazeeka!” Grace akajisifia mawazoni, akacheka.

~~~~~~~~~~~~~~

Haya tena, mambo yameanza kuchanganya kwa mapacha wa Mama G.

-       Geb anaanza kupokelewa na Nanaa mwenye mimba ya Malii.

-       Grace kaondoka nyumbani, kwa kuchoshwa na familia yake, ametua jijini Arusha, na Man naye yupo.

Mama G amebakishwa peke yake akilia. Anamwita Mungu yupi? Ameshaanza kuvuna alichopanda.

-       Hata Magesa ambaye ni kama mtoto wake, anamkataa. Liv ambaye ndiye wajina wake pia hamtaki.

-       Amevunja ndoa ya mwanae bila kutarajia. Aliyokusudia kumfanyia Nanaa, yanamrudi yeye mwenyewe kwa mwanae Grace.

Mpaka lini, kwa umbali gani? Hakuna ajuaye. Lakini amebaki na kilio cha Grace

akiwasimulia yanayoendelea kwenye maisha yake.

-       Udhalilishwaji wa hali ya juu anaopitia kwa wakati ule.

-       Watoto wake aliokuwa akiwahangaikia pia hawana muda naye! Ilibaki ikimuumiza sana si mama G tu, hata Geb pacha mwenzie.

Geb anaumizwa zaidi kuona anayofanyiwa na Danny sasa hivi, hasa baada ya kumvumilia Danny mpaka hapo alipofikia.

Usikose kujua kitakachoendelea kati ya Grace & Man.

-       Man ni nani? Kwa nini na yeye yupo pale hotelini? Aliyosema Geb yanatimia kwa dada yake?

-       Geb & Nanaa! Geb amemwambia Nanaa akimkubali tu, atamkimbiza kanisani haraka sana.

§  Na mtoto wa Malii!?

-       Itakuaje kwa Nanaa ambaye ni mgonjwa na bado amebeba mambo mengi sana moyoni? Amekiri kuwa mambo yamebadilika sio kama zamani kukubali kila kitu kwa haraka. Ameomba apewe muda. Wa nini? Kwa nini? 

-       Mama G!?

o   INAENDELEA…

 

CONVERSATION

0 Comments:

Post a Comment